Showing posts with label TAKUKURU. Show all posts
Showing posts with label TAKUKURU. Show all posts

6 Mar 2012

Usiniite mnafiki,au mpindisha maneno.Uthibitisho kuwa hata Rais Jakaya Kikwete hana imani na TAKUKURU upo katika habari ifuatayo (ANGALIA MAANDISHI MEKUNDU)


Rungu la Kikwete lilimwokoa Siyoi
Monday, 05 March 2012 09:17

Rais Jakaya Kikwete
NAPE, WASSIRA WADAIWA KUSIMAMA KIDETE ATOSWE, JK AKATUMIA 'RUNGU' KUZIMA HOJA,WABUNGE WOTE CHADEMA KUHAMIA ARUMERU
Joseph Zablon, Dar na Moses Mashalla, Arusha 

USHINDI wa Siyoi Sumari kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Arumeru Mashariki, unadaiwa kuitesa Kamati Kuu (CC) ya chama hicho, baada ya baadhi ya wajumbe kukuna vichwa kuhusu mbinu na mikakati ya kutengua ushindi alioupata katika duru ya pili dhidi ya William Sarakikya.

Katika Mkutano Mkuu wa jimbo hilo uliofanyika, Februari 20 ulimchagua Siyoi ambaye ni mtoto wa aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, marehemu Jeremiah Sumari kwa kura 361, akifuatiwa na Sarakikya aliyepata kura 259. Hata hivyo, CC ya CCM iliyoketi Februari 27, iliagiza kurejewa kwa upigaji kura kati ya wagombea hao.
Katika duru hilo la pili la uchaguzi uliofanyika Machi Mosi mwaka huu, Siyoi alipata ushindi wa kishindo wa kura 761 na kumtupa mbali mpinzani wake, Sarakikya aliyepata kura 361. 

Juzi katika kikao hicho cha CC, ushindi huo wa mara ya pili wa  Siyoi uliipasua tena kamati hiyo kuu yenye mamlaka ya juu ya uamuzi ndani ya chama hicho, baada ya baadhi ya wajumbe kudaiwa kutaka atoswe na apitishwe Sarakikya kutokana na tuhuma za matumizi makubwa ya fedha wakati wa kampeni.

Vyanzo vya habari vya kuaminika kutoka katika kikao hicho cha CC, vilifafanua kwamba waliosimama kidete kutaka Siyoi atoswe ni Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira.

Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, Nape alipinga Siyoi kurejeshwa akizingatia matukio mbalimbali ya tuhuma za matumizi makubwa ya fedha yaliyokuwa yakifanywa na baadhi ya watu ili wamchague mgombea huyo, kitu ambacho hakikupaswa kuvumiliwa. 

Hoja hiyo ya Nape iliungwa mkono na Wassira ambaye naye alitaka Siyoi atoswe kutokana na tuhuma hizo za matumizi makubwa ya fedha kutoka kwa baadhi ya wapambe wake waliotaka mgombea huyo achaguliwe.


Lakini inadaiwa kuwa Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete alisema kikao hicho kisingeweza kumkata Sumari kwa sababu tu ya tuhuma hizo za rushwa zilitolewa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), mkoani humo.


Chanzo kingine kilimnukuu mwenyekiti huyo akisema kwamba, Arusha ni mkoa wenye siasa za aina yake hivyo ni muhimu kuwa makini kwani siku za nyuma kuliwahi kuibuka tuhuma za rushwa kwa wabunge wa CCM kukamatwa lakini, mahakama ikawaachia huru.

Chanzo hicho kiliongeza kwamba, Rais Kikwete alisisitiza kuwa hata tuhuma za rushwa zilizotolewa zilikuwa zikigusa wengine kwani iliwahi kupendekezwa kwamba Elishalia Kaaya ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC), ndiye apitishwe na wengine wang'olewe. 

Katika kikao hicho, Rais Kikwete pia alinukuliwa akihoji kuwa endapo Siyoi angekatwa jina kungekuwa na uhakika wa chama kushinda kwa kumsimamisha Sarakikya? Hakupata jibu kama mgombea huyo wa pili angeweza kushinda kiti hicho.

Hata hivyo, chanzo hicho kilisema baada ya mwenyekiti kutumia rungu kumpitisha Siyoi alimpa angalizo: “Basi na wewe usiende kutamba huko mitaani kwamba umeangusha watu, fanya kampeni, ushinde jimbo tuangalie mambo mengine mbele.”

Ilielezwa zaidi kwamba Rais Kikwete aliungwa mkono na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, aliyeeleza kuwa haoni sababu ya kumwondoa Siyoi katika kinyang'anyiro hicho kwani ushindi wake ulikuwa mkubwa. 


Chanzo na Kwa habari Kamili: Mwananchi

10 Mar 2010

TAkukuru
Katika toleo jana la gazeti la Mwananchi kuna habari kwamba Mbunge wa Nyang’hwale,James Musalika, alilazimika ‘kuingia mitini’ kuwakwepa makachero wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) waliokwenda katika ‘hafla’ kati ya mbunge huyo na wapiga kura.Kwa mujibu wa Mwananchi,hatua hiyo ya wanadola wa TAKUKURU ni katika utekelezaji wa ‘ruhusa’ waliyopewa hivi karibuni na Rais Jakaya Kikwete ‘kudhibiti wanasiasa wanaotoa rushwa kwenye chaguzi’.

26 Feb 2010



Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia Rushwa TAKUKURU Dr. Edward Hosea akimkaribisha Rais Jakaya Mrisho Kikwete kufungua mkutano mkuu wa Mwaka wa taasisi hiyo.Picha kwa hisani ya MJENGWA

Hivi karibuni,uongozi wa kampuni ya magari ya Toyota ya Japan ulifanya jambo moja la kiungwana kwa kuwaomba radhi wateja wake kutokana na hitilafu za kiufundi katika modeli moja ya magari yake.Japo sakata hilo bado ni bichi hasa kwa vile inaelekea hitilafu hiyo bado haijapatiwa ufumbuzi,na tayari kuna habari za kushuka kwa hisa za kampuni hiyo katika masoko mbalimbali ya mitaji duniani,ni dhahiri hatua ya kuomba radhi imeonyesha kwamba kwa namna flani kampuni hiyo inatambua wajibu wake na inawajali wateja wake.

Majuzi,Rais Jakaya Kikwete alimwaga sifa kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) huku akijigamba kwamba serikali ya awamu ya nne imekuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya rushwa.Binafsi sidhani kama kauli hiyo ya JK inaendana na hali halisi ya utendaji na ufanisi wa TAKUKURU.

Kimsingi,tatizo haliko kwenye taasisi hiyo pekee bali kwenye medani nzima ya utawala bora.Angalia,kwa mfano,kauli za Waziri mwenye dhamana ya Utawala Bora,Mheshimiwa Sophia Simba,wakati wa sakata lililowahusisha wafanyabiashara wawili mashuhuri Bwana Reginald Mengi na Bwana Rostam Aziz.Badala ya kuhamasisha wananchi wanaojitokeza kuwaumbua hadharani mafisadi,Waziri Simba aliamua kuelemea upande mmoja ambapo bila aibu alimkemea Bwana Mengi huku akimlinda Bwana Rostam.

TAKUKURU hiyohiyo inayopongezwa na JK haijafanikiwa kujisafisha na tuhuma za namna ilivyouhadaa umma kuhusu suala la utapeli wa kampuni ya Richmond.Kamati ya Bunge iliyoundwa kuchunguza sakata hilo ilipendekeza Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Dr Edward Hosea,uamuzi ambao uko mikononi wa aliyemteua Hosea,yaani JK mwenyewe.Kwa hali ilivyo,na ukitilia maanani pongezi alozotoa JK kuhusu ufanisi katika mapambano dhidi ya ufisadi,ni dhahiri kuwa Rais hana mpango wa kumwajibisha Dr Hosea.

Nimesema tatizo liko kwenye utawala bora kwa vile hata chama tulichokipa dhamana ya kutuongoza-CCM-kimeendelea kufanya dhihaka linapokuja suala la utawala bora.Hivi inaingia akilini kweli kusikia kuwa Mbunge wa Bariadi,Bwana Andrea Chenge,bado ni mwenyekiti wa kamati ya maadili ya chama hicho tawala licha ya kuhusishwa kwake na tuhuma za ufisadi wa ununuzi wa rada!?Tusisahau kuwa pamoja na mageuzi ya kisiasa ya miaka ya tisini,bado chama tawala kimeendelea kuwa na nguvu pengine zaidi ya serikali,hoja kubwa ikiwa serikali hiyo imeundwa kutokana na ushindi wa chama husika.Kinachopuuzwa ni ukweli kuwa chama hicho hakikuomba ridhaa ya wanachama wake pekee bali Watanzania kwa ujumla.

Ni dhahiri kwamba kunakosekana utashi na udhati wa kupambana na ufisadi.Na kikwazo kikubwa kimeendelea kuwa kuweka mbele maslahi binafsi na ya chama badala ya maslahi ya umma/taifa.Pengine,na kwa hakika,badala ya kutetea mapungufu,ni muhimu kwa CCM na serikali yake kuiga mfano wa kampuni ya Toyota.Imetuangusha sana sio tu kwa kulegea katika mapambano dhidi ya ufisadi bali pia kwa ushiriki wake kwa kuwalinda watuhumiwa wa ufisadi.Laiti chama hicho kingekuwa na dhamira na utashi wa kukabiliana na ufisadi basi ni dhahiri Kamati ya Mwinyi inayoshughulikia mpasuko ndani ya chama hicho (wengine wanadai hakuna mpasuko) ingekuwa na kazi nyepesi tu ya kupendekeza wahusika wafikishwe kwenye vyombo vya sheria ili wasafishwe au waadhibiwe huko.Ikumbukwe kuwa tuhuma zinazowakabili watuhumiwa hao hazijaiathiri CCM pekee bali Watanzania wote kwa ujumla.

Nimalizie kwa kukumbushia usemi wa Kiingereza kwamba To err is human but to rectify is greatness,yaani (kwa tafsiri isiyo rasmi) kukosea ni ubinadamu lakini kujirekebisha ni uungwana.

10 May 2009

PICHANI,NI MBUNGE WA IGUNGA,ROSTAM AZIZ,AKIKABIDHI KINACHODAIWA KUWA DOSSIER LENYE TUHUMA DHIDI YA MFANYABIASHARA RAGINALDMENGI.ANAYEKABIDHIWA NI AFISA UCHUNGUZI WA TAKUKURU GWAKISA.Picha hii ni kwa mujibu wa gazeti la The African.

HUU NI NI UPUUZI.YAANI HAINGII AKILINI HATA KIDOGO.JAMANI,HIVI LINI MMEWAHI KUONA TAKUKURU WAKIKABIDHIWA USHAHIDI/TUHUMA MBELE YA VYOMBO VYA HABARI AS SEEN IN THE PICTURE ABOVE?

HUYU ROSTAM AMEKUWA MITHILI YA MUNGU MTU: ALIPOTAJWA TU NA MENGI,MAWAZIRI WAZIMA NA BUSARA ZAO (SOPHIA SIMBA NA KAPTENI MKUCHIKA) WAKALIPUKA KUMTETEA (JAPO SASA WAMEKAA KIMYA ROSTAM ALIPORUDIA KILEKILE ALICHOFANYA MENGI).KISHA TAKUKURU NAO KATIKA HALI INAYOONYESHA NAMNA GANI TAASISI HIYO NI WABABAISHAJI WA DARAJA LA JUU WAKAANDAA MITHILI YA PRESS CONFERENCE YA KUMPOKEA ROSTAM NA KINACHODAIWA KUWA NI USHAHIDI WAKE DHIDI YA MENGI (JAPO KUNA MADAI KUWA WAJANJA WAMEMWINGIZA MJINI KWA KUMUUZIA "CHENI BANDIA"-ISOMEKE DATA FEKI).

HAWA TAKUKURU NI WAZEMBE ZAIDI YA WAZEMBE.HIVI UBABAIKAJI KAMA HUO WALIOFANYA KWA ROSTAM WANGEUELEKEZA KWA KAGODA SI TUNGEPIGA HATUA FLANI?AU WANGEKUWA "FASTA" NAMNA HIYO KATIKA,SIO KUITETEA BALI KUICHUNGUZA IPASAVYO KAMPUNI YA RICHMOND,KWA HAKIKA TUSINGEKUWA HAPA TULIPO SASA.

MBONA WENZETU MNAJIDHALILISHA KIASI HICHO?NI HIZO FEDHA ZA ROSTAM AU NJAA ZENU?THIS IS MORE THAN TOO MUCH.IT'S ABSURD,CRAZY AND UTTERLY NONSENSE.

29 Mar 2009

SHAHIDI katika kesi ya kuomba na kupokea rushwa ya sh 600,000 inayomkabili Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Mbelekese, wilayani Iramba, Singida, Iddi Mughenyi, juzi alipata kipigo kutoka kwa mwanasheria wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kwenye viwanja vya Mahakama ya Wilaya ya Iramba, kwa madai kuwa alimgeuka katika ushahidi alioutoa mahakamani hapo.

Mtuhumiwa alipata kipigo kutoka kwa mwanasheria huyo aliyetambulika kwa jina moja la Mchumi, kwa madai kwamba alimgeuka katika ushahidi aliuotoa mahakamani hapo.

Tukio hilo la aina yake limedaiwa kutokea muda mfupi baada ya Mughenyi kutoa ushahidi katika kesi namba 14/2009 inayomkabili ofisa mtendaji huyo.

Akizungumza kwa njia za simu kutoka Iramba, mmoja wa watumishi wa mahakama hiyo ambaye hakutaka kutajwa jina, alisema kuwa kuna kila dalili kuwa ushahidi uliotolewa na shahidi huyo haukumridhisha mwanasheria Mchumi, kwa madai kwamba ulikuwa kinyume cha walivyokubaliana.

“Idd Mughenyi ni shahidi wa upande wa TAKUKURU kwenye kesi hiyo ambayo Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Mbelekese anatuhumiwa kuomba na kupokea rushwa, lakini juzi aliposimama kizimbani aliikana taasisi hiyo, kitendo ambacho kinawezekana kilimuudhi mwanasheria huyo ambaye ndiye alikuwa mwendesha mashtaka katika kesi hiyo,” alifafanua mtumishi huyo wa mahakama.

Aidha, mtumishi huyo alisema baada ya kesi hiyo kuahirishwa na kutoka nje ya mahakama, ndipo Mchumi alipomweka chini ya ulinzi shahidi huyo na kumtaka apande kwenye gari ili waende ofisi za TAKUKURU Wilaya ya Iramba.

Alisema kutokana na shahidi huyo kugoma kupanda gari kwa madai ya kutofahamu kosa, ndipo mwanasheria huyo alipoanza kumpiga makofi hadi kumuumiza kwenye jicho la upande wa kushoto na kumchania shati.

Alibainisha tukio hilo lilishuhudiwa na baadhi ya mahakimu, na kuongeza kuwa waliwaamru askari kwenda kuamua ugomvi huo, kisha kuwapeleka kituo cha polisi.


RUSHWA NI RUSHWA,IWE NDOGO AU KUBWA.LAKINI INGEPENDEZA ZAIDI KUONA TAKUKURU IKITUMIA MISULI MINGI KWENYE RUSHWA KUBWA NA UFISADI SAMBAMBA NA HIZO RUSHWA NDOGO.MAPAPA WA KAGODA NA RICHMOND (achana na yule Mdosi aliyepandishwa kizimbani) BADO WANAPETA URAIANI SAMBAMBA NA MAFISADI WA RADA.

24 Dec 2008

SAFARI YA MAPAMBANO DHIDI YA UFISADI BADO NI NDEFU NA YENYE VIKWAZO LUKUKI.KATIBA NA SHERIA ZINAZOWATOFAUTISHA VIONGOZI NA WANANCHI WA KAWAIDA ZINATUMIKA KAMA KINGA DHIDI YA MATENDO AMBAYO KWA NAMNA MOJA AU NYINGINE YANAHUSU UVUNJAJI WA SHERIA.PIA KINGA HIZO ZINAWEZA KUWA KICHOCHEO KIZURI KWA VIONGOZI WAPYA KWANI KAMA WATANGULIZI HAWAKUCHUKULIWA HATUA WALIPOBORONGA (KWA VILE WANA KINGA) THEN KWANINI WALIOPO MADARAKANI WAOGOPE KUBORONGA?HIVI KAMA WENZETU HUKO MAREKANI WANADIRIKI KUMHOJI RAIS MTEULE,IWEJE VIGUMU KWETU KUMHOJI RAIS MSTAAFU?ANYWAY,SOMA STORI HII HAPO CHINI KISHA TUENDELEE NA MJADALA WETU
Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, hachunguzwi kwa kosa au tuhuma yoyote ya jinai, imeelezwa. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), katika taarifa yake kwa umma iliyotolewa Dar es Salaam jana, ilisema uvumi kuwa Rais huyo mstaafu anachunguzwa na vyombo vya dola ikiwamo taasisi hiyo, hauna ukweli wowote. 

Tamko la taasisi hiyo limekuja huku kukiwa na uvumi katika baadhi ya vyombo vya habari kuwa kiongozi huyo anachunguzwa na Takukuru, kutokana na vitendo vingi vya ufisadi vinavyodaiwa kufanywa wakati wa uongozi wake. 

Tayari mawaziri wawili Basil Mramba na Daniel Yona waliowahi kushika nyadhifa nyeti katika Serikali ya Awamu ya Tatu ukiwamo uwaziri wa Fedha, wameshafikishwa mahakamani kwa tuhuma za kutumia madaraka yao vibaya na kuisababishia serikali hasara ya Sh bilioni 11.7. 

Lakini pia baadhi ya watuhumiwa katika kesi za kuchota mabilioni ya fedha katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu (BoT), ambao wamefikishwa mahakamani, wanadaiwa kufanya wizi huo kati ya mwaka 2004 na 2005 kipindi ambacho Rais Mkapa alikuwa madarakani. 

Ofisa Uhusiano wa Takukuru, Doreen Kipwani alisema jana kuwa, taasisi yake haina uwezo wa kumchunguza kiongozi huyo kutokana na Katiba ya nchi kutotoa nafasi hiyo katika Ibara ya 46 (3) ya Katiba ya Tanzania. Kapwani alieleza kuwa taasisi yake inaheshimu Katiba na ina wajibu wa kuilinda na kuheshimu matakwa hayo ya Katiba. 

“Takukuru inawafahamisha wananchi kwamba uvumi huu hauna ukweli wowote, hatumchunguzi kiongozi huyu kwa kosa au tuhuma yoyote ya kijinai,” alisema. “Ni kwa msingi huu, Takukuru imeona ni vyema kuwafahamisha wananchi ukweli dhidi ya uvumi huu. 

Tukumbuke wakati wote kwamba taifa letu lina Katiba ya Nchi ambayo imeweka misingi mikuu ya kuendesha nchi yetu, haki na wajibu wa kila Mtanzania. Katiba kama sheria mama imeweka pia mipaka katika kushughulikia mambo mbalimbali ya nchi na kwa mantiki hii, haina budi kuheshimiwa wakati wote.” 

Kifungu hicho cha Katiba kinaeleza kuwa “Ni marufuku kumshitaki au kufungua mahakamani shauri lolote la jinai au la kumdai mtu aliyekuwa anashika madaraka ya Rais baada ya kuacha madaraka hayo kutokana na jambo lolote alilofanya yeye kama Rais wakati alipokuwa bado anashika madaraka ya Rais kwa mujibu wa Katiba hii.” 

Kapwani alisisitiza kuwa Takukuru itaendelea kufanya kazi zake kwa mujibu wa Katiba na sheria ya nchi na sio vinginevyo. Katika siku za karibuni, baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vinaripoti kuwa Mkapa anachunguzwa na Takukuru licha ya kuwa ana kinga ya kutoshitakiwa. 

Vyombo hivyo vimekuwa vikimwandama kwa madai kuwa ufisadi mkubwa umefanyika katika kipindi ambacho alikuwa madarakani. Watu wenye mtazamo huo wamekuwa wanataka kiongozi huyo aondolewe kinga na afikishwe mahakamani kujibu tuhuma mbalimbali za ufisadi. 

Wiki hii, Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo alieleza kusudio la kuwasilisha hoja binafsi katika kikao kijacho cha Bunge kuomba kifungu kinacholinda marais wastaafu kutoshitakiwa kirekebishwe. Mkapa anatajwa katika tuhuma kuhusu ununuzi wa ndege ya Rais, ununuzi wa rada, wizi wa mabilioni ya EPA, uuzaji wa nyumba za serikali, mikataba yenye utata kama ya NetGroup, Alex Stewart na ubinafsishaji wa mgodi wa Kiwira.
CHANZO: Habari Leo

UFAFANUZI HUO WA TAKUKURU HAUWEZI KUZIMA KELELE ZA WANAOTAKA KUMUONA TUHUMA DHIDI YA MKAPA ZINATHIBITISHWA KWENYE VYOMBO VYA SHERIA.PAMOJA NA KUILINDA NA KUIHESHIMU KATIBA,TAKUKURU INA WAJIBU WA KULINDA NA KUTETEA RASLIMALI ZA WATANZANI ZINAZOFUJWA NA MAFISADI.LAKINI TUKIACHANA NA EXCUSE HIYO YA TAKUKURU (WAMESHATOA LUKUKI) THIS IS A WAKE UP CALL KUHUSU HIZI KINGA DHIDI YA VIONGOZI WASTAAFU (NA PENGINE HATA KWA WALIO MADARAKANI).WAKATI WAZO LA KINGA NI ZURI LIKITUMIWA VIZURI,KWA MFANO DHIDI YA WANAOTAKA KUDHALILISHA VIONGOZI KWA SABABU BINAFSI AU KISASI,WAZO HILO NI HATARI KWA VIONGOZI WALIOZITUMIA VIBAYA OFISI ZAO WALIPOKUWA MADARAKANI.MAHALA PEKEE PANAPOWEZA KUMSAFISHA MKAPA NI MAHAKAMANI NA WALA SIO KWA KAULI ZA KULINDANA KAMA HIZO ZA TAKUKURU.

11 Feb 2008

Uongozi wa kisiasa wa Tanzania,kama ilivyo sehemu mbalimbali duniani,umekuwa ukitegemea watu kutoka fani mbalimbali za maisha.Tuna viongozi wa dini (kama Mchungaji Lwakatware),Wasomi (kama Prof Mwandosya,Prof Msola,Prof Mwakyusa),wanajeshi (kama Kapteni John Komba,Kapteni Jaka Mwambi,Luteni Yusufu Makamba) na hata wasanii kama Khadija Kopa .Hivi karibuni,JK alielezea kutoridhishwa kwake na athari zinazoweza kutokana na kuwa na viongozi ambao pia ni wafanyabisahara.Ana hoja ya msingi hapo,lakini nadhani tatizo la msingi sio fani aliyotoka au anayoendela nayo kiongozi husika bali ni utashi alionao katika kuwahudumia Watanzania wenzake.Kadhalika,mkanganyiko uliopo kwenye kanuni za maadili ya uongozi ziko shaghala baghala,hasa baada ya kuuawa kwa Azimio la Arusha na kuzaliwa Azimio la Zanzibar.Endelea na makala yangu hii kwenye gazeti la Mtanzania.
MTANZANIA UGHAIBUNI-

Watanzania wengi wameipokea kwa furaha kauli ya Rais Jakaya Kikwete kuhusu umuhimu wa kutenganisha biashara na utumishi wa umma.Ni kauli mwafaka kwani hata katika Maandiko Mtakatifu tunafundishwa kwamba ni vigumu kutumikia mabwana wawili.

Naamini kwa mtazamo wa wengi,wafanyabiashara kama Watanzania wengine wana kila haki ya kushiriki katika shughuli za siasa ikiwa ni pamoja na kugombea ubunge au hata kuteuliwa mawaziri.Tatizo linakuja pale maslahi ya biashara zao yanapoingiliana na utekelezaji wa majukumu yao katika kuuhudumia umma.

Inaweza kuwa sio sahihi kuwalaumu wafanyabisahara wanaochanganya biashara na siasa pale ilhali hakuna miongozo maalumu (kama ya Marekani na Uingereza).Ndio maana wazo la kufanyika mchakato wa kuleta sheria na kanuni zitakazoweka bayana mazingira ambayo kwa upande mmoja hayatawanyima nafasi wafanyabiashara kushiriki kwenye siasa,na upande mwingine biashara zao kutoathiri majukumu waliyokabidhiwa na taifa,lina umuhimu mkubwa.

Pamoja na pongezi hizo ni muhimu kuangalia chanzo cha tatizo lililopo hivi sasa.Ni ukweli usiopingika kwamba wakati wanasiasa wengi wameendelea kuhubiri kwamba siasa ya Ujamaa na Kujitegemea bado ni mhimili wa taifa letu,hali halisi tuliyo nayo sasa inapingana kabisa na matamshi hayo.

Azimio la Arusha lilisaidia kuweka wazi mwelekeo wa taifa letu.Makala moja kama hii haiwezi kutosha kuelezea undani wa Azimio hilo lakini kilicho wazi ni kwamba Baba wa Taifa,ambaye kimsingi ndiye anayekubalika kama mwasisi wa itikadi hiyo,alikuwa na ndoto ya kuona jamii ya Watanzania inayoishi kwa usawa na haki.

Baadaye likaja Azimio la Zanzibar.Pengine mie ni mzembe wa kujua kilichomo katika Azimio hilo lakini naamini kwamba kuna Watanzania wengi ambao hadi leo hawajui kilichomo kwenye Azimio hilo.Labda ni kutokana na ufahamu mdogo uliopo miongoni mwa wananchi wengi kuhusu Azimio la Zanzibar ndio maana wengi wetu tunarahisisha majibu kwamba lilikuwa tamko rasmi la kifo cha Azimio la Arusha.Na katika hili,CCM inastahili kubeba lawama zote kwani haijafanya jitihada zozote za makusudi kuuelewesha umma kuhusu madhumuni na kulichomo kwenye Azimio hilo (la Zanzibar).

Kuna mapungufu makubwa katika suala zima la uwazi pindi yanapojiri masuala nyeti kwa taifa letu.Mfano mzuri ni kwamba wengi wetu tulikuwa hatufahamu kwamba hadi uteuzi wake unatenguliwa na Rais,aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu aliyeondolewa madarakani,Dkt Daudi Ballali,hakuwa mtumishi wa serikali.Pengine taratibu zinasema hivyo lakini kwa vile mtu anayekalia nafasi hiyo ndiye mwenye kushika dhamana ya fedha za Watanzania wote,nadhani kulikuwa na kila sababu ya wenye fedha zao (Watanzania) kufahamishwa kuhusu hilo badala ya kusubiri mpaka litokee tatizo la ufisadi kwenye taasisi hiyo muhimu kwa taifa.

Hadi muda huu,ukiwauliza viongozi wa CCM kwamba je Azimio la Arusha bado ni mwongozo muhimu kwa maendeleo na mwelekeo wa taifa,sanasana utachoambulia ni hadithi ndefu zisizotosha kutoa jibu moja la kueleweka.Ni dhahiri muuliza swali atakumbana na ugumu wa aina hiyohiyo pindi akiuliza iwapo nchi yetu bado inafuata siasa ya Ujamaa na Kujitegemea.Na haiishii hapo kwani majibu yataendelea kuwa tete pindi mtu akiuliza iwapo CCM bado ni chama cha wakulima na wafanyakazi.

Na ni katika hilo la wakulima na wafanyakazi ndipo napoona kuna tatizo la msingi.Inasemekana Azimio la Zanzibar lilihalalisha watumishi wa umma (wafanyakazi) kumiliki mali kinyume na katazo lililowekwa na Azimio la Arusha.Laiti wakati wanasiasa wetu walipokutana Zanzibar kuua Azimio la Arusha wangeangalia mbali,ni dhahiri wangebaini uwezekano wa kutokea mgongano kati ya biashara na utumishi wa umma.Haraka ya kupitishwa Azimio hilo inaweza kuwa sababu muhimu ya wanasiasa hao kutoangalia mbali.Lakini pia haraka hiyo inaweza kuwa ilichochewa na ukweli kwamba wakati wanasiasa wengi walikuwa wakituimbia ngonjera za Ujamaa na Kujitegemea majukwaani,majumbani mwao walikuwa wakicheza ngoma za ubepari.

Dhana hapo ni kwamba Azimio la Zanzibar lilipitishwa chapchap ili wajamaa wa hadharani waliokuwa mabepari wa kificho waweze kuendesha maisha yao bila hofu na bughudha ya kuonekana wanatenda kinyume na imani ya taifa letu kwa wakati huo.Hawa ni pamoja na wale ambao walikuwa wakituaminisha kwamba ni watu wa karibu na Baba wa Taifa kumbe moyoni walikuwa wakiomba dua Mwalimu aondoke madarakani ili watumie vile walivyokuwa wakikusanya kwa kificho katika zama hizo za Ujamaa na Kujitegemea.Na wengine japo Mwalimu aliwasaidia kuwaingiza madarakani akidhani ni waumini wa siasa zake,wamestaafu wakiacha skandali lukuki.

Kama kuna madhara mabaya zaidi ya mfumo wa chama kimoja basi ni kule kutoruhusu mawazo tofauti na ya watawala,hata kama mawazo hayo ni ya kuchochea maendeleo ya taifa.Kinadharia kila Mtanzania ana uhuru wa kutoa mawazo yake alimradi asivunje sheria halali za nchi,lakini kiuhalisia bado kuna chembechembe zilizorithiwa kutoka katika mfumo wa chama kimoja ambapo mawazo tofauti ni sawa na uhaini.

Katika zama za chama kimoja,hoja kama ile ya “chama kushika hatamu” zilisaidia baadhi ya mafisadi wa wakati huo kupata kinga dhidi ya wale maovu yao.Sote tulikuwa ni Watanzania tusio na tofauti,tunaoamini kwamba ili nchi yetu iendelee tunahitaji ardhi,watu,siasa safi na uongozi bora.Mwalimu aliamini kuwa hiyo ni njia sahihi ya maendeleo kwani alishuhudia namna ilivyofanikiwa sehemu kama China na Cuba.Kosa lake ni kuamini kwamba walio karibu yake walikuwa na imani ya dhati kama yeye.Angalau leo tunawajuwa wanafiki hawa,lakini kwa sababu za “kulinda umoja wa kitaifa” na kutaka “wapumzike kwa amani” tunaendelea kuwaheshimu kwa kutowaumbua hadharani.

Kumkosoa mzazi ni kosa,na kwa mwananchi wa kawaida au hata kiongozi kumkosoa Rais inaweza kutafsiriwa kuwa ni utovu wa nidhamu.Hata hivyo,kutoa ushauri kwa heshima na taadhima ni jambo linalokubalika.Ni kwa kuzingatia hilo ndio maana naamini kwamba wakati Watanzania wengi wanakubaliana na mtizamo wa Rais Kikwete kuhusu kutenganisha siasa na biashara,ni vema katika utekelezaji wa dhamira yake hiyo akaweka maanani namna Baba wa Taifa alivyosalitiwa na baadhi ya watu wake wa karibu.

Nasema hivyo kwa sababu naamini hata zikiwekwa sheria nzuri namna gani za maadili ya uongozi,pasipo kutengeneza mazingira yatakayozuia wasimamizi wa sheria hizo kuzihujumu,itakuwa ni kazi bure.Mwanasiasa anaweza kabisa kutangaza kwamba biashara zake za awali zimekabidhiwa kwa wadhamini flani,lakini pasipo usimamizi mzuri mfanyabiashara huyo anaweza kuendelea kuendesha biashara zake huku akiwa mwanasiasa japo machoni mwa umma anaonekana ametekeleza sheria hiyo tarajiwa ya kutenganisha biashara na siasa.

Mfano mzuri wa ninachosema ni hili sakata linaloendelea la fedha za EPA huko Benki Kuu.Yayumkinika kubashiri kwamba kama itafikia hatua ya watu flani kupelekwa mbele ya vyombo vya sheria,kuna uwezekano watu hao wakawa ni wamiliki “hewa” ambao majina yao yalitumika tu kuficha wamiliki halali.Katika mazingira ambapo taasisi kama TAKUKURU ilikuwa ya kwanza kudai mradi wa Richmond haukuwa na harufu ya rushwa ilhali sasa tunaona suala hilo likiwaka moto huko bungeni,tutarajie nini pindi wakipewa jukumu la kuhakikisha mfanyabishara anayetaka kuingia kwenye siasa kweli amekabidhi biashara yake kwa wadhamini kama sheria itakavyokuwa inataka?

Mwisho,kikao kinachoendelea cha bunge kimeonyesha dalili kwamba baadhi ya wawakilishi wetu wamechoka kupiga mihuri kupitishwa miswada inayoonekana mizuri machoni lakini inaishia kwa mashirika kama ATC kununua ndege mbovu,TANESCO kujikuta hohehahe kwa kulipa madeni yaliyosababishwa na walafi flani wasio na uchungu na taifa au kuletewa umeme hewa ulioahidiwa na makampuni ya kisanii.Hoja hapa sio kuitupilia mbali miswada ya manufaa kwa taifa au kuchochea upinzani dhidi ya serikali bali kuwabana mafisadi wote wananaotumia nyadhifa zao kulikamua taifa letu.
BAADA YA POLITIKI ZA BONGO,HEBU ANGALIA HIZI ZA NAS KUHUSU THE N-WORD


20 Jan 2008

Makala hii ilitoka kwenye gazeti la Mtanzania siku ya Alhamisi 17Jan 2008.

Hatimaye ugavana wa Dkt Daudi Ballali katika Benki Kuu ya Tanzania umetenguliwa.Sijui kama utenguzi huo ni sawa na tunachosoma,kuona na kusikia kwenye vyombo mbalimbali vya habari kwamba Balali amefukuzwa kazi.Pengine la muhimu kwa sasa ni kwamba mtu huyo ametolewa katika wadhifa huo japo la muhimu zaidi ni kuweka rekodi vizuri kwa minajili ya kuondoa utata uliojitokeza hasa katika neno “KUTENGUA”.

Kuna wanaosema kwamba Ballali ametolewa kafara hasa kwa kuzingatia ukweli kwamba sio rahisi wizi mkubwa namna hiyo uwe umefanywa na mtu mmoja tu.Ni vigumu pia kuamini kwamba uamuzi wa gavana huyo wa zamani kuyazawadia makampuni yaliyotajwa kwenye ufujaji wa fedha hizo ulifanywa na mtu mmoja pekee (Balalli).

Sakata hili lilisabaisha,linasababisha na litaendela kusababisha maswali mengi zaidi kuliko majibu.Sijui kuna wazalendo wangapi hapo Benki Kuu, lakini nashawishika kuhoji uzalendo wao kwani japo si kila mtumishi angeweza kufahamu alichokuwa akifanya Balali na washirika wake,ni dhahiri wapo waliokuwa katika nafasi ya kutoa taarifa kwa vyombo husika lakini wakaamua kukaa kimya.

Nadhani kuna waliojua kinachoendela lakini wakaa kimya kwa vile nao walikuwa washiriki katika ufisadi huo.Hawa hawana cha kujitetea kwani hawana tofauti na Balalli na wanachostahili ni adhabu tu.Kikwazo kikubwa kinachojitokeza katika uwezekano wa kuwaadhibu waungwana hawa ni ukweli kuwa baadhi yao wamepewa nafasi ya kujichunguza wenyewe (kwa vile bado wako madarakani) na sote tunaelewa kwamba hawawezi kujihukumu.Sanasana wataishia kuharibu ushahidi muhimu katika uchunguzi mzima wa ufisadi huo.

Kundi la pili ni wale waliokuwa wakifahamu kinachoendelea lakini hawakuchukua hatua kwa sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kauli za utetezi zilizokuwa zikitolewa na watu mbalimbali pindi tuhuma za ufisadi huo zilipoanza kuibuka.Tunakumbuka kwamba kuna wakati huko bungeni lilitolewa tishio la kumfikisha Dr Slaa mbele ya vyombo vya sheria akituhumiwa kwamba ameghushi nyaraka zinazohusiana na sakata hilo.Yayumkinika kusema kwamba kauli kama hizo zinaweza kuwa ziliwakwaza baadhi ya watumishi wa Benki Kuu (waliokuwa na ufahamu wa ufisadi huo) kuripoti kuhusu uhuni uliokuwa ukiendelea hapo.
Imeripotiwa pia kwamba moja ya makampuni ya ukaguzi wa mahesabu ya benki hiyo iliripoti kuhusu kasoro zilizokuwepo lakini ikaishia kuona mkataba wake na benki hiyo ukisitishwa.Ni rahisi kukubaliana na “busara” hii kwamba kama kampuni iliyolipwa kuchunguza mahesabu imepuuzwa je “nani atanisikiliza mie niliyeajiriwa kufanya majukumu mengine katika Benki Kuu”.

Miongoni mwa madhara ya kulea ubadhirifu ni kujengeka kwa imani (miongoni mwa wasiojihusisha na ubadhirifu huo) kwamba ubadhirifu sio dhambi kwani ingekuwa haukubaliki basi wahusika wasingeendelea nao pasipo kuchukuliwa hatua.Yeyote aliyehusika na skandali hiyo lakini bado yuko madarakani ni sawa na kansa ambayo isipodhibitiwa inasambaa katika mwili mzima.Ni kama katika familia yenye watoto kadhaa na baadhi yao wanajihusisha na tabia zisizofaa.Ni dhahiri wale wanaoepuka tabia hizo (ilhali wenzao wanaendelea nazo) wanaweza kushawishika kuiga tabia hizo hususan kama wanaona wenzao wananufaika kwa namna flani.

Nakumbuka hivi karibuni,mkongwe wa siasa Mzee Kingunge Ngombale Mwiru alinukuliwa na gazeti moja akieleza masikitiko yake kuhusu namna uzalendo unavyopungua miongoni mwa Watanzania.Ni kweli uzalendo umepungua sana na tusipokuwa makini utapotea kabisa lakini kuwa na wasiwasi au kulalamika pekee hakuwezi kusaidia kurekebisha mambo.Ni dhahiri kwamba moja ya mambo yanayochangia kupungua uzalendo ni pamoja na ufisadi kama huo uliofanyika hapo Benki Kuu.

Hivi mtu atakuwaje mzalendo iwapo wakati yeye anahangaika kutafuta fedha za kumwezesha kupata angalau mlo mmoja wa siku kuna wajanja wanatumbukiziwa mamilioni ya shilingi kwenye makampuni yao pasipo kuvuja tone moja la jasho.Kibaya zaidi na pengine katika kuwaringia walipa kodi wanaoibiwa,mafisadi hawaogopi kuonyesha namna wizi wao “unavyolipa” kwa kuporomosha mahekalu ya gharama kubwa,magari ya thamani ya kutisha na vimbwanga vingine chungu mbovu.Ni kama mtu anakupora mke halafu kesho yake unamwona anatamba nae mtaani.Hii inaongeza chuki na hasira kwa aliyeibiwa.

Kila zinapojitokeza tuhuma za ufisadi huwa nashindwa kujizuia kuhoji uwezo wa TAKUKURU katika jukumu lake la kuzuia na kupambana na rushwa.Taasisi hii imekuwepo kwa muda mrefu sasa lakini bado ni legelege licha ya jitihada kadhaa zilizokwishafanywa iwe na ufanisi zaidi.Naafikiana na baadhi ya hoja kwamba matendo mengi ya ulaji fedha za umma hayafanyiki hadharani,hivyo kusababisha ugumu katika kuyabaini.Hata hivyo,katika sakata hili la ufisadi hapo BoT,tetesi zilikuwepo mtaani na magazetini kwa muda mrefu.Kama ilivyozeleka,kauli za TAKUKURU zilikuwa “taarifa hizo tunazo na tunazifanyia uchunguzi”.Ikumbukwe kwamba katika mazingira ambayo matatizo yanazaliana kila kukicha,kuchelewa kutatua tatizo moja ni sawa na kutengeneza mlima wa matatizo hayo ambapo mwisho wake itakuwa ni suala lisilowezekana kabisa kuyaondoa.

Pengine umefika wakati mwafaka kwa wawakilishi wetu huko bungeni kuhoji uhalali wa kuendelea kuwa na taasisi hiyo ya kuzuia na kupambana na rushwa.Kanuni ya haki katika sheria inatamka waziwazi kwamba haki sio tu itendeke bali pia ionekane imetendeka.Tunaweza kuitumia kanuni hiyo kwa TAKUKURU pia kwamba mapambano dhidi ya rushwa yasiishie tu kuwa ya dhamira bali yaonekane hadharani kuwa yapo na yana ufanisi unaotarajiwa.

Naweza kuonekana mtu wa ajabu iwapo nitashauri kuvunjwa kwa TAKUKURU lakini nina hoja ya msingi napofikiri hivyo.Mamilioni ya fedha yanayoelekezwa kwa taasisi hiyo kupambana na rushwa hayajasaidia lolote katika kupunguza tatizo hilo.Mabadiliko mbalimbali ya kisheria yaliyolenga kuipa meno taasisi hiyo nayo yameshindwa kuifanya iwajibike ipasavyo.Binafsi sioni cha ziada kinachoweza kubadili ulegelege wa taasisi hiyo zaidi ya kuivunjilia mbali na kasha majukumu yake kuhamishiwa kwenye taasisi nyingine kama vile kitengo cha upelelezi katika jeshi la polisi (CID).

Kwa kuzingatia rekodi ya TAKUKURU katika uendeshaji wa kesi inazopeleka mahakamani,sintoshangaa iwapo wanaotajwa kwenye sakata hilo wataishia kuibuka washindi kwenye kesi hizo.Tumeshuhudia namna taasisi hiyo ilivyokuwa “ikipelekeshwa” kwenye kesi dhidi ya Balozi wa zamani wa Tanzania nchini Italia.Kama kesi ya mtu mmoja imekuwa ngoma nzito namna hiyo,tutarajie nini kwenye lundo la kesi linalowahusu watu wenye uwezo mkubwa wa kifedha?

Wengi wanatafsiri vurugu zinazoendelea nchini Kenya kuwa ni matokeo ya ukabila.Lakini baadhi ya wachambuzi wa uchumi wananyumbulisha kwamba vurugu hizo ni sehemu tu ya mapambano ya kiuchumi kati ya wenye nacho na wasio nacho.Migongano ya kidini au kikabila hujichomoza zaidi kwenye jamii isiyo na uwiano wa kimapato kwani mara nyingi washiriki kwenye vurugu hizo huamini kwamba pindi zikifanikiwa zitarekebisha maisha yao ya kila siku.Tuna kila sababu ya kuzuia nchi yetu inayosifika kwa amani na utulivu isiingie kwenye machafuko yanayoweza kusababishwa na wengi wanaoona wachache wakinufaika kwa “ulafi wa kula keki ya taifa” huku wao (wengi hao) wakiendelea kutaabika.Kinachowezekana leo kisingoje kesho.

2 Jan 2008


Makala yangu ndani ya toleo la wiki hii la gazeti la RAIA MWEMA inatoa changamoto ya kuwa na mashujaa watakaoweza kupambana na dhuluma,ujambazi na ufisadi dhidi ya nchi yetu.Nimetumia mifano ya mashujaa wawili,Wesley Autrey na John Smeaton kupigia mstari umuhimu wa kufanya maamuzi ya haraka (yasiyohitaji semina elekezi au kuundiwa tume ya kuchunguza tume) yatakayowanufaisha wengi.Ili kukabiliana na mafisadi na wababaishaji wengine ni lazima tuwe na "have-a-go heroes" katika fani mbalimbali,hususan uandishi wa habari na sheria,ambao wataibana TAKUKURU inapokurupuka kusema dili la Richmond lilikuwa safi ilhali Bunge limeunda tume ya kuchunguza ishu hiyo,au watambana Mwapachu anaposema uhalifu utadhibitiwa ilhali miezi kadhaa sasa imeshapita tangu akabidhiwe orodha ya wahalifu na hatujaskia kilichoendelea,au kuwabana wale wababaishaji waliotishia kwenda mahakamani baada ya kutajwa hadharani kuwa ni mafisadi,au hata kumuuliza JK kuhusu kauli yake ya mwanzoni kabisa kwamba anawajua wala rushwa na anawapa muda wabadilike...je kwa mtazamo wameshabadilika au hiyo deadline aliyoitoa kwa wala rushwa hao haijapita?

Pamoja na habari na makala nyingine zilizokwenda shule,bingirika na uungane nami mtumishi wako hapa

12 Sept 2007

Asalam aleykum,

Katika makala yangu iliyopita,nilizungumzia kuhusu kile ambacho wachambuzi wa siasa za kimataifa wanakiona kama kurejea kwa kasi kwa mbio za silaha (arms race) zenye uwezo mkubwa na wa kisasa zaidi kuliko hapo awali au sasa.Nchi za Magharibi zikiongozwa na Marekani zimeonekana kuguswa na namna Russia inavyoongeza kasi katika teknolojia na uzalishaji wa silaha za kisasa.Muda mfupi kabla ya kuandaa makala hii,nimeona taarifa moja inayoeleza kuwa Russia imefanikiwa kufanya majaribio ya kile inachokiita “Baba wa Mabomu Yote” (Father of all Bombs).Teknolojia hiyo mpya inaelezwa kuwa na uwezo mara nne zaidi ya ile ya Marekani inayojulikana kama “GBU-43 Massive Ordnance Air Blast” (MOAB) au “Mother of all Bombs” (yaani “Mama wa Mabomu Yote”) ambayo ilifanyiwa majaribio yenye mafanikio mwaka 2003.Tofauti na teknolojia ya awali ya mabomu,hilo la kisasa la Russia ni la “thermobaric,” yaani linatumia oksijeni iliyopo hewani (atmospheric oxygen) kusababisha mlipuko badala ya kutumia kemikali nyingine (oxidizing agent) kuleta matokeo hayo (mlipuko).Silaha za ki-“thermobaric” zina tabia ya kutoa nishati kubwa zaidi kuliko zile zisizotumia teknolojia hiyo,na inaelezwa kwamba bomu hilo jipya la Russia lina uwezo wa kuteketeza kabisa maisha katika eneo mzunguko la maili nne.

Kinachochochea mbio za silaha ni sawa na kile wanafalsafa wanachokiita “domino effect” yaani badiliko (change) moja linapelekea badiliko jingine jirani,nalo linapekea badiliko jingine,na jingine kwa jingine,na kadhalika.Yaani ni kama kugongwa gari la kwanza kwenye foleni ndefu ambapo la kwanza litaligonga la pili,la pili litaligonga la tatu,na kadhalika,na kadhalika.Kwa Russia kutambulisha mafanikio yake hayo,ni dhahiri kwamba Wamarekani nao watakuna vichwa ili waibuke na teknolojia kali zaidi ya hiyo ya Russia (pengine wataamua kuiita “babu wa mabomu yote” maana tayari tuna “baba” na “mama,” na si ajabu Russia nao watajibu mapigo kwa kuja na “bibi wa mabomu yote”).Wajuzi wa mambo wanadai kuwa miongoni mwa mambo yanayoichochea Russia kuelekeza nguvu zake kwenye uboreshaji wa teknolojia ya silaha ni faida kubwa inayopata nchi hiyo kwenye biashara ya mafuta na gesi,na ukweli kwamba Rais Putin alikuwa shushushu mwandamizi ndani ya shirika la kijasusi la uliokuwa Muungano wa Jamuhuri za Kisovieti (USSR) ambapo shirika hilo lilikuwa sehemu muhimu ya maendeleo ya teknolojia ya silaha.
Habari nyingine “nyepesi” kutoka Russia zinasema kwamba jiji la Ulyanovsk nchini humo limetoa “off” kwa wafanyakazi wote ili wapate fursa ya kufanya tendo la ndoa katika maadhimisho ya “Siku ya Kutunga Mimba jijini Ulyanovsk” (the Day of Conception in Ulyanovsk).Ruhusa hiyo ya mapumziko imetolewa kama sehemu ya mpango wa manispaa ya jiji hilo ujulikanao kama “Give Birth to a Patriot” (Zaa Mzalendo) ambapo watakaofanikiwa kudunga au kudungwa wanaweza kuibuka na zawadi ya gari,fedha au friji.Jiji hilo ndipo alipozaliwa Vladmir Lennin, na mpango huo wa kuhamasisha uzazi ni sehemu ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Lenin mwezi huu.Washindi wanatarajiwa kupatikana kwa kuzingatia heshima ya ndoa yao pamoja na sifa bora kama wazazi,na watapatikana kutokana na maamuzi ya jopo la majaji.Mambo hayo!!

Kabla ya kugeukia masuala ya huko nyumbani,ngoja nizungumzie suala moja ambalo mie binafsi linanigusa.Nilipokuwa Mlimani (UDSM) nilibahatika kuchukua somo liitwalo “Gender and Family Relations” (yaani Jinsia na Mahusiano ya familia).Naomba kukiri kwamba kabla ya hapo,sikuwa na uelewa wa kutosha kuhusu nafasi ya mwanamke katika jamii na picha nzima ya usawa wa kijinsia katika jamii mbalimbali.Sasa majuzi nilisoma gazeti la Guardian la hapa Uingereza na kukutana na habari isemayo kwamba serikali (ya hapa) ina mpango wa kuwachukulia hatua wanaume wanaonunua huduma ya ngono.Kimsingi,huduma nyingi,ikiwemo ngono,huhusisha mtoaji huduma na mpokeaji huduma,lakini katika dunia yetu ambayo tumezowea kuyaona makosa ya wanawake pekee ilhali yetu wanaume yakionekana ni ya “ya kishujaa,” suala la ukahaba limeendelea kwa kiasi kikubwa kuwa kosa la wanawake wanaojihusisha na biashara hiyo kuliko wateja wao ambao ni wanaume (hapa sizungumzii ukahaba kati ya watu wa jinsia moja).Neno “malaya” ni maarufu zaidi kuliko neno “fuska” na baadhi ya wachambuzi wa mahusiano ya jamii wanadai hiyo inasababishwa na tabia ya kuona matendo hasi (negative) ya mwanamke kuwa mabaya zaidi ya yale hasi ya mwanaume.Hata linapokuja suala la nyumba ndogo,tunashuhudia kuwa ni rahisi kwa mwanaume kuwa nazo hata 10 kama ana uwezo wa kuzimudu lakini mwanamke akijaribu hilo basi muda si mrefu anaweza kujikuta anafungashiwa virago vyake.Nchi za Magharibi zimepiga hatua flani katika kuleta usawa wa kijinsia,na miongoni mwa mitihani mikubwa katika eneo hilo ni ugombea (candidacy) wa Hillary Clinton kwenye kinyang’anyiro cha kuteuliwa kuwa mgombea urais wa Marekani kwa tiketi ya chama cha Democrat.Na mshawasha zaidi unaeletwa na mgombea mwingine kutoka jamii ambayo hadi sasa bado inaonekana ni ya kuongozwa zaidi badala ya kuongeza,yaani watu weusi (Blacks).Historia inasubiri kuandikwa iwapo Hillary atafanikiwa kuwa mwanamke wa kwanza kuwa rais wa Marekani,au Barack Obama atafanikiwa kuwa Mweusi wa kwanza kuwa rais.Bibi,mama na dada zetu wanastahili pongezi (au hukumu) sawa na sie akina kaka,baba na babu.

Sasa mambo ya huko nyumbani.Nilipigwa na butwaa niliposoma habari katika gazeti moja la nyumbani kuwa huko Mwanza kampeni za kugombea uongozi wa CCM ziligeuka kuwa uwanja wa vita pale washabiki wa kambi za wagombea flani walipoamua “kufanyiana kweli” na kutupiana mawe.Sijui wangapi walijeruhiwa katika patashika hiyo lakini nachoshindwa kuelewa ni namna kila raslimali,ikiwemo vurugu,inavyotumika kutafuta uongozi wa kisiasa.Hivi kuna nini huko kwenye uongozi hadi watu watake kutoana roho?Yaani ukereketwa umekolea namna hiyo hadi watu wawe tayari kuweka rehani usalama wao kwa ajili ya mgombea flani?Cha kusikitisha ni kwamba si ajabu wapambe hawa hawa ndio watakuwa wa kwanza kulalamika kuwa mgombea wao “hafai” pale atapowatelekeza baada ya kupata anachohitaji (uongozi).Pasipo busara za haraka kutumika tunaweza kujiwekea katika mahali pabaya sana kama tutawaruhusu baadhi ya watu kuhatarisha amani kwa vile tu wanataka kupata uongozi.

Nimesoma pia ushauri wa aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM,Philip Mangula,ambaye baada ya kubwagwa huko Iringa alitahadharisha kwamba kuna wakati itafika uongozi wa chama hicho utagombewa kwa mfumo wa tenda (bid) na “bidder” mkubwa ndiye atakayeibuka kidedea.Pengine ana hoja ya msingi hapo,lakini inaweza kufunikwa na ukweli kwamba haya anayoyaona sasa yamekuwa yakitokea kwa muda mrefu,na kipindi hicho alikuwa katika nafasi nzuri zaidi ya sio tu kukosoa bali hata kukomesha matumizi ya “takrima” kwenye kusaka uongozi.Hata wazo lake kwamba ni vema kwa wanachama wa CCM wenye madaraka mengine (kama ubunge au uwaziri) wakatoa mwanya kwa wale wasio na madaraka (japo sio kosa,si ajabu baada ya uchaguzi huu kumkuta mtu akiwa na vyeo zaidi vitano) mawazo hayo yangekuwa na “mwangwi” mkubwa zaidi iwapo yangetolewa katika kipindi ambacho Mangula alikuwa madarakani.Yayumkinika kusema kuwa ni vigumu kurekebisha mapishi pindi ukiwa nje ya jiko,na majaribio ya kufanya hivyo nje ya jiko yanaweza kutafsiriwa tofauti na baadhi ya watu.

Na huko Morogoro,baada ya kushindwa kwenye uchaguzi wa miongoni mwa nafasi katika mkoa huo,Waziri Ngasongwa nae “aliwatolea macho” TAKUKURU kwa kile alichodai walishindwa kuzuwia baadhi ya wagombea kutoa “takrima” kwa wapiga kura.Swali pana zaidi ni je waziri anadhani taasisi hiyo ilishindwa (kwa mujibu wake) kutekeleza majukumu yake kwa vile ni sehemu ya mapungufu yake ya kila siku au ni katika tukio hilo tu?Iwapo jibu ni hilo la pili basi wapo wanaoweza kuhisi kuwa waziri ameweza kuona matatizo hayo kwa vile tu yamemgusa yeye binafsi. “Bottom line” ni kwamba iwapo mlolongo wa vimbwanga vinavyoendelea kwenye uchaguzi wa CCM vitachukuliwa kuwa ni mambo ya kawaida tu basi tunaweza kufika mahala tukajilaumu huku tukisema “laiti tungejua wakati ule…”Bahati mbaya,kwa wakati huo tutakuwa tumechelewa kuweza kufanya mabadiliko yoyote ya msingi.Ushauri huu sio wa kupandikiza chuki bali ni kwa ajili ya hatma ya taifa letu kwa manufaa yetu sasa na kwa vizazi vijavyo.

Neno la mwisho kabisa ni kuungana na wapenzi na mashabiki wa msanii maarufu anti Shenaz ambaye alikutana na mauti kwenye ajali ya basi huko Mbeya.Kwa tunaomfahamu,dada huyo alikuwa akipendezesha kila shughuli aliyokuwepo.Na tofauti na umaarufu wake,alikuwa mcheshi na asiye na chembe ya dharau.Mungu airehemu roho ya marehemu,Amina.

Alamsiki


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.