30 Apr 2015



“KAKA, kinachotokea hapa kilitarajiwa...na ilikuwa suala la ‘when’ na sio if”, hii ni kauli ya rafiki yangu mmoja Mwafrika Kusini baada ya kumuuliza kuhusu vurugu dhidi ya wahamiaji katika nchi hiyo ambazo zimesababisha vifo, majeruhi, wahamiaji kuhifadhiwa katika kambi kama wakimbizi na wengine kadhaa kuondoka nchini humo.
Ni suala la kusikitisha sana kuona taifa lililoweka historia duniani kwa kukabiliana na makaburu na mfumo wao wa ubaguzi wa rangi (Apartheid) na hatimaye kuushinda, linageuka kuwa taifa hatari dhidi ya wahamiaji kutoka nchi nyingine za Afrika.
Lakini kama alivyotanabaisha rafiki yangu niliyemnukuu hapo mwanzoni, matarajio makubwa waliyokuwa nayo Waafrika weusi nchini Afrika Kusini baada ya kumalizika kwa mfumo wa kibaguzi wa makaburu yameendelea kuwa ndoto tu kwa wengi wao. Uzoefu unaonyesha kuwa katika jamii yoyote ile kwa kadiri inavyokabiliwa na matarajio makubwa ambayo ni magumu kufikiwa, moja ya waathirika wa hali hiyo ni wahamiaji.
Pengine mfano mzuri ni huku nchi za Magharibi ambapo baada ya kuyumba kwa uchumi wa dunia, hali ya maisha imekuwa ngumu, na kauli za upinzani dhidi ya wahamiaji- kutoka kwa wanasiasa na hata raia wa kawaida- zimesambaa.
Kwa hapa Uingereza ambapo tunatarajia kufanya Uchaguzi Mkuu Mei 7, mwaka huu, moja ya mada kubwa kwa wanasiasa imekuwa suala la uhamiaji. Wanasiasa wanalazimika aidha kukabiliana na wanasiasa wenzao wanaolaumu kuwa wahamiaji wanachangia hali mbaya ya uchumi au kuonekana wanajali vilio vya wananchi wenye malalamiko ya aina hiyo.
Ni kwa sababu hiyo, chama cha kibaguzi cha UKIP kinachoongozwa na Nigel Farage kimetokea kujipatia umaarufu mkubwa hasa kwa vile kinabainisha waziwazi ‘chuki’ yake dhidi ya wahamiaji. Huko Ufaransa, chama cha kibaguzi cha National Front nacho kimekuwa maarufu kutokana na msimamo wake mkali dhidi ya wahamiaji. Hali ipo hivyo pia nchini Italia na Udachi, huku Ujerumani ikishuhudia mashambulizi ya mara kwa mara dhidi ya wahamiaji. Kimsingi, katika nchi nyingi za Magharibi, kuyumba kwa uchumi wa dunia kumeambatana na kuimarika kwa vyama vya mrengo mkali wa kulia (far right) ambavyo kimsingi ni vya kibaguzi na vinapinga vikali wahamiaji. Vile vile, sauti za wananchi wa kawaida kuzitaka serikali zao kudhibiti ujio wa wahamiaji zimekuwa zikiimarika na kuongezeka.
Tukirejea kinachojiri Afrika Kusini, ni rahisi kuwashutumu wenzetu hao kwa vitendo vya ubaguzi dhidi ya wahamiaji hasa ikizingatiwa kuwa baadhi ya waathirika wa vurugu dhidi ya wahamiaji ni raia wa nchi zilizoisaidia Afrika Kusini kwa kiwango kikubwa katika mapambano dhidi ya mfumo wa kibaguzi wa Makaburu. Ni rahisi pia kuwalaumu kwa sababu hata kama ingekuwa kweli kuwa wahamiaji wanasababisha ukosefu wa ajira kwa ‘wazawa’ bado haikubaliki kuwafanyia vurugu, kuwajeruhi na hata kuwauwa. Hilo halikubaliki hata chembe.
Hata hivyo, busara kidogo tu zapaswa kutukumbusha kuwa ni vigumu ‘kuingiza akili’ kichwani mwa mtu mwenye njaa (masikini). Tumbo lina tabia moja: mara nyingi, linapohitaji chakula halina subira, au busara. Linachohitaji ni chakula tu, na mara nyingi halijali chakula hicho kinapatikana kwa njia zinazokubalika au la. Ushuhuda wa hili ni katika msimu wa uchaguzi huko nyumbani ambapo mara kadhaa tunashuhudia watu wazima na akili zao wakifungiwa sehemu au kusafirishwa kama magunia kutoka sehemu moja au nyingine ili ‘kulinda kura za mgombea’ kama si kumhakikishia ushindi. Wanaodhalilishwa hawafanyi hivyo kwa mahaba ya kisiasa bali njaa zao.
Mie ni miongoni mwa waumini wa kanuni isiyo rasmi kuhusu uhusiano kati ya umasikini na fursa za uongozi wa kisiasa. Kwamba, watawala hawafanyi bidii kukabiliana vya kutosha na umasikini kwa sababu umasikini unawapa fursa ya kuwahadaa wapiga kura na hatimaye kuwanunua kwa urahisi. Umasikini wa wapigakura ni mtaji mzuri kwa wanasiasa wenye fedha za kununua kura.
Ni vigumu kumkumbusha mpiga kura kuwa ‘ah huyu mbunge alitoa ahadi kadhaa katika uchaguzi uliopita lakini wala hatujamsikia akisema lolote huko bungeni. Hatujawahi japo kuona picha zake akiwa bungeni,’ pale mwanasiasa husika ana rundo la fedha za kutuliza njaa za wapigakura.
Doti za khanga, pishi za mchele, kilo za sukari na ‘takrima’ kama hizo humlainisha mpigakura mwenye njaa asahau kabisa kuhusu miaka mitano ijayo ya utapeli wa kisiasa kama ilivyotokea miaka mitano iliyopita. Njaa yahitaji mlo, hayo madhara yatajulikana mbele ya safari. “Kwani akiwa mbunge tena nitakufa?” Wanajipa moyo wapigakura wenye njaa wanaosubiri kwa hamu ‘fadhila’ za mgombea.
Kwa Afrika Kusini, sababu kubwa ya chuki dhidi ya wahamiaji ni matatizo mbalimbali yanayowakabili Weusi nchini humo ambayo yanakinzana na matarajio makubwa waliyonayo kutoka kwa utawala wa ‘Waafrika wenzao’ baada ya ‘kuwapora madaraka’ makaburu.
Lakini kibaya zaidi, ni mchanyato wa umasikini, ukosefu wa elimu na ‘dozi’ ya uchochezi. Moja ya vichocheo vya vurugu dhidi ya wahamiaji nchini humo ni kauli iliyotolewa na Chifu wa Wazulu, Goodwill Zwelithini, dhidi ya kufurika kwa wahamiaji nchini humo. Kana kwamba hiyo haitoshi, mtoto wa Rais Jacob Zuma, Edward, amekuwa mstari wa mbele kuhamasisha wahamiaji wafukuzwe nchini humo akidai wanachangia uhalifu na hali ngumu ya uchumi. Kadhalika, wanasiasa kadhaa Weusi pia wamekuwa wakitoa kauli za kuchochea chuki dhidi ya wahamiaji.

Chambuzi mbalimbali zilizofanyika kabla na baada ya vurugu hizo dhidi ya wahamiaji zimeonyesha kuwa sio tu idadi ya wahamiaji ni ndogo mno kuathiri uchumi wa Afrika Kusini bali pia kinachofanya soko la ajira nchini humo kuvutia na kuvuta wafanyakazi kutoka nchi nyingine ni ukweli kuwa ‘ni rahisi kwa mzawa kuishi bila kazi kwa vile anapatiwa msaada na serikali’ ilhali kwa mhamiaji ni lazima afanye kazi au biashara ili aweze kumudu gharama za maisha.
Lakini pia, huko nyuma, Rais Jacob Zuma aliwahi kunukuliwa akiwalaumu Waafrika Kusini weusi kwa ‘uvivu,’ kutegemea serikali iwapatie kila kitu badala ya kujishughulisha wenyewe. Sasa kwa vile takribani katika kila nchi inayomudu kuwasaidia raia wake wasio na kazi, msaada wa serikali huwa ni wa kujikimu tu, haishangazi kuona ‘wazawa’ wakiwachukia wahamiaji wanaojituma kwa biashara na ajira na kujipatia kipato cha zaidi ya kujikimu tu
Kwa mtazamo mpana, na hili ni funzo kwa nchi nyingine za Afrika ikiwa pamoja na Tanzania yetu, ni ukweli kwamba umasikini ni bomu linalosubiri muda wa kulipuka. Kwa nchi yetu, hali si nzuri. Sio tu kwamba umasikini unazidi kushamiri na kuongezeka, vitendo vya ufisadi vinavyofanywa na baadhi ya watawala wetu vinakuwa kama ‘kuchoma kisu kwenye jeraha bichi.’ Haiingii akilini kwa mlalahoi ambaye hana uhakika wa mlo ujao kusikia viongozi fulani wamekwapua mabilioni ya shilingi huko Benki Kuu.
Na wakati faraja ya masikini inaweza kupatikana katika neno la Mungu, mtu fukara anaposikia habari kuwa Askofu wake kuzawadiwa mamilioni ya ufisadi, anaweza kushawishika kutumia vibaya msemo wa ‘mtaji wa masikini ni nguvu zake mwenyewe,’ hasa ikizingatiwa kuwa nguvu anazotumia shambani zinaishia kunenepesha kitambi cha viongozi wa vyama vya ushirika na kuongeza idadi ya ‘nyumba ndogo’ zao. Kwanini asishawishike kuzitumia nguvu hizo kwenye uhalifu?
Tofauti na Afrika Kusini ambapo ‘adui’ anaonekana mhamiaji ‘anayepora ajira za wazawa,’ adui wa fukara wa Tanzania ni Mtanzania mwenzie anayetumia madaraka yake kufanya ufisadi, na hivyo kuongeza ufukara kwa mlalahoi huyo.
Tunaweza kujidanganya kuwa ‘Tanzania ni kisiwa cha amani’ lakini tusisahau kuwa ‘mwenye njaa hana amani.’ Amani yetu ni ya kufikirika zaidi kuliko uhalisia. Amani si ukosefu wa mapigano tu bali pia kuridhika nafsini, tumbo lililoshiba, mfuko wenye hela ya matumizi, jitihada za kujipatia kipato halali zinapozaa matokeo tarajiwa. Kimsingi, ukosefu wa amani usioambatana na vurugu ni kichocheo kikubwa cha vurugu zinazopelekea kuvunja amani waziwazi. Na hicho ndicho kinachojiri nchini Afrika Kusini. Sio sahihi lakini nenda kamwambie mwenye njaa kuhusu ‘wewe kuwa na njaa ilhali mie ninakula hadi kusaza ni kitu sahihi’ kama atakuelewa. Wanasema ‘njaa haina akili,’ na mwenye njaa yupo tayari kwa lolote ili kutuliza njaa yake.
Nimalizie makala hii kwa kutoa rai kwa wanasiasa wetu, hasa wakati huu tunapoelekea kwenye Uchaguzi Mkuu, kuweka kipaumbele katika kupambana na umasikini sambamba na kukabiliana na ufisadi ambao kwa kiasi kikubwa unachangia mno kushamiri na kukua kwa umasikini.
TUZIPOZIBA UFA TUTAJENGA UKUTA

29 Apr 2015

Inasikitisha, inaumiza, inashangaza, na inaacha maswali mengi kuliko majibu kila tunaposikia “ajali yauwa...ajali yajeruhi...” Ndio, matukio ya ajali huko nyumbani yamekuwa kama jambo la kawaida kutokana na mfululizo wake, lakini hali ilivyo sasa ni ya kutisha.
Huko nyuma niliandika takriban makala mbili kuhusu suala hili la ajali, sio tu kwa vile tukio lolote linalopelekea kupotea kwa uhai wa wenzetu linaumiza nafsi bali pia kutokana na ukweli kwamba kwa hapa Uingereza ajali ndogo tu ni tukio linalokamata hisia za takriban nchi nzima, kinyume na ilivyozoeleka huko nyumbani.

Wakati ajali zinaendelea kuteketeza maisha ya Watanzania wenzetu, angalau kwa mara ya kwanza Taifa linaonekana kuguswa, na tayari zimeanza harakati za uhamasishaji dhidi ya ajali katika mitandao mbalimbali ya kijamii. Hata hivyo, ukweli mchungu unabaki kuwa ajali bado zinaonekana kama matukio ya kawaida tu.
Sijui lini taifa limeonyesha kuguswa na vifo vilivyotokana na ajali kiasi cha angalau bendera kupepea nusu mlingoti. Sijui sababu ni kwamba ajali zimezoeleka mno, au kwa vile ‘ajali haina kinga,’ au kwa sababu wahanga wengi wa ajali za barabarani ni ‘watu wa kawaida.’
Kabla sijaanza kuandika makala hii nilisoma habari kuhusu vurugu zilizotokea huko Korea ya Kusini katika maadhimisho ya mwaka mmoja tangu itokee ajali mbaya ya feri iliyosababisha vifo takriban 300. Hakuna anayefahamu kinachojiri baada ya kifo, lakini yayumkinika kuamini kuwa marehemu wasingependa kukumbukwa kwa vurugu. Lakini vurugu zilizotokea huko Korea ya Kusini ni ishara ya wananchi kukerwa na jinsi serikali yao ilivyoshughulikia janga hilo, hata kama haikuisababisha.
Hapa simaanishi kwamba Watanzania nao waingie mtaani na kufanya vurugu kuisukuma serikali ichukue hatua stahili dhidi ya ajali. Hata hivyo, ni muhimu angalau kuiamsha serikali kwa kuifahamisha kuwa hatuwezi kuangalia tu maisha ya Watanzania yakiteketea kama hayana thamani kutokana na mfululizo wa ajali. Busara kwamba ‘ajali haina kinga’ hai-apply katika nyingi ya ajali zinazotokea huko nyumbani.
Kwa mtizamo wangu, chanzo kikubwa cha ajali ni rushwa. Rushwa inayowezesha madereva wasio na sifa kuwa barabarani huku wakihatarisha uhai wa abiria wao. Rushwa inayoruhusu magari mabovu yabebe abiria na kuweka rehani uhai wa abiria. Rushwa inayofumbia macho makosa ya madereva barabarani na hivyo kuwapa imani kuwa hakuna kitu kiitwacho ‘kosa kinyume cha sheria za usalama barabarani’ alimradi dereva ana uwezo wa ‘kumpoza’ askari wa usalama barabarani.
Wanasema ‘rushwa huuwa.’ Na katika janga hili la mfululizo wa ajali, rushwa inauwa kweli kweli, na inaendelea kugharimu maisha ya Watanzania wenzetu kila kukicha.
Rushwa imekuwa sehemu ya maisha ya kawaida ya Mtanzania, na sintoshangaa iwapo baadhi ya wasomaji ‘wataniona mtu wa ajabu’ kwa kuhitimisha kuwa rushwa ni chanzo kikuu cha ajali huko nyumbani. Kwa wengi, rushwa ni tukio la muda mfupi tu linalorahisisha au kuwezesha upatikanaji wa huduma au bidhaa. Hata hivyo, ukweli mchungu ni kwamba rushwa ni kama kansa, inaitafuna jamii taratibu, na siku ya siku, madhara yake makubwa hujitokeza hadharani.
Mfano mmoja kuhusu athari za rushwa ni suala la ugaidi nchini Kenya. Wachambuzi wa masuala ya usalama wanahitimisha kuwa kwa kiasi kikubwa tu, rushwa katika vyombo vya dola nchini Kenya imewarahisishia magaidi wa Al-Shabaab kutimiza malengo yao kuishambulia nchi hiyo.
Kwa huko nyumbani tumeshuhudia matatizo mengine ya kijamii yanavyorutubishwa na rushwa. Mfano rahisi ni kushamiri kwa biashara ya madawa ya kulevya. Tanzania yetu sasa ni miongoni mwa vituo vikuu vya biashara hiyo duniani, na kilichotufikisha katika nafasi hiyo isiyopendeza hata kidogo ni urahisi wa kuingiza na kutoa madawa ya kulevya nchini mwetu. Niwe mkweli, kila ninaposikia polisi wamekamata kiasi fulani cha madawa ya kulevya, hisia yangu ya kwanza ni madawa hayo yaliyokamatwa yataishia kumnufaisha mtendaji fulani wa taasisi zenye wajibu wa kuyadhibiti.
Takriban kila dereva na abiria anafahamu jinsi askari wa usalama barabarani walivyogeuza rushwa kuwa haki yao. Kibaya zaidi, madereva wengi nao wamejenga fikra kuwa kutoa rushwa kwa askari wa usalama barabarani ni wajibu wao. Hili ni janga: rushwa kama haki wa wapokeaji na wajibu kwa watoaji.
Wakati mmoja nikiwa safarini huko nyumbani, basi nililopanda lilisimamishwa na askari wa usalama barabarani, na baada ya dakika kadhaa, baadhi ya abiria walisikika wakimhasisha dereva ‘amalizane na trafiki’ (ampe rushwa) ili safari iendelee. Hivi ndivyo rushwa ilivyoota mizizi katika Tanzania yetu.
Kwa upande mwingine, janga la ajali kuonekana kama jambo la kawaida tu ni mwendelezo wa kasumba inayolikwamisha mno taifa letu: kuzowea matatizo. Angalia tatizo la mgao wa umeme lilivyodumu miaka nenda miaka rudi pasipo Watanzania kutumia nguvu ya umma kuilazimisha serikali na Tanesco yake imalize tatizo hilo. Mgao wa umeme umekuwa stahili ya Watanzania, na kikubwa wanachoweza kufanya ni kuitukana Tanesco matusi yasiyoandikika hapa, kana kwamba matusi hayo yatamaliza tatizo hilo la miaka nenda miaka rudi.
Kwenye sekta ya huduma, hali ni hivyohivyo. Ukifuatilia kwenye mitandao ya jamii, idadi ya matusi yanayoelekezwa kwa makampuni ya huduma mbalimbali, kwa mfano makampuni ya simu, ni kubwa na inakua kila siku, lakini ‘mashujaa hao wa matusi’ hawataki kabisa kujifunza kuwa matusi yao hayabadili chochote, na ndio maana kila kukicha inawalazimu waje na matusi mapya kama si kuyarudia yale ya zamani.
Lakini kwa hali ilivyo sasa kuhusu janga la ajali, ‘usugu’ huo wa kuyazowea matatizo inabidi ifikie kikomo. Taifa lolote linalojali mustakabali wake lazima liamke inapofikia hatua ya watu 969 kupoteza maisha kutokana na ajali katika kipindi cha takriban miezi mitatu tu. Naam, tangu mwaka huu uanze, tumepoteza wenzetu takriban 300 kila mwezi kutokana na ajali, kwa mujibu wa takwimu zilizopatikana wiki iliyopita.
Katika sehemu kubwa ya makala hii nimezungumzia rushwa kama chanzo kikuu cha janga la ajali. Hata hivyo, kwa mtizamo wangu, kingine kinachochangia baadhi ya ajali ni ‘uzembe’ wa wengi wa abiria: kukaa kimya pale madereva wanapohatarisha maisha ya abiria kwa uendeshaji usiozingatia sheria za usalama barabarani. Na pengine cha kukera zaidi ni tabia iliyojengeka miongoni mwa abiria wengi kuwasifia madereva wanaodhani ni kosa la jinai kuendesha motokaa taratibu hata kwenye eneo hatari.
Inasikitisha na kuchukiza kusikia abiria wakimshangilia dereva anayeendesha basi kwa kasi au ku-overtake gari jingine pasi kuona kama kuna gari jingine linakuja kwa mbele au la. Dereva anayeshangiliwa kwa uendeshaji gari wa hatari anajenga imani kwamba huo ndio udereva stahili, vinginevyo abiria wangemkemea.
Ifike mahali Watanzania tuache kukubali kilicho pungufu (not settling for less). Ukinunua tiketi kwa ajili ya safari umenunua pia haki na stahili zako ambazo kamwe hupaswi kumruhusu dereva azichezee. Ni wazi kuwa umoja na mshikamano wa abiria kukemea madereva wanaokiuka sheria za usalama barabarani unaweza kusaidia kupunguza baadhi ya ajali zinazoepukika.
Nimalizie makala hii kwa kutoa salamu zangu za rambirambi kwa ndugu na jamaa wa Watanzania wenzetu waliopoteza maisha katika ajali mfululizo.
Pia ninaomba kufikisha ujumbe huu kwa askari wa usalama barabarani: kila shilingi mnayodai kama rushwa ili kufumbia macho ukiukwaji wa sheria za barabarani inachangia ajali na vifo vya Watanzania wenzetu. Mikono ya kila askari aliyepokea rushwa na kisha gari husika likapata ajali ina damu ya waliokufa katika ajali husika.
Kadhalika, ninatoa wito kwa madereva, hususan wa magari ya abiria, kuthamini uhai wa abiria wao, kwa kuepusha ushindani hatari barabarani, mwendo kasi na kuheshimu sheria za usalama barabarani.
Lakini kubwa zaidi kwa Watanzania wote ni kupambana na kansa hii ya rushwa ambayo sasa inalitafuna taifa kwa kuchangia ajali hizi mfululizo, kama inavyosababisha madhara mengine makubwa katika nyanja mbalimbali za maisha.

ANGALIZO: Makala hii ilichapishwa katika toleo la tarehe 22.04.15 lakini iliwekwa mtandaoni juzi. Samahani kwa kuchelewesha kui-post.


26 Apr 2015

Embedded image permalink
Moja ya taarifa zilizozagaa kwenye vyombo mbalimbali vya habari ni kuhusu kushuka kwa thamani ya shilingi.Lakini shilingi au sarafu nyingine inashukaje thamani yake? Haya ni maswali ambayo ninaamini watu wengi wasio wachumi watakuwa wanajiuliza muda huu.

Nami pia ninajiuliza maswali hayo kama yalivyo kwenye kichwa cha habari.Ninajiuliza kwa sababu mie si mchumi, na jaribio langu pekee la kuingia fani ya uchumi lilikuwa wakati napata elimu ya sekondaria ambapo nilisoma Book Keeping hadi kidato cha nne na Commerce hadi kidato cha pili.

Naujua uchumi 'kijuu-juu' tu, na sana ni katika mahusiano yake na siasa au jamii, lakini kwa vile mie ni dhaifu sana wa hisabati, uchumi unaohusisha tarakimu ni 'no-go area.'

Kwahiyo, samahani msomaji mpendwa kama maswali hayo kwenye kichwa cha habari yalikupa hisia kwamba labda nitayajibu. Hapana. Ni maswali ninayotaka yapatiwe majibu na serikali au/na wataalamu wa masuala ya uchumi.

Kwa sie tunaoishi nje ya Tanzania, dalili kuu ya kushuka kwa thamani ya shilingi yetu ni pale tunapotuma fedha nyumbani kusaidia ndugu na jamaa zetu. Huo ndio muda unatulazimisha kufahamu viwango vya kubadilishia fedha. Kwahiyo kama ninataka kutuma shilingi laki kadhaa za Kitanzania, inanilazimu kufahamu ninatakiwa kutuma paundi za Kiingereza ngapi.Sasa kwa vile zoezi hili la kutuma misaada nyumbani ni la mara kwa mara, inakuwa rahisi kutambua kama 'shilingi ipo imara au imeyumba,' kwa maana kwamba unalinganisha, kwa mfano, "kutuma shilingi laki nne mwezi uliopita ilinigharimu takriban paundi mia na sitini, lakini safari hii imenigharimu paundi laki na arobaini."

Je Mtanzania wa kawaida anafahamu vipi kuhusu kuporomoka kwa thamani ya shilingi wakati hana sarafu ya kigeni ya kufanya mlinganisho? Na sio tu kufahamu kama thamani ya shilingi imepanda au imeshuka, lakini pia anapaswa kujua kama ina athari zozote kwake.

Kidogo ninachoelewa ni kwamba kuporomoka kwa shilingi kunaweza kuwa na 'faida' flani. Wanadai thamani ya sarafu ikishuka, bei ya bidhaa za nchi husika katika masoko ya kimataifa inashuka pia.Kushuka huko kwaweza kuwasukuma wanunuzi katika masoko hayo 'kuchangamkia tenda,' na hiyo inaweza kupelekea nchi kuuza mazao yake kwa wingi, na wakati huohuo hiyo inaweza kuhamasisha wakulima wa mazao au wauza bidhaa za export kuongoze uzalishaji. Sina uhakika sana kuhusu hilo kwa vile kama nilivyotanabaisha hapo juu, mie ni mbumbumbu wa uchumi.Sina A wala B ninalojua katika eneo hili.

Nimalizie makala hii kwa kutoa changamoto kwa serikali sio tu kuwafahamisha wananchi kuhusu kushuka kwa thamani ya shilingi yetu bali pia kueleza sababu za kushuka huko na athari au faida zake kwa Mtanzania. Kadhalika, ninatoa changamoto kwa wataalamu wetu wa uchumi kuisaidia jamii kwa kutupa somo kuhusu suala hili.Na nitumie fursa hii kumkaribisha mtaalam yeyote kunitumia makala kuhusu suala hjilo nami nitaichapisha hapa bloguni au kuituma kwa jarida la RAIA MWEMA ninaloandikia makala kila wiki.

23 Apr 2015


Unapoingia mtandaoni kwa minajili ya ku-search kitu, uwezekano mkubwa utaenda kwenye mtambo wa kutafuta habari (search engine) wa Google. Sasa, kwenye mtandao huo, ukiingiza neno pale kwenye kiboksi cha kutafutia habari, wenyewe utaanza kubashiri maneno kulingana na herufi husika zinavyotengeneza neno. Mfano rahisi ni huo pichani juu.Ukitafuta 'What is Tanzania..." kabla hujamaliza, Google itaanza kukupa ubashiri wa unachotafuta. Kitu hicho kinajulikana kama Google autocomplete

Sasa hapa chini ni ramani ya dunia kwa mujibu wa Google autocmplete. Yaani ramani hiyo ya dunia, na kama ilivyogawanywa kwa kila bara ni kwa mujibu wa jinsi watu wanavyo-search habari kuhusu nchi husika. Kwa mfano autocomplete searches nyingi kuhusu Canada ni passport, kwa Brazil ni makahaba...na kwa Tanzania yetu ni SAFARI...Well, sio BIA YA SAFARI bali safari za utalii.


Null


Null



Null

Null

Null

CHANZO: i100


18 Apr 2015

KWA siku kadhaa sasa kumekuwa na mjadala mkali, hususani katika mitandao mbalimbali ya kijamii kuhusu sheria mpya ya kukabiliana na uhalifu wa mtandaoni (Cyber Crime Act 2015).


Kabla ya kuuzungumzia mjadala huo, ningependa kumpongeza Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, kwa kufanya tukio la kihistoria la kuuweka hadharani muswada husika katika mtandao wa kijamii wa Twitter ili ujadiliwe.
Ninatambua kuna uwezekano wa baadhi ya watu kudai haistahili pongezi kwa sababu, kwanza hilo ni jukumu la kila mtendaji wa serikali, na pili, kuleta muswada huo siku chache kabla haujawasilishwa kwa hati ya dharura Bungeni kusingewapa wadau nafasi ya kutosha kuujadili.



Katika hilo la kwanza, ni muhimu tutambue kuwa Tanzania yetu ya sasa imefikia mahala ambapo kiongozi akitimiza wajibu wake anastahili kupongezwa kwani hata asipotimiza wajibu anaolipwa mshahara kuutekeleza hatoathirika. Ni wazi basi, hata kama January angeamua kutouweka muswada huo hadharani, isingemwathiri lolote.



Kuhusu muswada huo kuwasilishwa kwa hati ya dharura, ninaafikiana na wanaolalamikia hatua hiyo kwa sababu licha ya dhamira nzuri na umuhimu wa kuwa na sheria ya kudhibiti uhalifu wa mtandaoni, bado kulikuwa na haja ya wananchi kupewa elimu ya kutosha kuhusu masuala kadhaa, hasa ikizingatiwa kuwa Watanzania wengi bado ni ‘wageni’ katika masuala ya mtandao (wa intaneti.)



Na pengine kabla ya kuingia kwa undani katika kuzungumzia mjadala huo na muswada huo ambao ulipitishwa na bunge na hadi wakati ninaandika makala hii ulikuwa ukisubiri kuidhinishwa na Rais Jakaya Kikwete ili uwe sheria kamili, ni muhimu kuweka wazi msimamo wangu kwamba ninaunga mkono muswada na sheria husika.



Ninaunga mkono kwa sababu kuu tatu: kitaaluma/kitaalamu, kijamii na binafsi. Kwa upande wa kitaaluma/kitaalamu, huko nyuma niliwahi kufanya kazi katika sekta ya usalama, na kwa muda mrefu nimekuwa nikijihusisha na stadi zinazohusu sekta hiyo.



Kwa hiyo, utaalamu na uelewa nilionao, unanisukuma kuunga mkono haja ya, na umuhimu wa kuwa na sheria ya kukabiliana na uhalifu wa mtandaoni.



Kwa kifupi tu, pamoja na faida zake nyingi, mtandao unaweza na umeshaweza kutumika vibaya na kusababisha madhara makubwa.



Pamoja na kurahisisha mawasiliano na kufanikiwa kuiunganisha dunia na kuwa kama kijiji (ninaandika makala hii nikiwa hapa Uskochi, na nikimaliza na kubonyeza ‘send’ inamfikia mhariri wa gazeti hili muda huohuo, tofauti na njia za zamani ambapo ingelazimu kutuma makala hii kwa barua, na kuchukua siku kadhaa njiani), mtandao umekuwa kichaka cha maovu hasa kutokana na teknolojia husika kuwezesha mawasiliano pasipo watu kukutana ana kwa ana.



Kwa mfano, wakati kabla ya ujio wa teknolojia ya mtandao, ilikuwa vigumu kwa ‘mwizi’ kuiba fedha za mwenye akaunti benki bila kufika katika benki husika (au kuziiba wakati mwenye akaunti anaenda kuweka fedha hizo au kuzichukua benki), kwa sasa teknolojia ya mtandao inamwezesha mwizi aliyepo hata mbali na benki au mwenye akaunti kuziiba fedha hizo. Japo pengine hili halijashamiri sana huko nyumbani, ukweli ni kwamba wizi wa aina hiyo umetawala sehemu mbalimbali duniani.



Lakini kiusalama, mtandao umetokea kuwa moja ya nyenzo muhimu za magaidi, ambavyo vikundi maarufu vya kigaidi duniani kama Al-Qaeda, ISIS, Boko Haram na Al-Shabaab, vimekuwa vikiutumia vyema mtandao katika harakati zao dhalimu za ugaidi.



Katika tukio linaloweza kuonekana la kufikirika tu, magaidi wanaweza kutumia mitandao ya kijamii au hata ‘Whatsapp’ kusambaza ujumbe unaoweza kutishia amani na kusababisha madhara makubwa.



Sheria ya kukabiliana na uhalifu wa mtandaoni imekuja wakati mwafaka hasa kwa kuzingatia uwepo wa taarifa zinazoashiria tishio la ugaidi, kufuatilia shambulio la kigaidi lililofanywa hivi karibuni na magaidi wa Al-Shabaab huko Garissa, nchini Kenya na kusababisha vifo takriban 150.



Ninathamini sana haki za raia kuwasiliana pasipo hofu ya serikali au taasisi zake za usalama kuyafuatilia mawasiliano yao, lakini pia ninatambua kuwa ili serikali iweze kutekeleza jukumu lake la kulinda usalama wa raia, inalazimika kufahamu mawasiliano yasiyo na nia nzuri kwa taifa letu.



Katika zama hizi hatari tunazoishi, ni vigumu mno kupata uwiano stahili kati ya uhuru na sheria kwani wahalifu wanaweza kuutumia uhuru huo kwa dhamira mbaya inayoweza kupelekea raia wasiweza kuutumia uhuru wao vyema.



Kijamii, Tanzania yetu imefika mahala pabaya, angalau huko kwenye mitandao ya kijamii. Na kama kuna sehemu inayoweka ushahidi wa wazi kuhusu hicho ninachoongelea, basi ni kwenye mtandao wa kijamii unaohusu picha, Instagram, ambao kadri siku zinavyozidi kwenda ndivyo unavyozidi kuwa uwanja wa matusi na kila lisilopendeza machoni.



Kwa upande wa blogu, licha ya kuwa bado tuna blogu nyingi zinazoitumikia jamii ipasavyo, kumeibuka utitiri wa blogu za ngono na matusi huku nyingine zikijipa uhuru wa kuwachafua watu na kuwasababishia madhara makubwa katika maisha yao. Ilikuwa lazima tufike mahala tuseme ‘sasa yatosha.’ Hakuna uhuru usioambatana na kuzingatia wajibu.



Mwaka jana, binti mmoja wa Kitanzania alikumbana na madhila ya unyanyasaji mkubwa katika mtandao wa kijamii wa Twitter, na siku chache baadaye alikutwa amekufa. Japo hakuna uthibitisho wa moja kwa moja kati ya unyanyasaji huo wa mtandaoni na kifo cha binti huyo, yayumkinika kuhisi kuwa matukio hayo mawili yalikuwa na uhusiano japo hata kama ni wa mbali. Na baada ya tukio hilo la kusikitisha, zilisikika kelele mbalimbali za kuitaka serikali ichukue hatua madhubuti kukabiliana na unyanyasaji wa mtandaoni (cyber bullying).



Sababu yangu ya tatu ya kuunga mkono sheria hiyo ya kupambana na uhalifu wa mtandaoni ni ya binafsi. Baada ya kifo cha binti huyo, nilisimama kidete na baadhi ya wanaharakati wa haki za jamii kuhamasisha mapambano dhidi ya unyanyasaji wa mtandaoni, kosa ambalo ni sehemu ya uhalifu wa mtandaoni.



Katika hali ya kushangaza na kusikitisha, liliibuka kundi lililoanzisha mashambulizi makali dhidi yetu tuliokuwa tukikemea vitendo vya unyanyasaji wa mtandaoni. Binafsi, niliandamwa hadi kiasi cha kuitwa muuaji hadharani, jambo ambalo linaniumiza nafsi hadi muda huu. Nilishindwa kabisa kuelewa kwanini dhamira nzuri ya kukemea maovu igeuke kuwa kosa lililowaudhi watu hao.



Naomba ieleweke kuwa sababu hii ya tatu ni ya binafsi na ningesihi isiangaliwe pekee bali pamoja na hizo mbili niliotaja hapo awali, ili isilete hisia kuwa mimi ni mbinafsi ninayeunga mkono sheria hiyo kwa vile ‘itawakomoa’ waliowahi kuninyanyasa mtandaoni huko nyuma.
Wakati jamii inaweza kuuhitaji muda mrefu kujadiliana kuhusu haja ya kuwa na sheria ya kukabiliana na uhalifu mtandaoni, ni muhimu kukumbuka kuwa wahanga wa uhalifu huo hawana muda wa kusubiri. Waingereza wanasema kumcheleweshea mtu haki yake ni sawa na kumnyima haki hiyo (justice delayed is justice denied).



Wahanga wa uhalifu wa mtandaoni wanastahili haki sawa kama hao wenye hofu kuwa sheria hiyo inaweza kutumiwa na serikali kukandamiza uhuru wa mawasiliano.



Wakati ninatambua mapungufu makubwa ya vyombo vyetu vya dola katika kusimamia na kutoa haki, na hivyo kuelewa vema hofu ya wanaopinga sheria hiyo, ni muhimu pia kutambua kuwa serikali ikiwa na nia ya kuminya haki haihitaji sana kuwa na sheria rasmi.
Tumeshuhudia gazeti la MwanaHalisi likifungiwa kwa kutumia ‘visingizio’ vingine, na wakati huo hatukuwa na sheria ya makosa ya uhalifu wa mtandaoni.



Ni kweli kwamba serikali na taasisi zake zinaweza kuitumia vibaya sheria hiyo kuminya uhuru wa mawasiliano, lakini pia ni muhimu tutambue kuwa serikali hiyohiyo ina sheria nyingine kadhaa, na pengine ‘kali’ zaidi ya hiyo ya kuzuwia uhalifu wa mtandaoni, na ikitaka kuzitumia kuminya uhuru, inaweza kufanya hivyo muda wowote.



Kuna sheria kama ile ya Usalama wa Taifa ya mwaka 1970 na sheria ya kukabiliana na ugaidi ya mwaka 2002, ambazo zinaipa serikali uwanja mpana tu wa kuzitumia vibaya ikitaka kufanya hivyo.



Kimsingi, mjadala unaoendelea kuhusu sheria hiyo unatokana na suala ambalo nimekuwa nikiliongelea mara kadhaa katika makala zangu: upungufu wa imani ya wananchi wengi kwa serikali yetu. Imefika mahala wananchi wengi hawaiamini serikali, na ndio maana baadhi ya wanaopinga sheria hiyo wanadai imeletwa haraka kwa minajili ya kuisaidia CCM katika uchaguzi mkuu ujao.



Hofu kuwa sheria hiyo inaweza kutumika vibaya ina mantiki, lakini tatizo sio sheria hiyo ambayo kwa hakika imechelewa sana, bali mfumo wa kifisadi unaoathiri nyanja mbalimbali za maisha ya Mtanzania. Hakuna polisi anayeweza kumkamata mtu kwa vile tu kafanya umbeya kwenye ‘Whatsapp’ yake iwapo mfumo tulionao unazingatia sheria na haki.



Kwa bahati mbaya hilo linaweza kutokea kwa sababu baadhi ya polisi wetu wanaofahamika kwa tabia yao ya kupenda rushwa. Je tupuuzie madhila yanayowakumba wahanga wa uhalifu wa mtandaoni hadi tutakapokomesha rushwa kwenye taasisi kama jeshi la polisi au ‘tuue ndege wawili kwa jiwe moja,’ kwa maana ya kuendeleza mapambano dhidi ya mfumo wa kifisadi sambamba na kutumia ipasavyo sheria hiyo mpya kukabiliana na uhalifu wa mtandaoni?



Wakati kwa kiasi kikubwa mjadala kuhusu sheria hiyo unafanywa kistaarabu, na tayari kuna petition imewekwa mtandaoni kumsihi Rais Kikwete asiridhie sheria hiyo, kuna kundi dogo la wanufaika wa uhalifu wa mtandaoni linalojaribu kujificha katika hoja kuwa sheria hiyo ni mbaya.



Na pengine la kusikitisha zaidi ni kuona dhamira nzuri ya Naibu Waziri January Makamba kuuweka hadharani muswada husika ikichukuliwa na baadhi ya ‘wanyanyasaji wa mtandaoni’ kumshambulia yeye binafsi kana kwamba sheria hiyo ni yake binafsi. Tatizo hapa ni kuweka mkazo kwa mtu badala ya suala husika.



Nimalizie makala hii kwa kusisitiza kuwa ninaamini sheria hiyo dhidi ya uhalifu wa mtandaoni ina umuhimu mkubwa kwa usalama wa taifa letu na kwa Watanzania kwa ujumla. Sheria husika haiwalengi raia wema bali wahalifu wa mtandaoni.



Badala ya kuwekeza nguvu nyingi kuhofia madhara yake, ni muhimu kama jamii tujiongoze kistaarabu na kukumbushana wajibu wetu kama raia wema. Tusiwe vigeugeu wa kuilaumu serikali kila tunapokutana na picha za ngono au maiti mtandaoni lakini serikali ikisikia kilio chetu kuhusu haja ya kuchukua hatua kali, na hivyo kuja na sheria kama hiyo ya kukabiliana na uhalifu wa mtandaoni, twaishia kuilaumu pia.


Kwa mujibu wa tovuti ya Bunge letu la Muungano, kama nilivyoi-access saa 11.02 alfajiri kwa saa za hapa Uingereza, marehemu wabunge hawa hapa chini wameendelea kuorodheshwa kwenye tovuti hiyo sio tu kama bado wapo hai bali pia ni wabunge katika majimbo husika.

Ninaamini kabisa kuwa taasisi muhimu kama Bunge ina fungu la kutosha kwa ajili ya huduma zake mbalimbali, ikiwa ni pamoja na tovuti yake. Na hata ingekuwa haina fungu, kufanya marekebisho kwenye tovuti hiyo ni jambo la dakika chache tu, na lisilo na gharama yoyote.

Hakuna ubaya kwa wabunge marehemu kuendelea kuwepo katika tovuti ya Bunge iwapo ukweli kwamba waheshimiwa hao sasa ni marehemu utabainishwa, hususan katika kipengele kinachoonyesha muda wa utumishi wao katika mhimili huo muhimu wa dola.

Pengine hili ni suala dogo lakini kwa hakika Bunge ni moja ya vitambulisho vya taifa letu, na tovuti yake ni njia rahisi kwa Watanzania na wasio-Watanzania kupata habari na taarifa zinazoihusu taasisi hiyo. 

Licha ya kasoro hiyo, nilipofanya search ya majina ya baadhi ya wabunge, hakukuwa na matokeo yoyote.Ukitaka kuhakikisha, tafuta jina la Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, kwa mfano.








Ni matumaini yangu kuwa Ofisi ya Bunge letu itarekebisha kasoro hii haraka iwezekanavyo

CHANZO: Screenshot za picha kutoka tovuti ya Bunge la Jamuhuri ya Muungano

14 Apr 2015



Sikiliza Katibu Mkuu wa CHADEMA Dkt Slaa akihojiwa na kitumo kimoja cha redio cha WIBC 93. FM cha Marekani

Bonyeza HAPA kusikiliza

12 Apr 2015

Wakati mitandao mbalimbali ya kijamii ikiendelea mjadala kuhusu sheria ya kudhibiti uhalifu wa mtandaoni (Cyber Crime Act 2015), ukweli mchungu unabaki kuwa uhalifu huo upo, na unaendelea kuwaathiri watu kila siku.

Jamii inaweza kuendelea kubishana hata kwa miaka 100 kama twahitaji sheria hiyo au la, lakini wahalifu wa mtandaoni wanaendelea kutusumbua kila kukicha. Wakati sheria hiyo haiwezi kumaliza kabisa tatizo la uhalifu wa mtandaoni, angalau kwa kiasi flani itasaidia kumfanya mhalifu atafakari mara mbili kuhusu madhara ya uhalifu wake pindi akikamatwa.

Na kama kuna eneo ambalo wahalifu wa mtandaoni hulipendelea zaidi ni wizi wa nywila, au kwa kimombo PASSWORD. Lakini kinachowafanya wahalifu hao kupendelea wizi wa nywila sio kwa vile wakifanikiwa kuiba watakuwa na 'control' ya akaunti yako bali pia ukweli kwamba watu wengi hufanya makosa wakati wanapofungua akaunti mtandaoni kwa kuchagua nywila dhaifu.

Pengine ushamsikia shushushu mmoja maarufu kabisa duniani aitwaye EDWARD SNOWDEN. Kama hujawahi kumsikia, basi ngoja nikuhabarishe.Huyu jamaa alikuwa anafanya kazi kama mchambuzi katika moja ya taasisi kubwa za ushushushu nchini mMarekani, inayojulikana kakma NSA, yaani National Security Agency. Hawa jamaa kazi yao ni kunasa mawasiliano- iwe ya email, simu au njia nyingine yoyote ile. Sasa Bwana Snowden, kwa kukerwa na ukiukwaji wa haki za binadamu uliokuwa unafanywa na mwajiri wake, akaamua kumwaga siri hadharani.Akawapatia wanahabari, hususan wa gazeti la Guardian la hapa Uingereza, data kibao zilizokuwa zikionyesha jinsi NSA ilivyokuwa ikiwapeleleza Wamarekani na watu wengike kibao duniani.

Sasa, kama ilivyo kawaida kwa taasisi za ushushushu, ukiweka hadharani madhambi yao unakuwa adui yao.Hivyo ilimlazimu Bwana Snowden kutoroka Marekani, na kwa sasa amepata hifadhi ya ukimbizi nchini Russia.

Siku nafasi ikiniruhusu nitaelezea kwa kirefu kuhusu mkasa wa shushushu huyu.Ila kwa leo nitazungumzia ushauri alioutoa hivi karibuni kuhusu nywila imara, itakayowapa kibarua wahalifu wa mtandaoni kuihujumu.

Snowden akiongea katika mahojiano na mtangazaji wa televisheni na mchekeshaji, John Oliver, alieleza kuwa nywila za watu wengi ni dhaifu mno kiasi kwamba inamgharimu mhalifu wa mtandaoni chini ya sekunde moja kuhujumu nywila yenye tarakimu nane.

"Nywila yangu ina tarakimu tano," alieleza Oliver. "Huo sio utani.Kwahiyo hiyo ni mbaya,sawa?" Snowden alikubaliana nae kwamba hiyo ni mbaya sana.

Kwahiyo watu wafanyeje kuhusu nywila zao? Wakati pendekezo la Oliver kuwa na nywila kama 'limpbiscuit4eva' lilionekana halifai,Snowden alikuwa na ushauri mzuri.Sahau kuhusu nywila zinazotumia maneno ya kawaida na badala yake tumia maneno marefu (paraphrases) ambayo ni rahisi kuyakumbuka, kwa mfano 'margaretthatcheris110%SEXY.' Mhalifu wa mtandaoni hawezi kuhisi neno kama hilo na wakati huohuo wewe utabaki na kumbukumbu ya neno hilo refu.


Kwa sie tunaotumia Kiswahili, ushauri wangu ni kujaribu kutumia mchanganyiko wa majina ya ndugu katika familia yenu na namba flani, bila kusahau herufi kubwa japo moja na tarakimu zisizo namba au herufi kama vile £ au % au $.

Unaonaje kama baada ya kusoma makala hii ukibadili nywila yako kuwa imara zaidi na hivyo kukuwezesha kukabiliana na jitihada za wahalifu wa mtandaoni kuihujumu nywila yako?



11 Apr 2015



Rais Barack Obama wa Marekani akipeana mkono na Rais Raul Castro wa Cuba, walipokutana katika mkutano wa nchi za Americas jijini Panama City,  Panama.

Tukio hili ni la kihistoria kufuatia uhasama mkubwa kati ya nchi hizo mbili.



10 Apr 2015

Africa is home to some of the richest countries in the world, in part due to its oil-rich soil and human capital. With GDPs going up as high as $594.257 Billion.
According to statistics provided by the International Monetary Fund(IMF), these are currently, according to the figures provided at the time, the Top 10 richest countries in Africa.
1. Nigeria: GDP – $594.257 billion
The most populous country in Africa is a major contender on this list, its manufacturing sector being the third largest in Africa while it contributes a considerable share of the world’s oil. Taking into account this country’s population of 170 million, Nigeria is on track to becoming one of the 20 largest economies in the world by 2020.

2. South Africa: GDP – $341.216 billion
South Africa is popularly known for its mineral resources such as gold and diamond but the Gold Rush ended back in the 19th century. There are more things to look forward to in South Africa besides its jewels. Major cities like Johannesburg and Cape Town offer a unique experiences that can offer scenic routes to mountain ranges by the ocean.

3. Egypt: GDP – $284.860 billion
Egypt has one of the longest histories of any modern country, arising in the tenth millennium BCE as one of the world’s first nation states.

4. Algeria: GDP – $227.802 billion
Oil and gas exports have placed Algeria on this list. Much of its wealth is received from oil deposits deep within the North African soil. Also rich in natural minerals, it is suggested that the ancientRomans collected stones and marbles from quarries in what is now known as Algeria. You can find onyx, red and white marbles, iron, lead, and zinc in large quantities. It’s capital city, Algiers offers rare beauty in the intricate architecture of its most famous buildings.

5. Morocco: GDP – $112.552 billion
Morocco was named the first most competitive economy in North Africa. Tourism, telecoms, textiles and agriculture are Morocco’s biggest biggest money pullers.

6. Sudan: GDP – $112.552 billion
More than once, we have mentioned oil and gas as the main source of income for countries on this list. Sudan also falls into that category but in a more diverse way. It depends on oil but with a third of its GDP contributed by agriculture. Cotton and peanuts constitute its major agricultural exports. You may not notice a “Made in Sudan” tag on the shirt you buy in Khartoum but cotton from Sudan has fueled the textile industry in many parts of the world.

7. Kenya: GDP – $53.40 billion
The capital, Nairobi, is a regional commercial hub. The economy of Kenya is the largest by GDP in Southeast and Central Africa. Agriculture is a major employer; the country traditionally exports tea and coffee and has more recently begun to export fresh flowers to Europe. The service industry is also a major economic driver. Kenya is a member of the East African Community. Compared to other African countries, Kenya enjoys relatively high political and social stability.

8. Angola: GDP – $49.857 billion
Angola has a large deposit of oil and gas resources, diamonds, and bountiful agricultural land. Still recovering from the 27-year civil war that lasted from 1975-2002, Angola has made efforts to revive its economy with heavy oil and agricultural exports. Cities like Luanda are undergoing major reconstruction to make Angola a top African destination.

9. Libya: GDP – $49.341 billion
The Libyan economy depends primarily upon revenues from the oil sector, which accounts for 80% of GDP and 97% of exports. Libya holds the largest proven oil reserves in Africa and is an important contributor to the global supply of light, sweet crude.Apart from petroleum, the other natural resources are natural gas and gypsum.The International Monetary Fund estimated Libya’s real GDP growth at 122% in 2012 and 16.7% in 2013, after a 60% plunge in 2011.

10. Tunisia: GDP – $49.122 billion
Oil, tourism and car manufacturing parts are the name of the game in Tunisia. It is one of the wealthiest countries in Africa so you won’t wander too far into its cities like Tunis before finding a pleasant spot to relax. The city is covered with bits of opulence from as far back as the 12th century. Year-round sunshine and the affordable Tunisian lifestyle have drawn tourists here who now call this place home.


SOURCE: IT NEWS AFRICA

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.