Showing posts with label NYERERE. Show all posts
Showing posts with label NYERERE. Show all posts

5 Apr 2014


Kimsingi, mchakato wa kupata Katiba mpya umegeuka kuwa hukumu ya Muungano wa 'Tanganyika' (Tanzania Bara) na Zanzibar. Mengi yamesahongelewas na nisingependa kuyarudia hapa, lakini suala jipya lililojitokeza ni sahihi za Marehemu Baba wa Taifa na Marehemu Karume.

Kuna taarifa kwamba baadhi ya nyaraka hazina sahihi ya Marehemu Karume, hali inayoweza kuashiria kuwa uamuzi wa Muungano ulifanywa na Nyerere pekee. Japo historia inaeleza tofauti, kwa kawaida, hati ya mkataba huwa na angalau na sahihi za wahusika wawili au zaidi kutegemea mazingira ya mkataba husika.

Lakini hata hiyo sahihi ya Nyerere yenyewe imezua utata. So far, kuna sahihi mbili (yawezekana zipo nyingine). Lakini sio tu sahihi kuwa zaidi ya moja, katika moja ya nyaraka za Muungano kuna maneno yameongezwa. Maelezo yanayotolewa ni kuwa kompyuta ilitumika...bila hata kuuliza kompyuta ilitumika kwa malengo gani, swali la msingi ni je Tanzania- au Tanganyika ilikuwa na kompyuta mwaka 1964?

Licha ya sahihi ya Nyerere, kuna taarifa pia ikwamba hata sahihi ya Katibu wa Bunge wa wakati huo, Pius Msekwa nayo ina walakini. 

Mara kadhaa katika maandiko yangu nimebainisha kuwa haileti maana kujadili muundo wa Muungano pasipo wajjumbe wa Bunge la Katiba kupatiwa nyaraka muhimu zinazohusu Muungano huo. Maelezo yaliyotolewa na wahusika ni kwamba eti kuna nakala moja tu ya moja ya nyaraka muhimu za Muungano, kwahiyo haiwezi kupelekwa Dodoma kwa kuhofia inaweza kupotea. Huu sio utoto tu bali ni ubabaishaji wa hali ya juu. Kwanini wahusika wasichapishe nakala kisha kuzi-certify as true copies of the original?

Anyway, hebu analia katika picha ya hapo juu kuhusu ipi ni sahihi halisi ya Mwalimu Nyerere.

Nihitimishe bandiko hili kwa kuyumkinisha kuwa utata unaojitokeza kuhusu nayaraka muhimu za Muungano unaashiria kwamba kuna mtu flani mahala flani anaongopa (someone somewhere is lying). Tusichojua ni kwanini?

TIME WILL TELL 

14 Oct 2008

27 Jun 2008

Katika toleo la wiki hii la jarida la Raia Mwema nazungumzia dalili zakutimia kwa utabiri wa Mwalimu Nyerere kwamba upinzani wa kweli unaweza kutoka ndani ya CCM.Kwa namna mambo yanavyokwenda mramba ndani ya chama hicho nidhahiri kwamba kuna tofauti kubwa za kiimani na kimtazamo miongoni mwa viongozi wake.Ili kutokukunyima uhondo zaidi,bingirika na makala hiyo,pamoja na nyinginezo zilizopanda vidato,kwa KUBONYEZA HAPA

2 Mar 2008

MTANZANIA UGHAIBUNI

Sakata la mkataba wa Kampuni ya Richmond linaelekea kuchukua mwelekeo mpya kila kukicha. Ni rahisi kutafsiri kwamba suala hili lisipopatiwa ufumbuzi wa kudumu linaweza kuwa na madhara makubwa kwa nchi na kwa chama tawala, CCM.

Tangu ripoti ya “Tume ya Mwakyembe” ilipowekwa hadharani katika kikao kilichopita cha Bunge la Jamhuri ya Muungano, kumejitokeza kauli kadhaa za utatanishi ambazo japo zinaweza kuwa ni za kawaida tu, tafsiri ya ndani inaashiria matatizo makubwa huko tuendako.

Naomba niwe muwazi zaidi katika makala hii, na ningependa kutamka bayana kwamba sina nia ya kumshushia heshima yeyote nitakayemtaja. Lengo kuu la makala hii ni kuikumbusha kila pande inayoguswa na sakata hilo kutambua kwamba taifa letu ni muhimu zaidi kuliko maslahi ya mtu mmoja.

Naikumbuka sana siku taifa lilipotangaziwa kifo cha Baba wa Taifa.Watanzania wengi walitokwa na machozi sio tu kwa vile hawangemwona tena Mwalimu bali pia ni ile hali ya kutokuwa na uhakika taifa letu lingekuwaje bila Nyerere.Naamini kwamba laiti Mwalimu angekuwepo, baadhi ya upuuzi kama huo wa mkataba wa Richmond wala usingetokea, lakini ndio hivyo tena, hatuko naye duniani.

Wanaoilaumu “Tume ya Mwakyembe” kuwa imewaonea wanasahau kwamba tume hiyo haikuundwa baada ya Mwakyembe na wenzake kutuma maombi ya kuwa kwenye tume hiyo.Inashangaza wanaolalamika sasa kwamba ripoti ya tume hiyo ilikuwa na ajenda za kumalizana kisiasa,ilhali hawakuipinga wakati inaundwa na pale ilipokuwa ikitimiza majukumu yake.Ina maana ajenda hizo za kisiasa zilianza baada ya akina Mwakyembe kuwa wajumbe wa tume au zilikuwapo kabla.Kama zilikuwapo kabla,kwanini basi waliotajwa kuhusika na kuliingiza taifa katika hasara kubwa kwa mkataba huo wa kizembe hawakulalamika?

Na iwapo ajenda hizo zilianza baada baada ya wajumbe hao kuingia kwenye tume,kwanini basi watajwa walikimbilia kujiuzulu (huku wengine wakigoma waziwazi kujiuzulu kwa kuendelea kung’ang’ania madaraka) badala ya kudai haki itendeke?Ni rahisi kuhitimisha kuwa kelele zinazoendelea hivi sasa ni za mfa maji.

Nakumbuka kwenye miaka ya tisini nilipokuwa mwanafunzi wa sekondari ya wavulana ya Tabora (Tabora Boys) tulibahatika kutembelewa na Komandoo Salmin Amour.Nayakumbuka baadhi ya maneno yake ambayo kimsingi yalikuwa na lengo la kutupa changamoto ya mafanikio ya kielimu na hatimaye kufanikiwa maishani (japo sio kila mara kufanikiwa kielimu ni tiketi ya moja kwa moja ya kufanikiwa kimaisha).Alitueleza kwamba madaraka ni mazuri na kutupa mifano ya namna yeye kama rais alivyokuwa na wasaidizi kibao wa kuhakikisha kila kitu kinakwenda vema.

Nilikubaliana na Komando wakati huo,na nakubaliana nae sasa,kwamba madaraka ni mazuri na matamu,na ndio maana tunashuhudia hizi kelele zinazoendelea kutoka kwa waliokumbwa na zahma ya kisiasa baada ya skandali ya mkataba wa kampeni ya Richmond.Hakuna dhambi kwa madaraka kuwa matamu kwani hata njia ya kuyafikia sio nyepesi.Inahitaji jitihada na juhudi za kutosha kufikia hatua ya kuongoza watu wenye akili timamu.Na inatarajiwa kwamba mtu akishapata bahati ya kuwa kiongozi atatambua kwamba wengi,kama sio wote,wa aliokuwa akiwaongoza ni watu wenye akili timamu,uwezo wa kufanya maamuzi na wanaostahili heshima.

Waziri Mkuu aliyepita,Edward Lowassa,ameendelea kuonyesha kwamba japo aliamua kubwaga manyanga kwa hiari yake,alifanya hivyo huku roho ikimuuma.Nasema hivyo kwa sababu kauli zake za hivi karibuni zinaashiria wazi kwamba bado ana kinyongo kikubwa na matokeo ya uchunguzi wa “Tume ya Mwakyembe.”

Lowassa anaamini kwamba atarejea tena kwenye ulingo wa juu wa kisiasa kama Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi ambaye alipokuwa Waziri alilazimika kujiuzulu kutokana na skandali iliyoikumba Wizara yake.Tofauti ya msingi kati ya Mwinyi na Lowassa ni ukweli kwamba wakati Mwinyi alijiuzulu kutokana na tukio lililotokea mbali kabisa na mahala alipokuwa akifanyia kazi (lilitokea Shinyanga wakati ofisi ya Mwinyi ilikuwa Dar es Salaam),Lowassa alijikuta akikumbwa na shutuma kuhusu mkataba huo kwa vile katika hatua flani ulipita machoni mwake na akaamua “kusikiliza maamuzi ya wataalamu.”

Uongozi ni pamoja na kuwa na maamuzi ya haraka na yanayoangalia athari zinazoweza kujitokeza mbeleni iwapo yatafanyika maamuzi potofu.Haiyumkiniki kwamba Waziri Mkuu mzima anaweza kusikiliza ushauri mbovu na kuafikiana nao pasipo kujiridhisha iwapo ushauri huo ni wa manufaa kwa taifa.Hilo pekee linamvua sifa ya uongozi mtu yeyote aliye katika nafasi ya juu kitaifa.

Hivi kama mkataba wa Richmond ungekuwa na madhara ya moja kwa moja kwa familia ya Lowassa,kiongozi huyo angeendelea kusikiliza ushauri asio na uhakika na matokeo yake au angetaka kujiridhisha kwamba kilichokuwa kikifanyika hakingekuwa na madhara kwa familia yake?

Tukimweka kando Lowassa kwa muda,tumeshuhudia vituko vingine kutoka kwa Mkurugenzi wa TIC Emmanuel Ole Naiko ambaye anadai kuna dalili za “mauaji ya halaiki” dhidi ya watu wenye asili ya wilaya ya Monduli.Hizi ni hoja mufilisi ambazo kama zitaachwa bila kudhibitiwa zinaweza kuliingiza taifa kwenye matatizo yasiyo na msingi.


Hivi Ole Naiko amefanya utafiti wa kutosha kiasi gani kuthibitisha kwamba kuna mpango wa “ethnic cleansing” dhidi ya watu wa Monduli?Kwa hakika serikali inapswa kumhoji kwa undani mtu huyu mwenye heshima kubwa ndani na nje ya nchi kutokana na matamshi hayo ambayo yanaweza kabisa kuathiri hata utendaji wa ofisi yake (hakuna mwekezaji aliye tayari kuwekeza kwenye nchi inayoelekea kwenye “ethnic cleansing.”)

Kuna tetesi kwamba upo mkakati mkubwa wa “kujibu mashambulizi” dhidi ya ripoti ya “Tume ya Mwakyembe.” CCM imekuwa ikituaminisha kila siku kwamba vikao nje ya chama ni majungu,sasa basi inapaswa kuhakikisha kwamba wote wenye kudhani hawakutendewa haki wawasilishe malalamiko yao kwa ngazi hsuika katika chama hicho au hata bungeni.

Kama taarifa tunazozisoma katika vyanzo mbalimbali kwamba kuna mgawanyiko mkubwa ndani ya CCM kutokana na skandali la Richmond zina ukweli, basi ni muhimu kwa uongozi wa juu wa chama hicho kuachana na itifaki zake za kawaida za kuwasifia hata wanaostahili kukemewa na badala yake kuwawekwa “kiti moto” waeleze malalamiko yao mbele ya vikao halali badala ya kuendeleza mbinu za chini chini ambazo zinaweza kabisa kuathiri hali ya usalama wa nchi yetu.

Tusirejee makosa yaliyojitokeza katika mkataba wa Richmond ambapo baadhi ya watu walitahadharisha mapema kuhusu uhalali wa kampuni hiyo lakini wakapuuzwa.Kuna watu wanataka urais kwa kutimia njia yoyote ile hata kama kwa kufanya hivyo wanahatarisha uhai wa chama.

Lakini wakati tunawalaumu wanaolalamika kwamba wameonewa na “Tume ya Mwakyembe” tunapaswa pia kujiuliza kama hawapati jeuri hiyo kutokana na uzembe unaendelea wa kutowachukulia hatua wahusika.Pengine jeuri waliyonayo inatokana na ukweli kwamba wanaamini kuwa hakuna mwenye jeuri ya kuwachukulia hatua hasa ikizingatiwa kuwa baadhi yao wameishia kupongezwa kwa “ushujaa wao” badala ya kushutumiwa kwa hasara waliyoisababisha kwa taifa.

Nadhani anachopaswa kufanya Lowassa,Ole Naiko na wengine wote waliohusishwa na mkataba wa Richmond ni kutafuta msaada wa kisheria kuona haki inatendeka upande wao iwapo wanaamini kuwa hawakutendewa haki,badala ya kuendeleza hizi porojo ambazo kwa hakika zinaweza kuua kabisa ndoto zao za kurejea kwenye ulingo wa juu wa siasa za nchi yetu.Mahakama zipo,vikao vya chama vipo,sasa kwanini kelele za kuonewa zisipelekwe huko?TANZANIA NI MUHIMU ZAIDI KULIKO MASLAHI YA MTU BINAFSI.

BAADA YA KUMALIZA KUSOMA MAKALA HII,UNAWEZA KUANGALIA VITUKO VYA SIASA ZA URUSI AMBAVYO VIMEZAA TERM MPYA YA NANO PRESIDENT (as in iPod Nano).BONYEZA HAPA

HALAFU KWA WALE AKINA DADA "WENYE ULIMI MZITO",CLIP IFUATAYO INAWEZA KUWA YA MSAADA WA INA FLANI



14 Feb 2008





KATIKA TOLEO LA WIKI HII LA GAZETI LA RAIA MWEMA,MAKALA YANGU INAZUNGUMZIA YALIYOJIRI KUTOKANA NA SAKATA LA RICHMOND.KWA SABABU ZILIZO NJE YA UWEZO WANGU,MAKALA HIYO HAIKO KWENYE ONLINE VERSION YA GAZETI HILO.PIA KWA VILE VICHWA VYA MAKALA ZANGU HUWEKWA NA MHARIRI KUNA UWEZEKANO KICHWA CHA HABARI KILICHOPO KWENYE PRINTED VERSION YA GAZETI NI TOFAUTI NA CHA HAPO JUU.

Nianze makala hii kwa kutoa pongezi tatu muhimu. Kwanza, kwa Mheshimiwa Mizengo Pinda kwa kuteuliwa kuwa Waziri Mkuu.CV yake katika utumishi wa umma “imetulia”.

Pili, nampongeza “mwana wa pakaya” ("mtoto wa nyumbani" kwa Kindamba), Jaji Kiongozi mpya Salum Masati, mzaliwa wa Ifakara, ambaye kuteuliwa kwake kumeuweka mji huo katika ramani ya uongozi wa kitaifa (angalau sasa Ifakara inaweza kujulikana kitaifa kwa jambo zaidi ya mchele na mafuriko ya Mto Kilombero.) 

Tatu, ni pongezi kwa mashujaa wote “walioshikia bango” suala la Richmond.Mungu awazidishie ujasiri zaidi na kuwapa ulinzi wake dhidi ya hujuma za mafisadi. Kwa kelele za kizalendo kama za akina Mheshimiwa Anne Kilango, tunaamini kuwa maslahi ya taifa yatawekwa mbele katika mjadala wa ufisadi wa BoT

Binafsi, sakata la Richmond liliniingiza kwenye msukosuko mkubwa baada ya “kupiga ngumi chini ya mkanda”. Novemba mwaka 2006,niliandika makala katika gazeti flani la huko nyumbani. Makala hiyo ilitokana na habari kwamba aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa, angefanya kikao na wabunge wa CCM kuandaa mkakati wa kuzima mjadala bungeni kuhusu suala la Richmond. 

Katika makala yangu, nilikosoa utaratibu uliozoeleka wa viongozi wa CCM kuitisha vikao “vya kuwaziba midomo” wabunge wake kila linapojiri jambo linalogusa hisia za wengi. Sikuona mantiki ya Lowassa kuwaita wabunge wa chama chake kuwaweka sawa kwani tatizo la umeme lilikuwa mwiba mkali kwa Watanzania wote bila kujali itikadi zao za kisiasa. Kikao kilifanyika na agizo la kuweka mbele maslahi ya chama lilizingatiwa,na hatimaye ishu ya Richmond haikujadiliwa.

Kilichopuuzwa wakati huo ni hekima kwamba kuficha ugonjwa hakusaidii kuponya maradhi. Pengine suala hilo lingejadiliwa muda huo wala tusingefika hapa tulipo sasa. Waingereza wana msemo “sehemu mbaya ya uamuzi mbovu ni pale inapofika hatua ya kuujutia”. 

Pamoja na kushutumu mtindo huo wa kuwekana sawa ambao naamini unatumiwa kuficha maovu, makala yangu pia iligusia staili ya uongozi wa Lowassa ya kuwaumbua hadharani baadhi ya watendaji kwa madai ya utendaji wao mbovu wa kazi. 

Japo alikuwa sahihi kukemea viongozi wasiowajibika ipasavyo, kuwaumbua hadharani ulikuwa mkakati dhaifu wa kujitafutia umaarufu wa kisiasa. Nilieleza kwamba zilikuwapo fursa mbalimbali kwa Lowassa kuwakaripia, kuwakosoa au hata kuwaumbua viongozi hao (kwa mfano kuwaita ofisini kwake, kuwaandikia maonyo au hata kuwapigia simu) pasipo haja ya kufanya hivyo kwenye mikutano ya hadhara. Nilihofia kwamba licha ya kuwashushia hadhi watendaji walioumbuliwa hadharani, staili hiyo ya Lowassa ingeweza kutafsiriwa kuwa ni mbinu ya kujitafutia umaarufu wa kisiasa machoni mwa wananchi ilhali tatizo liko kwenye mfumo wa uongozi. 

Siku chache baadaye, Mwandishi wa Habari wa aliyekuwa Waziri Mkuu, Saidi Nguba, alijibu makala yangu gazetini (na baadaye kunitumia barua pepe na comments kwenye blogu yangu) kumtetea bosi wake huku akidai suala la CCM kuitisha vikao vya ndani ni utaratibu walijiwekea wao wenyewe na haulengi kuwaziba midomo wabunge kwa vile “wabunge tulionao si watu wa kuzibwa midomo.” 

Mwanahabari huyo alitoa orodha ndefu ya “mafanikio” ya Lowassa ikiwa ni pamoja na idadi ya wanafunzi waliopata nafasi za kuendelea na masomo (japo hakugusia upungufu wa walimu, madawati, nk.) Alimalizia kwa kunikumbusha kuwa kama mwanafunzi niliyeko nje ya nchi nikisomeshwa kwa fedha za Watanzania masikini ninapaswa kufanya utafiti wa kutosha kabla ya kukosoa “mambo nisiyoyajua.”

Nilimjibu kwa kumfahamisha kwamba kuwa mwanafunzi ninayesomeshwa kwa fedha za walipa kodi masikini ni sababu tosha ya kukemea mambo mabovu ili kuhalalisha kwamba fedha inayotumika kunisomesha haipotei bure.

Pia nilimfahamisha kwamba wazazi wangu ni miongoni mwa Watanzania hao walipa kodi masikini, na kama masikini na walipa kodi wengine, wana haki ya kufahamu na kukosoa utendaji wa serikali waliyoiweka madarakani. Kuhoji utendaji wa serikali sio upinzani, na hata kama ungekuwa ni upinzani basi ni kwa manufaa ya Taifa letu.

Kusomeshwa kwa fedha za masikini haimaanishi anayesomeshwa asitoe mawazo yake (usahihi au upotofu wa mawazo hayo ni suala jingine). Nilipingana na utetezi wake kuhusu “mafanikio” ya staili ya Lowassa kuwaumbua baadhi ya watendaji hadharani na kumkumbusha kuwa hata Rais akitaka kumkosoa Waziri Mkuu wake hatofanya hivyo hadharani bali atamwita chemba. 

Mwandishi huyo mkongwe atakubaliana nami kwamba wakati Lowassa alituaminisha majukwaani kuwa ni “Sokoine mpya” (kwa kuwabana viongozi wazembe papo kwa hapo), “nyuma ya pazia” hakuwa tofauti na hao aliokuwa akiwaumbua hadharani kwani uoza wa Richmond umetokea ofisini kwake.

Naamini (mwandishi huyo) alikuwa akitekeleza tu majukumu yake ya kazi. Pengine moyoni aliafikiana na hoja zangu lakini ulikuwa ni wajibu wake kumtetea bosi wake. Natamani kusikia maoni yake sasa yake kuhusu sakata zima la Richmond.Naamini kwamba wengi wa watetezi wa mkataba huo sasa wataona mantiki za makelele yetu.

Hatimaye Lowassa amejiuzulu huku akijitetea kwamba suala zima la Richmond lilikuwa njama za watu waliokuwa wanataka Uwaziri Mkuu. Kuna msemo wa kiingereza kwamba “hukumu ya umma ni mbaya zaidi ya ile inayotolewa mahakamani.”

Wakati Lowassa anailamu Kamati ya “Kamati ya Mwakyembe” kwa kutompatia nafasi ya kujitetea, kelele zilizosikika mitaani kusherehekea kujiuzulu kwake ndio “hukumu ya umma” huku wengine wakidai kuwa Mzimu wa Nyerere “umemrudi.” 

Hivi mwongozo wa Bunge unasemaje pindi Mbunge anapoituhumu Tume Teule ya Bunge kuwa imesema uongo (kama alivyodai Lowassa)? Wakati nakerwa na UNAFIKI wa kupongeza “ushujaa wa Lowassa kujiuzulu”, ni muhimu Lowassa athibitishe uongo wa tuhuma dhidi yake kwani kama hoja ni kutoitwa kujitetea basi hata Zitto Kabwe alisimamishwa ubunge bila kupewa fursa ya kujitetea. 

Na kwanini alikimbilia kujiuzulu badala ya kudai haki yake, kama kweli aliamini ameonewa? Iweje Kazaura na Msabaha na wengineo wakati walipohojiwa nje ya kiapo waashirie mhusika ni Lowassa na sio mtu mwingine katika kabineti lenye mawaziri 60?Naamini kilio cha Lowassa kimesikika kwa vyombo vya dola. Niandike kwa herufi kubwa: LOWASSA ANAHITAJI KUHOJIWA.

Apewe haki hiyo anayodai kunyimwa na Kamati ya Bunge, lakini pia umma pia unahitaji hivyo kuhusu hizo shs milioni 152 kwa siku za Richmond. Wote waliohusika katika skandali hilo wana uhaba mkubwa wa uzalendo. Walithamini zaidi matumbo yao (na pengine “nyumba ndogo” zao) kuliko maisha ya Watanzania wenzao.

Hakuna haja ya kuwapeleka jela kwani watatuongezea tu gharama ya kuwahudumia chakula gerezani. La muhimu ni kuwafilisi kila walichovuna kwenye “dili” hilo. Katika hili, tuweke pembeni sheria za mapatano (laws of reconciliation) za Agano Jipya na kurejea kwenye sheria za kisasi (laws of retaliation) za Agano la Kale, yaani jino kwa jino na jicho kwa jicho. Wametufilisi nasi lazima tuwafilisi.

KUNA MWANANCHI AMENITUMIA E-MAIL YENYE UJUMBE WA KUFURAHISHA KWA NAMNA FLANI.IKO KWENYE POWERPOINT FORMAT.

11 Feb 2008

Uongozi wa kisiasa wa Tanzania,kama ilivyo sehemu mbalimbali duniani,umekuwa ukitegemea watu kutoka fani mbalimbali za maisha.Tuna viongozi wa dini (kama Mchungaji Lwakatware),Wasomi (kama Prof Mwandosya,Prof Msola,Prof Mwakyusa),wanajeshi (kama Kapteni John Komba,Kapteni Jaka Mwambi,Luteni Yusufu Makamba) na hata wasanii kama Khadija Kopa .Hivi karibuni,JK alielezea kutoridhishwa kwake na athari zinazoweza kutokana na kuwa na viongozi ambao pia ni wafanyabisahara.Ana hoja ya msingi hapo,lakini nadhani tatizo la msingi sio fani aliyotoka au anayoendela nayo kiongozi husika bali ni utashi alionao katika kuwahudumia Watanzania wenzake.Kadhalika,mkanganyiko uliopo kwenye kanuni za maadili ya uongozi ziko shaghala baghala,hasa baada ya kuuawa kwa Azimio la Arusha na kuzaliwa Azimio la Zanzibar.Endelea na makala yangu hii kwenye gazeti la Mtanzania.
MTANZANIA UGHAIBUNI-

Watanzania wengi wameipokea kwa furaha kauli ya Rais Jakaya Kikwete kuhusu umuhimu wa kutenganisha biashara na utumishi wa umma.Ni kauli mwafaka kwani hata katika Maandiko Mtakatifu tunafundishwa kwamba ni vigumu kutumikia mabwana wawili.

Naamini kwa mtazamo wa wengi,wafanyabiashara kama Watanzania wengine wana kila haki ya kushiriki katika shughuli za siasa ikiwa ni pamoja na kugombea ubunge au hata kuteuliwa mawaziri.Tatizo linakuja pale maslahi ya biashara zao yanapoingiliana na utekelezaji wa majukumu yao katika kuuhudumia umma.

Inaweza kuwa sio sahihi kuwalaumu wafanyabisahara wanaochanganya biashara na siasa pale ilhali hakuna miongozo maalumu (kama ya Marekani na Uingereza).Ndio maana wazo la kufanyika mchakato wa kuleta sheria na kanuni zitakazoweka bayana mazingira ambayo kwa upande mmoja hayatawanyima nafasi wafanyabiashara kushiriki kwenye siasa,na upande mwingine biashara zao kutoathiri majukumu waliyokabidhiwa na taifa,lina umuhimu mkubwa.

Pamoja na pongezi hizo ni muhimu kuangalia chanzo cha tatizo lililopo hivi sasa.Ni ukweli usiopingika kwamba wakati wanasiasa wengi wameendelea kuhubiri kwamba siasa ya Ujamaa na Kujitegemea bado ni mhimili wa taifa letu,hali halisi tuliyo nayo sasa inapingana kabisa na matamshi hayo.

Azimio la Arusha lilisaidia kuweka wazi mwelekeo wa taifa letu.Makala moja kama hii haiwezi kutosha kuelezea undani wa Azimio hilo lakini kilicho wazi ni kwamba Baba wa Taifa,ambaye kimsingi ndiye anayekubalika kama mwasisi wa itikadi hiyo,alikuwa na ndoto ya kuona jamii ya Watanzania inayoishi kwa usawa na haki.

Baadaye likaja Azimio la Zanzibar.Pengine mie ni mzembe wa kujua kilichomo katika Azimio hilo lakini naamini kwamba kuna Watanzania wengi ambao hadi leo hawajui kilichomo kwenye Azimio hilo.Labda ni kutokana na ufahamu mdogo uliopo miongoni mwa wananchi wengi kuhusu Azimio la Zanzibar ndio maana wengi wetu tunarahisisha majibu kwamba lilikuwa tamko rasmi la kifo cha Azimio la Arusha.Na katika hili,CCM inastahili kubeba lawama zote kwani haijafanya jitihada zozote za makusudi kuuelewesha umma kuhusu madhumuni na kulichomo kwenye Azimio hilo (la Zanzibar).

Kuna mapungufu makubwa katika suala zima la uwazi pindi yanapojiri masuala nyeti kwa taifa letu.Mfano mzuri ni kwamba wengi wetu tulikuwa hatufahamu kwamba hadi uteuzi wake unatenguliwa na Rais,aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu aliyeondolewa madarakani,Dkt Daudi Ballali,hakuwa mtumishi wa serikali.Pengine taratibu zinasema hivyo lakini kwa vile mtu anayekalia nafasi hiyo ndiye mwenye kushika dhamana ya fedha za Watanzania wote,nadhani kulikuwa na kila sababu ya wenye fedha zao (Watanzania) kufahamishwa kuhusu hilo badala ya kusubiri mpaka litokee tatizo la ufisadi kwenye taasisi hiyo muhimu kwa taifa.

Hadi muda huu,ukiwauliza viongozi wa CCM kwamba je Azimio la Arusha bado ni mwongozo muhimu kwa maendeleo na mwelekeo wa taifa,sanasana utachoambulia ni hadithi ndefu zisizotosha kutoa jibu moja la kueleweka.Ni dhahiri muuliza swali atakumbana na ugumu wa aina hiyohiyo pindi akiuliza iwapo nchi yetu bado inafuata siasa ya Ujamaa na Kujitegemea.Na haiishii hapo kwani majibu yataendelea kuwa tete pindi mtu akiuliza iwapo CCM bado ni chama cha wakulima na wafanyakazi.

Na ni katika hilo la wakulima na wafanyakazi ndipo napoona kuna tatizo la msingi.Inasemekana Azimio la Zanzibar lilihalalisha watumishi wa umma (wafanyakazi) kumiliki mali kinyume na katazo lililowekwa na Azimio la Arusha.Laiti wakati wanasiasa wetu walipokutana Zanzibar kuua Azimio la Arusha wangeangalia mbali,ni dhahiri wangebaini uwezekano wa kutokea mgongano kati ya biashara na utumishi wa umma.Haraka ya kupitishwa Azimio hilo inaweza kuwa sababu muhimu ya wanasiasa hao kutoangalia mbali.Lakini pia haraka hiyo inaweza kuwa ilichochewa na ukweli kwamba wakati wanasiasa wengi walikuwa wakituimbia ngonjera za Ujamaa na Kujitegemea majukwaani,majumbani mwao walikuwa wakicheza ngoma za ubepari.

Dhana hapo ni kwamba Azimio la Zanzibar lilipitishwa chapchap ili wajamaa wa hadharani waliokuwa mabepari wa kificho waweze kuendesha maisha yao bila hofu na bughudha ya kuonekana wanatenda kinyume na imani ya taifa letu kwa wakati huo.Hawa ni pamoja na wale ambao walikuwa wakituaminisha kwamba ni watu wa karibu na Baba wa Taifa kumbe moyoni walikuwa wakiomba dua Mwalimu aondoke madarakani ili watumie vile walivyokuwa wakikusanya kwa kificho katika zama hizo za Ujamaa na Kujitegemea.Na wengine japo Mwalimu aliwasaidia kuwaingiza madarakani akidhani ni waumini wa siasa zake,wamestaafu wakiacha skandali lukuki.

Kama kuna madhara mabaya zaidi ya mfumo wa chama kimoja basi ni kule kutoruhusu mawazo tofauti na ya watawala,hata kama mawazo hayo ni ya kuchochea maendeleo ya taifa.Kinadharia kila Mtanzania ana uhuru wa kutoa mawazo yake alimradi asivunje sheria halali za nchi,lakini kiuhalisia bado kuna chembechembe zilizorithiwa kutoka katika mfumo wa chama kimoja ambapo mawazo tofauti ni sawa na uhaini.

Katika zama za chama kimoja,hoja kama ile ya “chama kushika hatamu” zilisaidia baadhi ya mafisadi wa wakati huo kupata kinga dhidi ya wale maovu yao.Sote tulikuwa ni Watanzania tusio na tofauti,tunaoamini kwamba ili nchi yetu iendelee tunahitaji ardhi,watu,siasa safi na uongozi bora.Mwalimu aliamini kuwa hiyo ni njia sahihi ya maendeleo kwani alishuhudia namna ilivyofanikiwa sehemu kama China na Cuba.Kosa lake ni kuamini kwamba walio karibu yake walikuwa na imani ya dhati kama yeye.Angalau leo tunawajuwa wanafiki hawa,lakini kwa sababu za “kulinda umoja wa kitaifa” na kutaka “wapumzike kwa amani” tunaendelea kuwaheshimu kwa kutowaumbua hadharani.

Kumkosoa mzazi ni kosa,na kwa mwananchi wa kawaida au hata kiongozi kumkosoa Rais inaweza kutafsiriwa kuwa ni utovu wa nidhamu.Hata hivyo,kutoa ushauri kwa heshima na taadhima ni jambo linalokubalika.Ni kwa kuzingatia hilo ndio maana naamini kwamba wakati Watanzania wengi wanakubaliana na mtizamo wa Rais Kikwete kuhusu kutenganisha siasa na biashara,ni vema katika utekelezaji wa dhamira yake hiyo akaweka maanani namna Baba wa Taifa alivyosalitiwa na baadhi ya watu wake wa karibu.

Nasema hivyo kwa sababu naamini hata zikiwekwa sheria nzuri namna gani za maadili ya uongozi,pasipo kutengeneza mazingira yatakayozuia wasimamizi wa sheria hizo kuzihujumu,itakuwa ni kazi bure.Mwanasiasa anaweza kabisa kutangaza kwamba biashara zake za awali zimekabidhiwa kwa wadhamini flani,lakini pasipo usimamizi mzuri mfanyabiashara huyo anaweza kuendelea kuendesha biashara zake huku akiwa mwanasiasa japo machoni mwa umma anaonekana ametekeleza sheria hiyo tarajiwa ya kutenganisha biashara na siasa.

Mfano mzuri wa ninachosema ni hili sakata linaloendelea la fedha za EPA huko Benki Kuu.Yayumkinika kubashiri kwamba kama itafikia hatua ya watu flani kupelekwa mbele ya vyombo vya sheria,kuna uwezekano watu hao wakawa ni wamiliki “hewa” ambao majina yao yalitumika tu kuficha wamiliki halali.Katika mazingira ambapo taasisi kama TAKUKURU ilikuwa ya kwanza kudai mradi wa Richmond haukuwa na harufu ya rushwa ilhali sasa tunaona suala hilo likiwaka moto huko bungeni,tutarajie nini pindi wakipewa jukumu la kuhakikisha mfanyabishara anayetaka kuingia kwenye siasa kweli amekabidhi biashara yake kwa wadhamini kama sheria itakavyokuwa inataka?

Mwisho,kikao kinachoendelea cha bunge kimeonyesha dalili kwamba baadhi ya wawakilishi wetu wamechoka kupiga mihuri kupitishwa miswada inayoonekana mizuri machoni lakini inaishia kwa mashirika kama ATC kununua ndege mbovu,TANESCO kujikuta hohehahe kwa kulipa madeni yaliyosababishwa na walafi flani wasio na uchungu na taifa au kuletewa umeme hewa ulioahidiwa na makampuni ya kisanii.Hoja hapa sio kuitupilia mbali miswada ya manufaa kwa taifa au kuchochea upinzani dhidi ya serikali bali kuwabana mafisadi wote wananaotumia nyadhifa zao kulikamua taifa letu.
BAADA YA POLITIKI ZA BONGO,HEBU ANGALIA HIZI ZA NAS KUHUSU THE N-WORD


24 Jan 2008

Siku chache zilizopita Wamarekani waliadhimisha siku ya Dakta Martin Luther King Jr,mmoja wa wapigania haki za Waamerika Weusi.Historia inamkumbuka Dkt King (aliyezaliwa mwaka 1929 na kuuawa kwa risasi mwaka 1968)kama nguzo muhimu katika kupigania haki za Waamerika Weusi nchini humo.Pengine kilichomfanya wanaharakati huyo akubalike zaidi ni imani yake ya kudai haki kwa njia za amani.

Miaka mitano kabla ya kuuawa,mwaka 1963,Dkt King alitoa hotuba ambayo hadi leo imeendelea kuwa na mvuto mkubwa sio nchini Marekani pekee bali pia sehemu mbalimbali duniani katika mapambano ya kudai usawa.Katika hotuba hiyo iliyopewa jina “I Have a Dream” (“Nina Ndoto”,kwa tafsiri isiyo rasmi),Dkt King alieleza matamanio yake kuona Waamerika Weusi na Weupe wakiishi pamoja kwa amani na usawa.Hotuba hiyo iliyotolewa mbele ya watu zaidi ya laki mbili,inakubalika miongoni mwa wengi kama moja ya hotuba za muhimu kabisa katika historia ya Marekani.Mwaka 1999,hotuba hiyo ilichaguliwa na wasomi kuwa ni hotuba bora kabisa za karne ya 20.

Miongoni mwa nukuu muhimu katika hotuba hiyo ni pamoja na (kwa tafsiri yangu isiyo rasmi) “…nina ndoto kwamba siku moja taifa hili litasimama na kuishi kama inavyotamkwa kwenye imani yake….nina ndoto kwamba siku moja watoto wangu wanne wataishi katika taifa ambalo hawatahukumiwa kutokana na rangi ya ngozi zao bali tabia/utu wao….nina ndoto kwamba siku moja watoto wa waliokuwa watumwa na watoto wa waliokuwa wamiliki watumwa watakaa pamoja katika meza ya undugu…”

Msukumo uliotokana na uongozi wa harakati za Dkt King ulisaidia sana kubadili historia ya Marekani hususan usawa kwa (Wamarekani) Weusi, na kupelekea mabadiliko mbalimbali dhidi ya sheria za kibaguzi.Miongoni mwa sheria hizo ni pamoja na “Civil Rights Act” ya mwaka 1964 iliyoharamisha ubaguzi kwenye sehemu mbalimbali katika jamii.Mwaka uliofuata, “Voting Rights Act” ilipitishwa na kufuta kipengere kilicholazimisha wapiga kura watarajiwa kufanya testi za kupima uwezo wa kusoma na kuandika (wengi wa waathirika wa kipengere hicho walikuwa Wamarekani Weusi ambao walikuwa na maendeleo duni kielimu kutokana na kubaguliwa).

Maadhimisho ya siku ya Dkt King yamekuwa yakitoa changamoto nzuri kwa jamii ya Wamarekani kutafakari mahusiano kati ya Weupe na Weusi.Wengi hujiuliza iwapo ndoto za Dkt King zimetimia kweli,zinaelekea kutimia au hazina dalili ya kutimia kabisa.Ni maswali magumu ambayo yanahitaji uchambuzi wa kina kuyajibu,na pengine hata kwa uchambuzi wa kina bado inaweza kuwa vigumu kupata jawabu moja linalokubalika.Kingine kinacholeta ugumu wa kupata jawabu ni tofauti ya vizazi.Kwa walioishi nyakati za ubaguzi wa rangi na kushuhudia harakati za Dkt King wanaweza kuwa na mtizamo tofauti kuhusu kutimia kwa ndoto za mwanaharakati huyo ukilinganisha na kizazi cha hivi karibuni ambacho kinamwelewa Dkt King kupitia kumbukumbu za historia tu.

Hata hivyo ni rahisi kukubaliana kwamba harakati za Dkt King na wenzie zimesaidia kuleta mabadiliko makubwa ikiwa ni pamoja na hayo ya kisheria niliyotaja awali.Wapo wanaokwenda mbali zaidi na kutoa mifano ya mafanikio ya Waamerika Weusi maarufu kama Jenerali Colin Powell na Condoleeza Rice ambao wameshika nafasi nyeti katika uongozi wa taifa hilo.Lakini mfano mzuri zaidi ni Barack Obama,seneta Mweusi anayewania kuteuliwa kugombea urais wa nchi hiyo kupitia chama cha Democrats.Akiteuliwa kuwa mgombea,ataweka historia ya pekee nchini humo,na akifanikiwa kushinda urais basi hiyo itakuwa zaidi ya kuweka historia (tuite kuandika historia upya).Hata kama atashindwa,mafaniko aliyokwishafikia hadi sasa ni hatua muhimu katika kutimia kwa ndoto za Dkt King.

Afrika nayo imetoa akina Dkt King kadhaa,na kwetu Tanzania tunajivunia Baba wa Taifa marehemu Julius Nyerere ambaye (kama Dkt King) alikuwa na ndoto zake kadhaa ambazo kimsingi zilihusu kuwa jamii yenye usawa.Ndoto za Mwalimu zilivuka mipaka ya Tanzania kuhakikisha kuwa Afrika yote inakuwa huru.Mchango wa Mwalimu katika mapambano ya ukombozi kusini mwa Afrika utaendelea kukumbukwa milele.Na pengine hapo ndipo baadhi yetu tunagundua mabadiliko ya vizazi yanavyochangia kusahaulisha historia.

Mara nyingi napokutana na vijana Waafrika wenzangu (wanaoishi hapa Uingereza) kutoka nchi kama Zimbabwe,Zambia,Angola,Msumbiji,Afrika Kusini,Namibia na Uganda,nabaini kwamba wengi wao aidha wamesahau au wanapuuza mchango wetu katika ukombozi wa nchi zao (kwa Uganda ni kumng’oa Nduli Idi Amini).Angalau Wazimbabwe wanaweza kuwa na kisingizio kwamba kutokana na ubabe wa Mugabe,baadhi yao wanaweza kutoona faida ya kumkimbiza mkoloni na kujipatia uhuru.

Lakini pengine si busara sana kuwalaumu wanaopuuza mchango wa Mwalimu na Tanzania kwa ujumla katika ukombozi wa nchi zao kwani inawezekana kabisa wanafuatilia kinachoendelea nchini mwetu na kugundua kwamba baadhi yetu tumetupilia mbali kabisa jitihada za Baba wa Taifa kuhakikisha tunajenga jamii yenye usawa.Kwa vile dunia ni kama kijiji,katika zama hizi za utandawazi,majirani zetu hao watakuwa wanasoma na kusikia habari kuhusu ufisadi nchi mwetu,na pengine kubaki wanajiuliza “hivi hawa si ndio waliokuwa wanapigania usawa barani Afrika?Mbona wenyewe wako sasa wanafanyiana hivi?”.

Mwalimu alifariki huku baadhi ya ndoto zake zikiwa hazijatimia.Wachambuzi wazuri wa siasa wanadai kwamba baadhi ya ndoto hizo zilishindikana hata kabla hajang’atuka (kwa mfano upinzani wake wa awali dhidi ya ushirikiano na mashirika ya fedha ya kimataifa).Lakini nadhani Mwalimu aliumia zaidi kuona Azimio la Arusha likizikwa hai na Azimio “la kimyakimya” la Zanzibar (naliita hivyo kwani sijawahi kuona “document” yoyote rasmi inayoelezea kilichomo kwenye Azimio hilo).

Wakati Dkt King anaweza kufarijika huko aliko iwapo angeweza kufahamu baadhi ya mambo yanayoendelea sasa nchini Marekani (hususan kuhusu Obama) nashindwa kuhisi ni lipi litakalokuwa linampa furaha Mwalimu huko aliko tukiweka pembeni suala la amani na utulivu.Na hata katika hilo (la amani na utulivu) wapo wanaodai kuwa ni ya kufikirika zaidi kwani ni ukweli usiopingika kwamba masikini ni wengi zaidi kuliko matajiri,na yayumkinika kusema kwamba matumbo ya masikini hao hayana amani wala utulivu.

Kadhalika,kuna wanaodai kwamba kigezo cha amani na utulivu kimekuwa kikitumiwa vizuri zaidi na mafisadi wanaoamini kwamba Watanzania ni wapole sana na hawako tayari kuchezea lulu ya amani na utulivu kwa vile tu flani kakwiba mabilioni ya umma.Pengine mafisadi hao wako sahihi kwani tumekuwa tukishuhudia baadhi ya watu wakiua,wakapewa dhamana za chapchap na kuendela na maisha yao kama kawaida huku hatima ya kesi zao ikisubiri isahaulike akilini mwa watu.Wakati hayo yakitokea,magereza yetu yamejaa wamachinga wanaotafuta ridhiki mitaani na wafungwa wengine ambao inawezekana kabisa walijiingiza kwenye wizi wa nyanya au kuku kwa vile tu hawakuwa na njia nyingine ya kujipatia kipato.Uhalifu ni uhalifu,na kila mhalifu anastahili adhabu lakini inatatiza kuona wahalifu wengine wakiendelea kula raha kana kwamba waliyofanya si kinyume cha sheria.

Tofauti kubwa kati ya ndoto ya Dkt King na Mwalimu ni kwamba wakati Wamarekani Weusi wanafanya kila jitihada kuenzi jitihada za Dkt King kwa kuendeleza mapambano dhidi ya ubaguzi na kupigania usawa,sie tuko kwenye mgawanyiko mkubwa kati ya wachache walionacho wasiosubiri kuongezewa bali wanapora, na wengi wasio nacho ambao hata kile kidogo walicho nacho kinaporwa.Hili ndio tishio kubwa,sio tu kwa ndoto za Mwalimu,bali hata kwa hiyo lulu yetu ya amani na utulivu.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.