Showing posts with label LIBERALS. Show all posts
Showing posts with label LIBERALS. Show all posts

2 Aug 2007

Asalam aleykum,

Wanasema kuwa siasa inahitaji kuwa na mvuto (appeal).Lakini mvuto wa mwanamama Myra Bushell,mshindi wa uchaguzi mdogo wa kanseli kwa tiketi ya chama cha Liberal Democrats cha hapa Uingereza,ni zaidi ya mvuto wa kawaida unaohitajika kwenye siasa.Myra aligombea na kushinda nafasi ya uwakilishi kwenye kanseli ya Bideford huko Devon,huku akiwa ni mcheza-uchi/nusu uchi kwenye vilabu (stripper) na mwendesha huduma ya ngono-kwa-simu (phone-sex-line) ambayo anachaji pauni 1.50 kwa dakika (takriban shilingi 3500 za huko nyumbani).Yeye anajitetea kuwa hayo ni maisha yake binafsi nje ya siasa,lakini tayari wajumbe watatu wa kanseli hiyo wameshajiuzulu kupinga vitendo vya mwanasiasa huyo ambaye pia ana tovuti yake ya huduma za ngono.Myra anajitetea kwamba wakati anautumikia umma kama mwanasiasa,anapaswa pia kumudu gharama za maisha,na ndio maana amekuwa akijihusisha na shughuli hizo “nyeti.” Habari njema kwake ni kwamba katibu (clerk) wa kanseli hiyo,George McMauchlan,ametamka bayana kuwa Myra hajavunja sheria yoyote ya maadili ya kazi ya ujumbe wa kanseli kwa vile “shughuli zake binafsi nje ya siasa” haziathiri utendaji wake wa kazi.Kaazi kweli kweli!!


Tukiachana na habari hizo za mwanasiasa “stripper”, kwa takriban wiki nzima iliyopita,medani za sera za nje za Marekani ilikuwa imetawaliwa na habari kwamba taifa hilo lilikuwa linajiandaa kutekeleza mpango wa kuziuzia silaha baadhi ya nchi za Kiarabu na Mashariki ya Kati.Wanufaika wakubwa wa mpango huo ni pamoja na Saudi Arabia,Misri,na kama ilivyo ada,Israel.Hata hivyo,mpango huo umezaa mvutano wa namna flani kwenye duru za siasa za ndani za Marekani kwani wapo wanaodhani kwamba hoja ya serikali ya Bush kuwa inaziuzia silaha nchi kama Saudi Arabia na Misri ili,pamoja na mambo mengine,kudhibiti kujitanua kijeshi kwa Iran,inaweza kupingana na ukweli kuwa rafiki wa leo anaweza kuwa adui wa kesho,na silaha unazompatia leo kujilinda zinaweza kutumika kesho kukudhuru.Na mpango huu umekuja wakati wachambuzi wa siasa za kimataifa wanaoona kuna kuyumba kwenye urafiki wa muda mrefu kati ya Marekani na Saudi Arabia.Hivi karibuni,Saudi iliweka bayana mtizamo wake kuhusu vita ya Irak kwa kusema kuwa uvamizi wa Marekani nchini Irak unachochea machafuko na suluhisho pekee ni kwa majeshi ya kigeni kuondoka nchini Irak.Pia kumekuwepo shutuma za hapa na pale kwamba Saudi Arabia inavisapoti vikundi vya madhehebu ya Sunni nchini Irak ili kuvikabili vikundi vya madhehebu ya Shia ambavyo inadaiwa vinapata sapoti ya Iran.Kitakwimu na kujiografia,Saudi ni taifa la ki-Sunni wakati Iran ni la ki-Shia,na mahusiano kati ya nchi hizo mbili sio mazuri.Saudi kwa upande wake inahofia sana kukua kwa nguvu za kijeshi za Iran,hasa kwa vile hadi sasa,ukitoa Israel,Saudi ni taifa lenye nguvu kubwa katika eneo la Ghuba na Mashariki ya Kati.

Wakati mwingine ni vigumu kuzielewa sera za nje za Marekani kwani kwa jinsi flani ilipaswa kujifunza kutokana na maamuzi yake ya zamani ambayo kwa namna moja au nyingine yamekuwa yakiiumiza kichwa katika kipindi hiki tulichonacho,kwa mfano msaada wake wa silaha kwa Irak wakati Saddam alipokuwa rafiki wa nchi hiyo,na misaada yake kwa mujahidina wa Afghanistan wakati wa vita dhidi ya Muungano wa nchi za Kisovieti (USSR).Tawala za nchi nyingi za Kiarabu na Ghuba sio za kidemokrasia (kwa vipimo vya nchi za magharibi),na miongoni mwa sababu zinazodaiwa kuchangia kuibuka kwa siasa za msimamo mkali wa kidini katika nchi hizo kushindwa kwa tawala hizo kuleta mabadiliko ya manufaa ya kisiasa,kiuchumi na kijamii.Lakini katika kukoroga zaidi mambo,baadhi ya tawala hizo zimekuwa zikuvikumbatia na kuvifadhili vikundi vyenye msimamo mkali wa kidini ili tawala hizo ziendelee kuwa madarakani.Kwa uchambuzi mwepesi,yayumkinika kusema kuwa hatma ya tawala hizo kwa muda mrefu sio ya kuaminika sana,na Marekani inaweza kujutia huko mbeleni kwa kuzilinda tawala hizo kwa misaada ya kijeshi.

Na taarifa zaidi kutoka Irak zinaeleza kuwa “picha haziivi” kati ya mkuu wa majeshi ya Marekani nchini humo,Jenerali David Petraeus,na Waziri Mkuu wa Irak,Nour al-Maliki.Inasemekana kuwa Maliki alishamuomba Rais Bush amwondoe Jenerali huyo msomi mwenye shahada ya kwanza katika sayansi (Bachelor of Science),shahada ya uzamili katika Utawala wa Umma (M.A in Public Administration) na shahada ya uzamifu kwenye siasa za kimataifa (PhD in International Relations) na alishakuwa (assistant) Professor kwenye US Military Academy. “Bifu” (kupingana) kati ya Maliki na Jen Petraeus kunatokana na baadhi ya maamuzi yanayopingana kati ya watu hao muhimu kwa mafanikio au kutofanikiwa kwenye sera ya Bush kuhusu Irak.Inaelezwa kuwa Maliki haafikiani na mpango majeshi ya Marekani unaoelekea kuasisiwa na Jen Petraeus wa kuvipatia silaha vikundi vya madhehebu ya Sunni ili vipambane na wapiganaji wa Al-Qaeda nchini humo.Maliki ambaye ni muumini wa madhehebu ya Shia anaelekea kuhofia kuwa silaha hizo zinaweza kutumika dhidi ya vikundi vya madhehebu ya Shia,au kwa mtizamo wa muda mrefu,kuchangia vita vya wenyewe kwa wenyewe pindi majeshi ya Marekani yatakapoondoka (kama kuna kuondoka kweli).

Baada ya mjadala wa siasa za kimataifa,hebu tegeukie mambo mengine ya huko nyumbani.Nitahadharishe kuwa naamini baadhi ya ntakayoandika hapa yatawaudhi watu flani lakini kuudhika kwao kutakuwa na maana moja tu kwangu:kwamba ujumbe umefika na wabadilike badala ya kununa.Binafsi,nadiriki kusema kuwa mzazi makini hawezi kumrushusu binti yake kuingia kwenye mambo ya u-Miss.Kwanini?Kwa sababu inaelekea wengi wa mabinti wanaotafuta u-miss huwa aidha wanarubunika kuwa wenye tabia mbovu baada ya kupata majina au pengine fani nzima ya u-miss ni kichocheo cha umalaya (samahani kwa maneno makali).Yaani kila kukicha utaskia sijui Miss nanihii katembea na mume wa mtu,au Wema Sepetu kapigwa picha za utupu,au Faraja Kotta kalibwaga buzi lake lililoiba fedha wapi sijui,na vituo vingine mia kidogo.Kuna kasoro kwenye fani ya u-miss lakini jamii inaelekea imelifumbia macho suala hilo.Lundenga,Chipungahelo na wadau wengine wa fani ya u-miss wana jukumu la kuithibitishia jamii kuwa tatizo haliko kwenye fani hiyo bali ni kwa baadhi tu ya washiriki.Na kama tatizo ni washiriki basi watuambie bayana inakuwaje wanaweza kupenya katika ngazi mbalimbali hadi kifikia levo ta taifa na kuanza kutuonyesha madudu yao.Rafiki yangu mmoja mwandishi wa habari aliwahi kunidokeza kuwa fani hiyo imetawaliwa sana na viongozi,wadhamini na mapromota walafi wa kula uroda ambao wanarahisishiwa kazi na mabinti wenye tamaa ya umaarufu wa chapchap,ambao kwao sio ishu kuvua “makufuli” yao ili wakwae u-miss.Ujumbe wangu kwenu ni simpo:msipokuwa makini mtaondoka kwa kilo mbili,na kwa vile mnathamini sana umaarufu,basi kudhoofika kwa afya zenu kutatawala sana kurasa hizohizo zinazoripoti kila siku namna mnavyoibemenda Amri ya Sita kama hamna akili nzuri.Mkikasirika shauri yenu lakini mmezidi kufanya mambo ya aibu.

Halafu kuna mambo mawili yamenisikitisha sana.La kwanza ni hii tabia ya ubabe inayoelekea kumkolea msanii TID.Binafsi,nazipenda sana kazi za kijana huyu,na mwanzoni nilikuwa namtofautisha na wasanii wengine wa bongo kwa vile amewahi kukaa ugahibuni kwa muda wa kutosha na amekuwa akipata mialiko ya nje mara kwa mara.Lakini pengine kwa kutotambua kuwa taswira (image) ya msanii ni muhimu katika kumuweka au kumporomosha kwenye chati,ameendelea kushika vichwa vya habari kwa matukio yasiyopendeza.Wimbo wake naoupenda sana unaitwa “chagua moja”,nami ujumbe wangu kwake ni mfupi:chagua moja kati ya kujiporomosha wewe mwenyewe kwa matendo yasiyofaa au jirekebishe tabia zako ili uendelee kubaki kuwa “Top In Dar.” Usikasirike,ni somo jepesi tu hilo.

Jingine lililonikera ni gazeti la RISASI ambalo katika toleo lake la Julai18-20 lilikuwa na habari kwamba “Warembo TZ wapiga picha za X tupu…zasambazwa mitaani,baadhi yao ni washiriki wa kusaka mataji ya u-miss.” Kinachosikitisha sio kama iwapo habari hiyo ni ya kweli au ya kubuni bali ni picha zilizotumika kwenye habari hiyo.Rafiki yangu mmoja aliyeko Marekani amenifahamisha kuwa wasichana walioko kwenye picha hizo ni wacheza filamu za ngono (porn stars) wa Marekani na wala sio Watanzania.Kwa kuthibitisha alichokuwa anasema,alinipatia tovuti ambazo zina picha za Wamarekani hao weusi.Kama picha zilizotumiwa na RISASI ni feki basi yayumkinika kusema kuwa hata habari yenyewe ni feki.Hivi ni uzembe wa mhariri kucheki ukweli wa habari husika au ndio kuwafanya Watanzania wajinga kwa kuwapa habari “sensational” ambazo hazina ukweli?Nyie ni watu wazima ambao mmeshatengeneza faida ya kutosha kwa kuandika udaku lukuki wa kweli,sasa tamaa ya nini hadi mfikie hatua ya kunyofoa mapicha kwenye mtandao na kuzusha habari?Shame on you!

Alamsiki

18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Asalam aleykum,

Mwaka juzi gazeti maarufu duniani la TIME lilimtangaza George W.Bush kuwa “mtu wa mwaka (2004)” –au “Person of the Year” kwa lugha ya kwa mama.Katika uchambuzi wake kuhusu Bush,gazeti hilo lilimnukuu Rais huyo wa Marekani akisema kwamba “inapotokea kuwa hoja au mawazo yako yanazua mjadala au upinzani basi ni dalili kwamba yana uzito…kwa maana yangekuwa ya kipuuzi wala watu wasingejishughulisha nayo.”Alikuwa anazungumzia upinzani anaokumbana nao katika utendaji wa kazi zake za kila siku.Sio siri kuwa Bush anachukiwa na watu wengi hata ndani ya nchi yake.Lakini japo mie sio shabiki wake,namhusudu kwa jinsi anavyoweza kufanya mawazo yake yakubalike hata kwa wale ambao aidha hawayapendi au hawaafikiani nae.

Mwaka jana wakati nakuja huko nyumba,nilibahatika kukaa kiti kimoja na mama mmoja wa Kimarekani.Ni mtu mwongeaji sana,nami niliitumia nafasi hiyo kumdadisi siasa za Marekani hasa kuhusu mgawanyiko mkubwa wa kiitikadi nchini humo baina ya wale wa mrengo wa kulia(conservatives) na wale wa mrengo wa kushoto (liberals).Mwanamama huyo ambaye alinifahaisha baadaye kuwa ni mwanaharakati wa mazingira,alieleza kuwa kwa kiasi kikubwa mgawanyiko huo unachangiwa na siasa za Bush na maswahiba zake kama Dick Cheney,Donald Rumsfield,Paul Wolfowitz,na wengineo ambao wanajulikana kiitikadi kama “neo-conservatives” (sijui wanaitwaje kwa lugha yetu ya Taifa!).Miongoni mwa imani za hawa jamaa ni kuhakikisha kuwa Marekani inatumia ipasavyo nafasi yake kama Taifa lenye nguvu kabisa duniani.Kwa maana hiyo,ni “haki” yake kutumia “ubabe” wake kikamilifu ikiwa ni pamoja na kuvamia zile nchi zinazoonekana kuwa “korofi”.Ipo siku nitawazungumzia kwa kirefu jamaa hawa ambao takriban wote ni wadau wa taasisi moja isiyo ya kiserikali iitwayo “The Project for The New American Century” (Mradi wa Karne Mpya ya Marekani,kwa tafsiri isiyo rasmi).Turudi kwa yule mama.Basi akanambia kuwa japo yeye binafsi ni mpinzani wa Bush na hao neo-conservatives wenzake kuna wakati huwa “anamzimia sana” kutokana na jinsi anavyoweza kufanya maamuzi yake yatekelezwe hata pale kwenye upinzani mkubwa.Waingereza wana msemo “kama humuwezi unayeshindana nae basi bora uungane nae tu,”na ndio maana hata wale wasioafikiana na Bush mwishowe hujikuta hawana jinsi bali kuendana na mawazo au maamuzi yake.

Muda mfupi uliopita nilipata ujumbe kutoka kwa rafiki yangu flani aliyeko huko nyumbani akinijulisha kuwa kuna mwandishi mmoja ameandika makala katika gazeti flani la kila siku (la hapo Bongo) kupingana nami katika hoja ya makala yangu moja ya hivi ambayo nilimfananisha Rais Jakaya Kikwete na kiongozi wa chama cha Conservatives cha hapa Uingereza,David Cameron.Kwa mujibu wa ujumbe niliopata,mwandishi huyo aliyepingana nami anadai sikuwa sahihi kuwalinganisha wanasiasa hao .Kwa bahati mbaya hadi natayarisha makala hii nilikuwa sijapata hoja zote zilizotolewa kukosoa makala yangu.Kwa mantiki hiyo itakuwa vigumu kujibu hoja baada ya hoja bali nachoweza kusema kwanza ni kwamba makala ya mwandishi huyo ni uthibitisho tosha kuwa gazeti hili la KULIKONI ni kipenzi cha wengi,na ndio maana linazaa hoja na makala katika magazeti mengine.Pili,kama gazeti la TIME lilivyomnukuu Bush naamini makala yangu hiyo ilikuwa na uzito ndio maana ikamsukuma mwandishi huyo kuijadili japo hakuafikiana na nilichokiandika,kwa kuwa laiti ingekuwa ya kipuuzi asingepoteza muda wake kupingana nayo.”

Kwa faida ya mwandishi huyo,Kikwete anashabihiana sana na David Cameron katika maeneo flani.Kwa mfano,wote wawili wako katika vyama ambavyo kabla ya wao kushika hatamu za uongozi kwa kiasi flani vilikuwa vinaonekana kama ni vya “wateule wachache” tu.Ushindi wa tsunami kwa Kikwete ni dalili tosha kuwa hata baadhi ya wanachama wa vyama vya upinzani walimpigia kura kuonyesha kuwa kuteuliwa kwake kuwa mgombea urais kuliiongezea nguvu CCM.Hoja nyingine japo inaweza kuwa si nzito sana ni kwamba wanasiasa hao wana sifa inayofanana ya kuwa handsome,na kwa taarifa yako u-handsome unalipa sana kwenye siasa.Lakini kingine ni lugha zao wanazotumia.Wanaongea lugha za watu wa kawaida wa mtaani,yaani wanajua wananchi wanatarajia nini kwao.Ndio,Cameron anafuata siasa za mrengo wa kulia kuelekea kati (right-centre) na Kikwete kama mwana CCM nadhani atakuwa ni wa siasa za mrengo wa kushoto kuelekea kati (left-centre),na japo Cameron ni Mwingereza na Kikwete ni Mtanzania,la muhimu hapa ni jinsi wananchi wanavyowahusudu kutokana na utendaji wao.Kura za maoni hapa Uingereza zinaonyesha kuwa Cameron amempiku Tony Blair kwa kupendwa na wananchi na naamini kuwa hata kama Watanzania wataamshwa usingizini kupiga kura za maoni,Kikwete ataibuka kidedea kwa sana.Kwenye siasa umaarufu wa mwanasiasa haugemei sana kwenye itikadi zake au chama chake,sehemu aliyozaliwa au umri wake bali kukubalika kwake miongoni mwa wananchi,na hicho ndicho kilichonipelekea kuwafananisha wanasiasa hao.

Mwisho,siamini kuwa mwandishi wa makala hiyo alikuwa anatafuta umaarufu kupitia makala yangu au gazeti hili la KULIKONI,bali alikuwa anatumia haki yake ya kikatiba kutoa mawazo yake.Nampa changamoto aendelee kusoma gazeti hili ilimradi isiwe kwa nia ya kupinga kila kitu hata kama ameishiwa na hoja.Kama alivyoimba Mista Two (Joseph Mbilinyi) kwenye wimbo wake “Sugu” kwamba huwezi kuizuia mvua kunyesha,KULIKONI ni kama jua na mvua,halizuiliki.

Alamsiki.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.