Showing posts with label BRADLEY EFFECT. Show all posts
Showing posts with label BRADLEY EFFECT. Show all posts

17 Oct 2010

Moja ya mambo yaliyokuwa yakiwaumiza vichwa wafuasi wa Barack Obama wakati wa kinyang'anyiro kati yake na Hillary Clinton kupata mgombea urais wa Marekani kwa tiketi ya chama cha Democrats mwaka 2008 ni theory inayofahamika kama Bradley Effect.Kwa kifupi kabisa,Bradley Effect (au Wilder Effect) ni hali inayoweza kutokea kwenye kura za maoni katika chaguzi nchini Marekani panapokuwa na mgombea Mweupe (White) na asiye mweupe (non-White).Pengine ili wasionekane wabaguzi wa rangi,wahojiwa Weupe katika kura za maoni hueleza kuwa chaguo lao ni mgombea asiye Mweupe au husema kuwa hawajafanya uamuzi kuhusu chaguo lao (Undecided).

Kwahiyo,matokeo ya kura ya maoni yanaweza kuonyesha mgombea asiye Mweupe anapendwa zaidi kuliko mgombea Mweupe lakini inapofika kwenye hatua ya kupiga kura (ambapo mpiga kura anakuwa peke yake),wapiga kura Weupe wanampigia Mweupe mwenzao.

Asili ya Bradley Effect ni katika kinyang'anyiro cha uchaguzi wa uchaguzi wa gavana wa jimbo la California mwaka 1982 ambapo licha ya mgombea Mweusi,Meya wa Jiji la Los Angeles Tom Bradley kuongoza kura za maoni,aliishia kushindwa uchaguzi huo kwa mgombea Mweupe George Deukmejian.

Baadhi ya wachambuzi wa chaguzi nchini Marekani wanaamini pia kuwa Bradley Effect ilijitokeza tena kwenye mchakato wa kumpata mgombea wa chama cha Democrats kwenye jimbo la New Hampshire ambapo licha ya Obama kuongoza katika kura za maoni,Hillary Clinton aliibuka mshindi kwenye jimbo hilo (japokuwa baadaye Obama alifanikiwa kuibuka mshindi wa jumla,na kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya Democrats,na hatimaye kushinda nafasi ya urais).

Katika post hii najaribu kubashiri (hypothesize) namna Bradley Effect inavyoweza kuwa sababu ya mgombea wa CCM,Jakaya Kikwete,kuongoza katika tafiti za  taasisi za Redet na Synovate kuhusu nafasi za wagombea urais katika uchaguzi mkuu wa Tanzania hapo Oktoba 31.Hapa ntawazungumzia wagombea wawili tu,Kikwete na mgombea urais kwa tiketi ya Chadema,Dokta Wilbroad Slaa.

Japo Bradley Effect 'halisi' inahusu mgombea Mweupe na asiye Mweupe,sababu inayopelekea matokeo ya kura kutorandana na mwelekeo wa kura za maoni inaweza kutumika kuelezea kwanini kura za maoni za Redet na Synovate zilimpa Kikwete ushindi na sio Dokta Slaa.Kama ilivyo kwenye chambuzi mbalimbali,kuna mambo flani inabidi 'kupuuzwa' ili kufikia matokeo yanayokusudiwa.Katika uchambuzi huu,naomba 'nipuuze' urafiki kati ya taasisi hizo na CCM na badala yake nikazanie kwenye uwezekano wa Bradley Effect pekee.

Inawezekana kabisa kuwa wahojiwa kwenye tafiti za Redet na Synovate ni wananchi waliotoa majibu 'kuwaridhisha watafiti',yaani walisema wanampenda zaidi Kikwete kuliko Dokta Slaa.Moja ya sababu za kutoa majibu ya aina hiyo ni mazingira halisi ya Tanzania ambapo licha ya 'siasa za mkono wa chuma' za zama za chama kimoja kuonekana kama historia,ukweli unabaki kuwa baadhi ya wananchi wanaamini kuwa kusema lolote lisilowapendeza watawala ni kujitafutia matatizo.

Naomba kufafanua kidogo katika hilo.Nilipokwenda Tanzania mwaka 2005 kufanya fieldwork ya utafiti wangu wa shahada ya uzamifu (PhD) nilikumbana na wakati mgumu kuwahoji baadhi ya maustaadh (mada yangu inahusu masuala ya Waislam na Uislam nchini Tanzania) kwa vile baadhi yao walidhani mie ni wakala wa serikali niliyetumwa kuwachunguza ili 'serikali iweze kuwadhibiti zaidi'.Bahati mbaya,fieldwork hiyo ilifanyika wakati jeshi la polisi lilikuwa linamsaka mwanaharakati wa Kiislam,Sheikh Issa Ponda.Ilichukua kitambo kujenga uaminifu kati yangu na maustaadh hao.

Kuna wanaoilaumu Redet na Synovate kuhusu aina ya watu waliohojiwa wakidai kuwa huenda wahojiwa walikuwa watu walio karibu na CCM (kwa mfano mabalozi wa nyumba kumi).Uwezekano wa Bradley Effect  'yetu' (yaani isiyohusiana na ishu za ubaguzi wa rangi) ni mkubwa kwa vile wahojiwa wanaweza kutoa majibu yasiyoonyesha 'wanambagua mgombea wao' na hivyo kusema huyo ndio chaguo lao japo mioyoni wana dhamira na/au chaguo tofauti.

Of course,inawezekana tafiti hizo za Redet na Synovate 'zilipikwa' ili kuendana na matakwa ya CCM.Inawezekana pia kuwa aina ya watu waliohojiwa ni ambayo isingetoa majibu tofauti na 'ushindi kwa Kikwete'.Lakini,kama makala hii inavyojaribu kubashiri,inawezekana kabisa kuwa wahojiwa 'waliwazuga' jamaa wa Redet na Synivate 'ili isiwe shida'.Nani yuko tayari kuona genge lake au kibanda cha biashara kinabomolewa kwa vile tu amechoshwa na namna CCM inavyozidi kuahidi maisha bora lakini wanaonufaika ni mafisadi pekee?Mtu wa aina hii haoni shida 'kudanganya leo' kisha 'akaungama siku ya kupiga kura' kwa 'kumwadhibu Kikwete na CCM kwenye sanduku la kura ambapo hakutokuwa na wa kumtoa mimacho kwanini hajampigia kura Kikwete au CCM'.

Huu ni ubashiri tu.Unaweza kuwa sio sahihi lakini kama zilivyo bashiri nyingine-hususan zinazoambatana na mifano hai-unaweza kuwa na ukweli ndani yake.Kadhalika,Bradley Effect 'yetu' inaweza kutoa matokeo ya kuwashangaza wote wenye imani kuwa CCM na Kikwete watarudia kupata ushindi wa kishindo kama wa mwaka 2005.

Pengine kuna watakaohoji kwanini Bradley Effect 'yetu' haiwezi kutumika kwenye utafiti mwingine (wa TCIB) unaoonyesha kuwa Dokta Slaa anaongoza.Jibu langu ni kwamba watoa maoni hawana cha kupata (nothing to gain) kuwadanganya watafiti kuwa wanampenda Dokta Slaa wakati ukweli wanayempenda ni Kikwete.Likewise,kwenye tafiti za Redet na Synovate,inawezekana baadhi ya wahojiwa walikuwa na cha kupoteza laiti wangesema hawampendi Kikwete (si unajua kuhusu umoja na mshikamano ndani ya chama?).Vilevile,yawezekana wahojiwa hawakuwa na cha kupoteza (nothing to lose) kwa kudanganya kuwa wanampenda Kikwete (kwa minajili ya kuwaridhishwa watafiti na 'kulinda ugali wao') kisha wakamnyima kura katika usiri wa chumba cha kupigia kura.

Mwisho,naomba kusisitiza tena kuwa hypothesis hii imejaribu kupuuza sababu za 'wazi' kama vile upendeleo wa watafiti,uoga wa wahojiwa,na kubwa zaidi,UCHAKACHUAJI.

22 Oct 2008


Barack Obama akifanikiwa kushinda urais hapo Novemba 4 atakuwa ameweka historia kwa kuwa Mweusi wa kwanza kuwa rais wa Marekani.Lakini mafanikio ya Obama yanawasumbua wachambuzi wa siasa (hususan za tabia za uchaguzi wa Marekani).Hayawasumbui kwa vile Obama na wao ni wabaguzi.La hasha,bali ni namna hisia kwamba Bradley effect ingemwangusha zinavyoelekea kuwa wrong.

Nilishakiri katika post yangu moja huko nyuma kwamba awali nilitamani Hillary Clinton apitishwe kuwa mgombea wa Democrats.Sababu yangu kuu ilikuwa ni katika hofu kwamba Obama angeshinda nomination basi Weupe wangeungana bila kujali itikadi zao kuhakikisha mtu mweusi haingii White House.Baada ya kumbwaga Hillary,nililazimika kukubaliana na busara za stadi za siasa kwamba lolote linawezekana katika fani hiyo.

Tukirejea kwenye kinachowasumbua wachambuzi wa siasa ni namna Bradley effect inavyoelekea kushindwa kuwa na impact kwa Obama,hasa kipindi hiki ambacho sio tu anapambana na Mweupe bali Mweupe kutoka chama cha weupe wahafidhina (Republican).Kuna wanaoamini kwamba Bradley effect ni uzushi (myth) wa aina flani.I dont.Lakini kama sio myth basi kwanini Obama anazidi kupaa kwenye opinion polls?

Binafsi nadhani hii ni REVERSE BRADLEY EFFECT.Yaani,wapiga kura Weusi hawaonyeshi dhamira zao hadharani (kwa wanaochukua opinion polls) kwamba watamsapoti Mweusi mwenzao.Kwa lugha nyingine,wanashusha matarajio ya support ya Weusi kwa Mweusi mwenzao.Lakini kwa vile Weusi ni wachache Marekani,na hata kama wangefanya nacho-hypothesize hapo juu bado wasingeweza kuifanya hali kuwa kama ilivyo sasa,nachoamini zaidi ni tabia "mpya" ya Weupe kudai hadharani kuwa hawajaamua wampigie kura nani (undecided) au Weupe (hasa wa Republicans) kuongopa hadharani kwamba wanamsapoti McCain ilhali dhamira na sapoti yao ni kwa Obama.

Weusi wa Obama ni issue kwenye uchaguzi huu,nami ni muumini wa hoja kwamba kama Obama angekuwa Mweupe basi muda huu tungeshafuta uwezekano wa McCain kuwa rais hapo Novemba.Kwanini nasema hivyo?Wamarekani wengi wamechoshwa na Republicans na uhafidhina kwa ujumla.Bush ameendelea kuwa one of the most unpopular US presidents ever,na Democrats wanaonekana kama ndio watakaoleta ufumbuzi wa matatizo ya Marekani.Sababu zote hizo ni tosha kumfanya mgombea anayekubalika wa Democrats kuwa mbali sana kwenye kura za maoni.Kwanini Obama anamwacha McCain kwa wastani wa kura 10 tu?Jibu la haraka ni Weusi wake.

Whether Bredley effect ni hype au ndio ujio wa Reverse Bredley effect itajulikana baada ya exit polls hapo Novemba 4.However,no matter what happens to Obama,alipofika ni historia tosha,japo itanoga zaidi akishinda kiti hicho.

16 Jan 2008


Wiki iliyopita ilitawaliwa na surprises mbili:huko New Hampshire,Marekani,Hillary Clinton aliibuka mshindi kwenye primaries za chama cha Democrats,kinyume kabisa na utabiri wa awali wa waendesha kura za maoni na wachambuzi wa siasa za nchi hiyo.Na huko nyumbani,ugavana wa Daudi Balali ulitenguliwa.Wakati ili kuelewa nini kinaweza kuwa chanzo cha tofauti kati ya utabiri (kwamba Hillary angeshindwa) na matokeo (ambapo mwanamama huyo alishinda) kunahitaji upeo wa namna flani kuhusu siasa za Marekani na tabia ya chaguzi katika nchi hiyo (kwa mfano phenomenon kama Bradley effect),utenguzi wa ugavana wa Balali haukuhitaji hata short course ya uchambuzi wa siasa kubaini kwamba he had to go,pengine mapema zaidi ya wiki iliyopita.

Makala yangu ndani ya gazeti la Raia Mwema wiki hii inazungumzia surprises hizo mbili.Inakwenda mbali zaidi kwa kuhoji iwapo ufisadi uliopelekea Balali kupoteza unga wake ulihusisha mtu mmoja pekee.Kadhalika,inahitimisha kwamba kufanikiwa kwa ufisadi huo ni failure kwa TAKUKURU na jeshi la Polisi,taasisi ambazo kimsingi zilipaswa kuchukua hatua mapema kuzuia na/au kupunguza uhalifu huo.

Pamoja na makala nyingine zilizokwenda shule ndani ya Raia Mwema,bingirika na makala hiyo hapa.

9 Jan 2008


Baada ya Barack Obama kuibuka kidedea huko Iowa,kuna wengi walioanza kuamini kwamba sura mpya imefunguliwa katika siasa za Marekani.Mimi sikuwa mmoja wao,na ushahidi unapatikana kwenye makala zangu zilizopita kuhusu ushindi huo wa Obama.Katika toleo la wiki hii la gazeti la Raia Mwema nimejaribu kuangalia namna imani na matumaini ya Obama yalivyomfikisha hapa alipo sasa.Napenda kusisitiza kwamba makala hiyo iliandaliwa kabla ya matokeo ya primaries huko New Hampshire ambapo Hillary Clinton ameibuka mshindi na kuwafanya baadhi ya wachambuzi wa siasa na waendesha kura za maoni "kulamba matapishi yao".

Nikipata muda mwafaka nitachambua kwa kirefu nini nachodhani kimechangia kugeuza upepo uliokuwa ukivuma kuelekea kwa Obama huko New Hampshire.Lakini kwa kifupi,nadhani waendesha kura za maoni waliokuwa wakimpa Obama nafasi kubwa ya ushindi huku wakitabiri kuwa Hillary ataanguka walisahau namna Bradley effect inavyoweza kuwazuga watu pindi panapokuwa mgombea Mweupe na Mweusi.Kwa kifupi kabisa,Bradley effect ni tabia katika chaguzi za Marekani  ambapo  wapiga kura watarajiwa ambao hawajafikia uamuzi watampa nani kura zao (undecided voters) hutoa mtizamo tofauti na namna watakavyopiga kura.Kimsingi,tabia hii huchochewa na ubaguzi wa rangi ambapo undecided voters Weupe huweza kudai kuwa hawajaamua wampe nani kura au kudai kuwa watampa kura mgombea Mweusi lakini huishia kumpa kura mgombea Mweupe.

Kama nilivyosema awali,makala yangu kwenye Raia Mwema inahusu namna imani inavyoweza kuyapa nguvu matumaini ili kufikia malengo flani.Nafasi ya Obama imetumiwa kama kielelezo tu cha namna imani mbalimbali huko nyumbani (kwa mfano,kwamba maisha bora kwa kila Mtanzania yanawezekana) zinavyoshindwa kuleta matumaini yanayokusudiwa kutokana na ufisadi,uzembe na ubabaishaji.Pamoja na makala nyingine zilizokwenda shule katika gazeti la Raia Mwema,bingirika na makala yangu hapa.

Baada ya kusoma makala hii sio vibaya ukiburudika na warembo hawa wa Blu3 na kitu chao Hitaji


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.