27 Apr 2011


Ukisikia kimbembe cha zule ndio hiki kinachoikabili CCM kwa sasa.Japo chama hiki tawala ni mahiri sana kwa usanii,lakini ni dhahiri kuwa yanayoendelea sasa ndani ya chama hicho yanaweza kabisa kuwa dalili za mwanzo wa mwisho.Hebu jionee vimbwanga hivi katika stori zifuatazo:


Barua za kuwang’oa kina Lowassa zakamilika
• Yadaiwa ziko mezani kwa Msekwa

na Mwandishi wetu

Barua za makada watatu wanaotuhumiwa kwa ufisadi ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Rostam Azizi, Edward Lowassa, na Andrew Chenge, za kuwataka wajiondoe katika nafasi za uongozi ndani ya chama hicho, ziko tayari.

Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima Jumatano umethibitisha kwamba makada hao, waasisi wa mtandao uliomwingiza Rais Jakaya Kikwete madarakani mwaka 2005, wanaweza kupokea barua zao wakati wowote kuanzia leo Jumatano.

Kwa mujibu wa vyanzo vya habari, barua hizo ni sehemu ya utekelezaji wa maazimio ya Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) iliyomaliza kikao chake hivi karibuni mjini Dodoma.

Inadaiwa makada hao maarufu na wenye ushawishi mkubwa ndani ya nje ya chama hicho tawala, walipewa siku 90 tangu siku ya kikao, wapime wenyewe uzito wa kashfa zinazowakabili na wajiengue kwenye nafasi za uongozi, vinginevyo chama kitawaengua katika kikao kijacho cha NEC.

“Barua za Lowassa, Chenge na Rostam ziko tayari, na suala lao liko mikononi mwa Makamu Mwenyekiti, Pius Msekwa, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Chama. Wiki hii watakabidhiwa,” kilisema chanzo chetu cha habari kutoka ndani ya CCM.

Pamoja na mambo mengine, barua hizo zimeorodhesha tuhuma zao na kurejea maazimio ya NEC yanayowahusu.

Alipohojiwa na Tanzania Daima Jumatano juu ya barua hizo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alithibitisha kwamba tayari barua hizo zimeshaandaliwa. Naye alisema watakabidhiwa barua hizo wakati wowote kuanzia leo Jumatano.

“Kinachofanyika sasa ni utekelezaji wa maazimio ya NEC, si jambo geni. Ninachojua, tulikuwa tunasubiri mapumziko ya Sikukuu ya Pasaka yapite, kila mtu ale Pasaka yake,” alisema Nape.

Wakati barua hizo zikisubiriwa kwa hamu, baadhi ya makada wajumbe wa NEC wamekaririwa na vyombo kadhaa vya habari na katika mazungumzo yasiyo rasmi wakisema hakukuwa na azimio lolote lililopitishwa la kuwataka makada hao wapewe siku 90 za kujiengua. Vilevile, wamekanusha kuwapo kwa azimio lolote la kuwaandikia barua.

Hata hivyo, Nape amekuwa akisema kwa waandishi na katika mikutano ya hadhara kwamba NEC ilitoa azimio hilo. Baadhi ya makada wasiokubaliana na kauli za Nape, katika hali ya kuwaonea huruma au kuwatetea watuhumiwa, wamekuwa wakidai kwamba kauli za Nape zimetoka nje, si ndani ya kikao cha NEC.

Lakini baadhi yao wamekuwa wakidokeza kuwa si rahisi Nape kujitungia maneno makali ya aina hii, huku wengine wakisema anatumwa na wakubwa “kuwashughulikia” kina Rostam.

Katika kujaribu kuthibitisha kwamba Nape anazungumza jambo lisilotokana na maazimio ya NEC, baadhi ya makada wanakumbushia kauli za hivi karibuni za mtangulizi wake, John Chiligati, ambaye amepata kutaja mara kadhaa taarifa zisizosahihi za maazimio ya vikao vya Kamati Kuu na NEC, tofauti na kilichojadiliwa ndani ya vikao hivyo.

Wanasema, kwa mfano, Chiligati alipata kulalamikiwa kwa kutoa taarifa potofu kuhusu maamuzi ya Kamati Kuu kuhusu uamuzi wa ama kuilipa au kutoilipa fidia kampuni ya uzalishaji umeme ya Dowans ambayo inaidai TANESCO shilingi bilioni 94.

Vilevile, wanasema Chiligati aliwahi kutoa maazimio ya kupotosha aliposoma maazimio ya NEC kuhusu utata ulioibuka baada ya kukatwa kwa jina la Hussein Bashe katika kinyang’anyiro cha uteuzi wa mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM kwa jimbo la Nzega katika uchaguzi mkuu wa mwaka jana.

Hata hivyo, Nape anasisitiza kuwa kauli yake ni ya chama na inatokana na maazimio ya NEC. Katika mikutano ya hadhara inayodaiwa ni ya kujitambulisha, amekuwa akisisitiza kwamba Lowassa, Rostam na Chenge wametakiwa kujiondoa kwenye ujumbe wa NEC ndani ya siku 90, vinginevyo watang’olewa kwa nguvu.

Ndiye pia aliyesema kwamba wataandikiwa barua za kuwaorodheshea tuhuma zao na kuwataka waondoke kwenye uongozi wa chama. Hata hivyo, hakuna kiongozi hata mmoja aliyesema kama makada hao watavuliwa pia ubunge.

Lowassa ni Mbunge wa Monduli, Chenge anawakilisha jimbo la Bariadi Magharibi, na Rostam Azizi ni mwakilishi wa Igunga.

Wadadisi wa mambo ya siasa wanasema kilichotokea mjini Dodoma ni muendelezo wa minyukano ndani ya CCM na kwamba hoja kuu inayosababisha haya si ufisadi, bali urais katika uchaguzi wa mwaka 2015, hasa kwa kuwa baadhi yao wanasemekana wanatamani kugombea au kuunga mkono baadhi ya wagombea.

Nguvu yao ya kifedha na ushawishi wao ndani ya chama ni baadhi ya mambo yanayoogopwa na washindani wao ndani ya chama tawala. Ingawa wote watatu wamekuwa watu wa karibu sana na Rais Kikwete, habari zinasema kumekuwapo na taarifa za kuchongeana miongoni mwao, zikichochewa na makachero wanaomwaminisha Rais Kikwete kwamba sifa yake iliyopotea mbele ya jamii inaweza kurudi iwapo ataondokana na watatu hao.

Rais Kikwete naye anatumia ushauri huo kama fursa ya kurejesha matumaini ya wananchi kwake na CCM, akitumia kaulimbiu ya kujivua gamba.

Hata hivyo, wachambuzi wa masuala ya kisiasa na wakosoaji wa Rais Kikwete wamesema kujivua gamba kunakofanywa naye ni unafiki mtupu, kwani kama lengo ni kupiga vita ufisadi, naye yu miongoni mwa waliotajwa kwa ufisadi pamoja na Chenge, Rostam na Lowassa.

Baadhi ya makada wamesema kwamba kama CCm inaazimia kuondoa mafisadi, basi kiwaondoe viongozi wote waliopatikana kwa pesa za kifisadi za EPA.

Katika orodha ya viongozi waliofaidika na ufisadi wa EPA, anatajwa pia Rais Kikwete, kwa maelezo kwamba pesa hizo zilitumika kununua kura ili ashinde.

Wanasema hata kuvunja Kamati Kuu na kuingiza wajumbe wengine hakukusaidia kuisafisha, kwani walioingia ni wachafu kama waliotoka, maana historia zao na wasifu wao vinafahamika.

Wengine wanakwenda mbali na kusema kwamba iwapo Rais Kikwete atatekeleza azima yake hii, atakuwa anaandaa anguko lake lisilotarajiwa, maana atakuwa anaongeza idadi ya maadui miongoni mwa watu wanaomjua vema, waliomjenga na kumsaidia hadi hapo alipo


Mafisadi CCM waandaa mamilioni kujisafisha
*Wadaiwa kuandaa vijana kupinga hatua dhidi yao

Na John Daniel

KUNDI la mafisadi wanaokabiliwa na hatihati ya kuvuliwa uongozi na pengine uanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wamebuni mbinu mpya
kujihami kwa kutumia haramu kwa kuandaa vijana kufanya maandamano kumpinga Rais Jakaya Kikwete na chama chake.

Kundi hilo linapinga vikali uamuzi wa CCM kupitia Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), kuwapa muda wa kujiengua wenyewe kabla ya kufukuzwa baada ya siku 90.

Habari za uhakika kutoka vyanzo vyetu vimeeleza kuwa kundi hilo limepitisha bajeti ya mamilioni ya fedha kwa ajili ya kuwandaa vijana kufanya maandamano kupinga uamuzi wa kuondolewa NEC na hata CCM kwa ujumla, mara tu baada ya kukabidhiwa barua muda wowote kuanzia wiki hii.

"Tayari wameapa kuwa wakiondolewa ni lazima Rais Kikwete naye aondoke kwa kuwa ndiye aliyepitisha maamuzi ya kuwafukuza, wanapanga vijana kwa kuwarubuni kwa fedha haramu ili waandamane mara tu watakapopewa barua.

"Wiki iliyopita walikutana wakapitisha zaidi ya milioni 500 kumshughulikia Bwana mkubwa (Rais Kikwete), wanataka kumchafua ili kummaliza nguvu kuwashughulikia," kilisema chanzo kingine.

Habari hizo zilieleza kuwa mbali na Rais Kikwete anayeelezwa na kundi hilo kukabiliwa na tuhuma na ufisadi, akiwa miongoni mwa watu 11 waliotangazwa na Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dkt. Willibrod Slaa, na familia yake, akiwamo mwanawe Ridhiwan anayedaiwa kuwa mali kuliko kipato chake, pia kundi hilo linasaka kwa udi na uvumba majalada ya mawaziri wanne wa sasa kwa lengo la kuwaunganisha katika tuhuma za ufisadi, kwa kinachoelezwa kuwa ni kampeni ya 'tuchafuke wote'.

"Kati ya fedha hizo sh. milioni 18 zitatumwa katika mikoa 20 kugawiwa vijana ili wafanye maandamano ya kupinga kuondolewa na kuwapakazia wengine wanaotaka waondoke nao kama njia ya kujitakasa.

"Fedha zinazobaki zinatumika kununua mafaili ya watu wengine kutafuta makosa yao ya aina yoyote akiwamo Waziri wa Afrika Mashariki, Bw. Sitta (Samwel) Prof. Mwandosya, (Mark), Dkt. Mwakyembe (Harrison) na Membe au Magufuli," kilisema chanzo chetu.

Ilielezwa kuwa kundi hilo limekuwa likifanya vikao katika maeneo maeneo mbalimbali kwa lengo la kutaka kujisafisha na ufisadi, au kupunguza makali kwa kutaja wengine.

"Mmoja wao amejiandaa kuzungumza na waandishi wa habari kuwapa nyaraka za uongo ili kuwachafua watu wengine, walengwa wakuu ni Rais na familia yake, mawaziri wanne na wengine wadogo," kilisema chanzo kingine.

"Usifikiri hatujui hayo, mbinu zote wanazofanya tunazijua, hatuwezi kupambana na wajinga, tunasubiri tuone mwisho wao, lakini hata ninyi waandishi lazima mjue kuwa Watanzania wanaosoma vitu mnavyoandika wanajua yote," alisema kigogo mmoja wa serikali bila kutoa ufafanuzi.

Mbinu nyingine iliyotajwa mara baada ya uamuzi wa NEC Dodoma ni kuwatumia viongozi wa vyama vya siasa kutoa tuhuma mpya ili ionekane kwamba wameonewa na kupoteza lengo la kuwaondoa.

Pamoja na kwamba hakutaja jina, Chama cha demokrasia na Maendeleo ndicho kimetaja watuhumiwa wapya wa ufisadi, huku Katibu Mkuu wake, Dkt. Slaa akipinga madai ya kutumiwa kufanya hivyo kwa nia ya kuwachafua.

Katika tuhuma hizo, alizungumzia uuzaji wa nyumba za serikali bila kufuata utaratibu zilizoelekezwa na Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa na aliyekuwa waziri wake wa Ujenzi, Dkt. John Magufuli; Kuhusu fedha za EPA na mahali zilipo zile zilizorejeshwa akielekeza tuhuma hizo kwa Rais Kikwete na John Malecela na Philip Mangula waliodaiwa kuhusika katika wizi wa fedha za EPA, hasa zile zilizoingia katika kampeni ya CCM mwaka 2005.

Katika hatua nyingine kundi hilo la mafisadi wa linadaiwa kuwalenga baadhi ya viongozi wa dini kuwasafisha kwa kutangaza msimamo kuwa wameonewa na hakuna mtakatifu au wao wametolewa kafara.

Majira ilipomtafuta Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi, Bw. Nape Nnauye kujua kama wana taarifa hizo alikiri na kuongeza kuwa haziwasumbui kwa kuwa mfa maji hakosi kutapatapa.

"Kwanza nilishasema nilipokuwa uwanja wa Manzese, niliwaambia wananchi kuwa mafisadi wamejipanga kumchafua Mwenyekiti wetu na familia yake"

CHANZO: Majira

Diwani matatani kwa kumwita Chiligati fisadi

na Francis Godwin, Iringa

DIWANI wa kata ya Mgama, wilayani Iringa Vijijini, Denis Lupala (CCM), yuko matatani baada ya kumwita Naibu Katibu Mkuu CCM, Tanzania Bara, Kapteni John Chiligati, kuwa ni fisadi na anapaswa kuvuliwa gamba kama Katibu Mkuu aliyepita Luteni Yusuf Makamba na wenzake.

Diwani huyo anadaiwa kutoa kauli hiyo hivi karibuni mkoani Iringa wakati Chiligati na viongozi wengine wapya wa sekretarieti ya CCM taifa alipofanya ziara mkoani humo kwa ajili ya kujitambulisha.

Diwani hayu ambaye tayari ameitwa na sekretarieti ya wilaya na Kamati ya Maadili kujadiliwa kwa utovu kwa Chiligati na viongozi wengine waandamizi wa CCM ambao alipendekeza watimuliwe.

Akithibitisha kuitwa kwenye vikao hivyo, Lupala alisema alipewa barua ya kuitwa kuhusu tuhuma hizo, lakini hakuhojiwa.

‘Kweli waliniita na mwanzoni niliambiwa kikao kitanijadili kwa utovu wa nidhamu niliouonyesha badala yake tulijadili tukio la jukwaa kuanguka wakati Chiligati akihutubia,” alisema diwani huyo.

Hata hivyo alijigamba kuwa alikuwa amejiandaa kupangua hoja zao kwani hadi sasa binafsi hataki Chiligati abaki kwenye nafasi hiyo kwa madai kuwa anapaswa kuvuliwa gamba kama viongozi wenzake aliokuwa nao kwenye sekretarieti iliyopita.

“Nilijipanga vizuri kuwajibu viongozi wa wilaya iwapo wangejaribu kutaka kuniadhibu kwa kumwita Chiligati fisadi. Ni ukweli usiopingika kuwa kati ya watu wanaovuruga CCM Chiligati ni mmojawapo na hana sifa ya kuwa kiongozi ndani ya CC na nasema kuwa niko tayari kuwajibika kwa kusema ukweli dhidi ya Chiligati,” alisema diwani huyo.

Hata hivyo habari zaidi zinasema kuwa diwani huyo anatarajiwa kuitwa wakati wowote kuanzia sasa kujibu tuhuma alizozielekeza kwa Chiligati.

Wakati wa mkutano wa hadhara, diwani huyo wa CCM alipata nafasi ya kuuliza swali na kuanza kumrushia madongo Chiligati kwamba ni fisadi na ajiuzulu nafasi yake.

Pia alitaka Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa, Andrew Chenge (Bariadi Mashariki) na Rostam Aziz (Igunga) na wengine kufilisiwa mali zao na kunyang’anywa kadi za uanachama.

Hata hivyo alishindwa kuendelea na hoja yake baada ya baadhi ya wanachama na viongozi wa CCM kuingilia kati na kusitisha swali lake kwa Chiligati.


26 Apr 2011




Makala hii ya Profesa Mbele imenigusa sana (kama ilivyo kwa maandiko yake mengi ambayo kwa hakika ni hazina kubwa kwa Taifa).Tanzania haina uhaba wa wazalendo,ndani na nje ya nchi hiyo,lakini tatizo ni kasumba ya kutowaenzi wazalendo hao.Na namna bora ya kuwaenzi ni kufanyika kazi ushauri wao wa kitaaluma na/au kitaalamu.

Makala husika ni hii:

Wa-Tanzania wanalalamika sana kuhusu mikataba bomu ambayo inalisababishia Taifa hasara kubwa. Tafsiri yao, kwa ujumla, ni kwamba tunaingizwa katika janga hili na mafisadi ambao wanasaini kwa makusudi mikataba hii, kwamba hao ni wa-Tanzania wenye ubinafsi na uroho, na hawana uchungu na nchi, bali wanatafuta namna ya kunufaika wao. Mafisadi wetu hao wanashirikiana na mafisadi wa nje kuitafuna nchi yetu.

Kwa ujumla, nami nina hisia hizo. Kwanza kuna ukweli usiopingika kuwa maadili katika nchi yetu yanazidi kuporomoka. Vile vile nazingatia usemi wa wahenga kuwa lisemwalo lipo, na kama halipo laja. Pia tunaona taarifa kutoka sehemu mbali mbali za dunia kuhusu uozo wa rushwa katika masuala ya mikataba, zabuni, na kadhalika.

Lakini msimamo wangu hauishii hapa. Naamini kuwa hata kama tukiondoa kabisa rushwa na ufisadi, tukawa na watu wanaojali maslahi ya nchi na hao ndio wakawa wanaosaini mikataba yetu, bado tutaendelea kulizwa na mikataba bomu.

Kitakachosababisha janga hili ni kuanguka kwa elimu katika Tanzania. Kama ninavyosema daima katika blogu hii na sehemu zingine, wa-Tanzania tumejichimbia kaburi kwa kutothamini elimu ipasavyo. Ushahidi ni ufahamu wa lugha ulivyo duni, na utamaduni wa kununua na kusoma vitabu ulivyofifia au kutoweka miongoni mwetu.

Nikifafanua suala la lugha na kulihusisha na suala la mikataba, napenda kusema kuwa tupende tusipende, mikataba ya kimataifa itaendelea kuandikwa kwa ki-Ingereza, nasi tutajikuta tunasaini bila kuelewa vizuri kilichomo. Kuna matapeli wengi duniani, ikiwamo katika uwanja wa biashara na uwekezaji.

Wajanja, kwa kutambua umbumbumbu wetu, watachukulia mwanya huu kama mbinu ya kutukomoa. Laiti tungekumbuka msisitizo wa Mwalimu Nyerere pale tulipopata Uhuru, kuhusu maadui watatu tuliopaswa kupambana nao: umaskini, maradhi na ujinga.

Mwaka jana, serikali ya CCM ilitamka mara kwa mara kwamba imefanya marekebisho katika mikataba ya madini, ili kuziba mianya iliyokuwepo, iliyokuwa inatukosesha mapato tunayostahili. Sasa hapo nina suali. Ni nini kilichotufanya tusione hizo dosari tangu mwanzo? Kama si ufisadi, labda ni huu ujinga ninaoongelea. Binafsi, nakerwa kwamba serikali haijatuelezea undani wa suala hilo.
Kwa makala hiyo na nyingine za Profesa Mbele,mtembelee kwenye blogu zake, MBELE na HAPA KWETU. Pia katika blogu hizo kuna orodha ya vitabu mbalimbali vilivyoandikwa naye.


Wakati habari kuhusu chama tawala CCM "kujivua magamba" zinaendelea kukamata nafasi ya juu,ni vema tukakumbushana magamba halisi yanayopaswa sio kuvuliwa tu bali kutekeketezwa kwa moto wa gesi.CCM wanaweza kutuchezea shere kwa usanii wao lakini ukweli unabaki kuwa ni migongano ya kimaslahi miongoni mwao ndio inayopelekea hizi ngonjera za kujivua magamba.Ufisadi katika taasisi za umma na serikalini kwa ujumla ndio magamba halisi yanayopaswa kuchunwa kwa nguvu badala ya kuwaruhusu wenye magamba hayo wajivue kwa hiari.By the way,tangu lini uchafu ukajiondoa wenyewe pasipo kutumika nguvu ya sabuni na mkono aumashine ya kufulia?

Soma habari hii ujionee mwenyewe namna Tanzania yetu inavyozidi kuwa shmba la bibi

Kashfa mpya ya Ufisadi Tanesco
Tuesday, 26 April 2011 10:14

CAG ADAI IMEILIPA DOWANS BILIONI MOJA ISIVYO HALALI
Mwandishi Wetu
SHIRIKA la Umeme Tanzania (Tanesco), limeingia katika kashfa nyingine ya ufisadi baada ya kubainika kuwa limeilipa Kampuni ya kufua umeme ya Dowans dola za Marekani 1.2 milioni ikiwa ni gharama ya kusafirisha mitambo ya kampuni hiyo kuja nchini kwa ndege badala ya dola 120,000.

Matumizi hayo ya ziada yanayokadiriwa kufikia Sh1.4 bilioni za Tanzania yanaelezwa kwamba yaliingizwa katika akaunti ya Dowans kimakosa.

Hata hivyo, mpaka sasa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), amesema Tanesco imeshindwa kumpelekea ripoti ya matumizi ya fedha hizo alizoziita kuwa ni ufisadi.

Mbali na hivyo CAG amelitaka shirika hilo limpelekee mchanganuo wa matumizi ya dola za Marekani 4,865,000 sawa na Sh6.8 bilioni.

Jana, alipotakiwa kufafanua kuhusu ripoti hiyo, CAG Ludovic Utoh alisema: “Nashukuru kwa kunipigia, lakini nyie si mnazo ripoti hizo, mnaweza mkasoma na kuendelea kuripoti.”

Kwa mujibu wa gazeti la The East African, toleo la Aprili 25, mwaka huu, ripoti ya CAG iliyoishia Juni 30, 2010 inaonyesha kuwa Tanesco ilifanya malipo hayo kupitia akaunti ya gharama za mikutano.

Taarifa hiyo imeonyesha kuwa Tanesco ilishindwa kutoa maelezo kuhusu malipo hayo kwa ajili ya kukodisha ndege maalumu ya kusafirishia mitambo hiyo. Pia inaonyesha kuwa kiasi cha Sh13,000,000 ziliripotiwa kimakosa kama Sh1,300,000,000 kwenye kifungu cha matumizi ya vikao na pia kiasi cha Sh11.0 bilioni kinachohusu malipo kupitia barua ya mkopo (letter of credit) na kuingizwa katika akaunti ya makusanyo ya shirika kupitia benki ya NBC.
CAG pia alibaini kuingizwa mara mbili kwa Sh101 milioni katika akaunti ya mitambo ya Tanesco kinyume na taratibu.

CAG alisema kuwa ndani ya Tanesco hakufanyiki usuluhishi wa mapato yatokanayo na mauzo katika matawi yake kukiwemo pia jumla ya Sh103,000,000 za masurufu ambazo hazijarejeshwa. Pia umeme unaozalishwa na ule unaouzwa unaonyesha kwamba shirika hilo linapata hasara kutokana na sababu za kiufundi.

Ripoti hiyo inasema, Tanesco ilionyesha hasara za uniti 1,188 KwH’m kutoka katika uniti 4,831 KwH’m inazozalisha ikionyesha kwamba kuna hasara katika mapato. Hasara hizo zinachangiwa na kuwepo kwa wateja wasio waaminifu, bili za uongo na uunganishaji haramu wa umeme.

Imeeleza kwamba hata wateja waliokatiwa umeme, wanaendelea kutumia huduma hiyo kama kawaida licha ya kudaiwa wastani wa dola za Marekani 65,000.CAG, Utouh alikaririwa akisema manunuzi katika shirika la Tanesco yalirekodiwa kimakosa na kwa udanganyifu.

Utouh alisema wakati wa ukaguzi, iligundulika kwamba Tanesco, hawakuwa wakifanya ‘reconciliation’ (upatanisho) ya mwezi kati ya mauzo na mapato.Kwa mujibu wa CAG, kuna hasara katika idara za uzalishaji na usambazaji wa umeme kwenda wateja.

“ Kuna mapendekezo niliyoyatoa yanayotakiwa kuchukuliwa hatua na Serikali, Bunge, Kamati ya Hesabu za Serikali, Bodi ya Wakurugenzi na maofisa watendaji wakuu kupitia ripoti ya fedha iliyoishia Juni 30,2009,” ilisema ripoti hiyo.

Katika ripoti hiyo, CAG alisema katika ripoti ya mwaka uliopita ya ukaguzi katika mamlaka za umma na bodi nyingine kuna mapendekezo 15 yaliyotolewa kwa utekelezaji: “Lakini hadi sasa mapendekezo hayo hayajatekelezwa kikamilifu.”

Alisema mapendekezo hayo ambayo hayajatekezwa yanahitaji ufumbuzi wa Serikali ili kuyawezesha mashirika mengine ya umma kufanya vizuri.

Badra Masoud, Meneja mahusiano wa Tanesco hakuweza kupatikana jana kuzungumzia suala hiyo baada ya simu yake kuita muda wote bila kupokelewa huku simu ya Mkurugenzi wa Tanesco William Mhando ikiwa haipatikani.

CHANZO: Mwananchi


Wait a minute!Hivi jina "Mzee wa Kijiko" si lilikuwa la mwanamuziki wa dansi Ally Choki

Well,mazingaombwe ya kuibuka kwa watu wanaodai kupewa nguvu na Mungu kuponyesha magonjwa sugu yanaendelea baada ya mkazi mmoaj kuibuka na kudai anatibu kwa kijiko.Hebu soma mwenyewe habari kamili hapa chini

Fatuma Maumba, Mtwara

BAADA ya Mchungaji mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ambilikile Masapila kuanza kutoa dawa ya kikombe katika Kijiji cha Samunge, kilichopo Loliondo Mkoa wa Arusha, mkoani Mtwara ameibuka mtu mmoja anayetibu kwa kutoa dawa ya kijiko.

Kutokana na kuwapo kwa mtu huyo, Ahmad Linangwa maarufu kama Mzee wa Kijiko, wananchi wengi wamekuwa wakifurika katika Kijiji cha Moma Wilaya ya Mtwara Vijijini, Mkoa wa Mtwara kwa ajili ya kupata dawa ya kijiko.

Akizungumza na MTANZANIA nyumbani kwake kijijini hapo juzi, Linangwa alisema kabla ya kuanza kutoa dawa hiyo inayotibu magonjwa sugu ukiwamo ukimwi, awali aliota na kupewa maelekezo na Mwenyezi Mungu namna ya kuchanganya miti ya aina tatu kwa ajili ya kupata dawa hiyo.

“Pamoja na kupewa maelekezo hayo Aprili 18 mwaka huu, pia niliambiwa baada ya kuchanganya miti hiyo, nivilige kitu kama goroli kisha nichanganye na maji pori ambayo nitayagema kwenye mti unaoitwa Mtamba.

“Nikishafanya hivyo, maji hayo niwape wagonjwa nao watapona magonjwa yanayowasumbua,” alisema Linangwa.

Kwa mujibu wa Lingangwa, kabla ya kuanza kuwapa wagonjwa dawa hiyo, alianza kuinywa yeye wakati alipokuwa porini akiiandaa.

“Nilianza kuinywa nikiwa kule porini, nilipomaliza kuinywa, nilikimbilia nyumbani haraka ili kama ni sumu iniue wakati nimeshafika nyumbani lakini sikufa.

“Kwa hiyo watu waje watumie dawa hii, haina masharti yoyote kwani kama mtu anatumia dawa za hospitali anaweza kuendelea na dawa hizo bila wasiwasi, kama unakunywa pombe, au unavuta sigara, dawa yangu haina matatizo,” alisema Mzee wa Kijiko.

Kutokana na kuwapo kwa matibabu hayo, nauli kwa pikipiki na bajaji zimepanda kutoka Mtwara Mjini hadi kijijini Moma.

CHANZO: New Habari

23 Apr 2011



Ningetamani kuitasiri ripoti hii kutoka kimombo kwenda lugha ya taifa Kiswahili lakini ni ndefu (kurasa zaidi ya 20).Tovuti hii ipo tayari kutoa msaada wa bure kwa yeyote atakayeshindwa kuielewa katika "Lgha hii ya Malkia Elizabeti".

Loliondo Technical Report

CHANZO: Jamii Forums


Nimekutana nayo huko Jamii Forums:

Kichuguu;

Mimi kama mmoja wa wanachama waandamizi wa Jamii Forums ambapo nimekuwa mwanchama kwa karibu miaka mitano sasa tangu ikiwa Jambo Forums kabla ya kubadili jina na kuwa Jamiiforums nimekerwa sana na matamshi ya Makamu Mwenyekiti wa CCM kuwa forums hii ni ya vijana wa CHADEMA. Naona kuwa amenivunjia sana heshima yangu mbele ya wenzangu kwa kunipa image ya kuwa mimi ni mpiga propaganda wa CHADEMA.

Baada ya kutafakari kwa kina matamshi ya Pius Msekwa na jinsi yalivyoathiri image yangu kama mwanachama wa JamiiForums, nimeamua kumfungulia mashtaka ya defamation kwenye mahakama ya Douglas County hapa Omaha Nebraska nchini Marekani. Nimejadiliana na mwanasheria wangu ambaye amenipatia kifungu cha sheria kinachoniruhusu kumshitaki raia wa nchi ya nje kwenye mahakama hii, iwapo marekani ina uhusiano wa kibalozi na nchi ya mshitakiwa. Sasa hivi tuko katika hatua za mwisho mwisho za kukusanya ushahidi imara.

Nimeshapata nakala za magazeti ya kiswahili na kiingereza ila nimekuwa natafuta video clip yenye kumwonyesha Msekwa akiwa anasema maneno hayo. Vile vile bado tunashauriana kiwango cha malipo ya Punitive Damages na Compensatory Damages; mwanasheria anashauri kuwa viwango hivyo vipimiwe zaidi kwa kuangalia jinsi gani Msekwa binafsi na chama chake walivyofaidika au watakavyofaidika kutokana na matamshi yake hayo, na kwa kiasi kidogo jinsi gani yalivyoathiri image yangu binafsi kama mwanachama mwanadamizi ambaye hujitambulisha kwa wenzagu wote kuwa mimi ni Premium Member wa JamiiForums.

Tukikamailisha taratibu zote, nitawaarifuni au mtasikia kwenye vyombo vya habari Msekwa akiwa subpoenaed kwenye kesi hii ambayo pamoja na mambo mengine ninataka kuwadhibiti wanasiasa wasiwe wanaropoka mambo bila kuwa na uhakika nayo.

Ngoma inogile


TUHUMA za ufisadi ambazo Dk. Willibrod Slaa amemshushia Rais Jakaya Kikwete, zimezima mbwembwe na majigambo ya “mapambano dhidi ya ufisadi” ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), MwanaHALISI limeelezwa.

Mwishoni mwa wiki, ikiwa ni wiki moja tangu CCM itangaze “kujivua gamba” la ufisadi, Dk. Slaa amemtuhumu Rais Kikwete kushindwa kusimamia rasilimali za taifa kwa kuruhusu au kunyamazia wizi wa Sh. 249 bilioni.

Fedha hizi ni zile za mfuko wa madeni ya taifa.

Aidha, Dk. Slaa amesema Rais Kikwete ameshindwa pia kusimamia matumizi ya Sh. 70 bilioni zinazodaiwa kurejeshwa na wezi waliokiri kuiba kutoka akaunti ya EPA “ambazo hadi sasa hazijulikani matumizi yake.”

“Udhaifu huu wa Kikwete na serikali yake umechangia ufisadi wa kiwango cha juu katika matumizi ya fedha za umma,” ameeleza Dk. Slaa.

Kwa mujibu wa nyaraka za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ambazo Dk. Slaa amenukuu, Sh. 70 bilioni zilidaiwa kuingizwa katika Benki ya Rasilimali (TIB) na baadaye zikadaiwa kuwa zilitolewa ili kuanzisha benki ya wakulima ambayo haijaanzishwa.

Dk. Slaa alidondosha makombora hayo kwenye mkutano mkubwa wa hadhara katika uwanja wa Chipukizi mkoani Tabora, Jumamosi alasiri.

Kwenye mkutano huo, Dk. Slaa aliwataja pia rais mstaafu Benjamin Mkapa, makamu mwenyekiti mstaafu wa CCM John Malecela, katibu mkuu mstaafu wa CCM, Philip Mangula, waziri wa ujenzi, John Magufuli na ofisa wa ngazi ya juu wa mamlaka ya mapato ya taifa (TRA), Placidius Luoga kuwa wameshiriki ufisadi.

“Hawa, kwa njia mbalimbali, ama wameruhusu au wameidhinisha au wamenyamazia ufujaji wa raslimali za taifa,” Dk. Slaa aliuambia mkutano wa hadhara uliohudhuria na umati wa wananchi.

Hii ni mara ya pili kwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuanika majina ya wale kinaowaita “vigogo wala nchi” kwa kuwahusisha na ufujaji wa fedha na raslimali za taifa.

Akiwa na wanasheria wa chama hicho, Mabere Marando na Profesa Abdallah Safari, Dk. Slaa alisoma jina moja baada ya jingine na kutoa maelezo juu ya ushiriki wa kila mmoja katika alichoita kufisidi taifa.

Tayari kishindo cha CHADEMA mjini Tabora kimeleta kizaazaa ndani ya CCM na kufanya nderemo za juu ya kujivua gamba kuonekana kama tamthiliya.

Haya yanatokea wakati katibu mkuu mpya Wilson Mukama anasema atapambana na “mafisadi” na kwamba atawaandikia barua kuwataka wajiondoe kwenye chama.

Naye katibu mwenezi mpya, Nape Nnauye, akinusa kishindo cha Tabora, amejiingiza katika malumbano na CHADEMA. Jumapili mjini Zanzibar, alidai kuwa CHADEMA kinatumiwa na “mafisadi” ili kumchafua Rais Kikwete na mtoto wake Ridhiwani.

Lakini kwenye mkutano wa Tabora, hakuna kiongozi yeyote wa CHADEMA aliyetaja jina la Ridhiwan, jambo ambalo limetafsiriwa kuwa Nnauye alitarajia kuona jina la mtoto huyo wa rais katika orodha ya watuhumiwa.

Wakionekana wamejipanga na kufanya kile walichokiamini, Dk. Slaa na timu yake walianza kueleza kile walichoita, “wizi mkubwa usioweza kuvumilika” uliofanywa na viongozi wa CCM na watendaji serikalini.

Alikuwa Profesa Safari aliyeanza kumtuhumu Mkapa kuwa ameingiza nchi katika matatizo makubwa kwa kuruhusu uuzaji holela wa nyumba za serikali. Alisema nyumba hizo ni sharti zirejeshwe serikalini na bila masharti.

“Tunataka nyumba hizo zirejeshwe mara moja. Iwapo hilo halikufanyika, tutatumia nguvu ya umma kuzirejesha,” alieleza Prof. Safari huku akishangiliwa.

Naye Marando alisema hakuna kiongozi yeyote ndani ya CCM, akiwamo Rais Kikwete, anayeweza kujinasua katika tuhuma za wizi wa mabilioni ya shilingi za EPA zilizokwapuliwa ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Akiongea huku akiwa na nyaraka kadhaa mkononi alizodai zilitumika kukwapulia mamilioni hayo, Marando alisema katika wizi huo, Mkapa ndiye kinara mkuu.

Aliwataja wengine waliohusika na wizi huo kuwa ni Rais Kikwete, Rostam Aziz na Edward Lowassa. Marando aliituhumu serikali kwa kushindwa kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wakuu wa wizi wa EPA, badala yake imeshitaki “vidagaa.”

“Mimi nimepata nyaraka zinazoonyesha kuwa John Kato, ndiye William Kemhondo na Francis William ni Barack Goda. Wote hawa wawili ni wafanyakazi wa kampuni ya Caspian Limited, inayomilikiwa na Rostam Aziz.

Akasema yuko tayari kuendesha kesi dhidi ya Kagoda bure na kuahidi kuwa haitafika mwaka 2015 kabla hajawatia gerezani watuhumiwa wote.

Ndipo ikafuata zamu ya Dk. Slaa. Akaanza kueleza wizi ulivyotokea na akasoma tuhuma ya kila mmoja. Akasema orodha yake ya sasa, itaongezeka kwa kadri nyaraka na ushahidi unavyokusanywa na kupitiwa na timu ya wanasheria wa chama chake.

Akiongea kwa staili ileile ya Mwembeyanga, ambako alitangaza orodha ya kwanza ya watuhumiwa 11 wa ufisadi, miaka mitatu iliyopita, Dk. Slaa alisema, “Kuna watu wananituhumu kwamba mimi namsakama Kikwete kwa kuwa ni muislamu. Mimi siangalii dini ya mtu, kabila lake wala sura yake.”

Akivuta pumzi, Dk. Slaa alisema, “Ninachoangalia ni nchi yangu. Ndiyo maana huko nyuma niliwahi kumkemea Sumaye (Fredrick Sumaye) ambaye ni ndugu yangu, kabila langu na dini moja. Lakini pale serikali ilipolegalega katika kusimamia rasilimali za taifa, nilimkemea bila woga.” Ndipo alianza:

Jakaya Kikwete: Huyu ameshindwa kusimamia rasilimali za taifa kwa kuruhusu au kunyamazia wizi wa Sh. 249 bilioni pamoja na Sh. 70 bilioni zilizorejeshwa na wanaodaiwa kuwa wezi wa EPA. Fedha hizo, kwa mujibu wa nyaraka za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), zilidaiwa kuingizwa katika Benki ya Rasilimali (TIB) na baadaye zikadaiwa kuwa zilitolewa ili kuanzisha benki ya wakulima.

Nyaraka zinaonyesha kuwa pamoja na fedha hizo kutolewa TIB, hadi sasa kinachoitwa benki ya wakulima hakijaanzishwa. Alitoa siku 90 kwa Kikwete kueleza mahali ziliko fedha hizo, vingevyo yeye na chama chake wataamini kuwa fedha hizo zilitumiwa na CCM katika uchaguzi mkuu uliopita.

“Huyu Kikwete amefadhiliwa na wezi, ndiyo maana ameshindwa kuchukua hatua kwa wezi hao,” alieleza.

Dk. Slaa amesema anatoa siku 90 kwa serikali kueleza zilipo fedha za DECI, Sh. 70 bilioni za EPA, Sh. 249 bilioni kutoka deni la taifa na mabilioni mengine ambayo yamegunduliwa na mkaguzi wa hesabu za serikali.

Katika tuhuma za Mwembeyanga, CHADEMA walimtuhumu Kikwete, kwa wadhifa wake wakati huo, kusaini “mikataba mibovu” ya madini na makampuni ya kimataifa, iliyosababisha upotevu wa utajiri mkubwa na kuifanya serikali ishindwe kuhudumia vizuri wananchi wake.

Inadaiwa Kikwete alisaini mkataba na kampuni ya SAMAX Limited iliyopewa leseni ya kuchimba dhahabu katika eneo la Lusu, wilayani Nzega, Mkoa wa Tabora, mradi ulioleta mateso kwa maelfu ya wachimbaji wadogo baada ya kuondolewa kwenye makazi yao kwa nguvu.

SAMAX iliuza mradi wake kwa Ashanti Goldfields ya Ghana kwa kiasi cha dola za Marekani 253 milioni. Nao Ashanti waliuza mgodi huo kwa kampuni ya Resolute Limited ambao ndio wanamiliki mgodi wa Golden Pride ulioko Lusu, Nzega uliofunguliwa Novemba 1998.

Kikwete anadaiwa pia kusaini mkataba na kampuni ya Kahama Mining Corporation Ltd (KMCL) ambayo ni kampuni tanzu ya Sutton Resources ya Canada.

Mara zote wananchi waliswagwa nje ya makazi yao ya miaka mingi ili kupisha wawekezaji na hawakulipwa fidia kwa mali zao. Takriban wananchi 400,000 waliokuwa wakiishi na kuchimba dhahabu katika eneo la Bulyanhulu, Kahama waliachwa bila makazi.

Baadaye Sutton iliuza KMCL na Bulyanhulu kwa kampuni ya dhahabu ya Barrick Gold Corporation ya Toronto, Canada kwa dola 280 milioni. Leo hii Bulyanhulu ni moja ya migodi tajiri kwa dhahabu katika Bara la Afrika.

Benjamin Mkapa: Anatuhumiwa kushiriki au kubariki, au kunyamazia ukwapuaji wa fedha za EPA na kubariki uuzaji wa nyumba za serikali.

Kwa mujibu wa upinzani, ufisadi mkubwa ulitendeka chini ya utawala wa Mkapa.

Aidha, Mkapa anatuhumiwa kushiriki, moja kwa moja au kwa kutumia ndugu na/au washirika wa karibu wa familia yake, kumilikisha asilimia 85 ya hisa za kampuni ya Kiwira Coal Mines Ltd., inayochimba mkaa wa mawe huko Kiwira, Mkoani Mbeya kwa kampuni ya Tanpower Resources Limited inayomilikiwa na baadhi ya watu wa familia yake.

John Malecela: Ametuhumiwa kusaidia baadhi ya watuhumiwa waliokwapua mabilioni ya shilingi katika akaunti ya EPA. Upinzani ulionyesha hata baadhi ya vimemo vya Malecela vinavyodaiwa kutumika katika kufanikisha wizi.

Dk. Slaa amesema nyaraka ambazo Marando amemkabidhi zinaonyesha kuwa Malecela alisaidia wizi kufanyika.

Philiph Mangula: Ametuhumiwa kusaidia wizi wa EPA kwa maslahi ya chama chake na wao binafsi. Dk. Slaa alisema vimemo alivyoandika Mangula vilikuwa vya kumwelekeza gavana wa benki kuu wakati huo, Daudi Balali.

John Magufuli: Ametuhumiwa kutumia madaraka ya umma kwa maslahi binafsi. Magufuli ametajwa kuwa ndiye aliyepeleka katika baraza la mawaziri waraka uliotaka serikali iuze nyumba za umma na kutumia ruhusa hiyo kujimilikisha moja ya nyumba hizo.

Mbali na yeye kujiuzia nyumba hizo, Magufuli akagawa baadhi ya nyumba za serikali kwa ndugu na jamaa zake; hata mtu mmoja “chini ya mwaka miaka 18.”

Placidius Luoga: Anatajwa kwa kuingizia serikali hasara ya Sh. 800 bilioni kwa hatua yake ya kuzuia magari ya kampuni ya Tango Transport ya mjini Dar es Salaam, kwa miaka 10 kwa kisingizio cha kutolipa kodi.

Dk. Slaa amesema hatua hiyo ilisababisha mhusika kwenda mahakamani na sasa serikali imeamriwa kumlipa mlalamikaji kiasi hicho cha fedha. Dk. Slaa ameeleza kuwa serikali imeanza kulipa na tayari imetoa Sh. 500 milioni.

Pamoja na kuingiza hasara kiasi hicho kwa serikali, Luoga bado ni mwajiriwa TRA.

Katika orodha ya Mwembeyanga iliyotaja watuhumiwa 11, Edward Lowassa alituhumiwa kuhusika na kashfa ya kampuni ya City Water iliyopewa uendeshaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA) mwaka 2002.

Mwanasheria Tundu Lissu aliyefafanua dai hilo alisema, anajua kilichomo katika mkataba huo ndiyo maana anamtuhumu Lowassa kuwa mhusika katika kadhia hiyo.

Lissu ni mmoja wa mawakili wa serikali katika shauri la City Water kwenye Mahakama ya Kimataifa nchini Uholanzi ambayo inashughulikia usuluhishi wa mgogoro unaotokana na kukatishwa kwa mkataba wa City Water.

Kabla ya kukatishwa mkataba, Citywater walikwishasababisha hasara ya dola 12.5 milioni, hivyo kuthibitisha onyo lililotolewa na Benki ya Dunia mapema juu ya uwezo duni wa kampuni hizo.

Lowassa anatajwa pia kwa kuhusika kwake na kashfa ya kampuni ya Richmond Development Corporation (RDC) iliyopewa zabuni ya kuzalisha megawati 100 za umeme wa dharura mwaka 2006.

Miongoni mwa watuhumiwa ufisadi katika orodha ya mwaka 2007, ni pamoja na Nazir Karamagi, Daudi Balali, Nimrod Mkono, Rostam Aziz, Patrick Rutabanzibwa, Gray Mgonja, Basil Mramba na Andrew Chenge.

Karamagi anatuhumiwa kukaidi maoni ya Kamati ya Ushauri ya Madini ambayo ilimtaka asisaini mkataba wa Buzwagi hadi hapo serikali itakaporekebisha sheria na sera ili ipate mapato zaidi.

Gavana Balali alituhumiwa mambo mengi ikiwa ni pamoja na kufumbia macho ufujaji wa mali za umma unaofikia Sh. 522, 459,255,000 kupitia mradi wa ujenzi wa majengo pacha ya BoT jijini Dar es Salaam na Gulioni huko Zanzibar; na hongo ya dola 5 milioni kutoka kampuni ya Skanska Jensen ya Sweden ambayo ilipigwa marufuku kushiriki zabuni ya ujenzi wa majengo ya BoT.

Balali alituhumiwa pia kuidhinisha malipo ya dola za Marekani 118,396,460.36 kwa kampuni muflisi ya Meremeta Ltd., kupitia benki ya nchini Afrika Kusini. Meremeta ilikuwa ikichimba dhahabu Buhemba, wilayani Musoma.

Gavana alituhumiwa pia kudhinisha malipo ya dola za Marekani 13,736,628.73 kwa kampuni ya Tangold Ltd., kwa madai kuwa ni ugharimiaji wa “mali na madeni ya Meremeta Ltd yaliyohamishiwa kwenye kampuni mpya ya Tangold ambayo inamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100.”

Hata hivyo, iligundulika kuwa Tangold Limited ni kampuni ya kigeni iliyosajiliwa kwa mara ya kwanza nchini Jamhuri ya Mauritius na baadaye kuandikishwa nchini Tanzania kama tawi la kampuni ya kigeni.”

Wakurugenzi wa Tangold Limited, kwa mujibu wa taarifa zilizoko BRELA, ni pamoja na Daudi Balali. Gray S. Mgonja, Andrew J. Chenge, Patrick W.R. Rutabanzibwa na Vicent F. Mrisho.

Andrew Chenge alituhumiwa, miongoni mwa mengine mengi, kuishauri vibaya serikali na kuwa mkurugenzi katika kampuni ya kigeni ya Tangold Limited iliyoshiriki na/au kufaidika na malipo haramu ya dola 13,736,628.73.

Basil Mramba alituhumiwa, pamoja na mambo mengine, kushinikiza kampuni ya Alex Stewart (Assayers) Government Business Corporation ya Washington DC, Marekani, kupewa kazi ya kukagua hesabu za makampuni ya uchimbaji dhahabu nchini.

Rostam Aziz alituhumiwa kushiriki katika ukwapuzi wa mamilioni ya shilingi kutoka BoT uliofanywa na kampuni ya Kagoda Agriuculture Limited.

Nimrod Mkono alitajwa kutokana na barua ya CAG iliyobainisha kuwa Benki Kuu ilikuwa ikilipa kampuni yake ya Mkono & Co. Advocates, malipo makubwa zaidi, kuhusiana na kesi ya Valambhia, ambamo BoT inadaiwa jumla ya Sh. 60 bilioni

CHANZO: Mwanahalisi

22 Apr 2011


Makala yangu katika toleo la wiki hii la jarida mahiri la Raia Mwema inazungumzia suala lililokamata hisia za Watanzania wengi kwa sasa la CCM kujivua magamba.Makala hiyo inachambua chanzo cha magamba hayo na namna inavyomwia vigumu Mwenyekiti wa CCM,Rais Kikwete kufanikisha azma yake ya kukisafisha chama hicho (if at all ana azma hiyo).

Jarida hilo pia limesheni makala nyingine moto moto,sambamba na habari za uhakika ikiwa ni pamoja na zile zinazohusu ufisadi mpya wa "Stimulus Package".Zaidi,BONYEZA HAPA KUSOMA MAKALA HIYO na HAPA kusoma jarida zima.


Nina miaka kadhaa sijawahi kwenda kanisani.Sijisifu wala kujisikia vizuri.Kila mara ninapoongea na Baba huwa nalazimika kumdanganya kuwa siku hizi nakwenda kanisani.Ninatoka familia ya kidini hasa,na huenda leo hii ningekuwa padre kama nisingeamini kuwa sina wito.Hata hivyo,familia yetu imemtoa mmoja wetu kwa Bwana,na sasa yeye ni sista.
Mdogo wangu mpendwa,Sista Maria-Solana Chahali

Leo ni Ijumaa Kuu,siku ambayo Bwana wetu Yesu Kristo alikufa msalabani kwa ajili yetu.Nimesema sijatia mguu kanisani kwa miaka kdhaa lakini najitahidi kadri ninavyoweza kuishi kulingana na matakwa ya Bwana.Sio kwenda kanisani au kuimba mapambio kutakompatia mwanadamu uzima wa milele bali matendo.Japo ni muhimu kujumuika na waumimni wenzetu makanisani,la muhimu zaidi ni kuishi kwa mfano wa Bwana Yesu ambaye licha ya upendo wake usiomithilika alikuwa tayari kufa msalabani kwa dhambi zetu ili atuletee ukombozi.

Wakati tovuti hii inakutakia wewe msomaji mpenda Ijumaa Kuu njema,siku hii inaweza kuadhimishwa ipasavyo kwa kutafakari kuhusu upendo wa Bwana,kujitoa kwake kwa jili yetu na upeno kwa ujumla.Kama humpendi jirani yako unayemwona kila siku utakuwa mnafiki kudai unampenda Bwana mbaye hujawahi kumwona.Yesu ni upendo na amani.


Jarida la kimataifa la TIME la nchini Marekani limechapisha orodha yake ya kila mwka ya watu wenye ushawishi mkubwa zaidi duniani (the Time 100 Most Influential People in the World).

Kinarani katika orodha hiyo ni Wael Ghonim,mwanaharakati aliyahamasisha mageuzi ya kidemokrasia nchini Misri kwa kutumia vyombo vya habari vya jamii (social media) na hatimaye kupelekea kuanguka kwa utawala wa kidikteta wa aliyekuwa Rais wa nchi hiyo,Hosni Mubarak.


BONYEZA PICHA IFUATAYO kusoma orodha kamili



Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.