Showing posts with label MWALIMU JULIUS NYERERE. Show all posts
Showing posts with label MWALIMU JULIUS NYERERE. Show all posts

14 Oct 2016


HISTORIA FUPI YA MWALIMU NYERERE
MPAKA MAUTI YALIPOMFIKA

Tarehe ya kuzaliwa 13 Aprili 1922
Mahali pa kuzaliwa Butiama
Tarehe ya kifo 14 Oktoba 1999
Rais wa Tanzania
Alingia ofisini 1964
Aliondoka ofisini 1985
Alitanguliwa na (alikuwa rais wa kwanza)
Alifuatwa na Ali Hassan Mwinyi
Dini Mkristo Mkatoliki
Elimu yake Chuo Kikuu cha Edinburgh - Uskoti Digrii
anazoshika M.A. ya historia na uchumi
Kazi mwalimu, mwanasiasa Mengine Nyerere alikuwa
mwenyekiti wa chama cha TANU na baadaye wa CCM.
Mara nyingi aliitwa "Mwalimu Nyerere".
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alikuwa rais wa
kwanza wa Tanzania. Alizaliwa Butiama, mkoani Mara
pembezoni mwa Ziwa Nyanza tarehe 13 Aprili, 1922.
Alifariki dunia 14 Oktoba, 1999. Aliiongoza Tanzania toka
mwaka 1961 hadi mwaka 1985.
Yeye ni mwasisi wa itikadi ya ujamaa na kujitegemea.
Kabla ya kuingia kwenye siasa alikuwa ni mwalimu. Kazi
hii ndiyo ilimpatia jina ambalo lilimkaa maisha yake yote la
"Mwalimu." Mwalimu Nyerere ni kati ya viongozi wachache
wa Afrika ambao wameacha madaraka kwa hiyari baada
ya kutawala kwa muda mrefu. Alipostaafu urais mwaka
1985 alirudi kijijini kwake Butiama ambako aliendesha
shughuli za kilimo. Aliendelea kuwa na athari kubwa
katika siasa ya Tanzania hadi kifo chake.
Maisha Ya Mwalimu
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alizaliwa mwaka 1922
( katika kijiji cha Butiama, wilaya ya Musoma, mkoa wa
Mara, Tanzania (wakati ule: Tanganyika). Alikuwa
mojawapo kati watoto 26 wa Nyerere Burito, chifu wa
kabila la Wazanaki. Alipokuwa mtoto Nyerere alichunga
mifugo ya babake; katika umri wa miaka 12 aliingia shule
akitembea kilomita 30 hadi Musoma. Baada ya kumaliza
shule ya msingi aliendelea kusoma shule ya wamisionari
Wakatoliki huko Tabora. Katika umri wa miaka 20
alibatizwa akawa mkristo Mkatoliki hadi mwisho wa
maisha yake.
Mapadre wakaona akili yake wakamsaidia kusoma ualimu
huko Makerere, Kampala, Uganda kuanzia 1943 - 1945.
Makerere akaanzisha tawi la Umoja wa wanafunzi
Watanganyika pia amejihusisha na tawi la Tanganyika
African Association (TAA). Baada ya kumaliza masomo ya
ualimu alirudi Tabora akifundisha shule ya St.Mary´s.
Mwaka 1949 alipata skolashipu ya kwenda kusoma
kwenye Chuo Kikuu cha Edinburgh huko Uskoti /Uingereza
akasoma M.A. ya historia na uchumi(alikuwa mtanzania
wa kwanza kusoma katika chuo kikuu cha Uingereza na
mtanzania wa pili kupata shahada ya elimu ya juu nje ya
Tanzania).
Aliporejea Tanganyika kutoka masomoni, Nyerere
alifundisha Historia, Kingereza na Kiswahili katika shule ya
St. Francis iliyo karibu na Dar es Salaam. Mwaka 1953
alichaguliwa kuwa raisi wa chama cha Tanganyika African
Association (TAA), chama ambacho alikisaidia kukijenga
alipokuwa mwanafunzi katika chuo kikuu cha Makerere.
Mwaka 1954 alikibadilisha chama cha TAA kwenda katika
chama cha Tanganyika African National Union (TANU)
ambacho kilikuwa cha kisiasa zaidi kuliko TAA. Ndani ya
mwaka mmoja chama cha TANU kilikuwa tayari chama cha
siasa kinachoongoza Tanganyika.
Uwezo wa mwl. Nyerere uliwashitua uongozi wa kikoloni
na kumlazimisha Nyerere kuchagua kati ya siasa na kazi
ya ualimu. Nyerere alisikika akisema kuwa alikuwa
mwalimu kwa kuchagua na mwanasiasa kwa bahati
mbaya. Alijiuzuru ualimu na kuzunguka nchini Tanganyika
kuzungumza na watu wa kawaida na machifu ili kuleta
muungano katika mapigano ya uhuru. Pia alizungumza
kwa niaba ya TANU katika Trusteeship council na Fourth
committee ya Umoja wa Mataifa (UN) huko New York.
Uwezo wake wa kimaongezi na kuunganisha watu
ulimwezesha kufanikisha Tanganyika kupata uhuru bila
umwagaji wa damu. Ushirikiano mzuri aliouonyesha
aliyekuwa gavana wa wakati huo bwana Richard Turnbull
ulisaidia pia kuharakisha upatikanaji wa uhuru. Nyerere
aliingia katika bunge la kikoloni mwaka 1958 na
kuchaguliwa kuwa waziri mkuu mwaka 1960. Mwaka 1961
Tanganyika ilipata uhuru wake na tarehe 9/12/1961
Nyerere alichaguliwa kuwa waziri mkuu wa Tanganyika
huru na mwaka mmoja baadae Nyerere alikuwa raisi wa
kwanza wa jamhuri ya Tanganyika. Nyerere alikuwa kiungo
muhimu katika muungano wa Tanganyika na Zanzibar
kutengeneza Tanzania baada ya mapinduzi ya Zanzibar
mwaka 1964 yaliyomtoa madarakani sultani wa Zanzibar
Jamshid bin Abdullah.
Sifa zake
Bado anakumbukwa na watanzania hasa wa hali ya chini
kutokana na sera zake za kujali utu na ubinadamu.Pia
ataendelea kukumbukwa na waafrika kote barani hasa kwa
mchango wake mkubwa wakati wa harakati za kupigania
uhuru katika nchi mbali mbali barani Afrika.
Ni mmoja wa viongozi wachache wanaokumbukwa kwa
kutojilimbikizia mali pamoja na kutawala kwa miaka zaidi
ya 24.
Mwishoni mwa maisha yake Nyerere aliishi kama mkulima
wa kawaida kijijini kwake Butiama. Alipatwa na kansa ya
damu (leukemia) na kufariki Uingereza wakati wa kutibiwa
katika mji wa London tarehe 14 Oktoba, 1999. Alizikwa
mahali pa kuzaliwa kwake, kijiji cha Butiama.
Machapisho ya mwl.Julius K. Nyerere.
• Freedom and Socialism.Mkusanyiko wa maandiko na
hotuba, 1965-1967 (1968)
• Freedom & Development, Uhuru Na Maendeleo (1974)
• Ujamaa - Essays on Socialism' (1977)
• Crusade for Liberation (1979)

CHANZO: Jamii Forums


30 Sept 2014

Rais Jakaya Kikwete amezilaumu sera za uchumi za Tanzania baada ya nchi yetu kupata uhuru akidai zimepelekea hali duni ya kiuchumi.

Alieleza kuwa sera hizo ni moja ya sababu zinazoifanya Tanzania kuwa katika kundi la Nchi Masikini Zaidi Duniani (The Least Developed Countries - LCD) tangu utaratibu huo wa kuzigawanya nchi kutokana na viwango vyake vya kiuchumi na maendeleo uanze miaka ya 70.

Akihutubia Alhamisi iliyopita jijini Washington DC, nchini Marekani katika Kongamano la Shirika la Misaada la nchi hiyo (USAid Forum) kuhusu vikwazo vya maendeleo na jinsi ya kutokomeza umasikini uliokithiri, Rasi Kikwete alisema kwamba itikadi iliyoongozwa na kuaminiwa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere imeshindwa kuzaa matunda.

Akieleza kwanini nchi 33 kati ya 48 masikini zaidi duniani zipo Afrika, Rais alieleza kuwa nyingi ya nchi hizo (25) ni wahanga wa migogoro, lakini baadhi kama Tanzania zimekuwa na amani na utulivu lakini zimeendelea kuwa katika kundi hilo, akiamini kuwa ni matokeo ya sera mbovu za kiuchumi katika miongo miwli unusu baada ya uhuru.

"Nchi yangu pendwa Tanzania ni mfano hai wa nchi iliyojaaliwa amani na utulivu tangu ipate uhuru lakini ni moja ya nchi masikini zaidi duniani tangu mwaka 1971wakati mgawanyo wa nchi kutokana na hali yake ya kiuchumi na maendeleo uanze.Licha ya mazingira yasiyo mwafaka kimataifa, sera za  kiuchumi baada ya uhuru ambazo hazikufanikiwa zina mchango mkubwa (katika umasikini wa Tanzania," alisema.

Rasi kikwete aliwaeleza washiriki wa Kongamano hilo akiwamo Makamu wa Rasi wa Benki ya Dunia, Mark Diop, na Mtawala wa USAid Dr Rajiv Shah, kwamba mwelekeo wa kiuchumi ulianza kubadilika baada ya mageuzi ya kiuchumi kuanzia  miaka ya 80.

"Tumebaki katika barabara ya mageuzi tangu wakati huo na tumekuwa na mafanikio mazuri. Nchi yetu sasa inafanya vizuri kiuchumi, na muongo uliopita ulikuwa wa mafanikio zaidi.Kwa ujumla, uchumi ulikuwa kwa wastani wa asilimia 3.5 katika miaka ya 90 hadi wastani wa asilimia 7 katika muongo uliopita," alieleza.

Rais Kikwete, hatahivyo, alikiri kwamba kukua kwa uchumi hakujaendana sawia na kupunguza umasikini. Katika miongo miwili iliyopita, umasikini wa kipato ulipungua kutoka asilimia 39 mwaka 1990 hadi asilimia 28.2 mwaka 2012, ikiwa ni kupungua kwa takriban asilimia 11.

"Hii inaeleza kwanini hatutomudu kufikia kiwango cha Malengo ya Maendeleo ya Milenia (Millenium Development Goals - MDG) ya kupunguza umasikini uliokithiri kwa nusu ya kipimo kilichowekwa mwaka 1990."

"Hata hivyo, tumekuwa na mafanikio katika kupunguza maradufu idadi ya watu wanaoishi chini ya kiwango cha umasikini wa chakula. Punguzo hilo ni kutoka asilimia 21.6 mwaka 1990 hadi asilimia 9.7 mwaka 2012, ikiwa ni kupungua kwa takriban asilimia 12."

CHANZO: Habari hii imetafsiriwa kutoka gazeti la The Citizen

MAONI YANGU: Huko nyuma, Rais Kikwete, kama ilivyo kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda, aliwahi kutamka bayana kuwa hajui kwanini Tanzania ni masikini. Labda hizo safari za mfululizo huku ughaibuni zimempata mwangaza mpya, na sasa anashutumu sera za kiuchumi za Mwalimu Nyerere.

Japo kuna hoja za kitaalum zinazosapoti hoja yake kuhusu mchango wa mapungufu ya sera za kichumi katika umasikini wa Tanzania yetu, alichokwepa kuzungumzia ni mchango wa ufisadi unavyorutubisha kukua kwa umasikini wa nchi yetu. 

Japo baadhi ya wasomi wana mtizamo kama huo wa Kikwete kwamba sera za uchumi za Nyerere zilifeli, na kwamba hata kung'atuka kwake kulitokana na sababu hiyo - huku wengine wakienda mbali zaidi na kudai Nyerere alipaswa kuwaomba msamaha Watanzania baada ya experiement yake ya Ujamaa kufeli - ukweli unabaki kuwa jithada za kurekebisha mapungufu hayo zimekwazwa mno na ufisadi. 

Tanzania yetu imekuwa miongoni mwa mataifa yanayopokea lundo la misaada lakini kwa kiasi kikubwa misaada hiyo imeishia katika kutunisha akaunti za vigogo, sambamba na kuongeza idadi ya mahekalu yao, misururu ya magari yao ya thamani na hata kuongeza idadi ya 'nyumba ndogo' zao.

Kila ukimsikia JK anapozungumzia umasikini wa nchi yetu au kuzorota kwa uchumi wetu, jambo moja la wazi ni kukwepa kwake kutaja rushwa/ufisadi kama moja ya sababu kuu. Pengine nafsi inamsuta kwa vile kila anayefahamu siasa za nchi yetu anatambua mchango wa awamu zake mbili katika kustawisha ufisadi.

Kadhalika, JK amekuwa muumini wa kasumba ya 'kitaalamu' ya kuangalia takwimu kama tarakimu tu na kupuuzia kuwa tarakimu hizo zinamaanisha watu. Ni rahisi kwa Rais wetu kudai kuwa tumepiga hatua zaidi ya ilivyokuwa katika zama za Ujamaa kwa kuangalia takwimu na kupuuzia hali halisi huko mtaani.

Kwa wenye uwezo wa kutafsiri, anachofanya JK kwa sasa ni kujaribu kutengeneza kinachoitwa LEGACY ya utawala wake, kujitenga na ukweli kuwa yeye ni sehemu ya tatizo  - kama ambavyo utitiri wa safari zake huko nje unavyokwangua kipato chetu kiduchu - na kutupia lawama wengine, sambamba na kujaribu kuonyesha kuwa amekuwa akifanya jithada kubwa kuikomboa Tanzania yetu kutoka katika lindi la umasikini. Muda utaongea, na mengi kuhusu utawala wa JK yatazungumzwa baada ya kumaliza miaka yake 10 hapo mwakani. 

14 Oct 2013



Tanganykia President Julius Nyerere








Soma hotuba mbalimbali za Mwalimu HAPA


NANI KAMA NYERERE?

SEHEMU kubwa ya viongozi wakuu wa Serikali ya Awamu ya Nne na zilizopita awamu ya pili na tatu, wakiwamo baadhi ya mawaziri wamekuwa wakitenda kinyume cha hotuba ya kwanza ya Mwalimu Julius Nyerere kwa Baraza la Mawaziri, miaka 50 iliyopita (mwaka 1961), Raia Mwema-toleo maalumu, imebaini.
Tafsiri ya utendaji wa wengi wa mawaziri ni kinyume cha hotuba hiyo ya Nyerere, alipoahidi yeye na viongozi wenzake kutumikia nchi na wananchi, bila kujitafutia faida au fahari ya cheo katika kauli mbiu iliyohimi kujituma ya Uhuru na Kazi.
Katika hotuba yake kwanza kwa Baraza la Mawaziri lenye mawaziri 11 tu, Nyerere aliwaambia mawaziri hao na wazee waliokuwa wakimsikiliza; “Na kwa msaada wa Mwenyezi Mungu, tutajitahidi kuwatumikieni bila kujitafutia faida zetu wenyewe au fahari ya cheo.”
Raia Mwema-toleo maalumu limebaini kuwa katika kipingi hiki cha miaka 50 ya Uhuru wa iliyokuwa Tanganyika, licha ya Nyerere kusimamia kauli hiyo kwa dhati na kutokuwa na ‘suluhu’ katika uamuzi wa kuwashughulikia waliokwenda kinyume na waliokiuka ahadi hiyo, hali imekuwa ni tofauti katika awamu zilizofuatia.
Hali halisi ni kwamba, ingawa wamekuwapo baadhi ya viongozi wenye dhamiri ya dhati kutumikia umma katika awamu hizo, kasoro za wengine, tena waliowengi, zimekuwa zikifunika uadilifu wa wachache mbele ya umma.
Na zaidi ya hapo, kiwango cha kuwavumilia viongozi wanaojitafutia faida binafsi na kulewa fahari ya cheo ni kikubwa na kwa ujumla wamekuwa wakitetewa sana tofauti na Awamu ya Kwanza chini ya Mwalimu Nyerere.
Awamu ya Mwalimu Julius Nyerere
Katika awamu ya kwanza, Nyerere mara kadhaa alikuwa akieleza alivyopewa nchi katika mazingira duni kiuchumi, kielimu na kwamba dawa pekee ilikuwa ni kujitegemea.
Ingawa hali ya uchumi haikuwa nzuri, kasi au mwenendo katika nyanja kama elimu, ulikuwa bora. Elimu iliyotolewa ilikuwa na ubora mkubwa kiasi cha kuwafanya wahitimu wa chuo kikuu nchini kushindana kitaaluma na wahitimu wa chuo chochote duniani.
Si kwamba kila kitu kilikwenda sawasawa, nchi ilishindwa kutatua matatizo ya msingi kwa umma, kwa mfano, ufinyu wa upatikanaji wa huduma za afya, barabara, nishati na bidhaa muhimu kama nguo na chakula wakati mwingine.
Hata hivyo, alifanikiwa katika masuala mawili makubwa. Kuijenga nchi katika umoja na kiwango kikubwa cha uzalendo.
Wananchi walikosa huduma muhimu, wakati mwingine walikabiliwa na njaa lakini kamwe hawakuwa na njaa ya umoja wala uzalendo.
Licha ya matatizo hayo ya msingi katika maisha ya wananchi, Nyerere alipendwa na umma, Baraza lake la Mawaziri liliaminika, hakusika kuchukua hatua kwa yeyote mwenye kudhaniwa tu (si kupeleka ushahidi) kwamba si mwadilifu.
Kwa bahati nzuri au mbaya, nchi iliingia vitani mwaka 1978 dhidi ya Uganda, ikiwa katika umoja na kiwango kikubwa cha uzalendo, lakini ikiwa dhaifu katika nguvu za kiuchumi.
Watu walikuwa bado na imani na Mwalimu Nyerere na Baraza lake la Mawaziri licha ya kutakiwa “kufunga mikanda” kwa miezi 18, yaani uchumi ukipita katika hali ngumu kuwahi kutokea nchini.
Kubwa zaidi ambalo ni kipimo cha uongozi bora ni kwamba, matatizo yote yaliyomgusa raia mmoja mmoja, hayakupoteza imani yao kwa Rais na Serikali yake.
Hapa ndipo viongozi wengine wanapomweka Nyerere katika nafasi ya kung’ara zaidi yao kwa vigezo vya uadilifu na nidhamu katika Baraza lake la Mawaziri.
Kwa namna fulani katika uchumi, Nyerere aliweka misingi ambayo sasa haipo, hiyo ni pamoja na viwanda.
Alhaji Ali Hassan Mwinyi
Katika Serikali ya Awamu ya Pili, chini ya Alhaji Ali Hassan Mwinyi, sambamba na kufungua fursa za kiuchumi na uhuru wa kuanzisha vyombo vya habari kwa manufaa ya wananchi, fursa za kufunga milango ya uadilifu ni kama pia zilipata nafasi.
Kwa lugha nyingine ni kama vile milango ya uchumi iliyokuwa haijafunguliwa na Nyerere, ambaye pia kwa mantiki hiyo hiyo alifungua milango ya uadilifu, nidhamu na uzalendo kwa taifa, kinyume chake, Mwinyi alifungua milango ya uchumi na kufunga milango ya uadilifu iliyofunguliwa na Nyerere.
Mwinyi alifanikiwa tofauti na Mwalimu Nyerere kuchangamsha shughuli za uchumi kwa kuruhusu hata watumishi wa umma kufanya biashara, bidhaa adimu zikiwamo nguo, sabuni na nyinginezo kupatikana kwa wingi, hata hivyo, michakato yote hiyo ilikosa nguvu ya uadilifu kwa wasaidizi wake, wakiwamo mawaziri.
Watumishi wa umma, wakiwamo mawaziri ndiyo waliotumbukia katika biashara. Ofisi za umma ziligeuka vijiwe vya mipango ya biashara hata za magendo, Serikali ya Alhaji Mwinyi ikawa inatajwa  kuwa “imekwenda likizo.”
Ingawa fursa za kibiashara zilifunguliwa, uzembe katika ukusanyaji kodi ulivuka mipaka, Serikali ni kama iliekea kufilisika na nchi wahisani, wakasitisha misaada kutokana na uzembe huo uliokwenda sambamba na kushamiri kwa rushwa kubwa.
Wakati ule wa Alhaji Mwinyi kila kitu kilikuwa ruksa; biashara, magendo, rushwa kubwa, uvivu serikalini na hasa kutokukusanya kodi. Ni hali hiyo iliyombatiza Mzee Mwinyi jina la Mzee Ruksa
Kwa hiyo, Mwinyi alifungua milango ya uchumi na kufunga milango ya uadilifu, uzalendo miongoni mwa viongozi na nidhamu.
Awamu ya Benjamin Mkapa
Akiwa ameingia Ikulu akitabiriwa kufungua mlango wa uadilifu uliofungwa na Mwinyi, Mkapa akaanza vizuri miezi ya awali kwa kuunda Tume ya Rushwa, chini ya aliyekuwa Waziri Mkuu wa Mwinyi, Jaji Joseph Warioba.
Hata hivyo, mapendekezo ya tume hii hayakufanyiwa kazi yote. Wakati Nyerere alifanya utaifishaji, Mkapa akafanya ubinafsishaji. Michakato hii miwili tofauti yake ni kwamba, utaifishaji ulifanyika bila kuandaa watalaamu wazalendo kuendeleza hasa viwanda na maeneo mengine ya uzalishaji yaliyotwaliwa na Serikali.
Yaani Serikali ya Awamu ya Kwanza ilimiliki njia kuu za uchumi, bila kuandaa watalaamu wa kuendesha umikili huo kwa niaba ya umma. Hili ni kosa linalohifadhiwa kihistoria katika uchumi wa Tanzania.
Kwa upade wa ubinafsishaji, wasimamizi wa mchakato huo walishiriki si katika kusimamia kwa niaba ya wananchi, bali ni kama vile walisimamia kwa niaba ya familia, rafiki au wanasiasa wenzao.
Wakubwa wakajitafutia utajiri nao wakageuka wawekezaji ili kutekeleza sera ya uwekezaji waliyoibuni awali. Lakini Mkapa alifanikiwa kurekebisha uchumi wa nchi, kodi ilianza kukusanywa, barabara zikajengwa na hatimaye, wafadhili wakarejesha misaada yao na pia kufuta baadhi ya madeni katika mfumo wa kuzifutia madeni nchi zenye umasikini wa kutupwa Highly Indebted Poor Countries - HIPC).
Ingawa Mkapa aliweka nidhamu ya matumizi ya fedha serikalini, lakini wizi uliendelea humo serikalini kwa viongozi kuonyesha kiwango kikubwa cha kukosa uadilifu ikilinganishwa na Serikali ya Mwalimu Nyerere.
Ufisadi katika mikataba ukaanza (madini), wizi wa fedha za umma katika ununuzi wa kimataifa ukaibuka (ununuzi wa rada ya kijeshi) na hata wizi wa mabilioni Benki Kuu ya Tanzania.
Awamu ya Nne ya Jakaya Kikwete
Ni dhahiri awamu hii ina mazuri na mabaya yake kama zilivyokuwa awamu zilizotangulia. Na pengine kati ya mabaya ambayo hayatasahaulika kwa kirahisi ni kashfa ya kufua umeme ya Richmond iliyosababisha Baraza la Mawaziri kuvunjwa na kuundwa upya mwaka 2008.
Matokeo ya kashfa hiyo ni kushuka kwa uchumi katka miaka iliyofuata kutokana na uamuzi mbaya ambao umesababisha kwa karibu miaka mine sasa nchi kuwa katika matatizo makubwa ya nishati ya umeme, yaliyoshusha uzalishaji viwandani na hata katika biashara ndogondogo za raia wa kawaida wanaotegemea umeme katika kuendesha shughuli zao.
Bado hakuna hatua za dhahiri kwa watuhumiwa wa kashfa kubwa za ufisadi nchini, ikiwamo ya rada, baadhi ya watuhumiwa waliosalia katika sakata la wizi katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA).
Lakini baadhi ya mambo yamesogezwa mbele hayo yakiwa ni pamoja na ongezeko la vyuo vikuu nchini, vikiwamo vya Serikali, achilia mbali shule za kata.
Bado safari ya Kikwete madarakani haijakamilika lakini dhahiri kwa kuwa imekumbwa na matukio ya baadhi ya wanasiasa, akiwamo waziri mkuu na mawaziri kujiuzulu; kashfa ya Katibu Mkuu wa Wizara ya  Nishati na Madini ya uchangishaji fedha, tuhuma kama za uuzwaji nje wa wanayama na kampuni za madini kutokulipa kodi, awamu hii nayo haiwezi kulinganishwa na ya Nyerere kewa maana ya uadilifu.
Ujumbe wa Nyerere kwa mawaziri
Pengine wanasiasa, watawala na watendaji wa sasa wanahitaji kila mara kurejea ujumbe wa Mwalimu Nyerere wa miaka 50 iliyopita,  alioutoa katika Baraza lake la kwanza la Mawaziri.
Nyerere kwa wakati huo akiwa Waziri Mkuu wa kwanza wa Tanganyika alihutubia wazee na mawaziri wake jijini Dar es Salaam akisema; “…mimi na wenzangu, ni watumishi wenu ninyi mnaonisikiliza. Tunajua kuwa mnatuamini, nanyi tunawaamini.
“Na ni ninyi tu mnaotupa nguvu zetu, tunazozihitaji kwa kazi kubwa iliyo mbele yetu. Kwa msaada wa Mwenyezi Mungu, na imani mliyonayo juu yetu, tunapata, na tutazidi kupata nguvu za kuendesha serikali yenu.
Akaendelea; “…mawazo niliyopata kushirikiana nanyi jioni hii. Kwanza, kazi. Kwani ni kazi peke yake itakayotuondolea umasikini wetu. Pili, umoja. Kwani bila umoja, hatuna nguvu ya kuendelea na jambo lolote. Tatu, Undugu. Ili uhuru usilete utengano baina yetu na Waafrika wenzetu au binadamu wenzetu.
“Katika jitihada ya kutimiza shahada hizo, mimi pamoja na wenzangu, tutawatumikieni kwa uwezo wetu wote. Na kwa msaada wa Mwenyezi Mungu, tutajitahidi kuwatumikieni bila kujitafutia faida zetu wenyewe au fahari ya cheo.”
- See more at: http://www.raiamwema.co.tz/nani-kama-mwalimu-nyerere#sthash.jSL7Dcdq.dpuf

14 Oct 2011

14 Oct 2010




Siku kama leo,mwaka 1999 Tanzania ilimpoteza muasisi wa taifa,Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.Kilichowaliza Watanzania wengi ni hofu na mashaka kuhusu hatma ya taifa lao.Pamoja na mapungufu yake ya kibinadamu,Mwalimu alijitahidi kadri awezavyo "kuita koleo ni koleo na sio kijiko kikubwa".Ni katika ujasiri huo wa Mwalimu ndipo alisimama kidete mwaka 1995 kukataa jitihada za Jakaya Kikwete na Edward Lowassa kuingia Ikulu.Miaka 10 baadaye,huku Mwalimu akiwa kaburini,Jakaya Kikwete na swahiba wake Lowassa walifanikiwa kuukwaa uongozi wa Taifa letu.

Bahati nzuri,Mungu hamfichi mnafiki.Japo leo hii Mwalimu ni marehemu na hana namna ya kuwalaumu Watanzania kwa kupuuza ushauri wake kuhusu Kikwete na Lowassa,uamuzi wa wanasiasa hao wawili kupuuza ushauri wa Mwalimu na hatimaye kuwania na kushinda uongozi wa juu wa taifa letu umetusaidia kufahamu kwanini Nyerere aliwapinga in the first place.Bahati nzuri zaidi,Lowassa alikuwa majeruhi wa papara zake,na akalazimika kujiuzulu baada ya kuliingiza taifa kwenye mkenge wa kusaini mkataba na kampuni ya briefcase ya Richmond.Bahati mbaya,na kutokana na Katiba yetu kumlinda rais kupita kiasi,Kikwete alisalimika japo haihitaji utafiti wa kichakachuaji wa Redet au Synovate kutambua kuwa Richmond na mrithi wake Kagoda,kama ilivyo kwa skandali za EPA,Meremeta,Tangold,nk ni ishu zilizokuwa na baraka za mkuu wa nchi,yaani Jakaya Mrisho Kikwete.

Miaka mitano ya utawala wa Kikwete inapaswa kuwafumbua macho kwanini Nyerere hakutaka Kikwete awe rais.Na kama tuna imani na Nyerere hadi leo,basi tutazidi kuonekana watu wa ajabu iwapo tutatoa nafasi nyingine kwa Jakaya kulikongoroa taifa letu.Wasiwasi wa Nyerere kwa Kikwete ulielemea zaidi kwenye aina ya watu waliomzunguka mwanasiasa huyu.Kwa bahati mbaya,Nyerere hakuwa hai mwaka 2005 kushuhudia namna Kikwete alivyotumia kila aina ya hila na hujuma kukwaa urais akisaidia na kila aina ya binadamu huku wengi wao wakiwa ni watu hatari kabisa kwa ustawi wa taifa letu.Watu hao ambao hawana tofauti na kundi hatari la Mafia bado wapo na ndio wanaohangaika huku na kule kuhakikisha 'mlinzi' wao-Kikwete-anarejea tena madarakani kwa vile wanafahamu laiti mzalendo kama Dokta Wilbroad Slaa akiingia Ikulu basi makazi ya mafisadi hao yatakuwa Keko kama sio Segerea...

Tuweke kando siasa za haiba.Tuweke kando tabasamu mwanana la Jakaya Kikwete-tabasamu linalowanufaisha zaidi mafisadi kuliko walalahoi.Tuweke kando hayo maji ya bendera ya CCM waliyokunywa wakereketwa.Tuangalie mwelekeo wa taifa letu.Tujiulize hatma ya taifa hili huku tukitambua kuwa hatuna pa kukimbilia pindi Kikwete na watu wake wakituingiza matatizoni zaidi ya ilivyo sasa.

Kampeni zinazoendelea zimeshashuhudia kila aina ya ufisadi unaofanywa na wafuasi wa Kikwete.Wengi wao hawafanyi uhuni huo kwa vile wanampenda Kikwete bali wanalinda nafasi zao na maslahi yao.Hawako tayari kuona Dokta Slaa anaingia Ikulu kwa vile wanafahamu bayana kuwa "watanyang'anywa mapande makubwa ya keki ya taifa" wanayoyafakamia kwa ulafi mkubwa.

Njia bora ya kumwenzi Baba wa Taifa ni kusema HAPANA kwa ufisadi na mafisadi.Na njia ya kufanya hivyo ni kupiga KURA NYINGI ZA HAPANA KWA KIKWETE na CCM yake.Watanzania wasitegemee miujiza kutoka kwa mtu huyu aliyetuthibitishia bayana kuwa hajui chanzo cha umasikini wa nchi yetu,asiyehitaji kura za Wafanyakazi,anayedhani mimba za wanafunzi wa kike ni kimbelembele chao tu,anayeamini kuwa waathirika wa ukimwi wameukwaa ugonjwa huo kwa kimbelembele chao,na asiyetaka kuomba msamaha kwa wimbo la ufisadi lililoshamiri katika miaka yake mitano ya utawala.

Naamini Baba wa Taifa angekuwa hai leo,angesimama hadharani na kumkataa Kikwete kwa vile sababu zilizopelekea amkatae 1995 sio tu bado zipo bali zimethibitika kwa vitendo kati ya 2005-2010.Uhuru uliopiganiwa na Nyerere na wenzake haukumaanisha uhuru wa mafisadi kama mmiliki wa KAGODA ambaye hadi leo anahifadhiwa na Kikwete na wasaidizi wake.

Ewe Mtanzania,unataka Kikwete na CCM wafanye nini zaidi hadi ufikie hatua ya kusema SASA YATOSHA (Enough is enough)?Kama kosa lilishafanywa 2005 kwa kumpa nafasi ya majaribio na amefeli,hakuna haja ya kumpa fursa ya kurejea tena.Na bahati nzuri safari hii tuna Mtanzania mzalendo (Dokta Slaa) ambaye ujasiri wake kama mbunge umefunika utendaji wa Kikwete,Lowassa,Chenge,Rostam Aziz,Karamagi,Kingunge,Msabaha,Marehemu Ballali,Idris Rashid,Basil Mramba,Yona na wababaishaji wengineo.Katika uchaguzi huu hatuna sababu ya kutojikwamua na makucha ya ufisadi kwa vile tuna alternative iliyo bora ambayo ni Dokta Slaa.

NJIA PEKEE YA KUMWENZI MWALIMU NI KUENZI BUSARA ZAKE ZA KUMKATAA KIKWETE MWAKA 1995.TULIPUUZA BUSARA HIZO MWAKA 2005,PENGINE KWA VILE NYERERE HAKUWEPO KUTUONYA.LAKINI MUNGU AMETUSAIDIA KUTONYESHA BAYANA KWANINI NYERERE ALIMKATAA KIKWETE.KWAHIYO,NJIA MWAFAKA YA KUMWENZI BABA WA TAIFA (NA KUMWOMBA MSAMAHA KWA KUPUUZA USHAURI WAKE WA 1995) NI KUMWONDOA KIKWETE MADARAKANI KWA NJIA YA KURA HAPO OKTOBA 31.KUMWONDOA KIKWETE NDIO NJIA MWAFAKA YA KUONDOKANA NA UFISADI.YEYE NDIO SHINA NA HAO WAPAMBE NI MATAWI TU.TUKIONG'OA SHINA LA UFISADI BASI MMEA MZIMA WA UFISADI UTAKUWA HISTORIA.

INAWEZEKANA.TIMIZA WAJIBU WAKO

16 Oct 2009


NDUGU YANGU Mpayukaji Msemaovyo anasema:

Naitwa Mchumiatumbo mwana wa Tapeli.

Ingawa wakati naandika waraka huu vijana wenzangu wapatao 166 wamo wakimenyeka toka Mwanza hadi Butiama, kama ishara ya kumbukizi ya safari yako adhimu ya ukombozi ukiliungua mkono marehemu azimio la Arusha, mimi sitafanya hivyo.

Nina sababu. Kwanza mimi ni mnafiki wala mjamaa kama wewe. Nina roho nyepesi hasa nionapo vitu kama pesa madaraka na sifa.

Mimi ni mbabaishaji na muongo; au msanii kama washikaji wasemavyo. Ni fisadi through and through. Ninanuka kiasi cha kutostahili hata kukaribia kaburi lako achia mbali nyumba yako, wanao, mkeo, watu wako hata taifa lako. Nisingependa walevi na wazinzi kufagia makaburi ya mitume mwalimu. Hivyo, kwanza nakuwa mkweli kwa nafsi yangu na kwako na umma wako.

Tatu, nitaunga mkono azimio lipi iwapo ninaoona wamenizunguka wakiwaibia watu wako ni wale wale walioliua azimio la Arusha? Nitaadhimisha vipi iwapo miiko ya uongozi na usawa wa binadamu vimetoweka na nafasi yake kuchukuliwa na ufisadi, ujambazi wa mchana, ubabaishaji na uongo?

Nne, mwalimu, sitaki kujidanganya na kukudanganya. Kile ulichopigania kwa sasa hakuna. Ulipigania uhuru na maendeleo. Sasa kuna utumwa na kuporomoka. Ulitekeleza ujamaa na kujitegemea. Sasa tuna uhujumaa na kujimegea. Ulipigania mstakabali wa nchi toka kwa wakoloni wawe wavumbuzi, wamisionari na watawala. Sasa mstakabali huo umo mikononi mwa wawekezaji, na wafadhili wa makuadi wao. Ulipigania ardhi ya Tanzania kabla haijaingia mikononi mwa vijifalme vya kifamilia. Nitakuenzi kwa udhu upi iwapo kila nipitapo Loliondo nakaribishwa kwenye falme za kiarabu utadhani hapa ni uarabuni?

Nitapata wapi mshipa wa kukuenzi wakati nakung’ong’a? Je mwalimu una habari? Yale madini uliyosema vizazi vijavyo vingeyaendeleza na kufaidika nayo yaliuzwa na jamaa yako Tunituni uliyempigia debe usijue jizi.

Tano, mwalimu siwezi kukuenzi wakati nakuchukia na kukudharau. Ningekupenda na kukuheshimu ningeshika urithi wako na kuheshimu wosia wako wa kupendana na kutohujumiana. Nakumbuka wakati ukianga dunia ulikuwa ukiwalilia watanzania wako baada ya kugundua makosa uliyofanya kuwaweka mikononi mwa nunda wala watu. Nami ni mmojawapo.

Je una habari mkoani mwako watu wameishamiminiwa risasi za moto kutokana na kukatiza kwenye ardhi ya mwekezaji na si mtanzania? Una habari mkoani mwako uchafuzi wa mazingira unatishia maisha ya ndugu zako? Hapa kweli nina sababu ya kukuenzi? Je kukuenzi ni matendo au maneno mwalimu?

Ingawa ukiwa kuzimu bado unaliletea sifa taifa langu, sifichi wala kuchelea kukwambia kuwa waliohai wanaliletea aibu na fedheha baada ya kulibinafsisha huku wakibinafsisha hata akili na roho zao. Mwalimu nilikufahamu sana . Ulikaa madarakani kwa kitambo kirefu ukiacha nyuma familia isiyo na ukwasi zaidi ya utu. Uliowawezesha wamefikia hata kuchukua ule mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira uliozawadiwa na rafiki yako Mao Tse Tung.

Mwalimu, vinyamna mwitu na mbwa hawa walitutenda kweli. Walitudanganya kuwa uwekezaji ndiyo sera na njia pekee ya kutukomboa tusijue walikuwa wakimaanisha kinyume. Wengine walituahidi maisha bora kwa wote tusijue wote ni wao washirika zao, watoto zao na wake zao hata nyumba ndogo zao. Tupo msambweni mwalimu wakati huu tunapozidi kuuzana na kuhadaana. Je unaweza kuamini kuwa kwa sasa hakuna tofauti ya polisi na kibaka? Nina ushahidi. Juzi polisi aliuawa kama kibaka na wananchi wenye hasira na kukata tamaa huku polisi tena wakubwa wakiwapiga risasi wafanyabiashara wakidai ni vibaka!

Wakati wa uongozi wako matupinkele au zeruzeru kwa lugha rahisi walikuwa salama. Baada ya kuingia pepo la utajiri usioulizwa ulivyopatikana, maskini hawa wanatolewa kafara na wanganga njaa wa kienyeji. Hivyo ndugu zetu hawa wanauawa hata zaidi ya swala mwalimu na hawana mtetezi zaidi ya vijikesi viwili vitatu vya kuondolea lawama. Tembo kwa sasa wana ulinzi madhubuti zaidi ya ndugu hawa.

Zama zako uliongoza. Uongozi ulikuwa utumishi wa umma na si uchumia tumbo na utumikishaji na uhujumu wa umma. Ikulu ilikuwa mahali patakatifu siyo pa deal. Uongozi ulikuwa uongozi na si uongo kama sasa. Siasa ilikuwa baraka si balaa kama sasa.

Wale watoto wa wachunga mbuzi na maskini wa kunuka uliowatoa kwenye umaskini na kuwasomesha sasa ni matajiri wa kutupwa. Yupo mpumbavu mmoja jizi aliyewahi kuita shilingi bilioni moja vijisenti ukiachia mbali wengine uliowaachia laana kuwa walikuwa wamejilimbikizia chumo la wizi. Na kweli maneno yako hayakuanguka. Kwani wezi wenzao waliwabeba na kuwakweza hatimaye tamaa zao na upofu vikawadondosha.

Mwalimu sitakuenzi,. Siwezi kujidanganya na kuidanganya dunia. Nitakuenzije iwapo kipato changu kinatokana na rushwa, uwekezaji, uuzaji mihadarati, uongo, ahadi hewa, uhujumu na mengine mengi yapinganayo na dhamira ya dira yako mwalimu?

Hivi kweli panya anaweza kumuenzi paka zaidi ya kufaidi ‘uhuru’ baada ya paka kuondoka? Je nune aweza kuishi nje ya kinyesi cha ng’ombe zizini? Si haki nune kuwa mwalimu wa usafi wakati mlo wake na makazi yake ni kwenye uchafu hata anenepe na kunawiri vipi.

Mwalimu naogopa kuja Butiama au kusimama mbele ya kadamnasi ya maadhimisho yako na kukupamba wakati nilisha kuvua nguo. Naogopa. Maana mama Maria hata wanao wananijua. Inawezekana nikakulamba uchogo na kukupaka mafuta kwa mgongo wa chupa kiasi cha kumkera mmojawapo akaamua kunizodoa na nikazidi kudhalilika ingawa niliishadhalilika muda mrefu.

Mwalimu ulikuwa na akili inayochemka. Yangu mimi ni bongolala. Ulikuwa msafi na mwadilifu. Mie ni mchafu sina mfano. Mkeo hakuwa akitumia ofisi yako kuubia umma. Mie wangu nami wote tu wezi. Nikiiba huku yeye anaibia kule. Hata watoto nimewaingiza. Nataka hata ikibidi wawe marais kama siyo mawaziri. Je hapa mwalimu nitakuwa na cha kukuenzi?

Mwalimu ulileta elimu bure kwa wote. Mie nashabikia kuchangia gharama ingawa kimsingi hakuna gharama za kuchangia zaidi ya kutunisha mfuko wa walaji wakubwa. Ulipigania ardhi. Mie natamani niwe rais niiuzie mbali nipate changu nifiche ughaibuni. Mwalimu ulichukia wafanya biashara wezi. Mie hawa ndiyo washitili wangu.

Mwalimu ulisisitiza usawa wa binadamu. Mie naamini binadamu si sawa wala si mfano wa Mungu kama wachungaji wasemavyo. Usawa ni mambo ya kizamani. Kwangu, heshima ya binadamu haitokani na ubinadamu wake bali pochi lake. Hukusikia wahenga wakisema mwalimu kuwa aso kitu si mtu bali kinyama mwitu? Mtu chake bwana. Kwa imani yangu mie si mfano wa Mungu bali mfano wa shetani kutokana na uroho na roho mbaya vyangu. Mungu si mwizi wala muongo wala mbabaishaji kama mimi mwalimu.

14 Oct 2009


Na Fredy Azzah

MAKAMU Mwenyekiti wa CCM, Pius Msekwa, amesema kashfa za ufisadi zinazowakabili baadhi ya viongozi wake, zimekiumbua chama hicho pamoja na serikali yake.

Akiwahutubia wanafunzi wa matawi ya CCM ya vyuo vikuu vilivyopo jijini Dar es Salaam, wakati wa maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 10 ya kifo cha Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere jana, alisema ufisadi ambao umewakumba wengi umesababishwa na tabia ya viongozi kulindana na kutosimamia kikamilifu maadili ya uongozi yaliyoainishwa ndani ya katiba ya CCM.

Alisisitiza kuwa tabia hiyo ni kinyume na misingi ambayo Baba wa Taifa, aliwaachia Watanzania....ENDELEA

WAKATI HUOHUO

WASOMI na wanazuoni nchini, wamesema nchi haina dira na kwamba kuna mpasuko mkubwa ambao usiposhughulikiwa mapema, nchi inaweza kuingia kwenye machafuko.

Wakizungumza juzi katika baraza lililopewa jina la Mbongi, lililoandaliwa na Kigoda cha Taaluma cha Mwalimu Julius Nyerere, walisema mpasuko hiyo ni pamoja na ya udini, ukabila, ukanda, matatizo ya vitambulisho Zanzibar pamoja na hofu ya kuvunjika muungano...ENDELEA

CHANZO: Mwananchi

13 Oct 2009


WAKATI TUNAADHIMISHA KIFO CHA MWASISI WA TAIFA LA TANZANIA,MWALIMU JULIUS KAMBARAGE NYERERE,TUNAPASWA PIA KUTAFAKARI MAMBO KADHAA AMBAYO KWA KIASI KIKUBWA HAYAKUPATA FURSA YA KUJADILIWA WAKATI WA UHAI WA NYERERE,NA KUYAJADILI BAADA YA KIFO CHAKE INAWEZA KUTOA TAFSIRI POTOFU YA UTOVU WA NIDHAMU.

MENGI YAMEONGELEWA KUHUSU MCHANGO WA NYERERE KATIKA HARAKATI ZA UHURU WA TANGANYIKA,NA NDOTO YAKE YA UMOJA ILIYOZAA TAIFA LA TANZANIA KWA KUUNGANA NA ZANZIBAR,PAMOJA NA MCHANGO WA TANZANIA KATIKA MAPAMBANO YA UHURU KUSINI MWA BARA LA AFRIKA.

BAADHI YA MISINGI ALIYOJENGA NYERERE BADO IPO LICHA YA JITIHADA KUBWA ZA "WANAFUNZI WAKE" KUIBOMOA.WATANZANIA BADO TUNASIFIKA KWA NAMNA TUNAVYOTHAMINI UNDUGU WETU (USHAHIDI UKIWA NENO "NDUGU" KABLA YA MAJINA YETU JAPO WAWAKILISHI WETU BUNGENI WANAITWA WAHESHIMIWA).

KAMA KATUNI YA KIPANYA INAVYOONYESHA HAPO JUU,NYERERE PIA ALITUFANYA TUWE WAPOLE KUPITA KIASI.UPOLE HUO ZAMA ZA CHAMA KIMOJA ULIIMARISHWA NA SHERIA ZILIZOTULAZIMISHA KUAMINI KUWA KIONGOZI YUKO SAHIHI WAKATI WOTE.MADHARA YA IMANI HIYO NI HUJUMA INAYOFANYA NA BAADHI YA WANASIASA KUAHIDI MAMBO WASIYOWEZA KUTEKELEZA LAKINI KWA VILE WATANZANIA NI WAPOLE,NA WANAOAMINI KILA ASEMACHO KIONGOZI,WAMEENDELEA KUTUTAWALA NA SI AJABU WAKAENDELEA KUTUTAWALA ZAIDI.WANAFAHAMU KUWA WANAOWATAWALA HAWANA JEURI YA KUHOJI AHADI ZISIZOTEKELEZEKA ACHIULIA MBALI VITENDO VYA UFISADI VINAVYOFANYWA NA WATEULE WA VIONGOZI HAO.

PAMOJA NA HESHIMA YANGU KUBWA NILIYONAYO KWA BABA WA TAIFA,NALAZIMIKA KUMLAUMU KWA UZAZI NA KULEA TABAKA AMBALO LEO HII TUNALIITA MAFISADI.SIAMINI KABISA KUWA BAADHI YA WANAFUNZI WA MWALIMU WALIKURUPUKA GHAFLA KUWA MATAJIRI KUPINDUKIA HUKUN WAKIKUMBATIA WAGENI NA MARAFIKI ZAO.NAAMINI KUWA WATU HAWA HAWAKUWAHI KUWA WAJAMAA JAPO WALIIMBA NA KUCHEZA UJAMAA MAJUKWAANI WAKIWA NA MWALIMU.

TUMWANGALIE MTU KAMA KINGUNGE NGOMBALE MWIRU.HUYU ALIKUWA SWAHIBA WA MWALIMU NA TULIAMBIWA KUWA DINI YAKE NI UJAMAA.HIVI KWELI KINGUNGE AMEBADILIKA GHAFLA KUWA MTETEZI WA MAFISADI AU ALIKUWA ANAMZUGA TU MWALIMU ZAMA ZA UTAWALA WAKE?

BAADHI YA MADUDU TUNAYOSHUHUDIA LEO YALIANZA ZAMA ZA MWALIMU.KULIKUWA NA KIJITABIA CHA MTU AKIHARIBU HAPA ANAHAMISHIWA PALE,KAMA AMBAVYO AKINA MATTAKA WALIVYOSHINDWA KUIOKOA TRC LAKINI WAKAPELEKWA BIMA.SI KWELI KWAMBA NYERERE HAKUENDEKEZA URAFIKI,MAANA ISINGEKUWA HIVYO BASI ASINGEMPIGIA DEBE MKAPA,RAIS AMBAYE BAADA YA KUTOKA IKULU AMEACHA WATANZANIA WENGI WAKISHANGAA KWA NAMNA ALIVYOTUMIA FURSA HIYO KUJITAJIRISHA (REJEA ISHU YA KIWIRA).

BAADHI YA WACHAMBUZI WA SIASA ZA AFRIKA WANAMTUHUMU MWALIMU KUWA WAKATI ANASTAAFU MWAKA 1985 ALIACHA TAIFA LIKIWA KATIKA HALI MBAYA SANA KIUCHUMI.KUNA WANAODAI KWAMBA UAMUZI WA KUNG'ATUKA UNAOPIGIWA MSTARI KAMA MFANO WA KUIGWA ULIKUWA MATOKEO YA KUKWEPA MAJUKUMU.WAPO WANAOKWENDA MBALI ZAIDI NA KUDAI KWAMBA MWALIMU ALIPASWA KUWAOMBA MSAMAHA WATANZANIA KWA KULIFIKISHA TAIFA LILIPOFIKA WAKATI ANASTAAFU.

HATA SIASA YA UJAMAA NAYO IMEZUA MJADALA KWA BAADHI YA WACHAMBUZI WA SIASA.KUNA WANAOONA KUWA NYERERE ALIKUWA MUUMINI PEKEE WA ITIKADI HIYO HUKU AKIWA AMEZUNGUKWA NA KUNDI LENYE BAADHI YA MATAPELI WA KISIASA WALIOKUWA WANAMUUNGA MKONO JAPO NAFSINI MWAO WALIKUWA NA MAWAZO TOFAUTI.NA MFANO UNAOREJEWA MARA NYINGI NI UAMUZI WA KUUA AZIMIO LA ARUSHA MARA BAADA YA MWALIMU KUTOKA MADARAKANI NA KULETA AZIMIO LA ZANZIBAR.

TATIZO JINGINE LA UJAMAA LIKO KWENYE UKWELI KWAMBA ULIKUWA MITHILI YA JARIBIO,AMBALO KWA KIASI KIKUBWA HALIKUFANIKIWA HADI MWALIMU ANAONDOKA MADARAKANI.KUTOKUFANIKIWA HUKO KULICHANGIWA NA NAMNA UJAMAA ULIVYOSAMBAZWA,AMBAPO MATUMIZI YA NGUVU YALIKUWA JAMBO LA KAWAIDA.REJEA NAMNA OPERESHENI VIJIJI VYA UJAMAA ILIVYOWAATHIRI BAADHI YA WATANZANIA KWA KUONDOLEWA MAHALA WALIPOJIJENGA NA KUPAZOWEA NA KUPELEKWA "UGENINI."HOJA HAPA SI KWAMBA WAZO LA UJAMAA LILIKUWA ZURI AU BAYA BALI KAMA LILIKUWA LINATEKELEZEKA HASA IKIZINGATIWA KWAMBA TANZANIA ILIKUWA TEGEMEZI KIUCHUMI TANGU ILIPOPATA UHURU WAKE 1961.

KUDHANI KWAMBA MAFISADI WALIIBUKA GHAFLA NI KUKWEPA KUDADISI CHANZO CHA TATIZO.MAFISADI WENGI NI TABAKA LILILOIBUKA MIAKA YA MWISHO WA HARAKATI ZA UHURU NA BAADA YA KUPATIKANA UHURU.NI KIKUNDI CHA WARASIMU WALIOTUELEKEZA NAMNA YA KUFANYA JAPO WAO WENYEWE HAWAKUFANYA HIVYO.TABAKA HILI LILIKUWA LINASUBIRI MWALIMU AONDOKE MADARAKANI LIANZE "KUFANYA VITU VYAKE",AND SURE THEY DID!

NYERERE ALIZUNGUKWA NA LUNDO LA WANAFIKI.KISICHO NA HAKIKA NI KAMA ALIFAHAMU UNAFIKI WAO NA KUWAVUMILIA AU WALIMZIDI AKILI.YOTE MAWILI HAYAMTOI LAWAMANI KWA VILE PINDI KIONGOZI ANAPOCHAGUA WASAIDIZI WENYE MAPUNGUFU,AIDHA KWA KUTOJUA AU KWA MAKUSUDI,NI LAZIMA ABEBE LAWAMA KWA UTEUZI MBOVU.

UJAMAA,REGARDLESS YA KUWA ITIKADI YA MAJARIBIO,UNGEWEZA KUZAA MATUNDA MEMA IWAPO UNGEGUSA KILA MTANZANIA PASIPO KUJALI NAFASI YAKE KATIKA JAMII.NI DHAHIRI KUWA LAITI HILO LINGETIMIA BASI TUSINGESHUHUDIA AWAMU YA PILI (BAADA YA NYERERE) IKIENDESHA TAIFA KWA MTINDO WA LAISSEZ FAIRE (BORA LIENDE) NA AWAMU YA TATU IKITUAMINISHA UJIO WA ZAMA ZA UWAZI NA UKWELI HUKU WATU WANAUZIANA MGODI WA KIWIRA KWA BEI YA KISHKAJI.YA UFISADI KILA MMOJA WETU ANAFAHAMU HALI ILIVYO.

KWA VILE MIE NI MKRISTO,NA KWA VILE MILA ZETU ZINAKATAZA KUWASEMA VIBAYA MAREHEMU,BASI NAUNGANA NA WATANZANIA WENZANGU KUMTAKIA MWALIMU PUMZIKO LA MILELE NA MWANGA WA MILELE,APUMZIKE KWA AMANI,AMINA.HATA HIVYO,KAMA SIE WAKATOLIKI TUNAVYOAMINI KUWA ROHO ZA MAREHEMU ZIKO "HAI" TUKIZIKUMBUKA KWA SALA,BILA SHAKA MWALIMU ANAJUTA KUCHAGUA "MARAFIKI" AMBAO BAADA YA KUONDOKA KWAKE WAMEGEUZA TANZANIA KUWA SHMBA LA BIBI,WANACHUMA WATAKAVYO,WANAKWIBA WATAKAVYO,LAKINI KWA VILE ALITUGEYUZA WAPOLE NA WAGUMU KUDAI HAKI ZETU,TUNAENDELEA KUVUMILIA MACHUNGU.

MWISHO,KWA VILE LAWAMA PEKEE HAZIWEZI KUSAIDIA KUTUFIKISHA TUENDAKO,JUST LIKE MAKALA NDEFU ZA KUMBUKUMBU YA MWALIMU ZISIVYOWEZA KUWAKWAMUA WALALAHOI,NI MUHIMU KUITUMIA SIKU HII KUJIULIZA SWALI HILI MUHIMU.JE NYERERE NA WAPIGANIA UHURU WENZAKE WALIPAMBANA NA MKOLONI KWA MINAJILI YA KUMUONDOA MTU MWEUPE NA KUMUWEKA MKOLONI MWEUSI (MAFISADI,et al)?

ANGALAU MKOLONI ALIKUWA NA EXCUSE YA KUTUNYONYA NA KUTUPELEKESHA.HAKUWA MTANZANIA,HAKUWA NA UCHUNGU NA NCHI HII,NA HAKUFIKISHWA ALIPOFIKIA KWA JITIHADA ZA WATANZANIA.LAKINI MAFISADI NI WATANZANIA WENZETU,WANALAZIMIKA KUWA NA UCHUNGU NA NCHI YETU KWA VILE KWA VYOVYOTE VILE BAADHI YA WAATHIRIKA WA UFISADI WAO NI NDUGU ZAO WA MBALI (WA KARIBU WAMESHATENGENEZEWA ULAJI SOMEWHERE).

NJIA BORA YA KUMUENZI MWALIMU NI KUREKEBISHA PALE ALIPOKOSEA (KWA MFANO KUWALEA VIONGOZI WALIOMZUGA KUWA NI WAJAMAA LAKINI WAKAGEUKA MAFISADI MARA BAADA YA KUONDOKA KWAKE) NA KUIANGALIA TANZANIA KAMA NCHI YETU SOTE NA SI YA WATEULE WACHACHE (AMBAO MARA NYINGI HAWATAKI KUSIKIA SAUTI TOFAUTI NA YAO UNLESS IWE NI VIGEREGERE AU MAKOFI YA PONGEZI).TUMUENZI MWALIMU KWA KUKATAA NCHI YETU KUWA SHAMBA LA BIBI HUKU WAWEKEZAJI UCHWARA WAKIJA NA BRIEF CASES TUPU NA KUONDOKA WAKIWA MAMILIONEA.TUKATAE WEZI KAMA WA KAMPUNI YA KAGODA NA MATAPELI KAMA WA RICHMOND,NA UJAMBAZI KAMA WA MEREMETA,TANGOLD,NK KUENDELEA HUKU WAHUSIKA WAKITUPUUZA KWA KUGOMA KUTUELEZA UKWELI.


5 Oct 2009


KWANGU,MISINGI MIKUU YA NYERERE ILIKUWA UJENZI WA JAMII YENYE USAWA NA INAYOTHAMINI UTU WA BINADAMU.UHURU BILA USAWA NI POROJO.UMOJA KATIKA LINDI LA UMASIKINI NI SAWA NA USINGIZI WA PONO KWENYE UTANDO WA BUIBUI.NA MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA HAYAWEZI KUPATIKANA KATIKA SIASA ZA KUKUMBATIA MAFISADI SAMBAMBA KUKEMEA WAPAMBANAO NA UFISADI,KUTOJUA VIPAUMBELE VYA NCHI,NA KUENDELEZA AHADI ZA MAENDELEO ILHALI ZILE ZA AWALI HAZIJATEKELEZWA.

JK AMEKUMBUKA MISINGI YA MWALIMU.MSOME KATIKA HABARI IFUATAYO:

Mwandishi Maalum, Mwanza

RAIS Jakaya Kikwete ametaja misingi mikuu mitatu iliyowekwa na Baba wa Taifa, Hayati Julius Nyerere katika kulijenga taifa la Tanzania, misingi ambayo rais alisema ni kumbukumbu yao kuu kwa kiongozi huyo wa harakati za Uhuru wa Tanganyika.

Rais Kikwete aliwashangaa Watanzania ambao wanabeza Uhuru wa Tanzania na kufurahia wakati jina la Tanzania linaposhambuliwa na wageni.

Aliitaja misingi hiyo mikuu kuwa ni uhuru, umoja wa taifa la Tanzania, na safari ya kujenga maisha bora kwa kila Mtanzania iliyoanza hata kabla ya Tanganyika kupata uhuru wake rasmi Desemba 9, 1961.

Rais Kikwete alisema hayo mjini Mwanza juzi alipozungumza na vijana wa CCM ambao wanaanza safari ya kuelekea kijijini Butiama mkoani Mara, ikiwa ni matembezi ya kumuezi Mwalimu Nyerere ambaye alifariki miaka 10 iliyopita baada ya kuugua saratani ya damu.

Mwalimu Nyerere alifariki Oktoba 14, 1999 akiwa amelazwa hospitali ya St Thomas jijini London, Uingereza.

Vijana 166 kutoka mikoa yote ya Tanzania wanashiriki katika matembezi hayo ya siku 10 ambayo yatapitia njia ambayo Mwalimu Nyerere alitembea mwaka 1967 katika kuunga mkono na kuhamasisha Azimio la Arusha.

Kauli mbiu ya matembezi hayo ni “Uhuru na Kazi” na miongoni mwa mambo ambayo vijana hao watafanya njiani ni kukarabati Shule ya Msingi ya Mwisenge ambako Mwalimu Nyerere alipata elimu yake ya msingi.

Rais Kikwete alisema kuwa urithi mkuu ambao Mwalimu aliwaachia Watanzania ni misingi hiyo mikuu ambayo imeendelea kulifanya Taifa la Tanzania kuwapo na kuwa imara.

Rais Kikwete alisema kuwa kila taifa duniani lina waasisi wake ambao wanastahili kuendelea kukumbukwa siyo tu kwa uasisi pekee, bali pia kwa mambo ambayo waliyasimamia, waliyaamini na waliyajenga.

"Wamarekani wanaye George Washington… sisi tunaye Mwalimu Julius Kambarage Nyerere… na kila nchi ina muasisi wake ambaye anakumbukwa kwa aliyoyasimamia," alisema JK.

"La kwanza la kumkumbuka Mwalimu ni uhuru wa nchi yetu. Huyu alikuwa ni kiongozi aliyeambiwa achague kati ya siasa ama kazi ya ualimu… huyu mzee wetu akachagua siasa na utumishi wa umma bila hata kujua atakula nini.

"Akachagua kupigania uhuru wa nchi yetu. Kama mnavyojua nyote hii kazi ya siasa ni kamari... unakwenda kugombea ukijua kuna kupata ama kukosa... lakini yeye alifanya uamuzi sahihi wa kupigania uhuru,"

Rais Kikwete alisema kuwa uhuru siyo mipaka bali ni heshima ya nchi na ndiyo maana Tanzania haitasita kumkabili yoyote ambaye atajaribu kuchezea uhuru huo.

Alisisitiza: "Mwaka 1978 yule msanii na profesa wa historia na jiografia, Idi Amin alivamia nchi yetu… na sisi tukamfurumusha ili kulinda uhuru wetu na wako wenzetu ambao walipoteza maisha yao kwa ajili ya kulinda uhuru wetu. Wamelala Kaboya (mkoani Kagera) na tutaendelea kuwaenzi kwa sababu walijitolea kulinda uhuru wetu."

Rais Kikwete pia aliwashangaa watu wote ambao wanafurahia wakati heshima ya Tanzania inapobezwa na wageni.

"Uhuru siyo mipaka kama nilivyosema. Uhuru ni heshima ya taifa letu. Wako wale wenzetu wanaofurahi wakati wageni wanaposhambulia nchi yetu. Ni wajibu wetu sote kuhakikisha kuwa uhuru wetu hauchezewi na mtu yoyote,"alisema.

Kuhusu umoja wa taifa, Rais Kikwete alisema Mwalimu alihakikisha kuwa uhuru wa nchi unazaa umoja ili nchi iwe moja na isigawanyike vipande vipande kwa sababu yoyote ile.

"Aliondoa viashiria vyote vya kuvunja umoja wa taifa tokea mwanzo kabisa. Aliondoa uchifu ili kuondoa nguvu za ukabila. Alitambua hatari ya dini na akataifisha shule zote za dini ili vijana wetu waelimishwe na kulelewa kama vijana wa taifa moja na siyo vijana wa dini tofauti,"alisema Kikwete.

Rais Kikwete alisema kuwa hata kabla ya uhuru, Mwalimu alitambua kuwa ili uhuru na umoja viweze kudumishwa ni lazima wananchi wake wapate maisha bora na ndiyo maana akawatambua maadui wakuu watatu – ujinga, maradhi na umasikini- na njia za kukabiliana na maadui hao.

CHANZO:
Mwananchi

BAADHI WANAHOJI KUHUSU MANTIKI YA UHURU ALIOPIGANIA BABA WA TAIFA NA WENZAKE.TULIMKIMBIZA MKOLONI ILI TUJITAWALE NA KUFAIDI RASLIMALI ZETU KWA HAKI NA USAWA.JAPO SIO EXCUSE,LAKINI MKOLONI HAKUTUJALI KWA VILE HAKUWA MTANZANIA.LEO HII WANAOTUTENDA VIBAYA ZAIDI YA WAKOLONI NI WATANZANIA WENZETU,WENGI WAO WAKIWA WALIOSOMOSHWA KWA SHIDA NA FEDHA ZA WATANZANIA WENZAO.KUNDI JINGINE NI LA MABWANYENYE WALIOPTA URAIA KWA VIJISENTI VYAO NA WAKOLONI -MAMBOLEO WALIOREJEA KWA JINA LA WAWEKEZAJI.NYERERE HAKUPIGANIA UHURU ILI WAGENI WAJE NA DOLA MOJA NA KUONDOKA NA MAMILIONI YA DOLA,AU AKINA LOWASSA KUTUINGIZA MKENGE KWENYE RICHMOND,NA USANII MWINGINE WA KISIASA.

UHURU PASIPO UONGOZI BORA NI SAWA NA KUWA NA VOGUE LENYE DEREVA MLEVI AU KIPOFU;LITATUMBUKIA MTARONI KAMA SI KUPORWA NA MAJAMBAZI.UHURU ILHALI TUMEBANWA NA NIRA ZA MAFISADI NI UTANI MBAYA KWA WALIOPIGANIA UHURU WA NCHI YETU.WEZI WA KAGODA WAMEHIFADHIWA HADI LEO,MASHIRIKA YA UMMA YAMEGEUKA KICHAKA CHA WATU KUHUJUMU KISHA WABADILISHIWE (REJEA MATTAKA NA ATCL),WAZEMBE WANAENDELEA KULINDWA KWA VILE TU KUWABADILISHA KTATHIBITISHA MAPUNGUFU YA ALIYEWATEUA IN THE FIRST PLACE,NA HADITHI NYINGINE ZA KUSIKITISHA.

HATUKUPIGANIA UHURU KUPATA HESHIMA FEKI MACHONI MWA JUMUIYA YA KIMATAIFA BALI AMANI NAFSINI NA MIILINI MWETU KAMA WATANZANIA.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.