Showing posts with label IRAK. Show all posts
Showing posts with label IRAK. Show all posts

12 Aug 2014


Hali nchini Iraki ni tete kufuatia uamuzi wa Rais wa nchi hiyo Fouadi Masoum (I guess wewe kame mie tulikuwa hatumfahamu mtu huyu wala kujua kama Iraki ina rais) 'kumtimua' Waziri Mkuu Nuri al-Maliki, aliyekuwa madarakani kwa miaka minane, na kumteua Haidar al-Abadi kuchukua wadhifa huo.

Hata hivyo, Maliki sio tu  amegoma kuondoka madarakani bali pia amemwaga wanamgambo na vikosi maalum vya jeshi (special forces) mitaani, na kupelekea kizaazaa cha aina yake.

Marekani, ambayo ilisaidia kumweka madarakani Maliki mwaka 2003 imempongeza Waziri Mkuu mpya al-Abadi, msaidizi wa zamani wa Maliki, kuashiria kuunga mkono mabadiliko hayo.

Akihutubia kwa njia ya televisheni (naam, pamoja na vurugu zote nchini Iraki bado televisheni zinafanya kazi) amesema hatua ya Rais kufanya mabadiliko hayo ni ukiukwaji hatari wa Katiba, huku akiambatana na 'wapambe' wake, ameahidi kutatua 'kero' hiyo.

Mkwe wake, Hussein al-Maliki, ameyaelezea mabadiliko hayo kuwa ni kinyume cha sheria, na kudai yatabadilishwa kortini. "Hatutokaa kimya," alidai.

Hata hivyo, Marekani imemwonya Maliki kutotumia nguvu za dola kung'ang'ania madaraka.

Mwislamu wa madehebu ya Shia, Maliki analaumiwa na washirika wake wa zamani huko Marekani na Iran kwa kuwasukuma waumini wa madhehebu ya SUnni katika mapambano yaliyopelekea 'sintofahamu' inayoendelea sasa kwa kikundi cha Sunni cha ISIS kudhamiria kuigeuza nchi hiyo kuwa taifa la Kiislam. Viongozi wengi wa ki-Sunni na Kikurdi wamekuwa wakipiga kelele kuwa Maliki anastahili kuachia ngazi, huku hata baadhi ya viongozi wenzake wa ki-shia wakiwa na msimamo kama huo.

CHANZO: Habari hii imetafsiriwa kutoka vyanzo mbalimbali mtandaoni

2 Nov 2007

Ama kweli ni rahisi kupanga sera na kutegemea ifanikiwe lakini ni habari nyingine kwa mpanga sera kuwa sehemu ya utekelezaji huo.Hilo limejihidhirisha katika taarifa kutoka nchini Marekani ambapo maafisa wa mambo ya nje wa nchi hiyo wamefahamishwa kwamba watakuwa wakipelekwa nchini Irak kama sehemu ya utekelezaji wa majukumu yao ya kazi.Pamoja na kukumbushwa kwamba wakati wanakubali ajira waliapa kufanya kazi mahala popote watakapopangiwa na mwajiri wao,maofisa hao wameonekana kutoafikiana na pango huo ambapo baadhi yao wamefikia hatua ya kuuita “mpango wa kujipeleka kwenye hukumu ya kifo” hasa kwa vile “ziara” za aina hiyo tayari zimeshagharimu maisha ya maofisa watatu tangu kuanza kwa vita ya Irak.Maofisa wanaokaidi agizo hilo wanakabiliwa na hatari ya kuchukuliwa hatua kali ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi.Nadhani pamoja na hatari inayoweza kuwakabili maofisa wanaopelekwa huko,nadhani utekelezaji wa agizo hilo utawasaidia kufahamu namna hali halisi ilivyo kwenye uwanja wa mapambano ni ambayo ni ngumu zaidi kuliko urahisi wa kuandaa sera,mikakati na mipango mizuri.



Kwa hapa UK,moja ya masuala ambayo kwa siku kadhaa sasa yametawala duru za habari ni kuhusu “Muungano” wa Uingereza (the United Kingdom of Great Britain and Northern Ireland). Kumekuwa na mjadala wa muda mrefu kuhusu mambo makuu mawili: kwa upande mmoja ni umuhimu wa Muungano huo (miongoni mwa wale wanaopendelea kuona unadumu milele) na upande mwingine ni hoja kwamba muungano huo unazipunja baadhi ya sehemu zinazounda nchi hii.Katika uchaguzi mkuu uliopita,chama tawala cha Labour kilibwagwa na chama cha SNP (Scottish National Party) kwa upande wa Scotland.Hofu ya awali kwa Labour na “wapenda Muungano” baada ya ushindi wa SNP ilikuwa kwenye ukweli kwamba miongoni mwa malengo ya muda mrefu ya SNP ni kuiona Scotland ikiwa nchi huru inayojiendesha pasipo kuelekezwa na “serikali” ya London.Na katika manifesto yao ya uchaguzi,SNP hawakuogopa kutamka bayana matamanio yao uhuru wa Scotland.Chama hicho kilikuwa kinaelewa bayana kwamba sera hiyo ingeweza kuwapatia ushindi au kushindwa kwenye uchaguzi huo,kwani suala la uhuru wa Scotland ni miongoni mwa mambo yanayowagawa sana watu hawa.Kura mbalimbali za maoni kuhusu suala hilo zimekuwa na matokeo yanayothibitisha mgawanyiko huo,ambapo takriban nusu ya Waskotishi wanadhani uhuru ni wazo zuri huku takriban nusu nyingine wakipinga wazo hilo.Jeuri ya madai ya uhuru inachangiwa na kile Waskotishi wengi wanachokiona kama utajiri katika eneo hili (mafuta) ambao wanadhani unapaswa kuwanufaisha zaidi wao sambamba na kuwa na maamuzi ya namna ya kutumia utajiri huo badala ya kusubiri maelekezo kutoka England.Lakini wapo wanaoonya kwamba Scotland haiwezi kujimudu yenyewe kwa kutegemea tu utajiri wa mafuta,na baadhi ya wachumi wamekwenda mbali zaidi kwa kuonyesha pengo la bajeti litakaloikumba Scotland pindi ikijitoa kwenye Muungano huu.

Mjadala bado unaendelea na ni vigumu kusema bayana iwapo uhuru utapatikana au Muungano utaendelea.Majuzi,kiongozi wa chama pinzani cha Conservatives,David Cameron amewasha tena moto kuhusu suala hilo baada ya kutamka kwamba ana nia ya kusukuma sheria itakayowabana wabunge wa Scotland waliopo kwenye bunge la jumla la Uingereza (yaani linalojumuisha wabunge wa England,Wales,Scotland na Northern Ireland) wasipige kura kwenye masuala yanayoihusu England pekee.Hili ni suala linalujulikana kama “the West Lothian Question” (jina linalotokana na swali lililoulizwa mwaka 1977 na mbunge wa jimbo la Scotland la West Lothian,Tam Dalyell,wakati wa mjadala wa bunge kuhusu kuanzisha serikali-devolved governments-za Scotland na Wales).Swali hilo lilihusu uhalali wa wabunge wa “nchi” hizo mbili kushiriki katika mijadala na maamuzi yanayowahusu watu wa England pekee,ilhali wabunge wa England hawana nafasi kama hiyo kwa vile hawaingii kwenye mabunge ya sehemu hizo.Chama cha Labour kimemshutumu Cameron kwa kile walichokiita sera za kuvunja Muungano lakini kwa vyovyote vile hoja hiyo ni habari njema kwa Alec Salmond (First Minister wa Scotland) na chama chake cha SNP pamoja na wale wote wanaotaka uhuru.

Na kuna mambo yanayoshangaza kuhusu Muungano huu.Kwa mfano,wakati noti zinazotolewa na benki ya England (English Pounds) zinatumika nchi nzima,na zinakubalika mahala popote duniani kama sarafu halali ya nchi hii,noti zinazotolewa na mabenki ya Scotland (ambazo zina thamani sawa na English pounds) zinakataliwa katika baadhi ya maeneo ya England.Nilipokuja huko nyumbani mwaka jana,nilishindwa kabisa kubadilisha Scottish pounds na ilinilazimu nizitume huku ili zibadilishwe kuwa English pounds.Sheria za elimu ya juu na huduma za afya pia zinatofautiana kwa namna flani,ambapo kwa Scotland huduma nyingi zinatolewa bure ilhali kwa England zinaendelea kulipiwa.Scotland pia imekuwa ikilalamikia suala la uhamiaji ambapo sheria zinazotawala ni zile za nchi nzima ilhali mahitaji ya “nguvu-kazi” kutoka nje (kupitia uhamiaji wa wageni) unaathiriwa na sheria “kali” zinazotawala nchi zote zilizopo kwenye Muungano huu. Wakati Scotland imekuwa ikiendesha program kadhaa za kuvutia wageni,ikiwa ni pamoja na kuwashawishi wale walio hapa waifanye “nchi” hii kuwa makazi ya pili (second home) au makazi ya kudumu,kelele za wanasiasa huko England ni kwamba wageni wamezidi na lazima serikali idhibiti zaidi wahamiaji.

Masuala ya muungano ni nyeti na yamekuwa chanzo cha matatizo katika sehemu mbalimbali duniani.Lakini tofauti na wenzetu hawa ambao wanadiriki kutoa mawazo yao hadharani na kukaribisha mijadala kuhusu suala hilo,huko nyumbani kuzungumzia kuhusu Muungano inaelekea kuwa sio wazo la busara sana kwa mwanasiasa anayotaka mafanikio.Kuna kile kinachoitwa “jinamizi la Mwalimu kwa atakayetaka kuvunja Muungano” ambacho kimsingi nakiona ni kama kikwazo kwa wale wote wanaodhani kwamba ni muhimu kuwa na mjadala kuhusu hatima ya Muungano wetu.Tukiendelea kuogopa kuujadili,yayumkinika kusema kwamba tunautengenezea mazingira mazuri ya kuuharibu.Sio siri kwamba wenzetu wa Visiwani wamekuwa wakipiga kelele sana kwamba Muungano unawaumiza,lakini hofu yangu kubwa ni pale wenzao wa Bara nao “watakaposhikilia bango” hoja hiyo ya kuumizwa na mzigo wa Muungano.Na “the West Lothian Question” ya Uingereza “ina-fit” kabisa mazingira yalivyo huko nyumbani ambapo wabunge kutoka Zanzibar wamekuwa wakishiriki (katika bunge la Muungano) katika kujadili na kutoa maamuzi katika baadhi ya mambo ambayo yanayowahusu Wabara pekee ilhali wabunge wa Bara hawana nafasi hiyo kwani hawaingii kwenye Baraza la Wawakilishi huko Zanzibar.

Nafahamu kuwa kuna kitu kama “tume” au “kamati” iliyoundwa kujadili kero za Muungano,lakini japo sijui imefikia hatua gani katika majadiliano yao,yayumkinika kusema kwamba kasi nzima ya kulitafutia ufumbuzi wa kudumu suala hilo sio ya kuridhisha.Pengine katika kuepuka maamuzi yanayotoka juu kwenda chini (yaani kutoka kwa viongozi kwenda kwa wananchi) japo waathirika au wafaidika wakubwa ni hao wa chini,sio wazo baya kufikiria kuitisha kura ya maoni ili kupata mawazo ya wadau wakubwa wa Muungano huo (wananchi).Ashakum si matusi,lakini ni vema Muungano ukavunjika kwa ridhaa kuliko ukadumu kwa manung’uniko,kwani manung’uniko hayo yasipopatiwa tiba yanaweza kabisa kuuvunja Muungano huo pasipo kusubiri ridhaa ya wadau.Kikubwa nilichojifunza katika mjadala wa Muungano wa Uingereza ni namna ambavyo unavyoendeshwa kwa uwazi na upana zaidi kiasi kwamba sauti zote,zinazopinga na kukubali suala hilo,zinasikika waziwazi.Ukiniuliza iwapo Muungano wetu ni muhimu,jibu nitakalokupa hata niwapo usingizini ni “ndio”.Hata hivyo,umuhimu wa Muungano huo hauondoi haja ya kuufanya uwe bora zaidi,wa manufaa kwa pande zote mbili na wenye mazingira yatakayoufanya udumu daima dumu.Tusipoziba ufa leo,kesho tutajenga ukuta.

Mwisho, napenda kutoa pongezi kwa kizazi kipya cha vijana wabunifu. Hivi karibuni, mchora katuni na mtangazaji maarufu Masudi “Kipanya” alizindua duka la nguo za lebo yake ya “KP Wear”. Na msanii wa bongoflava AY nae anaelekea kufuata mkondo huo. Hawa na wengineo wenye mawazo kama hayo wanatumia vizuri umaarufu walionao kwenye jamii na wanastahili sapoti yetu. Wito wangu kwao ni kwamba wanapomiminiwa sifa kwa jitihada zao, wazitumie sifa hizo kuwa chemchem ya kusaka mafanikio zaidi. Pia wanaweza kwenda mbali zaidi kwa kutumia mianya ya biashara ya kimataifa kama vile katika e-Bay ili kuwawezesha Watanzania popote walipo duniani kunufaika na ubunifu wao. Kwa lugha ya mtaani, mie “nawapa tano”.Tanzania ya “masupastaa” wanaovuma kwa ubunifu wao,na sio kwa skendo,inawezekana.

Alamsiki


28 Oct 2007

Asalam aleykum,

Kwanza nianze kwa salamu za rambirambi kwa familia,ndugu,jamaa na marafiki wa marehemu Salome Mbatia,aliyetutoka hivi majuzi kutokana na ajali ya gari.Sote ni wasafiri,mwenzetu ametutangulia tu,Bwana ametoa Bwana ametwaa,jina lake lihimidiwe milele.Baada ya rambirambi hizo naomba kuzungumzia suala moja ambalo kwa naona kwa namna flani linaathiri umoja wetu wa kitaifa.Jambo hilo ni kuendekeza itikadi za chama kwenye matukio ambayo kimsingi ni ya kitaifa zaidi kuliko kichama.Katika picha mbalimbali kuhusu msiba wa marehemu Mbatia nimeona “makada” lukuki wa chama tawala wakiwa katika magwanda yao ya kijani na nyeusi.Nikabaki najiuliza,hivi waungwana hao wangevaa mavazi yao ya kawaida wangeonekana hawana majonzi ya msiba huo?Au walivaa mavazi hayo kwa maagizo ya kiongozi flani?Kama ni maagizo kutoka ngazi za juu,mbona viongozi wakuu wa chama hicho walikuwa kwenye mavazi yao ya kawaida tu (hasa suti nyeusi)?JK,Malecela,Karume,Makamba,nk wote walikuwa wamevalia suti nyeusi na wala sio magwanda ya kijani na nyeusi,pengine kwa sababu msiba huo ulikuwa wa kitaifa,na hata jeneza la marehemu halikuvikwa bendera ya CCM bali ya Taifa.

Nafahamu marehemu Mbatia alikuwa mwanachama,kada na kiongozi wa chama dume,lakini marehemu pia alikuwa naibu waziri wa serikali ambayo japo inaongozwa na CCM lakini inawatumikia Watanzania wote bila kujali itikadi zao.Katika utekelezaji wa majukumu yake ya unaibu waziri,marehemu Mbatia alikuwa akigusa maisha ya kila Mtanzania,awe mwanachama wa CUF,TLP,Chadema,au kama sie tusio memba wa chama chochote.Nafahamu waliovaa magwanda ya CCM watasema kuwa walitinga mavazi hayo kutokana na nafasi ya marehemu katika chama,lakini sote tunafahamu kuwa alama za chama (mfano bendera,vipeperushi,mavazi,nk) zina tabia ya kuvuta hisia hasi katika mikusanyiko ya isiyo ya kichama.Nafahamu pia kwamba kila mwombolezaji alikuwa na haki ya kuvaa vyovyote atakavyo lakini pia naamini wengi wetu tunapojiandaa kwenda kwenye misiba huwa tunatafakari nini cha kuvaa,na kuepuka mavazi ambayo yanaweza kuleta hisia tofauti.

Hakuna dhambi kuweka maslahi ya chama mbele ya chama kingine lakini ni dhambi kubwa kuweka maslahi ya chama mbele ya maslahi ya taifa.Chama cha siasa kinaweza kufa lakini taifa lazima liendelee kuwa hai.Mtu anaweza kuamua kuhama chama kimoja na kuingia kingine kadri apendavyo,lakini ni mbinde kwelikweli kuhama utaifa wako na kuchukua mwingine kirahisi namna hiyo.Nafahamu kuna watakaopingana nami,lakini binafsi naamini kwamba kuna wenzetu wamekuwa wakituletea “politiki” hata pale pasipostahili.Yaani matukio kadhaa ya kitaifa yamekuwa yakiporwa na hao wanaotaka kutuonyesha namna gani walivyo wakereketwa kwenye siasa.Na katika hili sio wanachama wa kawaida tu bali hata baadhi ya viongozi wenye nyadhifa serikalini.Kuweka kando mambo ya chama na kuzungumzia masuala ya kitaifa hakumfanyi kiongozi wa serikali kukosa sifa za uongozi.Kuna vikao na mikutano ya chama,na huko ndiko mahala pa kupiga propaganda za vyama.

Kwa kawaida huwa naanza makala zangu na habari za ughaibuni lakini niliona ni vema katika makala hii nikaanza na mada hiyo ya msiba wa marehemu Mbatia,na “kuwananga” wale walioleta mambo ya siasa kwenye msiba huo wa kitaifa.Huku ughaibuni,duru za kisiasa zinaelekea zaidi eneo la Ghuba ambapo kwa upande mmoja hali ya usalama ni ya wasiwasi huko kaskazini mwa Irak kwani majeshi ya Uturuki yameripotiwa kufanya mashambulizi kadhaa dhidi ya Wakurd.Waturuki wanadai kuwa lengo la mashambulizi hayo ni kuwadhibiti wapiganaji wa kikundi cha PKK kinachipigania kuunda kwa taifa huru la Wakurd.Kwa upande mwingine,kuna dalili kwamba Marekani inajiandaa kuivamia Iran.Majuzi,Marekani ilitangaza vikwazo kadhaa dhidi ya Iran,lakini zaidi ya hapo kuna taarifa kwamba jeshi la anga (US air force) limeomba fedha za dharura dola milioni 88 kwa ajili ya kufanya marekebisho kwenye ndege za kivita ziitwazo B2 ili ziweze kuhimili uzito wa mabomu yanayojulikana kama “Big Blu” au “the Mother of All Bombs” (mama wa mabomu yote).Mabomu hayo yana uzito wa takriban tani 13 kila moja,na yana uwezo mkubwa zaidi wa kupenya vizuizi (ardhi,miamba,nk).Inasemekana kuwa majengo ya kituo cha nyuklia cha Iran huko Natanz yapo futi 75 chini ya ardhi,Inaelezwa pia kwamba tayari Marekani imeshatambua “targets” 1000 nchini Iran ambazo zitakuwa za kwanza kushambuliwa pindi mambo yatapokuwa mambo.

Mahesabu ya kisiasa yanaashira pia kwamba wazo la mkutano kati ya Israel na Palestina utakaofanyika hivi karibuni huko Annapolis,Marekani (ambao unatarajiwa “kuzaa” taifa la Palestina) ni miongoni mwa dalili za Marekani kujipanga kuivamia Iran.Yaani mantiki hapo ni kwamba kwa kuunda taifa la Palestina,kelele za mataifa ya Waarabu wa Sunni kama Saudi Arabia na Misri zitakuwa sio kubwa sana pindi Iran itakaposhambuliwa na Marekani.Hata hivyo,wazo la kuishambulia Iran linaangaliwa kwa wasiwasi na baadhi ya wajuzi wa siasa za kimataifa na diplomasia.Kuna wanaodhani kwamba ni vema Marekani ikamaliza kibarua ilichojipachika huko Irak na Afghanistan kabla ya kukimbilia kuivamia Iran.Pia wanaonya kwamba uvamizi dhidi ya Iran unaweza kuzua wimbi kubwa la ugaidi wa kimataifa (pengine kutokana na madai kwamba Iran imekuwa ikivisaidia baadhi ya vikundi vinavyodaiwa kuwa vya kigaidi,mfano Hizbollah),kukongoroa kabisa hali ya usalama nchini Irak na pengine kusababisha bei ya mafuta kupanda zaidi ya dola 100 kwa pipa.

Sababu zinazotolewa na Marekani kuhusu umuhimu wa kuidhibiti Iran ni pamoja na kwamba dunia itakuwa mahala salama zaidi iwapo Iran haitakuwa na uwezo wa kutengeneza au kumiliki silaha za nyuklia (ilishasemwa huko nyuma kuwa dunia itakuwa salama zaidi pindi Saddam Hussein atapong’olewa madarakani).Ukweli ni kwamba Iran yenye uwezo wa kinyuklia ni tishio kwa swahiba mkuu wa Marekani,Israel.Pia kuna wanaotaka Bush aingie kwenye vitabu vya historia kwa “kuiadhibu na kuidhibiti Iran na hivyo kuepusha madhara yanayoweza kutokea pindi nchi hiyo ikiweza kutengeneza na kumiliki silaha za maangamizi”.Waumini wa mawazo haya wanatambua kuwa Bush amebakiwa na muda mchache kabla hajafungasha virago vyake kutoka jengo lilipo namba 1600 Pennsylvania Avenue (makazi ya rais,White House),na wanadhani kwamba asipotumia muda huu kuishikisha adabu Iran,basi inaweza kuwa vigumu mno kufanya hivyo mbeleni hususan iwapo mgombea yoyote wa chama cha Democrats atamrithi Bush.

Nirejee tena huko nyumbani.Hapa nina mawili.Kwanza,katika kikao kilichopita cha Bunge tulisikia namna baadhi ya watendaji katika Wizara ya Maliasili na Utalii wanavyoendeleza ufisadi.Waziri alieleza kuwa ameshakabidhi orodha ya wahusika mahala panapostahili,na akaahidi kuendelea kuwabana mafisadi katika wizara hiyo.Tukio la hivi karibuni ambapo magogo kadhaa yalikamatwa yakiwa tayari kusafirishwa nje,limezuia “mchezo wa kuigiza” ambapo wakati Waziri anasema hivi baadhi ya watendaji wake wanadiriki kumpinga hadharani kwa kusema vinginevyo.Hivi hawa wanaompinga Waziri wanapata jeuri hiyo wapi?Nimeona kwenye gazeti la “Habari Leo” ambapo Waziri Maghembe alieleza kwamba amejipanga vizuri kukabiliana na matatizo yote ndani ya wizara yake,ikiwa ni pamoja na tatizo la ufisadi.Yayumkinika kutabiri kuwa dhamira yake nzuri inaweza isifanikiwe kutokana na kiburi kilichojengwa na baadhi ya anaowaongoza katika wizara hiyo ambapo bila kujali protokali au nidhamu wanadiriki kupinga hadharani na kauli halali ya serikali (kupitia waziri wake).Hivi jeuri,kiburi na kujiamini kwa “wazalendo” hao inatoka wapi?

Mwisho,ni ushindi wa Simba dhidi ya Yanga.Mwenye kununa na anune,lakini ndio hivyo tena,milioni 50 hazikufanikiwa kumaliza uteja wa watani wetu wa mtaa wa Jangwani.Nilishatabiri katika makala za nyuma kuwa atakaefungwa kwenye mapambano wa watani wa jadi ataingia kwenye mgogoro.Mie nadhani kufungwa huko ni sehemu ndogo tu ya tatizo linaloikabili Yanga.Ukiangalia maelezo aliyotoa Mwenyekiti wa klabu hiyo pale mfadhili wao alipojitoa (kwa muda!?) ambapo alieleza kwa undani na kwa kuzingatia vipengele vya sheria kuhusu utata uliopo kwenye suala zima la klabu hiyo kugeuzwa kampuni.He!!muda si mrefu Mwenyekiti huyohuyo alisikika tena akipita huku na kule kuomba radhi.Je ina maana yale maelezo aliyotoa awali hayakuwa sahihi?Mie naamini yalikuwa,bado yako na yataendelea kuwa sahihi kama kweli Yanga (na Simba pia) wanataka wafike sehemu wakajiendesha wenyewe kwa mafanikio na kuachana na utegemezi.Yote yanawekana iwapo kila mmoja atatimiza wajibu wake.

Alamsiki

2 Aug 2007

Asalam aleykum,

Wanasema kuwa siasa inahitaji kuwa na mvuto (appeal).Lakini mvuto wa mwanamama Myra Bushell,mshindi wa uchaguzi mdogo wa kanseli kwa tiketi ya chama cha Liberal Democrats cha hapa Uingereza,ni zaidi ya mvuto wa kawaida unaohitajika kwenye siasa.Myra aligombea na kushinda nafasi ya uwakilishi kwenye kanseli ya Bideford huko Devon,huku akiwa ni mcheza-uchi/nusu uchi kwenye vilabu (stripper) na mwendesha huduma ya ngono-kwa-simu (phone-sex-line) ambayo anachaji pauni 1.50 kwa dakika (takriban shilingi 3500 za huko nyumbani).Yeye anajitetea kuwa hayo ni maisha yake binafsi nje ya siasa,lakini tayari wajumbe watatu wa kanseli hiyo wameshajiuzulu kupinga vitendo vya mwanasiasa huyo ambaye pia ana tovuti yake ya huduma za ngono.Myra anajitetea kwamba wakati anautumikia umma kama mwanasiasa,anapaswa pia kumudu gharama za maisha,na ndio maana amekuwa akijihusisha na shughuli hizo “nyeti.” Habari njema kwake ni kwamba katibu (clerk) wa kanseli hiyo,George McMauchlan,ametamka bayana kuwa Myra hajavunja sheria yoyote ya maadili ya kazi ya ujumbe wa kanseli kwa vile “shughuli zake binafsi nje ya siasa” haziathiri utendaji wake wa kazi.Kaazi kweli kweli!!


Tukiachana na habari hizo za mwanasiasa “stripper”, kwa takriban wiki nzima iliyopita,medani za sera za nje za Marekani ilikuwa imetawaliwa na habari kwamba taifa hilo lilikuwa linajiandaa kutekeleza mpango wa kuziuzia silaha baadhi ya nchi za Kiarabu na Mashariki ya Kati.Wanufaika wakubwa wa mpango huo ni pamoja na Saudi Arabia,Misri,na kama ilivyo ada,Israel.Hata hivyo,mpango huo umezaa mvutano wa namna flani kwenye duru za siasa za ndani za Marekani kwani wapo wanaodhani kwamba hoja ya serikali ya Bush kuwa inaziuzia silaha nchi kama Saudi Arabia na Misri ili,pamoja na mambo mengine,kudhibiti kujitanua kijeshi kwa Iran,inaweza kupingana na ukweli kuwa rafiki wa leo anaweza kuwa adui wa kesho,na silaha unazompatia leo kujilinda zinaweza kutumika kesho kukudhuru.Na mpango huu umekuja wakati wachambuzi wa siasa za kimataifa wanaoona kuna kuyumba kwenye urafiki wa muda mrefu kati ya Marekani na Saudi Arabia.Hivi karibuni,Saudi iliweka bayana mtizamo wake kuhusu vita ya Irak kwa kusema kuwa uvamizi wa Marekani nchini Irak unachochea machafuko na suluhisho pekee ni kwa majeshi ya kigeni kuondoka nchini Irak.Pia kumekuwepo shutuma za hapa na pale kwamba Saudi Arabia inavisapoti vikundi vya madhehebu ya Sunni nchini Irak ili kuvikabili vikundi vya madhehebu ya Shia ambavyo inadaiwa vinapata sapoti ya Iran.Kitakwimu na kujiografia,Saudi ni taifa la ki-Sunni wakati Iran ni la ki-Shia,na mahusiano kati ya nchi hizo mbili sio mazuri.Saudi kwa upande wake inahofia sana kukua kwa nguvu za kijeshi za Iran,hasa kwa vile hadi sasa,ukitoa Israel,Saudi ni taifa lenye nguvu kubwa katika eneo la Ghuba na Mashariki ya Kati.

Wakati mwingine ni vigumu kuzielewa sera za nje za Marekani kwani kwa jinsi flani ilipaswa kujifunza kutokana na maamuzi yake ya zamani ambayo kwa namna moja au nyingine yamekuwa yakiiumiza kichwa katika kipindi hiki tulichonacho,kwa mfano msaada wake wa silaha kwa Irak wakati Saddam alipokuwa rafiki wa nchi hiyo,na misaada yake kwa mujahidina wa Afghanistan wakati wa vita dhidi ya Muungano wa nchi za Kisovieti (USSR).Tawala za nchi nyingi za Kiarabu na Ghuba sio za kidemokrasia (kwa vipimo vya nchi za magharibi),na miongoni mwa sababu zinazodaiwa kuchangia kuibuka kwa siasa za msimamo mkali wa kidini katika nchi hizo kushindwa kwa tawala hizo kuleta mabadiliko ya manufaa ya kisiasa,kiuchumi na kijamii.Lakini katika kukoroga zaidi mambo,baadhi ya tawala hizo zimekuwa zikuvikumbatia na kuvifadhili vikundi vyenye msimamo mkali wa kidini ili tawala hizo ziendelee kuwa madarakani.Kwa uchambuzi mwepesi,yayumkinika kusema kuwa hatma ya tawala hizo kwa muda mrefu sio ya kuaminika sana,na Marekani inaweza kujutia huko mbeleni kwa kuzilinda tawala hizo kwa misaada ya kijeshi.

Na taarifa zaidi kutoka Irak zinaeleza kuwa “picha haziivi” kati ya mkuu wa majeshi ya Marekani nchini humo,Jenerali David Petraeus,na Waziri Mkuu wa Irak,Nour al-Maliki.Inasemekana kuwa Maliki alishamuomba Rais Bush amwondoe Jenerali huyo msomi mwenye shahada ya kwanza katika sayansi (Bachelor of Science),shahada ya uzamili katika Utawala wa Umma (M.A in Public Administration) na shahada ya uzamifu kwenye siasa za kimataifa (PhD in International Relations) na alishakuwa (assistant) Professor kwenye US Military Academy. “Bifu” (kupingana) kati ya Maliki na Jen Petraeus kunatokana na baadhi ya maamuzi yanayopingana kati ya watu hao muhimu kwa mafanikio au kutofanikiwa kwenye sera ya Bush kuhusu Irak.Inaelezwa kuwa Maliki haafikiani na mpango majeshi ya Marekani unaoelekea kuasisiwa na Jen Petraeus wa kuvipatia silaha vikundi vya madhehebu ya Sunni ili vipambane na wapiganaji wa Al-Qaeda nchini humo.Maliki ambaye ni muumini wa madhehebu ya Shia anaelekea kuhofia kuwa silaha hizo zinaweza kutumika dhidi ya vikundi vya madhehebu ya Shia,au kwa mtizamo wa muda mrefu,kuchangia vita vya wenyewe kwa wenyewe pindi majeshi ya Marekani yatakapoondoka (kama kuna kuondoka kweli).

Baada ya mjadala wa siasa za kimataifa,hebu tegeukie mambo mengine ya huko nyumbani.Nitahadharishe kuwa naamini baadhi ya ntakayoandika hapa yatawaudhi watu flani lakini kuudhika kwao kutakuwa na maana moja tu kwangu:kwamba ujumbe umefika na wabadilike badala ya kununa.Binafsi,nadiriki kusema kuwa mzazi makini hawezi kumrushusu binti yake kuingia kwenye mambo ya u-Miss.Kwanini?Kwa sababu inaelekea wengi wa mabinti wanaotafuta u-miss huwa aidha wanarubunika kuwa wenye tabia mbovu baada ya kupata majina au pengine fani nzima ya u-miss ni kichocheo cha umalaya (samahani kwa maneno makali).Yaani kila kukicha utaskia sijui Miss nanihii katembea na mume wa mtu,au Wema Sepetu kapigwa picha za utupu,au Faraja Kotta kalibwaga buzi lake lililoiba fedha wapi sijui,na vituo vingine mia kidogo.Kuna kasoro kwenye fani ya u-miss lakini jamii inaelekea imelifumbia macho suala hilo.Lundenga,Chipungahelo na wadau wengine wa fani ya u-miss wana jukumu la kuithibitishia jamii kuwa tatizo haliko kwenye fani hiyo bali ni kwa baadhi tu ya washiriki.Na kama tatizo ni washiriki basi watuambie bayana inakuwaje wanaweza kupenya katika ngazi mbalimbali hadi kifikia levo ta taifa na kuanza kutuonyesha madudu yao.Rafiki yangu mmoja mwandishi wa habari aliwahi kunidokeza kuwa fani hiyo imetawaliwa sana na viongozi,wadhamini na mapromota walafi wa kula uroda ambao wanarahisishiwa kazi na mabinti wenye tamaa ya umaarufu wa chapchap,ambao kwao sio ishu kuvua “makufuli” yao ili wakwae u-miss.Ujumbe wangu kwenu ni simpo:msipokuwa makini mtaondoka kwa kilo mbili,na kwa vile mnathamini sana umaarufu,basi kudhoofika kwa afya zenu kutatawala sana kurasa hizohizo zinazoripoti kila siku namna mnavyoibemenda Amri ya Sita kama hamna akili nzuri.Mkikasirika shauri yenu lakini mmezidi kufanya mambo ya aibu.

Halafu kuna mambo mawili yamenisikitisha sana.La kwanza ni hii tabia ya ubabe inayoelekea kumkolea msanii TID.Binafsi,nazipenda sana kazi za kijana huyu,na mwanzoni nilikuwa namtofautisha na wasanii wengine wa bongo kwa vile amewahi kukaa ugahibuni kwa muda wa kutosha na amekuwa akipata mialiko ya nje mara kwa mara.Lakini pengine kwa kutotambua kuwa taswira (image) ya msanii ni muhimu katika kumuweka au kumporomosha kwenye chati,ameendelea kushika vichwa vya habari kwa matukio yasiyopendeza.Wimbo wake naoupenda sana unaitwa “chagua moja”,nami ujumbe wangu kwake ni mfupi:chagua moja kati ya kujiporomosha wewe mwenyewe kwa matendo yasiyofaa au jirekebishe tabia zako ili uendelee kubaki kuwa “Top In Dar.” Usikasirike,ni somo jepesi tu hilo.

Jingine lililonikera ni gazeti la RISASI ambalo katika toleo lake la Julai18-20 lilikuwa na habari kwamba “Warembo TZ wapiga picha za X tupu…zasambazwa mitaani,baadhi yao ni washiriki wa kusaka mataji ya u-miss.” Kinachosikitisha sio kama iwapo habari hiyo ni ya kweli au ya kubuni bali ni picha zilizotumika kwenye habari hiyo.Rafiki yangu mmoja aliyeko Marekani amenifahamisha kuwa wasichana walioko kwenye picha hizo ni wacheza filamu za ngono (porn stars) wa Marekani na wala sio Watanzania.Kwa kuthibitisha alichokuwa anasema,alinipatia tovuti ambazo zina picha za Wamarekani hao weusi.Kama picha zilizotumiwa na RISASI ni feki basi yayumkinika kusema kuwa hata habari yenyewe ni feki.Hivi ni uzembe wa mhariri kucheki ukweli wa habari husika au ndio kuwafanya Watanzania wajinga kwa kuwapa habari “sensational” ambazo hazina ukweli?Nyie ni watu wazima ambao mmeshatengeneza faida ya kutosha kwa kuandika udaku lukuki wa kweli,sasa tamaa ya nini hadi mfikie hatua ya kunyofoa mapicha kwenye mtandao na kuzusha habari?Shame on you!

Alamsiki

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.