19 Jan 2017

WAKATI Marekani ikijiandaa kwa sherehe ya kuapishwa kwa Rais Mteule Donald Trump hapo keshokutwa, rais huyo mteule amejikuta kwenye ‘kitimoto’ baada ya kumshambulia mjumbe wa Congress (bunge ‘dogo’ la nchi hiyo),mmoja wa wanasiasa wakongwe na mpinzani wa muda mrefu wa ubaguzi wa rangi, John Lewis.
Kama ilivyozoeleka, Trump alitumia akaunti yake katika mtandao wa kijamii wa Twitter kufanya mashambulizi hayo baada ya Lewis, ambaye anaheshimika mno nchini humo kwa kushirikiana na nguli wa haki za watu weusi, marehemu Dk. Martin Luther King, Junior, kueleza bayana kuwa hamwoni Trump kama rais halali wa Marekani. Pia alieleza kuwa itakuwa sio sahihi kukalia kimya ‘mambo yasiyopendeza’ ya Trump.
Kadhalika, Lewis alieleza bayana kuwa kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 30 hatohudhuria sherehe za kumwapisha rais mpya, na anasusia kuapishwa kwa Trump kama njia ya kuonyesha upinzani wake kwa rais huyo mpya.
Trump alimshambulia Lewis katika ‘tweets’ zake ambapo alidai kuwa mwana Congress huyo anapaswa kutumia muda mwingi zaidi kushughulikia eneo analoliwakilisha, ambalo kwa mujibu wa Trump, lipo katika hali mbaya na limegubikwa na uhalifu.
Tweets za Trump dhidi ya Lewis zilizosababisha watumiaji kadhaa wa mtandao huo wa kijamii kumlaani rais huyo mtarajiwa, hasa kwa vile wikiendi iliyopita ilikuwa ya maadhimisho ya kumbukumbu ya Dk. King, siku yenye umuhimu mkubwa kwa Wamarekani weusi.
Hayo yamejiri siku chache tu baada ya Trump kuwa katika ‘vita kubwa ya maneno’ dhidi ya ‘jumuiya ya ushushushu’ (intelligence community), taasisi 16 za ushushushu za nchi hiyo. Sababu kuu ya ‘ugomvi’ kati ya Trump na mashushushu hao ni taarifa iliyowasilishwa kwa Rais Barack Obama, na Trump mwenyewe, kuhusu hujuma za Urusi kwenye uchaguzi mkuu uliopita nchini Marekani.
Taarifa hivyo, ilitanabaisha kuwa Rais wa Urusi, Vladimir Putin ndiye aliyetoa maagizo ya ‘kumsaidia Trump’ na ‘kumuumbua Hillary Cinton, aliyekuwa mpinzani mkuu wa Trump.
Lengo la makala hii sio kujadili siasa za Marekani au vituko vya Trump, bali kutumia matukio hayo kuelezea hali ilivyo sasa huko nyumbani – Tanzania, ambapo kwa kiasi kikubwa suala la uwepo au kutokuwepo kwa baa la njaa linazidi kutawala duru za habari.
Kuna masuala kadhaa yanatokea kwa wakati mmoja. Kubwa zaidi ni kauli ya Rais Dk. John Magufuli sio tu kukanusha taarifa za uwepo wa baa la njaa bali pia kusisitiza kuwa ‘serikali haina shamba’ la kuiwezesha kuwapatia chakula wananchi wanaolalamikia njaa.
Jingine ni tishio kali kutoka kwa Rais Magufuli dhidi ya ‘magazeti mawili’ aliyodai yanaandika habari za uchochezi. Pia aliyashutumu kuwa yamenunuliwa na mfanyabiashara mmoja wa nafaka ili yaandike kuhusu taarifa za uwepo wa baa la njaa, kwa minajili ya mfanyabiashara huyo kuuza nafaka zake.
Binafsi sijashangazwa na tishio la Rais kwa magazeti. Uamuzi wake wa kukaa mwaka mzima bila kuongea na wanahabari ulipaswa kutufahamisha mtazamo wake kwa vyombo vya habari. Ikumbukwe kuwa hata wakati wa kampeni zake za urais mwaka 2015 hakufanya mahojiano na vyombo vingine vya habari, pengine ni kwa bahati tu, alifanya mahojiano na gazeti hili la Raia Mwema tu.
Na hii si mara ya kwanza kwa Rais kuvitupia lawama vyombo vya habari, wiki chache zilizopita alivishutumu kwa kumchonganisha na Rais mstaafu Jakaya Kikwete. Japo haikuwekwa wazi, lawama hizo zilitokana na habari zilizoandikwa na baadhi ya magazeti kuwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilikuwa na mpango wa kupiga mnada mizigo ya taasisi ya WAMA iliyo chini ya mama Salma Kikwete. Kusema magazeti yalizusha habari hiyo ni kuyaonea kwa sababu chanzo cha habari kilikuwa taasisi ya serikali, TRA.
Binafsi nabaki najiuliza, hivi kweli kama kuna magazeti yanalipwa kufanya uchochezi, yangekuwepo huru hadi kufikia hatua ya Rais ‘kuyananga’ bila kuyataja jina? Je, Idara Habari (MAELEZO) na wizara yenye dhamana ya vyombo vya habari, na waziri husika (Nape Nnauye) wamelala usingizi mzito kutojua hayo hadi Rais aliposhtuka na kuweka suala hilo hadharani?
Kwa mtazamo wangu, nadhani tishio la Rais limelenga kutisha vyombo vyote vya habari na sio magazeti hayo mawili tu. Kwamba wanahabari wasiandike kitu kisichompendeza Rais.
Rais hataki kusikia habari kuhusu tishio la baa la njaa. Hata wito wa viongozi wa kidini Wakristo na Waislam kuwataka waumini wao wafanye sala/dua kuombea mvua na kuepushwa na baa la njaa haujamfanya Rais kubadili msimamo wake.
Na muda mfupi kabla ya kuandaa makala hii nimeona video ya mkutano wa Rais huko Magu, ambapo wakati akihutubia, baadhi ya wananchi walisikika wakisema “njaa baba,” na Rais akawajibu “njaa… unataka nikakupikie mimi chakula?”
Binafsi sidhani kama Rais anahitaji ‘kisingizio’ cha kufungia magazeti, yawe mawili au yote. Lakini pia Rais asiwe mkosefu wa shukrani kwa mchango wa magazeti katika kumfikisha Ikulu, kwa kufikisha ujumbe wake binafsi na chama chake wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu mwaka 2015.
Lakini ni muhimu pia Rais atambue kuwa hizi sio zama za Radio Tanzania, Uhuru na Mzalendo, na Daily News na Sunday News pekee. Huu ni mwaka 2017, tupo katika zama za digitali ambapo upashanaji wa habari una njia lukuki, kuanzia Whatsapp hadi mitandao ya kijamii kama Twitter, Facebook, Instagram, nk. Katika zama hizi, kufungia chombo cha habari hakuzui usambazaji wa habari muhimu miongoni mwa wananchi.
Nihitimishe makala hii kwa wito huu kwa Rais wangu, mara kadhaa amekuwa akituomba sisi wananchi tumsaidie katika uongozi wake. Na moja ya misaada ambayo watu wengi wamekuwa wakimpatia ni kumsihi apunguze ukali, ajaribu kutumia lugha ya kidiplomasia, na asiogope kukosolewa.

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

12 Jan 2017

MIONGONI mwa kauli maarufu zaidi za Rais John Magufuli ni ile ya kuwaomba Watanzania wamwombee na msema kweli ni mpenzi wa Mungu.
Kwa bahati mbaya au pengine kwa makusudi, Rais amekuwa mtu wa kwanza kukiuka kauli hizo au kuziweka katika mazingira magumu kutekelezeka.
Nianze na hiyo kauli ya kuwataka Watanzania wamwombee. Pengine wakati ambao alielezea kwa undani mantiki ya kauli hiyo ni wakati wa uzinduzi wa bunge mwaka jana, ambapo alizungumzia kwa undani ugumu unaoikabili vita dhidi ya rushwa na ufisadi.
Katika hotuba hiyo, aliwafahamisha Watanzania kuwa wanaohusika na rushwa na ufisadi sio watu wadogo, kwa maana kwamba ni watu wenye uwezo mkubwa. Na kwamba licha ya dhamira yake na jitihada zake, angehitaji sio tu ushirikiano wa wananchi bali sala na dua zao pia.
Niwapeleke kando kidogo kabla ya kubainisha kwa nini nimeandika Rais amekuwa mtu wa kwanza kukiuka kali zake mwenyewe. Katika sosholojia, kuna kanuni moja inayofahamika kama ‘Social Exchange.’ Kwa kifupi, pamoja na mambo mengine, kanuni hii inaelezea kuhusu uhusiano (interactions) kati ya watu katika jamii.
Kanuni hiyo inatanabaisha kuwa uhusiano kati yetu katika jamii huongozwa na ‘zawadi’ (rewards) na ‘gharama’ (costs). Na watu wengi huongozwa na kanuni (formula) hii: thamani (ya mtu) = zawadi – gharama. ‘Zawadi’ ni vitu vizuri kama vile pongezi, shukrani, kuombewa dua, nk ilhali gharama ni hasara, mtendewa kutoonyesha shukrani, kupuuzwa, nk.
Mfano rahisi: ukipita mtaani, ukakutana na ombaomba, ukampatia hela kidogo, kisha akanyoosha mikono angani kukushukuru, basi kuna uwezekano mkubwa wa kumsaidia tena siku nyingine. Na si ombaomba tu, bali hata ndugu, jamaa au rafiki au ‘mtu baki’ ambaye anashukuru anaposaidiwa.
Lakini laiti ukimpatia msaada ombaomba, au mtu mwingine, kisha asionyeshe kujali msaada huo, basi uwezekano wa kumsaidia tena ni hafifu. Kwa mujibu wa kanuni yetu ya ‘thamani = zawadi – gharama,’ msaidiwa akionyesha shukrani inakuwa zawadi yenye thamani zaidi ya gharama, ilhali kwa asiyeonyesha shukrani gharama inakuwa kubwa kuliko zawadi. Natumaini hizi ‘hisabati’ hazijakuchanganya ndugu msomaji.
Kimsingi, kanuni hiyo inaambatana na matarajio ya ‘nipe nikupe’ (give and take). Kwamba katika kila tunalofanya, tunakuwa na matarajio fulani. Kwamba tunapokwenda kwenye nyumba za ibada, tuna matarajio ya kumridhisha Mola kwa vile tunafuata anachotarajia kwetu: sala/ibada kwake.
Tunapokuwa watu wa msaada, au wakarimu, au wema, nk tunatarajia wale tunaowafanyia hivyo wathamini tabia zetu hizo nzuri.
Turejee kwa Rais Magufuli. Hivi karibuni, akiwa ziarani mkoani Kagera, aliwaambia wananchi kuwa, ninamnukuu; “Serikali na wananchi kila mmoja abebe msalaba wake mwenyewe.’’ Alitoa kauli hiyo alipozungumzia misaada kwa waathirika wa tetemeko la ardhi lililoyakumba maeneo ya Ukanda wa Ziwa hususan Mkoa wa Kagera.
Mwaka jana nilipokuwa naomba kura kwenu, sikuomba tetemeko la ardhi litokee hapa, hili ni jambo ambalo liko nje ya uwezo wangu, tunaomba kila mmoja aweze kutumia msaada uliotolewa ili kurejesha miundombinu ya makazi yenu” alieleza Dk. Magufuli.
Bila kuingia kiundani kuchambua mantiki ya kauli hiyo ya Rais, yayumkinika kuhitimisha kuwa kama “kila mtu abebe mzigo wake mwenyewe” basi na ombi lake maarufu kwa wananchi la “mniombee” alibebe yeye mwenyewe. Ajiombee.
Naandika hivyo kwa sababu, kiustaarabu tu, kuna baadhi ya maneno hayastahili kusemwa katika mazingira ya maombolezo, misiba, nk. Rais ni kama mzazi. Na japo kila mzazi ana jukumu la kuwa mkweli, anapaswa pia kuwa na busara ya kuchagua maneno yanayoweza kuwasilisha ujumbe bila kuumiza mioyo ya watu.
Hivi Rais angeeleza kwa lugha ya upole kuwa uwezo wa serikali ni mdogo na haitomudu kumjengea nyumba kila mwananchi, lakini itashirikiana na wananchi kadri itakavyoweza, ikiwa ni pamoja na kuendelea kuhamasisha misaada kwa waathirika, asingeeleweka? Au angeonekana sio ‘Rais kamili’?
Kwa mujibu wa ‘social exchange theory,’ matarajio ya Watanzania wanaaombwa na Rais wao kuwa wamwombee si kumsikia akiwaambia “kila mtu abebe mzigo wake mwenyewe” hususan mbele ya watu wanaoendelea kukabiliana na athari za janga la tetemeko la ardhi.
Lakini kama hilo la “kila mtu atabeba msalaba wake mwenyewe” halitoshi, Rais Dk. Magufuli akakiuka kauli yake maarufu ya “msema kweli mpenzi wa Mungu” kwa kutoa maelezo yasiyo sahihi, kwamba (ninamnukuu) “Kuna nchi kama Japan na Italia, zimekuwa zikikumbwa na matetemeko mengi, haijawahi kutokea serikali yao ikawajengea nyumba upya isipokuwa inarejesha miundombinu ya taasisi za umma kama vituo vya afya, shule na barabara.”
Sio heshima wala nidhamu kusema “Rais amedanganya” lakini alichoongea kina kasoro. Kwa Italia, baada ya tetemeko lililotokea mwezi Agosti mwaka jana, Waziri Mkuu wa zamani Mateo Renzi alishughulikia upitishwaji wa sheria ya kuidhinisha Euro bilioni 4.5 kwa ajili ya waathirika na miundombinu. Euro bilioni 3.5 kwa ajili ya waathirika na euro bilioni kwa ajili ya majengo ya umma.
Kutegemea eneo, sheria iliidhinisha malipo kati ya asilimia 50 hadi 100 kwa wananchi ambao nyumba zao ziliharibiwa na tetemeko hilo.
Huko Japan nako, mara tu baada ya tetemeko kubwa la ardhi la mwaka 2011, serikali ilichukua hatua kadhaa kuwasaidia waathirika ikiwa ni pamoja na fedha za rambirambi kwa kila familia iliyopoteza ndugu katika janga hilo (Yen milioni 5), fedha kwa familia zenye majeruhi (Yen milioni 3), misaada ya fedha kwa kila familia na mikopo yenye masharti nafuu kwa kila familia (Yen milioni 3.5), mikopo maalumu kwa watu/biashara waliokuwa na madeni kabla ya tetemeko,  ahueni ya kodi mbalimbali kwa waathirika wote, malipo kwa waliopoteza ajira (unemployment benefits), mkakati maalumu wa utengenezaji ajira mpya, na hatua nyinginezo.
Kanuni za tawala zetu za kiafrika zipo wazi: “kiongozi huwa hakosei, na akikosea huwa amenukuliwa vibaya, na kama ikithibitika amekosea haina haja ya kumradhi.” Sitarajii kusikia tamko lolote kwamba “Kauli ya Rais kuwa ‘Kuna nchi kama Japan na Italia, zimekuwa zikikumbwa na matetemeko mengi, haijawahi kutokea serikali yao ikawajengea nyumba upya’ haikuwa sahihi. Anaomba radhi.”
Wakati wa kampeni zake za kuwania urais na hata baada ya kushinda urais, Dk. Magufuli amekuwa akituomba mara kwa mara kuwa tumsaidie. Makala hii ni mwitikio wa ombi hilo. Ni mchango wangu wa msaada kwake kumsihi ajaribu kuepuka lugha inayoweza kujenga tafsiri mbaya.
Kadhalika, suala la kusaidia wenzetu waliokumbwa na tatizo sio la kisheria, kisera au ki-kanuni, au kwa vile fulani hakufanya, bali ni suala la utu. Na utu ni kama pale Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba alipomtembelea mzazi wa msanii Chid Benz, kuangalia uwezekano wa kumsaidia msanii huyo aliyeathirika na matumizi ya dawa za kulevya. Ni utu kwa sababu, kisheria, anachofanya msanii huyo (kununua na kutumia mihadarati) ni kosa la jinai (Ibara ya 15 ya Sheria mpya ya Kupambana na Kudhibiti Dawa za Kulevya ya mwaka 2015).
Nihitimishe makala hii kwa kumshauri Rais Magufuli kwamba pamoja na dhamira yake nzuri kuitumikia nchi yetu kwa uwezo wake wote, na licha ya Watanzania kuwa na matumaini makubwa kwake, ni muhimu sana ajaribu ‘kupunguza makali’ kwenye lugha yake. Kama nilivyoeleza katika makala yangu iliyopita, ‘lugha ya ukali’ inaweza kujenga nidhamu ya uoga, kitu ambacho kitakwaza jitihada za Rais wetu kuijenga Tanzania tunayostahili. Ninatumaini Rais ataupokea ushauri huu na kutoona kuwa anakosewa heshima kwa kusahihishwa pale alipokosea.
Mungu ibariki Tanzania

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

11 Jan 2017

Kwamba Rais wa Russia, Vladimir Putin na watu wake wa karibu, walitaka mgombea urais wa chama cha Republican cha Marekani, Donald Trump, ashinde uchaguzi wa Urais uliofanyika Novemba mwaka jana, wala sio siri. 

Ilishafahamika kabla ya uchaguzi huo kuwa Putin na "watu wake" hawakutaka Trump awe rais kwa vile wanampenda bali walikuwa na ajenda na maslahi binafsi. Hata hivyo, hadi muda huu ilikuwa haifahamiki ni kitu gani hasa kilichokuwa kikimfanya Rais huyo wa Russia na mashushushu wake kupigana kufa na kupona kuhakikisha Trump anashinda katika uchaguzi huo, kitu ambacho kwa hakika kilitokea.

Kadhalika, Putin na Russia walishapata ushindi hata kabla ya uchaguzi baada ya duru za kiintelijensia, ndani na nje ya Marekani, kuthibitisha kuwa kiongozi huyo wa Russia na mashushushu wake walikuwa wakihujumu uchaguzi huo. Kiintelijensia, huo ni ushindi hata kama matokeo yake hayakujulikana muda huo.

Kwa 'kumwezesha Trump kushinda,' Putin na mashushushu wake waliibuka na ushindi mkubwa zaidi, pengine wa kihistoria katika 'vita ya muda mrefu ya kijasusi kati ya Russia na Marekani.' Kwa 'macho ya kawaida,' nchi hizo mbili zilionekana kama zina maelewano bora kuliko ilivyokuwa katika zama za Vita Baridi. Lakini 'kizani,' nchi hizo zimekuwa kwenye vita kali ya kijasusi, na ambayo inaelezwa kuwa pengine ni kubwa kuliko ilivyokuwa katika zama za Vita Baridi. Hiyo ni mada ya siku nyingine.

Ijumaa iliyopita, wakuu wa taasisi za ushushushu za Marekani walikutana na Rais Mteule Trump kumfahamisha kuhusu uchunguzi wao uliohitimisha kwamba Russia ilihujumu uchaguzi wa Rais wa Marekani, ambao Trump aliibuka kidedea.


Awali kabla ya mkutano huo nyeti, bosi mkuu wa taasisi za ushushushu za Marekani, Mkurugenzi wa Idara ya Usalama wa Taifa (DNI), James Clapper (pichani chini), aliieleza kamati ya bunge la seneti kuwa hujuma zilizofanywa na Russia zipo katika sura nyingi zaidi ya kudukua taarifa za chama cha Democrats, na kumhujumu mpinzani wa Trump, mwanamama Hillary Clinton.

2017-01-05t153806z-1958236086-rc17375221c0-rtrmadp-3-usa-russia-cyber-clapper.jpg

Lakini sasa taarifa zilizopatikana baada ya mkutano wa wakuu hao wa taasisi za ushushushu na Trump zinaeleza kuwa Russia ina kitu kinachofahamika kishushushu kama 'compromising information' kumhusu Trump. Maelezo ya kina kuhusu 'compromising information' yapo katika kitabu changu cha SHUSHUSHU (kinunue hapa), lakini kwa kifupi, ni taarifa ambazo mashushushu wanazo dhidi ya mtu na wanaweza kuzitumia kumshurutisha afanye wanachohitaji wao. Mfano hai, mwanasiasa mmoja huko nyumbani aliwahi kunaswa akifanya 'kitu flani,' kikanukuliwa na 'wahusika,' na amebaki kuwa 'compromised' pengine milele.


Muhtasari wenye kurasa mbili ulioambatana na taarifa ya taasisi hizo za kishushushu za Marekani kuhusu hujuma za Russia ulijumuisha madai kwamba mashushushu wa Rusia wana 'compromosing information' kuhusu Trump. 

Taarifa hiyo imechangiwa na kazi iliyofanywa na jasusi mmoja mstaafu wa Uingereza ambaye kazi zake huko nyuma zinachukuliwa na taasisi za kishushushu za Marekani kuwa ni za kuaminika.

Imefahamika kuwa shirika la ushushushu wa ndani la Marekani, FBI, hivi sasa lipo katika uchunguzi kubaini ukweli kuhusu hizo 'compromising information' kuhusu Trump.

Hata hivyo, inaelezwa kwamba tetesi kwamba Russia 'ina nyeti kuhusu Trump' zimekuwa zikizagaa kitambo japo hazikuwahi kuzungumzwa na taasisi za kishushushu.

Taarifa moja ya kishushushu 'iliyotolewa usiri' (unclassified) iliyowekwa hadharani Ijumaa iliyopita ilitanabaisha kuwa Putin binafsi alitoa amri ya Russia kumsaidia Trump  kwa kumuumbua mpinzani wake, Hillary. 

Taarifa hiyo ilibainisha kuwa Idara ya ushushushu wa kijeshi ya Russia, GRU, ilikitumia kikundi cha wadukuzi cha WikiLeaks kuvujisha baruapepe mbalimbali kumhusu Hillary na wasaidizi wake wakati wa kampeni za urais zilizomalizika Novemba mwaka jana na Trump kuibuka mshindi.

Endelea kutembelea tovuti hii kwa habari kama hizi kuhusu USHUSHUSHU (bonyeza hapo juu kabisa mwa ukurasa huu palipoandikwa 'intelijensia') na habari nyinginezo.

CHANZO: Habari hii imetokana na vyanzo mbalimbali ikiwa ni pamoja na HIKI.

9 Jan 2017


Moja ya vipimo kuwa unaitumia vema mitandao ya kijamii ni idadi na aina ya marafiki unaotengeza kupitia mitandao hiyo. Binafsi, nimetengeneza marafiki wengi mno, wanaotoka kada mbalimbali za maisha: wanasiasa, wanataaluma, wasanii, wajasiamali, wakulima, wanafunzi/wanavyuo, na takriban kila kada ya watu.

Ni kwa sababu hiyo ndio maana sio tu ninaiheshimu sana mitandao ya kijamii lakini pia huwa makini kulinda 'hadhi' yangu mtandaoni. Kadri unavyotengeneza marafiki wengi ndivyo unavyokuwa katika nafasi kupata madhara makubwa zaidi iwapo mtu atakuchafua. 

Mmmoja ya watu nilofahamiana kupitia mitandao ya jamii ni Mhadhiri wa chuo kikuu cha London (University of London), katika Shule ya Stadi za Asia na Afrika (School or Oriental and African Studies - SOAS).

Nilifahamiana na Dkt Hannah mwishoni mwa mwaka jana huko kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter. Na kilichotufanya tufahamiane ni kuvutiwa na mapenzi yake kwa Kiswahili. Kila siku, Dokta Hannah hutwiti 'neno la siku' (word of the day) la Kiswahili, kisha kulielezea kwa Kiingereza.

Awali nilidhani ana asili ya Tanzania au nchi inayoongea Kiswahili, kwa sababu Kiswahili chake ni fasaha kabisa. Ikabidi nimdadisi. Kwa mshangao mkubwa, kumbe mhadhiri huyu ni Mwingereza wa asili, na wala Kiswahili sio lugha yake ya asili. Alijifunza tu wakati anafanya tafiti zake huko Tanzania na katika nchi nyingine za Afrika Mashariki. 

Licha ya kuwa mhadhiri, Dkt Hannah ni 'postdoctoral research fellow' (huu utakuwa mtihani wangu na wake kutafuta neno stahili la Kiswahili). Kwa kifupi, mtu anayefanya 'postdoctoral fellowship' ni mhitimu wa shahada ya uzamifu anayeendelea na tafiti za kitaaluma. 

Eneo lake kuu la utafiti ni jinsi lugha zinavyokutana na zinavyobadilika, mkazo wake ukiwa kwenye lugha za Kibantu katika eneo la Afrika Mashariki.

Kwa sasa anafanya utafiti kuhusu mabadiliko ya kisarufi katika lugha za makabila ya Tanzania na Kenya, yaani Kirangi, ki-Mbugwe, ki-Gusii, Kikurya, ki-Ngoreme, ki-Suba Simbiti.

Habari njema zaidi ni kwamba Dkt Hannah amekubali kushiriki jitihada za kuenzi, kudumisha, kuboresha na kukitangaza Kiswahili kupitia kampeni maarufu ya #ElimikaWikiendi. Taarifa zaidi kuhusu ushiriki wake zitatolewa wakati mwafaka. 

Tovuti binafsi ya Dkt Hannah ipo HAPA na unaweza kum-follow Twitter anatumia @itsthegibson

Orodha ya machapisho yake ya kitaaluma:
 

Book Chapters

Gibson, Hannah and Koumbarou, Andriana and Marten, Lutz and van der Wal, Jenneke (2017) 'Locating the Bantu conjoint/disjoint alternation in a typology of focus marking.' In: van der Wal, Jenneke and Hyman, Larry M., (eds.), The conjoint/disjoint alternation in Bantu. Mouton de Gruyter . (Trends in Linguistics. Studies and Monographs) (Forthcoming)
Gibson, Hannah and Marten, Lutz (2016) 'Variation and grammaticalisation in Bantu complex verbal constructions: The dynamics of information growth in Swahili, Rangi and siSwati.' In: Nash, Léa and Samvelian, Pollet, (eds.), Approaches to Complex Predicates.Leiden: Brill, pp. 70-109. (Syntax and Semantics)

Journal Articles

Gibson, Hannah (2016) 'A unified dynamic account of auxiliary placement in Rangi.' Lingua, 184. pp. 79-103.
Seraku, Tohru and Gibson, Hannah (2016) 'A Dynamic Syntax modelling of Japanese and Rangi clefts: Parsing incrementality and the growth of interpretation.' Language Sciences , 56 (2016). pp. 45-67.
Gibson, Hannah and Wilhelmsen, Vera (2015) 'Cycles of negation in Rangi and Mbugwe.' Africana Linguistica, 21. pp. 233-257.
Marten, Lutz and Gibson, Hannah (2015) 'Structure building and thematic constraints in Bantu inversion constructions.' Journal of Linguistics, 52 (3). pp. 565-607.
Gibson, Hannah (2015) 'The dynamics of structure building in Rangi: At the Syntax-Semantics interface.' Cambridge Occasional Papers in Linguistics, 8. pp. 41-55.
Gibson, Hannah (2013) 'Auxiliary placement in Rangi: A case of contact-induced change?' SOAS Working Papers in Linguistics, 16. pp. 153-166.

Book Reviews



5 Jan 2017

KHERI ya mwaka mpya 2017. Kama ilivyo kawaida ya safu hii, kila makala ya mwanzo wa mwaka hujikita kwenye ubashiri wa masuala mbalimbali yanayotarajiwa katika mwaka mpya husika.
Kutokana na ufinyu wa nafasi, ubashiri kuhusu mwaka huu mpya utaelemea zaidi katika mwenendo wa siasa kitaifa na kimataifa.
Kimataifa, mtihani wa kwanza kabisa wa siasa za kimataifa utaanza Januari 20, 2017 siku ambayo Rais mteule wa Marekani, Donald Trump ataapishwa rasmi.
Ni vigumu kubashiri nini kinaweza kutokea siku ya kwanza tu tangu Trump aapishwe, lakini kilicho bayana ni uwezekano mkubwa kwa tajiri huyo, aliyeshinda urais katika mazingira ya kushangaza yaliyoambatana na kila aina ya hadaa, si tu kuendelea kuwa ‘kituko’ bali pia hata kuhatarisha usalama wa kimataifa.
Wakati wa kampeni za urais, profesa mmoja wa historia ya siasa, Allan Lichtman, alibashiri kuwa Trump angeshinda licha ya kura za maoni kuonyesha mgombea kwa tiketi ya Democrats, Hillary Clinton akiongoza. Nilikerwa sana na ubashiri wa profesa huyo.
Baada ya Trump kumbwaga Hillary, Profesa Lichtman aliibuka na ubashiri mwingine, akidai kuwa urais wa tajiri huyo utakuwa wa muda mfupi tu kwani atang’olewa madarakani pengine kabla ya kutimiza mwaka madarakani. Nami ambaye awali nilikerwa na profesa huyo sasa natamani ubashiri wake utimie.
Na kwa hakika kati ya mambo yanayoweza kutokea mwaka huu ni Trump kuondolewa madarakani. Lakini hilo si kubwa kulinganisha na uwezekano wa machafuko nchini humo hususan, baada ya wapigakura kubaini kuwa ‘waliingizwa mkenge’ na tajiri huyo.
Ikumbukwe huyu atakuwa ndiye rais wa kwanza aliyeingia rasmi madarakani kwa udanganyifu na hadaa.
Jingine kuhusu Trump ni uwezekano wa kuwatibua washirika wa Marekani miongoni mwa mataifa ya Kiislamu, kama vile Saudi Arabia, Jordan na Pakistan. Uwezekano huo unatokana zaidi na msimamo wa kibaguzi wa Trump na wengi wa wasaidizi wake.
Kadhalika, kuna uwezekano uswahiba kati ya Trump na Rais wa Urusi, Vladimir Putin, ‘ukatumbukia nyongo,’ kwa sababu mataifa hayo yana mgongano wa kimaslahi. Vilevile, kuna uwezekano wa dalili za mgogoro kati ya Marekani na China kupanuka zaidi, chanzo kikiwa Trump huyohuyo.
Kwingineko kimataifa, Uholanzi itafanya uchaguzi wake mkuu Machi, Ufaransa Aprili hadi Juni, na Ujerumani Oktoba.
Chaguzi hizo ni mtihani mgumu kwa nchi hizo kutokana na tishio kubwa kutoka kwa vyama vyenye mrengo mkali wa kulia ambavyo vinazidi kupata umaarufu barani Ulaya kutokana na matishio ya ugaidi, ambayo pia yanahusishwa na sera za kukaribisha wahamiaji.
Chaguzi nyingine zinazotarajiwa kugusa hisia ni nchini Hong Kong (Machi), Iran (Mei) na Korea ya Kusini (Desemba).
Japo kuna dalili za amani huko Syria kufuatia jitihada zinazofanywa na Russia, kuna uwezekano kwa nchi hiyo kujikuta kwenye machafuko zaidi hasa ikizingatiwa kuwa serikali ya Rais Bashir Assad inamiliki sehemu tu ya nchi hiyo, huku sehemu nyingine zikiwa chini ya makundi mbalimbali.
Hali ya usalama nchi Uturuki inatarajiwa kuendelea kuwa tete, kutokana na matishio makuu mawili, ya vikundi vya Kikurdi vinavyopigania uhuru na kikundi cha kigaidi cha ISIS, ambacho pia kinatarajiwa kuendelea kuwa tishio katika eneo la Ghuba, nchi za Ulaya Magharibi na Marekani.
Barani Afrika, mwaka huu kuna chaguzi kadhaa, lakini ambazo zinavuta hisia zaidi ni nchini Kenya mwezi Agosti na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ambako hali bado ni ya wasiwasi kutokana na jitihada za Rais Joseph Kabila kutaka kung’ang’ania kuwa madarakani ingawa tayari kuna maneno kwamba amekubali kuachia ngazi.
Kuhusu majirani zetu wa Kenya, tatizo mara zote limekuwa kwenye siasa za ukabila. Kwa bahati mbaya, nchi hiyo itaingia kwenye uchaguzi wake mkuu wakati ‘kirusi cha ukabila kikiwa hai na chenye nguvu.’
Tukigeukia huko nyumbani, mwaka huu utashuhudia CCM ikifanya uchaguzi wake ndani. Tunasubiri kuona jinsi ambavyo Mwenyekiti wa Taifa, Rais Magufuli, atachezesha kete zake.
Ifahamike kuwa licha ya mwonekano kuwa ‘CCM ni wamoja,’ ukweli ni kwamba ndani ya chama hicho kuna ‘mambo yanayoendelea chinichini.’
Kwa upande mmoja, kwa muda mrefu CCM imekuwa hifadhi ya ‘watu mbalimbali wenye wasifu usiopendeza,’ ikiwa ni pamoja na mafisadi. Hawa ni wahanga wa wazi wa jitihada za Rais Magufuli kupambana na ufisadi. Yayumkinika kuhisi kuwa wanaweza kutumia uchaguzi huo kama fursa ya kujipangia vema kumdhibiti Dk. Magufuli katika uchaguzi wa mgombea urais mwaka 2020.
‘Wapinzani wa Magufuli’ ndani ya CCM wanapewa nguvu na mtazamo wa baadhi ya wananchi mitaani kwamba hali ya maisha inazidi kuwa ngumu pasipo dalili za kupatikana nafuu hivi karibuni.
Wakati wengine twaelewa kuwa ‘inabidi tupitie maumivu kabla ya kupata nafuu,’ kwa baadhi ya wananchi ‘mtaani’ wanaona kama utawala wa Magufuli ni wa ‘kuwapa maumivu mfululizo pasi dalili ya ahueni.’
Nje ya CCM, changamoto kubwa kwa utawala wa Rais Magufuli ni kuibuka kwa nidhamu ya uoga, ambapo taratibu kunaanza kujengeka hisia kuwa ‘kiongozi atayediriki kupishana kimtazamo na Rais, atatumbuliwa.’
Nidhamu ya uoga haiwezi kuleta tija wala ufanisi. Wakati ninaandaa makala hii nilipewa taarifa kuhusu tishio la janga la njaa kwenye wilaya kadhaa lakini inadaiwa kuwa watendaji katika maeneo hayo wanahofia kutoa taarifa kwa wakichelea kutumbuliwa.
Ili dhamira ya Dk. Magufuli kuiletea neema Tanzania itimie kwa kuongeza kasi ya uzalishaji mali na mchango wa sekta mbalimbali kwenye uchumi, sambamba na kukabiliana na rushwa na ufisadi, ni lazima Watanzania wawe ‘kitu kimoja.’
Serikali ya Dk. Magufuli inapaswa kuepuka ‘ugomvi usio wa lazima’ hasa matamshi ya kuwafanya watu wazima wajione kama watoto, ‘maguvu’ badala ya busara, na kutofanya haki za Watanzania kuwa zawadi kutoka kwa watawala.
Uamuzi wa kufuta matangazo ya moja kwa moja ya Bunge, kuzuwia mikutano na maandamano ya vyama vya siasa, viongozi wa Upinzani kubughudhiwa mara kwa mara, kubinya uhuru wa habari  ambao japo waweza kutumika vibaya, ni muhimu katika ujenzi wa utawala bora. Na bila kuuma maneno, Rais Magufuli asizuwie kukosolewa.
Kwa upande wa vyama vya Upinzani, dalili za suluhu katika mgogoro wa CUF ni ndogo. Kadhalika, ‘afya’ ya ACT Wazalendo inaweza kuendelea kudhoofika, tatizo likiwa ugumu wa ‘siasa za chama cha mtu mmoja.’
Kwa Chadema, kunaweza kuibuka harakati za kudai mabadiliko ndani ya chama hicho hasa kutokana ukweli kuwa chama hicho kwa sasa hakina ajenda ya kitaifa zaidi ya ‘kudandia hoja.’
Nihitimishe makala hii kwa kukumbushia kuwa ubashiri si ‘sayansi yenye uhakika wa asilimia 100 (exact science). Ubashiri huu umetokana na uchambuzi mienendo (trends) mbalimbali na si uhakika kuwa ‘lazima itakuwa hivi au vile.’
Niwatakie tena heri ya mwaka mpya 2017.


3 Jan 2017



Kuna msemo wa kisiasa unaosema "in politics, perception is reality." Maana yake katika tafsiri isiyo rasmi ya Kiswahili ni kwamba 'katika siasa, kitu kinavyoonekana ni sawa na uhalisi wake. 

Kwa mantiki hiyo, kura ya maoni iliyobandikwa na gazeti la Raia Mwema katika akaunti yake kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter ikiwa na swali kama linavyoonekana katika 'tweet' husika hapa chini, inaweza kuwa na uzito.

Ndio, siyo kura ya kisayansi lakini idadi ya watu 448 'waliopiga kura' (hadi wakati ninaandaa makala hii) ni sampuli ya kutosha kwa kura ya maoni. 
Natambua makada wa CCM hawatopendezwa na makala hii, na huenda kuna watakaohoji kwanini niipe uzito kura ya maoni ya Twitter. Jibu langu ni hilo kwenye sentensi ya kwanza, "in politics, perception is reality." Lowassa kuongoza katika kura hiyo ya maoni kunajenga perception flani ambayo kwenye siasa ni reality. 

Neno la tahadhari kuhusu kura hiyo ya maoni ni kwamba bado inaendelea na haijafikia tamati. Kwahiyo, matokeo ya mwisho yanaweza kuwa tofauti, hasa ikzingatiwa kuwa tofauti ya asilimia ni kiduchu.

Pengine moja ya vitu vinavyompunguzia umaarufu Rais Magufuli ni baadhi ya kauli zake...kama hii hapa pichani chini. Ikumbukwe kuwa moja ya sifa ya uongozi bora ni pamoja na kutumia lugha isiyojenga picha ya dharau au kukosa huruma kwa wananchi. Na tukiamini kuwa 'in politics, perception is reality,' basi picha hasi inayoweza kutokana na baadhi ya kauli za Rais Magufuli zaweza kujenga taswira hasi kumhusu yeye na uongozi wake, hata kama hatamki kwa nia mbaya.




29 Dec 2016


ATIMAYE mwaka 2016 unafikia ukingoni ambapo siku nne zijazo tutaingia mwaka mpya 2017. Makala hii inafanya tathmini ya jumla ya matukio makubwa zaidi, hususan ya kisiasa, kitaifa na kimataifa.
Tukio kubwa zaidi kimataifa ni kuyumba kwa itikadi ya siasa za kiliberali katika nchi za Magharibi, suala lililokwenda sambamba na kukua kwa siasa za mrengo mkali wa kulia. Kadhalika, nchi kadhaa za Magharibi zinaendelea kushuhudia ujio wa zama mpya za siasa, zinazojulikana kama ‘post-truth,’ ambazo kwa tafsiri fupi ni ‘kupigia chapuo uongo, na upinzani dhidi ya ukweli.’
Ni katika mazingira hayo, kulijitokeza mshtuko mkubwa katika nchi hizi za Magharibi, na pengine duniani kwa ujumla, pale Uingereza ilipoamua kujitoa kwenye Umoja wa Ulaya (EU) katika kura ya maoni iliyofanyika mwezi Juni. Kampeni za kura hiyo zilijenga msingi imara wa siasa za ‘post-truth.’
Miezi mitano baadaye, Marekani nayo ilikumbwa na wimbi hilo la siasa za ‘post-truth,’ pale mfanyabiashara bilionea, Donald Trump, aliyekuwa na kila sifa mbaya ya kumnyima japo ‘ujumbe wa nyumba kumi,’ alifanikiwa kumbwaga mwanasiasa mkongwe, Hillary Clinton. Trump na wafuasi wake walitumia kila aina ya hadaa huku wakisaidiwa na mlipuko wa habari zisizo za kweli hususan katika mitandao ya kijamii.
Kinachotisha kuhusu zama hizi za siasa za ‘post-truth’ ni ukweli kwamba zimekumbatiwa na vyama vya siasa na vikundi vyenye mrengo mkali kabisa wa kulia, pamoja na vyama/vikundi vya kibaguzi.
Kinachoendelea kusaidia ‘uongo kuwa muhimu kuliko ukweli’ ni ukweli kwamba tabaka la siasa, tabaka la uongozi, tabaka la wanataaluma na wataalamu, tabaka la wafanyabiashara, na makundi kama hayo, yanaangaliwa kama yaliyoweka pamba masikioni. Hayasikii vilio vya tabaka la watu wa chini, na hata wakisikia hawafanyii kazi vilio hivyo.
Ndio maana, watu ‘hatari’ kama vile Nigel Farage wa hapa Uingereza, Donald Trump huko Marekani, Marine Le Pen wa Ufaransa, Norbert Hofer wa Austria (ambaye almanusura ashinde urais wa nchi hiyo), Geert Wilders wa Uholanzi, Frauke Petry wa Ujerumani na kadhalika, wamemudu kutumia uongo na hadaa kwa ufanisi kutokana na ‘ukweli’ kupoteza maana yake.
Mashambulizi ya kigaidi huko Ufaransa, Ubelgiji na Ujerumani na kuendelea kuwepo kwa tishio la vitendo hivyo kumeongeza umaarufu wa siasa za mrengo mkali wa kulia ambazo zinahusisha ugaidi na sera za ukarimu kwa wahamiaji.
Mwaka 2017 unatarajiwa kushuhudia michuano mikali ya kisiasa barani Ulaya ambapo nchi zinazotupiwa jicho zaidi ni Ufaransa na Ujerumani zinazokabiliwa na hatari ya kuwa chini ya utawala wa wanasiasa wenye mrengo mkali kabisa wa kulia.
Kwa huko nyumbani, tishio kubwa halikuwa kwenye siasa bali ajali zinazoendelea kugharimu maisha ya Watanzania kwa idadi kubwa, japo janga hilo halionekani kuwasumbua wananchi na viongozi.
Kwenye ulingo wa siasa, Rais ‘mpya’ Dk. John Magufuli ndiye aliyetawala zaidi katika anga za siasa. Kwa upande mmoja, hali hiyo ilitokana na matumaini makubwa waliyonayo wananchi kwake, na kwa upande mwingine, udhaifu unaozidi kukua miongoni mwa vyama vya upinzani.
Hata hivyo, kwa kulinganisha kasi aliyoanza nayo na hali ilivyo sasa, yayumkinika kusema kuwa ‘kasi ya Magufuli imepungua.’ Huku ‘tumbua majipu’ ikizidi kuwa ya msimu (na baadhi ya utumbuaji ukituhumiwa kufanywa kutokana na majungu), sera iliyowapa matumaini makubwa, ya kuanzishwa kwa mahakama maalumu ya ufisadi iliyogeuka kuwa kichekesho ambapo tangu mahakama hiyo ianzishwe imeendesha kesi moja tu.
Na kituko kikubwa zaidi ni pale waziri mwenye dhamana ya mahakama hiyo, Dk. Harrison Mwakyembe, alipotuhadaa kuwa uchache wa kesi katika mahakama hiyo ni dalili ya mafanikio, yaani ufisadi umepungua.
Lakini kama kuna suala ambalo baadhi yetu tunapata shida mno kumwelewa Rais Magufuli ni ‘kutengeneza maadui wasio wa lazima.’ Hatua za kuzuia mikutano na maandamano ya vyama vya upinzani na kukatisha matangazo mubashara ya vikao vya Bunge ni hatua ambazo sio tu hazikuwa na tija bali hazikuwa na umuhimu wowote.
Matumizi ya sheria ya makosa ya mtandao pale tu rais anapotukanwa, huku maelfu kwa maelfu ya Watanzania wakiendelea kuwa waathirika wa matusi imetufanya baadhi ya ‘tulioupigia debe’ muswada wa kuanzisha sheria hiyo tujilaumu.
Jinsi serikali ilivyowatimua wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kana kwamba walijichagua wenyewe kujiunga na masomo, na kuwakashifu kuwa ni ‘vilaza,’ uamuzi wa kutishia ajira za mahakimu wasio na shahada za chuo kikuu, kupuuza jitihada za Rais (mstaafu) Jakaya Kikwete za kuwashawishi Watanzania wa Diaspora kushiriki katika harakati za maendeleo huko nyumbani na badala yake ‘kuwaharamisha’ kwa kuwazuia kumiliki ardhi, na hatua kama hizo, ni baadhi ya mambo yaliyotawala zaidi mwaka huu katika siasa za Tanzania.
Hata hivyo, Serikali ya Awamu ya Tano imefanikiwa kurejesha nidhamu ya kazi, angalau kwa kujenga mwamko wa wananchi kutegemea kipato halali badala ya shughuli zilizo kinyume cha sheria. Na japo matukio ya ujambazi yameendelea kutawala, kumekuwa na dalili nzuri ya kupungua biashara ya dawa za kulevya na ujangili. Na kama tetesi kuhusu uwezekano wa mabadiliko ya baraza la mawaziri hivi karibuni ni za kweli, basi huenda ‘timu mpya’ ikaufanya mwaka ujao kuwa ‘mwema’ zaidi kwa Watanzania.
Nimalizie makala hii kwa kuahidi kuwaletea ubashiri wa mwenendo wa mambo mbalimbali kwa mwaka kesho katika makala ijayo.
Nawatakia heri ya mwaka mpya 2017

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali 

23 Dec 2016

Aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Maradhi ya Binadamu (NIMR), Dk. Mwele Malecela.


  • Virusi vya Zika viligundulika kuwepo Tanzania mwaka 1952
  • Dkt Mwele na wanasayansi wenzie 'wanakuna vichwa' wakisumbuliwa na swali la kitafiti je, virusi vya Zika vilivyoko kwenye nchi za Afrika mashariki vina madhara sawa na vile vya Brazil?
  • Alichowasilisha ni ripoti ya utafiti kuhusu virusi vya Zika, na sio kutangaza mlipuko wa ugonjwa huo.
  • Sheria iliyoanzisha NIMR ilimpa ruhusa/ mdaraka ya kutoa taarifa husika.
  • Waziri husika alikabidhiwa ripoti  (kumbukumbu namba NIMR/HQ/D13) MIEZI MINNE kabla Dokta Mwele hajatoa ripoti hiyo hadharani.


ANGALIZO: Japo ninafahamiana na Dokta Mwele Malecela (kama dada-rafiki), makala hii ya kiuchunguzi ni jitihada zangu binafsi kupata undani na usahihi kuhusu hatua iliyochukuliwa na Rais Magufuli wiki iliyopita kutengua wadhifa wa Dkt Mwele wa Ukurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR). Ikumbukwe sasa tunaishi katika zama za 'post truth politics' (siasa za hadaa/uongo) ambapo moja ya tabia muhimu ni kupingana na ukweli na kuugeuza uwe uongo, na uongo uwe ukweli. Ni jukumu la kila mmoja wetu kupambana na janga hili ambalo limetawala mno mwaka huu 2016 na kupelekea 'balaa' la Brexit (Uingereza kujitoa katika Umoja wa Ulaya) na Donald Trump kushinda Urais huko Marekani. 

Dokta Mwele Malecela ni nani?

Kwa faida ya wasiomjua vizuri Dkt Mwele, historia yake kwa kifupi ni kama ifuatavyo: Amekuwa mtumishi wa NIMR kwa miaka 30 mfululizo, ambapo alianza ngazi ya awali kabisa kama mwanasayansi 'wa ngazi ya mwanzo' (junior scientist). Yaani kama jeshini basi tungesema alianza kama 'private' na kupanda ngazi hadi kuwa Jenerali. Hili linaweza kuonekana ni jambo dogo lakini ukweli ni kwamba dunia ina mahitaji makubwa ya wansayansi, hususan katika nchi zilizoendelea. Mahitaji hayo ni makubwa zaidi kwa wanasayansi wa kike ambao kwa hakika ni wachache mno. Kuitumikia NIMR kwa miaka 30 mfululizo licha ya vishawishi mbalimbali vya ajira bora zaidi kama mwanasayansi wa kimataifa, Dokta Mwele aliweka mbele maslahi ya nchi yake Tanzania.

Lakini pengine kubwa zaidi kuhusu mwanasayansi huyo ni ndoto yake ya tangu utotoni ya kuwa mwanasayansi mtafiti. Kwa kuzingatia kwamba wakati anakua, baba yake, Mzee John Malecela alikuwa katika nyadhifa mbalimbali kitaifa na kimataifa, kubwa zaidi ikiwa Uwaziri Mkuu. Kwa wadhifa huo wa baba yake, Dkt Mwele angeweza 'kupata chochote,' pengine hata kujikalia tu nyumbani na 'kula maisha.' Hata hivyo, aliwekeza nguvu zake katika kufikia malengo yake ya kuwa mtafiti. 

Kielimu, alifanikiwa kuhitimu shahada ya kwanza chuo kikuu cha Dar es Salaam (BSc in Zoology) na baadaye kupata shahada ya uzamili (MSc) na ya Uzamifu (PhD) katika stadi kuhusu parasitolojia (Medical parasitology) katika taasisi maarufu ya London School of Hygiene and Tropical Medicine ya chuo kikuu cha London, hapa Uingereza.



Watanzania wengi wamemfahamu Dokta Mwele katitka kazi yake kubwa ya kutokomeza magonjwa yasiopewa kipuambele hususan matende na mabusha. Katika sehemu nyingi za Tanzania kama Pangani na Mtwara alijulikana kama mama matende. Kazi hii ilimpatia nishani ya kutambulika kwa kazi hii muhimu kutoka seriakli ya marekani (Neglected Tropical Disease Champion Award). Hivi sasa takwimu za Mtwara zinaonyesha kushuka kwa ugonjwa wa matende na mabusha kutoka asilimia 60-80 mwaka 2002 hadi asilimia 0 mwaka 2014. Juhudi hizi zimeendeshwa na Watanzania wakiongozwa na Mtanzania.

Wasifu mfupi wa Dokta Mwele upo HAPA na maelezo yake mwenyewe kuhusu safari yake hadi kuwa mwanasayansi wa kimataifa yapo HAPA 

Ni kutokana na ueledi wake mkubwa kitaaluma na kitaalamu, kitaifa na kimataifa, watu wengi wamepatwa na mshtuko mkubwa kufuatia uamuzi wa Rais Magufuli kumwondoa Dokta Mwele madarakani.



Japo taarifa ya Ikulu kuhusu uamuzi huo wa Rais haikutoa sababu yoyote, ni siri ya wazi kuwa ulitokana na taarifa aliyoitoa Dkt Mwele kwa waandishi wa habari kuhusu utafiti wa virusi vya ugonjwa wa Zika. Kwamba taarifa yake ilitafsiriwa vibaya au kulikuwa na mpango wa makusudi kumwondoa katika nafasi hiyo, ni jambo ambalo kwa sasa tunaishia kuhisi tu. Kilicho bayana ni kwamba hakutangaza MLIPUKO wa ugonjwa wa Zika bali aliripoti tu kuhusu MATOKEO ya utafiti uliofanywa na taasisi ambao ulibani kuwa sampuli 88 za damu kati ya 533 zilikuwa na virusi vya ungonjwa huo.

Historia ya Zika na uwepo wake Tanzania


Kabla ya kuingia kwa undani zaidi, ni muhimu kujielimisha vya kutosha kuhusu ugonjwa wa Zika na 'mahusiano yake na Tanzania yetu.' Kwa kifupi ugonjwa huu sio mgeni na uko katika kanda za tropiki zenye mbu na uligunduliwa kwa mara ya kwanza katika msitu zika (zika forest) Uganda mwaka 1947. Swali ambalo liko kwenye vichwa vya watafiti wa virolojia wa Afrika mashariki ni kuwa je, virusi vya zika vilivyoko kwenye nchi za Afrika mashariki vina madhara sawa na vile vya Brazil? 

Ifuatayo ni historia fupi ya Zika na uwepo wake Tanzania [Tafsiri ya Kiswahili katika maandishi mekundu]

Historia ya ZIKA

Kuanza kusambaa kwa virusi vya Zika kuliambatana na hali ya watoto kuzaliwa wakiwa na vichwa vidogo isivyo kawaida kunakohusiana na kutokamilika maendeleo ya ubongo (kwa kitabibu, 'microcephaly') na ugonjwa unaofahamika kama 'Guillain-Barre syndrome.' Baada ya kugundulika katika nyani nchini Uganda mwaka 1947, virusi hivyo viligundulika katika binadamu mwaka 1952. Mlipuko wa kwanza wa maradhi yanayotokana na maambukizo ya Zika uliripotiwa katika kisiwa cha Yap mwaka 2007. Hivi sasa kuna nchi kadhaa ambazo zimekumbwa na mlipuko wa  virusi vya Zika.

Zika: Asili na kusambaa kwa virusi hivyo vinavyosambazwa na mbu

Maelezo yafuatayo yanatoa muhtasari wa kusambaa kwa maambukizi ya Zika tangu yalipogunduliwa mwaka 1947 hadi mwezi Februari mwaka huu 2016 



1947: Wanasayansi waliokuwa katika uchungui wa kawaida wa homa ya manjano katika msitu wa Zika nchini Uganda wanabaini virusi vya Zika katika nyani.

1948: Virusi (vya Zika) vyatambuika katika mbu aina ya Aedes Africanus, kwenye msitu wa Zika


1969 - 1983 Uwepo wa Zika unasambaa hadi Asia ya Ikweta, ikiwa ni pamoja na India, Indonesia, Malaysia na Pakistani, ambapo virusi vya Zika vyagundulika katika mbu. Kama ilivyokuwa Afrika, maambukizi ya virusi hivyo yabainika lakini pasipo milipuko, na maradhi kwa binadamu yaendelea kuonekana adimu na ya wastani.

2007: Zika yasambaa kutoka Afrika na Asia na kusababisha mlipuko mkubwa wa kwanza katika binadamu katika kisiwa cha Yap kilichopo kwenye Bahari ya Pasifiki, Shirikisho la Mikronesia. Kabla ya tukio hili, hakukuwahi kuwepo mlipuko wa Zika na kesi 14 tu za uwepo wa Zika zilikuwa zimeripotiwa dunia nzima.

2013 - 2014: Milipuko ya Zika katika visiwa vingine vinne katika Bahari ya Pasifiki; French Polynesia, Kisiwa cha Easter, Visiwa vya Cook, na New Caledonia. Mlipuko katika Kisiwa cha French Polynesia wapelekea hofu ya maelfu ya maambukizi ya Zika, na uchunguzi wa kina waanza.Matokeo ya uchunguzi yaripotiwa kwa Shirika la Afya Duniani (WHO) Novemba 24, 2015 na Januari 27, 2016.

Machi 2, 2015 Brazili yaifahamisha WHO kuhusu ripoti ya maradhi yanayoambatana na vipele kwenye ngozi katika majimbo ya Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo. Kuanzia mwezi Februari 2015 hadi tarehe 29 Aprili 2015, takriban kesi 7000 za maradhi yanayoambatana na vipele kwenye ngozi yaripotiwa. Kesi zote hizo ni za wastani na hakuna taarifa za vifo. Hakukuwa na hisia kuhusu Zika wakati huu na wala hakukufanyika vipimo vya kugundua maambukizi ya virusi hivyo. 

Februari Mosi 2016: WHO yatangaza rasmi kuwa mahusiano ya hivi karibuni kati ya maambukizi ya Zika na dalili za 'microcephaly' na matatizo  megine ya ki-nyurolojia ni janga la afya kimataifa.

Historia hiyo inatufundisha nini?

Kwahiyo, kwa kuangalia tu historia ya virusi vya ugonjwa wa Zika, ni dhahiri kuwa taarifa ya Dokta Mwele, ambayo wala haikuwa yake binafsi bali ya taasisi za NIMR na Chuo Kikuu cha Bugando, haikukiuka kanuni au utaratibu wowote, kitu ambacho kinazua maswali kuhusu uamuzi wa Rais Magufuli kutengua wadhifa wa mwanasayansi huyo wa kimataifa.

Uamuzi wa Rais Magufuli kutengua ukurugenzi Mkuu wa Dkt Mwele NIMR:

Lakini kinachoashiria kuwa 'kuna namna' katika hatua hiyo ya Rais ni masuala yafuatayo:

Kwanza, taarifa iliyotolewa na Dokta Mwele ilishawasilishwa kwa Waziri husika kwa kufuata taratibu zilizopo, tarehe 12 mwezi Agosti 2016 na kupokelewa wizarani tarehe 16 mwezi huohuo. (kumbukumbu namba NIMR/HQ/D13) Kwa maana hiyo, sio kwamba Waziri husika alikuwa hana taarifa kuhusu matokeo ya utafiti huo. 

Na kwa vile alishawasilisha taarifa ya utafiti huo kwa Waziri, Dokta Mwele alikuwa na wajibu wa kutoa matokeo ya utafiti kwa watafiti na umma wa Watanzania wote. Sheria ya bunge namba 23 ya mwaka 1979 ya kuundwa kwa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (www.nimr.or.tz) kipengele cha "vi" kinaitaka taasisi kutoa matokeo ya utafiti wote unaofanyika ndani ya Tanzania. 

Dokta Mwele amekuwa akitoa taarifa hii kwa miaka saba ambayo amekuwa mkurugenzi mkuu. Ni lazima ieleweke kuwa hakuwa anatangaza MLIPUKO wa Zika - kazi ambayo ni ya Waziri/wizara - bali ripoti ya utafiti kuhusu Zika, na hivyo ni vitu viwili tofauti. Yayumkinika kuhisi kwamba tatizo hapa ni siasa kuwekwa mbele ya utaalamu na taaluma.

Kadhalika, wakati macho yameelekezwa kuhusu Zika pekee, Dokta Mwele siku hiyo aliongelea pia kuhusu utafiti wa magonjwa ya chikungunya, dengue na virusi vya West Nile.

Kumekuwa na nguvu kubwa inayotumika kujenga picha kuwa Dokta Mwele amekuwa insubordinate kwa Waziri husika. Lakini ukweli ni kwamba ramani hizo hapo juu zimethibitisha uwepo wa virusi vya Zika nchini Tanzania kwa muda mrefu. Kadhalika, utafiti uliofanywa na NIMR umesaidia kuongeza kile kiutafiti kinachofahamika kama 'body of evidence' ya kuelewa zaidi kuhusu kuenea kwa virusi vya ugonjwa huo na ugonjwa wenyewe.

Pili, Dokta Mwele aliongea na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) Alhamisi Desemba 15, 2016 kueleza alichosema kuhusu utafiti huo wa Zika. Kipindi hicho kilirushwa na BBC saa 12 asubuhi ya siku iliyofuata, Ijumaa Desemba 16, 2016. Sio kweli kwamba Dokta Mwele 'alifanya utovu wa nidhamu kwa kuongea na waandishi wa habari baada ya Press conference ya Waziri.' Ukweli ni kwamba aliongea kabla ya Waziri. Jitihada zinazofanyika kujenga picha ya 'utovu wa nidhamu' zaweza kutafsiriwa tu kama mbinu ya kuhalalisha hatua 'ya kionevu' iliyochukuliwa dhidi ya mwanasayansi huyo.

Pili, Dokta Mwele aliongea na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) Alhamisi Desemba 15, 2016 kueleza alichosema kuhusu utafiti huo wa Zika. Kipindi hicho kilirushwa na BBC saa 12 asubuhi ya siku iliyofuata, Ijumaa Desemba 16, 2016. Sio kweli kwamba Dokta Mwele 'alifanya utovu wa nidhamu kwa kuongea na waandishi wa habari baada ya Press conference ya Waziri.' Ukweli ni kwamba aliongea kabla ya Waziri. Jitihada zinazofanyika kujenga picha ya 'utovu wa nidhamu' zaweza kutafsiriwa tu kama mbinu ya kuhalalisha hatua 'ya kionevu' iliyochukuliwa dhidi ya mwanasayansi huyo.

Wakati uchunguzi huu unafanyika, ilibainika kuwa kuna jitihada za makusudi zinazoendelea mitandaoni 'kumchafua' Dokta Mwele. Kwa 'macho ya juu juu,' ni kama wananchi tu wanatoa maoni yao kuhusu suala hilo, lakini kwa yeyote atakayeangalia kwa 'jicho la tatu,' hatoshindwa kubaini kuwa kuna co-ordinated efforts' za kumchafua mwanasayansi huyo. Kwa bahati nzuri, juhudi hizo zinagonga mwamba kutokana na wananchi wengi kuonekana kumuunga mkono Dokta Mwele huku baadhi wakiamini kuwa ameonewa tu.

Kwa muda mrefu kulikuwa na kile kilichohisiwa kuwa jitihada za makusudi kuhakikisha Dokta Mwele anang'oka katika wadhifa huo. Miongoni mwa jitihada hizo ni pamoja na kuvujishwa hadharani mawasiliano ya kiofisi (yaliyopaswa kubaki ndani ya NIMR pekee) na tuhuma za ufisadi ambazo uchunguzi uliofanyika ulibaini kuwa hazikuwa na ukweli.

Mwaka jana, wakati Dokta Mwele alipochukua fomu za kuwania kuteuliwa kuwa mgombea wa urais kwa tiketi ya CCM, zilifanyika jitihada za kudukua mawasiliano yake, na uchunguzi ulibaini uhusika wa mwanasiasa mmoja maarufu wa chama hicho ambaye pia anahusishwa na jitihada za muda mrefu 'kuhakikisha Dokta Mwele anang'oka NIMR.' 

Hitimisho: 

Ripoti hii ya kiuchunguzi inaonyesha bayana ukweli kuhusu Dokta Mwele ameondolewa madarakani bila ya hatia yoyote. HAKUFANYA KOSA LOLOTE. Sheria ya NIMR inamruhusu kuripoti kuhusu tafiti mbalimbali kama hiyo ya kuhusu virusi vya Zika. Pia Waziri husika alipewa ripoti ya utafiti huo miezi minne kabla ya Dokta Mwele kuitangaza hadharani. 


Katiba inampa nguvu Rais kuteua na kutengua viongozi wa taasisi mbalimbali za umma. Rais Magufuli alitumia nguvu hiyo ya Kikatiba kuchukua uamuzi huo dhidi ya Dokta Mwele. Hata hivyo, pengine Rais atapata wasaa wa kujiuliza kwanini waziri husika alikuwa na taarifa za utafiti huo tangu mwezi wa Agosti mwaka huu lakini hakuziwasilisha kwake?  Kadhalika, kama Waziri husika hataki kuona ripoti za tafiti mbalimbali zikitangazwa na 'watu walio chini yake' basi na awasilishe muswada bungeni ili sheria iwezeshe hilo.

Mara kadhaa Rais Magufuli amekuwa akiwakumbusha Watanzania kuwa msema kweli ni mpenzi wa Mungu. Basi itakuwa vema asiishie kwenye kuhubiri tu kuhusu usemwa kweli bali sasa atekeleze kwa vitendo na kutafakari upya ukweli kuwa Dokta Mwele hajatendewa haki. Licha ya Dokta Mwele kuwa mchapakazi, kitu ambacho NIMR inajua, Watanzania wanajua na ulimwengu unajua, pia hana kosa katika suala hili. Hii haimaanishi kumfundisha kazi Rais au kumwekea shinikizo bali kushauri haki itendeke.

Kwa upande mwingine, japo ni dhahiri kuwa kutakuwa na nafasi luki za kimtaifa zinazomsubiri Dokta Mwele, hatua iliyochukuliwa dhidi yake inaweza kuwa na athari kubwa katika namna watafiti wanafanya kazi nchini Tanzania. Ikifika mahala watafiti kuhofi kutangaza matokeo ya tafiti zao hata kama wamefuata taratibu zote, watakaoathirika zaidi ni Watanzania.

Na mwisho, kwa vile tumebahatika kuwa na Rais msomi na mwanasayansi basi ni matarajio yetu kuwa ataweka kipaumbele kwenye ukweli kuliko majungu, maana sayansi is all about ukweli na sio hisia. Kadhalika, ni matarajio ya Watanzania kuwa Rais hatoruhusu siasa kuingilia utaalam na/au taaluma. Ikumbukwe kuwa moja ya vikwazo vikubwa vya maendeleo yetu ni siasa kuingilia kila eneo. Ili azma za Tanzania, kwa mfano sera ya 'Tanzania ya viwanda' zitimie, ni lazima tuwasikilize watafiti. Na linapokuja suala la afya ambalo ndio uhai wetu, hatuna hiari wala uchaguzi kuwapuuza wataalamu katika sekta hiyo kama Dokta Mwele.

MUNGU IBARIKI TANZANIA



Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.