Showing posts with label MPAYUKAJI. Show all posts
Showing posts with label MPAYUKAJI. Show all posts

11 Dec 2011


Mmoja ya mabloga ninaowaheshimu,Bwana Nkwazi Mhango (pichani juu) amenishushia tuhuma nzito akidai nimepokea hongo ya mafisadi kama inavyoonekana kwenye baruapepe ifuatayo (BONYEZA PICHA KUIKUZA)

Kama hukuweza kuisoma vizuri basi nainukuu hapa chini


Anonymous has left a new comment on your post "Nova Kambota: VIVA KAMANDA LOWASSA":

Chahali umenisononesha. Umeingiwa na nini hadi unampamba huyu fisadi wa kunuka? Sikuamini kuona naweka shairi langu la kumjibu huyu mtoto changudoa wa maadili wa Lowassa na ukalifuta. Kweli binadamu si viumbe wa kuamini. Hata hii futa kwa maslahi yako. Ila jua legacy uliyokwisha ijenga ina thamani kuliko hiyo hongo ya mabaki ya ufisadi.
Nkwazi Mhango


Publish
Delete
Mark as spam

Moderate comments for this blog.

Posted by Anonymous to Kulikoni Ughaibuni at 11/12/2011 01:16


Lakini cha kusikitisha ni ukweli kwamba baruapepe yenye shairi la Mhango analodai nililifuta (kutokana na hongo ya mafisadi) lilinifikia masaa mawili na dakika 31 baada ya barua pepe ya lawama.Kama ulivyoona katika picha ya hapo juu,Mhango alinitumia braua pepe ya kwanza (ya lawama) saa 7 na dakika 11 usiku kwa muda wa hapa Uingereza (angalia kulia juu kwenye email utaona imeandikwa Sent: Sun 11/12/2011 01.17).

Sasa angalia picha ya email ya shairi la Mhango hapa chini (cha muhimuni ametuma muda gani)

Kama picha inavyoonyesha,shairi la Mhango lilitumwa saa 9 na dakika 48 usiku kwa saa za hapa kama inavvoonekana katika picha hapo juu (kulia juu kuna maandishi kuhusu muda ambapo inasomekana bayana Sent on 11/12/2011 03.48

Anyway,nimekuwa nikimheshimu sana Bwana Mhango (na mmoja wa ushuhuda wa heshima yangu kwake ni makala hii ya Januari MWAKA 2008 isemayo MPAYUKAJI MSEMAOVYO...AU MSEMAKWELI? (bonyeza link kuisoma)

Tangu nianze uandishi wa blogu na makala sijawahi kupata tuhuma nzito kama hizi.Kinachosikitisha zaidi ni ukweli kwamba Mhango anafahamu fika nimetoka wapi katika vita yangu ya jeshi la mtu mmoja (one-man army) dhidi ya ufisadi.Anafahamu pia masahibu yaliyonikumba kutokana na mapambano hayo.Kwa hakika ngepaswa kuwa mtu wa mwisho kabisa kusema hayo aliyosema.Lakini kama alivyoandika mwenyewe,KWELI BINADAMU SI VIUMBE WA KUWAAMINI.

Natumaini baada ya kubaini kuwa alikurupuka kunilaumu kabla ya kuangalia vema kama shairi lake limeshanifikia,atafanya uungwana wa kuniomba samahani.

3 Oct 2010




Blogu hii inapenda kutoa salamu za pongezi kwa mpambanaji na mwanaharakati mahiri,Mwalimu Nkwazi Mhango (a.k.a Mpayukaji Msemaovyo) mwenye makazi yake nchini Kanada kwa kutuletea mpambanaji mwingine wa kiume.Ujio wa mwanaharakati huyu mchanga unaweza kuwa dalili njema hasa kwa vile tupo kwenye mchakato wa kuwatimua mafisadi wanaofakamia keki ya taifa letu kama hawana akili nzuri.

Naungana na Mwalimu Nkwazi na familia yake kumtakia kijana wetu afya njema na kila mafanikio ili pindi muda utapowadia ajumuike nasi katika harakati zetu za kupigania usawa katika jamii.

27 Jul 2010


Mtunzi wa kitabu hiki maridhawa si mwingine bali ni mchambuzi na mwandishi mahiri wa makala,Mwalimu Nkwazi Nkuzi Mhango,Mtanzania mwenye makazi yake nchini Kanada.Licha ya ualimu na uandishi wa habari,Mhango pia ni mwanaharakati wa haki za binadamu.Miongoni mwa safu maarufu za Mwalimu Nkwazi (pichani chini) ni zile zinazopatikana katika gazeti la Tanzania Daima,ambapo hutumia jina la MPAYUKAJI MSEMAOVYO.Kadhalika,mwandishi huyu ni hodari katika fani ya kublogu,na "uwanja wake" unafahamika kama Free Thinking Unabii .Vilevile,unaweza kusoma makala za Mwalimu Nkwazi katika jarida la The African Executive
Usikose nakala ya kitabu hiki ambacho kinakuja wakati mwafaka kabisa kwa Watanzania waliochoshwa kuona nchi yao ikigeuzwa "shamba la bibi" na mafisadi wanaopita huku na huko "kuomba ridhaa yetu" warejee madarakani kutufisadi zaidi.

5 Jan 2010


Naomba kuiwasilisha kama ilivyo

Zitto Kabwe: Kumbikumbi huruka na kuliwa na kunguru

TAFAKURI

Mwanahalisi Toleo Na. 168

.
Na Nkwazi Mhango

ZITTO Kabwe mbunge wa Kigoma Kaskazini, amekiri kumpa magari matatu ofisa habari za zamani wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), David Kafulila.

Magari hayo anayatoa kama msaada kwa Kafulila ili aweze kushinda kampeni za ubunge katika jimbo la Kigoma Kusini. Hizi ni habari zinazozua maswali mengi, ikiwamo utajiri na uwezo wa Zitto kiuchumi.

Je, inakuwaje Zitto aweze kumiliki magari matatu wakati kipato chake kinajulikana? Lakini la pili, Kafulila na Zitto wanawezaje kuanza kampeni za ubunge wakati Tume ya Taifa ya Uchaguzi haijatangaza?

Tayari Zitto amekaririwa akisema, “Ni jambo la msingi kupunguza idadi ya wabunge wa CCM…ndiyo maana nimeamua kumsaidia Kafulila katika chama alichopo (NCCR-Mageuzi). Nipo tayari kujitolea kwa kijana mwingine anayegombea, hata kwa chama kingine, isipokuwa CCM.”

Kwa maneno ya Zitto ni kwamba anamuunga mkono Kafulila, ingawa bado anadai yuko CHADEMA. Ni ajabu kidogo. Je, kama CHADEMA wataamua kusimamisha mgombea Kigoma Kusini wakati Zitto ana mtu wake, atamuunga mkono nani kati ya mgombea wa chama anachodai kimemlea na kumkuza na kumfikisha hapo alipo na rafiki yake kipenzi?

Si vizuri kumsemea Zitto wala Kafulila. Kuna haja ya CHADEMA kuuliza swali hili kabla mambo hayajafika huko. Kwa sasa, Zitto ama kwa kujua au vinginevo, anaanza kujiona maarufu kuliko chama, kama Jakaya Kikwete-kwa mujibu wa maneno ya katibu mkuu wa CCM, Yusufu Makamba.

Ifahamike. Kumbikumbi akaribiapo mauti huotesha mbawa na kuruka na kuishia kuliwa na kunguru.

Inapofikia mtu akafikia kujiona bora kuliko chama, huyu bila shaka hakifai chama wala chama hakimfai. Na lazima kuna tatizo, tena kubwa tu. Hivyo, uwezekano wa kukitosa chama wakati mbaya, hasa ule wa uchaguzi, ni mkubwa. CHADEMA wasingoje kufika huko.
Siasa za Tanzania zina bahati mbaya. Chama kinamlea mtu hadi kufikia umaarufu kama alivyo Zitto Kabwe sasa. Halafu mtu huyu aliyefinyangwa na kulelewa na chama, analewa sifa kiasi cha kujiona bora kuliko chama.

Mwisho wake huwa mbaya kwa mhusika na chama. Daniel arap Moi wa Kenya alifikia hatua ya kulewa sifa hizi pale alipoitwa profesa wa siasa. Alifanya ubabe hadi akakikosesha dola chama chake cha KANU.

Kuna haya ya wanasiasa kuchagua kati ya chama na urafiki. Tumekuwa tukimshutumu Kikwete na CCM kwa kuendekeza urafiki na kujuana. Hata wapinzani wanamlaumu kwa hili, hasa kwa kusema anaendesha nchi “kishikaji.” Hili sina mjadala nao wala sitaki kuingia undani wake. Lakini CHADEMA waangalie wasitoe kibanzi kwenye jicho la mwenzao wakaacha boriti kwao.

Zitto kwa watu wa nje ya chama chake anaonekana kuwa mguu mmoja ndani na mwingine nje. Ushahidi ni shaka juu ya msimamo wake. Kwenye mkutano wa Opesheni Sangara kule Tanga watu wanataka kujua kama Zitto bado yumo chamani au la.

Ni rahisi mtu kukanusha, lakini ushahidi wa mazingira unaweza kupaaza sauti kuliko mwenye kukanusha. Ingawa Zitto anasisitiza kuwa yuko CHADEMA, matendo husema zaidi ya maneno matupu.

Inakuwaje Kafulila awe mali kuliko chama? Zitto anapaswa kubanwa ajibu swali hili kwa usahihi na majibu yanayoingia akilini siyo kupiga siasa. Je, kwa kumuunga mkono Kafulila, hata dhidi ya uamuzi wa CHADEMA, Zitto hadhihirishi asivyokubaliana na hukumu aliyopewa Kafulila?

Kama chama kilimuona Kafulila ana makosa na kikafuata taratibu zote za kumtimua, naye akaamua kujitoa na kutoa kashfa nyingi, maana yake ni kwamba kuna mgongano hata kama wahusika hawataki kulikubali hili.

Litakuwa jambo la ajabu kwa mtu wa cheo na elimu ya Zitto kutoliona hili. Wenzake wamekaa chini wakamtimua Kafulila na kutaja makosa yake-kuvujisha siri za CHADEMA.
Yeye bado anamtetea. Je, huku si kutetea madhambi yake au kuonyesha kuwa kipenzi chake kimeonewa? Kwanini asimtetee kwa namna inayoeleweka badala ya kuendelea kukidhoofisha chama?

Ifahamike. Tunaelekea kwenye uchaguzi mwakani. Kwa uzoefu wangu, wanasiasa nyemelezi watavitelekeza vyama vyao, hasa baada ya kuahidiwa vinono na CCM. Nani mara hii amesahau akina Masumbuko Lamwai, Tambwe Hiza, Walid Aman Kabourou, Shaib Akwilombe, Salum Msabaha na wengine wengi? Kwanini uone ubaya wa chama baada ya kutimuliwa?

Ingawa kuhama vyama ni haki ya wahusika, wengi wa wanasiasa, hasa waliojirejesha CCM baada ya kukosa ukuu kwenye vyama vyao, wameonyesha kuwa nyemelezi na “changudoa.”
Ukiwaondoa watu kama Wifred Rwakatare na wengine wachache, wengi wamedhihirisha wanavyosaka madaraka badala ya kutumikia umma. Wamejivua nguo hata kama baadhi yao wanapewa madaraka ya kufinyangwa kama ilivyo sasa ofisi ya propaganda ya CCM, ambayo imegeuka dampo la wanasiasa nyemelezi.

Hivyo basi, CHADEMA wangembana Zitto wajue msimamo wake kwamba ni nani hasa atamuunga mkono kati ya mgombea wa chama chake na rafiki yake Kafulila.
Ni heri CHADEMA wakamkosa Zitto mapema kuliko kuwachenga saa za mwisho. Huu si wakati wa kucheza pata potea.

Bado Zitto ni mdogo kisiasa na kiumri. Ubunge wa kipindi kimoja hauwezi kumfanya awe yote katika yote hadi kuwa maarufu kuliko chama. Na chama kinapozidiwa umaarufu na mtu mmoja, kama CCM, kijue kinaelekea kuzimu. Nisingetaka CHADEMA wafike huko ingawa dalili zinaonyesha ukomavu wa hali ya juu katika kuyakata mawimbi haya na majaribu makubwa.
Zitto kaamua kumuunga mkono Kafulila wazi wazi, hata kabla ya chama chake kuamua kumsimamisha mgombea Kigoma Kusini. Anajiona si mchezaji bali mwamuzi. Je, alitaka kujenga mtandao ndani ya chama ili baadaye apate madaraka?
Na ikumbukwe. Hii si mara ya kwanza kwa Kabwe kupimana misuli na chama. Nani amesahau mvutano uliotokea hivi karibuni kwenye uchaguzi wa mwenyekiti wa chama? Je, Kabwe anatingisha kiberiti kwa ajili ya kuchukua uamuzi katika chaguzi ujao?

Kwa makala zaidi kutoka kwa MPAYUKAJI tembelea blogu yake HAPA

4 Jan 2010


Je mama Kikwete ameanza kampeni kwa ajili ya mumewe?

na Nkwazi Mhango

Siku hizi mke wa rais, Salma Kikwete, anaonekana kwenye kurasa za mbele za magazeti karibu kila siku akiwa mikoani akihamasisha hili na lile. Wengi wanahoji. Kwanini sasa na si tangu mwanzo mume wake alipoingia ikulu? Na kwanini asiseme wazi kuwa anampigia kampeni mumewe? Maana, inajulikana alivyo mwana CCM damu damu tena mjumbe wa vikao vyake?

Watetezi wake wanaweza kusema anafanya kazi ya shirika lake lisilo la kiserikali la WAMA. Haiwezekani mumewe akawa mkuu wa serikali naye akawa na shirika lisilo la kiserikali kusiwe na mgongano wa kimaslahi kisheria. Uzoefu tulioupata toka kwa Anna Mkapa ungetosha kumsaidia rais Jakaya Kikwete kuondokana na aina hii ya ufisadi sugu na unyemelezi kwa kutumia mgongo wa ikulu kama angekuwa ni mtu wa kujifunza na kudhamiria kutenda haki kwa taifa.

Ngo yake ni ya mashaka-kwanini ianzishwe baada ya mumewe kuwa rais? Kuanzisha NGO baada ya mume kuwa rais ni ishara tosha ya ufisadi na usasi wa ngawira. Mbona hatuoni wake wa viongozi wa vyama vingine wakiwa na NGOs? Hata wakiwa nazo nani atazichangia iwapo wanaochangia NGOs za wake wa marais wanatafuta kuwa karibu na ikulu ili waihujumu nchi kwa kupata upendeleo kama ilivyokuwa kwa EOTF ambayo ilitumiwa na watu wengi kuliibia taifa? Mke wa Kaisari hapaswi kutenda tendo lenye kuweza kutia shaka au doa utawala wa mumewe.

Tuliishi na kumuona baba wa taifa Mwalimu Julius Nyerere. Mkewe-mama Maria-hakuwahi kujihusisha na upuuzi mdogo mdogo wa kutafuta pesa kwa mgongo wa mumewe.

Niliwahi kuwaandikia barua EOTF na WAMA kuwaonya juu ya hatari ya kuitumia ikulu. Hawakuwahi kunijibu zaidi ya kufumba macho na kuendelea kutengeneza pesa kwa mgogo wa ikulu. Ila nafurahi. WAMA wamefanya jambo moja (la maana la kuondoa aibu)-kuondoa maneno yasemayo WAMA Foundation the office of the First Lady of the United Republic of Tanzania kwenye wavuti wao. Niliandika baruapepe ifuatayo kwa WAMA tarehe 3 Septemba 09:

Kama mzalendo, nimejaribu kukusanya baadhi ya maoni kuhusiana jinsi ufisadi unavyoingia ikulu kiasi cha kututatiza. Kwa sasa Anna Mkapa mke wa rais wa zamani na mumwe wako msambweni. Ukiangalia kinachofanywa na WAMA hakina tofauti na Fursa sawa kwa Wote (Wake za wakubwa).
Kuondoa aibu, nimejitolea kuwasiliana nanyi ili angalau mjue tunavyojihisi kwenye wimbi hili la ufisadi wa kutumia madaraka ya waume zenu. Mama Salma NGO yako ni ulaji mtupu kusema ukweli. Acha kuna kesho. Ni uamuzi wako kuamua. Kuna kesho wakati madaraka yatakuwa mikononi mwa wengine. Hasa nikizingatia kilichompata Regina Chiluba ambacho kinapaswa kumpata hata Anna Mkapa, nimeona bora niseme hata kama nitapuuziwa. Ila najua ujumbe utafika. Someni alama za nyakati na mjue kuwa madaraka yana mwisho na yanalevya. Kuna siku mtakumbuka mchango huu.
Kila la heri,

Bahati mbaya sana , hata wavuti wa Kurungenzi ya habari Ikulu unaonekana kutangaza biashara ya WAMA badala ya wizara za serikali! Ajabu hakuna anayestuka wala kupiga kelele!

Kama umma ukishupaa NGO hii inaweza kufutwa hata na mahakama kutokana na mgongano wa maslahi ukiachia mbali kuwa kichaka cha ufisadi kutokana na uwezekano wa kuchangiwa pesa chafu kutokana na kutokuwapo sheria makini ya kuchuja na kutangaza wafadhili wa WAMA.

Hata hivyo nimefarijika kuwa sauti yangu imesikika na fedheha imeondoka. Maana neno Jamhuri ya Muungano, kisheria, halipaswi kutumiwa na mtu au taasisi yoyote isipokuwa mihimili mitatu ya dola yaani Bunge, Mahakama na Utawala. Cheo cha Ofisi ya First lady hakimo katika katiba yetu.

Kwanini mapenzi kwa wanawake na watoto yaanze baada ya kuupata urais kama siyo gea ya kuitumia vibaya ikulu? Ina maana rais na washauri wake hawalioni hili au wameridhia kwa sababu NGO ya mke wa rais inaweza kutumika kama kivuli cha kuanza kampeni hata kabla ya tume kutanganza hivyo? Inabidi tustuke. Ajabu hata wapinzani hawajaliona hili!

Tanzania inaweza kuwa nchi pekee ambapo rais na mkewe wote ni marais. Kikwete ni rais wa jamhuri huku mkewe akiwa rais wa WAMA. Ukitaka kujua hili jikumbushe mapokezi anayopewa na coverage anayopata Salma kwenye vyombo vya habari. Ajabu ukitafuta uhalali wake kikatiba haupo!

Hata kama anajulikana kwa ubabe na upayukaji wake, bado mke wa rais wa Kenya Lucy Kibaki hana mamlaka kama aliyo nayo Salma ambaye anaweza kuingia mkoa wowote kwa kisingizio cha NGO yake na kufanya shughuli za kisiasa kama kulakiwa na viongozi wa mikoa na kukagua miradi ya maendeleo ukiachia mbali kutoa kauli mbiu zinazoonyesha wazi kumpigia debe mumewe.

Salma anchomzidi Lucy ni ile hali ya kufanya kitu waitacho waingereza one woman show. Kwani kila lilipo jina WAMA yupo yeye. Hii maana yake ni kwamba yeye ni dikteta na mpenda madaraka anayetaka kufanya kila kitu peke yake. Kwanini hatuoni makamu wake au hata wasaidizi wengine wakifanya shughuli za WAMA kama kweli ni ya umma kama anavyodai? Kuthitibitisha hili, tembelea tovuti ya WAMA uone ukweli huu. Hii haiwezi ikawa taasisi ya wanawake na watoto wa Tanzania .

Kuonyesha kuna namna ya kampeni na kutumia mamlaka ya mume wake, hivi karibuni, Mama Kikwete amewahi kutoa namba yake ya simu ya mkononi ambayo ni 0754-294450 kwa wanawake mkoani Singida ili waweze kumpigia au kumtumia ujumbe mfupi wa maneno pindi waume zao watakapowanyanyasa kutokana na kitendo cha wao kwenda kupima kwaajili ya kujua afya zao. Japo kwa juu hili linaweza kuonekana ni jambo bora, kwa mtu anayejua mipaka ya mamlaka yake na utaratibu wa utawala kisheria, angeshauri wahusika waelekeze madai yao kunakohusika-polisi, vituo vya kutetea haki za binadamu hata wizarani.
Licha ya kuwa ubabe, hii ni kampeni ya wazi kuonyesha wahusika wanawajali wananchi jambo ambalo si kweli. Kwanini hasira zake zisielekezwe kwenye kumshauri mumewe kupambana na ufisadi kama ana uchungu na nchi hii? Yaani hajui kuwa ujinga na umaskini ndivyo vyanzo vya haya yote? Sijui hata kwenye kupokea misaada anauliza usafi wa mtoaji.

Kwa nijuavyo upenzi wa sifa wa watawala wetu na watu wao, kama utafanyika uchunguzi huru juu ya matumizi ya MAWA, ushingae pesa inayotumiwa kwenye ziara ikawa kubwa kuliko hiyo inayowafikia walengwa. Bahati mbaya sijwahi kusoma popote taarifa ya mahesabu ya mwaka ya si WAMA wala EOTF.

Wengi wanaweza kuona kama tunamuandama mke wa rais au kutotambua umuhimu wa kupigania haki za akina mama. Kwanini mke wa rais wakati tuna wizara yenye watendaji wanaolipwa pesa ya kodi yetu? Kwanini misaada hiyo anayopokea isipelekwe wizarani au kwenye mashirika huru kama kweli ana uchungu na walengwa na si kujipatia umaarufu, pesa na kubwa zaidi kutumia ikulu kwa manufaa binafsi yawe yake au mumewe na marafiki zake?

Je Salma Kikwete ameanza kampeni kwa ajili ya mumewe hata kabla ya kipenga kupulizwa? Je akina mama wa Tanzania wataingia mkenge wake huku waume na kaka zao wakizidi kuteswa na sera za Kikwete za kuvumilia mafisadi? Je atawalainisha wasahau kuwa Kikwete hajatimiza ahadi hata moja? Je watahoji uhalali wa NGO yake na kumwambia ukweli kuwa ni ya mashaka na ulaji?

16 Oct 2009


NDUGU YANGU Mpayukaji Msemaovyo anasema:

Naitwa Mchumiatumbo mwana wa Tapeli.

Ingawa wakati naandika waraka huu vijana wenzangu wapatao 166 wamo wakimenyeka toka Mwanza hadi Butiama, kama ishara ya kumbukizi ya safari yako adhimu ya ukombozi ukiliungua mkono marehemu azimio la Arusha, mimi sitafanya hivyo.

Nina sababu. Kwanza mimi ni mnafiki wala mjamaa kama wewe. Nina roho nyepesi hasa nionapo vitu kama pesa madaraka na sifa.

Mimi ni mbabaishaji na muongo; au msanii kama washikaji wasemavyo. Ni fisadi through and through. Ninanuka kiasi cha kutostahili hata kukaribia kaburi lako achia mbali nyumba yako, wanao, mkeo, watu wako hata taifa lako. Nisingependa walevi na wazinzi kufagia makaburi ya mitume mwalimu. Hivyo, kwanza nakuwa mkweli kwa nafsi yangu na kwako na umma wako.

Tatu, nitaunga mkono azimio lipi iwapo ninaoona wamenizunguka wakiwaibia watu wako ni wale wale walioliua azimio la Arusha? Nitaadhimisha vipi iwapo miiko ya uongozi na usawa wa binadamu vimetoweka na nafasi yake kuchukuliwa na ufisadi, ujambazi wa mchana, ubabaishaji na uongo?

Nne, mwalimu, sitaki kujidanganya na kukudanganya. Kile ulichopigania kwa sasa hakuna. Ulipigania uhuru na maendeleo. Sasa kuna utumwa na kuporomoka. Ulitekeleza ujamaa na kujitegemea. Sasa tuna uhujumaa na kujimegea. Ulipigania mstakabali wa nchi toka kwa wakoloni wawe wavumbuzi, wamisionari na watawala. Sasa mstakabali huo umo mikononi mwa wawekezaji, na wafadhili wa makuadi wao. Ulipigania ardhi ya Tanzania kabla haijaingia mikononi mwa vijifalme vya kifamilia. Nitakuenzi kwa udhu upi iwapo kila nipitapo Loliondo nakaribishwa kwenye falme za kiarabu utadhani hapa ni uarabuni?

Nitapata wapi mshipa wa kukuenzi wakati nakung’ong’a? Je mwalimu una habari? Yale madini uliyosema vizazi vijavyo vingeyaendeleza na kufaidika nayo yaliuzwa na jamaa yako Tunituni uliyempigia debe usijue jizi.

Tano, mwalimu siwezi kukuenzi wakati nakuchukia na kukudharau. Ningekupenda na kukuheshimu ningeshika urithi wako na kuheshimu wosia wako wa kupendana na kutohujumiana. Nakumbuka wakati ukianga dunia ulikuwa ukiwalilia watanzania wako baada ya kugundua makosa uliyofanya kuwaweka mikononi mwa nunda wala watu. Nami ni mmojawapo.

Je una habari mkoani mwako watu wameishamiminiwa risasi za moto kutokana na kukatiza kwenye ardhi ya mwekezaji na si mtanzania? Una habari mkoani mwako uchafuzi wa mazingira unatishia maisha ya ndugu zako? Hapa kweli nina sababu ya kukuenzi? Je kukuenzi ni matendo au maneno mwalimu?

Ingawa ukiwa kuzimu bado unaliletea sifa taifa langu, sifichi wala kuchelea kukwambia kuwa waliohai wanaliletea aibu na fedheha baada ya kulibinafsisha huku wakibinafsisha hata akili na roho zao. Mwalimu nilikufahamu sana . Ulikaa madarakani kwa kitambo kirefu ukiacha nyuma familia isiyo na ukwasi zaidi ya utu. Uliowawezesha wamefikia hata kuchukua ule mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira uliozawadiwa na rafiki yako Mao Tse Tung.

Mwalimu, vinyamna mwitu na mbwa hawa walitutenda kweli. Walitudanganya kuwa uwekezaji ndiyo sera na njia pekee ya kutukomboa tusijue walikuwa wakimaanisha kinyume. Wengine walituahidi maisha bora kwa wote tusijue wote ni wao washirika zao, watoto zao na wake zao hata nyumba ndogo zao. Tupo msambweni mwalimu wakati huu tunapozidi kuuzana na kuhadaana. Je unaweza kuamini kuwa kwa sasa hakuna tofauti ya polisi na kibaka? Nina ushahidi. Juzi polisi aliuawa kama kibaka na wananchi wenye hasira na kukata tamaa huku polisi tena wakubwa wakiwapiga risasi wafanyabiashara wakidai ni vibaka!

Wakati wa uongozi wako matupinkele au zeruzeru kwa lugha rahisi walikuwa salama. Baada ya kuingia pepo la utajiri usioulizwa ulivyopatikana, maskini hawa wanatolewa kafara na wanganga njaa wa kienyeji. Hivyo ndugu zetu hawa wanauawa hata zaidi ya swala mwalimu na hawana mtetezi zaidi ya vijikesi viwili vitatu vya kuondolea lawama. Tembo kwa sasa wana ulinzi madhubuti zaidi ya ndugu hawa.

Zama zako uliongoza. Uongozi ulikuwa utumishi wa umma na si uchumia tumbo na utumikishaji na uhujumu wa umma. Ikulu ilikuwa mahali patakatifu siyo pa deal. Uongozi ulikuwa uongozi na si uongo kama sasa. Siasa ilikuwa baraka si balaa kama sasa.

Wale watoto wa wachunga mbuzi na maskini wa kunuka uliowatoa kwenye umaskini na kuwasomesha sasa ni matajiri wa kutupwa. Yupo mpumbavu mmoja jizi aliyewahi kuita shilingi bilioni moja vijisenti ukiachia mbali wengine uliowaachia laana kuwa walikuwa wamejilimbikizia chumo la wizi. Na kweli maneno yako hayakuanguka. Kwani wezi wenzao waliwabeba na kuwakweza hatimaye tamaa zao na upofu vikawadondosha.

Mwalimu sitakuenzi,. Siwezi kujidanganya na kuidanganya dunia. Nitakuenzije iwapo kipato changu kinatokana na rushwa, uwekezaji, uuzaji mihadarati, uongo, ahadi hewa, uhujumu na mengine mengi yapinganayo na dhamira ya dira yako mwalimu?

Hivi kweli panya anaweza kumuenzi paka zaidi ya kufaidi ‘uhuru’ baada ya paka kuondoka? Je nune aweza kuishi nje ya kinyesi cha ng’ombe zizini? Si haki nune kuwa mwalimu wa usafi wakati mlo wake na makazi yake ni kwenye uchafu hata anenepe na kunawiri vipi.

Mwalimu naogopa kuja Butiama au kusimama mbele ya kadamnasi ya maadhimisho yako na kukupamba wakati nilisha kuvua nguo. Naogopa. Maana mama Maria hata wanao wananijua. Inawezekana nikakulamba uchogo na kukupaka mafuta kwa mgongo wa chupa kiasi cha kumkera mmojawapo akaamua kunizodoa na nikazidi kudhalilika ingawa niliishadhalilika muda mrefu.

Mwalimu ulikuwa na akili inayochemka. Yangu mimi ni bongolala. Ulikuwa msafi na mwadilifu. Mie ni mchafu sina mfano. Mkeo hakuwa akitumia ofisi yako kuubia umma. Mie wangu nami wote tu wezi. Nikiiba huku yeye anaibia kule. Hata watoto nimewaingiza. Nataka hata ikibidi wawe marais kama siyo mawaziri. Je hapa mwalimu nitakuwa na cha kukuenzi?

Mwalimu ulileta elimu bure kwa wote. Mie nashabikia kuchangia gharama ingawa kimsingi hakuna gharama za kuchangia zaidi ya kutunisha mfuko wa walaji wakubwa. Ulipigania ardhi. Mie natamani niwe rais niiuzie mbali nipate changu nifiche ughaibuni. Mwalimu ulichukia wafanya biashara wezi. Mie hawa ndiyo washitili wangu.

Mwalimu ulisisitiza usawa wa binadamu. Mie naamini binadamu si sawa wala si mfano wa Mungu kama wachungaji wasemavyo. Usawa ni mambo ya kizamani. Kwangu, heshima ya binadamu haitokani na ubinadamu wake bali pochi lake. Hukusikia wahenga wakisema mwalimu kuwa aso kitu si mtu bali kinyama mwitu? Mtu chake bwana. Kwa imani yangu mie si mfano wa Mungu bali mfano wa shetani kutokana na uroho na roho mbaya vyangu. Mungu si mwizi wala muongo wala mbabaishaji kama mimi mwalimu.

18 Jan 2008


Nimekuwa mwandishi wa makala magazetini tangu mwaka 1998,takriban miaka 10 sasa.Mtu aliyenipa changamoto la kufanya hivyo anaitwa Albert Memba,mwandishi wa zamani wa habari za michezo katika gazeti la Nipashe na Guardian.Huyu jamaa anaimudu lugha vilivyo.Nilianzaia kwenye magazeti "ya udaku" kama Sanifu (lilifariki zamani hizo) na baadaye Kasheshe na Komesha,ambako nilikuwa naandika unajimu "wa kuchekesha usio na chembe ya ukweli" (tuuite humorous horoscope) kwa kutumia jina la uandishi Ustaadh Bonge (hadi leo baadhi ya rafiki zangu wanaendelea kuniita hivyo).Baadaye nikamahimia kwenye uandishi wa makala za mambo muhimu zaidi ya vichekesho na udaku.Anyway,ni hadithi ndefu.

Nilipata wazo la ku-blog katikati ya mwaka juzi.Nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sintampongeza Ndesanjo Macha,kwani mwongozo wake wa namna ya kuanzisha blogu ndio ulionifanya niwe hapa nilipo.Wazo la kuanzisha blog hii lilitokana na ukweli kwamba gazeti lililokuwa linatoa makala zangu halikuwa na tovuti,hivyo awali blog hii ilikuwa kwa ajili ya kuwawezesha watu wote wanaojua Kiswahili popote walipo duniani wapate fursa ya kusoma makala hizo ambazo hazikuwa mtandaoni.Baadaye nikatanua wigo wa uandishi wa makala kwa kuanza kuandika kwenye magazeti ya Mtanzania na Raia Mwema ambako makala zangu hutoka mara moja kwa wiki.

Mmmoja ya watu waliosaidia sana kuitangaza blog ni hii ni rafiki yangu Haki Ngowi.Huyu hana hiana linapokuja suala la kupromoti blog ya bloga mwenzie.Nakumbuka waungwana flani waliwahi "kunitosa" nilipowatumia ombi la kubadilishana vinganishi (exchange links) kwa vile sikuwa naendana na maudhui ya blog yao.Nawashukuru kwani walinipa changamoto kubwa sana.

Mie ni muumini wa msemo "beauty should never be imprisoned",kitu kizuri shurti kisifiwe.Lakini mpewa sifa asibweteke bali anapaswa kuendeleza jitihada (sio kwa ajili ya kupata sifa zaidi) bali kuhalalisha kwamba waliompa sifa hapo awali hawakuwa "wanampaka mafuta kwa mgongo wa chupa",au kwa lugha ya mtaani, hawakuwa "wanamzuga".Nawashukuru nyote mnaonitumia barua-pepe za pongezi kuhusu makala zinazotoka kwenye magazeti nayoandikia pamona na zile zinazotoka kwenye blog hii.Nyie ndio chachu ya ya mafanikio ya makala hizo.

Nina tabia moja ambayo imenitengenezra marafiki na maadui wengi,nayo ni kusema ukweli.Huwa sioni aibu kukiri kwamba nimejifunza kitu flani kutoka mahala flani,kama ambavyo huwa sioni dhambi kumkosoa mtu naedhani amekosea jambo flani.Huko nyuma nilishawahi kuingia kwenye mgogoro na kampuni flani ya magazeti kwa vile tu niliwakosoa pale nilipoona wamepotoka.Tofauti na matarajio yangu,waungwana hao wakaanza kuhoji kuhusu maendeleo yangu ya elimu.Binafsi,huwa sipendi kabisa majadiliano kuhusu masuala ya shule yangu kwani naamini ni suala binafsi (only exception,ni pale majadiliano hayo yanapokuwa ya kitaaluma).

Kuna bloga anaitwa Mpayukaji Msemaovyo.Laiti kungekuwa na mashindano ya kutafuta blogu zenye "kiwango cha juu cha uchungu kwa nchi" basi naamini Mpayukaji angekamata nafasi ya juu kabisa.Simsifii kwa vile tu napenda anachaondika,bali ni ukweli kwamba blog yake imekuwa ni darasa zuri kwangu kujifunza "uchungu kwa nchi yangu na mapambano dhidi ya ufisadi na mafisadi".Uzuri wa makala za Mpayukaji,ambazo hupatikana pia kwenye gazeti la Tanzania Daima,ni ile tabia yake ya kuliita jiwe ni jiwe na sio tofali (calling a spade a spade).Unajua,kuna kusifia kitu kwa matarajio ya kupewa asante flani (kitu ambacho nakipinga kwa nguvu zote) na kuna kusifia kitu kwa vile kina kila sababu ya kusifiwa,na hicho ndicho nachokifanya hapa.Kuna wakati huwa nasoma makala za Mpayukaji huko Tanzania Daima mpaka najikuta naijiwa na taswira ya nyuso za mafisadi zinavyokunjamana kwa hasira iliyochanganyika na aibu+maumivu (truth pains) kutokana na uzito wa hoja za Mpayukaji.

Nitaendelea kuwapongeza waandishi na bloggers wengine ambao wanawatumia Watanzania kwa upenyo huu "mpya" uliojitokeza (mtandao) kuwasilisha vilio,kero,manung'uniko,lawama na hata pongezi kuhusu taifa letu.Pia nitaendela kuwapongeza wenzetu wanaotuletea habari kwa njia ya picha kwani taswira (image) inaweza kuwakilisha maneno elfu kadhaa kwa wakati mmoja.

(Picha ya Mpayukaji nimeipata kutoka kwenye profile ya blogu yake pasipo idhini yake,nitaomba idhini baadaye).

Almanusura nisahau.Hivi huko nyumbani watoto wangapi wanaoamua kutoroka majumbani kwao kutokana na sababu moja au nyingine?Je kuna mahauzigeli wangapi wanaoamua kutoroka kwa waajiri wao kutokana na manyanyaso yaliyopita kiasi?Katika mfumo ambao mnyonge licha ya kutokuwa na haki ananyang'anywa hata ile haki ndogo aliyozaliwa nayo (utu),kundi hili linabaki kuwa halina mtetezi.Clip hii ya Ludacris ft Mary J. Blidge katika wimbo Runaway Love inaweza kutukumbusha wajibu wetu kama jamii


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.