Showing posts with label Scottish Independence. Show all posts
Showing posts with label Scottish Independence. Show all posts

26 Sept 2014

Mahojiano na dadangu Fina Mango katika kipindi chake cha Makutano Show kinachorushwa na kituo cha redio cha Magic FM, Dar es Salaam. Masahihisho: Katika mhojiano hayo nimeeleza kwa makosa kuwa Great Britain inaundwa na England yenye mji mkuu London, Wales yenye mji mkuu Cardiff, na GLASGOW yenye mji mkuu Edinburgh. Niliitaja Galsgow kimakosa badala ya Scotland. Kadhalika, katika mahojiano hayo kuna sehemu nimesema kimakosa kwamba moja ya ugumu ulioikabili kambi ya NO ni jinsi ya kuitetea hoja ya mafuta. Nililenga kusema 'kambi ya YES na sio NO. Naomba samahani sana kwa makosa hayo yaliyotokana na kile Waingereza wanaita 'heat of the moment.'

24 Sept 2014

Scotland's First Minister and leader of the Scottish National Party (SNP) Alex Salmond (C). (Reuters/David Moir)
Chama tawala hapa Uskochi cha Scottish Nationalist Party (SNP) kimekuwa chama cha tatu kwa ukubwa kwa Uingereza nzima baada ya kuvuna wanachama wapya kwa asilimia 66% katika muda wa siku nne tu baada ya kushindwa katika kura ya uhuru wa Uskochi.

Jumla ya wanachama wapya 26,000 wamejiunga na chama hicho tangu Alhamisi iliyopita, na hivyo kutunisha idadi ya wanachama wake hadi kufikia zaidi ya 51,000, takriban maradufu ya idadi ya awali ya wanachama wake.

Takwimu hizo zimeleta mshangao mkubwa kufuatia kambi ya 'Ndiyo' iliyokuwa ikiongozwa na chama hicho tawala kushindwa katika kura ya uhuru kwa asilimia 45 kwa 55, na hatimaye kiongozi wake, Waziri Mkuu wa Uskochi, Alex Slmaond, kutangaz aanaachia ngazi mwezi Novemba mwaka huu.

Takwimu hizo pia zinamaanisha kuwa SNP imefanikiwa kuvuta asilimia 10 ya ya wakazi wa Uingereza nzima, na kuipiga kikipiga kikumbo chama cha Liberal Democrats kwa idadi ya wanachama wenye kadi za uanachama.

Wabunge wa chama hicho waliokutana Hollyrood, katika mji mkuu Edinburgh, walionyesha kuridhishwa na takwimu hizo mpya na mwelekeo wa jumla wa Uskochi kufuatia kura ya aidha Uskochi iwe huru au iendelee kubaki sehemu ya muunganowa Uingereza.

"Devolution (kuipatia Uskochi mamlaka zaidi badala ya uhuru) ililenga kuua utaifa (wa Uskochi)," alisema mbunge mmoja wa SNP. "Kisha matokeo ya kura ya uhuru na kujiuzulu kwa Salmond. Lakini matokeo yamekuwa kinyume kabisa."

Inadaiwa pia kuwa wanachama wapya 3000 wamejiunga chama cha Scottish Greens huku chama kingine cha Scottish Socialist Party kikivuatia wanachama wapya. Vyama vyote hivyo viwili vilikuwa vikisapoti uhuru wa Uskochi.

Jumla mpya ya idadi ya wanachama wa SNP ilikuwa 50000 mnamo saa 6 na dakika 40 jana, kulinganisha na wanachama 25642 Alhamisi iliyopita siku ya upigaji kura ya uhuru.

CHANZO: Imetafsiriwa kutoka vyanzo mbalimbali mtandaoni

21 Sept 2014

Scotland
Kura ya kuamua hatma ya Uskochi kama ibaki kuwa sehemu ya United Kingdom au iwe nchi huru imekwisha, wak asilimia 55 ya wapigakura kusema HAPANA na 45 kusema NDIYO.Kwa matokeo hayo, muungano unaounda UK, wenye umri wa miaka 307 umesalimika.

Wakati nitaielezea kwa undani zaidi kura hiyo ya uhuru wa Uskochi katika makala yangu ya Jumatano ijayo ndani ya jarida la RAI MWEMA,katika post hii nitazungumzia kinachoanza kuonekana kama 'Uskochi kuingizwa mkenge' kufatia kuanza kuparaganyika kwa baadhi ya ahadi za msingi zilizopelekea ushindi wa kundi lililotaka Uskochi iendelee kuwa sehemu ya Muunganowa UK.

Mmoja wa wanasiasa wanaotajwa kama waliofanikisha kuunusuru Muunganowa UK ni Waziri Mkuu wa zamani, Gordon Brown, ambaye kama Waziri Mkuu wa sasa, David Cameron, kiongozi wa chama cha upinzani cha Labour Ed Milliband, Naibu Waziri Mkuu na kiongozi wa chama cha Liberal Democrats, Nick Clegg, na kiongozi wa 'kampeni ya Better Together' ya kuunga mkono muungano ambaye pia alikuwa 'Waziri wa Fedha' wa serikali ya Labour, Alistair Darling, kwa pamoja waliwaahidi wapigakura ya uhuru wa Uskochi kuwa wakikataa uhuru 'watazawadiwa' kwa nchi hiyo kupatiwa mamlaka zaidi ya kiutawala na kimaamuzi.

Mamlaka hizo zinafahamika kama 'Devo Max.'Kimsingi Devo Max, kifupisho cha Maximum Devolution,  inamaanisha Bunge la Uskochi kuwa na nguvu katika kila kitu ispokuwa ulinzi na mambo ya nje. Hata hivyo licha ya ahadi kuwa Uskochi itapatiwa mamlaka zaidi, uwezekano wa kupatia Devo Max kwa maana halisi ya nguvu zote kabisa zinazohitajiwa ni kama haupo.

Kwa sasa, na hadi wakati inapigwa kura ya uhuru au la, Uskochi imepewa mamlaka ya kujiamulia mambo yake yenyewe katika sekta za elimu, afya, huduma za jamii, makazi, utalii, mazingira, uvuvi, misitu, kilimo, sheria na usalama wa raia, na baadhi ya maeneo katika sekta ya usafiri. Kwa upande mwingine, serikali kuu ya Uingereza (Westminster) ina mamlaka katika sekta ya ulinzi, hifadhi ya jamii (social security), mafao kwa jamii (benefits)- kwa hapa Uingereza, watu wasio na kazi wanalipwa fedha ya kujikimu na kodi ya nyumba na serikali,gesi na mafuta, nishati ya nyuklia, uhamiaji, ajira, mawasiliano ya radio na runinga, biashara na viwanda sera za nje, masuala ya walaji (cunsumer affairs) na Katiba. 

Sasa kilichoahidiwa na Cameron na wenzake kushawishi Waskochi wakatae uhuru kuhusiana na Devo Max hakipo bayana sana. Miongoni ya yaliyomo kwenye ajenda ni Uskochi kuwa na mamlaka zaidi ya ukusanyaji kodi na mafao ya makazi kwa wasio na ajira. Suala la gesi na mafuta na kodi za mashirika (corporation tax) hayapo kabisa katika makubaliano hayo ambayo kimsingi bado hayajafikiwa.

Lakini hata kabla shamrashamra za kusherehekea kusalimika kwa Muungano wa UK hazijaisha, kizaazaa kimeibuka katika jinsi ya kutekeleza ahadi hiyo ya kutoa mamlaka zaidi kwa Uskochi. Kwa upande mmoja, ahadi hiyo iumevutia madai ya mamlaka zaidi kutoka Wales na Northern Ireland kama nchi ambazo pamoja na Uskochi na England zinaunda muunganowa UK. Kwa upande mwingine, baadhi ya 'mikoa' yenye wakazi wengi, kama vile Manchester, Yorkshire, Cornwall, nk nayo imeanza kudai kupatiwa mamlaka zaidi ya kiutawala.

Ttatizo kubwa zaidi lipo katika kupata mwafaka kati ya chama tawala Conservatives na wapinzani wao wa Labour. Ili Uskochi iweze kupatiwa mamlaka iliyoahidiwa, Bunge la Muungano huko Westminster litalazimika kufanya mabadiliko ya katiba. Hilo tu ni tatizo pia, kwani kwa mujibu wa taratibu za hapa UK, mabadiliko ya katiba ya nchi hii ni zoezi linalohitaji muda mrefu. Lakini muda haupo upande wa Serikali Kuu kwa vile kuna matarajio makubwa kutoka kwa Waskochi waliokataa uhuru.

Hata urasimu wa mabadiliko ya Katiba ukiwekwa kando, bado kuna tatizo linalowakabili Cameron na Conservatives wenzie na Milliband na Labour yake. Kwa Cameron, ile kuahidi tu kuwa ataipatia Uskochi mamlaka zaidi, wabunge wengi tu katika chama hicho nao wameanza kudai mamlaka zaidi kwa majimbo yao. Kwa Milliband, tatizo ni kubwa zaidi. Kwa sasa, chama cha Labour kina wabunge 49 kutoka Uskochi katika Bunge Kuu la Muungano, ambao pia wanapiga kura katika maamuzi yanayoihusu England pekee. Hii imerejesha kinachoitwa 'swali la Lothian ya Magharibi' (the West Lothian Question), yaani kuhoji kwanini wabunge kutoka Uskochi katika Bunge la Muungano waruhusiwe kupigia kura masuala yanayoihusu England pekee ilhali wabunge kutoka England hawana fursa hiyo. Hii inalingana na 'kilio' cha baadhi ya wanasiasa wa Tanzania Bara wanaodhani si sawia kwa wabunge kutoka Zanzibar katika Bunge la Muungano kuhusika katika maamuzi ya masuala yanayohusu Bara pekee ilhali hakuna mbunge wa Bara mwenye mamlaka kama hiyo katika Bunge la Zanzibar. Kama ilivyo huko nyumbani, hakuna mbunge wa England katika Bunge la Uskochi, kama ambavyo hakuna mbunge kutoka Bara katika Bunge la Zanzibar.

Wakati chama cha Labour kitaanza Mkutano wake Mkuu hapo kesho na ajenda kuu ya Milliband ilipangwa kuwa kuzungumzia taasisi muhimu ya huduma za afya (National Health Service-NHS) sasa anaweza kulazimika kuzungumzia uwezekano wa chama hicho kupunguziwa nguvu katika Bunge Kuu la Uingereza iwapo mpango wa kuwanyima malaka ya kimaamuzi wabunge kutoka Uskochi katika Bunge la Muungano utatekelezwa.

Na siku hiyohiyo ambapo Labour wanaanza mkutano wao mkuu, Cameron anatarajiwa kutoa hotuba kuhusu kinachoiwa 'kura za Waengland kwa sheria za England' (English votes for English laws), kwa maana ya kura zinazopigwa katika Bunge Kuu katika masuala yanayohusu England zipigwe na wabunge wa England pekee, na wale wa kutoka Uskochi wasiruhusiwe kupiga kura hizo.

Tayari Cameron ameanza kumlaumu Milliband kwa upinzani wake dhidi ya mpango huo, akidai kuwa kiongozi huyo wa Labour anaisaliti England. Kwa upande wake, Labour inamshutumu Cameron na chama chake kwa kile inachokiona kama jitihada za kupinguzia Labour nguvu katika Bunge la Muungano.

Mhanga wa 'mgogoro' huo ni Uskochi kwani pasi kufikiwa mwafaka kati ya vyama hivyo viwili, uwezekano wa Uskochi kutekelezewa ahadi ya kuongezewa mamlaka ya kiutawala sio tu utachukua muda mrefu bali pia unaweza kukwama kabisa.

Na Waziri Mkuu wa Uskochi, Alex Salmond, aliyetangaza kuachia ngazi mwezi Novemba tayari ameingilia kati suala hilo na kuwakumbusha Cameron na Milliband kwamba tofauti zao zitapelekea waliopiga kura ya kukataa uhuru wa Uskochi kujiona kama 'wameingizwa mkenge' kwa kupewa ahadi za hadaa.

Kwa mtizamo wangu ninadhani mwamuzi ni muda (time will tell) lakini kama nilivyosapoti kambi iliyotaka uhuru wa Uskochi, imani yangu kutoka kwa Cameron, Milliband na wanasiasa wengine wa Westminster ni ndogo. Na hoja hii ilijitokeza wakati wa kampeni za kampeni za uhuru ambao kuna waliohoji, kama tupo 'Better Together' hivi sasa, kwanini basi mambo hayaendi sawia-kwa maana ya wanasiasa wa Westminster kuahidi mengi lakini kutekeleza machache. Kadhalika, kwa kukataa uhuru wa Uskochi kwa ahadi kutoka kwa wanasiasa, Waskochi wanaweza kuwa wamerudi kulekule kwa kurejea hatma yao mikononi mwa wanasiasa, tofauti na suala zima la kura ya uhuru lilivyoendeshwa  kwa kiasi kikubwa na wananchi wenyewe kwa mustakabali wao





20 Sept 2014


Kwanza ninaomba kukiri bayana kuwa nimehuzunishwa na matokeo ya kura ya maoni kuhusu uhuru wa Uskochi. Hiyo inatokana na ukweli kwamba sio tu nilikuwa naunga mkono kambi ya 'Yes' iliyokuwa inataka uhuru wa taifa hili bali pia nilipiga kura ya 'Ndiyo.'

Lakini kwa vile uamuzi wa iwapo Uskochi iwe nchi huru au iendelee kubaki sehemu ya United Kingdom ulipaswa kuamuliwa kwa wingi wa kura-hata ingekuwa moja tu- sina budi kuafiki matokeo na kukubaliana na ukweli. Ukweli kwamba asilimia 55 ya wapiga kura wametaka Uskochi iendelee kuwa sehemu ya UK huku waliotaka uhuru wakiwa asilimia 45 inamaanisha wengi wa Waskochi wanataka iwe hivyo. Na ukweli unabaki kuwa ukweli hata kama ni mchungu.

Hata hivyo, wakati ninatambua umuhimu wa sie kama Watanzania kujifunza kuhusu kura hiyo ya uhuru wa Uskochi, binafsi ninaona kuna unafiki mkubwa katika suala hili zima la 'tujifunze kutoka Uskochi.' Naomba nieleweke. Ni vema tujifunze kutoka kwa hawa wenzetu kuhusu hatma ya Muungano wetu lakini ninadhani ni unafiki kuamua kuchagua jema moja na kupuuzi mema mengine lukuki ya kujifunza kutoka kwa hawa wenzetu.

Eneo la kwanza la unafiki huo ni katika suala la uraia pacha. Moja ya hoja kuu iliyouwa wazo la uraia pacha kwa Watanzania walio nje ya nchi hiyo ni dhana fyongo kwamba uraia pacha ni tishio kwa usalama wa Tanzania. Si wanasema 'tujifunze kutoka Uskochi'? Sasa kwa taarifa tu ni kwamba katika kupiga kura hiyo ya uhuru wa Uskochi, baadhi ya wakazi wa taifa hili ambao japo si wazaliwa wala raia wa hapa waliruhusiwa kupiga kura. Kila mkazi wa Uskochi ambaye anatoka nchi za Jumuiya ya Madola aliruhusiwa kupiga kura. Na mie- hata kama ningekuwa sina sababu nyingine zilizoniruhusu kupiga kura- ningeweza kupiga kura kwa kigezo cha kuzaliwa Tanzania ambayo ni mwanachama wa Jumuiya ya Madola.


Ni muhimu sana kutambua kuwa haki ya kupiga kura ni moja ya haki muhimu mno kwa mwananchi kwa sababu inachangia upatikanaji wa uongozi wa mahala husika, sambamba na ushiriki katika maamuzi yanayohusu mustakabali wa taifa husika, kama ilivyo kwa suala la kura ya uhuru wa Uskochi.

Je Waskochi ni wendawazimu kuruhusu hata watu wasio na urai wa nchi hii kupiga kura? Hapana. Wenzetu wanathamini na kutambua mchango wa kila mwenye uhusiano na nchi hii, iwe wa kuzaliwa, asili au makazi. 

Na je kwa Waskochi kuruhusu  wakazi wa nchi hii ambao sio wazaliwa wa hapa, au wasio na uraia wa hapa, kupiga kura imehatarisha usalama wake? 

Naomba ieleweke kuwa haki ya kupiga kura haimfanyi mhusika kupewa uraia wa hapa bali ni moja ya vitambulisho muhimu sana. Kwa mfano, daftari la wapiga kura ni moja ya nyenzo muhimu katika uchunguzi unaofanywa na taasisi za fedha (credit check) kabla ya kutoa mkopo au hata kufungua akaunti ya benki. Kimsingi, kuwemo kwenye daftari hilo kunampatia mkazi wa hapa haki flani ambazo japo si sawa na uraia zinamsaidia katika maeneo mbalimbali.

Oh yes, tujifunze kutoka taifa tajiri la Uskochi linalowaenzi wageni wasio raia wa taifa hili ilhali masikini sie tunawahofia Watanzania wenzetu ambao kwa sababu moja au nyingine wamelazimika kuchukua uraia wa nchi nyingine. Hapo kuna neno sahihi zaidi ya unafiki?

Twende katika maeneo mengine. Moja ya kumbukumbu muhimu kwenye runinga wakati matokeo ya kura hiyo yanatangazwa ni kuonekana kwa mkimbizi wa kisiasa kutoka Papua New Guinea, Benny Wanda, (pichani) akielezea anachojifunza kutoka kwa zoezi hilo la kidemokrasia 
Benny Wenda from West Papua, Indonesia

Wanda alikuja Uskochi kama mgeni wa kikundi kinachoitwa Radical Independence kujifunza jinsi kura ya maoni kuhusu uhuru inavyoandaliwa na kufanyika. Katika mahojiano yake na kituo cha televisheni cha BBC, kiongozi huyo alieleza jinsi alivyoguswa mno na jinsi uhuru ulivyokuwa ukitafutwa kwa uhuru mkubwa, akitolea mfano kutokuwepo kwa wanajeshi au polisi au vifaru mitaani tofauti na hali ilivyo nchi kwake wakati wa harakati za kudai uhuru kutoka Indonesia. Naam, tunasema tujiefunze kutoka Uskochi, lakini kimatendo ni kama picha hii hapa chini inavyoonyesha, na hapa sio katika harakati za wananchi kudai uhuru bali kutumia tu haki yao ya kikatiba kupinga uhuni unaofanywa dhidi ya upatikanaji wa Katiba mpya huko Dodoma 




Hebu tuache unafiki. Hivi kama hiyo haki 'kidogo' tu ya kuandamana kwa amani kwa minajili ya kutetea upatikanaji wa Katiba yenye maslahi kwa Watanzania wote, sambamba na kuokoa mabilioni ya fedha yanayotafunwa kwa Bunge 'feki' la Katiba huko Dodoma linazua haya, je tunaweza kukaribia japo kiduchu walipofika Waskochi kupiga kura kwa amani na utulivu kuhusu hatma ya nchi yao?

Na hata tukiweka kando hilo la matumizi makubwa ya nguvu za dola kunyamazisha sauti za wananchi, sambamba na kulazimisha matakwa ya watawala, bado kuna unafiki mwngi ne mwingi tu kama unavyotanabaishwa na picha zifuatazo


Picha hiyo juu inapigia mstari hoja yangu kuhusu unafiki. Naam, gazeti la serikali Daily News latoa rai kuwa tujifunze kutoka Uskochi, lakini picha iliyopo katika ukurasa huo inakinzana kabisa na hali ilivyo hapa Uskochi. Picha hiyo ni ya Rais Jakaya Kikwete akihutubia nchini Marekani ambapo amekwenda TENA kwa ziara ya WIKI MBI. Ni majuzi tu alikuwepo huko kwa siku kibao, lakini katika kuendeleza spirit ya 'safari ni safari' ameenda tena nchi humo.Ni hivi, ni nadra mno kusikia Waziri Mkuu wa Uskochi Alex Salmond akizurura huku na kule, au Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameron akiwa kiguu na jia hapa na pale, au hata Malkia Elizabeti kuwa msafiri wa kila kukicha. Na hawa ni viongozi wa taifa hili tajiri kabisa lakini sio wazururaji kama Rais wetu.

Ndio rais lazima asafiri lakini sio kila baada ya wiki kadhaa, tena kurejea sehemu zilezile alizokwishatembelea. Hivi tangu 2014 hii ianze Kikwete ameshakwenda Marekani mara ngapi? Ndio, tujifunze kutoka Uskochi kuhusu kura ya uhuru wao lakini pia tujifunze kuhusu umuhimu wa viongozi kama Kikwete kutambua kuwa Tanzania yetu ni maskini isiyoweza kubeba gharama zisizo za lazima za Rais wake kusafiri kila anapojiskia.

Natambua ukweli kuwa kutokana na umasikini wetu, kuna haja ya viongozi wetu kwenda nje kusaka misaada. Lakini ni nani asiyejua kuwa asilimia kubwa ya misaada hiyo inaishia kwenye akaunti za mafisadi? Kadhalika, busara kidogo tu inaweza kutufundisha kwamba safari hizo za mara kwa mara za Kikwete zinatafuna sehemu ya fedha zinazosakwa kama misaada kwa nchi yetu.


Katika gazeti hili hapo juu tunakutana tena na wito wa kujifunza kutoka kwa kura ya uhuru wa Uskochi, lakini chini yake kuna habari kwamba deni la taifa limepaa hadi kufikia shilingi TRILIONI 42, kwa tarakimu ni shilingi  42,000,000,000,000 Na wakati hali yetu ikiwa mbaya kiasi hicho, bado twashuhudia serikali yetu ikifanya matumizi ya kitajiri kwa mfano kuruhusu uhuni unaoendelea huko Dodoma kwa jina la Bunge la Katiba, huku Kikwete akiendlea na safari zake za uuvumbuzi wa dunia.


Na picha ya hapo juu inathibiths unafiki wa kauli ya 'tujifunze kutoka Uskochi.' Kwa kifupi, zoezi zima la hadi kufikia kupigwa kura ya maoni liliambatana na uwazi na haki kwa kiwango cha juu kabisa. Japo ajenda ya uhuru ilikuwa katika manifesto ya chama tawala hapa Uskochi cha SNP, suala la uhuru lilibaki kuwa mikononi mwa Waskochi wote. Sasa kama mnavyoona hapo kwenye picha, kichwa kikuu cha habari kinahusu mwanasiasa wa upinzani Lema kupigwa marufuku na wafuasi wake kuandamana. Hivi haiwezekani wakaruhusiwa kuandamana huku wakisindikizwa na polisi? Na uzoefu umeonyesha kuwa mara nyingi polisi wakiridhia, maandamano hufanyika na kumalizika kwa amani. Mara nyingi pia, uamuzi wa polisi kulazimisha wananchi wasiandamane hupelekea vurugu na maafa yasiyo ya lazima


Pichani juu ni maandamano ya wanauonga mkono Uskochi kubaki sehemu ya UK, yaliyofanyika jana jioni hapa Glasgow, na polisi walikuwepo kwa minajili ya kuhakikisha hakuna uvunjifu wa amani lakini sio kuyazuwia maandamano hayo.

Nimalizie makala hii ndefu kidogo kwa kutilia mkazo kuwa tuna mengi ya kujifunza kutoka Uskochi na sio suala hilo la kura ya maoni pekee. Wanasiasa wa Uskochi na pengine Uingereza kwa ujumla wametoa darasa zuri kwa wababaishaji wetu huko nyumbani ambao licha ya kuwalipa mamilioni ya shilingi kwa mwezi kama mishahara na posho lakini tunachoishia kushuhudia ni matusi, vijembe, malumbano na upuuzi mwingine kwenye vikao vya Bunge la kawaida na hili la Katiba.

Ndiyo, umoja ni nguvu, na kura ya maoni ya uhuru wa Uskochi kumalizika kwa nchi hiyo kubaki sehemu ya United Kingdom kunatukumbusha sie wana-Muungano wa Tanganyika na Zanzibar juu ya umuhimu wa mshikamano lakini ni muhimu kutambua kuwa mazingira waliyopitia Waskochi kufikia hapa yameletwa heshima na utambuzi wa haki za kibinadamu, kidemokrasia sambamba na kuangalia mustakabali wa nchi hii sio kwa leo na kesho tu bali pia miaka mingi ijayo.





10 Sept 2014

Royal sources made clear that there had been no suggestion from anyone in Government or opposition for the Queen to take a public stand
Malkia Elizabeti wa Pili, mtawala wa 'Muungano wa Uingereza' (United Kingodm) ametanabaisha kuwa kamwe hatoingilia hatma ya kura itayoamua iwapo Uskochi iendelee kuwa sehemu ya 'Muungano wa Uingereza' ua iwe taifa huru.

Hatua hiyo ya nadra imetokana na maoni ya baadhi ya wabunge hapa Uingereza kwamba Malkia aingilie katik katika suala hilo.

Waziri Mkuu (First Minister) wa Uskochi anaweza kuingia matatizoni baada ya kauli yake jana kwamba alikutana na Malkia na akaambiwa kuwa mwanamama huyo yupo tayari kuwa Malkia wa Uskochi iliyo huru.

Lakini makazi ya Malkia ya Buckingham Palace yameweka bayana msimamo kwamba Malkia hajihusishi na siasa na walio katika nyadhifa za kisiasa wanapaswa kuhakikisha hali hiyo inabaki hivyo.

Vynazo vimethibitisha kuwa Malkia siku ya kupiga kura- tarehe 18 mwezi huu- Malkia Elizabeth atakuwa katika makazi yake ya faragha kwenye ukanda wa Nyanda za Juu wa Uskochi (Scottish Highlands)

Japo makazi ya Malkia yamesisitiza kuwa mtawala huyo haingilii masuala ya kisasa lakini wachambuzi wanaeleza kuwa huhitaji kuwa mtaalam wa siasa kumaizi kuwa Malkia anatamani 'Muungano wa Uingereza' uendelee, na kutumia swali la kuamsha tafakuri la 'Hivi Baba Mtakatifu (Papa) ni Mkatoliki? (kwa maana ya kuwa ili mtu awe Papa shurti awe Mkatoliki)

CHANZO: Habari hii imetafsiriwa isivyo rasmi kutoka tovuti ya gazeti la Daily Mail la hapa Uingereza

7 Sept 2014

Zikiwa zimebaki siku 11 tu kabla ya wakazi wa hapa Uskochi kupiga kura ya kuamua iwapo taifa hili liwe huru au liendelee kubaki katika 'Muungano wa Uingereza', kwa mara ya kwanza kabisa, kura ya maoni kuhusu 'uhuru' huo inaonyesha  wanaotaka 'uhuru' huo wanaongoza kwa asilimia 51.

Japo kitakwimu, hiyo ni sawa na sare, ukweli kwamba haijawahi kutokea kwa wanaotaka uhuru kuongoza katika kura yoyote ile ya maoni unaleta uwezekano japo kidogo wa kura ya 'Ndio' kwa wanaotaka uhuru kufanikiwa.

Kura mpya ya maoni iliyofanywa na taasisi ya kura za maoni inayoheshimika sana hapa Uingereza, YouGov, inayochapishwa Jumapili hiiinaonyesha wanaotaka uhuru wanaongoza kwa asilimia 51 huku wasiotaka uhuru wakiwa na asilimia 49, ukiondoa wapiga kura ambao hawajafikia uamuzi (undecided).

Kadhalika, gazeti la Sunday Times lililoipa kazi ya kusanya maoni taasisi hiyo ya YouGov linaeleza kwamba Malkia wa Uingereza sasa ameshtushwa na ameagiza kupatiwa maendeleo ya kila siku kuhusiana na kura hiyo.

Serikali 'Kuu' ya Waziri David Cameron sasa inatarajiwa kufanya jitihada za dakika za majeruhi kuokoa 'Muungano' huo wa zaidi ya miaka 300 usivunjike, kwa kutoa madaraka zaidi kwa serikali ya Uskochi.

Kampeni ya 'Better Together' inayopigania kuendelea kwa 'Muungano' huo imekuwa ikiongoza katika kura zote za maoni. Kampeni ya 'Yes' inayounga mkono 'uhuru' ilikuwa nyuma kwa asilimia 22 takriban mwezi mmoja tu uliopita.

Blogu hii itaendelea kuwaletea maendeleo zaidi kuhusu kura hiyo muhimu kwa hatima ya taifa la Uskochi na 'Muungano wa Uingereza.'

26 Aug 2014

debate pair
The poll followed an ill-tempered referendum debate in which Salmond forced Darling onto the back foot.
Alistair Darling defeated by a 71% to 29% margin, according to Guardian/ICM poll of Scots who watched the debate





Alex Salmond emerged as the clear winner of the second Scottish independence debate, besting Alistair Darling by a 71% to 29% margin, according to an instant Guardian/ICM poll of Scots who had watched the debate.
Salmond will be delighted to decisively overturn the verdict in the first round, in which a similar ICM poll found Alistair Darling had won by 56% to 44%.
The poll followed an ill-tempered referendum debate in which Salmond forced Darling onto the back foot on the currency, the NHS and Labour's decision to partner with the Conservatives in the Better Together campaign against independence.
The headline figures exclude viewers who say they don't know who won the debate – with these included the figures are 65% for Salmond, 26% for Darling, and 9% who were not sure.
As in the first debate, Alex Salmond was deemed to have the "more appealing personality", this time enjoying an 54% to 32% advantage on this count. But the difference this time came on the question of who had the best arguments. While Darling had the advantage last time around, this time Salmond leapt ahead to take a commanding 56% to 36% lead.

Morale in the yes camp will be boosted by the extraordinarily emphatic win that Salmond notched up among those who had gone into the evening planning to vote for independence – 98% of those expressing a view gave it to the first minister, and only 2% to Darling. In contrast, things were much more balanced among no voters – 59% gave Darling the edge, but a substantial 41% felt Salmond had the better night.
ICM weighted the sample to representative of the Scotland population by age, gender, region and previous voting behaviour (reported 2011 vote for the Holyrood election). But it is important to bear in mind that this is a survey of voters who actually watched the debate, as opposed to the electorate as a whole. Going in to the debate, this sample was more pro-independence than most polls of voters as a whole have suggested – splitting 44% yes to 46% no with 10% not sure. Over the course of the debate, there was little change in this balance. The don't knows dropped back two percentage points to eight, while both yes and no edged up one each to 45% and 47% respectively as a fraction of viewers made up their mind.
ICM pre-recruited a sample of 1,155 people who said they would be watching the debate live and who agreed to complete the survey immediately afterwards, which they were duly sent. All participants were recruited from ICM's own online panel plus those of two of the biggest suppliers of Scottish panel in the market research industry. The post-debate survey data is based on 505 completed interviews. ICM is a member of the British Polling Council and abides by its rules.
SOURCE: The Guardian

1 Jun 2012


Ya Zanzibar si mageni, hata Uskochi yapo
Evarist Chahali
Toleo la 241
30 May 2012


WIKI iliyopita, Waziri wa Kwanza (First Minister, cheo ambacho ni kama Waziri Mkuu) wa Uskochi, Alex Salmond, alizindua kampeni za chama chake cha Scottish Nationalist Party (SNP) kuhamasisha kura ya ‘Hapana’ katika referendum (kura ya maoni ) ya uhuru wa nchi hii inayotarajiwa kufanyika huko mbeleni.
Hoja ya Uskochi kujitenga na Uingereza (kwa maana ya kile kinachoitwa The United Kingdom of Great Britain-England, Uskochi na Wales- and Northern Ireland) imekuwa ikivuma kwa muda mrefu na imepata nguvu zaidi baada ya Salmond na SNP yake kuingia madarakani mwaka 2007.
Kimsingi, sera kuu ya mwanasiasa huyo na chama chake ilikuwa kuhakikisha kuwa hatimaye Uskochi inajitenga kutoka Uingereza.
Walipoingia madarakani tu, SNP walieleza bayana kuwa wana mpango wa kufanyareferendum kusikia maoni ya Waskochi kuhusu wazo hilo la kujitenga.
Hata hivyo, kikwazo ambacho wamekuwa wakikumbana nacho tangu mwanzo ni ukweli kwamba pamoja na tofauti za hapa na pale, ni vigumu kuchora mstari unaoweza kuwatenganisha Waskochi na Waingereza wengine.
Mwingiliano katika takriban kila nyanja ya maisha unawafanya watu hawa kuwa wamoja zaidi kuliko tofauti.
Na wakati naandaa makala hii, Salmond amepata ‘habari mbaya’ kutoka kwa mwendesha kura za maoni (pollster) maarufu hapa Uingereza, Peter Kellner, Rais wa taasisi ya kura za maoni ya YouGov.
Kwa mujibu wa Kellner, kura ya maoni iliyoendeshwa na YouGov Ijumaa iliyopita inaonyesha kuwa wakati ni asilimia 33 tu ya Waskochi wanataka ‘uhuru’ (kujitenga), asilimia 57 wanataka Uskochi iendelee kubaki sehemu ya Uingereza.
Mwendesha kura za maoni huyo amemtahadharisha Salmond kuwa ‘ana mlima mrefu wa kupanda’ kubadili upeo wa wengi wa Waskochi kuhusu nchi yao kujitenga na Uingereza.
Kadhalika, alieleza kuwa kuna ‘vitisho’ kadhaa vinavyoweza kuchangia Waskochi wengi kupinga wazo la kujitenga, na akatoa mfano wa hoja kama wawekezaji kujiondoa Uskochi (kwa kutokuwa na uhakika kama Uskochi itamudu ‘kusimama yenyewe’),  kupoteza ruzuku inayotolewa na Serikali Kuu ya Uingereza (ambayo ni kubwa zaidi ya kodi inayolipwa na Uskochi), matumizi ya sarafu ya pauni ya Kiingereza (British Pound) ambapo kama Uskochi itaamua kutumia sarafu hiyo baada ya kujitenga, Uingereza inaweza kuanzisha hatua za ukalifu (austerity measures) zitakazoathiri uchumi wa Uskochi.
Kadhalika, Salmond ametahadharishwa kwamba hofu nyingine zinazoweza kuwatisha Waskochi kuunga mkono wazo la kujitenga ni pamoja na gharama kubwa za kuendesha nchi kamili (hasa katika kipindi hiki ambapo uchumi wa dunia unayumba) kama vile kumudu kuwa na jeshi kamili, ofisi za ubalozi nchi za nje na gharama za uendeshaji wa taasisi za utumishi wa umma (civil service).
Kimsingi,  katika zoezi lolote lile la kupiga kura, hali ya kutokuwa na uhakika au hofu ya “huko mbele hali itakuwaje” inatosha kuwafanya wapiga kura wengi kuamua kubaki na chama kilichopo au muundo uliopo (iwapo ni referendum ya jambo fulani).
Mbinu hii inatumiwa sana na vyama tawala (ikiwa ni pamoja na CCM) kwenye chaguzi ambapo ujumbe huwa mithili ya ‘zimwi likujualo halikuli likakwisha’ (kwa maana ya chama unachokifahamu ni bora zaidi ya kile kinachoahidi tu pasipo kuwa na mifano hai ya uongozi wa nchi).
Hata hivyo, Salmond na SNP yake wanaendelea na jitihada zao huku wakijipa imani kuwa utajiri mkubwa uliopo Uskochi (kuna mafuta huko Bahari ya Kaskazini) utawezesha kumudu gharama za kuendesha nchi endapo Waskochi wataafiki wazo la kujitenga na Uingereza.
Wakati hayo yakijiri hapa Uskochi, mwishoni mwa wiki huko nyumbani kumekumbwa na habari za kusikitisha ambapo maandamano ya kupinga Muungano huko Zanzibar yaligeuka kuwa machafuko makubwa.
Kama nilivyoeleza katika ujumbe wangu wa Makala za Sauti (Audio Messages, unaoweza kusikia hapa http://goo.gl/r6ngT ), machafuko hayo huko Zanzibar na suala zima la Muungano vinapaswa kuangaliwa kwa mtizamo mpana zaidi.
Binafsi, ninaona kuwa asili ya tatizo la Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni waasisi wake, yaani Marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na Abeid Karume. Hapa naomba nieleweke vizuri.
Wazo la Muungano lilikuwa zuri kwa kuzingatia sababu mbalimbali, kubwa zaidi ikiwa ni ukaribu wa asili za watu wa Bara na wa Visiwani.
Lakini tatizo ambalo pengine lilichangiwa zaidi na mazingira ya kisiasa wakati huo, Nyerere na Karume walidhani kuwa ridhaa yao ilikuwa inawakilisha ridhaa ya Watanganyika na Wazanzibari wote.
Kuna ‘busara’ moja ya Kiingereza inayosema kuwa “jambo zuri si lazima liwe na manufaa. Kwa mfano, wakati kumpa chakula kingi mtu mwenye njaa ni jambo zuri lakini matokeo yake yanaweza kupelekea hata kifo kwenye mtu huyo mwenye njaa kali aliyeishia kupewa chakula kingi.”
Ndiyo, kula chakula kingi ukiwa na njaa kali ni hatari, na ndiyo maana watu wanapofunga au wakiwa hawajala muda mrefu huanza mlo kwa kinywaji cha moto (uji au chai).
Sasa, wazo la Muungano lilikuwa zuri lakini kutosaka ridhaa ya wengi ndiko kumetufikisha hapa tulipo sasa. Kwa muda mrefu kumekuwa na manung’uniko kuhusu Muungano, hususan miongoni mwa Wazanzibari.
Hoja kuu imekuwa ni kwamba wanapunjwa, wanaonewa na wengine wanakwenda mbali zaidi na kudai lengo la Muungano lilikuwa ‘kuimeza Zanzibar.’
Kwa bahati mbaya, siasa za Zanzibar zina tofauti kwa kiasi fulani na za Bara. Kwa Visiwani, dini ina nafasi ya kipekee katika siasa. Kwa hiyo, mara nyingi masuala ya kisiasa yanaweza pia kubeba hisia za kidini, jambo ambalo pasipo uangalifu linaweza kuzua balaa kubwa.
Ninapenda kusisitiza kuwa pamoja na hatari zinazoweza kujitokeza kwa kuchanganya dini na siasa, uzoefu na historia vimeonyesha kuwa laiti busara na maslahi ya jamii yakiwekwa mbele ya hisia binafsi, dini inaweza isiwe na madhara katika siasa.
Huko Marekani, kwa mfano, dini bado ina nafasi ya kipekee. Pengine mfano mzuri zaidi ya namna dini inavyoweza kutoharibu siasa ni Ujerumani ambapo chama cha Kansela Angela Merkel (Christian Democratic Union-CDU) ni cha Kikristo. CDU ndio chama kikubwa zaidi cha siasa katika taifa hilo tajiri.
Kadhalika, chama kinachotawala nchini Uturuki, Justice and Development Party-AKP, ni chama cha Kiislamu. Hata hivyo, chama hicho kimefanikiwa kuifanya Uturuki iendelee kuwa taifa lisiloelemea kwenye siasa zinazoongozwa na dini.
Hata hapa Uingereza, Malkia ambaye ndiye mkuu wa nchi (kiheshima zaidi kuliko kiutendaji) pia ni Mkuu (kiheshima) wa Kanisa la Anglikana, na japo Ukristo ni kama ‘dini ya taifa’ lakini nchi hii inaendeshwa kwa sheria za ‘kidunia’ na si za kidini.
Hata hivyo, tatizo la dini ni ukweli kwamba licha ya kugusa hisia binafsi za muumini, mambo ya kidini hayahitaji uthibitisho wa kisayansi (au kidunia).
Tofauti na dini, siasa ni suala la itikadi zaidi kuliko imani (japo imani kwenye itikadi inaweza kuwafanya wafuasi wa chama kukiona kina umuhimu kama dini). Kadhalika, masuala ya dini yanahusisha ‘maisha ya baadaye baada ya haya ya duniani’ ilhali siasa imejikita zaidi kwenye masuala ya sasa au ya hapahapa duniani.
Balaa linakuja pale muumini wa dini anapoanza kuamini kuwa anapopinga Muungano,  kwa mfano, anafanya kazi ya kiroho na inampendeza Muumba. Ni vigumu sana kumdhibiti mtu wa aina hii kwani hata harakati zake zikihatarisha maisha yake, au akaishia kufa, anaamini kuwa atalipwa na Muumba wake.
Kimsingi machafuko yaliyotokea Zanzibar yamechangiwa zaidi na wanasiasa wetu ambao kwa kiasi kikubwa wamekuwa wanachelea kile kinachofahamika kama ‘kuogopa laana ya waasisi wa Muungano pindi Muungano huo ukiwavunjikia mikononi mwao.’
Badala ya kuzishughulikia kero za Muungano na kuzipatia ufumbuzi wa kudumu, watawala wetu wamekuwa wakijikita zaidi kwenye kujaribu kutuaminisha kuwa wanalishughulikia suala hilo kwa dhati ilhali wanaligusa juu juu tu.
Tumekuwa na Tume ya Kero za Muungano miaka nenda miaka rudi lakini ufanisi wake umekuwa wa kufikirika zaidi kuliko uhalisia.
Tuache unafiki, ‘kelele’ za kudai mabadiliko ya muundo wa Muungano (na hata hizo za kutaka uvunjiliwe mbali) haziwezi kwisha kwa kuzipuuza au kuwa na ‘tume ya milele’ ya kushughulikia kero hizo pasipo kuja na ufumbuzi.
Lakini kingine ni kuwanyamazia mafashisti wanaohubiri chuki dhidi ya wenzao kwa kisingizio cha kero za Muungano. Huko Zanzibar, baadhi ya wanasiasa wamediriki kudai ni Wabara wanaosababisha Wazanzibari kukosa ajira. Lakini huo ni mlolongo tu wa shutuma za aina hiyo, kwani huko nyuma Wabara walishawahi kutuhumiwa kuwa ndio waliopelekea ukimwi Visiwani humo.
Kwa vile hadi wakati huu ninaandaa makala hii bado hali huko Visiwani haijatulia, naomba nihitimishe kwa kutoa pendekezo la umuhimu wa kuwa na kura ya maoni itakayofidia kosa lililofanywa huko nyuma la kusaka ridhaa ya wananchi kuhusu Muungano.
Kama kura hiyo ya maoni itaamua tuwe na serikali tatu, basi hilo liheshimiwe. Kama itaamuliwa Muungano uvunjwe, basi na iwe hivyo (by the way, kuvunjika kwa Muungano hakutomaanisha kufa kwa Tanzania Bara au Zanzibar, kama ambavyo kuvunjika kwa ndoa hakumaanishi kifo kwa mume au mke aliyetalikiana na mwenzie).
Mwisho kabisa, wakati nikiwasihi viongozi wetu kuharakisha kura ya maoni ninayoamini itasaidia kuleta ufumbuzi wa kudumu wa matatizo ya Muungano wetu, ni muhimu kabisa kwa Serikali zote mbili (ya Muungano na ya Zanzibar) kuchukua hatua kali dhidi ya magaidi waliogeuza ‘madai halali kuhusu Muungano’ kuwa sababu ya kuwashambulia Wabara na kuchoma moto makanisa na mali zake.
Wanachofanya wahalifu hawa hakilengi kusaka suluhu ya Muungano bali wanapenda mbegu za uhasama wa kidini kati ya Wakristo na Waislamu.
Mungu Ibariki Tanzania


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.