18 Mar 2019


 
Leo Machi 18, 2019 ni siku ambayo lazima iingie kwenye vitabu vya kumbukumbu kwa sababu kuu tatu, ambazo zote zinamhusu mwanasiasa mkongwe Seif Sharif Hamad na Chama cha Wananchi (CUF)

Sababu ya kwanza, leo ni siku ambayo mwanasiasa huyo, maarufu kwa jina la Maalim Seif, "ametimuliwa" rasmi kutoka chama alichoshiriki kukiasisi (CUF).
Kibaya zaidi, "kutimuliwa" huko kumekuwa na baraka kisheria, baada ya Mahakama Kuu kumtambua Profesa Ibrahim Lipumba kuwa mwenyekiti halali wa chama hicho.

Ikumbukwe tu Lipumba alitangaza kujiuzulu uenyekiti kwa sababu anazozijua yeye kabla ya kuamua kurejea kwenye wadhifa huo "kwa mabavu." Kwa bahati mbaya – au pengine makusudi – sheria na kanuni za CUF zilikuwa zinatoa mwanya kwa Lipumba (au mwanasiasa mwingine yeyote yule) kufanya "uhuni" kama huo.

Sababu ya pili, ni kwamba leo CUF imekabidhiwa rasmi kwa Lipumba. Kisheria. Mahakama imetenda haki kwake kwa sababu japo alichofanya ni uhuni, kisheria uhuni huo ulihalalishwa na CUF yenyewe.

Hili la Lipumba kukabidhiwa chama si jambo dogo. Kuna mawili hapa. Moja, hii inaweza kuwa fursa nzuri kwa Lipumba kukijenga chama hicho na hatimaye kukirejesha kwenye nafasi ya kuaminika kama "mbadala wa CCM."

Lakini la pili, na hili ndilo ninahisi litatokea, ni mwanzo wa mwisho wa CUF. Sio siri kuwa Lipumba amesaidiwa sana na CCM kuipora CUF kutoka mikononi mwa Maalim Seif. CCM hawajafanya hayo kwa vile wanampenda Lipumba.Hapana. Wanamtumia tu kumdhibiti Maalim Seif ambaye licha ya kila hujuma zilizokuwa zikifanywa na CCM na taasisi zake, ameendelea kuwa mwanasiasa maarufu zaidi kuliko wote katika siasa za Zanzibar.

Sasa, baada ya Lipumba kutumika "kummaliza Seif ndani ya CUF," kuna uwezekano wa aina mbili tu. Wa kwanza ni kwa mwanasiasa huyo msomi kukubali kuendelea kutumika kama kibaraka wa CCM huku CUF ikigeuka kuwa CCM-B, na wa pili, ni kujaribu kusimama kama chama halisi cha upinzani na hapohapo "kumwagiwa radhi na CCM" na hatimaye kupelekea kifo cha chama hicho.

Uwezekano mkubwa zaidi ni huo wa kwanza - ukibaraka. Kwamba CUF haitokufa. CUF itaendelea kushiriki chaguzi mbalimbali. CUF itajenga taswira ya chama kamili cha upinzani. Lakini uwepo huo wa CUF hautokuwa kwa manufaa ya chama hicho au siasa za upinzani bali kwa manufaa ya CCM.

Kuna kila dalili kuwa CCM itaisaidia CUF kujitanua nchi nzima kwa sababu moja kuu: uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 utakuwa mbovu kuliko chaguzi zote zilizowahi kutokea Tanzania. Kuna uwezekano mkubwa tu kwa baadhi ya vyama vikuu vya upinzani kutishia kususia uchaguzi huo. Na hapo ndipo CUF ya Lipumba itakapotumika kuhalalisha "ushindi wa Magufuli/CCM."

CCM itaisaidia CUF kuweza kusimamisha wagombea takriban kila jimbo kwa upande wa Tanzania Bara. Lakini pia CCM itaisaidia CUF kuendelea kuwa chama imara cha upinzani huko Zanzibar, ambako uimara wake utasaidia kugawa kura dhidi ya CCM na wagombea wake.

Hata hivyo, "laana ya kutumika" itaikumba CUF baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 na kama isipoishia kusambaratika basi itabaki "chama jina" kama TLP ya Mrema.

Kuhusu uamuzi wa Maalim Seif kuhamia ACT- Wazalendo, japo hatua hiyo inaweza kuwashangaza baadhi ya watu, ukweli mchungu baada ya Mahakama Kuu kuhalalisha "uhuni" wa Lipumba, sambamba na "uhuni" wake mwingine majuzi ambapo "alijitangaza" kuwa Mwenyekiti kupitia "uchaguzi mkuu hewa" ambao pia "ulimtimua Maalim Seif" kwa kuteua mtu mwingine kushika wadhifa wa Katibu Mkuu.

Kwa kuzingatia muda mfupi uliosalia kabbla ya uchaguzi mkuu wa mwakani, Maalim Seif kuendelea kutafuta haki yake mahakamani kungeweza kumkuta akiwa bado kwenye korido za mahakama wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu ujao. Ni vigumu mno kwa chama cha siasa kushiriki kikamilifu kwenye uchaguzi mkuu huku kikiwa kinakabiliwa na mpasuko katika uongozi wake wa juu.

Kwahiyo, kimkakati, uamuzi huo wa Maalim Seif unaeleweka, na unaweza kuwa ni mbinu muhimu kwake kuendelea kuwa relevant kisiasa.

Hata hivyo, kuna uwezekano wa aina mbili kuhusu mustakabali wa Maalim Seif na wa chama chake kipya cha ACT- Wazalendo.

Uwezekano wa kwanza ni kwa chama hicho kuibuka kuwa tishio katika siasa za Tanzania. ACT – Wazalendo ni chama kizuri lakini ambacho hakikui. Kimeendelea kuwa "chama cha mtu mmoja" chini ya uongozi wa Zitto Kabwe. Kwa muda mwingine, chama hicho kimekuwa cha kiharakati zaidi kuliko cha kisiasa.

Mapungufu hayo yanaweza kubadilika kwa njia kuu tatu. Kwanza, Maalim Seif hajawahi kupata fursa nzuri ya kunadi mvuto wake kwenye majukwaa ya siasa za Tanzania Bara. ACT-Wazalendo wanaweza kuwa Jukwaa muhimu katika hilo.

Pili, Zitto  hajawahi kupata jukwaa mwafaka kunadi mvuto wake wa kisiasa huko Zanzibar. Kwa kuungana na Maalim Seif, hii inaweza kuwa ndio fursa mwafaka kwake.

Tatu, ACT-Wazalendo kama chama inaweza kupata fursa mwafaja kabisa ya kuwa chama cha kitaifa badala ya kuwa "chama cha Kigoma."

Haya yote yatawezekana tu endapo kutakuwa na "kujitoa mhanga" kati ya mwenyeji Zitto na mgeni Maalim Seif. Kwa mara ya kwanza, Zitto atajikuta akiongoza chama ambacho ndani yake kuna mwanasiasa maarufu zaidi yake. Naam, Maalim Seif ni mkongwe zaidi kisiasa kuliko Zitto. Endapo Zitto "atajitoa mhanga" (make a sacrifice) na kukubali "kumezwa" na umaarufu wa Maalim Seif, basi chama hicho kitakuwa na fursa kubwa ya kupanuka zaidi na hata kuja kuwa chama kikuu cha upinzani katika pande zote za Muungano.

Lakini endapo kutakuwa na mgongano wa ego kati ya wanasiasa hao, basi mustakabali wa chama hicho utakuwa mashakani. Lakini pengine uwezekano wa hili kutokea ni mdogo kutokana na ukweli kwamba suala la Maalim Seif kujiunga na ACT-Wazalendo sio limetokea tu ghafla. Ni dhahiri kuwa kulikuwa na majadiliano ya muda mrefu na yayumkinika kuhisi kwamba tofauti kati ya wanasiasa hao wawili (Maalim Seif na Zitto) zilifanyiwa kazi wakati wa majadiliano hayo.

Suala jingine ambalo linaweza kuijenga ACT-Wazalendo "mpya" (ya Zitto na Maalim Seif) au kuibomoa ni mtihani ulioikumba Chadema mwaka 2015.

Kwa mwelekeo ulivyo ndani ya CCM ambapo Magufuli hafanyi siri kuwa anataka chama hicho kiwe chini ya uongozi wa watu wake (wengi wao wakiwa wana-Kanda ya Ziwa wenzake), kuna uwezekano mkubwa wa kuibuka wimbi kubwa tu la wanasiasa wenye majina watakaotaka kuhamia Upinzani. Na endapo Zitto na Maalim Seif watakuwa "dream team" ya kuaminika, basi ACT-Wazalendo inaweza kuwa na mvuto zaidi kwa "wakimbizi kutoka CCM" kuliko Chadema.

Si ajabu kwa wanasiasa kama Nape Nnauye, Mwigulu Nchemba, Bernard Membe kujiunga na ACT-Wazalendo endapo chama hicho kitaonekana kuwa kinaweza kutoa ushindani wa dhati dhidi ya CCM hapo mwakani.

Sasa, wakati kupokea "majina makubwa" kutoka CCM husaidia kuongeaza umaarufu wa chama, uzoefu umeonyesha kuwa wengi wao wenye majina hayo makubwa ni wanafiki wanaokwenda upinzani kwa sababu zao binafsi na sio kwa maslahi ya vyama husika vya upinzani.
Kibaya zaidi, kila ujio wa "wahamiaji" hao ni fursa mwafaka kwa CCM kupandikiza "mamluki" wake kama ilivyotokea kwa Chadema ilipompokea Lowassa mwaka 2015.

Je ACT-Wazalendo "mpya" inaweza kutoa upinzani wa dhati dhidi ya CCM hapo mwakani? Jibu fupi ni "muda ndio utaongea" (time will tell). Jibu pana zaidi ni kwamba japo uwezekano huo upo lakini sidhani kama muda unatosha kukitanua chama hicho nchi nzima hususan katika kipindi hiki ambacho chama pekee cha siasa kinachoruhusiwa kufanya shughuli za siasa ni CCM tu.

Hata hivyo, endapo mkazo wa ACT-Wazalendo utakuwa katika sio tu kuongeza idadi ya wanachama bali kujenga kuaminika kwa "Watanzania wasio na vyama," basi huenda chama hicho kikafanya vizuri kwenye uchaguzi mkuu huo.

Ni hivi, kundi muhimu kabisa la wapigakura katika uchaguzi mkuu wowote ule nchini Tanzania ni "Watanzania wasio na vyama." Kwamba, hakuna chama cha upinzani kinachohitaji kupoteza muda wake kuwashawishi wafuasi wa CCM wakipigia kura, kama ambavyo CCM haina muda na wafuasi wa upinzani kuwashawishi waipigie kura. Vilevile, si CCM wala vyama vya upinzani vinavyohitaji kuwashawishi wanachama/wafuasi wao wapigie kura vyama vyao. Watu wanaohitaji kushawishiwa ni hao wasio na vyama. Na habari njema ni kwamba kundi hilo ndilo lwenye idadi kubwa zaidi ya wapiga kura.

Kwa mujibu wa takwimu zisizo rasmi, CCM ina takriban wanachama milioni 8 ilhali wapinzani wana wanachama takriban milioni 5. Kwa makadirio, takriban Watanzania milioni 25 walijiandikisha kupiga kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015. Kwahiyo, milioni 8 wa CCM jumlisha milioni 5 wa upinzani jumla inakuwa milioni 13. Ukichukua milioni 25 kutoa miloni 13 unabakiwa na milioni 12. Kwa makadirio, hawa ni "wapigakura wasio na vyama." Na kimahesabu, hata nusu tu ya kundi hili likielemea upande mmoja, upande huo unaweza kabisa kushinda uchaguzi husika. Of course, hapo tunaweka kando hujuma za kawaida za kuibeba CCM kwenye takriban kila uchaguzi mkuu.

Nimalizie kwa kukumbusha kuwa uchambuzi huu sio exact science. Umeelemea kwenye uelewa wa kutosha wa mchambuzi kuhusu siasa za Tanzania.

Kadhalika, uchambuzi huu ni endelevu. Utafanyiwa marejeo mara kwa mra kila kutakapokuwa na umuhimu wa kufanya hivyo


1 Jan 2019

Image result for happy new year 2019

Heri ya mwaka mpya 2019.

Kila mwaka mpya, blogu hii huwaletea ubashiri kuhusu masuala mbalimbal yanayotarajiwa kutokea nchini Tanzania katika mwaka husika. 

Hata hivyo, ni muhimu kutanabaisha mapema kuwa ubashiri huu sio exact science. Unatokana tu na ufahamu mkubwa wa mwandishi kuhusu siasa za Tanzania sambamba na mwenendo wa mabo ulivyokuwa mwaka jana 2018.

Moja ya matukio yanayotarajia kutikisha Tanzania ni jaribio la kumpindua Rais Magufuli. Jaribio hilo ni mwendelezo wa lile lililoshindikana mwezi Novemba mwaka jana na mwandishi alikuwa mtu pekee aliyeliweka hadharani.

Iwapo jaribio hilo litafanikiwa au la ni nje ya uwezo wa blogu hii kubaini hilo, lakini wahusika ni kundi lilelile lililojaribu kumdhuru Magufuli Novemba mwaka jana, kundi linalohusisha baadhi ya viongozi wa juu wa Idara ya Usalama wa Taifa.

Haitokuwa jambo la kushangaza endapo baadhi ya wahusika "wakadhibitiwa mapema" japo blogu hii haiwezi kueleza kwa hakika "kudhibitiwa" huku kutahusisha hatua gani. 

Sambamba na hilo ni ubashiri wa mabadiliko makubwa ya uongozi wa juu wa Idara ya Usalama wa Taifa.

Tukiweka hilo kando, inabashiriwa kuwa uhusiano kati ya Tanzania na nchi wahisani/jumuiya za kimataifa utakuwa mbaya zaidi ya ilivyokuwa mwaka jana, japo hatimaye Magufuli atafyata mkia na kuwaangukia wahisani hao kufuatia hali mbaya ya fedha serikalini.

Kadhalika, sokomoko la korosho sio tu litaendelea kupelekea watendaji kadhaa wa serikali kupoteza madaraka - sio kutokana na kufeli kwao bali kufanywa mbuzi wa kafara - lakini pia litajitokeza kwenye mazao mengine/sekta nyingine pia. 

Hata hivyo kama ambavyo tayari serikali imeanza "kubadili gia angani" katika suala la korosho, huko kwenye mazao mengine/sekta nyingine nako hatimaye serikali itaufyata lakini sio kabla ya kusababisha mkanganyiko mkubwa.

Inabashiriwa kuwa "hama hama" ya wabunge na madiwani wa upinzani kwenda CCM itarejea kwa kasi kubwa, hatua itakayolenga zaidi kudhoofisha jitihada za wapinzani kushikamana na kupambana na Magufuli.

Inabashiriwa pia kuwa baadhi ya miradi mikubwa inayopigiwa chapuo na serikali ya Magufuli itakwama kutokana na hali mbaya ya kifedha. 

Kadhalika kuna uwezekano wa ATC kuanzisha safari za kimataifa lakini itakuwa kwa muda mfupi tu baada ya ndege kuzuiwa nje ya nchi kutokana na madeni ya serikali nje ya nchi.

Vilevile, inabashiriwa kuibuka upya na kushamiri kwa "kelele" za kutaka muhula wa urais uongezwe kutoka miaka mitano ya sasa hadi miaka saba au zaidi. 

Inabashiriwa pia kuwa muswada wa mabadiliko ya sheria ya vyama vya siasa utapita licha ya upinzani mkali kutoka kwa vyama vya upinzani. 

Sambamba na tukio hilo ni uwezekano kwa Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe na mbunge wake Esther Matiko kuhukumiwa kifungo katika kipindi cha vuguvugu la kupitishwa sheria hiyo kandamizi.

Kadhalika, inabashiriwa kuwa kunaweza kufanyika jaribio la kumdhuru Mbunge wa Chadema Tundu Lissu kabla hajarejea nyumbani baada ya kuwa nje ya nchi kitambo kwa matibabu kufuatia jaribio la kutaka kumuua. Inabashiriwa kuwa kutakuwa na jitihada za makusudi za kumzuwia mbunge huyo machachari kurudi nyumbani.

Inabashiriwa pia kuwa baadhi ya wanachama maarufu wa CCM watavuliwa uanachama katika jitihada za Magufuli kutunisha misuli yake katika uongozi wa chama hicho. Walengwa ni wana-CCM ambao majina yao yanatajwa kama potential candidates katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.

Maamuzi ya kiuendawazimu ya Wakuu wa Mikoa/Wilaya yataendelea kutawala mwaka huu, wahusika wakuu wakiwa walewale waliovuma kwa maamuzi ya hovyo mwaka jana.

Habari njema kwa Watanzania wengi ni anguko la Daudi Albert Bashite na mpambe wake Musiba. 

Habari nyingine njema ni jinsi utawala wa Magufuli sio tu utawaleta viongozi mbalimbali wa upinzani karibu zaidi lakini pia kuna uwezekano wa viongozi hao kupata ujasiri na kushawishi wafuasi wao kuingia mtaani kudai haki kwa nguvu.

Kwa upande mwingine, hali ya uchumi itazidi kuwa ngumu kutokana na sababu za ndani na nje ya nchi.Ndani ya nchi ni pamoja na ukweli kwamba serikali ya Magufuli imeingia mwaka huu 2019 ikiwa na hali mbaya kifedha japo kumekuwa na jitihada kubwa za kutoa takwimu feki kuashiria kuwa uchumi uko vizuri. Kwa nje ni uwezekano wa mtikisiko wa kiuchumi kama ule wa mwaka 2008 ambao utatikisa sekta ya fedha/uchumi kimataifa.

Mwisho, kuna uwezekano wa kutokea shambulio la kigaidi - halisi au la kutengenzwa. Halisi ni kutokana na tishio linaloendelea huko Msumbiji ambako sio tu kuna "magaidi" kutoka Tanzania wanaosumbua huko bali pia kuna vikosi vya JWTZ vinavyosaidiana na jeshi la nchi hiyo kukabiliana na mashambulizi ya kigaidi nchi humo.

Uwezekano wa kutengenezwa tishio la ugaidi ni mbinu inayoweza kutumiwa katika kipindi ambapo serikali ya Magufuli itakuwa inaandamwa na suala linaloipelekesha.

Nimalizie makala hii kwa kutakia heria ya mwaka mpya 2019 na kusisitiza tena kuwa ubashiri huu sio exact science. 





19 Oct 2018



Kwamba Daudi Albert Bashite ni mhusika mkuu katika utekelezaji wa mpango wa kijahili wa kutemka mfanyabashara maarufu Mohammed Dewji sio suala la siri. Na wala haihitaji uelewa mkubwa wa uchungui wa matukio ya kihalifu kubaini uhusika wa Bashite.

In fact, kabla ya Mo kutekwa, mfanyabiashara mwingine maarufu jijini Dar naye alinusurika kutekwa na vijana wa Bashite. Na majuzi, mfanyabiashara huyo amelazimika kumwaga shehena ya bidhaa baharini baada ya Bashite kutishia kumbambikia kesi kuhusu shehena hiyo.

Ni siri ya wazi kwamba Bashite amekuwa akiwanyanyasa wafanyabishara mbalimbali, akidai mamilioni ya shilingi, huku aktishia kuwabambikizia kesi za madawa ya kulevya iwapo watakataa. Huyo Mo mwenyewe “alishatolewa upepo” mara kadhaa na Bashite.

Kwa upande mwingine, Bashite amefika hapo alipo kwa kubebwa na watawala wetu. Baada ya kumpiga Mzee Warioba kwenye mchakato wa Katiba mpya, Rais wa Awamu ya Nne Jakaya Kikwete akamzawadia Bashite ukuu wa wilaya. 

Na katika mazingira ya kushangaza, Rais Magufuli akaona Bashite hastahili kuwa mkuu wa wilaya bali apewe ukuu wa mkoa kabisa. Ninaweza kusema bila kuuma maneno kuwa huu ni mmoja wa maamuzi mabovu kabisa ya Rais Magufuli. Na huenda akatambua hilo huko mbeleni akiendelea kumkumbatia jahili huyo.
Baada ya kupewa ukuu wa mkoa, Bashite akatokea kuwa mtu wa karibu kabisa wa Magufuli. Hata alipovamia studio za Clouds Media Group, Mkuu huyo wa nchi akawamtetea vikali kijana huyo aliyetenda kosa la jinai. Hiyo ikampa Bashite jeuri na kiburi kikubwa.

Mara kadhaa, Magufuli alikuwa akimmwagia sifa Bashite akidai ndio Mkuu wa Mkoa mchapakazi kuliko wote. Mchapakazi kwa kufeli kisha kufojic heti na jina lake? Mchapakazi kwa kudai rushwa kwa wafanyabishara mbalimbali? Mchapakazi kwa yeye na “mlevi mbwa” Kitwanga kumpa yule mbwa Musiba shilingi milioni 7 za kututangaza akina sie kuwa ni watu hatari?

Kumdekeza Bashite na kumpendelea hata pale alipofanya uahlifu ndio kumemfanya haramia huyu kufikia hatua ya kufanikisha mpango wa kumteka Mo Dewji. Bashite ni kiumbe hatari kabisa na janga kubwa kuliko yote katika historia ya Tanzania. Na amin nawaambia, hata alindwe vipi na baba yake, mwisho wa jahili huyu utakuwa mbaya sana. 

Na sio kama ninamtetea Magufuli, ila hili la kumteka Mo, ni mpango binafsi wa Bashite alioufanya kwa niaba ya washirika wake kutoka nje ya nchi. 

Naamini hadi kufikia muda huu, watu wa Kitengo wameshamfahamisha Magufuli kuwa ‘mwanae’ Bashite ndio aliyemteka Mo, na anajua alipo. 

Na hapo ndio tunabaki kujiuliza: je Magufuli atakuwa tayari kuhatarisha urais wake na “kumbeba” tena Bashite? Tayari kuna dalili hizi maana mpaka wakati ninaandika makala hii, Bashite alikuwa hajakamatwa wala kuhojiwa, achilia mbali kutumbuliwa.
Magufuli anaachia fursa adimu ya kujitenga na kijana huyo mhuni ambaye amefanya jithada kubwa kuuharibu utawala wa “baba yake.” Kama kuna mtu mmoja amechangia sana kumfarakanisha Magufuli na Watanzania wengi si mwingine bali Bashite.

Kwa kumchukulia hatua Bashite, Magufuli angeuwa ndege wengi kwa jiwe moja. Kwanza, kumtimua Bashite kungemfanya aonekane kuwa sio tu amekerwa na kutekwa kwa Mo Dewji na bali pia “kujisafisha” yeye mwenyewe dhidi ya tuhuma kuwa huenda waliomteka Mo ni watu wa serikali yake Magufuli.

Lakini pia, kwa kumtumbua Bashite, Magufuli angejiweka kando na mtu ambaye amefanya kila linalowezekana kuchafua jina la “baba yake.” Kama nilivyotanabaisha awali, Bashite amechangia mno kuwafanya Watanzania wengi tu kutoipenda serikali ya Awamu ya Tano.

Pengine kubwa zaidi ya yote ni ukweli kwamba, kwa Magufuli kuchukua hatua dhidi ya Bashite itamsaidia kujenga mahusiano bora na wafanyabiashara wakubwa ambao wamekuwa wahanga wakubwa wa uonevu wa Bashite.

Lakini kubwa zaidi katika hili ni Magufuli kuepusha uwezekano wa wafanyabiashara hao kuungana na maadui wake (Magufuli) hususan ndani ya CCM ambako kuna makundi kadhaa yenye dhamira ya kumfanya awe Rais wa muhula mmoja kama sio kumng’oa kabla ya uchaguzi mkuu ujao.

Ni vigumu kubashiri kwa hakika kuwa hatimaye Magufuli atamwaga Bashite lakini kilicho bayana ni kwamba ana option moja tu: amlinde ahatarishe uraia wake au ambwage ajitengenezee mazingira mazuri ya urais wake. Ifahamike mapema kuwa ikitokea Magufuli kamtumbua Bashite basi Tanzania italipuka kwa mayowe na vigelegele kana kwamba imeshinda Kombe la Dunia.

Mwisho, hatua za Magufuli dhidi ya Bashite ndio ufumbuzi pekee wa sakata la kutekwa kwa Mo. Yaani akikamatwa na kuhojiwa, ataeleza Mo yuko wapi, na hivyo kuwezesha kupatikana kwa mfanya biashara huyo tajiri si Tanzania tu bali pia ni mmoja wa matajiri wakubwa Afrika na duniani kwa ujumla. Ni matumaini yangu kuwa Magufuli atatambua kuwa akiendelea kumlea Bashite basi huenda “akaondoka nae.”


12 Oct 2018



NANI KAMTEKA MO DEWJI? UCHAMBUZI WA KIINTELIJENSIA KWA KUTUMIA MBINU YA 'CONTRARIAN' IJULIKANAYO KAMA DEVIL'S ADVOCATE

Changamoto kuu mbili katika kufanya uchambuzi wa kiintelijensia (intelligence analysis) ni, moja, kutambua taarifa stahili/mwafaka za kuzifa
nyia uchambuzi husika, na mbili, ni kitu kinachofahamika kama 'cognitive bias,' yaani kwa lugha nyepesi ni kama upendeleo/ubaguzi wa aina flani ambao unatokea akilini bila kuamua kwa makusudi.

Kwa mfano, mchambuzi ambaye ni kada wa CCM akipewa jukumu la kuchambua suala linalohusu Chadema, basi anaweza kuwa anaendeshwa na ubaguzi flani kichwani pasi yeye kukusudia.
Kwahiyo, hata katika uchambuzi huu wa kiintelijensia, huenda kukawa na cognitive bias, lakini hilo sio lengo langu, na ninadhamiria kuongozwa na taarifa zilizopo kuliko hisia zangu binafsi.

Kuna mbinu kadhaa za kufanya uchambuzi wa kiintelijensia, na miongoni mwa mbinu hizo ni "Contrarian Techniques" ambazo ni "Devil's Advocacy," "Team A/Team B," "High Impact/Low Probability Analysis" na "'What If' Analysis."

Katika uchambuzi huu, nitatumia mbinu ya Devil's Advocacy ambayo hutumika zaidi katika mazingira ambayo tayari kuna hisia flani 'kali' kuhusu suala husika.

Tukio ninalolifanyia uchambuzi wa kiintelijensia ni kama nilivyotanabaisha kwenye kichwa cha habari, nalo ni la kutekwa kwa Mkurugenzi wa kundi la Makampuni ya Mohamed Enterprises, Mohammed Dewji almaarufu 'Mo.' Tukio hilo lilitokea jijini Dar es Salaam jana alfajiri, katika eneo la ukumbi wa Colosseum.

Mbinu ya uchambuzi wa kiintelijensia ya Devil's Advocacy ni mwafaka katika tukio hili kwa sababu kuu moja: utafutaji wa taarifa za kiintelijensia uliofanywa tangu baada ya kupatikana taarifa za tukio hilo, kwa kutumia njia kuu moja ya ukusanyaji taarifa za kiintelijensia – Open Source Intelligence (OSINT) – unaonyesha kuwa serikali inatupiwa lawama kuwa ndiyo iliyohusika kwenye tukio hilo.

Na kama ilivyoelezwa awali, mbinu ya Devil's Advocacy ni mwafaka katika mazingira ambayo tayari kuna hisia flani 'kali' kuhusu suala husika, na hapa hisia hiyo kali ni uhusika wa serikali.

Katika kutumia mbinu hii, kuna hatua kadhaa zinazopaswa kufuatwa na mchambuzi, na miongoni ni kama ifuatavyo:

·        →Kuorodhesha hisia mbalimbali
·       → Kuchagua hisia kuu moja au mbili katika hizo mbalimbali, inayoonekana kuwa na uzito zaidi
·        →Rejea taarifa zilizopatikana kuhusiana na tukio husika
·        →Onyesha ushahidi unaoweza kufanya hisia husika kuwa na uzito zaidi.

Kwahiyo tuanze uchambuzi huu kwa kuorodhesha hisia mbalimbali kuhusiana na kutekwa kwa Mo Dewji. Hisia hizi zimekusanywa kwa kutumia ukusanyaji taarifa kupitia vyanzo vya wazi, yaani Open Source Intelligence (OSINT).

Hisia hizo ni kama ifuatavyo:

·        Mo Dewji ametekwa na serikali
·        Mo Dewji ametekwa na watu wanaohusiana na serikali lakini hawakutumwa na serikali (rogue elements)
·        Mo Dewji ametekwa na watu wanaotaka kuichafua serikali
·        Mo ametekwa na wahalifu
·        Mo ametekwa na washirika/maadui zake kibiashara
·        Mo hajatekwa, ni maigizo tu.

Tupitie kila hisia ili kuweza kubakiwa na hisia kuu moja au mbili.

Mo Dewji ametekwa na serikali:

Uzito wa hisia: Rekodi ya serikali sio nzuri katika usalama wa raia mbalimbali, kuanzia "kupotea" kwa kada wa Chadema Ben Saanane na kwa mwanahabari Azory Gwanda, na idadi isiyojulikana ya watu waliopotea huko MKIRU. Kadhalika, matukio yanayohusisha 'watu wasiojulikana' na shambulizi dhidi ya Mbunge Tundu Lissu yanaongeza uzito kwenye hisia hii. Vilevile ukweli kwamba eneo la Colosseum limezungukwa na nyumba mbalimbali za viongozi na taasisi muhimu zenye ulinzi mkali, na hakukuwa na jitihada za kukabiliana na watekaji, zinaweza kuashiria uhusika wa serikali.

Mapungufu ya hisia: Serikali haina incentive katika kumteka Mo Dewji. Kwamba kama kulikuwa na tatizo lolote kama ni kisiasa au kiuchumi basi angeweza tu kukamatwa au "kubebeshwa kesi ya kodi" na TRA au "kesi ya ufisadi" na TAKUKURU. Ieleweke kuwa Mo Dewji alijiweka mbali na masuala ya siasa, na yayumkinika kuamini kuwa hana maadui wa kisiasa. Kadhalika, high profile ya Mo Dewji ilitosha kuijulisha serikali kuwa lolote litakalomtokea mfanyabiashara huyo litakuwa na athari kubwa kwake.

Hitimisho: Mapungufu dhidi ya hisia hii ni makubwa zaidi ya uzito wake. Kwahiyo inaondolewa.

Mo Dewji ametekwa na rogue elements ndani ya serikali:

Uzito wa hisia hii: Kwa kurejea matukio mbalimbali hususan yanayohusishwa na Daudi Albert Bashite, yayumkinika kuhisi uwepo wa mkono wa rogue elements huko TISS au kwingineko. Uzito zaidi kwenye hoja hii unachangiwa na jinsi Bashite alivyojaribu kuwa mstari wa mbele kuelezea kuhusu suala hilo, badala ya kuwaachia polisi wafanye kazi yao.

Mapungufu ya hisia hii: Huenda mkakati huo ungefahamika mapema kwa taasisi kama TISS na hivyo kuweza kuzuiliwa kabla haijatekelezwa. Hata hivyo, kuna mapungufu katika hoja hii ambayo ni ishara zinazoashiria mapungufu makubwa ya kiutendaji ya TISS, kiasi kwamba inawezekana taarifa hizi hawakuzipata.

Hitimisho: Hisia hii ina mantiki, na itaendelea kuwepo katika uchambuzi huu

Mo Dewji ametekwa na watu wanaotaka kuichafua serikali

Uzito wa hisia hii: Uzito upo kwenye ukweli kwamba upinzani mkubwa dhidi ya serikali ya Rais John Magufuli upo zaidi ndani ya CCM kuliko nje ya chama hicho. Ikizingatiwa kuwa kuna takriban miezi 24 tu kabla ya uchaguzi mkuu ujao, wapinzani wa Magufuli wanaweza kufanya tukio hilo kwa minajili ya kumchafua, na pengine kujenga hoja ya kumwekea vikwazo kwenye kugombea urais mwaka 2020. Kwa kuzingatia incentives, wapinzani hao wana kila cha kunufaika na kidogo cha kupoteza (a lot to gain and only a little to lose).

Mapungufu ya hisia hii: Mkakati mkubwa kama huu ungeweza kunaswa kirahisi tu na vyombo vya dola kama vile TISS na hivyo kuweza kuudhibiti. Hata hivyo, kama ilivyokuwa kwenye hisia iliyopita, kuna ishara za mapungufu ya kiutendaji kwa taasisi hiyo, hali ambayo inaweza kuwa iliruhusu mpango huu kutekelezwa.

Hitimisho: Hisia hii ina mantiki, na inaendelea kubaki kwenye uchambuzi huu.

Mo Dewji ametekwa na wahalifu:

Uzito wa hisia hii:  Kuna taarifa za uwepo wa magenge ya kihalifu ya kimataifa nchini Tanzania. Taarifa ambazo hazijathibitishwa kuwa watekaji ni 'wazungu' zinaweza kusaidia kuipa uzito zaidi hisia hii.

Mapungufu ya hisia hii: katika mazingira ya kawaida, wahalifu hao wasingependelea sehemu kama Colesseum kuwa eneo la utekaji kwa sababu kuna idadi kubwa na nyumba za viongozi na taasisi za serikali ambazo zina ulinzi mkali. Hata hivyo, yawezekana kuwa wahalifu hao walishafanya reconnaissance ya kutosha na kubaini mapungufu husika.

Hitimisho: Hisia hii japo ina mantiki lakini kiuhalisia inaonekana kuwa sio yenye nguvu. Kwahiyo inaondolewa.

Mo Dewji ametekwa na washirika/maadui wake kibiashara:

Uzito wa hisia hii: mfanyabiashara wa kimataifa kama Mo Dewji hawezi kukosa maadui. Lakini pia masuala ya biashara za kimataifa yanaweza kuzua migongano hata miongoni mwa washirika katika biashara husika. Kama ilivyokuwa kwenye hisia iliyotangulia, yawezekana watekaji hao walishasoma mapungufu ya kiusalama katika eneo la tukio.

Mapungufu ya hisia hii: Kama ilivyokuwa kwenye hisia iliyopita, mazingira ya eneo la tukio hayakuwa mwafaka kwa watu wenye lengo la kumdhuru mtu kuyatumia kutekeleza lengo hilo. Hata hivyo, yawezekana wahusika walishabaini mapungufu ya kiusalama katika eneo hilo.

Hitimisho: Hisia hii ina mantiki lakini uwezekano wa washirika/maadui wa Mo Dewji kumteka katika mazingira yalivyokuwa, haiingii sana akilini. Hisia hii inaondolewa kwenye uchambuzi huu.

Mo Dewji hajatekwa ni maigizo tu:

Uzito wa hisia hii: Kwa kuzingatia matukio ya huko nyuma, yawezekana tukio hili ni mchezo wa kuigiza tu.

Mapungufu ya hisia hii: Mchezo wa kuigiza ili iweje? Hakukuwa na tukio la muhimu ambalo jamii ilipaswa "kuzugwa na kutekwa kwa Mo Dewji." 

Hisia hii inaondolewa kutokana na kukosa mashiko.
Kwahiyo, hisia zinazosonga mbele ni mbili,
       Mo Dewji ametekwa na watu wanaohusiana na serikali lakini hawakutumwa na serikali (rogue elements)
       Mo Dewji ametekwa na watu wanaotaka kuichafua serikali

Hisia hizi mbili zinaweza kimsingi kuwa moja, kwa sababu watu wenye nia ya kuichafua serikali wanaweza kuzitumia rogue elements kufanya kazi hiyo. Lakini pia rogue elements hizo zinaweza kuwatumia watu wanaotaka kuichafua serikali kutekeleza azma hiyo.

Na kwa minajili ya kuweka rekodi sawia, kiongozi wa rogue elements hizo ni Daudi Albert Bashite, bila shaka. Na hili linaweza kuongezewa uzito na ukweli kwamba jana Bashite alijigeuza kama RPC au Mkuu wa Kanda Maalum ama sio msemaji wa Jeshi la Polisi. Je ni ile "mchawi aliyemroga marehemu hujifanya mwenye uchungu kuliko wafiwa"?

Uchambuzi wa kiintelijensia sio sayansi timilifu kwa asilimia 100 (it's not exact science), na kwa maana hiyo inawezekana kabisa sababu ikawa nyingine nje kabisa ya hizi nilizozichambua.

Ninachofanya hapa sio kujifanya mjuaji bali kuchangia kwenye 'body of knowledge,' sambamba na kuhamasisha mjadala kuhusu suala hili ambalo linaweza kuwa na athari kubwa kwa Tanzania.

Hitimisho: Ingependeza kuhitimisha makala hii kwa kutamka bayana kuwa "hisia kuu ni hii" lakini hisia mbili zilizoweza kuvuka mchujo zinabaki kuwa mtazamo ninaona ni mwafaka zaidi.
Je wewe una mawazo gani?


21 May 2018



Kuna msemo usiopendeza kwamba, ukitaka kumficha kitu Mswahili, basi weka kwenye kitabu. Waswahili wengi wanaogopa maandishi kuliko virusi vya UKIMWI, except maandishi hayo yatakapohusu UBUYU, our nation's favourite.

Sasa, kwa vile lawama hazijengi, nimeamua kuendeleza utaratibu niliouanzisha huko Facebook ambapo mara kwa mara nilikuwa nawapatia watu machapisho mbalimbali BURE. Kwahiyo, angalau mara moja kwa wiki, nitakuwa naweka post yenye link ya kupakua kitabu chenye umuhimu kwako. Series hiyo ya vitabu takriban kila wiki ninaipa jina "Let's Read / Na Tusome."

Leo tunaanza na chapisho hili muhimu kuhusu "ushushushu." Ni mwongozo wa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) kuhusu "kuzuga watu" (trickery) na hadaa (deception). Baadhi yenu mtakuwa mlishakipakua nilipokiweka mara mbili huko Facebook.

Pakua HAPA


Sambamba na vitabu, from time to time nitajitahidi kubandika makala mpya mara nyingi zaidi ya ilivyo sasa ambapo inaweza kupita mwezi mzima bila kubandika post yoyote ile.Tarajia mada za mbinu za kimaisha (life hacks), usalama wa mtandaoni (cybersecurity), nyeNzo za mtandaoni (internet tools), afya, na kadhalika. Hakikisha unatembelea blogu hii mara kwa mara.


21 Apr 2018


Jana ilitolewa taarifa kwa vyombo vya habari  kuwa Rais John Magufuli amemteua "Msalika Robert Makungu kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora." Hata hivyo, kwa makusudi, taarifa haikueleza kabla ya uteuzi huo, Makungu alikuwa na wadhifa gani, japo ilieleza kuwa anakwenda mkoani Tabora kuchukua nafasi ya Dokta Thea Ntara ambaye amestaafu.



"Kilichofichwa" kwenye taarifa hiyo ni ukweli kwamba Makungu alikuwa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa (DDGIS) ambaye aliteuliwa wakati mmoja na Mkurugenzi Mkuu wa Idara hiyo, Dokta Modestus Kipilimba, Agosti mwaka jana.

Japo taarifa husika haikutumia neno "kutumbuliwa," lakini haihitaji ufahamu wa mfumo wa utawala wa Idara ya Usalama wa Taifa kumaizi kwamba kutoka u-Naibu Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo nyeti hadi u-Katibu Tawala wa Mkoa ni kushushwa cheo (demotion). 

Kwa mujibu wa vyanzo vyangu vya kuaminika ndani ya taasisi hiyo, kilichopelekea hatua hiyo inayoelezwa kuwa ngumu kwa  Magufuli ni tofauti kati ya watendaji hao wakuu wa taasisi hiyo, yaani Makungu na aliyekuwa bosi wake, yaani Kipilimba.

Inaelezwa kuwa tofauti kati yao ilikuwa kubwa kiasi cha Kipilimba kutishia kujiuzulu iwapo Magufuli asingechukua hatua dhidi ya Makungu.

Hata hivyo, Makungu alikuwa "mtu wa Magufuli" kwa sababu ni wote wanatoka Kanda ya Ziwa, na ni miongoni mwa "circle ya karibu ya Magufuli" ambayo pamoja na watu wengine, inayojumuisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Katibu Mkuu wa Hazina Dotto James, na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga.

Kwahiyo wakati  ingetarajiwa Magufuli "angemkumbatia poti wake Makungu" lakini kwa mujibu wa vyanzo vyangu, umuhimu wa Kipilimba kwa Magufuli ni mkubwa zaidi. 

Tukio hilo ambalo halikuvuta hisia za wengi hasa kwa vile lilitokea muda mfupi baada ya kupatikana taarifa za kifo cha mlimbwende maarufu Agnes Masogange aliyefariki jijini Dar jana.

Japo wadhifa wa "Naibu Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa" (DDGIS) sio wa muda mrefu tangu uanzishwe (Makungu alikuwa mtu wa pili kushika wadhifa huo baada ya Jack Zoka kuwa wa kwanza), kitendo tu cha Mkurugenzi katika taasisi hiyo kutolewa na kupelekwa mkoani ni cha kushangaza na kinaingia moja kwa moja kwenye kumbukumbu za kihistoria.

Hata hivyo, kabla ya Makungu "kutumbuliwa" tayari kuna Mkurugenzi mwingine ambaye aliondolewa kwenye wadhifa wake kama  nilivyoripoti kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter

Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana wakati huo, kuondoka kwa mwanamama huyo kulichangiwa na mtazamo wake wa kutaka mabadiliko ndani ya taasisi hiyo ambao ulikinzana na wahafidhina wasiotaka mabadiliko yoyote kwa taasisi hiyo.

Wakati hayo yanatokea, Zoka, aliyekuwa Balozi wa Tanzania huko Canada nae alitolewa katika wadhifa huo hivi karibuni. Nilieleza kwa kirefu kuhusu tukio hilo katika makala HII

Kama ambavyo Zoka aliandamwa na lawama kwamba alikuwa akiongoza mkakati wa kuhujumu vyama vya upinzani, Makungu pia ametoka katika nafasi hiyo akikabiliwa na lawama kama hizo.


Kwa upande wangu binafsi kama afisa wa zamani katika taasisi hiyo, wakati fulani nililazimika kumwandikia barua Makungu kutokana na taarifa flani zilzonikera. Na katika barua hiyo nilimkumbusha kuwa cheo ni dhamana, na hakina mwamana.


Tatizo kwa wenzetu wengi wanaposhika madaraka ni ile hali ya kujisahau wakidhani watafia wakiwa kwenye madaraka. Hupuuzia ukweli kuwa ipo siku watatoka katika nafasi zinazowapa jeuri na kujikuta "mtaani." Maisha hayatabiriki, leo unalala ukiwa DDGIS kesho unaamka ukiwa RAS.



Kuhusu iwapo hatua hiyo ya Magufuli kuwa na atahri zozote, kwa sasa ni mapema mno kubashiri. Baadhi ya maafisa waliopo kazini na wastaafu  wa Idara ya Usalama wa Taifa walidokeza kwamba taarifa hiyo ya kuondolewa kwa Makungu imewashtua wengi

 Kwa upande mwingine, wakati yote haya yanatokea, haijafahamika hali ikoje kwa "Idara ya Usalama wa Taifa nje ya Idara ya Usalama wa Taifa," yaani kile kikosi kilicho chini ya Daudi Alabert Bashite.



Kwamba Kipilimba ameweza kumn'goa "poti wa Magufuli" Makungu, basi huenda pia akawezesha kung'oka kwa Bashite, mtu anayeutia doa utawala wa Magufuli kwa kila hali.



Ni muhimu pia kujumuisha tweet ya mtu mmoja ambaye hujitambulisha kama Gavana wa zamani wa Benki Kuu, Daudi Balali.


Nimalizie makala hii kwa kukushauri uwe ukiitembelea blogu hii mara kwa mara upate fursa adimu ya kusoma uchambuzi exclusive kama huu wa leo.

16 Apr 2018






Africa Confidential Toleo la 28 Machi 2018


27 Machi 2018

Hatua za kidikteta za Magufuli zinakumbana na upinzani unaoongezeka lakini ndio Ameshika uelekeo huo na anatishia wanaomkosoa

Katikati ya muhula wake wa kwanza, Rais John Magufuli anakabiliwa na shinikizo. Huku akikabiliwa na tishio kubwa kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), vikundi vya kiraia, viongozi wa kanisa, na sasa vijana kwenye mitandao ya kijamii, anaonekana kufurahia mapambano hayo. Dola pia inatishiwa na makundi yenye silaha yaliyokuwa viongozi wa serikali na chama mkoani Pwani (MKIRU). Majibu ya serikali kukabiliana na changamoto hizo yametawaliwa na ukatili ambao haujawahi kuonekana kamwe, na kupelekea kulaaniwa kutoka kila upande.

Kuongezeka kwa vurugu za kisiasa, hasa wakati wa uchaguzi mdogo wa jimbo la Kinondoni, kulipelekea lawama dhidi ya utawala wa mabavu wa Magufuli. Ubalozi wa Marekani ulitaka kufanyike uchunguzi kuhusu utekaji na mauaji ya kiongozi wa upinzani jijini Dar es Salaam wakati wa kampeni. Umoja wa Ulaya baadaye ulionyesha wasiwasi wake kuhusu "mwenendo wa hivi karibuni unaotishia kanuni za demokrasia" baada ya polisi kutumia risasi katika maandamano ya Chadema katika mkesha wa siku ya kupiga kura Februari 17, hali iliyopelekea majeruhi watatu na kuuawa kwa mpita njia.

Wiki mbili baada ya matamko hayo, Wizara ya Mambo ya Nje ilijibu kwa taarifa yenye kurasa tatu na nusu ikiyahusisha matukio ya huko MKIRU na "vikundi vya ndani na nje ya nchi vinavyochukizwa na jitihada za Magufuli kuondoa ufisadi, biashara ya mihadarati, ujangili, ukwepaji kodi na kujenga uwajibikaji."

Vikundi hivyo vyenye silaha, ambapo baadhi vinadaiwa kuwa na mahusiano na Al-Shabaab ya Somalia, vimewauwa viongozi wa Chama Cha Mapinduzi na baadhi ya watendaji wa serikali. Tatizo hilo lilianza tangu mwaka 2014 lakini likafikia kilele mwaka 2017 baada ya operesheni ya kikatili ya vyombo vya dola kushambulia. Serikali inajaribu kuushawishi umma kwamba maandamano ya amani dhidi ya haki za kiraia na mauaji hayo ya MKIRU ni pande mbili za kitu kimoja. Ni watu wachache tu wanaoshawishika kuamini.
Katika ujumbe wao kwa msimu wa Kwaresma, maaskofu wa Katoliki walionya kwamba kuendelea kwa ukandamizaji wa kisiasa kutapelekea migawanyiko itakayohatarisha misingi ya kitaifa ya umoja na mshikamano. Walieleza kwamba kuzuwia shughuli za kisiasa sio halali na kunakiuka katiba. Kituo ch Demokrasia (TCD), ambacho huvileta pamoja vyama vya siasa kilitoa tamko la pamoja na viongozi wa Kikristo na Kiislamu kudai mapitio ya Katiba. Hii ilifuatiwa na kauli ya kuunga mkono ya vikundi zaidi ya 100 vya kiraia.

Jumapili ya Majivu Machi 25 ilishuhudia maaskofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (ELCT) wakitoa tamko kali wakiilaani utekaji watu, utesaji watu, upoteaji watu, mashambulizi ya silaha dhidi ya wanasiasa, mauaji yanayotokana na itikadi za kisiasa, vitisho, kesi za kubambikizwa, na unyanyaswaji wa raia unaofanywa na vyombo vya dola. Pia walitaka katiba mpya iwepo kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020. "Taifa huongozwa na katiba ambayo ndio msingi wa sheria zote", walisema. "Haiongozwi na ilani za vyama."

Pia kuna changamoto za kisheria. Mahakama Kuu inatarajiwa kusikia kesi mbili za kikatiba zilizoletwa na watetezi wa haki za binadamu ikiwa ni pamoja na Chama cha Wanasheria TLS, Umoja wa Watetezi wa Haki za Binadamu (the Tanzania Human Rights Defenders Coalition), na Taasisi ya sheria na haki za binadamu (the Legal and Human Rights Centre). Kesi zote zinaongozwa na Fatma Karume wa kampuni ya uwakili ya IMMA, ambayo ofisi zake zilichomwa moto Agosti mwaka jana. Akiwa anatoka kwenye familia yenye nguvu ya Karume, amekuwa mwiba kwa utawala uliopo madarakani. TLS inaongizwa na mmoja wa wateja wake, kiongozi wa Chadema Tundu Lissu, ambaye bado yupo Ubelgiji anakopata matibabu ya majeraha ya risasi kufuatia jaribio la kumuuwa.

Kumekuwa na ukosoaji ndani ya CCM pia. Nape Nnauye, mbunge aliyetimuliwa uwaziri mwaka jana, ametoa wito wa kuifanyia marekebisho Idara ya Usalama wa Taifa (TISS) akieleza "kwa macho makavu" kuwa kama ambavyo taasisi hiyo imekuwa ikifanya kazi kwa manufaa ya dola, pia imekuwa ikiitumikia CCM, inaendeshwa kisiasa.

Mbunge mwingine wa CCM, Hussein Bashe, ambaye awali hakufahamika kuwa na mtazamo huru, na aliongoza kampeni ya Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa kuwania urais, naye ametokea kuwa mtetezi wa uhuru wa kujieleza na mawazo mbadala.

Haya na matamko mengine yanaashiria demokrasia ya Tanzania ipo katika kipindi kigumu. Akiongea kwenye shughuli ya TCD ambayo ilipelekea wito wa katiba mpya, Askofu Benson Bagonza wa Kanisa la Kilutheri alitanabaisha kuwa kamwe hajawahi kuona polisi wakitumia risasi dhidi ya waandamanaji. "Nini kimebadilika?" aliulizwa.

Moja ya majibu kwa swali lake hilo ni "hakuna kikubwa (kilichobadilika)." Kunapokuwa na upinzani mkali kwenye chaguzi zilizopita, dola na chama tawala vimekuwa vikikimbilia kwenye ukatili. Kufanya vema kwa Chadema katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 kulipelekea angalau miaka miwili ya ukatili. Ilianza Januari 2011 ambapo polisi walitumia risasi dhidi ya maandamano ya wafuasi wa Chadema Arusha.
Februari 2012, wanaharakati 16 wa haki za binadamu walikamatwa kwa kuunga mkono mgomo wa madaktari. Agosti mwaka huohuo, polisi walimuua kwa risasi muuza magazeti huko Morogoro wakati wa maandamano ya Chadema. Mwezi uliofuata, mwandishi wa habari Daudi Mwangosi aliuawa na polisi kufuatia kupigwa na bomu la kutoa machozi huku akiwa amekandamizwa chini na polisi. Katika mwezi huohuo, kiongozi wa maandamano ya madaktari, Steven Ulimboka alitekwa, akateswa na kuachwa ajifie mwenyewe kwenye msitu nje ya jiji la Dar es Salaam, tukio linalodhaniwa kufanywa na maafisa wa TISS. Baadaye mwaka huo huo, na pia Mei 2013, njia za kikatili zilitumika kukabiliana na maandamano yaliyoambana na wimbi kubwa la machafuko katika historia ya Tanzania.

CCM inakabiliwa na changamoto kubwa kudumisha utawala wake. Kwa kutoongelea suala la ufisadi mkubwa (katika kampeni zake za uchaguzi mkuu wa) mwaka 2015, ilitoa fursa kwa Chadema kupata mafanikio (ya kuridhisha) katika uchaguzi huo. Wimbo la ukandamizaji linaloendelea hivi sasa, linailenga Chadema, na pia linachangiwa na hofu kuhusu vikundi vyenye msimamo mkali vyenye silaha (kama ilivyokuwa huko MKIRU).

Sintofahaumu hiyo inaweza kueleza ukatili mkubwa uliotumika kukabiliana na kilichokuwa kikijiri katika mkoa wa Pwani. Miili kadhaa iliyofungwa kwenye 'viroba' iliyokutwa inaelea maeneo ya (Msasani) Peninsula jijini Dar es Salaam inaashiria jinsi hali ilivyokuwa.

Wizara ya Mambo ya Nje ilitoa tamko masaa tu baada ya tovuti ya African Arguments ya Royal African Society kuchapisha habari iliyoeleza kuhusu matumizi ya silaha za moto dhidi ya waandamanaji huko wilayani Rufiji katika ofisi za halmashauri ya mji.

Kwa kuunganisha vitendo vya vikundi hivyo vilivyokuwa vinavyotumia silaha (huko MKIRU) na upinzani dhidi ya mageuzi yanayofanywa na Magufuli, inatoa kisingizio kwa dola kutumia nguvu dhidi ya makundi yote mawili (vikundi vya MKIRU na upinzani dhidi ya Magufuli).

Mkuu wa Majeshi Jenerali Venance Mabeyo aliwataka Watanzania kuwa wazalendo dhidi ya tishio kwa amani, umoja, uhuru na mshikamano. Kichekesho ni kwamba aliyasema hayo katika maadhimisho ya viongozi waliopambana na utawala wa mkoloni mwaka 1907 katika Vita ya Maji Maji. Jinsi dola inavyopambana na vurugu na upinzani inarejesha kumbukumbu za jinsi serikali ya mkoloni ilivyopambana na upinzani dhidi yake.

Mafanikio yoyote ya kuelezea kuhusu tishio linaloukabili demokrasia nchini Tanzania yatategemea zaidi makundi mbalimbali ndani ya CCM na tabaka tawala. Wanaoonekana kama wapinzani ndani ya CCM kama Nape na Bashe watabaki ndani ya chama hicho kwa gharama yoyote, wakicheza mchezo mrefu wa subira hadi uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 ambapo inatarajiwa Magufuli atamaliza muda wake.

Viongozi wa dini – Magufuli anajitambulisha kama Mkatoliki mcha Mungu – wanaweza kufanikiwa kumshawishi kupunguza matumizi ya vyombo vya dola dhidi ya upinzani. Lakini wanaharakati na wanasiasa wa upinzani wanafahamu fika kuwa kudhibitiwa kwa asilimia 100.

MHALAKI (SOCIALITE) AONGOZA MAPAMBANO KUPITIA MTANDAO WA KIJAMII WA INSTAGRAM

Mashtaka yanayofunguliwa na taasisi za kiraia na matamko ya viongozi wa dini ni kitu kimoja, lakini wito wa kufanyika maandamano unaotolewa na bloga mwenye makazi yake Los Angeles (Marekani), Mange Kimambi, ni changamoto tofauti kabisa kwa Magufuli. Kimambi amekuwa sura ya hadharani ya wito wa maandamano ya nchi nzima tarehe 26 Aprili dhidi ya Magufuli.

Akifahamika zaidi kwa masuala ya fasheni na habari zinazohusu watu maarufu, akaunti ya Instagram ya Kimambi imekuwa ikihamasisha na kuyapa umaarufu maandamano hayo, yanayotarajiwa kufanyika siku ya Muungano, ambayo ni kumbukumbu ya Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar.

Kimambi anayedhaniwa kuwa anashirikiana na wanaharakati nchini Tanzania, anachukuliwa kwa uzito mkubwa na mamlaka za nchi hiyo. Akiongea kwenye tukio moja Machi 9 kijijini kwake Chato, Magufuli alisema "tusubiri na tuone wakiandamana, na watanitambua." Siku chache kabla, Waziri wa Mambo ya Ndani Mwigulu Nchemba aliwatuhumu waandaaji wa maandamano hayo kuwa wanapanga kuuwa watu na kisha kuvitupia lawama vyombo vya dola. Maonyo mengine yametolewa na angalau makamanda wa polisi wa mikoa saba. Inafahamika kuwa viongozi wa serikali na chama (tawala) wameelekezwa kuhamasisha upinzani dhidi ya maandamano hayo na tayari watu kadhaa wameshakamatwa.

Kimambi ni mwanaharakati ambaye haingekuwa rahisi zamani kumtarajia. Alipata umaarufu mwaka 2009 kupitia blogu yake ya 'U-Turn' ambayo ilikuwa ikisimulia kuhusu maisha yake kama mhalaki huko Dubai. Baadaye alihamia katika makazi yake ya sasa, Los Angeles, kabla ya kuanza kuiteka Instagram mwaka 2015, ambapo alimpigia Magufuli kampeni yenye ufanisi, licha ya yeye kushindwa kuteuliwa kugombea ubunge jimbo la Kinondoni.

Alimgeuka Magufuli takriban Mei 2016 ambapo alipinga vikali kusitishwa kwa matangazo ya moja kwa moja ya vikao vya bunge. Anachanganya upinzani wa kisiasa na nguvu yake kama mhalaki anayeweza kumjenga au kumbomoa mtu kwa kutumia mitandao ya kijamii. Awali ilikuwa kuhusu picha zake binafsi na "selfies" lakini baadaye mabadiliko yakajitokeza. Kufikia mwishoni mwa mwaka 2016, akaunti yake ikawa sehemu kuu ya harakati za mtandaoni za upinzani dhidi ya serikali, na sehemu ya kuona nyaraka mbalimbali zilizovuja.

Akaunti yake imechukua nafasi ya Jamii Forums, jukwaa la maoni mtandaoni lililokuwa kitovu cha upinzani mtandaoni, na ambalo waanzilishi wake wanakabiliwa na kesi mahakamani na wamekuwa wakisumbuliwa na mamlaka kwa muda mrefu.

Huku akiwa na wafuasi zaidi ya milioni 1.4* kwenye Instagram, uwezo wa Kimambi kuwafikia watu unawazidi wanasiasa wote wa Tanzania, japo kuna shaka kuhusu maandamano ya April 26. Kujitokeza kwa watu wengi kwenye maandamano hayo kutategemea uwezo wa waandaaji wake wa maandamano hayo nchini Tanzania, ambao wanaokabiliana na utawala usio na huruma – polisi watamwaga risasi kwa ajili ya kuuwa, kama ambavyo wamefanya huko nyuma.

Haitojalisha hata kama hakuna mtu atayejitokeza kuandamana Aprili 26. Kutoka umbali wa kilomita 26,000, Kimambi tayari ameweza kufanya zaidi ya kutikisa mkia wa chui kwa kutumia simu ya mkononi tu. Na laiti ikitokea asalimisha yeye mwenyewe, mara moja kukamatwa kwake kutakuwa tukio kubwa kabisa litakaloiweka Tanzania kwenye macho na masikio ya dunia nzima.

MAELEZO YANGU: Makala hii ni tafsiri ya neno kwa neno ya makala ya gazeti maarufu la duniani la habari za kuchunguza kuhusu bara la Afrika la AFRICA CONFIDENTIAL Toleo laMachi 28, 2018 lililokuwa na kichwa cha habari "Enemies Without And Within."

Nimejitahidi kadri nilivyoweza kufanya tafsiri ya karibu kabisa kutoka Kiingereza kwenda Kiswahili. Ni vigumu kufanya tafsiri timilifu kwa asilimia 100 hasa pale mwandishi na mtafsiri ni watu wanaoongea lugha mbili tofauti. Ni rahisi kwa mtu aliyeandika mwenyewe kufanya tafsiri ya alichoandika kuliko kazi hiyo kufanywa na mtu mwingine.
* Idadi ya "followers" kwenye akaunti ya Mange kwa sasa ni watu milioni 1.8.






Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.