13 Jul 2012


Takriban wiki moja baada ya Naibu Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa, Dkt Asha-Rose Migiro, kurejea nyumbani Tanzania baada a kukitumikia chombo hicho cha kimataifa kwa kipindi cha miaka mitano, vyanzo vya habari ndani ya Umoja huo vinadokeza kuwa utendaji kazi dhaifu na kushindwa ku-fit katika 'taasisi hiyo kubwa na ngumu' ndio sababu zilizopelekea Mtanzania huyo kunyimwa fursa ya kurefusha mkataba wake wa kazi.

"Wadhifa wa Naibu Katibu Mkuu ni mgumu na wenye mahitaji mengi; unahitaji mtu mwenye uzoefu wa kuongoza Sekretariaeti (ya Umoja huo).Changamoto kubwa kwake ilikuwa kutofahamu siasa za chombo hicho na kutengeneza 'marafiki' (alliances)," kilieleza chanzo kimoja kwa Vox Media kupitia maongezi ya simu.

Imefahamika kuwa Dkt Migiro alijaribu kulishawishi Kundi la Afrika (Africa Group),linalounda asilimia 28 ya wanachama wote wa Umoja wa Mataifa,kuomba limsaidie 'kumpigia debe' ateuliwe tena,ombi ambalo lilikataliwa.

"Hakuwa maarufu miongoni mwa wanadiplomasia, kwahiyo hakuna aliyemsikliza. Pia ukumbuke kuwa uteuzi wake ulipingwa sana," kilieleza chanzo hicho.

Jijini Dar es Salaam, mjumbe mwandamizi wa zamani wa Sekretarieti ya chama tawala CCM  aliyewahi kufanya kazi na Dkt Migiro kabla hajateuliwa kushika wadhifa huo wa Umoja wa Mataifa alieleza kuwa uteuzi huo katika chombo hicho cha kimataifa ulitokana na ukaribu wa Dkt Migiro na Rais Jakaya Kikwete.

Inafahamika kuwa Rais Kikwete na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon walijenga urafiki katika kipindi wote wawili walipokuwa mawaziri wa mambo ya nchi za nje wa mataifa yao.

Ilipofika wakati kwa Ban Ki-moon kuomba kura kushika wadhifa wake wa sasa, Tanzania ilikuwa mstari wa mbele kumsapoti,na kura ya Kikwete ilisaidia Migiro kuteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu.

Lakini Ki-moon alipoamua hivi karibuni kufanya mapitio ya timu yake nzima kwa minajili ya kukabiliana na upinzani mkubwa dhidi ya timu hiyo, ililazimika Dkt Migiro 'atoswe' kutokana na "utendaji kazi dhaifu na ukosefu wa uzoefu unaohitajika kwa watendaji wa ngazi za juu katika Umoja wa Mataifa."

CHANZO: Habari hii imetafsiriwa kutoka Vox Media.Shukrani za pekee kwa mdau @mactemba kwa kunitumia kiungo (link) cha habari hii.


9 Jul 2012

Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa Jack Zoka


MBOWE ASEMA MPANGO HUO UNARATIBIWA NA KIGOGO WA USALAMA WA TAIFA, MKUCHIKA ASEMA NI TUHUMA NZITO, AZIVUTIA KASI

Geofrey Nyang’oro
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema),kimetoa tuhuma nzito kikidai kigogo mmoja (jina tunalo) wa Idara ya Usalama wa Taifa anaratibu mpango wa kuwaua viongozi wake waandamizi akiwamo Katibu Mkuu, Dk Willbrod Slaa na Mbunge wa Ubungo, John Mnyika.

Kwa sababu hiyo, chama hicho kimeitisha kikao cha Kamati Kuu (CC) leo kujadili mambo mbalimbali na Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe amesema ajenda kuu itakuwa kuzungumzia usalama wa viongozi wao kutokana na vitisho hivyo.

Kuhusu tuhuma hizo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika amesema tuhuma hizo ni nzito na atazijibu kwa maandishi.

Katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika Dar es Salaam jana, Mbowe alitaja majina ya baadhi ya maafisa idara hiyo (majina tunayahifadhi) na kudai kuwa mmoja kati yao ndiye anayeratibu shughuli hiyo na tayari yupo mjini Dodoma kwa ajili ya kuongoza  kundi linalotaka kumdhuru Mnyika.

Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, alisema mbali na viongozi hao wawili, mwingine aliyedai kuwa anafuatiliwa ni Mjumbe wa Kamati Kuu, Godbless Lema akidai kwamba, taarifa zinaonyesha kuwa wanafuatiliwa kwa saa 24.
Mbowe alidai kwamba idara hiyo ambayo haifanyi shughuli za siasa, inatumia ofisi yake vibaya kwa kufuatilia viongozi hao wakidhani chama hicho kina mambo ya siri kinayotaka kuyafanya katika nchi hii.

“Sisi Chadema hatuna mambo ya siri tunayotaka kufanya katika nchi hii. Matatizo ya Watanzania yapo wazi na yanajulikana na kila mmoja, Serikali ya CCM itekeleze sera na ahadi zao kwa wananchi na si vitisho,” alisema Mbowe na kuongeza:

“Tunaomba wananchi waelewe kuwa viongozi wao wako hatarini, lakini Chadema hatutarudi nyuma katika kutetea haki  za wanyonge hata kwa kufa na hatuwezi kupeleka malalamiko yetu polisi sababu nao ni sehemu ya tatizo.”

Alisema chama chake kimekuwa kikihusishwa na mambo mengi ukiwamo mgomo wa madaktari unaoendelea na kusema Chadema hakiko nyuma ya mgomo huo na hakijawahi kukutana na kufanya kikao na madaktari.

“Wametuhusisha na mambo mengi na sasa wanasema tuko nyuma ya mgomo wa madaktari, taarifa hizo siyo za kweli na wala hatujawahi kukaa nao kikao chochote kujadili masuala yao, madaktari wana madai ya haki zao. Hapa tunaingia kwenye utaratibu wa kutesana ili kupata taarifa, mmesikia Dk Ulimboka aliteswa ili aseme Chadema iko nyuma ya mgomo,” alidai Mbowe.

Hata hivyo, Mbowe alisema suala la kutokuwa nyuma ya mgomo huo haliwanyimi fursa ya kutetea makundi ya watu wanaodai haki zao wakimwamo madaktari na kusema anaunga mkono tamko la viongozi wa dini.
“Viongozi wa dini wametoa tamko lao jana (juzi), wakitaka Serikali kuwarudisha madaktari na kumalizia suala hilo kwa njia ya mazungumzo,” alisema.

Alisema Chadema kinaunga mkono tamko hilo akisema si busara kuwa fukuza kwa sababu Serikali imetumia gharama kuwaandaa.

Dk Slaa anena

Kwa upande wake, Dk Slaa alisema Chadema kimeamua kutotoa madai yake polisi akidai kuwa imepokea madai mengi kutoka kwa viongozi na wanachama ya kutendewa visivyo lakini hakuna hata moja lililowahi kufanyiwa kazi.

Kuhusu kitisho la kuuawa alidai kwamba alianza kutishiwa siku nyingi na kusisitiza kuwa hilo haliwezi kuwanyamazisha.

“Taarifa za sasa wanaanza na Mnyika na kufuatia mimi, ninachosema wafanye watakavyo hatutaacha kufanya kazi yetu, hata nilipoibua tuhuma za EPA niliwaambia watuhumiwa wengine wa sakata hilo ni Usalama wa Taifa,” alisema Dk Slaa.

Dk Slaa alitaja baadhi ya mambo ambayo alidai kuwa hayakushughulikiwa yalipowasilishwa polisi kuwa ni vinasa sauti alivyowekewa kwenye chumba alichokuwa amelala wakati wa vikao vya Bunge Mjini Dodoma.
Alisema vifaa hivyo vilichukuliwa na polisi kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi lakini hadi leo hakuna taarifa iliyotolewa hata kwake licha ya kuwa mhusika mkuu.

Mnyika: Namwachia Mungu

Akizungumzia madai hayo, Mnyika alisema anamuachia Mungu kwa kuwa ndiye aliyetoa uhai hata kwa hao wanaofikiria kutekeleza kitendo hicho.

Mnyika alidai kuwa baada ya kupata taarifa hizo ambazo alisema zimeandaliwa kwa ama kunyeshwa sumu au kuvamiwa na majambazi, alikutana na familia yake na uongozi wa chama chake ambao kwa pamoja wamemtaka aendelee na kazi ya kutetea rasilimali za taifa.

“Nilipopata taarifa hizi nimekutana na viongozi wangu wa chama na jana usiku (juzi), nilikutana na familia yangu, kwa pamoja wameniambia niendelee na kazi hii ninayoifanya kwani nimetumwa na wananchi na sauti ya wengi ni sauti ya Mungu, ”alisema Mnyika.

Kwa upande wake, Lema alisema  taarifa za kufuatiliwa na watu hao wanaodaiwa kuwa ni wa Usalama wa Taifa alizipata kwa mmoja wa vyanzo vyake kutoka serikalini.

“Nilipigiwa simu na mtu mmoja kutoka serikalini aliyeniambia kuna gari nyuma linanifuatilia, nilipogeuka niliona na kusimama kisha nikashuka na kubadili gari na lenyewe likaendelea kunifuatilia katika gari nililokuwa nimepanda,” alidai  Lema.

Lema alidai kwamba hata juzi asubuhi alikutana nalo katika nyumba aliyofikia na alipolikaribia watu hao walishusha vioo na kumsalimu wakimwita ni Mbunge wa Arusha aliyeko kwenye likizo.

CHANZO: Mwananchi




Naomba nivamie eneo ambalo ninaweza kujiita 'mgeni' (foreign territoty).Hili ni uchambuzi wa muziki,au kwa usahihi zaidi,uchambuzi wa video za muziki.

Nikurejeshe nyuma kidogo.Zamani hizooo,niliwahi 'kuota' kuwa mshiriki wa muziki.Well,sio kuwa mwanamuziki per se bali kujishughulisha na utengenezaji muziki.Nilipokuwa sekondari nilimudu kutunga nyimbo kadhaa kwa kwaya ya shule.Niliweza kutunga aya na sauti lakini tatizo lilikuwa kwenye namna ya uchezaji.Hadi leo,mie na kucheza ni kama kibaka na polisi.Kwa kifupi sijui ku-dance.

Ndoto za kuwa mtengeneza muziki (prodyuza) zilichangiwa zaidi na jinsi ninavyothamini 'michango isiyoonekana.' Hapa ninamaanisha kazi za watu kama watengeneza filamu, watengeneza muziki au hata mashushushu.Hawa ni watu wanaowezesha mengi na pengine laiti wangekuwa wanaonekana na 'products' zilizokwishakamilika basi sifa nyingi zingewaendea wao kuliko ilivyo sasa.

Tunapoona filamu nzuri,sifa nyingi huenda kwa actor au actress.Lakini kimsingi kazi kubwa inayoweza kupelekea filamu ikapata umaarufu hufanywa na mtengenezaji filamu.Kwenye filamu,uzuri wa filamu husika ni mkusanyiko wa jitihada za mwongozaji filamu (yaani director) na mtengenezaji filamu (yaani producer).

Nimeutaja ushushushu.Jamaa hawa ndio kila kitu.Ukiona nchi inakwenda vyema ujue wanafanya kazi yao kwa ufanisi.Ukiona mambo yanayumba basi ujue ndugu zetu hawa wana mushkeli mahala flani.Lakini kimsingi ni kuwa hawaonekani.Kama ilivyo kwa director au prodcuer wa filamu,sifa za kazi husika hulekezwa kwa wengine (kwenye filamu ni actors/actresses) na kwenye mwenendo wa nchi sifa huelekezwa kwa askari au taasisi nyingine za serikali.

Tofauti na filamu na ushushushu ambapo ni mara nyingi ni mkusanyiko wa wengi,kwenye muziki mara nyingi ni jithada za mtu mmoja au wawili. Mara nyingi producer wa muziki ndiye anayebuni ladha ya wimbo kwa maana ya kuunda beatsjapo jukumu la mwisho la ku-flow linabaki kwa msanii husika.Pia inawezekana wimbo ukawa umetungwa na mtu mwingine kisha kumpatia msanii au producer.La msingi hapa ni kuwa producer au mtunzi wa wimbo (kama si msanii mwenyewe) ni watu ambao hawapati sifa za kutosha ukilinganisha na msanii husika.

Kwahiyo moja ya ndoto zangu udogoni ilikuwa kuwa music producer...lakini kama tujuavyo katika maisha sio kila tutakacho ndio tupatacho.Ndoto hiyo 'ilikufa kifo cha asili' baada ya kuelekeza nguvu zangu kwenye  maeneo mengine ya maisha.Lakini hadi leo nina mapenzi ya dhati na muziki hususan wa kufokafoka.

Lengo la makala hii ni kuchambua kazi mbili za wasanii mahiri wa Bongoflava,Fid-Q na Solo Thang,ambao hivi karibuni wametambulisha video zao mpya.

Naomba nisisitize kuwa licha ya mapenzi yangu kwa muziki,mie si mtaalam (expert) wa eneo hilo.Uchambuzi wangu huu ni wa ki-layman (i.e. wa mtu asiye na upeo wa kutosha katika mada husika).

Jingine la kupigia mstari ni desturi iliyojengeka miongoni mwetu kuwa pindi ukionyesha mapungufu ya kitu flani basi wewe ni HATER.Binafsi,nimefika nilipofika kwa sababu siku zote nimekuwa nikipokea na kufanyia kazi maoni mbalimbali hata yale yanayokinzana na imani au mtazamo wangu.Kupewa sifa kuna tatizo moja: hakuwezi kukusaidia kutambua wapi umekwenda kombo.Ofkoz, kazi nzuri lazima isifiwe lakini pengine ili kumsaidia aliyefanya kazi hiyo ni vema kumfahamisha wapi arekebishe au penye mapungufu.Na hiki ndio nitakachofanya katika makala hii.

Video za muziki ninazozichambia ni ile ya SIHITAJI MARAFIKI ya FID-Q na MISS TANZANIA ya SOLO THANG.Kwa kifupi,video zote ni za ubora wa hali ya juu.Wasanii wote wawili wamechagua location za kuvutia wakati wanarekodi video zao.Kadhalika,ubora wa picha ni wa kiwango cha juu.


Wasanii hawa wana sifa moja inayolingana: ni mahiri mno katika uwasilishaji wa ujumbe uliomo kwenye wimbo husika.Wote wana uwezo wa hali ya juu wa kucheza na maneno, neno pekee la Kiingereza unaloweza kulitumia kuwaelezea ni LYRICAL ASSASSINS (Usitishwe na hiyo 'assassins' kwani ni neno tu linalotumiwa kutanabaisha namna msanii anavyoweza 'kucheza na maneno' kwenye tungo husika).

Wakati Solo Thang anamzungumzia Miss Tanzania,Fid-Q anazungumzia marafiki.Ujumbe katika tungo zote mbili haupo wazi sana na inambidi msikilizaji 'asome kati ya mistari' (reading between the lines) kuelewa kinachoongelewa.Usipokuwa makini unaweza kudhani Solo 'anawapaka' warembo lakini kimsingi MISS TANZANIA imebeba ujumbe mzito hususan kwa mabinti warembo wenye kuendekeza tabia zisizopendeza machoni kwa jamii.

Ujumbe wa Solo unapigia mstari mtizamo wa wengi kuhusu urembo kama fani (iwe u-Miss au uanamitindo).Yayumkinika kusema kuwa machoni wa wengi fani hizo mbili hutizamwa 'kwa jicho baya' hasa kutokana na tabia kama za huyo 'Miss Tanzania anayezungumziw na Solo.' Huu ni ukweli i.e. ni mtazamo wa wengi japo si kila Miss au mwanamitindo ana tabia zisizopendeza katika jamii.Inawezekana Solo anamzungumzia Miss Tanzania flani?Jibu la swali hili analo yeye mwenyewe lakini kwa vile ni mahiri mno wa 'kucheza na maneno' yayumkinika kuamini kuwa kuna ujumbe mpana pengine zaidi ya uelewa wetu.

Kwa upande wake Fid-Q, SITAKI MARAFIKI haimaanishi marafiki si muhimu bali kwa kutumia kipaji chake kikubwa cha kuwasilisha ujumbe kwa namna inayohitaji tafakuri,msanii huyo anaweka wazi mtazamo wake kuhusu mahusiano katika jamii,kwa kutumia mfano mwafaka wa marafiki.Nadhani ushaskia msemo  'MARAFIKI WA NINI KAMA MAADUI WANANISAIDIA.' Mara nyingi,marafiki zetu hupenda kututendea mazuri tu tunayotarajia kutoka kwao na pengine kuepuka kutueleza 'hapa umechemka.' Lakini maadui zetu huwa mahiri wa kuonyesha kasoro zetu (hata kama ni kwa uchache) japo kimsingi matarajio yao huwa ni kuonyesha mabaya yetu.Kwa hiyo pasipo kukusudia,maadui zetu wanaweza kuwa na mchango flani chanya katika maisha yetu kwa sababu hawana unafiki katika kunyooshe akidole mapungufu yetu.

Kwa anayezifahamu vema kazi za Fid-Q na Solo Thang ni wazi hatokuwa na wasiwasi kuhusu namna watakavyouwasilisha ujumbe kwenye tungo mpya.Kama nilivyoeleza hapo juu,wasanii hawa wana uwezo wa hali ya juu wa 'kucheza na lugha na maneno.' Uwezo huo unawasiaidia sana katika kuwasilisha ujumbe katika namna inayomwacha msikilizaji 'ameterazika' (ameridhika)

Sasa nigeukia eneo linaloweza kuniingiza matatizoni: mapungufu katika kazi hizo za wasanii hao.Kimsingi si mapungufu bali ni pungufu kwani ni moja tu,na si kubwa sana.Ukiangalia video zote mbili utabaini jambo hili: katika video ya Fid-Q,tangu mwanzo hadi mwisho wa video yake amevaa vazi lilelile.Kwa Solo,kwa kiwango kikubwa katika video hiyo yupo katika T-shirt ileile japo kuna vipande ambapo anaonekana amevaa shati.

Kama nilivyotanabaisha,hii ni kasoro ndogo inayoweza kabisa kufunikwa na ladha ( flavour) ya muziki, ujumbe uliomo katika wimbo,na kiwango cha video.Hata hivyo,kama inavyotanabaishwa kwenye na Andrew Goodwin kwenye Kanuni ya Video ya Muziki (Music Video Theory) vinavyoonekana katika video ya muziki (visuals) vinaweza kuwa na mchango mkubwa sio tu kuiboresha video husika bali pia kuiunganisha na hadhira.

Pengine ili uelewe ninachoelezea hapa nitolee mfano msanii kama Lady Gaga.Mavazi yake ni burudani tosha-japo sio aina ya mavazi unayoweza kumwambia fundi cherahani akutengenezee.Msanii kama Michael Jackson alifahamika sio tu kwa miziki yake bali pia mavazi yake.Kwa sanii wa hip-hop wa Marekani,mavazi ni moja ya vitu muhimu mno,na baadhi ya mapendezeo yao katika mavazi yamepelekea mwamko wa fasheni,kwa mfano mashati ya 'DOGI DOGI' yaliyokuwa yanapendelewa na wasanii wa rap/hiphop wa pwani ya magharibi ya Marekani (West Coast rappers) kwa mfano Snoop Dogg na Ice Cube



Nadhani sababu pekee iliyowafanya Fid-Q na Solo wasionekane katika mavazi tofaut tofauti katika video zao ni MUDA.Hapa ninabashiri kuwa hawakuwa na muda wa kutosha kurekodi video zao kwa muda mrefu ambao ungewapa nafasi za kubadili mavazi mara kadhaa.Naomba nisistize kuwa kasoro hiyo ndogo haijapoteza hata chembe ladha ya kazi zao bora kabisa.Nimeipigia mstari kasoro hii kwa minajili ya kuwasaidia wasanii hao huko mbeleni wajaribu kutumia muda zaidi katika kurekodi video zao.Kanuni nyepesi ya kurekodi kitu chochote kile ni hii: kadri unavyojipa muda wa kutosha ndivyo unavyomudu kurekodi vitu vingi zaidi ambavyo wakati wa kuhariri utaondoa vile usivyovitaka na kuacha vile unavyovitaka.

Lakini kasoro hiyo ndogo inarekebishika.Ninaamini tulichoshuhudia katika video ya SIHITAJI MARAFIKI na MISSI TANZANIA ni matoleo ya mwanzo tu (iwapo Fid na Solo wana mtizamo kama wangu).Si ajabu kwa msanii kutoa video ya mwanzo kisha kutoa video nyingine rasmi kwa ajili ya wimbo husika.Mfano mzuri ni huu wa kundi la TOK katika wimbo wao Footprints Hii ni version ya awali

Hii ni version rasmi

Pengine kitawachowarahisishia Solo na Fid-Q kutengeneza video 'r(kama wataona kuna haja ya kufanya hivyo) ni ukweli kwamba tayari wana video nzima ya asili,ambapo wakiamua kuongeza chochote inakuwa ni suala la kuongeza tu vipande vipya katika original version.Hili si lazima,as long as wao wameridhika na versions walizoweka hadharani.

Ukiweka kando kasoro hiyo ndogo,Solo Thang ameendelea kuwa mithili ya balozi wetu wa Bongoflava katika anga za kimataifa ambapo anafanyia kazi zake kutoka nchini Ireland.Lakini licha ya kuwa nguli (legend) wa bongoflava na 'wadhifa' huo wa ubalozi wa kimataifa,msanii huyu ni miongoni mwa wachache ambao ni down-to-earth sana na anayejali sana kuishirikisha hadhira,hususan kupitia Twitter na Facebook.Kadhalika,ana blogu yake anayotumia kuwafahamisha wapenzi wa muziki wake kuhusu kazi zake.

Kwa upande wa Fid-Q, mkongwe huyu wa muziki wa kufokafoka huko nyumbani amekuwa mahiri sana katika matumizi ya mitandao ya kijamii kutangaza kazi zake na kuishirikisha hadhira.Huko Twitter ana utaratibu wa kujibu maswali angalau mara moja kwa wiki kwa kutumia hashtag #AskFidQ. Hii inatoa fursa kwa wengi kumuuliza maswali mbalimbali.Kadhalika,anaendesha kitu kinachofahamika kama Hip-Hop Darasa,ambapo pamoja na mambo mengine anatoa elimu kwa kizazi kipya cha Hip-hop huko nyumbani.Taarifa za hivi karibuni zinaonyesha kuwa kipindi chake maarufu mtandaoni cha Fidstyle Friday kitaanza kuonyeshwa kwenye runinga katika kituo cha East Africa Television (EATV).Haya ni maendeleo makubwa.

Basi nimalizie kwa kuwapongeza Fid-Q na Solo Thang kwa kazi zao bora kabisa.Naomba wasitafsiri kasoro ndogo niliyobainisha hapo juu kuwa ni HATING. Sote tunapenda kuona wasanii wetu wakifanikiwa na kuteka anga sio huko nyumbani tu bali Afrika na duniani kwa ujumla.Natambua kuna wataosema "huyu nae,anajifanya anajua kila kitu" lakini lengo langu si kujifanya mjuaji bali kutoa mchango wangu kwa wasanii wetu.

Nimalizie makala hii na video zifuatazo za wasanii hao



5 Jul 2012


MOJA ya matokeo yasiyopendeza ya ujio wa mageuzi ya kisiasa katika miaka ya tisini ni ukweli kwamba kwa kiasi kikubwa hayajamsaidia mwananchi wa kawaida mtaani.
Mageuzi hayo - hasa katika nyanja ya siasa na uchumi, yameendelea kuonekana kama ni kwa ajili ya kikundi kidogo katika jamii huku yakitanua pengo kati ya walio nacho na wasio nacho.
Kwenye siasa, ujio wa vyama vingi haujafanikiwa kwa kiwango cha kutosha kuweka mbele maslahi ya wananchi na badala yake umekuwa kama fursa kwa baadhi ya wanasiasa kujinufaisha.
Utitiri wa vyama vya Upinzani umekuwa turufu muhimu kwa chama tawala kutoyumbishwa au kuwajibishwa vya kutosha; hasa kwa vile Upinzani usio na umoja ni rahisi kudhibitiwa na hata kuhujumiwa na chama kimoja imara na chenye uzoefu wa harakati za siasa. Hapa ninaizungumzia CCM.
Tumeshuhudia baadhi ya vyama vikiibuka nyakati za chaguzi tu, na badala ya kutoa upinzani kwa CCM, vyama hivyo vimekuwa vikigawa kura za wapinzani na hivyo kukinufaisha chama tawala.
Kuna hisia kwamba CCM, kwa kutambua kuwa ushirikiano na/au umoja wa wapinzani ni tishio kwa ustawi na uhai wake, imekuwa ikivisaidia vyama hivyo dhaifu katika nyakati za chaguzi kwa minajili ya kugawa kura za wapinzani.
Pengine hoja hiyo inapewa nguvu na namna baadhi ya vyama hivyo vinavyoendesha kampeni zake ambapo badala ya kuelekeza mashambulizi kwa chama tawala, huwageukia wapinzani wenzao.
Lakini hata kama tuhuma hizo dhidi ya CCM hazina ukweli wowote, kilicho wazi ni kwamba vyama vingi vya upinzani nchini havina maslahi yoyote kwa Mtanzania. Baadhi ya vyama vimegeuka kama kampuni za kifamilia ambapo kiongozi ndio chama ilhali hakuna jitihada zozote za ufunguzi wa matawi mapya au kuongeza idadi ya wabunge au/na madiwani.
Yayumkinika kuhitimisha kuwa adui mkubwa wa vyama vya upinzani ni ubinafsi miongoni mwa baadhi ya viongozi wa vyama hivyo; hususan wale ambao wamegeuza vyama hivyo kuwa mali zao binafsi.
Tukiangalia kwa upana zaidi, tatizo la upinzani dhaifu unaotokana na mgawanyiko (badala ya ushirikiano) miongoni mwa wapinzani linachangiwa pia na ukweli kuwa katika mazingira ya Tanzania yetu, hivi sasa siasa imegeuka kuwa ajira.
Kama ambavyo madhehebu mbalimbali yamevamia na walaghai wanaotumia dini kama chanzo cha mapato yao binafsi, siasa nayo imevamiwa na kundi la wahuni ambao wamebaini kuwa sio tu fani hiyo ni chanzo kizuri cha mapato lakini pia inatoa kinga dhidi ya uhalifu wowote wanaojihusisha nao.
Na ndio maana kila kunapofanyika uchaguzi tunashuhudia baadhi ya wanaowania nafasi za uongozi wakimwaga mamilioni ya fedha ili wachaguliwe. Na kwa kutambua udhaifu wa vyombo vya dola katika kuwabana watoa rushwa kwenye chaguzi, baadhi ya matapeli hao wa kisiasa hufanikiwa kushinda chaguzi hasa kutokana na ukweli kuwa wapiga kura wengi “wana njaa” na wapo radhi kunadi kura zao kwa pishi za mchele na doti za kanga.
Tukiangalia kwenye mageuzi ya kiuchumi, manufaa kwa Mtanzania wa kawaida mtaani yameendelea kuwa haba. Kana kwamba itikadi ya Ujamaa na Kujitegemea ilikuwa ikiwafunga mkono baadhi ya viongozi kutekeleza imani yao ya ubepari kwa vitendo, mara baada ya kile kinachofahamika kama Azimio la Zanzibar, nchi yetu imeshuhudia matendo kadhaa maovu pengine zaidi ya mkoloni tuliyemtimua mwaka 1961.
Siku zote huwa natoa ‘excuse’ kwa wakoloni kwamba; angalau wao walikuwa na sababu ya kutoihurumia Tanzania yetu kwani hawakuwa Watanzania, na hata nchi hiyo ingetumbukia mtaroni wao wasingeathirika kwani wana makwao. Sasa sijui tuwaelewe vipi Watanzania wenzetu ambao matendo yao ya kuibaka nchi yetu kiuchumi yanazidi kuipeleka nchi yetu mahali pasipostahili.
Hawa hawana ‘excuse’ hasa kwa sababu wengi wao walizaliwa na kukulia Tanzania, na hata nyadhifa walizonazo zimechangiwa na mzigo uliobebwa na Watanzania wenzao kwa njia ya kodi.
Kibaya zaidi, kiasili takriban kila Mtanzania anahusiana na Mtanzania mwingine (kwa wenye uelewa wa historia wanafahamu asili za makabila yetu hususan ya Kibantu). Mtu anayeruhusu madawa ya kulevya yaingie nchini alimradi akaunti yake inazidi kufurika “vijisenti” anapaswa kufahamu baadhi ya watumiaji wa madawa hayo ni watu wanaohusiana nae kikabila kama si kiukoo.
Lakini hata kama hawahusiani, nguvu kazi inayoathiriwa kutokana na matumizi ya madawa hayo inaweza kumwathiri hata mpokea rushwa huyo; kwani sote tunajua kuwa nchi haiwezi kujengwa na 'jeshi la mateja' (watumia madawa ya kulevya).
Kijamii, japo mageuzi hayakuwa ya moja kwa moja, lakini madhara yaliyojitokeza yanaweza kuonekana zaidi katika nyanja za utamaduni, sambamba na kwenye mila na desturi zetu.
Eneo moja ninaloweza kulitumia kama mfano ni katika matumizi ya lugha yetu ya taifa Kiswahili. Binafsi, katika takriban muongo mmoja nilioishi hapa Uingereza sijawahi kuwaona au kuwasikia Waingereza wakiendesha majadiliano/mazungumzo yao kwa lugha ya kigeni.
Na hiyo si kwa Waingereza pekee. Nchi nyingi duniani zimekuwa zikienzi sana lugha zao kwani ni utambulisho muhimu wa utaifa wao.
Sasa akina sie ambao licha ya kuwa na lugha ya taifa Kiswahili tuna lundo la lugha zetu za asili, tunaendelea kuichukulia lugha ya Kiingereza kama kioo cha elimu au ubora wa mtu.
Juzijuzi, nilitoa changamoto kwa Watanzania wenzangu wanaotumia mtandao wa kijamii wa twitter kwamba ni muhimu kwetu kuenzi lugha yetu ya taifa badala ya kuendeleza mijadala yetu kwa Kiingereza.
Japo ninakiri kuwa nyakati fulani nami nimekuwa nikitumia Kiingereza huko twitter(angalau kwa kisingizio kuwa baadhi ya watu wangu wa karibu hapa hawaelewi Kiswahili), kwa kiwango kikubwa nimekuwa nikijitahidi kuenzi lugha yangu ya taifa Kiswahili.
Na kwa sie tulio mbali na nyumbani, kuna wakati tunatamani tuwe kama wenzetu Wachina au Wahindi (kwa mfano) ambao kila wanapokutana wanawasiliana kwa kutumia lugha zao.
Unaingia mtandaoni ukiwa na hamu ya kuwasiliana na wenzio kwa Kiswahili, lakini wao wanakazania lugha nyingine (huku wengine wakikaza misuli ili waimudu lugha hiyo ya kigeni).
Lakini tatizo si kwenye lugha pekee; bali hata kwenye mila na tamaduni zetu. Ukiangalia baadhi ya zinazoitwa kazi za sanaa unaweza kuhisi kuwa ‘mwisho wa dunia’ unakaribia.
Nilishawahi kuandika katika makala moja huko nyuma kuhusu baadhi ya vikundi vya burudani ambavyo sio tu vinatumia majina yenye maana mbaya (kwa mfano ‘Kitu Tigo’), lakini hiyo burudani yenyewe ni laana tupu.
Na kana kwamba ibilisi anazidi kupata wafuasi, burudani za aina hiyo zimetokea kupata umaarufu mkubwa.
Ukiangalia kwenye eneo ambao pengine lingeweza kuwa mkombozi wetu kisanaa, yaani filamu za Kitanzania, hutolaumiwa ukihitimisha kuwa baadhi ya wanaoingia kwenye fani hiyo wapo ‘kibiashara binafsi’ zaidi kuliko kisanii.
Hivi kuna ugumu gani kuwaiga Waafrika wenzetu wa Nigeria ambao sekta yao ya filamu ya Nollywood inatamba ndani na nje ya Afrika; hususan kwa sababu filamu zao zimeelemea zaidi katika uhalisia wa maisha ya Mwafrika, na wengi wa wasanii wanavuma kwa vipaji vyao na si kutengeneza vichwa vya habari visivyopendeza magazetini.
Lakini kwa wengi wa ‘mastaa’ wetu wa filamu, umaarufu wao unaenda sambamba na taarifa za kufumaniwa, kuvaa nguo nusu-utupu na uhayawani mwingine!
January Makamba
Katika kuelekea kuhitimisha makala hii, ningependa kutoa pongezi za kipekee kwa mwanasiasa kijana, January Makamba, ambaye kwa namna fulani anafanya jitihada binafsi za kuleta matokeo chanya ya mageuzi niliyoongelea katika makala hii.

Mwanasiasa huyu wa CCM ni mmoja ya wachache wanaotumia vyema mitandao ya kijamii kuushirikisha umma.
Wiki hii ameandika makala moja nzuri sana kuhusu u-liberali mamboleo ambapo kimsingi anachoongelea kinashabihiana kwa karibu na dhima ya makala hii.
Katika makala hiyo yenye kichwa cha habari ‘Kubadili Dhana’ (Changing the Paradigm), January anachambua jinsi zaidi ya miaka 30 ya dhana hiyo ya u-liberali mamboleo ilivyoshindwa kuzaa matunda ya maana kwa nchi zinazoendelea na hata zile zilizoendelea.
Anaeleza kuwa kushindwa kwa dhana hiyo kunajidhihirisha katika kuyumba kwa uchumi wa soko, kuendelea kutumia jembe la mkono, utajiri kuendelea kuwa mikononi mwa wachache, uhaba wa kidemokrasia, machafuko, kushindwa kukabiliana na maradhi, nk.
Licha ya kuvutiwa na jitihada zake binafsi za kuushirikisha umma; hususan kupitia mitandao ya kijamii, mwanasiasa huyu analeta picha adimu ya mafanikio ya mageuzi ambapo anachepuka nje ya dhana iliyozoeleka ya u-mungu mtu wa viongozi wetu (yaani kiongozi anaonekana jukwaani tu akihutubia huku akitoa maagizo pasipo kusikia mawazo ya wananchi wa kawaida) na ‘kujichanganya’ na wananchi pasipo kujali kaliba zao.
Ukidhani sifa hizo si stahili kwake, jaribu kujiuliza ‘ukiweka kando ‘undugu’ wakati wa kampeni za kuomba kura’ ni lini ulipata fursa ya kuongea na japo diwani wako-achilia mbali Naibu Waziri kama January-kumfahamisha matatizo mbalimbali yanayoikabili eneo analoongoza?
Viongozi wengi hulea dhana potofu kwamba kuwa karibu na wananchi wa kawaida kunawashushia hadhi. Ni katika mazingira ya aina hii ndio maana matendo na kauli za wengi wa viongozi wetu ni kama wanaishi sayari nyingine - hawajui hali halisi mtaani ikoje.
Wengine wanajijengea ukuta wa mawasiliano kati yao na wanaowaongoza ili kukwepa maswali kuhusu ahadi zao hewa walizotoa wakati wanaomba kura.
Nihitimishe kwa kutoa wito kuwa mageuzi ya kweli yanaweza kuletwa na wananchi wenyewe; kwani wao ndio wanaojua nini wanahitaji kwa ajili yao na jamii/nchi yao.

















Picha kwa Hisani ya MO BLOG

4 Jul 2012




Hatimaye ninyi wasomaji makini wa blogu hii mmeitembelea mara MILIONI MOJA.Japo kuna blogu kadhaa za Kitanzania zilizopita idadi hiyo,binafsi najiskia faraja kubwa hasa kwa vile nimemudu kufikisha idadi hii ya watembeleaji pasipo msaada wa picha.Kimsingi,blogu za uchambuzi/habari pekee hazipati watembeleaji wengi kwani wengi wa Watanzania wanapendelea zaidi picha kuloko maneno.

Nawashukuru sana kwa kutumia muda wenu muhimu kufika hapa.Sina cha kuwalipa zaidi ya kuwaahidi kuwatumikia kwa uadilifu zaidi na kufanya marekebishi kila inapobidi.

MUNGU AWABARIKI SANA 

26 Jun 2012



TAARIFA KWA UMMA
UBAGUZI UNAOFANYWA NA SERIKALI KWA VIONGOZI WETU NGAZI YA CHINI

Ndugu wanahabari

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kupitia Kurugenzi ya Kampeni na Uchaguzi inapenda kutoa taarifa kwa umma na kukemea ubaguzi unaofanywa na baadhi ya watendaji wa serikali dhidi ya viongozi wa vyama vya siasa, hususan wale wa chama kikuu cha upinzani na chama mbadala, CHADEMA.

Chama kupitia Kurugenzi ya Kampeni na Uchaguzi kimepata taarifa kutoka ngazi ya chini ya uongozi, yaani misingi na matawi kwamba mabalozi wa nyumba kumi wa CHADEMA wamekuwa wakibaguliwa katika utendaji kazi wao wa kila siku na watendaji wa serikali, huku watumishi hao wakiendelea kutoa ushirikiano kwa mabalozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Ndugu wanahabari kupitia kwenu, tunaomba umma wa Watanzania ufahamu mambo mawili muhimu hapa;

Kwanza; balozi wa nyumba kumi wa chama cha siasa si sehemu ya uongozi wa kiserikali. Suala hili limewahi kusisitizwa na serikali yenyewe kwa kutoa kauli bungeni. Ngazi rasmi ya uongozi wa kiserikali inaanzia serikali za mitaa/kitongoji.

Lakini pia suala hili la ngazi za uongozi wa kiserikali na kuwa mabalozi si sehemu ya uongozi huo linaoneshwa pia katika katiba yetu ya sasa (pamoja na ubovu wake uliotusukuma tudai iandikwe upya).

Pili; Sheria ya Vyama vya Siasa ya Mwaka 1992, inavitambua vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu kuwa vyote viko sawa mbele ya sheria. Halikadhalika  kutokana na sheria hiyo, katiba za vyama vyote vya siasa ni sawa, hasa baada ya kuwasilishwa na kupitishwa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa na kupitishwa.

Kwa mantiki ya masuala hayo mwili hapo juu, Kurugenzi ya Kampeni na Uchaguzi, inatumia fursa hii kutoa tamko kwa umma kuwa mabalozi wa CHADEMA na CCM, wana haki sawa mbele ya sheria, kwa sababu wanatokana na vyama vilivyo sawa mbele ya sheria, halikadhalika katiba za vyama hivyo ziko sawa mbele ya sheria.

Mabalozi wa CHADEMA wanapatikana kwa mujibu wa Katiba Mpya ya Chama ya Mwaka 2006, Sura ya Saba, ambayo inazungumzia ngazi, uongozi na majukumu ya vikao.

Tofauti pekee ya mabalozi wa CHADEMA na CCM ni kwamba mabalozi wa CHADEMA wanavaa magwanda wale wa CCM wanavaa magamba. Lakini pia wanatofauti ya tabia;
Mabalozi wetu wanasimamia ukweli, wakati wale wa CCM wanasimamia uongo, mabalozi wa CHADEMA wanasimamia uadilifu, wale wa CCM wanasimamia ufisadi, wakati mabalozi wetu wanasimamia na kutumikia wananchi, wale wa CCM wanatumikia maslahi ya chama chao na yao binafsi.

Pamoja na kazi zingine, baadhi ya majukumu ya balozi wa CHADEMA ni pamoja na kuwa mwakilishi wa chama na wanachama. Ana wajibu wa kuwatambua wanachama wenzake, wananchi wote na pia anaufahamu wa kutosha wa masuala mbalimbali katika eneo lake la nyumba kumi.

Tunasema hivyo kwa sababu wakati mwingine kutokana na kukosa mtandao mpana mpaka chini katika kaya za watu na wakati mwingine ukubwa wa maeneo ya kitongoji/mtaa unakuwa kikwazo, mamlaka za serikali katika kutekeleza majukumu mbalimbali zinashindwa  kumtambua kila mwananchi, hivyo zinalazimika kuhitaji mtu/watu wa kusaidia kazi hiyo katika nafasi za uongozi walizoaminiwa katika maeneo madogo ambayo ni rahisi watu kutambuana. Hapo ndiyo dhana ya kuwa na kiongozi wa kaya kadhaa kwa jina la balozi unatokea.

Mabalozi wetu CHADEMA kwa sababu wanatokana na taasisi inayotambulika kisheria, makini na imara wanafanya kazi kwa barua na mhuri wa chama.

Kupitia tamko hili, Kurugenzi ya Kampeni na Uchaguzi ya CHADEMA, inawataka watendaji wa ngazi zote wa serikali kuacha mara moja tabia ya kuwabagua mabalozi wa CHADEMA kwani wanatokana na watu, wanatambua na wanaweza kutimiza wajibu wanaopaswa kufanya.

Chama pia kinatumia fursa hii kutoa mwito kwa mabalozi wote wa CHADEMA nchi nzima ambao wanakutana na vikwazo vya watendaji wa serikali katika kutimiza majukumu yao mbalimbali ya kila siku, watoe taarifa rasmi kwa ngazi za juu zao, ili ngazi hizo husika nazo ziwasilishe kunakohusika, kwa ajili ya chama kuchukua hatua zaidi.

Imetolewa leo Juni 24, 2012 Dar es Salaam na
Msafiri Abdulrahaman Mtemelwa
Mkurugenzi wa Kampeni na Uchaguzi CHADEMA 

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.