Kama nilivyoahidi jana, leo nawaletea mahojiano maalum (exclusive interview) na msanii mahiri wa Bongoflava,Hamis Mwinjuma,almaaruf Mwana F.A.Pamoja na mambo mengine,blogu hii ilionelea umuhimu wa kufanya mahojiano na msanii huyo kwa sababu kuu mbili.Kwanza,yayumkinika kum-describe MwanaFA kama mmoja wa wasanii wenye elimu ya hali ya juu baada ya kuhitimu masomo yake hapa Uingereza.Pili,ilitarajiwa kwamba kwa kuwa kwake nje ya nchi kwa muda mrefu kimasomo atakuwa katika nafasi nzuri ya kutupa mwanga kuhusu nafasi ya bongoflava ndani na nje ya Tanzania.Basi nisimalize ladha bali tiririka na mahojianio hayo hapa chini.
KULIKONI UGHAIBUNI (K.U.):Kwanza,blogu hii inatoa shukrani kwa kukubali ombi la kufanya mahojiano nawe.Pili ni pongezi kwa kuhitimu masomo yako ya Shahada ya Uzamili nchini Uingereza.
Umekuwa ukifahamika zaidi kwa jina la Mwanafalsafa,na wakati mwingine Binamu.Je nini asili au maana ya majina hayo?
MwanaF.A: Nashukuru ndugu yangu.
Mwanafalsafa nilipewa na producer wangu wa kwanza,Dj Boniluv..nilikuwa na wimbo unaitwa ‘mwanafalsafa’(upo kwenye album yangu ya kwanza) na Boni akadhani itakuwa busara nikilitumia jina hilo sababu ya aina ya uandishi wa mashairi nnaoufanya(kujaribu kuzungumzia vitu kwa uzito)..Binamu lilikuja baadae,na linaelezea mahusiano yangu na hadhira nnayoongea nayo,kwamba nawaambia watu vitu ambavyo kaka na dada zao wangeshindwa kuwaambia,pengine sababu ya heshima za kindugu walizonazo,lakini mimi kwa ukaribu na urafiki wa ki’binamu naweza kuwawasilishia.
K.U:Ukiwa mmoja wa wasanii wakongwe wa bongoflava,je ni kipi kinachokuwezesha kubaki kwenye form kwa muda mrefu kiasi hiki?
MwanaF.A:ah,kitu cha kwanza najua nimekuwa mwenye bahati,na namshukuru Mungu kwa hilo..sababu naamini kuna wengi walikuwa na vipawa vya kuweza kubaki lakini hawapo kwa sababu moja ama nyingine..huwa najaribu kusema vitu watu wanavyotaka kuvisikia,na pengine hawakuvitegemea,natafuta namna ya kuzunguka na ideas na kuzijengea hoja..then kilichobaki ni siasa za mziki.
K.U:Tuje kwenye maisha yako nje ya Tanzania.Kama msanii unaonaje nafasi ya bongoflava kwenye anga za kimataifa?:
MwanaF.A:sio kubwa kwa kweli,ina safari ndefu SANA..kuna mambo ambayo kimsingi tunatakiwa kuanza kwa kuyakubali kwanza,mathalani mipaka ya lugha..hili sio suala dogo,na nasema hivyo sababu ili kufanya vizuri nyumbani itakubidi kufanya kwa Kiswahili,ambapo nje ya nyumbani ni shida kukivusha..ubora wa mziki wetu na kukosa kwake uhalisi(kuna hiphop,r&b,afro pop,zouk,kwaito,lingala nk kwenye bongo flava) vinaiweka kwenye hali ngumu sana wakati wa kuutafutia nafasi.Pengine,tungeanza kwa kufanyia kazi vitu viwili hivi,lugha na uhalisi.
K.U: Je katika kipindi ulichokuwa nje ya Tanzania ulifanya kazi zozote za kisanii kushirikiana na wasanii wa nje au una mpango wa aina hiyo?:
MwanaF.A:sikuweza kwa kweli..nilikaribia kufanya kazi na producer Amit,lakini ratiba zangu na zake zikawa zinapishana mno so sikuweza tena..nna mpango wa kufanya kazi na wasanii wan je ndio lakini bado naifikiria Africa kwanza..so nawaza Nigeria na South Africa kwa kuanzia.
K.U: Umaarufu unaambatana na usumbufu.Je wakati uko masomoni Uingereza,ulimudu vipi kukabiliana na hali hiyo (i.e. muingiliano wa umaarufu wako katika masomo yako)?
MwanaF.A:nimekuwa nikisoma kwa muda sasa wakati najulikana julikana na watu(siuiti umaarufu)..see,nimekuwa nafanya mziki wa kusikika na kuonekana kwa takriban miaka 9 sasa na nimezoea kukabiliana na vikwazo nnapotaka langu liwe..nilisoma IFM kwa miaka kadhaa na bado niliweza kukabana na mazingira ya kujulikana na shule,so nje ilikuwa rahisi zaidi,sababu watu wachache zaidi wananijua kulingana na nyumbani.
K.U: Ni dhahiri kuwa kutokana na kiwango chako cha juu kitaaluma,utakabiliwa na majukumu mengine kama kikazi,nk.Je unataraji kubalansi vipi maisha yako kama msanii na majukumu mengine ya kimaisha (mfano kikazi)?:
MwanaF.A:kwa kuanzia nimempa AY majukumu ya kusimamia sehemu kubwa ya kazi zangu za mziki ili nipate nafasi ya kumudu kufanya mambo mengine kwa kuwa yeye ana kampuni inayojihusisha na masuala ya mziki(Unity Entertainment)..hii inanibakisha na kufanya mziki na shows tu ambapo ni maisha niliyoyazoea..bado naendelea kufikiri namna bora zaidi ya kutogonganisha majukumu..najaribu kutoweka mipaka kwenye idadi ya vitu nnavyoweza kuvifanya,napigana na haya maisha na najaribu kunyoosha mambo kwa kadri nnavyoweza.
K.U:Je unadhani hatua uliyopiga kitaaluma inaweza kuzaa matarajio mapya kwa washabiki wako hususan kwenye ujumbe uliomo kwenye tungo zako?
MwanaF.A:yeah,naishi najifunza..kila hatua ya maisha nnayopitia ni somo kwangu na nadhamiria kuwaambia watu wangu vingi nnavyojifunza..so hata hatua za kitaaluma nnazopiga zinaniongeza uelewa wa vitu na nimepanga kushiriki na hadhira yangu,sio kwa namna ya kishule,bali kwa namna ambayo mitaa itaelewana nayo.
K.U:Swali linaloshabihiana na hilo lililotangulia.Je kwa hatua uliyopiga kitaaluma,jamii itarajie mtazamo mpya kwenye tungo zako?
MwanaF.A:jibu lake ni exactly kama lililopita.
Nnachoweza kuking’arisha hapa ni kuwa sitaki kuchanganya sana shule yangu na huu mziki isipokuwa kwenye namna ya biashara na vitu vichache vitakavyohitaji mawili matatu nnayojifunza kila kukicha...huhitaji masters degree kutengeza mziki mzuri....huu ni wa mtaa na ntaendelea kuufanya kwa ajili ya mitaa,kama unanielewa vizuri..mara nyingi nyumbani unaweza kuhukumiwa kwa kujua.
K.U:Kama msanii msomi kabisa una ushauri gani kwa wasanii wengine kuhusu suala la kujiendeleza kielimu?
MwanaF.A:namna pekee ya kuliangalia hili kwa wasanii ni kuwa,tusiache maisha yetu yakawa sehemu ya mziki tunaoufanya,bali mziki wetu uwe sehemu ya maisha tunayoishi..niliamua kurudi shule sababu nilikuwa nataka kubaki kuwa mtoto wa mama Hamis,na kwa kufanya kile ambacho ningekifanya kama nisingekuwa mwanamuziki...mziki,HASA HUU WETU, una siasa nyingi na hautoi ahadi ya kukupa uwezo wa kuyamudu maisha yako yote yaliyobaki na familia yako,hivyo ni busara kuwa na mipango ya ziada.
K.U: Kwa uzoefu wako baada ya kuwa nje ya Tanzania kwa muda mrefu,una ushauri gani kwa wasanii wenzio kuhusu uwezekano wao kuvusha kazi zao za sanaa nje ya mipaka ya Tanzania?
MwanaF.A:ni kama nilishajibu na hili mkuu..tunapaswa kuondoka kwenye denial state kwanza..tukubali kuufanyia marekebisho ya kimsingi mziki wetu then tukimbizane na chochoro za kuuvusha..vinginevyo tutaendelea kuimbia wa’Tz 200-300 kwenye maonyesho yetu ya nje kila wakati.
K.U: Mwisho,una ujumbe gani kwa mashabiki wako.Je wategemee vitu vipya hivi karibuni?
MwanaF.A:yeah,maskio yakae wazi..nawadondokea punde tu.
Blogu hii inakutakia kila la heri katika shughuli zako.
MwanaFA: Ahsante sana,nashukuru..na pole kwa kuchukua muda mwingi kujibu..mbio za maisha tena..na naamini wewe na watembeleaji wa blogu mtanielewa.
.









