29 Mar 2015



Kwa muda mrefu, baadhi ya watumiaji wa mtandao wa kompyuta (Internet) wamekuwa na wakati mgumu kufuatia kushamiri kwa unyanyasaji mtandaoni, kwa kimombo CYBERBULLYING.

Kwa kiasi kikubwa, tatizo hili linaakisi tabia zetu nje ya mtandao. Mtu aliyezowea kunyanyasa wenzie mtaani, akiingia mtandaoni anaweza kuendeleza tabia hiyo kirahisi. Kadri mtandao unavyozidi kuwa sehemu ya maisha yetu ya kila siku ,ndivyo unavyoakisi maisha yetu 'ya kawaida' nje ya mtandao. 

Kwa upande mwingine, mtandao unatoa fursa ya watu wenye tabia tofauti kukutana. Ndio maana si ajabu kukuta mtu mmoja akiweka bandiko kuhusu dini, mwingine akaweka bandiko kuhusu matusi.

Licha ya tabia, mtandao pia huwakutanisha watu wenye sifa tofauti: wapole na wakorofi, wapenda amani na wagomvi, wenye elimu na mbumbumbu, wenye aibu na wasio na mishipa ya aibu, nk. 

Kadhalika, mtandao unatoa fursa mbalimbali, nzuri na mbaya. Kwa mfano, mtandao unatuwezesha kuwa karibu na viongozi wa nyanja mbalimbali, kutoka mawaziri hadi viongozi wa taasisi binafsi.Uzuri wa fursa hiyo ni pamoja na kurahisisha mawasiliano baina ya watu wanaotoka 'madaraja' tofauti ya kijamii. Kadhalika, fursa hiyo inatuwezesha kujifunza kutoka kwao, sambamba na kufuatilia masuala mbalimbali ambayo kutokana na nafasi zao yanagusa maisha yetu binafsi au ya jamii kwa ujumla.

Fursa hiyo pia inatuwezesha kuwa karibu na watu mbalimbali, muhimu na wa kawaida. Katika mazingira ya kawaida, ni vigumu kufahamiana na Waziri, kwa mfano, labda kuwe na undugu, kufahamiana au mahusiano kikazi.

Hata hivyo, mtandao pia unatoa fursa 'mbaya.' Binadamu tupo tofauti, kuna wenzetu ambao wakiiona fursa wanaitumia kwa manufaa, lakini kuna wengine sio tu hawataki kujifunza 'mazuri' ya wenzao (ambayo wao hawana) pia hujenga chuki na jitihada za kuwachafua au kuwadhalilisha wenzao wenye 'mazuri.' Kwa mfano, unaweza kukutana na mtu ambaye hakubahatika kupata elimu ya kutosha, au hakusoma kabisa. Anapokutana na mwenye elimu kiasi au ya juu, badala ya kutumia fursa hiyo kama 'darasa nje ya shule' anaanzisha chuki na uhasama usio na manufaa.

Kama dunia ilivyo uwanja wa fujo, ndivyo ilivyo kwa mtandaoni. Kuna mazuri na mabaya. Kuna baadhi yetu ambao tumenufaika sana kwa uwepo wetu mtandaoni, kwa maana ya kutengeneza urafiki na watu muhimu, lakini pia kuna nyakati tumejikuta tukikutana na 'maadui.'

Ofkoz, mtandano sio sehemu ya kubadilisha mawazo, kujifunza au kuuliza maswali tu bali pia ni sehemu ya burudani. Utani ni ruksa lakini utani wenyewe usizidi kiwango. Na kanuni ya mtaani kuwa usimtanie mtu asiyekutania, ina-apply mtandaoni pia.

Kwa bahati mbaya kuna wenzetu ambao hulazimisha utani.Wengine huenda mbali zaidi kwa kulazimisha kumjua mtu zaidi ya anavyojijua yeye mwenyewe.

Kwa bahati nzuri, hatimaye serikali imesikia kilio dhidi ya unyanyasaji wa mtandaoni na Jumanne ijayo inatarajia kuwasilisha muswada kuhusu uhalifu wa mtandaoni ambao pamoja na mambo mengine unaharamisha unyanyasaji wa mtandaoni (cyberbullying) 

Katika muswada huo unajulikana kwa kimombo kama The Cyebrcrimes Act, 2015, ibara ya 23 inaharamisha unyanyasaji mtandaoni (cyberbullying) na kutaja adhabu husika. 

Muswada unafafanua maana ya cyberbullying, kwamba "mtu hataruhusiwa kuanzisha au kutuma mawasiliano ya kielektroniki kwa kutumia kompyuta kwa mtu mwingine kwa malengo ya 'kumsukuma kwa nguvu' (coerce), kumtisha, kumyanyasa au kumsababishia msongo wa mawazo, na mtu atakayekiuka kipengele hocho atakuwa anafanya kosa, na adhabu yake ni sio chini ya shilingi milioni tatu au kifungo cha sio chini ya mwaka mmoja au adhabu zote pamoja."  

Muswada kamili ni huu hapa chini (kwa bahati mbaya au makusudi, watawala wetu hawakuona umuhimu wa kuupatia tafsiri ya Kiswahili)



Wakati muswada huu ni habari njema kwa wahanga wa unyanyaswaji mtandaoni, unatarajiwa pia angalau kupunguza kushamiri kwa matusi na picha zisizofaa mtandaoni. Sio siri kwamba baadhi ya mitandao ya kijamii, hususan Instagram, imegeuka uwanja wa matusi.

Kibaya zaidi, umahiri wa matusi umegeuka moja ya vyanzo vya umaarufu mtandaoni. Kama nilivyobainisha hapo juu,mtandao unatoa fursa 'mbaya' kwa wenzetu  wasio  na cha kuelimisha, kujadili au hata kujivunia hadharani, na matokeo yake ni kuwabughudhi watu wengine au kubandika picha zisizofaa kama mbinu ya kusaka sifa za kipuuzi.

Hata hivyo, ni muhimu kukumbushana kuwa Tanzania yetu haina uhaba wa sheria.Tatizo kubwa ni katika kuziheshimu na kuzitekeleza. Twaweza kuwa na sheria kali dhidi ya uhalifu wa mtandaoni lakini utekelezaji ukiwa hafifu basi sheria hizo zitabaki maandiko tu vitabuni.

Kadhalika, ni muhimu kutahadharisha kwamba sheria hii ya uhalifu wa mtandaoni isitumiwe vibaya na serikali kuwanyima wananchi uhuru wa mawasiliano, au kibaya zaidi, kuitumia kwa minajili ya kuficha maovu na kuwalinda waovu. Sitarajii kuona sheria hii ikitumika iwapo chombo cha habari kitaibua utovu wa maadili wa kiongozi, kwa mfano.

Mwisho, ni matarajio yangu kuwa vitendo vya uhalifu wa mtandaoni, ikiwa ni pamoja na cyberbullying, vitapungua kufuatia sheria hii, iwapo itapitishwa na bunge. Angalau sasa, cyberbullies watafikiria mara mbili kabla ya kumwaga sumu zao kuwanyanyasa watu wasio na hatia.

26 Mar 2015

The United States said on Wednesday it had information of “possible terrorist threats” to locations frequented by Westerners in Uganda’s capital, Kampala, and warned that an attack could take place soon.
The U.S. Embassy in Kampala issued the warning in a statement posted on its website.
"The U.S Embassy has received information of possible terrorist threats to locations where Westerners, including U.S. citizens, congregate in Kampala, and that an attack may take place soon," it said.
"Out of an abundance of caution, the U.S. mission has canceled some non-essential events scheduled at local hotels in the coming days," it added.
Uganda is a close security ally of the United States in East Africa. The embassy issued similar alerts last year about possible attacks in Uganda.
The embassy cautioned that foreigners staying in or visiting hotels should expect increased security sweeps.
Uganda is one of the countries that contributes forces to an African Union peacekeeping mission battling the Islamist militant group al Shabaab in Somalia.
Al Shabaab, which is aligned with al Qaeda, attacked a shopping mall in Nairobi, capital of neighboring Kenya, in 2013. In 2010, it bombed sports bars in Uganda where people were watching soccer’s World Cup on television. Dozens were killed in both attacks.
SOURCE: Matthew Aid



Naibu Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,Mohamed Thabit Kombo akimpongeza Mwenyekiti wa Mfuko huo,Doris Mollel kwa kuona jukumu la kusaidia jamii katika kuokoa maisha ya watoto njiti.






Naibu Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,Mohamed Thabit Kombo akizungumza wakati wa hafla ya kutambulisha Mfuko wa Doris Mollel,iliyofanyika kwenye Hoteli ya Hyatt Regency,jijini Dar es salaam.




Mwenyekiti wa Mfuko huo,Doris Mollel akizungumza na wageni waalikwa waliofika kwenye hafla ya kutambulisha Mfuko wa Doris Mollel,uliofanyika kwenye Hoteli ya Hyatt Regency,jijini Dar es salaam.



Naibu Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,Mohamed Thabit Kombo (pili kushoto),Balozi Mwanaid Maajar (kulia),Mwenyekiti wa Mfuko huo,Doris Mollel (katikati) pamoja na wadau wengine wa Mfuko huo wakishiriki kwa pamoja kukata keki,kuashiria uzinduzi rasmi wa Mfuko wa Doris Mollel,uliofanyika kwenye Hoteli ya Hyatt Regency,jijini Dar es salaam.



Sehemu ya Wageni waalikwa katika hafla ya kutambulisha Mfuko wa Doris Mollel,iliyofanyika kwenye Hoteli ya Hyatt Regency,jijini Dar es salaam.



Picha ya pamoja na baadhi ya wadau waliohudhulia hafla hiyo.


Kutoka kulia ni HEENA ambaye ni mmoja kati ya washirika wakubwa wa mfuko huo, wakiwa wameshikana mikono na muanzilishi wa mfuko huo miss DORIS MOLLEL pamoja meneja wa mfuko huo RAHAB MBISE mara baada ya kuzindualiwa kwa mfuko huo jijini Dar es samaam


Meneja wa mfuko huo RAHAB MBISE akizungumza wakati wa uzinduzi huo uliofanyika jjini Dar es salaam




Mrembo wa singida aliyeshika nafasi ya tatu katika mashindano ya miss tanzania mwaka wa 2014 DORIS MOLEL leo amezindua rasmi rasmi DORIS MOLEL foundation ambayo ni mahususi kwa ajili ya kusaidia watoto ambao wamekuwa wanazaliwa wakiwa bado hawajatimia NJITI ambapo amewataka watu mbalimbali kujitokeza kumpa saport katika shighuli hiyo.

Uzinduzi huo ambao umefanyika leo jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi pamoja na wadau wanaohusika katika kuwasaidia watoto hao. wengi wamepongeza jitihada zinazoonyeshwa na mrembo huyo kwani watoto wanaozaliwa wakiwa na tatizo hilo wamekuwa wakusahaulika sana nchini tanzania jambo ambalo limetajwa kuwaadhiri watoto hao pamoja na wazazi wao.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mrembo DORIS ambaye ni mmoja  kati ya watu walioathiriwa na tatizo hilo (alizaliwa akiwa njiti) alisema kuwa ameamua kuwasaidia watoto na wazazi  wenye matatizo hayo baada ya yeye kupitia katika kipindi kama hicho ambapo alisema kunahitajika msaada mkubwa kutoka kwa watu wa mbalimbali.

Mimi nilizaliwa nikiwa njiti nilikuwa sijafikisha uzito halali wa kuzaliwa lakini nilizaliwa na mama akanisaidia hadi leo hii mnaniona hapa ni miss Tanzania na ni mtu nayekubalika na jamii,hivyo nimeona kuna haja ya kuwasaidia watoto kama mimi ambao wamezaliwa hivyo ili waweze kukua na afya njema na baadaye kutimiza malengo ya maisha yao,”alisema mrembo huyo.

Alisema kuwa baada ya kuchaguliwa kuwa mrembo namba tatu wa Tanzania alifikiria kitu cha kufanya ili arudishe shukrani kwa Watanzania na baada ya kutembea katika maeneo mbalimbali aligundua kuwa watoto wanaokumbwa na matatizo hayo bado wamekuwa hawapewi kipaumbele katika kusaidiwa jambo ambalo limemsukuma yeye kuanza kufanya mchakato huo.

Aidha alisema kuwa ipo haja ya serikali pamoja na wadau mbalimbali kuunga mkono jitihada hizo kwa lengo la kuokoa kizazi kikubwa ambacho kinazaliwa na matatizo kama hayo ambapo kwa takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya watoto laki mbili wanazaliwa wakiwa njiti kwa mwaka nchini Tanzania.

Uzinduzi huo uliambatana na  uchangiaji wa mfuko huo kwa ajili ya kuwasaidia watoto hao, ambapo watu mbalimbali wachangia na kuwaomba Watanzania wengine kuendelea kumsaidia mrembo huyo kuhakikisha kuwa anatimiza lengo lake.

Baadhi ya watu waliojitokeza kumpa nguvu katika shughuli hiyo leo ni pamoja na muandaaji wa mashindani ya miss tanzania ambapo ndiko mrembo huyo alikotokea bwana hashimu lundenga, Mwenyekiti mstaafu wa Bodi ya Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA) Mzee Iddi Simba, Naibu Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mohamed Thabit Kombo pamoja na viongozi mbalimbali kutoka Bara na Viusiwani




25 Mar 2015


Wiki mbili zilizopita niliandika makala iliyoonya tabia iliyoanza kuzoeleka kwa baadhi ya viongozi waandamizi wa CCM kufanya mzaha kuhusu ugaidi. Kwa muda mrefu sasa, viongozi wa chama hicho hususan Nape Nnauye na Mwigulu Nchemba wamekuwa wakiihusisha Chadema na ugaidi. Lakini tabia hiyo haikuanzia kwa Chadema pekee kwani huko nyumaCUF nayo ilikumbwa na tuhuma kama hizo kutoka kwa CCM.

Katika makala hiyo ambapo nileleza kwa kirefu kiasi kuhusu hatari inayoikabili dunia hivi sasa kutoka kwa vikundi vinavyoongoza kwa ugaidi kwa muda huu, yaani ISIS, Al-Qaeda, Boko Haram na Al-Shabaab, nilitahadharisha kwamba tabia ya CCM kuufanyia mzaha ugaidi, kwa maana ya kuzusha tu 'Chadema ni magaidi au CUF ni magaidi', inaweza kutugharimu huko mbeleni. Nilibainisha kuwa mzaha huo unaweza kuwarahisishia magaidi halisi dhima ya kushambulia nchi yetu, kwani 'tayari tuna magaidi wa ndani- kwa maana ya tuhuma za CCM dhidi ya Chadema na CUF.

Vilevile nilitanabaisha kwamba kuufanyia mzaha ugaidi kunaufanya uzoeleke, uonekane ni kama jambo la kawaida tu ambalo halikauki midomoni mwa akina Nape na Mwigulu.Lakini pengine baya zaidi ni vyombo vyetu vya dola kuwekeza nguvu kubwa kudhibiti 'magaidi hewa' hali inayoweza kuwapa upenyo magaidi halisi.

Kwa bahati mbaya, tahadhari niliyoitoa kwenye makala hiyo inelekea kubeba uzito, baada ya kupatikana taarifa kwamba kikundi hatari kabisa cha magaidi cha ISIS kina mpango wa kujienga na hatimaye kufanya mashambulizi katika ukanda wa Afrika Mashariki, ikiwa ni pamoja na Tanzania.

Kwa mujibu wa taarifa za kituo cha televisheni cha Aljaazera, mawasiliano ya hivi karibuni ya kikundi hicho cha kigaidi yanaonyesha kuwa kinajaribu kujijenga Afrika Mashariki, eneo ambalo limekuwa likisumbuliwa na magaidi wa Al-Shabaab na Al-Qaeda kwa vipindi tofauti.

Hivi karibuni, kikundi cha kigaidi cha Boko Haram cha Nigeria kimetoa ahadi ya utiifu kwa ISIS, hatua iiliyotafsiriwa na wachunguzi wa masuala ya ugaidi kuwa inaweza kuongeza nguvu za ISIS katika maeneo mbalimbali ya bara la Afrika.

Hata hivyo, kitu ambacho hakikufahamika kwa wengi ni kwamba tukio hilo la Boko Haram kuonyesha utii wa ISIS lilitanguliwa wiki chache kabla ya ujumbe uliotumwa kwa kiongozi wa Al-Shabaab , Abu Ubaidah, kumwomba afanye kama walivyofanya Boko Haram (kutangaza utii kwa ISIS)

Ujumbe huo uliwasilishwa na  Hamil al-Bushra, jina linaloaminika kutumiwa na vyanzo viwili vya habari vinavyohusishwa na ISIS.

Katika ujumbe huo, Bushra aliwapongeza Al-Shabaab na kuwahamasisha wafanya mashambulizi Kenya, Ethiopia na TANZANIA.

Soma habari kamili HAPA

12 Mar 2015

SIKU chache zilizopita, kikundi hatari cha kigaidi cha Boko Haram cha nchini Nigeria kilitangaza utiifu wake kwa kikundi kingine hatari kabisa cha kigaidi cha ISIS.
Hizi si habari njema hata kidogo kwani ushirikiano wowote kati ya makundi ya kigaidi, hususan, yaliyopo maeneo tofauti, unamaanisha kusambaa kwa vitendo vya kigaidi.
Ujumbe ulitolewa na Boko Haram, ambao hata hivyo bado haujathibitishwa (ni nadra kuthibitisha ujumbe wao ), uliwekwa kwenye akaunti ya kikundi hicho katika mtandao wa kijamii wa twitter, ambayo inaaminika kuwa ya kiongozi wa Boko Haram, Abubakar Shekau.
Kikundi hicho kilianza mashambulizi ya kigaidi mwaka 2009 maeneo ya Kaskazini mwa Nigeria, lengo kuu likiwa kuanzisha utawala unaoendeshwa kwa sheria za Kiislamu. Tayari kikundi hicho kimeshasababisha mauaji ya raia kadhaa, na hivi karibuni kimekuwa kikijaribu kusambaza unyama wake kwa nchi jirani za Cameroon, Niger na Chad.
Awali, ilifikiriwa kwamba Boko Haram ina mahusiano na kikundi kingine kikubwa na hatari cha Al-Qaeda, ambacho kilikuwa maarufu sana kabla ya kuibuka kwa ISIS.
Kwa upande wake, ISIS kimekuwa kikifanya unyama ambao pengine haujawahi kuonekana katika historia ya vikundi vya kigaidi, licha ya mashambulizi ya kujitoa mhanga, kikundi hicho kimeshawachinja mateka wake kadhaa na kuweka unyama huo hadharani.

Hivi karibuni, ilifahamika kuwa gaidi anayedaiwa kuwa ndiye ‘mchinjaji’ mkuu, anayejulikana kama Jihadi John, aliwahi kufika Tanzania na kuzuiliwa kuingia, kabla ya kuelekea Syria, ambako pamoja na Iraki, ni maeneo yanayosumbuliwa na kikundi hicho.
Lengo kuu la ISIS ni kuanzisha himaya (Caliphate) ya Kiislam, na kiongozi wake, Abu Bakr al-Baghdad, amejitangaza kuwa ndiye mkuu wa himaya hiyo ambayo wanalenga kuisambaza dunia nzima.

Kinachoifanya ISIS kuonekana hatari zaidi, licha ya unyama wake, ni uwezo wake mkubwa wa kifedha, sambamba na ufanisi wa kimuundo kana kwamba ni dola kamili yenye serikali.
Tangazo la Boko Haram kuahidi utiifu kwa ISIS si la kushangaza sana, japo wafuatiliaji wa masuala ya ugaidi walishangazwa kwanini hali hiyo haikutokea mapema zaidi, hasa ikizingatiwa kuwa mbinu na malengo ya vikundi hivyo yanashabihiana.

Huu ni mtihani mkubwa kwa wana-intelijensia duniani hasa ikizingatiwa kuwa ISIS, kama ilivyokuwa Al-Qaida, si tu imefanikiwa kuwavutia ‘wapiganaji’ kutoka sehemu mbalimbali duniani, bali pia ina dhamira kubwa ya kusambaza unyama wake takriban kila kona ya dunia.
Kwa tafsiri ya haraka, Boko Haram wanaweza kunufaika na ushirikiano wake na ISIS na pengine kufanikiwa kusambaza kampeni yao ya kigaidi katika maeneo mengine ya Afrika.
Lengo la makala hii sio kujadili vikundi hivyo vya kigaidi. Kilichonishawishi kuandika makala hii yenye utangulizi unaohusu vikundi hivyo vya ugaidi ni tamko la hivi karibuni la Katibu wa Uenezi na Itikadi wa CCM, Nape Nnauye kuwa kikosi cha ulinzi cha Red Brigade cha Chadema ni kundi la kigaidi.

Lakini Nape si mwanasiasa wa kwanza wa CCM kutoa tamko zito kama hilo. Mwaka juzi, Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho (Bara), Mwigulu Nchemba, aliandika waraka mrefu katika mtandao wa kijamii wa Jamii Forums kuizungumzia Red Brigade ya Chadema, ambapo pamoja na mambo mengine alidai ina malengo ya “uhaini, ni ugaidi, ni maandalizi ya kupindua nchi au kuvuruga kabisa amani tuliyonayo.”
Kwa upande wake, Nape alidai makundi ya vijana wa ulinzi vya chama hicho (Red Brigade) yameandaliwa kwa ajili ya kuingia msituni kwa shughuli za ugaidi. Alitoa kauli hiyo wilayani Mpwapwa kwenye ziara ya hivi karibuni ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, mkoani Dodoma.
“Chadema wanaandaa vijana kupitia Red Brigade ili kuingia msituni na kuchukua madaraka ya nchi kwa mabavu. Wanafanya hivyo kwa sababu wanajua hawawezi kuchaguliwa kwa njia ya kura wakati wa uchaguzi mkuu,” alidai mwanasiasa huyu muumini wa siasa za uhasama, na kuongeza kuwa, “Taarifa tulinazo ni kwamba Red Brigade ni vikosi vinavyoandaliwa kwa ajili ya vitendo vya ugaidi na shughuli nyingine za ovyo. Taarifa ni kwamba hili ni kundi la kigaidi, wataanzishaje kundi la usalama wakati tunavyo vyombo vya ulinzi na usalama wa nchi yetu?”
Huu ni uhuni wa kisiasa. Na baya zaidi, ni mwendelezo wa kasumba ya muda mrefu kwa Nape na Mwigulu kuufanyia mzaha ugaidi kwa kuvihusisha vyama vya upinzani hususan Chadema.
Lakini kabla ya kuwajadili wanasiasa hawa wawili ‘wanaaombea uwepo wa ugaidi nchini mwetu,’ ni vema kutambua kuwa kamwe kauli zao hazijawahi kupingwa na Mwenyekiti wa Taifa wa CCM, Rais Jakaya Kikwete au kiongozi mwingine yeyote yule wa chama hicho tawala. Wakati Julai mwaka, Rais Kikwete alisema si sahihi kwa vyama vya siasa kuanzisha vikundi vya mgambo kwani vitendo hivyo ni viashiria vya uvunjifu wa amani nchini, chama anachokiongoza (CCM) pia kina kikundi cha Green Guard, kama ilivyo Blue Guard kwa CUF.
Kwa maana hiyo, kwa Nape na Mwigulu kukemea Red Brigade ya Chadema ilhali CCM nayo ina Green Guard si tu ni unafiki bali pia wanaweza kuwa wanatumika kama ‘kipaza sauti’ cha Rais Kikwete na CCM kwa ujumla.

Lakini sote tunafahamu siasa zetu za upinzani zilivyo ambapo ‘kurushiana madongo’ ni sehemu ya kawaida. Hata hivyo, jaribio lolote la kuhusisha ugaidi na ‘madongo’ ya kawaida litatugharimu kama taifa. Ugaidi si jambo la kufanyia mzaha hata kidogo.
Moja ya madhara ya kuufanya ugaidi kama jambo la kawaida ni kuwarahisishia magaidi halisi fursa ya kutudhuru. Hivi, kwa mfano, magaidi tulio jirani nao zaidi kuliko Boko Haram, ISIS na Al-Qaeda, yaani Al-Shabaab wa Somalia, wakitaka kufanya ugaidi nchini mwetu (Mungu aepushie) hawawezi kutumia upenyo wa ‘Red Brigade wa Chadema ni magaidi’ kuficha dhamira yao ovu?
Vyombo vyetu vya usalama vinaweza kulazimika kuwekeza nguvu kubwa kuwadhibiti ‘magaidi wa kufikirika’ wa Red Brigade, na hiyo yaweza kutoa fursa kwa magaidi halisi kufanya unyama wao.
Tayari tumeshaona jinsi vyombo vya usalama vinavyotumia nguvu kubwa kulinda maslahi ya CCM, ikiwa ni pamoja na kuwakandamiza wapinzani wake, huku ufisadi, ujangili, biashara ya madawa ya kulevya, na sasa mauaji ya albino vikistawi kana kwamba ni shughuli halali.
Kichekesho, majuzi wakati Rais Kikwete anazindua studio za kituo cha Televisheni cha Azam jijini Dar alitoa karipio kali kwa vyombo vya habari akisema serikali haitavumilia vyombo vya habari visivyosimamia uadilifu, weledi pamoja na kutumika katika kuchochea ghasia. Kwanini ukali huo wa Rais wetu uwe kwa vyombo vya habari tu ilhali wahuni wa kisiasa wakiruhusiwa kufanyia mzaha tishio la ugaidi?

Nimalizie makala hii kwa kuwahamasisha Watanzania wenzangu kuwapuuza wanasiasa mufilisi wanaojaribu si tu kujenga chuki miongoni mwetu bali pia kufanyia mzaha tishio la ugaidi.
Sote ni mashuhuda wa unyama unaofanywa na Boko Haram, ISIS, Al-Qaeda, Al-Shabaab na makundi mengine ya kigaidi, na ninaamini hakuna mtu anayeweza kudiriki kutamani uharamia huo utokee katika nchi yetu. Siasa za chuki za kipuuzi ni hatari sana kwa mustakabali wa Tanzania yetu.
Inahitaji kauli chache tu za kupandikiza mbegu za chuki, lakini ni vigumu mno kung’oa chuki pindi mbegu hizo zikifanikiwa kuotesha chuki.

10 Mar 2015

Tafsiri: Mimi sishangazwi hata kidogo. Viongozi wa Kanisa na wanasiasa wakubwa wanashiriki katika mila hii ya kishetani. Kiongozi mmoja mkubwa wa kanisa mwenye usharika mkubwa jijini Dar es Salaam, anayemiliki benki, alikamatwa akiwa na albino amefungwa nyuma ya gari lake. Alitoroka eneo la tukio na kesi yake haikuripotiwa kwa sababu alitoa rushwa. Yeye pia ni muuza madawa ya kulevya mkubwa na mtakasaji fedha haramu. Kwahiyo tunatarajiwa Umoja wa Mataifa utaanza kuwafungulia watu hawa mashtaka ya ukatitili dhidi binadamu ili Watanzania walichukulie suala hili kwa makini.

Kwa umoja wetu na upendo wetu kwa ndugu zetu albino, tuunganishe kumsaka mwanaharamu huyu anayejiita mchungaji ilhali anafanya matendo ya kishetani. 

Mie ni muumini katika nguvu ya umma. Na nguvu ya umma si kuandamana tu bali hata katika kufichua maovu katika jamii. Ni na imani ya asilimia 100 kuwa kuna mtu au watu flani, sehemu flani wanamfahamu 'mchungaji' huyu. Kadhalika ninaamini kuna mtu au watu flani wanamfahamu mwanasiasa au mfanyabiashara au mganga au muuaji anayejihusisha na mauaji ya albino. Sasa pengine hofu ya kumripoti inachangiwa na kuchelea matokeo hasa ikizingatiwa kuwa polisi wetu hawaaminiki.

Tutumie nguvu ya umma. Kama una taarifa ya uhakika (ikiwa na uthibitisho itakuwa vema zaidi) basi ninaomba uwasiliane nami kwa barua-pepe CHAHALI at ABOUT dot ME au nitumie meseji Facebook https://www.facebook.com/evarist.chahali.1 au nenda kwenye tovuti hii http://swarmsecret.com/ kisha tweet kwa @chahali nami sio tu nitaweka hadharani suala hilo bali nitatumikia kila tone la nguvu zangu kuhakikisha mtu huyo anachukuliwa hatua za kisheria, ndani au nje ya Tanzania yetu.

Vinginevyo, ukifanikiwa kupata taarifa za mchungaji huyo au mtu yeyote anayejihusisha na unyama huo, 

Kwa pamoja tunaweza katika hili

SHUKRANI: Asante Ndugu Alfred Kiwuyo kwa kutufahamisha kuhusu habari husika

5 Mar 2015

"NI wajinga wa kisiasa pekee wanaoweza kudharau mchango wa Marehemu Komba katika siasa za Tanzania. Nimeona kuna watu wanabwabwaja sana!" Hii ni kauli ya Profesa Kitila Mkumbo aliyoitoa Jumapili iliyopita, katika mtandao wa kijamii wa Twitter.
MSOMI huyo ambaye pia ni mwanasiasa alitamka hivyo kufuatia mpasuko mkubwa uliojitokeza (angalau katika mtandao wa intaneti) kufuatia taarifa za kifo cha mwanasiasa maarufu na Mbunge wa Mbinga Magharibi (CCM) Kapteni John Komba, kilichotokea Jumamosi jijini Dar es Salaam.
Japo inafahamika kwa idadi ya Watanzania wanaitumia mtandao wa intaneti ni ndogo sana kulinganisha na idadi ya Watanzania wote, kwa kiasi fulani mada zinazotawala mtandaoni huweza kuakisi hali halisi iliyopo 'mtaani.' Ni kwa mantiki hiyo, ninashawishika kuhisi kuwa mpasuko uliojitokeza mtandaoni kufutia kifo cha Kapteni Komba waweza pia upo mitaani pia.
Mpasuko huo ulichukua sura ya makundi mawili, moja likionekana kufurahia kifo cha mwanasiasa huyo huku likifanya marejeo ya kauli zake mbalimbali hasa ile ya wakati wa Bunge Maalum la Katiba kuwa angeingia msituni iwapo pendekezo la muundo wa Muungano wa serikali tatu lingepitishwa.
Kundi jingine lilikuwa la waombolezaji, wananchi walioguswa na kifo hicho, huku wakilaani vikali 'jaribio lolote la kumlaumu marehemu.' Katika kundi hili, kulijitokeza 'mapadri na mashehe' walionukuu Biblia Takatifu na Kuran Tukufu kukumbushia umuhimu wa kuenzi marehemu na kuheshimu kifo.
Lakini ndani ya makundi hayo kulijitokeza 'waliouma na kupuliza,' yaani kwa upande mmoja wakionyesha jinsi walivyokwazwa na baadhi ya kauli za marehemu Komba hususani zilizokua zinachochea chuki na uhasama wa kisiasa na kijamii, lakini upande mwingine wakidai kuwa 'si vizuri kumsema vibaya marehemu.'
Kama nilivyotanabaisha hapo juu, sina hakika hali ikoje huko mitaani lakini yayumkunika kuhisi kuwa idadi ya waombolezaji ni kubwa kuliko ya 'wanaomwandama marehemu.' Idadi kubwa ya waombolezaji yaweza kusababishwa zaidi na 'uoga wetu wa kawaida kwa kifo' kuliko kuguswa na kifo husika.
Japo sote twatambua kwa uhai wetu una kikomo kwa njia ya kifo, na japo hatuna la kufanya kubadili ukweli huo mchungu, twaendelea kukiogopa kifo huku vifo vya watu wa karibu au tunaowafahamu vikitukumbusha tena na tena kuwa kifo kipo.
Kwa namna flani ya kusikitisha, kuna nyakati vifo huwa nafasi ya kushuhudia unafiki wa baadhi yetu kama wanadamu. Ni mara ngapi tumeshuhudia, kwa mfano, baadhi ya vijana wakiteketeza uhai wao kwa matumizi ya madawa ya kulevya, lakini jamii ikiwatelekeza, na kisha kumwaga lundo la rambirambi pale wanapofariki? Sawa, rambirambi ni ishara ya kuguswa na kifo, lakini ina faida gani hasa pale upendo ungeweza kuepusha kifo hicho?
Kwa upana zaidi, kuna haja gani kumpenda mtu baada ya kufariki ilhali alipokuwa hai alichukiwa? Upendo huo wa ghafla ni nini zaidi ya unafiki kwani wakati mwafaka tunapohitaji upendo ni tunapokuwa hai.
Kilichojitokeza baada ya kifo cha marehemu Kapteni Komba, ambapo baadhi ya wenzetu wameonekana 'kufurahia,' ni mwendelezo wa chuki katika Tanzania yetu, huku baadhi ya wanasiasa wa CCM wakiwa ndio wahusika wakuu.
Sawa, sio vema kuzungumzia 'mabaya' ya marehemu Komba, kwa mfano, lakini kwa bahati mbaya au makusudi, ukiweka kando umahiri wake katika nyimbo za maombolezo ya kifo cha Baba wa Taifa, marehemu Julius Nyerere, kumbukumbu muhimu ya hivi karibuni ni lugha kali aliyoitumia wakati wa Bunge Maalum la Katiba.
Yeye, pamoja na 'waeneza chuki' wengine walifikia hatua inayoweza kutafsiriwa kama kumtakia kifo Jaji Joseph Warioba kwa vile tu Tume aliyoongoza kukusanya maoni ya Katiba ilipendekeza muundo wa Muungano wa serikali tatu.
Lakini ishara kuwa chuki inazidi kutawala katika Tanzania yetu zilianza kujitokeza kwa wazi zaidi pale Rais Jakaya Kikwete alipolazwa nchini Marekani kwa matibabu ya tezi dume. Wakati idadi kubwa tu ya Watanzania ilijitokeza kumtakia Rais wetu uponyaji wa haraka, kulikuwa na kundi dogo ambalo halikuficha hisia zao, kiasi cha baadhi yao kutaka Rais asirudi akiwa hai. Kwa lugha nyingine, wenzetu hawa walikuwa wanamwombea kifo Rais wao.
Kwa bahati mbaya au makusudi, hakuna jitihada zilizofanyika japo kuanzisha mjadala tu kuhusu ustawi wa chuki katika nchi yetu. Na matokeo yake, leo hii twashuhudia baadhi ya wenzetu wanaoonekana kufurahia kifo cha mwanasiasa wetu mahiri.
Ni rahisi kuitazama chuki hii kama ujinga, kama alivyotanabaisha Profesa Kitila, lakini binafsi ninaamini hili ni swali gumu lisilostahili majibu rahisi. Kwa mtizamo wangu, moja ya sababu za chuki hiyo inaweza kuwa ni pengo la kitabaka kati ya watawala na watawaliwa, sambamba na pengo linalozidi kukua kati ya wenye nacho na wasio nacho.
Lakini chuki hiyo inachangiwa pia na jeuri ya watawala wetu, kusahau kuwa 'kesho kuna kifo,' kuropoka kila baya hasa kwa wapinzani wao kisiasa, na kuwadharau wananchi ambao kimsingi ndio waajiri wa watawala hao.
Kauli za baadhi ya wanasiasa mahiri kwa 'kusema ovyo' kama ile ya 'vijisenti' ya Mbunge wa Bariadi (CCM) Andrew Chenge, hii ya majuzi ya 'shilingi milioni 10 za kununulia mboga (labda ni tembo mzima)' ya Profesa Anna Tibaijuka, ile ya Profesa Muhongo kuwa 'Watanzania hawawezi kuendesha biashara ya gesi na mafuta bali wanamudu biashara ya matunda tu,' na nyinginezo nyingi, zinachangia kushamiri kwa hasira za baadhi ya wananchi kwa baadhi ya viongozi wao.
Tuna wanasiasa kama LivingstonLusinde, maarufu kama 'kibajaji’, Nape Nnauye, William Lukuvi, Stephen Wassira na Mwigulu Nchemba (japo huyu amekuwa na nafuu sasa), ambao wakizungumzia vyama vya upinzani wanaweza kumwaminisha msikilizaji kuwa wapinzani ni viumbe hatari kuliko magaidi wa Al-Shabaab, Boko Haram au ISIS.
Wanajitahidi sana kupamba mbegu za chuki, na kwa hakika wamefanikiwa kwa kiasi fulani. Lakini uongozi wa juu wa chama hicho tawala haujawahi kukemea kauli hizo za chuki, yayumkinika kuhisi kuwa ujenzi wa chuki ni miongozi wa sera zisizo rasmi kwa chama hicho, kama ilivyo ufisadi.
Ni muhimu kwa watawala wetu kujifunza kitu katika chuki hii inayolitafuna taifa letu. Kinachotufanya tuendelee kumlilia Baba ya Taifa hadi leo ni matendo yake ya kuigwa mfano wakati wa uhai wake.
Yawezekana kama binadamu mwingine, Mwalimu aliwahi kuwakwaza baadhi ya Watanzania, lakini 'hukumu ya jumla' kwa matendo yake wakati wa uhai wake ni kwamba aliweka mbele maslahi ya taifa kuliko maslahi yake binafsi. Tunamkumbuka na kumlilia kwa sababu tunaona ombwe kubwa lililotokana na kifo chake.
Sasa, japo 'marehemu hasemwi vibaya,' sidhani kama kuna atakayeshangaa sana kuona kifo cha mwanasiasa mahiri kwa matusi, vijembe, mipasho na mambo mengine mabaya kikipelekea furaha katika sehemu flani ya jamii. Ndio, dini zetu zinasisitiza kuwaenzi marehemu, lakini dini hizo pia zinasisitiza umuhimu wa heshima wakati wa uhai wetu.
Na pia licha ya ukweli si kila Mtanzania ni mcha-Mungu, wingi wa wacha-Mungu katika nchi yetu umeshindwa kuzuwia mauaji ya albino, ufisadi na 'dhambi'nyingine lukuki.
Nimalizie makala hii kwa kutoa salamu zangu za rambirambi kwa familia ya marehemu Kapteni Komba, ndugu, jamaa, marafiki na Chama Cha Mapinduzi kwa ujumla.
Njia mwafaka ya kumwenzi marehemu ni kudumisha mema yake, na kujifunza katika mapungufu yake. Kadhalika, kifo hiki kinapaswa kutuamsha na kuanza mjadala wa kitaifa kuhusu kudidimia kwa upendo, umoja na mshikamano wetu.
Mwenyezi Mungu aipumzishe roho ya marehemu Kapteni Komba mahala pema peponi. Yeye ametangulia tu, sote twaelekea huko.

26 Feb 2015

Tanzania Tanzania, nakupenda kwa moyo wote,

Nchi yangu Tanzania, jina lako ni tamu sana
Nilalapo nakuwaza wewe, niamkapo ni heri mama wee
Tanzania Tanzania, nakupenda kwa moyo wote.”


Huu ni ubeti wa wimbo maarufu ambao ‘zamani hizo’ tulipouimba tulijisikia ‘raha’ flani kuhusu nchi yetu. Tulikuwa na kila sababu za kuipenda Tanzania kiasi cha kuiota tulipolala.
Peleka mbele (fast-forward) hadi zama hizi tunaoishi, hutolaumiwa ukijiuliza ‘ninaipenda Tanzania kwa lipi hasa, maana kila kukicha tunakumbana na habari au matukio yanayoweza kumfanya mtu amlaumu Muumba kwa kumfanya azaliwe katika nchi yetu.

Tuweke kando ufisadi unaokurupuka kila kukicha, tusahau kuhusu wawakilishi wetu wanaotugharimu mamilioni ya shilingi kila mmoja kwa mwezi kisha wakifika bungeni inakuwa ni matusi, vijembe, na upuuzi kama huo. Tufumbie macho nchi yetu inavyouzwa rejareja kwa kisingizio cha uwekezaji huku baadhi ya wawekezaji hao wakija na briefcase tupu na kuondoka na mabilioni. Na tusamehe aibu ya kugeuka ombaomba wa kimataifa huku Rais wetu akiwa ziarani nje mara kwa mara kwa ‘kisingizio’ hicho.

Twaweza kuweka kando kila jambo ‘baya’ kuhusu Tanzania yetu lakini haiwezekani kabisa kupata kisingizio katika unyama wa hali ya juu unaoendelea nchini mwetu dhidi ya ndugu zetu maalbino. Kinachofanywa kwao si dhambi tu bali ni aibu kubwa kwa taifa letu.
Majuzi tu rafiki yangu mmoja hapa Uskochi aliniuliza, “Evarist, hivi asili yako ni Zimbabwe au Tanzania?” Nami bila uoga nilimjibu kuwa ninatokea Tanzania. Kisha likafuata bomu, “Nimeona kipindi flani kwenye televisheni kinaonyesha jinsi maalbino wanavyouawa Tanzania kwa imani kuwa viungo vyao vinaleta utajiri. Ni kweli?” Nilipatwa na mchanganyiko wa aibu na hasira. Aibu kwa sababu nchi yangu inaonekana kuwa na viumbe wa ajabu kabisa wanaomudu kudiriki unyama huo. Pia nilipatwa na hasira kwa sababu ni ukweli usiopingika kuwa laana ya mauaji ya albino limeachwa kustawi kana kwamba uhai wa Watanzania wenzetu maalbino hauna thamani.

Wiki iliyopita, vyombo vya habari huko nyumbani viliripoti kuhusu tukio la kusikitisha ambapo maiti ya mtoto albino, Yohana Bahati, aliyetekwa tarehe 15 mwezi huu, uliokotwa ukiwa umekatwa miguu na mikono. Taarifa ya mauaji ya kinyama ya mtoto huyo asiye na hatia yoyote imesambaa sehemu mbalimbali duniani huku vyombo vya habari vya kimataifa vikiipa uzito mkubwa.

Aibu gani hii kwa nchi inayojigamba kuwa ni ‘kisiwa cha amani na utulivu’ huku ikitumia mabilioni ya shilingi katika kampeni za kimataifa kutangaza vivutio vyetu?

Kwa bahati nzuri, Watanzania wengi hususan kwenye mitandao ya kijamii wameonekana kuguswa mno na unyama huu kiasi cha kupelekea kampeni ya ‘Stop Albino Killings.’ Katikati ya wiki iliyopita, kampeni hiyo ilivuma katika mtandao wa kijamii wa Twitter hadi kufanikiwa kufikisha ‘impressions’ zaidi ya milioni moja.

Cha kusikitisha, hadi wakati ninaandika makala hii, Rais Jakaya Kikwete ambaye akaunti yake ya Twitter imerejea hewani baada ya kupotea kwa siku kadhaa, ameshindwa kujumuika na Watanzania lukuki pamoja na watu wengine duniani, kuunga mkono kampeni hiyo.
Na kana kwamba ni chama anachoongoza Rais Kikwete, CCM, kimeona suala hilo ni mzaha flani wa kupuuzwa, licha ya kutounga mkono kampeni hiyo, Jumapili iliyopita kiliweka bandiko katika mtandao huo kikijigamba kuwa, ninanukuu, “Tumeendelea kuimarisha vyombo vya ulinzi na usalama kulinda amani na utulivu...” Haya ni matusi. Amani na utulivu gani ilhali Watanzania wenzetu albino wanachinjwa kinyama zaidi ya kuku (maana tunapochinja kuku hatumkati mikono, mguu au kucha zake hadi muda wa matayarisho ya kumpika)?

Kadhalika, katika hali inayoweza kutafsiriwa kama serikali yetu kupuuza mauaji ya albino , hakuna kiongozi yeyote wa ngazi za juu wa serikali aliyeona umuhimu wa kushiriki katika mazishi ya mtoto Yohana. Siku alipozikwa, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alikwenda kuhani msiba wa chifu mmoja huko Iringa. Hivi hata tukiweka kando protokali, serikali ilishindwa kumtumia japo Waziri mmoja kumwakilisha Rais Kikwete?

Binafsi, pamoja na nyingi ya ‘tweets’ zangu wiki iliyopita za kuhamasisha kampeni hiyo inayoandikwa #StopAlbinoKillings, pia nilitanabaisha kuwa mauaji hayo ya albino ni zaidi ya suala la kisheria bali la kibinadamu. Nilisema hivyo kwa sababu, kwa upande mmoja, sheria dhidi ya ukiukwaji wa haki za binadamu na za mauaji zipo lakini hazijatumika ipasavyo kukabiliana na tatizo hilo, na kwa upande mwingine, hata pale sheria zinapofanya kazi ipasavyo, hazimaanishi kuwa zitamaliza kabisa uhalifu flani. Hata hivyo, sheria zikitumika ipasavyo huwezi japo kwa kiasi flani kukwaza uhalifu (deterrence).

Wakati matukio ya mauaji ya kinyama ya albino yakiendelea huko nyumbani, mwezi uliopita serikali ilipiga marufuku waganga wa kienyeji sambamba na kupiga marufuku wapiga ramli wote ambao wanaelezwa kuchangia mauaji ya watu hao wenye ulemavu wa ngozi. Haihitaji ujuzi wa kuchambua matamko ya serikali kumaizi kuwa amri hiyo ilikuwa ni porojo kama zilivyo porojo nyingine kuhusu ufisadi, ujangili, madawa ya kulevya, nk.

Lakini pia ni muhimu kujiuliza, kwanini mauaji ya albino yamekuwa yakiongezeka kila tunapokaribia uchaguzi mkuu. Katika mazingira ya kawaida tu ni rahisi kutambua kuwa baadhi ya wanasiasa wetu ni wateja wa waganga wa kienyeji wanaotoa masharti ya kupatiwa viungo vya albino ili ‘kuwasafishia mambo’ wanasiasa hao.

Na katika suala hilo linalohusiana na ushirikina, nina mifano miwili hai. Nina ndugu yangu kiukoo ambaye ni mganga huko wilayani Kilombero. Wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, mmoja wa wagombea urais alilala katika makazi ya mganga huyo ili ‘kutengenezwa’ kwa ajili ya uchaguzi huo.

Kadhalika, wakati huohuo, mmoja wa watendaji wakuu wa taasisi moja nyeti alikumbwa na kashfa ya kuajiri waganga wa kienyeji ili wamsaidie kupata ukurugenzi mkuu. Japo hakufanikiwa katika azma yake hiyo, mtendaji huyo kwa sasa ni mwakilishi wetu katika nchi moja jirani.

Mifano hiyo hai inaonyesha ni kwa jinsi gani imani za kishirikina zilivyoota mzizi katika Tanzania yetu. Na suala la ushirikina si kwa wanasisasa au ‘vigogo’ wengine pekee kwani wakazi wengi wa jiji la Dar es Salaam, kwa mfano, wanafahamu kuhusu misururu ya magari inayoelekea Mlingotini hasa mwishoni mwa wiki katika kinachoaminika kwenda kutafuta huduma za waganga wa kienyeji.

Nilipokuwa mwanafunzi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam nilisoma Sosholojia ya Dini ambapo pamoja na mambo mengine tulifundishwa kuhusu imani za asili. Kimsingi, kabla ya ujio wa ‘dini za kimapokeo’ yaani Uislam na Ukristo, ‘dini’ kuu ilikuwa imani za asili. Takriban kila jamii ilikuwa na wataalamu wa tiba, ambao kwa mazingira ya sasa ni sawa na waganga wa asili. Uji0 wa dini za kimapokeo haukufanikiwa kuondoa imani za asili, lakini ‘kwa bahati mbaya’, wakati utabibu wa asili zama hizo ulilenga katika kutatua ya mtu binafsi, ‘mabadiliko’ katika fani hiyo yalipelekea ‘matibabu’ hayo kujumuisha kudhuru watu wengine.

Kwa mujibu wa maelezo ya ndugu yangu anayejishughulisha na uganga wa jadi huko wilayani Kilombero, kuna waganga wanaozingatia ‘asili ya fani hiyo’ ambao kamwe hawakubali kufanya tiba za kumdhuru mtu. Hata hivyo, alinieleza kuwa kutokana na ukosefu wa maadili, tamaa na ugumu wa maisha, idadi kubwa ya waganga sio tu ‘wanadhuru walengwa’ bali pia hutumia dawa zinazotokana na madhara kwa binadamu, kwa mfano viungo kama hivyo vya albino.

Tufanyeje? Ni vigumu kupata ufumbuzi mwepesi kwa tatizo hili kubwa. Amri ya serikali kupiga marufuku waganga wa kienyeji na ramli ni ya kipuuzi, kwa sababu kama serikali hiyohiyo inashindwa kuwadhibiti mafisadi wanaokwapua mabilioni sehemu kama Benki Kuu penye CCTVs lukuki itawezaje kuwabana waganga na wapiga ramli wanaofanya shughuli zao kwa siri?

Binafsi, kama nilivyobainisha awali, ufumbuzi wa tatizo la mauaji ya albino ni wapaswa kuwa wa kibinadamu (humanity) zaidi kuliko kisheria (legislative). Wanunuzi wa viungo vya albino twaishi nao katika jamii zetu, kama ilivyo kwa wahalifu wanaiwinda na kuuwa ndugu zetu hao. Kadhalika, waganga wanaotumia viungo vya binadamu twaishi nao katika jamii zetu. Kinachohitajika ni kuweka mbele ubinadamu wetu ili kuwadhibiti maharamia hao.

Japo serikali ina jukumu la msingi la kuhakikisha usalama wa raia wake, na Katiba yetu inasisitiza umuhimu wa haki ya kuishi, sote twafahamu kuhusu uzembe wake katika masuala yanayohusu ‘wanyonge.’ Mazingira tu wanayoishi watawala wetu ni kinga tosha kwao na jamaa zao kudhuriwa na wanaiwinda viungo vya binadamu. Na taarifa kwamba baadhi ya wanasiasa na ‘vigogo’ wengine ni wateja wa waganga wanaohitaji viungo vya albino zinafanya utegemezi kwa serikali kuwa ‘kazi bure.’

Nimalizie kwa kuhamasisha wakazi wa jiji la Dar kujitokeza kwa wingi katika maandamano yanayotarajiwa kufanyika hivi karibuni kulaani mauaji ya albino na kushinikiza hatua kali kuchukuliwa dhidi ya wahusika. Sambamba na hilo, ninashauri maandamano hayo yafanyike nchi nzima ili kufikisha ujumbe kuwa hatuwezi kuvumilia mateso na mauaji kwa ndugu zetu albino.

Na kwa Watanzania wanaotumia mitandao ya kijamii, ninawasihi waendelee kutumia ‘hashtag’ #StopAlbinoKillings angalau mara moja kwa siku.

#StopAlbinoKillings (Zuwia Mauaji ya Albino)

19 Feb 2015


WIKI iliyopita kuliibuka video ‘ya kutisha’ ambayo msemaji katika video hiyo alidai kuwa yeye na wenzake ni kundi ambalo limekuwa likivamia vituo vya Polisi na kupora silaha.
Kadhalika, msemaji huyo ambaye licha ya kujitambulisha kama Abu (magaidi wengi hupendelea jina hilo japo si kila Abu ni gaidi) hakubainisha jina la kikundi chake.


Vilevile, msemaji huyo aliyeficha sura yake kwa kifunika-uso (balaclava) na miwani nyeusi ya jua (sunglasses) alidai kuwa kundi lake limefanikiwa kupora silaha katika vituo vya Polisi huko Ushirombo, Ikwiriri na Tanga, na walifanya hivyo pasipo kutumia silaha yoyote.
La kuogofya zaidi, msemaji huyo alidai kwamba tayari wana mtaji wa ‘roho tano za polisi,’ akimaanisha wameshauwa polisi watano.


Japo nina ujuzi wa wastani tu kuhusu masuala ya ugaidi, zaidi kwa kufuatilia habari zinazohusu suala hilo na harakati za vikundi vya kigaidi duniani, nikiri kwamba nilipoiona video hiyo kwa mara ya kwanza niliamini. Sababu kubwa ya kuiamini ni kwamba tishio lililomo kwa video hiyo lilionekana halisi.


Hata hivyo, baada ya kuiangalia mara kadhaa, nilijikuta nikipatwa na maswali kadhaa. Miongoni mwa maswali hayo ni:


Kwanini msemaji anaonekana kama anafikisha ujumbe kwa Inspekta Jenerali wa Polisi ‘kwamba hawezi kazi’ kwa vile ameshindwa kuwakamata ‘magaidi’ hao? Kwa uchambuzi wa haraka, katika hilo ni kama ‘magaidi’ hao wana lengo la kumchafua tu IGP.


Katika video hiyo, ‘magaidi’ hao wanamtaja Rais kwa kumuita ‘Mheshimiwa Rais.’ Hii si lugha ya kawaida kwa magaidi halisi.Kwa sababu pamoja na mambo mengine, malengo yao huendeshwa na chuki kwa utawala uliopo madarakani. Licha ya kumuita Rais ‘Mheshimiwa,’ msemaji anaonekana kumshawishi ‘Mheshimiwa Rais’ kuwa hana polisi, na kwamba hawajaona jeshi dhaifu kama la polisi. Hapa tena inaonekana lengo la msemaji au kikundi hicho ni kulichafua jeshi la polisi.

Ni kawaida kwa vikundi vya kigaidi wanapotoa tishio kama hilo la kwenye video hiyo kutaja madai yao. Labda kama video hiyo ni mwanzo wa mfululizo wa video, ingetarajiwa msemaji huyo kueleza kuwa lengo lao ni nini na madai yao ni yapi.
Linaloshabihiana na hilo ni video hiyo kutotajwa mlengwa wa ‘hasira’ zao ni nani. Pamoja na msemaji kutumia maneno ya Kiarabu na kutamka ‘ujumbe kwa vijana wa Kiislamu’, hakuna mahala katika video hiyo ambapo wanazungumziwa wasio- Waislam (kwa mfano Wakristo) wala serikali au taasisi zake au taasisi binafsi au mtu/kundi la watu.
Pamoja na maswali hayo, haimaanishi kuwa ujumbe huo ni wa ‘kizushi’ tu. Kama nilivyeoeleza awali, tishio lililomo katika video hiyo linaonekana kuwa halisi. Tatizo ni katika uwasilishaji wake kama nilivyoonyesha hapo juu. Hata hivyo, kasoro hizo zaweza kuwa ni za kiufundi tu.
Kinachochanganya zaidi ni ukweli kwamba takriban siku moja baada ya kuibuka video hiyo, zilipatikana habari za mapambano makubwa kati ya jeshi la polisi likisaidiwa na Jeshi la Wananchi (JWTZ) na kikundi kimoja kwenye Mapango ya Amani huko Tanga.
Mkanganyiko zaidi ni kuhusu utambulisho wa kikundi hicho. Wakati baadhi ya vyombo vya habari vimeliita kundi hilo ‘magaidi wa Al-Shabaab,’ vingine vimedai ni kikundi chenye uhusiano (affiliated) na magaidi hao wa Somalia, huku vyombo vingine vya habari vikieleza kuwa kundi hilo ni genge tu la wahuni (thugs), kama maelezo ya Kamanda Chagonja wa polisi yalivyotanabaisha.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana katika vyombo mbalimbali vya habari, baadhi ya wakazi wa eneo husika wamedai kuwa kundi hilo ni la kigaidi, huku wakililaumu jeshi la polisi kwa kuficha ukweli, na kuhoji iweje nguvu kubwa kiasi hicho itumike kukabiliana na genge la wahuni tu.
Taarifa zinadai kuwa polisi mmoja aliuawa katika mashambulio hayo na wengine kadhaa kujeruhiwa. Hata hivyo, Kamanda Chagonja alinukuliwa akidai kuwa ‘wahuni’ hao walifanikiwa kutoroka.
Wakati kiongozi huyo mwandamizi wa jeshi la polisi akieleza kuwa genge hilo si la magaidi, huhitaji uelewa wa fani ya uchunguzi wa kipelelezi kujiuliza “amejuaje ilhali hawakufanikiwa kumkamata japo mhusika mmoja wa kundi hilo?”
Nadhani moja ya matatizo ya mwanzo kabisa katika sakata hili la Amboni na lile la video ya ‘magaidi’ ni ukweli kwamba jeshi la polisi haliaminiki kabisa na linachukiwa na Watanzania wengi.
Sababu za kuchukiwa zipo wazi; ukiukwaji wa hali ya juu wa haki za binadamu, sambamba na ukandamizwaji demokrasia kwa uonevu wa waziwazi dhidi ya vyama vya upinzani na viongozi na wanachama wao, pamoja na rushwa iliyokithiri ndani ya chombo hicho cha dola, kama ilivyothibitishwa na utafiti mmoja wa hivi karibuni.
Hadi wakati ninaandika makala hii kumeshajitokeza madai kuwa matukio hayo mawili ni mkakati wa jeshi la polisi kuandaa mazingira ya kuvibana vyama vya upinzani. Baadhi ya watu wanadai kuwa jeshi la polisi linaweza kuwa linaandaa mkakati wa kupiga marufuku shughuli za kisiasa za wapinzani, kama vile mikutano ya hadhara na maandamano, kwa kigezo cha ‘tishio la ugaidi.’
Baadhi ya wananchi wanayahusisha matukio hayo na ‘hadithi’ ya aliyekuwa Mkuu wa Jeshi hilo, IGP Omari Mahita, alipotoa tuhuma nzito siku moja kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 kuwa chama cha CUF kimeingiza makontena ya visu na majambia kwa minajili ya kuvuruga uchaguzi huo.
Pengine kilichonichekesha wakati ninatafakari kuhusu matukio haya mawili, ni bandiko la mwanachama wa mtandao mahiri wa kijamii, Jamii Forums, aliyehitimisha kuwa, ninamnukuu, “Chagonja na sinema ya mwaka: Unajivamia, unajiteka, unajitorosha, unajisaka, na hatimaye unatangaza kujitafuta kwa udi na uvumba. Matukio yote haya hayana majina ya waathirika. Kweli siasa zimefika mahali pake. Tutashuhudia mengi 2015”
Huwezi kuwalaumu wanaohisi matukio hayo mawili ni ‘mchezo mchafu tu’ hasa ikizingatiwa kuwa licha ya polisi kutoaminiwa na kuchukiwa, chama tawala CCM ni mahiri kwa ‘uzushi’ dhidi ya wapinzani wake.

Ninaamini wengi mwakumbuka kuhusu tuhuma lukuki dhidi ya Chadema, kutoka chama cha Kikristo, cha Wachagga, na hatimaye cha kigaidi. Tumeshuhudia pasi aibu CCM ikijaribu kuwahusisha wapinzani na maafa yaliyofanywa na jeshi la polisi, hadi kufikia hatua ya kudai kuwa Chadema ndio waliomuuwa mwandishi Daudi Mwangosi aliyeuawa kikatili na jeshi la polisi.
Kwa hiyo tupo njia panda. Yawezekana kabisa kuwa tukio la video yenye tishio la kigaidi ni ya magaidi kweli na kundi lililokuwa limejificha Mapango ya Amboni kuwa ni la kigaidi halisi, lakini rekodi za polisi na CCM zinaleta ugumu katika kuamini kipi ni cha kweli na kipi ni usanii tu.
Hilo lina madhara makubwa kwa sababu kama kweli matukio hayo ni ya kigaidi, kinachohitajika si nguvu za vyombo vya dola pekee bali ushirikiano wa hali ya juu kutoka kwa wananchi. Lakini hali ilivyo sasa hasa kuhusu jeshi la polisi ni mbaya, japo watawala wetu hawaonekani kujali.
Na iwapo matukio hayo ni ya kigaidi kweli, tuna matatizo mawili makubwa: mipaka yetu ipo ‘porous’ sana (inapenyeka kirahisi, na ushuhuda ni jinsi ‘unga’ unavyoingizwa na kutoka kirahisi kana kwamba ni bidhaa halali inayoingizwa na kutolewa nchini kihalali). Na tatizo la pili ni rushwa.
Japo ni vigumu kuzuwia ugaidi kwa asilimia 100, nchi ilivyotapakaa rushwa inafanya mapambano dhidi ya ugaidi kuwa magumu mno kwa vile rushwa inawawezesha magaidi kununua fursa ya kufanya hujuma zao kirahisi.
Nimalizie makala hii kwa kutoa wito kwa mamlaka husika kuyachukulia matukio hayo mawili kwa uzito mkubwa, sambamba na kumsihi Rais Jakaya Kikwete kuupa uzito uhasama kati ya wananchi na polisi.
Kadhalika, pamoja na kutokuwa na imani nalo, ninalisihi jeshi la polisi kujaribu kuwa wazi katika kuripoti matukio mbalimbali yanayohusu usalama wa raia na nchi kwa ujumla.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.