18 Jul 2014

Waziri wa Mambo ya Ndani, Mathias Chikawe
NIANZE makala hii kwa kuwatakia ndugu zangu Waislamu mfungo mwema katika mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani, japo salamu hizi nimechelewa kidogo, ambapo sasa mfungo huo umeingia kumi la pili (Maghfirah).
Ni matarajio yangu kuwa ndugu zetu Waislamu watatumia mwezi huu wa toba kuliombea taifa letu kwani mwelekeo wake si mzuri.
Sisi kama Watanzania tuna tatizo kubwa la kupuuzia masuala ya msingi kwa mustakabali wa taifa letu. Hivi katika mazingira ya kawaida tu, inawezekana vipi nchi iandamwe na matukio ya ‘kigaidi’ ya milipuko kadhaa ya mabomu na kupelekea vifo na majeruhi kadhaa lakini hakuna japo mtu mmoja aliyewajibishwa?
Majuzi nimemsikia Waziri wa Mambo ya Ndani, Mathias Chikawe akihojiwa na Radio France International kuhusu matukio hayo ya ‘kigaidi.’ Ninaomba kuwa mkweli, majibu ya Waziri huyo si tu yalikuwa ya kibabaishaji bali pia yalizidi kuonyesha ombwe kubwa linaloukabili utawala wa Rais Jakaya Kikwete.
Waziri Chikawe alieleza kuwa tayari kuna watu sita waliotiwa nguvuni kufuatia tukio la awali la mabomu jijini Arusha, na wengine wawili wamekamatwa kuhusiana na tukio la hivi karibuni. Alidai kuwa inadhaniwa kuwa makundi hayo mawili yana uhusiano. Lakini alipoulizwa ni kundi gani hasa linahusika na mashambulizi hayo, akaishia kudai kuwa ni magaidi.
Kadhalika, Waziri huyo alidai kuwa hatua madhubuti zimechukuliwa kudhibiti matukio hiyo, ambapo “takriban mitaa yote imedhibitiwa kuhakikisha vitendo hivyo vya kigaidi havitokei tena.”
Vilevile alithibitisha kuwa wahusika ni Watanzania, baadhi kutoka Arusha na wengine Tanga, lakini walipata mafunzo ya ugaidi ‘kwingineko’ (bila kusema ni ndani au nje ya Tanzania).
Ndugu msomaji, huhitaji kuwa mtaalamu wa masuala ya usalama kuhitimisha kwamba Waziri Chikawe alikuwa akitimiza tu wajibu wake kujibu maswali aliyokuwa akiulizwa. Busara ndogo tu yaweza kukufahamisha kwamba kama wakati tukio la hivi karibuni linatokea tayari kulikuwa na watuhumiwa sita mbaroni basi kwa hakika kuna mapungufu makubwa mahala flani.
Waziri Chikawe hawezi kukwepa lawama kwa vile Wizara yake inahusika moja kwa moja na usalama wa raia kupitia Jeshi la Polisi, kimsingi wanaopaswa kubebeshwa lawama kubwa zaidi ni Idara ya Usalama wa Taifa. Moja ya majukumu makuu ya taasisi hiyo ni kukabiliana na vitendo vya ugaidi, kwahiyo ‘mafanikio’ ya magaidi-kwa maana ya mwendelezo wa vitendo vyao vya kinyama huko nyumbani-ni dalili ya kushindwa kazi kwa Idara hiyo.
Ninafahamu bayana kuwa wahusika hawatopendezwa na lawama hizi lakini ni muhimu kwao kuelewa kwamba kamwe tusitarajie miujiza kumaliza tatizo hili linalozidi kukua. Ugaidi una sifa ya kupata hamasa kutokana na mafanikio ya mashambulizi yaliyotangulia. Na kwa maana hiyo, pasipo hatua madhubuti, ni wazi tutaendelea kushuhudia matukio hayo yakijirudia.
Mara kadhaa tumeishia kusikia watu flani wamekamatwa kutokana na matukio ya mabomu lakini hadi muda huu vyombo vya dola havijawahi kuona japo umuhimu wa kuufahamisha umma maendeleo ya uchunguzi wao kufuatia kukamatwa kwa watu hao.
Majuzi, aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Jaji Amiri Manento, alitoa maoni yake kwamba Jeshi la Polisi linapaswa kubebeshwa lawama kutokana na matukio ya mabomu, kwa kushindwa kuyazuia yasitokee tena.
Jaji Manento alisema katika tukio la kwanza la mlipuko wa bomu kwenye mkutano wa CHADEMA jijini Arusha, Jeshi la Polisi lilishindwa kutekeleza wajibu wake kutokana na kusikiliza kauli za viongozi wa kisiasa. Alihusisha hali hiyo na ukiukwaji wa haki za binadamu .
Na siasa za kihuni zimechangiwa sana ustawi wa matukio haya ya mabomu. Wengi tunakumbuka jinsi Mwigulu Nchemba alivyofanya kila jitihada kuwahadaa Watanzania kwamba tukio la mabomu katika mkutano wa CHADEMA huko Arusha lilisababishwa na CHADEMA wenyewe.
Hiyo ilikuwa baada ya jitihada mufilisi za CCM kumtwisha kiongozi mwandamizi wa CHADEMA Wilfred Lwakatare kesi ya ugaidi.
Mwanzoni mwa makala hii nimewalaumu Watanzania kwa kupuuzia mambo ya msingi kwa mustakabali wa taifa letu. Pasi haja ya kutoa mifano mingi, rejea jinsi wananchi walivyokubali kwamba mgao wa milele wa umeme ni kama haki yao ya kikatiba, huku licha ya kuambiwa kuwa kuna mabilioni ya fedha zao zilizoibiwa na kufichwa huko Uswisi, hakuna harakati zozote za angalau kupigia kelele ufisadi huo.
Majuzi nimeshuhudia picha kadhaa zinazoonyesha jinsi hali ilivyo mbaya katika hospitali ya taifa Muhimbili. Nikajisemea moyoni, kama hali ipo hivi katika hospitali ya taifa, hali ikoje huko kwenye hospitali teule, za mikoa, wilaya au kwenye vituo vya afya?
Lakini nani anajali? Ushindi wa Ujerumani katika Kombe la Dunia mwishoni mwa wiki iliyopita unaweza kuwa na umuhimu mkubwa kwa Watanzania wengi kuliko hatma ya usalama wao kutokana na matukio mfululizo ya mabomu, mgao wa umeme, hali mbaya katika hospitali zetu, nk.
Ndio, wenye jukumu la kushughulikia yote hayo ni viongozi tuliowakabidhi dhamana ya kutuongoza, lakini ni wajibu wa kila mwananchi kuwabana viongozi wasiotekeleza majukumu yao ipasavyo. Ninaamini kuwa kinachowapa jeuri viongozi wengi kutowajibika ipasavyo ni ukweli kwamba aliyewateua hatowawajibisha na wananchi hawatojali.
Nikirejea kwa watu wa Usalama wa Taifa, angalau wanapohusishwa na kushamiri kwa ufisadi huko nyumbani, wanaweza kuwa na ‘excuse isiyokubalika’ kuwa labda wananufaika kimaslahi. Lakini wanaweza kuwa na maelezo gani wanaposhindwa kudhibiti janga hili la ugaidi?
Nihitimishe makala hii kwa kumshauri Rais Kikwete kuchukua hatua stahili dhidi ya watendaji wake wanaozembea kukabili tishio na matukio ya ugaidi.
Asisubiri mpaka bomu limdhuru kiongozi ndio atambue kuwa ugaidi ni hatari (na sifa nyingine ya ugaidi ni kuwa haubagui -haichagui kati ya mlalahoi au kigogo japo hadi sasa wahanga wamekuwa walalahoi pekee).
Japo inampendeza kusikia Rais wetu anawathamini wasanii kiasi cha kuwaletea mastaa kutoka Marekani ‘kuwapa somo kuhusu sanaa’ lakini angewatendea haki Watanzania wote laiti angeweza pia kuwaletea wataalamu wa masuala ya ugaidi ili kuwasaidia wanausalama wetu ambao kwa hakika wameshindwa kazi.
Mungu Ibariki Tanzania

10 Jul 2014

HATIMAYE mbio za kuelekea Ikulu hapo mwakani zimeanza rasmi baada ya mwanasiasa kijana, Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia na Mbunge wa Bumbuli (CCM), January Makamba, kutangaza kuwa atagombea urais.
Habari hiyo imetawala mno katika mitandao ya kijamii na ukiweka kando michuano ya Kombe la Soka la Dunia inayoendelea nchini Brazil, tangazo la mwanasiasa huyo limeonekana kuwagusa wengi.
Na kama pongezi ni ishara ya ushindi, basi kwa hakika uamuzi wake wa kugombea nafasi hiyo kubwa kabisa nchini unaonekana kuunngwa mkono japo kwenye mitandao ya kompyuta.
Ninampongeza January kwa ujasiri wa kutamka dhamira yake ya urais hadharani. Huko nyuma nilishawahi kuzungumzia umuhimu wa wanasiasa wanaotaka urais kujitokeza hadharani mapema ili tupate fursa ya kuwaelewa vizuri na pengine kuwapa ‘hukumu’ stahili.
Utaratibu wa kutangaza nia ya kuwania urahisi mapema ni kama jambo la kawaida kwa siasa za nchi za Magharibi, hususan, huko Marekani.
Hata hivyo, pamoja na faida yake kwa wananchi, na pengine kwa mgombea kutambulika na hata kupata kuungwa mkono zaidi, moja ya athari zake ni kwa mtarajiwa kuwapa maadui zake ‘silaha’ za kummaliza mapema.
Kadhalika, kwa kutangaza nia mapema, mtarajiwa anaweza kujikuta amechokwa mapema hata kabla ya uchaguzi, hususan, kama ana mapungufu yaliyofichika.
Ifahamike kuwa kwa kujitangaza kugombea urais mapema, mwanasiasa anawapa fursa wananchi kumchunguza-kwa mema na mabaya- na iwapo kuna kasoro zilizofichika au ambazo hazikuwahi kupewa umuhimu mkubwa, basi anaweza kujitengenezea mazingira ya kushindwa mapema.
Sasa  tuangalie nafasi ya January kufanikiwa kuwa rais ajaye wa Tanzania. Moja ya sifa kubwa ya mwanasiasa huyo inatajwa kuwa ukaribu wake na wananchi wa kawaida. Kwa sisi tunaotumia muda mwingi kwenye mitandao ya kijamii tunaweza kuafikiana na hoja hiyo. Lakini ‘maisha ya mtandaoni’ si lazima yawe ndo maisha ya mtu kihalisia (real life).
Kingine kinachoweza kumsaidia mwanasiasa huyo ni ujana wake. Japo sina takwimu za hakika, yayumkinika kuhitimisha kuwa idadi kubwa ya wapigakura huko nyumbani ni vijana. Kwahiyo kama ujana wa January waweza kutafsiriwa katika sapoti kutoka kwa vijana wenzie basi anaweza kuwa na nafasi nzuri.
Na siku chache baada ya kutangaza nia yake ya kuwania urais hapo mwakani, waziri mkuu mstaafu Jaji Joseph Warioba alinukuliwa na vyombo vya habari akishauri kuwa ni vema kwa wazee kuwaachia vijana nafasi za uongozi. Hiyo ni sapoti kubwa kwa January hasa ikizingatiwa kuwa licha ya kebehi zilizoelekezwa kwake kufuatia uongozi wake katika ‘Tume ya Warioba,’ mwanasiasa huyo bado anaheshimika miongoni mwa Watanzania wengi.
Hata hivyo, moja ya vikwazo vikubwa kwa January kufanikiwa kuwa mrithi wa Rais wa sasa, Jakaya Kikwete, ni utaratibu wa kumpata mgombea urais ndani ya CCM. Binafsi, sitilii sana maanani mizengwe iliyozoeleka ndani ya chama hicho kila linapokuja suala la kupata mgombea (hata wa nafasi ya uenyekiti wa serikali ya mtaa, achilia mbali urais) bali nafasi ya Zanzibar katika suala la mgombea urais kwa tiketi ya CCM.
Inafahamika kuwa awali chama hicho tawala kilikuwa na utaratibu usio rasmi wa ‘uongozi wa kupokezana’ kwa maana baada ya Mtanzania Bara kumaliza awamu zake, ni zamu ya Zanzibar kutupatia rais. Hata hivyo, baada ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere (m-Bara) kung’atuka na kumwachia rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi (Mzanzibari), ambaye naye baada ya kustaafu alirithiwa na rais mstaafu Benjamin Mkapa (m-Bara), ilitarajiwa kuwa rais wa Awamu ya nne angetoka Zanzibar.
Wenye uelewa wa siasa za nchi yetu wanadai kuwa kilichovuruga utaratibu huo (angalau kwa muda) ni nguvu ya mtandao uliomwingiza Rais Kikwete madarakani. Inadaiwa kuwa mtandao huo uliojipenyeza kila mahali ulifanikiwa kuzima matakwa ya wana-CCM Zanzibar kuwa “Awamu ya nne ilikuwa zamu yao.”
Je, January ana raslimali za kutosha kisiasa kuweza kuwashawishi Wazanzibari wamruhusu agombee na hivyo kuwanyima fursa nyingine ya urais baada ya miaka 20 ya Mkapa na Kikwete?
Kuna tatizo jingine ambalo japo si kubwa lakini laweza kumkwamisha mwanasiasa huyo kijana. Utaratibu mwingine usio rasmi kuhusu urais ni wa nafasi hiyo kuzunguka kati ya Mkristo na Mwislamu. Nyerere alikuwa Mkristo, Mwinyi Mwislamu, Mkapa Mkristo na Kikwete Mwislamu. Je, uwezekano wa kuwa na rais mwingine Mwislamu hauwezi kuzua manung’uniko? Binafsi sioni kama hoja hiyo ina msingi kwa sababu uongozi bora hauna dini, lakini ni vema kufahamu kuwa japo tunapinga udini lakini hisia hizo zipo na hazikwepeki.
Kikwazo kingine kwa January, angalau kwa wasio wana-CCM, ni u-CCM wake. Yayumkinika kuhitimisha kwamba kuna idadi ya kutosha ya Watanzania wanaokiona chama hicho tawala kama chanzo kikuu cha matatizo yanayoikabili nchi yetu.
Si siri kwamba CCM imegeuka kuwa kichaka cha kuhifadhi mafisadi, na kuna wanaodhani kuwa dhamira ya CCM kubaki madarakani ni si tu ukweli kuwa chama chochote cha siasa kilicho madarakani lazima kitataka kuendelea kutawala bali pia uwepo wake madarakani ni kulinda maslahi binafsi ya viongozi wake na washiriki wao.
Je, January, na wengine watakaokuja,  watawashawishi vipi Watanzania kuwa licha ya kuwa viongozi wa ngazi ya juu katika chama hicho tawala, wapo tofauti kimtizamo au vitendo na viongozi wengine wa CCM? Na katika hilo kuna suala la kumbukumbu.
Kuna uwezekano mwanasiasa huyo akaulizwa “sawa, wewe ni msafi lakini ulishafanya nini kuondoa uchafu unaokikabili chama chako?”
Baadhi yetu tunadhani kuwa uhusiano kati ya CCM na mafisadi ni kama ule unaofahamika kibaiolojia kama ‘symbiotic,’ kwamba ustawi wa mafisadi unategemea uhai wa CCM na wa CCM unaowategemea mafisadi.
Ndiyo maana jitihada fyongo za chama hicho ‘kujivua magamba’ zilikwama kwa sababu, tofauti na nyoka anavyoweza kujivua ‘gamba’ akasalimika, jaribio hilo la CCM lilikuwa kama kobe kujivua gamba; lazima atakufa!
Hapo juu nimetaja kuwa ujana wa January waweza kuwa ‘asset’ katika dhamira yake ya kuingia Ikulu. Hata hivyo, binafsi ninapingana vikali kabisa na mtizamo kwamba ujana (au hata uzee) ni sifa muhimu ya rais tunayemhitaji.
Hivi wakati huu ambapo nchi yetu inabakwa mchana kweupe na mafisadi kupitia skandali kama za EPA, Richmond, ESCROW, nk hatuna viongozi vijana ndani ya CCM? Mbona hatuwasikii wakipiga kelele dhidi ya ufisadi huo?
Majambazi wanaofanya kila jitihada za kufilisi nchi yetu hawana umri maalumu; wauza madawa ya kulevya, matapeli wa kisiasa, na wahalifu wengine ni pamoja na vijana. Na hata uzalendo hauna umri. Mzee au kijana anaweza kuipenda nchi yake na akaitumikia kwa uadilifu kama ambavyo kijana au mzee anavyoweza kuibomoa nchi.
Na kingine kisichonipendeza kuhusu ‘ubaguzi’ dhidi ya wazee ni uwezekano wa ‘domino effect,’ yaani leo itakuwa “wazee hawafai kutuongoza,” kesho itakuwa “wanawake hawafai kushika uongozi,” na katika hali ya hatari kabisa, twaweza kufikia hatua ya “Wakristo/Waislam hawafai kutuongoza.”
Nihitimishe makala hii kwa kurejea pongezi zangu kwa January Makamba kwa kutangaza mapema dhamira yake ya kutaka kuwania uraia hapo mwakani, hatua ambayo angalau imeamsha mjadala muhimu kuhusu rais ajaye.
Ni matarajio yangu kwamba wanasiasa wengine wenye nia ya kuongoza taifa wataiga mfano huo ili kuwasaidia Watanzania wawaelewe kwa undani ili hatimaye wafanye uamuzi sahihi katika sanduku la kura.
Ni muhimu kutambua kwamba uchaguzi huo una umuhimu mkubwa kwa hatma ya kila Mtanzania na uhai wa Tanzania yetu.
Kadhalika, kwa vile inatarajiwa kuwa uamuzi wa January ‘kutangaza nia’ waweza kusababisha ‘wenye nia’ wengine kujitokeza hadharani, ni muhimu kwa Watanzania kujiandaa kuwauliza swali hili: “nchi yetu kamwe haijawahi kuwa na uhaba wa wanasiasa wanaoahidi mambo mazuri lakini wakiingia madarakani ‘wanazisahau ahadi zao’, je una lipi ulilokwishaifanyia Tanzania la kutufanya tukuone tofauti na wapiga porojo wengine?”

26 Jun 2014

 
 
Ziara ya Makamu wa Rais wa China, Li Yuanchao, nchini Tanzania imeambatana na tatizo la lugha, ambapo kiongozi huyo amekuwa akihutubia hadhara mbalimbali kwa Kichina pasipo mtafsiri wa Kiswahili.


Serikali imetangaza  kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwa MAJENEZA
KWA kila anayefuatilia makala zangu kwa karibu hatashindwa kubaini kuwa moja ya vyanzo vya mada za makala hizo ni kwenye mijadala mbalimbali ya mitandao ya kijamii, hususan twitter. Mara kadhaa nimekuwa nikipata cha kuandika katika makala hizi kutokana na mijadala hiyo inayohusu masuala mbalimbali.
Na kwa hakika, mitandao ya kijamii imekuwa na umuhimu wa kipekee kwangu hasa katika jitihada zangu za kukuza uelewa nje ya mazingira ya kitaaluma. Lakini pengine faida kubwa zaidi imekuwa katika kutengeneza marafiki muhimu kutoka nyanja mbalimbali za maisha. Nimefahamiana na wanasiasa, wasanii, wasomi, wanahabari na wengineo. Wakati kwa bahati mbaya au makusudi, baadhi ya watumiaji wa mitandao ya kijamii huko nyumbani (Tanzania) wameigeuza kuwa sehemu za kutafutia umaarufu kama sio kuwabughudhi wenzao, kwangu mitandao hiyo imekuwa fursa ya kutengeneza ‘mduara wa watu muhimu’ sambamba na ‘kisima cha kuchota elimu ya bure.’
Lengo la makala hii sio kuzungumzia umuhimu wa mitandao ya kijamii japo ningependa kuwahamasisha ‘wanaoikwepa’ watumie hamasa hii kuijaribu, na nina uhakika wataafikiana nami juu ya umuhimu wake. Makala hii inalenga kuzungumzia kinachoendelea huko Mashariki ya Kati, hususan nchini Iraq.
Nimeanza makala hii na umuhimu wa mitandao ya kijamii kwa sababu majuzi nilifanya maongezi na dada mmoja ambaye kwa asili ni Mkenya lakini ameishi sehemu mbalimbali duniani kutokana na wazazi wake kuwa wanadiplomasia. Nilifahamiana naye huko twitter hasa baada ya kuvutiwa na ‘tweets’ zake kuhusu masuala mbalimbali ya kimataifa. Kumbe pasi kufahamu, naye pia alikuwa akiguswa na ‘kelele’ zangu kuhusu maovu mbalimbali yanayoikabili Tanzania yetu.
Binti huyo ana uelewa mkubwa kuhusu siasa za Mashariki ya Kati, na kwa hakika ‘darasa’ alilonipatia kuhusu mapigano  yanayoendelea nchini Iraq kati ya waumini wa madhehebu ya Sunni na Shia lilinifungua upeo wangu zaidi ya nilivyokuwa nikielewa kupitia vyanzo vingine mbalimbali. Kikubwa zaidi, aliweza kwa ufanisi mkubwa kunifahamisha madhara ya kinachoendelea katika eneo hilo la Mashariki ya Kati na athari zake kwa nchi za Afrika Mashariki, hasa kwa sababu, kwa mujibu wa uelewa wake, uhusiano wa kidiplomasia kati ya baadhi ya mataifa ya eneo hilo na nchi za Afrika Mashariki umekuwa wa kimkakati (strategic) zaidi kuliko tunavyodhani (nitaongelea suala hili katika makala zijazo).
Lakini kubwa zaidi ni mjadala wetu kuhusu chanzo cha ukosefu wa amani nchi Iraq na jinsi kinachotokea huko kinavyoweza kulinganishwa na hali ilivyo katika nchi zetu, Kenya kwake na Tanzania kwangu.
Kwa mujibu wa taarifa za kiintelijensia za Marekani, Waziri Mkuu wa Iraq, Nouri al-Maliki, alikwishaonywa miaka miwili iliyopita kuhusu hisia miongoni mwa waumini wa madhehebu ya Sunni nchini humo kuwa wanatengwa. Hata hivyo, si Maliki wala serikali yake waliochukua hatua stahili kushughulikia tatizo hilo. Kimsingi, kuna lawama kadhaa zinazoelekezwa kwa Serikali ya Maliki kwa kushindwa kwake kujifunza kuhusu siasa za upatanishi (reconciliatory politics) kati ya Watutsi na Wahutu nchini Rwanda na Weusi na Makaburu nchi Afrika Kusini.
Miaka michache iliyopita nilipokuja huko nyumbani kwa ajili ya utafiti wa vitendo (fieldwork) kuchunguza kuibuka kwa ‘Uislamu wa msimamo mkali’ nchini Tanzania, moja ya hoja iliyojitokeza mara kwa mara ni hisia miongoni mwa Waislamu wengi kwamba wanatengwa. Nilizungumzia suala hili katika makala zilizopita lakini kwa sasa nadhani kuna umuhimu wa kuliangalia kwa kurejea kinachojiri nchini Iraq.
Kimsingi hisia hizo za kutengwa ni zaidi ya miongoni mwa baadhi ya Waislamu pekee. Hebu msomaji mpendwa angalia tofauti kati ya mbunge anayelipwa zaidi ya shilingi milioni 10 kwa mwezi na mlalahoi ambaye hana uhakika wa mlo wake wa siku inayofuatia. Unaweza pia kuangalia sekta ya afya ambapo watawala wetu wakipatwa na mafua tu wanakwenda ng’ambo kuangalia afya zao ilhali inafahamika kuwa hali ni mbaya sana katika takriban kila hospitali zetu.
Kilichonisukuma zaidi kuzungumzia suala hili ni taarifa kwamba katika jitihada zake za kuongeza mapato kwa ajili ya bajeti ya mwaka ujao wa fedha, Serikali imeanzisha kodi ya nyongeza ya thamani (VAT) kwenye majeneza. Hivi kweli Serikali yetu imeishiwa kabisa mbinu za kukusanya mapato hadi ifikie hatua ya kukifanya kifo kiwe ghali kiasi hicho?
Ndio, tatizo la waumini wa madhehebu ya Shia na Sunni nchini Iraq ni la kidini zaidi, lakini ukweli unabaki kuwa uwepo wa hisia za kubaguliwa, kutengwa, kunyanyaswa au kupuuzwa na watawala kunaweza kuzua balaa kubwa katika nchi husika.
Ikumbukwe kuwa pamoja na kuandamwa na tuhuma kuhusu ufisadi wa kampuni ‘feki’ ya Richmond kulikosababisha kujiuzulu, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, amekuwa akikumbushia mara kwa mara kuhusu kile Anachokiita ‘bomu la wakati,’ yaani tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana. La muhimu hapa sio kama ‘kelele’ zake ni za uchungu wa dhati au anasaka tu ‘kura za vijana,’ bali ukweli kwamba ukosefu wa ajira ni tatizo ambalo lisipopatiwa ufumbuzi wa haraka linaweza kuzua matatizo makubwa huko nyumbani.
Ninachojaribu kubainisha hapa ni jinsi mazingira ya baadhi ya wananchi kuhisi wanatengwa yanavyojengeka kama ilivyokuwa nchini Iraq. Sina maana wala kutabiri kuwa kinachojiri nchini humo kitatokea Tanzania, na Mola aepushe hilo, lakini ni vema kwa watawala wetu kutambua kuwa mazingira hayo ni kile Waingereza wanakiita ‘recipe for disaster.’
Tuna makundi mbalimbali katika nchi yetu yanayohisi kutengwa na watawala wetu. Haiingii akilini kwa Serikali kuamua kutoza VAT kwa majeneza badala ya kwa mfano, kupunguza safari mfululizo za Rais Jakaya Kikwete nje ya nchi ambazo zinatafuna mamilioni ya fedha za walipakodi. Ndio, Rais lazima asafiri lakini sio mara kwa mara, zaidi hata ya viongozi wa nchi tajiri kama Marekani ambazo zinamudu gharama za Rais kuwa ziarani hata kila siku ya mwaka.
VAT kwenye majeneza ni mkakati fyongo wa kuongeza mapato sio tu kwa vile karakana zinazotengeneza majeneza zinalipa kodi za uendeshaji biashara bali pia sio ubinadamu kuwa na ‘kodi ya kifo’ ilhali tungeweza kuokoa fedha nyingi tu kwa Serikali yetu kuwa na matumizi yanayoendana na umasikini wetu.
Nimalizie makala hii kwa kuwasihi watawala wetu wafumbue masikio na macho yao na kujifunza yanayojiri katika sehemu nyingine duniani kama huko Iraq kuhusiana na athari za mazingira ambapo makundi fulani katika kujiona yanatengwa, yanabaguliwa, yanadharauliwa au yanakandamizwa. Watanzania walio wengi hawatendewi haki na watawala wetu ambao ni wepesi wa kutoa ahadi zisizotekelezeka wakati wanaomba kura lakini wepesi wa kuchukua uamuzi unaowafanya watawaliwa kuhisi watawala hao wanaishi sayari tofauti kabisa (kwa mfano uamuzi wa VAT kwa majeneza).
Wito wangu kwa Rais Kikwete ni kuwaagiza watendaji wake waachane na ‘kodi hiyo ya laana’ ya VAT kwa majeneza. Ninarejea kumkumbusha kuwa amebakiwa na takriban miezi 18 tu madarakani kutengeneza legacy nzuri ya kukumbukwa na kuenziwa na Watanzania atakapostaafu hapo mwakani. Kadhalika, ninamsihi atumie muda huu uliobaki kufanya jitihada zaidi kuleta usawa kati ya makundi mbalimbali katika Tanzania yetu, hususan pengo linalozidi kukua kati ya wenye nacho na wasio nacho.
- See more at: http://www.raiamwema.co.tz/ipo-siku-watawaliwa-hawa-wataamua-%E2%80%98liwalo-na-liwe%E2%80%99#sthash.eJ7DR5WJ.dpuf

14 Jun 2014

Tunaomba radhi kwa picha hizi ambazo ni graphic. Tumejitahidi kuficha sura ya marehemu
Mwili wa mtu aliyeuawa kutokana na shambulio hilo la bomu

Mtu mmoja ameuawa na wengine kadhaa kujeruhiwa katika shambulio la bomu karibu na msikiti huko Zanzibar. Kwa mujibu wa polisi, shambulio hilo lilitokea katika eneo la Stone Town kwenye sehemu ya biashara ya Darajani.

Mashuhuda wa tukio hilo walieleza kwamba miongoni mwa majeruhi ni waumini waliokuwa wanatoka kuswali katika msikiti ulio jirani na eneo hilo.

"Tunafanya uchunguzi kutambua aina ya bomu, waliohusika na shambulio hilo na lengo lao. Tunaomba wananchi kutupatia taarifa," alisema afisa mwandamizi wa jeshi la Polisi, Mkadam Khamisi.

Taarifa zaidi kuhusu tukio hili la kusikitisha zitawajia kadri zinavyopatikana

12 Jun 2014

Wakati taarifa zinatanabaisha kuwa nchi yetu ipo hoi kifedha,

Embedded image permalink

 huku deni la taifa likizidi kupaa, na serikali ikikuna kichwa kutengeneza bajeti ya kueleweka kwa mwaka ujao wa fedha, 

Embedded image permalink
haya ndio matumizi ya viongozi wajuu wa chama Tawala CCM



CHANZO: Jamii Forums

Nakuachia wewe msomaji na kila anayeipenda Tanzania kwa dhati kutoa hukumu hapo mwakani katika uchaguzi mkuu.

31 May 2014

Licha ya kuwa sehemu muhimu za kubailishana mawazo, na pengine kufahamiana na watu mbalimbali, mitandao ya kijamii (social networks) ina upande wa pili ambao kwa hakika unaweza kuyafanya maisha yako yawe magumu mtandaoni. Pengine umeshawahi kusikia kuhusu watu wanaoitwa TROLLS. Pengine ushawahi kukutana nao, iwe Twitter au Facebook au hata Instagram. TROLL ni mtu anayeamua kukuandama kwenye mtandao wa kijamii pasipo sababu ya msingi.

Mara nyingi TROLLS humwandama mtu mwenye umaarufu bila kujali umaarufu huo unatokana na nini. Mtandao wa kijamii unaopendelewa zaidi na TROLLS ni Twitter. Na mara nyingi TROLLS humwandama mtu mwenye followers wengi, pengine lengo likiwa ni kusababisha madhara makubwa kwa mtu huyo. Hapa ninamaanisha kuwa kwa mfano TROLL anapo-tweet kitu kibaya dhidi yako, anatamani watu wengi wakione. Sasa ukiwa na followers wengi, lengo la TROLLS kukudhalilisha linafanikiwa kwa kiasi kikubwa kwani kila follower wako ataona kitu hicho.

Kuna wanaotetea tabia hiyo chafu wakidai kuwa ni sehemu tu ya utani huku wengine wakidai ni uhuru wa kuongea (freedom of speech). Lakini ukweli ni kwamba TROLLS husukumwa na kauli za chuki (hate speech). Katika mazingira ya kawaida tu, mtu anayekudhalilisha hadharani anakuwa na lengo moja tu: kukudhalilisha. Ndio, uhuru wa kujieleza (freedom of expression/speech) ni kitu kizuri lakini sote twafahamu kuwa hakuna uhuru bila wajibu. Huwezi kumwandama au kumdalilisha mtu hadharani kisha ukajitetea kuwa unatumia uhuru wako wa kujieleza. Uhuru wa kujieleza shurti uambatane na wajibu wa kutowabughudhi watu wengine.

Jana nimekumbana na TROLL mmoja huko Twitter. Huyu jamaa tulikuwa tunaelewana kitambo. Sio marafiki as such lakini mara nyingi tulikuwa tukijadialana kuhusu masuala mbalimbali. Yeye ni mwana-CCM, kwa maana ya kuisapoti CCM,ilhali mie sio kama ni mpinzani wa chama hicho tawala bali ninapinga matendo mengi yasiyopendeza, hususan ufisadi. Kwahiyo mara kadhaa mie na huyu ndugu tulikuwa tukijikuta katika malumbano ya hoja, japo mara zote yalikuwa ya kistaarabu.

Siku moja nikabaini kuwa ameni-unfollow. Nikiri kwamba nilishtushwa na uamuzi wake huo kwa sababu sikuwa na uhasama nae, na hata siku moja sikuwahi kutamka neno baya dhidi yake. Hata hivyo, niliheshimu uamuzi wake huo hasa ikizingatiwa kuwa awali ni yeye ndiye aliyeanza kuni-follow na mie nikam-follow back. Kwa maana hiyo, kama nafsi yake ilivyomtuma kuni-follow mwanzoni, niliamini kuwa nafsi yake hiyohiyo ndiyo iliyomtuma kuni-unfollow.Ila kwa hakika uamuzi wake huo wa kuni-unfollow pasi sababu ulinishangaza.

Nirejee tukio la jana. Hapa chini ndio tweet niliyoifahamu uwepo wake kupitia kwa dadangu yangu mmoja aliyenijulisha kwa Whatsapp, 


Huhitaji kuwa muelewa wa kauli za kashfa kutambua kuwa lengo la mtu huyu halikuwa jema. Ila kukuweka mahala pazuri kuelewa anachoongelea, ni vema nikiambatanisha maelezo na picha ya 'event' (tukio) anayoongelea. Jumatano ya tarehe 28 mwezi huu, nilialikwa jijini London kutoa mada katika semina kuhusu Rushwa na Haki za Binadamu nchini Tanzania. Semina hiyo iliandaliwa kwa ushirikiano kati ya Kundi la Wanasheria wa Kimataifa wa Haki za Binadamu (Solicitors International Human Rights Group) na Taasisi za Stadi za Juu za Sheria (Society for Advanced Legal Studies). Semina hiyo ilifanyika Institute of Legal Studies ya Chuo Kikuu cha London (University of London)

Pengine kutokana na kutokuwa na uelewa wa events zinazoendeshwa kitaasisi, mtu huyo alitamani kuona picha zangu nyingi nikiwa katika tukio hilo ili kuthibitisha kuwa kweli nilihudhuria na kutoa mada. Lakini licha ya ukweli kwamba sikwenda kwenye tukio hilo kwa ajili ya kupiga picha, pia mie kama mtoa mada ningeonekana kituko kuwa busy na kujipiga picha badala ya kutekeleza jukumu lililonipeleka hapo. Vilevile, yeyote anayeyafahamu vema maisha yangu mtandaoni atatambua kuwa sina tabia ya kujipiga picha, na kwa hakika picha zangu binafsi ni chache mno mtandaoni. Nina sababu zangu za msingi kutotaka kuweka picha zangu mtandaoni, na hilo ni suala binafsi.

Lakini hata tukiweka kando sababu nilizotoa hapo juu, mtu huyu ambaye awali alini-unfollow alikuwa anahitaji nini katika picha zangu? Je akishaziona zitamsaidia nini yeye? Na ukiangalia hiyo tweet yake utabaini ameweka inverted comas kwenye 'usalama wa taifa' kana kwamba mtajwa (mie) ninatumia ndivyo sivyo uhusiano wangu na taasisi hiyo. Sijawahi kuficha kuwa niliwahi kuwa mtumishi wa taasisi hiyo, lakini hilo ni suala langu binafsi ambalo sidhani kama linahitaji kumnyima raha mtu mwingine. Kuwa shushushu sio dhambi, na kwa hakika ninajivunia utumishi wangu katika taasisi hiyo kwa miaka kadhaa, sio kwa sababu ya 'ujiko' bali ukweli kwamba taaluma ya intelijensia inahusiana na kiwango cha juu kabisa cha akili (intelligence) na uzalendo. 

Kilichonisikitisha zaidi katika tukio hilo ni mtu mwingine aliyekuwa anani-follow na mie ninam-follow kuamua ku-RT (retweet) tweet hiyo ya kebehi. Huyu jamaa aliye-RT tuna historia ndefu kidogo. Awali tulikuwa 'marafiki' katika Twitter, ikatokea tukatibuana, nikam-block, lakini katika kuukaribisha mwaka mpya mmoja (nadhani mwaka juzi) alinisihi tusahau tofauti zetu na tuishi mtandaoni kwa amani. Nikam-unblock, na tukaendeleza 'urafiki' wetu huko Twitter. Nilitarajia kuwa kama 'rafiki' angetambua wazi dhamira ya mtu aliye-tweet kuhusu ushiriki wangu katika event hiyo ya London. Na kwa vile ninaamini ni mwelewa, angebaini pia kuwa kui-RT tweet hiyo sio tu kuna lengo la kunifikishia ujumbe bali pia ni kama ana lengo la kuisambaza tweet hiyo ninayoitafsiri kuwa ya kashfa (offensive/malicious)..

Ilinisikitisha kwa sababu kama nilivyoeleza awali, huyu ndugu tulikuwa marafiki, tukatibuana, nikam-block kwa sababu kama hii aliyotenda jana, akataka suluhu,nikaafikiana nae, lakini cha ajabu karejea hukohuko alikotoka. Huu si uungwana hata kidogo na ndio maana nimem-block tena, safari hile milele daima.

Huu ni mfano hai wa TROLLS, watu wanaoamua kukuandama pasi sababu ya msingi. Lakini tafiti mbalimbali zinabainisha kuwa wengi wa TROLLS ni watu wenye matatizo ya kiakili. Hawa ni watu wanaokerwa kuona mtu flani anakubalika kwa jamii (angalau katika mawazo yao), au anapiga hatua flani (na pengine si hatua bali mtizamo wao fyongo tu), au anapata sifa (na pengine sio sifa bali ni sehemu ya kawaida tu ya maisha ya mtu). Ni viumbe wanaosukumwa na chuki, watu wasiopenda kuona flani ana amani. Ni magaidi wa mtandaoni wanaosukuwa na chuki. Ni watu waliokosa kitu flani lakini wanataka kufidia pengo la walichokosa kwa kumwandama mtu aliyenacho. Kwa mfano, chuki ya TROLL yaweza kusababishwa na uhaba wa elimu na hivyo kuwaandama watu walioelimika dhidi yake.

Nieleze bayana kuwa sihitaji kuweka ushahidi wa nifanyacho maishani mwangu, iwe ni kuhudhuria semina, kutoa mada katika semina au jinsi ninavyoishi. Ninaamini kuwa masuala binafsi yanapaswa kubaki binafsi (private things should remain private). Sababu kubwa ya kutopendelea kubandika picha zangu mtandaoni ni hiyo. Sipendi kuyaweka maisha yangu binafsi hadharani. 

Lakini hata kama kulikuwa na umuhimu wa picha za tukio hilo kuwa hadharani (na taasisi husika itaziweka kwenye tovuti yake), kulikuwa na haja gani ya mtu au watu kutaka ushahidi wa picha hizo? Halafu kuna namna ya kistaarabu ya kutaka ushahidi badala ya kukimbilia kuhisi kuwa  "event ilibuma (haikufanikiwa, ni kitchen party..." na kushauri kui-Adobe (akimaanisha kutengenza picha feki za tukio hilo.

Binafsi sikumbuki idadi ya seminars, conferences,workshops na mikusanyiko mingine ambayo nimeshawahi kuhudhuria maishani. Ni mingi mno lakini cha muhimu sio idadi ya misanyiko ya aina hiyo bali umuhimu wake kwangu bainfsi na kwa jamii. Semina hiyo ya London ilikuwa na umuhimu mkubwa kwangu binafsi na kwa Watanzania kwa ujumla, kwa sababu mie binafsi nimekuwa nikijihusisha na vita dhidi ya rushwa na pia rushwa na ukiukwaji wa haki za binadamu ni matatizo sugu huko nyumbani.

Hivi kweli serioulsy mtu anaweza kushauri kutengeneza picha feki kwa Adobe ili kuidanganya jamii kuhusu ushiriki wake kwenye tukio flani? Ili iweje na imsaidie nani? Ama kwa hakika shule ni kitu muhimu sana. Kuna wenzetu wanaishi kwa SIFA na wanahangaika kusaka SIFA kwa gharama yoyote ile. Na kwa hakika, wakipata fursa kama hiyo niloipata juzi basi wangemwaga mapicha lukuki ya kila dakika ya uwepo wao hapo. 

Kama nilivyosema awali, kilichonipeleka katika semina hiyo ni umuhimu wake kwangu na kwa nchi yangu kwa ujumla. Kamwe sijawahi kufanya jambo kwa minajili ya kusaka sifa au maonyesho. Nilizaliwa na kukulia katika kile Waingereza wanakiita humble background. Na ukubwani, nikapata ajira inayohitaji 'maisha ya kificho' kwa aina flani. Simlazimishi mtu kunitafsiri tofauti, kwa sababu siishi kwa kumridhisha mtu flani bali Mola wangu pekee.

Mwisho, ni vema kwa mtu huyo kutambua madhara ya TROLLING. Pengine kwa huko nyumbani ni jambo la kawaida kumsambulia mtu mtandaoni pasi sababu lakini kwa wenye uelewa wa sheria za mtandaoni wanafahamu athari za kudhani ukiwa kwenye keyboard ya kompyuta yako una uhuru wa kuandika chochote kile hata kama kina madhara ya kisheria. Ukweli kwamba hakuna Mtanzania hata mmoja aliyewahi kuchukuliwa hatua za kisheria kwa 'kashfa mtandaoni' sio sababu ya kumwaminisha mtu kuwa kashfa mtandaoni sio kosa kisheria. Japo sitamani kuwa Mtanzania wa kwanza kumchukulia hatua za kisheria mtu anayenikashifu mtandaoni, lakini pindi ikibidi nitafanya hivyo ili iwe fundisho kwa kila anayedhani TROLLING ni ruksa kwa Watanzania.

Mwisho kabisa ni wito wangu kwa Watanzania wenzangu hasa mtandaoni. Tusikatishane tamaa kwa sababu ya chuki binafsi. Kama mtu anajituma kufanya jambo flani iwe lake binafsi au kwa maslahi ya taifa lake basi kama haiwezekani kumsapoti basi ni vema kukaa kimya tu. Kwanini ukerwe na jambo lisilokuhusu? Ni matumaini yangu kuwa waraka huu utasaidia sio tu kupunguza chuki zisizo na msingi mtandaoni bali utasaidia kuhamasisha mapambano dhidi ya TROLLS. Kamwe usiumie kimyakimya mtu anapokubughudhi mtandaoni, maana hicho ndicho kinachowapa nguvu TROLLS-kukuona unateseka kimyakimya. Ni muhimu kukabiliana nao hata kama silaha yao kuu ni kashfa na matusi. Kuna sheria kali tu dhidi ya watu wa aina hiyo, na ikibidi ni muhimu kujikinga au kutafuta haki kwa kutumia sheria hizo.

Pia napenda kuwashukuru TROLLS hao wawili, aliyepost tweet ya kejeli na huyo aliye-RT. Japo kitendo chao kimenisikitisha lakini kwa upande mwingine kimenihamasisha. You see, kama kuna mtu anakerwa na jambo zuri unalofanya kwa ajili yako au kwa ajili ya jamii, njia bora ya kumdhibiti sio kuacha jambo hilo bali kuliendeleza zaidi. Labda siku moja atachoka kuwa hater, au pengine atakufa kwa presha kutokana na mwendelezo wako katika jambo hilo.

I hope ujumbe umefika kwa wahusika, na samahani kwa waraka huu mrefu.

PEACE AND LOVE 


25 Apr 2014

NI dhahiri sasa kuwa mjadala wa Katiba mpya, hususan kipengele cha muundo wa Muungano, unaelekea kulipeleka taifa mahali pabaya. Japokuwa dalili za Bunge Maalumu la Katiba linaweza kuishia kuwa jukumu ghali kwa walipakodi masikini, hasa baada ya kusikika madai ya baadhi ya wajumbe wa Bunge hilo kuwa posho ya shilingi 300,000 kwa siku haitoshi, lakini Watanzania wengi walikuwa na imani kwamba ‘upepo huo mbaya’ ungepita na hali ingekuwa shwari.
Hata hivyo, kadiri siku zinavyozidi kwenda ndivyo hali inavyozidi kuwa mbaya. Kinacholeta wasiwasi zaidi kwa sasa ni kuibuka kwa dalili za ubaguzi wa waziwazi, sambamba na jitihada hatari za kumwaga petroli kwenye moto kwa kuingiza udini kwa nguvu kwenye siasa.
Lakini pasi ‘kuuma maneno’ naomba nielekeze lawama zangu kwa Rais Jakaya Kikwete na chama chake - CCM. Pamoja na wasiwasi uliokuwepo awali, kwamba huenda Rais Kikwete angeendeleza desturi iliyoota mizizi ndani ya CCM kwamba kila wazo lililoanzia vyama vya upinzani (kama hilo la umuhimu wa kuwa na Katiba mpya) ni baya, na hivyo angekwamisha uwezekano wa kupata Katiba mpya, alitushtua wengi alipoonyesha dalili za kuwa amepania kwa dhati kuweka historia kwa kufanikisha suala hilo muhimu.
Mambo yalionekana kwenda vizuri licha ya jitihada za hapa na pale ndani ya CCM kulifanya suala la Katiba mpya kuwa la kiitikadi zaidi kuliko la kitaifa. Wengi mtakumbuka vijembe walivyopigwa baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani walipotaka kukutana na Rais Kikwete. Badala ya kupongeza kile kilichoonekana kama mwanzo mpya wa siasa za maridhiano, baadhi ya wanasiasa huko CCM waliwakebehi wapinzani kuwa wanataka kwenda Ikulu kunywa chai tu!
Dalili za mwanzo kuwa hatma ya suala la Katiba mpya ipo shakani zilianza kujichomoza zaidi baada ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, chini ya Jaji Joseph Warioba kuweka hadharani Rasimu ya Kwanza ya Katiba mpya, ambapo pendekezo la muundo wa Muungano wa Serikali tatu liliwekwa bayana. Taratibu, CCM, chini ya uongozi wa Kikwete, ilianza harakati za chini chini kujaribu kuingilia mchakato wa Katiba mpya, ikiwa ni pamoja na jitihada za kubinafsisha mchakato huo.
Lakini Mungu si Athumani au John, pamoja na vizingiti vya hapa na pale, hatimaye Rais Kikwete alitangaza majina ya wajumbe 201 kutoka makundi mbalimbali ya jamii, kuingia katika Bunge la Katiba. Lakini kabla ya hapo, tayari Rais Kikwete alishatangaza mkoani Mbeya wakati wa maadhimisho ya kuzaliwa kwa CCM kwamba msimamo wa chama hicho ni Serikali mbili. Japo alitangaza msimamo huo kama Mwenyekiti wa taifa wa CCM, katika mazingira ya kawaida tu, isingewezekana kuwapo kwa mitizamo tofauti kati ya Kikwete wa CCM na Kikwete Rais.
Kuanzia hapo ikawa kama ‘jini lililopo kwenye chupa’ (a genie in the bottle) limefunguliwa. Zikaanza harakati za waziwazi ‘kulazimisha’ matakwa ya chama tawala kwamba muundo wa Muungano lazima ubaki kuwa wa Serikali mbili. Mara zikapatikana taarifa kuwa CCM imetengeneza rasimu yake ya siri.
Mara tu baada ya kikao cha Bunge Maalum la Katiba kuanza, ishara kuwa hali huko mbele inaweza kuwa si shwari zikawa zinajitokeza kila kukicha. Baada ya mshikemshike wa madai ya posho, likaibuka suala la utaratibu wa kupiga kura (yaani kura zipigwe kwa usiri au uwazi.)
Lakini kwa vile tangu awali CCM walionyesha kuwekeza nguvu zao kubwa katika suala la muundo wa Muungano wakitaka Serikali mbili, suala hilo limeteka takriban kila kipengele cha Katiba mpya, na kwa bahati mbaya au makusudi, mjadala wa muundo wa Muungano unazidi kutishia umoja na mshikamano wa taifa letu.
Japo lugha za matusi na kashfa si jambo geni kwenye vikao vya Bunge la Jamhuri, hali imezidi kuwa mbaya kwenye kikao cha Bunge Maalumu la Katiba, tunasikia baadhi ya wajumbe wakiwatuhumu wenzao kuwa mashoga, huko wengine wakienda mbali na kuhoji Uafrika wa wenzao. Lakini kama nilivyobainisha hapo juu kuwa tumeshazoea matusi na lugha chafu bungeni, kuna waliokuwa na imani kuwa “wakimaliza kutukanana, watarejea kwenye suala lililowakutanisha huko Dodoma.”
Mara vikaanza kuibuka vitisho kuwa iwapo Katiba mpya itaridhia Serikali mbili, jeshi litatwaa madaraka. Na aliyeanzisha vitisho hivi si mwingine bali Rais Kikwete katika hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge hilo la Katiba, wiki chache zilizopita.
Lakini wakati Rais Kikwete aliliongelea suala hilo katika jukwaa la kisiasa (bungeni), mmoja wa wasaidizi wake akaamua kulitoa suala hilo katika anga za siasa na kulipeleka kwenye nyumba za ibada. Hapa ninamzungumzia William Lukuvi.
Inaniwia vigumu kupata maneno stahili ya kumwelezea mwanasiasa huyo ambaye ghafla ametokea kuwa mtu mwenye kauli chafu, hatari na za kiharamia.
Huyu mtu bila aibu wala uoga amediriki kwenda kanisani na kutangaza waziwazi kuwa jeshi litaasi pindi uamuzi wa kuwa na Serikali tatu utakapopitishwa. Naomba nitamke bayana kwamba nahisi Lukuvi ana matatizo kutokana na hatua yake ya kwenda kanisani kufanya mahubiri ya kushawishi jeshi kuasi.
Lakini anayempa jeuri Lukuvi ni Rais Kikwete, kwani naye aligusia suala hilo kwenye hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge la Katiba. Kwa hiyo anachofanya Lukuvi ni kusambaza tu ujumbe ulioanzishwa na Rais Kikwete.
Na wakati Rais Kikwete akiwakemea “wanasiasa wanaomtukana Nyerere na Karume” amekalia kimya matusi ya Lukuvi kwa Mwenyezi Mungu (naam, kutumia nyumba ya ibada kujenga chuki na kuhamasisha uasi wa jeshi ni matusi kwa Mungu.)
Ni watu wenye upeo mdogo tu watakaochukia kusikia kwamba Nyerere na Karume wana mchango katika matatizo tuliyonayo kuhusu Muungano, hasa kwa uamuzi wao wa kulifanya suala hilo kama lao binafsi bila kuangalia madhara yake miaka kadhaa ijayo.
Mara kadhaa Rais Kikwete amekuwa akiasa kuhusu athari za kuchanganya siasa na dini. Amewahi kudai kuwa kuna maadui wa nje wanaotumia suala la dini kwa minajili ya kututenganisha.
Lakini kipi cha kushangaza ilhali kwenye chaguzi kadhaa wamekuwa wakitumia nyumba za ibada kupandikiza chuki dhidi ya wapinzani wao?
Japo hainisumbui sana iwapo Katiba mpya haitopatikana, napata wasiwasi kuona uhuni wa kisiasa (political thuggery) ukihalalishwa kwa kisingizio cha ‘kuhubiri athari za Serikali tatu.’
Lakini nani wa ‘kuokoa jahazi’? Rais Kikwete anakemea wanaowatukana Nyerere na Karume, lakini anapuuza matusi ya wasaidizi wake kwa Jaji Warioba.
Nimalizie makala hii kwa kumkumbusha Rais Kikwete kwamba mwakani ataondoka madarakani na kurejea uraiani. Asipotengeneza mazingira mazuri kwake na kwa Watanzania, janga hili linalopikwa na akina Lukuvi litamwathiri naye pia.
Ni muhimu kwa Rais kuweka kando ushabiki wa kisiasa na kuchukua hatua za makusudi kuepusha nchi kutumbukia kwenye machafuko yanayochochewa na mahubiri ya ubaguzi na kuitumia dini kwa minajili ya kisiasa.

18 Apr 2014

NIANZE kwa kutoa pole kwa Watanzania kwa janga la mafuriko ambalo linaendelea kusababisha madhara makubwa katika maeneo mbalimbali huko nyumbani.
Japo taarifa zinazosikika zaidi kuhusu mafuriko hayo ni za hali ilivyo Jijini Dar es Salaam, taarifa zinaonyesha kuwa janga hilo linaendelea kusababisha madhara katika sehemu nyingine mbalimbali za nchi yetu.
Kwa vile Taifa bado lipo katika kipindi cha majonzi kufuatia wenzetu kadhaa waliokwishapoteza maisha kutokana na mafuriko hayo, sambamba na maelfu waliopoteza mali zao, inaweza kuwa si wakati mwafaka sana kuanza kunyoosheana vidole. Hata hivyo, kituko kimoja kilichojitokeza mwishoni mwa wiki iliyopita kinaleta haja ya kuwekana sawa wakati tunakabiliana na janga hili.
Jumamosi iliyopita, kulipatikana taarifa iliyoambatana na picha inayomwonyesha Mstahiki Meya wa Manispaa ya Ilala, Jerry Silaa, akiwasili mjini Mwanza kwa shughuli za kichama. Ikumbukwe kwamba siku hiyo hali ilikuwa mbaya sana Jijini Dar es Salaam kutokana na mafuriko yaliyosababishwa na mvua kubwa zinazoendelea kuonyesha sehemu mbalimbali huko nyumbani.
Ili kukupa mlolongo sahihi wa matukio, naomba ninukuu kauli husika kuhusiana na tukio hilo. Awali, kutokana na kushangazwa na uwepo wa Meya Silaa jijini Mwanza huku wananchi wake wakikabiliwa na janga la mafuriko, nilibandika picha iliyoambatana na maelezo
Meya wa Ilala Jerry Silaa katika shughuli za kichama muda huu huko Mwanza,” na kuuliza “Mheshimiwa, una taarifa za mafuriko Dar?” Kisha nikaandika tena, “Hawa ndio viongozi wenu. Manispaa ya Ilala ipo katika mafuriko, Meya wa Ilala Jerry Silaa yupo kichama Mwanza.
Baada ya muda mfupi, Meya Silaa alijibu, namnukuu,
Nakuomba radhi kama ungependa niwe Dar nikizuwia mvua isinyeshe.” Kisha akaandika tena “I hate cheap politics (nachukia ‘siasa nyepesi’). Mabonde yote yamejengwa. Mnategemea mito itapumulia wapi? I have remarkable record kwenye rescue missions (nina rekodi ya kupigiwa mfano kwenye jitihada za uokoaji.)” Lakini hakuishia hapo, akaendelea kudai kwamba, “Kwangu wahanga (wa mafuriko) ni kwa wanaoathirika kwa madaraja kukatika iliyosababishwa na watu kujenga mabondeni.” Na katika ‘kuhitimisha’ mjadala huo, Meya Silaa akatoa tuhuma kwamba “Najua viongozi wengi huwa wanaombea watu hata wafe wakabebe jeneza kuonekana wanajali lakini ni unafiki.”
Naomba niweke wazi ya kuwa sina tatizo na Meya Silaa binafsi ila kwa hakika kauli zake zilizosheheni dharau na kiburi zilinikera sana. Na si mimi pekee bali Watanzania kadhaa katika mitandao mbalimbali ya kijamii pia walishutumu kauli za kiongozi huyo wa Manispaa ya Ilala.
Hata hivyo, pamoja na ushauri wa wengi kwamba hata kama hakuwa na nia mbaya katika kauli hizo basi labda aombe radhi, Mheshimiwa huyo alipuuzia ushauri huo. Mie ni muumini mkubwa wa uhuru wa kujieleza. Hata hivyo, ni muhimu kutambua kwamba uhuru pasi nidhamu ni uhuni. Japo kila kiongozi ana uhuru wa kujieleza kama mwananchi yeyote yule, uhuru huo unaambatana na wajibu wa kiongozi husika kwa umma.
Kwa busara za kawaida tu, shughuli za kichama zilizompeleka Meya Silaa huko Mwanza hazikuwa na uzito mkubwa zaidi ya janga la mafuriko Jijini Dar es Salaam ambapo manispaa ya mheshimiwa huyo ilikuwa ni miongoni mwa maeneo yaliyoathiriwa sana.
Lakini busara zaidi zingeweza kutumika baada ya mheshimiwa kutambua kuwa suala hilo limezua hisia hasi miongoni mwa wananchi, na angeweza kujibu kistaarabu tu, kwa mfano, “ninatarajia kurejea Dar es Salaam  haraka kushirikiana na wananchi wenzangu katika janga hili” badala ya kauli ya kebehi kuwa ‘anaomba radhi kwa anayependa awepo Dar es Salaam  kuzuwia mvua isinyeshe.’
Hivi Rais Jakaya Kikwete alipofanya ziara ya maeneo mbalimbali yaliyoathiriwa na mafuriko hayo alifanya hivyo ili kuzuwia mvua au mafuriko hayo? Na je Makamu wa Rais Dk. Bilal na viongozi wengineo walionusurika katika ajali ya helikopta wakati wakitaka kuanza ukaguzi wa athari za maafa ya mafuriko walitarajia wangezuwia mafuriko hayo?
Ninaamini Meya Silaa anafahamu fika kwamba tunapokwenda kuwajulia hali wagonjwa haimaanishi kuwa tutawaponyesha, tunapokwenda misibani haimaanishi kuwa tutawafufua marehemu. Kumjulia hali mgonjwa au kujumuika msibani ni ustaarabu tuliyojijengea katika mila zetu kuonyesha kuwa TUNAJALI. Na kisaikolojia inaonyesha kuwa mhanga wa tukio lolote lile hupata faraja pindi anapotambua kuwa kuna wanaomjali.
Katika moja ya majibu yangu kwake, nilimfahamisha bayana Meya Silaa kwamba tatizo kubwa la wengi wa viongozi wetu ni kuzowea kusifiwa tu lakini wakikosolewa hukimbilia kudai ni ‘cheap politics.’
Waingereza wanasema “wrong is just that, wrong” (kisicho sahihi kipo hivyo hivyo, hakipo sahihi). Kiongozi kuzipa kipaumbele shughuli za kichama ilhali wananchi wanahangaika na janga la mafuriko si sahihi, na hakuna excuse katika mazingira ya aina hiyo.
Japo Meya Silaa anaweza kuwa sahihi kulaumu ujenzi wa mabondeni kama moja ya sababu zinazochangia mafuriko, lakini kwa hakika mamlaka husika kwa mfano Manispaa ya Ilala inayoongozwa na Meya Silaa zinahusika kwa namna moja au nyingine. Kuwalaumu tu wakazi wa mabondeni hakuwezi kuleta ufumbuzi wa tatizo. Ni muhimu kuelewa kwanini wakazi hao wa mabondeni wanaendelea kuishi maeneo hayo licha ya tishio la mafuriko.
Kwa uelewa wangu, wengi wao ni masikini ambao wanaoishi katika ‘nyumba za mbavu za mbwa’ na ni vigumu mno kwao kumudu kununua ama kujenga nyumba bora katika maeneo salama, achilia mbali huo uwezo wa kununua japo kiwanja.
Lakini eneo jingine ambalo pengine Meya Silaa hawezi kuligusia ni ujenzi unaokiuka taratibu za mipango-miji, unaofanywa na matajiri ambao fedha zao zinawawezesha kupindisha kila aina ya sheria. Wanaoishi mabondeni ni wahanga wanaathiriwa zaidi na kanuni za kiasili za maji kujaa kwenye mabonde, lakini ujenzi holela unaoathiri mfumo wa maji taka ni uingiliaji wa makusudi wa jitihada za binadamu kukabiliana na mafuriko.
Mvua ikinyesha maji yanajaa, na kwa vile mitaro inayopaswa kuyaongoza maji hayo katika maeneo maalumu imezibwa, maji hayo yatamwagikia eneo lolote lile, hata kama si bondeni.
Kuhusu kauli za Meya Silaa, nilimfahamisha kwamba ana bahati ni meya wa manispaa nchini Tanzania kwani laiti angekuwa  meya kwa hapa Uingereza, kisha akaenda mji mwingine kwa shughuli za kichama ilhali wananchi wake wanakabiliana na janga la mafuriko, kungekuwa na uwezekano mkubwa wa harakati za kumng’oa madarakani. Moja ya sifa ya uongozi si tu kujali wananchi bali pia kuonyesha uongozi hasa katika nyakati za majanga.
Kauli hizo zisizopendeza za Meya Silaa zimekuja katika kipindi ambacho Taifa letu lipo katika mchakato wa kupata Katiba mpya. Pengine tukio hili laweza kuwa angalizo muhimu kuhusu Katiba hiyo mpya.
Kwa mfano, je, Katiba hiyo itamwezesha mwananchi wa kawaida kumwajibisha kiongozi ‘mwenye kauli zisizofaa’? Suala hapa si tu katika kauli za kiongozi (iwapo zinafaa au la) bali suala zima la uwajibikaji.
Nimalizie makala hii kwa kurejea kauli ya Rais Jakaya Kikwete wakati alipofanya ziara katika maeneo mbalimbali kuangalia athari za mafuriko, kwamba “mafuriko hayaepukiki na wajibu wa Serikali ni kuwasaidia waathirika.”
Mafuriko kama maji kujaa kutokana na wingi wa mvua hayaepukiki, lakini mafuriko kama ukosefu wa miundombinu bora ya kukabiliana na mafuriko ni suala lililo ndani ya uwezo wetu. Kuna tofauti kati ya mafuriko yanayosababishwa na maji kuvuka kingo za Mto Kilombero huko Ifakara, na mafuriko katika maeneo yasiyo mabondeni jini Dar yanayochangiwa na mfumo duni wa kushughulikia majitaka.
Na japo ninaafikiana na kauli ya Rais kwamba wajibu wa serikali ni kuwasaidia waathirika (sijui ni wapi hao tukirejea kauli ya Meya Silaa) lakini kuna mengi yaliyo ndani ya uwezo wa serikali yanayoweza kupunguza idadi ya waathirika wa majanga kama mafuriko. Kubwa zaidi ni kujijengea uwezo wa kukabiliana na majanga badala ya kusubiri janga litokee ndipo tuanze kutafutana. 


13 Apr 2014



Huu ni mtizamo wangu, na nilimfahamisha Mstahiki meya Jerry Silaa pia: huyu mtu ana bahati sana kwamba ni Meya wa manispaa nchini Tanzania, ambapo ukisahapata uongozi upo huru kufanya lolote lile- baya au zuri, la busara au la kipuuzi- pasi kuchelea matokeo. Laiti huyu mtu angekuwa Meya wa eneo lolote lile hapa Uingereza, basi Jumatatu angekumbana na wito wa kumtaka aachie ngazi. Ndio, uwepo wake Dar (Ilala) usingezuwia mafuriko, lakini sote twatambua kuwa nyakati za majanga zinahitaji viongozi kuonyesha uongozi kwa dhati (showing leadership). Kilichompeleka Mwanza ni shughuli za kichama, ambazo ninaamini zingeweza kusubiri hadi janga linalowasibu anaowaongoza limeshughulikiwa. 

Japo mwanzoni alileta majibu ya dharau baada ya kusoma 'tweets' hizo mbili za mwanzo hapo juu, lakini akakumbana na hasira za wananchi wengi ambao hawakupendezwa na majibu yake. Lakini kwa vile neno 'samahani' halipo kwenye kamusi za wengi wa viongozi wetu, Mstahiki Meya 'aliingia mitini' kimyakimya...na hajaonekana tena huko twitter hadi wakati ninaposti bandiko hili.

Swali la msingi: Hivi Katiba Mpya tunayohangaika kuipata huko Dodoma itaweza kweli kutengeneza mazingira yatakayowawezesha wananchi kuwashughulikia 'wahuni wa kisiasa' (political thugs)? Jeuri kubwa inayowafanya watawala wetu kufanya (including kusema) chochote ni kutochelea matokeo. Na japo Katiba tuliyo nayo sasa ina sheria nzuri tu za kumpatia mwananchi kile anachostahili (kwa maana ya haki zake), tatizo limebaki katika usimamizi wa sheria hizo, na pengine kubwa zaidi, sheria hizo kubaki kama maandiko tu yasiyoheshimiwa. Je Katiba Mpya (laiti ikipatikana) itaheshimiwa?

Finally, ninaamini Mstahiki Meya Silaa nafsi itamsuta na atakatisha ziara yake huko Mwanza na kuungana na wananchi katika harakati za kukabiliana na athari za mafuriko Dar (kwa yeye ni Manisapaa ya Ilala). See, kwenda kumwona mgonjwa hakumaanishi kutamfanya aopone bali kwaonyesha kuwa flani anajali. Kadhalika, tunapokwenda kwenye misiba haimaanishi kuwa tutamfufua marehemu, lakini ile tu kuwafariji wafiwa kunaonyesha kuwa tunajali. Nam ,Meya Slaa akiwa Illa/Dar hatozuiwa athari za mafuriko (au kama alivyosema mwenyewe "hawezi kzuwia mvua") lakini kibanadamu tu anapaswa kuwa na wahanga wa mafuriko (japo yeye ana-pick and choose nani anastahili kuitwa mhanga).

11 Apr 2014

KWA familia nyingi huko nyumbani, takriban kila usiku huambatana na kukusanyika mbele ya runinga kuangalia tamthilia mbalimbali.
Hali kama hiyo hujitokeza pia mchana wa mwisho wa wiki ambapo tamthilia hizo hurejewa kwa kujumuisha ‘vipande’ vya wiki nzima.
Nyingi ya tamthilia hizo huwa katika lugha ya kigeni, lakini wengi wa wanaozifuatilia wanamudu kuzielewa bila matatizo. Hata hivyo, yayumkinika kuhisi kwamba hata magwiji wa ufuatiliaji wa tamthilia hizo sasa wanapata wakati mgumu si tu kufuatilia bali hata kuelewa ‘tamthilia’ nyingine ndefu inayoendelea huko Dodoma. Hapa ninamaanisha kikao cha Bunge Maalumu la Katiba.
Pengine ni vema nikawakumbusha wasomaji msimamo wangu kuhusu suala la Katiba mpya, ambao nimeutanabahisha katika makala zangu kadhaa zilizopita.
Kwanza, pamoja na kutambua haja ya kuwa na Katiba bora zaidi ya tuliyonayo sasa, ukweli kwamba matatizo mengi yanayoikabili nchi yetu hayatokani na ukosefu wa sheria bali usimamizi na utekelezaji wake, sioni jinsi Katiba mpya (kama itapatikana) itakavyoweza si tu kuwa ‘mwarobaini’ wa matatizo yetu bali pia kuheshimiwa.
Pili, muundo wa Muungano ndio suala linaloonekana kutawala mjadala wa Katiba mpya, na ninarejea tena kukiri kwamba ninachoona muhimu kwangu si idadi ya serikali zinazounda Muungano- ziwe mbili kama ilivyo sasa, tatu kama ilivyopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, au hata serikali moja kama inavyodaiwa kuwa ndio ‘muundo halisi’ wa Muungano- bali jinsi serikali husika inavyoweza kutimiza majukumu yake na kuwahudumia Watanzania kwa ufanisi.
Kwahiyo basi, kwa lugha nyepesi, msimamo wangu katika suala hili la muundo wa Muungano ni “wowote ule utakaowapatia Watanzania wanachostahili.” Na kwa hakika, malumbano yanayoendelea kuhusu suala hili la muundo wa Muungano yamegubika masuala mengine muhimu yaliyoleta haja ya kuwa na Katiba mpya.
Sasa, kwa vile mazingira yanaashiria kwamba kupatikana au kutopatikana kwa Katiba mpya kunategemea muafaka katika suala hilo la muundo wa Muungano, basi hata sie ‘tusiolitilia maanani sana’ tunalazimika kulijadili kwa marefu na mapana. Hiki ni kikwazo ambacho bila kukivuka chaweza kuondoa uwezekano wa kupatikana Katiba mpya.
Mwanzoni mwa makala hii, nimefananisha kikao cha Bunge Maalumu la Katiba na tamthilia. Lakini kichekesho ni kwamba wakati tamthilia nyingi za kigeni zinazotawala kwenye runinga za huko nyumbani zinaeleweka licha ya kuwa katika lugha za kigeni, hii ya Bunge la Katiba si tu inazidi kutoeleweka bali inapoteza ladha kila kukicha.
Hakuna haja ya kurejea mlolongo wa matukio yaliyokwishakujitokeza katika Bunge hilo, hasa kwa vile takriban yote yanakera; kuanzia madai ya nyongeza ya posho hadi Bunge hilo kugeuka ulingo wa kuonyeshana umahiri wa vijembe na lugha zisizopendeza.
Lakini sasa kuna suala jipya ambalo si tu linazidisha ugumu wa mjadala wa muundo wa Muungano bali pia linatishia hata uhai wa Muungano wenyewe. Suala hili ni nyaraka mbalimbali za kuthibitisha uhalali/uhalisia wa Muungano.
Ningependa kukiri kwamba sielewi nyaraka hizo za Muungano ni ngapi, lakini ninachofahamu ni kwamba moja ni hiyo inayofahamika kama Hati ya Muungano. Sasa, katika mazingira yanayoweza tu kuonekana katika filamu ya kutisha (horror movie), sahihi ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere inaonyesha dalili ya ‘kuchakachuliwa.’ Mlolongo wa maswali unaibuka hapo: je, sahihi hiyo imechakachuliwa au hati nzima imechakachuliwa na ndiyo maana sahihi inazua utata? Nani aliyefanya ‘uhuni’ huo? Na kubwa zaidi, kwa nini?
Lakini ukidhani kizaazaa pekee ni katika suala hilo la sahihi ya Nyerere tu, basi subiri mpaka utakapofahamu kwamba madai kuwa Hati ya Muungano ambayo awali ilidaiwa ipo Umoja wa Mataifa (UN) nayo yana walakini baada ya UN kudai haina hati hiyo. Swali jingine, iko wapi? Kwa nini ilidaiwa ipo UN ilhali si kweli? Nani huyo anayedanganya? Kwa nini?
Kabla ya kuandika makala hii nimekutana na maelezo ya mchambuzi mmoja kwenye mtandao mmoja wa kijamii akieleza kwamba kwa uelewa wake, hati iliyowasilishwa katika Bunge Maalumu la Katiba huko Dodoma, na yenye sahihi za Nyerere na Pius Msekwa sio ‘Hati ya Muungano’ (Articles of the Union) bali ni Sheria ya Muungano (the Act of the Union) iliyotungwa na Bunge wakati huo kupitisha Articles of the Union, na kusainiwa na Nyerere na Msekwa (kama Katibu wa Bunge wakati huo).
Na hata hati hiyo ingekuwa ndio Hati halisi ya Muungano, bado kuna tatizo jingine la sahihi za Nyerere na Msekwa kuwa na walakini. Kadhalika, inaelezwa kwamba hati hiyo imeongezwa maneno ‘kwa kompyuta’ japo kila mwenye uelewa anafahamu kwamba kompyuta hazikuwapo nchini katika miaka hiyo ya 1960.
Mchambuzi huyo anahitimisha kwamba hati ‘zilizotoweka’ ni nakala halisi ya Serikali ya Tanganyika, nakala halisi ya SMZ, nakala halisi ya Bunge la Tanganyika, nakala halisi ya Baraza La Wawakilishi, nakala halisi ya Mwanasheria Mkuu, nakala halisi ya Nyerere, na nakala halisi ya Karume.
Maswali kadhaa yanajitokeza, ikiwa ni pamoja na, je nakala hizo ‘zimetoweka’ kweli au hazijawahi kuwapo? Nani anahusika na kutoweka huko? Kwa nini? Na maswali mengine lukuki.
Vilevile, gazeti moja la Kiingereza la huko nyumbani, katika toleo lake la juzi, liliripoti kwamba aliyekuwa Katibu wa kwanza wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Salum Rashid, alieleza kwamba Mzee Karume hakuwahi kusaini hati yoyote kuhusu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Utata huo unaogubika uhalali na/au uhalisia wa Muungano umenifanya kuhisi kwamba kuna mtu/watu fulani mahala fulani anadanganya/wanadanganya. Swali: ni nani? Na kwa nini anadanganya/wanadanganya?
Niliwahi kuandika katika moja ya makala zangu huko nyuma kwamba pamoja na nia nzuri ya kuunganisha Tanganyika na Zanzibar, Nyerere na Karume walikosea kufanya suala hilo kama la ‘wao binafsi’ na si la Watanganyika na Wazanzibari wote.
Pamoja na dhamira zao nzuri, sidhani kama viongozi hao waliangalia mbali zaidi ya ajenda ya umoja na mshikamano, hivyo kutotilia maanani uwezekano wa matatizo ya kisheria au hata ridhaa ya wananchi huko mbele. Na, binafsi naona mapungufu haya kama moja ya vyanzo vikuu vya matatizo ya Muungano.
Lakini pengine badala ya kuwalaumu waasisi hao wa Muungano ni muhimu kutambua mazingira ya kisiasa ya wakati huo. Hicho kilikuwa kipindi cha kujenga Taifa, huku mfumo wa kisiasa ukiwa hauruhusu mawazo tofauti na ya watawala. Hivi tumeshawahi kujiuliza wazo la kuunganisha Tanganyika na Zanzibar lilikuwa la kidemokrasia kiasi gani, kwa maana ya kusaka ridhaa ya wadau halisi wa Muungano huo, yaani Watanganyika na Wazanzibari?
Kwa bahati mbaya (au kwa makusudi), kwa kiasi kikubwa chama tawala CCM kinataka kurejea kosa hilohilo lililopelekea kuzaliwa Muungano ‘wenye matatizo.’ Wanataka kulazimisha matakwa yao ya muundo wa Muungano wa serikali mbili. Kuna busara moja inafundisha hivi, “Si kila tendo jema ni sahihi. Kwa mfano, kumpa chakula ‘kigumu’ mtu mwenye njaa ni tendo zuri, lakini kumpa chakula kingi kigumu mtu mwenye njaa kali ni hatari kwani inaweza kumfanya mtu huyo kuvimbiwa na hata kupoteza maisha.”
Dhamira ya CCM kutaka kunusuru muundo wa sasa wa Muungano (wa serikali mbili) inaweza kuwa nzuri. Lakini kulazimisha dhamira hiyo (pasi kujali uzuri wake) ni jambo hatari. Na hata kama CCM walitaka kulazimisha dhamira yao hiyo basi angalau wangejiandaa vya kutosha badala ya kukurupuka, na sasa tunashuhudia matatizo mengine makubwa zaidi yanayozua utata wa Muungano mzima wanaotaka kuinusuru.
Nihitimishe kwa kuishauri CCM na wote wanaotaka kulazimisha muundo wa Muungano wa serikali mbili, kwamba suluhu pekee ni kwa suala hilo kupelekwa kwa wananchi ili hatimaye waamue kuhusu muundo wa Muungano wanaotaka. Na si tu kulipeleka suala hilo kwa wananchi bali pia kutowatisha kwa minajili ya kuwalazimisha wafuate matakwa ya chama hicho tawala.
Ni ushauri mwepesi lakini kila anayeijua CCM anafahamu kuwa ni chama ‘kisichoshaurika’ wala ‘kuambilika.’ Kwao, wapo tayari Watanzania wakose Katiba mpya iwapo dhamira ya chama hicho kung’ang’ania muundo wa Muungano wa serikali mbili itakwama.
Kama ambavyo hata tukipata Katiba mpya inaweza kutokuwa na manufaa pasipo nia ya dhati kuiheshimu na kuitekeleza kwa ufanisi, pasipo nia ya dhati ya kusaka muafaka katika suala la muundo wa Muungano na hatma ya Katiba mpya kwa ujumla, kikao cha Bunge Maalumu la Katiba kitaishia kuwa tamthilia ambayo si tu inakera bali pia ya gharama kubwa kwa wananchi.
PENYE NIA PANA NJIA

5 Apr 2014


Kimsingi, mchakato wa kupata Katiba mpya umegeuka kuwa hukumu ya Muungano wa 'Tanganyika' (Tanzania Bara) na Zanzibar. Mengi yamesahongelewas na nisingependa kuyarudia hapa, lakini suala jipya lililojitokeza ni sahihi za Marehemu Baba wa Taifa na Marehemu Karume.

Kuna taarifa kwamba baadhi ya nyaraka hazina sahihi ya Marehemu Karume, hali inayoweza kuashiria kuwa uamuzi wa Muungano ulifanywa na Nyerere pekee. Japo historia inaeleza tofauti, kwa kawaida, hati ya mkataba huwa na angalau na sahihi za wahusika wawili au zaidi kutegemea mazingira ya mkataba husika.

Lakini hata hiyo sahihi ya Nyerere yenyewe imezua utata. So far, kuna sahihi mbili (yawezekana zipo nyingine). Lakini sio tu sahihi kuwa zaidi ya moja, katika moja ya nyaraka za Muungano kuna maneno yameongezwa. Maelezo yanayotolewa ni kuwa kompyuta ilitumika...bila hata kuuliza kompyuta ilitumika kwa malengo gani, swali la msingi ni je Tanzania- au Tanganyika ilikuwa na kompyuta mwaka 1964?

Licha ya sahihi ya Nyerere, kuna taarifa pia ikwamba hata sahihi ya Katibu wa Bunge wa wakati huo, Pius Msekwa nayo ina walakini. 

Mara kadhaa katika maandiko yangu nimebainisha kuwa haileti maana kujadili muundo wa Muungano pasipo wajjumbe wa Bunge la Katiba kupatiwa nyaraka muhimu zinazohusu Muungano huo. Maelezo yaliyotolewa na wahusika ni kwamba eti kuna nakala moja tu ya moja ya nyaraka muhimu za Muungano, kwahiyo haiwezi kupelekwa Dodoma kwa kuhofia inaweza kupotea. Huu sio utoto tu bali ni ubabaishaji wa hali ya juu. Kwanini wahusika wasichapishe nakala kisha kuzi-certify as true copies of the original?

Anyway, hebu analia katika picha ya hapo juu kuhusu ipi ni sahihi halisi ya Mwalimu Nyerere.

Nihitimishe bandiko hili kwa kuyumkinisha kuwa utata unaojitokeza kuhusu nayaraka muhimu za Muungano unaashiria kwamba kuna mtu flani mahala flani anaongopa (someone somewhere is lying). Tusichojua ni kwanini?

TIME WILL TELL 

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.