Showing posts with label EDWARD LOWASSA. Show all posts
Showing posts with label EDWARD LOWASSA. Show all posts

18 Feb 2018


Nianze makala hii kwa kutoa salamu zangu za pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Daniel John, ambaye hadi alipouawa kinyama alikuwa Katibu wa Chadema kata ya Hananasifu, na pia kwa familia, ndugu,jamaa na marafiki wa marehemu Acqulina Akwilin (samahani kama nimekosea jina).

Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe, mwili wa marehemu Daniel uliokotwa kwenye ufukwe wa Coco jijini Dar es Salaam ukiwa na majeraha. Alieleza kuwa awali marehemu alichukuliwa na Land Rover nyeupe na watu waliohifanya askari polisi, lakini tangu wakati huo Polisi hawakuwa na taarifa zozote za kiuchunguzi, na hata jitihada za kupatikana mwili huo zilifanywa na Chadema wenyewe.




Kwa upande wa marehemu Acquilina, kifo chake kilisababishwa na kasumba hatari inayozidi kuzoeleka kwa watumishi wa vyombo vya dola kufanya mzaha katika matumizi ya silaha za moto, ambapo katika tukio husika, polisi waliokuwa wakizuwia maandamano ya wafuasi wa Chadema, walitumia risasi za moto,na moja kati ya risasi hizo ilipelekea kifo cha binto huyo, ambaye hadi mauti yanamfika alikuwa mwanafunzi katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) akisomea shahada ya ununuzi na ugavi.
Ni muhimu kutambua kuwa vifo vyote hivi viwili vingeweza kuepukika laiti utu na ubinadamu wetu ungewekwa mbele ya chuki za kisiasa. Huhitaji kuwa mjuzi wa uchunguzi wa mauaji kufahamu kuwa vifo hivyo ni matokeo ya chuki, hujuma, uonevu na kila aina ya baya dhidi ya chama kikuu cha upinzani, Chadema, kuhusiana na kampeni za uchaguzi mdogo katika jimbo la Kinondoni, ambalo kama ilivyo kwa jimbo la Siha, ni "piga ua" kwa CCM ishinde. Yaani chama hicho tawala kilitarajiwa kutumia kila mbinu kuhakikisha inashinda katika majimbo hayo mawili.

Lakini kabda sijaingia kwa undani katika mada hii - ambayo lazima nikiri kwamba inanipa wakati mgumu sana kuiandika kwa sababu nimebanwa na mchanganyiko wa majonzi na hasira, sambamba na hofu ya kuona taifa langu likisukumwa kuelekea kwenye upotevu wa amani na mshikamano wetu – naomba kuweka wazi masuala matatu ya msingi kunihusu mie mwandishi wa mwakala hii.

Kwanza, mimi licha ya kuwa na makazi nje ya Tanzania kwa takriban miaka 15 sasa bado no Mtanzania. Utanzania wangu ni haki nilioirithi kutoka kwa wazazi wangu, na itabaki hivyo milele. Naeleza hili kwa sababu kuwa wabaguzi wanaopenda kutuhukumu Watanzania tunaoishi huku ughaibuni, na kutaka tuonekane kama Utanzania wetu sio kamili. Kwa mantiki hiyo, kama Mtanzania, nina kila haki ya kutoa maoni yangu kuhusu mustakabali wa taifa letu, hususan katika nyakati hizi ambapo kuna dalili za wanaotaka kulipeleka kubaya taifa letu.

Pili, mwaka 2015 nilishiriki kikamilifu katika kampeni zilizomwingiza madarakani Rais John Magufuli. Kwa upande mmoja nililazimika kumkampenia Magufuli kwa vile nilikuwa nina "sababu binafsi" dhidi ya aliyekuwa mpinzani wake mkuu, mgombea urais wa tiketi ya UKAWA, Edward Lowassa. Wanasema "adui ya adui yako ni rafiki yako."Kwa upande mwingine, nililipwa kutoa huduma ya ushauri wa kitaalamu (usadi, yaani consultancy kwa kimombo) hususan kwenye mitandao ya kijamii. Natanabaisha hili ili asije akakurupuka mtu na kusema "ah ulishiriki kutupigia kampeni kwa vile tulikupa pesa."

Tatu, huko nyuma nilikuwa mtumishi wa Idara ya Usalama wa Taifa. Na kabla ya kuanza utumishi katika taaluma hiyo muhimu na nyeti, nilikula kiapo kwa nchi yangu, kiapo ambacho nitaishi nacho hadi ninaingia kaburini. Kiapo hicho sio cha kukitumikia chama flani au viongozi wake bali Tanzania yetu. Nchi ni muhimu  kuliko vyama vya siasa au wanasiasa.

Mtu aliyepikwa na kuiva kwenye taaluma ya uafisa usalama wa taifa, katika nchi yoyote ile, anapaswa kubaki kuwa mtiifu kwa nchi yake bila kujali yupo ndani au nje ya ajira ya taasisi inayohusika na usalama wa taifa wa nchi husika.

Wanasema hata nje ya ajira rasmi, kila mtu aliyewahi kuwa afisa usalama wa taifa anaendeshwa na "sense of public duty born in their previous lives" yaani wajibu kwa umma uliozaliwa katika maisha yao huko nyuma. Jasusi mmoja mstaafu anaeleza “...I have obligations, professional obligations. If there’s a national security emergency or possible national security issue, I should report it."


Kwahiyo, hata kama "maafisa wenzangu wa zamani" wataamua kukaa kimya kwa sababu moja au nyingine – wengi wanahofia usalama wa maisha yao – sie wengine hatuwezi kukaa kimya, hasa kwa vile baadhi yetu tumeshalipa gharama kubwa kwa kelele zetu. Kukaa kimya ni sawa na kuafiki uhuni unaoendelea ambao ni tishio kwa usalama wa taifa.

Lakini licha ya wajibu huo unaotokana na utumishi wetu kwa nchi huko nyuma, Rais Magufuli amefanikiwa kuvifunga mdomo vyombo vya habari kiasi kwamba haviwezi kusema lolote kuhusu "mabaya" yake, na amefanikiwa kuvijengea nidhamu ya uoga vyombo hivyo vya habari kiasi kwamba habari pekee zenye umuhimu kwao ni za kumtukuza na kumpamba "mungu-mtu" huyo. Kwahiyo na sie tuliopikwa na kuiva kuhusu ujasiri, kujitoa mhanga na kutokuwa waoga tukiufyata na kukaa kimya - ilhali media zetu ndio zishapigwa kufuli - hali itazidi kuwa mbaya.


Baada ya kuweka wazi nafasi yangu, sasa tuangalie kwa kina kinachoendelea huko nyumbani hasa kuhusiana na uchaguzi mdogo kwenye jimbo la Kinondoni na Siha na kuuawa kwa Daudi na Acquiline.

Ni muhimu kutambua kwamba ukandamizaji dhidi ya vyama vya upinzani sio kitu kilichoanza chini ya utawala wa Magufuli bali hali hiyo imedumu mfululzo tangu kuanzishwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi mwaka 1992. Labda kilicho tofauti kwa zama hizi ni "ujasiri" wa Magufuli kutoficha chuki yake dhidi ya vyama vya upinzani. Yaani angalau akina Mwinyi,Mkapa na Kikwete walikuwa "wanauma na kupuliza." Kwamba angalau walikuwa na "mshipa wa aibu" na walijitahidi japo kutowaonea Wapinzani waziwazi.

Kwa wanaojua "yanayojiri nyuma ya pazia" watakwambia kuwa hujuma dhidi ya vyama vya upinzani ni miongoni mwa vipaumbele vikubwa kwa CCM na serikali zake, na hiyo imepelekea kujengeka "symbiotic relationship" kati ya chama hicho tawala na taasisi za dola, ambapo kila mmoja anategemea uhai wa mwenzie.

Lakini kama kuna kitu kinachokera zaidi kuhusu hujuma dhidi ya demokrasia ni pale CCM na taasisi zake hasa za dola wanapoweka mbele maslahi yao mbele ya utu na uhai wa Watanzania. Na hili halijaanza jana au katika kampeni za chaguzi ndogo katika majimbo ya Kinondoni na Siha.

Uchaguzi mkuu wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995 ulihusisha matukio mengi tu ambayo kwa makusudi hayapo kwenye kumbukumbu za wazi (japo yamehifadhiwa mahala flani).

Lakini kama wanavyosema "amekula asali sasa anachonga mzinga," baada ya hujuma za kimyakimya za mwaka 1995 kuzaa matunda, CCM na taasisi zake ikanogewa, na matokeo yake ni kwamba uchaguzi mkuu uliofuata, mwaka 2000 uliweka doa kubwa kwa historia ya Tanzania yetu ambapo kwa mara ya kwanza nchi yetu ilizalisha wakimbizi kufuatia unyama uliofanyika huko Zanzibar na kupelekea vifo kadhaa (idadi halisi ya vifo haijawahi kuwekwa hadharani japo "wenyewe" walisema zaidi ya watu 19 ndio waliokufa kwenye machafuko hayo. Wasichosema pia ni idadi ya watu waliobakwa, kuteswa na kuwekwa kizuizini.

Kwamba hujuma hizo za CCM dhidi ya demokrasia zilipelekea vifo na majeruhi ni kitu kibaya kabisa. Lakini kitu kingine kibaya ni ukweli kwamba hakuna mtu hata mmoja aliyechukuliwa hata kutokana na unyAma waliofanyiwa Wazanzibari hao.

Kwa namna ya kipekee, CCM ikawa kama imepewa ruhusa ya kutumia vyombo vyake vya dola kufanya lolote itakalo ili ifanikishe hujuma zake dhidi ya Wapinzani na demokrasia kwa ujumla, kisha iibuke na ushindi.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 ulikuwa na "uchafu kupindukia." Kundi lililofahamika kama "mtandao" lilijipenyeza katika kila sekta, kuanzia kwenye vyombo vya habari, taasisi za dola hadi kwenye taasisi za dini. Yayumkinika kabisa kuhitimisha kwamba yaliyojiri wakati "mtandao unafanya jitihada za kumwingiza mtu wao Ikulu" ni mabaya zaidi ya haya tunayoshuhudia sasa tangu Magufuli aingie madarakani.

Kwanini basi hayo yaliyojiri kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 hayajulikani? Jibu ni kwamba, wakati mbinu iliyotumika mwaka 1995 na 2000 ilitegemea zaidi vyombo vya dola, uchaguzi wa mwaka 2005 na 2010 ulitegemea zaidi nguvu ya fedha, nyingi zikiwa fedha haramu. Na sehemu ya fedha hiyo ilitumika "kununua ukimya" wa wanahabari wengi tu. 

Lakini si fedha tu bali pia kuna hujuma mbalimbali – nyingine chafu na za kuchefua – zilizotawala safari za ushindi wa chama tawala kwenye chaguzi hizo.


Image result for lowassa kikwete 2005

Labda tofauti nyingine kuhusu mwaka 2005 na 2010 ni ukweli kwamba wakati chaguzi hizo zilihusisha "kikundi binafsi" yaani hicho cha wanamtandao ambacho hakikuwa taasisi ya serikali au chama.

Lakini muda wote huo, CCM ilikuwa kama imepwa ruhusa na Watanzania kuendeleza hujuma zake dhidi ya Wapinzani na demokrasia kwa ujumla. Hakujawahi na utashi miongoni mwa Watanzania kutaka kukabiliana kwa dhati za uhuni/uhalifu wa kisiasa. Na kwa bahati mbaya, kwa vile vipaumbele vya Watanzania wengi ni kwenye "ubuyu" na "kubeti/mkeka" basi habari mbaya ni uwezekano wa CCM kuendelea kufanya itakavyo kwa muda mrefu sana.

Sio kama kwa kubashiri kuwa unyanyasaji wa CCM utaendelea muda mrefu sana ninamaanisha kuwa nimekata tamaa. Hapana. Ninakuwa mkweli tu. Tatizo ni zaidi ya CCM na uhuni wake. Watanzania wenyewe ni sehemu ya mfumo unaowezesha CCM kufanya uhuni/uhalifu huo.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ulihusisha pia matuki kadhaa yaliyojiri "nyuma ya pazia." Na ukitaka kufahamu kuwa Tanzania yetu haijawahi kuhangaishwa na mauaji ya kisiasa – kuanzia yale ya mwaka 2001 huko Zanzibar hadi haya ya Daudi wa Hananasifu na dada Acquilina – ni kifo cha Mchungaji Christopher Mtikila.


Kwahiyo, na ninaandika haya kwa uchungu mkubwa uliochanganyika na hasira, kuuawa kwa Daudi na Acquilina kutaishia kuwa moja tu ya matuko yaliyowahi kutokea katika Tanzania yetu. Tutawasikia wanasiasa wetu wa vyama vya upinzani wakiongea kwa hisia kubwa. Tutashuhudia pia wanafiki wengi tu miongoni mwa wasanii wetu nao wakijifanya kuguswa na vifo hivyo, lakini wakiwa makini kuepuka kumuudhi "Bashite na baba yake" au kuitibua CCM. Tutashuhudia pia kundi la wanafiki hatari ndani ya CCM wakijifanya kuumizwa na mauaji hayo, na kutaka uchunguzi ufanyike, ilhali nao ni kondoo waliojivika ngozi ya mbwa mwitu.



Kama ambavyo "mauaji mengine ya kisiasa" yalivyoruhusiwa kupita kimyakimya, ndivyo unyama huu uliofanywa dhidi ya Daudi na Acquilina utakavyoruhusiwa uishe kimyakimya.

Kwa upande mmoja tusitarajie Rais Magufuli awajibike – sio kwa yeye binafsi kujiuzulu kwa sababu hilo litakuwa kutarajia zaidi ya muujiza – kwa kumtimua Waziri husika na watendaji katika jeshi la polisi. Kwa upande mwingine, hakuna wa kumshinikiza Rais Magufuli achukue hatua stahili dhidi ya wahusika.

Na nisingependa kuuma maneno hapa. Yeye Magufuli mwenyewe ni chanzo muhimu cha siasa hizi za uhasama zinazoendelea kuitafuna Tanzania yetu. Huyu ni mtu ambaye wala hapati shida kuonyesha chuki zake za waziwazi dhidi ya Wapinzani, Upinzani na demokrasia kwa ujumla.


Kama ilivyo kwa madikteta wengine duniani, Magufuli amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kutumia ajenda yake ya ufisadi kama kisingizio cha kusigina haki za binadamu nchini Tanzania, na kubinya kila fursa ya haki za kidemokrasia na uhuru wa habari. Kama nilivyoeleza awali, amefanikiwa kuviziba midomo vyombo vya habari na ndio maana hata habari za kusikitisha kuhusu mauaji ya Daudi na Acquiline hazijaripotiwa vya kutosha.

Kwa kuviziba midomo vyombo vya habari Magufuli amefanikiwa kuzuwia "habari asizozipenda" na ndio maana hadi muda huu ni Watanzania wachache tu wanaofahamu kilichojiri huko MKIRU katika kilichoitwa "operesheni dhidi ya ugaidi." Kuna siku yaliyojiri huko – na ambayo yamechangia "kupotea" kwa mwandishi wa gazeti la Mwananchi Azory Gwanda – yatajulikana hadharani. Haijalishi itachukua miaka mingapi.


Lakini "yaliyojiri MKIRU" ni uthibitisho mwingine wa hicho nilichoeleza hapo juu kuwa Watanzania wenyewe ndio wanaopaswa kubeba lawama nyingi katika kasumba ya CCM kutojali uhai katika harakati zake za kukandamiza demokrasia. Kwamba kama yaliyojiri MKIRU yameachwa yaishe kienyeji, kwanini tutegemee hali tofauti kwa vifo vya Daudi na Acquiline?

Kama ndugu zetu wa Chadema (na kila mpenda haki) "wamekubali yaishe" kuhusu kifo cha Kamanda Mashaka, "kupotea" kwa kada Ben Saanane (hata zile kampeni za #BringBackBenAlive zimejifia kifo cha asili), na hawasumbuliwi na serikali ya Magufuli kupuuzia jaribio la mauaji dhidi ya Tundu Lissu, kwanini tutarajie jipya katika mauaji yaliyofanywa dhidi ya Daudi na Acquiline?

Yaani Mnadhimu Mkuu wa upinzani anamwagiwa risasi hadharani wakati mkutano wa bunge unaendelea huko Dodoma, na tunaambiwa kuwa tukio hilo lilitokea katika eneo lenye ulinzi mkubwa na lenye CCTV, kwanini basi wanaosumbuliwa na tukio hilo wasitafute njia stahili za japo kuifanya serikali ione aibu na kufanya japo "uchunguzi wa kizushi"?

Kuhusu hujuma "za kawaida" za uchaguzi, kama kila aina ya uhuni uliofanywa na CCM kwenye chaguzi ndogo za madiwani katika kata 43 uliofanyika Novemba mwaka jana uliruhusiwa upite "kimya kimya" – kwa maana kwamba hakuna hatua zozote zilizochukuliwa dhidi ya uhuni huo – kwanini basi chaguzi hizi ndogo katika jimbo la Siha na Kinondoni zilitarajiwa kuwa tofauti?

Na katika hili, inapaswa wana-Chadema wajiulize kuhusu busara za viongozi wao kuamua kushiriki katika chaguzi hizo ndogo Siha na Kinondoni ilhali mazingira yaliyokuwepo yalikuwa yaleyale yaliyopelekea chama hicho kususia chaguzi nyingine ndogo tatu katika majimbo ya Longido, Singida Kaskazini na Songea Mjini uliofanyika mwezi uliopita.

Hadi wakati ninaandika makala hii, tayari Tume ya Uachaguzi ilikuwa imeshamtangaza mgombea wa CCM jimbo la Siha, Godwin Mollel kuwa mshindi kwa tofauti kubwa tu ya kura dhidi ya mgombea wa Chadema. Hata kama CCM wameiba kura, ukubwa wa tofauti kati ya kura za mgombea wao na huyo wa Chadema zinaashiria kuwa chama hicho kikuu cha upinzani kilipitisha mgombea fyongo.


Na kama ilivyotarajiwa mgombea wa CCM jimbo la Kinondoni, Maulid Mtulia, naye ametangazwa mshindi.


Mie mtumishi wako nilishabashiri mapema tu kuwa chama hicho tawala kingeshinda majimbo hayo, "iwe isiwe."

Ushindi kwa wagombea hao wa CCM ulipaswa kupatikana kwa gharama yoyote kwa sababu laiti wangeshindwa, kinachoelezwa kama "mkakati wa Magufuli kuua upinzani kwa kununua wabunge na madiwani wa Upinzani"  kingemfanya achekwe hata huko kwenye chama chake.

Na kwa vile hadi sasa wabunge na madiwani waliohama upinzani na kujiunga na CCM wamefanikiwa kurudi madarakani baada ya chama hicho tawala kuwapa fursa ya kuwa wagombea wake kwenye chaguzi ndogo, na kuwasaidia kwa hali na mali washinde, tutarajie wabunge na madiwani wengin zaidi kuhama vyama vya upinzani na kujiunga na CCM. Kisa? "Dili hilo linalipa," kwa CCM na kwa wanasiasa hao wanaohama.

Na unadhani mbunge au diwani "mwenye moyo mwepesi" akiona jinsi chama chake "kilivyochukulia poa" yaliyowasibu akina marehemu Mashaka na Daudi, na yaliyowasibu Ben Saanane na Lissu, kwanini iwe ngumu kwake kushawishika kuhama?

Ningetamani sana kuhitimisha makala hii kwa kushauri nini kifanyike lakini itakuwa kupoteza muda wangu na muda wako msomaji. Ni vigumu mno kuwashauri watu waliokubali kwamba mgao wa umeme ni stahili yao kwa zaidi ya miaka kumi sasa, na ambao kila mara umeme unaporudi wanashangilia kana kwamba wamepewa upendeleo flani.

Kama Watanzania wameshindwa kuilazimisha Tanesko iache mgao wa umeme, wataweza kweli kuilazimisha CCM iache hujuma dhidi ya vyama vya upinzani na demokrasia kwa ujumla? Ndio maana bila utu wala aibu, chama hicho tawala kinapata ujasiri wa kukifanyia mzaha kifo cha Acquiline ambapo kwa kudai polisi (haohao waliomuua binti huyo) wachukue hatua dhidi ya Mbowe. Utterly disgusting!


Na kama mauaji mbalimbali ya kisiasa huko nyuma yameachwa yapite na kusahaulika, kwanini tutarajie miujiza kwenye mauaji haya ya sasa dhidi ya wapendwa wetu Daudi na Acquline?

Na ukweli mchungu ni kwamba Magufuli ataendelea kuwapelekesha Watanzania atakavyo ka sababu si watangulizi wake -Mwinyi, Mkapa na Kikwete – wenye jeuri ya kumwambia "Ee bwana ee, huku unakoipeleka nchi siko." Hawawezi kwa sababu nao ni kama "mateka." Madhambi waliyofanya kwenye tawala zao yanawafanya wahofie hatma yao pindi wakimkosoa "mungu-mtu" aliyepo madarakani.

Na wakati wastaafu au watumishi wa zamani wa Idara za Usalama wa Taifa kwenye nchi kama Marekani wamekuwa mstari wa mbele kukemea kila tendo linalotishia usalama wa nchi hiyo – kwa mfano 'ndoa' kati ya Rais Donald Trump na Russia – wastaafu wetu sie hawana jeuri ya kufungua mdomo sio tu kwa vile wanahofia kuathiri posho na marupurupu yao bali kwa vile nao ni mateka wa "madudu" waliyofanya walipokuwa madarakani. Ukiwa mchafu unajinyima uhuru wa kukemea uchafu.


Basi niishie hapa kwa kurejea tena salamu zangu za pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Daudi na Acquiline. Ni vigumu kuwaambia maneno yanayotosha kuwaliwaza lakini la muhimu ni kuendelea kuzikumbuka roho za marehemu hao, hasa katika kipindi hiki cha Kwaresma ambapo sisi Wakristu tunaadhimisha mateso ya Bwana Yesu Kristo. Pumziko la Milele awape Bwana, na Mwanga wa Milele awaangazie, wapumzike kwa amani. Amen


3 Jan 2017



Kuna msemo wa kisiasa unaosema "in politics, perception is reality." Maana yake katika tafsiri isiyo rasmi ya Kiswahili ni kwamba 'katika siasa, kitu kinavyoonekana ni sawa na uhalisi wake. 

Kwa mantiki hiyo, kura ya maoni iliyobandikwa na gazeti la Raia Mwema katika akaunti yake kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter ikiwa na swali kama linavyoonekana katika 'tweet' husika hapa chini, inaweza kuwa na uzito.

Ndio, siyo kura ya kisayansi lakini idadi ya watu 448 'waliopiga kura' (hadi wakati ninaandaa makala hii) ni sampuli ya kutosha kwa kura ya maoni. 
Natambua makada wa CCM hawatopendezwa na makala hii, na huenda kuna watakaohoji kwanini niipe uzito kura ya maoni ya Twitter. Jibu langu ni hilo kwenye sentensi ya kwanza, "in politics, perception is reality." Lowassa kuongoza katika kura hiyo ya maoni kunajenga perception flani ambayo kwenye siasa ni reality. 

Neno la tahadhari kuhusu kura hiyo ya maoni ni kwamba bado inaendelea na haijafikia tamati. Kwahiyo, matokeo ya mwisho yanaweza kuwa tofauti, hasa ikzingatiwa kuwa tofauti ya asilimia ni kiduchu.

Pengine moja ya vitu vinavyompunguzia umaarufu Rais Magufuli ni baadhi ya kauli zake...kama hii hapa pichani chini. Ikumbukwe kuwa moja ya sifa ya uongozi bora ni pamoja na kutumia lugha isiyojenga picha ya dharau au kukosa huruma kwa wananchi. Na tukiamini kuwa 'in politics, perception is reality,' basi picha hasi inayoweza kutokana na baadhi ya kauli za Rais Magufuli zaweza kujenga taswira hasi kumhusu yeye na uongozi wake, hata kama hatamki kwa nia mbaya.




17 Mar 2016


Nilianza kumsikia Balozi Mwapachu tangu nikiwa mtoto mdogo. Huyu ni miongoni mwa yale majina ambayo miaka nenda miaka rudi utayasikia, kama sio kwenye uwaziri basi ni kwenye ukurgenzi wa taasisi flani, au uongozi wa tume flani kama sio ubunge. Wenzetu hawa ni kama watu waliozaliwa ili kuwa viongozi. Lakini hio sio dhambi wala kosa, maana yawezekana kuzeekea kwao katika uongozi ni matokeo ya uongozi wao wa kupigiwa mstari.

Hold on, nimesema 'uongozi wa kupigiwa mstari'? May be, maana dunia hii tunayoishi sasa hata sifa za uognzi hazijulikani ni zipi. Na sababu ya wazi ya sifa za uongozi kupoteza maana yake ni ubabaishaji, usanii,ufisadi, ujambazi, na kila baya unaloweza kulihusisha na tasnia ya uongozi.

Sie wengine tulikulia zama za chama kimoja. Tulishuhudia uongozi uliotukuka wa Mwalimu Nyerere. Ndio, kulikuwa na kasoro zake, kama vile viongozi kuonekana kama miungu-watu, lakini hawakuonekana miungu-watu kwa sababu ya utajiri wao bali angalau waliutumikia umma kwa namna moja au nyingine.

Tuliwaona viognozi mashambani, tuliwaona wakishiriki katika shughuli za ujenzi wa taifa, matengenezo ya barabara, ushiriki katika ujenzi wa miradi ya maendeleo, na vitu kama hivyo. Kumbuka, enzi hizo tulikuwa nchi ya ujamaa na kujitegemea, na miongoni mwa features za kujitegemea ilikuwa kutumia raslimali zetu, sio siku hizi zama za kutembeza bakuli kwa wafadhili, kisha kinachopatikana 'kinapigwa panga,' watu wanaporomosha mahekalu, wanaongeza idadi za magari yao ya kifahari, na sensa ya nyumba ndogo zao inazidi kukua.

Kwanini nimeandika 'kwa hasira' hivi? Jana nimesikia kituko kilichonichefua. Mmoja wa Watanzania wenye majina makubwa katika medani za uongozi, Balozi Juma Mwapachu, jana alitangaza kurejea CCM baada ya kukihama chama hicho tawala wakati tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu.

Kama nilivyosema awali, nimekuwa nikimsikia Juma Mwapachu tangu nikiwa mdogo. Lakini, mwaka jana nilipata fursa ya kuwasiliana nae. Sio uso kwa uso bali kupitia kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter. Sijui tulikuwa tunajadili nini lakini moja ya ajenda iliyojitokeza ni sapoti yake kwa Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, ambaye baadaye aliteuliwa kuwa mgombea Urais kwa tiketi ya UKAWA. 

Balizo Mwapachu alijitokeza kuwa miongoni mwa watetezi wakuu wa Lowassa, huku nyakati kadhaa akitukumbusha 'yeye ni nani.' Wapo walioungana nae mkono lakini baadhi yetu tulimpinga waziwazi na kueleza bayana kuwa ni 'wazee' kama yeye walioifikisha Tanzania yetu mahali hapa pasipoeleweka. Baadaye akapotea mtandaoni, pengine kwa sababu 'wazee' kama yeye hawajazowea sana 'mbinde' za social media.

Alipotangaza kuachana na CCM na kumfuata Lowassa, halikuwa jambo la kushangaza kwa sie tuliowahi kushuhudia akimtetea huko Twitter. Baada ya kuhama CCM akajitahidi kutumia uweledi wake kueleza, kwanza kwanini CCM ni 'kimeo,' na pia kwanini Lowassa ndio ufumbuzi wa matatizo yanayoikabili Tanzania. Baadhi ya aliyoyasema yalikuwa na ukweli, lakini baadhi yetu hatukumuelewa kwa sababu moja tu: "alikuwa wapi siku zote hizo?" Yaleyale ya akina Lowassa, Kingunge, Sumaye na wengineo waliogeuka wakosoaji wakubwa wa mfumo walioshiriki kuuasisi huko CCM, mfumo wa wateule wachache huku mamilioni ya walalahoi wakiishia kuahidiwa hili kama sio lile.

Sasa jana akaamua kubadili gea angani, akatangaza kurudi CCM. Good, kuhama sio dhambi. Tatizo la msingi ni baadhi ya sababu alizoeleza kuwa zilimpelekea kuhama CCM na sasa kuamua kurejea.

Anadai 'alilewa' na ahadi ya Lowassa kuwa angepewa Uwaziri wa Mambo ya Nje. Hivi inaingilia akilini kweli kwa mtu kama huyo ambaye alikuwa miongoni mwa 'vijana wa Nyerere' kuhama chama alichokiasisi baba wa taifa kwa sababu tu alitarajia kupewa uwaziri wa mambo ya nje? Pengine sio kosa kwa sababu ni watu wangapi wasiotaka madaraka?

Lakini ili umuelewe vema ni muhimu kurejea posts zake mbalimbali huko Facebook na kwingineko alivyokuwa akiwahadaa vijana kuhusu ajenda ya mabadiliko. Kwanini nasema alihadaa? Kwa sababu mwenyewe amekiri jana kuwa kilichomvutia kwa Lowassa ni ahadi ya uwaziri wa mambo ya nje. Kule anahubiri kuhusu mabadiliko, huku anawazia uwaziri wa mambo ya nje. Baada ya Lowassa kushindwa kupata urais, na ndoto ya Mwapachu kuwa waziri wa mambi ya nje kuota mbawa, kaamua kurejea CCM. 

Tabia kama hizi zinaweza kuigharimu CCM huko mbeleni. Watu walioikimbia wakati wa shida (kwa maana ya mapambano ya kumwingiza mgombea wake Ikulu) wanaruhusiwa kurejea kiulaini tu na kigeugeu chao kurushwa na vyombo vya habari kana kwamba ni matukio yenye umuhimu mkubwa kihistoria.

Laiti ningekuwa na mamlaka huko CCM, ningemweka benchi Mwapachu kwa sababu kama alivyoondoka akiwa hana umuhimu wowote kwa chama hicho, ndivyo alivyorudi akiwa na umuhimu mdogo zaidi ya ule ambao hakuwa nao wakati anahama.

Nimalizie makala hii ya dharura kwa kutamka bayana kuwa Tanzania yetu imefikishwa hapa na vipongozi kama hawa, walafi wa madaraka licha ya kuwepo madarakani miaka nenda miaka rudi, viongozi wasio na msimamo, wanaoweza kuhadaa umma kuhusu mabadiliko ilhali mabadiliko pekee wanayopigania ni ya maslahi yao binafsi.

Nigusie jambo moja dogo baada ya majuzi kutangazwa viongozi wapya na wa zamani kuongoza mikoa yetu kama ma-RC. Sina tatizo na wengi walioteuliwa lakini kilichonisikitisha ni kuona baadhi ya sura zilezile za miaka nenda miaka rudi zikirudishwa kwenye uongozi. Kama mtu alikataliwa na wapigakura jimboni kwake kwanini apelekwe kuongoza watu wa mkoa mwingine? 

Na lini vijana wapya watapewa fursa ya kuongoza Watanzania wenzao iwapo tunaendelea ku-recycle sura zilezile? Mimi ni sapota mkubwa wa Rais Magufuli, tangu wakati wa kampeni hadi sasa. Ninaridhishwa mno na uongozi wake. Hata hivyo, hiyo haimaanishi akikosea sintomkosoa. Na kama nina moja la kumkosoa ni kutujazia sura za watu waliokaa kwenye uongozi miaka nenda miaka rudi [na usidhani ninalaumu kuhusu hilo kwa vile nilikuwa/nina matarajio ya uongozi. Licha ya kuridhiska na kidogo ninachopata hapa, pia ninaamini kuwa ili kuitumikia Tanzania yetu sio lazima mtu awe kiongozi. Just be a good mwananchi]

Yayumkinika kuhisi kuwa watu wa aina hiyo hawana cha kupoteza wakiboronga na kutimuliwa, kwa sababu baadhi yao tayari wanakula pensheni za ubunge au ukurugenzi wa kitu gani sijui. Wakitimuliwa, watanufaika kwa nyongeza ya fedha tu.

Na sintoshangaa pengine Mwapachu karudi CCM kubahatisha kupewa 'pande' la ubalozi. Na huwezi kumlaumu sana kwa sababu medani ya uongozi wetu imekuwa ni suala la ku-recycle watu walewale, wengi wakiwa ndio walioifikisha Tanzania yetu hapa tusipostahili kuwa.





28 Aug 2015


KABLA sijaingia kwa undani katika makala hii, ambayo niliahidi katika toleo la wiki iliopita, nitajadili kwa kina kuhusu mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Magufuli, ningependa kumpa pole mwanasafu mwenzangu Johnson Mbwambo, kutokana na wingi wa ujumbe mfupi wa maneno (sms) na vitisho kila anapoikosoa Chadema.
Mimi pia nimekuwa mhanga mkubwa wa tabia hiyo ya kukera ambayo imejitokeza mara baada ya mgombea wa urais kwa tiketi ya Chadema/UKAWA kujiunga na chama hicho. Hali kwangu ni mbaya zaidi kutokana na uwepo wangu mkubwa kwenye mitandao ya kijamii.
Nimeitwa kila aina ya jina na kutukanwa kila aina ya tusi, huku tuhuma kubwa kila ninapoikosoa Chadema au UKAWA ikiwa eti ‘nimenunuliwa na CCM’ au ‘kuahidiwa kitu fulani’.

Kuna ‘wastaarabu’ ambao wananilaumu bila kutumia lugha chafu. Wanadai kuwa mtizamo wa machapisho yangu katika gazeti hili na katika blogu yangu ulikuwa ni kuiunga mkono Chadema na kuikosoa CCM. Sasa wananilaumu kwa vile eti ‘nimewasaliti’ na kwa kuikosoa Chadema au UKAWA, ninaiunga mkono CCM.
Awali suala hili lilinisumbua sana kwa sababu wengi wa watu hawa walikuwa wakiilaumu serikali ya CCM kwa kuja na muswada wa kupambana na uhalifu wa mtandaoni (Cybercrime Bill) na kudai ulilenga kuwanyima uhuru wao wa kujieleza.
Iweje leo watu haohao wafanye kilekile walichokuwa wakiilaumu serikali: kutunyamazisha wenzao wenye mitizamo tofauti nao? Hivi hapa kuna neno sahihi zaidi ya unafiki?
Hatimaye nimefanikiwa kuelewa chanzo cha tatizo hilo ni kipi: kukata tamaa, kuchanganyikiwa, na kukosa mwelekeo.

Chuki kubwa waliyonayo dhidi ya CCM, sambamba na matamanio ya kukiona chama hicho tawala kinaondoka kwa gharama yoyote ile, kumepelekea watu hao kuweka imani isiyo na ukomo kwa mgombea urais kwa tiketi ya chama chao, yaani Lowassa.
Sasa yeyote atakayeongea chochote kile kinachoonekana kupunguza nafasi ya Lowassa kuingia Ikulu anaonekana kama adui wa mabadiliko.
Wakati nimeanza kuzoea matusi na lugha chafu inayoelekezwa kwangu, wasiwasi wangu mkubwa ni hatma (aftermath) ya uchaguzi mkuu katika nafasi ya Rais.
Ninabaki kujiuliza, hivi hawa watu wenye matumaini makubwa kupindukia kuwa mgombea wao ataingia Ikulu, watakuwa katika hali gani iwapo matokeo yatakuwa kinyume?
Je watakubali tu matokeo na kufanya post-mortem kistaarabu au ndio tutajikuta tunarudi katika hali iliyojitokeza huko Zanzibar baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2000 (Mola aepushe)?
Sasa niingie kwenye mada ya wiki hii. Kama nilivyoeleza katika makala tangulizi, nchi yetu itaingia katika uchaguzi huku kwa kiasi mazingira ya uchaguzi yakiwa yanaipendelea CCM.
Na pengine hili ndilo kosa kubwa wanalofanya wafuasi wa UKAWA; kutarajiwa matokeo tofauti katika uchaguzi unaofanyika katika mazingira yaleyale ‘yaliyowaliza’ katika chaguzi zilizotangulia.

Kwamba watu wengi wamechoshwa na CCM wala si suala la mjadala. Maelfu kwa maelfu ya watu wanaojitokeza kwenye shughuli za kisiasa za Lowassa sio kuashiria cha umaarufu wa mwanasiasa huyo bali hiyo kiu ya kuoina CCM inatoka madarakani. Lakini busara kidogo tu zatosha kutufahamisha kuwa kutaka kitu na kupata kitu ni vitu viwili tofauti.
Watanzania wengi waliochoshwa na CCM, wanataka kuiona inaondoka madarakani hata kesho. Lakini kuwezesha matakwa hayo yatimie si suala rahisi. Naomba nieleweke hapa, Ninasema SI RAHISI lakini sijasema HAIWEZEKANI.
Kudhani kuwa CCM itaondoka kwa kutumia wanasiasa walewale ambao wamechangia kuwafanya Watanzania wengi watake chama hicho kiondoke madarakani ni sawa na kutwanga maji kwenye kinu.
Naam, Lowassa anaweza kuwezesha Chadema/UKAWA kuitoa CCM madarakani lakini sababu zilizofanya CCM ichukiwe haziwezi kuondoka.
Kwahiyo faida kubwa iliyonayo CCM ni mfumo wa uchaguzi na kiutawala ambao unakitengenezea mazuri chama chake na yeye binafsi kufanya vizuri katika uchaguzi huo.
Lakini licha ya faida hizo za kimfumo, Magufuli anaingia katika uchaguzi huo akiwa katika CCM ileile iliyoshinda chaguzi zote zilizotangulia, kihalali au la, lakini safari hii inakutana na upinzani ambao Kimsingi umetengenezwa katika mazingira ya ‘zimamoto’.

Jinsi UKAWA ilivyoundwa na maendeleo yake hadi kufikia hatua ya kusimamisha mgombea mmoja, yaweza kuwa ni moja ya vikwazo kwa umoja huo kufanikiwa kwenye uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika takriban miezi mawili na kitu kutoka sasa.
Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Lakini umoja tunaozungumzia hapa ni ule wenye kujengwa katika misingi ya kuaminiana. Tayari Tumeshuhudia Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbrod Slaa, akijiweka kando na aliyekuwa Mwenyekiti wa CUF, Prof Ibrahim Lipumba akijiuzulu.
Ni rahisi kutoa majibu rahisi, kwa mfano kuwatuhumu wanasiasa hao ni wenye uchu wa madaraka, lakini ukweli ni kwamba ‘kujitenga’ kwao sio tu kuna athari bali pia kunaashiria mpasuko wa aina fulani katika umoja huo.
Kwahiyo Magufuli na CCM kwa ujumla wataingia katika uchaguzi huo wakiwa kitu kimoja, kwa kiasi kikubwa, ilhali UKAWA wakikabiliwa na ‘sintofahamu’ flani, sio tu ya kuhusu Dkt Slaa na Prof Lipumba, bali pia hizi taarifa zinazosikika kutoka katika baadhi ya majimbo ambapo ‘ndoa’ ya vyama hivyo imeshindikana, yaani licha ya kuafikiana kusimamisha mgombea mmoja, vyama vinavyounda umoja huo vimejikuta vikisimamisha wagombea tofauti.
Jingine limejitokeza katika uzinduzi wa kampeni za CCM Jumapili iliyopita ambapo chama hicho tawala, kama baadhi yetu tulivyotarajia, kimejaribu kujenga picha kuwa Chadema/UKAWA sasa ni kama kikosi cha pili cha CCM (CCM-B).

Magufuli na timu yake wakiweza kujenga hoja za kueleweka kwanini Lowassa na Chadema/UKAWA yake ni sawa tu na CCM ya waasi, kuna uwezekano wa wapigakura kutafuta hifadhi katika ‘jini linalokujua halikuli likakwisha.’CCM ‘halisi’ ni ‘jini’ wanalolijua, na pengine wasingetaka kufanya majaribio kwa ‘jini’ wasilolijua.
Kana kwamba hiyo haitoshi, Magufuli na CCM kwa ujumla wanaweza kurahisishiwa kazi na ‘historia ya mahusiano kati ya Chadema na Lowassa. Kama kuna mwanasiasa wa CCM aliyeandamwa mno na Chadema kuhusu tuhuma za ufisadi basi si mwingine bali Lowassa.
Kwa kuzingatia muda uliopo, kati ya mwanasiasa huyo kuhama CCM na kujiunga na Chadema na tarehe ya uchaguzi mkuu, yayumkinika kuhitimisha kuwa ni vigumu mno kumsafisha.

Kimsingi, Chadema/UKAWA wamejiambukiza tatizo walilokuwa wakilipiga vita kwa nguvu zao zote. Hakuna ubishi kuwa mafanikio ya chama hicho kikuu cha upinzani yalichangiwa zaidi na msimamo wake mkali dhidi ya ufisadi.
Sasa leo hii wakisimama jukwaani sio tu na mwanasiasa anayetuhumiwa kujihusisha na ufisadi lakini pia Chadema wenyewe walimwandama kwa tuhuma hizo, kisha wajaribu kumsafisha au kukemea ufisadi, ni mkakati wenye dalili ya kutokuwa na mafanikio.
Awali kulikuwa na hisia za ‘mafuriko ya Lowassa’ kuikumba CCM, kwa maana ya wanasiasa wenye nguvu ndani ya chama hicho tawala kumfuata huko Chadema/UKAWA.
Kuna wawili watatu waliohama lakini si wenye ushawishi au nguvu kubwa ya kuiathiri CCM. Na tayari CCM, imewashusha hadhi na kuwaita ‘makapi’ sambamba na kujenga picha kuwa ni wenye uchu wa madaraka.
Kuhama kwa Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye, kutoka CCM na kujiunga na UKAWA kunazidi ‘kuchanganya madawa.’ Kubwa zaidi ni kile kilichoonekana kuwa uhasama wa muda mrefu kati ya wanasiasa hao.
Wakati hii ingeweza kuwa turufu kubwa kwa UKAWA, kuwa na mawaziri wakuu wa zamani wawili ndani ya upinzani, lakini tayari zimeanza kusikika tetesi kuwa “Sumaye ameingia UKAWA kama ‘Plan B’ endapo lolote litamtokea Lowassa kiafya.”
Lakini makala hii si ya kuzungumzia mapungufu ya Chadema/UKAWA bali ni kumjadili Magufuli, japo ni vigumu kuzungumzia fursa alizonazo za kuibuka mshindi kwenye uchaguzi mkuu pasipo kujadili ‘urahisi’ unaotokana na kinachoendelea huko UKAWA.
Tukiweka pembeni niliyobainisha hapo juu, matumaini kuwa urais wa Magufuli utakuwa tofauti na huu wa Rais Jakaya Kikwete ni mdogo.
Hilo nilishaliongelea huko nyuma, ambapo yayumkinika kudhani kuwa mgombea huyo wa chama tawala anaweza kuwa na deni la fadhila kwa mtangulizi wake, hasa kwa kuzingatia ‘mahesabu’ yaliyofanyika katika machakato wa CCM kumpata mgombea wake.
Laiti Chadema/UKAWA wasingekuwa na kibarua cha kumsafisha mgombea wao, Lowassa, wangeweza kuwa katika nafasi nzuri kujenga picha kwa wapigakura kuwa miaka mitano ya utawala wa Magufuli haitokuwa tofauti na kumi ya Kikwete, na pengine kupigilia mstari kuwa mengi ya yaliyojiri katika utawala uliopo madarakani yanamhusu mgombea huyo wa CCM pia.
Hata hivyo, iwapo jitihada za kumsafisha Lowassa na kumtenganisha na CCM zitafanikiwa, basi UKAWA na mgombea wao wanaweza kufanya vizuri.
Mwisho, kama kuna kitu kinachoweza kuigharimu CCM na Magufuli ni kupuuzia ukweli kuwa kuna wapigakura wengi wamepoteza imani kwa chama hicho.
Na laiti mwenendo wa kampeni za Magufuli utafuata ‘busara’ za Rais mstaafu Benjamin Mkapa kutumia lugha isiyo ya kistaarabu ya ‘mpumbavu na lofa’ basi sintoshangaa kuona Lowassa akinufaika na ‘kura za huruma’.

Ni muhimu kwa CCM kuongoza kwa mfano ikiwa ni pamoja na kuachana na kampeni za chuki au za ‘utoto wa kisiasa’ (political immaturity), iwaeleze Watanzania wapi ilipokosea hadi baadhi yao kutamani iondoke madarakani, na nini itawafanyia kurekebisha makosa yake.

20 Aug 2015

KAMA nilivyoahidi katika makala iliyopita, wiki hii ninaendelea na uchambuzi wangu kuhusu Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Na kama ilivyokuwa katika makala kadhaa zilizotangulia, uchambuzi wangu utaelemea kwenye kinyang’anyiro cha nafasi ya urais.
Wakati katika makala iliyopita nilijadili fursa na vikwazo kwa wagombea ‘wakuu’ wawili, yaani Dk. John Magufuli wa CCM na Edward Lowassa wa Chadema/UKAWA, wiki hii nitaingia kwa undani zaidi, huku lengo likiwa kuitumia makala hii kufanya uchambuzi kwa mgombea mmoja, na makala ya wiki ijayo itamwangalia mgombea mwingine.
Nianze na Lowassa wa Chadema/UKAWA. Kati ya makala iliyopita na hii, si siri kuwa habari inayotawala zaidi ni kile kinachoitwa ‘mafuriko ya Lowassa’. Shughuli zote zilizomhusisha mwanasiasa huyo katika kipindi hicho kimeandamana na umati mkubwa mno wa watu, kuanzia alipochukua fomu za kuwania urais jijini Dar es Salaam hadi katika mikutano ya kutambulishwa huko Mbeya, Arusha na Mwanza.
Wingi wa watu wanaojitokeza katika shughuli zinazomhusu Lowassa, iwe ni kwa kuandamana au kuhudhuria mikutano, kumewapa matumaini makubwa wafuasi wake kwamba njia ya Waziri Mkuu huyo wa zamani kuelekea Ikulu ni nyeupe.
Sambamba na mahudhurio hayo makubwa, wanachama kadhaa wa CCM wamehama chama hicho tawala na kujiunga na Chadema. Lakini kubwa zaidi ni kuhama kwa baadhi ya viongozi ‘ waliokuwa na majina’ ndani ya CCM.
Kwamba maandamano na mikutano ya Lowaasa inajaza watu wengi mno, hilo halina mjadala. Kwamba matukio yajayo ya mwanasiasa huyo yataendelea kujaza watu pia si suala la mjadala. Kadhalika, kwamba kuna wanachama na viongozi zaidi wa CCM watamfuata Lowassa huko Chadema pia ni jambo la kutarajiwa.
Tusichoweza kuhitimisha kwa uhakika muda huu ni iwapo hamahama hiyo ya baadhi ya wana-CCM na viongozi wao kumfuata Lowaasa huko Chadema itaweza kutafsiriwa katika ushindi katika uchaguzi mkuu ujao hapo Oktoba 25, takribani miezi mawili kutoka sasa.
Licha ya uwepo wa hamasa kubwa kuhusu kujiandikisha katika daftari za wapigakura lililoboreshwa na teknolojia ya kuhifadhi rekodi kwenye kompyuta (Biometric Voter Register kwa kifupi BVR), hadi muda huu Tume ya Taifa ya Uchaguzi haijatoa idadi kamili ya watu waliojiandikisha.

Lakini licha ya hilo, tayari kuna dalili za kasoro katika suala la BVR ambapo zimepatikana taarifa kadhaa za waliojiandikisha kutoyaona majina yao wakati wanaofanya uhakika. Ukubwa au udogo wa kasoro hiyo bado haujafahamika kwa vile Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) haijalitolea ufafanuzi suala hilo.
Hapa nitaunganisha masuala hayo mawili ya hapo juu, yaani idadi kubwa ya watu wanaojitokeza katika shughuli za Lowassa na zoezi la kujiandikisha BVR.
Yayumkinika kuhitimisha kuwa ili wingi wa watu wanaojitokeza katika shughuli za mwanasiasa huyo ziwe na manufaa kwake na chama chake kwa ujumla, basi, kwanza wengi wa watu hao, kama si wote, lazima wawe wamejiandikisha kupiga kura. Bila hivyo wingi wao utabaki kuwa historia tu.
Lakini kwa uzoefu tulionao wengi, kujiandikisha kupiga kura ni suala moja, kufanikiwa kupiga kura ni suala jingine, na kumpigia kura mgombea fulani na kura hiyo kumsaidia ashinde ni suala jingine kabisa.
Nimeshazungumzia katika makala zangu zilizotangulia kuwa moja ya faida kubwa kwa CCM ni mahusiano ya upendeleo kati yake na taasisi mbalimbali za umma. Na ninatarajia wengi wenu ndugu wasomaji mmekuwa mkisikia vilio vya wanasiasa wa upinzani takribani tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi kwamba wanaohisi kura zao zinahujumiwa na chama tawala kwa kusaidiwa na taasisi za umma ‘zinazokipendelea’ chama hicho.
Japo mara zote tuhuma hizo zimeendelea kubaki kuwa tuhuma tu, ushahidi wa kimazingira unaelekea kuzisapoti tuhuma hizo.
Binafsi, nimekuwa nikifuatilia pilika za uchaguzi mkuu kupitia mtandaoni, hususani kwenye mitandao ya kijamii (social media). Majuzi, niliwatahadharisha mashabiki wa Lowassa kuhusu furaha yao inayotokana na wingi wa wahudhuriaji katika shughuli za hadhara zinazomhusu mwanasiasa huyo.
Niliwakumbusha kuhusu chaguzi zilizopita, hususan ‘kasi ya (Agustino Lyatonga) Mrema,’ aliyekuwa mgombea urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 1995 kupitia chama cha NCCR-Mageuzi, jinsi alivyokuwa maarufu na kujaza halaiki ya watu kwenye mikutano yake, lakini akaishia kubwagwa na mgombea wa CCM, Benjamin Mkapa.
Niliwakumbusha pia kuhusu wingi wa watu waliojitokeza katika mikutano ya kampeni za Dk. Willibrord Slaa, aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema katika uchaguzi mkuu uliopita, mwaka 2010, lakini akishindwa na mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete.
Katika chaguzi zote hizo, pamoja na ule wa mwaka 2000 na 2005, kulikuwa na malalamiko kdhaa kuwa ‘CCM iliiba kura,’ lakini tuhuma hizo zilijifia zenyewe kutokana na kutokuwepo ushahidi halisi, sambamba na vikwazo vya kikatiba kupinga matokeo ya Urais.

Lakini kukumbushia yaliyojiri katika chaguzi hizo kulipelekea mimi kushambuliwa vikali, nikituhumiwa kuwa na ‘chuki binafsi’ dhidi ya Lowassa, huku wengine wakinituhumu kuwa nimenunuliwa na CCM. Na nikakumbushwa kuwa “nenda na wakati, hii ni 2015, achana na habari za 1995”.
Siwezi kuwalaumu watu ambao hawataki kusikikia lolote ‘baya’ kuhusu Lowassa, au jambo linaloweza kuwa kikwazo kwake kupata urais.
Kwa bahati mbaya, ujio wa mwanasiasa huyo huko Chadema unaoonekana kuwabadili wana-Chadema wengi, angalau huko mtandaoni, ambapo watu waliokuwa wakijadili hoja kiungwana, sasa wamekuwa mahiri wa matusi kwa kila anayeelekea kumpinga Lowassa.
Nitawalaumu kwa matumizi ya matusi badala ya kujenga hoja za kistaarabu, lakini sintowalaumu kwa kuwa ‘desperate.’ Wanasema mtu akielemewa na mafuriko basi atang’ang’ania hata unyasi ili ajiokoe.

CCM imewafikisha Watanzania wengi katikia hali hii tunavyoshuhudia. Sapoti kubwa kwa Lowassa sio kwa vile ni mchapakazi au anatarajiwa kuleta ‘miujiza’ bali ni kukata tamaa miongoni mwa Watanzania wengi, Tunasikia watu wakisema “ukiiweka CCM na jini, nitapiga kura yangu kwa jini”.
Lakini wakati kuwa na matumaini yanayotokana na kukata tamaa si tatizo sana, ni muhimu kuzingatia hali halisi. Kuna wanaodai ‘safari hii CCM haiwezi kutuibia kura’ Je kuna tofauti gani ya kimazingira ya uchaguzi katika ya mwaka huu na uchaguzi mkuu wa mwaka 1995,2000,2005 na 2010? Tume ya uchaguzi ni ileile, taasisi mbalimbali za umma zinazoshughulikia uchaguzi huo bado zipo vilevile, na vyombo vyetu vya dola bado vina ‘mentality’ ileile ya kuwaona Wapinzani kama wahaini, na hata Lowassa amekiri kuwa alipokuwa CCM alidhani vyombo vya dola vyalaumiwa bure tu na Wapinzani…hadi alipoonjeshwa ‘jeuri ya polisi’ hivi majuzi.
Lakini tukiweka kando kuhusu tatizo hilo ambalo niliona kama la kimfumo, yaani mfumo unaoipendelea CCM, kuna tatizo jingine ambalo pengine halijawa kubwa sana. Hili ni uwezo mdogo wa Lowassa katika kujieleza.
Unapofanikiwa kukusanya umati wa maelfu ya watu, kisha ukahutubia kwa dakika tano, na katika muda huo mfupi usiseme lolote la maana la kuwafanya waliohudhuria wakumbuke si ukubwa wa umati bali uzito wa hotuba ya aliyewajaza kwa wingi mahala husika, basi hapo kuna tatizo.
Na tatizo hili laweza kuwa turufu kwa mgombea wa CCM, Dk. Magufuli, ambaye anasifika kwa umahiri si tu wa kuongea bali kutoa takwimu nyingi kichwani kana kwamba ni mashine yenye kumbukumbu (memory) kubwa.
Ukizungumzia hilo kwa wana-Chadema/UKAWA, wanasema “nani anataka hotuba? Sisi tunachotaka ni kuondoa CCM tu”. Ninabaki ninajiuliza, “hivi wakifanikiwa ukiondoa CCM, nini kitafuata?” Sipati jibu.
Kwa kifupi, kinachowapa matumaini wana-Chadema/UKAWA na mashabiki wa Lowassa ni hayo ‘mafuriko.’ Iwapo yataweza kujitafsiri katika kura, muda utatupatia jibu (time will tell).
Na iwapo ‘mafuriko’ hayo yatamwezesha Lowassa kuingiza Ikulu, ninadhani hata wana-Chadema/UKAWA wengi hawajui jinsi gani atakavyowezesha kubadili kile kinachowafanya Watanzania wengi wachukizwe kuhusu CCM.

Kwa upande mmoja, kuahidi mabadiliko ni kitu kimoja, kutekeleza ahadi hiyo ni kitu kingine. Kwa upande mwingine, kuwa na nia ya kuleta mabadiliko ni kitu kimoja, uwezo wa kufanikisha nia hiyo ni kitu kingine, na hata pale nafasi ya kuleta mabadiliko inapopatikana, nyenzo na mazingira vyaweza kuwa kikwazo cha kutimiza azma hiyo.
Nihitimishe makala hii kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi huu katika toleo lijalo ambapo nitamzungumzia mgombea wa CCM, Dk. Magufuli kama nilivyomjadili Lowassa katika makala hii.

30 Jul 2015


Kama unavyoona hapo pichani juu, mara baada ya kusikia taarifa kwamba Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa anatarajia kujiunga na vyama vinavyounda Muunganowa Katiba ya Wananchi (UKAWA), niliandika tweet hiyo pichani. Kimsingi, binafsi nilishindwa kabisa kuamini kuwa Dkt Willibrord Slaa, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema hadi alipotangaza kujiuzulu, angeweza kukaa chama kimoja na Lowassa. Nilishindwa kabisa kupata picha kichwani kumwona Dkt Slaa akiwa jukwaani anamnadi Lowassa. Nilijaribu ku-imagine kwamba labda kwa vile kuingia kwa Lowassa Chadema kunaweza kukiingiza chama hicho na Ukawa Ikulu, na hivy pengine Dkt Slaa angeweza kumsapoti japo kwa shingo upande, lakini nafsini niliona huo sio tu ungekuwa muujiza - na mie si muumini wa miujiza - bali pia ungekuwa usaliti wa hali ya juu.


Siwezi kujisifu kuwa tweet hiyo ya 'kumsuta' Dkt Slaa imesaidia kumfanya achukue uamuzi huo wa kujiuzulu lakini ninachoweza kusema ni kuwa ninamshukuru kwa kufanya maamuzi magumu ya kujiuzulu hasa ikizingatiwa kuwa neno 'KUJIUZULU' halipo katika kamusi ya wengi wa wanasiasa wetu hata pale wakiwa wanaandamwa na kashfa. Lakini pia ninampongeza Dokta Slaa kwa kusimamia anachooamini.

Kwa hakika Dokta Slaa alisimama kidete kupigana kwa nguvu zake zote dhidi ya ufisadi. Na sifa kubwa ya mwanasiasa huyo ilikuwa umakini wake katika kuwasilisha hoja. Hakuwa mtu wa jazba wala mjivuni. Na kwa hakika alikuwa mwenye kuapanga hoja zake na kuziwasilisha kwa umakini mkubwa. Kwa kifupi, Dokta Slaa aliweza kuwasiliana na umma, iwe katika hotuba au maongezi kama DOKTA hasa, maana moja ya sifa ya usomi ni jinsi ya kuwasiliana na jamii kwa ufasaha.

Kuna watakaokuwa wamefurahi kuona Dokta Slaa amechukua hatua ya kujiuzulu, sio furaha ya kuungana naye kwa kuchukua uamuzi huo mgumu bali kwa vile aidha walikerwa na msimamo wake mkali dhidi ya mafisadi na ufisadi, au walimwona kama mmoja ya sababu zilizopokea Zitto Kabwe kung'olewa Chadema. Furaha hiyo ni ya 'kimburula' kwa sababu Dokta Slaa alikuwa mmoja wa wanasiasa wachache kabisa waliosimama kwa dhati na wanyonge kupigania haki zao. Ukimwondoa marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, sioni mwanasiasa mwingine yeyeote yule aliyewajali mno Watanzania kama Dokta Slaa. Na japo nina furaha kutokana na kukataa kushirikiana na Lowassa, na ninampongeza kwa kuwa na msimamo thabiti, kwa upande mwingine nina masikitiko makubwa kuona lulu hiyo ya taifa ikiachana na siasa wakati bado twaihitaji mno.
Dokta Slaa alifanya kazi yake kwa uadilifu mkubwa na kwa hakika kuna idadi kubwa tu ya Watanzania iliyoamini kuwa siku moja angeweza sio tu kuwa Rais wetu bali pia angeweza kuibadili Tanzania yetu. Na kwa kujiuzulu, amethibitisha ni mwasiasa wa aina gani. Badala ya kutanguliza maslahi binafsi na kujiunga na chama kingine cha siasa au kuanzisha chama chake, Dokta Slaa amechukua uamuzi wa kiungwana. Ametambua kuwa tatizo sio CCM pekee bali mfumo mzima wa siasa za Tanzania yetu, kuanzia chama tawala hadi huko Upinzani. Uamuzi wa kujiuzulu utamlindia hadhi yake milele. 

Mimi ni muumini mkubwa wa 48 Laws of Power, na ninaomba nitanabaishe jinsi uamuzi huo wa Dokta Slaa unavyoendana na baadhi ya Laws hizo. Law 34 of Power inasema (ninainukuu)

The way you carry yourself will often determine how you are treated: In the long run, appearing vulgar or common will make people disrespect you. For a king respects himself and inspires the same sentiment in others. By acting regally and confident of your powers, you make yourself seem destined to wear a crown.
Kwa tafsiri ya Kiswahili ni kwamba "Matendo yako ndio yatakavyofanya watu wakuchukuliaje. Katika muda mrefu, kuonekana mtu wa ovyo ovyo kutafanya watu wasikuheshimu. Kwa sababu mfalme hujiheshimu mwenyewe na kuhamasisha watu wengine kujiheshimu na kumheshimu. Kwa matendo makubwa na ya uhakika wa nguvu zako, utaonekana mtu stahili kushika hatamu." 
Na kwa hakika uamuzi wa Dokta Slaa kujiuzulu unamfanya aendelee kuwa sio tu mtu mwenye msimamo bali pia ataendelea kushikilia hadhi na heshima yake kama mtu aliyeuchukia ufisadi kwa dhati hadi kuamua kujiuzulu baada ya fisadi Lowassa kujiunga na UKAWA.
Kuna wanaoweza kumbeza kwa kusema amekimbia vita. Well, Law 36 of Power inatuasa, nanukuu,

...It is sometimes best to leave things alone. If there is something you want but cannot have, show contempt for it...
Kwa tafsiri ya Kiswahili, "Wakati mwingine ni vema kuacha vitu kama vilivyo Kama kuna kitu unakitaka lakini huwezi kukipata, kichukie tu." Na hicho ndicho alichokifanya Dokta Slaa. Alichukia ufisadi na kuwachukia mafisadi kwa dhati. Lakini ghafla akajikuta analetewa fisadi ashirikiane nae kupinga ufisadi. Waingereza wana msemo "You can't put a drug addict in charge of a pharmacy," yaani huwezi kulikabidhi teja liwe msimamizi wa duka la madawa (ambayo kwa kawaida yana madawa baadhi ya madawa kama Heroin ambayo ndio 'chakula' cha mateja). Kwa vyovyote vile, ingekuwa vigumu mno kwa Dokta Slaa kutimiza azma yake ya kupambana na ufisadi akiwa pamoja na Lowassa. Na ndio maana akaamua bora akae kando. Kama ninavyotamka mara kadhaa, huhitaji kuwa kiongozi ili ulete mabadiliko, kuwa raia mwema tu (You don't have to be a leader to bring change. Just be a good citizen).

Law 47 of Power inasema, ninanukuu,

The moment of victory is often the moment of greatest peril. In the heat of victory, arrogance and overconfidence can push you past the goal you had aimed for, and by going too far, you make more enemies than you defeat. Do not allow success to go to your head. There is no substitute for strategy and careful planning. Set a goal, and when you reach it, stop.

Kwa Kiswahili inamaanisha, "Ushindi unapowadia ndio wakati ambao unaweza kuangamia. Katikati ya ushindi, dharau na kujiamini kupita kiasi vyaweza kukusukuma zaidi ya lengo kusudiwa, na kwa kupitiliza lengo hilo, watengeneza maadui zaidi ya uliowashinda. Kamwe usiruhusu mafanikio kupanda kichwani mwako. Hakuna mbadala wa mkakati na mipango makini. Weka lengo, na ukilitimiza, simama."
Hakuna asiyefahamu alichotimiza Dokta Slaa katika mapambano yake dhidi ya ufisadi. Kubwa lilikuwa kuwaamsha Watanzania, na kwa hakika wengi wamefunguka macho dhidi ya ufisadi na wanauchukia kwa dhati. Angeweza kujikaza kisabuni na kusimama pamoja na Lowassa ili aendeleze mapambano dhidi ya ufisadi, lakini sote twafahamu ingekuwa vigumu mno. Na uamuzi wake wa kujiondoa madarakani ni sawa na inavyosema sheria hiyo hapo juu, 'ukitimiza leno, simama.'
Vilevile, Dokta Slaa amefuata vizuri Law 5 of Power inayoonya kuwa "So much dependes on reputation, guard it with your life," yaani "Hadhi ni kitu muhimu sana, ilinde kwa nguvu zote." Sasa, sote tulikuwa tukiitambua Chadema kama kiongozi wa vita dhidi ya ufisadi, lakini ghafla wametusaliti na kumkaribisha papa wa ufisadi katika chama chao. Kwa vile ni mtu makini na msafi, Dokta Slaa ameona kuwa kwa kufanya hivyo, Chadema imejishushia hadhi yake katika uongozi wa mapambano dhidi ya ufisadi, na akaamua kuilinda hadhi yake kwa kujitenga nao. 
Nimalizie makala hii kwa kurudia kumshukuru Dokta Slaa kwa yote aliyoitendea Tanzania yetu. Tunaouchukia ufisadi tutaendelea kumwenzi na kumkumbuka milele. Nitajitahidi huko mbeleni kufanya mawasiliano na Dokta Slaa ili ikiwezekana niweke kumbukumbu ya huduma yake bora kabisa kwa Watanzania kwa kuandika kitabu kinachomhusu. Nitawa-update kuhusu hilo.
MUNGU AKUBARIKI SANA DOKTA SLAA. TANZANIA ISIYO NA UFISADI INAWEZEKANA PASIPO HAJA YA KUWATEGEMEA MAFISADI. 



Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.