9 Mar 2012

Wednesday, 07 March 2012 19:31

Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa
ATHIBITISHA YUKO HOSPITALINI, ASEMA ASINGEPENDA KUELEZEA KWA UNDANI KUHUSU AFYA YAKE  
Ramadhan Semtawa
UTATA umegubika afya ya Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa baada ya taarifa mbalimbali kueleza kuwa yuko hospitalini nchini Ujerumani kwa matibabu.Takriban juma moja sasa kumekuwa na taarifa mbalimbali zikizungumzia afya ya Lowassa lakini hakukuwa na taarifa rasmi kutoka chanzo chochote kati ya Serikali, familia yake au Bunge kuzungumzia afya ya Mbunge huyo wa Monduli.

Jana, Lowassa akizungumza na mwandishi wetu kwa simu alisema kwamba yuko hospitali, bila kufafanua kuwa ni nje au ndani ya nchi, wala kueleza kinachomsibu.

Mahojiano hayo kati ya Lowassa na mwandishi wetu yalikuwa kama ifuatavyo:

Swali: Asalaam alaykum Mheshimiwa Lowassa.
Jibu: Waalaykum Salaam.

Swali: Mimi naitwa... (jina la mwandishi) kutoka gazeti la Mwananchi. Kwanza pole kwa matatizo ya kiafya yanayokusumbua.
Jibu: Ahsante.

Swali: Nimekupigia pamoja na kukupa pole, nilitaka kujua unaendeleaje na matibabu?
Jibu: Niko hospitalini kwa sasa naomba niache mambo mengine tutaongea baadaye.

Swali: Lakini, ni matibabu gani hasa unayopata?
Jibu: ... (akimtaja mwandishi) naomba niache niko hospitalini sasa hivi mambo mengine tuongee baadaye.

Lowassa alitoa majibu hayo majira ya saa nane mchana na alipopigiwa tena saa 10.20 jioni, alijibu kama ifuatavyo:

Swali: Naam, Mheshimiwa Lowassa nimekupigia tena mimi... (mwandishi akajitambulisha).
Jibu: ... Unataka nikuambie nini tena? Nilishakwambia niko hospitalini niache!

Swali: Sawa, natambua uko hospitalini, lakini wewe ni kiongozi ambaye umewahi kuwa Waziri Mkuu, hivyo Watanzania wangependa kujua maendeleo ya afya yako kutokana na utata ulioibuka na kama je, umelazwa hapo hospitalini au uko katika matibabu ya kawaida?
Jibu Niache, ninachokwambia niko hospitalini sasa unataka nini tena? Nisingependa kuzungumzia afya yangu kwa undani.

Bunge

Akizungumzia suala hilo juzi, Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashillilah alisema ofisi hiyo haijapata maombi rasmi ya mbunge huyo kwenda nje kwa ajili ya matibabu.

Dk Kashillilah alisema kwa utaratibu, Ofisi ya Bunge inashirikiana na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa ajili ya kuwapeleka wabunge wanaoumwa nje ya nchi baada ya kupata rufaa ambayo inatokana na ushauri wa kitaalamu wa madaktari wa ndani.

Alisema hadi juzi, hakuwa akijua aliko Lowassa na kama ana matatizo ya kiafya kama inavyozungumzwa au la: “Mimi ndiyo Ofisi ya Bunge na ndiyo nakwambia hatujapata maombi ya kutaka mheshimiwa Lowassa apelekwe nje ya nchi.”

Mtendaji huyo mkuu wa Bunge alisema wapo baadhi ya wabunge ambao huwa wanakwenda nje kwa vipindi maalumu kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa kawaida wa afya baada ya matibabu lakini, katika orodha hiyo Lowassa hayumo.

“Tunao utaratibu wa baadhi ya waheshimiwa wabunge kwenda nje kwa mujibu wa ratiba zao kwa ajili ya kufanyiwa uangalizi wa kawaida wa afya zao. Lakini, hadi sasa (juzi) katika orodha hiyo mheshimiwa Lowassa hayumo,” alisema Dk Kashillilah.

Hata hivyo, kwa mujibu wa nafasi yake ya utumishi serikalini aliyokuwa nayo, Lowassa anaweza kupata matibabu nje ya nchi kwa kupitia utaratibu wa Serikali bila ya kuhusisha Bunge.

Juhudi za kupata Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Haji Mponda au Naibu wake, Dk Lucy Nkya zilishindikana kutokana na simu zao kufungwa na kutopatikana ofisini.

CHANZO: Mwananchi

8 Mar 2012


Tanzania nchi ya vituko na viporo vya utatuzi wa kero

Kitendawili bila majibu kwa mgomo wa madaktari
Arumeru wanausalama walinda ‘usalama wa rushwa’
MIONGONI mwa habari zilizogusa hisia za wengi wiki iliyopita ni tishio la madaktari kuwa ifikapo Jumatano hii (Machi 7)  watarejea kwenye mgomo iwapo viongozi wawili wa Wizara ya Afya, Waziri Dk. Haji Mponda na Naibu wake, Dk. Lucy Nkya hawatakuwa wameng’olewa kwenye nyadhifa hizo.
Ni vigumu kuelewa kwa nini Rais Jakaya Kikwete anaendelea kuwalinda Mponda na Nkya, lakini uzoefu unapaswa kutukumbusha kuwa ni nadra kwa watawala wetu kusikia vilio vya watawaliwa, isipokuwa nyakati za uchaguzi.
Kimsingi, kilichofanywa na Serikali hapo awali kuwashawishi madaktari kusitisha mgomo wao na kurejea kazini ni sawa na kuahirisha tatizo pasipo kujihangaisha namna ya kulikabili litaporejea tena.
Msimamo wa madaktari hao ulikuwa wazi kwa Serikali, ambapo pamoja na kutaka watimiziwe madai ya kutaka kuboreshewa maslahi na mazingira yao ya kazi, walitamka bayana viongozi wanne wa Wizara ya Afya waondolewe madarakani.
Lakini kabla ya Serikali kuamua kukaa chini na madaktari, ilishajichanganya kwa kujaribu kutumia ubabe kama njia ya kumaliza mgomo. Awali, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alitoa tishio kwamba daktari atakayegoma kurejea kazini, angekuwa amejifukuzisha kazi huku ikiahidiwa kwamba madaktari kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) wangeziba pengo kubwa lililojitokeza.
Pengine kwa kutambua kuwa katika siku za hivi karibuni kauli za Pinda zimekuwa kama za mtu anayesema kwa minajili ya kusikia tu sauti yake mwenyewe, madaktari walipuuza tishio hilo na nguvu kazi iliyoahidiwa kutoka jeshini ikiishia kuwa kituko kama si utani mbaya (bad joke).
Baada ya kugundua kuwa ‘imeshikwa pabaya’ ndipo Serikali kupitia Pinda ikajirudi na kuwaahidi madaktari kuwa ingetimiza matakwa yao. Na siku chache baadaye, ikatangaza kuwasimamisha kazi Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Blandina Nyoni na Mganga Mkuu wa Serikali, Deo Mtasiwa.
Japo uamuzi huo wa kuwasimamisha kazi Nyoni na Mtasiwa ulipokewa na kueleweka vizuri, bado inaniwia vigumu kuelewa kwa nini Mponda na Nkya walisalimika na wanaendelea kukumbatiwa hadi leo.
Kwa kiasi kikubwa, kusita kwa Serikali kuchukua hatua dhidi ya Waziri huyo na Naibu wake ndio kumesababisha kurejea tena kwa sakata hili la mgomo. Lakini kingine kinachokera zaidi ni ukweli kwamba japo Nyoni na Mutasiwa wamesimamishwa kazi, hakuna taarifa zozote kutoka serikalini kuhusu hatua zaidi dhidi yao.
Yayumkinika kuhisi inasubiriwa ‘upepo utulie’ kabla watendaji hao hawajapangiwa madaraka mengine. Ndio Tanzania yetu ilivyo.
Kilio cha madaktari na tishio lao la mgomo ni dalili tu ya tatizo kubwa linalohitaji dhamira ya dhati ya Serikali kulishughulikia. Asilimia kubwa ya watumishi wa umma wanakabiliwa na matatizo kama hayo yanayowasibu madaktari, kubwa zaidi likiwa maslahi na mazingira ya kazi duni.
Lakini kilio cha watumishi wa umma ni mithili ya ‘tone kwenye bahari’ ukilinganisha na hali ngumu ya maisha inayowakabili asilimia kubwa ya Watanzania. Cha kusikitisha zaidi ni kukosekana kwa dhamira ya dhati kwa upande wa Serikali kuboresha maisha ya Mtanzania, awe mtumishi wa umma au sekta binafsi, aliyejiajiri au mkulima, na kila kundi katika jamii.
Mara zote nimekuwa nikiamini kuwa kikwazo kikubwa cha maendeleo yetu si kukosekana kwa sera nzuri na mipango mizuri, au mawazo mazuri. Kinachotukwaza zaidi ni kutokuwapo nia ya kutekeleza sera, mipango au mawazo hayo, sambamba na usimamizi mbovu pale tunapojaribu kuitekeleza.
Rais Kikwete alipoingia madarakani mwaka 2005 sio tu aliahidi maisha bora kwa kila Mtanzania bali pia alibainisha kuwa suala hilo (la maisha bora) linawezekana. Na hakuwa anatania (angalau kwenye ukweli wa mambo) kuwa maisha bora yanawezekana katika nchi iliyojaliwa kila aina ya utajiri japo tunaendelea kuwa masikini wa kutupa huku tukiwa nchi ya tatu kwa kupokea misaada mingi zaidi duniani (mbele ya Iraq na Afghanistan).
Rais Kikwete hajajihangaisha kupima ufanisi wa dhamira yake ya kuwaletea maisha bora Watanzania, lakini ninachokumbuka kuna wakati kauli mbiu hiyo ya maisha bora kwa kila Mtanzania ‘ilikarabatiwa’ na kuongezwa vikorombwezo kama ‘maisha bora hayawezi kushuka kutoka mbinguni.’ Unaweza kujiuliza kwa nini kaulimbiu hiyo ilipotolewa mara ya kwanza haikuwa ‘maisha bora kwa kila Mtanzania yanawezekana lakini hayawezi kushuka kutoka mbinguni.’
Kwa kutathmini dhamira hiyo ya Kikwete tangu aitangaze hadi leo hii, yayumkinika kuhitimisha kuwa ilikuwa ni porojo tu za kutaka kura za Watanzania. Ninasema hivyo kwa sababu ni rahisi kupata idadi ya safari za Rais kwenda nje ya nchi kuliko kuwa na takwimu sahihi za uboreshwaji wa maisha ya Mtanzania. Hapa ninazungumzia takwimu halisi za mtaani na sio kauli za kisiasa za akina (Waziri wa Fedha) Mustafa Mkulo kuwa uchumi unakua.
Hivi kuna ugumu gani kujifunza kutoka kwa majirani zetu wa Rwanda, taifa lililojitutumua na kutoka kwenye mauaji ya kimbari na kuibuka kuwa moja ya mifano adimu ya mafanikio ya kiuchumi barani Afrika.
Nchi hiyo ambayo sasa inafananishwa na economic tigers wa Kusini Mashariki mwa Asia (kwa mfano Malaysia) imepiga hatua kubwa katika kupunguza umasikini huku uchumi wake ukikua kwa kasi.
Rwanda imediriki kufika ilipo sasa kwa sababu Rais Paul Kagame yupo makini, sio kufanya safari za kuzunguka dunia, bali kuhakikisha kuwa nchi yake inapiga hatua kimaendeleo. Sidhani kama Wanyarwanda watakuwa na tatizo iwapo Kagame ataamua ‘kushindana na Kikwete kufanya safari za nje ya nchi’ kwa sababu uchumi unaokua nchini humo unaweza kumudu gharama kubwa zinazotokana na safari za aina hiyo.
Kwa bahati mbaya, shinikizo la madaktari kuitaka serikali iboreshe maslahi na mazingira yao ya kazi linakuja wakati tunaelekezea kwenye msimu mwingine wa kuteketeza fedha katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Arumeru Mashariki.
Na dalili za awali za uteketezaji fedha za umma ni taarifa za uwepo wa makachero wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na wenzao wa Idara ya Usalama wa Taifa kwenye mchakato wa CCM kupata mgombea wake kwenye uchaguzi huo.
Licha ya ukweli kwamba taasisi hizo sio za kisiasa na hivyo hazikupaswa kuwepo kwenye shughuli hiyo ya ndani ya CCM, uwepo wao ambao umegharimiwa na fedha za umma haukuweza kuzuia utoaji na upokeaji wa rushwa.
Siwezi kuilaumu sana TAKUKURU kwa vile kuwepo au kutokuwepo kwake hakuna faida kwa Mtanzania zaidi ya kumwongezea hasira na mzigo wa kugharamia uendeshaji wa taasisi hiyo butu. Lakini nina swali au changamoto kwa Idara ya Usalama Taifa; hivi haioni kama inajidhalilisha inapotuma maofisa wake kwenda kwenye chaguzi za ndani za CCM, kisha rushwa ikamwagwa kana kwamba ni halali, na hatimaye maofisa hao wakarejea ofisini kuripoti tu jinsi rushwa ilivyotawala?
Zamani, sio tu kuwa uwepo wa maofisa Usalama wa Taifa ulitosha kuwatisha wahalifu (kwa mfano hao wanaomwaga rushwa kwenye michakato ya uchaguzi ya CCM) lakini ilikuwa sio rahisi kubaini uwepo wao (na hivyo kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi).
Lakini siku hizi imekuwa kama desturi kusikia wakijazana kwenye vinyang’anyiro vya kupata wagombea wa CCM lakini wakiishia kuwa watazamaji tu kwani rushwa imeendelea kuwa turufu muhimu kwa wanachama wa chama hicho tawala kumudu kupata kura za kutosha.
Fedha zinazotumika kugharimia uwepo wa wanausalama hawa zingeweza kuelekezwa kwenye maeneo mengine muhimu, na hilo licha ya kupunguza migongano kati ya serikali na watumishi wake na wananchi wengine kwa ujumla, ingesaidia pia kuepusha aibu ya wanausalama hao kuwa waangalizi wa namna rushwa inavyofanikisha ushindi wa wanaowania kuteuliwa.
Tutashuhudia katika kampeni za uchaguzi huo mdogo wa Arumeru Mashariki jinsi Serikali itakavyotapanya fedha za Watanzania (pasipo kujali ukweli si kila mlipakodi wa nchi yetu ni mwana-CCM) kuhakikisha inashinda uchaguzi huo. Tutashuhudia pia nyenzo za umma (kama magari) zikitumika kisiasa na kuwabebesha Watanzania mzigo wasiostahili. Chama kinachopata wagombea kwa njia ya rushwa hakina njia nyingine ya kuomba kura zaidi ya kutoa rushwa.
Ni mazingira haya ya serikali yetu kumudu gharama zisizo muhimu (kama safari mfululizo za Rais Kikwete nje ya nchi na matumizi makubwa ya fedha za umma kwenye shughuli za kisiasa za CCM), yanayofanya vilio vya madaktari (na watumishi wengine wa umma pamoja na wananchi kwa ujumla) kuwa sio tu vya msingi bali pia vya lazima.





BONYEZA ORODHA HIYO HAPO JUU KUANGALIA ORODHA KAMILI NA NYINGINEZO




I didn't forget about your birthday; I just wanted to help prolong the celebration.

I didn't really forget your special day, I just figured you deserved more than one.

Even though this message comes to you a little late, the wish it brings for happiness is good on any day date.

Happy belated birthday.





6 Mar 2012

Usiniite mnafiki,au mpindisha maneno.Uthibitisho kuwa hata Rais Jakaya Kikwete hana imani na TAKUKURU upo katika habari ifuatayo (ANGALIA MAANDISHI MEKUNDU)


Rungu la Kikwete lilimwokoa Siyoi
Monday, 05 March 2012 09:17

Rais Jakaya Kikwete
NAPE, WASSIRA WADAIWA KUSIMAMA KIDETE ATOSWE, JK AKATUMIA 'RUNGU' KUZIMA HOJA,WABUNGE WOTE CHADEMA KUHAMIA ARUMERU
Joseph Zablon, Dar na Moses Mashalla, Arusha 

USHINDI wa Siyoi Sumari kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Arumeru Mashariki, unadaiwa kuitesa Kamati Kuu (CC) ya chama hicho, baada ya baadhi ya wajumbe kukuna vichwa kuhusu mbinu na mikakati ya kutengua ushindi alioupata katika duru ya pili dhidi ya William Sarakikya.

Katika Mkutano Mkuu wa jimbo hilo uliofanyika, Februari 20 ulimchagua Siyoi ambaye ni mtoto wa aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, marehemu Jeremiah Sumari kwa kura 361, akifuatiwa na Sarakikya aliyepata kura 259. Hata hivyo, CC ya CCM iliyoketi Februari 27, iliagiza kurejewa kwa upigaji kura kati ya wagombea hao.
Katika duru hilo la pili la uchaguzi uliofanyika Machi Mosi mwaka huu, Siyoi alipata ushindi wa kishindo wa kura 761 na kumtupa mbali mpinzani wake, Sarakikya aliyepata kura 361. 

Juzi katika kikao hicho cha CC, ushindi huo wa mara ya pili wa  Siyoi uliipasua tena kamati hiyo kuu yenye mamlaka ya juu ya uamuzi ndani ya chama hicho, baada ya baadhi ya wajumbe kudaiwa kutaka atoswe na apitishwe Sarakikya kutokana na tuhuma za matumizi makubwa ya fedha wakati wa kampeni.

Vyanzo vya habari vya kuaminika kutoka katika kikao hicho cha CC, vilifafanua kwamba waliosimama kidete kutaka Siyoi atoswe ni Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira.

Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, Nape alipinga Siyoi kurejeshwa akizingatia matukio mbalimbali ya tuhuma za matumizi makubwa ya fedha yaliyokuwa yakifanywa na baadhi ya watu ili wamchague mgombea huyo, kitu ambacho hakikupaswa kuvumiliwa. 

Hoja hiyo ya Nape iliungwa mkono na Wassira ambaye naye alitaka Siyoi atoswe kutokana na tuhuma hizo za matumizi makubwa ya fedha kutoka kwa baadhi ya wapambe wake waliotaka mgombea huyo achaguliwe.


Lakini inadaiwa kuwa Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete alisema kikao hicho kisingeweza kumkata Sumari kwa sababu tu ya tuhuma hizo za rushwa zilitolewa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), mkoani humo.


Chanzo kingine kilimnukuu mwenyekiti huyo akisema kwamba, Arusha ni mkoa wenye siasa za aina yake hivyo ni muhimu kuwa makini kwani siku za nyuma kuliwahi kuibuka tuhuma za rushwa kwa wabunge wa CCM kukamatwa lakini, mahakama ikawaachia huru.

Chanzo hicho kiliongeza kwamba, Rais Kikwete alisisitiza kuwa hata tuhuma za rushwa zilizotolewa zilikuwa zikigusa wengine kwani iliwahi kupendekezwa kwamba Elishalia Kaaya ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC), ndiye apitishwe na wengine wang'olewe. 

Katika kikao hicho, Rais Kikwete pia alinukuliwa akihoji kuwa endapo Siyoi angekatwa jina kungekuwa na uhakika wa chama kushinda kwa kumsimamisha Sarakikya? Hakupata jibu kama mgombea huyo wa pili angeweza kushinda kiti hicho.

Hata hivyo, chanzo hicho kilisema baada ya mwenyekiti kutumia rungu kumpitisha Siyoi alimpa angalizo: “Basi na wewe usiende kutamba huko mitaani kwamba umeangusha watu, fanya kampeni, ushinde jimbo tuangalie mambo mengine mbele.”

Ilielezwa zaidi kwamba Rais Kikwete aliungwa mkono na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, aliyeeleza kuwa haoni sababu ya kumwondoa Siyoi katika kinyang'anyiro hicho kwani ushindi wake ulikuwa mkubwa. 


Chanzo na Kwa habari Kamili: Mwananchi

5 Mar 2012


ngoma inaitwa AGAIN and AGAIN,
msanii ni SEMY PAGE toka kundi la Macube rymers,akiwa amemshirikisha msanii BIG BOSS
ngoma imetengenezwa kwenye studio za M LAB producer akiwa Kanye Mujwahuki
hii ni nyimbo yake ya kwanza kama solo artist baada ya kutoka na ngoma ya kundi iliyokwenda kwa jina la HIRA.



Picha,Caption na Track kwa hisani ya DJ CHOKA

Mahojiano mafupi na msanii Linah akizungumzia (japo kwa ufupi) kuhusu historia yake kimuziki, maendeleo katika muziki wa kizazi kipya na ziara yake hapa Marekani kwa mwaka 2012.


3 Mar 2012

Waishi na fisi kwa miaka 44 sasa
Friday, 02 March 2012 20:44


Wakazi wa Kijiji cha Chela, Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga Mussa Serikali (kushoto), Doi Lukondya (katikati) na Matandalwa Lukondya wakiwa wamewashikilia fisi nyumbani wanaowafuga kwa ajili shughuli za burudani kama walivyokutwa hivi karibuni.
Na Shija Felician, Kahama
FAMILIA moja katika Kijiji cha Chela, Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga imesimulia jinsi inavyoishi na fisi kwa miaka 44 sasa.Kijiji cha Chela ndiko alikozaliwa Waziri wa Maliasili na Utalii ambaye pia ni Mbunge wa Msalala (CCM), Ezekiel Maige na fisi hao walionekana hadharani wakati Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alipofika katika kijiji hicho akiwa katika ziara mkoani Shinyanga wiki iliyopita. 

Familia inayofuga fisi hao ni ile inayounda kikundi cha burudani ya ngoma za jadi ambacho ni maarufu katika Kanda ya Ziwa kikijulikana kwa jina la Bununguli na kwamba fisi hao ni moja ya nyenzo za kufanikisha kazi yao.
Mmoja wa wanafamilia wanaomiliki ngoma hiyo, Lukondya Mabiti Jinoja anasema aina ya fisi wanaofuga wanajulikana kama nhawa kwa lugha ya Kisukuma na kwamba fisi wa aina hiyo wana maumbo makubwa kuliko wale waitwao mbitimululu wenye maumbile madogo yasiyovutia.

Alisema ingawa fisi hao wameanza kuwatumia na kuonekana hadharani siku za karibuni, familia yake imeanza kuishi na wanyama hao tangu mwaka 1968.

“Ni miaka mingi inafikia 44 au 45 na katika muda wote huo tumejifunza mbinu mbalimbali za namna ya kuwakamata na tumefanikiwa kuishi nao kwa muda wote bila kupata madhara yoyote,” anasimulia Jinola.
Jinoja ambaye ni Mwenyekiti wa Bununguli, alisema wakati wa maonyesho ya burudani za ngoma, fisi hao hutumika kunogesha na kuvutia umati wa watazamaji wa ngoma hizo.

Wanawakamataje?
Jinola anasema mara nyingi ukamataji wa fisi hao hufanywa kwa kutumia mbinu za kijadi ambazo hata hivyo, hakutaka kuziweka wazi.

“Hawa mafisi hukaa kwenye mapango, kwa hiyo sisi huenda tukiwa kundi kubwa kuwavizia taratibu na tukiwakaribia huwa tunawavamia, tukiwakamata tu huwa tunawahifadhi kwenye masanduku yetu makubwa na kuwafungia, kisha huyabeba hadi nyumbani tunakowafuga,” alisema Jinola.

Alisema fisi hufugwa kama ilivyo wanyama wengine ambao ni mbwa au paka na kwamba baada ya kuishi nao kwa siku kadhaa, huzoeana nao na baadaye huwa wapole wasiokuwa na madhara kwa binadamu.Hata hivyo, Jinoja alisema changamoto kubwa waliyonayo ni uwezo wa kuwalisha kwani fisi mmoja ana uwezo wa kula kati ya kilo mbili hadi nne za nyama kwa siku moja kulingana na ukubwa wake.

“Natumia wastani wa kilo 16 za nyama kila wiki kuwalisha fisi wangu wanne, ni kazi kubwa kweli lakini tunajitahidi kadri tunavyoweza,” alisema.Hata hivyo, alisema baada ya familia hiyo kufanikisha mpango wa kuishi na fisi hao sasa wameweka mikakati wa kufuga chui siku zijazo.


CHANZO: Mwananchi


Pata Windows 8 (ya majaribio) kwa KUONYEZA HAPA

1 Mar 2012

Wazee wa iliyokuwa Jumuia ya Afrika Mashariki wakiwa wamekaaa katikati ya jiji la Dar es Salaam wakijadili malipo yao yaliyocheleweshwa na serikali hadi leo.…

Nimekutana na picha hiyo hapo juu kwenye mtandao wa Global Publishers.Kwa kweli imenisikitisha sana kuona wazee wetu waliotumikia taifa letu kwa uadilifu wakihangaishwa miaka nenda miaka rudi kupewa mafao yao ya utumishi katika iliyokuwa Jumuiya ya Nchi za Afrika Mashariki.

Hazipiti wiki kadhaa kabla ya kusikia Rais wetu yuko kiguu na njie kwenda nje ya nchi huku akiambatana na msururu wa watu kwenye msafara.Watendaji wengine wa serikali wanatumia magari ya thamani kubwa huku ofisi zao zikisheheni samani kutoka ng'ambo.Matumizi ya viongozi wetu hayaendani kabisa na umasikini wetu.Mabilioni yalitapanywa mwezi Disemba mwaka jana katika maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru.Hivi fedha hizi zisingeweza kumaliza adha inayowakabili wazee wetu hawa?

Jamii inayopuuza wanyonge (kwa mfano wazee hawa) ni kama inasaka ugomvi usio wa lazima na Muumba.Kosa la wazee hawa ni lipi hadi wahangaishwe kiasi hiki?Chonde chonde viongozi wetu-hususan Rais Kikwete-waoneeni huruma wazee wetu hawa.Wanachodai sio posho za vikao kama za wabunge bali ni jasho lao halali.Wenzao wa Uganda na Kenya walishalipwa stahili zao zote.Kama wao waliweza kwanini sie tushindwe?

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.