Showing posts with label RAIA MWEMA. Show all posts
Showing posts with label RAIA MWEMA. Show all posts

3 Jan 2017



Kuna msemo wa kisiasa unaosema "in politics, perception is reality." Maana yake katika tafsiri isiyo rasmi ya Kiswahili ni kwamba 'katika siasa, kitu kinavyoonekana ni sawa na uhalisi wake. 

Kwa mantiki hiyo, kura ya maoni iliyobandikwa na gazeti la Raia Mwema katika akaunti yake kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter ikiwa na swali kama linavyoonekana katika 'tweet' husika hapa chini, inaweza kuwa na uzito.

Ndio, siyo kura ya kisayansi lakini idadi ya watu 448 'waliopiga kura' (hadi wakati ninaandaa makala hii) ni sampuli ya kutosha kwa kura ya maoni. 
Natambua makada wa CCM hawatopendezwa na makala hii, na huenda kuna watakaohoji kwanini niipe uzito kura ya maoni ya Twitter. Jibu langu ni hilo kwenye sentensi ya kwanza, "in politics, perception is reality." Lowassa kuongoza katika kura hiyo ya maoni kunajenga perception flani ambayo kwenye siasa ni reality. 

Neno la tahadhari kuhusu kura hiyo ya maoni ni kwamba bado inaendelea na haijafikia tamati. Kwahiyo, matokeo ya mwisho yanaweza kuwa tofauti, hasa ikzingatiwa kuwa tofauti ya asilimia ni kiduchu.

Pengine moja ya vitu vinavyompunguzia umaarufu Rais Magufuli ni baadhi ya kauli zake...kama hii hapa pichani chini. Ikumbukwe kuwa moja ya sifa ya uongozi bora ni pamoja na kutumia lugha isiyojenga picha ya dharau au kukosa huruma kwa wananchi. Na tukiamini kuwa 'in politics, perception is reality,' basi picha hasi inayoweza kutokana na baadhi ya kauli za Rais Magufuli zaweza kujenga taswira hasi kumhusu yeye na uongozi wake, hata kama hatamki kwa nia mbaya.




29 Dec 2016


ATIMAYE mwaka 2016 unafikia ukingoni ambapo siku nne zijazo tutaingia mwaka mpya 2017. Makala hii inafanya tathmini ya jumla ya matukio makubwa zaidi, hususan ya kisiasa, kitaifa na kimataifa.
Tukio kubwa zaidi kimataifa ni kuyumba kwa itikadi ya siasa za kiliberali katika nchi za Magharibi, suala lililokwenda sambamba na kukua kwa siasa za mrengo mkali wa kulia. Kadhalika, nchi kadhaa za Magharibi zinaendelea kushuhudia ujio wa zama mpya za siasa, zinazojulikana kama ‘post-truth,’ ambazo kwa tafsiri fupi ni ‘kupigia chapuo uongo, na upinzani dhidi ya ukweli.’
Ni katika mazingira hayo, kulijitokeza mshtuko mkubwa katika nchi hizi za Magharibi, na pengine duniani kwa ujumla, pale Uingereza ilipoamua kujitoa kwenye Umoja wa Ulaya (EU) katika kura ya maoni iliyofanyika mwezi Juni. Kampeni za kura hiyo zilijenga msingi imara wa siasa za ‘post-truth.’
Miezi mitano baadaye, Marekani nayo ilikumbwa na wimbi hilo la siasa za ‘post-truth,’ pale mfanyabiashara bilionea, Donald Trump, aliyekuwa na kila sifa mbaya ya kumnyima japo ‘ujumbe wa nyumba kumi,’ alifanikiwa kumbwaga mwanasiasa mkongwe, Hillary Clinton. Trump na wafuasi wake walitumia kila aina ya hadaa huku wakisaidiwa na mlipuko wa habari zisizo za kweli hususan katika mitandao ya kijamii.
Kinachotisha kuhusu zama hizi za siasa za ‘post-truth’ ni ukweli kwamba zimekumbatiwa na vyama vya siasa na vikundi vyenye mrengo mkali kabisa wa kulia, pamoja na vyama/vikundi vya kibaguzi.
Kinachoendelea kusaidia ‘uongo kuwa muhimu kuliko ukweli’ ni ukweli kwamba tabaka la siasa, tabaka la uongozi, tabaka la wanataaluma na wataalamu, tabaka la wafanyabiashara, na makundi kama hayo, yanaangaliwa kama yaliyoweka pamba masikioni. Hayasikii vilio vya tabaka la watu wa chini, na hata wakisikia hawafanyii kazi vilio hivyo.
Ndio maana, watu ‘hatari’ kama vile Nigel Farage wa hapa Uingereza, Donald Trump huko Marekani, Marine Le Pen wa Ufaransa, Norbert Hofer wa Austria (ambaye almanusura ashinde urais wa nchi hiyo), Geert Wilders wa Uholanzi, Frauke Petry wa Ujerumani na kadhalika, wamemudu kutumia uongo na hadaa kwa ufanisi kutokana na ‘ukweli’ kupoteza maana yake.
Mashambulizi ya kigaidi huko Ufaransa, Ubelgiji na Ujerumani na kuendelea kuwepo kwa tishio la vitendo hivyo kumeongeza umaarufu wa siasa za mrengo mkali wa kulia ambazo zinahusisha ugaidi na sera za ukarimu kwa wahamiaji.
Mwaka 2017 unatarajiwa kushuhudia michuano mikali ya kisiasa barani Ulaya ambapo nchi zinazotupiwa jicho zaidi ni Ufaransa na Ujerumani zinazokabiliwa na hatari ya kuwa chini ya utawala wa wanasiasa wenye mrengo mkali kabisa wa kulia.
Kwa huko nyumbani, tishio kubwa halikuwa kwenye siasa bali ajali zinazoendelea kugharimu maisha ya Watanzania kwa idadi kubwa, japo janga hilo halionekani kuwasumbua wananchi na viongozi.
Kwenye ulingo wa siasa, Rais ‘mpya’ Dk. John Magufuli ndiye aliyetawala zaidi katika anga za siasa. Kwa upande mmoja, hali hiyo ilitokana na matumaini makubwa waliyonayo wananchi kwake, na kwa upande mwingine, udhaifu unaozidi kukua miongoni mwa vyama vya upinzani.
Hata hivyo, kwa kulinganisha kasi aliyoanza nayo na hali ilivyo sasa, yayumkinika kusema kuwa ‘kasi ya Magufuli imepungua.’ Huku ‘tumbua majipu’ ikizidi kuwa ya msimu (na baadhi ya utumbuaji ukituhumiwa kufanywa kutokana na majungu), sera iliyowapa matumaini makubwa, ya kuanzishwa kwa mahakama maalumu ya ufisadi iliyogeuka kuwa kichekesho ambapo tangu mahakama hiyo ianzishwe imeendesha kesi moja tu.
Na kituko kikubwa zaidi ni pale waziri mwenye dhamana ya mahakama hiyo, Dk. Harrison Mwakyembe, alipotuhadaa kuwa uchache wa kesi katika mahakama hiyo ni dalili ya mafanikio, yaani ufisadi umepungua.
Lakini kama kuna suala ambalo baadhi yetu tunapata shida mno kumwelewa Rais Magufuli ni ‘kutengeneza maadui wasio wa lazima.’ Hatua za kuzuia mikutano na maandamano ya vyama vya upinzani na kukatisha matangazo mubashara ya vikao vya Bunge ni hatua ambazo sio tu hazikuwa na tija bali hazikuwa na umuhimu wowote.
Matumizi ya sheria ya makosa ya mtandao pale tu rais anapotukanwa, huku maelfu kwa maelfu ya Watanzania wakiendelea kuwa waathirika wa matusi imetufanya baadhi ya ‘tulioupigia debe’ muswada wa kuanzisha sheria hiyo tujilaumu.
Jinsi serikali ilivyowatimua wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kana kwamba walijichagua wenyewe kujiunga na masomo, na kuwakashifu kuwa ni ‘vilaza,’ uamuzi wa kutishia ajira za mahakimu wasio na shahada za chuo kikuu, kupuuza jitihada za Rais (mstaafu) Jakaya Kikwete za kuwashawishi Watanzania wa Diaspora kushiriki katika harakati za maendeleo huko nyumbani na badala yake ‘kuwaharamisha’ kwa kuwazuia kumiliki ardhi, na hatua kama hizo, ni baadhi ya mambo yaliyotawala zaidi mwaka huu katika siasa za Tanzania.
Hata hivyo, Serikali ya Awamu ya Tano imefanikiwa kurejesha nidhamu ya kazi, angalau kwa kujenga mwamko wa wananchi kutegemea kipato halali badala ya shughuli zilizo kinyume cha sheria. Na japo matukio ya ujambazi yameendelea kutawala, kumekuwa na dalili nzuri ya kupungua biashara ya dawa za kulevya na ujangili. Na kama tetesi kuhusu uwezekano wa mabadiliko ya baraza la mawaziri hivi karibuni ni za kweli, basi huenda ‘timu mpya’ ikaufanya mwaka ujao kuwa ‘mwema’ zaidi kwa Watanzania.
Nimalizie makala hii kwa kuahidi kuwaletea ubashiri wa mwenendo wa mambo mbalimbali kwa mwaka kesho katika makala ijayo.
Nawatakia heri ya mwaka mpya 2017

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali 

22 Dec 2016

Aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Maradhi ya Binadamu (NIMR), Dk. Mwele Malecela.
IJUMAA iliyopita, kulijitokeza tukio ambalo hadi wakati ninaandika makala hii limezua utata. Usiku wa siku hiyo, Rais Dk. John Magufuli alitengua wadhifa wa aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Maradhi ya Binadamu (NIMR), Dk. Mwele Malecela.
Siku moja kabla, Dk. Mwele alizungumza na waandishi wa habari kuwaeleza kuhusu matokeo ya utafiti wa takriban mwaka mzima kati ya NIMR na Chuo Kikuu cha Bugando kuhusu ugonjwa huo na ilibainika kuwa kati ya sampuli za damu 533, 88 zilikutwa na virusi vya ugonjwa wa zika.
Hata hivyo, siku iliyofuata, serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto ilitoa taarifa kuwa ugonjwa huo haujaingia nchini, kana kwamba taarifa ya Dk. Mwele ilizungumzia kuingia kwa ugonjwa huo.
Pengine kabla ya kuingia kwa undani katika kujadili suala hili, ni vema niweke bayana ukweli kuwa Dk. Mwele ni dada-rafiki yangu, na nimesikitishwa sana na tukio hilo, hususan jinsi wadhifa wake ulivyotenguliwa.
Ni kwamba, wakati taarifa ya wadhifa wake kutenguliwa ilitolewa usiku wa Ijumaa iliyopita, saa chache baadaye, Jumamosi asubuhi, kukatangazwa uteuzi wa Profesa Yunus Mgaya kuchukua wadhifa ulioachwa wazi na Dk. Mwele.
Kama nilivyoeleza awali, hadi wakati ninaandika makala hii kuna utata unaoendelea kuhusu suala hilo. Hiyo imetokana na vitu kadhaa. Kwanza, taarifa ya Ikulu kuhusu uamuzi wa Rais Magufuli kutengua ukurugenzi wa Dk. Mwele haikueleza kwa nini rais alichukua uamuzi huo, tena usiku.
Kadhalika, utata huo unachangiwa na hisia kuwa huenda ‘siku za Dk. Mwele zilikuwa zinahesabika,’ kwani katika mazingira ya kawaida, sio rahisi mkurugenzi wa taasisi nyeti kama NIMR kuondolewa madarakani usiku kisha mbadala wake akapatikana asubuhi.
Hisia hizo zinachangiwa pia na ukweli kuwa Dk. Mwele ni mtoto wa Waziri Mkuu wa zamani, mzee John Malecela. Miezi minane iliyopita, familia ya mwanasiasa huyo mkongwe ilikumbwa na ‘balaa’ kama hili, ambapo Rais Magufuli alimwondoa madarakani mke wa mzee Malecela, mama Anne Kilango, aliyekuwa mkuu wa Mkoa wa Shinyanga.
Tofauti na wadhifa wa Dk. Mwele ulivyotenguliwa bila maelezo, tukio la mama Kilango liliambatana na maelezo kwamba alitangaza kwenye vyombo vya habari kuwa mkoa wake hauna watumishi hewa jambo ambalo lilisababisha Ikulu kufanya uchunguzi wake na kubaini wafanyakazi hewa 45 katika awamu ya kwanza huku awamu ya pili ya uchunguzi bado ukiendelea.
Katika mazingira ya kawaida, huwezi kumlaumu mtu anayeweza kuhoji “tatizo lilikuwa utendaji kazi wa mama Kilango na Dk. Mwele au ‘mlengwa’ ni mzee Malecela?”
Wasomi kadhaa waliozungumzia hatua ya rais dhidi ya Dk. Mwele wameonyesha kushangazwa kwao, hasa ikizingatiwa kuwa rais naye ni miongoni mwa wasomi. Kwamba, alichofanya Dk. Mwele ni kuripoti tu matokeo ya utafiti husika, lakini kukajitokeza mkanganyiko katika tafsiri ya ripoti ya matokeo hayo.
Laiti busara ingetumika, basi Dk. Mwele angefahamishwa tu kuwa taarifa yake imezua mkanganyiko, na angeitisha mkutano na waandishi wa habari kutoa ufafanuzi. Ikumbukwe kuwa dada huyo ni mmoja wa wanasayansi wachache kabisa kutoka Afrika na hususan Tanzania wanaoheshimika mno kimataifa.
Japo sijapata idhini yake ‘kutoa siri hii,’ mwishoni mwa mwaka jana alinieleza kuwa anahitajiwa na taasisi moja ya kimataifa inayohusiana na masuala ya afya duniani, lakini akasema hayupo tayari kuacha kuwatumikia Watanzania wenzake. Binafsi nilimshauri akubali tu nafasi hiyo kwa vile atakapoitumikia dunia, atakuwa akiitumikia Tanzania pia. Hata hivyo, Dk. Mwele alikataa nafasi hiyo.
Vile vile, baada ya jina lake kutopitishwa kuwania kuteuliwa katika nafasi ya urais kwa tiketi ya CCM mwaka jana, Dk. Mwele alielekeza nguvu zake kumuunga mkono mgombea aliyepitishwa, Dk. Magufuli na kila jioni alitumia muda wake baada ya kazi kufanya ‘majukumu ya kisomi’ katika kampeni za chama chake. Na licha ya kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, baadhi ya vijana aliowakabidhi majukumu ya kampeni za Dk. Magufuli hawajalipwa stahili zao hadi leo (licha ya Dk. Mwele kufuatilia suala hilo kwa zaidi ya mwaka sasa). Linganisha hilo na makada ‘waliozawadiwa’ nafasi mbalimbali licha ya kampeni zao ndani au nje ya chama dhidi ya Dk. Magufuli alipokuwa mgombea.
Mwaka jana nilipata fursa ya kuandika wasifu wake kwenye blogu yangu. Pamoja na mengineyo mengi, alieleza kuwa tangu alipokuwa binti mdogo alikuwa na ndoto ya kuwa mtafiti wa maradhi. Na licha ya kuwa mtoto wa waziri mkuu, ambapo alikuwa na fursa ya ‘kufanya chochote atakacho,’ alifuata ndoto yake ya kitaaluma na kitaalamu, akatumia muda mwingi ‘vichakani na misituni’ kujifunza kuhusu maradhi mbalimbali ya binadamu. Kwa hakika, safari yake tangu utotoni hadi kupata shahada ya uzamivu na hatimaye kuwa mkurugenzi mkuu wa kwanza wa kike wa NIMR, inatoa hamasa kubwa.
Kuna wanaoona kuvuliwa madaraka kwa Dk. Mwele ni kama mwendelezo wa kile kilichomkumba aliyekuwa Msajili wa Hazina, Lawrence Mafuru, ambaye kutenguliwa kwa wadhifa wake hivi karibuni kunatafsiriwa kama matokeo ya yeye kutoa maoni yake ya kitaalamu kuhusu suala fedha za taasisi za serikali kuwekwa kwenye akaunti za muda maalumu (fixed deposits).
Nihitimishe makala hii kwa kumpa pole Dk. Mwele huku nikiamini kuwa muda si mrefu ataipatia fahari Tanzania kama mwanasayansi wa kimataifa. Kadhalika, inasikitisha kuona tukio hili ilhali majuzi tumeshuhudia teuzi za baadhi ya mabalozi zikifanywa kwa kigezo cha ukada

8 Dec 2016


KESHOKUTWA, Desemba 9, Tanzania itatimiza miaka 55 tangu ipate uhuru. Siku hiyo hiyo, nami nitatimiza miaka kadhaa tangu nizaliwe. Naam, mimi na nchi yangu ‘tulizaliwa tarehe inayofanana’ japo katika miaka tofauti.
Nijiongelee mwenyewe kwanza. Wakati kwa watu wengi, siku zao za kuzaliwa huandamana na sherehe na chereko mbalimbali, maadhimisho ya siku yangu ya kuzaliwa huwa ni ibada – kumshukuru Mungu kwa kuniweka hai na baraka nyingine anazonijalia – na kufanya tafakuri ya wapi nimetoka, nilipo na ninapoelekea.
Moja ya mafanikio makubwa kwangu kwa mwaka huu ni uamuzi niliouchukua Aprili Mosi kuachana na moja ya tabia hatari kabisa maishani ya uvutaji wa sigara. Hadi nilipochukua uamuzi huo, tabia hiyo hatari kiafya na kiuchumi ilikuwa na ‘umri’ wa miaka ishirini na ushee.
Katika kusherehekea siku yangu ya kuzaliwa, nimeamua kugawa bure kitabu changu cha kielektroniki, kinachoitwa “Mwongozo wa Kitabibu wa Jinsi ya Kuacha Sigara na Ushauri wa Mvutaji Mstaafu.” Ni mwendelezo wa utamaduni mpya, ambapo zamani tulizoea kuona wanaosherehekea siku za kuzaliwa wakizawadiwa, lakini sasa namna maarufu ya kuadhimisha sherehe hiyo ni kutoa zawadi.

Hiyo ni kwa upande wangu. Sijui ‘mwenzangu’ Tanzania atakuwa na ‘zawadi’ gani ya kutupatia katika maadhimisho yake ya siku ya kuzaliwa. Hata hivyo, siku chache kabla ya siku hizo, kuna jambo moja ambalo linaonekana kugusa hisia za wengi. Nalo ni uteuzi wa mabalozi wapya ulifanywa na Rais Dk. John Magufuli wiki iliyopita.
Kwa mujibu wa baadhi ya vyombo vya habari, uteuzi wa makada waandamizi wa chama tawala CCM umetafsiriwa kuwa ni ‘hesabu za kisiasa.’ Sina hakika hesabu hizo zina malengo gani, lakini nahisi labda ni Magufuli analenga kujiimarisha katika uongozi wake kama Mwenyekiti wa Taifa wa CCM.
Kama hilo ni kweli, basi uteuzi huo wa makada sio habari njema kwetu sisi wenye matarajio ya kuona teuzi mbalimbali zikifanywa kulingana na uwezo wa kutekeleza majukumu au uchapakazi na sio ukada.
Pengine nitumie fursa hii kukumbusha kuwa kuna wimbi kubwa la mabadiliko linaloendelea duniani, hususan huku nchi za Magharibi. Muda mfupi kabla sijaanza kuandika makala hii, Austria imenusurika kuwa taifa la kwanza kurejea kuwa chini ya utawala wa mrengo mkali kabisa wa kulia. Hofu kuwa mgombea urais Norbert Hofer wa chama chenye mrengo mkali wa kulia cha Freedom Party angeshinda ilipotea baada ya mchakato wa kupiga kura kumalizika, na mgombea binafsi Alexander Van der Bellen kushinda kwa asilimia 53. Lakini muda mfupi baada ya habari hiyo njema kutoka Austria, mambo hayakwenda vizuri nchini Italia, ambapo Waziri Mkuu Matteo Renzi alishindwa kwenye kura ya maoni ya mabadiliko ya katiba ya nchi hiyo, na kulazimika kujiuzulu. Wapinzani wake katika kura hiyo walikuwa ni pamoja na chama chenye mrengo mkali wa kulia cha Northern League na kile cha upinzani wa tabaka tawala (anti-establishment) cha Five Star Movement (F5S).
Sasa macho yanaelekezwa huko Ufaransa na baadaye Ujerumani na Uholanzi ambako kwa nyakati tofauti watakabiliwa na kazi ya upigaji kura. Mtihani mkubwa katika nchi hizo ni jinsi ya kukabiliana na wimbi linalozidi kukua la upinzani dhidi ya tabaka tawala na mfumo wa utawala unaoonekana kutosikiliza sauti za wananchi wa kawaida. Kwa bahati mbaya, wimbi hilo lipo mikononi mwa vyama vya siasa za mrengo mkali wa kulia na vya kibaguzi.
Katika mazingira kama hayo tunahitaji mabalozi wanaoelewa kwa nini wametumwa kutuwakilisha huko nje, na sio wanaojua wameteuliwa kutokana na nafasi zao za kisiasa nchini.
Na wiki chache kabla ya maadhimisho ya miaka 55 ya uhuru wetu, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Serikali ya Mapinduzi Dk Mohammed Ali Shein alisaini sheria inayofanya masuala ya mafuta na gesi ya Zanzibar kuwa sio suala la Muungano, hatua ambayo ni uvunjifu wa Katiba mchana kweupe. Hilo limefanyika kwa vile Shein na SMZ wanajua hakuna mwanasiasa kutoka Bara mwenye jeuri ya kugusia suala hilo, ikiwa ni pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano, Dk. Magufuli.
Lakini pamoja na hayo, Tanzania yetu itasherehekea miaka 55 ya kuzaliwa kwake ikiwa nchi yenye amani, angalau amani kwa maana ya kutokuwa vitani au kwenye machafuko. Kazi kubwa kwa watawala wetu ni kutumia nguvu zao zote kuhakikisha kuwa amani hiyo inadumishwa kwa nguvu zote.
Happy birthday Tanzania.

24 Nov 2016


KAMA nilivyoahidi katika toleo lililopita la gazeti hili, wiki hii ninaendelea na uchambuzi kuhusu uchaguzi wa Rais wa Marekani uliofanyika wiki mbili zilizopita na kushuhudia mgombea wa chama cha Republican, Donald Trump, akiibuka mshindi dhidi ya mpinzani wake mkuu, Hillary Clinton wa Democrat.

Makala yangu katika toleo la wiki iliyopita ilibeba swali ‘je Trump atabadilika?” Swali hilo lilitokana na ukweli kwamba kauli za Trump na tabia yake kwa ujumla, kabla ya kuwa mgombea, akiwa katika mchakato wa chama chake kupata mgombea, na wakati wa kampeni kama mgombea wa chama chake, zilisheheni kasoro lukuki; ubaguzi dhahiri wa kidini, unyanyasaji wa wanawake na dhihaka kwa walemavu, kupandikiza chuki dhidi ya Wamarekani wasio weupe, chuki dhidi ya wageni, na mengineyo mengi yaliyoibua wachambuzi wa siasa kutodhani kuwa Trump angeweza kushinda katika uchaguzi huo.
Lakini tatizo halikuwa kwa Trump pekee bali pia watu waliomzunguka na baadhi ya makundi ya wafuasi wake. Moja ya kundi muhimu kwa ushindi wa bilionea huyo ni lile linalofahamika kama ‘alt-right’ (kifupi cha ‘alternative right’ yaani mbadala wa wahafidhina/wenye mrengo wa kulia). Kundi hili limekuwa ‘mwiba’ sio kwa waliberali pekee bali pia hata wahafidhina wenye msimamo wa wastani.
Na kundi hilo hatari ndilo analotoka mmoja wa wateule wa awali kabisa wa Trump, Steve Bannon, aliyeteuliwa kuwa mkuu wa mikakati wa Trump. Bannon alikuwa mmoja wa viongozi wa kampeni ya bilionea huyo na kabla ya hapo alikuwa mwenyekiti wa gazeti ‘hatari’ la mtandaoni, Breitbart. Gazeti hatari kwa sababu lengo lake kuu ni kuamsha hisia za makundi fulani kwa kubeza, kulaani na hata kutukana makundi kama vile Wamarekani weusi (gazeti hilo lilidai kuwa kiasili ni wahalifu), Walatino, wahamiaji, Waislam (gazeti hilo limewaita kila jina baya), watetezi wa haki za wanawake ikiwa pamoja na waathirika wa vitendo vya kubakwa, na takriban kila baya usilotarajia kuliona kwenye gazeti maarufu ambalo mwezi uliopita pekee, tovuti yake ilitembelewa na wasomaji zaidi ya milioni 19.
Kwa kumteua Bannon, ni wazi kuwa Trump ameamua kukumbatia makundi yaliyomuunga mkono hata kama yanajenga taswira isiyopendeza kwa urais wake. Tayari makundi mbalimbali ya utetezi wa haki za kiraia Marekani yanamtaka Trump kutengua uteuzi wa Bannon, mtu mwenye ajenda za kibaguzi na muumini wa ‘ukuu wa watu weupe’ (white supremacist).
Lakini taswira ya kuogofya kuhusu aina ya watu ambao Trump atawakumbatia katika urais wake haijaishia kwa Bannon pekee bali pia hata chaguo lake la mshauri wake wa masuala ya usalama wa taifa, Luteni Jenerali (mstaafu) Michael Flynn na Mwanasheria Mkuu, Seneta Jeff Sessions. Wakati Jenerali Flynn alitimuliwa na utawala wa Rais Barack Obama kutokana na kile kinachoelezwa kuwa kasoro za kiuongozi, Sessions ana tuhuma za ubaguzi wa rangi. Kadhalika, msimamo wa Jenerali huyo kuhusu masuala ya ugaidi wa kimataifa unaotajwa kuwa unaweza kuikosanisha Marekani na mataifa ya kiislamu kwa vile anaamini kuwa tatizo la ugaidi linachangiwa na Uislamu na sio magaidi kutumia kisingizio cha Uislamu kuhalalisha unyama wao.
Mteule mwingine wa Trump kushika nafasi ya ukuu wa shirika la ujasusi la nchi hiyo, CIA, Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi, Mike Pompeo, naye anatazamwa kama mtu anayeweza kulirejesha shirika hilo katika zama zake za hatari kabisa, hasa kutokana na msimamo wake mkali kupindukia kwenye masuala ya intelijensia na usalama. Ikumbukwe kuwa katika zama zake hatari, CIA ilishiriki katika operesheni chafu kama vile mauaji ya Rais wa zamani iliyokuwa Zaire, Patrice Lumumba.
Tukiweka kando dalili za awali za mwelekeo wa serikali ya Trump, tugeukie kwanza swali muhimu: “..kwa nini Hillary Clinton alishindwa na Trump.” Sababu zinaweza kuwa nyingi, lakini za muhimu zaidi ni pamoja na ukweli kwamba Hillary alikuwa mmoja wa wanasiasa wanaochukiwa mno Marekani, japo chuki dhidi yake ilikuwa pungufu kidogo kulinganisha na Trump.
Kadhalika, kasoro kubwa iliyomwandama Hillary ni kuonekana kama sio mwaminifu hususan kutokana na skandali iliyomwandama muda wote wa kampeni yake kuhusu matumizi ya ‘server’ binafsi kwa mawasiliano ya barua-pepe alipokuwa ‘Waziri wa Mambo ya Nje.’
Vile vile, Hillary alishindwa kuwa na kauli mbiu yenye kueleweka kirahisi, kulinganisha na mpinzani wake, Trump, ya ‘Ifanye Marekani jabali tena’ (Make America Great Again). Sambamba na hilo ni ukweli kwamba ilikuwa vigumu mno kwa Democrat kuendelea kuwa Ikulu baada ya miaka minane ya urais wa Barack Obama. Kwa Marekani, ni ngumu sana kwa chama kilichokuwa madarakani kwa mihula miwili mfululizo kushinda muhula wa tatu.
Kingine kilichomwangusha Hillary ni kuzidiwa kwa kura na Trump miongoni mwa Wamarekani weupe, hususan wale ambao hawana elimu ya chuo. Kuongeza majeraha zaidi, ngome zake kuu, yaani wanawake, Wamarekani weusi na Walatino hawakumpigia kura nyingi kama ilivyotarajiwa huku Trump naye akifanikiwa kupata kura za kutosha katika makundi hayo yaliyotarajiwa kumwangusha.
Pengine kubwa zaidi ni kilichotukumba sote tuliokuwa tunafuatilia kwa karibu uchaguzi huo. Ilionekana kama jambo lisilowezekana kwa Trump kushinda urais. Kauli zake zilikuwa chafu kupita maelezo, hasa ile aliyorekodiwa akiwatusi wanawake na kujigamba kuwa ‘ukiwa mtu maarufu wanawake wanakupapatikia,’ kashfa dhidi ya walemavu, wanawake, Waislamu na Walatino (aliowaita wabakaji), na kila neno chafu ambalo mgombea japo wa ukiranja shule ya msingi, achilia mbali urais wa Marekani, hakupaswa kuropoka.
Ni kwamba, katika mazingira ya kawaida, na kwa kuamini kuwa Wamarekani wana akili timamu, isingewezekana Trump kushinda uchaguzi huo. Na katika kutupatia matumaini zaidi, takriban kura zote za maoni (opinion polls) zilionyesha Hillary akiongoza kati ya asilimia mbili na 14. Japokuwa kulikuwa na tahadhari kuwa kura hizo za maoni zilikuwa na walakini, wengi wetu tuliamini kuwa suala sio iwapo Hillary angeshinda bali angeshinda kwa kiasi gani.
Na hii inaleta swali, kwa nini takriban kura zote za maoni ziliashiria kuwa Hillary angeshinda lakini ikawa kinyume chake? Hali kama hiyo ilitokea kwenye uchaguzi mkuu wa Uingereza, Mei mwaka jana na ikajirudia kwenye kura kuhusu Uingereza kubaki au kujitoa kwenye Umoja wa Ulaya. Katika kura zote hizo, matokeo yalikuwa tofauti kabisa na ubashiri wa kura za maoni.
Moja ya maelezo kuhusu ‘ubashiri fyongo’ wa kura za maoni, sio kwenye uchaguzi huo wa Marekani tu bali pia kwenye uchaguzi mkuu wa UK mwaka jana na kwenye kura ya ‘Brexit’ Juni mwaka huu, ni kile ambacho Profesa Timur Kuran wa Chuo Kikuu cha Harvard huko Marekani amekieleza katika kitabu chake ‘ukweli faraghani, uongo hadharani’ (Private Truths, Public Lies), katika kanuni (theory) yake inayojulikana kama ‘preference falsification.’ Kwa kifupi, kanuni hiyo inaeleza kuwa baadhi ya watu wanaohojiwa kwenye kura za maoni kuhusu masuala yanayogusa hisia za jamii hutoa majibu wanayoona yanaendana na ‘mtazamo wa jamii’ japo misimamo yao ni kinyume.
Kwa mfano, katika suala la Brexit, kwa kuzingatia kanuni ya Profesa, kulikuwa na hisia kuwa wanaotaka Uingereza ijitoe Umoja wa Ulaya ni wabaguzi wa rangi (racists). Kadhalika, kwa vile Trump alishatoa kauli kadhaa za kibaguzi na makundi mbalimbali ya kibaguzi kama vile KKK yalitangaza kumuunga mkono, ilijengeka picha kuwa ‘wafuasi wa Trump ni wabaguzi.’ Kwa hiyo, baadhi ya waliohojiwa kwa minajili ya opinion pools za Brexit na Trump ‘walibaki na ukweli wao faraghani na kuongea uongo hadharani,’ na katika mazingira hayo, uungwaji mkubwa kutaka UK ijitoe EU na hiyo ya Trmp miongoni mwa wapigakura haikuweza kuonekana kwa waendesha kura za maoni (pollsters).
Kwa upande mwingine, Hillary alikuwa mwathirika wa zama mpya za ‘siasa za uongo,’ wenyewe wanaita ‘post-truth politics,’ ambapo vitu muhimu kwenye mijadala na kampeni za kisiasa, kama vile ukweli na hoja za kitaalamu, vinazidiwa nguvu na kauli za uongo lakini za kugusa hisia na imani za watu. Kampeni ya Brexit hapa Uingereza ilitawaliwa na ‘post-truth politics’ na ikawezesha kambi iliyotaka Uingereza ijitoe ishinde kwenye kura ya maoni, na kwa mara nyingine tena imemwezesha Trump kushinda huko Marekani.
Kama nilivyoandika katika makala yangu kwenye toleo lililopita, tatizo la ‘post-truth politicis’ ni ‘waumini’ wa aina hiyo ya siasa. Takriban wote, angalau kwa kuangalia aina ya watu na vikundi vyao, ni waumini pia wa siasa za kibaguzi za mrengo mkali wa kulia.
Ndio, ‘post-truth politics, ni matokeo ya tabaka tawala, tabaka la wanasiasa, tabaka la wasomi na mfumo wa siasa, uchumi na jamii kushindwa kusikiliza vilio vya wananchi wa kawaida, lakini kwa bahati mbaya au makusudi, viongozi wa siasa hizo ni watu hatari zaidi ya viongozi waliopo kwenye mfumo tulionao sasa, angalau kwa nchi za Magharibi.
Je ‘post-truth politics,’ na ufanisi wake kwa Brexit na ushindi wa Trump ni vitu vinavyoweza kuenea kwa upana zaidi? Hilo ni suala la muda. Kipimo cha kwanza ni uchaguzi mkuu nchini Ufaransa Aprili hadi Juni mwakani, na kura ya maoni/chaguzi nchini Italia, Austria na Ujerumani.
Hata hivyo, baadhi ya wachambuzi wa kisiasa wanadai kuwa ‘siasa za umaarufu’ (populist politics) kama hizo za ‘post-truth’ zina ‘uhai’ (life-span) wa kati ya miaka mitano hadi saba tu. Kwa hiyo wanabashiri kuwa hazitodumu kwa muda mrefu, na pengine hiyo itazifanya zisisambae sehemu kubwa ya dunia.
Kwa huko nyumbani, na pengine Afrika kwa ujumla, ‘siasa za hadaa/uongo’ zimekuwa sehemu muhimu ya siasa zetu za kila siku. Tofauti na kinachojiri huku nchi za Magharibi ni kwamba siasa za uongo zinatumiwa na watu wanaotaka kuondoa mfumo uliopo madarakani ilhali kwa akina ‘siye’ siasa za aina hiyo ndio zimeweka mfumo uliopo madarakani.
Je ‘siasa za hadaa/uongo’ zinaweza kuung’oa mfumo uliowekwa madarakani kwa hadaa/uongo? Mwamuzi ni muda. Hata hivyo, ukweli kuwa kuna vuguvugu la kushinikiza mapinduzi dhidi ya mfumo ulioshindwa kuutumiakia umma unaweza kuwa chachu kwa nchi kama zetu kuwahamasisha kuwa ‘imetosha.’ Na kama Trump licha ya kasoro zake zote ameweza kushinda urais kwa kisingizio cha ‘kupigania haki za wanyonge dhidi ya mfumo uliowatelekeza,’ basi yayumkinika kuhisi kuwa hata akina sie tunaweza kukumbwa na hali hiyo, japo binafsi naona uwezekano huo ni mdogo kwa sasa.
Na pengine ‘post-truth politics’ na wimbi la kudai mapinduzi dhidi ya mfumo ulioshindwa kuhudumia umma vinaweza visiwe na matokeo bora kwa nchi zetu za Afrika kutokana na kushamiri rushwa, siasa za kujuana na uwezo wa mfumo uliopo madarakani kutumia kila aina ya nguvu kusambaratisha jitihada zozote za kuupinga.
Mwisho, moja ya athari tarajiwa za Trump – kama akiendelea na msimamo wake wa kibaguzi – ni pamoja na bara la Afrika kutokuwa kipaumbele cha sera za nje za Marekani, kama ambavyo yawezekana uadui kati ya Marekani na nchi za kiislamu kuzorota maradufu, hususan kutokana na imani fyongo ya Trump na baadhi ya wasaidizi wake kuuhusisha Uislam na ugaidi.
Nihitimishe makala hii kwa upande mmoja kuikumbusha CCM kuwa wimbo wa upinzani dhidi ya mfumo unaoonekana kuwapuuza wananchi wa kawaida unapamba moto, na kwa vile CCM ni sehemu ya mfumo ambao baadhi ya Watanzania wanaona umewatelekeza, basi ni muhimu kujirekebisha. Kwa upande mwingine, Brexit na urais wa Trump ni funzo kwa vyama vya upinzani kuwa kusimama upande wa waliochoshwa na mfumo unaowapuuza kunaweza kusaidia kuleta ushindi kwa chama/mfumo mbadala.
Nimalizie makala hii kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi huu katika toleo lijalo, kwa kuangalia athari za urais wa Trump duniani kwa ujumla hususan barani Afrika, kwa nini Hillary ameshindwa na kwa nini kura za maoni zilibashiri matokeo ya uchaguzi huo “ndivyo sivyo” na nini tunaweza kujifunza kutokana na uchaguzi huo

17 Nov 2016

JUMANNE iliyopita inaweza kuingia kwenye vitabu vya kumbukumbu mbaya kutokana na uchaguzi mkuu nchini Marekani ambao mshindi alikuwa mgombea wa chama cha kihafidhina cha Republican, Donald Trump.
Trump – mwongo wa waziwazi, mnyanyasaji wa wanawake, mzinzi, mbaguzi wa rangi, mbaguzi wa kidini na mwasisi wa harakati za kibaguzi dhidi ya uraia wa Rais wa sasa wa nchini hiyo, Barack Obama, alifanikiwa kumshinda mpinzani wake mkuu, mgombea wa chama cha Democrat, Hillary Clinton.
Kibaya zaidi ni kwamba mfumo fyongo wa uchaguzi wa rais wa nchi hiyo ulimwezesha Trump kuwa mshindi licha ya kupata kura pungufu (60,350,241) dhidi ya mpinzani wake Hillary (aliyepata kura 60, 981, 118). Kura hizo zilizopigwa siku ya uchaguzi hujulikana kama popular vote, lakini kura muhimu zaidi na zinazoamua mshindi wa uchaguzi ni zinazofahamika kama electoral votes. Mshindi hutakiwa kupata kura hizi 270 au zaidi.
Inabidi kuelezea kwa kifupi kuhusu mfumo huo unaokanganya. Kimsingi, Wamarekani hawamchagui Rais wao moja kwa moja, badala yake kila jimbo lina watu wanaofahamika kama electors (wachaguzi) ambao hukutana mwezi Desemba mara baada ya kura zilizopigwa na kila aliyejiandikisha kupiga kura Novemba 8 ya mwaka wa uchaguzi.
Kama tulivyoona kwenye matangazo ya runinga, kila jimbo lina idadi yake ya "wachaguzi." Na jumla ya wachaguzi hao kutoka majimbo yote 51 ya Marekani ni 538.
"Wachaguzi" hao nao huchaguliwa na vyama vyao. Kila chama kina kanuni zake za uchaguzi wa "wachaguzi" hao. Uchaguzi wao hufanyika kwa hatua mbili. Kwanza, chama huchagua orodha ya "wachaguzi watarajiwa" na pili, "wachaguzi halisi" huchaguliwa na wapigakura siku ya uchaguzi. Majina ya wanaogombea kuwa “wachaguzi" yanaweza kuonekana katika karatasi ya kura au yasionekane, kutegemea kanuni husika.
Hakuna sheria inayowabana "wachaguzi" kumpigia kura mgombea aliyeshinda popular vote. Na ni katika mazingira haya ndio maana kumekuwa na jitihada za kuwashawishi "wachaguzi" hao kutompigia kura Trump, ili kumkwamisha na hatimaye kumwezesha Hillary achaguliwe. Hata hivyo, uwezekano wa hilo kutokea ni mdogo. Kihistoria, asilimia 99 ya "wachaguzi" hupiga kura kwa mshindi wa "popular vote."
Kila jimbo lina "ikulu" yake (state capitol), na hapo ndipo "wachaguzi" kutoka kila jimbo hukutana Desemba kupiga kura zao. Masanduku ya kura walizopiga hufunguliwa mwezi Januari katika kikao cha "Baraza la Wawakilishi".
Iwapo katika matokeo kutakuwa hakuna mgombea mwenye kura nyingi, au wagombea wawili watakuwa na kura sawa, Baraza la Wawakilishi litamchagua Rais miongoni mwa wagombea watano wenye kura nyingi zaidi.
Kila jimbo hupewa "kura za wachaguzi" (electoral votes) kulingana na jumla ya maseneta na wawakilishi. Kiwango cha chini kwa kila jimbo ni kura tatu. Majimbo makubwa huwa na kura nyingi kwa vile uwakikishi katika Baraza la Wawakilishi hutegemea idadi ya wakazi katika jimbo husika.
Tukirejea kwenye matokeo ya uchaguzi, Trump alipata kura za “wachaguzi” 290 huku Hillary akiambulia 228. “Wachaguzi” katika kila jimbo watakutana Desemba 17 kupiga kura zao, huku matarajio makubwa yakiwa wataheshimu jinsi wingi wa kura za “wachaguzi” alizoshinda Trump.
Kwa hiyo japo kinadharia kuna uwezekano wa “wachaguzi” hao kuamua kumnyima kura Trump na badala yake kumpa kura hizo Hillary, hali itakayosababisha matokeo ya uchaguzi huo kubadilika, uwezekano huo kiuhalisi ni mdogo mno.
Tathmini ya uchaguzi huo inahitaji zaidi ya makala moja, na katika makala hii nitagusia mambo muhimu kwa kifupi tu kwa matarajio ya kuendeleza mada hii katika makala zijazo.
Ushindi wa Trump umetokana na nini? Nchi za Magharibi zinapitia zama mpya ya siasa inayofahamika kama “post-truth politics.” Hii ni aina ya siasa inayotawaliwa na hisia na ushawishi kuliko ukweli au hoja za kitaalamu. Aina hii mpya ya siasa ilikuwa na ufanisi sana hapa Uingereza, katika kampeni za kura ya kuamua iwapo nchi hii iendelee kuwa mwanachama wa Umoja wa Ulaya (EU) au ijitoe. Wanasiasa wa kambi iliyotaka Uingereza ijitoe walishutumiwa mara kadhaa kwa kutumia takwimu za uongo na kujenga hoja za chuki dhidi ya wageni na EU kwa ujumla, huku wakipinga kwa nguvu zote takwimu za kitaalam zilizoonyesha bayana madhara ya nchi hii kujitoa EU.
Tulipopiga kura Juni 23 mwaka huu, kambi hiyo iliyotumia hadaa na hoja za chuki ndiyo iliyoibuka mshindi, japo tayari nchi hii inashuhudia kipindi kigumu kiuchumi kama ambavyo wataalamu mbalimbali walivyoonya wakati wa kampeni.
Ukweli (facts) una sehemu tukufu katika siasa za kidemokrasia za Magharibi. Kila wakati demokrasia ilipokwenda mrama, kila ilipotokea wapigakura kufanyiwa ulaghai au wanasiasa kukwepa maswali, tulikimbilia kwenye ukweli kama mkombozi.
Lakini kwa sasa, ukweli unaonekana kupoteza nafasi yake katika kujenga mwafaka. Tovuti ya kutofautisha ukweli na uongo ya PolitiFact ilibaini kuwa takriban asilimia 70 ya hoja za Donald Trump ziliangukia makundi ya “karibu na uongo” “uongo” and “uongo kabisa." Lakini hiyo haikumzuia kushinda urais wa Marekani
Kadiri siasa zinavyozidi kuwa za uhasama na kutawaliwa na ufanisi wa wahusika kwenye nyenzo za teknolojia kama vile runinga na mitandao ya kijamii, "afya" ya ukweli (facts) kwenye mijadala na midahalo inakuwa tete. Matarajio ya wasikilizaji, watazamaji na wasomaji yanaelemea zaidi kwenye ushawishi wa mtoa hoja hata kama hoja hizo ni za uongo wa waziwazi.
Taratibu, nafasi ya wajuzi, wasomi, wazoefu na makundi mengine tuliyozoea kuyaamini kutupatia mwongozo sahihi inazidi kudidimia na mbadala wake ni hoja za kugusa hisia za watu hata kama zinapanda mbegu za mfarakano, kutumia uongo hata pale unapoonekana waziwazi ilimradi tu unaweza kuvutia kuungwa mkono na sehemu ya hadhira, kupandikiza hasira ili kuipa nguvu hadhira kuchukua hatua hata kama zinapanda athari na kwa ujumla, kutotoa fursa kwa ukweli (facts).
Aina hii mpya ya siasa ni hatari, sio tu kwa sababu unafanya ukweli kuwa uongo na uongo kuwa ukweli, bali pia kwa vile imetokea kuwa chaguo mwafaka la wanasiasa waumini wa siasa za mrengo mkali wa kulia; wabaguzi wa rangi, wabaguzi wa kidini; na viumbe hatari kama hao.
Nitazungumzia zaidi mada hii siku nyingine.
Kwa upande mwingine, ushindi wa kambi iliyotaka Uingereza ijitoe EU (licha ya hoja zao za uongo na kupandikiza chuki) na ushindi wa Trump huko Marekani ni ujio wa mapinduzi ya kimfumo; upinzani wa umma dhidi ya tabaka la wanasiasa, wasomi na taasisi za kisiasa na uchumi. Hii ingepaswa kuwa habari njema lakini tatizo ni kwamba wanaoendesha kampeni ya mapinduzi haya ni wanasiasa hatari kabisa katika nchi zao na kimataifa.
Ushindi wa Trump umepokelewa kwa shangwe kubwa na viongozi wa vyama vya kisiasa vya kibaguzi na vyenye mrengo mkali wa kulia, kama Marine LePen wa Ufaransa, Victor Orban wa Hungary, Frauke Petry wa Ujerumani, Heinz-Christian Strache wa Austria na Geert Wilders wa Uholanzi. Na kwa hapa Uingereza, mwasisi wa harakati za nchi hii kujitoa EU, Nigel Farage, amekuwa mwanasiasa wa kwanza wa nchi hii kukutana na Rais-Mteule, Donald Trump.
Kwa hali ilivyo Marekani hivi sasa ambapo kuna maandamano mbalimbali ya kupinga ushindi wa Trump, mustakabali utategemea zaidi jinsi kiongozi huyo atakavyomudu kubadilika na kuwa kiongozi wa Wamarekani wote na sio kundi la Wamarekani weupe wasio na elimu ya chuo, Wakristo wenye msimamo mkali, na magenge ya wabaguzi wa rangi kama vile kundi la Klu Klux Klan (KKK) pekee.
Je, Trump atabadilika? Kwa jinsi ambavyo kila kitu kuhusu Trump ni vigumu kukibashiri kwa ufasaha (mwenyewe anasema kutotabirika ni siri ya mafanikio), jibu fupi ni kwamba; “…hakuna ajuaye isipokuwa Trump mwenyewe.” Jibu refu ni kwamba awali kauli zake kuwa atachukua mazuri na kuacha mabaya ya mpango wa bima ya afya ya jamii ujulikanao kama Obamacare (ambao Trump aliahidi kuufuta mara moja wakati wa kampeni) ziliashiria dalili za mabadiliko.
Pia taarifa kuwa amezitoa hofu nchi za Japan na Korea Kusini kuhusu msaada wa kijeshi wa Marekani kwa nchi hizo, zilileta dalili ya matumaini kwamba huenda ameanza kubadilika. Japan inakabiliwa na tishio kutoka China, na Korea Kusini inakabiliwa na tishio kutoka Korea Kaskazini, na Jeshi la Marekani ni ngao muhimu kwa mataifa hayo.
Vile vile, tovuti ya kampeni za uchaguzi ya Trump iliondoa tamko lake la kuwazuia Waislamu kuingia nchini humo pindi akishinda urais. Hatua hiyo Ilitafsiriwa kuwa ni dalili za ‘msema ovyo’ huyo kulegeza msimamo.
Hata hivyo, tayari Trump ameeleza kuwa ataanza utekelezaji wa dhamira yake ya kuwatimua wahamiaji haramu wanaokadiriwa kuwa zaidi ya milioni 11 nchini humo, ambapo ametangaza kuwa ataanza kuwatimua ‘wageni haramu’ milioni tatu mara tu baada ya kuapishwa.
Nihitimishe makala hii kwa kugusia vitu viwili. Kwanza, kushamiri kwa wimbi la “post-truth politics” na “mapinduzi dhidi ya tabaka la wanasiasa, wataalam au taasisi za siasa na uchumi” hasa kwa vile mwezi ujao, Italia itakuwa na kura ya maoni kuhusu katiba za nchi hiyo na Austria itakuwa na uchaguzi mkuu, Uholanzi itakuwa na uchaguzi wa bunge mwezi Machi mwakani, Ufaransa itakuwa na uchaguzi mkuu Aprili hadi Juni mwakani, na Ujerumani itakuwa na uchaguzi wa wabunge mwezi Septemba mwakani. Mataifa yote hayo yanakabiliwa na vuguvugu kubwa la upinzani dhidi ya Umoja wa Ulaya na chuki dhidi ya wageni, pamoja na “post-truth politics.”
Pili, moja ya makundi yaliyomsaidia sana Trump kushinda urais ni linalofahamika kama ‘alt-right.’ Kwa lugha rahisi, hawa ni zaidi ya wahafidhina. Ni wabaguzi wa rangi na dini, wapinzani wa harakati za wanawake na wanaosherehesha unyanyasaji wa wanawake, na kwa kifupi, “watu waliofanikiwa kuhamasisha kuwahadaa watafiti wa kura za maoni kuhusu nafasi ya Trump katika uchaguzi wa rais Marekani.”
Nimalizie makala hii kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi huu katika toleo lijalo, kwa kuangalia athari za urais wa Trump duniani kwa ujumla hususan barani Afrika, kwa nini Hillary ameshindwa na kwa nini kura za maoni zilibashiri matokeo ya uchaguzi huo “ndivyo sivyo” na nini tunaweza kujifunza kutokana na uchaguzi huo.
ITAENDELEA TOLEO LIJALO


3 Nov 2016


JUMAMOSI wiki hii, Rais Dk. John Magufuli atatimiza mwaka mmoja kamili tangu aingie madarakani kama Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kufanya tathmini ya tangu Magufuli atangaze nia ya kuwania urais kwa tiketi ya CCM, na hatimaye kuchaguliwa kuwa mgombea wake, kabla ya kushinda uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka jana na kuapishwa, kabla ya kuanza jukumu zito la kuiongoza nchi yetu, ni kitu kinachohitaji kitabu kizima.
Bahati nzuri, huko nyuma niliandika kitabu kuhusu ‘safari’ hiyo ya Dk Magufuli, japo tathmini iliisha kwenye takriban miezi mitatu tangu aingie rasmi madarakani. Wakati huu, ninaandaa kitabu kitakachochambua mwaka mzima wa kiongozi huyo tangu aingie madarakani.
Hata hivyo, hata bila kutumia kitabu, yawezekana kufanya muhtasari wa tathmini ya kipindi cha mwaka mmoja wa Magufuli na serikali yake ya Awamu ya Tano kwa ujumla. Na njia nyepesi ya kufanya tathmini hiyo ni kuangalia maeneo tunayoweza kuyaita mafanikio na yale yasiyo mafanikio.
Katika mafanikio, Rais Magufuli amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kutimiza ahadi alizotoa binafsi kama mgombea wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu na zilizotolewa na chama chake katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM. Moja ya ahadi hizo ilikuwa mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi. Katika eneo hili, Rais Magufuli amefanikiwa mno.
Kwa vile tayari Magufuli na serikali yake wameonyesha kuwa mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi ni kitu kinachowezekana, ni rahisi kwa baadhi ya watu kuona kuwezekana huko ni suala la kawaida tu. Ni rahisi pia kusahau ugumu uliotawala suala hilo kwa miaka kadhaa, kiasi kwamba baadhi ya tafiti kuhusu maoni ya wananchi kuhusu rushwa na ufisadi zilionyesha kuwa idadi kubwa tu ya wananchi “walishasalimu amri” kwa rushwa na ufisadi kuwa ndio hatima yao. Kwamba hata zifanyike jitihada za aina gani, rushwa na ufisadi vitaendelea kushamiri.
Kwa hiyo, licha ya kupambana na vitendo vya rushwa na ufisadi, Dk. Magufuli amekuwa akipambana na mfumo pia ulitoa mizizi kwenye saikolojia ya taifa letu. Kwa mafanikio yaliyokwishapatikana hadi muda huu, huku tukisubiri kuanza rasmi kwa mahakama ya ufisadi, kwa hakika Magufuli anastahili pongezi.
Ndio, kuna changamoto kadhaa kwenye sekta mbalimbali kama vile afya na elimu, lakini ni muhimu kufahamu kuwa ili tuwe na ufanisi kwenye sekta mbalimbali ni lazima kwanza tujenge nidhamu ya mapato na matumizi, sambamba na kubana mianya ya rushwa na ufisadi, ambayo kimsingi ndio iliyodidimiza sekta hizo. Sasa, kama ambavyo maradhi huingia mwilini na pengine kusambaa kwa kasi lakini huchukua kitambo kuyatibu, ndivyo ambavyo tunahitaji ustahimilivu kabla ya jitihada za Magufuli hazijaanza kuonekana kwa wingi na kwa wazi zaidi zikileta mabadiliko katika maeneo mbalimbali.
Eneo jingine ambalo Magufuli amefanikiwa ni kurejesha heshima ya kazi. Kwa muda mrefu, kulikuwa na imani fyongo kwamba ‘uhalifu unalipa’ (crime pays) na wenzetu waliofanya bidii kwenye kazi halali au kujiajiri kwa biashara au kilimo walionekana kama vituko. Lakini sasa tunashuhudia wimbi kubwa la wenzetu wakiwekeza kwenye kilimo na shughuli nyingine za kujiingizia kipato halali. Kadhalika, imani kwamba mtu anaweza kuishi kwa kutegemea kipato halali imeanza kurejea kwa kasi. Hili nalo si jambo dogo kwa sababu sio tu linahusu mfumo bali pia saikolojia ya taifa.
Awali nilikuwa miongoni mwa wasiopendezwa na jinsi Serikali ya Magufuli ilivyoonekana kuvibana vyama vya upinzani. Na katika kuthibitisha hilo, niliandika makala moja kuishauri serikali kuhusu suala hilo. Hata hivyo, nilichokishuhudia tangu wakati huo hadi sasa, kinaweza kuhalalisha umuhimu wa serikali kuchukua msimamo mkali dhidi ya baadhi ya vyama vya siasa au wafuasi wa vyama hivyo.
Sawa, kila mwananchi ana haki ya kumkosoa rais au serikali yake. Hata hivyo, kuna kukosoa kwa ajili ya kujenga na kukosoa kwa ajili ya kubomoa. Kwa makusudi, baadhi ya Watanzania wenzetu huko kwenye upinzani, pengine kutokana na kukosa ajenda yoyote kwa maendeleo ya vyama vyao, wamewekeza nguvu kubwa mno kuchochea chuki kwa wananchi dhidi ya serikali yao.
Kwa vile hatupaswi kutoa fursa yoyote ile ya kuruhusu uvunjifu wa amani, hasa katika kipindi hiki ambapo serikali ya Magufuli inafanya jitihada kubwa za kuiweka Tanzania yetu katika mahali inapostahili kuwepo, ninaunga mkono hatua za serikali dhidi ya yeyote anayejaribu kuchochea uvunjifu wa amani. Demokrasia ya kuchochea wananchi dhidi ya serikali yao ni uhuni. Watanzania wanahitaji maendeleo na sio kuwachonganisha na serikali yao.
Kama kuna eneo ambalo ninaweza kumkosoa Rais Magufuli ni kuhusu baadhi ya watu aliowakabidhi dhamana ya kumsaidia. Awali alieleza kuwa angeunda baraza la mawaziri dogo tu lenye ufanisi na atakayevurunda atawajibishwa. Nina hakika rais anawafahamu vema baadhi ya mawaziri ‘mizigo’ ambao wana kila dalili ya kumchafua kwa wananchi. Naam, wakiboronga wao, atakayelaumiwa ni aliyewateua. Ingekuwa vema rais akitumia maadhimisho haya ya mwaka mmoja madarakani kutathmini utendaji wa baadhi ya mawaziri wake na wale walioshindwa kuendana na kasi yake, wapumzishwe.
Sambamba na hilo ni doa la kisiasa huko Zanzibar linaloendelea kuchafua sura ya Tanzania. Wakati ni Wazanzibari wenyewe wanaoweza kufikia mwafaka wa kudumu wa mgogoro wa muda mrefu wa kisiasa visiwani humo, kuna haja kubwa tu kwa Serikali ya Muungano ‘kutomwagia petroli kwenye moto,’ kwa maana ya kujiepusha na kauli ambazo zinaweza kuchochea mfarakano zaidi visiwani humo.
Nimalizie makala hii kwa kukupongeza Rais Magufuli kwa kutimiza mwaka mmoja tangu uapishwe kuwa rais wetu. Wengi wanaokupinga au kukulaumu ni watu waliozoea kula vya bure, waliovuna wasichopanda, waliofakamia keki ya taifa kifisadi, watu ambao zama za Ujamaa tuliwaita kupe. Endelea kukaza uzi ili mabadiliko unayokusudia na yanayohitajiwa mno na Watanzania yatimie. Asante kwa kuanzisha safari ya Tanzania yetu kuelekea mahali inapostahili kuwa na kamwe usiyumbishwe na wanaotaka kutukwaza.

13 Oct 2016

NIANZE makala hii kwa kueleza masikitiko yangu kutokana na tukio lililoripotiwa wiki iliyopita ambapo walimu wanafunzi kadhaa walionekana katika video wakimwadhibu mwanafunzi katika namna isiyofaa na isiyokubalika kabisa. Laiti mtu akiiona video husika bila ya maelezo anaweza kudhani mwanafunzi aliyekuwa akipigwa na walimu hao wanafunzi alikuwa mwizi.
Pamoja na kukerwa mno na kitendo hicho, sikushangazwa na suala zima la vurugu (violence) dhidi ya mwanafunzi husika. Sikushangazwa kwa sababu jamii yetu imekuwa ikisherehesha vurugu. Ni mara ngapi tumeshuhudia polisi wetu wakitumia nguvu nyingi zaidi hata pale ambapo busara tu ingetosha? Ni watumishi wa nyumbani wangapi ambapo tulichokishuhudia kwenye video husika ndio maisha yao ya kila siku, kwa maana ya unyanyasaji wanaofanyiwa na waajiri wao na hawana sehemu ya kukimbilia?
Na je, ni watoto wangapi – hususan watoto wa kambo – ambao kila siku ya maisha yao ni zaidi ya unyanyasaji aliofanyiwa mwanafunzi wa kwenye video husika? Je, ni Watanzania wenzetu wangapi ambao ulemavu wao wa ngozi yaani ualbino umekuwa chanzo cha wao kuwindwa, kukatwa viungo na kuuawa? Na wazee wetu wangapi wameuawa katika mikoa ya Kanda ya Ziwa kwa vile tu wana macho mekundu (imani fyongo kuwa ni dalili ya ushirikina)?
Na kuhusu vurugu shuleni, kama hilo tukio la walimu hao wanafunzi, sheria za nchi zimehalalisha vurugu kwa kuendelea kuruhusu adhabu za kikoloni kama hiyo ya viboko. Tatizo letu ni kuamini zaidi katika adhabu badala ya kukarabati tabia. Angalia magereza zetu zilivyojaa vibaka na wezi wa kuku badala ya kuwapa kifungo cha nje na kuweka mkazo katika kuwageuza kuwa raia wema.
Tukio hilo sio tu liifumbue macho serikali kuhusu umuhimu wa mitandao ya kijamii katika kutuhabarisha yale ambayo pengine vyombo vyetu vya habari vya asili visingeweza kuripoti (na hili ni angalizo kwa Rais Dk John Magufuli kuhusu matamanio yake kuona malaika wakishuka na kuifunga mitandao ya kijamii) bali pia liiamshe kuhusu suala la viboko shuleni. Adhabu ya viboko imepitwa na wakati, ni kandamizi, ni mwendelezo wa vurugu dhidi ya watoto na si ya kistaarabu.
Baada ya kuzungumzia suala hilo la kipigo cha walimu hao kwa mwanafunzi, nigusie mada ya wiki hii ambayo pia inahusu elimu. Mwishoni mwa mwezi uliopita, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipiga marufuku wanafunzi kwenda shuleni pekupeku au na nguo zilizochanika.
Alitoa maagizo hayo katika ziara yake mjini Kibiti, Pwani wakati akizungumza na wananchi wa eneo hilo kwenye mkutano wa hadhara. Waziri Mkuu alisema;  “Zile fedha mlizokuwa mnatumia kulipa ada na michango sasa zitumieni kununua sare na chakula cha watoto wenu, ni marufuku mtoto kwenda shule huku akipekua au akiwa amevaa sare zilizochanika,”
Hivi kweli Majaliwa anadhani wazazi wa watoto wanaokwenda shuleni wakiwa pekupeku au na nguo zilizochanika wanafanya hivyo kama ‘fasheni’ ya suti za waheshimiwa wetu? Hivi kweli Majaliwa hajui kuwa ni umasikini wa kupindukia unaosababisha baadhi ya Watanzania wenzetu kutomudu uwezo wa kuwanunulia watoto wao viatu na sare nzuri?
Moja ya masuala yaliyonikera sana katika miaka 10 ya Awamu ya Nne ni pale viongozi wakuu wa serikali, Rais na Waziri Mkuu wake, wakieleza bayana kuwa hawajui kwa nini Tanzania ni masikini. Lakini angalau wao, licha ya kutoelewa chanzo cha umasikini wetu, hawakuja na amri ya kushangaza kama hiyo ya Majaliwa.
Pamoja na heshima kubwa niliyonayo kwa Waziri Mkuu wetu, ninaomba kutofautiana naye kuhusu amri hiyo. Anachopaswa kufanya ni kutilia mkazo sera zitakazoziwezesha familia masikini sio tu kumudu fedha za kuwanunulia watoto wao sare na viatu, bali angalau kuwa na uhakika wa mlo ujao.
Ni hivi, Waziri Mkuu, kimsingi amri yako ina- criminalise umasikini, kwamba ni kosa kisheria kwa mzazi kuwa masikini kiasi cha kushindwa kumnunulia mwanaye sare bora za shule.
Amri hiyo ya Waziri Mkuu inaonesha jinsi baadhi ya viongozi wetu walivyo mbali na wananchi wanaowaongoza kiasi cha kutoelewa shida wanazokabiliana nazo katika maisha yao.
Nihitimishe makala hii kwa kumsihi Majaliwa atafakari upya kuhusu amri yake hiyo na kwa vile ninaamini anawajali Watanzania wote, wenye kujimudu kimaisha na masikini wasiomudu kununua sare bora za shule kwa watoto wao, atatengua amri hiyo.

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

7 Oct 2016


NIMEKUWA mfuatiliaji mkubwa wa habari na eneo moja ninalolipa umuhimu mkubwa ni habari za teknolojia.
Ufuatiliaji huo wa habari za teknolojia umenifanya niwe na wasiwasi, kwa upande mmoja na matumaini kwa upande mwingine. Wasiwasi wangu mkubwa ni hatma ya Bara la Afrika ambalo kwa kiasi kikubwa linaichukulia teknolojia kama anasa ilhali wenzetu hususan nchi zilizoendelea wanachukulia teknolojia kama sehemu ya mahitaji muhimu kwa binadamu kama ilivyo chakula, makazi na mavazi.
Matumaini yangu katika teknolojia yanatokana na ukweli kwamba licha ya kutelekezwa kwa kiwango kikubwa, matumizi japo kidogo ya teknolojia katika sehemu mbalimbali za dunia inayoendelea, kwa mfano huko nyumbani Tanzania, yanaleta mabadiliko makubwa. Angalia jinsi mfumo wa kusafirisha fedha wa m-pesa unavyofanya kazi, ‘apps’ kama Whatsapp zinavyowezesha watu mbalimbali kuepuka gharama kubwa za simu na ujumbe wa maneno, barua-pepe zinavyotuwezesha kuwasiliana papo kwa papo bila kwenda posta kutuma au kupokea barua na maendeleo mengine mbalimbali.
Nimebahatika kushuhudia zama kabla ya ujio wa intaneti na mitandao ya kijamii, televisheni, simu za mkononi na takriban kila aina ya teknolojia ya kisasa inayoifanya dunia kuwa kama kijiji. Kadhalika, nilikuwa miongoni mwa Watanzania wa awali kukumbatia teknolojia mpya (nilikuwa miongoni mwa Watanzania wa kwanza kabisa kufungua blogu Aprili 2006).
Jumamosi iliyopita niliweza kuangalia mechi ya watani wa jadi, Simba na Yanga, kupitia mtandao wa kijamii wa Facebook. Hii ilinikumbusha miaka kadhaa huko nyuma ambapo tegemeo pekee la kusikia matangazo ya mpira lilikuwa Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) ambayo wakati mwingine iliwalazimu wasikilizaji kupanda juu ya miti ili kudaka vema mawimbi ya radio.
Lakini pengine lililo kubwa zaidi kuhusu teknolojia ni jinsi uchaguzi mkuu wa mwaka jana ulivyoandika historia ya kuwa wa kwanza kabisa ‘kujenga ndoa’ kati ya teknolojia na siasa. Tulishuhudia jinsi mitandao ya kijamii, hususan Facebook na Twitter, ‘apps’ kama Whatsapp na Instagram, na majukwaa ya uchapishaji kama vile blogu na ‘webforums’ (kama Jamii Forums) zilivyotumika kwa ufanisi mkubwa katika kampeni za urais, ubunge na udiwani.
Na kwa hakika, ushindi wa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Rais wa sasa Dk. John Magufuli, ulichangiwa na kampeni zilizofanyika kwenye mitandao ya kijamii, apps na webforums. Kama kuna Rais wa Tanzania anayepaswa kuthamini mno mchango wa teknolojia kwenye siasa basi ni Magufuli.
Hata hivyo, katika mazingira ya kushangaza kabisa, Dk. Magufuli alisikika akieleza kuwa anatamani malaika washuke na kusimamisha mitandao ya kijamii kwa mwaka moja na itaporudi hewani (baada ya mwaka huo mmoja) ishuhudie maendeleo yaliyofikiwa.
Watetezi wa rais wanadai kuwa kauli hiyo ni ya utani tu, lakini nikiwa miongoni mwa watu walioshiriki kikamilifu kumpigia kampeni Magufuli nikiwa maili kadhaa kutoka huko nyumbani lakini nikawezeshwa kufanya hivyo kwa kutumia maendeleo ya teknolojia kama vile matumizi ya mitandao ya kijamii na blogu, nilisikitishwa na kauli hiyo ya Magufuli.
Ni kweli kwamba baadhi ya wenzetu wamekuwa wakiyatumia vibaya maendeleo ya teknolojia, kwa kujenga chuki miongoni mwa Watanzania, upinzani dhidi ya kila kitu hata chenye manufaa kwa taifa, kugeuza mitandao ya kijamii kuwa uwanja wa matusi, na kadhalika.
Hata hivyo, wanaotumia vibaya teknolojia ni wachache kulinganisha na sisi tunaoitumia kwa nia nzuri. Hivi kama kosa la wachache linafanya wote kuwa wabaya, je itakuwa sahihi kudai kuwa malaika washuke na kuifunga serikali kwa muda fulani kwa vile ilikuwa na watumishi hewa zaidi ya 10,000 na watumishi kadhaa wasio hewa lakini ni majipu?
Na hata kama kuna haja ya kuifunga mitandao hiyo, Dk. Magufuli hahitaji malaika bali sheria dhidi ya makosa ya mitandao ya kijamii (Cyber Crime Act 2015) iliyokwishawatia hatiani watu 10 kwa tuhuma za “kumtukana rais kwenye Facebook au Whatsapp?”
Wito wangu kwa Rais Magufuli ni kwamba awe mstahimilivu. Kazi anayofanya ni nzuri na inawapendeza Watanzania wengi. Sasa kuna haja gani asumbuliwe na hizo kelele za hapa na pale ilhali anayofanya ni makubwa zaidi ya kelele hizo?
Kadhalika, kwa vile tu rais wetu hapendezwi na kitu fulani haimaanishi kitu hicho sio halali kikatiba. Kama ambavyo wengi wetu tunatumia uhuru na haki yetu kikatiba kumpongeza Magufuli, katiba yetu inatoa haki na uhuru pia kwa wenzetu kumkosoa rais wetu alimradi wasitumie lugha isiyokubalika kisheria.

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.