25 Aug 2010



Takukuru yakamata mgombea aliyejitoa
Adaiwa kuwa alishawishiwa kwa fedha
Awekwa chini ya ulinzi Makao Makuu Dar

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Makao Makuu jijini Dar es Salaam, imemkamata na kumhoji aliyekuwa mgombea ubunge kwa tiketi ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) katika Jimbo la Musoma Vijijini, Michael Makenji, kwa tuhuma za kupokea rushwa.

Makenji anadaiwa kupokea Euro 1,000 (Sh. 1,850,000) kisha kujitoa katika kinyang’anyiro hicho.
Habari zilizolifikia gazeti hili zinaeleza kuwa Makenji alihojiwa na maofisa wa Takukuru juzi jioni kuhusiana na tuhuma hizo na kwamba hadi jana alikuwa akiendelea kushikiliwa kwa ajili ya mahojiano zaidi.

Makenji ni miongoni mwa wanachama wa Chadema waliochukua fomu za kuomba kuteuliwa kugombea katika jimbo hilo, lakini hakurejesha fomu kwa msimamizi wa uchaguzi hivyo jimbo hilo kubaki na mgombea pekee wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nimrod Mkono (pichani mwenye kibandiko).

Habari zinaeleza kuwa Makenji baada ya kutorejesha fomu kwa msimamizi wa uchaguzi Jimbo la Musoma Vijijini, alikwenda katika ofisi za Makao Makuu ya Chadema jijini Dar es Salaam, lakini baadaye baadhi ya wanaChadema walimtilia shaka kutokana na mawasiliano kati yake na baadhi ya watu.

Chanzo chetu cha uhakika kimebainisha kuwa, baada ya wanaChadema kumtilia shaka, walimuweka chini ya ulinzi na kukuta taarifa mbalimbali alizokuwa anatumiana na watu hao kupitia ujumbe mfupi wa simu.Taarifa za ndani ya Chadema zinasema kwamba baada ya mgombea huyo kuhojiwa na kupekua kwenye simu yake ya mkononi, alipatikana na ujumbe kadhaa zilizoashiria kwamba kulikuwa na mkono wa mtu katika kujitoa kwenye kinyang’anyiro cha ubunge.

Miongoni mwa jumbe hizo (sms) ambazo ziko sehemu ya zilizotumwa zilisema:
“Mzee ameshanikatia tiketi ya kwenda Dar sasa muhimize amalizie kiasi kilichobaki maana hali yangu ya kiuchumi si nzuri.”
Nyingine ilisomeka: “Tumeshamaliza kama tulivyokubaliana.” Na mwingine ukisema: “Niko Makao Makuu ya Chama niko chini ya ulinzi.” Ujumbe huo ulionekana kujibiwa hivi: “Nani kakwambia uende huko watakuua. Siwezi kuja huko kukutetea.” Simu iliyotuma ujumbe huo unadaiwa ni ya kiongozi mmoja mwandamizi wa chama hicho.

Chadema baada ya kuona hali imekuwa hivyo, waliamua kuwasiliana na Takukuru na baada ya muda mfupi, maofisa wa taasisi hiyo walifika na kumchukua Makenji.Hata hivyo, Takukuru haikuwa tayari kuthibitisha tukio hilo licha ya jitihada za NIPASHE kuwatafuta maofisa wake tangu juzi jioni.

Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hoseah, juzi jioni alisema alikuwa katika mkutano mjini Arusha na kuahidi kuwa angepiga simu baadaye kutoa ufafanuzi. Hata hivyo, hadi tunakwenda mitamboni hakufanya hivyo.

Ofisa Uhusiano wa Takukuru, Doreen Kapwaya, jana alisema kuwa maofisa wa Makao Makuu wangeweza kulizungumzia, lakini mwandishi wetu alipokwenda katika ofisi hizo, aliambiwa kuwa ofisa anayeshughulikia kesi hiyo alikuwa katika kikao.

Hata hivyo, ofisa huyo aliyetambulika kwa jina moja la Kassim, alipoulizwa baadaye jioni, alisema: “Sina comment (sina la kusema) katika hilo, labda kama ungefuata zile taratibu zetu za kila siku kwa kupitia kwa ofisa Uhusiano wetu hadi kwa Mkurugenzi Mkuu.”

Dk. Hoseah alizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu majira ya saa 18:20 jana jioni, alisema: “Sina taarifa, kwa sasa nipo nje ya Dar es Salaam, nani amekuambia hayo.”

Uongozi wa Chadema ulipoulizwa kuhusiana na taarifa hizo, ulithibitisha kuwepo kwa tukio hilo na kueleza kwamba mtuhumiwa (Makenja) alikiri kupewa kiasi hicho cha pesa.

“Kimsingi ni kwamba Idara yetu ya Ulinzi na Usalama ilimhoji mgombea wetu na akakiri kupewa fedha hizo, tena kwa maandishi ndipo tukawasiliana na Takukuru kwa hatua zaidi…lakini tunawasiliana na mamlaka mbalimbali ili kuona hatua stahili za kumchukulia kwa sababu amekiuka kanuni na sheria za uchaguzi,” alisema Kaimu Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika.

Kufuatia hali hiyo, Mnyika alisema chama hicho kimelazimika kuwaandikia barua wagombea wake ambao hawakurudisha fomu ili kujua tatizo lililokwamisha kufanya hivyo.Alisema chama kimeamua kuchukua hatua hiyo ili kubaini kama kinafanyiwa hujuma na kwamba watakaobainika kutorudisha fomu makusudi, kitawachukulia hatua kwa mujibu wa sheria za uchaguzi.

CHANZO: Nipashe



Well,not really.But a quick look at the above picture showing members of the notorious Tanzania Police Field Force Unit (FFU)  in their anti-riot gear could mislead you into thinking they were bracing themselves for a chemical or biological attack of some sort!

Photo courtesy of Mzee wa Sumo

24 Aug 2010

Tangu tukio la mashambulizi ya kigaidi ya September 11 mwaka 2001,Marekani inaelekea kupata sababu nyingine ya kuhalalisha ubabe wake.Miongoni mwa wahanga wakubwa wa aftermath ya mashambulizi hayo ni Waislamu,ndani na nje ya nchi hiyo.

Hivi karibuni kumejitokeza mzozo kuhusu ujenzi wa kituo cha utamaduni cha Kiislamu karibu na eneo yalipokuwa majengo maarufu ya Twin Towers ambayo yalishambuliwa na magaidi kwa kubamizwa na ndege.Licha ya ukweli kuwa miongoni mwa waliofariki au kujeruhiwa ni Waislam,kwa Wamarekani wengi mashambulizi hayo yalikuwa kama tangazo la vita vipya kati yao na Waislam na Uislam.


Urais wa Barack Obama,ambaye mmoja wa wazazi wake alikuwa Muislam,ni kama umeongeza mafuta kwenye moto wa chuki dhidi ya Waislam.Katika kutambua uhuru na haki ya kila Mmarekani,Rais Obama aliweka msimamo wake hadharani kuwa anaunga mkono ujenzi wa kituo hicho cha kidini,kauli iliyopelekea upinzani mkubwa dhidi yake huku wengine wakimnyooeshea kidole kudai naye ni Muislam,kana kwamba kuwa muumini wa dini hiyo ni dhambi. 

Japo taifa hilo kubwa na lenye nguvu za kutosha limeendelea kudumisha misingi ya imani ya kidini (hususan Ukristo) matendo ya Wamarekani walio wengi hayana tofauti na waumini wa shetani.Sote tunatambua kuwa dini mbalimbali zinahamasisha amani,upendo na kusamehe waliotukosea.Sasa,hata kama Wamarekani wanaamini kuwa waliofanya mashambulizi hayo walitenda hivyo kutokana na imani yao ya Uislamu haimaanishi kuwa kila muumini wa dini hiyo aendelee kunyanyaswa kwa makosa ya wengine.Kimsingi,wengi wa magaidi wana asili au dini flani lakini hatuendelei kuwanyanyasa watu wengine ambao hawakushiriki katika vitendo vya ugaidi lakini wana asili au dini moja na magaidi husika.Wanaofanya mashambulizi ya kigaidi huko Ireland ya Kaskazini ni Wakatoliki na Waanglikana,lakini hatuhitimishi kuwa kila Mkatoliki au Muanglikana na gaidi.

Hata Marekani kama nchi imeshafanya unyama mkubwa sehemu mbalimbali duniani hususan katika zama za Vita Baridi kati yake na Urusi.Nani asiyejua mchango wa Wamarekani katika kifo cha Patrice Lumumba,au sapoti yao kwa Savimbi?Na nani asiyefahamu namna Wamarekani Weupe walivyojenga taifa hilo kwa biashara ya kinyama ya utumwa dhidi ya watu Weusi?Lakini hatumhukumu kila Mmarekani kuwa ni gaidi au mtwana mwenye kumiliki watumwa.

Yanayotokea sasa dhidi ya Waislamu ni mwendelezo tu wa hisia za ubaguzi zilivyoshamiri miongoni mwa Wamarekani walio wengi.Hadi leo,miaka kadhaa baada ya kuharamisha ubaguzi wa rangi,Wamarekani wasio Weupe wameendelea kubaguliwa kwa namna moja au nyingine.Again,urais wa Mmarekani Mweusi Obama umewasha upya moto wa ubaguzi wa rangi.

Japo siungi mkono ugaidi,ni dhahiri kuwa siasa za kinafiki za nchi hiyo zimechangia sana kuzalisha magaidi.Osama bin Laden,kiongozi wa mshambulizi ya September 11ni zao la mafunzo na ufadhili wa Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA).Yayumkinika kuhitimisha kuwa tatizo la baadhi ya sera za mambo ya nje za Marekani ni ufupi wa upeo (short-sightedness).Katika zama za Vita Baridi,nchi hiyo iliona kuwa ni jambo mwafaka kufadhili mujahidina waliokuwa wanapambana na Urusi.Guess what?Mujahidina hao ndio Osama na Taliban wa leo!

Ungedhani kuwa nchi hiyo ingejifunza kutokana na foreign policy blunders zake kama hiyo ya kusapoti Mujahidina lakini wapi!Makosa kama hayo yameendelea kurudiwa huko Irak na Afghanistan pasipo kuangalia madhara ya muda mrefu.Licha ya sapoti kwa vikundi vinavyotarajiwa kuunga mkono harakati za Wamarekani,nchi hiyo imeendelea kutoa sapoti kwa baadhi ya tawala za kidikteta alimradi uimara wa tawala hizo ni kwa maslahi ya Marekani.Miongoni mwa marafiki wakubwa wa nchi hiyo ni pamoja na utawala wa kifalme wa Saudia na utawala wa kidikteta nchini Misri.Matokeo ya muda mrefu ya uswahiba huu ni kuibuka kwa upinzani wa ndani dhidi ya tawala hizo,ambao in long run unaweza kabisa kuwa na madhara kwa Marekani yenyewe.

Kadhalika,tawala hizo dhalimu zimechangia baadhi ya wananchi wao kukimbilia kwa vikundi vyenye misimamo mikali ya kidini ambayo inaonekana kwa wananchi hao kama yenye kuleta tumaini katika kuwapatia ufumbuzi wa matatizo yao.Kwenye sosholojia ya dini tunafundisha kuwa miongoni mwa sababu za kuwepo dini ni kimbilio la wenye shida.Tawala dhalimu zinaweza kuwa chanzo cha kuibuka na kushamiri kwa vikundi vyenye misimamo mikali ya kidini kwa vile wananchi wanaviona vikundi hivyo kama sehemu ya ufumbuzi wa matatizo yao.

Siasa za jino kwa jino na jicho kwa jicho,sambamba na kuendeleza ubaguzi kwa watu wasio na hatia ni hatari zaidi kwa usalama wa Marekani kuliko ujenzi wa kituo cha utamaduni kinachopigiwa kelele sasa.Actually,uwepo wa taasisi kama kituo hicho cha utamaduni unaweza kusaidia sana katika kujenga maelewano na mshikamo miongoni mwa Wamarekani pasipo kujali tofauti zao za kiimani.

23 Aug 2010

Wakati wa kuelekea kampeni za uchaguzi mkuu wa hapa Uingereza kulijitokeza tetesi za wasiwasi kuhusu afya ya aliyekuwa Waziri Mkuu Gordon Brown.Katika kilichotafsiriwa kama kukata mzizi wa fitina,mtangazaji maarufu wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC),Andrew Marr,alimuuliza Brown katika mahojiano naye kuhusu tetesi hizo.Katika tetesi hizo ilidaiwa kuwa Brown alikuwa akitumia dawa za kutuliza mara kwa mara.

"Jambo ambalo kila mtu amekuwa akiongelea katika kijiji cha Westminster...Watu wengi katika nchi hii wamekuwa wakitumia dawa walizoelekezwa kununua na daktari (prescription drugs)...Je wewe ni mmoja wao?",aliuliza Marr."Hapana.Nadhani uulizaji swali wa aina hii umekuwa ukiingia sana kwenye ulingo wa siasa za Uingereza",alijibu Brown.Jitihada za mwanahabari huyo kutaka kudadisi zaidi zilizimwa na Brown aliyesema ameshajibu swali hilo.


Nimekumbuka tukio hilo kufuatia kuanguka kwa mara nyingine kwa Rais Jakaya Kikwete na namna vyombo vingi vya habari vilivyokwepa kuripoti tukio hilo kwa uwazi.Hata video iliyomwonyesha Kikwete akianguka iliondolewa mtandaoni kwa haraka,kwa sababu wanazojua waliyoiondoa.Na hata video yenyewe ya tukio hilo ilionyesha "kiduchu" tu kuanguka kwa JK kisha ikaelekezwa kwenye umati wa watu hapo Jangwani.Inaelezwa pia kuwa baadhi ya vituo vya runinga huko nyumbani havikuonyesha tukio hilo katika taarifa zao za habari.

Kichekesho ni kwamba kabla hajakumbwa na dhahma ya kuanguka,JK alijigamba kuwa serikali yake imeboresha uhuru wa habari.Sasa uhuru wa habari ambao tukio la kusikitisha na kuhudhunisha linalomkumba Rais wetu linabanwa ni uhuru kweli au hadithi tu?Na hapa simpingi JK kuwa amejitahidi kudumisha uhuru wa habari bali tatizo langu lipo kwa wanahabari wenyewe.

Je,kulikuwa na maagizo kwamba,kwa mfano,clip ya kuanguka kwa JK iodolewe mtandaoni?Kama jibu ni ndiyo,basi uhuru wa habari anaozungumzia JK una walakini.Lakini kama jibu ni hapana basi wanahabari walioamua kuminya habari hiyo wana maswali ya kuwajibu wasomaji wao na Watanzania kwa ujumla.

Natambua kuwa pamoja na majigambo ya JK uhuru wa habari unaodumishwa zaidi ni ule wa "habari za kawaida" na sio zinazogusa masuala ya watawala.Baadhi yetu ni wahanga wa matumizi hayohayo ya uhuru wa habari na uhuru wa kujieleza.Ukizungumzia mafisadi walio ndani ya CCM,baadhi ya "wenye nchi" wanakurupuka kudai ni utovu wa nidhamu dhidi ya serikali.Yaani kukemea maovu inakuwa nongwa!?

Tukio la kuanguka kwa JK lilikuwa haki ya kila Mtanzania kufahamishwa na wanahabari.Ikumbukwe kuwa ni Watanzania haohao ndio waliompigia kura kiongozi huyo kuwa Rais wao,na mkutano wake wa Jumamosi ulikuwa na madhumuni ya kuwaomba ridhaa ya kuwaongoza tena.Jakaya Kikwete alikuwa hapo kama mgombea wa CCM,na japo hatuwezi kutenganisha urais wake na ugombea wake huko CCM,ukweli unabaki kuwa katika harakati hizi za kampeni anapaswa kuchukuliwa kama wagombea wengine wa vyama vilivyosimamisha wagombea wao.

Japo mkono mrefu wa dola uko makini zaidi katika udhibiti wa habari "zisizopendeza",yayumkinika kusema kwamba baadhi ya wanahabari na vyombo vya habari hawawezi kukwepa lawama.Nachoshindwa kuelewa kwanini  mara nyingi "habari zisizopendeza machoni mwa watawala" zinaminywa ni kama hali hiyo inasababishwa na uoga tu wa wanahabari au/na vyombo vya habari au ni lile tatizo sugu la kujikomba kwa watawala?

Kama sababu ni uoga,basi hayo ni mapungufu ya wazi kwa mwanahabari au chombo cha habari husika.Hata hivyo,inawezekana uoga huo kuwa ni matokeo ya mfumo wa siasa za chama kimoja ambapo ilikuwa mithili ya kosa la jinai "kumsema vibaya" kiongozi (yaani kusema au kuandika kitu kisichompendeza kiongozi).Tuliaminishwa kuwa viongozi wetu ni kama miungu-watu,hawawezi kukosea,kila wanalofanya ni jema na siku zote wako sahihi.Uoga huu unapaswa kuepukwa kwa vile tupo katika  mfumo mpya wa siasa za uwingi zisizo na nafasi ya "zidumu fikra sahihi za A au B".

Kujikomba ni tatizo sugu si kwa baadhi ya Watanzania tu bali hata baadhi ya Waafrika kwa ujumla.Kwa mbali,kujikomba ni matokeo ya mfumo wa ujima na hatimaye ujamaa ambapo mhusika hujibidiisha "kufanya jambo zuri" hata kama hajaombwa.Kwa bahati mbaya,"jambo hilo zuri" linaweza kuwa lisilo na manufaa kwa jamii.Kwahiyo,mwanahabari aliyebania tukio la kuanguka kwa JK anaweza kuwa alifanya hivyo akiamini kuwa "ni vibaya kumwonyesha Rais akianguka hadharani".Lakini imani hiyo potofu ilimaanisha baadhi ya Watanzania kukoseshwa haki ya kuona kilichomsibu mgombea wa CCM ambaye pia ni Rais wao.

Simnyooshei mtu kidole bali hii ni changamoto tu kwa wanahabari na vyombo vya habari.


Riyadh,Saudia,April 16

Wafanyabiashara wa Saudi Arabia wameiomba Tanzania kama wanaweza kukodi hekta nusu milioni (500,000) za ardhi inayofaa kwa kilimo hususan cha mpunga na ngano kama sehemu ya mpango wa kujitosheleza kwa chakula kwa falme hiyo ya jangwani.

Maofisa waandamizi wa chemba ya biashara ya jiji la Riyadh walitoa ombi hilo wakati wa ziara ya Rais Jakaya Kikwete katika falme hiyo.

"Tanzania ipo tayari kufanya biashara nanyi.Kuna heka milioni 100 (hekta milioni 40.5)za ardhi nzuri yenye rutuba",Kikwete aliwaambia wafanyabiashara hao.

Samir Ali Kabbani,mkuu wa kamati ya kilimo ya chemba hiyo alisema kwamba wamepata majibu mazuri sana."Kikwete ametuambia kwamba Tanzania inaweza kutukodisha ploti ambazo kila moja ina ukubwa wa hadi hekta 10,000 kwa kipindi cha miaka 99",Kabbani alilieleza Shirika la Habari la Reuters baada ya mkutano huo na Kikwete.

Maofisa na wafanyabiashara wa Kisaudi walitrajiwa kuitembelea Tanzania wiki chache baada ya mkutano huo.

"Wanaweza kukodi ardhi kutoka serikalini",January Makamba,msaidizi wa Rais Kikwete,aliieleza Reuters."Lakini inabidi tuhakikishe kuwa hatuishii kwenye hali kama ile ya Nigeria:hifadhi kubwa ya mafuta lakini foleni kubwa kwenye vituo vya kuuzia mafuta",alisema Makamba.

Maafisa wa Saudia wanaiona Tanzania kama sehemu mwafaka kutokana na mazingira ya kijiografia,kisiasa na wingi wa maji na ardhi ya kilimo.Makampuni kadhaa ya nchi hiyo tayari yameanza kuwekeza katika miradi ya kilimo huko Indonesia na Ethiopia.

Agosti mwaka jana Indonesia ilisema kuwa mjumuiko wa makampuni ya Bin Ladin ya Saudi Arabia unatarajia kuwekeza dola bilioni 4.3 katika hekta 500,000 za kilimo cha mpunga.Mahitaji ya ngano kwa Saudia kwa mwaka yanakadiriwa kufikia tani milioni 2.5,na mwaka juzi nchi hiyo iliagiza kutoka nje karibu tani milioni 1 za mchele,kwa mujibu wa Idara ya Kilimo ya Marekani.

CHANZO: Reuters


22 Aug 2010

What A good NewS???
Well,your top-above-the-rest blog,ANGALIA BONGO,has officially  moved to a new world.
Thanxx
Admin(Angaliabongo)

Blogu hii ya KULIKONI UGHAIBUNI inafungua ukurasa mpya na kuweka historia ya kipekee katika fani ya habari nchini Tanzania kwa kutangaza hadharani kuwa inam-endorse mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chadema,Dokta Wilbroad Slaa.

Kuna sababu lukuki za kufanya hivyo lakini hapa nitaziorodhesha chache.Kwanza,blogu hii inataka kuachana na unafiki unaojidhihirisha katika baadhi ya vyombo vya habari vyetu ambapo wahusika wanadai hawafungamani na upande wowote lakini matendo yao yanawasuta kwa kupendelea chama tawala huku wakivibinya kwa nguvu baadhi ya vyama vya upinzani.Hapa simsimangi mtu bali nadhani ni vema kuweka msimamo wazi ili kama chombo cha habari ni wakala wa CCM na JK basi ni vema wasomaji wakafahamishwa bayana.

Pili,blogu hii inaamini kuwa kila Mtanzania mwenye uchungu wa dhati kwa nchi yetu anapaswa kumsapoti Dkt Slaa.Katika utumishi wake kwa umma,mgombea huyo wa Chadema ametuthibitishia kuwa ni mtetezi halisi wa haki za wanyonge na ustawi wa taifa letu.Ni nani asiyefahamu namna Dkt Slaa alivyohatarisha maisha yake kwa “kuwavua nguo mafisadi hadharani” alipotangaza ile “list of shame”?Walitishia kumpeleka mahakamani lakini hakuna mmoja wao aliyediriki kufanya hivyo,na sanasana baadhi yao wakaishia kuburuzwa mahakamani na serikali katika “kujikosha”.Blogu hii inaamini kuwa Dokta Slaa ni mkombozi na suluhisho mwafaka la matatizo lukuki yanayotukabili.

Tatu,binafsi naamini kuwa mgombea wa CCM,Jakaya Mrisho Kikwete,ameshindwa kabisa kutimiza matarajio ya Watanzania licha ya ahadi lukuki alizozitoa wakati wa kampeni zake mwaka 2005 na anazoendelea kuzitoa hadi leo.Ungetegemea kuwa mwezi huu wa toba Kikwete angemwogopa Mola wake na kutubu kwa Watanzania kwamba kuna maeneo mengi tu ambapo yeye na chama chake wamewaangusha Watanzania.Lakini kama ilivyo jeuri ya wanasiasa wengi wa Kiafrika,JK ameendeleza wimbo wa “mafanikio ya Awamu ya Nne”.Yani hata kushamiri kwa ufisadi na “uchakachuaji” wa kura za maoni ndani ya CCM ni mafanikio!

Sababu ya nne inashabihiana na hiyo ya tatu.Naamini kuwa afya ya mgombea wa CCM,Jakaya Kikwete,inapaswa kuwekwa kwenye darubini na wapiga kura wanapofanya maamuzi ya kumchagua rais wa awamu ya tano.JK ameshaanguka hadharani mara tatu na kila mara tunapewa excuse moja baada ya nyingine.Mwaka 2005 tuliambiwa “swaumu na uchovu wa kampeni”.Alipoanguka Mwanza tuliambiwa uchovu wa safari (kana kwamba safari hizo ni zile za Wamachinga wanaotembea juani kwa mguu!).Na jana kaanguka tena jukwaani halafu tunaambiwa sababu ni swaumu.Kwani Makamba hajafunga?Au Rais Karume naye “kobe”?Kuna tatizo zaidi ya swaumu au uchovu lakini kwa vile viongozi wetu wamezowea sifa na sio kasoro basi kuweka hadharani kinachomsibu kiongozi huyo inaonekana ni sawa na uhaini.Blogu hii imaanimi kuwa ili Tanzania ijikwamue katika lindi la umasikini wa kutupwa,sambamba na kukabiliana na janga la ufisadi,tunahitaji kiongozi mwenye afya timilifu,kimwili na kiakili.Hatujui JK ameshaanguka matra ngapi asipokuwa hadharani lakini haihitaji hata cheti cha short course ya utabibu kumaizi kuwa JK ana matatizo ya kiafya yanayofichwa,aidha kutokana na uoga wa wanaopaswa kuujulisha umma kuhusu hilo au maagizo yake mwenyewe kuwa “yuko fiti”.All in all,uzito wa matatizo yanayoikabili Tanzania unahitaji mtu aliye fiti kweli,na sio kwa anavyodhani yeye au anavyotaka umma uamini hivyo ilhali ni kinyume na hali halisi.

Kama nilivyoandika mwanzoni,kuna sababu nyingi zilizopelekea blogu hii kuamua kum-endorse Dkt Slaa lakini chache zilizotajwa hapo juu zinawakilisha hizo nyingine.Nawakaribisha ndugu zangu wa Chadema kuitumia blogu hii kufikisha habari kwa Watanzania pasipo hofu ya kuwa habari hizo zitachujwa,kuminywa au “kuchakachuliwa”.

Natambua bayana kuwa baadhi ya wasomaji wa blogu hii sio wafuasi wa Dkt Slaa au Chadema lakini napenda kuwakikishia kuwa endorsement hii haimaanishi kashfa,matusi,dharau au mambo yasiyofaa dhidi ya wagombea wa vyama vingine.Kuweka wazi msimamo wangu haimaanishi chuki dhidi ya vyama hivyo na wagombea wake bali ni imani yangu kuhusu nani anayeweza kuipatia Tanzania “uhuru wa pili” (mapambano dhidi ya Watanzania wenzetu wanaotafuna raslimali zetu zaidi ya alivyofanya mkoloni).

Mwisho,nawahamasisha bloga wenzangu na vyombo vingine vya habari kwa ujumla kuweka bayana misimamo yao ili kuepuka lawama zinazoweza kujitokeza pale habari za vyama flani zinaponyimwa fursa katika vyombo hivyo.Endorsement ya mgombea au chama ni jambo la kawaida katika nchi za Magharibi lakini hii ni mara ya kwanza kwa chombo cha habari cha Kitanzania kufanya hivyo,na kwa hakika najivunia kuweka historia hiyo.

21 Aug 2010

20 Aug 2010

Pamoja na kumtetea mwanaye,JK alisema (namnukuu)"...hata kama aliyegombea hakuridhishwa na mazingira ya namna aliyeshinda alivyoshinda, ndiyo ameshapata,hivyo jambo la msingi ni kuacha makundi yaliyokuwepo wakati wa kura za maoni, bali wajielekeze katika kutafuta ushindi wa kishindo huku wakijiandaa kwa kugombea kipindi kingine..."SWALI.Je kama kutoridhishwa huko kunatokana na matumizi ya rushwa?Au kwa vile Awamu ya Nne ilikuwa na huruma kwa mafisadi basi wagombea waliofisadiwa nao waige mfano wa serikali hiyo?Soma habari kamili HAPA.

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.