Showing posts with label MAGAMBA. Show all posts
Showing posts with label MAGAMBA. Show all posts

1 Dec 2011


Tatizo kuu CCM si mafisadi pekee, bali hata wanaowalea

Evarist Chahali Uskochi

HATIMAYE mchezo wa kuigiza wa “kujivua gamba” umefikia kikomo. Baadhi yetu tulihisi tangu mwanzo kuwa usanii huo haukuwa tofauti na ahadi tamu zinazosheheni kwenye kila ilani ya uchaguzi inayotumiwa na CCM kuombea kura lakini mwisho wa siku ahadi hizo huishia kuwa porojo tu.

Kuna sababu lukuki kwa baadhi yetu kubashiri kwamba kama CCM itafanikiwa kuvua magamba basi chama hicho kitakuwa katika hatari kubwa ya kupoteza uhai wake. Japo magamba yaliyopaswa kuvuliwa na CCM hayakuwa mithili ya yale ya viumbe hai lakini kimsingi kiuhalisia kung’oa gamba la kiumbe kama kobe kunaweza kabisa kupelekea kifo cha kiumbe huyo. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa chama tawala.

Kwa muda mrefu sasa Chama Cha Mapinduzi kimekuwa tegemezi sana kwa watu wenye fedha pasipo kujali watu hao wamepataje fedha hizo. Yayumkinika kabisa kuhitimisha kuwa hata utaratibu usio rasmi kwamba ili kupata nafasi ya uongozi wa kisiasa nchini-hasa kwenye nafasi za udiwani na ubunge-mgombea anapaswa kuwa na mamilioni ya fedha za kununuliwa kura ni matokeo ya CCM kukumbatia wenye fedha, na hatimaye kupelekea uwezo wa kifedha kuwa kigezo muhimu cha ushindi kwa mgombea kuliko uwezo wake kiuongozi.

Lakini sababu kubwa kabisa iliyotengeneza kifo cha ajenda ya magamba tangu siku ya kwanza ni mwasisi wa wazo hilo, yaani Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete. Japo Watanzania tunasifika kwa usahaulifu lakini naamini wengi wetu tunakumbuka jinsi Rais Kikwete alivyopigana kufa au kupona kuwapigia kampenia na kuwatetea kwenye kampeni za Uchaguzi Mkuu uliopita, wanasiasa ambao baadaye waliitwa magamba.

Kikwete alisisitiza kwamba wanasiasa hao ni watuhumiwa tu na hawajafikishwa mbele ya vyombo vya sheria na hivyo hakuona ubaya kusimama majukwaani kuwaombea kura. Alikwenda mbali zaidi na kunadi uadilifu na uongozi wao bora, jambo lililoibua hisia kuwa hakuwa anawasaidia tu kupata kura, bali pia alikuwa anawatengenezea kinga pindi zikitokea jitihada za kuwachukulia hatua.

Ni hivi, laiti watuhumiwa hao wa ufisadi (au magamba) wangefikishwa mahakamani wangeweza kabisa kutumia hotuba za Kikwete kwenye kampeni zao kama utetezi wa tuhuma dhidi yao kwani sote tunajua kuwa kama Rais anaamini watu hao ni safi, basi hakuna hakimu au jaji ambaye angediriki kuwa na mtizamo tofauti.

Kwa lugha nyingine, Kikwete alikuwa akiwapatia watuhumiwa hao wa ufisadi kinga dhidi ya mashtaka ndani na nje ya Mahakama. Na kama wasemavyo Waingereza, hukumu ya umma ina nguvu kubwa zaidi ya hukumu halisi inayotolewa mahakamani. Hapa ninamaanisha kwamba “hukumu ya hawana hatia hadi watiwe hatiani” iliyotolewa hadharani na Kikwete kwa watuhumiwa wa ufisadi ilikuwa na nguvu kubwa kwa umma, hasa katika mazingira ya siasa za umungu-mtu wa Rais.

Kama ambavyo mara kadhaa nimeonyesha kutoelewa anayepaswa kubebeshwa lawama katika baadhi ya maamuzi ya Kikwete ni yeye mwenyewe au washauri wake nilipata tabu kumwelewa alipojipa jukumu la “kuwabeba” watuhumiwa wa ufisadi kwenye kampeni za Uchaguzi Mkuu uliopita. Haikuhitaji busara kwa Rais Kikwete kutambua kuwa wanasiasa hao waliokuwa wakituhumiwa kwa ufisadi hawakuamka tu ghafla na kujikuta wanatuhumiwa bali kulikuwa na mlolongo wa matukio uliowaingia katika tuhuma hizo.

Angeweza kabisa kuepuka hali ya kuonekana anawatetea na laiti busara zingetumika basi angewaachia jukumu la kuomba kura na kujisafisha kwa umma mikononi mwao. Ndiyo maana miezi michache baadaye alipokurupuka na ajenda ya kuwashughulikia watu hao hao aliowasafisha majukwaani ilikuwa ni dhahiri kuwa usanii huo usingezaa lolote la maana.

Lakini kuna kubwa zaidi lililojiri katika vikao vya CCM vilivyomalizika wiki iliyopita mjini Dodoma. Kwa mujibu wa vyombo vya habari, mmoja wa watuhumiwa wa ufisadi aliweka bayana jinsi Kikwete alivyofanya maamuzi ambayo hatimaye yalisababisha mwanasiasa huyo kuishia kuwa mtuhumiwa wa ufisadi. Kwa lugha nyingine, mwanasiasa huyo alikubali kubebeshwa mzigo wa lawama ambao kimsingi ulipaswa kubebwa na Kikwete.

Wakati usanii wa kujivua magamba unashika kasi kwenye vyombo vya habari kulizuka msamiati mpya wa “mapacha watatu” ambao ulimaanisha wanasiasa watatu waliokuwa wakituhumiwa kwa ufisadi na ambao kimsingi ndio walikuwa walengwa wakuu wa ajenda ya kujivua gamba. Wanasiasa hao ni Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, Mbunge wa zamani wa Igunga, Rostam Aziz na Mbunge wa Bariadi Mashariki, Andrew Chenge.

Kwa wanaofuatilia kwa karibu harakati za Rais Kikwete tangu aliposhindwa kwenye mchujo wa kupata mgombea urais kwa tiketi ya CCM mwaka 1985 hadi alipofanikiwa kuingia Ikulu mwaka 1995 ni wazi kuwa “mapacha watatu halisi” ni Kikwete, Lowassa na Rostam ambao kwa pamoja, waliweza kutengeneza mtandao wenye nguvu kubwa uliompa ushindi Kikwete.

Sasa katika mazingira ya kawaida tu, ingewezekanaje Kikwete ambaye kimsingi ndiye mwenye maamuzi ya mwisho ndani ya CCM awasaliti “mapacha wenzie” Lowassa na Rostam? Naomba ieleweke simaanishi kuwa angetaka kwa dhati kufanya hivyo asingeweza.

Nimesema “mazingira ya kawaida” kwa maana ya Kikwete tunayemfahamu sote: mwanasiasa anayeonekana kukumbuka sana fadhila alizofanyiwa na watu waliomsaidia kuingia Ikulu na kiongozi ambaye anachelea sana kuwaadhibu watendaji wake hata pale ambapo kuchelea huko kunaishia kumfanya aonekane kiongozi dhaifu na mwoga wa kuchukua maamuzi magumu.

Laiti Kikwete angetaka “liwalo na liwe” dhidi ya maswahiba zake ambao baadaye alionelea wanapaswa kuchukuliwa hatua ili kuinusuru CCM basi angeweza kabisa kuitumia Idara ya Usalama wa Taifa “kuwaandama” wanasiasa hao kwa minajili ya kuwadhibiti “wasimgeuke au kumdhuru.” Kama ambavyo taarifa za kiintelijensia zinavyosukuma haki za kikatiba za wananchi kuandamana kufinyangwa, basi ingewezekana kabisa kutumia mbinu hiyo kuhakikisha kuwa “magamba yakishang’olewa hayachipui tena.”

Na wala usidhani kwamba kungekuwa na haja ya matumizi ya “mbinu chafu” kuyadhibiti “magamba” bali wahusika wangeweza kukumbushwa “Rais ni nani” kwa njia nyepesi tu ya kile kinachofahamika kama ufuatiliaji wa waziwazi (overt surveillance).

Hii ni mbinu inayotumika kumfikishia ujumbe mlengwa kuwa anafuatiliwa, wafuatiliaji hawajihangaishi kujificha bali wanataka anayefuatiliwa afahamu kuwa anafuatiliwa na hivyo kumdhibiti kufanya jambo lolote lile “baya.”

Kwa hiyo laiti mwasisi wa wazo la kujivua magamba-Rais Kikwete angekuwa na dhamira ya kweli ya kutaka mkakati huo ufanikiwe basi wala kusingekuwa na haja ya Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, kupita huku na kule akiwahadaa Watanzania kuhusu umakini wa suala hilo.

Sina hakika kama Nape alikuwa anafahamu “ngoma aliyokuwa anaicheza” lakini kilicho dhahiri ni kwamba muda huu anatambua kuwa “hakuna mwenye uwezo au uthubutu wa kumtenganisha Kikwete na watu ambao hakufahamiana nao mtaani (bali wametoka mbali pamoja).”

Lakini kifo cha usanii wa “kujivua magamba” kinaweza kutoa fundisho kwa CCM kuacha mtindo wa kudandia hoja za vyama vya upinzani hususan CHADEMA. Wenye kumbukumbu nzuri watakuwa wanafahamu jinsi CCM ilivyopinga kwa nguvu zote madai ya CHADEMA kuwa chama hicho tawala si tu kinakumbatia mafisadi bali pia kimegeuka kuwa kichaka cha kuwahifadhi mafisadi.

Sasa baada ya kuona kuwa CHADEMA inapata umaarufu mkubwa kutokana na msimamo wake thabiti dhidi ya ufisadi, CCM nayo ikakurupuka na ajenda ya kusaka umaarufu ikisingizia inataka kujisafisha. Lakini hata kama chama hicho tawala kungekuwa na dhamira ya dhati kutekeleza mpango huo ingewawia vigumu kufanikiwa kwa sababu ufisadi na CCM ni kama samaki na maji; ukimtoa samaki majini umemuuwa na ukiwaondoa mafisadi CCM basi umeua chama.

Nimalizie makala hii kwa ushauri wa bure kwa chama tawala. Tatizo la msingi si magamba bali aliyeyawezesha magamba hayo kukomaa. Kama ambavyo ni vigumu kudhibiti malaria kwa kugawa vyandarua na dawa za kukinga au kutibu ugonjwa huo pasipo kuangamiza mazalia ya mbu, ndivyo ambavyo ni vigumu kwa CCM kupambana na mafisadi pasipo kuwabana viongozi ambao si tu wapo madarakani kwa msaada wa mafisadi bali pia uhai wao wa kisiasa umewekwa rehani kwa mafisadi hao.

8 Jun 2011






Mafisadi CCM wageuka mbogo

Na Jabir Idrissa - Imechapwa 01 June 2011

SASA ni piga ni kupige ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Wanaotuhumiwa kwa ufisadi, wanakataa kujiuzulu, MwanaHALISI limeelezwa.

Taarifa zinasema walipoitwa mbele ya viongozi wakuu wa chama hicho – makamu mwenyekiti Pius Msekwa na katibu mkuu, Wilson Mukama - wanaoitwa na CCM kuwa “watuhumiwa wakuu wa ufisadi nchini,” walishikilia msimamo kuwa hawawezi kujiuzulu kwa kuwa hawana hatia.

Wanaotakiwa kujiuzulu na viongozi wakuu wa CCM ni Edward Lowassa, Rostam Aziz na Andrew Chenge. Mkutano wa kuwashawishi wajiuzulu, ulifanyika Alhamisi na Ijumaa wiki iliyopita katika ofisi ndogo za chama hicho zilizopo Lumumba, Dar es Salaam.
Taarifa zinasema katika mkutano huo, Msekwa na Mukama waliomba Lowasa ajiuzulu ili kukiokoa chama hicho, lakini yeye alipinga kwa hoja kuwa hana hatia.

MwanaHALISI lilipowasiliana na Msekwa kutaka kufahamu kilichojadiliwa katika mkutano wake na viongozi hao, haraka alisema, “…Umetoa wapi habari hizo?”

Alipoelewa ni vyanzo vya ndani ya chama na serikali, Msekwa alisema, “Hayo ni mambo ya ndani ya chama. Hatuwezi kuyaleta magazetini.”
Lowassa alipoulizwa juu ya kuwapo kwa kikao hicho, alisema ni kweli wamekutana. Hata hivyo, alisema hawezi kueleza walichojadili kwenye vyombo vya habari.

Rostam hakupatikana kueleza upande wake. Hata hivyo, MwanaHALISI limeelezwa na mtoa taarifa wake kuwa mbunge huyo wa Ingunga alitoka kwenye ukumbi wa mkutano akiwa amenuna na kuvurumisha “maneno makali.”

Anasema Rostam alitoka pale akiwa amenuna na kusema yeye hana hatia yoyote na kwa hiyo hastahili kushambuliwa. Amesema yote yanayotokea sasa yanatokana na uadui wa siasa za urais wa mwaka 2005 na ule wa 2015.


Hili linatokea wakati uongozi wa juu wa chama hicho ukishindwa kukabidhi barua ya kuwataka watuhumiwa hao wajiuzulu.
Kuchelewa kwa utekelezaji wa maazimio ya kuwawajibisha Lowassa, Rostam na Chenge kumezaa majungu na umbeya. Hivi sasa taarifa zinasema, Mukama anadaiwa kugoma kuandika barua ya kuwataka watuhumiwa hao kuachia nafasi zao za ujumbe wa Halmashauri Kuu ya taifa (NEC) wanazozishikilia.

Baada ya Mukama kugoma kuandika barua hizo kwa hoja kuwa kilichoamuriwa na NEC hakifahamu kwa kuwa alikuwa hajateuliwa, ndipo Nape Nnauye, katibu wa itikadi na uenezi alipoandika barua hizo na kuzipeleka kwa Msekwa.

Naye Msekwa alizipokea barua na kuzirekebisha. Akazirejesha kwa Nape ili azipeleke kwa Mukama kuzisaini. Mukama akagoma. Zikapelekwa kwa mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete, ambaye taarifa zinasema, “amezifungia kabatini.”

Kwa mujibu wa taarifa za ndani ya kikao hicho, Lowassa alifika Lumumba saa nne asubuhi. Mazungumzo kati yake, Msekwa na Mukama inakadiriwa yalichukua takribani saa moja.

Katika mazungumzo hayo, Msekwa ananukuliwa akimweleza Lowassa “unatakiwa ujiuzulu nyadhifa zako za uongozi katika chama ili kutekeleza maagizo ya NEC na falsafa ya chama ya kujivua gamba.”

Akijibu hoja hiyo, mtoa taarifa anasema Lowassa alijibu, “Kuhusu Richmond (kampuni feki ya kufua umeme wa dahurula), ukweli unafahamika…Katika hili, mimi sina makosa. Rais anafahamu hilo na kila mmoja anajua hivyo.”

Anasema Lowassa alisema kama kuwajibika kwa makosa yaliyotokana na Richmond tayari amefanya hivyo kwa niaba ya chama chake na serikali pale alipoamua kujiuzulu wadhifa wake wa uwaziri mkuu.
Anasema mbali na kueleza hilo, Lowassa alisikika akisema, “nilikutana na Rais Kikwete. Aliyonieleza si haya.”

Alisema Rais Kikwete alimweleza kuwa hakuna maazimio yoyote ya NEC yaliyomtaka kujiuzulu. Akahoji, “Sasa nimwamini nani, ninyi mnaotaka nijiuzulu au rais aliyesema hakuna azimio kama hilo?”

Habari zinasema mara baada ya Lowassa kuwaeleza viongozi wake msimamo juu ya mazungumzo yake na Kikwete, ndipo Msekwa aliposikika akisema, “Lowassa acha mbio za urais.”

Naye Lowassa hakumkawiza Msekwa. Alijibu, “Lini nimetangaza kugombea urais? Lakini hata kama ninataka kufanya hivyo, ni haramu kugombea nafasi hiyo? Je, kuna mliowaandaa?”

Ni kauli hiyo ya Lowassa, iliyomshutua Msekwa na kusema, “Hapana. Hapana. Hakuna tuliyemuandaa…Haya mambo ya urais yatatuvuruga.”
Akihitimisha hoja zake kabla ya kumalizika kwa mkutano huo, mtoa taarifa anasema Lowassa alikitaka chama chake kuisaidia serikali kutekeleza wajibu wake kwa wananchi, badala ya kufanyia kazi kile alichoita, “majungu ya wanasiasa.”

Naye Chenge taarifa zinasema aliwaambia viongozi aliokutana nao kuwa yeye si fisadi na hafahamu maana ya ufisadi. Akataka kama tuhuma wanazomtuhumu wanaweza kuzithibitisha wamfikishe mahakamani ili aweze kujitetea. Hakuna maelezo ya ziada.

Hata hivyo, watu waliokaribu na kiongozi huyo wanasema, Chenge amejipanga kuhakisha kwamba hang’oki katika kiti chake cha NEC; ikibidi kuondolewa kwa nguvu ametishia kuondoka CCM na kujiunga na upinzani.

Kwa upande wa Rostam Aziz, taarifa zinasema alitakiwa kujiuzulu ujumbe wa NEC kwa tuhuma za kuingiza nchini kampuni feki ya Richmond na baadaye Dowans.

Mtoa taarifa anasema, mara baada ya kuelezwa tuhuma hizo, Rostam alihoji, “Haya ni maamuzi ya NEC?” Naye Msekwa akajibu, “NEC imetaka chama kijivue gamba kuanzia ngazi ya taifa hadi chini kwa kuondoa watu wote wanaotuhumiwa ufisadi.”

Habari zinasema, katika mazungumzo kati ya viongozi hao na Rostam, hakuna mahali popote ambapo Msekwa na Mukama walitaja ushiriki wa mbunge huyo wa Igunga, katika wizi wa fedha za umma kupitia kampuni ya Kagoda Agriculture Limited.

Kampuni ya Kagoda ni miongoni mwa makampuni 22 yaliyothibitika kuchota mabilioni ya shilingi kwenye akaunti ya madeni ya nje (EPA) ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Gazeti hili limeshindwa kufahamu mara moja kilichosababisha Msekwa na wenzake kushindwa kumweleza Rostam ushiriki wake katika Kagoda. Hata hivyo, kwa zaidi ya miaka minne sasa, CCM imekuwa ikituhumiwa kunufaika na fedha za EPA hasa Sh. 40 bilioni zilizoibwa na Kagoda.

Wakati suala hilo likichukua sura hiyo, taarifa zilizofikia gazeti hili zinasema baadhi ya vigogo wa chama hicho wamepanga kupeleka hoja katika vikao vijavyo vya (CC) na (NEC) kushinikiza kufukuzwa ndani ya chama hicho wanaoitwa, “wasaliti ndani ya chama.”

Wanaopangiwa mkakati wa kufukuzwa ni spika wa zamani wa Bunge, Samwel Sitta na mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe wanaotuhumiwa kuanzisha Chama cha Jamii (CCJ) wakati wakiwa bado wanachama na viongozi wa CCM.

Wengine ni Nape Nnauye, Victor Mwambalaswa na Daniel Porokwa.
Habari kutoka ndani ya CCM zinawanukuu makada mawili; rais mstaafu, na mjumbe mmoja wa NEC wakitaka chama chao kuwafukuza waasisi wa CCJ kwa kukosa uaminifu.

MwanaHALISI limeelezwa na aliyekuwa naibu katibu mkuu wa CCJ, Dickson Ng’hily kwamba Sitta na Mwakyembe waliokuwa waanzilishi wa chama hicho, walimkatiza masomo yake nchini Afrika Kusini ili kusaidia kupatikana usajili wa chama hicho.

Ng’hily ambaye mahojiano yake yatachapishwa kikamilifu katika toleo lijalo amesema, aliyemwingiza yeye CCJ ni Sitta na Dk. Mwakyembe na anasikitishwa na hatua ya viongozi hao kutaka kuficha ukweli.

“Hawa watu ndio waanzilishi hasa wa CCJ. Mimi na Makonda tulipewa jukumu la kutafuta usajili wa chama. Lakini naona wenzangu wameamua kuficha ukweli kwa maslahi binafsi. Hii si sahihi,” ameeleza.

Ng’hily anaonyesha nyaraka za muhtasari wa vikao walivyoshiriki viongozi wakuu wa CHADEMA, John Mnyika, Anthony Komu na Tundu Lissu kuwa ni miongoni mwa watu walioshiriki katika majadiliano ya kuunganisha nguvu kati ya CCJ ya Sitta na CHADEMA.

“Tulikubaliana kama CCJ itakosa usajili, basi mheshimiwa Sitta atagombvea urais kupitia CHADEMA. Lakini kama tutafanikiwa kusajili chama chetu, basi Sitta angegombea urais kupitia CCJ na CHADEMA wangetuunga mkono,” anaeleza Ng’hily.

Kuibuka kwa Ng’hily kuelezea ushiriki wa Sitta na Dk. Mwakyembe katika kuanzisha na kusimamia usajili wa CCJ kumekuja wiki tatu baada ya Fred Mpendazoe kumtaja Nape Nnauye kuwa ni miongoni mwa waanzilishi wa kwanza wa CCJ.

Mpendazoe aliuambia mkutano mkubwa wa hadhara mjini Njombe kuwa yeye, Sitta na Mwakyembe ndio walianzisha CCJ; bali yeye alitangulia kutoka CCM ili kurahisisha usajili wa chama hicho. Wenzake walikuwa wamfuate baadaye.

CHANZO: Mwanahalisi

20 May 2011


CCM Arusha kwachafuka

Thursday, 19 May 2011 22:42

CHATANDA ATAKIWA KUNG'OKA, GARI LAKE NUSURA LICHOMWE MOTO NA UVCCM
Moses Mashalla, Arusha
HALI si shwari chama tawala mkoani Arusha mara baada ya gari la Katibu wa CCM hapa, Mary Chatanda kunusurika kuchomwa moto na baadhi ya wanachama wa Umoja wa Vijana wa chama hicho(UVCCM).Wanachama wa umoja huo kutoka wilaya mbalimbali za Mkoa wa Arusha waliandamana katika Jengo la Makao Makuu ya CCM Mkoa wa Arusha, wakishinikiza Chatanda pamoja na Mjumbe wa Baraza la Vijana mkoani Arusha, Mrisho Gambo "wajivue gamba".

Hali hiyo ilijitokeza jana katika jengo la makao makuu ya chama hicho wakati Kikao cha Kamati ya Siasa Mkoa kikiendelea ambapo, hali iliyosababisha dereva wa gari la katibu huyo wa CCM kulitoa nje ya jengo hilo na kisha kulikimbiza mahali kusikojulikana.

Vijana hao walikuwa wameshika mabango yenye ujumbe mbalimbali huku wakipaza sauti zilizokuwa zikimtaka Chatanda kuondoka katika nafasi yake ya uongozi kwa madai kwamba amekuwa akikivuruga CCM mkoani Arusha.

Wakizungumza na waandishi wa habari, wanachama hao kutoka wilaya za Monduli, Longido, Arusha, Arumeru, Karatu na Ngorongoro walisema pamoja na wao kutoa malalamiko mbalimbali juu ya Chatanda na Gambo, lakini uongozi wa CCM taifa umekuwa ukiwakumbatia viongozi hao na kudai sasa wamechoka.

Walisema malaliko yao kuwa Chatanda amekuwa akikivuruga chama chao ikiwa ni pamoja na kusababisha kukosa ushindi wa Jimbo la Arusha Mjini lililoenda kwa Chadema huku wakisema kwamba ikiwa atakataa kung'oka watajua cha kufanya.

“Hatumtaki Chatanda na hatumtaki Mrisho Gambo hawa watu kwanza ni wasaliti, lakini pia wamechangia sisi kushindwa kuchukua jimbo hili kwani walikuwa wanaiunga mkono Chadema tunataka waondoke mara moja hadi kieleweke,” ilisikika sauti ya mmoja wa vijana hao.

Miongoni mwa jumbe ambazo zilikuwa zimeandikwa kwenye mambango hayo ni "Chatanda umehujumu uchaguzi kwa siasa zako za makundi zilizojaa chuki, ubinafsi na ubabe usio na manufaa kwa Chama Cha Mapinduzi", "Chatanda kwa siasa zako za ubabe umetuchonganisha na viongozi wa dini”, na nyingine kadha wa kadha.

Hali hiyo ilisababisha Mwenyekiti wa UVCCM mkoani Arusha, James Ole Millya aliyekuwa kwenye kikao cha kamati ya siasa kutoka nje na kwenda ukumbini kuwatuliza wanachama hao, lakini juhudi zake ziligonga mwamba.

Akizungumza na wanachama hao, Milya aliwataka wapunguze jazba na kusema kuwa yeye ni mjumbe ametumwa kusikiliza madai yao hivyo wampatie na kisha taufikisha ujumbe huo.

“Jamani ninawaomba mtulie sidhani kama mtafanya fujo ninaomba mnipatie ujumbe mnitume niufikishe jamani nami nitaufikisha tulieni jamani,” alisema Milya

Hata hivyo, ushawishi wa Milya haukuzaa matunda na kuamua kurudi kikaoni kwani wanachama hao waliendelea kupaza sauti zao kwa wakidai kuwa wanamtaka katibu huyo aondolewe mkoani Arusha kwa kuwa amekuwa akiingilia uamuzi wa umoja wao na kuendelea kumkubatia Gambo.

“Mheshimiwa tunakipenda sana chama chetu na tunakuheshimu sana, tunaomba Chatanda aondoke la sivyo tutachoma gari lake, tukikutana nalo tutamondoa kwa nguvu,” alisema kwa jazba mmoja wa vijana hao.

Vijana wavamia kikao cha kamati ya siasa
Wakati hayo yakiendelea wanachama hao walikosa uvumilivu na kisha kuvamia ofisi ambapo Kikao cha Kamati ya Siasa mkoa kilipokuwa kikifanyika huku wakitishia kubomoa mlango kitendo kilichosababisha viongozi mbalimbali wa CCM mkoani hapa kuhaha kutuliza tafrani hiyo.

Maafisa usalama wakiwemo askari kanzu walikuwa wametanda katika maeneo ya jengo hilo huku wengine wakionekana wakizungumza na viongozi wa UVCCM kujua chanzo cha vurugu hizo.

Chatanda ajifungia ukumbini
Hadi tunakwenda mitamboni, Chatanda alikuwa bado amejifungia ndani ya ukumbi wa mkutano na hakuna taarifa yoyote ya CCM Mkoa aliyotolewa kuhusiana na tukio hilo.

Tuhuma dhidi ya Chatanda kutoka ndani ya chama chake zimekuja siku chache tangu ashutumiwe kuwa mmoja wa waliosababisha mgogoro mkubwa wa kisiasa mkoani Arusha baina ya vyama vya CCM na Chadema.

Mgogoro huo unafuatia Chadema kupinga katibu huyo wa CCM wa Mkoa wa Arusha kushiriki katika vikao vya Baraza la Madiwani na kupiga kura ya kumchagua meya wa Jiji la Arusha, hali Iliyosababisha maandamano makubwa ambayo yalisababisha vifo vya watu watatu.

Wakati CCM wakidai kuwa Chatanda ni mjumbe halali wa vikao vya baraza hilo, Chadema wamekuwa wakipinga kwa maeleo kwamba mwanamama huyo ni mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Tanga hivyo hana sifa ya kushiriki vikao vya Arusha.
CHANZO: Mwananchi

11 May 2011

Mwangalie huyo kijana (well,may be mzee.You can't tell the difference,can you?) wa kwanza kulia.Sidhani kama anayoongea Nape yanamwingia akilini.Na wa tatu kutoka kulia,mwanamama aliyeshika tama,ni kama aliamrishwa kuhudhuria mkutano huo.Sio kashfa au dharau,lakini ni wazi kuwa sura za wahudhuriaji zinatia huzuni.Zimejaa mawazo,hazionyeshi matumaini....yet wamehudhuria.Ukiwaangalia akinamama hao hapo chini,japo kuna kijitabasabu cha kujipa matumaini,lakini hizo flana za njano na khanga zimeficha mengi...ngozi zao zinaonyesha waziwazi namna maisha yao ya kila siku yalivyo magumu katika harakati za kupeleka mkono kinywani.


Lakini bado wanahudhuria mikutano ya porojo.Wanajua wanadanganywa,kwani huhitaji kwenda shule kujua una njaa ilhali anayepiga porojo ameshiba.Mng'aro tu wa ngozi ya Nape as opposed to msinyao wa ngozi za wasikilizaji wake unaelezea mengi.Wanaambiwa kuwa CCM imejivua magamba,sasa itaendeshwa kisayansi,sijui imekuwa mpya...lakini hawaambiwi ni kwa namna gani ugumu wa maisha ya walalahoi hao utapungua...ni lini nao watapata fursa ya kunawiri kama akina Nape....

Lakini bado wanahudhuria mikutano hii ya porojo.Ndio maana katika kichwa cha habari nimehoji: WAMEROGWA?

Picha kwa hisani ya Jamii Forums

5 May 2011


Makala yangu katika toleo la wiki hii la jarida maridhawa la Raia Mwema inafanya uchambuzi linganifu kuhusu,kwa upande mmoja,tuhuma zilizomwandama Rais Obama kuwa sio raia wa Marekani,na hatimaye uamuzi wake kutoa cheti chake cha kuzaliwa,na kwa upande mwingine ni tuhuma za ufisadi zinazomwandama Rais Kikwete,na jinsi kutochukua hatua kadhaa kunazifanya tuhuma hizo kuwa na uzito.

Kadhalika,makala hiyo inawagusa jamaa zangu wa Usalama wa Taifa,kwa kuangalia wnavyofanikisha upatikanaji wa taarifa zinazowahusu wanasiasa wa CCM wanaotajwa kama magamba.Lakini ninaibua maswali kadhaa huku nikiwatahadharisha kuhusu uwezekano wa kuzua skandali kama ile ya Watergate ya nchini Marekani ambapo Rais Nixon,pamoja na mambo mengine alitumia nafasi yake kuamrisha ukusanyaji wa taarifa za kiintelijensia dhidi ya wapinzani wake wa kisiasa.

Pamoja na makala hiyo unayowaza kuisoma kwa KUBONYEZA HAPA,jarida hili la Raia Mwema limesheheni habari na chambuzi za kiwango cha juu kabisa. 


4 May 2011


CCM yamvua gamba Azzan
Wednesday, 04 May 2011 19:34 newsroom

NA SELINA WILSON

KAMATI ya Siasa ya CCM Mkoa wa Dar es Salaam, imemfungia kwa miezi 18 Mbunge wa Kinondoni Idd Azzan, kutogombea nafasi yoyote ndani ya Chama. Pia, imempa onyo kali kwa kosa la kutumia vibaya madaraka yake na kuzichafua mamlaka za CCM Mkoa. Adhabu hiyo imekuja kufuatia Azzan kuwatuhumu wajumbe wa Kamati ya Siasa na Sekretarieti ya Mkoa kuwa ni mafisadi na wala rushwa, hivyo kutaka wajivue gamba. Kwa mujibu wa taarifa, adhabu hiyo imetolewa kwa kujibu Kanuni za Uongozi na Maadili toleo la Februari, Ibara ya 8 (iii).

Katibu wa Itikadi na Uenezi ya CCM Mkoa Dar es Salaam, Juma Simba, alisema jana kuwa uamuzi huo ulitolewa jana baada ya kupokea taarifa ya kamati ya maadili na kuijadili. “Kamati ya Siasa imeona shutuma nzito kama vile ufisadi, rushwa na kushindwa kutekeleza wajibu kwenye vyombo vya habari kwa mamlaka za vikao, Sekretarieti na Kamati ya Siasa ni kukipaka matope Chama, hivyo imetoa adhabu ya karipio,” alisema. Hata hivyo, alisema kuwa baada ya Kamati ya Siasa kujadili tuhuma hizo, ilimpa nafasi Azzan kujitetea kwa mujibu wa Katiba ya CCM, Ibara ya 14 (4), ambapo ilionekana kuwa amefanya makosa kwa makusudi kuzichafua mamlaka za Chama. Azzan alidaiwa kutoa maneno hayo, ambayo yaliripotiwa kwenye vyombo mbalimbali vya habari matoleo ya Aprili 13, mwaka huu.

Simba alisema kuwa baada ya kuchapishwa kwa taarifa hizo, Chama kilimuandikia barua Azzan kikimtaka kufuata taratibu kwa kuwasilisha malalamiko yake badala ya kutumia vyombo vya habari. Hata hivyo, Simba aliongeza adhabu hiyo haina lengo la kumfunga mdomo Azzan wala kumsafisha kiongozi yeyote wa CCM Mkoa, na kwamba anapaswa kuwasilisha tuhuma zake kwa kufuata utaratibu. Hivi karibuni Azzan alikaririwa na vyombo vya habari akiipa siku 30 Kamati ya Siasa na Sekretarieti ya CCM Mkoa, kujivua gamba kutokana na kukithiri kwa rushwa na ufisadi.

CHANZO: Uhuru

3 May 2011



Hapana,leo sio April 1-Siku ya Wajinga- bali habari ifuatayo ni ya kweli na wala si kanyaboya flani.Baada ya usanii uliodumu kwa takriban mwezi mzima,hatimaye CCM imerejea kwenye asili yake.Wengine tulishashtukia mapema usanii uliobeba jina la "kujivua magamba".Tangu lini nyoka akageuka mjusi baada ya kujivua magamba?Na tangu lini mchawi akageuka mtu mwema kwa vile tu kavua tunguri?

Enewei,habari kamili ni hii:

CCM yatoa msimamo

*Mukama asema maazimio ya NEC yamepotoshwa
*Ataka chama kiheshimu taratibu, aisulubu Chadema
Na Mwandishi Wetu

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Wilson Mukama, amesema Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM, haijawahi kutoa maazimio ya kuwataka watuhumiwa wa ufisadi kujiuzulu nyadhifa zao ndani ya siku 90, ila wenye kutoa kauli hizo wanapotosha.

Mukama alikuwa akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari vyote nchini, walipokutana jijini Dar es Salaam jana. Alitoa kauli hiyo baada ya kuhojiwa ataje majina ya mafisadi ni akina nani, na kwamba barua wanazosema watapewa zitakabidhiwa lini kwa wanachama hao wa CCM.

Akizungumza kwa tahadhari kubwa, Mukama alisema NEC ilitoa maazimio 26, na kati ya hayo, azimio namba 15 lilikuwa likiwataka watuhumiwa wa ufisadi, “kupima, kutafakari na kuchukua hatua wenyewe,” ila akaongeza kuwa wakati Mwenyekiti, Rais Jakaya Kikwete anafunga kikao cha NEC, alisema watuhumiwa wasipochukua hatua wenyewe chama kitawachukulia hatua.

“Kwa maana hiyo, kuna watu wame-hype information (wamepotosha taarifa kwa propaganda)… sijui hizi siku 90 zimetoka wapi? Kwanza NEC haikutani kila baada ya siku 90. NEC inakutana kila baada ya siku 120, yaani miezi minne au mara tatu kwa mwaka… Mimi nasema maamuzi ya NEC hayakutaja majina ya watu. Kitu hiki hakipo. Mtuache kama Chama tuna taratibu zetu, wala hatuhitaji mashinikizo kutoka popote,” alisema Mukama.

Mukama alisema yeye anaamini katika utaratibu wa kuendesha chama kama taasisi, hivyo kauli za watu zinazotoa siku 90 si za chama, bali chama kinasimamia maamuzi yanayotokana na kumbukumbu rasmi ambazo ni maazimio 26 ya NEC na hotuba rasmi ya Mwenyekiti wao wakati anafunga kikao cha NEC.

Msimamo huu wa Katibu Mkuu Mukama, umekuwa tofauti na kauli zilizotolewa na Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara), Pius Msekwa, Naibu Katibu Mkuu (Bara), John Chiligati na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, ambao wamekuwa wakitamba kuwa baada ya siku 90 chama kitawafukuza kwenye chama watuhumiwa wa ufisadi ikiwa wao watashindwa kujiondoa sasa.

Hata hivyo, Mukama alisema watu wanaotuhumiwa wanapaswa kufikiri na kuchukua hatua wenyewe wanazoona zinafaa kwa nia ya kujenga chama chao upya. Alisema falsafa ya kujivua gamba imefanyiwa kazi kwa Kamati Kuu na sekretarieti ya chama kujiuzulu, hivyo hakuna sababu ya watu kupotosha falsafa hiyo na kukilazimisha chama kufanya maamuzi ya kujiua.

Wakati huo huo, Mukama alikishambulia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuwa kitakufa kabla ya CCM, kwani chama hicho kimeanzishwa kwa shinikizo la Shirika la Fedha Ulimwenguni (IMF). “You can quote me on this (nikariri katika hili) Chadema kilianzishwa kwa shinikizo la IMF. Yule aliyetofautiana na Nyerere ndiye aliyekwenda kukianzisha,” alisema Mukama bila kufafanua.

Katika mkutano huo, Mukama aliambatana na Katibu wa Idara ya Siasa na Mambo ya Nje, January Makamba, Katibu wa Fedha na Uchumi, Mwigulu Mchemba na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye.

Mukama alisema CCM haijapoteza mwelekeo, na itaendelea kujijenga upya kwa nia ya kutumikia vyema wananchi, huku akisisitiza kuwa mabadiliko yaliyofanywa yalikuwa ya lazima kukipa uhai mpya chama hicho.

CHANZO: New Habari

30 Apr 2011



Kuna wapuuzi wanajaribu kutuminisha usanii unaoitwa "kujivua magamba" kwa chama tawala CCM kilichozaa serikali iliyopo madarakani.Lakini hata tukiweka kando ukweli kwamba nyoka anayejivua magamba anakuwa hatari zaidi kuliko awali,porojo hizi za kuchefua za CCM ni miongoni tu mwa jitihada zake kuwapumbaza Watanzania kuhusu matatizo ya msingi yanayotishia uhai wa taifa letu.

Wakati akili za Watanzania zimeelekezwa Samunge "kwa Babu wa Loliondo" na "magamba" ya akina Lowassa,Chenge na Rostam,mafisadi wanaitumia vizuri nafasi hiyo kubaka uchumi wetu kwa kasi ya kimbunga.Hebu angalia habari zifuatazo ambazo ni mwendelezo tu wa mkakati wa kuiflisi Tanzania yetu.

CAG abaini ufisadi wa Sh50 bilioni serikalini

Saturday, 30 April 2011 10:00

Boniface Meena

MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), amebaini ufisadi wa Sh50.6 bilioni serikalini ukiwamo wa malipo yanayotia shaka ya Sh15.7 bilioni katika kipindi cha mwaka wa fedha 2009/2010.

Katika ripoti yake ya ukaguzi iliyoishia Juni, 30, 2010, CAG amesema fedha nyingi zilitumika kufanya ununuzi bila kufuata taratibu.

Katika ripoti yake, amesema wizara, idara, wakala na sekretarieti za mikoa, zilitumia fedha katika kipindi cha mwaka 2009/2010 kufanya ununuzi ambao haukuwa kwenye mpango wa mwaka.

Alisema matumizi hayo ni kinyume cha kifungu cha 45 cha Sheria ya Ununuzi ya Umma ya mwaka 2004 kinachozitaka taasisi za ununuzi kuweka mpango wa mwaka kwa lengo la kuepuka ununuzi wa dharura, kupata thamani ya fedha, kupunguza gharama za matumizi na kufanya ununuzi sahihi kwa njia ya kandarasi.

"Ukaguzi umebainisha kwamba katika mwaka wa fedha 2009/2010, taasisi zilizoonyeshwa hapa chini zilifanya ununuzi yenye thamani ya Sh50.6 bila kufuata kifungu cha sheria," imeeleza sehemu ya ripoti hiyo.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kati ya fedha hizo, Sh650.7 milioni zilitumika katika Ofisi ya Makamu wa Rais, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto, kununulia samani kwa maofisa wanaoishi katika nyumba binafsi

Wizara nyingine ni Nishati na Madini, Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Maliasili na Utalii, Habari, Vijana na Michezo na Tume ya kurekebisha Sheria.

"Ununuzi wa samani kwa maofisa hao ulikuwa si sawa kwa kuwa hawana stahili ya kununuliwa vitu hivyo na ni kinyume cha waraka wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma (Utumishi) Na. C/CA/134/213/01/G/69 wa Januari 30, 2006, unaohusu malipo ya posho ya nyumba na ununuzi wa samani kwa nyumba za Serikali kwa maofisa wenye stahili," imesema ripoti hiyo.

CAG ameeleza pia kuwa eneo jingine ambalo fedha hizo zimetumika vibaya ni matengenezo ya magari ya serikali na taasisi zake ambako Jumla ya Sh176.7 milioni zimeliwa.

Alisema wakati kanuni ya 5 ya Kanuni za Ununuzi wa Umma (mali, kazi, huduma zisizo za ushauri na uuzaji wa mali ya umma kwa zabuni) ya mwaka 2005, ikitaka wizara, idara, wakala na sekretarieti za mikoa kutengeneza magari yake Temesa (Wakala wa Ufundi na Umeme), au kupeleka katika karakana zilizoidhinishwa na wakala huyo, magari mengi yalikuwa yanatengenezwa kwenye karakana binafsi.

"Magari hayo yametengezwa kwenye karakana hizo bila kuwa na kibali kutoka Temesa kama sheria inavyotaka."

CAG amebaini pia kuwa serikali na taasisi zake imetumia Sh13.8 bilioni kulipia mali na vifaa ambavyo hata hivyo, havikupokewa au vilipokewa pungufu.

"Hii ni kinyume na kanuni ya 122 ya kanuni za Ununuzi ya Umma (mali, kazi, huduma zisizo za ushauri na uuzaji wa mali ya umma kwa zabuni) ya mwaka 2005," alisema.

Taarifa hiyo ilisema katika kipindi cha mwaka wa fedha 2009/2010, wizara, idara, sekretarieti za mikoa mitatu zilifanya malipo yenye shaka yanayofikia Sh15.7 bilioni.

Malipo hayo yalikosa viambatanisho ambavyo vingeonyesha taarifa za kina pasipo kuacha shaka yoyote kuhusiana na usahihi wa malipo hayo.

CHANZO: Mwananchi

Mamilioni yafujwa Mambo ya Nje

na Mwandishi wetu

WIZARA Ya Mambo ya Nje na Ushirikinao wa Kimataifa imegumbikwa na ufisadi mkubwa wa upotevu wa mamilioni ya dola katika ubalozi wake wa heshima nchini Israel na ubalozi wa Marekani.

Imebainika kuwa dola za Marekani milioni 615 zimeyeyuka katika ubalozi wake Israel na hivyo jana kuifanya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali kumuweka kiti moto Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Hayo yalibainika jana katika kikao cha pamoja cha Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC), kilichoketi chini ya mwenyekiti wake, John Cheyo, ambaye alihoji matumizi ya fedha hizo ambayo yalipingana na ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Cheyo, alisema mwaka 2008/2009 imeonekana katika ubalozi huo kupotea kwa kiasi hicho cha fedha hasa katika utoaji wa viza na kutotolewa risiti kwa wahusika.

“Hapa inaonyesha Balozi wa heshima Madam Rinit Hershkovity wa Israel alitumia fedha za serikali vibaya na kamati yetu inahitaji kupata maelezo ya kina inakuaje kiasi cha dola milioni 615 za Marekani kupotea katika mazingira ya kutatanisha.”

“Hii kamati si ya kuchezea hasa katika kudai matumizi ya fedha za walipa kodi wa nchi hii sasa tunahitaji majibu mazuri na hatua zilizochukuliwa juu ya mtu huyu aliyefanya ufisadi wa aina hii,” alisema Cheyo.

Akijibu maswali hayo Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya nje na ushirikiano wa Kimataifa, John Haule, alisema serikali ilipogundua ubadhirifu huo ililazimika kuufunga ubalozi huo toka Februari 2, mwaka 2009 na kumtaka balozi huyo kurejesha fedha hizo.

Haule, alisema kwa kuwa yeye ni mgeni katika wizara hiyo amegundua kukabiliwa na changamoto ya kuweka mahesabu sawa ikiwemo kupambana na matumizi mabaya ya fedha za umma.

“Mwenyekiti mimi ni mgeni toka niripoti wizarani; nina siku 21, lakini hivi sasa tumefanikiwa kuufunga ubalozi wa heshima wa Israel; hata hivyo bado ninakiri kuwa nina kazi ya kurekebisha mifumo ya fedha na utendaji wa kazi,” alisema Haule.

Majibu hayo ya Katibu Mkuu Haule, yalimuinua Mbunge wa Kibiti, Abdul Marombwa (CCM), ambaye alitaka kufahamua matumizi ya kiasi cha cha dola za Marekani 7,600,000 zilizotolewa kwa ajili ya kununua jengo la ghorofa sita nchini Marekani kwa kiasi cha dola 10.4 milioni.

Alisema ripoti ya watalaamu ilionyesha kuwa badala ya kufanya kazi hiyo wizara iliagiza kutumika kiasi cha dola milioni 151.0 huku kukiwa hakuna haja ya kufanya hivyo.

“Ripoti hiyo ilibainisha kazi iliyofanyika sio ukarabati bali ni kukata vyumba… sasa kwa hili tunahitaji maelezo ya kina, na hatua zote hizo hakuna kibali kilichothibitisha matumizi ya fedha hizo wala uhalali wa matumizi hayo,” alisema Marombwa.

Hata hivyo hali hiyo ilimfanya katibu mkuu wa wizara ya mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa kumwachia naibu katibu Mkuu wake kutoa maelezo ya kina kwa kamati hiyo ambaye alisema kuwa hivi sasa wanalazimika kuzifunga balozi nyingi za heshima kutokana kutokuwepo udhibiti.

Kwa mujibu wa ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), inaonyesha kuwa zaidi ya euro 144,202 hazijalipwa kwa mujibu wa jalada namba TZBR/A.20/11 la Agosti 26, 2009 na kuonyesha kuwa deni hilo bado halijalipwa hadi sasa.

Balozi ambazo zimekumbwa na upotevu wa fedha na kuthibitishwa na CAG ambazo hadi sasa hazijatoa maelezo ya kina kuhusu matumizi yake ni pamoja na Italia waliotakiwa kurejesha kiasi cha sh 6,060,519.00 ambapo wahusika walitakiwa kufanya hivyo.

Mbali na upotevu wa fedha hizo kati ya mwaka 2007/2008 ubalozi ulitakiwa kuwasilisha kibali cha ukaguzi na kufanya matuzi ya sh 517,741,802 zilizotumika kinyume cha sheria


27 Apr 2011


Ukisikia kimbembe cha zule ndio hiki kinachoikabili CCM kwa sasa.Japo chama hiki tawala ni mahiri sana kwa usanii,lakini ni dhahiri kuwa yanayoendelea sasa ndani ya chama hicho yanaweza kabisa kuwa dalili za mwanzo wa mwisho.Hebu jionee vimbwanga hivi katika stori zifuatazo:


Barua za kuwang’oa kina Lowassa zakamilika
• Yadaiwa ziko mezani kwa Msekwa

na Mwandishi wetu

Barua za makada watatu wanaotuhumiwa kwa ufisadi ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Rostam Azizi, Edward Lowassa, na Andrew Chenge, za kuwataka wajiondoe katika nafasi za uongozi ndani ya chama hicho, ziko tayari.

Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima Jumatano umethibitisha kwamba makada hao, waasisi wa mtandao uliomwingiza Rais Jakaya Kikwete madarakani mwaka 2005, wanaweza kupokea barua zao wakati wowote kuanzia leo Jumatano.

Kwa mujibu wa vyanzo vya habari, barua hizo ni sehemu ya utekelezaji wa maazimio ya Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) iliyomaliza kikao chake hivi karibuni mjini Dodoma.

Inadaiwa makada hao maarufu na wenye ushawishi mkubwa ndani ya nje ya chama hicho tawala, walipewa siku 90 tangu siku ya kikao, wapime wenyewe uzito wa kashfa zinazowakabili na wajiengue kwenye nafasi za uongozi, vinginevyo chama kitawaengua katika kikao kijacho cha NEC.

“Barua za Lowassa, Chenge na Rostam ziko tayari, na suala lao liko mikononi mwa Makamu Mwenyekiti, Pius Msekwa, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Chama. Wiki hii watakabidhiwa,” kilisema chanzo chetu cha habari kutoka ndani ya CCM.

Pamoja na mambo mengine, barua hizo zimeorodhesha tuhuma zao na kurejea maazimio ya NEC yanayowahusu.

Alipohojiwa na Tanzania Daima Jumatano juu ya barua hizo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alithibitisha kwamba tayari barua hizo zimeshaandaliwa. Naye alisema watakabidhiwa barua hizo wakati wowote kuanzia leo Jumatano.

“Kinachofanyika sasa ni utekelezaji wa maazimio ya NEC, si jambo geni. Ninachojua, tulikuwa tunasubiri mapumziko ya Sikukuu ya Pasaka yapite, kila mtu ale Pasaka yake,” alisema Nape.

Wakati barua hizo zikisubiriwa kwa hamu, baadhi ya makada wajumbe wa NEC wamekaririwa na vyombo kadhaa vya habari na katika mazungumzo yasiyo rasmi wakisema hakukuwa na azimio lolote lililopitishwa la kuwataka makada hao wapewe siku 90 za kujiengua. Vilevile, wamekanusha kuwapo kwa azimio lolote la kuwaandikia barua.

Hata hivyo, Nape amekuwa akisema kwa waandishi na katika mikutano ya hadhara kwamba NEC ilitoa azimio hilo. Baadhi ya makada wasiokubaliana na kauli za Nape, katika hali ya kuwaonea huruma au kuwatetea watuhumiwa, wamekuwa wakidai kwamba kauli za Nape zimetoka nje, si ndani ya kikao cha NEC.

Lakini baadhi yao wamekuwa wakidokeza kuwa si rahisi Nape kujitungia maneno makali ya aina hii, huku wengine wakisema anatumwa na wakubwa “kuwashughulikia” kina Rostam.

Katika kujaribu kuthibitisha kwamba Nape anazungumza jambo lisilotokana na maazimio ya NEC, baadhi ya makada wanakumbushia kauli za hivi karibuni za mtangulizi wake, John Chiligati, ambaye amepata kutaja mara kadhaa taarifa zisizosahihi za maazimio ya vikao vya Kamati Kuu na NEC, tofauti na kilichojadiliwa ndani ya vikao hivyo.

Wanasema, kwa mfano, Chiligati alipata kulalamikiwa kwa kutoa taarifa potofu kuhusu maamuzi ya Kamati Kuu kuhusu uamuzi wa ama kuilipa au kutoilipa fidia kampuni ya uzalishaji umeme ya Dowans ambayo inaidai TANESCO shilingi bilioni 94.

Vilevile, wanasema Chiligati aliwahi kutoa maazimio ya kupotosha aliposoma maazimio ya NEC kuhusu utata ulioibuka baada ya kukatwa kwa jina la Hussein Bashe katika kinyang’anyiro cha uteuzi wa mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM kwa jimbo la Nzega katika uchaguzi mkuu wa mwaka jana.

Hata hivyo, Nape anasisitiza kuwa kauli yake ni ya chama na inatokana na maazimio ya NEC. Katika mikutano ya hadhara inayodaiwa ni ya kujitambulisha, amekuwa akisisitiza kwamba Lowassa, Rostam na Chenge wametakiwa kujiondoa kwenye ujumbe wa NEC ndani ya siku 90, vinginevyo watang’olewa kwa nguvu.

Ndiye pia aliyesema kwamba wataandikiwa barua za kuwaorodheshea tuhuma zao na kuwataka waondoke kwenye uongozi wa chama. Hata hivyo, hakuna kiongozi hata mmoja aliyesema kama makada hao watavuliwa pia ubunge.

Lowassa ni Mbunge wa Monduli, Chenge anawakilisha jimbo la Bariadi Magharibi, na Rostam Azizi ni mwakilishi wa Igunga.

Wadadisi wa mambo ya siasa wanasema kilichotokea mjini Dodoma ni muendelezo wa minyukano ndani ya CCM na kwamba hoja kuu inayosababisha haya si ufisadi, bali urais katika uchaguzi wa mwaka 2015, hasa kwa kuwa baadhi yao wanasemekana wanatamani kugombea au kuunga mkono baadhi ya wagombea.

Nguvu yao ya kifedha na ushawishi wao ndani ya chama ni baadhi ya mambo yanayoogopwa na washindani wao ndani ya chama tawala. Ingawa wote watatu wamekuwa watu wa karibu sana na Rais Kikwete, habari zinasema kumekuwapo na taarifa za kuchongeana miongoni mwao, zikichochewa na makachero wanaomwaminisha Rais Kikwete kwamba sifa yake iliyopotea mbele ya jamii inaweza kurudi iwapo ataondokana na watatu hao.

Rais Kikwete naye anatumia ushauri huo kama fursa ya kurejesha matumaini ya wananchi kwake na CCM, akitumia kaulimbiu ya kujivua gamba.

Hata hivyo, wachambuzi wa masuala ya kisiasa na wakosoaji wa Rais Kikwete wamesema kujivua gamba kunakofanywa naye ni unafiki mtupu, kwani kama lengo ni kupiga vita ufisadi, naye yu miongoni mwa waliotajwa kwa ufisadi pamoja na Chenge, Rostam na Lowassa.

Baadhi ya makada wamesema kwamba kama CCm inaazimia kuondoa mafisadi, basi kiwaondoe viongozi wote waliopatikana kwa pesa za kifisadi za EPA.

Katika orodha ya viongozi waliofaidika na ufisadi wa EPA, anatajwa pia Rais Kikwete, kwa maelezo kwamba pesa hizo zilitumika kununua kura ili ashinde.

Wanasema hata kuvunja Kamati Kuu na kuingiza wajumbe wengine hakukusaidia kuisafisha, kwani walioingia ni wachafu kama waliotoka, maana historia zao na wasifu wao vinafahamika.

Wengine wanakwenda mbali na kusema kwamba iwapo Rais Kikwete atatekeleza azima yake hii, atakuwa anaandaa anguko lake lisilotarajiwa, maana atakuwa anaongeza idadi ya maadui miongoni mwa watu wanaomjua vema, waliomjenga na kumsaidia hadi hapo alipo


Mafisadi CCM waandaa mamilioni kujisafisha
*Wadaiwa kuandaa vijana kupinga hatua dhidi yao

Na John Daniel

KUNDI la mafisadi wanaokabiliwa na hatihati ya kuvuliwa uongozi na pengine uanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wamebuni mbinu mpya
kujihami kwa kutumia haramu kwa kuandaa vijana kufanya maandamano kumpinga Rais Jakaya Kikwete na chama chake.

Kundi hilo linapinga vikali uamuzi wa CCM kupitia Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), kuwapa muda wa kujiengua wenyewe kabla ya kufukuzwa baada ya siku 90.

Habari za uhakika kutoka vyanzo vyetu vimeeleza kuwa kundi hilo limepitisha bajeti ya mamilioni ya fedha kwa ajili ya kuwandaa vijana kufanya maandamano kupinga uamuzi wa kuondolewa NEC na hata CCM kwa ujumla, mara tu baada ya kukabidhiwa barua muda wowote kuanzia wiki hii.

"Tayari wameapa kuwa wakiondolewa ni lazima Rais Kikwete naye aondoke kwa kuwa ndiye aliyepitisha maamuzi ya kuwafukuza, wanapanga vijana kwa kuwarubuni kwa fedha haramu ili waandamane mara tu watakapopewa barua.

"Wiki iliyopita walikutana wakapitisha zaidi ya milioni 500 kumshughulikia Bwana mkubwa (Rais Kikwete), wanataka kumchafua ili kummaliza nguvu kuwashughulikia," kilisema chanzo kingine.

Habari hizo zilieleza kuwa mbali na Rais Kikwete anayeelezwa na kundi hilo kukabiliwa na tuhuma na ufisadi, akiwa miongoni mwa watu 11 waliotangazwa na Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dkt. Willibrod Slaa, na familia yake, akiwamo mwanawe Ridhiwan anayedaiwa kuwa mali kuliko kipato chake, pia kundi hilo linasaka kwa udi na uvumba majalada ya mawaziri wanne wa sasa kwa lengo la kuwaunganisha katika tuhuma za ufisadi, kwa kinachoelezwa kuwa ni kampeni ya 'tuchafuke wote'.

"Kati ya fedha hizo sh. milioni 18 zitatumwa katika mikoa 20 kugawiwa vijana ili wafanye maandamano ya kupinga kuondolewa na kuwapakazia wengine wanaotaka waondoke nao kama njia ya kujitakasa.

"Fedha zinazobaki zinatumika kununua mafaili ya watu wengine kutafuta makosa yao ya aina yoyote akiwamo Waziri wa Afrika Mashariki, Bw. Sitta (Samwel) Prof. Mwandosya, (Mark), Dkt. Mwakyembe (Harrison) na Membe au Magufuli," kilisema chanzo chetu.

Ilielezwa kuwa kundi hilo limekuwa likifanya vikao katika maeneo maeneo mbalimbali kwa lengo la kutaka kujisafisha na ufisadi, au kupunguza makali kwa kutaja wengine.

"Mmoja wao amejiandaa kuzungumza na waandishi wa habari kuwapa nyaraka za uongo ili kuwachafua watu wengine, walengwa wakuu ni Rais na familia yake, mawaziri wanne na wengine wadogo," kilisema chanzo kingine.

"Usifikiri hatujui hayo, mbinu zote wanazofanya tunazijua, hatuwezi kupambana na wajinga, tunasubiri tuone mwisho wao, lakini hata ninyi waandishi lazima mjue kuwa Watanzania wanaosoma vitu mnavyoandika wanajua yote," alisema kigogo mmoja wa serikali bila kutoa ufafanuzi.

Mbinu nyingine iliyotajwa mara baada ya uamuzi wa NEC Dodoma ni kuwatumia viongozi wa vyama vya siasa kutoa tuhuma mpya ili ionekane kwamba wameonewa na kupoteza lengo la kuwaondoa.

Pamoja na kwamba hakutaja jina, Chama cha demokrasia na Maendeleo ndicho kimetaja watuhumiwa wapya wa ufisadi, huku Katibu Mkuu wake, Dkt. Slaa akipinga madai ya kutumiwa kufanya hivyo kwa nia ya kuwachafua.

Katika tuhuma hizo, alizungumzia uuzaji wa nyumba za serikali bila kufuata utaratibu zilizoelekezwa na Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa na aliyekuwa waziri wake wa Ujenzi, Dkt. John Magufuli; Kuhusu fedha za EPA na mahali zilipo zile zilizorejeshwa akielekeza tuhuma hizo kwa Rais Kikwete na John Malecela na Philip Mangula waliodaiwa kuhusika katika wizi wa fedha za EPA, hasa zile zilizoingia katika kampeni ya CCM mwaka 2005.

Katika hatua nyingine kundi hilo la mafisadi wa linadaiwa kuwalenga baadhi ya viongozi wa dini kuwasafisha kwa kutangaza msimamo kuwa wameonewa na hakuna mtakatifu au wao wametolewa kafara.

Majira ilipomtafuta Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi, Bw. Nape Nnauye kujua kama wana taarifa hizo alikiri na kuongeza kuwa haziwasumbui kwa kuwa mfa maji hakosi kutapatapa.

"Kwanza nilishasema nilipokuwa uwanja wa Manzese, niliwaambia wananchi kuwa mafisadi wamejipanga kumchafua Mwenyekiti wetu na familia yake"

CHANZO: Majira

Diwani matatani kwa kumwita Chiligati fisadi

na Francis Godwin, Iringa

DIWANI wa kata ya Mgama, wilayani Iringa Vijijini, Denis Lupala (CCM), yuko matatani baada ya kumwita Naibu Katibu Mkuu CCM, Tanzania Bara, Kapteni John Chiligati, kuwa ni fisadi na anapaswa kuvuliwa gamba kama Katibu Mkuu aliyepita Luteni Yusuf Makamba na wenzake.

Diwani huyo anadaiwa kutoa kauli hiyo hivi karibuni mkoani Iringa wakati Chiligati na viongozi wengine wapya wa sekretarieti ya CCM taifa alipofanya ziara mkoani humo kwa ajili ya kujitambulisha.

Diwani hayu ambaye tayari ameitwa na sekretarieti ya wilaya na Kamati ya Maadili kujadiliwa kwa utovu kwa Chiligati na viongozi wengine waandamizi wa CCM ambao alipendekeza watimuliwe.

Akithibitisha kuitwa kwenye vikao hivyo, Lupala alisema alipewa barua ya kuitwa kuhusu tuhuma hizo, lakini hakuhojiwa.

‘Kweli waliniita na mwanzoni niliambiwa kikao kitanijadili kwa utovu wa nidhamu niliouonyesha badala yake tulijadili tukio la jukwaa kuanguka wakati Chiligati akihutubia,” alisema diwani huyo.

Hata hivyo alijigamba kuwa alikuwa amejiandaa kupangua hoja zao kwani hadi sasa binafsi hataki Chiligati abaki kwenye nafasi hiyo kwa madai kuwa anapaswa kuvuliwa gamba kama viongozi wenzake aliokuwa nao kwenye sekretarieti iliyopita.

“Nilijipanga vizuri kuwajibu viongozi wa wilaya iwapo wangejaribu kutaka kuniadhibu kwa kumwita Chiligati fisadi. Ni ukweli usiopingika kuwa kati ya watu wanaovuruga CCM Chiligati ni mmojawapo na hana sifa ya kuwa kiongozi ndani ya CC na nasema kuwa niko tayari kuwajibika kwa kusema ukweli dhidi ya Chiligati,” alisema diwani huyo.

Hata hivyo habari zaidi zinasema kuwa diwani huyo anatarajiwa kuitwa wakati wowote kuanzia sasa kujibu tuhuma alizozielekeza kwa Chiligati.

Wakati wa mkutano wa hadhara, diwani huyo wa CCM alipata nafasi ya kuuliza swali na kuanza kumrushia madongo Chiligati kwamba ni fisadi na ajiuzulu nafasi yake.

Pia alitaka Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa, Andrew Chenge (Bariadi Mashariki) na Rostam Aziz (Igunga) na wengine kufilisiwa mali zao na kunyang’anywa kadi za uanachama.

Hata hivyo alishindwa kuendelea na hoja yake baada ya baadhi ya wanachama na viongozi wa CCM kuingilia kati na kusitisha swali lake kwa Chiligati.


26 Apr 2011


Wakati habari kuhusu chama tawala CCM "kujivua magamba" zinaendelea kukamata nafasi ya juu,ni vema tukakumbushana magamba halisi yanayopaswa sio kuvuliwa tu bali kutekeketezwa kwa moto wa gesi.CCM wanaweza kutuchezea shere kwa usanii wao lakini ukweli unabaki kuwa ni migongano ya kimaslahi miongoni mwao ndio inayopelekea hizi ngonjera za kujivua magamba.Ufisadi katika taasisi za umma na serikalini kwa ujumla ndio magamba halisi yanayopaswa kuchunwa kwa nguvu badala ya kuwaruhusu wenye magamba hayo wajivue kwa hiari.By the way,tangu lini uchafu ukajiondoa wenyewe pasipo kutumika nguvu ya sabuni na mkono aumashine ya kufulia?

Soma habari hii ujionee mwenyewe namna Tanzania yetu inavyozidi kuwa shmba la bibi

Kashfa mpya ya Ufisadi Tanesco
Tuesday, 26 April 2011 10:14

CAG ADAI IMEILIPA DOWANS BILIONI MOJA ISIVYO HALALI
Mwandishi Wetu
SHIRIKA la Umeme Tanzania (Tanesco), limeingia katika kashfa nyingine ya ufisadi baada ya kubainika kuwa limeilipa Kampuni ya kufua umeme ya Dowans dola za Marekani 1.2 milioni ikiwa ni gharama ya kusafirisha mitambo ya kampuni hiyo kuja nchini kwa ndege badala ya dola 120,000.

Matumizi hayo ya ziada yanayokadiriwa kufikia Sh1.4 bilioni za Tanzania yanaelezwa kwamba yaliingizwa katika akaunti ya Dowans kimakosa.

Hata hivyo, mpaka sasa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), amesema Tanesco imeshindwa kumpelekea ripoti ya matumizi ya fedha hizo alizoziita kuwa ni ufisadi.

Mbali na hivyo CAG amelitaka shirika hilo limpelekee mchanganuo wa matumizi ya dola za Marekani 4,865,000 sawa na Sh6.8 bilioni.

Jana, alipotakiwa kufafanua kuhusu ripoti hiyo, CAG Ludovic Utoh alisema: “Nashukuru kwa kunipigia, lakini nyie si mnazo ripoti hizo, mnaweza mkasoma na kuendelea kuripoti.”

Kwa mujibu wa gazeti la The East African, toleo la Aprili 25, mwaka huu, ripoti ya CAG iliyoishia Juni 30, 2010 inaonyesha kuwa Tanesco ilifanya malipo hayo kupitia akaunti ya gharama za mikutano.

Taarifa hiyo imeonyesha kuwa Tanesco ilishindwa kutoa maelezo kuhusu malipo hayo kwa ajili ya kukodisha ndege maalumu ya kusafirishia mitambo hiyo. Pia inaonyesha kuwa kiasi cha Sh13,000,000 ziliripotiwa kimakosa kama Sh1,300,000,000 kwenye kifungu cha matumizi ya vikao na pia kiasi cha Sh11.0 bilioni kinachohusu malipo kupitia barua ya mkopo (letter of credit) na kuingizwa katika akaunti ya makusanyo ya shirika kupitia benki ya NBC.
CAG pia alibaini kuingizwa mara mbili kwa Sh101 milioni katika akaunti ya mitambo ya Tanesco kinyume na taratibu.

CAG alisema kuwa ndani ya Tanesco hakufanyiki usuluhishi wa mapato yatokanayo na mauzo katika matawi yake kukiwemo pia jumla ya Sh103,000,000 za masurufu ambazo hazijarejeshwa. Pia umeme unaozalishwa na ule unaouzwa unaonyesha kwamba shirika hilo linapata hasara kutokana na sababu za kiufundi.

Ripoti hiyo inasema, Tanesco ilionyesha hasara za uniti 1,188 KwH’m kutoka katika uniti 4,831 KwH’m inazozalisha ikionyesha kwamba kuna hasara katika mapato. Hasara hizo zinachangiwa na kuwepo kwa wateja wasio waaminifu, bili za uongo na uunganishaji haramu wa umeme.

Imeeleza kwamba hata wateja waliokatiwa umeme, wanaendelea kutumia huduma hiyo kama kawaida licha ya kudaiwa wastani wa dola za Marekani 65,000.CAG, Utouh alikaririwa akisema manunuzi katika shirika la Tanesco yalirekodiwa kimakosa na kwa udanganyifu.

Utouh alisema wakati wa ukaguzi, iligundulika kwamba Tanesco, hawakuwa wakifanya ‘reconciliation’ (upatanisho) ya mwezi kati ya mauzo na mapato.Kwa mujibu wa CAG, kuna hasara katika idara za uzalishaji na usambazaji wa umeme kwenda wateja.

“ Kuna mapendekezo niliyoyatoa yanayotakiwa kuchukuliwa hatua na Serikali, Bunge, Kamati ya Hesabu za Serikali, Bodi ya Wakurugenzi na maofisa watendaji wakuu kupitia ripoti ya fedha iliyoishia Juni 30,2009,” ilisema ripoti hiyo.

Katika ripoti hiyo, CAG alisema katika ripoti ya mwaka uliopita ya ukaguzi katika mamlaka za umma na bodi nyingine kuna mapendekezo 15 yaliyotolewa kwa utekelezaji: “Lakini hadi sasa mapendekezo hayo hayajatekelezwa kikamilifu.”

Alisema mapendekezo hayo ambayo hayajatekezwa yanahitaji ufumbuzi wa Serikali ili kuyawezesha mashirika mengine ya umma kufanya vizuri.

Badra Masoud, Meneja mahusiano wa Tanesco hakuweza kupatikana jana kuzungumzia suala hiyo baada ya simu yake kuita muda wote bila kupokelewa huku simu ya Mkurugenzi wa Tanesco William Mhando ikiwa haipatikani.

CHANZO: Mwananchi

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.