Showing posts with label REDET. Show all posts
Showing posts with label REDET. Show all posts

17 Oct 2010

Moja ya mambo yaliyokuwa yakiwaumiza vichwa wafuasi wa Barack Obama wakati wa kinyang'anyiro kati yake na Hillary Clinton kupata mgombea urais wa Marekani kwa tiketi ya chama cha Democrats mwaka 2008 ni theory inayofahamika kama Bradley Effect.Kwa kifupi kabisa,Bradley Effect (au Wilder Effect) ni hali inayoweza kutokea kwenye kura za maoni katika chaguzi nchini Marekani panapokuwa na mgombea Mweupe (White) na asiye mweupe (non-White).Pengine ili wasionekane wabaguzi wa rangi,wahojiwa Weupe katika kura za maoni hueleza kuwa chaguo lao ni mgombea asiye Mweupe au husema kuwa hawajafanya uamuzi kuhusu chaguo lao (Undecided).

Kwahiyo,matokeo ya kura ya maoni yanaweza kuonyesha mgombea asiye Mweupe anapendwa zaidi kuliko mgombea Mweupe lakini inapofika kwenye hatua ya kupiga kura (ambapo mpiga kura anakuwa peke yake),wapiga kura Weupe wanampigia Mweupe mwenzao.

Asili ya Bradley Effect ni katika kinyang'anyiro cha uchaguzi wa uchaguzi wa gavana wa jimbo la California mwaka 1982 ambapo licha ya mgombea Mweusi,Meya wa Jiji la Los Angeles Tom Bradley kuongoza kura za maoni,aliishia kushindwa uchaguzi huo kwa mgombea Mweupe George Deukmejian.

Baadhi ya wachambuzi wa chaguzi nchini Marekani wanaamini pia kuwa Bradley Effect ilijitokeza tena kwenye mchakato wa kumpata mgombea wa chama cha Democrats kwenye jimbo la New Hampshire ambapo licha ya Obama kuongoza katika kura za maoni,Hillary Clinton aliibuka mshindi kwenye jimbo hilo (japokuwa baadaye Obama alifanikiwa kuibuka mshindi wa jumla,na kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya Democrats,na hatimaye kushinda nafasi ya urais).

Katika post hii najaribu kubashiri (hypothesize) namna Bradley Effect inavyoweza kuwa sababu ya mgombea wa CCM,Jakaya Kikwete,kuongoza katika tafiti za  taasisi za Redet na Synovate kuhusu nafasi za wagombea urais katika uchaguzi mkuu wa Tanzania hapo Oktoba 31.Hapa ntawazungumzia wagombea wawili tu,Kikwete na mgombea urais kwa tiketi ya Chadema,Dokta Wilbroad Slaa.

Japo Bradley Effect 'halisi' inahusu mgombea Mweupe na asiye Mweupe,sababu inayopelekea matokeo ya kura kutorandana na mwelekeo wa kura za maoni inaweza kutumika kuelezea kwanini kura za maoni za Redet na Synovate zilimpa Kikwete ushindi na sio Dokta Slaa.Kama ilivyo kwenye chambuzi mbalimbali,kuna mambo flani inabidi 'kupuuzwa' ili kufikia matokeo yanayokusudiwa.Katika uchambuzi huu,naomba 'nipuuze' urafiki kati ya taasisi hizo na CCM na badala yake nikazanie kwenye uwezekano wa Bradley Effect pekee.

Inawezekana kabisa kuwa wahojiwa kwenye tafiti za Redet na Synovate ni wananchi waliotoa majibu 'kuwaridhisha watafiti',yaani walisema wanampenda zaidi Kikwete kuliko Dokta Slaa.Moja ya sababu za kutoa majibu ya aina hiyo ni mazingira halisi ya Tanzania ambapo licha ya 'siasa za mkono wa chuma' za zama za chama kimoja kuonekana kama historia,ukweli unabaki kuwa baadhi ya wananchi wanaamini kuwa kusema lolote lisilowapendeza watawala ni kujitafutia matatizo.

Naomba kufafanua kidogo katika hilo.Nilipokwenda Tanzania mwaka 2005 kufanya fieldwork ya utafiti wangu wa shahada ya uzamifu (PhD) nilikumbana na wakati mgumu kuwahoji baadhi ya maustaadh (mada yangu inahusu masuala ya Waislam na Uislam nchini Tanzania) kwa vile baadhi yao walidhani mie ni wakala wa serikali niliyetumwa kuwachunguza ili 'serikali iweze kuwadhibiti zaidi'.Bahati mbaya,fieldwork hiyo ilifanyika wakati jeshi la polisi lilikuwa linamsaka mwanaharakati wa Kiislam,Sheikh Issa Ponda.Ilichukua kitambo kujenga uaminifu kati yangu na maustaadh hao.

Kuna wanaoilaumu Redet na Synovate kuhusu aina ya watu waliohojiwa wakidai kuwa huenda wahojiwa walikuwa watu walio karibu na CCM (kwa mfano mabalozi wa nyumba kumi).Uwezekano wa Bradley Effect  'yetu' (yaani isiyohusiana na ishu za ubaguzi wa rangi) ni mkubwa kwa vile wahojiwa wanaweza kutoa majibu yasiyoonyesha 'wanambagua mgombea wao' na hivyo kusema huyo ndio chaguo lao japo mioyoni wana dhamira na/au chaguo tofauti.

Of course,inawezekana tafiti hizo za Redet na Synovate 'zilipikwa' ili kuendana na matakwa ya CCM.Inawezekana pia kuwa aina ya watu waliohojiwa ni ambayo isingetoa majibu tofauti na 'ushindi kwa Kikwete'.Lakini,kama makala hii inavyojaribu kubashiri,inawezekana kabisa kuwa wahojiwa 'waliwazuga' jamaa wa Redet na Synivate 'ili isiwe shida'.Nani yuko tayari kuona genge lake au kibanda cha biashara kinabomolewa kwa vile tu amechoshwa na namna CCM inavyozidi kuahidi maisha bora lakini wanaonufaika ni mafisadi pekee?Mtu wa aina hii haoni shida 'kudanganya leo' kisha 'akaungama siku ya kupiga kura' kwa 'kumwadhibu Kikwete na CCM kwenye sanduku la kura ambapo hakutokuwa na wa kumtoa mimacho kwanini hajampigia kura Kikwete au CCM'.

Huu ni ubashiri tu.Unaweza kuwa sio sahihi lakini kama zilivyo bashiri nyingine-hususan zinazoambatana na mifano hai-unaweza kuwa na ukweli ndani yake.Kadhalika,Bradley Effect 'yetu' inaweza kutoa matokeo ya kuwashangaza wote wenye imani kuwa CCM na Kikwete watarudia kupata ushindi wa kishindo kama wa mwaka 2005.

Pengine kuna watakaohoji kwanini Bradley Effect 'yetu' haiwezi kutumika kwenye utafiti mwingine (wa TCIB) unaoonyesha kuwa Dokta Slaa anaongoza.Jibu langu ni kwamba watoa maoni hawana cha kupata (nothing to gain) kuwadanganya watafiti kuwa wanampenda Dokta Slaa wakati ukweli wanayempenda ni Kikwete.Likewise,kwenye tafiti za Redet na Synovate,inawezekana baadhi ya wahojiwa walikuwa na cha kupoteza laiti wangesema hawampendi Kikwete (si unajua kuhusu umoja na mshikamano ndani ya chama?).Vilevile,yawezekana wahojiwa hawakuwa na cha kupoteza (nothing to lose) kwa kudanganya kuwa wanampenda Kikwete (kwa minajili ya kuwaridhishwa watafiti na 'kulinda ugali wao') kisha wakamnyima kura katika usiri wa chumba cha kupigia kura.

Mwisho,naomba kusisitiza tena kuwa hypothesis hii imejaribu kupuuza sababu za 'wazi' kama vile upendeleo wa watafiti,uoga wa wahojiwa,na kubwa zaidi,UCHAKACHUAJI.

9 Oct 2010


Majuzi tumemsikia Mwenyekiti Mwenza wa REDET,Dokta Benson Bana akilipuka tena na utafiti wao wa kuchakachua kuhusu mwenendo wa uchaguzi,ambapo kwa mujibu wao wanadai mgombea wa CCM,Jakaya Kikwete anaongoza kwenye kura za maoni.

Huko nyuma nilishawahi kuandika post moja kuhusu Dokta Bana,na tabia yake ya ulipukaji.Katika post hiyo nilikuwa nazungumzia kauli ya Mhadhiri huyo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwamba tuhuma zilizokithiri dhidi ya ufisadi zinaweza kusababisha taifa kukosa viongozi wazuri.Yani mhadhiri mzima alikosa busara ya kufahamu kuwa kukalia kimya ufisadi hakuwezi kusababisha taifa kupata viongozi wazuri.

Bana na Redet yake wanadhani Watanzania ni wajinga ndio maana wakakurupuka na uchakachuaji huo wakiamini wanaisaidia CCM na Kikwete.Sio ubishi wala kulazimisha matokeo tunayotaka sie bali hali halisi ya mwenendo wa kampeni inaonyesha dhahiri kuwa CCM na Kikwete wamekaliwa kooni na Dokta Wilbroad Slaa na Chadema,huku uthibitisho mkubwa ukiwa kwenye vioja kama kauli ya vitisho ya Mnadhamu Mkuu wa JWTZ Brigedia Jenerali Shimbo.

Hivi huyo Kikwete angekuwa 'anapendwa' na zaidi ya asilimia 70 ya wapiga kura watarajiwa (potential voters) angekuwa anahangaika huku na kule ku-recycle lundo la ahadi zake za mwaka 2005?

Lakini tungetarajia nini kutoka kwa Dokta Bana na REDET yake?Waseme umaarufu wa Kikwete umeshuka?Waseme Dokta Slaa anaongoza kura za maoni?Hayo hayawezekani katika utawala huu wa kifisadi unaotaka kusikia habari njema tu hata kama hazina ukweli.Tunafahamu kuwa Synovate walishindwa kutueleza nani anaongoza kura za maoni kwa vile CCM ilihofia matokeo ya ripoti hiyo yangewaadhiri.Sasa kwa vile REDET 'wameshafungulia mbwa' sintoshangaa Synovate nao wakikurupuka na ripoti yao iliyochakachuliwa itakayoonyesha Kikwete na CCM wanaongoza.

Haina haja ya kuwashutumu wachakachuaji hawa.Dawa yao iko kwa wapiga kura waliochoshwa kuona nchi yao ikigeuzwa maabara ya uchakachuaji kwenye kila eneo.Hebu pata picha iwapo kila Mtanzania aliyechoshwa na ufisadi akipiga kura ya kuwaadhibu mafisadi na hatimaye Kikwete akan'goka madarakani,Dkt Bana na REDET yake watakuwa katika hali gani!

Hilo linawezekana.Wapiga kura wasianze kukata tamaa kuwa CCM wataiba kura.Of course wataiba lakini ili 'kura zitoshe' watalazimika kufanya wizi wa 'mchana mweupe' (day light robbery) jambo ambalo sio rahisi sana,japo linawezekana.Wanaweza tu kuchakachua matokeo kama,kwa mfano Dokta Slaa akipata asilimia 51 na Kikwete asilimia 49.Hapo watarejea uchakachuaji kama ule wa Zanzibar.Lakini kama ni tofauti ya double digits,wanaweza kupatwa na kigugumizi katika kufanikisha ujambazi huo.

Ni muhimu kutovunjwa moyo na hujuma hizi.Yatupasa kufahamu kuwa Kikwete na CCM yake ni kama mgonjwa mahututi ambaye yuko tayari hata kuning'inia kwenye uzi ili asalimike.Tutashuhudia vituko zaidi ya huo uchakachuaji wa REDET au vitisho vya akina Brigedia Shimbo.Cha muhimu ni kusimamia dhamira yetu.

Inawezekana.Timiza wajibu wako

19 Apr 2010

Kuna busara moja inayotuasa kuwa mpuuzi husema kwa vile anajiskia kusema (hata kama ni upuuzi) ilhali mwenye busara husema tu pale anapokuwa na kitu cha kusema (ikimaanisha kama hana cha kusema,au haoni umuhimu wa kusema kitu,atakaa kimya. Busara zaidi zinatuasa kuwa makini na tunayosema hadharani kwa vile mara nyingi jamii humtambua zaidi mtu kwa kauli zake.Sema upuuzi,utaonekana mpuuzi.Sema ya busara,utaonekana mwenye busara.Sasa kuna huyu msomi,Dokta Benson Bana,ambaye licha ya kuwa mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam,ni mkuu wa idara ya Sayansi za Siasa na Uongozi na pia ni Mwenyekiti Mwenza wa REDET.Yayumkinika kusema Dkt Bana amekuwa mahiri zaidi wa kutoa kauli zisizoendana na wasifu wake kitaaluma kuliko umahiri wa wa usomi wake

Na leo,kwa mujibu wa habari katika gazeti la Mwananchi,msomi huyo 'amelipuka' tena kwa kauli kwamba tuhuma zilizokithiri dhidi ya ufisadi zinaweza kusababisha taifa kukosa viongozi wazuri wakati wa uchaguzi mkuu wa Oktoba.Huhitaji kuwa na hata asilimia moja ya kiwango cha elimu ya Dkt Bana kutambua kuwa tuhuma zilizotapakaa kuhusu ufisadi ni matokeo ya kuwepo kwa ufisadi.Msomi huyu anaishi Tanzania lakini yaelekea hafahamu mazingira yanayomzunguka,na hilo linaleta wasiwasi mkubwa kuhusu mchango wa wanataaluma katika maendeleo ya nchi yetu.

Katika habari hiyo Dk Bana aliwataka watu "waaache siasa chafu za kuhubiri na kudai kuwa watuhumiwa wa ufisadi hawafai kupewa kura au kuchaguliwa katika nafasi mbalimbali za uongozi kana kwamba wameshathibitika".Huu ni zaidi ya ubabaishaji wa kitaaluma,na kwa kiasi flani inaaibisha Udaktari wa Filosofia tunaohenyea akina sie.Kwanza,Dkt Bana amepata wapi mamlaka ya kuwataka wananchi waache kulalamikia ufisadi?Usomi hautoi mamlaka ya kuizuia jamii kulalamikia maovu yanayoisumbua.Pili,kwa mtizamo wa msomi huyu,kwa vile tuhuma za ufisadi hazijathibitika basi watu wakae kimya hadi 'miujiza itapotokea kwa watawala wetu kuamua kuchukua hatua za kisheria dhidi ya mafisadi'!Hii ni sawa na kuingiliwa ndani na kibaka halafu ukakaa kimya kwa vile tu wewe sio chombo cha sheria.Ukifanya hivyo,hata hao polisi watakuona mpumbavu na unawapotezea muda.La kufanya ni kumdhibiti kibaka au kupiga kelele kuwashtua majirani wakusaidie kumdhibiti.

Binafsi,pamoja na kuheshimu uhuru wa kutoa mawazo,nadhani tatizo kubwa la Dkt Bana ni tabia yake ya 'kusema chochote' hata kama hana cha kusema.Inaelekea aidha hafahamu athari za tabia hiyo au anapuuza tu.Matokeo yake ni kuonekana mbabaishaji wa namna flani.Si lazima jina lake lionekane magazetini au kusikika radioni kama hana la muhimu kuieleza jamii.Eti anatuasa kuwa "si vizuri kwa watu kunyimwa kura kwa sababu ya kutuhumiwa kwa ufisadi hadi hapo watakapothibitika na kutaka wanasiasa waache kuhukumu wenzao bila kosa".Kwanini hajiulizi inakuwaje watu hao wanatuhumiwa ufisadi in the first place?Kwanini ni wao na si Dokta Bana,kwa mfano?

Hivi lipi lililo muhimu zaidi kwa Tanzania kama taifa: kukosa viongozi bora kwa vile wanatuhumiwa kwa ufisadi au kupata viongozi bora watakaowajibika kulitumikia taifa kupambana na ufisadi?Wasiwasi wa Dkt Bana ulipaswa kuwa kwenye athari za ufisadi kwa jamii na sio tuhuma za wananchi dhidi ya mafisadi.Ni mlevi tu atakayeshindwa kuelewa kuwa kinachoumiza Watanzania kwa sasa ni UFISADI na sio TUHUMA DHIDI YA MAFISADI.

Mwanataaluma huyu anaongoza taasisi ya REDET ambayo mara imekuwa ikishutumiwa kwa upendeleo inapotoa taarifa za kura zake za maoni (opinion polls) kuhusu CCM na vyama vingine vya siasa.Sina hakika kuwa matokeo ya kura hizo huwa 'yanapikwa' ili kuridhisha watawala lakini kinachozua maswali dhidi ya polls hizo ni kutoendana na hali halisi na dalili za upendeleo.

Wito wangu kwa Dkt Bana ni huu: wakati mwingine jaribu kuitendea haki taaluma yako kwa kukaa kimya pale usipokuwa na cha kuongea.Kwa kufanya hivyo,utawatendea haki pia wasomi wenzako,taasisi unazoongoza na fani nzima ya usomi.Ni muhimu pia unapotoa matamshi mazito ukajitahidi kutumia theories za kusapoti matamshi hayo badala ya kutoa hisia zenye mwelekeo wa kijiweni.


.

28 Apr 2009



YAH,WANASEMA NI SUALA LA MTIZAMO: KUSEMA GLASI IKO HALF EMPTY AU HALF FULL.HABARI MBILI ZIFUATAZO ZINADHIHIRISHA MANTIKI YA MSEMO HUO.

Na Boniface Meena

UMAARUFU wa Rais Jakaya Kikwete unaonyesha kuendelea kuporomoka, kwa mujibu wa ripoti ya matokeo ya utafiti uliofanywa na taasisi ya Mpango wa Utafiti wa Elimu ya Demokrasia nchini (Redet).

Ripoti hiyo pia inaonyesha kuwa utendaji kazi wa Rais Kikwete, ambaye aliingia madarakani mwaka 2005 kuongoza serikali ya awamu ya nne, umeshuka kwa asilimia 28 mwaka jana ukilinganisha na matokeo ya utafiti ya mwaka 2006.

Pamoja na kushuka kwa asilimia hiyo, utafiti huo umeonyesha kuwa wananchi waliohojiwa wanaridhika zaidi na utendaji wa Rais Kikwete, kuliko wanavyoridhishwa na utendaji kazi wa baraza lake la mawaziri ambalo utendaji wake umekubaliwa na asilimia 18 tu.

Kwa mujibu wa utafiti huo, watu wanaoridhika sana na utendaji kazi wa Kikwete ni asilimia 39.5 tu kulinganisha na asilimia 69 iliyoonyesha kuridhika naye sana mwaka 2006.

Akitoa taarifa ya utafiti huo jana kwa waandishi wa habari, mtafiti mkuu wa Redet, Dk Benadetha Killian alisema kuwa ukilinganisha takwimu za Oktoba 2006 na Oktoba 2007, asilimia ya wale wahojiwa ambao wanasema wanaridhika sana na utendaji kazi wa Rais Kikwete imepungua kutoka asilimia 69 Oktoba 2006 hadi asilimia 44 mwezi Oktoba 2007 na sasa imefikia asilimia 39.5 hadi Novemba mwaka jana.

Dk. Killian alisema kuwa ukichambua undani wa mwenendo huo utaona kwamba wakati idadi ya wanaosema wanaridhika sana iliteremka kwa tofauti ya asilimia 23, kati ya mwaka 2006 na 2007, kasi ya kutoridhika sana imepungua ukilinganisha na matokeo ya mwaka 2007/08 wakati idadi ya wahojiwa ambao walisema wanaridhika sana ilipungua kwa tofauti ya asilimia 4.5 tu.

Kwa mujibu wa Dk. Killian, ukusanyaji wa maoni kwa ajili ya utafiti huo ulifanyika katika mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani na sampuli ilichaguliwa katika ngazi tatu ambazo ni wilaya na vijiji/mitaa na katika kila ngazi sampuli ilipatikana kwa kutumia mtindo wa sampuli nasibu.

"Katika kila wilaya, watafiti walitakiwa kuchagua vijiji viwili (kwa maeneo ya shamba) au mitaa miwili (kwa maeneo ya mjini) kwa kutumia njia ya sampuli nasibu. Katika kila wilaya, jumla ya watu 50 walichaguliwa kwa ajili ya kuhojiwa, 25 kutoka kila kijiji/mtaa," alisema.

"Na kati ya watu 50 waliohojiwa katika kila wilaya, 25 walitakiwa wawe wanawake na wengine 25 wawe wanaume na uchaguzi wote wa wahojiwa ulifanyika kwa kutumia njia ya sampuli nasibu."

Alisema ukiacha masuala mengine ya utendaji wa mawaziri, waliohojiwa walitakiwa kutoa tathimini yao kuhusu utendaji kazi wa Rais Kikwete katika kipindi cha takriban miaka mitatu ya utawala wake kwa kutoa maoni yao kama wanaridhika sana, wanaridhika kiasi au hawaridhiki.

Dk. Killian alisema kati ya wote waliohojiwa, asilimia 39.5 walisema wanaridhishwa sana na utendaji wa Rais Kikwete, asilimia 39.0 walisema wanaridhika kiasi na asilimia 19.3 walisema hawaridhiki na utendaji kazi wa mkuu huyo wa nchi.

Alisema hata hivyo kwa ujumla, matokeo ya utafiti wa Novemba mwaka jana yanaashiria kwamba, utendaji kazi wa Rais Kikwete bado unaonekana kuridhisha idadi kubwa ya watu pale ambapo makundi mawili ya wahojiwa yanapojumlishwa pamoja yaani wale wanaosema wanaridhika sana asilimia 39.5 na wale wanaosema wanaridhika kiasi asilimia 39 ikiwa inafanya idadi hiyo ya wahojiwa wote kufikia asilimia 78.5.

Dk Killian alisema sababu za kuridhika au kutoridhika na utendaji kazi wa serikali ya Rais Kikwete ni kutoridhishwa na ahadi yake ya kuboresha hali ya maisha. Asilimia 31.0 ya waliohojiwa walisema ameshindwa kuboresha hali ya maisha, wakati asilimia 24 walisema hajatimiza ahadi na asilimia 12.2 walisema hafuatilii utekelezaji wa ahadi zake.

"Sababu nyingine zilizotolewa na wahojiwa ni kuchagua viongozi wasiofaa asilimia 10.8, ameshindwa kupambana na rushwa asilimia 8.0, lakini pamoja na kwamba utafiti huu ulifanywa kipindi ambacho "vigogo" walikuwa wanapelekwa mahakamani kuhusiana na tuhuma za matumizi mabaya ya ofisi na wengine kutuhumiwa na wizi wa fedha za akaunti ya madeni ya nje (EPA), ni asilimia 6 tu ndiyo waliotaja moja kwa moja suala hili kama sababu ya kutoridhishwa au kuridhishwa kiasi na utendaji kazi wa rais," alisema.

Alisema sababu za wananchi kutoridhika na utendaji wa serikali iliyo madarakani ni kutofuatilia utekelezaji asilimia 30.7, serikali kujihusisha na rushwa asilimia 29 na inapitisha mikataba mibovu asilimia 10.0.

Utafiti huo pia unaonyesha kuwa bunge ndio linaongoza kwa kutoridhisha wananchi baada ya asilimia kubwa ya waliohojiwa kueleza kuwa hawaridhishwi na taasisi hiyo ya kutunga sheria.

Bunge limeonekana kutoridhisha wengi tofauti na taasisi za serikali kama polisi, taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa nchini, serikali za mitaa na kadhalika.

Dk. Killian alisema bunge linaongoza kwa kuwa na asilimia kubwa ya kiwango cha kutoridhika ambacho ni asilimia 77.4, ikifuatiwa na serikali za mitaa asilimia 75.6 wakati baraza la mawaziri linashika nafasi ya tatu kwa asilimia 63.

Kwa upande wa utendaji kazi wa Rais Amani Abeid Karume wa Zanzibar, utafiti unaonyesha kuwa asilimia 44 tu ya wote waliohojiwa wanaridhika sana, wakati asilimia 24 wanaridhika kiasi na asilimia 26 walisema hawaridhiki.

Alisema kiwango cha utendaji wa Rais Karume kimeonekana kupanda kwa asilimia 9 ukilinganisha na utafiti wa Oktoba 2007 wakati asilimia 35.5 tu ilimkubali baada ya kuporomoka kutoka asilimia 47.8 aliyopata kipindi cha hadi Oktoba 2006 na baadaye kupanda kutoka asilimia 35.5 Oktoba 2007.

CHANZO: Mwananchi



Nyota ya Kikwete Bado Yang'ara
na mwandishi Wetu


Watanzania walio wengi, zaidi ya asilimia 80, bado wana imani na Rais Jakaya Kikwete, kuliko miaka minne iliyopita alipochaguliwa kuwa Rais. Pia asilimia kubwa ya Watanzania inaridhishwa na utendaji kazi wa Rais na Serikali yake.

Kura ya maoni iliyoendeshwa na taasisi ya uchunguzi inayojitegemea ya REDET kuhusu utendaji wa Serikali ya Kikwete katika miaka mitatu iliyopita ya uongozi wake, inaonyesha kuwa asilimia 83.7 ya Watanzania wana imani naye.

Kundi hilo la Watanzania wanaothibitisha kuwa na imani na Rais Kikwete likigawanywa katika makundi ya ulinganisho wa imani, asilimia 50 inasema ina imani sana kwa kiongozi huyo, asilimia 33.7 inasema ina imani kiasi cha kutosha kwake.

Asilimia hiyo ni kubwa kuliko ile ya ushindi wa urais mwaka 2005, alipochaguliwa kwa kishindo ambapo alichaguliwa kwa asilimia 82. Hakuna mwanataaluma yeyote wa REDET ambaye alikubali kuzungumza na gazeti hili kuhusu kura hiyo ya maoni licha ya kupatikana kwa nakala ya matokeo ya utafiti huo.

Lakini habari zinasema matokeo kamili ya kura hiyo yanatarajiwa kutangazwa rasmi wiki ijayo na uongozi wa REDET. Kubwa zaidi katika ripoti hiyo, ni ukweli kuwa asilimia ya Watanzania wenye kuridhishwa na utendaji kazi wa Rais Kikwete bado iko juu.

Utafiti huo wa kisayansi na wa kina uliofanyika katika sehemu mbalimbali za nchi mijini na vijijini unaonyesha kuwa asilimia 78 ya Watanzania wanaridhishwa na utendaji kazi wake. Matokeo ya kura hizo yamethibisha kwa mara nyingine, ukweli ambao umebakia bila kubadilika kuhusu imani ya wananchi kwa Rais Kikwete na utendaji wake tangu alipoingia madarakani.

Kura zote za maoni ambazo zimefanyika tangu wakati huo, zimekuwa zikionyesha kuwa kiwango cha imani ya wananchi wake na kwa utendaji kazi wake kimebakia kwenye eneo la asilimia 80. Kura hizo pia zinaonyesha kuwa imani ya wananchi kwa wasaidizi wake wakuu ni ya juu.

Zinaonyesha pia kuwa asilimia 82.7 wana imani na Makamu wa Rais, Dk. Ali Mohammed Shein akiwa nyuma ya Rais kwa asilimia moja, wakati Waziri Mkuu Mizengo Pinda anavutia asilimia 84. Utafiti huo pia unathibitisha kuwa wananchi kiasi cha asilimia 70 wana imani na Baraza la Mawaziri, wakati asilimia 66 wana imani na wakuu wa mikoa. Imani ya wananchi inashuka kidogo kwa Bunge ambalo lina asilimia 65.

Katika namna ambayo pia itakipa nguvu na kuifurahisha CCM, asilimia ya Watanzania ambao wanasema wanaridhishwa na utendaji kazi wa chama hicho ni 72.8 wakati asilimia 75.6 wanasema wana imani na chama hicho. Matokeo hayo yatakifurahisha chama hicho kwa sababu asilimia hiyo kubwa ya kukubaliwa na Watanzania imebakia ya kiwango hicho hicho kwa karibu miaka 17 tangu kuanzishwa kwa vyama vya upinzani nchini.

Mwaka 1992 wakati CCM na serikali zilipoongoza mageuzi ya kuingia katika mfumo wa vyama vingi, ilikuwa baada ya uchunguzi uliothibitisha kuwa ni asilimia 20 tu ya Watanzania waliokuwa wanataka mfumo wa vyama vingi. Kwa namna moja au nyingine, asilimia hiyo imebakia na kujithibitisha mara nyingi kupitia njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na kupitia uchaguzi mkuu ambao umefanyika tangu wakati huo na hasa uliopita uliomwingiza Rais Kikwete madarakani mwaka 2005. Kwa upande wa vyama vya upinzani, asilimia ya Watanzania ambayo inasema haina imani na vyama hivyo inabakia juu kwa asilimia zaidi ya 31.



CHANZO: HabariLeo



































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































































Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.