16 Oct 2015



 Makala hii ilipaswa kuchapishwa katika toleo la wiki hii la Raia Mwema, Jumatano Oktoba 14 lakini ikashindikana kwa sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu. Hata hivyo, ilichapihswa jana katika gazeti-dada la Raia Tanzania. Hebu angalia kwanza picha na nukuu ya 'mwanamabadiliko' Kingunge, kisha usome makala husika chini ya picha hiyo

BONYEZA MAKALA KUIKUZA IWE UKURASA MZIMA

10 Oct 2015

HATIMAYE tumebakiwa na takriban wiki mbili tu kabla ya Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika hapo Oktoba 25. Wakati kampeni hizo zikielekea ukingoni, matukio mawili makubwa yamejitokeza Jumapili iliyopita.
Tukio la kwanza ni kifo cha mwanasiasa nguli, Mwenyekiti wa chama cha siasa cha Democratic (DP), Mchungaji Christopher Mtikila. Tukio jingine lililotokea siku hiyo hiyo ni uamuzi wa mwanzilishi wa CCM na TANU, na mkongwe wa siasa za Tanzania, Kingunge Ngombale Mwiru. Nimeona ni vema kuyajadili matukio haya kwa sababu yote yanahusiana na Uchaguzi Mkuu, kwa namna moja au nyingine.
Tuanze na hilo la pili. Kwanza, tangazo la Kingunge kujiondoa uanachama wa CCM lilistahili liwe na mvuto mkubwa kama Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere alipotangaza kung’atuka. Lakini ukweli ‘mchungu’ ni kwamba tukio hilo limeonekana kama mwanachama wa kawaida tu wa CCM kuamua kujiondoa katika chama hicho.
Lakini, pili, uamuzi wa Kingunge kujiondoa CCM, haukuwa jambo la kushtua, kwa vile kwa muda mrefu sasa, kada huyo, rafiki wa karibu wa Baba wa Taifa, alikwishajitambulisha yupo upande gani katika siasa za uchaguzi. Kingunge, alipigana kwa hali na mali kuhakikisha mgombea ‘ chaguo lake,’ Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, anashinda katika mchujo wa chama hicho tawala kupata mgombea wake.
Niliwahi kuandika huko nyuma kuwa laiti busara ingemwongoza mzee huyo – hasa ikzingatiwa kuwa katika mila zetu za Kiafrika, wazee hutazamwa kama ‘visima’ vya busara na hekima – basi asingejiweka upande wa mgombea fulani au hata kama angefanya hivyo, licha ya kuwa ni haki yake ya kidemokrasia na kikatiba, basi labda angefanya kwa usiri.
 Nilitahadharisha hivyo kwa sababu, kwa kuegemea upande mmoja ilhali kuna pande nyingi katika jambo husika kuna matokeo ya aina mbili, kuwa sahihi au kukosea. Sasa, kama matokeo ya kuwa sahihi ni kudumisha hadhi na kukosea ni kupoteza hadhi, kila mwenye busara anatarajiwa kuwa makini katika jambo hilo.
Kitendo cha Kingunge kumuunga mkono Lowassa katika mchakato wa CCM kumpata mgombea wake, na hatimaye jina la kada huyo kukatwa katika mchujo, ilikuwa na athari kwa hadhi ya Kingunge kama mkongwe wa siasa. Bila kujali kuwa Lowassa alionewa au alistahili kukatwa, ukweli tu kwamba hakupitishwa ni sawa na kufeli kwa waliokuwa wakimuunga mkono, ikiwa ni pamoja na Kingunge.
Niliposoma tamko lake la kujiengua CCM nilibakiwa na maswali kadhaa, kubwa likiwa “...hivi huyu ndiye Kingunge yule yule wa zama za Nyerere au huyu ni toleo jipya? Na pengine bila hata kwenda mbali sana na kurejea zama za Nyerere, Kingunge huyu huyu alikuwa mstari wa mbele katika kampeni zilizomwingiza madarakani Rais Jakaya Kikwete, mwaka 2005. Yeye ni sehemu muhimu ya takriban kila analolaumu kuhusu CCM.
Matarajio ya wengi kwa Kingunge yalikuwa angekuwa mrithi wa Baba wa Taifa, si kwa sababu ya umri wake tu bali uumini wake katika Itikadi ya Ujamaa. Kingunge alikaa kimya wakati nguzo kuu ya itikadi hiyo, Azimio la Arusha ikizikwa katika kile kinachofahamika kama Azimio la Zanzibar. Kada huyo licha ya kuwa kimya katika masuala mbalimbali yanayoifanya CCM kupoteza umaarufu, hususan suala la ufisadi, alijitokeza kuwa mtetezi mkubwa wa watu waliotuhumiwa katika orodha maarufu ya watu waliotuhumiwa na Chadema kuwa ndio ‘mapapa wa ufisadi,’ iliyojulikana kama ‘List of Shame.’
Kimsingi, Kingunge aliwananga Chadema na kuwaita waongo, wazushi na wanafiki, wanaosema uongo na hakuna ushahidi, hakuna kiongozi fisadi. Leo hii, mwanasiasa anayeamini kuwa ndio chaguo sahihi kuingoza Tanzania, yaani Lowassa, kajiunga na waongo, wazushi, na wanafiki hao.
Kingunge ni mwathirika wa makosa yake mwenyewe kimkakati. Alipaswa tangu awali, achague kuwa mtetezi wa wananchi kama Baba wa Taifa, au mtetezi wa tabaka tawala. Japo ninatambua madhara ya kuwa mtetezi wa wananchi, kwa maana ya kutengeneza maadui wengi kisiasa, lakini ukweli usiopingika ni kwamba heshima na hadhi ya mtu wa aina hiyo hudumu milele. Tunawakumbuka akina Nyerere na Sokoine si kwa vile tu walikuwa viongozi wetu bali kwa sababu walisimama upande wa wananchi tulio wengi kuliko kulinda tabaka la watawala walio wachache.
Katika hitimisho langu baada ya kupokea taarifa za Kingunge kujiuzulu uanachama wa CCM, niliandika katika mtandao wa kijamii wa Twitter kuwa Kingunge aliwahi kuwa kama Muhmmad Ali wa siasa za Tanzania. Lakini tangazo lake la kujiuzulu CCM leo ni kama Ali angetangaza sasa kuwa anajiuzulu masumbwi. Alikwikushajiuzulu miaka kadhaa iliyopita. Nilichomaanisha ni kuwa, umuhimu wa mkongwe huyo wa siasa za nchi yetu ulisha- expire (kwisha muda wa matumizi) kitambo, na kubaki au kuondoka kwake CCM hakukuwa na faida kwa yeyote zaidi yake mwenyewe. Ninamsikitikia kwa sababu alipaswa kukumbukwa kwa mazuri mengi ya zama za Nyerere lakini dalili ni kwamba ataishi kukumbukwa zaidi kwa jithada za kumbeba Lowassa kwa gharama ya hadhi yake.
Tukiweka hilo kando, taarifa za kifo cha Mchungaji Mtikila kimeonekana kuwashtua Watanzania wengi. Binafsi, nilipopata taarifa hizo, kwanza nilidhani ni utani tu, lakini nilipogundua kuwa zina ukweli, hisia zangu zikaanza kupatwa na wasiwasi fulani.
Wakati tayari kuna taarifa zisizo rasmi mbalimbali zinazosambaa kwa kasi mtandaoni kuhusu chanzo halisi cha kifo cha Mchungaji Mtikila, licha ya taarifa za polisi kuwa chanzo cha ajali iliyosababisha kifo chake ni mwendo kasi wa gari alilokuwa akitumia huku akiwa hajavaa mkanda wa kiti cha gari, ukweli kwamba mwanasiasa huyo machachari alikuwa na ‘mabomu’ kuhusu mmoja wa wagombea urais, ilitosha kuniongezea wasiwasi huo.
Ni muhimu, katika hatua hii kukumbushia kuwa miongoni mwa sababu za umaarufu wa Mtikila ni kile ambacho wengi walikitafsiri kama ‘conspiracy theories,’ yaani hoja zinazoonyesha kubeba ukweli, zikiambatana na aina fulani ya ushahidi, lakini zinabaki vigumu kuzithibitisha.
Kwa mujibu wa taarifa zinazosambaa mtandaoni, Mtikila alikuwa akijipanga kuzuia ugombea wa mmoja wa wagombea urais, kwa hoja mbalimbali, ikiwa ni pamoja na madai yake kuwa mgombea huyo ni sehemu ya mkakati wa kimataifa kuihujumu nchi yetu. Kadhalika, Mchungaji huyo alinukuliwa akiongea kwenye kituo kimoja cha televisheni huko nyumbani (Tanzania) akisisitiza kwa nini anaamini mgombea huyo ni janga kwa taifa.
Sasa, japo kifo ni mapenzi ya Mola, lakini katika mazingira ya kawaida tu, kama anajitokeza mtu kumpinga mwanasiasa hadharani huku akipania kumwekea vikwazo katika safari yake ya Ikulu, kisha mtu huyo akafariki kwa ajali siku chache kabla ya uchaguzi, hisia za kibinadamu zinaweza kuhisi kuna namna hapo.
Kwa bahati mbaya, au pengine makusudi, jeshi la polisi limeonekana kuwa na haraka mno kutangaza chanzo cha ajali iliyosababisha kifo cha mwanasiasa huyo. Iwapo uchunguzi wa vyanzo vya ajali katika nchi zilizoendelea huchukua siku kadhaa licha ya taasisi zao za uchunguzi kuwa na nyezo za hali ya juu, iweje jeshi letu la polisi linalosifika kwa uchunguzi wa mwendo wa konokono lipate uwezo wa ghafla wa hali ya juu kuweza kutambua chanzo cha ajali hiyo siku moja tu baadaye?
Kwa mtizamo wangu, na ili kuwaridhisha Watanzania kuwa kifo cha mwanasiasa huyo hakina mkono wa mtu, polisi walipaswa kufanya uchunguzi wa kina, ikiwa ni pamoja na kupata taarifa ya uchunguzi wa kitabibu kuhusu chanzo cha ajali kabla ya kukurupuka na sababu ambazo ni rahisi kuhisi kuwa ni za kufikirika.
Kwa bahati mbaya, kifo cha Mtikila kilitokea siku moja na tukio la Kingunge kujivua uanachama wa CCM, suala lililosababisha baadhi ya watu kuyahusisha matukio hayo mawili. Pengine ni ‘coincidence’ tu lakini ni nadra kwa Tanzania yetu kukumbwa na matukio makubwa ya kisiasa ndani ya siku moja.
Nimalizie makala hii kwa kuwasihi Watanzania wenzangu kufanya sala na dua kuombea Uchaguzi Mkuu ufanyike na kuhitimishwa kwa amani na usalama.
Kauli zinazoashiria kuchochea machafuko sio tu ziepukwe bali pia zikemewe vikali. 
Tukumbuke kuwa, wakati uchaguzi utafanyika na kupita, Tanzania yetu ni lazima ibaki kuwa nchi moja na yenye usalama kwa kila raia wake. Waingereza wanasema; there is life after election (maisha yetu yataendelea baada ya uchaguzi), kwa hiyo ni muhimu kutotumia fito za kujengea nchi yetu kuchapana wenyewe.
Mungu ibariki Tanzania

5 Oct 2015



TAHADHARI YA PICHA YA MAITI: Mwili wa marehemu baada ya 'ajali.' Je nani aliyepiga picha hii na kuisambaza? Je lengo lilikuwa 'ushahidi kuwa amekufa kweli?'

Kumepatikana waraka ambao unadaiwa kuwa ndio uliopelekea kifo cha Mchungaji Mtikila. Awali, nilibandika maswali kadhaa kuhusu utata unaozunguka kifo hicho kiasi cha kuhisi huenda si 'Mapenzi ya Mungu' bali ni 'mkono wa mtu.' Katika waraka huo hapa chini, ukurasa wa 2,4 na 6 hazipo (sijui kwa nini)










UPDATE: Nimekutana na clip yenye sehemu ya mahojiano na Mchungaji Mtikila, akibainisha kuhusu tuhuma hizo zilizo kwenye waraka huo hapo juu 






Kwanza ni salamu zangu za rambirambi kwa Mchungaji Christopher Mtikila kama nilivyozi-post katika 'disposable website' (tovuti inayokuwa mtandaoni kwa muda tu) hapa 



Baada ya salamu hizi za rambirambi, tuelekee kwenye mada husika. Kwanza, ninaomba kukiri kwamba mara baada ya kusikia taarifa za ajali iliyopelekea kifo cha Mchungaji Mtikila, hisia yangu ya sita ilihoji 'mbona kama kuna mkono wa mtu?' Ninadhani mnakumbuka niliwahi kuzungumzia huko nyuma kuhusu 'hisia ya sita' (katika ule mfululizo wa makal za ushushushu). Siwezi kwa hakika kueleza kwanini nilipatwa na hisia hiyo lakini ilitokea tu, na imenikaa kichwani tangu muda huo.

Baadaye nikakutana na mabandiko yafuatayo huyo Jamii Forums 



 Maswali tata kifo cha Mchungaji Mtikila1. Gari yake haijaharibika kabisa na tunaaambiwa iliacha njia na kupinduka tunajua sababu kubwa ya magari kuacha njia ni kupasuka kwa matairi lakini hili gari la Mchungaji Mtikila hakuna tairi liliposuka. Sasa tuambiwe sababu ya kuacha njia na kupinduka ni nini? 

2. Mchungaji Mtikila hana alipoumia au kubleed damu.(Labda iwe kafa kwa mshtuko wa moyo au internal wounds. Kwenye picha anaoekana hajaumia hata kidogo hata nguo alivozavaa zikiwa hazijachanika hata kidogo.Sasa tuambiwe sababu gani nyingine iliyopelekea kifo chake? 

3.Tunaambiwa ajali alipata SAA 11 alfajiri Chalinze kwaa asili ya eneo la Chalinze ni eneo bize sana kwanini picha iliyosambaa inaonesha ni asubuhi kabisa kumekucha ina maana ajali yake haikushtukiwa na watumiaji wengine wa Barabara mpaka asubuhi. 

Angalizo sijamlaumu mtu yeyote kwenye hii ajali ila ni maswali ambayo nilikuwa najiulza binafsi sasa nawaomba msichafue hali ya hewa.

Na nyingine inayorandana na hiyo 



Mazingira ya kifo cha Mchungaji Mtikila bado kinatia shaka kuu mbele ya jamii na nachelea kusema huyu Mzee ameuawa na genge la mafisadi ili wafanikiwe kisiasa kwani Mtikila alikuwa ameshakusanya vielelezo vyote vya kuwashughulikia.
1. Jeshi la Polisi Watanzania tunaomba mtusaidie kumuhoji kwa kina huyu mtu anaeitwa Mchungaji Patrick Mgaya. Huyu alikuwa ni mmoja wa waliopata ajali pamoja na marehemu Mtikila. Ikumbukwe kuwa Magaya ni mmoja wa mashabiki muhimu sana wa Mgombea Urais kupitia Ukawa ndg Edward Lowassa.Taarifa za siri zinasema kuwa Mchungaji Mgaya na Mchungaji Mtikila walikutana takribani mwezi mmoja uliopita tu na kwamba kuna wasiwasi kuwa alipewa kazi maaluum ya kuhahakisha amamuua Mtikila.


Taarifa kutoka nyumbani kwa marehemu zinasema kuwa Mchungaji Mtikila akiwa na Mchungaji Patrick Mgaya walianza safari siku ya Ijumaa jioni kwenda mkoani Njombe ambapo waliambatana na madereva wawili ambao Mchungaji Mtikila hakuwafahamu. Aliewafahamu watu hawa wote ni Mchungaji Magaya ambae ndie aliekodisha gari waliokwenda nayo Njombe kupitia kwa Ndg Victor James Manyii ambaye mbali ya kutoa gari aliyokodisha pia alitoa madereva wawili ambao pamoja na Mchungaji Mgaya wao hawakufa isipokuwa Mchungaji Mtikila pekee.


Ajali hii imeacha maswali mengi kuliko majibu. Kwa mfano ukiangalia shingo ya marehemu Mtikila utaona kuna kitu kama kamba ambayo inaweza kuleta tafsiri kuwa ilitumika kumnyonga marehemu. Pili, kwanini mwili wa marehemu hauna hata kovu wala mchirizi wowote wa damu? Je, ni nani alimpiga picha Marehemu Mtikila? Je, Patrick Mgaya ni nani? Kabla kuwa mchungaji alikuwa anafanyakazi gani? Je gari lile lilipinduka lenyewe au liligongwa? Na kama lilipinduka ni kwanini liharibike eneo la mbele pekee?Je Ni chombo gani kilikuwa cha kwanza kumpiga picha na kusambaza kwenye mitandao?
Patrick Mgaya alipopiga simu nyumbani kwa marehemu alisema wamepata ajali na kwamba kulikuwa na majeruhi wengi sana akamaliza kwa kusema mtuombee kisha akakata simu, je, hao majeruhi wengi ni akina nani? Vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama muhojini Mchungaji Patrick Mgaya maana zipo dalili kuwa kuna mengi anayoyafahamu kuhusu tukio hili. Pia fuatilieni uhusiano uliopo kati ya Rais Paul Kagame, Patrick Mgaya na EADWARD LOWASSA. Pia nashauri Jeshi la Polisi kumuhoji mtu anaeitwa Dr. Jean Bosco Ngendahimana ambae anaishi nyumbani kwa marehemu pale Mikocheni.
Wale wote wenye misimo thabiti juu ya kuchukia Rushwa na Ufisadi wachukue tahadhari. Nasema hivyo sababu Humphrey Polepole alivamiwa nyumbani kwake Mbezi na Dkt. SLAA anapokea sms za vitisho. Vyombo vya dola viwe macho.


Binafsi ninafanya jitihada za angalau kujiridhisha iwapo ajali hiyo na kifo ni 'kazi ya Mungu' au kuna mkono wa binadamu. Ila ninachofahamu ni kwamba hadi mauti yanamkuta, Mchungaji Mtikila alikuwa na 'mabomu' aliyotaraji 'kuyalipua' ndani ya siku hizi chache zilizosalia kabla ya uchaguzi.

Ukipata taarifa zozote kuhusu suala hili ninaomba uwasiliane nami kwa Twitter @chahali au Facebook facebook.com/evarist.chahali.1


23 Sept 2015

BAADA ya harakati na pilika lukuki za vyama vyetu na wanasiasa kusaka fursa ya kumrithi Rais wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete, hatimaye tumefikia takriban mwezi mmoja tu kabla ya ‘siku ya hukumu’ kutimia.
Kufikia Septemba 23, tumebakiwa na mwezi mmoja na siku mbili kabla Watanzania hawajapiga kura kumchagua rais mpya, sambamba na kuwachagua wabunge na madiwani katika uchaguzi utakaofanyika Oktoba 25, 2015.
Pengine ni mapema mno kufanya tathmini inayoweza kutoa mwelekeo wa chama kipi kitaibuka kidedea au mgombea gani wa urais atashinda, lakini angalau sote twatambua kuwa kwa upande wa urais, mshindi atakuwa aidha Dk. John Magufuli, mgombea kwa tiketi ya chama tawala CCM au Edward Lowassa, mgombea wa Ukawa kupitia Chadema.
Pamoja na changamoto nyingine zitakazomkabili mshindi katika uchaguzi huo, moja kubwa ni kuwaunganisha Watanzania kuwa kitu kimoja baada ya uchaguzi. Sio siri kwamba Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu umetugawa mno. Na sio kati ya wafuasi wa vyama pinzani tu bali hata walio ndani ya vyama husika na sie wengine tunaojitambulisha kama tusio na vyama.
Kwa upande wa CCM, mchakato wa kumpata mgombea wake umeacha makovu kama ilivyokuwa katika chaguzi zilizotangulia maara baada ya chama hicho kuruhusu ushindani katika kumpata mgombea wake. Wakati CCM ilipompitisha Rais Benjamin Mkapa mwaka 1995 kulikuwa na manung’uniko kwamba kada huyo ‘alibebwa’ na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, na ‘kuwawekea ngumu’ makada wengine Kikwete na Edward Lowassa waliokuwa wakiwania fursa hiyo pia.
Mchakato wa CCM kumpata mgombea wake katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 uliacha majeraha makubwa zaidi, hasa kwa vile Mwalimu hakuwepo kusimamia mchakato huo, na kwa upande mwingine, Rais aliyekuwa madarakani, Mkapa, ni kama alizidiwa nguvu na kundi la mtandao wa Kikwete. Uchaguzi huo uliacha mpasuko mkubwa zaidi ambao umeigubika CCM hadi muda huu.
Lakini kilichojiri katika uchaguzi wa mwaka huu ni kikubwa zaidi kiasi kwamba kwa mara ya kwanza kabisa, chama hicho tawala kinakabiliwa na upinzani mkali ambao kimsingi ni matokeo ya mpasuko uliokigubika chama hicho tangu mwaka 2005. Kwa mara ya kwanza, CCM sio tu kinakabiliwa na upinzani uliotokana na ushirikiano wa vyama mbalimbali lakini pia mpinzani wake katika nafasi ya urais ni kada wake wa zamani, Lowassa, ambaye hadi anaondoka CCM alikuwa na nguvu kubwa kabisa katika chama hicho.
Kwa upande wa vyama vikuu vya upinzani, hali kwao pia ni tofauti kwa kiasi kikubwa. Kwa mara ya kwanza vyama vikuu vitatu, Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi, vikishirikiana na NLD, vimeweza kuruka kihunzi kilichowakwaza katika kila uchaguzi, yaani kuafikiana kusimamisha mgombea mmoja. Awali, wazo zima la umoja wa vyama hivyo unaojulikana kama Ukawa, kumsimamisha mgombea mmoja lilionekana kama ndoto ya alinacha, hasa kwa kuzingatia historia. Kwamba kila jitihada iliyofanyika huko nyuma kujenga ushirikiano miongoni mwa vyama vya upinzani haukuweza kufanikia.
Lakini kadri siku zilivyokwenda, taratibu wazo la ushirikiano wa vyama hivyo likaanza kujenga picha kamili kuwa safari hii wamedhamiria kuwa kitu kimoja. Hata hivyo, kosa la msingi na ambalo pengine litawagharimu katikia uchaguzi wa mwaka huu ni kutotumia vema fursa kubwa waliokuwa nayo kukamilisha mchakato wa kumpata mgombea wao na kumnadi kabla CCM hawajafanya hivyo. Ninachomanisha hapa ni kwamba, kwa vile vyama vya upinzani vinauelewa vema mchakato wa CCM kupata mgombea wake- ni kama vita ya wenyewe kwa wenyewe ambayo waweza kudhani itakipasua chama hicho kikongwe- wangetumia fursa hiyo wao kujimmarisha na mgombea wao kiasi kwamba CCM baada ya kumpata mgombea wao wangekutana na mgombea wa Ukawa ambaye sio tu amejiandaa vya kutosha lakini pia anatambulika kwa wapigakura.
Hatimaye, kitendawili cha kwa nini Ukawa walikuwa wakisuasua kumtangaza mgombea wao kiliteguliwa baada ya Lowassa kukatwa CCM na hatimaye kujiunga na Chadema na baadaye kupitishwa kuwa mgombea urais. Kumbe muda wote tulipokuwa tunahoji kwanini Ukawa hawatangazi mgombea wao, wenzetu walikuwa wanamsubiri kitakachodondoka kutoka CCM.
Licha ya ujio wa Lowassa huko Ukawa kuonekana umeleta msisimko na matumaini makubwa kwamba angalau upinzani mwaka huu una mgombea ‘anayeweza kuisumbua CCM,’ kisichoongelewa sana ni mpasuko wa kawaida tu kati ya wanaodhani ni sahihi kumtumia Lowassa katika azma ya kuing’oa CCM madarakani na wale wanaoona kuwa suala hilo sio tu ni usaliti lakini pia linaonyesha mapungufu ya vyama hivyo vya upinzani, kwa maana ya kwamba ilivibidi visubiri mtu kutoka CCM ili kufanikisha azma yao ya kuingiza Ikulu.
Tukiweka kando mazingira ambayo CCM na Ukawa wamepitia hadi tulipo sasa, kuna mambo kadhaa yanaanza kujitokeza ambayo yanaweza kutoa taswira ya matokeo ya uchaguzi huo japo ni muhimu kutambua kuwa, kwanza, si rahisi kubashiri kwa usahihi kabisa matokeo ya uchaguzi wenye ushindani kama wa mwaka huu, na pili, kama wiki moja katika siasa ni sawa na takriban mwaka (kwa maana ya lolote laweza kutokea) muda uliosalia kabla ya uchaguzi ni kipindi kirefu kinachoweza kuathiri ubashiri wowote utakaofanyika muda huu.
Miongoni mwa mambo ya msingi yaliyojitokeza katika kampeni zinazoendelea ni pamoja na lile ambalo wana-Ukawa hawataki kabisa kulisikia, nalo ni mapungufu ya mgombea wao, yaani Lowassa. Sote twaifahamu CCM, na japo mgombea wake, Magufuli ni mgombea kama Lowassa, lakini kimsingi kwa huko Ukawa Lowassa si mgombea tu lakini yeye ndio kama Ukawa yenyewe. Kwa lugha nyingine, uchaguzi huu unakuwa kama vita kati ya CCM na Lowassa, hasa kwa sababu mgombea wa CCM anajinadi kichama zaidi ilhali Lowassa anajinadi na kunadiwa kama Lowassa zaidi.
Moja ya madhara ya wazi ya suala hilo ni uwezekano wa Ukawa kupoteza viti vingi vya ubunge kwa gharama ya kumnadi zaidi Lowassa. Niliwahi kuandika kwenye mtandao wa kijamii wa twitter kuwa nina wasiwasi kuwa mmoja au hata wawili wa viongozi wakuu wa vyama vinavyounda Ukawa kwa upande wa Bara, yaani Freeman Mbowe wa Chadema, James Mbatia wa NCCR-Mageuzi na Emmanuel Makaidi wa NLD, anaweza kushindwa katika uchaguzi huo. Pamoja nao ni viongozi wengine wakuu wa vyama hivyo ambao pia ni wabunge, hususan kwa upande wa Chadema.
Iwapo hilo litamtokea, na iwapo Ukawa watashindwa, basi hatma ya vyama hivyo itakuwa mbaya. Kwa Chadema, yayumkinika kuhisi kuwa salama yake pekee ni kufanikiwa kwa jaribio (experiment) la kumtumia Lowassa kuiong’a CCM. Ikishindwa, kuna uwezekano mkubwa chama hicho kikaingia katika mgogoro wa ‘kumsaka mchawi’ ambao waweza kutishia uhai wa chama hicho kilichokubali kutelekeza ajenda yake ya kupambana na ufisadi ili kumtengenezea mazingira mazuri Lowassa.
Kwa NCCR-Mageuzi, ili Mbatia aendelee kubaki kiongozi wa chama hicho itambidi lazima ashinde ubunge anaowania huku akitegemea Lowassa kushinda urais. Kinyume cha hapo yeye na chama chake watakuwa matatani, na hatma ya uhai wa chama hicho kuwa tete. Angalau kwa NLD, Makaidi anaweza kuendelea kuwa kiongozi wa chama hicho hasa ikizingatiwa kuwa kwa muda mrefu ‘chama hicho kimekuwa ni yeye na yeye ndio chama hicho,’ angalau kwa mwonekano.
Lakini kubwa zaidi ni upungufu wa Lowassa kisera na kujinadi. Ajenda ya mabadiliko imekuwa shaghala baghala kiasi kwamba watu wanaimba na kuhubiri mabadiliko pasipo hata kubainisha yatakuwaje. Ukiuliza unaambiwa la muhimu ni kuiondoa CCM kwanza, mengine baadaye. Baadaye lini? Hakuna mwenye jibu.
Kwa upande mwingine, Lowassa ameshindwa kabisa kujinadi. Haiingii akilini kuona umati mkubwa unaojitokeza kwenye mikutano yake ya kampeni ukiishia kuambulia hotuba ya dakika chache tu. Sawa, tumeshasikia hotuba nyingi za wanasiasa na nyingi zimebaki kuwa hotuba tu pasi kubadilisha chochote, lakini huu ni wakati wa uchaguzi, na hotuba ya mgombea ni fursa nzuri ya kubainisha nini atawafanyia wapiga kura na wananchi kwa ujumla pindi wakimchagua. Laiti Lowassa angetumia vema ‘mafuriko’ ya wanaojitokeza kumsikiliza, basi hata hiyo utata kuhusu ajenda ya mabadiliko isingekuwepo kwani angeweza kuwaeleza Watanzania kwa undani kuhusu suala hilo.
Kwa upande wa CCM, licha ya mgombea wake kusimama kama mgombea anayewakilisha chama na si ‘mtu binafsi,’ mtihani mkubwa umekuwa ni jinsi ya kumshambulia Lowassa pasipo kumjengea huruma kwa wapigakura. Lakini mtihani mwingine umekuwa ni kipi hasa cha kukizungumzia kuhusu Lowassa na Ukawa ambao kwa kiasi kikubwa wananadi ajenda ya mabadiliko pasi kuielezea kwa undani. Kwa kutambua hilo, Magufuli amekuwa akijinadi kwa kutumia rekodi yake mwenyewe na zile za chama chake badala ya kuelekeza mashambulizi kwa mpinzani wake. Ni wazi, ili umshambulie mpinzani wako basi angalau awe na cha maana cha kukishambulia, vinginevyo yaweza kutafsiriwa kama uonevu.
Nimalizie makala hii kwa ahadi ya kuendelea na uchambuzi zaidi kuhusu Uchaguzi Mkuu, kwa matarajio ya kuwa na nafasi nzuri ya kufanya ubashiri wa matokeo angalau siku chache kabla ya uchaguzi huo, sambamba na kukumbushana wajibu wetu kijamii kuutumia uchaguzi huo kama fursa ya kuboresha mustakabali wa Tanzania yetu.

10 Sept 2015

ANGALIZO: Makala hii iliandikwa kwa ajili ya kuchapishwa katika toleo la wiki iliyopita lakini haikuchapishwa kutokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu. 

HATIMAYE ‘wapinzani wakuu’ katika Uchaguzi Mkuu ujao, yaani chama tawala CCM na Ukawa wamefanikiwa kuzindua rasmi kampeni zao na kuwaeleza wapigakura nini watarajie kutoka kwa vyama hivyo.
Kabla ya kuingia kwa undani kuchambua uzinduzi wa kampeni za vyama hivyo pamoja na ilani zao, ningependa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kwamba historia inaandikwa katika Uchaguzi Mkuu huu. Mie ni mpenzi wa teknolojia, na kubahatika kwangu kuwa huku kwa wenzetu ambao teknolojia sasa ni sehemu ya maisha yao ya kila siku, sio tu kumeniongezea mapenzi hayo bali kutamani isambae katika sehemu mbalimbali duniani.
Kwa mara ya kwanza kabisa, teknolojia imekuwa na mchango muhimu katika historia ya chaguzi nchini Tanzania. Pengine hili halionekani sana kwa wenzetu mlio huko nyumbani, lakini kwa sie tulio mbali, teknolojia imekuwa ikituwezesha kufuatilia mengi ya yanayojiri katika pilika za uchaguzi kana kwamba yanatokea huku tulipo muda huu.

Na eneo la teknolojia ambalo linahusika zaidi na habari za harakati za uchaguzi huko nyumbani ni kile kinachofahamika kitaalam kama Web 2.0, yaani maendeleo ya teknolojia ya mtandaoni yanayohusisha vitu vinavyowekwa mtandaoni na watumiaji wa kawaida. Tumeingia katika zama ambapo badala ya kusubiri taarifa ya habari ya Redio Tanzania enzi zile, sasa mtu aliyepo Ifakara, kwa mfano, anaweza kutuma habari mtandaoni na ikapatikana dunia nzima.
Teknolojia inawezesha habari mbalimbali za uchaguzi kupatikana katika namna inayofahamika kama ‘in real time’ yani kitu kinatokea na kuripotiwa muda huo huo na kuwafikia wasomaji/watazamaji/wasikilizaji muda huo huo.
Licha ya Katiba yetu kutunyima fursa Watanzania tulio nje ya nchi, teknolojia imetuwezesha kushiriki katika siasa zinazohusiana na uchaguzi huu kwani baadhi yetu tunaweza kumudu kuandika habari zinazohusu kana kwamba tupo huko, ingawa ukweli ni kutokana na kufuatilia kinachoendelea huko kupitia mtandaoni. Ni katika mazingira hayo, wakati huu nimekuwa nikiandika kitabu kuhusu uchaguzi huo (kinatarajia kuchapishwa mwezi huu) kwa kutegemea taarifa na habari zilizopatikana kupitia teknolojia ya mtandao kwa takriban asilimia 100.
Tukiachana na tukio hilo la kihistoria, uzinduzi wa kampeni za CCM na Ukawa umeweza kupigia mstari hisia zilizokuwepo awali kwamba Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu una upinzani ambao kwa hakika haijawahi kutokea katika historia ya taifa letu. Cha kusikitishwa, hata hivyo, ni kwamba badala ya ushindani huo kuelemea kwenye sera, suala lililogusa wengi, angalau huko mtandaoni, ni idadi ya wahudhuriaji.
Badala ya wafuasi kushindana kuhusu ubora au mapungufu ya sera, suala liloonekana muhimu zaidi ni ‘uzinduzi wa nani uliohudhuriwa na watu wengi zaidi.’ Lakini hili si la kushangaza sana kwa tunaofuatilia mengi ya yanayoendelea huko nyumbani. Watanzania wengi wanaendeshwa na matukio. Na kibaya zaidi, ni wepesi wa kusahau. Kwa wana-CCM, wingi wa watu kwenye uzinduzi wa kampeni zao waonekane ni kila kitu bila kujali iwapo chama chao kimebadilika na kutambua kuwa kina deni kubwa kutoka kampeni na awamu zilizotangulia.
Kwa wana-Ukawa, hali sio tofauti. Wanaonekana kupuuzia ukweli kuwa hata katika chaguzi zilizopita, walikuwa wakipata umati mkubwa katika kampeni zao lakini haukuweza kuwasaidia kushinda nafasi ya urais.
Uzoefu watuonyesha kuwa uzinduzi wa kampeni huwa fursa nzuri kwa chama husika kuelezea japo kwa ufupi kuhusu mipango yake ya kuwatumikia wananchi iwapo kitapewa ridhaa ya kuwaongoza. Kwa kulinganisha uzinduzi wa kampeni za CCM na Ukawa, yayumkinika kuhitimisha kuwa Magufuli alimudu kuelezea japo kwa kifupi kuhusu ilani ya chama chake, na pengine kutoa mwanga kwa wapigakura watarajie nini kutoka kwake iwapo atashinda uchaguzi huo.
Lowassa, kwa upande mwingine, ameshindwa kufuta ‘tuhuma’ dhidi yake kwamba amekuwa akishindwa kutumia vema fursa ya umati mkubwa unaojitokeza kumsikiliza, na hotuba zake zimekuwa fupi mno.
Japo ‘watetezi wa Lowassa’ wanadai kuwa kinachohitajika si hotuba ndefu au maneno mengi bali vitendo, lakini utetezi huo hauondoi hisia kwamba mwanasiasa huyo ana upungufu katika kubainisha kwa maneno mpiango au mikakati yake. Ni muhimu kutambua kuwa asilimia kubwa ya wapiga kura sio wanachama au wafuasi wa vyama vya siasa, na moja ya vityu vinavyoweza kuwasaidia kufanya uamuzi kuhusu nani wampe kura yao ni yanayobainishwa katika hotuba za wagombea.
Lakini kingine ambacho ninaweza kukieleza kama kosa la kimkakati ni maelezo ya Ukawa kupitia Chadema kuwa ilani yao itawekwa kwenye tovuti yao. Ndio, nimebainisha hapo juu kuhusu mchango wa teknolojia katika uchaguzi mkuu huu. Hata hivyo, takwimu za hivi karibuni zaonyesha kuwa ni takribani Watanzania milioni nane tu wenye kuweza kupata huduma (access) ya Intaneti. Na tukichukulia makadirio ya idadi ya sasa ya Watanzania kuwa ni watu milioni 50 (ninasisitiza ni makadirio tu), basi takriban watu milioni 40 hawataiona ilani ya uchaguzi ya Ukawa/Chadema kwa vile hawana Intaneti.
Na hadi muda huu ninapoandika makala hii, kilichopo kwenye tovuti ya Chadema ni hotuba tu ya Lowassa aliyoitoa siku ya uzninduzi wa kampeni. Nimejaribu kuuliza iwapo hotuba hiyo ndio ilani ya Chadema/Ukawa lakini sijapewa jibu.
Kwa upande wa CCM, bado ninaona kuna tatizo la kuendeleza ahadi badala ya kukiri makosa katika maeneo ambayo, baadhi yetu twaamini yamechangia kuimarisha vyama vya upinzani kama vile Chadema. Chama hicho tawala kinapaswa kutambua kwamba hali ya nchi yetu sio nzuri, na binafsi ninaiona hiyo ndio sababu kuu ya sapoti kubwa anayopata Lowassa: imani ya wanaomuunga mkono kwamba “hata kama ana mapungufu yake, atatusaidia kuiondoa CCM madarakani.”
Hadi muda huu sijaona jitihada za maana kwa Magufuli na CCM kuwa honest kwa Watanzania kwa kuwaeleza bila ‘kuuma maneno’ kuwa “jamanai, hapa tulikosea na tunakiri makosa. Ili kurekebisha makosa hayo na kutoyarudia tena, tutafanya hili na lile.” Hatua ya kwanza ya kuondoa tatizo ni kulitambua na kulibainisha, kisha kuandaa mkakati wa kuliondoa. Kukiri kosa si upungufu bali dalili ya uelewa wa changamoto zinazomkabili mhusika.
Lakini Lowassa na Ukawa yake wasitegemee sana hisia kuwa ‘upungufu wa CCM, ni ubora wao.’ Laiti CCM wakifanikiwa kubainisha upungufu wao na kueleza jinsi watakavyoyakabili, Ukawa watalazimika kuwaeleza Watanzania nini wao watakifanya bila kujali CCM wanasema nini.
Wakati Magufuli na CCM wameendeleza mlolongo wa ahadi zilezile zilizozoeleka masikioni mwa wapigakura, kuna maeneo ambayo binafsi ninayaona ‘hatari’ kwa Lowassa na Ukawa. Kwa mfano, Lowassa ametoa ahadi ya kuwaachia huru watuhumiwa wa ugaidi huko Zanzibar, jambo ambalo limepelekea moja ya Jumuiya za Kikristo kumlaumu kwa vile miongoni mwa kesi zinazowakabili watuhumiwa hao ni ya mauaji ya padre huko Visiwani. Kutafuta pointi rahisi za kisiasa kwaweza kuwa na madhara makubwa kwa mwanasiasa.
Nimalizie makala hii kwa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuwa watumie fursa hii ya kampeni kuwapima kwa makini wagombea wote, si wa urais tu bali pia katika nafasi za ubunge na udiwani, na kuwachagua wale tu wanaowaamini watawatumikia kwa dhati. Pia nitumie fursa hii sio tu kukipongeza chama cha ACT Wazalendo kwa uzinduzi wa kampeni unaoweza kuhitimishwa kuwa bora zaidi ya wa CCM na ACT bali pia kuonyesha dalili kuwa chama hicho kinaweza kuwa ngome kuu ya upinzani huko mbeleni.
Nitaendelea na uchambuzi kuhusu uchaguzi mkuu katika makala zijazo.

28 Aug 2015

Hii ni simulizi ya kusikitisha kuhusu mwanaharakati wa mazingira kutoka Sweden, Susanna Nordlund, ambaye amekuwa akifanya harakati dhidi ya uporwaji wa ardhi na manyanyaso kwa wakazi wa Loliondo.

Kilichonigusa katika harakati za Susann ni ukweli kwamba ni raia wa kigeni anayepigani haki za Watanzania lakini amekuwa akifanyiwa hujuma na unyanyaswaji mkubwa.

Chini ni stori yake kama nilivyoitafsiri kwa idhini yake:

Ripoti fupi jinsi nilivyokamatwa Loliondo:

Niliwekwa rumande siku mbili katika kituo cha polisi cha Loliondo na pia nilikaa rumande usiku mmoja katika kituo cha polisi cha Arusha.

Sikuruhusiwa kuwasiliana na mtu yeyote, kompyuta yangu iliharibiwa, na badala ya kuelekwa kortini, nilifukuzwa Tanzania.


Wiki iliyopita safari yangu ya hivi karibuni huko Loliondo -sehemu ya dunia ambayo siku zote ipo akilini mwangu- ilikatishwa ghafla baada ya mtu fulani kuniripoti kwa mamlaka za eneo hilo. Nilipania kukutana na watu ambao hawapo online lakini wana taarifa kuhusu vitisho dhidi ya ardhi yao vinavyofanywa na 'wawekezaji.'


Niliwasili Wasso kwa basi tarehe 20 Juni mwaka huu, na sikuwa na mengi ya kufanya wakati ninatafuta gari la kuelekea vijijini. Nilipata ofa moja nzuri lakini dereva akadai kuwa haendi kwenye vijiji hivyo mchana. Hatimaye tarehe 23 nilipata gari kwenda Kirtalo kwa nusu siku. Nikiwa njiani, nilipata ujumbe kwamba mmoja wa madereva wa kampuni ya utalii ya Thomson Safaris alimpigia simu kijana mmoja kumweleza kuwa ameniona na rafaki yangu flani katika nyumba ya wageni ya Domel. Nilikutana na watu hapo Kirtalo, rafiki yangu alibaki hapo, na nilirudi Wasso na dereva. Njiani, tulikutana na gari lililokuwa na Diwani wa Oloipiri  'rafiki wa wawekezaji' William Alais. Mpango wangu ulikuwa kwenda Mondorosi na Sukenya siku inayofuata.

Nilirudi nyumba ya kulala wageni na kuingiza kwenye kompyuta niliyoelezwa na watu huko vijijini lakini baadaye nikaptiwa na usingizi. Nilipoamka, tayari ilikuwa usiku na nikaenda kupata chakula katika nyumba ya kulala wageni ya Honest, hasa baada ya kuona mengi hapo Domel. Gari moja liliwasili, na waliokuwa ndani ya gari hilo walishuka na kuniijia. Afisa Uhamiaji Angela aliniuliza ninafanya nini Tanzania na akataka kuona hati yangu ya kusafiria. Nilimweleza ratiba yangu ya safari na mipango yangu, bila kumtajia dhima yangu kufahamu kuhusu waporaji ardhi ya wafugaji.

Nilikuwa na nakala tu ya hati yangu ya kusafiria, na niliombwa kufuatana na maafisa Uhamiaji na askari polisi kwenda Oloip nilipokuwa nakaa. Nilijaribu kutuma meseji wka marafiki lakini nilinyang'anywa simu yangu. Niliambiwa kuwa Idara ya Uhamiaji ilikuwa ilikuwa ikinifahamu vema kutokana na taarifa za mtandaoni, jambo lililonipa ahueni nikidhani ningeweza kusimulia maoni yangu kuhusu kinachoendelea. Nilifahamishwa kuwa niko chini ya ulinzi na kutakiwa kupakia vitu vyangu. Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Hashimu Shaibu Mgandilwa, ambaye nilimtambua baada ya kumwona katika vyombo vya habari, alikuwepo pia, japo hakujitambulisha, na alikuwa akiongea na maofisa wa Uhamiaji. Wakati tunaondoka hapo kwenda kwenye gari la Idara ya Uhamiaji, kitambu cha kuandikisha wageni kilichukuliwa, na nikapelekwa kituo cha polisi cha Loliondo.

Baada ya kufika kituo cha polisi, niliambiwa kuwa sababu ya kukamatwa kwangu ni kuwa niliingia Tanzania kama mgeni haramu.

Mwaka 2010, nilitembelea Loliondo kama mtalii kuwauliza watu kama Thomson Safaris- kampuni ya Kiamerika ya kutembeza watalii ambayo inadai kumiliki ekari 12617 za ardhi ya Wamasai, na kudaiwa kuwanyanyasa watu- inaendana na ilichoandika kwenye tovuti yake. Nilipatwa na shauku kuhusu suala hili baada ya maongezi mtandaoni. Mengi kwenye tovuti ya kampuni hiyo si ya kweli, lakini pia nilifanya kosa la kumuuliza Afisa Mtendaji wa Kata ya Soitsambu , ambaye alimpigia simu aliyekuwa Mkuu wa Wilaya wakati huo, Elias Wawa Lali, ambaye alinijibu siku iliyofuata. 
Siku iliyofuata, nilifuatwa na polisi na kupelekwa katika Kamati ya Usalama. Nilituhumiwa vitu mbalimbali, kama vile kufanya utafiti bila kibali. Hati yangu ya kusafiria ilichukuliwa na ilinibidi kwenda Uhamiaji Arusha kuichukua, ambapo huko nako niliambiwa kuwa mie ni 'mgeni haramu' na kutakiwa kuondoka nchini humo.
Baada ya hapo ndio nilianzisha blogu yangu - Mtizamo kutoka kwenye kichuguu cha mchwa (A view from a Termite Mound) - kuhusu 'wawekezaji' huko Loliondo ambao ni tihshio kwa haki za ardhi - Thomson Safaris na wengine wanaofahamika zaidi OBC kutoka Falme za Kiarabu- ambao wamekuwa wakijitahidi kuishawishi serikali ya Tanzania kutangaza kilometa za mraba 1500 jirani na Mbuga ya Taifa ya Serengeti kuwa ni eneo lililohifadhiwa, na kuiondoa jamii ya Kimasai katika eneo hilo lenye umuhimu mkubwa kwa maisha yao. Mwaka 2009, suala hili lilipelekea wanavijiji kuondolewa kwa nguvu baada ya kurudi tena katika eneo hilo.
Nilirudi tena mwaka 2011 na 2013 bila matatizo yoyote lakini nimekuwa nikipata zaidi taarifa kuhusu adha zinazowakabili wakazi wa maeneo hayo kupitia watu wanaotumia mitandao ya kijamii (social media). Blogu yangu ni nyenzo muhimu kwa sababu sio tu serikali na 'wawekezaji' wanasambaza taarifa potofu bali pia taasisi na watu wanaopinga unyanyasaji huo wamekuwa wakichanganywa na taarifa potofu. Wenyeji wa Loliondo wanaopinga vitisho kuhusu ardhi yao wamekuwa wahanga wa unyanyasaji mkubwa, hususan kutuhumiwa kuwa ni Wakenya, lakini tishio kubwa zaidi ni kutoka kwa baadhi ya wakazi wanaonufaika na unyanyasaji huo kwa urafiki wao na 'wawekezaji.'
-------------------------------------------------------------------------
Kituo cha Polisi Loliondo

Baada ya kufikishwa kituo cha polisi Loliondo, nilitakiwa kuorodhesha vitu vyangu vyote. Lieleza bayana kuwa ninaamini kukamatwa kwangu kulitokana na 'siasa chafu' kuhusiana na suala la ardhi, na kwamba wanaopaswa kukamatwa ni hao wanaohatarisha maisha ya wanavijiji. Hata hivyo, niliambiwa nipo chini ya ulinzi, na sina haki yoyote. Afisa Uhamiaji Angela alinieleza kuwa nitapatiwa simu yangu siku inayofuata. Kisha nikaingizwa rumande nikiwa na kikoi changu ambacho nilikitumia pia kama blanketi. Nililala kwenye sakafu ya zege kwenye selo yenye kiza. Baadaye nilipewa chupa ya maji ya kunywa ambayo nilitumia kunawa uso, lakini sikunywa maji mengi kwa vile selo haikuwa na choo. Baadaye niliona ndoo inayotumika kama choo.

Loliondo ni sehemu yenye baridi nyakati za usiku, na madirisha ya selo hayakuwa na glasi bali nondo tu. Kulikuwa na mbu wengi na sikuwa na kinga ya kuzuwia mbu (mosquito repellent). Nilikuwa mfungwa wa kisiasa. Nilitetemeka kwa baridi, lakini maneno kutoka Kirtalo kuhusu blogu yangu yalinipa nguvu. Unyanyasaji dhidi  yangu ulikuwa kama kichekesho, na baadhi ya watu walionyesha dalili za kuniunga mkono.

Asubuhi, nilipewa kifungua kinywa na kuruhusiwa kwenye bafuni, na kupatiwa maji ya kunawa uso kabla ya kurudi selo. Kwenye kuta za selo, kulikuwa namnaandishi kadhaa yaliyoashiria baadhi ya mahabasu walikuwemo humo bila mlo kwa siku kadhaa. Baadaye, nilichukuliwa na Angela kwenda ofisi ya Uhamiaji kuchukuliwa maelezo yangu. Alikuwa mkarimu kwangu na kunipatia peremende. Nilitoa maelezo yangu, na kueleza nilichokuwa ninafanya Loliondo, lakini bila kutaja majina kwa kuhofia watanyanyaswa. Angela alinieleza kuwa nitapelekwa kwenye nyumba ya kulala wageni kuoga kabla ya kupelekwa Arusha. Hata hivyo, alionekana kutofahamu kabisa kuhusu suala la haki za ardhi.

Nilirudishwa kituo cha polisi na kusubiri kwa muda mrefu wakati maofisa Uhamiaji wanafanya kikao na Mkuu wa Wilaya. Nilipata mlo na kuendelea kusubiri. Baadaye nilirudishwa tena rumande.

Mkuu wa Wilaya wa zamani, Elias Wawa Wali, alifanya kazi yake kibadhirifu akiitumikia serikali na 'wawekezaji' dhidi ya wanavijiji lakini hakuonekana kuwa na dhamira ya kufanya mabo mbaya zaidi. Mtangulizi wake, DC Hashimu Shaibu Mgandilwa, alikuwa na mawazo ya ajabu kabisa, kwa mfano kuwaamuru viongozi wa chini yake kutembea umbali wa kilometa nane kutoka Wasso hadi Liliondo, na kuishia kutupwa rumande baada ya askari mmoja mla rushwa kupigwa na wanakijiji Mei 6 mwaka huu.

Ilikuwa usiku nilipoamshwa, ANgela alikuja akiwa na bosi wake na mtu mwingine, na tuliondoka sote kuelekea Arusha. Tulipofika Olduvai nilipatiwa vitu vya kufanya usafi mwilini na baadaye tulisimama katika hoteli ya kifahari ya Serena Lodge kupata kifungua kinywa. Sina hakika kama gharama zililipwa kwa fedha za walipakodi wa Tanzania au na hoteli hiyo. Niltamani kuona ana angalau mtalii anayeonekana kama Mswidi lakini haikuwezekana. Nilitaraji kuwa albda taarifa zangu zimeshafika Ubalozi wa Uswidi. 

Tulipofika Arusha, sikurejeshewa simu yangu. Angela, yule afisa Uhamiaji, alikagua vitu vyangu na kukuta orodha ya majina, na hilo halikumfurahisha. Ilikuwa ni orodha tu ya majina ya watu ambao nilipanga kufanya maongezi nao.

Baada ya hapo ilifuatia kusubiri kwa muda mrefu. Koo ilikuwa imenikauka na nilikuwa na uvimbe kufuatia kung'atwa na mbu. Nywele zangu, ambazo kwa kawaida huzisha kila usiku, zilikuwa ovyo ovyo. Nilijilaza kwenye benchi, na baadaye nikasikia mlango ukifunguliwa. Wanasheria waliotumwa na Onesmo Olengurumwa wa Kituo cha Haki za Binadamu waliwasili. Niliwaeleza kilichotokea na wakaniambiwa watashughulikia nipate dhamana ikiwezekana.  Nilishakuwa nimewekwa rumande kitambo sasa na haikuwa haki kuninyima mawasiliano na watu wengine. Nilitaraji kuwa baada ya kutoka rumande itafuatia kesi mahakamani.

Baada ya muda mrefu nilielezwa kuwa nitarudishwa kituo cha polisi. Muda wote huo nilipokuwa nasubiri, sikupewa taarifa yoyote kuhusu inachoendelea. Ufahamu wangu mdogo wa Kiswahili ulichangia pia kutoelwa kinachoendelea. Niliwekwa tena rumande. Humo rumande nilkutana na mahabusu wengine, Sidamu aliyedai ni mtaalam wa wizi kwenye ATM na Mary aliyeiba maji kwa ajili ya kumwagia kwenye shamba lake.

Masaa kadhaa baadaye nilichukuliwa kwenda ofisi ya Uhamiaji na kuchukuliwa alama za vidole. Mchana, nilifahamishwa kuwa mie ni 'mgeni haramu' na sintoruhusiwa tena kuingia Tanzania. Niliambiwa kwamba kitu pekee ninachoweza kufanya ni kuandika barua Wizara ya Mambo ya Ndani. Niliomba majina ya watu ninaoweza kuwasiliana nao kwa barua-pepe lakini sikupewa, na sikurudishiwa simu yangu. 

Nilisindikizwa hadi Namanga, nikiwa kati ya watu wawili katika gari. Mpakani Namanga kulifuatia kusubiri kwingi na kupigwa picha. Niliomba nakala ya hati ya kutangazwa 'mgeni haramu' lakini sikupewa. Nilisema kwamba ningerejea tena siku moja, na afisa mmoja wa Uhamiaji alimweleza mwenzie, "haogopi kitu."

Baada ya kuingizwa Kenya nilipatiwa simu yangu, na dereva mkarimu alinipeleka hotelini. Nilapata fursa kuangalia mitandao ya kijamii na kulikuwa na taarifa za kukamatwa kwangu. Pia nilipata wasaa kuwafahmisha ndugu na jamaa kuwa nimeachiwa huru. Familia yangu haikufahamishwa lolote nilipokamatwa, na maofa wa Ubalozi wa Uswidi hawakuruhusiwa kuwasiliana nami bila idhini yangu (ningewezaje kutoa idhini ilhali walizuwia mawasiliano yangu na mtu yeyote yule?)

Kompyuta yangu ambayo huwa nayo muda wote iligoma kuwaka. Kesho yake nilimpata mtaalam wa kompyuta hapo Namanga ambaye alibaini ilikuwa na matatizo.
Tarehe 30 nilifahamishwa kuwa mwandishi mmoja, Manyerere Jackton ameandika kwa kirefu kuhusu mimi katika gazeti la kila wiki la Jamhuri. Kesho yake niliweza kuiona habari husika........ na ilikuwa na uongo mwingi. Kama nilivyotarajia, mwandishi huyo alijaribu kunifarakanisha na Tina Timan ambaye sijawahi kukutana nae. Huyu ni anayelezwa kuwa ni mwanaharakati kutoka Kenya, japo amekuwa akiishi Tanzania kwa muda mrefu na ana watoto hapo. Mwandishi huyo amekuwa akichochoea vitu vingi dhidi ya wanavijiji wa Loliondo.

Manyerere- au mtoa habari wake- alidai kuwa nilisema kwamba ningehakikisha serikali ya Uswidi inakata misaada kwa Tanzania kama seriali haitoendelea kunisumbua. Licha ya kwamba sina uwezo huo, lakini kila anayenifahamu anajua nisingeweza kusema maneno kama hayo. Kitu pekee nilichosema kuhusu nchi yangu ni katika nchi yoyote yenye demokrasia, mtalii nanaweza kuongelea siasa na mtu mwingine, baada ya kuambiwa pale kituo cha polisi kuwa "hakuna sehemu yoyote duniani mtalii anaruhusiwa kuongelea siasa." Huu ni unafiki wa hali ya juu katika nchi ambayo ni mhanga wa ukoloni mamboleo. 

Katika habari hiyo, Kamishna wa Uhamiaji Abdullah Khamis Abdullah alimpongeza DC Mgandilwa kwa 'kudumisha amani wilayani kwake.' Sio tu uwepo wa Mkuu wa wilaya ni zao la ukoloni bali pia afisa huyo amekuwa akiwatenda wanavijiji kama ilivyokuwa zama za ukoloni.

Mwandishi huyo alinituhumu kuwa mie na 'washirika wangu' tumekusanya mabilioni ya shilingi kwa ajili ya wafugaji wanaonyanyaswa na kuzifadhili NGO za kuchochea vurugu katika vijiji husika. Sijawahi kuksanya fedha zozote wala kutoa chochote kwa NGO. Mie ni bloga tu.

Tishio baya zaidi ni kuwapeleleza wanavijiji wote wanaonisaidia, na kwa kukosa mwelekeo,miongoni mwa wahanga ni mmiliki wa nyumba ya kulala wageni niliyofikia kama mteja mwingine yeyote yule.Itanilazimu nimlipe fedha zake za huduma ya malazi, kupitia huduma ya kuta fedha ya Western Union, mara baada ya kurudi nyumbani, kwani nilichukuliwa kutoka sehemu hiyo ghafla.

Sijui kwanini sikufunguliwa kesi mahakamani. Ingekuwa fursa nzuri kuweka wazi kinachoendelea Loliondo, na kuuliza iwapo watalii hawaruhusiwa kuuliza mwaswali wawapo Tanzania, na iwapo watalii wanaooblogu wanahitaji viza maalumu kuingia katika nchi hiyo.

Sasa dhamira yangu ni kuendelea kuandika kuhusu Loliondo katika uhai wangu wote, na kwa hakika nitarudi tena.

NYONGEZA: Uchunguzi uliofanywa na mafundi wa kampuni ya Samsung umethibitisha kuwa Hard Drive ya kompyuta yangu ilichomolewa nilipokuwa Tanzania.

Pia,Manyerere alinitumia barua pepe kwamba amesoma blogu yangu na anaitetea nchi yake dhidi ya 'ukoloni mamboleo' wangu, akisema 'Tanzania ni kwa ajili ya Watanzania.' Jibu la wazi lilikuwa mshangao kwanini amekuwa akiandika makala mbalimbali za kichochezi dhidi ya wanavijiji wa Loliondo kwa maslahi ya wawekezaji kutoka nje. Badala ya kunijibu swali hilo, mwandishi huyo alijibu haraka kwa kunitumia picha za mtu aliyekuwa akitoa habari Loliondo, na kujigamba kuwa kila nyendo zangu 'haramu' nikiwa huko ilikuwa ikifuatiliwa japo hakubainisha uharamu wa nyendo zangu katika nchi ya kidemokrasia.

Habari hii imetafsiriwa kutoka blogu ya Susanna, kama ilivyoandikwa HAPA. Kadhalika, waweza kuwasiliana na mwanaharakati huyo wa haki za ardhi, kwa barua-pepe [email protected]

MTIZAMO WANGU: Nimemfahamu Susanna kutokana na kuguswa kwake na kujishughulisha kwake na haki za ardhi huko Loliondo. Nina imani wasomaji wengi mnafahamu kuhusu maslahi ya taifa letu yanavyowekwa rehani katika maeneo kadhaa yenye raslimali za taifa letu. Haiingii akilini, mwanaharakati kama Susanna aache shughuli zake huko Uswidi, aende Tanzania kuwachochea wanavijiji. 'Kosa' la dada huyo ni kuwa mtetezi wa wanyonge. Imekuwa kawaida sasa kwa kila anayejaribu kukemea maovu kuitwa adui wa taifa letu. Kwa hakika inaumiza sana kuona watu wanaojali maslahi ya taifa letu wananyanyaswa kiasi hiki na kutangazwa 'maadui wa taifa.' 








Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.