Showing posts with label USALAMA WA TAIFA. Show all posts
Showing posts with label USALAMA WA TAIFA. Show all posts

27 May 2016


Makala hii imechapishwa katika toleo la wiki hii la gazeti la RAIA MWEMA lakini tovuti ya gazeti hilo haijaweka habari mpya, kwahiyo nimeonelea ni vema nikiitundika hapa (na sina hakika lini Raia Mwema wata-update tovuti yao). Kichwa cha habari cha makala hii gazetini kinaweza kuwa tofauti na hiki nilichotumia kwenye blogu. 

Ijumaa iliyopita itabaki kuwa siku ya kumbukumbu kwa muda mrefu katika siasa za nchi yetu na medani nzima ya uongozi wa taifa letu. Siku hiyo, kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi mno, Rais wa nchi yetu alimtimua waziri wake mwandamizi ‘bila kuuma maneno’

Tukiweka kando zama za utawala wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, tangu tupate uhuru hadi alipong’atuka mwaka 1985, kipindi ambacho kutokana na urefu wake kilishuhudia majeruhi kadhaa wa kisiasa, kwa zaidi ya miaka 30 Tanzania yetu haijashuhudia kulichofanywa na Rais Dkt John Magufuli mwishoni mwa wiki iliyopita ‘alipomtumbua’ aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga kwa kosa la kuingia bungeni akiwa amelewa.

Uzito wa hatua hiyo unatokana zaidi na mambo makuu matatu. Kwanza, Kitwanga ni rafiki wa muda mrefu wa Rais Magufuli, na wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka jana, alimtambulisha kama mtu anayemfahamu vizuri, waliyesoma pamoja Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Bila kujali uzito wa kosa la Kitwanga, ilihitaji ujasiri mkubwa kwa Magufuli kumtimua ‘hadharani’ rafiki yake huyo.

Pili, uzito wa hatua hiyo unatokana na hicho nilichokiandika katika paragrafu iliyotangulia; katika miaka 10 ya utawala wa Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi wa Awamu ya Pili, miaka 10 ya utawala wa Rais Mstaafu Benjamin Mkapa wa Awamu ya Tatu, na miaka 10 iliyomalizika mwaka jana ya utawala wa Rais Mstaafu Jakaya Kikwete wa Awamu ya Nne, hakujawahi kutokea hatua kama hiyo aliyochukua Rais Magufuli.

Kila ilipojitokeza kasoro ya kiutendaji, marais waliotangulia waliishia aidha kufanya mabadiliko ya baraza la mawaziri pasipo maelezo ya kutosha kuwa “uwaziri wa flani umetenguliwa kwa sababu flani” au pengine waziri kutolewa wizara moja na kupelekwa wizara nyingine. Na hali hiyo ya ‘boronga hapa uhamishiwe kule’ ilikuwepo pia katika zama za Awamu ya Kwanza ya Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere.

Kwa kifupi, Dokta Magufuli amevunja mwiko wa kisiasa uliodumu kwa muda mrefu mno, na kwa hilo tu anastahili kila aina ya pongezi, sio tu kwa sababu ya kuandika upya historia ya taifa letu bali ukweli kwamba hatua hiyo inamtambulisha Rais wetu kama mtu anayeweka mbele zaidi maslahi ya taifa letu kuliko maslahi binafsi.

Tatu, miaka nenda miaka rudi, baada ya kuingia kwenye mfumo wa siasa za vyama vingi, marais wetu kama wenyeviti wa chama tawala CCM, wamekuwa wakijitahidi kadri wawezavyo kujifanya ‘viziwi’ kila zinapojitokeza ‘kelele’ kutoka vyama vya upinzani. Kabla ya ‘kutumbuliwa,’ baadhi ya vyama vya upinzani vilikuwa vikimlalamikia Rais Magufuli kuwa ‘anamlinda Kitwanga’ kuhusiana na kashfa ya ufisadi ya Lugumi, na vilikuwa vikipiga kelele kumtaka ‘amtumbue’ Kitwanga.

Sasa, katika mazingira ya kawaida tu, ingeweza kuwa vigumu kwa Dkt Magufuli kumtimua Kitwanga kwa kuhofia “kuwapa wapinzani ushindi wa bure” katika suala hilo. Kwamba, wapinzani wangeweza kujigamba kuwa shinikizo lao ndio limepelekea Rais ‘kumtumbua’ rafiki yake.

Na katika hilo, ni muhimu kutambua kuwa Dkt Magufuli “ana wabaya wake ndani ya CCM,” na angeweza kuchelewa kumtimua Kitwanga kwa vile “wabaya wake hao” wangeweza kutafsiri kitendo hicho kama udhaifu, kwa maana ya “kuendeshwa na kelele za Wapinzani.”

Kwa kiwango kikubwa, hatua hiyo ya Dkt Maguguli imepokelewa vizuri na Watanzania wengi, hasa ikizingatiwa kuwa licha ya ‘kumtumbua Kitwanga,’ suala zima la kuchukua hatua stahili pale inapohitajika ni kama kitu kigeni kwa wananchi wengi, ikizingatiwa kuwa kwa muda mrefu nchi yetu imekuwa ikiongozwa kwa siasa za kulindana. Kwahiyo, ahadi za Dkt Magufuli wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu na baada ya kuapishwa kuwa rais, kwamba hatomwonea aibu mtu yeyote zimethibitika zaidi katika suala hilo la ‘kumtumbua’ Kitwanga.

Hata hivyo, Tanzania yetu imegawanyika kuliko wengi tunavyoiona. Na mgawanyiko mkubwa wa nchi yetu ni athari ya moja kwa moja ya uchaguzi mkuu uliopita. Kuna kundi kubwa tu la wenzetu ambao hadi dakika hii hawataki kuamini kuwa “mgombea wao alishindwa.” Hapa namzungumzia mgombea urais kwa tiketi ya UKAWA, Edward Lowassa. Sasa kwa wenzetu hao, Dkt Magufuli sio tu “hakushinda kihalali” bali pia ni “dikteta anayetumbua watu bila kuzingatia sheria, mwenye jazba, nguvu ya soda” na kila baya unaloweza kumuongelea kiongozi.

Waungwana hawa walikuwa wakipiga kelele mno kumtaka Rais amwajibishe ‘swahiba wake’ Kitwanga ili kuwezesha uchunguzi wa kashfa ya Lugumi ufanyike kwa ufanisi zaidi hasa kwa vile nafasi ya Kitwanga kama Waziri mwenye mamlaka juu ya Jeshi la Polisi ingeweza kuathiri uchunguzi huo.

Akina sie pia tulimshauri Rais afikiri kutengua uwaziri wa Kitwanga, lakini tunapopishana na wenzetu hao ni kwamba hata baada ya Rais “kusikiliza kilio cha kumtaka amtumbue Kitwanga” bado wanamlaumu. Baadhi wanadai kuwa “kumtumbua Kitwanga ili kuuwa suala la Lugumi.” Wengine wanakwenda mbali zaidi na kudai “suala hilo ni mchezo wa kuigiza usioingia akilini.” Wanasema eti “Kitwanga ametolewa kafara ili kuwanusuru vigogo flani.”

Lawama kwa Dkt Magufuli hata baada ya kuweka kando urafiki na kuchukua hatua stahili dhidi ya swahiba yake, zinaweza kumvunja moyo. Tukumbuke, yeye ni binadamu kama sie. Na ni wazi, unapokubali lawama kutoka kwa mtu wako wa karibu ili tu kukidhi matakwa ya jamii, kisha ukaishia kulaumiwa na baadhi ya wanajamii, inavunja moyo. Hata hivyo, ninatumaini kuwa Dkt Magufuli hatoyumbishwa na lawama hizo. Kimsingi, zilikuwepo, zipo na zitaendelea kuwepo kwa sababu tatizo sio anachofanya bali imani fyongo ya “wenzetu” kuwa aliyepaswa kuwa rais ni yule “mtu wao.”

Kama kuna lawama au kasoro inayoweza kujadiliwa basi ni kuhusu utaratibu wa kiusalama uanaofahamika kama “vetting.” Kabla ya kuteuliwa, jina la Kitwanga lilipelekwa Idara ya Usalama wa Taifa kwa ajili ya kufanyiwa vetting. Swali, je Idara hiyo ilishindwa kubaini kuwa “Kitwanga ana kasoro ya ulevi ambayo sio tu ingeweza kuathiri utendaji kazi wake bali pia ingeweza kuhatarisha usalama wa taifa”? Je inawezekana kuwa Idara hiyo ilitekeleza jukumu lake ipasavyo lakini ‘mfanya uteuzi’ akapuuzi ushauri wa mashushushu hao?

Huu sio muda wa kunyoosheana vidole. Kama Idara yetu ya Usalama wa Taifa ilizembea kwenye vetting basi na ijirekebishe haraka. Kama ‘mfanya uteuzi’ alipuuzia ushauri wa mashushushu hao basi ameshapata funzo muhimu.

Ikumbukwe kuwa hadi muda huu hatufahamu kuwa ‘tatizo la ulevi wa Kitwanga’ limeathiri vipi utendaji wake wa kazi kama Waziri wa wizara nyeti ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Kiusalama, hakuna kitu majasusi kutoka nchi za nje wanaombea kama kukutana na mtendaji wa serikali katika eneo nyeti ambaye ana udhaifu kama huo wa ulevi. Na ninaamini kuwa ndugu zangu wa Idara ya Usalama wa Taifa wanafahamu fika jinsi majirani zetu walivyojaza majasusi ndani ya Tanzania yetu, hususan baada ya ujio wa Dkt Magufuli unaoanza kuifanya nchi yetu kuwa tishio kiuchumi kwa majirani zetu.

Ni matumaini yangu makubwa kuwa kutafanyika uchunguzi wa kina kuhakikisha kuwa mapungufu ya Kitwanga hayakuathiri usalama wa taifa letu kwa maana ya kwamba hakuna aliyetumia ‘ulevi wake’ kum- “blackmail” ili atoe siri za serikali.

Kiu kubwa kwa Watanzania kwa muda huu ni kuona Bunge litachukua hatua gani dhidi ya ‘mwenzao.’ Hata hivyo, ishara mbaya zimeanza kuonekana baada ya Naibu Katibu wa Bunge, John Joel, kunukuliwa akidai kuwa “hakuna kifungu chochote cha kanuni za Bunge kinachomzuwia mtu kuingia Bungeni akiwa amelewa.” Yaani hawa waheshimiwa wana kinga dhidi ya Kanuni za Utumishi wa Umma zinazokataza “tabia inayovunja heshima ya utumishi kwa umma hata nje ya mahali pa kazi” kwa mfano ulevi.

Lakini kubwa zaidi ni kuona kuwa ‘kutumbuliwa’ kwa Kitwanga haukuathiri uchunguzi wa suala tete la Lugumi. Kimsingi, kwa kutolewa uwaziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kamati Teule ya Bunge inayochunguza suala hilo sasa haina kisingizio chochote cha kutowapatia Watanzania kile wanachostahili: ukweli kamili kuhusu suala hilo.
Nimalizie makala hii kwa kumpongeza Rais Dkt Magufuli kwa kuwakumbusha watendaji wote wa serikali kuwa “zama za nchi kujiendesha yenyewe (autopilot) zimekwisha, na sasa ‘Hapa Ni Kazi Tu’.” Kwamba kiongozi atakayezembea atatumbuliwa bila kuonewa haya. Kadhalika, hongera nyingi kwa Rais wetu kwa kuweka mbele zaidi maslahi ya taifa kuliko maslahi binafsi, umekubali lawama kuliko fedheha. Mwenyezi Mungu akulinde katika utendaji kazi wako, wenye hila mbaya washindwe na uendelee kuwatumikia Watanzania kwa uwezo wako wote.

Mungu Mbariki Rais wetu Dkt John Magufuli.
Mungu Wabariki Watanzania wote wenye kuitakia mema nchi yetu.

Mungu Ibariki Tanzania.

16 Jun 2013


Washington- Rais Obama atapokwenda Afrika Kusini mwa Sahara mwezi huu, taasisi zenye jukumu la usalama wake hazifanyi lelemama.

Mamia wa mashushushu wa Kikosi cha Ulinzi wa Rais wa Marekani (US Secret Service) watasambazwa katika maeneo ya usalama huko Senegal, Afrika ya Kusini na Tanzania. Manowari ya Jeshi la Vita la Marekani inayotumika kubeba ndege za kivita au nyambizi, ikiwa na matabibu waliokamilika, itakuwa imeegeshwa pwani kwa ajili ya dharura.

Ndege za kijeshi za kubeba mizigo zitasafirisha magari 56, ikiwa ni pamoja na 'limousines' 14 na magari ya mizigo matatu yote yakiwa na makasha ya vioo visivyopenya risasi vitakavyowekwa katika madirisha ya hoteli atakazofikia Obama na familia yake. Ndege za kivita zitakuwa 'zikizurura' angani kwa zamu, kuwezesha ulinzi wa masaa 24 katika 'anga ya Rais' ili ziweze kuchukua hatua pindi ndege ya adui itakapoingilia kati.

Maandalizi haya mahsusi ya kiusalama-ambayo yataigharimu Serikali ya Marekani makumi ya mailioni ya dola- yapo kwenye nyaraka ya siri iliyopatikana kwa gazeti hili (la Washington Post). Wakati maandalizi hayo yanaendana na mengineyo katika safari nyingine, nyaraka husika inatoa picha ya jitihada za hali ya juu katika kumlinda Amiri Jeshi Mkuu wa wa majeshi ya Marekani anapokuwa ziarani nje ya nchi hiyo.

Safari yoyote ya Rais, kama za wiki hii huko Ireland ya Kaskazini na Ujerumani, zina changamoto na gharama kubwa kilojistiki.Lakini safari hii ya Afrika inakuwa ngumu zaidi kutokana na sababu mbalimbali, na inaweza kuwa yenye gharama zaidi kuliko zote katika utawala wa Obama, kwa mujibu wa watu walio karibu na maandalizi hayo.

Famili ya Obama inatarajiwa kutembelea nchi hizo tatu kuanzia June 26 hadi Julai 3 ambapo maafisa wa Marekani ndio watakaokuwa na jukumu la kuhudumia takriban kila kitu, badala ya kutegemea hudma za polisi, jeshi na hospitali katika nchi wenyeji.

Rais Obama na mkewe pia WALIPANGA KUFANYA ZIARA KWENYE MBUGA ZA WANYAMA ('SAFARI' kwa Kiingereza), ambayo ingehitaji kikosi cha kupambana na mashambulizi dhidi ya Rais kubeba silaha maalum zenye risasi maalum za kumudu kuwaangamiza duma, simba na wanyama wengine hatariu wa mwituni endapo wangekuwa tishio, kwa mujibu wa nyaraka hiyo 

Lakini maafisa walisema Alhamisi kuwa ZIARA HIYO (YA MBUGANI) IMEAHIRISHWA [ NA HII NDIO SABABU ILIYOPELEKEA UZUSHI WA BAADHI YA MABLOGA KUWA ZIARA YA OBAMA KUJA TANZANIA IMEFUTWA] na badala yake imeandaliwa ziara ya kutembelea Kisiwa cha Robben pembezoni mwa pwani ya Cape Town, Afrika Kusini, ambapo Nelson Mandela alifungwa kama mfungwa wa kisiasa.

Gazeti hili lilipowauliza maafisa wa  Ikulu ya Marekani (White House) kuhusu ZIARA YA MBUGANI ('safari') mapema mwezi huu,walisema hawajafikia uamuzi wa mwisho kuhusu suala hilo.Afisa mmoja wa Ikulu hiyo alieleza Alhamisi kuwa kufutwa kwa ziara hiyo ya mbugani hakukuhusiana na udadisi uliofanywa na gazeti hili hapo awali.

"Hatuna nyenzo zisizo na ukomo kufanikisha safari ya Rais, na tumeipa kipaumbele ziara ya Kisiwa cha Robben badala ya ziara ya MASAA MAWILI mbugani nchini Tanzania," alieleza msemaji Josh Earnest. "Kwa bahati mbaya, hatuwezi kufanya mambo yote mawili." [HEBU ANGALIA HAPA JINSI BLOGA HUSIKA ALIVYOCHAPIA SENTENSI HIYO NA HATA JINA LA MSEMAJI HUYO WA IKULU]

Nyaraka za ndani za kiutawala zilizosambazwa mwezi April zilionyesha kuwa familia ya Obama ilipanga kufanya ziara zote mbili- ya mbugani na kisiwani, kwa mujibu wa mtu anayefahamu maandalizi hayo.

Marais wa zamani, Bill Clinton na George W. Bush pia waliwahi kufanya ziara za mataifa mbalimbali ya Afrika, ambazo zilihitaji maandalizi magumu kama haya. Bush alikwenda mwaka 2003 na 2008, akiambatana na mkewe katika safari zote hizo. Mabinti wawili wa Bush pia walisafiri naye katika ziara ya kwanza, ambayo ilijumuisha 'safari' kwenye hifadhi ya wanyama katika mpaka wa Botswana na Afrika Kusini.

"Hata katika nchi zilizoendelea za Ulaya ya Magharibi, kiwango cha huduma kinachohitajika kwa ajili ya ziara ya rais ni cha hali ya juu," alisema Steve Atkiss, ambaye alikuwa mwandaaji wa ziara akiwa msaidizi maalum wa hudma kwa Bush. "Kadri unavykwenda mbali zaidi, katika maendeo yenye maendeleo duni, kwa hakika ni changamoto ya kilojistiki."

Ikulu ya Marekani na Mashushushu wa Secret Service wamekataa kuzungumzia mipango ya kiusalama, na wasiaidizi wa kiutawala wametahadharisha kuwa maandalizi ya safari ya rais hayajahitimishwa.

Safari za nje za Obama zinakuja wakati taasisi za serikali, ikiwa pamoja na Secret Service, zinapambana na kukata matumizi kwa lazima. Walinzi hao wa Rais walilazimika kukata dola milioni 84 katika bajeti yao ya mwaka huu, na mwaka huu Idara hiyo ilifuta ziara za wageni kutembelea Ikulu ya Marekani (kiutalii) ili kuokoa dola 74,000 kwa wiki ambazo ni gharama za watumishi kufanya kazi nje ya muda (overtime).

Taarifa nyingi kuhusu ziara za Rais nje ya nchi hufanywa siri kwa sababu za kiusalama wa taifa, na kuna ufahamu kidogo  tu kwa umma kuhusu gharama za jumla. Ripoti kutoka Ofisi ya Uwajibikaji wa Serikali ilionyesha kuwa ziara ya Clinton barani Afrika mwaka 1998 alipozuru nchi sita iliigharimu Serikali ya Marekani angalau dola miloni 42.7.Kiwango hicho kilitumika zaidi na Jeshi, ambalo lilifanya safari 98 kusafirisha watendaji na magari,na kuandaa maendeo ya dharura za kimatibu katika nchi tano.

Kiwango hicho hakikujumuisha gharama za Secret Service ambazo zinachukuliwa kama siri.

Ziara ya Obama inaweza kugharimu kati ya dola milioni 60 hadi milioni 100 kwa kuzingatia gharama za safari za nyuma barani Afrika. Nyaraka ya Secret Service kuhusu ziara hiyo,ambayo ilionwa na gazeti hii, iliyowasilishwa na mtu anayeguswa na gharama za ziara hiyo, haikuonyesha Idara hiyo itatumia kiasi gani cha fedha.

"Miundombinu inayoambatana na ziara za Rais zipo nje ya uwezo wetu," alisema Ben Rhodes, Naibu Mshauri wa Usalama wa taifa wa Obama katika mawasiliano ya kimkakati. "Mahitaji ya kiusalama hayapangiw na Ikulu, hupangwa na Secret Service."

Maafisa wa zamani na wa sasa wa usalama wa serikali waliohusika na ziara za rais walibainisha kuwa watendaji wa Ikulu nao husaidia katika kuainisha mahitaji hayo, kwani hupanga sehemu za kutembelea na mipaka yake. Secret Service na Jeshi hufuatilia maandalizi hayo ya ziara yaliyowasilishwa kwao kwa kutaja mahitaji ya kiusalama.

Maafisa wa Ikulu ya Marekani wamesema kuwa dhamira ya ziara hiyo imekuwepo kitambo sasa, na itakuwa ya kwanza kwa Obama kama Rais kutembelea Afrika Kusini mwa Sahara licha ya 'kusimama' kwa masaa 22 nhini Ghana kwa msaa 22. Demokrasia changa zilizomo kwenye ratiba ya ziara hiyo ni washirika muhimu wa kiusalama katika eneo hilo, Rhodes alisema.

Obama atafanya mikutano na kila kiongozi wa nchi atakayotembela kwa minajili ya kujenga ushirikiano bora wa kiuchumi katika wakati huu ambapo China inawekeza vya kutosha barani Afrika. Pia atapigia mstari  programu za afya, ikiwa ni pamoja na mapambano dhidi ya Ukimwi.

Mke wa Rais, ambaye alitembelea Afrika Kusini na Botswana bila ya mumewe mwaka 2011, atashiriki kwenye baadhi ya amtukio katika ziara hiyo. Hilo pia ni changamoto la kilojistiki kwa vile naye atahitaji maandalizi tofauti ya kiusalama kuhusu walinzi na magari, kwa mujibu wa nyaraka hiyo.

Msemaji wa Secret Service, Ed Donovan, alikataa kuzungumzia maandalizi ya ziara hiyo. "Siku zote huwa tunatoa kiwango stahili cha ulinzi kutengeneza mazingira salama," alisema.

Kwa mujibu wa nyaraka ya Secret Service, Obama atakaa siku moja Dakar, Senegal, siku mbili Johannesburg,Afrika Kusini, na siku moja Dar es Salaam, Tanzania.

KATI YA MAGARI 56 KWA AJILI YA ZIARA HIYO NI 'LIMOUSINES' KWA AJILI YA RAIS NA MKEWE , GARI MAALUM LA MAWASILIANO YA SIMU NA VIDEO, GARI LA KUZUWIA MAWASILANO YA MAWIMBI (FREQUENCIES) YA RADIO KUZUNGUKA GARI LA RAIS, GARI LILILOJITOSHELEZA LA WA WAGONJWA (ambulance) AMBALO LINAMUDU KUKABILIANA NA MAAMBUKIZI YA KIBAIOLOJIA NA KIKEMIKALI NA GARI LA VIFAA VYA MIONZI YA X-RAY

Mashushushu wa Secret Service husafirisha magari kama hayo, pamoja na vioo vya kuzuwia risasi, katika ziara nyingi, ikiwa ni pamoja na zile za ndani ya Marekani, msemaji wa Ikulu alieleza. Lakini kwa vile kuna nchi tatu zinazohusika katika ziara hiyo, kunahitajika seti tatu za maandalizi hayo,kwa sababu hakuna muda wa kutosha wa kuhamisha vifaa, kwa mujibu wa nyaraka hiyo.

Mashushushu 100 wanahitajika kama 'waangalizi' - kumudu maeneo ya kumzunguka Rais- katika kila mji atakaozuru. 66 wanahitajika kumpokea Obama jijini Dar es Salaam. Kabla 'safari' ya Mbuga ya Taifa ya Mikumi haijaahirishwa wiki iliyopita, ziada ya mashushushu 35 ilijumuishwa kwenye maandalizi hayo ili kumlinda Rais, mkewe na mabinti zao wawili, kwa mujibu wa nyaraka hiyo.

Kadhalika, kati ya mashushushu 80 hadi 100 watasafiri na kufanya kazi kwa shifti kwa masaa 24, kwa ajili ya ulinzi wa Obama na familia yake, vikosi vya kupambana na mashambulizi (counterassault teams) na waandaaji wa lojistiki.

Nyaraka hiyo ya maandalizi ya ziara haionyeshi idadi ya mashushushu watakaohusika na ziara hiyo, japo baadhi watafanya kazi katika kituo zaidi ya kimoja.

Maafisa walisema Secret Service haitaki ziara ya Rais pasipo kituo cha hali ya juu cha jirani cha kukabili maradhi. Kitengo cha utabibu cha Ikulu hufanya maamuzi kuhusu hospitali gani Rais awapo ziarani nje ya nchi kinakidhi viwango, kwa kufanya ziara kwenye nchi husika, maafisa walieleza.

Katika nchi zinazoendelea, Jeshi la Majini la Marekani huweka 'hospitali inayoelea' kwenye manowari ya kubeba ndege au nyambizi, jirani.

"Hivi  ndivyo inavyohitajika kuilinda taasisi ya  urais wa Marekani," alisema Atkiss kuhusu mahitaji husika, "pasi kujali nani ni rais."


6 Aug 2011


Kwanza nitoe ufafanuzi wa neno "Dola ya Kiusalama", ambalo ni tafsiri yangu isiyo rasmi ya security state.Kwa kifupi,dola ya kiusalama inaruhusu bughudha na unyanyasaji kwa wananchi wasio na hatia kwa kisingizio cha maslahi ya usalama wa taifa.

Kwa makusudi,Tanzania yetu inaelekea kurejeshwa kwenye zama hizo za wanausalama kupewa ruhusa ya kumbughudhi mwananchi yoyote yule kwa kisingizio cha "kusaka taarifa za kiusalama." Of course,sheria za nchi zinavipatia mamlaka vyombo vya usalama kufanya uchunguzi wao katika namna inavyoweza kutafsiriwa kama unyanyasaji wa wananchi,lakini hilo si tatizo kubwa iwapo uchunguzi huo unafanyika kwa maslahi ya umma.

Taarifa nilizonazo ni kwamba wanausalama wetu wameanza kuwasumbua baadhi ya wananchi wasio na hatia wakishinikiza kufahamu "chanzo cha tetesi za ufisadi mkubwa huko JWTZ".Usidhani kuwa wanasaka chanzo hicho kwa minajili ya kusaidiana nacho katika uchunguzi wa suala hilo (kama upo).Wanataka kumfunga mdogo.

Huu ni uhuni wa kitaaluma.Kama huyo anayetuhumiwa kukibwa fedha za umma anaona amekashifiwa,kwanini asiende mahakamani?Nini kinafichwa katika suala hili?Natambua kuna wanaodai kuwa suala hili ni nyeti sana na linaweza kupelekea uasi huko jeshini (ambapo asilimia kubwa ya askari wanaishi maisha magumu kulinganisha na makamanda wao).Lakini hoja hiyo haina uzito kushinda ukweli kwamba fisadi ni fisadi,awe raia au kamanda wa jeshi,na hatua za kisheria lazima zichukuliwe dhidi yake.

Watawala wanataka kulificha suala hili chini ya zulia.Lakini itambulikwe kuwa tunaishi zama tofauti na huko nyuma.Iwapo suala hili halitashughulikiwa kikamilifu na kiuadilifu,basi wahusika wakae wakijua kuwa kuna siku litalipuka upya.

Na nyie mnaojaribu kunyanyasa wananchi kuwashinikiza wawaambie vyanzo vya tetesi za ufisadi jeshini ACHENI MARA MOJA.Hatupendi kuharibu hadhi ya nchi yetu kwa nchi na taasisi wafadhili lakini mkiendeleza uhuni huu tutashawishika kuweka hadharani jinsi mnavyojaribu kufunika ufisadi kwa kuwanyanyasa wanaoibua taarifa hizo.

Nimechukua hatua zaidi kwa kum-tweet Rais Jakaya Kikwete (@jmkikwete) kama invyoonekana mwanzoni mwa makala hii.

5 May 2011


Makala yangu katika toleo la wiki hii la jarida maridhawa la Raia Mwema inafanya uchambuzi linganifu kuhusu,kwa upande mmoja,tuhuma zilizomwandama Rais Obama kuwa sio raia wa Marekani,na hatimaye uamuzi wake kutoa cheti chake cha kuzaliwa,na kwa upande mwingine ni tuhuma za ufisadi zinazomwandama Rais Kikwete,na jinsi kutochukua hatua kadhaa kunazifanya tuhuma hizo kuwa na uzito.

Kadhalika,makala hiyo inawagusa jamaa zangu wa Usalama wa Taifa,kwa kuangalia wnavyofanikisha upatikanaji wa taarifa zinazowahusu wanasiasa wa CCM wanaotajwa kama magamba.Lakini ninaibua maswali kadhaa huku nikiwatahadharisha kuhusu uwezekano wa kuzua skandali kama ile ya Watergate ya nchini Marekani ambapo Rais Nixon,pamoja na mambo mengine alitumia nafasi yake kuamrisha ukusanyaji wa taarifa za kiintelijensia dhidi ya wapinzani wake wa kisiasa.

Pamoja na makala hiyo unayowaza kuisoma kwa KUBONYEZA HAPA,jarida hili la Raia Mwema limesheheni habari na chambuzi za kiwango cha juu kabisa. 


23 Oct 2010



Makala yangu katika jarida la Raia Mwema toleo la wiki iliyopita ililenga kuchokoza mjadala kuhusu "mashushushu".Nilijaribu kutengeneza mazingira ya kumwezesha msomaji kuhitimisha iwapo madai ya mgombea urais kwa tiketi ya Chadema,Dokta Wilbroad Slaa,kuwa Serikali ya Rais Jakaya Kikwete imesambaza Maafisa Usalam wa Taifa nchi nzima ili wamsaidie Kikwete kurejea Ikulu (wachakachue kura).Katika toleo la wiki hii la jarida hilo,jamaa mmoja anayejiita Almas Kajia ametoa majibu kwa niaba ya Idara yab Usalama wa Taifa.Nasema "anayejiita" kwa vile ameshindwa japo kuweka barua pepe yake au namba ya simu just in case ningehitaji kumjibu one to one.

Anyway,naomba nichapishe makala yake nzima,japo unaweza pia kuisoma katika jarida la Raia Mwema.

Kazi ya mashushushu ni usalama si kuhujumu uchaguzi
Almasi Kajia
Oktoba 20, 2010
RAIA Mwema namba 155 la Oktoba 13-19, 2010 liliandika makala iliyokuwa ikiuliza kama mashushu hutumiwa kuhujumu uchaguzi.
Makala hiyo iliyochapishwa katika safu hii ya Raia Mwema Ughaibuni ya Evarist Chahali anayeishi Uskochi, ilikuwa na kichwa kidogo cha habari “Dk. Slaa aibua madai fikirishi”.
Mashushu ambao mwandishi anaulizia kama wanaweza kutumiwa kuhujumu uchaguzi ni maafisa Usalama wa Taifa wa Tanzania na uchaguzi anaozungumzia ni Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31, 2010.
Katika makala yake, mwandishi ameanza kwa kujisifu kwamba ana ufahamu wa kutosha juu ya Usalama wa Taifa au intelijensia, ameisomea fani ya Usalama wa Kimataifa na kwamba anaijua vizuri Idara ya Usalama wa Taifa ya Tanzania.
Pamoja na sifa, tambo na majigambo yote haya, mwandishi anasema anachojaribu kuandika hakisemeki au hakizungumziki na anasema kwa kutekeleza kile anachotaka kukifanya lazima tujiulize maswali magumu na pengine ya kuogofya.
Napenda niseme kwamba kuanzia mwanzo kabisa katika kupitia makala yote ya mwandishi huyu hakuna chochote alichoandika ambacho hakizungumziki na hakuna swali lolote gumu wala la kuogofya ambalo amelidhihirisha katika makala yake.
Nilichogundua katika makala yake ni kuwa kama huo si mtindo wake wa kuwavutia wasomaji napenda kuamini kwamba yeye ni mshika bango wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na ameendeleza tu yale yanayofanywa na chama hicho yasiyofurahisha kila mtu, ni mambo yanayorandana na afanyayo Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na mgombea urais kupitia chama hicho, Dk. Willibrod Slaa.
Hata hivyo, ameeleza mambo ya msingi sana katika kuthibitisha kwamba amejifunza fani ya usalama wa kimataifa kwa kusema kwamba uimara wa taifa lolote duniani unategemea uimara wa idara yake ya usalama wa taifa na kulegalega kwa mambo katika nchi yoyote duniani kunaashiria upungufu wa idara hiyo.
Lakini katika hali ambayo sikutarajia, mwandishi anakiri kwamba kwa miaka mingi sasa, Idara ya Usalama wa Taifa ya Tanzania ni miongoni mwa idara bora duniani. Hilo pengine lilitokana na maelezo yake kwamba anaifahamu vya kutosha Idara hiyo.
Wapo waandishi wengine ambao wamekuwa wakiandika habari kama hizo, lakini wakiwa na mitazamo inayotofautiana. Jambo ambalo linanishangaza au pengine linanitia shaka katika makala yake ni kama Idara anayoisifu hivyo imekwishakupoteza sifa hizo na kama ni hivyo je, hiyo ndiyo sababu ya yeye kuanza kuwa na shaka kama Idara hiyo sasa inaweza kutumika kuhujumu matokeo ya uchaguzi?
Amesema idara ya usalama wa taifa duniani kote hufanya kazi kwa siri kubwa kabisa na usiri huo ni sehemu ya utekelezaji wa kazi zake. Anasema usiri ni muhimu kabisa na wa lazima katika ukusanyaji wa taarifa nyeti.
Jambo ambalo wasomaji walitakiwa walijue kutoka kwa mwandishi ni ikiwa usiri wa Idara ya Usalama wa Taifa ndio utakaotumika kuhujumu matokeo ya uchaguzi na kama hilo ndio lengo ni kwa nini Idara hiyo ifanye hivyo, kwa kutumiwa na CCM au kwa utashi wake yenyewe?
Mwandishi amezitaja nchi za Uingereza na Marekani kama mifano kwamba mara chache wakuu wa vyombo vya intelijensia huitwa kutoa ufafanuzi kwa mambo yanayohusu usalama wa Taifa wa nchi hizo.
Kwamba aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Central Intelligence Agency (CIA) ya Marekani, George Tennet aliitwa kueleza juu ya ushahidi kwamba Iraki ilikuwa na mipango ya kutengeneza silaha za maangamizi.
Anasema katika nchi hizo mbali na kuondoa katika orodha baadhi ya mambo ambayo ni siri, mabunge yao yana kamati zinazoshughulikia masuala ya usalama na zinawaita viongozi wa idara hizo kutoa ufafanuzi katika masuala yanayohusu intelijensia pale inapokuwa lazima kufanya hivyo.
Suala hili halifanyiki kwa siri anayoizungumzia mwandishi na kama nia yake ingekuwa ni kulifahamu hilo angemuuliza Dk. Slaa ambaye amekuwa mbunge kwa miaka 15 na anafahamu kwamba ipo Kamati ya Bunge ambayo inafanya kazi kama zile zinazofanywa na mabunge ya Uingereza na Marekani.
Amerejea swali lake kama Idara ya Usalama wa Taifa inaweza kutumiwa na CCM kuhujumu uchaguzi na akaunganisha masuala mengine mawili kwamba; hakuna ofisa usalama atakayefurahi na tuhuma za Slaa zikibainika kama ni uongo na Watanzania watakuwa na hofu kama itabainika kwamba tuhuma hizo ni za kweli.
Swali kwamba Idara ya Usalama wa Taifa ilikuwa wapi wakati ukitokea ujambazi wa EPA na je, Idara hiyo ilikuwa ikifanya nini wakati mikataba ya kifisadi ikitokea. Mwandishi anajihami mapema kwa kusema kwamba maswali haya yatazua uhasama kati yake na idara hiyo.
Labda niseme tu kwamba si maofisa wa Idara ya Usalama tu watakaochukia bali Watanzania hawatafurahi kuona tuhuma hizi za Dk. Slaa ambazo ni za uongo zinazidi kuendelezwa na watu wenye hadhi za kisomi kama mwandishi mwenyewe kwa ahadi ambazo nina hakika hazitatimia.
Wananchi wa kawaida ambao wamekwishakuelewa kwamba Chadema ina tabia ya kuzua mambo na ambao wanaamini kwamba nchi hii ina ulinzi wa kutosha, hawawezi kuingiwa na hofu kwa kutegemea tu propaganda za askari wetu kutoka Uskochi.
Ninachotarajia mimi ni kwamba Idara ya Usalama wa Taifa haitamjibu mwandishi. Nililo na uhakika nalo ni kwamba itanyamaza bila kusema chochote kwa kuwa mwandishi mwenyewe amesema kuwa Idara hiyo inafanya kazi zake kwa siri kubwa kabisa.
Ninahisi kwamba mara zote Idara hii inaacha wajinga wajielimishe wenyewe. Swali kwamba Idara ya Usalama wa Taifa ilikuwa wapi wakati ufisadi wa EPA ukitokea sio la msingi bali jambo la muhimu ambalo Mtanzania wa kawaida anaweza kusema ni kwamba suala la EPA limeshughulikiwa sana na Serikali na baadhi ya wahusika wamefikishwa mahakamani.
Naamini kwamba ufisadi si sera ya Serikali wala ya Chama tawala-CCM- na ni vyema ikubalike kwamba, kwa sasa pengine tofauti na ilivyokuwa huko nyuma, ufisadi ni suala la mtizamo na hulka ya mtu kuliko kuonekana kama mtindo wa maisha wa baadhi ya Watanzania.
Serikali ya Tanzania inazingatia utawala wa sheria na tungejali sana suala la mtu kumiliki vitu kama gari, nyumba nzuri, vitu ambavyo wengine hawana, mtu huyu akaonekana kuwa fisadi, Watanzania wengi wangeishia jela.
Amezungumza mengi ikiwa ni pamoja na ikiwa Msajili wa Vyama vya Siasa ambaye shughuli zake si za siri anaonyesha wazi kuipendelea CCM kwa kuingilia majukumu ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi, hali ikoje katika Idara ya Usalama wa Taifa.
Nilijaribu kuhoji pale mwanzo kama mwandishi alikuwa anahisi nini juu ya usiri aliousifia sana, usiri wa Idara ya Usalama wa Taifa, kama usiri huo ndio utatumika kuhujumu matokeo ya uchaguzi.
Kinachojidhihirisha hapa ni kwamba mwandishi anataka Watanzania waamini kwamba Idara ya Usalama wa Taifa kwa kutumia kigezo cha usiri, inaingilia Tume ya Taifa ya Uchaguzi kama alivyofanya Msajili wa Vyama vya siasa kwa nia ya kuhujumu matokeo ya uchaguzi (kama kweli alifanya hivyo).
Inaonekana anaamini kwamba usiri huu ndiyo utakaotumika kukipatia ushindi CCM kwa kuihujumu Chadema.
Lakini kila mtu anajua kwamba kazi ya Idara hiyo kama chombo cha usalama ni kuhakikisha Usalama wa Taifa ambao ni pamoja na uchaguzi kuendeshwa kwa amani, si kuuhujumu.
Inavyoonekana, mwandishi mara zote anaiangalia Idara ya Usalama wa Taifa kama chombo chenye uamuzi wa mwisho kwa kila kitu na anasema kwamba Idara hiyo inamfahamu mmiliki wa Kagoda, ama kwa njia zisizo rasmi au njia rasmi.
Hivi kama kweli kazi za Idara hiyo ni za siri ni vipi itathubutu kutekeleza au hata kama imetekeleza, ieleze wazi kwamba imefanya hivi na hivi kwa watuhumiwa wa aina yoyote, achilia mbali wa Kagoda.
Binafsi nina shaka juu ya uelewa wake wa usalama wa kimataifa na ufahamu wake juu ya Idara hii ambayo anadai ni moja ya idara bora duniani na inayotenda kazi zake kwa usiri.
Ni utaalamu gani anaozungumzia mwandishi unaoweza kutumika kushinikiza Serikali kwa njia zilizo rasmi na zisizo rasmi. Nimejaribu kudadisi kwa wajuzi wa masuala ya Usalama wa Taifa, nikaambiwa kwamba kazi ya idara hiyo duniani kote ni kutoa ushauri na si kushinikiza kama mwandishi anavyotaka tuamini.
Nilitaka kujua kama ameifahamu Idara hiyo vipi kwa kuhadithiwa au pengine alishawahi kuwa mtumishi kwenye chombo hicho nyeti? Kwa yote mawili nilipata jibu moja kwamba hata kama alihadithiwa au alifanya kwenye Idara hiyo, kulingana na kanuni za usiri ambao ameukiri yeye mwenyewe, hawezi kusimama hadharani na kusema kwamba amekuwa mtumishi wa chombo hicho.
Anasema pia kwamba idara ya usalama wa taifa kote duniani ni kama nusu jeshi (paramilitary) na viongozi wake wanaogopwa kupindukia na uamuzi wao hauhojiwi.
Katika udadisi wangu, niliambiwa mambo mawili kwamba kuogopwa kupindukia kunatokana na usiri wa idara zenyewe na nikaamini kwamba usichokijua ni sawa na usiku wa giza.
Kwamba wanaoiogopa idara ni wasioifahamu na anachotaka kusema mwandishi ni kwamba wasomaji waendelee kuiogopa Idara yao ya Usalama wa Taifa.
Nafikiri hilo si la lazima kwa sababu wananchi wana haki ya kukifahamu chombo ambacho kwanza kinahakikisha kuwa Taifa ni salama na kinatumia kodi za wananchi katika utendaji wake wa kazi wa kila siku. Hakuna sababu ya kukiogopa, ni chombo chao na ambacho kimewekwa kisheria.
Mwandishi ametaka pia wasomaji wake wapime madai fikirishi ya Dk. Slaa ambayo yametolewa kama tuhuma ikiwa hadithi au ni kitu kinachowezekana. Ukiyavulia nguo maji sharti uyakoge na kwa hilo mwandishi haamini kwamba anachosema Dk. Slaa ni hadithi tu, anaamini kwamba ni ukweli ingawa hoja yake imejengwa katika nadharia tu.

Ukisoma kwa makini utagundua kuwa Bwana Almasi Kajia (tukiamini kuwa hilo ndilo jina lake halisi) ameelemea zaidi kwenye kujadili wasifu wangu kama mwandishi badala ya kujibu maswali muhimu niliyotoa katika makala ya mwanzo.Lakini kwa vile sipendi malumbano,naweza kufupisha kwa kuhitimisha kuwa makala yake imeshindwa kuthibitisha kuwa HAIWEZEKANI IDARA YA USALAMA WA TAIFA KUTUMIWA NA SERIKALI YA KIKWETE KUCHAKACHUA KURA.Yah,anaweza kusema madai ya Dokta Slaa ni nadharia kwa vile hata fedha za EPA zilipoibiwa tuliambiwa kuwa huo ni uzushi tu (na wahusika wakatishia kumfikisha Dokta Slaa mahakamani).

Haihitaji taaluma ya usalama japo wa mgambo kutambua kuwa fedha za EPA ziliibiwa wakati taasisi zenye jukumu la kuzuwia zikiwa kazini.Mkataba wa kitapeli wa Richmond ulisainiwa wakati wenye jukumu la kuuzuwia wanakenua meno tu.Same story kuhusu Kiwira,IPTL,Buzwagi,Meremeta,Tangold na skandali nyingine za ufisadi.

Wakati naandaa makala hiyo sikutegemea pongezi kutoka kwa wahusika.Nafahamu kuwa hawapendi kukosolewa sio kwa vile wako sahihi bali wanatambua kuwa aina yoyote ile ya ukosoaji inawafumbua macho kuonyesha udhaifu na mapungufu yao.Na hawataki hilo lijulikane kwa vile linaweza kupelekea Nguvu ya Umma kudai majibu kwa nguvu.

Mafisadi wangependa sana kuona kila Mtanzania akiwa mbumbumbu.Wanasali kwa bidii kusijitokeza wahaini wa kuhoji maswali magumu.Si mmesikia tishio kwa gazeti la Mwananchi kwa vile tu haliandiki kile watawala wamezowea kusikia?Wameleweshwa na sifa kiasi kwamba ukiwakosoa ni sawa na kuwatukana.

Finally,naomba kuthibitisha kuwa nilipoandika kuwa naifahamu taasisi hiyo vizuri nilikuwa na sababu zangu za msingi.Sihitaji kufafanua kwa vile hayo ni mambo binafsi.Lakini they and I know very well kuwa hilo la kuifahamu vyema halina ubishi.Mambo mengine hayawezi kuzungumzwa hadharani.

Nilichofarijika ni kile alichowahi kutamka Rais wa zamani wa Marekani,George W.Bush kwamba "ukisema au kufanya jambo flani,kisha watu waka-react basi ujue ulichoongea kimewagusa" maana laiti ingekuwa upumbavu au uzushi tu,Bwana Almasi asingepoteza  muda wake kunijibu.

AJIKUNAYE UJUE KAWASHWA

14 Oct 2010


Awali nilitundika taarifa ifuatayo baada ya kuiona huko Jamii Forums kabla ya post husika kufutwa.Mzembe mmoja akanitumia email akidai mie ndio mtunzi wa taarifa hiyo.Mchumia tumbo huyo alikuwa na kila sababu ya kukasirika just like mafisadi wanavyokasirika kusikia uwezekano wa Dokta Slaa kuingia Ikulu baada ya Uchaguzi hapo Oktoba 31.Anyway,naiwasilisha tena kama ilivyo (lengo sio kumridhisha huyo mzushi aliyenituhumu bali kusambaza ujumbe husika)

Taarifa ya Siri-Mikakati ya Kuiba Kura Inavyoendelea
From:
From:
To Journalists   


To:Yahya Mkombe ; Yahya Charahani ; Waziri Kindamba ; Tobias Nsungwe; Thisday [The Editor] ; Theodatus Muchunguzi ; Tanzania Daima ; Tanzania Daima ; Sweya ; Stephen Ernest Kasambo ; Stella Mchiwa ; Stanslaus Kirobo ; Sosthenes Paulo Mwita ; Sofia Machagga ; Siyovelywa Hussein; Sisa Suzy ; Simon Mkina ; Simbaulanga ; Siahanna; Sherbanu Mussa ; Sauli Giliard ; Sarah Mwaga ; Sani; Samson Mwigamba ; Salehe Mohamedi ; Said Michael ; Saed Kubenea ; Rusibamayila ; Ruhazi Ruhazi ; Rookie ; Robert Nyimbo ; Richard Lupembe ; Reginald Simon Miruko ; Ramadhani Semtawa; Raia Mwema ; Prudence Karugendo ; Privatus Karugendo ; Peter Nyanje ; Patien Celkanah ; Paschally Mayega ; Othman Juhudi; Oscar Mkoma ; Oneo Yolazi ; Omari Kaseko ; Omar; Nthelezi Nesaa ; Nombo ; Nkwanzi Nkuzi ; Nikita Naikata; Ngwada ; Ngowe ; News Editor [Thisday] ; News [The Citizen]; Ndyesu ; Ndimara Tegambwage ; Ndesanjo Macha ; Nathan; Nadra Mussa ; Mzee Mwanakijiji ; Mwitete ; Mwesigwa; Mwenyekiti wa Baraza ; Mwankemwa ; Mwanahalisi; Mwachapite ; Mutahungurwa ; Musa Ngarango ; Mumba Mabu; Mum China ; Mtoha ; Matinde Nyagonda ; Mary Fwaja; Martin Malera ; Makwaia wa kuhenga ; Majid Mjengwa ; Mabala wa Mabalaa; Lusungu Hemed ; Lula wa Ndali Mwanzela ; Lukawe ; Ludger Bernard Nyoni ; Lucy Ngowi ; Lucy Mchiwa ; Leo Jasson ; Lawrence Kilimwiko; Laumbe ; Latrix ; Kyembe ; Kwariko Mahmoud ; Kumburu ; Kobelo ; Kiwango ; Kitambo Robert: Padre ; Kililui; Kiangosekazi wa nyoka ; Kevin Makyao ; Kaselema Luhanga; Kambi Mbwana ; Kally ; Kagomba ; Kady Fanny; Julius Samwel ; Joseph Petro ; Joseph Moses Ndumbaro ; Joseph Mgullo; Joseph Kulangwa ; Joseph Kulagwa ; Johnson Mbwambo ; Johnson Mbwambo ; John Mnyika ; Jeff Msangi ; Ipimilo ; Innocent Mwesiga; Ibrahim Lipumba ; Hoja ; Hilda Super ; Herry Gasp ; Henry Kimani ; Hellen [Mama] ; Haruna Sauko Mohamed ; Haruna Sauko Mohamed; Haruna Sauko Mohamed ; Happines Katabazi ; Halifa Shabani ; Hakielimu ; Habibu Miradji ; Habib Miradji ; Godfrey Mogellah ; Gloria William; Gervas Zombwe ; Freddy Macha ; Fred Macha ; Financial Times; Financial Times ; Ezekiel Kamwaga ; Evarist Chachali Uskochi ; Endakig ; Emmanuel Elias ; Elias Mhegera ; Edward Kinabo; Edison Kamukara ; Duhu Daniel ; Deusdedit Jovin ; Deus Bugaywa ; Deogratius Temba ; Dawson Mongi ; David Mhando ; Dattani ; Daniel Mwaijega ; Coster ; Chesi Mpilipili ; Che Chenjah; Charles Semiono ; Charles Nkwabi ; Charles Mullinda ; Charles Kayoka; Charles G. Mnyeti ; Changamoto ; Changamoto ; Chacha Nyakega ; Catherine Justus ; Carol Njiro ; Bwire ; Bwire; Business Times ; Bollen Ngetti ; Beatrice Kawanara ; Beatrice Kallaghe ; Balinangwe Mwambugu ; Bai ; Ayub Rioba ; Asubuhi Njema; Ansbert Ngulumo ; Angetile Osiah ; Angela Semaya; Angel Tenga ; Amina Emmanuel ; Amani ; Alloyce Komba; Alli Gilla ; Alfred Chonya ; Aghan Daniel ; Adam Lusekelo; Absalom Kibanda ; Abdulhamid Njovu ; Abass Juma Msahaury 
Kama nilivyoipokea nami nawatumia. Napenda kuwajulisha mikakati michafu ya kupora na kuzuia maamuzi ya umma yanayofanywa na ccm kwa uratibu wa usalama wa taifa. Baada ya kubaini dalili za kuanguka vibaya katika uchaguzi wa mwaka huu idara ya usalama wa taifa imeandaa mikakati ya kuiba kura ili kuzuia CHADEMA msiingie ikulu. Mikakati hii inaeleweka vizuri kwa tume ya taifa ya uchaguzi ambayo inashirikiana bega kwa bega na idara ya usalama wa taifa kumtengenezea jk ushindi bandia wa 80%.
Wana hakika watanzania watagundua wizi huo na watakataa matokeo ndiyo maana kwanza waliwatumia viongozi wa dini waliotembelea makao makuu ya CHADEMA wawasihi CHADEMA wakubali matokeo yatakapotangazwa na juzi wamelitumia jeshi kutisha wananchi watakaoamua kupinga matokeo ya kupikwa yanayoandaliwa na NEC/Usalama wa taifa. MAJID KIKULA ambaye ni Government Security Officer ndiye mratibu wa zoezi la kuiba kura, ni mtaalamu aliyebobea katika kazi za aina hii aliratibu vizuri zoezi kama hilo mwaka 2005.
Pia mwaka 2007 alitumwa kenya kwenda kumsaidia Kibaki kupora ushindi wa Odinga. Kikula ww.yahooanatumia muda wake mwingi hivi sasa ofisi za tume ya uchaguzi kwa ajili ya uratibu wa uvurugaji daftari la kudumu la wapiga kura akiifanya kazi hiyo kwa karibu na baadhi ya watendaji wa NEC na maafisa kadhaa wa usalama wa taifa kutoka Kurugenzi ya IT ya idara ya Usalama (DITA) ambao wako ndani ya NEC kwa zaidi ya miezi sita sasa, nitawapatia majina yao.
Pia kuna vijana wataalamu wa IT waliochukuliwa kutoka maeneo mbalimbali wamepewa nyumba upanga mtaa wa Undali. Shughuli kubwa wanayofanya ni kuandaa utaratibu wa ku-access remotely daftari la kudumu la wapiga kura. Hawa wanafanya kazi chini ya SALVA RWEYEMAMU na MINDI KASIGA kutoka Kurugenzi Ya Mawasiliano Ikulu. Wapo vijana kadhaa leo nawapa majina ya wawili; MAHARAGE CHANDE ambaye ni mfanyakazi wa VODACOM na EDGAR MASATU wanafanya kazi kwa karibu na NZOWA wa Idara Ya Usalama ambaye ndiye aliyeratibu shambulio la kumwagiwa tindikali KUBENEA. Pia kuna kundi linalojumuisha wataalamu wa printing wa kiwanda cha uchapaji cha usalama wa taifa kilichopo MALINDI ambao hivi karibuni walikuwa mjini TANGA kwa semina fupi ya jinsi ya kughushi kura kupitia fake ballot paper, timu hii inaongozwa na Ndg. SINYAU.
Kwa hiyo utaona kwamba imeandaliwa mikakati mingi kuufanikisha uovu huo ili mmoja ukikwama basi mwingine utatumika ila wameamua ni lazima JK ashinde kwa 80%.
Ndani ya Idara Ya Usalama Wa Taifa maafisa wengi wamechoshwa na uongozi mbovu wa CCM hivyo wanataka mabadiliko ya uongozi idara imechukua hatua kadhaa kuhakikisha maafisa wote wa idara wanampigia kura JK, wote wameagizwa kuwasilisha vitambulisho vyao vya kupigia kura ili vinakiliwe namba ili atakayepigia upinzani afukuzwe kazi baada ya uchaguzi.
Fuatilieni kwa karibu haya niliyowaeleza nimeyapata kwa nafasi yangu ndani ya TISS. Huyu KIKULA mfuatilieni kwa karibu ni hatari. HAKIKISHENI DUNIA NA WATANZANIA WOTE WANAJUA MAPEMA HILA HIZI. Jambo la kujiuliza maafisa Usalama Wa Taifa wanafanya nini ndani ya Tume Ya Uchaguzi wakati huu
.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.