Showing posts with label AZIMIO LA ARUSHA. Show all posts
Showing posts with label AZIMIO LA ARUSHA. Show all posts

11 Feb 2008

Uongozi wa kisiasa wa Tanzania,kama ilivyo sehemu mbalimbali duniani,umekuwa ukitegemea watu kutoka fani mbalimbali za maisha.Tuna viongozi wa dini (kama Mchungaji Lwakatware),Wasomi (kama Prof Mwandosya,Prof Msola,Prof Mwakyusa),wanajeshi (kama Kapteni John Komba,Kapteni Jaka Mwambi,Luteni Yusufu Makamba) na hata wasanii kama Khadija Kopa .Hivi karibuni,JK alielezea kutoridhishwa kwake na athari zinazoweza kutokana na kuwa na viongozi ambao pia ni wafanyabisahara.Ana hoja ya msingi hapo,lakini nadhani tatizo la msingi sio fani aliyotoka au anayoendela nayo kiongozi husika bali ni utashi alionao katika kuwahudumia Watanzania wenzake.Kadhalika,mkanganyiko uliopo kwenye kanuni za maadili ya uongozi ziko shaghala baghala,hasa baada ya kuuawa kwa Azimio la Arusha na kuzaliwa Azimio la Zanzibar.Endelea na makala yangu hii kwenye gazeti la Mtanzania.
MTANZANIA UGHAIBUNI-

Watanzania wengi wameipokea kwa furaha kauli ya Rais Jakaya Kikwete kuhusu umuhimu wa kutenganisha biashara na utumishi wa umma.Ni kauli mwafaka kwani hata katika Maandiko Mtakatifu tunafundishwa kwamba ni vigumu kutumikia mabwana wawili.

Naamini kwa mtazamo wa wengi,wafanyabiashara kama Watanzania wengine wana kila haki ya kushiriki katika shughuli za siasa ikiwa ni pamoja na kugombea ubunge au hata kuteuliwa mawaziri.Tatizo linakuja pale maslahi ya biashara zao yanapoingiliana na utekelezaji wa majukumu yao katika kuuhudumia umma.

Inaweza kuwa sio sahihi kuwalaumu wafanyabisahara wanaochanganya biashara na siasa pale ilhali hakuna miongozo maalumu (kama ya Marekani na Uingereza).Ndio maana wazo la kufanyika mchakato wa kuleta sheria na kanuni zitakazoweka bayana mazingira ambayo kwa upande mmoja hayatawanyima nafasi wafanyabiashara kushiriki kwenye siasa,na upande mwingine biashara zao kutoathiri majukumu waliyokabidhiwa na taifa,lina umuhimu mkubwa.

Pamoja na pongezi hizo ni muhimu kuangalia chanzo cha tatizo lililopo hivi sasa.Ni ukweli usiopingika kwamba wakati wanasiasa wengi wameendelea kuhubiri kwamba siasa ya Ujamaa na Kujitegemea bado ni mhimili wa taifa letu,hali halisi tuliyo nayo sasa inapingana kabisa na matamshi hayo.

Azimio la Arusha lilisaidia kuweka wazi mwelekeo wa taifa letu.Makala moja kama hii haiwezi kutosha kuelezea undani wa Azimio hilo lakini kilicho wazi ni kwamba Baba wa Taifa,ambaye kimsingi ndiye anayekubalika kama mwasisi wa itikadi hiyo,alikuwa na ndoto ya kuona jamii ya Watanzania inayoishi kwa usawa na haki.

Baadaye likaja Azimio la Zanzibar.Pengine mie ni mzembe wa kujua kilichomo katika Azimio hilo lakini naamini kwamba kuna Watanzania wengi ambao hadi leo hawajui kilichomo kwenye Azimio hilo.Labda ni kutokana na ufahamu mdogo uliopo miongoni mwa wananchi wengi kuhusu Azimio la Zanzibar ndio maana wengi wetu tunarahisisha majibu kwamba lilikuwa tamko rasmi la kifo cha Azimio la Arusha.Na katika hili,CCM inastahili kubeba lawama zote kwani haijafanya jitihada zozote za makusudi kuuelewesha umma kuhusu madhumuni na kulichomo kwenye Azimio hilo (la Zanzibar).

Kuna mapungufu makubwa katika suala zima la uwazi pindi yanapojiri masuala nyeti kwa taifa letu.Mfano mzuri ni kwamba wengi wetu tulikuwa hatufahamu kwamba hadi uteuzi wake unatenguliwa na Rais,aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu aliyeondolewa madarakani,Dkt Daudi Ballali,hakuwa mtumishi wa serikali.Pengine taratibu zinasema hivyo lakini kwa vile mtu anayekalia nafasi hiyo ndiye mwenye kushika dhamana ya fedha za Watanzania wote,nadhani kulikuwa na kila sababu ya wenye fedha zao (Watanzania) kufahamishwa kuhusu hilo badala ya kusubiri mpaka litokee tatizo la ufisadi kwenye taasisi hiyo muhimu kwa taifa.

Hadi muda huu,ukiwauliza viongozi wa CCM kwamba je Azimio la Arusha bado ni mwongozo muhimu kwa maendeleo na mwelekeo wa taifa,sanasana utachoambulia ni hadithi ndefu zisizotosha kutoa jibu moja la kueleweka.Ni dhahiri muuliza swali atakumbana na ugumu wa aina hiyohiyo pindi akiuliza iwapo nchi yetu bado inafuata siasa ya Ujamaa na Kujitegemea.Na haiishii hapo kwani majibu yataendelea kuwa tete pindi mtu akiuliza iwapo CCM bado ni chama cha wakulima na wafanyakazi.

Na ni katika hilo la wakulima na wafanyakazi ndipo napoona kuna tatizo la msingi.Inasemekana Azimio la Zanzibar lilihalalisha watumishi wa umma (wafanyakazi) kumiliki mali kinyume na katazo lililowekwa na Azimio la Arusha.Laiti wakati wanasiasa wetu walipokutana Zanzibar kuua Azimio la Arusha wangeangalia mbali,ni dhahiri wangebaini uwezekano wa kutokea mgongano kati ya biashara na utumishi wa umma.Haraka ya kupitishwa Azimio hilo inaweza kuwa sababu muhimu ya wanasiasa hao kutoangalia mbali.Lakini pia haraka hiyo inaweza kuwa ilichochewa na ukweli kwamba wakati wanasiasa wengi walikuwa wakituimbia ngonjera za Ujamaa na Kujitegemea majukwaani,majumbani mwao walikuwa wakicheza ngoma za ubepari.

Dhana hapo ni kwamba Azimio la Zanzibar lilipitishwa chapchap ili wajamaa wa hadharani waliokuwa mabepari wa kificho waweze kuendesha maisha yao bila hofu na bughudha ya kuonekana wanatenda kinyume na imani ya taifa letu kwa wakati huo.Hawa ni pamoja na wale ambao walikuwa wakituaminisha kwamba ni watu wa karibu na Baba wa Taifa kumbe moyoni walikuwa wakiomba dua Mwalimu aondoke madarakani ili watumie vile walivyokuwa wakikusanya kwa kificho katika zama hizo za Ujamaa na Kujitegemea.Na wengine japo Mwalimu aliwasaidia kuwaingiza madarakani akidhani ni waumini wa siasa zake,wamestaafu wakiacha skandali lukuki.

Kama kuna madhara mabaya zaidi ya mfumo wa chama kimoja basi ni kule kutoruhusu mawazo tofauti na ya watawala,hata kama mawazo hayo ni ya kuchochea maendeleo ya taifa.Kinadharia kila Mtanzania ana uhuru wa kutoa mawazo yake alimradi asivunje sheria halali za nchi,lakini kiuhalisia bado kuna chembechembe zilizorithiwa kutoka katika mfumo wa chama kimoja ambapo mawazo tofauti ni sawa na uhaini.

Katika zama za chama kimoja,hoja kama ile ya “chama kushika hatamu” zilisaidia baadhi ya mafisadi wa wakati huo kupata kinga dhidi ya wale maovu yao.Sote tulikuwa ni Watanzania tusio na tofauti,tunaoamini kwamba ili nchi yetu iendelee tunahitaji ardhi,watu,siasa safi na uongozi bora.Mwalimu aliamini kuwa hiyo ni njia sahihi ya maendeleo kwani alishuhudia namna ilivyofanikiwa sehemu kama China na Cuba.Kosa lake ni kuamini kwamba walio karibu yake walikuwa na imani ya dhati kama yeye.Angalau leo tunawajuwa wanafiki hawa,lakini kwa sababu za “kulinda umoja wa kitaifa” na kutaka “wapumzike kwa amani” tunaendelea kuwaheshimu kwa kutowaumbua hadharani.

Kumkosoa mzazi ni kosa,na kwa mwananchi wa kawaida au hata kiongozi kumkosoa Rais inaweza kutafsiriwa kuwa ni utovu wa nidhamu.Hata hivyo,kutoa ushauri kwa heshima na taadhima ni jambo linalokubalika.Ni kwa kuzingatia hilo ndio maana naamini kwamba wakati Watanzania wengi wanakubaliana na mtizamo wa Rais Kikwete kuhusu kutenganisha siasa na biashara,ni vema katika utekelezaji wa dhamira yake hiyo akaweka maanani namna Baba wa Taifa alivyosalitiwa na baadhi ya watu wake wa karibu.

Nasema hivyo kwa sababu naamini hata zikiwekwa sheria nzuri namna gani za maadili ya uongozi,pasipo kutengeneza mazingira yatakayozuia wasimamizi wa sheria hizo kuzihujumu,itakuwa ni kazi bure.Mwanasiasa anaweza kabisa kutangaza kwamba biashara zake za awali zimekabidhiwa kwa wadhamini flani,lakini pasipo usimamizi mzuri mfanyabiashara huyo anaweza kuendelea kuendesha biashara zake huku akiwa mwanasiasa japo machoni mwa umma anaonekana ametekeleza sheria hiyo tarajiwa ya kutenganisha biashara na siasa.

Mfano mzuri wa ninachosema ni hili sakata linaloendelea la fedha za EPA huko Benki Kuu.Yayumkinika kubashiri kwamba kama itafikia hatua ya watu flani kupelekwa mbele ya vyombo vya sheria,kuna uwezekano watu hao wakawa ni wamiliki “hewa” ambao majina yao yalitumika tu kuficha wamiliki halali.Katika mazingira ambapo taasisi kama TAKUKURU ilikuwa ya kwanza kudai mradi wa Richmond haukuwa na harufu ya rushwa ilhali sasa tunaona suala hilo likiwaka moto huko bungeni,tutarajie nini pindi wakipewa jukumu la kuhakikisha mfanyabishara anayetaka kuingia kwenye siasa kweli amekabidhi biashara yake kwa wadhamini kama sheria itakavyokuwa inataka?

Mwisho,kikao kinachoendelea cha bunge kimeonyesha dalili kwamba baadhi ya wawakilishi wetu wamechoka kupiga mihuri kupitishwa miswada inayoonekana mizuri machoni lakini inaishia kwa mashirika kama ATC kununua ndege mbovu,TANESCO kujikuta hohehahe kwa kulipa madeni yaliyosababishwa na walafi flani wasio na uchungu na taifa au kuletewa umeme hewa ulioahidiwa na makampuni ya kisanii.Hoja hapa sio kuitupilia mbali miswada ya manufaa kwa taifa au kuchochea upinzani dhidi ya serikali bali kuwabana mafisadi wote wananaotumia nyadhifa zao kulikamua taifa letu.
BAADA YA POLITIKI ZA BONGO,HEBU ANGALIA HIZI ZA NAS KUHUSU THE N-WORD


24 Jan 2008

Siku chache zilizopita Wamarekani waliadhimisha siku ya Dakta Martin Luther King Jr,mmoja wa wapigania haki za Waamerika Weusi.Historia inamkumbuka Dkt King (aliyezaliwa mwaka 1929 na kuuawa kwa risasi mwaka 1968)kama nguzo muhimu katika kupigania haki za Waamerika Weusi nchini humo.Pengine kilichomfanya wanaharakati huyo akubalike zaidi ni imani yake ya kudai haki kwa njia za amani.

Miaka mitano kabla ya kuuawa,mwaka 1963,Dkt King alitoa hotuba ambayo hadi leo imeendelea kuwa na mvuto mkubwa sio nchini Marekani pekee bali pia sehemu mbalimbali duniani katika mapambano ya kudai usawa.Katika hotuba hiyo iliyopewa jina “I Have a Dream” (“Nina Ndoto”,kwa tafsiri isiyo rasmi),Dkt King alieleza matamanio yake kuona Waamerika Weusi na Weupe wakiishi pamoja kwa amani na usawa.Hotuba hiyo iliyotolewa mbele ya watu zaidi ya laki mbili,inakubalika miongoni mwa wengi kama moja ya hotuba za muhimu kabisa katika historia ya Marekani.Mwaka 1999,hotuba hiyo ilichaguliwa na wasomi kuwa ni hotuba bora kabisa za karne ya 20.

Miongoni mwa nukuu muhimu katika hotuba hiyo ni pamoja na (kwa tafsiri yangu isiyo rasmi) “…nina ndoto kwamba siku moja taifa hili litasimama na kuishi kama inavyotamkwa kwenye imani yake….nina ndoto kwamba siku moja watoto wangu wanne wataishi katika taifa ambalo hawatahukumiwa kutokana na rangi ya ngozi zao bali tabia/utu wao….nina ndoto kwamba siku moja watoto wa waliokuwa watumwa na watoto wa waliokuwa wamiliki watumwa watakaa pamoja katika meza ya undugu…”

Msukumo uliotokana na uongozi wa harakati za Dkt King ulisaidia sana kubadili historia ya Marekani hususan usawa kwa (Wamarekani) Weusi, na kupelekea mabadiliko mbalimbali dhidi ya sheria za kibaguzi.Miongoni mwa sheria hizo ni pamoja na “Civil Rights Act” ya mwaka 1964 iliyoharamisha ubaguzi kwenye sehemu mbalimbali katika jamii.Mwaka uliofuata, “Voting Rights Act” ilipitishwa na kufuta kipengere kilicholazimisha wapiga kura watarajiwa kufanya testi za kupima uwezo wa kusoma na kuandika (wengi wa waathirika wa kipengere hicho walikuwa Wamarekani Weusi ambao walikuwa na maendeleo duni kielimu kutokana na kubaguliwa).

Maadhimisho ya siku ya Dkt King yamekuwa yakitoa changamoto nzuri kwa jamii ya Wamarekani kutafakari mahusiano kati ya Weupe na Weusi.Wengi hujiuliza iwapo ndoto za Dkt King zimetimia kweli,zinaelekea kutimia au hazina dalili ya kutimia kabisa.Ni maswali magumu ambayo yanahitaji uchambuzi wa kina kuyajibu,na pengine hata kwa uchambuzi wa kina bado inaweza kuwa vigumu kupata jawabu moja linalokubalika.Kingine kinacholeta ugumu wa kupata jawabu ni tofauti ya vizazi.Kwa walioishi nyakati za ubaguzi wa rangi na kushuhudia harakati za Dkt King wanaweza kuwa na mtizamo tofauti kuhusu kutimia kwa ndoto za mwanaharakati huyo ukilinganisha na kizazi cha hivi karibuni ambacho kinamwelewa Dkt King kupitia kumbukumbu za historia tu.

Hata hivyo ni rahisi kukubaliana kwamba harakati za Dkt King na wenzie zimesaidia kuleta mabadiliko makubwa ikiwa ni pamoja na hayo ya kisheria niliyotaja awali.Wapo wanaokwenda mbali zaidi na kutoa mifano ya mafanikio ya Waamerika Weusi maarufu kama Jenerali Colin Powell na Condoleeza Rice ambao wameshika nafasi nyeti katika uongozi wa taifa hilo.Lakini mfano mzuri zaidi ni Barack Obama,seneta Mweusi anayewania kuteuliwa kugombea urais wa nchi hiyo kupitia chama cha Democrats.Akiteuliwa kuwa mgombea,ataweka historia ya pekee nchini humo,na akifanikiwa kushinda urais basi hiyo itakuwa zaidi ya kuweka historia (tuite kuandika historia upya).Hata kama atashindwa,mafaniko aliyokwishafikia hadi sasa ni hatua muhimu katika kutimia kwa ndoto za Dkt King.

Afrika nayo imetoa akina Dkt King kadhaa,na kwetu Tanzania tunajivunia Baba wa Taifa marehemu Julius Nyerere ambaye (kama Dkt King) alikuwa na ndoto zake kadhaa ambazo kimsingi zilihusu kuwa jamii yenye usawa.Ndoto za Mwalimu zilivuka mipaka ya Tanzania kuhakikisha kuwa Afrika yote inakuwa huru.Mchango wa Mwalimu katika mapambano ya ukombozi kusini mwa Afrika utaendelea kukumbukwa milele.Na pengine hapo ndipo baadhi yetu tunagundua mabadiliko ya vizazi yanavyochangia kusahaulisha historia.

Mara nyingi napokutana na vijana Waafrika wenzangu (wanaoishi hapa Uingereza) kutoka nchi kama Zimbabwe,Zambia,Angola,Msumbiji,Afrika Kusini,Namibia na Uganda,nabaini kwamba wengi wao aidha wamesahau au wanapuuza mchango wetu katika ukombozi wa nchi zao (kwa Uganda ni kumng’oa Nduli Idi Amini).Angalau Wazimbabwe wanaweza kuwa na kisingizio kwamba kutokana na ubabe wa Mugabe,baadhi yao wanaweza kutoona faida ya kumkimbiza mkoloni na kujipatia uhuru.

Lakini pengine si busara sana kuwalaumu wanaopuuza mchango wa Mwalimu na Tanzania kwa ujumla katika ukombozi wa nchi zao kwani inawezekana kabisa wanafuatilia kinachoendelea nchini mwetu na kugundua kwamba baadhi yetu tumetupilia mbali kabisa jitihada za Baba wa Taifa kuhakikisha tunajenga jamii yenye usawa.Kwa vile dunia ni kama kijiji,katika zama hizi za utandawazi,majirani zetu hao watakuwa wanasoma na kusikia habari kuhusu ufisadi nchi mwetu,na pengine kubaki wanajiuliza “hivi hawa si ndio waliokuwa wanapigania usawa barani Afrika?Mbona wenyewe wako sasa wanafanyiana hivi?”.

Mwalimu alifariki huku baadhi ya ndoto zake zikiwa hazijatimia.Wachambuzi wazuri wa siasa wanadai kwamba baadhi ya ndoto hizo zilishindikana hata kabla hajang’atuka (kwa mfano upinzani wake wa awali dhidi ya ushirikiano na mashirika ya fedha ya kimataifa).Lakini nadhani Mwalimu aliumia zaidi kuona Azimio la Arusha likizikwa hai na Azimio “la kimyakimya” la Zanzibar (naliita hivyo kwani sijawahi kuona “document” yoyote rasmi inayoelezea kilichomo kwenye Azimio hilo).

Wakati Dkt King anaweza kufarijika huko aliko iwapo angeweza kufahamu baadhi ya mambo yanayoendelea sasa nchini Marekani (hususan kuhusu Obama) nashindwa kuhisi ni lipi litakalokuwa linampa furaha Mwalimu huko aliko tukiweka pembeni suala la amani na utulivu.Na hata katika hilo (la amani na utulivu) wapo wanaodai kuwa ni ya kufikirika zaidi kwani ni ukweli usiopingika kwamba masikini ni wengi zaidi kuliko matajiri,na yayumkinika kusema kwamba matumbo ya masikini hao hayana amani wala utulivu.

Kadhalika,kuna wanaodai kwamba kigezo cha amani na utulivu kimekuwa kikitumiwa vizuri zaidi na mafisadi wanaoamini kwamba Watanzania ni wapole sana na hawako tayari kuchezea lulu ya amani na utulivu kwa vile tu flani kakwiba mabilioni ya umma.Pengine mafisadi hao wako sahihi kwani tumekuwa tukishuhudia baadhi ya watu wakiua,wakapewa dhamana za chapchap na kuendela na maisha yao kama kawaida huku hatima ya kesi zao ikisubiri isahaulike akilini mwa watu.Wakati hayo yakitokea,magereza yetu yamejaa wamachinga wanaotafuta ridhiki mitaani na wafungwa wengine ambao inawezekana kabisa walijiingiza kwenye wizi wa nyanya au kuku kwa vile tu hawakuwa na njia nyingine ya kujipatia kipato.Uhalifu ni uhalifu,na kila mhalifu anastahili adhabu lakini inatatiza kuona wahalifu wengine wakiendelea kula raha kana kwamba waliyofanya si kinyume cha sheria.

Tofauti kubwa kati ya ndoto ya Dkt King na Mwalimu ni kwamba wakati Wamarekani Weusi wanafanya kila jitihada kuenzi jitihada za Dkt King kwa kuendeleza mapambano dhidi ya ubaguzi na kupigania usawa,sie tuko kwenye mgawanyiko mkubwa kati ya wachache walionacho wasiosubiri kuongezewa bali wanapora, na wengi wasio nacho ambao hata kile kidogo walicho nacho kinaporwa.Hili ndio tishio kubwa,sio tu kwa ndoto za Mwalimu,bali hata kwa hiyo lulu yetu ya amani na utulivu.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.