7 Sept 2014

Zikiwa zimebaki siku 11 tu kabla ya wakazi wa hapa Uskochi kupiga kura ya kuamua iwapo taifa hili liwe huru au liendelee kubaki katika 'Muungano wa Uingereza', kwa mara ya kwanza kabisa, kura ya maoni kuhusu 'uhuru' huo inaonyesha  wanaotaka 'uhuru' huo wanaongoza kwa asilimia 51.

Japo kitakwimu, hiyo ni sawa na sare, ukweli kwamba haijawahi kutokea kwa wanaotaka uhuru kuongoza katika kura yoyote ile ya maoni unaleta uwezekano japo kidogo wa kura ya 'Ndio' kwa wanaotaka uhuru kufanikiwa.

Kura mpya ya maoni iliyofanywa na taasisi ya kura za maoni inayoheshimika sana hapa Uingereza, YouGov, inayochapishwa Jumapili hiiinaonyesha wanaotaka uhuru wanaongoza kwa asilimia 51 huku wasiotaka uhuru wakiwa na asilimia 49, ukiondoa wapiga kura ambao hawajafikia uamuzi (undecided).

Kadhalika, gazeti la Sunday Times lililoipa kazi ya kusanya maoni taasisi hiyo ya YouGov linaeleza kwamba Malkia wa Uingereza sasa ameshtushwa na ameagiza kupatiwa maendeleo ya kila siku kuhusiana na kura hiyo.

Serikali 'Kuu' ya Waziri David Cameron sasa inatarajiwa kufanya jitihada za dakika za majeruhi kuokoa 'Muungano' huo wa zaidi ya miaka 300 usivunjike, kwa kutoa madaraka zaidi kwa serikali ya Uskochi.

Kampeni ya 'Better Together' inayopigania kuendelea kwa 'Muungano' huo imekuwa ikiongoza katika kura zote za maoni. Kampeni ya 'Yes' inayounga mkono 'uhuru' ilikuwa nyuma kwa asilimia 22 takriban mwezi mmoja tu uliopita.

Blogu hii itaendelea kuwaletea maendeleo zaidi kuhusu kura hiyo muhimu kwa hatima ya taifa la Uskochi na 'Muungano wa Uingereza.'

4 Sept 2014


NIANZE kwa kuomba samahani kwa kutoonekana kwenye toleo lililopita. Hali hiyo ilitokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu.
 
Pili, ninaomba kwa niaba ya wakazi wa Wilaya za Kilombero na Ulanga, kutoa shukrani za dhati kwa Rais Jakaya Kikwete kwa kutekeleza ahadi yake ya kuwapatia daraja linalounganisha Wilaya hizo mbili zilizopo mkoani Morogoro.
 
Kama mzaliwa wa Ifakara, ninatambua vema adha zilizokuwa zikiwakabili wakazi wa Wilaya hizo hususan, msimu wa masika ambao Mto Kilombero ulikuwa ukifurika na kusababisha usafiri wa pantoni kuwa wa matatizo.
 
Pamoja na hilo ni pongezi kwa wakazi wa Kilombero na Ulanga nilizopewa na Msaidizi wa Rais (Hotuba), Togolani Mavura, kwa kile alichokieleza kuwa ni ukarimu wa hali ya juu uliofanywa wakati wa ziara ya Rais Kikwete katika wilaya hizo.
 
Kupitia mtandao wa twitter, Mavura ‘alinifanya nitokwe na udenda’ aliponisimulia jinsi walivyoridhishwa na ladha ya samaki wa aina mbalimbali wanaopatikana maeneo hayo.
Baada ya samahani na pongezi hizo nielekee kwenye mada ya wiki hii. Wiki iliyopita binti wa Kitanzania alifariki katika tukio ambalo siwezi kulielezea kwa undani kwa vile ninaamini lipo mikononi mwa vyombo vya dola.
 
Hata hivyo, kwa kifupi, siku chache kabla ya kufariki, binti huyo, mkazi wa jijini Dar alinyanyaswa vikali katika mtandao wa kijamii wa twitter. Japo hakujapatikana taarifa iwapo manyanyaso hayo yana uhusiano na kifo chake, katika mazingira ya kawaida tu, kumnyanyasa mtu kisha akafariki siku chache baadaye ni jambo lisilopendeza.
 
Sasa kwa vile binti huyo alinyanyaswa mtandaoni kabla ya kifo chake, zilipopatikana taarifa kuwa amefariki, watumaji kadhaa wa mtandao huo ‘waliamsha sauti zao’ dhidi ya vitendo vya unyanyasaji mtandaoni. Hili ni tatizo kubwa japo halifahamiki sana, pengine kutokana na ukweli kwamba idadi ya Watanzania wanaotumia mitandao ya kijamii bado ni ndogo.
 
Kadhalika, yayumkinika kuhisi kwamba kwa watumiaji wageni wa mitandao hiyo, suala la unyanyasaji linaweza kuonekana kama ‘utaratibu’ wa kawaida tu katika ‘maeneo’ hayo, hasa kutokana na ukweli ni nadra kuona mtu akikemewa kwa kumnyanyasa mwenzie.
 
Binafsi, niliguswa na matukio hayo – unyanyasaji ulifonywa kwa binti huyo na kifo chake- na niliona kuwa hiyo ni fursa nzuri ya kuhamasisha mapambano dhidi ya unyanyasaji mtandaoni, ambao kwa Kiingereza unafahamika kama ‘cyber bullying.’
 
Kwa upande mmoja tatizo hilo linachangiwa na watumiaji wenyewe wa mitandao hiyo ambao aidha kwa uoga ama kutojali huwapa uhuru wanyanyasaji mitandaoni ‘uwanja huru’ wa kufanya watakavyo.
 
Pengine tatizo hilo ni la kitaaluma zaidi, kwani baadhi ya stadi za tabia za binadamu zinatanabahisha kuwa ni hulka ya angalau baadhi ya wanadamu kufarijika wanapoona wenzao wakitaabika.
 
Stadi hizi zinaeleza kwamba hata inapotokea ajali, baadhi ya wanaokimbilia kwenye eneo la tukio hawafanyi hivyo kwa minajili ya kwenda kutoa msaada kwa majeruhi bali kufahamu “wangapi wamekufa” kana kwamba kifo ni habari njema.
 
Pengine maelezo haya yanaweza kukufahamisha kwanini matukio ‘mema’ kama harusi, mahafali, nk hayana ‘mvuto’ mkubwa kama ajali, ugomvi, na mingineyo ‘yasiyopendeza.’
 
Na hilo linaweza kueleza vizuri kinachoendelea kwenye mitandao ya kijamii, na hususan, katika madhila aliyopitia binti huyo kabla ya kukutwa na mauti.
 
Kuna watu wengi tu walioshuhudia jinsi alivyokuwa akinyanyaswa lakini hawakuchukua hatua dhidi ya wanyanyasaji. Ninatambua umuhimu wa busara ya ‘kutoingilia yasiyokuhusu’ lakini kwa yeyote atakayesoma ‘tweets’ zake (ambazo bado zipo katika mtandao huo wa kijamii) hatoshindwa kubaini kuwa alikuwa katika wakati mgumu, na alihitaji msaada wa haraka.
 
Pengine msomaji waweza kuhoji kwanini sikuingilia kati. Ukweli ni kwamba mimi na marehemu tulikuwa ‘hatufuatani’ (not following each other) kama ilivyokuwa kwa hao waliokuwa wakimyanyasa. Na kwa taratibu za mtandao huo wa kijamii, ni vigumu kuona kinachotokea katika ‘ukurasa’ (timeline) wa mtu ‘usiyefuatana naye.’
 
Japo haipendezi kuona hadi mtu adhurike au apoteze maisha ndipo jamii ishituke kuhusu ‘jambo baya,’ ukweli ni kwamba kifo cha binti huyo kiliamsha kelele za wengi kukemea kuhusu unyanyasaji mtandaoni.
 
Cha kusikitisha, siku moja tu baada ya tukio hilo, kundi la vijana wanaosifika kwa unyanyasaji kwenye mitandao ya kijamii walianzisha ‘vita’ dhidi ya wote waliokuwa wakihamasisha mapambano dhidi ya unyanyasaji mtandaoni. Pengine kilichowasukuma vijana hao kuanzisha harakati yao hiyo mpya kilikuwa ni kile Waingereza wanakiita ‘guilt consciousness,’ yaani hali ya kujiskia unawajibika kwa ‘baya’ lililomtokea mwenzako.
 
Wengi wa vijana hawa walishiriki kumnyanyasa marehemu, na pengine kwa upeo mdogo wa kufikiri, waliona njia pekee ya ‘kuosha dhambi zao’ ni kuwaandama wanaokemea unyanyasaji mtandaoni.
Stadi mbalimbali kuhusu unyanyasaji (pamoja na huo wa mtandaoni) zinabainisha kuwa katika mazingira ya kawaida mnyanyasaji ni mtu mwenye mapungufu, na hutumia unyanyasaji kama fursa ya ‘kusawazisha’ (compensate) mapungufu yake. Kimsingi, unyanyasaji ni ugonjwa wa akili, ambapo mhusika hupata furaha kuona fulani anateseka kwa maneno au vitendo vya mnyanyasaji huyo.
 
Kuna tatizo jingine kubwa. Mitandao ya kijamii imetoa fursa kwa watu wa aina mbalimbali katika jamii kukutana pamoja. Katika mazingira ya kawaida, hiyo ni nafasi nzuri, kwani hata mtu ‘aliyekwepa umande’ aweza kuwa ‘rafiki wa kimtandaoni’ na msomi mwenye shahada kadhaa.
Nilipata kuandika huko nyuma jinsi kuwapo kwangu katika mitandao hiyo ya kijamii, hususan twitter, kulivyoniwezesha kufahamiana na mawaziri, wanasiasa, mabalozi, wasanii maarufu na hata watu wa kawaida ambao vinginevyo nisingeweza kufahamiana nao.
 
Fursa hiyo inaweza kutumiwa vibaya pia, ‘mtu asiye na chochote’ anaweza kuwa karibu na ‘watu muhimu’ na akiutumia vibaya ukaribu huo kwa kudhani kuwa ‘naye ni muhimu pia.’
Lakini baya zaidi, mitandao hiyo inatengeneza ‘wafuasi’ (followers), na kuna baadhi ya watumiaji wa mitandao hiyo wanaoweza kutafsiri visivyo wingi wa wanaowa-follow kuwa ni dalili ya kukubalika kwao katika jamii.
 
Mtu anaweza kujidanganya, kwa mfano, “mie na matusi yangu yote haya lakini nina followers elfu kadhaa. Kwa hakika matusi ni mtaji.” Na huwezi kumlaumu. Kwanini watu wenye akili timamu wamfuate mtu mwenye matusi au mnyanyasaji mtandaoni?
 
Inakuja sababu nyingine: kumfuata (following) mtu ‘maarufu’ (hata kama ni maarufu kwa matusi) kunaongeza uwezekano wa mtu kupata wafuasi wengi pia.
 
Nimekuwa nikilipigia kelele suala hili la unyanyasaji mtandaoni kwa muda mrefu, hasa ikizingatiwa kwamba nami ni miongoni mwa Watanzania wa mwanzo kabisa ‘kukumbatia’ teknolojia ya mawasiliano mtandaoni (nilianzisha blogu mwaka 2006 na kujiunga na twitter mwaka 2008).
Na kuwa kwangu huko kwa kipindi chote hicho nimeshuhudia mengi ikiwa ni pamoja na kuwa mhanga wa manyanyaso ya mtandaoni.
 
Labda kwa vile suala hili la unyanyasaji mtandaoni linawagusa Watanzania wachache, kwa maana ya idadi ya wanaotumia mitandao ya kijamii, mamlaka husika hazijafanya jitihada za kutosha kulishughulikia.
 
Mfano mzuri, karibuni hapa wakati tunahamasisha mapambano dhidi ya tatizo hilo, wahusika wa Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA) walikuwa kimya japo baadhi yao wapo kwenye mtandao huo wa kijamii.
 
Kadhalika, ‘kelele’ za wengi kuhusu suala hilo zilikosa kuungwa mkono na watu muhimu kama wanasiasa, wanaharakati na hata wengi wa wasanii wetu (ambao baadhi yao licha ya kuwa wahanga wa manyanyaso mtandaoni pia wanashuhudia mashabiki wao wakinyanyaswa). Huu ni usaliti wa wazi.
 
Hata hivyo, kwa upande wa wasanii ninawapongeza wawili, mmoja akiwa Lady Jaydee ambaye alieleza hadharani anavyofahamu jinsi tatizo hilo lilivyosambaa, na msanii mwingine maarufu ambaye siwezi kumtaja kwa vile aliwasiliana nami kwa faragha.
 
Nimalizie makala hii kwa kusema ya kuwa nimejaribu kufuata mafundisho ya Uislam katika kukabiliana na jambo baya kama hili. Katika dini hiyo, inafundishwa kwamba “ukiona jambo baya aidha lichukie au likemee au liondoe-hata kwa nguvu ikibidi.” Sasa, nimeuchukia unyanyasaji mtandaoni vya kutosha, nimeukemea vya kutosha, ila kwa hakika sijafanya jitihada za kuuondoa, kwa nguvu ikibidi. Na hilo ndilo nina furaha ya kulitangaza.
 
Kwa kuanzia, nimefungua ‘ukurasa’ katika mtandao wa picha wa Instagram kuwawezesha wahanga wa unyanyasaji mtandaoni kutumia mbinu ileile maarufu ya ‘cyber bullies’ ku-screenshot. Mhanga ata-screenshot alivyonyanyaswa mtandaoni na kui-post kisha tuiachie jamii imwelimishe mnyanyasaji haja ya kuacha vitendo hivyo. Hii sio ‘mob justice’ bali matumizi ya nguvu ya umma kuleta mabadiliko chanya kwa jamii.
 
Jingine, ninatarajia kufungua kesi dhidi ya mnyanyasaji mmoja maarufu, lengo likiwa si kumkomoa bali kufikisha ujumbe kwa wote wenye vitendo kama hivyo. Kimsingi, tatizo si hawa wanyanyasaji bali tabia wanayoiendekeza. Hatutibu joto la homa kwa kumnywesha mgonjwa maji ya baridi bali twampatia dawa ya homa. Lengo langu ni kuhamasisha nguvu ya umma kupambana na maovu.
 
Nani anajua, labda mafanikio katika hili yaweza ‘kuigwa’ pia katika mapambano dhidi ya maovu mengine katika jamii kama vile ufisadi.
 
INAWEZEKANA, TIMIZA WAJIBU WAKO

3 Sept 2014










Chanzo: CNET

 
DSC_0052
 
DSC_0053
 
DSC_0054
 
DSC_0055
 
DSC_0056
 
DSC_0057
DSC_0058
DSC_0059
 
DSC_0060
 
DSC_0061
 
DSC_0062
 
DSC_0063
 
DSC_0064
 
DSC_0065
 
DSC_0067
DSC_0068
 
DSC_0070
 
DSC_0071
 
DSC_0072
 
DSC_0073
DSC_0074
 
DSC_0075
 
DSC_0076
 
DSC_0077



Mnyanyasaji wa mtandaoni, Peter Nunn (pichani) anakabiliwa na uwezekano wa kifungo jela baada ya mahakama kumkuta na hatia ya kumtumia mbunge Stella Creasy  wa jimbo la Walthamstow kwa tiketi ya Chama cha Labour, hapa Uingereza, tweets za kutishia kumbaka.

Mnyanyasaji huyo alitumia mtandao wa kijamii wa Twitter kumwandama mbunge huyo aliyemwita mchawi katika tweets zake.

Nunn alijitetea kwamba hakuzungumzia suala la kumbaka mbunge huyo bali ujumbe  wake ulikuwa utani tu.

Kadhalika alikanusha kuendesha kampeni ya chuki dhidi ya mwanasiasa huyo wa kike, ambaye alikuwa akimsapoti mwanaharakati wa masuala ya wanawake  (feminist), Caroline Criado-Perez, katika kampeni ya  kudai noti ya Paundi 10 ya Uingereza iwe na picha ya mwanamke mwingine zaidi ya Malkia Elizabeth wa Pili ilivyo sasa.

Mnyanyasaji huyo ambaye ni dereva kutoka mji wa Bristol jana alipatikana na hatia ya kutuma ujumbe wa kudhalilisha na kutisha kwa kutumia mtandao wa wazi wa kielektroniki kati ya Juni 28 na Agosti 5 mwaka jana.

Jaji wa mahakama ya wilaya Elizabeth Roscoe alisema, "yeye (Nunn) anasema hadhani mbunge huyo na mwenzie walikwazwa na ujumbe wake. Hapana, siwezi kuamini maelezo hayo hata kidogo."

"Nina uhakika timilifu kabisa kuwa tweets zake zilikuwa na malengo mabaya."

Nunn alionekana kutahayari wakati hukumu hiyo dhidi yake inasomwa.katika mahakama ya City of London.

Baada ya hukumu hiyo, mbunge huyo ambaye hakuwepo mahakamani ali-tweet "sasa kesi ya mnyanyasaji Twitter imekwisha, ujumbe upo wazi: tishio ni tishio, iwe kwenye karatasi, picha au uso kwa uso."

Mnyanyasaji huyo alizana kampeni yake ya za kubughudhi Julai 29 mwaka jana, siku 5 baada ya Benki Kuu ya Uingereza kutangaza kuwa Jane Austen, mwandishi wa riwaya wa Kiingereza wa karne ya 18 atakuwa  sura mpya katika noti za Paundi 10.

Nunn aliposti tweets luluki dhidi ya kwa mwanasiasa huyo wa kike, ikiwa ni pamoja na video 6. Katika tweet yake moja, alieleza kuwa njia mwafaka ya kumbaka mbunge huyo ni kwa kumzamisha majini kwanza.

Baadaye ali-tweet "kama huwezi kutishia kumbaka mtu maarufu (celebrity), kuna haja gani ya kuwa nao?"

Nunn atahukumiwa tarehe 29 mwezi huu na waendesha mashtaka wameeleza kuwa wataomba kibali cha kumzuwia kuwasiliana na Mbunge huyo mwanamke.

CHANZO : Daily Express 

Miongoni mwa vyanzo vya 'matatizo' katika matumizi ya mitandao ya kijamii ni uelewa mdogo wa wengi wanaoitumia mitandao hiyo. Ni vigumu kubainisha sababu moja inayochangia uelewa huo mdogo lakini yayumkinika kuhisi kwamba baadhi ya wenzetu hawapendi kujishughulisha kusaka maarifa/ uelewa.

Lakini pengine kikwazo kikubwa zaidi katika kupata uelewa, si tu kwa matumizi ya mitandao pekee bali kila kitu, ni 'kiburi' cha aidha kutotaka kuuliza pale mhusika haelewi au kufinya anaelewa ilhali haelewi, au kibaya zaidi, kuwavunja moyo wale wanaojitahidi kueneza uelewa wa masuala mbalimbali (mara nyingi huitwa 'wajuaji' kana kwamba kujua kitu na kuki-share ni kosa la jinai).

Tuliopitia JKT twafahamu 'kanuni ya kwanza unapowasili kambini,' yaani kufahamu mahali pa kujisaidia (kichekesho ni kwamba mara nyingi kambi za porini - na nyingi ya kambi za JKT enzi hizo zilikuwa maporini- hazina vyoo, na vikiwepo ni kwa matumizi ya maafande tu. Makuruta hupaswa kutengeneza vyoo katika muda wao binafsi).

Kadhalika, japo ni jambo linalopuuzwa na wengi, ni muhimu kwa kila mtumiaji wa mtandao wa kijamii, na kwa hakika mtandao wowote ule, kujibidiisha kufahamu japo kanuni na taratibu za msingi za mtandao husika, hususan haki na wajibu wake na wa mwenye mtandao. Uelewa huu si tu ni muhimu kwa kurahisisha 'maisha yetu mtandaoni' bali pia waweza kumsaidia mtumiaji kuepuka matatizo ya kisheria pindi akikiuka taratibu na kanuni hizo.

Kwa mtandaoni, kila mtandao, uwe wa kijamii au 'wa kawaida,' una kanuni na taratibu zake. Moja ya taratibu muhimu ni pamoja na haki za mtumiaji na wajibu wake. Miongoni mwa haki hizo ni pamoja na 'taarifa za mtumiaji' wa mtandao husika. Ndio maana ikitokea mtandao ukaweka hadharani anwani ya mtumiaji pasi ridhaa yake, unaweza kufunguliwa mashtaka kwa kukiuka haki za mtumiaji.

Kadhalika, mtandao ukiruhusu (makusudi au kwa bahati mbaya) mtu asiye na mamlaka kisheria kuweka taarifa 'nyeti' za mtu mtandaoni pasi ridhaa ya mhusika, unaweza kujiingiza katika matatizo makubwa ya kisheria

Sasa nimeona huko katika mtandao wa Twitter 'harakati' zinazofanyika kuhusu haja ya kufungwa kwa akaunti ya Twitter ya ndugu yetu, marehemu Betty Ndejembi, aliyefariki hivi karibuni.

Na pengine harakati hizo zinaisaidia jamii kuonyesha umuhimu wa HARAKATI japo kuna baadhi ya wenzetu wanaotafsiri uana-harakati kama kosa la jinai.Binafsi nadhani tatizo la watu wa aina hii ni kuzowea mno kufanyiwa mambo na serikali, taasisi au watu wengine (kwa mfano wanasiasa) kiasi kwamba wanapoona mtu binafsi anachukua msimamo katika suala flani wanamtafsiri ndivyo sivyo. Harkati chanya ni kitu kizuri kwa jamii kwani zaondoa haja ya utegemezi kwa taasisi kama serikali na kuwezesha 'nguvu ya umma.'

Harakati hizo za kutaka akaunti ya marehemu ifungwe zimehusisha ombi kwa mwanasiasa mmoja maarufu ashughulikie suala hilo. Binafsi sina tatizo na waliotoa ombi hilo bali laiti wangejihangaisha japo ku-Google 'how to request Twitter to close a deceased account' (jinsi ya kuiomba Twitter ifunge akaunti ya mtu aliyefariki) wasingehitaji kutuma ombil hilo kwa mwanasiasa huyo. Naomba ieleweke kuwa si dhambi kuomba msaada kwa mtu yeyote yule, let alone mwanasiasa. Lakini kuna masuala ambayo yapo ndani ya uwezo wetu ila tatizo ni uelewa mdogo au kutokuwa na uelewa.

Taratibu za kuiomba Twitter ifunge akaunti ya mtu aliyefariki ziko hivi (tafsiri ya Kiswahili ni yangu):

"Kuwasiliana na Twitter kuhusu mtumiaji aliyefariki...

Kinapotokea kifo cha mtumiaji wa Twitter, twaweza kushirikiana na mtu mwenye mamlaka ya kushughulikia mali (estates) za marehemu au mwanafamilia aliyethibitishwa wa marehemu kuwezesha kufunga akaunti ya marehemu.

Ili kutuwezesha kushughulikia kufunga akaunti (ya marehemu), tafadhali tupatie taarifa zifuatazo:

1. Jina (username) la marehemu katika akaunti yake ya Twitter, yaani katika ishu ya marehemu Betty itakuwa @BettyNdejembi au twitter.com/BettyNdejembi 
2. Nakala ya cheti cha kifo cha marehemu. 
3. Nakala ya kitambulisho kilichotolewa na serikali (kwa mfano leseni ya udereva au hata hati ya kusafiria)
4. Tamko (statement) lililosainiwa linalojumisha vitu vifuatavyo-Jina la kwanza na la mwisho la anayetuma ombil la kufungwa kwa akaunti ya marehemu-Barua pepe ya mwombaji-Mawasiliano (simu, anwani,nk)-Uhusiano wa mwamobaji na marehemu au mali za marehemu (estate)-Dhima ya ombi kwa Twitter (kwa mfano ; ninaomba Twitter ifunge akaunti ya marehemu')-Maelezo mafupi ya kuthibitisha kuwa akaunti husika ni ya marehemu, iwapo jina lililopo kwenye akaunti hiyo halifanani la lililopo kwenye hati ya kifo cha marehemu)-Kiungo (link) cha tanzia (obirtuary) au nakala ya tanzia kutoka gazetini (sio lazima-optional) 
5 Tafadhali tutumie nyaraka hizo kwa faksi au barua-pepe kwa anwani ifuatayo: 
Twitter, Incc/o Trust & Safety1355 Market St., Suite 900San Fransisco, CA 94103Fax: 1-415-865-5405 
Zingatia: Hii ni namba ya Marekani, kwahiyo hakikisha ina namba sahihi ya kipiga simu za kimataifa (international dialing code) iwapo unatuma kutoka nje ya Marekani. 
Tunafanya mawasiliano yetu yote kwa kutumia barua-pepe, iwapo tutahitaji taarifa nyingine, tutawasiliana nawe kwa anwani ya barua-pepe uliyotupatia. Iwapo una swali lolote, waweza kuwasiliana nasi kwa [email protected]

Sasa, kwa kuangalia tu utaratibu huu, hutoshindwa kutambua kuwa hili ni suala la kifamilia zaidi kuliko lenye kuhitaji mwanasiasa ashughulikie, unless mwanasiasa husika ni mwanafamilia ya marehemu.

Kuna kitu twaweza kujifunza hapa. Kwa wenzetu huku nchi za Magharibi, kufanya maandalizi ya 'nini kifanyike baada ya kifo changu' ni jambo la kawaida. Licha ya huduma kama bima ya kifo, kuna taasisi mbalimbali zinazojishughulisha na huduma za maandalizi baada ya kifo kama vile kushughulikia maiti yako utapofariki ikiwa ni pamoja na mahali utapozikwa, usimamizi wa mirathi, nk.

Lakini pia kuna huduma mbalimbali za bure mtandaoni kuhusu hatma yetu mtandaoni baada ya vifo vyetu. Kimsingi, mada ya 'kifo na mtandao' (Death and the Internet) ina maingizo 242,000,000 katika tovuti ya kutafutia taarifa (search engine) ya Google

Ninatambua kuwa kwa mujibu wa mila na desturi mbalimbali za Kiafrika, kuchukua hatua hizi za maandalizi ya baada ya kifo kwaweza kutafsiriwa kama 'uchuro,' licha ya ukweli kwamba siku moja kila mmoja wetu atakuwa marehemu kwani kifo haikiepukiki.

Nimalizie kwa kutanabaisha kuwa lengo la makala hii sio kudhihaki harakati za wanaotaka akaunti ya marehemu Betty ifungwe (hasa nikiwa natambua uwepo wa 'uhuni usiopendeza hata chembe' wa baadhi ya watu wanaojifanya ku-tweet kana kwamba ni marehemu mwenyewe ana-tweet "kudai atendewe haki" japo tweet husika haikutoka katika akaunti ya marehemu) bali ni kuelimisha kuhusu utaratibu wa kuomba akaunti ya Twitter ya mtu aliyefariki ifungwe, suala ambalo kwa wenye uelewa  ni la kifamilia zaidi kuliko kuhitaji 'msaada' kutoka kwa wanasiasa. 

Ushauri wangu kwa wanaotaka kuona akaunti hiyo ikifungwa ni kuwasiliana na familia ya marehemu na kuwafahamisha utaratibu husika (iwapo hawafahamu). Ikumbukwe kuwa akaunti ya marehemu, iwe Twitter au katika mtandao wowote ule, ni mali ya marehemu, kama ilivyo akaunti yake ya benki, hati yake ya kusafiria, hati ya kiwanja, au mali yake yoyote ile. Ili, kwa mfano kuweza kufunga akaunti yake benki, ni lazima ipatikane ridhaa ya wenye mamlaka na marehemu, kwa mfano maelekezo katika wosia wake au maamuzi ya famili yake. Kadhalika, ili akaunti yake ya Twitter iweze kufungwa, ni lazima kupata ridhaa ya marehemu kupitia wosia wake au uamuzi wa wanafamilia yake.

Mungu amlaze marehemu Betty mahala pema peponi, Amen.


Wapiganaji wa dola ya Kiislam IS wamesambaza picha za video katika mitandao kwa lengo la kuonyesha kuchinjwa kwa mwandishi wa habari raia Marekani Steven Sotloff ambaye ni mmoja wa mateka wanaoshikiliwa na wapiganaji hao.

Mwandishi huyo Sotloff, mwenye umri wa miaka 31 ambaye alitekwa na wapiganaji hao mwezi August mwaka jana. Mwezi uliopita Sotloff alionekana mwishoni katika picha za video zilizoonyeshwa kuhusiana na kuchinjwa kwa mwandishi mwingine wa Marekani James Foley. 

Wapiganaji hao wa katika picha hizo pia wameonekana wakimtishia kumuua mateka mwingine anayedhaniwa kuwa ni raia wa Uingereza. 

Baada ya mauaji ya mwandishi wa awali Foley, mama mzazi wa mwandiashi wa Sotloff alitoa ombi maalumu kwa kiongozi wa wanajeshi hao Abu Bakr al-Baghdadi kutoa muua mtoto wake. Msemaji wa Ikulu ya White House Josh Earnest amesema kuwa maofisa wa Marekani wanaendelea na uchunguzi wa ripoti hiyo.

Marekani hivi karibuni ilifanya mashambulizi ya anga dhidi ya IS nchini Iraq. 

Mwandishi wa masuala ya usalama wa BBC Frank Gardner amesema hatua hiyo ya wapiganaji wa IS ni kulipa kisasi kwa Marekani

CHANZO: BBC Swahili

31 Aug 2014


Siku moja nilipokea barua-pepe kutoka kwa msomaji mmoja wa makala zangu katika jarida la Raia Mwema. Licha ya kupongeza kuhusu makala hizo, alinipa ombi ambalo kwa kiasi flani liliniacha na tabasamu. Namnukuu, "... tuna matatizo mengi huku kwetu, kila anayekuja anajali maslahi yake tu. Nakushauri ufikirie kuhusu kugombea katika jimbo letu mwakani." Nilimshukuru msomaji huyo kwa pongezi zake lakini nikamweleza bayana kuwa kamwe sintojiingiza katika uongozi wa kisiasa. Nilimfahamisha kuwa mie ni muumini wa falsafa kuwa yawezekana kuutumikia umma kwa ufanisi pasi haja ya kuwa kiongozi.

Falsafa hiyo inachangiwa na ukweli kwamba nimeshawahi kuwa kiongozi mara mbili, maishani mwangu. Mwaka 1991 nikiwa mwanafunzi wa kidato cha tano katika Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Tabora (Tabora Boys') nilichaguliwa kuwa kiranja mkuu.Lakini kwa vile shule hiyo ilikuwa ya mchepuo wa kijeshi, wadhifa wa kiranja mkuu ulikuwa ukijulikana kama Kamanda Mkuu wa Wanafunzi (Students' Chief Commander), na sare ziliambatana na 'vijimkasi' viwili mabegani.

Japo wadhifa huo ulinipa fursa ya kwanza ya uongozi, tukio moja la mgomo wa wanafunzi lililojiri wakati nipo madarakani sio tu lilinipa mtihani mgumu sana bali pia lilinionyesha sura nyingine chungu ya uongozi. Kwa upande mmoja nilipaswa kuwa kiungo kati ya uongozi wa shule na wanafunzi, lakini wakati huohuo nami ni mwanafunzi na walitarajia niwe upande wao, huku walimu nao wakitaka niwe upande wao. Kwa busara na skills nilizopata kabla ya tukio hilo, mgomo huo ulimalizika salama na sikujenga maadui upande wowote kwa vile nilisimamia kwenye kanuni na taratibu na haki.

Fursa nyingine ya uongozi ilijitokeza mwaka 2000 nilipokuwa mtumishi wa taasisi flani ya serikali huko nyumbani. Niliteuliwa kuwa mkuu wa wilaya ya kiutendaji (operational district/zone), nafasi niliyoshika hadi ninaondoka huko nyumbani miaka miwili baadaye. Ugumu mkubwa wa wadhifa huu ulikuwa kwenye 'kuwa macho masaa 24'...na wakati mwingine kukurupushwa usingizini na kuulizwa 'nifahamishe kilichotokea sehemu flani' ilhali sina habari ya nini kimetokea. Lakini jingine gumu lilikuwa kwenye kuwaongoza watu nilioanza ajira nao pamoja na wengine walionizidi miaka kadhaa ya uzoefu. Kadhalika, wasaidizi wetu mtaani walikuwa na matarajio makubwa ya 'uzalishaji' wao pamoja na maisha yao binafsi. Hata hivyo niliondoka nikiwa na rekodi ya kujivunia.

Kwa kifupi, fursa zote hio zilinifundisha kuwa uongozi ni mzigo mzito na unahitaji kujitolea kwa kiasi kikubwa. Ndio maana kila nikisikia mawazo ya kujihusisha na uongozi, jibu langu jepesi ni HAPANA.Not again. Sio kwamba ninakwepa majukumu lakini kwa muda mrefu sasa nimekuwa nikijihusisha na uraia kama uongozi, kwa maana ya kutumainia nguvu za raia katika ujenzi wa taifa. Ndio hizo kelele tunazopiga magazetini, hapa bloguni na kwenye mitandao ya kijamii.

Lengo la makala hii sio kuelezea historia yangu au uwezo wa uongozi bali suala lililojitokeza katika mtandao wa kijamii wa Twitter juzi. Nadhani wengi wenu wasomaji mnafahamu kilichomsibu Betty Ndejembi, aliyetutoka juzi. Kabla ya kufariki kwake aliandamwa na unyanyasaji wa kutosha katika mtandao huo. Baada ya kifo hicho, mie niliungana na 'wenye mapenzi mema kwa jamii' kukemea unyanyasaji mtandaoni, kwa kimombo 'cyberbullying.' Hata hivyo, katika kuhamasisha mapambano hayo sikumtaja wala kumtuhumu mtu kuwa ni mnyanyasaji wa wenzie mtandaoni. Nilichohamasisha ndicho hicho nilichoeleza hapo juu: sie watumiaji wa mtandao kama wahanga wa unyanyasaji wa mtandaoni kuunganisha nguvu zetu dhidi ya wanaofanya vitendo hivyo. Na kwa hakika mapokeo yamekuwa mazuri sana. Watu wengi wamewasiliana nami kunifahamisha jinsi walivyokuwa wahanga wa cyberbullying.

Wito wangu kwa jamii umekuwa sio kusubiri serikali au wanasiasa kuchukua hatua ya kukomesha tabia hiyo bali sie kama wananchi na wahanga wa tabia hiyo kuunganisha kuvu na kupambana nayo. Kwa lugha nyingine, sie wenyewe tuchukue uongozi wa mapambano dhidi ya wanyanyasaji wa mtandaoni.

Hata hivyo, jioni ya leo likaibuka kundi la watu waliaonza kunishambulia vikali kuhusiana na kampeni hiyo ya kupambana na unyanyasaji mtandaoni. Kikubwa ni tuhuma kwamba mie wanayeniita 'mwanaharakati wa cyberbullying' ni 'bully' (mnyanyasaji) pia. Na mmoja wao akapata ujasiri wa kupitia tweets zangu za nyuma na kuzi-screenshot ili 'kuthibitisha kuwa mie ni mnafiki nisyestahili kukemea cyberbullying.' Wakati mwingine huwa nashangazwa na 'ujasiri' wa aina hii ambao hata kwa mwenye uelewa mdogo tu wa sheria anaweza kujua athari zake.

Hadi hapo sikuona tatizo sana japo nilishangazwa na 'hasira' za watu hao ilhali sikuwahi kuwatuhumu kuwa wao ni bullies. Na hata asubuhi nilitwiti kuhoji ''kama tunapozungumzia ufisadi, hukasiriki kwa vile wewe si fisadi, kwanini tukizungumzia cyberbullying ukasirike ilhali wewe sio cyberbully?"

Lakini katika mwendelezo wa shutuma zao dhidi yangu, mmoja wao akavuka mstari wa kisheria. Siwezi kuliongelea kiundani suala hili kwa sababu za kisheria.

Awali nilipoamua kuungana na wengine kukemea unyanyasaji mtandaoni sikudhani kwamba itafika mahala pa kuchukua vitendo kulazimisha wanyanyasaji hao waache tabia hiyo. Hata hivyo, kwa kilichotokea leo, nimeamua kuhamia kwenye vitendo.

Tuna tatizo kama Watanzania, ni wepesi wa kulalamikia matatizo yanayotukabili lakini ni wagumu kuchukua hatua za vitendo kuyatatua. Mgao wa umeme, huduma mbovu za baadhi ya makampuni, tatizo la ajali zisizoisha, ufisadi, na kadhalika. Kwa kiasi kikubwa tumekuwa watu wa kulalamika tu kana kwamba malalamiko hayo yataleta mabadiliko.

Katika hili la unyanyasaji mtandaoni, asilimia kubwa ya watu wanaotaka 'kuishi kwa amani mtandaoni' wameunga mkono japo kwa maneno haja ya kukemea unyanyasaji mtandaoni. Lakini kama ilivyojitokeza leo jioni ambapo nimekuwa mhanga wa ushiriki katika harakati hizo, bado kuna wenzetu wanadhani wana hatimiliki ya kuwabughudhi watu mtandaoni watakavyo. Inabidi tuseme enough is enough. Kwa vile haijawahi kutokea huko nyumbani kwa mtu kuingia matatizoni kutokana na alichoandika mtandaoni, watu wengi tu wanaendelea kudhani kuwa akiwa mbele ya keyboard ya kompyuta yake ana uhuru wa kunyanyasa, kudhalilisha, kutukana na kufanya matendo mengine ambayo kimsingi ni makosa kisheria.

Ukweli ni kwamba tukiacha 'njia za asili' za kudhibiti 'wakorofi' kwenye mitandao ya kijamii, yaani aidha kuwa-mute, kuwa-unfollow au kuwa-block, kuna njia za ufanisi zaidi kama vile za kisheria alimradi kuna ushahidi wa kutosha.

Hatimaye nimefikia uamuzi wa kuchukua hatua za vitendo dhidi ya unyanyasaji mtandaoni (cyberbullying). Sifanyi hivi kwa minajili ya kuingia kwenye vitabu vya historia kama Mtanzania wa kwanza kupambana na cyberbullies kwa vitendo bali ninafanya huduma kwa umma. Huhitaji kuwa kiongozi ili kuitumikia jamii. Na sihitaji madaraka ili niweze kupambana na tabia hii isiyofaa. Hakuna miujiza itakayowalazimisha wanyanyasaji wa mtandaoni kuacha tabia hiyo. Kitu pekee ni pale wanapofunzwa madhara ya vitendo vya aina hiyo.

Japo ningependa kuwa sehemu ya kundi linalopambana na suala hili, hadi sasa hakuna dalili zozote za uwepo wa mkusanyiko wa kukabiliana na tatizo hili ambalo kwa hakika linawasumbua wengi. Lakini tukisema tusubiri mpaka watu wajipange na kuunda kikundi, wenzetu wengi zaidi watazidi kuwa wahanga wa unyanyasaji huo wa mtandaoni.

Natambua ugumu wa mapambano haya lakini kila mapambano ni magumu. Natambua kutakuwa na lawama na kukatishana tamaa lakini liwalo na liwe lazima mtu flani awe mfano kwa wenzie kwamba cyberbullying is not just wrong but also a criminal offence. 

Lengo la makala hii sio kumtisha wala kumzuwia mtu kunituhumu kuwa nami ni cyberbully. Ninaheshimu uhuru wa kujieleza alimradi hauvuki mpaka.Na kitu ambacho kamwe siwezi kukivumilia  ni uvunjifu wa sheria dhidi yangu.

Ni matumaini yangu kuwa kama inavyofundisha Biblia Takatifu kuwa 'ukipiga mchungaji kondoo watasambaa,' kumwajibisha mmoja wa wanaodhani mitandao ya kijamii ni fursa ya kuwanyima wenzao amani kutapeleka ujumbe kwa wengine wanaoamini hivyo pia. Mafundisho ya Kiislam yanatueleza kwamba "ukiona jambo baya basi aidha lichukie, au likemee au liondoe." Nimeshachukia unyanyasaji mtandaoni vya kutosha, nimeukemea vya kutosha, na sasa ni wakati wa kuuondosha kwa vitendo. Haitokuwa rahisi lakini nina hakika nitafanikiwa. Inshallah!

Na mwisho, lengo la harakati ninazoanza si kumkomoa mtu au watu flani. Hao waliotumia muda wao kunishambulia ni dalili tu za tatizo, ninacholenga kupambana nacho ni chanzo cha tatizo. Mtu anaposkia baridi kwa vile ana homa, huwezi kumtibu kwa kumpa maji ya moto bali tiba ya homa. Kadhalika, unyanyasaji mtandaoni hauwezi kukomeshwa kwa kubana watu flani tu bali kulikabili tatizo lenyewe. Ifike mahala mtu ajiulize mara mbili kabla ya kuposti 'maneno yasiyofaa' dhidi ya mtu mwingine mtandaoni.

Ili mabadiliko ya kweli yatokee hasa ya kuondoa jambo baya ni lazima kujitoa mhanga. Iwapo uamuzi wangu wa kupambana na tabia hii utapelekea madhara kwangu basi na iwe. Ninaamini kuwa mwenye haki ataanguka saba mara sabini lakini hatimaye atasimama. Nikisema 'mwenye haki' simaanishi kuwa harakati hizi ni za kutafuta haki yangu bali ya wanyonge mbalimbali wahanga wa unyanyasaji mtandaoni. Tukiwakalia kimya bullies sio tu watadhani tunaridhia vitendo vyao bali pia wataendelea kutengeneza victims.

INAWEZEKANA, NA NITATIMIZA WAJIBU WANGU



30 Aug 2014

Watanzania watatu, Hemedi Dendengo Sefu, Hassan Mohamed Nduli na Abdou, jana walitiwa hatihani na mahakama moja nchini Afrika Kusini kwa kosa la kula njama za kumuua aliyekuwa Mkuu wa Majeshi ya Rwanda Jenerali Faustin Kayumba Nyamwasa mwezi Juni mwaka 2010.

Watanzania hao walikuwa miongoni mwa watuhumiwa sita, ambapo wawili walikutwa hawana hatia, na mmoja, raia wa Rwanda, alitiwa hatiani. Watahukumiwa mapema mwezi ujao.

Hakimu aliyeendesha kesi hiyo alieleza kuwa lengo la mauaji hayo lilikuwa ni la kisiasa. Jenerali Kayumba alikimbilia uhamishoni Afrika Kusini baada ya kutibuana na rafiki yake wa zamani, Rais wa sasa wa Rwanda, Paul Kagame. Hata hivyo, Rwanda imekanusha kuhusika na mpango wa mauaji hayo.

Mwandishi wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) alieleza kuwa Mkuu huyo wa zamani wa Majeshi ya Rwanda alikuwepo mahakamani wakati hukumu hiyo inatolewa. "Mahakama imeeleza kwa usahihi kuwa mpango wa kuniua ulikuwa na malengo ya kisiasa," alisema Nyamwasa.

Mmoja wa Watanzania hao, Sefu, alitajwa kuwa ndiye aliyepangiwa kumpiga risasi Jenerali huyo.

CHANZO: Habari hii imetafsiriwa kutoka vynazo mbalimbali mtandaoni




Kikundi cha kigaidi cha Taliban huko Aghanistan kilikuwa kipo tayari kumwachia huru Sajenti wa Jeshi la Marekani Bowe Bergdahl ili kumpata mwanamama huyu. Magaidi wa ISIS nao walikuwa wapo tayari kumwachia mwandishi wa habari wa Marekani waliyemuua kwa kumkata kichwa, James Foley iwapo mwanamama huyo angeachiwa huru. Je kwanini takriban kila kikundi kikubwa cha kigaidi kinamhitaji Aafia Siddiqui?

Miaka miwili iliyopita, maafisa waandamizi wa masuala ya usalama wa taifa nchini Marekani walipokea 'ofa' ya kushangaza kutoka Pakistani. Iwapo Marekani wangekubali kumwachia mwanamke mmoja anayetumikia kifungo kirefu huko Texas kwa kosa la jaribio la kuua, basi Sajenti Bowe Bergdahl aliyetekwa na Taliban tangu mwaka 2009 angeachiwa huru.

Kwa mujibu wa taarifa za kiusalama, Rais Barack Obama na maafisa wake walikataa 'ofa' hiyo. Kumwachia mwanamke huyo, Bowe Bergdahl kunekinzana na msimamo wa Marekani wa kutofiki amakubaliano na magaidi. Kadhalika, kumwachia huru mwanamke huyo kungemrejesha uraiani mtu hatari kwa usalama.

Siddique, mwenye umri wa miaka 42, na anayefahamika kwenye anga za kupmbana na ugaidi kama 'Lady al-Qaeda' ameshahusishwa na mmoja wa magaidi wahusika wa  mashambulizi ya kigaidi ya Septemba 11 Khalidi Sheikh Mohammed, na wakati flani alikuwa katika orodha ya magaidi wanaosakwa zaidi (most wanted terrorist list).

Gaidi huyo wa kike alipata elimu yake katika chuo kikuu kinachoheshimika sana duniani cha M.I.T na ana shahada ya uzamifu (PhD). Mwaka 2008, alikamatwa akiwa na kemikali ya Sodium Cyanide, pamoja na nyaraka za jinsi ya kutengeneza silaha za kemikali, mabomu ya kusababisha madhara makubwa (smart bombs) na jinsi ya kuitumia Ebola kama silaha. Maofisa wa Shirika la Upelelezi la FBI walipojaribu kumhoji, mwanamke huyo alichukua silaha na kufyatua risasi.

Japo Marekani haikulipa uzito wazo la kubadilishana mwanamke huyo na 'mateka waliokuwa mikononi mwa magaidi,' Siddique amekuwa turufu muhimu kwa magaidi kila linapokuja suala la 'kubadilishana mateka' mbalimbali wa Marekani na Ulaya walio mikononi mwa magaidi.

Jumanne iliyopita, kikundi cha kigaidi cha ISIS kilidai gaidi huyo wa kike aachiwe huru ili nao wamwachie huru mwanamke mmoja wa Kimarekani aliyetekwa huko Syria alipokuwa akifanya kazi katika shirika la misaada ya kibinadamu. Maafisa wanaamini kuwa ISIS inawashikilia mateka angalau Wamarekani wengine wanne, ikiwa ni pamoja na mwandishi wa habari Steven Sotloff. Magaidi hao wanataka kulipwa Dola za Marekani milioni 6.6 ili wamwachie huru mwanamke huyo mtumishi wa shirika la misaada ya kibinadamu ambaye ndugu zake wameomba jina lake lihifadhiwe.

Wakati Ikulu ya Marekani imekuwa ikikataa katakata wazo la kumwachia huru mwanamke huyo gaidi ili kuwezesha kuachiwa huru kwa mateka wa nchi hiyo waliopo katika mikono ya magaidi, "Twafahamu kuna wanaotengeneza mazingira katika 'Wizara ya Ulinzi' ya kuangalia uwezekano wa kubadilishana mateka kwa kumtumia Siddique."

Mjadala mkubwa uliibuka baada ya kuchinjwa kwa Foley kuhusu aidha kulipa fedha kwa magaidi au kuwaachia wafungwa kama wanavyodai magaidi hao. Marekani, tofauti na nchi nyingi za Ulaya, huwa hailipi fedha kwa ajili ya kuachiwa huru raia wake waliotekwa. Na inaelezwa kuwa hiyo ni miongoni mwa sababu zinazowavunja moyo magaidi kuwateka nyara Wamarekani kwa minajili ya kudai fidia ili mateka hao waachiwe huru, kwa mujibu wa mtaalam mmoja wa ugaidi.

Siddique ni kama 'celebrity' flani nchini Pakistan, ambapo kifungo chake mwaka 2010 kilipelekea maandamano nchini humo (Pakistan). Matokeo ya kifungo cha Siddique yalikuwa hahabari zilizoongoza katika magazeti yote makubwa.

Hukohuko Pakistan, kikundi kijiitacho 'Brigedia ya Aafia Siddique'kimeshafanya mashambulizi kidhaa dhidi ya serikali ya nchi hiyo kama upinzani na malalamiko yao dhidi ya wanachokiona kama kifungo kisicho cha haki kwa mwanamke huyo hatari.

CHANZO: Jarida la Foreign Policy



Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.