Showing posts with label UCHAGUZI MKUU. Show all posts
Showing posts with label UCHAGUZI MKUU. Show all posts

23 May 2012




WEDNESDAY, MAY 23, 2012


Hukumu kesho itakuwa mahakama kuu kivukoni na sio mahakama ya kazi akiba

Nimepokea taarifa kwamba hukumu ya kesi ya uchaguzi dhidi ya ushindi wetu Jimbo la Ubungo kesho tarehe 24 Mei 2012 itatolewa katika Jengo la Mahakama Kuu (Kivukoni- Court No. 1) badala ya jengo ilipo mahakama ya kazi (akiba) ambapo kesi iliendeshwa. Kama tulivyotafuta kura pamoja, tukapanga mstari kupiga kura pamoja na tukakesha kuzilinda pamoja tujumuike pamoja kujua hatma ya kura zetu. Hukumu ya kesi inatarajiwa kuanza kusomwa saa nne asubuhi hata hivyo ni muhimu kuwahi mapema zaidi asubuhi kwa ajili ya itifaki za kuingia mahakamani. Maslahi ya Umma kwanza

26 Oct 2010

Add caption


WAINGEREZA WANA MSEMO "IF SOMEONE HAS SOMETHING BAD TO SAY ABOUT YOU,IT'S PROBABLY BECAUSE THEY HAVE DON'T HAVE NOTHING GOOD TO SAY ABOUT THEMSELVES",YAANI KWA KISWAHILI,UKIONA MTU ANA BAYA LA KUSEMA KUHUSU WEWE BASI PENGINE NI KWA VILE HANA JEMA LA KUSEMA KUHUSU YEYE MWENYEWE.

RAIS ALIYE MADARAKANI NI JAKAYA MRISHO KIKWETE.CHAMA KILICHO MADARAKANI NI CHAMA CHA MAPINDUZI.SASA CHA KUSHANGAZA,AJENDA KUBWA YA KIKWETE NA CCM IMEKUWA KUHUSU "KWANINI DAKTA SLAA HAFAI,KWANINI CHADEMA WAONGO,KWANINI AHADI ZA DKT SLAA/CHADEMA HAZITEKELEZEKI" NA UPUUZI MWINGINE KAMA HUO.HIVI RAIS ALIYEKUWA MADARAKANI MIAKA MITANO NA ANAYETOKA CHAMA AMBALO LIMETUTAWALA MIAKA NENDA MIAKA RUDI HAWANA LA KUTUELEZA KUHUSU WAO WENYEWE BALI KUMVALIA NJUGA DOKTA SLAA NA CHADEMA KANA KWAMBA AKINA LIPUMBA NA WAGOMBEA URAIS WENGINE WANAGOMBEA UBUNGE AU UDIWANI?

JIBU LIPO KWENYE HUO MSEMO WA WAINGEREZA.KIKWETE NA CCM HAWANA JIPYA AU ZURI LA KUWAELEZA WATANZANIA ZAIDI YA KUDURUFU AHADI ZA MWAKA 1995,2000 NA ZAIDI 2005.HAWANA JIPYA ZAIDI YA KUBAHATISHA MBINU YAO MAARUFU YA "TUPENI KURA TUMALIZIE TULIYOANZA AWAMU HII".YAANI TUWAPE TENA KURA WAMALIZIE KUMALIZA RASLIMALI ZA TAIFA? HELL NO!TUWAPE TENA MIAKA MITANO WAMALIZIE UBIA WAO NA MAFISADI KUSAFISHA KILA KILICHOPO.HAPANA,NO,NEVER!

WAMETUNYANYASA KIASI CHA KUTOSHA.
WAMETUDHARAU KIASI CHA KUTOSHA (NDIO MANA AHADI LEO HAWATAKI KUOMBA MSAMAHA KWA MAKOSA YA UFISADI)
WAMETUTESA KIASI CHA KUTOSHA.
UMEFIKA WAKATI WA KUWAAMBIA NOT ANY MORE. IMETOSHA.WAMETUIBIA VYA KUTOSHA LAKINI SASA TUKIWAREJESHA TENA MADARAKANI SIO TU WATATUFILISI BALI PIA TUTAONEKANA WAJINGA KWA KUWARUHUSU WATUFANYE WAJINGA.

CHAGUA DOKTA WILBROAD SLAA KWA TANZANIA MPYA YENYE NEEMA NA MAENDELEO
MSTAAFISHE KIKWETE KWA MANUFAA YA UMMA
WATIMUE MAFISADI TUREJESHE NCHI MIKONONI MWETU

INAWEZEKANA.TIMIZA WAJIBU WAKO KWA KUMPIGIA KURA DOKTA SLAA HAPO JUMAPILI



25 Oct 2010



Siku moja nilikuwa na mazungumzo na babu mmoja wa Kiskotish.Kwa vile ilikuwa ni safari ya masaa kadhaa kwenye treni kutoka mji mkuu wa Uingereza,London kuelekea mji wa kaskazini mashariki mwa Scotland,Aberdeen,tulipata wasaa wa kuongea mengi.Babu huyo ameshawahi kukaa Tanzania,na anajua maneno mawili matatu ya Kiswahili.Swali moja aliloniuliza,na ambalo limeendelea kuumiza kichwa changu hadi leo ni kwanini Tanzania ni masikini licha ya utajiri mwingi ilionao na watu wakarimu,wapenda amani na wenye kiu ya maendeleo.Sio siri,nilijiumauma kutoa jibu la kueleweka.

Uzuri kuhusu hawa wenzetu ni kwamba hawajui kumwonea mtu aibu.Babu huyo alinieleza waziwazi kuwa nimeshindwa kumpa jibu la kuridhisha sio kwa vile sifahamu kwanini Tanzania ni masikini bali nimeona aibu tu ya kutoa jibu sahihi.Na huo ni ukweli.Nilijua nikimwambia kwamba tatizo kubwa kwa maendeleo ya Tanzania ni uongozi,angeweza kuniuliza "kwani viongozi hao ni wakoloni au Watanzania wenzenu?"

Katika maongezi yetu babu huyo alinipa fundisho moja muhimu ambalo nadhani sote tunapaswa kulitilia maanani.Alinieleza kuwa zamani hizo wakati Uingereza inajengwa,Waingereza hawakuwa wanafikiria kuhusu mahitaji yao tu bali pia mahitaji ya vizazi vijavyo.Alifafanua kuwa kadri anavyoelewa,Waingereza wengi wanajibidiisha sio tu kwa ajili ya leo bali hata miaka 200 ijayo.Akanipa mfano wa namna walivyojenga treni za chini ya ardhi,hospitali zao kuubwa kama kijiji kizima,vyuo vilivyotapakaa sehemu kubwa za miji na maendeleo mengineyo.

Akatanabaisha kuwa wengi wa walioshiriki katika ujenzi huo wa Uingereza ya leo kwa sasa ni marehemu.Na akanikumbusha kuwa japo wakati wanajituma kujenga nchi yao walikuwa wanafahamun kuwa watafaidi matunda ya jitihada zao kwa muda mfupi tu kabla Mungu hajawachukua lakini hiyo haikuwakatisha tamaa kwa vile walifahamu kuwa vizazi vijavyo vingetaraji waliowatangulia wangetumia nafasi zilizokuwepo muda huo kuwaandalia mazingira mazuri ya kuishi.

Nifupishe stori.Jumapili ijayo tuna Uchaguzi Mkuu ambao binafsi nauona kama tukio muhimu kabisa kwa historia ya nchi yetu.Takriban miaka 50 baada ya uhuru kuna wenzetu wengi tu ambao wanaishi katika mazingira mabovu kuliko kabla ya ujio wa mkoloni.Lakini pia,kuna wachache ambao angalau wanamudu mahitaji ya msingi ya kila siku.Ni kundi hili ambalo ningependa kuelekeza rai yangu kwao.

Hebu tutafakari stori za huyo babu niliyekutana nae kwenye treni.Laiti kizazi chao kingeridhika na hali waliyokuwa nayo wakati huo basi huenda Uingereza ya leo isingekuwa imepiga hatua kama ilivyo sasa.Laiti wangekuwa wabinafsi wa kufikiria maslahi yao tu wasingejihangaisha na mipango ya maendeleo ambayo matunda yake yangeonekana baada ya vifo vyao.Lakini kwa vile waliweka mbele maslahi ya jamii badala ya maslahi binafsi,hawakusita kujenga msingi wa jamii ya Uingereza kwa wakati huo na karne kadhaa baadaye.

Tunaweza kuendelea kuwalaumu wakoloni kwa kukwaza maendeleo yetu.Lakini wakoloni walishaondoka takriban miaka 50 iliyopita.Sasa badala ya kupiga hatua,kuna nyakati tunajikuta tunarudi nyuma zaidi ya wakati wakoloni wanaondoka.

Na japo siwatetei wakoloni,lakini angalau wao walikuwa na excuse.Hawakuwa Watanzania wenzetu.Hawakuwa na uchungu na nchi yetu wala vizazi vijavyo.Vipi kuhusu viongozi wetu wa sasa?Hivi sio hawa waliosomeshwa bure buleshi lakini leo wanakataa katakata kuwa elimu ya bure haiwezekani?Kama iliwezekana wakati huo ambapo hatukuwa na maendeleo ya kutosha,kwanini ishindikane wakati huu ambapo tumeweza kugundua vyanzo mbalimbali vya mapato?

Tukiridhika na mishahara inayotuwezesha kwenda Twanga Pepeta kial wikiendi,au vikao vya bia kila jioni kisha tukasahau kuwa kuna wenzetu (na wengi wao ni ndugu zetu kabisa) huko vijijini hawana uhakika wa kifungua kinywa,wamesahau ladha ya chumvi kwenye mlo kwa vile chumvi imegeuka anasa japo iko kibwena huko Uvinza,sukari imegeuka muujiza hata huko Kilombero ambako wana kiwanda cha sukari na miwa inayozalisha sukari inaozeana mashambani.Kuna wenzetu ambao wali nyama au ugali nyama ni milo inayowezekana kwenye sherehe,misiba au wanapobahatika mara moja kwa mwaka kupelekwa hotelini licha ya maelfu kwa maelfu ya ng'ombe,mbuzi,kondoo na wanyama pori lukuki,sambamba na mchele,mahindi,mihogo,mtama,nk.

Sasa hali hii itaendelea hadi lini?Tunaweza kupuuza shida za wenzetu hawa ambao ni wengi kuliko sie lakini ni dhahiri kuwa ndani kabisa ya nafsi zetu tunateseka tunapokumbuka kuwa punje za wali tunazosafisha kwa minajili ya kuzitupa zinahitajika kwa udi na uvumba katika nyumba moja au nyingine.Hivi kama hawa "wazungu" na ubinafsi wao (hawa familia ni baba,mama na watoto.Habari za shangazi,binamu,mjomba,babu,bibi ni kama kachumbari kwenye mlo: inapendeza lakini sio muhimu). waliweza kuvikumbuka vizazi vijavyo na hivyo kujenga nchi zao hadi kufikia zilipo leo,wakni sie ambao familia ni zaidi ya mume,mke na watoto?

Kuna wenzetu wanaokumbatia mafisadi kwa vile tu wanahofia kuwa mafisadi hao wakiondoka basi nao hawatakuwa na namna ya kumudu maisha yao.Hiyo si kweli kwani hata nyakati za mkoloni kuna waliokuwa wanatumikia wakoloni na kuwakandamiza waafrika wenzao,lakini watu hao waliendelea kuwa hai,huru na kumudu maisha yao...tena kwa njia halali pasipo hofu ya kuonekana wasaliti.

Kura utakayopiga Jumapili ijayo ni zaidi ya kura yako binafsi.Ni kura kwa ajili ya memba wote wa ukoo wako (ambao katika mazingira ya kawaida kuna wengi tu wenye kuhangaika na maisha ya kila siku),rafiki zako wa zamani ambao baada ya kukosa nafasi ya kuendelea na masomo wakajaribu bahati zao kwenye kilimo lakini jitihada zao zinakwazwa na vyama vya ushirika vinavyojua kukopa zaidi kuliko kuuza mazao.Ni pamoja na wale ambao waliamua kufany kazi za wito kama ualimu au uuguzi lakini sasa wanajiuliza kama "wanafanya kazi ya Kanisa" kwani licha ya mshahara kuwa kijungujiko lakini pia hauna uhakika wa kufika katika muda stahili.Kuna wale jamaa zako walioamua kujiari lakini wanaandamwa na polisi na kubambikiwa kesi za bangi,uzururaji,nk kila wanaposhindwa kutoa rushwa kwa askari au mgambo.

Wafikirie hawa wakati unapiga kura.Weka kando mafanikio yako binafsi.

Na kwa wale wanaoteseka kwa vile watawala wamekuwa bize zaidi na kuongeza idadi ya magari yao ya kifahari,kuongeza idadi ya mahekalu yao,kuongeza idadi ya nyumba ndogo zao,na matumizi mengine ya anasa kama hayo,huu ndio wakati wenu wa kulipa kisasi.Kama mlibebwa kwa malori kwenda kwenye mkutano wa Kikwete au mgombea mwingine wa CCM,well,hakuwaomba bali walijipendekeza wenyewe.Hivi hamsangai ukarimu huu wa ghafla umetoka wapi?Hamjiulizi kuwa wakati mnahangaika kupeleka wagonjwa na akina mama wajawazito hospitalini kwa vile hakuna magari ya vimulimuli wao walikuwa wantembelea magari ya thamani huku wakiwatimulia vumbi,lakini ghafla leo wanawabeba kwenye malori mkawasikilize.MSIDANGANYIKE.Mkishawapa kura,hamtawaona tena mpaka mwaka 2015.

Japo nimesema kuwa uchaguzi huu una umuhimu wa kipekee,lakini ni muhimu kukumbuka kuwa tulikuwa na chaguzi kama hizi huko nyuma,na wa karibu zaidi ni wa mwaka 2005.Hivi hamkupata matumaini Kikwete alipoahidi maisha bora kwa kila mmoja wenu.Je mmeshayaona maisha hayo bora?Kama bado,kwanini mnataka kumwamwini tena safari hii japo amekaa madarakani miaka mitano na ameshindwa kutimiza ahadi aliyoweka mwenyewe bila kushikiwa mtutu wa bunduki (hakulazimishwa)?

Na yule mbunge aliyeahidi miujiza lakini akaishia kuongeza kitambi chake na idadi ya watoto kupitia hawara zake,kwanini umpe tena kura?Unataka aendelee kukusanifu?Maana ulifanya makosa mwaka 2005 ukiamini kuwa ahadi zake zilionyesha anakujali.Lakini miaka hii mitano iliyopita inatosha kukuthibitishia kuwa huyo ni tapeli wa kisiasa,na hakuna tapeli anayeaminika.Lakini sio yeye tu bali hata chama chake.

Hesabu umri wako.Halafu jiulize lini ulianza kuisikia CCM.Kumbuka magapi wameahidi katika miaka yote hiyo uliyokuwa unawafahamu.Linganisha maendeleo yako na hao wenye CCM halisi.Kwanini bado unaendelea kukiamini chama hiki?Kama waliahidi 1995 hawakufanya,lakini wakarejea tena kuahidi mwaka 2000,na hawakufanya.Na bila aibu wakarejea tena mwaka 2005,na safari hii wakiahidi kuwa wanajua matatizo yako na ya familia yako.Wakaahidi pia kuwa maisha yako yatakuwa bora kwa vile hilo linawezekana.Na wakaonyesha namna watakavyowezesha maisha bora kwa kila Mtanzania.Je wametimiza?

Lakini pengine wameshindwa kutimiza kwa sababu za kibinadamu.Sasa kwanini badala ya kukuomba msamaha na kueleza kwanini wameshindwa kukuletea maisha bora,wanakufanya mjinga kwa kukuahidi yaleyale waliyoahidi mwaka 2005 na kutoyatekeleza?Kumbuka: ukiwachagua tena hutokuwa na sababu ya kuwalaumu kwani wameshakuthibitishia kwa miaka kadhaa kuwa hawawezi kukusaidia lakini ukaendelea kuwaamini.Sasa,japo inakera kuona unaendela kuwaamini matapeli hawa,ni muhimu kukumbushana pale tunapokosea.Kufanya kosa si kosa bali kurejea kosa.Na umesharejea makosa hayo mara kadhaa.Sasa umefika wakati wa kusema IMETOSHA.

Nimalizie kwa kukumbusha kuwa katika uchaguzi huu tumebahatika kumpata Nyerere wa pili.Huyu ni Dokta Wilbroad Slaa.Kama ambavyo Nyerere alijitoa mhanga kuhakikisha mkoloni anaondoka,Dokta Slaa amethibitisha kuwa ni mzalendo mwadilifu ambaye ameamua kupambana na mafisadi hadi watokomee.Kama aliweza kuwakalia kooni mafisadi alipokuwa mbunge tu,jiulize atakayofanya atapokabidhiwa urais.Wakati akiwa mbunge silaha yake pekee ilikuwa ni maneno,lakini tukimkabidhi dola atakuwa na nyenzo mbalimbali za kuipeleka nchi yetu inapostahili kwenda.

Usihadaishwe na wasiwasi kuhusu wizi wa kura.Kuiba wataiba lakini ili waweze kuiba za kutosha kuwabakiza mafisadi madarakani itategemea zaidi idadi ya kura tutakazompa Dokta Slaa.Ni rahisi kuiba kura chache lakini ni vigumu kuiba maelfu au mamilioni ya kura.Wingi wa kura kwa Dokta Slaa utakuwa silaha muhimu ya kuwatia aibu mafisadi katika kujaribu kuchakachua kura au matokeo ya uchaguzi huo.

INAWEZEKANA.TIMIZA WAJIBU WAKO

20 Oct 2010



Serikali sasa yatishia kulifuta Mwananchi
Wednesday, 20 October 2010 07:52

Mwandishi Wetu
SERIKALI imetishia kulifunga au kulifutia usajili gazeti la Mwananchi kwa madai kwamba linaandika habari za uchochezi dhidi ya serikali ya awamu ya nne.Barua ya serikali yenye kumbukumbu namba ISC/N.100/1/VOL.V/76 iliyoandikwa kwa mhariri mtendaji wa gazeti la Mwananchi, inaonya kwamba kama gazeti hili litaendelea kuandika habari ambazo imeziita za uchochezi dhidi yake, haitasita kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa sheria za nchi.

Hata hivyo, barua hiyo haijaweka bayana habari hizo ilizozielezea kuwa ni za mtazamo hasi dhidi ya serikali na ambazo imedai kuwa ni za uchochezi.

“Kwa barua hii unatakiwa kuacha mara moja tabia ya kuandika habari za uchochezi na kuidhalilisha nchi na serikali kwa kisingizio cha uhuru wa habari na uhuru wa kutoa mawazo ulioanishwa katika katiba ya nchi yetu," inaeleza barua hiyo ya Oktoba 11 iliyosainiwa na Raphael Hokororo kwa niaba ya Msajili wa Magazeti.

"Aidha ukiendeleza tabia hiyo, serikali haitasita kuchukua hatua stahiki za kulifungia gazeti lako au kulifutia usajili kwa mujibu wa sheria za nchi.”

Barua hiyo, ambayo imebeba kichwa cha habari kisemacho "Karipio kali kwa kuandika habari zenye mwelekeo wa uchochezi wa kudhalilisha", ni mwendelezo wa barua nyingine iliyoandikwa na mkurugenzi wa Idara ya Habari, Clement Mshana kwenda kwa mhariri wa gazeti hili Septemba 24, 2010.

Katika barua hiyo ya Mshana, serikali imedai kuwa gazeti la Mwananchi limekuwa na mtazamo hasi dhidi ya serikali na ikamtaka mhariri ajieleze.

Barua hiyo yenye kumbukumbu namba ISC/N.100/1/VOL.V/70, bila ya kutoa mifano, inadai kuwa Mwananchi imekuwa ikiandika habari hasi tu kana kwamba serikali haina zuri linalofanywa kwa wananchi wake na kutaka maelezo.

“Katika kipindi kirefu sasa, na zaidi wakati huu wa kampeni za uchaguzi, gazeti lako limekuwa likiandika habari zenye mtazamo hasi dhidi ya serikali. Habari hizo zimekuwa zikidhalilisha serikali iliyo madarakani ya awamu nne,” inasema sehemu ya barua hiyo.

Katika majibu ya barua hiyo ya kwanza, Mwananchi Communications Ltd (MCL), ilieleza kuwa baada ya kutafakari kwa kina ilishindwa kuelewa msingi wa tuhuma hizo ambazo hazina mifano yoyote ya habari inayodaiwa kuwa ni hasi kwa serikali.

“Baada ya kupitia barua yako na kuitafakari, imetuwia vigumu kuelewa msingi wa tuhuma zako kwa gazeti hili kuhusu mtazamo hasi dhidi ya serikali bila hata kutoa mifano ya habari ambazo zinabeba tuhuma zako kwa gazeti hili hasa unaposema kuwa kwa kipindi kirefu sasa, hasa wakati huu wa kampeni za uchaguzi,” inasema barua hiyo yenye kumbukumbu namba MCL/RN/09/VOL.1.27 iliyoandikwa na mhariri mtendaji wa MCL, Theophil Makunga.

Barua hiyo ya MCL inaeleza kuwa kimsingi habari za kampeni za uchaguzi katika kipindi hiki zinahusu vyama vya siasa na kuhoji sababu za serikali kujiona inaandikwa vibaya na Mwananchi wakati ni vyama ndivyo vinavyoshiriki kwenye kampeni.

Mhariri wa Mwananchi anaeleza katika barua hiyo kuwa kwa sasa gazeti lake linaandika habari za wagombea uongozi kutoka vyama mbalimbali na sera zao ili wananchi wafanye uamuzi siku ya kupiga kura na hakuna chama kilichoandika barua ya malalamiko.

“Kwa taarifa yako tangu kuanza kwa kampeni za uchaguzi Agosti 21, 2010, gazeti la Mwananchi halijawahi kupata malalamiko kutoka chama chochote cha siasa kinachoshiriki katika kampeni hizo juu ya kuandikwa vibaya. Kimsingi Mwananchi linachofanya ni kuripoti wanachosema wagombea wa vyama mbalimbali au kufanyiwa katika mikutano ya kampeni,” inasema barua hiyo ya MCL kwenda kwa Msajili wa Magazeti.

Katika barua hiyo, MCL inaiomba serikali kutoa ufafanuzi zaidi kuhusu kuhusika kwa serikali katika kampeni za uchaguzi hadi gazeti hili lionekane lina mtazamo hasi.

“Kwa msingi huo, tunaomba ufafanuzi zaidi hapa; serikali inahusika vipi katika kampeni mpaka Mwananchi ionekane ina mtazamo hasi kwa serikali wakati vinavyoshiriki katika kampeni ni vyama vya siasa na wagombea wake,” inasema barua hiyo.

Baada ya barua hiyo, Msajili wa Magazeti alijibu kwamba majibu yaliyotolewa na MCL hayaridhishi na hivyo ofisi yake haikuridhika na utetezi huo.

“Kama tulivyoeleza kwenye barua yetu kwako kuwa katika kipindi kirefu sasa na zaidi wakati huu wa kampeni za uchaguzi, gazeti lako limekuwa likiandika habari zenye mtazamo hasi dhidi ya serikali. Gazeti lako sasa limeamua kufanya ‘house style’ yake ya kuandika habari zenye uchochezi na kudhalilisha nchi na serikali iliyopo madarakani,” inasema barua hiyo.

Katika onyo lake, serikali inasema kwamba picha, habari zinazopewa kipaumbele katika ukurasa wa kwanza wa gazeti zinatiwa chumvi kwa lengo la kuchochea wananchi waione serikali yao haijafanya chochote kwa maendeleo yao.

Akiongelea hatua hiyo ya serikali, Makunga alisema kwamba MCL imeshtushwa na karipio hilo ambalo halikuonyesha ni habari ipi ambayo gazeti la Mwananchi limekosea.

“Msajili hakunukuu hata sheria moja ya vyombo vya habari kuonyesha jinsi gani gazeti limekosea wala habari au kichwa cha habari chenye mtazamo hasi kwa serikali,” alisema Makunga.

Alisema Mwananchi imechukulia hatua hiyo ya msajili kuwa inatishia uhuru wa vyombo vya habari hasa katika kipindi hiki cha kampeni za uchaguzi ambacho kinahitaji uvumulivu baina ya taasisi mbalimbali katika jamii.

Makunga alisema kwa kuwa Mwananchi na msajili inaonekana kutokubaliana katika suala hilo, wameamua kupeleka taarifa Baraza la Habari Tanzania (MCT) liweze kufanya uchunguzi kwa mujibu wa katiba yao.

Alisema msimamo wa sera ya uhariri ya MCL inasimamia kwenye ukweli na weledi pasipo kushurutishwa na vikundi vyovyote vya nje na ndani.Makunga alisema Mwananchi itaendelea kuandika habari za ukweli bila ya kumuonea mtu au taasisi yoyote kwa maslahi ya Tanzania.

CHANZO: Mwananchi

17 Oct 2010

Moja ya mambo yaliyokuwa yakiwaumiza vichwa wafuasi wa Barack Obama wakati wa kinyang'anyiro kati yake na Hillary Clinton kupata mgombea urais wa Marekani kwa tiketi ya chama cha Democrats mwaka 2008 ni theory inayofahamika kama Bradley Effect.Kwa kifupi kabisa,Bradley Effect (au Wilder Effect) ni hali inayoweza kutokea kwenye kura za maoni katika chaguzi nchini Marekani panapokuwa na mgombea Mweupe (White) na asiye mweupe (non-White).Pengine ili wasionekane wabaguzi wa rangi,wahojiwa Weupe katika kura za maoni hueleza kuwa chaguo lao ni mgombea asiye Mweupe au husema kuwa hawajafanya uamuzi kuhusu chaguo lao (Undecided).

Kwahiyo,matokeo ya kura ya maoni yanaweza kuonyesha mgombea asiye Mweupe anapendwa zaidi kuliko mgombea Mweupe lakini inapofika kwenye hatua ya kupiga kura (ambapo mpiga kura anakuwa peke yake),wapiga kura Weupe wanampigia Mweupe mwenzao.

Asili ya Bradley Effect ni katika kinyang'anyiro cha uchaguzi wa uchaguzi wa gavana wa jimbo la California mwaka 1982 ambapo licha ya mgombea Mweusi,Meya wa Jiji la Los Angeles Tom Bradley kuongoza kura za maoni,aliishia kushindwa uchaguzi huo kwa mgombea Mweupe George Deukmejian.

Baadhi ya wachambuzi wa chaguzi nchini Marekani wanaamini pia kuwa Bradley Effect ilijitokeza tena kwenye mchakato wa kumpata mgombea wa chama cha Democrats kwenye jimbo la New Hampshire ambapo licha ya Obama kuongoza katika kura za maoni,Hillary Clinton aliibuka mshindi kwenye jimbo hilo (japokuwa baadaye Obama alifanikiwa kuibuka mshindi wa jumla,na kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya Democrats,na hatimaye kushinda nafasi ya urais).

Katika post hii najaribu kubashiri (hypothesize) namna Bradley Effect inavyoweza kuwa sababu ya mgombea wa CCM,Jakaya Kikwete,kuongoza katika tafiti za  taasisi za Redet na Synovate kuhusu nafasi za wagombea urais katika uchaguzi mkuu wa Tanzania hapo Oktoba 31.Hapa ntawazungumzia wagombea wawili tu,Kikwete na mgombea urais kwa tiketi ya Chadema,Dokta Wilbroad Slaa.

Japo Bradley Effect 'halisi' inahusu mgombea Mweupe na asiye Mweupe,sababu inayopelekea matokeo ya kura kutorandana na mwelekeo wa kura za maoni inaweza kutumika kuelezea kwanini kura za maoni za Redet na Synovate zilimpa Kikwete ushindi na sio Dokta Slaa.Kama ilivyo kwenye chambuzi mbalimbali,kuna mambo flani inabidi 'kupuuzwa' ili kufikia matokeo yanayokusudiwa.Katika uchambuzi huu,naomba 'nipuuze' urafiki kati ya taasisi hizo na CCM na badala yake nikazanie kwenye uwezekano wa Bradley Effect pekee.

Inawezekana kabisa kuwa wahojiwa kwenye tafiti za Redet na Synovate ni wananchi waliotoa majibu 'kuwaridhisha watafiti',yaani walisema wanampenda zaidi Kikwete kuliko Dokta Slaa.Moja ya sababu za kutoa majibu ya aina hiyo ni mazingira halisi ya Tanzania ambapo licha ya 'siasa za mkono wa chuma' za zama za chama kimoja kuonekana kama historia,ukweli unabaki kuwa baadhi ya wananchi wanaamini kuwa kusema lolote lisilowapendeza watawala ni kujitafutia matatizo.

Naomba kufafanua kidogo katika hilo.Nilipokwenda Tanzania mwaka 2005 kufanya fieldwork ya utafiti wangu wa shahada ya uzamifu (PhD) nilikumbana na wakati mgumu kuwahoji baadhi ya maustaadh (mada yangu inahusu masuala ya Waislam na Uislam nchini Tanzania) kwa vile baadhi yao walidhani mie ni wakala wa serikali niliyetumwa kuwachunguza ili 'serikali iweze kuwadhibiti zaidi'.Bahati mbaya,fieldwork hiyo ilifanyika wakati jeshi la polisi lilikuwa linamsaka mwanaharakati wa Kiislam,Sheikh Issa Ponda.Ilichukua kitambo kujenga uaminifu kati yangu na maustaadh hao.

Kuna wanaoilaumu Redet na Synovate kuhusu aina ya watu waliohojiwa wakidai kuwa huenda wahojiwa walikuwa watu walio karibu na CCM (kwa mfano mabalozi wa nyumba kumi).Uwezekano wa Bradley Effect  'yetu' (yaani isiyohusiana na ishu za ubaguzi wa rangi) ni mkubwa kwa vile wahojiwa wanaweza kutoa majibu yasiyoonyesha 'wanambagua mgombea wao' na hivyo kusema huyo ndio chaguo lao japo mioyoni wana dhamira na/au chaguo tofauti.

Of course,inawezekana tafiti hizo za Redet na Synovate 'zilipikwa' ili kuendana na matakwa ya CCM.Inawezekana pia kuwa aina ya watu waliohojiwa ni ambayo isingetoa majibu tofauti na 'ushindi kwa Kikwete'.Lakini,kama makala hii inavyojaribu kubashiri,inawezekana kabisa kuwa wahojiwa 'waliwazuga' jamaa wa Redet na Synivate 'ili isiwe shida'.Nani yuko tayari kuona genge lake au kibanda cha biashara kinabomolewa kwa vile tu amechoshwa na namna CCM inavyozidi kuahidi maisha bora lakini wanaonufaika ni mafisadi pekee?Mtu wa aina hii haoni shida 'kudanganya leo' kisha 'akaungama siku ya kupiga kura' kwa 'kumwadhibu Kikwete na CCM kwenye sanduku la kura ambapo hakutokuwa na wa kumtoa mimacho kwanini hajampigia kura Kikwete au CCM'.

Huu ni ubashiri tu.Unaweza kuwa sio sahihi lakini kama zilivyo bashiri nyingine-hususan zinazoambatana na mifano hai-unaweza kuwa na ukweli ndani yake.Kadhalika,Bradley Effect 'yetu' inaweza kutoa matokeo ya kuwashangaza wote wenye imani kuwa CCM na Kikwete watarudia kupata ushindi wa kishindo kama wa mwaka 2005.

Pengine kuna watakaohoji kwanini Bradley Effect 'yetu' haiwezi kutumika kwenye utafiti mwingine (wa TCIB) unaoonyesha kuwa Dokta Slaa anaongoza.Jibu langu ni kwamba watoa maoni hawana cha kupata (nothing to gain) kuwadanganya watafiti kuwa wanampenda Dokta Slaa wakati ukweli wanayempenda ni Kikwete.Likewise,kwenye tafiti za Redet na Synovate,inawezekana baadhi ya wahojiwa walikuwa na cha kupoteza laiti wangesema hawampendi Kikwete (si unajua kuhusu umoja na mshikamano ndani ya chama?).Vilevile,yawezekana wahojiwa hawakuwa na cha kupoteza (nothing to lose) kwa kudanganya kuwa wanampenda Kikwete (kwa minajili ya kuwaridhishwa watafiti na 'kulinda ugali wao') kisha wakamnyima kura katika usiri wa chumba cha kupigia kura.

Mwisho,naomba kusisitiza tena kuwa hypothesis hii imejaribu kupuuza sababu za 'wazi' kama vile upendeleo wa watafiti,uoga wa wahojiwa,na kubwa zaidi,UCHAKACHUAJI.

15 Oct 2010


Na Mwandishi wetu

Shirika lisilo la kiserikali linalojishughulisha na kutoa utafiti wa taarifa mbalimbali kwa lengo la kuwawezesha wananchi maamuzi kwa uelewa la Tanzania Citizens Information Bureau (TCIB) limetoa taarifa ya matokeo ya utafiti wa kura ya maoni kuhusu wagombea urais 2010.

Akizungumza na waadishi wa habari Mhadhiri Chuo Kikuu cha Dar es salaam idara ya Uchumi Dr. Vicent Leyaro amesma malengo ya TCIB ni kutoa msukumo kwa wananchi kushiriki katika harakati za kulinda na kendeleza misingi ya Demokrasia, Kutoa fursa kwa wananchi katika kutoa maoni yao juu ya mambo mbalimbali katika maisha na kujenga uwezo wa wananchi kwa njia ya tafiti na elimu katika nyanja za serikali, siasa, Mambo ya Kimataifa, ulinzi, elimu na maadili.
Kutoka kushoto ni Mhadhini kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Idara ya Uchumi Dr.Vicent Leyaro akizungumza na waandishi wa habari katika Hotel ya Courtyard juu ya utafiti wa (TCIB) akiwa na mwakilishi wa Mkurugenzi wa (TCIB) Bw. Steven Msechu.

Aidha Dr. Vicent Leyaro amesema washiriki katika kura hii ya maoni ni 3047 wenye wasifu wa aina mbalimbali ikiwa ni pamoja na watoto chini ya darasa la saba, elimu ya sekondari na elimu iliyo juu ya sekondari ambapo katika utafiti huo silimia kubwa ya vijana wamonekana kuunga mkono mgombea urais wa CHADEMA Wllbrod Slaa na asilimia kubwa ya wazee wameonyesha kumuunga mkono mgombea urais wa CCM Jakaya Kikwete.

Amesema Dr. Willbod Slaa ameongoza kwa asilimia kubwa katika mikoa ya Kilimanjaro 71%, Arusha 60.4%, Manyara79.8%, Iringa58.2% na Dar es salaam 42% ambapo Jakaya Kikwete ameongoza kwa asilimia kubwa katika mikoa Dodoma 59.3%, Morogoro 56%, Mbeya50%, Rukwa 54.3% na Ruvuma 55%.

Akihitimisha wakati akijibu maswali kwaa waandishi wa habari Dr. Vicent Reyaro amesema utafiti haukuangalia wala kupendelea sehemu ambazo mtu anapendwa sana kuliko sehemu nyingine na uchambuzi wa matokea kimkoa yanaonyesha kuwa wagombea wawili Jakaya Kikwete na Dr. Willbrod Slaa wanachuana vikali baadhi ya mikoa na mikoa mingine kufanya vibaya.

Hata hivyo utafiti huu wa kura ya maoni kuhusu wagombea urais hauukufanyika kwa upande wa Zanzibar japokuwa wananchi wa Zanzibar wanashiriki katika kupiga kura ya kuchagua rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Chanzo: Changamoto

Habari kwa hisani ya Jamii Forums

12 Oct 2010


Nimekumbana na post ifuatayo hapo Jamii Forums.Naiwasilisha kama ilivyo kisha tujiulize kwa pamoja (kama tuhuma hizo ni za kweli) wanafanya hivyo kwa faida ya nani?

Taarifa ya Siri - Mikakati ya Kuiba Kura Inavyoendelea USALAMA WA TAIFA
Napenda kuwajulisha mikakati michafu ya kupora na kuzuia maamuzi ya umma yanayofanywa na ccm kwa uratibu wa usalama wa taifa. Baada ya kubaini dalili za kuanguka vibaya katika uchaguzi wa mwaka huu idara ya usalama wa taifa imeandaa mikakati ya kuiba kura ili kuzuia chadema msiingie ikulu. Mikakati hii inaeleweka vizuri kwa tume ya taifa ya uchaguzi ambayo inashirikiana bega kwa bega na idara ya usalama wa taifa kumtengenezea jk ushindi bandia wa 80%. Wana hakika watanzania watagundua wizi huo na watakataa matokeo ndiyo maana kwanza waliwatumia viongozi wa dini waliotembelea makao makuu ya chadema wawasihi chadema wakubali matokeo yatakapotangazwa na juzi wamelitumia jeshi kutisha wananchi watakaoamua kupinga matokeo ya kupikwa yanayoandaliwa na nec/usalama wa taifa. Majid Kikula ambaye ni government security officer ndiye mratibu wa zoezi la kuiba kura, ni mtaalamu aliyebobea katika kazi za aina hii aliratibu vizuri zoezi kama hilo mwaka 2005. Pia mwaka 2007 alitumwa kenya kwenda kumsaidia kibaki kupora ushindi wa odinga.
Kikula anatumia muda wake mwingi hivi sasa ofisi za tume ya uchaguzi kwa ajili ya uratibu wa uvurugaji daftari la kudumu la wapiga kura akiifanya kazi hiyo kwa karibu na baadhi ya watendaji wa nec na maafisa kadhaa wa usalama wa taifa kutoka kurugenzi ya IT ya idara ya usalama (DITA) ambao wako ndani ya nec kwa zaidi ya miezi sita sasa, nitawapatia majina yao. Pia kuna vijana wataalamu wa IT waliochukuliwa kutoka maeneo mbalimbali wamepewa nyumba upanga mtaa wa undali shughuli kubwa wanayofanya ni kuandaa utaratibu wa ku-access remotely daftari la kudumu la wapiga kura. Hawa wanafanya kazi chini ya Salva Rweyemamu na Mindi Kasiga kutoka kurugenzi ya mawasiliano ikulu. Wapo vijana kadhaa leo nawapa majina ya wawili; Maharage Chande na Edgar Masatu wanafanya kazi kwa karibu na Nzowa wa idara ya usalama ambaye ndiye aliyeratibu shambulio la kumwagiwa tindikali Kubenea. Pia kuna kundi linalojumuisha wataalamu wa printing wa kiwanda cha uchapaji cha usalama wa taifa kilichopo MALINDI ambao hivi karibuni walikuwa mjini tanga kwa semina fupi ya jinsi ya kughushi kura kupitia fake ballot paper, timu hii inaongozwa na ndg SINYAU.
Kwa hiyo utaona kwamba imeandaliwa mikakati mingi kuufanikisha uovu huo ili mmoja ukikwama basi mwingine utatumika ila wameamua ni lazima jk ashinde kwa 80%. Ndani ya idara ya usalama wa taifa maafisa wengi wamechoshwa na uongozi mbovu wa ccm hivyo wanataka mabadiliko ya uongozi idara imechukua hatua kadhaa kuhakikisha maafisa wote wa idara wanampigia kura jk, wote wameagizwa kuwasilisha vitambulisho vyao vya kupigia kura ili vinakiliwe namba ili atakayepigia upinzani afukuzwe kazi baada ya uchaguzi. Fuatilieni kwa karibu haya niliyowaeleza nimeyapata kwa nafasi yangu ndani ya tiss. Huyu KIKULA mfuatilieni kwa  karibu ni hatari. HAKIKISHENI DUNIA NA WATANZANIA WOTE WANAJUA MAPEMA HILA HIZI. Jambo la kujiuliza maafisa usalama wa taifa wanafanya nini ndani ya tume ya uchaguzi wakati huu.



8 Sept 2010

Image and video hosting by TinyPic
Josephine Mushumbusi, amezungumza kupitia Mwanasheria Mkuu wa Chadema, ambaye pia ni wakili wa Dk Willibrod Slaa, Tundu Lissu, akaviambia vyombo vya habari kuhusu tuhuma zinazowakabili yeye na Dk. Slaa kuwa kwa mara nyingine, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimerejesha mfumo wa uchaguzi unaobadilishwa kuwa mfumo ya kijinga (a silly season). Akasema kwamba CCM wamekuwa wakikishambulia Chadema kuwa ni chama Wachagga; kwamba baadhi ya viongozi wake ndio walimuua Chacha Wangwe; na kwamba Dk Slaa ametumwa na kanisa Katoliki kugombea urais; lakini baada ya kuona hadithi hizo zimepuuzwa, sasa wameibuka na suala jipya na “ndoa za Dk. Slaa” wakidhani zitawasaidia kugeuza macho ya umma kutoka kwenye masuala muhimu ya wakati huu.

Akasema CCM hawataki Dk. Slaa na Chadema wajadili wizi, ubadhirifu wa fedha na mali za umma; hawataki wajadili wizi wa Sh. bilioni 772 zilizoibwa katika mwaka 2008/9 tu, kwa mujibu wa ripoti ya Mkaguzi na mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali; hawataki Chadema itaje majina ya wezi wa Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT); hataki Chadema wajadili jinsi JK na rafiki zake, akina Edward Lowasaa, Nazir Karamagi, Andrew Chenge na Rostam Azizi walivyofilisi taifa hili; hawataki Chadema ijadili madai halali ya wafanyakazi wa Tanzania na ahadi za ‘maisha bora kwa kila Mtanzania.’ CCM hawataki Chadema kijadili sera mbadala ambazo zinalenga kuwakomboa Watanzania kutoka lindi la umaskini.

Wanataka kulielekeza taifa zima katika kujadili masuala ya ‘chumbani’ kwa Dk. Slaa; analala na nani, ana wake wangapi, kawapata wapi na kadhalika; ili kwa kufanya hivyo mgombea wao awarubuni wananchi kwa ziara mikoani na ahadi kemkem zisizotekelezeka.

Tundu Lissu amesisitiza kuwa kila wanapoona wamebanwa, CCM huwa wanabuni njama za kukomoa washindani wao, kama walivyofanya huko nyuma. Alitoa mifano ya kilichotokea miaka ya 1995 na 2005.

Mwaka 1995: Kwa kumwogopa Mrema aliyekuwa tishio kwa CCM, walimtumia mwanamke mmoja, aitwaye Angelina, wakidai ni kimada aliyezaa na Mrema; akawa analala getini kwa Mrema, Masaki, Dar es Salaam. Wakamdhalilisha. Baada ya uchaguzi, Mrema akashindwa, na suala la Angelina halikujadiliwa tena.

Mwaka 2005 tishio la CCM ilikuwa Chama cha Wananchi (CUF), hasa Zanzibar. CCM wakamtumia Inspekta Jenerali wa Polisi, Omar Mahita, siku chache kabla ya uchaguzi, kudai kuwa amekamata lori lenye mapanga, majambia, visu na silaha nyingine zenye nembo ya CUF. Wakakipaka chama matope. Baada ya uchaguzi, hatukuelezwa lolote kuhusu visu hivyo.

Mwaka huo huo, katika uchaguzi wa ndani ya chama, baada ya kundi la JK kuona limezidiwa mno, likaamua kumzushia Dk. Salim Ahmed Salim likidai ni Mwarabu, na muuaji wa Rais Abeid Amani Karume. Wakamhujumu, Na baada ya uchaguzi hawakuzungumzia tena uarabu wa Dk. Salim.

Mwaka 2010: Tishio la CCM ni Chadema na Dk. Slaa. Baada ya kuona upepo unawaendea vibaya, CCM wameamua kufanya siasa za mtaro wa maji taka; hizi wanazotumia watu kumwandama Dk Slaa.

Tundu Lissu alisema kuwa Chadema hawako tayari kufanya siasa za majitaka; na kwamba Watanzania hawako katika kujadili mambo hayo, kama hali ya afya za wagombea, ambao baadhi wanadaiwa kuwa na virusi vya ukimwi kiasi cha kubadili damu kila baada ya miezi, na kwamba kwa sababu ya unyonge huo, baadhi yao waanguka mara kadhaa jukwaani.

Akasema wao hawatazungumzia baadhi ya wagombea urais wana wake wangapi, mahawara wangapi, na wamewaweka katika ofisi gani za umma, wapi wamepewa mikataba minono ya fedha kwa upendeleo, na kadhalika. Akasisitiza kwamba Chadema haitajibu uchafu unaosambazwa na vyombo vya habari, lakini akasema, “sauti yetu itasikika iwapo wataenda mahakamani.”
Akasema Chadema itazungumzia umaskini wa Watanzania na namna ya kuupunguza au kuuondoa; jinsi Tanzania ilivyo nchi ya tatu katika Afrika lakini wanakijiji wanalazimishwa kujenga shule za kata huku serikali ikifuja mabilioni ya pesa (kama hizo bilioni 772/- zilizotafunwa ndani ya mwaka mmoja.

Akasema Chadema itajadili malipo ya anasa kwa mawaziri, maisha duni ya polisi, walimu, wauguzi na makundi mengine yanayonyonywa katika jamii. Akasema Chadema itajadili jinsi ya kuboresha afya za wananchi.

Akasema, “hatutaki siasa za chumbani, bali za hadharani.”

Kwanini wamshambulie Dk Slaa? Kwa sababu ni Dk. Slaa.

- Ana rekodi ya kuwashinda CCM mara tatu, kwa miaka 15 mfululizo
- Amekuwa sauti kuu ya wananchi Bungeni, inayotetea masilahi ya umma
- Kuliko kiongozi yeyote aliyewahi kuwapo Tanzania ndani ya miaka 50, ni Dk Slaa pekee aliyetaja hadharani mafisadi 11 bla woga wowote. Walioathirika kwa ujasiri wake ndio hao wanaomsakama sasa kwa mambo ya chumbani badala ya mambo ya hadharani.


27 Aug 2010

Sheria ni msumeno: Rais Kikwete akisaini kwa mbwembe Sheria ya Gharama za Uchaguzi,ambayo Chadema wanamtuhumu kuikiuka na hivyo wanamwekea pingamizi.
Geofrey Nyang'oro na Lilian Mazula

SHERIA ni msumeno na sasa imgombea urais wa CCM, Jakaya Kikwete atalazimika kufanya kazi ya ziada isimdhuru baada ya Chadema kumwekea pingamizi rais huyo wa serikali ya awamu ya nne.Kikwete alisaini Sheria ya Gharama za Uchaguzi kwa mbwembwe mapema mwaka huu akitaka itumike mwaka huu, lakini Chadema imeitumia sheria hiyo kumwekea pingamizi, ikidai kuwa mgombea huyo wa CCM ameikiuka.

Katibu mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa Kikwete amekiuka sheria hiyo kwa kwa kutangaza ongezeko la mishahara ya wafanyakazi wa sekta ya umma akiwa kwenye mikutano ya kampeni.

"Wanasheria wetu wanashughulikia suala hilo kwa kusaidiana na naibu katibu mkuu, John Mnyika kukamilisha pingamizi hilo na kesho (leo) asubuhi tutawasilisha pingamizi letu kwa msajili wa vyama vya siasa,"alisema Dk Slaa ambaye pia ni mgombea urais kwa tiketi ya Chadema.

Dk Slaa alidai kuwa Kikwete alikiuka kipengele cha 6, sehemu ya 21 (1) cha sheria hiyo inayotoa tafsiri ya mambo yanayokatazwa wakati wa mchakato wa uteuzi wa wagombea na kampeni za uchaguzi.

Alisema Kikwete amekiuka kifungu hicho kwa kutangaza ongezeko la mishahara ya wafanyakazi akiwa katika majukwaa ya kampeni, jambo ambalo linaweza kutafsiriwa na sheria hiyo kuwa ni rushwa ya uchaguzi.

Alieleza kuwa Kikwete amekiuka sheria hiyo kwa kuwa yeye kama mgombea, hana mamlaka ya kuongeza mshahara wa wafanyakazi katika kipindi hiki cha kampeni.
Dokta Slaa

"Kwa kutungwa kwa Sheria ya Gharama za Uchaguzi na kusainiwa Julai 17 mwaka huu pamoja na marekebisho yake, tulitegemea kungesaidia kuleta mabadiliko," alisema Dk Slaa ambaye kitaaluma amebobea kwenye sheria.

"Kitendo cha Kikwete kukiuka sheria hiyo kimenishtua sana.

Watanzania tungependa kupewa ufafanuzi; fedha hizo za (mishahara) zimetoka wapi na kwa mamlaka ya nani kwa kuwa wenye mamlaka ya kuidhinisha matumzi ya fedha za umma ni Bunge," alisema Dk Slaa.
Alifafanua kuwa kwa mujibu wa katiba, Bunge ndilo lenye mamlaka ya kuidhinisha matumizi ya fedha ikiwa ni pamoja na ongezeko la mishara kwa wafanyakazi wa umma.

"Kitendo cha serikali kuamuru ongezeko hilo nje ya vikao vya bunge, ni ukiukwaji wa sheria za nchi na ndio mwanya uliosababisha kutoweka kwa fedha za Akaunti ya Madeni ya nje(EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT)," alisema Dk Slaa.

"Sehemu ya tano ya sheria hiyo sura ya 21.-(1) inaweka bayana vitendo vinavyokatazwa wakati wa uteuzi wakati wa kampeni za uchaguzi na inasomeka:

"(a)Kila mtu ambaye kabla au wakati wa kipindi cha kampeni, moja kwa moja au kwa namna nyingine yoyote, kupitia kwa mtu mwingine yeyote au kwa niaba yake, anatoa, anakopesha au anakubali kutoa au kukopesha, au anatoa, anaahidi au kumpatia au anajaribu kumpatia fedha yoyote au kitu chochote chenye thamani,

mpiga kura au kwa ajili ya mtu yeyote kwa niaba ya mpiga kura yeyote au kwa ajili ya mtu mwingine yeyote kwa nia ya kumshawishi kupiga kura, au kuacha kupiga kura au kumrubuni mtu yeyote kutendo hicho kwa niaba ya mpiga kura huyo kupiga kura au kuacha kupiga kura katika kura za maoni au uchaguzi wowote;

"Kikwete alisema yeye mwenyewe hahitaji kura za wafanyakazi, na akasisitiza katika hotuba yake iliyoitoa kwa wazee wa Dar es Salaam kuwa serikali haina uwezo wa kulipa mishahara hiyo na kama wanafanya hivyo kwa kushinikiza kigezo cha kura, yeye hazitaki; leo mishahara imeongezeka, fedha hizo zimetoka wapi?Tunataka utueleze matumizi hayo ya fedha za umma kinyume na utaratibu."

Kwa mujibu wa Dk Slaa mgombea urais anapaswa kulinda katiba na sheria zilizopo, ili kulifanya taifa liendelee kuwa katika hali ya amani na utulivu katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye uchaguzi mkuu.

Dk Slaa alisema kuwa kitendo cha rais kutumia nafasi hiyo kutangaza mishahara kwenye kampeni ni kujipa upendeleo kwa kushawishi watu kumpigia kura kwa kutumia nafasi aliyonayo.

Dk Slaa pia alitumia fursa hiyo kukemea kitendo cha kufanya maamuzi kwa kukiuka sheria zilizopo akieleza kuwa kufanya hivyo kunaweza kuhatarisha usalama wa nchi.

Dk Slaa pia alienda mbali zaidi na kuituhumu CCM kwamba imekiuka taratibu za uchaguzi kwa kutengeneza mabango yake ya mgombea nchini Canada.

"CCM wametumia Sh1.5 bilioni kutengeneza mabango nje ya nchi kwa kutumia fedha za serikali pia ankara ya malipo "invoice" inaonyesha imeandikwa 'VAT INVOICE' kitu ambacho hakieleweki," alisema Dk Slaa.
Alisema kuwa ni muhimu CCM kutoa ufafanuzi juu ya hilo kwa kuwa ushahidi upo na unaonyesha kuwa kuna mchezo mchafu umeanza kufanywa.

CHANZO: Mwananchi

26 Aug 2010

Na Frederick Katulanda, Mwanza na Sadick Mtuly

LICHA ya sheria na kanuni za Uchaguzi kuzuia matumizi ya magari ya serikali, msafara wa mgombea urais wa CCM Jakaya Kikwete umetumia magari kadhaa ya serikali katika mikoa ya Mwanza, Geita na Kagera.

Mbali na magari hayo, wakuu wa wilaya waliokuwa wameshiriki msafara wa mwenyekiti huyo wa CCM, walitumia magari yao ya kazi yakiwa yamewekwa namba binafsi huku wakivalia sare za chama hicho.

Ukiondoa magari maalumu ya walinzi wa mgombea huyo ambaye pia ni rais, magari mengine ya wakuu wa wilaya na wakuu wa idara mbalimbali za serikali, yalitumika na kuwekwa namba binafsi.

Kwa mujibu wa habari tulizozipata kutoka vyanzo vyetu zinaeleza kuwa hivi sasa Ikulu ya Dar es Salaam ina upungufu kwa kuwa wafanyakazi wa Ikulu hasa madereva pamoja na wapishi na wagawa vinywaji (waandazi), wanatumika katika kampeni za Rais Kikwete.

Wapishi na waandazi hao wamepelekwa mikoani kulingana na ziara za kampeni.

“Cha ajabu ni kuwa baadhi ya wafanyakazi wa Ikulu hasa madereva, wapishi na waandazi wanatumika katika kampeni za CCM kupitia Rais Kikwete.

“Wamegawanywa katika mikoa tofauti kulingana na ratiba za ziara za kampeni za rais,’’ kilisema chanzo chetu.

Juzi jijini Mwanza Mkuu wa wilaya Ilemela, Serenge Mrengo ambaye alifika majira ya saa 4:35 asubuhi uwanja wa ndege na gari lenye namba za STK 3551 huku wote wawili na dereva wake wakiwa wamevalia sare za CCM, lakini baada ya kusalimiana na viongozi wenzake, aliondoka.

Akiwa wilayani Geita, Mkuu wa wilaya hiyo Philemon Shelutete alitumia gari lake la serikali ambalo lilikuwa limebandikwa namba T 804 BCZ huku akiwa amevalia sare za CCM. Pia gari la Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita Benson Katala lilitolewa namba za serikali na kubandikwa namba T 180 BKW.

Mkuu wa mkoa wa Mwanza Abbas Kandoro alitetea hatua hiyo akisema sio kosa kwa kuwa Kikwete bado ni rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzanania.

Kandoro, alikiri kutumika kwa magari hayo ya serikali na kusema kuwa viongozi hao waliyatumia kumpokea na baadhi yao waliambatana naye katika ziara hiyo kwa kuwa mbali na kuwa mgombea wa CCM pia anayo hadhi ya urais.

“Huyu ni Rais, amekuja kama kiongozi licha ya kwamba anagombea, bado hajavuliwa urais, sasa ma-DC walikuja kama viongozi wa serikali kumpokea rais. Kama kuna mkuu wa wilaya alivaa shati la CCM alivaa kwa sababu ya mapenzi yake kwa chama,” alifafanua Kandoro ambaye alitumia gari binafsi la kiongozi mmoja wa CCM Kanda ya Ziwa.

"Makosa ni kiongozi wa serikali kufanya kazi za chama na sioni kama kuna kiongozi wa serikali ambaye alifanya kazi za chama,"alisema

Msafara wa Kikwete kuambatana na magari ya serikali haukuishia Mwanza na Geita pekee bali pia hata mkoani Kagera ambako magari mengi yalikuwa na namba za STK.

Katika hatua nyingine, uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Bugando umetoa ufafanuzi kwamba uamuzi wake wa kutoa gari la kubebea wagonjwa katika msafara wa mgombea urais wa CCM kuhakikisha usalama wa mgombea huyo.

Mkurugenzi wa Hospitali hiyo, Dk Charles Majinge alisema kwa kawaida jukumu la kutoa magari huwa lipo mikononi mwa uongozi wa mkoa ambao uliomba gari kwao na wao waliamua kutoa gari hilo la wagonjwa namba T 848 AWN.

“Sisi hatutoi ambulance kwa wagombea, ila tulitoa kwa Kikwete kutokana na kuwa ni kiongozi wa nchi. Kutoa magari huwa ni kazi ya uongozi wa mkoa, lakini sisi kama watalaamu wa matibabu tulichukua tahadhari na kuweka gari hilo,” alieleza Dk Majinge.

Alisema kwa vile akiwa jijini Mwanza aliwahi kuanguka, basi waliamua kuchukua tahadhari kuepuka kukosa huduma haraka iwapo jambo hilo lingejirudia akiwa mbali na hospitali ya rufaa.

Akizungumzia gari hilo, Kandoro alisema uwapo wake ni utaratibu wa kawaida katika misafara ya viongozi wa serikali.

“Huu ni utaratibu wa kawaida katika misafara ya viongozi, tumetoa kama utaratibu wa kawaida….unajua huyu ni kiongozi wa nchi, sasa unataka wakija na wagombea wengine wa upinzani nao tuwapatie magari ya wagonjwa, wao ni akina nani?” alieleza na kuhoji Kandoro ambaye pia aligombea kura za maoni kuwania kuteuliwa na CCM kuwa mgombea ubunge Jimbo la Kalenga na kushindwa.

Akizungumza kwa sharti la kutotaja jina gazetini mmoja wa viongozi ambao walikuwa wakishughulika na kuratibu msafara huo alieleza kuwa gari hilo la wagonjwa ni lile ambalo lilitolewa na serikali ya Ujerumani chini ya ushirikiano wa Jiji la Mwanza na Wurzburg.

“Gari hili liliandaliwa kutokana na maofisa wa usalama kuliomba na hili agizo limetolewa katika mikoa yote ambako atafika, kwani katika kampeni anakuwa amekwenda hadi katika wilaya ambazo haina hospitali na ikitokea dharura akimbizwe haraka hospitali huku akiendelea kupatiwa matibabu” alieleza kiongozi huyo wa chama.

Hata hivyo, alisema gari hilo wao kama chama hawakuambiwa wala kuelekezwa kulilipia kwa vile ofisi ya mkoa ilisema watachukua wao katika hospitali ya Bugando, baada ya kuwasiliana na ofisi ya mganga mkuu wa mkoa.

CHANZO: Mwananchi

USHAURI: Imefika wakati sasa kukomesha uhuni huu wa CCM dhidi ya Watanzania hususan wale wasio wanachama wa chama hicho tawala.Matumizi yoyote ya mali za umma zinazogharamiwa na walipakodi pasipo kujali itikadi za vyama zao ni ubadhirifu wa wazi.Haitowezekana kuwa na uchaguzi huru na wa haki iwapo raslimali za taifa zinatumika kwa manufaa ya chama tawala,tena pasipo ridhaa ya walipakodi.Wito wa blogu hii kwa kila mpenda haki na usawa ni kuuweka wazi uhuni huu kwa dunia ili ifahamike mapema kuwa CCM inatengeneza mazingira ya kuhujumu uchaguzi mkuu ujao.

TUSIPOZIBA UFA TUTAJENGA UKUTA


1 Aug 2010

Taarifa zinaeleza kuwa msanii mkongwe wa muziki wa Bongoflava,Joseph Mbilinyi a.k.a Sugu,ameshinda kura za maoni za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema)kuwania nafasi ya kuogmbea ubunge wa jimbo la Mbeya Mjini.

Kila la heri Mr Sugu.Jitihada zako zinapaswa kuwa fundisho kubwa kwa idadi kubwa ya wasanii (hususan wa Bongoflava) ambao kwa wao photo-ops (kuuza sura) na watawala wetu is everything despite having been USED AND ABUSED by same watawala kila unapojiri uchaguzi.

That's wassup,Sugu!

29 Jul 2010

Ni dhahiri kwamba kila Mtanzania mzalendo na mwenye uchungu na nchi yetu anatamani kuona mambo yakibadilika huko nyumbani.Nchi yetu ina takriban miaka 50 tangu ipate uhuru mwaka 1961.Ukiondoa uvamizi wa nduli Idi Amin mwaka 1978-79,nchi yetu imeendelea kuwa na sifa ya kipekee ya amani na utulivu huku tukishuhudia "nyumba za majirani zetu zikiteketea".Chama tawala CCM kimekuwa kikijigamba kuwa amani na utulivu huo ni matokeo ya sera zake nzuri na uongozi uliotukuka.Haihitaji kuwa mwanafunzi wa siasa kama mie kufahamu kuwa amani na utulivu tulionao unasababishwa na uvumilivu wa Watanzania.Na ni uvumilivu huo huo unaowafanya CCM watuone wajinga,watupelekeshe watakavyo na waifilisi nchi yetu huku tukifahamu fika namna ya kuwadhibiti.Imetosha.Uvumilivu una mwisho,na mwisho huo ni sasa.

Na hata hilo suala la amani na utulivu lina utata kinamna flani.Wachambuzi wa siasa wanabainisha kuwa kutokuwa na machafuko au vita si viashiria kamili vya amani na utulivu.Hebu jiulize msomaji mpendwa,wazee wetu wastaafu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wana amani gani wakati fedha zao ziliibiwa na wajanja (mafisadi)  katika serikali ya CCM?Je wakulima wanaokopwa na vyama vya ushirika kila unapojiri msimu wa mavuno wana amani gani wakati wanashuhudia namna mavuno yao yanavyorutubisha vitambi vya mafisadi wa vyama vya ushirika?Mabaamedi wana amani gani katika mishahara ya kijungujiko wanayopewa (na inayokatwa kila siku kila glasi au chupa inapovunjika)?Watoto zetu au wadogo zetu wana amani gani wanaposoma kwenye shule zisizo na madawati huku walimu wao wakinyong'onyea kutokana na mazingira duni ya kazi?Na je watumishi wa umma wana amani gani ilhali wanapodai haki zao wanaishia kudharauliwa kuwa kura zao hazihitajiki (as if mishahara yao ni fadhila kwa kumchagua kiongozi)?

Na madereva wa daladala na mabasi ya mikoani wana amani gani ilhali askari wa usalama barabarani wanawakamua kila siku kana kwamba rushwa ni sehemu ya sheria za usalama barabarani?Na huko magerezani kuna Watanzania wangapi wasio na amani kwa vifungo vya kubambikizwa kesi,kushindwa kutoa rushwa kwa polisi au hakimu au uonevu pasipo sababu?Na dada na mabinti zetu wenye sifa stahili za kupata ajira wana amani gani ilhali kila wanapofanya maombi ya kazi wanakumbana na masharti ya "ngono kwanza,kisha ajira"?Na wagonjwa wetu wana amani gani wanapolazwa sakafuni katika wodi za hospitali mbalimbali (na hii ilimtoa machozi Supamodo Naomi Campbell)?

Mtanzania ana amani gani wakati kila siku anashuhudia namna nchi yake inavyozidi kuhujumiwa na mafisadi?Wanaoamini katika utawala wa sheria wana amani gani wanaposhuhudia mtu kama Lowassa anapewa air time kwenye televisheni ya taifa inayoendeshwa kwa fedha za walipa kodi (na mahijiano hayo hayafanyikii gerezani)?Yani fedha za walipa kodi zinatumika kusafisha watuhumiwa wa ufisadi!

Na walalahoi wana amani gani wanaposhuhudia serikali waliyoiweka madarakani,na iliyoahidi maisha bora kwa kila Mtanzania,ikielekeza nguvu kubwa katika kukumbatia mafisadi huku viongozi wa serikali hiyo wakiishi maisha ya kifahari kana kwamba Tanzania ni nchi ya "dunia ya kwanza"?Na wasafiri wanaotegemea huduma za Reli ya Kati au Tazara wana amani gani wakati usafiri wao unategemea kudra za Mwenyezi Mungu ?

Yapo mengi ya kueleza kuhusu namna CCM inavyofanya kila jitihada ya kubomoa hata kile kidogo kilichobaki kwenye "amani na utulivu".Ni dhahiri kuwa chama hiki kimevimbiwa madarakana na hakijali kuona Tanzania ikielekea kwenye korongo lenye kina kirefu.CCM inaweza kufanya kila hila ili ibaki madarakani kama ilivyowazuga Waislamu mwaka 2005 kuwa ingewapatia Mahakama ya Kadhi,lakini baada ya ushindi wa "kishindo" kwenye uchaguzi mkuu uliopita suala hilo limeendelea kuwa ngonjera tu huku akina Msekwa wakisema hili,Pinda akisema lile na Chikawe akiongea vile.Huku ni kuchochea vurugu.

Tanzania haiwezi kupiga hatua katika mfumo wa sasa wa kifisadi ambapo madaraka yanatolewa kwa minajili ya ushkaji huku watawala wakijiona miungu watu wenye uwezo wa kufanya watakayo hata kama yanapelekea kuhatarisha "amani na utulivu" wetu.

It's high time to say enough is enough.Na namna pekee ya kuwaadhibu CCM ni kuwanyima kura katika uchaguzi mkuu ujao.Binafsi,nina imani kubwa na Dokta Wilbroad Slaa,mgombea urais kwa tiketi ya Chadema.Ameonyesha ukomavu wa hali ya juu katika kutetea hali zetu na kupambana kwa dhati dhidi ya ufisadi.Nafasi adimu kama hizi huwa hazijirudii.Tukifanya kosa la kuiacha CCM madarakani hapo Oktoba tutaishia kujilaumu.Nia tunayo,sababu tunazo (tena elfu kidogo) na uwezo tunao (siku ya kupiga kura).Mnaopewa rushwa ili muichague CCM pokeeni kwa vile rushwa hiyo ni fedha mlizoibiwa.Wato rushwa hao hawana uwezo wa kushinikiza muwapigie kura hasa ikizingatiwa kuwa hamkuwaomba wawahonge na wanachowanhonga is in fact fedha zenu wanazowaibia kwa ufisadi.

Inawezekana ukitimiza wajibu wako

9 Apr 2010

JK alisaini sheria hiyo kwa mbwembe kama alivyoahidi.Siku chache baadaye,Dkt Wilboard Slaa akaibua hoja kuhusu 'usanii' uliofanyika kuongeza vipengere katika Sheria hiyo.Spika na Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakatetea 'usanii' huo.Licha ya mlolongo wa matukio hayo kuashiria kuwa sheria hii yenye nia njema itabaki kuwa maandishi tu,walengwa wakuu wa sheria hiyo wameamua kuipuuza na 'misaada' inatolewa kama kawaida katika kujitengenezea mazingira ya ushindi kwenye uchaguzi. Dk. Nkya kujitosa ubunge Morogoro Kusini Mashariki

na Joseph Malembeka, Morogoro

NAIBU Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Dk. Lucy Nkya, ametangaza nia ya kuwania ubunge katika jimbo la Morogoro Kusini Mashariki.
Dk. Nkya alitangaza nia hiyo akiwa katika ziara ya kukagua maenndeleo na utekelezaji wa ahadi alizotoa baada ya kuchanguliwa kuwa mbunge wa Viti Maalum.

“Nawatakeni wanachama wenzangu ndani ya CCM muelewe kuwa na mimi nakuja huku mbali na kuwa kuna wenzangu waliotangaza nia hii,” alisema Dk.Nkya.

Dk. Nkya ambaye kwa nyakati tofauti alikabidhi vitu mbalimbali yakiwemo mabati, vipaza sauti, saruji, vyerehani, misumari, baiskeli na fedha taslimu sh 1,500,000 kwa wananchi na wana CCM katika kata mbalimbali aliwataka wana CCM kukiimarisha chama na wao kiuchumi.

“Sasa hivi tunakwenda kwenye hekaheka za uchaguzi ila nawatakeni mbali na siasa jiimarisheni kiuchumi kwa kulima mazao yanayokomaa kwa muda mfupi na yanayostahimili ukame tuepukane na janga la njaa,” alitahadharisha Dk. Nkya.

Dk. Lucy Nkya anakuwa miongoni mwa watu saba walioonyesha nia ya kuwania ubunge katika jimbo hilo. Wengine ni mbunge wa sasa wa jimbo hilo (Samir Lotto), Jamira Mohamed, Amani Mwenigoha, Gabriel Mkwawe, Semindu Pawa na Salumu Salum Mkangala.

CHANZO: Tanzania Daima.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.