17 Mar 2016


Nilianza kumsikia Balozi Mwapachu tangu nikiwa mtoto mdogo. Huyu ni miongoni mwa yale majina ambayo miaka nenda miaka rudi utayasikia, kama sio kwenye uwaziri basi ni kwenye ukurgenzi wa taasisi flani, au uongozi wa tume flani kama sio ubunge. Wenzetu hawa ni kama watu waliozaliwa ili kuwa viongozi. Lakini hio sio dhambi wala kosa, maana yawezekana kuzeekea kwao katika uongozi ni matokeo ya uongozi wao wa kupigiwa mstari.

Hold on, nimesema 'uongozi wa kupigiwa mstari'? May be, maana dunia hii tunayoishi sasa hata sifa za uognzi hazijulikani ni zipi. Na sababu ya wazi ya sifa za uongozi kupoteza maana yake ni ubabaishaji, usanii,ufisadi, ujambazi, na kila baya unaloweza kulihusisha na tasnia ya uongozi.

Sie wengine tulikulia zama za chama kimoja. Tulishuhudia uongozi uliotukuka wa Mwalimu Nyerere. Ndio, kulikuwa na kasoro zake, kama vile viongozi kuonekana kama miungu-watu, lakini hawakuonekana miungu-watu kwa sababu ya utajiri wao bali angalau waliutumikia umma kwa namna moja au nyingine.

Tuliwaona viognozi mashambani, tuliwaona wakishiriki katika shughuli za ujenzi wa taifa, matengenezo ya barabara, ushiriki katika ujenzi wa miradi ya maendeleo, na vitu kama hivyo. Kumbuka, enzi hizo tulikuwa nchi ya ujamaa na kujitegemea, na miongoni mwa features za kujitegemea ilikuwa kutumia raslimali zetu, sio siku hizi zama za kutembeza bakuli kwa wafadhili, kisha kinachopatikana 'kinapigwa panga,' watu wanaporomosha mahekalu, wanaongeza idadi za magari yao ya kifahari, na sensa ya nyumba ndogo zao inazidi kukua.

Kwanini nimeandika 'kwa hasira' hivi? Jana nimesikia kituko kilichonichefua. Mmoja wa Watanzania wenye majina makubwa katika medani za uongozi, Balozi Juma Mwapachu, jana alitangaza kurejea CCM baada ya kukihama chama hicho tawala wakati tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu.

Kama nilivyosema awali, nimekuwa nikimsikia Juma Mwapachu tangu nikiwa mdogo. Lakini, mwaka jana nilipata fursa ya kuwasiliana nae. Sio uso kwa uso bali kupitia kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter. Sijui tulikuwa tunajadili nini lakini moja ya ajenda iliyojitokeza ni sapoti yake kwa Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, ambaye baadaye aliteuliwa kuwa mgombea Urais kwa tiketi ya UKAWA. 

Balizo Mwapachu alijitokeza kuwa miongoni mwa watetezi wakuu wa Lowassa, huku nyakati kadhaa akitukumbusha 'yeye ni nani.' Wapo walioungana nae mkono lakini baadhi yetu tulimpinga waziwazi na kueleza bayana kuwa ni 'wazee' kama yeye walioifikisha Tanzania yetu mahali hapa pasipoeleweka. Baadaye akapotea mtandaoni, pengine kwa sababu 'wazee' kama yeye hawajazowea sana 'mbinde' za social media.

Alipotangaza kuachana na CCM na kumfuata Lowassa, halikuwa jambo la kushangaza kwa sie tuliowahi kushuhudia akimtetea huko Twitter. Baada ya kuhama CCM akajitahidi kutumia uweledi wake kueleza, kwanza kwanini CCM ni 'kimeo,' na pia kwanini Lowassa ndio ufumbuzi wa matatizo yanayoikabili Tanzania. Baadhi ya aliyoyasema yalikuwa na ukweli, lakini baadhi yetu hatukumuelewa kwa sababu moja tu: "alikuwa wapi siku zote hizo?" Yaleyale ya akina Lowassa, Kingunge, Sumaye na wengineo waliogeuka wakosoaji wakubwa wa mfumo walioshiriki kuuasisi huko CCM, mfumo wa wateule wachache huku mamilioni ya walalahoi wakiishia kuahidiwa hili kama sio lile.

Sasa jana akaamua kubadili gea angani, akatangaza kurudi CCM. Good, kuhama sio dhambi. Tatizo la msingi ni baadhi ya sababu alizoeleza kuwa zilimpelekea kuhama CCM na sasa kuamua kurejea.

Anadai 'alilewa' na ahadi ya Lowassa kuwa angepewa Uwaziri wa Mambo ya Nje. Hivi inaingilia akilini kweli kwa mtu kama huyo ambaye alikuwa miongoni mwa 'vijana wa Nyerere' kuhama chama alichokiasisi baba wa taifa kwa sababu tu alitarajia kupewa uwaziri wa mambo ya nje? Pengine sio kosa kwa sababu ni watu wangapi wasiotaka madaraka?

Lakini ili umuelewe vema ni muhimu kurejea posts zake mbalimbali huko Facebook na kwingineko alivyokuwa akiwahadaa vijana kuhusu ajenda ya mabadiliko. Kwanini nasema alihadaa? Kwa sababu mwenyewe amekiri jana kuwa kilichomvutia kwa Lowassa ni ahadi ya uwaziri wa mambo ya nje. Kule anahubiri kuhusu mabadiliko, huku anawazia uwaziri wa mambo ya nje. Baada ya Lowassa kushindwa kupata urais, na ndoto ya Mwapachu kuwa waziri wa mambi ya nje kuota mbawa, kaamua kurejea CCM. 

Tabia kama hizi zinaweza kuigharimu CCM huko mbeleni. Watu walioikimbia wakati wa shida (kwa maana ya mapambano ya kumwingiza mgombea wake Ikulu) wanaruhusiwa kurejea kiulaini tu na kigeugeu chao kurushwa na vyombo vya habari kana kwamba ni matukio yenye umuhimu mkubwa kihistoria.

Laiti ningekuwa na mamlaka huko CCM, ningemweka benchi Mwapachu kwa sababu kama alivyoondoka akiwa hana umuhimu wowote kwa chama hicho, ndivyo alivyorudi akiwa na umuhimu mdogo zaidi ya ule ambao hakuwa nao wakati anahama.

Nimalizie makala hii ya dharura kwa kutamka bayana kuwa Tanzania yetu imefikishwa hapa na vipongozi kama hawa, walafi wa madaraka licha ya kuwepo madarakani miaka nenda miaka rudi, viongozi wasio na msimamo, wanaoweza kuhadaa umma kuhusu mabadiliko ilhali mabadiliko pekee wanayopigania ni ya maslahi yao binafsi.

Nigusie jambo moja dogo baada ya majuzi kutangazwa viongozi wapya na wa zamani kuongoza mikoa yetu kama ma-RC. Sina tatizo na wengi walioteuliwa lakini kilichonisikitisha ni kuona baadhi ya sura zilezile za miaka nenda miaka rudi zikirudishwa kwenye uongozi. Kama mtu alikataliwa na wapigakura jimboni kwake kwanini apelekwe kuongoza watu wa mkoa mwingine? 

Na lini vijana wapya watapewa fursa ya kuongoza Watanzania wenzao iwapo tunaendelea ku-recycle sura zilezile? Mimi ni sapota mkubwa wa Rais Magufuli, tangu wakati wa kampeni hadi sasa. Ninaridhishwa mno na uongozi wake. Hata hivyo, hiyo haimaanishi akikosea sintomkosoa. Na kama nina moja la kumkosoa ni kutujazia sura za watu waliokaa kwenye uongozi miaka nenda miaka rudi [na usidhani ninalaumu kuhusu hilo kwa vile nilikuwa/nina matarajio ya uongozi. Licha ya kuridhiska na kidogo ninachopata hapa, pia ninaamini kuwa ili kuitumikia Tanzania yetu sio lazima mtu awe kiongozi. Just be a good mwananchi]

Yayumkinika kuhisi kuwa watu wa aina hiyo hawana cha kupoteza wakiboronga na kutimuliwa, kwa sababu baadhi yao tayari wanakula pensheni za ubunge au ukurugenzi wa kitu gani sijui. Wakitimuliwa, watanufaika kwa nyongeza ya fedha tu.

Na sintoshangaa pengine Mwapachu karudi CCM kubahatisha kupewa 'pande' la ubalozi. Na huwezi kumlaumu sana kwa sababu medani ya uongozi wetu imekuwa ni suala la ku-recycle watu walewale, wengi wakiwa ndio walioifikisha Tanzania yetu hapa tusipostahili kuwa.





15 Mar 2016

Rais Dkt John Magufuli amekutaa kukutana na ujumbe wa maseneta sita wa Marekani, tukuio lililojiri tarehe 18 ya mwezi uliopita. Ombi la maseneta hao kukutana na Rais liliwasilishwa na Waziri wa zamani wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, ambaye alikuwa mwenyeji wa maseneta hao walioongozwa na Seneta James Inhofe wa chama cha Republican kutoka jimbo a Oklahoma. Hata hivyo, Rais Magufuli alikataa ombi la kukutana na maseneta hao akidumisha taswira yake ya kujiweka mbali na wafanyabiashara na lobbyists.

Mwaka juzi, Seneta huyo mhafidhina alishutumiwa vikali na kundi moja la utetezi wa haki za wanyama baada ya kuhudhuria hafla moja ambapo njiwa walirushwa hewani na kutunguliwa kwa risasi.



Mtandao wa kiuchunguzi wa African Intelligence unaripoti kwamba waziri huyo ya zamani katika serikali ya Rais Mstaafu Jakaya Kikwete anajulikana kwa kuwa karibu na Wamarekani matajiri wanaohusiana na Mfuko wa Kuhifadhi Mazingira wa Friedkin. Mfuko huo unamiliki makampuni ya Tanzania Game Trackers Safaris, Wengert Windrose Safaris na Mwiba Holdings Limited. Kampuni hiyo ya mwisho imekuwa ikihusishwa mara kadhaa na kesi za ujangili


4 Mar 2016

MWISHONI mwa wiki iliyopita, mitandao kadhaa ya kijamii ilitawaliwa na shutuma dhidi ya tabia inayotoa mizizi kwa majirani zetu wa Kenya kutumia vivutio vya Tanzania kujitangaza kana kwamba vipo katika nchi hiyo.

Katika tukio la majuzi, video moja ilisambaa mtandaoni ikimwonyesha binti mmoja wa Kenya akihutubia mkutano mmoja wa kimataifa, huku akieleza bila aibu kuwa miongoni mwa vivutio vilivyopo nchini Kenya ni Bonde la Olduvai (Olduvai Gorge).


Tukio hilo ni moja tu katika mlolongo mrefu wa majirani zetu hao ‘kutupora’ umaarufu wetu, huku ‘uongo’ maarufu zaidi ukiwa kuutangaza Mlima Kilimanjaro kuwa upo Kenya. Hata Jumapili wiki hii nilipotembelea mtandao wa kijamii wa Twitter, nilikutana na ‘tweet’ moja inayodai kuwa Mlima huo unaonekana vizuri zaidi nchini Kenya (kuliko Tanzania).


Pamoja na lawama kadhaa zilizoelekezwa kwa majirani zetu hao, baadhi ya Watanzania walikwenda mbali zaidi na kuhoji kwa nini nchi jirani inapata ujasiri wa kujinadi kwa kutumia vivutio vyetu. Ukweli mchungu ni kwamba sisi wenyewe tumekuwa wazembe kwa kiasi kikubwa.


Uzembe huo unaonekana katika sura nyingi lakini pengine ya wazi zaidi ni katika ukweli mchungu kuwa licha ya madini ya Tanzanite kupatikana Tanzania pekee, nchi zinazoongoza kwa mauzo ya madini hayo ni India ikifuatiwa na Kenya. Hiki ni kichekesho kinachokera mno.


Binafsi, ninaona udhaifu katika kunadi vivutio vyetu na nchi yetu kwa ujumla unachangiwa na sababu kuu tatu. Ya kwanza, ni uhaba wa uzalendo. Mara kadhaa nimekuwa nikiandika kuhusu suala hili. Moja ya vitu muhimu alivyotuachia Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ni kuthamini Utanzania wetu. Na thamani hiyo ya asili yetu haikuwa kwa sababu tu ni nchi yetu bali pia katika mambo kadhaa ya kujivunia kama vile mchango wa taifa letu katika mapambano ya ukombozi kusini mwa bara la Afrika.


Leo hii baadhi yetu tukikutana na Waafrika Kusini au Wazimbabwe, kwa mfano, wanaikumbuka Tanzania kama nchi iliyoshirikiana nao katika mapambano ya kudai haki yao ya kujitawala. Hata hivyo, baadhi hutuhoji kwa nini Tanzania imepoteza umaarufu mkubwa wa enzi za Mwalimu Nyerere.


Sababu ya pili, inayoshabihiana na hiyo ya kwanza ni ubinafsi. Watanzania wengi wamekuwa wakiweka mbele zaidi maslahi yao binafsi kuliko maslahi ya taifa letu. Umaarufu binafsi umekuwa ukipewa kipaumbele zaidi kuliko umaarufu wa nchi yetu. Kibaya zaidi, wachache tunaojitahidi kuitangaza nchi yetu kwa namna moja au nyingine huishia kuzodolewa kuwa tunafanya hivyo kwa minajili ya kujikomba au kusaka ukuu wa wilaya.


Katika hilo la ubinafsi, kunapojitokeza mawazo ya kuitangaza nchi yetu kimataifa, badala ya kuangalia taasisi au watu wenye uwezo wa kutekeleza jukumu hilo kwa ufanisi, fursa huelekezwa kwa ndugu, jamaa na marafiki wasio na uwezo. Kipaumbele huwa kwenye fedha zilizotengwa kwa shughuli hiyo na wala sio matokeo chanya.


Sababu ya tatu ni kutowatumia vema Watanzania walio nje ya nchi. Kimsingi, kuwa Mtanzania nje ya nchi ni kama laana ya aina fulani. Kwa kiasi kikubwa tu, baadhi ya Watanzania wenzetu wanatuona sisi tulio nje ya nchi kama Watanzania vipande, yaani tusio kamili, na hatupaswi kujihusisha na masuala yanayohusu nchi yetu.


Baadhi yetu tunapojaribu kushiriki ujenzi wa taifa letu kwa njia kama hizi za maandiko huishia kukatishwa tamaa na kauli kama acha kutukebehi. Shida tunazopata hapa wazijua? Kana kwamba mtu akiwa nje ya Tanzania ndio amepoteza kila mawasiliano (connection) aliyonayo na nchi yetu, kuanzia ndugu, jamaa na marafiki hadi uraia.


Kama kuna nchi mbili barani Afrika ambazo zimenufaika sana kuwatumia raia wake wanaoishi nje ya nchi, nchi hizo ni Rwanda na Nigeria. Kwa Rwanda, takriban kila mwaka nchi hiyo hufanya makongamano katika nchi mbalimbali duniani, hususan hapa Uingereza na Marekani. Wiki iliyopita, Rais Paul Kagame yupo nchini Marekani, ambapo pamoja na mambo mengine anahamasisha Wanyarwanda walio nje ya nchi kushiriki katika ujenzi wa taifa lao.


Katika makongamano yaliyopita ya Rwanda hapa Uingereza, Rais Kagame alifanikiwa kuwashawishi Wanyarwanda kadhaa waliokuwa wanaishi hapa kurejea nyumbani na kuwapatia fursa mbalimbali zilizoendana na sifa, ujuzi na uzoefu wao walioupata walipokuwa hapa.
Kwa Nigeria, kabla ya kuunda serikali yake, na wakati huu ambapo nchi hiyo inapitia mageuzi makubwa ya kiuchumi, Rais Muhammad Buhari amekuwa akifanya jitihada kubwa kuwashawishi raia wa nchi yake waliotapakaa sehemu mbalimbali duniani kurejea katika taifa hilo ili kushiriki katika kulijenga na kuliboresha.


Sambamba na hatua hizo, badala ya kutumia fedha nyingi katika tenda za kuzipromoti nchi hizo nje ya nchi, kipaumbele kimekuwa katika kuwatumia raia wake kadhaa waliopo nje ya nchi hizo.


Licha ya kuvunjwa moyo, baadhi yetu tumeendelea na jitihada hizo za kuitangaza Tanzania yetu kwa kutumia njia mbalimbali. Kwa mfano, kwa muda sasa, binafsi nimekuwa nikijaribu kuitangaza Tanzania yetu kwenye mtandao wa kijamii wa twitter kwa mabandiko (tweets) yanayoambatana na hashtag #VisitTanzania (kwa kila habari au picha inayohusu vivutio vyetu) na #InvestInTanzania (kwa habari au picha zinazohusiana na fursa za uwekezaji huko nyumbani. Hata hivyo, mapokeo yamekuwa sio ya kuridhisha japo hainivunji moyo.


Kwa upande mwingine, licha ya uandishi wa vitabu kwa lugha ya Kiswahili kuchangia jitihada za kuitangaza Tanzania yetu kupitia lugha yetu ya taifa, ninaitumia pia fursa niliyoipata hivi majuzi ya kufundisha Kiswahili kwa kundi la wanafunzi wa shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu cha Glasgow, (wanaotarajia kuja huko nyumbani kwa ajili ya tafiti zao) kuitangaza nchi yetu kwa namna moja au nyingine.


Nihitimishe makala hii kwa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuhusu busara hii: “…usipoeleza mazuri yako wewe mwenyewe, wenzako wataeleza mabaya yako au kuyapora mazuri yako hayo.” Hicho ndio kinachofanywa na majirani zetu wanaojinadi kwa kutumia vivutio vyetu. Sisi wenye vivutio hivyo tumejisahau/tunazembea, wenzetu wanaojua umuhimu wa kujinadi wanatumia vyema kujisahau kwetu/uzembe wetu kwa manufaa yao.
Kadhalika, ninatoa wito kwa Serikali ya Rais Dk. John Magufuli kutumia vyema Watanzania wenye uwezo na fursa za kuinadi nchi yetu, ndani na nje ya Tanzania.


Mungu Ibariki Tanzania

26 Feb 2016

WIKI mbili zilizopita nilishiriki katika mjadala maalumu ulioendeshwa na Idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Ujerumani kuhusu siku 100 za utawala wa Rais John Magufuli.
Lengo la makala hii sio kuzungumzia mjadala huo bali mada ya hiyo muhimu kwa Dk. Magufuli na serikali yake ya Awamu ya Tano, pamoja na Watanzania kwa ujumla.
Katika baadhi ya makala za hivi karibuni nilieleza kuhusu kitabu nilichochapisha kuhusu Dk. Magufuli na safari yake ya kuelekea Ikulu, sambamba na mafanikio na changamoto kwa urais wake. Lakini nilikosolewa na watu kadhaa waliodai ni mapema mno kuzungumzia mafaniko ya kiongozi huyo katika muda mfupi aliokaa madarakani.
Hata hivyo, wakosoaji hao walikerwa na mafaniko tu na si changamoto kwake, ikiashiria bayana kuwa wangependa zaidi kuona Dk. Magufuli akikosolewa kuliko kupongezwa.
Mshiriki mmoja katika mjadala huo naye aligusia hoja hiyo na alitumia muda mwingi kukumbusha kuwa hata watangulizi wake (Dk. Magufuli) walianza urais wao kwa kasi kama hii tunayoshuhudia hivi sasa.
Sina tatizo sana na wanaodhani ni mapema mno kusherehekea ufanisi mkubwa unaoendelea kuonekana katika uchapakazi wa Magufuli na serikali yake. Kimsingi, hofu waliyonayo wanaodhani ni mapema mno ina mantiki, hasa kwa vile yalishatukumba huko nyuma.
Kwa mfano, katika awamu yake ya kwanza, Rais Benjamin Mkapa alifanikiwa kurejesha nidhamu ya matumizi na takwimu za uchumi wetu zilipaa. Hata hivyo, awamu ya pili ya uongozi wake ilikuwa na mengi yaliyoathiri mazuri mengi aliyofanya katika awamu yake ya kwanza.
Kadhalika, katika utawala wa Rais Jakaya Kikwete, mwanzoni ilonekana kuwa Tanzania imempata kiongozi ambaye sio tu anayajua matatizo yanayoikabili nchi bali pia mwenye nia ya dhati ya kuyatatua. Kaulimbiu ya Maisha Bora kwa Kila Mtanzania ilileta matumaini kwa kila Mtanzania. Vile vile, maelezo yake kwamba sio tu anawafahamu wala rushwa bali pia anawafahamu kwa majina ilileta hisia kuwa arobaini ya wala rushwa imewadia. Sote tunafahamu kilichojiri katika miaka 10 ya utawala wake.
Kwa mantiki hiyo, wenye kumbukumbu hizo zisizopendeza wana haki ya kuwa na hofu ya mwenendo wa kuridhisha wa utawala wa Dk. Magufuli na serikali yake inayoendeshwa kwa kuzingatia kaulimbiu ya Hapa Kazi Tu.
Hata hivyo, nilitumia mfano huu katika mjadala huo wa Idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Ujerumani, timu mbovu ya soka, ambayo miaka nenda rudi imekuwa ikiboronga, itakapokuwa na mechi muhimu, ikafunga goli la kwanza tu, basi mashabiki hawawezi kuacha kushangilia kisa huko nyuma ilikuwa kichwa cha mwendawazimu.
Mashabiki wataishangilia na kuihamasisha, ambapo hamasa hiyo ikichanganywa na goli moja walilokwishafunga, vyaweza kuipa nguvu timu hiyo ya kichovu kupata bao jingine na pengine mengi zaidi.
Kwa mashabiki wa soka wa ligi kuu ya hapa Uingereza, ni nani alidhani timu ya kawaida tu ya Leicester City ingekuwa miongoni mwa timu zenye nafasi kubwa ya kuchukua ubingwa kuliko wakongwe kama Manchester United?
Mfano huo unamaanisha kwamba kwa vile mwenendo wa Tanzania yetu katika awamu zilizopita ulianza kwa matumaini na kisha matumaini hayo kuyeyuka haimaanishi kuwa lazima iwe hivyo milele. Tukumbuke kuwa penye nia pana njia, pasipo na nia pana visingizio.
Pengine kabla ya kumhukumu Magufuli kama Rais ni vema kuangalia utendaji wake huko nyuma katika nyadhifa mbalimbali alizoshika. Kimsingi, moja ya ugumu mkubwa niliokumbana nao wakati naandika kitabu kinachomhusu ni uhaba wa maelezo kutoka kwake mwenyewe. Yaani machache yaliyo kwenye vyombo vya habari yanaelezea zaidi kuhusu aliyokuwa akitenda kuliko aliyoongea.
Wakati pekee ambapo kauli za Magufuli zilisikika zaidi ni wakati wa kampeni za kuwania urais. Na kauli hizo ndizo zilizotupatia ushawishi sisi wengine kuamini kuwa huyo ndiye kiongozi ambaye Tanzania inamhitaji. Sio tu alionyesha kujua kwa undani matatizo yanayoikabili nchi yetu bali pia alikuwa na mwelekeo kuhusu jinsi ya kuzikabili na kuzitatua.
Na kama ilivyokuwa kwenye zama za uwaziri, Magufuli tangu aingie Ikulu amekuwa mwingi wa vitendo kuliko maneno. Anapozungumza, unatamani aendelee maana hazungumzia kama kiongozi tu bali pia kama Mtanzania ambaye amechoshwa na mwenendo wa taifa letu na amedhamiria kubadilisha mwelekeo kwa uzuri.
Changamoto si lazima ziwe kikwazo kwa kiongozi. Kimsingi, changamoto ni kipimo kizuri kwa kiongozi kwa sababu kadri anavyozishughulikia zinaonyesha uwezo wake wa kiuongozi. Na itakuwa sio kumtendea haki kama akili yetu itaelekezwa kwenye changamoto tu (na ambazo baadhi amekuwa akizishughulikia vema) na kupuuzia mafaniko ya kihistoria aliyokwishapata.
Vile vile ni muhimu kutambua hali ya nchi yetu ilivyokuwa wakati Magufuli anaingia madarakani. Takriban kila eneo lilikuwa shaghalabaghala. Angeweza kabisa kujipa kisingizio kwa hotuba mfululizo kutueleza mlolongo wa matatizo na changamoto zilizopo huku akihitaji muda wa kuanza kuzishughulikia.
Lakini kama tunavyoshuhudia, na kwa vile sote tunamfahamu kama mtu wa vitendo zaidi kuliko maneno, anashughulikia matatizo na changamoto hizo zaidi ya kuongea tu.
Kuna tatizo kuhusu Zanzibar, ambalo kwa hakika linatia doa kuhusu Awamu ya Tano. Hata hivyo, kumlaumu Magufuli kwa vile ni Rais wa Tanzania nzima ni kupuuza mkanganyiko wa kikatiba kati ya ile ya Muungano na hiyo ya Zanzibar. Tunapoambiwa kuwa Magufuli hawezi kutatua mgogoro huo ni ukweli, na kama tunavyofahamu, ukweli una sifa moja kuu: hata ukiwa mchungu, hauwi uongo bali unabaki ukweli. Tungependa afanye kitu fulani kuhusu mgogoro huo lakini Katiba inambana.
Kuhusu ushauri wa nini kifanyike baada ya siku hizo 100 za urais, nafasi katika makala hii haitoshi kuelezea kwa kirefu lakini machache ni haya: mosi, asiingie mtego wa kutanguliza maslahi ya kisiasa badala ya maslahi ya nchi (na historia yaonyesha kuwa amekuwa akiongozwa na utaifa kuliko itikadi za kisiasa.
Pili, sambamba na mapambano endelevu kuhusu ufisadi, rushwa na uhalifu mwingine, aweke mkazo katika kuhamasisha uzalendo ambao umepotea kwa kiasi kikubwa. Hii itasaidia pia kupata uungwaji mkono kwenye mapambano yake dhidi ya ufisadi na uhalifu mwingine.
Tatu, kuhamasisha kilimo kwa vitendo badala ya sera mfululizo zilizoishia kuwa sera tu pasi mafanikio. Vile vile, aweke kipaumbele kuhakikisha kuwa licha ya kuwa mkombozi wa kiuchumi kwa wakulima, kilimo kinakuwa chanzo cha ajira.

Nne, haja ya kuyaangalia maendeleo ya sayansi na teknolojia kama mahitaji muhimu (basic needs) na sio anasa (luxury), kwa sababu katika miaka michache ijayo, tunapopuuza maendeleo ya sayansi na teknolojia tutabaki kuwa kama kisiwa.
Tano, kuendeleza mabadiliko ya Katiba ambayo yatazingatia maslahi ya nchi badala ya chama, na hili linaweza kutoa ufumbuzi wa migogoro isiyoisha kila kunapofanyika uchaguzi mkuu huko Zanzibar.
Sita, tumbua majipu ihamie kwenye chama tawala, hasa kwa vile huko ndiko kunakoweza kumkwaza zaidi kuliko vyama vya upinzani. Inakera mno kuona mwanasiasa mwenye lundo la tuhuma za ufisadi akichaguliwa kushika nafasi muhimu kwenye taasisi kama Bunge, kwa vile tu amepigiwa debe na wana-CCM wenzake.
Saba, hatujawa na mfumo wa kuthamini mchango wa Watanzania wenzetu, walio ndani au nje ya nchi yetu, wanaojitoa mhanga kupigania maslahi ya nchi yetu. Ifike mahala michango yao itambuliwe, si kwa kupewa vyeo bali hata kutambua rasmi (acknowledge) jitihada zao kwa pongezi tu.
Nane, kubwa zaidi ni mageuzi kwenye Idara ya Usalama wa Taifa (nimeyaeleza kwa kirefu katika kitabu nilichochapisha majuzi kuhusu taaluma hiyo nyeti).
Mwisho, kama alivyoeleza katika hotuba yake kwa wazee wa Jiji la Dar es Salaam, wakati tunajadili siku zake 100 tangu aingie aingie madarakani, je, sisi wenyewe kama wananchi tumefanya nini kwa nchi yetu katika siku hizo 100?
Tusijadili tu Magufuli ameifanyia nini Tanzania, tujiulize pia nasi tumeifanyia nini nchi yetu. Tusitarajie tu Magufuli atafanya nini, tutafakari nasi tunafanya au tutafanya nini kwa nchi yetu.
Hongera Magufuli kwa kutimiza siku 100 za urais wako kwa ufanisi wa kupigiwa mstari. Mungu akuongoze uendelee kuwa mtumishi bora wa umma, na atuongoze nasi wananchi kukuunga mkono na kutimiza wajibu wetu wa kiraia.
Mungu mbariki Rais Magufuli
Mungu Ibariki Tanzania yetu.
Mungu tubariki Watanzania

ANGALIZO: Makala hii ilipaswa kuchapishwa Jumatano mbili zilizopita lakini haikuchapishwa kwa sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu. Iliandikwa maalum kwa ajili ya tathmini ya siku 100 tangu Rais Dokta Magufuli aingie madarakani.



29 Jan 2016

KATIKA tasnia ya ushushushu kuna kitu kinachoitwa Moscow Rules (yaani Kanuni za Moscow). Hizi ni kanuni za zama za Vita Baridi ambazo majasusi waliopangiwa kazi nchini Urusi walipaswa kuzizingatia, kwa sababu nchi hiyo ilikuwa nguli wa kukabiliana na majasusi. Moja ya kanuni hizo inasema; “Once is an accident. Twice is a coincidence. Three times is an enemy action.” Kwa tafsiri isiyo rasmi; kitu kinachojiri mara moja ni ajali; kikijiri mara ya pili ulinganifu wa bahati mbaya, sio makusudi; kikijiri mara ya tatu ni kitendo cha adui.”

Nimeanza makala hii na angalizo hilo kwani ndio wazo lililoniingia kichwani mara baada ya kusoma kauli za aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, katika Serikali ya Awamu ya Nne, Bernard Membe.

Wiki iliyopita, Membe alinukuliwa na vyombo vya habari akimkosoa Rais Dk. John Magufuli, angalau katika maeneo matatu. Kwanza, Membe alidai kuwa kiuhalisi, Dk. Magufuli hajapunguza idadi ya wizara kama alivyoahidi bali amepunguza idadi ya mifuko, na kutanabaisha kuwa Rais hajabana matumizi yoyote kwa kupunguza ukubwa wa baraza la mawaziri, bali alichofanya ni kupunguza idadi ya mawaziri na sio wizara.

Alichofanya ni sawa na kuwa na mayai kumi halafu ukaamua kuyaweka kwenye mifuko kumi, maana yake ni kwamba utakuwa na mifuko kumi yenye mayai,” alisema waziri huyo wa zamani ambaye pia alikuwa miongoni mwa makada wa CCM waliowania kuteuliwa kugombea urais kwa tiketi ya chama hicho tawala.

Lakini unaweza kuwa na idadi hiyo hiyo ya mayai na ukaamua kuyagawanya; mayai matatu unayaweka kwenye mfuko mmoja, mawili kwenye mfuko mwingine na yaliyobaki kwenye mfuko mmoja. Maana yake ni kwamba utaendelea kuwa na mayai kumi lakini idadi ya mifuko imepungua. Hapa sasa utakuwa hujapunguza gharama za kuyatunza hayo mayai,”aliongeza Membe.

Membe alidai kwamba Magufuli ameendeleza wizara zile zile lakini kaamua kuzikusanya pamoja, na kuona kuwa mfumo huo mpya wa wizara unaweza kuathiri uwasilishaji wa bajeti bungeni kwa vile mawaziri sasa watahitaji muda mwingi zaidi kuliko ilivyokuwa awali.

Hilo tutaliona kwenye Bajeti ya Serikali ya mwaka huu. Tuone kama bajeti itaongezeka au itapungua? Kwa sababu kama wizara zimepungua kama tunavyoamini, lazima bajeti ipungue, sasa bajeti ikiongezeka au ikibaki vile vile maana yake hakuna kilichofanyika,”alitahadharisha.

Eneo la pili ambalo Membe alimkosoa Magufuli ni udhibiti wa safari za nje, akidai kuwa Tanzania si kisiwa. Membe, aliyekuwa mtetezi mkuu wa safari mfululizo za Rais (mstaafu) Jakaya Kikwete nje ya nchi, alisema kuwa safari za nje zina manufaa kwa taifa, na kusisitiza kuwa lazima Rais Magufuli asafiri kwenda nje ya nchi.

Tanzania si kisiwa, hata ukiwa tajiri namna gani lazima utoke nje ya nchi yako,” alisema Membe, na kutahadharisha kuwa nchi yetu inaweza kuwa kama Zimbabwe kwani ukijitenga, utatengwa.
Alisema nchi ina mabalozi 36 tu duniani kote kati ya nchi 194 zinazohitaji uwakilishi huo na kibaya zaidi, mabalozi hawaruhusiwi kuingia kwenye baadhi ya vikao, na hata wakiingia wakifika kwenye hatua ya uamuzi watazuiwa kushiriki.

Eneo la tatu ambalo japo hakumtaja Magufuli wala kukosoa moja kwa moja lakini linaloweza kutafsiriwa kama kuikosoa serikali kuhusu wafanyabiashara, ambapo alitahadharisha serikali kutowachezea.

Waziri huyo ambaye pia ni mbunge wa zamani wa Mtama (CCM) alipongeza kasi ya Magufuli katika vita dhidi ya ufisadi na kudhibiti mianya ya kukwepa kodi lakini akatahadharisha kuhusu haja ya kuwa mwangalifu katika kuwashughulikia wafanyabiashara. Alidai kuwa wafanyabiashara wana masikitiko makubwa dhidi ya serikali, na anaona suala hilo litaibuka kwa kishindo bungeni.

Licha ya maeneo hayo matatu, Membe alizungumzia kauli ya aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa, aliyedai wafanyabiashara waliomuunga mkono wananyanyaswa. Alieleza kuwa si dhambi kwa wafanyabiashara kufadhili vyama vya siasa wakati wa uchaguzi, na kwamba serikali ya chama kilichoshinda uchaguzi inapaswa kuwakusanya wafanyabiashara wote na kufanya nao kazi na sio kuwaburuza.

Kadhalika, mwanasiasa huyo alizungumzia kuhusu “timua timua” ya watumishi wa umma wanaohusishwa na tuhuma za ufisadi.

Ni rahisi kumshughulikia mtu usiyemfahamu lakini siyo rahisi kumshughulikia mtu unayemfahamu,” alidai Membe, na kuongeza kuwa haitokuwa shida kwa Magufuli kuwashughulikia watendaji aliowakuta serikalini ambao kimsingi hakuwateua, na hawafahamu. Alihoji iwapo Rais ataweza kuwatimua aliowateua mwenyewe.

Kauli hizo za Membe zimezua mjadala mkubwa, hususan kwenye mitandao ya kijamii. Japo kabla yake, aliyekuwa Naibu wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Makongoro Mahanga, alimkosoa Magufuli kuhusu ukubwa wa kabineti yake, ukweli kwamba Membe bado ni kiongozi wa juu wa CCM ilhali Mahanga alihamia upinzani, unaashiria mengi.

Lakini binafsi sikushangazwa na kauli hizo za Membe, hasa kwa vile awali, katika kitabu nilichokichapisha hivi karibuni kuhusu safari ya urais wa Magufuli, mafanikio na changamoto katika urais wake, nilibainisha kuwa moja ya changamoto zinazoweza kumkabili Rais huyo wa Awamu ya Tano ni maadui wa ndani ya chama chake.

Kimsingi, hoja zote za Membe hazina mashiko. Kuhusu anachoita ukubwa wa baraza la mawaziri, la muhimu kwa Watanzania si ukubwa au udogo bali uchapakazi. Ni bora kuwa na mawaziri, manaibu na makatibu wakuu hata 1,000 wachapakazi, kuliko kuwa na serikali ndogo inayokumbatia mafisadi.
Pia Membe alipaswa kufahamu kuwa utendaji kazi wa viongozi wa serikali unategemea sana utendaji kazi na msimamo wa bosi wao, yaani Rais aliyewateua. Ni dhahiri kuwa Membe anatambua kuwa Magufuli si mtu wa porojo, mtoa ahadi anazoshindwa kuzitekeleza mwenyewe (rejea kauli ya “ninawajua wala rushwa kwa majina” ya Kikwete), na kimsingi Watanzania na dunia nzima wanafahamu kuwa kaulimbiu ya Hapa Kazi Tu ya Magufuli ni tofauti na zama za nchi kujiendesha yenyewe (on autopilot).

Kuhusu safari za nje, Membe amepotoka mno, pengine kwa sababu kwa wadhifa wake wakati huo, alikuwa mmoja wa wasafiri nje ya nchi mara kwa mara. Kwanza, Rais Magufuli hajawahi kutamka kuwa hatosafiri. Kwa hiyo, kauli ya Membe kuwa lazima atasafiri ni fyongo.

Pili, zuio la safari za nje sio ‘blanket ban’ bali ni kwa safari zisizo na tija. Lakini kwa nini tushangazwe na kauli hiyo ya Membe ilhali tunafahamu misafara ya serikali iliyopita ilivyosheheni wajumbe kwa kutumia fedha za umma? Ni mtu mwenye matatizo tu anayeweza kutetea safari zenye manufaa zinazoligharimu taifa matrilioni ya shilingi huku faida tarajiwa zikiwa pungufu ya gharama husika.

Mwanadiplomasia msomi kama Membe alipaswa kuangalia hapo jirani tu kwa Rais Paul Kagame, kulinganisha idadi ya safari zake nje na zile za Kikwete kisha kuangalia hali ya uchumi kati ya nchi hizo mbili.

Vilevile ni rahisi kwa Membe kuzungumzia mafanikio ya safari hizo kwa vile ni Watanzania wachache wanaofahamu vituko vilivyoambatana na safari hizo. Ni mara ngapi safari hizo za ‘manufaa’ zilijumuisha shopping, kuhudhuria birthday parties, na matukio mengine yasiyo na tija kwa serikali?

Kuhusu wafanyabiashara, ni upuuzi wa hali ya juu kuhisi tu kuwa kuna uonevu dhidi ya mfanyabiashara yeyote. Kama kuwabana wafanyabiashara wakwepa kodi ni uonevu basi Magufuli aongeze dozi, maana hizi sio zama za Tanzania kuwa shamba la bibi.

Membe anadai wafanyabiashara wana masikitiko na suala hilo linaweza kuibuka bungeni. Anamaanisha Bunge limejaa wafanyabiashara au? Na kama masikitiko yao ni kutokana na Serikali ya Awamu ya Tano kuwabana ili wasikwepe kodi na kwamba masikitiko hayo yanaweza kusababisha kupoteza wawekezaji, basi na waondoke hata kesho. Hatuhitaji wakwepa kodi nchini. Kimsingi, wanaolalamika wala hawastahili kuitwa wafanyabiashara bali wahujumu wa uchumi wetu.

Na hoja yake kuhusu ‘timua timua’ haishangazi kwani moja ya udhaifu wa serikali ambayo Membe alikuwa waziri ilikuwa ni kuwaonea aibu wanaoboronga, na matokeo yake hali hiyo ilivutia waborongaji wapya kwani walishabaini kuwa hakuna wa kuwachukulia hatua. Hivi Membe anaweza kutuambia lolote kuhusu ahadi ya Riais Kikwete aliyoitoa Februari 2006 kwamba anawafahamu wala rushwa kwa majina na anawapa muda wajirekebishe? Sawa, Magufuli alipoingia Ikulu alikuta orodha hiyo ya wala rushwa aliowajua Kikwete na kuamua kuifanyia kazi?

Nimeeleza awali kuwa nimelizungumzia suala hilo kwa kirefu kitabuni. Sitaki kabisa kuamini kuwa kauli za Membe ni zake peke yake. Hisia zinanituma kuamini kuwa huu ni moshi tu unaoashiria moto unaowaka ndani kwa ndani ya CCM kati ya makundi makuu mawili: la Hapa Kazi Tu la Magufuli linalotaka kuiondoa Tanzania katika lindi la ufisadi unaoifanya nchi yetu kuzidi kuwa masikini, na kundi la wanufaika wa ufisadi linalomwona Magufuli kama mtu anayewaziba pumzi. Naam, ufisadi ni ‘lifeline’ ya watu walioigeuza nchi yetu Shamba la Bibi, wakivuna wasichopanda.

Nimalizie makala hii kwa kutoa wito kwa makada wa CCM, ambao wengi wao wanaimba Hapa Kazi Tu, lakini wakisikia madhambi yaliyofanywa na mwana-CCM fulani wanakimbilia kuwanyooshea vidole wapinzani. Wapinzani wakuu wa Magufuli hawapo Chadema au nje ya nchi bali wapo ndani ya chama hicho tawala. Na njia pekee ya kupambana nao ni kuweka mbele maslahi ya taifa badala ya kutanguliza umoja na mshikamano wa chama. Kuna usemi mchawi akimaliza kuroga mtaa hugeukia familia yake. Majipu yaliyomo ndani ya CCM yasipotumbuliwa mapema yatamkwaza Magufuli na nchi yetu kwa ujumla.


21 Jan 2016


 
MOJA ya mada zinazotawala vyombo vya habari huko nyumbani ni zoezi linaloendelea la bomoabomoa. Zoezi hilo limepokelewa kwa hisia tofauti huku baadhi ya wananchi wakiliunga mkono (hususan wasioguswa nalo) huku wengine wakiilaumu (hususan waathirika wa zoezi hilo)

Kwa upande mmoja serikali na mamlaka husika zipo sahihi kutekeleza zoezi hilo kwa vile suala hilo licha ya kuwa la muda mrefu lakini pia limekuwa na gharama kubwa, kwa serikali na mamlaka husika, kwa maana ya kuwakwamua wakazi wa mabondeni kila yanapojiri mafuriko, na kwa wakazi hao kukumbwa na hasira kubwa kila msimu wa masika.

Kwa maana hiyo, ilikuwa lazima kwa serikali kufika mahala kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa tatizo hilo. Na kwa kiasi kikubwa, hakukuwa na njia ya mkato au ufumbuzi rahisi. Na vyovyote ambavyo ingeamuliwa, ilikuwa lazima wakazi hao wa mabondeni waondoke, aidha kwa hiari yao wenyewe au kwa serikali na mamlaka husika kuwaondosha.

Tayari baadhi ya watu wameanza kuhusisha zoezi la bomoa bomoa na upungufu wa Rais Dk. John Magufuli. Sidhani kama wanamtendea haki. Sawa, tunatambua kuwa kubomolewa makazi na kukosa makazi mbadala si kitu kizuri. Lakini hata hivyo, si Dk. Magufuli au serikali yake iliyowashauri wakazi wa mabondeni kuendelea kuishi katika mazingira hatarishi.

Na kama nilivyoeleza awali, mara nyingi wakazi hao wanapokumbwa na mafuriko, serikali hulazimika kuingia gharama ili kunusuru maisha yao. Kwa hiyo, katika mazingira ya kawaida tu, kwa minajili ya kuepusha gharama hizo, ilikuwa lazima kwa serikali kuchukua hatua stahili.

Lakini pia serikali ina jukumu la kuhakikisha usalama wa raia wake. Kuendelea kuwaachia wakazi wa mabondeni kuishi katika mazingira hatarishi kungekuwa ni sawa na serikali hiyo kuzembea kutekeleza jukumu hilo la msingi, yaani jukumu la kuhakikisha usalama wa raia.
Hata hivyo, pamoja na dhamira nzuri ya serikali katika utekelezaji wa zoezi hilo, pengine ni muhimu kuupa nafasi ubinadamu. Kimsingi, makosa yaliyosababisha uwepo wa makazi hatarishi mabondeni ni ya pande zote mbili: serikali na mamlaka husika, kwa upande mmoja, na wakazi hao, kwa upande mwingine.

Si kwamba siku moja tuliamka na kukuta nyumba zimejengwa mabondeni au kwenye hifadhi za barabara. Misingi ya nyumba ilichimbwa, matofali na vifaa vingine vya ujenzi vililetwa, na ujenzi ukafanyika, na hatimaye wakazi hao kuhamia maeneo hayo, na muda wote huo, serikali na mamlaka husika walikuwepo na hawakuchukua hatua stahili. Japo sio kisingizio mwafaka kwa wakazi hao, lakini kwa serikali na mamlaka husika kutozuia ujenzi huo wakati huo inaweza kuwa ilichangia sio tu kuwafanya waliokwishajenga hapo kudhani wana ruhusa isiyo rasmi bali pia kuliwavuta wengine wasio na mahala pa kujenga.

Sasa, kama wasemavyo waswahili yaliyopita si ndwele, tugange yaliyopo na yajayo, la muhimu kwa sasa ni kupata ufumbuzi utakaozinufisha pande zote mbili.

Kwa vile ujumbe umekwishafika, kwa maana ya wakazi waliosalia mabondeni wamekwishaona yaliyowakuta wenzao, basi sidhani kama kuna ubaya wa kutoa muda wa kutosha na wa kiuhalisia wa kuwaagiza wakazi hao kuhama kwa hiari yao. Kumpa mtu wiki moja ahame sehemu aliyoishi kwa miaka kadhaa sio kuzingatia uhalisia.

Kama iliwezekana kuwapa wakwepa kodi matajiri siku kadhaa walipe madeni, licha ya ukweli kuwa kukwepa kodi ni kosa la jinai, na matokeo yake (tunaambiwa) wengi walitekeleza agizo hilo, basi kwa nini tusijaribu njia hiyo hiyo kwa wakazi wa mabondeni?

Kwa upande mwingine, japo ujenzi wa mabondeni sio tu ni kinyume cha sheria lakini pia unahatarisha maisha ya wakazi husika, madhara yake kwa jamii sio makubwa kama matatizo mengine ya dharura yanayohitaji kushughulikiwa haraka, hususan biashara ya dawa ya kulevya.

Ndio, makazi mabondeni yanahatarisha usalama wa wakazi wa maeneo hayo, lakini angalau hayahatarishi uhai wa wasiokaa mabondeni. Vipi kuhusu dawa za kulevya? Yanapoteza uhai wa vijana wetu kila kukicha huku yakichangia uhalifu kwa kiwango kikubwa. Naam, mtumia dawa za kulevya akikosa fedha ya kununulia dawa hizo, njia ya mkato ni kufanya uhalifu.

Kwa maana hiyo biashara ya dawa ya kulevya ina madhara makubwa kwa jamii kuliko makazi ya mabondeni. Lakini kinachoanza kuvunja moyo ni ukimya wa serikali katika kushughulikia suala hilo ambalo lilipewa kipaumbele cha hali ya juu na Rais Dk. Magufuli alipotangaza dira ya serikali yake wakati anazindua Bunge jipya.

Sambamba na suala la dawa za kulevya ni suala la ufisadi. Ndio, ziara za kushtukiza zimezaa matunda lakini kumekuwa na ukimya kidogo hapa katikati, na sio wa ziara hizo tu bali pia hata utekelezaji wa uanzishwaji wa mahakama maalumu ya kushughulikia kesi za ufisadi.

Siku chache zilizopita nilikutana na habari kuhusu Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Harrison Mwakyembe, kuwa amebaini kuna rushwa katika Mahakama. Hilo sio suala geni, na binafsi nilishangaa kusikia Waziri Mwakyembe amebaini sasa ilhali ripoti mfululizo za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) zimekuwa zikiitaja Mahakama kama miongoni mwa taasisi zinazoongoza kwa rushwa. Je, Waziri Mwakyembe hakuwa akizisoma au kuzisikia habari hizo?

Lakini kilichonikera zaidi ni ukweli kwamba wakati wa mjadala wa ufisadi wa Tegeta-Escrow, zilipatikana taarifa zilizoonyesha majina ya baadhi ya majaji waliopokea mgao uliotokana na ufisadi huo. Hadi leo, majaji hao hawajachukuliwa hatua. Kadhalika, ziliwahi kupatikana taarifa zilizowataja majaji waliotuhumiwa kuwasaidia watuhumiwa wa kesi za dawa za kulevya. Hata hao wanasubiri kuundwa kwa mahakama za ufisadi?

Na tuwe wakweli, hivi kuunda mahakama za ufisadi kunahitaji muda gani hasa ilhali tayari tuna mfumo wa mahakama unaoshughulikia kesi za jinai?

Rais Dk. Magufuli alituasa tumsaidie katika vita dhidi ya maovu mbalimbali yanayoikabili nchi yetu. Kumsaidia si kwa kupiga vigelegele pekee zinapofanyika ziara za kushtukiza au fulani anapofukuzwa kazi bali pia kukosoa pale inapobidi. Matarajio ya wananchi bado yapo juu, na hii ni muhimu sana kwa mafanikio ya mapambano dhidi ya uozo mwingi unaohitaji kushughulikiwa. Kasi hafifu ya kushughulikia matatizo ya ufisadi na uhalifu – kama biashara ya dawa za kulevya – sio tu yaweza kupunguza ari ya wananchi lakini pia yaweza kutoa mwanya kwa wahusika kubuni mbinu mpya, sambamba na kuvutia wahalifu wapya (hususan wale wanaobaini kuwa Shamba la Bibi limefungwa).

Nimalizie makala hii kwa kukumbushia haja ya kuitumia vizuri fursa hii kuikwamua Tanzania yetu kutoka kwenye lindi la umasikini, unaochangiwa na ufisadi na uhalifu mwingine, sambamba na kuweka vipaumbele vyetu sawia kwa kushughulikia matatizo ya haraka badala ya yale yanayoweza kushughulikiwa taratibu. Ndio, Waingereza wanasema “two wrongs don’t make a right,” yaani kufanya kosa la pili hakulifanyi kosa la kwanza kuwa jambo sahihi, na kwa maana hiyo sina maana kuwa kutochukuliwa hatua dhidi ya ‘wauza unga’ kunahalalisha kutofanya bomoa bomoa. Hata hivyo, haja ya kuwashughulikia wahalifu ni ya dharura mno kuliko ya wakazi wa mabondeni.



13 Jan 2016


WIKI iliyopita, watumiaji kadhaa wa mtandao wa kijamii wa Twitter nchini Kenya waliishambulia vikali Serikali ya Tanzania, na Rais Dk. John Magufuli, kutokana na kuanza kwa operesheni ya kudhibiti wahamiaji haramu inayoendelea huko nyumbani (Tanzania).
Aliyeanzisha chokochoko hiyo ni bloga mmoja maarufu nchini humo ambaye awali alimtaka Rais Uhuru Kenyatta kuchukua hatua dhidi ya alichokiita ubaguzi dhidi ya raia wa Kenya wanaoishi nchini Tanzania.’

Bloga huyo si mgeni kwa uchochezi. Ninaita uchochezi kwa sababu madai hayo ya ubaguzi hayakuwa na ukweli wowote. Lakini kwa tunaomfahamu, hatukushangazwa sana na madai hayo, kwa sababu hata huko nchini Kenya, bloga huyo ameshakumbana na misukosuko kadhaa kutokana na kauli zake tata.

Tweets zake kuhusu suala hilo zilisababisha Wakenya kadhaa mtandaoni kuzungumzia uonevu huo huku wakitumia hashtag #OperesheniTimua. Sina hakika kama hilo ndilo jina halisi la operesheni hiyo.

Binafsi niliona shutuma hizo dhidi ya Serikali ya Magufuli kama kichekesho fulani, hasa ikizingatiwa kuwa ni hivi majuzi tu, Wakenya lukuki walikuwa wakimsifu Rais wetu huyo kwa hatua zake mbalimbali za kudhibiti mapato na matumizi, sambamba na kupambana na rushwa, huku wakiilaumu Serikali ya Rais Uhuru.

Majirani zetu hao walikuwa mstari wa mbele katika kuipaisha ‘hashtag’ #WhatWouldMagufuliDo ambayo kimsingi ilikuwa ikionyesha jinsi watu mbalimbali duniani walivyoridhishwa na hatua hizo za Magufuli.

Sasa, tukiafikiana tu kuwa Magufuli amedhamiria kwa dhati kupambana na kila uozo uliopo, basi ni wazi kuwa ilikuwa suala la muda tu kabla serikali yake haijaanza kuvalia njuga suala la uhamiaji haramu. Na ninaamini kuwa majirani zetu wa Kenya hawakutarajia serikali yetu kuwafumbia macho wahamiaji haramu kutoka nchi yoyote ile hata kama ni jirani yetu Kilichonikera zaidi ni kuona tweet ya Naibu Rais wa Kenya William Rutto akifuata mkumbo wa kukemea #OperesheniTimua pasi kujiridhisha vya kutosha kuhusu tuhuma zilizotolewa na bloga husika.
Nilipotafakari kwa undani kuhusu suala hilo nikapatwa na hisia kuwa Tanzania legelege yenye sheria zisizofanya kazi ilikuwa ni habari njema kwa wasioitakia mema nchi yetu. Sio siri kwamba, uzembe mkubwa katika Idara ya Uhamiaji umechangia sana kushamiri kwa tatizo la wahamiaji haramu. Na sio siri pia kuwa majirani zetu, ikiwa ni pamoja na Kenya, walinufaika sana kutokana na uzembe huo.

Lakini zama hizo za raia wa kigeni kununua haki ya makazi nchini mwetu zaelekea kufikia ukingoni, na hiyo si habari njema kwa wanufaika. Lakini hata kama hatua hiyo inawakera basi angalau wangekuwa na ustaarabu katika kulizungumzia suala hilo kuliko kuzusha tuhuma za uongo. Japo ni kweli kwamba kuna raia wengi wa Kenya nchini Tanzania, operesheni hiyo ya kupambana na wahamiaji haramu haiwalengi raia wa kigeni – iwe ni kutoka Kenya au kwingineko – ambao wapo nchini Tanzania kihalali. Iwapo waathirika wengi wa operesheni hiyo ni Wakenya basi labda iwe kutokana na wengi wao kutokuwa nchini mwetu kihalali (nasisitiza labda kwa vile sina takwimu sahihi).

Baadhi ya majirani zetu hao waliochangia mjadala mkali kuhusu mada hiyo walifika mbali na kudai kuwa Tanzania itadhoofika kwa kuwafukuza Wakenya kwa vile inawategemea mno. Binafsi nadhani kauli za aina hii zina madhara zaidi kwa Wakenya wanaoishi kihalali nchini mwetu kuliko madhara kwa serikali na nchi yetu.

Wanaopandikiza chuki hiyo hawapo Tanzania, na endapo kauli zao zitaibua chuki dhidi ya raia wa nchi hiyo, hao wapiga kelele hawatoathirika moja kwa moja bali ndugu zao waliopo nchini mwetu. Lakini si jambo la kushangaza kuona mazuri ya Magufuli yakianza kukera baadhi ya watu. Walishazowea kuiona nchi yetu kama kituko. Na walinufaika na ulegelege uliokuwepo, ikiwa ni pamoja na upungufu katika udhibiti dhidi ya wahamiaji haramu.

Na katika hilo la kukerwa na utendaji unaotia moyo wa Magufuli si majirani zetu hao tu, majuzi nilisikia mahojiano ya kiongozi wa Chadema, Tundu Lissu, akitoa mtizamo wake kuhusu mwenendo wa Magufuli na serikali yake. Lugha yake haikuwa tofauti na inayosikika kwa wengi wa wafuasi wa vyama vya upinzani. Kwao, kufanikiwa kwa Magufuli ni kama kudidimia kwa vyama vyao.

Na hilo sio gumu kulielewa, kwa sababu kwa kiasi kikubwa kushamiri kwa upinzani nchini Tanzania ni matokeo ya udhaifu wa CCM, uliowapa wapinzani nafasi ya kusema chochote, kuliko uimara wa wapinzani binafsi. Kwa maana hiyo, hatua za Magufuli na serikali yake kupambana na mengi yaliyokuwa kero kwa Watanzania kunawanyima wapinzani fursa ya kuongea.

Lawama na shutuma za wapinzani zimevuka mipaka hadi kutugusa baadhi yetu ambao baada ya muda mrefu wa kukosoa mwenendo wa mambo katika nchi yetu, sasa tumepata ahueni kutokana na kazi nzuri ya Magufuli, na tunapata kila sababu ya kupongeza na kuinadi nchi yetu.

Binafsi, nimekuwa miongoni mwa waathirika wa shutuma hizo baada ya kuchapishwa kitabu kinachozungumzia safari ya urais wa Dk. Magufuli, mafanikio na changamoto kwa urais wake. Kuna wanaodai ni mapema mno kuzungumzia mafanikio ya kiongozi huyo, lakini bila kubainisha wakati gani ni mwafaka kuzungumzia mafanikio yake.

Kuna waliokwenda mbali zaidi na kudai kitabu hicho ni jitihada zangu binafsi kutafuta ukuu wa wilaya. Kwa uelewa wangu, shutuma hizo ni matokeo ya hadaa kubwa iliyofanyika kwa wafuasi wengi wa vyama vya upinzani kuwa vyovyote ambavyo ingekuwa, mgombea wao wa kiti cha urais, Edward Lowassa, lazima angeshinda kiti hicho.

Kuishi kinyume cha matarajio hewa si kitu rahisi, na huenda itachukua muda mrefu kwa wapinzani wa Magufuli kubaini kuwa kila zuri analofanya ni kwa maslahi ya Watanzania wote bila kujali tofauti zao za kiitikadi. Tanzania ya neema si tu kwa waliompigia kura Magufuli bali kila Mtanzania, hata aliyemnyima kura.

Wakati tunaweza kuwaelewa majirani zetu wanaokerwa kuona Tanzania imeamka, haingii akilini kuona baadhi ya Watanzania wenzetu wakijifanya vipofu wasioona mabadiliko makubwa na ya kasi yanayoletwa na Magufuli na serikali yake. Walihadaiwa kuhusu mabadiliko, sasa wanaletewa mabadiliko halisi wanaanza kulalamikia.

Katika mahojiano yake niliyoyataja awali, Lissu anamlinganisha Magufuli na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Sokoine, lakini si kwa uchapakazi wake na chuki yake kubwa dhidi ya wahujumu uchumi bali kile ambacho mwanasheria huyo anadai ni kutoheshimu sheria.

Pia alimfananisha Magufuli na Naibu Waziri Mkuu wa zamani, na sasa Mwenyekiti wa taifa wa TLP, Agustino Mrema, kuwa ni kiongozi anayefanya kazi ili aandikwe na vyombo vya habari. Mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Hivi kweli mazuri haya mengi yaliyojiri tangu Magufuli aingie madarakani ni kwa minajili ya kupata vichwa vya habari?

Nimalizie makala hii kwa kukumbusha kuwa kinyume na mabadiliko yaliyoahidiwa na Lowassa ambayo yalitarajiwa kutokea kama miujiza pasipo mipango madhubuti, tunachoshuhudia kwa Magufuli ni mabadiliko ya dhati yaliyobainishwa katika mikutano yake mbalimbali ya kampeni za uchaguzi, na kufafanuliwa kwa kirefu katika hotuba yake ya uzinduzi wa Bunge jipya.


 Ushauri wangu kwa Watanzania wenzangu ni kupuuzia wote wanaokerwa na mwenendo wa kutia matumaini wa Magufuli na serikali yake. Wanasema ukirusha jiwe kizani kisha ukasikia kelele, basi ujue limempiga mtu. Hizi kelele, kebehi au shutuma dhidi yake ni matokeo ya jitihada zake za kizalendo za kuathiri waliokuwa wakinufaika na mwenendo fyongo wa nchi yetu katika maeneo mbalimbali. 

6 Jan 2016

KWA miaka kadhaa, makala zangu za wiki ya mwanzo wa mwaka huzungumzia matukio mbalimbali yanayotarajiwa kutawala habari katika mwaka husika. Makala hii ni mwendelezo wa utamaduni huo. Inajaribu kufanya ubashiri wa baadhi ya matukio yanayotarajiwa kujiri katika mwaka huu, ndani na nje ya nchi yetu.

Nianze na ubashiri wa matukio ya kimataifa. Mwaka huu ni wa Uchaguzi Mkuu nchini Marekani. Kwa kuzingatia mwelekeo wa kampeni zinazoendelea nchini humo, ninabashiri kuwa Hillary Clinton atafanikiwa kushinda kuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chama cha Democrats, ilhali kuna uwezekano mkubwa wa Donald Trump kuibuka mgombea kwa tiketi ya Chama cha Republicans.

Hata hivyo, uwezekano huo unategemea mambo matatu muhimu. Kwanza, kwa wote wawili, nafasi zao kushinda au kushindwa zitategemea mwenendo wa uchumi wa taifa hilo kubwa duniani. Iwapo uchumi wa Marekani utaimarika zaidi, basi Hillary na chama chake watakuwa na fursa nzuri zaidi hasa kwa kutegemea uungwaji mkono wa Rais wa sasa wa nchi hiyo, Barack Obama, kujivunia rekodi ya uchumi chini ya chama chao. Uchumi ukiyumba, Trump, ambaye ni mfanyabiashara tajiri anaweza kuonekana kama chaguo sahihi kuwa rais ajaye wa nchi hiyo.

Jambo la pili, ambalo pia linawahusu wote wawili, ni hali ya usalama nchini humo. Iwapo hali itaendelea kuwa salama kama ilivyokuwa katika miaka minane ya Rais Obama, mgombea wa Democrats, ambaye ninabashiri atakuwa Hillary, atakuwa na nafasi nyingine nzuri ya kujivunia umahiri wa Rais kutoka Democrats kama Obama kulihakikishia usalama taifa hilo linalowindwa kwa udi na uvumba na vikundi mbalimbali vya ugaidi wa kimataifa. Iwapo kwa bahati mbaya kutatokea tukio lolote kubwa la ugaidi, basi hali hiyo yaweza kumnufaisha mgombea wa Republicans, ambaye ninabashiri atakuwa Trump, kwa kigezo chepesi tu kuwa Democrats wameshindwa kuiweka Marekani kuwa salama.

Jambo la tatu ni mwenendo binafsi wa wanasiasa hao wawili. Kwa upande wa Hillary, uwezekano wa yeye kuibuka mgombea wa Democrats utategemea uchunguzi unaoendelea kuhusu matumizi ya barua-pepe binafsi akiwa Waziri wa Mambo ya Nje. Japo Wamarekani wengi hawaonekani kuguswa na yaliyokwishafahamika kuwemo katika maelfu ya barua-pepe hizo, iwapo uchunguzi utabaini makosa makubwa zaidi, basi nafasi ya mwanamama huyo anayewania kuwa rais wa kwanza mwanamke wa taifa hilo itakuwa finyu, na huenda akalazimika kujiondoa katika kinyang’anyiro hicho.

Kikwazo kingine kwa Hillary ni tuhuma zilizoibuka hivi karibuni zinazoashiria uhusika wake katika tenda inayoihusisha Kampuni ya Symbion ambayo inahusu mradi wa uzalishaji umeme nchini Tanzania. Japo alichofanya mwanasiasa huyo sio kitu cha ajabu katika siasa za Marekani na hata katika nchi nyingine, ikigundulika kuwa taratibu zilikiukwa ili kupendelea marafiki zake, anaweza kuathirika vibaya na pengine kulazimika kujiondoa katika harakati zake za urais.

Wasiwasi mkubwa kuhusu Trump ni ile tabia yake ya kuwa kama bomu lililotegeshwa kwa muda (time bomb). Pamoja na kuendelea kung’ara katika kura za maoni miongoni mwa ‘wagombea’ wa Republicans, mwanasiasa huyo hana upungufu wa vioja, na fursa yake ya ushindi itategemea sana jinsi atakavyodhibiti mdomo wake kati ya sasa na wakati wa mchakato rasmi wa chama chake kuteua mgombea. Na hata akiruka kikwazo hicho, bado kuna wasiwasi iwapo Wamarekani watakuwa tayari kumchagua mwanasiasa asiyetabirika. Na endapo watamchagua, basi taifa hilo linaweza kutengwa na nchi nyingi duniani.

Iwapo Hillary hataibuka mshindi kwa tiketi ya Democrats, ninabashiri kuwa nafasi hiyo itakwenda kwa Bernie Sanders, ambaye hata hivyo ana nafasi finyu kumshinda mgombea yeyote atakayepitishwa na Republicans. Na iwapo Trump hatopitishwa, ninabashiri mbadala wake kuwa aidha Ted Cruz au Marco Rubio.

Katika anga hizo za kimataifa, ninabashiri kuwa hali nchini Burundi itakuwa mbaya zaidi ya ilivyokuwa mwaka jana. Kadhalika, ninabashiri hali ya usalama katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kuzorota, hasa baada ya jitihada za Rais Joseph Kabila kutaka kuendelea kubaki madarakani.

Kadhalika, ninabashiri kuwa kundi la kigaidi la Boko Haram litaendelea kuisumbua Nigeria, huku kundi jingine la kigaidi la Al-Shabaab likiendelea kuzisumbua Somalia na Kenya. Pia kuna uwezekano wa kuwepo matatizo ya kisiasa huko Afrika Kusini na Zimbabwe yanayoweza kusababisha kung’oka madarakani kwa viongozi wa nchi hizo.

Habari za ugaidi wa kimataifa zinatarajiwa kuendelea kutawala anga za kimataifa huku makundi mawili hatari ya ISIS na Al-Qaeda yakiendelea kuwa tishio duniani, hususan nchi za Magharibi.

Kadhalika, ninabashiri kuwa eneo la Ghuba na Mashariki ya Kati kuingia katika mgogoro mkubwa utakaoligawa eneo hilo kati ya Waislam wa madhehebu ya Sunni wakiongozwa na Saudi Arabia, na wale wa Shia wakiongozwa na Iran.

Kwa huko nyumbani, ninabashiri kuwa Rais Dk John Magufuli ataendelea na utumbuaji majipu, japo habari ninayobaishiri kuwa itatawala zaidi ni kuibuka kwa skandali mbalimbali zilizojitokeza wakati wa utawala wa Rais Jakaya Kikwete na ambazo umma haukuwahi kuzifahamu. Kimsingi, harakati za Dk. Magufuli kutumbua majipu zina kila ishara ya kukutana na madudu yaliyosheheni wakati wa utawala wa mtangulizi wake.

Kadhalika, ninabashiri uwezekano wa baadhi ya mawaziri au manaibu wao kufukuzwa kwa kushindwa kuendana na falsafa ya Hapa Kazi Tu. Kwa vile si vema kumwombea mtu mabaya, ninahifadhi majina ya mawaziri ninaodhani wanaweza kuwa waathirika wa awali.

Vile vile, ninabashiri uwezekano wa kuwepo jitihada za chini chini ndani ya CCM kukwamisha dhamira ya Dk. Magufuli kukabiliana na ufisadi, rushwa, ujangili, biashara ya dawa za kulevya, na maovu mengine. Hata hivyo, jitihada hizo hazitafanikiwa.

Kwa upande mwingine, ninabashiri kuwa Dk. Magufuli ataendelea kunga’ra ndani na nje ya nchi, na dunia itaelekeza macho yake nchini Tanzania kutokana na mafanikio makubwa ya kiuongozi na jitihada za kufufua na kuboresha uchumi.

Kingine ninachoweza kubashiri ni ujio wa sura mpya nyingi katika uongozi ngazi za mikoa na wilaya, huku ikitarajiwa kuwa kama ilivyokuwa kwa Baraza la Mawaziri na Makatibu wakuu, wasomi mbalimbali wakiteuliwa kushika nyadhifa za u-RC na u-DC.

Kwa upande wa vyama vya upinzani, ninabashiri uwezekano wa jitihada za kumng’oa Mwenyekiti wa taifa wa Chadema, Freeman Mbowe, japo haitakuwa jambo la kushangaza iwapo atanusurika. Kwa kiasi kikubwa, uhai wa kisiasa wa Mbowe utategemea uhusiano wake na aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Ukawa, Edward Lowassa.

Eneo ambalo ninashindwa kubashiri kwa uhakika ni hali ya kisiasa huko Zanzibar. Hata hivyo, ninaweza kubashiri bila uhakika kuwa CCM itafanikiwa kulazimisha marudio ya uchaguzi, na kuna uwezekano CUF wakasusia. Uwezekano mwingine ni kurejewa kwa kilichofanyika baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, yaani kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa. Ubashiri sio sayansi timilifu (exact science) kwa hiyo nitahadharishe kuwa baadhi ya niliyobashiri yanaweza kuwa kinyume.

Ubashiri huu umetokana na kufuatilia kwa karibu siasa za kimataifa na za huko nyumbani.


Nimalizie makala hii kwa kuwatakia tena heri na baraka za mwaka mpya 2016. Kwa huko nyumbani (Tanzania), kuna kila sababu ya mwaka huu kuwa mzuri kutokana na dalili za awali za utawala wa Dk. Magufuli kuiondoa Tanzania yetu katika lindi la ufisadi na rushwa, vitu vilivyochangia mno kudumisha umasikini wa nchi yetu. Lakini ili afanikiwe, ni wajibu wa kila Mtanzania kutimiza ‘Hapa ni Kazi Tu’ kwa vitendo.



Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.