21 Oct 2015




OKTOBA 25 mwaka huu, Tanzania itafanya Uchaguzi Mkuu wa Rais, wabunge na madiwani. Mchuano mkali zaidi unatarajiwa kuwa katika nafasi ya urais, ambapo licha ya vyama vinane kusimamisha wagombea wao katika nafasi hiyo, ushindani mkali ni kati ya mgombea wa chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli, na yule wa umoja wa vyama vinne vya upinzani (Ukawa), Edward Lowassa.
Ushindani huo unatokana na unachangiwa zaidi na ukweli kwamba mgombea urais kwa tiketi ya Ukawa, Lowassa, awali alijaribu kuwania nafasi hiyo akiwa mwanachama wa CCM, lakini jina lake halikupitishwa, na hatimaye alijiunga na moja ya vyama vinavyounda Ukawa, Chadema, na kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya umoja huo unaojumuisha pia chama cha National League for Democracy (NLD), NCCR- Mageuzi na Chama cha Wananchi (CUF).
Yayumkinika kuhitimisha kuwa Rais wa Tano wa Tanzania, atakayemrithi Rais wa sasa, Jakaya Kikwete, atakuwa kati ya Dk. Magufuli au Lowassa, huku mgombea urais kwa tiketi ya chama kipya cha Alliance for Change and Transparency (ACT- Wazalendo), Anna Mghwira akitarajiwa kushika nafasi ya tatu.
Dalili kuwa uchaguzi huo ungekuwa na ushindani mkubwa zilianza kujitokeza katika mchakato wa CCM kumpata mgombea wake, ambapo licha ya baadhi ya wanasiasa wa chama hicho waliokuwa na nia ya kuwania urais kujitokeza kutangaza nia takriban mwaka mzima kabla ya kuanza rasmi kwa mchakato huo, jumla ya makada 43 walichukua fomu za kuwania kuteuliwa kuwa wagombea urais, huku 38 kati yao wakifanikiwa kurejesha fomu.
Kwa upande wa Lowassa, jina lake lilianza kusikika katika duru za siasa za Tanzania kuhusu mrithi wa Rais Kikwete, mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010. Ikumbukwe pia kuwa Lowassa alikuwa na mchango mkubwa katika kampeni za urais mwaka 2005, ambapo hatimaye Rais Kikwete alishinda. Kadri Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu ulivyozidi kujongea, ndivyo jina la Lowassa lilivyozidi kuvuma. Kimsingi, mchakato wa CCM kupata mgombea wake uligubikwa zaidi na shauku ya Watanzania iwapo Lowassa angepitishwa au la.
Hata hivyo, hatimaye jina la Lowassa halikupitishwa, na badala yake akapitishwa Magufuli, hatua ambayo pia ilihitimisha tetesi za muda mrefu kuwa urafiki kati ya Lowassa na Rais Kikwete ulikuwa umefikia kikomo, hasa ikizingatiwa kuwa hoja iliyokuwa na nguvu katika harakati za Lowassa kuwania urais kupitia CCM ni hisia kuwa huenda Kikwete angemsaidia Lowassa kuwa mrithi wake.

Kwa upande wa Ukawa, umoja wa vyama vinne vya upinzani ulioundwa katika Bunge Maalumu la Katiba mwaka jana kwa lengo la kushinikiza matakwa ya wananchi yaheshimiwe katika mchakato wa kupata Katiba mpya, mchakato wa kumpata mgombea wao wa urais ulitawaliwa na ukimya kwa muda mrefu, kabla ya Lowassa kujiunga na Chadema na hatimaye kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya umoja huo. Ujio wa Lowassa uliamsha hamasa kubwa miongoni mwa wafuasi wa vyama vinavyounda umoja huo, sambamba na kuleta ushindani mkubwa dhidi ya CCM.
Hata hivyo, uamuzi wa Chadema kumpokea Lowassa, mwanasiasa ambaye chama hicho kilimwandama na tuhuma za ufisadi kwa muda mrefu, ulipokelewa kwa hisia tofauti na Watanzania wengi, huku baadhi wakiuona umaarufu wake kama mtaji muhimu kuwezesha kuishinda CCM, huku wengine wakidhani kitendo hicho ni cha usaliti, hususan kwa Chadema ambayo ajenda yake kuu ilikuwa kupambana na ufisadi.
Licha ya uamuzi wa Lowassa kujiunga na umoja huo wa wapinzani, ukweli kwamba kwa mara ya kwanza, vyama vya upinzani nchini humo vimeweza kushirikiana kwa kusimamisha wagombea mbalimbali katika nafasi ya urais, ubunge na udiwani, imeufanya uchaguzi huo kuwa wa kwanza katika historia ya Tanzania ambapo nafasi ya ushindi kati ya chama tawala na upinzani zinakaribiana.
Takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa idadi kubwa ya Watanzania sio wanachama wa chama chochote cha siasa. Na kundi hili licha ya kutarajiwa kuwa muhimu katika kuwezesha ushindi katika uchaguzi huo, pia linajumuisha wapiga kura wanaokabiliwa na uamuzi mgumu kujiunga mkono CCM na mgombea wake licha ya chama hicho kutuhumiwa kuwa kumechangia matatizo mengi yanayoikabili nchi hiyo, au kujiunga mkono Ukawa ambayo mgombea wake wa urais, Lowassa, licha ya kuhubiri kuhusu mabadiliko, anaonekana kama hana tofauti na chama hicho tawala, hasa ikizingatiwa alikuwa huko kwa muda mrefu.
Kwa tathmini hadi wiki hii ya mwisho kabla ya uchaguzi huo, chama tawala CCM 

kinatarajiwa kufanya vizuri zaidi ya vyama vya upinzani katika nafasi zote, yaani urais, ubunge na udiwani. Kwa upande wa urais, nguvu za CCM zimekuwa katika maeneo kadhaa ikiwa ni pamoja na kujenga picha kuwa mpinzani wao mkuu, Lowassa, hafai ndio maana jina lake lilikatwa katika mchakato wa chama hicho kupata mgombea wake.
Kujenga picha kuwa Lowassa, pamoja na viongozi wachache wa CCM walimfuata huko upinzani ni wenye uchu wa madaraka, wanaotumia malalamiko ya wananchi dhidi ya CCM kwa manufaa yao kisiasa.
Tuhuma za ufisadi dhidi ya Lowassa ambazo kimsingi zilitangazwa zaidi na vyama vya upinzani hususan Chadema. Katika hoja hiyo, CCM pia imejaribu kuionyesha Chadema na Ukawa kwa ujumla kama wanasiasa wasio na msimamo na walioikimbia ajenda yao ya kupinga ufisadi ili ‘kumsitiri’ Lowassa.
Kutofanikiwa kwa Lowassa na Ukawa kuelezea kwa undani kuhusu ajenda yao ya mabadiliko. CCM na mgombea wake Magufuli wamekuwa wakitumia muda mwingi kubainisha sera zao na jinsi watakavyotekeleza.
Takriban asilimia 85 ya Watanzania wanaishi maeneo ya vijijini ambayo kiasili ni ngome kubwa ya CCM kwenye chaguzi. Kwa upande mwingine, Ukawa hawajafanikiwa kujipenyeza vya kutosha katika maeneo hayo, ambapo pia kuna uelewa mdogo kuhusu muundo wa umoja huo.
Kwa mujibu wa takwimu za Tume ya Taifa ya Uchaguzi, idadi ya wanawake –kundi ambalo kiasili ni ngome muhimu ya CCM – ni kubwa zaidi ya wanaume, na hii inatarajiwa kukinufaisha chama hicho tawala na mgombea wake Magufuli.
Magufuli, amekuwa waziri kwenye awamu mbili za urais Tanzania, Awamu ya Tatu ya Rais Benjamin Mkapa, na hii ya Nne ya Rais Jakaya Kikwete, na anasifika kwa uchapakazi. Kwa upande mwingine, ugombea wa Lowassa umeendelea kugubikwa na kashfa ya Richmond iliyosababisha ajiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008.
Kadhalika, licha ya kuwa na mtandao mkubwa nchi nzima, kuanzia ngazi ya mtaa hadi taifa, CCM inanufaika na hoja inayojiri kwenye kila uchaguzi mkuu, kuwa kuwapa ushindi Wapinzani ni sawa na kuwapa fursa ya kufanya majaribio ya uongozi ilhali CCM ina uzoefu wa kutosha.
Mapema wiki hii ziliibuka tena taarifa kuwa mmoja wa viongozi wakuu wa Chadema alihamisha mabilioni ya shilingi kwenda nje ya nchi, fedha zinazodaiwa zilipatikana baada ya kiongozi huyo ‘kukiuza chama hicho’ kwa Lowassa.
Hata hivyo, changamoto kubwa kwa CCM ni kinachotafsiriwa kama hasira za Watanzania wengi kutokana na matatizo mbalimbali yanayoikabili nchi hiyo, ambayo CCM inabebeshwa lawama, kubwa zaidi likiwa ufisadi unaotajwa kama chanzo kikuu cha umasikini.
Wachambuzi mbalimbali wa siasa za Tanzania wanatafsiri kuwa ufuasi mkubwa kwa Lowassa na Ukawa unachangiwa zaidi na manung’uniko ya wananchi wengi dhidi ya CCM, kiasi cha kuwa radhi kumwamini mwanasiasa ambaye kwa muda mrefu ameandamwa na tuhuma za ufisadi. Kauli kama ‘bora kulipigia kura jiwe kuliko CCM’ sio tu imekuwa ikisikika mra kwa mara miongoni mwa wafuasi wa upinzani bali pia inaashiria manung’uniko hayo.
Kadhalika, kwa vyama vinne vya upinzani kuweza kushirikiana na kumsimamisha mgombea mmoja wa urais, na kuongezewa nguvu na ujio wa Lowassa pamoja na makada kadhaa waliohama CCM, kwa mara ya kwanza Wapinzani wanaona kuna uwezekano wa kukishinda chama hicho tawala. Mikutano yao ya kampeni imeshuhudia umati mkubwa japokuwa lawama kwa Lowassa imekuwa ni kuhutubia kwa muda mfupi mno.
Wakati Magufuli na CCM wanaonekana kujiamini na kuwa na uhakika wa ushindi, kwa upande wa Lowassa na Ukawa, licha ya kuwa na matumaini makubwa ya kushinda, wanaonekana kuwa na hofu ya kuhujumiwa na chama hicho tawala.
Kwenye nafasi za ubunge na udiwani, CCM inatarajiwa kusinda viti vingi zaidi kwa sababu licha ya kuwa na mtandao mzuri majimboni, Ukawa inaonekana kuwekeza nguvu zaidi katika kumnadi Lowassa kuliko katika kampeni zake majimboni. Kadhalika, takwimu zinaonyesha kuwa mgombea wa CCM, Magufuli, ametembelea maeneo mengi zaidi ya mgombea wa Ukawa, Lowassa.
Kwa upande wa vyama vingine vinavyoshiriki uchaguzi huo, inatarajiwa kuwa ACT-Wazalendo kitashika nafasi ya tatu nyuma ya CCM na Ukawa, na kinatarajiwa kuimarika zaidi baada ya uchaguzi huo hasa kwa vile inahisiwa kwamba iwapo Ukawa itashindwa, wafuasi wake wengi wanaweza kuiona ACT-Wazalendo kama mpinzani wa kweli dhidi ya CCM.
Kwa hitimisho, changamoto kubwa kwa chaguzi nyingi barani Afrika huwa kwa chama cha kikuu cha upinzani kukubali matokeo pindi kikishindwa. Kwa mara ya kwanza, Tanzania inafanya uchaguzi wake mkuu huku kambi ya upinzani ikiwa na imani kubwa kuwa itaibuka na ushindi.
Kadhalika, kadri uchaguzi unavyozidi kukaribia ndivyo Wapinzani (hasa Ukawa) wanavyozidi kuonyesha kutokuwa na imani na mfumo mzima wa uchaguzi. Bila kujali upande gani utakaoibuka na ushindi, mustakabali wa Tanzania unategemea busara za viongozi na wafuasi wa kila chama kuhamasisha amani badala ya vurugu. Ushindi mkubwa katika uchaguzi huo ni kwa Watanzania kuendelea kubaki na umoja na amani.
Pia, mshindi katika uchaguzi huo atakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazoikabili Tanzania, kubwa zaidi ikiwa kuleta uwiano kati ya utajiri wa raslimali lukuki katika nchi hiyo na hali ya maisha ya wananchi, kupunguza pengo kati ya matajiri na masikini, na kuwaunganisha Watanzania kuwa kitu kimoja baada ya uchaguzi huu ambao kwa kiasi kikubwa umejenga mpasuko kijamii na kisiasa.
Mwisho, kwa vile hii ni makala yangu ya mwisho kabla ya uchaguzi huo hapo Jumapili, na kwa vile safu hii imekuwa ikifuatilia maendeleo ya uchaguzi huo tangu mwanzo, basi si vibaya kufanya ubashiri wa matokeo katika nafasi ya urais. Na ubashiri kuwa Magufuli atashinda urais, na CCM itashinda viti vya jumla katika nafasi za ubunge na udiwani, huku Ukawa, hususan Chadema, ikipata viti pungufu zaidi ya ilivyokuwa katika uchaguzi mkuu uliopita.
Hata hivyo, mshindi halisi katika uchaguzi huo ni Tanzania na Watanzania wenyewe. Kuna maisha baada ya uchaguzi, kwa hiyo ni muhimu kwa upande utakaoshindwa kutanguliza mbele maslahi ya taifa, badala kufanya vurugu.
MUNGU UBARIKI UCHAGUZI MKUU. MUNGU IBARIKI TANZANIA.



Sababu Tisa kwanini CCM itashinda katika Uchaguzi Mkuu Jumapili hii, Oktoba 25

Na January Makamba

Tarehe 25 mwezi huu Oktoba, Watanzania watapiga kura kumchagua rais wao wa tano, wabunge na madiwani. Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu umekuwa na msisimko mkubwa zaidi tangu kuanzishwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi mwaka 1995. Mengi yamendikwa kuhusu uchaguzi huu, hususan kutokana na hisia kwamba safari hii Upinzani una nafasi ya kukiondoa madarakani moja ya vyama vikubwa na vyenye muundo bora barani Afrika, chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM). Matukio mbalimbali kuelekea uchaguzi huo yameleta shauku inayoweza kutengeneza hadithi ya kusisimua.

Nikiwa sehemu ya Timu ya Kampeni ya CCM,na kwa manufaa ya wote ambao wangependa kuwa na mtizamo tofauti, ninatoa sababu 9 kwanini tunaamini kuwa CCM itaibuka mshindi na kwanini Dkt John Pombe Magufuli atakuwa Rais ajaye wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

1.    Ugombea ‘fyongo’ (flawed) wa Edward Lowassa

Ilishabainika kuwa uchaguzi huu ungekuwa mgumu kwa CCM bila kujali nani angekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Upinzani. Lakini matokeo ya uchaguzi huu yalielemea upande wa CCM pale Upinzani ulipomchagua Lowassa kuwa mgombea wao. Ni rahisi kwa CCM kuchuana na Lowassa kuliko laiti mgombea wa Upinzani angekuwa Dkt Wilbrod Slaa, ambaye ndiye aliandaliwa kuwa mgombea kabla ya ‘ukusukumwa kando’ na nafasi hiyo kupewa Lowassa. Slaa alikuwa na uadilifu katika maeneo mengi, na aliaminika. Kwa Lowassa, ni vigumu na inanyima raha kuchuana na mfumo aliyoshiriki kujenga na ambao ulikuwa sehemu ya maisha yake hadi Agosti mwaka huu alipohamia Upinzani. CCM ilikuwa na nafasi ya kumpitisha Lowassa kuwa mgombea wake wa nafasi ya urais. Hatukufanya hivyo kwa sababu rahisi tu kwamba ingekuwa vigumu mno kumkabidhi kwa wananchi mgombea wa matarajio ya baadaye ambaye ni kiashirio cha yale yasiyowaridhisha wananchi kuhusu CCM. Kuna wanaoamini kuwa uchaguzi huu ni mgumu kwa vile Lowassa ndiye mgombea wa Upinzani. Sisi twaamini kwamba uchaguzi huu ungekuwa mgumu mara kumi zaidi laiti Lowassa angekuwa ndiye mgombea wetu.

2.    Upinzani umesalimisha ajenda yake ya kupinga ufisadi

Kipindi cha miaka 10 iliyopita kimetawaliwa na matukio mbalimbali ya kuwabainisha mafisadi na kuwachukulia hatua. Vyombo vya habari, taasisi za kiraia na Bunge vimefanya kazi nzuri kushughulikia suala hilo. Rais Jakaya Kikwete ameweka historia kwa kuamuru ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kupatikana kwa wananchi na kujadiliwa kwa uwazi Bungeni. Waziri Mkuu aliyekuwa madarakani, si mwingine bali Lowassa, alijiuzulu kwa sababu ya kashfa ya rushwa. Mawaziri kadhaa walitimuliwa kazi na manaibu waziri wawili wanatumikia vifungo jela. Huu ni uwajibikaji wa hali ya juu japokuwa kuna wanaoweza kudhani ni hatua ndogo. Umma umeamka.

Upinzani ulijenga hadhi yake kwa kuongelewa sana kuhusu ufisadi. Kilele cha Upinzani kilijiri mwaka 2007 katika mikutano mkubwa wa hadhara ambapo walitangaza majina 10 ya watu waliowaita mafisadi wakubwa zaidi, katika kilichokuja kufahamika kama Orodha ya Aibu (List of Shame). Lowassa alikuwa kinara kwenye orodha hiyo.

Ilitarajiwa kuwa Uchaguzi Mkuu huu uwe ‘hukumu’ kwa CCM kuhusu ufisadi. Upinzani ulitarajiwa kuitumia ajenda ya ufisadi ambayo inawagusa watu wengi. Lakini ghafla, kwa kumteua mwanasiasa, ambaye kwa jitihada zao wenyewe Wapinzani,  amefahamika zaidi kwa ufisadi, iliwalazimu kuzika ajenda hiyo. Kilichofuata baada ya hapo ni kituko na kichekesho. Wale mashujaa wa mapambano dhidin ya ufisadi walijikuta wakilazimika ‘kulamba matapishi yao.’ Wengi wao waliokuwa mahiri katika mitandao ya kijamii walilazimika kufuta historia ya baadhi ya waliyoyaandika mtandaoni walipokuwa wakikemea ufisadi, lakini si kabla ya maandiko yao kunaswa kwa ‘screenshots.’ Ulikuwa ni ukweli wa kushangaza. Ni Dkt Slaa na Professa Ibrahmi Lipumba, viongozi muhimu wa Upinzani tangu miaka ya Tisini, walioamua kujiuzulu nyadhifa zao kwa kukerwa na uamuzi wa Upinzani kumpokea Lowassa.Matokeo yake, Upinzani walijikuta wakichana kadi yao turufu- ajenda dhidi ya ufisadi. Ni nadra kwao kuongelewa suala hilo, na wanapojaribu kufanya hivyo, ni kwa kujitetea tu.

Jioni moja mwezi Agosti, nilimwona Mbunge wa Upinzani, Peter Msigwa, katika mdahalo kwenye runinga. Aliongelea kitu ambacho kilijumuisha mtizamo wa Upinzani kwa muda huo, na kiliniacha hoi. Alisema, kabla hawajampokea Lowassa, walifanya utafiti wao, na “ufisadi sio ajenda muhimu kwa taifa letu.” Alidai kwamba wenye ushahidi kuhusu ufisadi wa Lowassa wajitokeze hadharani.Alionekana kusahau kuwa walipomtaja Lowassa katika List of Shame, walitangaza hadharani kuwa wana ushahidi. Muda si mrefu uliopita, CCM ilikuwa ikiwaomba Wapinzani kuleta ushahidi kila yalipojitokeza madai ya ufisadi dhidi ya viongozi wa chama na serikali allegations were leveled against the party and its leaders. Haikupendeza kuingiza hoja za kisheria katika masuala ya kimaadili. Upinzani sasa umeamua kwa hiari yao kuchukua ‘chembemoyo’ wakati ambapo viongozi wa CCM wanaongelea ufisadi kwa ujasiri na msisitizo.

Uchaguzi huu Mkuu ni muhimu sana kwa Upinzani. Kimsingi, unaweza kuwa na madhara makubwa. Endapo watashindwa hapo Jumapili, ‘watapotea’ kwa muongo mzima ujao. Ndio maana inashangaza kuona wamechukua uamuzi wa kukimbia ajenda yao kuu ya kupambana na ufisadi  ambayo iliwatambulisha na kuwaimarisha. Na kuwapa nguvu kukubalika kwa wapigakura. Kuona wanatarajia kushinda ni miujiza mkubwa.

3.    Mabadiliko ambayo kamwe huwezi kuyaamini

Ukizinguka jijini Dar es Salaam utakutana na mabango ya Upinzani yanayodaia “Ni Muda wa Mabadiliko.” Lakini ukisikiliza mikutano yao ya kampeni, ni porojo na hasira tu. Wasemaji wakuu katika mikutano hiyo ni Waziri Mkuu wa zamani na kada wa muda mrefu wa CCM, Frederick Sumaye na Lowassa mwenyewe. Kwa pamoja, wamekuwa wana-CCM na katika nyadhifa  za juu serikalini kwa zaidi ya miaka 50. Kwa hiyo inasikitisha kusikiliza kauli zao – zinazokosa imani na kupalizwa na aibu – wakipambana na mfumo walioshiriki kujenga, uliojenga tabia zao za kisiasa, na ambao walikuwa wakiusifu miezi mwili tu iliyopita.
Kutokuwa wakweli na kuweka mbele maslahi binafsi kwawatuma kudai kuwa CCM haijafanya chochote katika miaka miaka 50 iliyopita. Inapotokea viongozi wawili waandamizi wa chama na serikali  kwa zaidi ya miaka 30, wote wakiwa walioshika Uwaziri Mkuu, kudai kuwa hakuna chochote kilichofanyika katika miaka 50 iliyopita, wajihukumu wenyewe. Si kwa muundo, mwonekano au ukweli, wanasiasa hao wanasimamia mabadiliko. Yayumkinika kuhitimisha kuwa mabadiliko wanayoongelea ni kuhusu kubadili chombo kilichowaingiza madarakani, mabadiliko ya sare tu za chama. Hawana habari na mabadiliko ya maisha ya wananchi wa kawaida. Wapigakura wameanza kushtukia ukweli huo.

4.    Migogoro na mkanganyiko ndani ya UKAWA

Huko nyuma, kila ulipojiri uchaguzi, Upinzani ulijaribu kuunganisha nguvu ili kuing’oa CCM madarakani.Na kila mara jitihada za ushirikiano zilishindikana. Mwaka 2014, mjadala kuhusu Katiba Mpya kuataka serikali tatu uliwapatia ajenda ya kuwaunganisha pamoja. Kisha wakaamua kutafsiri ushirikiano huo kuwa wa kisiasa, wakaafikiana kusimamisha mgombea mmoja katika nafasi ya urais na kugawana majimbo.

Baada ya hapo kukajitokeza unafiki wa wazi. Kuonyesha kuwa matamanio yaliwekwa mbele ya kanuni zilizopatikana kwa jitihada ngumu, chama ambacho jina lake linajumuisha maneno ‘demokrasia’ na ‘maendeleo’ kilitemea mate mchakato wake chenyewe wa kidemokrasia na mshikamano kupata mgombea wake wa urais, na kukurupuka kumpitisha kada wa muda mrefu wa CCM ambaye jitihada zake kuwania urais kwa tiketi ya chama hicho tawala ziligonhga mwamba.

Waliamini kwamba uamuzi wa Lowassa kuhama CCM ungekiathiri chama hicho tawala, wakitarajia vigogo kadhaa wangemfuata huo Upinzani. Badala yake, ujio wake huko ukapelekea kuondoka kwa wanasiasa wawili waliokuwa nguzo muhimu kwa Upinzani, Dkt Slaa na Prof Lipumba.Kadhalika, wanachama wengine muhimu waliohama na kujiunga na chama cha ACT- Wazalendo, ambacho hakikujiunga na UKAWA.
Kana kwamba hiyo haitoshi, makubaliano ya UKAWA kusimamisha mgombea mmoja  kila jimbo yalikumbwa na mushkeli katika majimbo kadhaa na kupelekea malalamiko yaliyosababisha ugumu katika kampeni za Lowassa.

Huko Masasi, mgombea mwenza wa Lowassa, Juma Duni, alilazimika kuokolewa jukwaani baada ya waliohudhuria mikutano wake wa kampeni kupiga kelele kuwa wataipigia kura CCM. Katika jimbo la Nzega, Lowassa alilazimika kuendesha ‘kura ya sauti’ kuwauliza waliohudhuria mikutano wake wa kampeni wanamhitaji mgombea gani kati ya wawili wa UKAWA waliokuwa wanachuana. Mpango mzima wa ushirikiano miongoni mwa vyama vinavyounda UKAWA umekwenda mrama.CCM sasa ipo katika nafasi nzuri ya kujinyakulia majimbo ambayo vinginevyo yangekwenda kwa wagombea wa Upinzani.

Lakini kilele cha unafiki wa UKAWA ni hiki. Umoja huo uliundwa ili kutetea Katiba Pendekezwa iliyoshauri muundo wa Muungano wa serikali tatu. Kanuni hiyo ya msingi iliwekwa kando pale UKAWA walipomchagua mgombea wao wa tiketi ya urais, Lowassa, ambaye alikuwa mtetezi mkubwa wa muundo wa Muungano wa serikali mbili. Kwa wengi wasioendeshwa na propaganda, uamuzi wa kutelekeza suala la msingi lililopelekea umoja wa vyama hivyo, kwa ajili tu ya imani ya kufikirika ya kushinda urais, yaashiria uchu wa madaraka na sio mabadiliko yanayohubiriwa kwa wananchi.


5.    Lowassa kushindwa kufanya kampeni nchi nzima

Lowassa anaonekana kutokuwa na uwezo wa kusafiri kwa urefu na upana wa Tanzania kufanya kampeni. Mara nyingi amekuwa akitumia usafiri wa anga kwenda mikoani ambako hufanya mikutano mikubwa kwenye makao makuu ya mikoa, kutembelea majimbo mawili au matatu ya jirani kwa helikopta, na kurejea jijini Dar es Salaam. Huko Tanga, kwa mfano, alifanya kampeni katika majimbo matatu tu kati ya tisa mkoani humo. Mkoani Ruvuma, alifanya kampeni katika majimbo matatu kati ya tisa, Kigoma majimbo mawili kati ya manane, na Kagera majimbo matatu tu.

Kinyume chake, mgombea wa CCM, Magufuli amekuwa barabarani tangu Agosti 23, huku akipumzika kwa siku tatu. Anatumia usafiri wa gari, akitembelea kijiji baada ya kijiji, na kufanya mikutano kati ya minane hadi 12 kwa siku. Aina hii ya kufanya kampeni ‘kwa rejareja’ inabaki kuwa nguzo pekee ya kujihakikishia ushindi kwenye uchaguzi mkuu nchini Tanzania, hususan katika maeneo ya vijijini ambayo usikivu na kuonekana kwa vyombo vya habari ni mdogo. Wakati Lowassa anavutia wahudhuriaji wengi katika mikutano yake katika miji mikubwa, Magufuli anajipatia wahudhuriaji wengi katika kila kona ya Tanzania. Kama idadi ya wahudhuriaji katika mikutano hiyo ya kampeni inamaanisha wingi wa kura, basi kwa hakika CCM itashinda. Lakini tofauti na Upinzani, CCM haidanganyiki na wingi huo wa wahudhuriaji katika mikutano ya kampeni. Rekodi ya mahudhurio makubwa ilikuwa ikishikiliwa na Agustino Lyatonga Mrema, mgombea maarufu wa kiti cha urais kwa tiketi ya Upinzani mwaka 1995 (ambaye pia alijiunga na Upinzani akitokea CCM). Hata hivyo alishindwa kwenye uchaguzi huo. Sie twategemea kitu kingine.

6.    Mfumo imara wa CCM katika uhamasishaji kuanzia ngazi ya chini kabisa.

Katika Tanzania, vyama vichache mno vinavyoweza kuchuana na uwezo wa CCM kuhamasisha wananchi. Wakati Wapinzani huhadaiwa na ‘mahaba’ wakati wa kampeni za uchaguzi, mahudhurio makubwa kwenye mikutano yao ya kampeni na vichwa vya habari magazetini, CCM hutumika nguvu yake ya kimuundo na kuwasha ‘mashine zake za kisiasa,’ kuanzia ngazi ya mtaa (ujumbe wa nyumba kumi) kwa nchi nzima. Kimuundo, jumiya ya wanawake wa CCM (UWT) pekee ni kubwa kuliko Chadema, chama kikuu cha upinzani. CCM Haihitaji kusafiri ili kufanya kampeni. CCM ipo kila mahala, ikifanya kampeni katika makundi madogo, vijijini na mitaani, kila siku na mbali ya upeo wa vyombo vya habari. Kwa wanaofahamu muundo wa chama hicho, ushindi kwake si jambo la kushangaza.

Kwenye miaka ya 1950s, wakati wa harakati za kusaka uhuru kutoka kwa mkoloni, uwezo wa TANU kuhamasisha ulikuwa nguzo muhimu kwa Tanganyika kupata uhuru wake.CCM imerithi vinasaba vya TANU. Mwalimu Nyerere aliijenga CCM kuwa imara kwa nyakati kama hizi. Mwaka jana, huku umaarufu wake ukiwa umepungua, CCM ilimudu kushinda uchaguzi wa serikali za mitaa kwa asilimia 80 dhidi ya umoja Huohuo wa Upinzani inaokabilina nao katika uchaguzi huu Mkuu.Tofauti haipo kwenye nini kinachoonekana kwenye vyombo vya habari au mitandao ya kijamii bali jinsi gani makada wa chama hicho tawala walivyofanya uhamasishaji katika kila mtaa na kijiji. Uchaguzi huo wa serikali za mitaa, ambao hufanyika mwaka mmoja kabla ya uchaguzi mkuu, hutoa dalili nzuri kuhusu matokeo ya uchaguzi mkuu.

7.    Umahiri wa Dkt Magufuli

Mwaka jana, baadhi ya waandishi wa habari walikiri kwamba ni vigumu mno kumshambulia na kumshinda Dkt Magufuli. Ana rekodi imara ya usafi, uchapakazi na anayetaka kuona matokeo sahihi. Hajawahi kuvutiwa na harakati za kisiasa, na ilikuwa mshangao alipotangaza kuwania urais. Na alipotangaza, hakufanya mbwembwe wala kijitangaza kwenye vyombo vya habari. Alizingatia kanuni za chama kwa ukamilifu. Dkt Magufuli analeta kumbukumbu za mgombea mwingine aliyekuwa hajulikani mwaka 1995 -  Benjamin Mkapa. Wakati umaarufu wa CCM ukiwa chini, huku ikikabiliwa na upinzani kutoka kwa Naibu Waziri Mkuu aliyehama kutoka chama hicho tawala, CCM ilimchagua turufu yake ambayo ilikuwa ngumu kuikabili.Miaka 20 baadaye, ikikabiliwa na upinzani wa Waziri Mkuu maarufu wa zamani aliyehama chama hicho na kujiunga na Upinzani, CCM imefanya tena ‘vitu vyake.’ Siku zote, CCM hujua ‘kufanya pigo la haja.’

8.    Ufanisi wa CCM katika maeneo ya vijijini

Mimi ni Mbunge wa jimbo lisilo mjini, lenye idadi ya wastani ya wapigakura. Mwaka 2010, katika uchaguzi ulionekana kuwa mgumu, CCM ilishinda jimbo langu kwa asilimia 80., na kitaifa kwa asilimia 61. Hivi sasa, tunatarajia ushindi wa CCM kuwa wa asilimia 90 hivi. Tanzania ina  majimbo kadhaa yaliyo kama jimbo langu. Upinzani hupenda kuwapuuza wananchi katika majimbo yasiyo ya mijini, kama jimbo langu, kwa kudai kuwa wanaichagua CCM kutokana na ujinga wao. Wasingeweza kukosea zaidi ya hivyo.

Popote walipo, watu hupiga kura kulingana na mahitaji yao. Mwaka 2000, vijiji vinne tu katika jimbo langu ndivyo vilikuwa na umeme. Leo, vijiji 44 vina umeme. Japo hatujaweza kutoa huduma zote kwa kiwango cha kumfurahisha kila mtu, lakini hali halisi yaonyesha wingi wa wanafunzi mashuleni, walimu zaidi, madaktari na manesi zaidi, zahanati nyingi zaidi zimejengwa, huduma za mawasiliano ya simu zinapatikana kwa wingi, barabara nyingi za lami, nk. Porojo kuwa hakuna kilichofanyika Kwahiyo wapigakura wasiichague CCM haieleweki katika maoneo hayo ambay kimsingi ndiyo yenye wapigakura wengi. Na wagombea wa CCM wanaposema watafanya zaidi ya waliyokwishafanya, kwa kuzingatia mafanikio yaliyokwishapatikana, wananchi wanawaamini. Hotuba za kampeni ni mwonekano na mantiki.

Chaguzi sio kuhusu ahadi tu bali jinsi gani ahadi hizo zitaandaliwa na kutekelezwa. Jukwaa ambalo kila chama kitanadi ajenda zake za uchaguzi hujengwa wakati wa uzinduzi wa kampeni za chama husika. Yahitaji mtu kuangalia tu uzinduzi wa kampeni za za Lowassa na Magufuli. Lowassa aliongea kwa dakika 9 tu  - akiahidi, pamoja na mambo mengine, kuwaachia huru wabakaji (sio kama ninazusha hili) wanaotumikia vifungo vyao na watuhumiwa ugaidi wanaosubiri kesi zao. Bila kujali alikuwa na malengo gani wakati anatoa ahadi hizo, makosa hayo hayastahili msamaha wa rais.  Kwa upande wake, Magufuli aliongea kwa dakika 58, akielezea kwa undani ajenda za maendeleo katika nyanja za elimu, ajira, afya, ufisadi, huduma za maji, na miundombinu. Kuanzia hapo, kwa muda wote wa kampeni, mwenendo umekuwa hivyo, kwa uzito wa ujumbe kwenye hotuba zake na muda wa kuhutubia

Wanaohudhuria mikutano ya Dkt Magufuli huondoka katika mikutano hiyo wakiwa na matumaini na wenye nguvu. Kwa upande mwingine, wahudhuriaji katika mikutano ya Lowassa huondoka wakiwa wamekanganywa. Siku ya kupiga kura, wapigakura wanamkumbuka jinsi mgombea alivyoonekana na alivyoongea, na jinsi walivyojisikia walipomwona jukwaani. Kwa kigezo hiki, ni bora ningekuwa upande wa Magufuli.  

9.    Uongo, uongo na takwimu

Tanzania haina utamaduni wa kura za maoni kupima nafasi za wagombea katika uchaguzi. Tuna utaratibu wa muda mrefu wa kupata maoni ya wananchi katika maamuzi makubwa ya kisera – kuingia mfumo wa vyama vingi vya siasa, marekebisho ya Katiba, na kadhalika. Mwaka 2005, kulifanyika kura ya maoni, iliyobashiri ushindi mkubwa kwa CCM. Na kwa hakika, CCM ilishinda kwa asilimia 80. Mwaka 2010, kura ya maoni iliyoendeshwa na kampuni ya Ipsos-Synovate iliashiria kuwa idadi ya kura za CCM ingepungua hadi kufikia asilimia 61. CCM ilipinga matokeo ya kura hiyo ya maoni ikidani kuwa yalikuwa kiasi kidogo sana. Matokeo ya uchaguzi huo yalikuwa kama yalivyotabiriwa katika kura hiyo ya maoni. CCM ilipata asilimia 61 ya kura zote.

Hivi karibuni, kura mbili za maoni zilichapishwa. Zote zilifanywa na taasisi huru zinazoheshimika. – Twaweza and Synovate-Ipsos tena- zote zikijihusisha na utafiti wa kusaka maoni. Taasisi mbili tofauti, zilizotumia mbinu tofauti za kufanya utafiti, katika nyakati tofauti, matokeo yaleyale. CCM itashinda kwa asilimia 62 ya kura zote.

Inaruhusiwa, na kwa yumkini ni jambo zuri, kupingana na sababu hizi tisa za kwanini CCM itashinda. Lakini namba zina tabia ya ukandamizaji. Ndio mwelekeo wa kura huwezi kubadilika. Lakini kwa kuzingatia yote yaliyokwishaongelewa kuhusu kinachodaiwa kuwa ufuasi mkubwa kwa Upinzani, basi muda huu ingetarajiwa tuwa tunajadiliana kuhusu ufuasi wa wengi kutoka Upinzani kuelekea CCM– na sio kutarajiwa ufuasi wa wengi kutoka CCM kuelekea Upinzani. Na ndiyo, kura za maoni zaweza kukosea, na tusiwekee mkazo sana.Lakini hoja hii sasa ndiyo hupendelewa zaidi na upande unaelekea kushindwa kwenye uchaguzi.


January Makamba ni Mbunge wa Bumbuli (CCM), Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM, na msomaji wa Kampeni za CCM 

16 Oct 2015



 Makala hii ilipaswa kuchapishwa katika toleo la wiki hii la Raia Mwema, Jumatano Oktoba 14 lakini ikashindikana kwa sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu. Hata hivyo, ilichapihswa jana katika gazeti-dada la Raia Tanzania. Hebu angalia kwanza picha na nukuu ya 'mwanamabadiliko' Kingunge, kisha usome makala husika chini ya picha hiyo

BONYEZA MAKALA KUIKUZA IWE UKURASA MZIMA

10 Oct 2015

HATIMAYE tumebakiwa na takriban wiki mbili tu kabla ya Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika hapo Oktoba 25. Wakati kampeni hizo zikielekea ukingoni, matukio mawili makubwa yamejitokeza Jumapili iliyopita.
Tukio la kwanza ni kifo cha mwanasiasa nguli, Mwenyekiti wa chama cha siasa cha Democratic (DP), Mchungaji Christopher Mtikila. Tukio jingine lililotokea siku hiyo hiyo ni uamuzi wa mwanzilishi wa CCM na TANU, na mkongwe wa siasa za Tanzania, Kingunge Ngombale Mwiru. Nimeona ni vema kuyajadili matukio haya kwa sababu yote yanahusiana na Uchaguzi Mkuu, kwa namna moja au nyingine.
Tuanze na hilo la pili. Kwanza, tangazo la Kingunge kujiondoa uanachama wa CCM lilistahili liwe na mvuto mkubwa kama Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere alipotangaza kung’atuka. Lakini ukweli ‘mchungu’ ni kwamba tukio hilo limeonekana kama mwanachama wa kawaida tu wa CCM kuamua kujiondoa katika chama hicho.
Lakini, pili, uamuzi wa Kingunge kujiondoa CCM, haukuwa jambo la kushtua, kwa vile kwa muda mrefu sasa, kada huyo, rafiki wa karibu wa Baba wa Taifa, alikwishajitambulisha yupo upande gani katika siasa za uchaguzi. Kingunge, alipigana kwa hali na mali kuhakikisha mgombea ‘ chaguo lake,’ Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, anashinda katika mchujo wa chama hicho tawala kupata mgombea wake.
Niliwahi kuandika huko nyuma kuwa laiti busara ingemwongoza mzee huyo – hasa ikzingatiwa kuwa katika mila zetu za Kiafrika, wazee hutazamwa kama ‘visima’ vya busara na hekima – basi asingejiweka upande wa mgombea fulani au hata kama angefanya hivyo, licha ya kuwa ni haki yake ya kidemokrasia na kikatiba, basi labda angefanya kwa usiri.
 Nilitahadharisha hivyo kwa sababu, kwa kuegemea upande mmoja ilhali kuna pande nyingi katika jambo husika kuna matokeo ya aina mbili, kuwa sahihi au kukosea. Sasa, kama matokeo ya kuwa sahihi ni kudumisha hadhi na kukosea ni kupoteza hadhi, kila mwenye busara anatarajiwa kuwa makini katika jambo hilo.
Kitendo cha Kingunge kumuunga mkono Lowassa katika mchakato wa CCM kumpata mgombea wake, na hatimaye jina la kada huyo kukatwa katika mchujo, ilikuwa na athari kwa hadhi ya Kingunge kama mkongwe wa siasa. Bila kujali kuwa Lowassa alionewa au alistahili kukatwa, ukweli tu kwamba hakupitishwa ni sawa na kufeli kwa waliokuwa wakimuunga mkono, ikiwa ni pamoja na Kingunge.
Niliposoma tamko lake la kujiengua CCM nilibakiwa na maswali kadhaa, kubwa likiwa “...hivi huyu ndiye Kingunge yule yule wa zama za Nyerere au huyu ni toleo jipya? Na pengine bila hata kwenda mbali sana na kurejea zama za Nyerere, Kingunge huyu huyu alikuwa mstari wa mbele katika kampeni zilizomwingiza madarakani Rais Jakaya Kikwete, mwaka 2005. Yeye ni sehemu muhimu ya takriban kila analolaumu kuhusu CCM.
Matarajio ya wengi kwa Kingunge yalikuwa angekuwa mrithi wa Baba wa Taifa, si kwa sababu ya umri wake tu bali uumini wake katika Itikadi ya Ujamaa. Kingunge alikaa kimya wakati nguzo kuu ya itikadi hiyo, Azimio la Arusha ikizikwa katika kile kinachofahamika kama Azimio la Zanzibar. Kada huyo licha ya kuwa kimya katika masuala mbalimbali yanayoifanya CCM kupoteza umaarufu, hususan suala la ufisadi, alijitokeza kuwa mtetezi mkubwa wa watu waliotuhumiwa katika orodha maarufu ya watu waliotuhumiwa na Chadema kuwa ndio ‘mapapa wa ufisadi,’ iliyojulikana kama ‘List of Shame.’
Kimsingi, Kingunge aliwananga Chadema na kuwaita waongo, wazushi na wanafiki, wanaosema uongo na hakuna ushahidi, hakuna kiongozi fisadi. Leo hii, mwanasiasa anayeamini kuwa ndio chaguo sahihi kuingoza Tanzania, yaani Lowassa, kajiunga na waongo, wazushi, na wanafiki hao.
Kingunge ni mwathirika wa makosa yake mwenyewe kimkakati. Alipaswa tangu awali, achague kuwa mtetezi wa wananchi kama Baba wa Taifa, au mtetezi wa tabaka tawala. Japo ninatambua madhara ya kuwa mtetezi wa wananchi, kwa maana ya kutengeneza maadui wengi kisiasa, lakini ukweli usiopingika ni kwamba heshima na hadhi ya mtu wa aina hiyo hudumu milele. Tunawakumbuka akina Nyerere na Sokoine si kwa vile tu walikuwa viongozi wetu bali kwa sababu walisimama upande wa wananchi tulio wengi kuliko kulinda tabaka la watawala walio wachache.
Katika hitimisho langu baada ya kupokea taarifa za Kingunge kujiuzulu uanachama wa CCM, niliandika katika mtandao wa kijamii wa Twitter kuwa Kingunge aliwahi kuwa kama Muhmmad Ali wa siasa za Tanzania. Lakini tangazo lake la kujiuzulu CCM leo ni kama Ali angetangaza sasa kuwa anajiuzulu masumbwi. Alikwikushajiuzulu miaka kadhaa iliyopita. Nilichomaanisha ni kuwa, umuhimu wa mkongwe huyo wa siasa za nchi yetu ulisha- expire (kwisha muda wa matumizi) kitambo, na kubaki au kuondoka kwake CCM hakukuwa na faida kwa yeyote zaidi yake mwenyewe. Ninamsikitikia kwa sababu alipaswa kukumbukwa kwa mazuri mengi ya zama za Nyerere lakini dalili ni kwamba ataishi kukumbukwa zaidi kwa jithada za kumbeba Lowassa kwa gharama ya hadhi yake.
Tukiweka hilo kando, taarifa za kifo cha Mchungaji Mtikila kimeonekana kuwashtua Watanzania wengi. Binafsi, nilipopata taarifa hizo, kwanza nilidhani ni utani tu, lakini nilipogundua kuwa zina ukweli, hisia zangu zikaanza kupatwa na wasiwasi fulani.
Wakati tayari kuna taarifa zisizo rasmi mbalimbali zinazosambaa kwa kasi mtandaoni kuhusu chanzo halisi cha kifo cha Mchungaji Mtikila, licha ya taarifa za polisi kuwa chanzo cha ajali iliyosababisha kifo chake ni mwendo kasi wa gari alilokuwa akitumia huku akiwa hajavaa mkanda wa kiti cha gari, ukweli kwamba mwanasiasa huyo machachari alikuwa na ‘mabomu’ kuhusu mmoja wa wagombea urais, ilitosha kuniongezea wasiwasi huo.
Ni muhimu, katika hatua hii kukumbushia kuwa miongoni mwa sababu za umaarufu wa Mtikila ni kile ambacho wengi walikitafsiri kama ‘conspiracy theories,’ yaani hoja zinazoonyesha kubeba ukweli, zikiambatana na aina fulani ya ushahidi, lakini zinabaki vigumu kuzithibitisha.
Kwa mujibu wa taarifa zinazosambaa mtandaoni, Mtikila alikuwa akijipanga kuzuia ugombea wa mmoja wa wagombea urais, kwa hoja mbalimbali, ikiwa ni pamoja na madai yake kuwa mgombea huyo ni sehemu ya mkakati wa kimataifa kuihujumu nchi yetu. Kadhalika, Mchungaji huyo alinukuliwa akiongea kwenye kituo kimoja cha televisheni huko nyumbani (Tanzania) akisisitiza kwa nini anaamini mgombea huyo ni janga kwa taifa.
Sasa, japo kifo ni mapenzi ya Mola, lakini katika mazingira ya kawaida tu, kama anajitokeza mtu kumpinga mwanasiasa hadharani huku akipania kumwekea vikwazo katika safari yake ya Ikulu, kisha mtu huyo akafariki kwa ajali siku chache kabla ya uchaguzi, hisia za kibinadamu zinaweza kuhisi kuna namna hapo.
Kwa bahati mbaya, au pengine makusudi, jeshi la polisi limeonekana kuwa na haraka mno kutangaza chanzo cha ajali iliyosababisha kifo cha mwanasiasa huyo. Iwapo uchunguzi wa vyanzo vya ajali katika nchi zilizoendelea huchukua siku kadhaa licha ya taasisi zao za uchunguzi kuwa na nyezo za hali ya juu, iweje jeshi letu la polisi linalosifika kwa uchunguzi wa mwendo wa konokono lipate uwezo wa ghafla wa hali ya juu kuweza kutambua chanzo cha ajali hiyo siku moja tu baadaye?
Kwa mtizamo wangu, na ili kuwaridhisha Watanzania kuwa kifo cha mwanasiasa huyo hakina mkono wa mtu, polisi walipaswa kufanya uchunguzi wa kina, ikiwa ni pamoja na kupata taarifa ya uchunguzi wa kitabibu kuhusu chanzo cha ajali kabla ya kukurupuka na sababu ambazo ni rahisi kuhisi kuwa ni za kufikirika.
Kwa bahati mbaya, kifo cha Mtikila kilitokea siku moja na tukio la Kingunge kujivua uanachama wa CCM, suala lililosababisha baadhi ya watu kuyahusisha matukio hayo mawili. Pengine ni ‘coincidence’ tu lakini ni nadra kwa Tanzania yetu kukumbwa na matukio makubwa ya kisiasa ndani ya siku moja.
Nimalizie makala hii kwa kuwasihi Watanzania wenzangu kufanya sala na dua kuombea Uchaguzi Mkuu ufanyike na kuhitimishwa kwa amani na usalama.
Kauli zinazoashiria kuchochea machafuko sio tu ziepukwe bali pia zikemewe vikali. 
Tukumbuke kuwa, wakati uchaguzi utafanyika na kupita, Tanzania yetu ni lazima ibaki kuwa nchi moja na yenye usalama kwa kila raia wake. Waingereza wanasema; there is life after election (maisha yetu yataendelea baada ya uchaguzi), kwa hiyo ni muhimu kutotumia fito za kujengea nchi yetu kuchapana wenyewe.
Mungu ibariki Tanzania

5 Oct 2015



TAHADHARI YA PICHA YA MAITI: Mwili wa marehemu baada ya 'ajali.' Je nani aliyepiga picha hii na kuisambaza? Je lengo lilikuwa 'ushahidi kuwa amekufa kweli?'

Kumepatikana waraka ambao unadaiwa kuwa ndio uliopelekea kifo cha Mchungaji Mtikila. Awali, nilibandika maswali kadhaa kuhusu utata unaozunguka kifo hicho kiasi cha kuhisi huenda si 'Mapenzi ya Mungu' bali ni 'mkono wa mtu.' Katika waraka huo hapa chini, ukurasa wa 2,4 na 6 hazipo (sijui kwa nini)










UPDATE: Nimekutana na clip yenye sehemu ya mahojiano na Mchungaji Mtikila, akibainisha kuhusu tuhuma hizo zilizo kwenye waraka huo hapo juu 






Kwanza ni salamu zangu za rambirambi kwa Mchungaji Christopher Mtikila kama nilivyozi-post katika 'disposable website' (tovuti inayokuwa mtandaoni kwa muda tu) hapa 



Baada ya salamu hizi za rambirambi, tuelekee kwenye mada husika. Kwanza, ninaomba kukiri kwamba mara baada ya kusikia taarifa za ajali iliyopelekea kifo cha Mchungaji Mtikila, hisia yangu ya sita ilihoji 'mbona kama kuna mkono wa mtu?' Ninadhani mnakumbuka niliwahi kuzungumzia huko nyuma kuhusu 'hisia ya sita' (katika ule mfululizo wa makal za ushushushu). Siwezi kwa hakika kueleza kwanini nilipatwa na hisia hiyo lakini ilitokea tu, na imenikaa kichwani tangu muda huo.

Baadaye nikakutana na mabandiko yafuatayo huyo Jamii Forums 



 Maswali tata kifo cha Mchungaji Mtikila1. Gari yake haijaharibika kabisa na tunaaambiwa iliacha njia na kupinduka tunajua sababu kubwa ya magari kuacha njia ni kupasuka kwa matairi lakini hili gari la Mchungaji Mtikila hakuna tairi liliposuka. Sasa tuambiwe sababu ya kuacha njia na kupinduka ni nini? 

2. Mchungaji Mtikila hana alipoumia au kubleed damu.(Labda iwe kafa kwa mshtuko wa moyo au internal wounds. Kwenye picha anaoekana hajaumia hata kidogo hata nguo alivozavaa zikiwa hazijachanika hata kidogo.Sasa tuambiwe sababu gani nyingine iliyopelekea kifo chake? 

3.Tunaambiwa ajali alipata SAA 11 alfajiri Chalinze kwaa asili ya eneo la Chalinze ni eneo bize sana kwanini picha iliyosambaa inaonesha ni asubuhi kabisa kumekucha ina maana ajali yake haikushtukiwa na watumiaji wengine wa Barabara mpaka asubuhi. 

Angalizo sijamlaumu mtu yeyote kwenye hii ajali ila ni maswali ambayo nilikuwa najiulza binafsi sasa nawaomba msichafue hali ya hewa.

Na nyingine inayorandana na hiyo 



Mazingira ya kifo cha Mchungaji Mtikila bado kinatia shaka kuu mbele ya jamii na nachelea kusema huyu Mzee ameuawa na genge la mafisadi ili wafanikiwe kisiasa kwani Mtikila alikuwa ameshakusanya vielelezo vyote vya kuwashughulikia.
1. Jeshi la Polisi Watanzania tunaomba mtusaidie kumuhoji kwa kina huyu mtu anaeitwa Mchungaji Patrick Mgaya. Huyu alikuwa ni mmoja wa waliopata ajali pamoja na marehemu Mtikila. Ikumbukwe kuwa Magaya ni mmoja wa mashabiki muhimu sana wa Mgombea Urais kupitia Ukawa ndg Edward Lowassa.Taarifa za siri zinasema kuwa Mchungaji Mgaya na Mchungaji Mtikila walikutana takribani mwezi mmoja uliopita tu na kwamba kuna wasiwasi kuwa alipewa kazi maaluum ya kuhahakisha amamuua Mtikila.


Taarifa kutoka nyumbani kwa marehemu zinasema kuwa Mchungaji Mtikila akiwa na Mchungaji Patrick Mgaya walianza safari siku ya Ijumaa jioni kwenda mkoani Njombe ambapo waliambatana na madereva wawili ambao Mchungaji Mtikila hakuwafahamu. Aliewafahamu watu hawa wote ni Mchungaji Magaya ambae ndie aliekodisha gari waliokwenda nayo Njombe kupitia kwa Ndg Victor James Manyii ambaye mbali ya kutoa gari aliyokodisha pia alitoa madereva wawili ambao pamoja na Mchungaji Mgaya wao hawakufa isipokuwa Mchungaji Mtikila pekee.


Ajali hii imeacha maswali mengi kuliko majibu. Kwa mfano ukiangalia shingo ya marehemu Mtikila utaona kuna kitu kama kamba ambayo inaweza kuleta tafsiri kuwa ilitumika kumnyonga marehemu. Pili, kwanini mwili wa marehemu hauna hata kovu wala mchirizi wowote wa damu? Je, ni nani alimpiga picha Marehemu Mtikila? Je, Patrick Mgaya ni nani? Kabla kuwa mchungaji alikuwa anafanyakazi gani? Je gari lile lilipinduka lenyewe au liligongwa? Na kama lilipinduka ni kwanini liharibike eneo la mbele pekee?Je Ni chombo gani kilikuwa cha kwanza kumpiga picha na kusambaza kwenye mitandao?
Patrick Mgaya alipopiga simu nyumbani kwa marehemu alisema wamepata ajali na kwamba kulikuwa na majeruhi wengi sana akamaliza kwa kusema mtuombee kisha akakata simu, je, hao majeruhi wengi ni akina nani? Vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama muhojini Mchungaji Patrick Mgaya maana zipo dalili kuwa kuna mengi anayoyafahamu kuhusu tukio hili. Pia fuatilieni uhusiano uliopo kati ya Rais Paul Kagame, Patrick Mgaya na EADWARD LOWASSA. Pia nashauri Jeshi la Polisi kumuhoji mtu anaeitwa Dr. Jean Bosco Ngendahimana ambae anaishi nyumbani kwa marehemu pale Mikocheni.
Wale wote wenye misimo thabiti juu ya kuchukia Rushwa na Ufisadi wachukue tahadhari. Nasema hivyo sababu Humphrey Polepole alivamiwa nyumbani kwake Mbezi na Dkt. SLAA anapokea sms za vitisho. Vyombo vya dola viwe macho.


Binafsi ninafanya jitihada za angalau kujiridhisha iwapo ajali hiyo na kifo ni 'kazi ya Mungu' au kuna mkono wa binadamu. Ila ninachofahamu ni kwamba hadi mauti yanamkuta, Mchungaji Mtikila alikuwa na 'mabomu' aliyotaraji 'kuyalipua' ndani ya siku hizi chache zilizosalia kabla ya uchaguzi.

Ukipata taarifa zozote kuhusu suala hili ninaomba uwasiliane nami kwa Twitter @chahali au Facebook facebook.com/evarist.chahali.1


23 Sept 2015

BAADA ya harakati na pilika lukuki za vyama vyetu na wanasiasa kusaka fursa ya kumrithi Rais wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete, hatimaye tumefikia takriban mwezi mmoja tu kabla ya ‘siku ya hukumu’ kutimia.
Kufikia Septemba 23, tumebakiwa na mwezi mmoja na siku mbili kabla Watanzania hawajapiga kura kumchagua rais mpya, sambamba na kuwachagua wabunge na madiwani katika uchaguzi utakaofanyika Oktoba 25, 2015.
Pengine ni mapema mno kufanya tathmini inayoweza kutoa mwelekeo wa chama kipi kitaibuka kidedea au mgombea gani wa urais atashinda, lakini angalau sote twatambua kuwa kwa upande wa urais, mshindi atakuwa aidha Dk. John Magufuli, mgombea kwa tiketi ya chama tawala CCM au Edward Lowassa, mgombea wa Ukawa kupitia Chadema.
Pamoja na changamoto nyingine zitakazomkabili mshindi katika uchaguzi huo, moja kubwa ni kuwaunganisha Watanzania kuwa kitu kimoja baada ya uchaguzi. Sio siri kwamba Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu umetugawa mno. Na sio kati ya wafuasi wa vyama pinzani tu bali hata walio ndani ya vyama husika na sie wengine tunaojitambulisha kama tusio na vyama.
Kwa upande wa CCM, mchakato wa kumpata mgombea wake umeacha makovu kama ilivyokuwa katika chaguzi zilizotangulia maara baada ya chama hicho kuruhusu ushindani katika kumpata mgombea wake. Wakati CCM ilipompitisha Rais Benjamin Mkapa mwaka 1995 kulikuwa na manung’uniko kwamba kada huyo ‘alibebwa’ na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, na ‘kuwawekea ngumu’ makada wengine Kikwete na Edward Lowassa waliokuwa wakiwania fursa hiyo pia.
Mchakato wa CCM kumpata mgombea wake katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 uliacha majeraha makubwa zaidi, hasa kwa vile Mwalimu hakuwepo kusimamia mchakato huo, na kwa upande mwingine, Rais aliyekuwa madarakani, Mkapa, ni kama alizidiwa nguvu na kundi la mtandao wa Kikwete. Uchaguzi huo uliacha mpasuko mkubwa zaidi ambao umeigubika CCM hadi muda huu.
Lakini kilichojiri katika uchaguzi wa mwaka huu ni kikubwa zaidi kiasi kwamba kwa mara ya kwanza kabisa, chama hicho tawala kinakabiliwa na upinzani mkali ambao kimsingi ni matokeo ya mpasuko uliokigubika chama hicho tangu mwaka 2005. Kwa mara ya kwanza, CCM sio tu kinakabiliwa na upinzani uliotokana na ushirikiano wa vyama mbalimbali lakini pia mpinzani wake katika nafasi ya urais ni kada wake wa zamani, Lowassa, ambaye hadi anaondoka CCM alikuwa na nguvu kubwa kabisa katika chama hicho.
Kwa upande wa vyama vikuu vya upinzani, hali kwao pia ni tofauti kwa kiasi kikubwa. Kwa mara ya kwanza vyama vikuu vitatu, Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi, vikishirikiana na NLD, vimeweza kuruka kihunzi kilichowakwaza katika kila uchaguzi, yaani kuafikiana kusimamisha mgombea mmoja. Awali, wazo zima la umoja wa vyama hivyo unaojulikana kama Ukawa, kumsimamisha mgombea mmoja lilionekana kama ndoto ya alinacha, hasa kwa kuzingatia historia. Kwamba kila jitihada iliyofanyika huko nyuma kujenga ushirikiano miongoni mwa vyama vya upinzani haukuweza kufanikia.
Lakini kadri siku zilivyokwenda, taratibu wazo la ushirikiano wa vyama hivyo likaanza kujenga picha kamili kuwa safari hii wamedhamiria kuwa kitu kimoja. Hata hivyo, kosa la msingi na ambalo pengine litawagharimu katikia uchaguzi wa mwaka huu ni kutotumia vema fursa kubwa waliokuwa nayo kukamilisha mchakato wa kumpata mgombea wao na kumnadi kabla CCM hawajafanya hivyo. Ninachomanisha hapa ni kwamba, kwa vile vyama vya upinzani vinauelewa vema mchakato wa CCM kupata mgombea wake- ni kama vita ya wenyewe kwa wenyewe ambayo waweza kudhani itakipasua chama hicho kikongwe- wangetumia fursa hiyo wao kujimmarisha na mgombea wao kiasi kwamba CCM baada ya kumpata mgombea wao wangekutana na mgombea wa Ukawa ambaye sio tu amejiandaa vya kutosha lakini pia anatambulika kwa wapigakura.
Hatimaye, kitendawili cha kwa nini Ukawa walikuwa wakisuasua kumtangaza mgombea wao kiliteguliwa baada ya Lowassa kukatwa CCM na hatimaye kujiunga na Chadema na baadaye kupitishwa kuwa mgombea urais. Kumbe muda wote tulipokuwa tunahoji kwanini Ukawa hawatangazi mgombea wao, wenzetu walikuwa wanamsubiri kitakachodondoka kutoka CCM.
Licha ya ujio wa Lowassa huko Ukawa kuonekana umeleta msisimko na matumaini makubwa kwamba angalau upinzani mwaka huu una mgombea ‘anayeweza kuisumbua CCM,’ kisichoongelewa sana ni mpasuko wa kawaida tu kati ya wanaodhani ni sahihi kumtumia Lowassa katika azma ya kuing’oa CCM madarakani na wale wanaoona kuwa suala hilo sio tu ni usaliti lakini pia linaonyesha mapungufu ya vyama hivyo vya upinzani, kwa maana ya kwamba ilivibidi visubiri mtu kutoka CCM ili kufanikisha azma yao ya kuingiza Ikulu.
Tukiweka kando mazingira ambayo CCM na Ukawa wamepitia hadi tulipo sasa, kuna mambo kadhaa yanaanza kujitokeza ambayo yanaweza kutoa taswira ya matokeo ya uchaguzi huo japo ni muhimu kutambua kuwa, kwanza, si rahisi kubashiri kwa usahihi kabisa matokeo ya uchaguzi wenye ushindani kama wa mwaka huu, na pili, kama wiki moja katika siasa ni sawa na takriban mwaka (kwa maana ya lolote laweza kutokea) muda uliosalia kabla ya uchaguzi ni kipindi kirefu kinachoweza kuathiri ubashiri wowote utakaofanyika muda huu.
Miongoni mwa mambo ya msingi yaliyojitokeza katika kampeni zinazoendelea ni pamoja na lile ambalo wana-Ukawa hawataki kabisa kulisikia, nalo ni mapungufu ya mgombea wao, yaani Lowassa. Sote twaifahamu CCM, na japo mgombea wake, Magufuli ni mgombea kama Lowassa, lakini kimsingi kwa huko Ukawa Lowassa si mgombea tu lakini yeye ndio kama Ukawa yenyewe. Kwa lugha nyingine, uchaguzi huu unakuwa kama vita kati ya CCM na Lowassa, hasa kwa sababu mgombea wa CCM anajinadi kichama zaidi ilhali Lowassa anajinadi na kunadiwa kama Lowassa zaidi.
Moja ya madhara ya wazi ya suala hilo ni uwezekano wa Ukawa kupoteza viti vingi vya ubunge kwa gharama ya kumnadi zaidi Lowassa. Niliwahi kuandika kwenye mtandao wa kijamii wa twitter kuwa nina wasiwasi kuwa mmoja au hata wawili wa viongozi wakuu wa vyama vinavyounda Ukawa kwa upande wa Bara, yaani Freeman Mbowe wa Chadema, James Mbatia wa NCCR-Mageuzi na Emmanuel Makaidi wa NLD, anaweza kushindwa katika uchaguzi huo. Pamoja nao ni viongozi wengine wakuu wa vyama hivyo ambao pia ni wabunge, hususan kwa upande wa Chadema.
Iwapo hilo litamtokea, na iwapo Ukawa watashindwa, basi hatma ya vyama hivyo itakuwa mbaya. Kwa Chadema, yayumkinika kuhisi kuwa salama yake pekee ni kufanikiwa kwa jaribio (experiment) la kumtumia Lowassa kuiong’a CCM. Ikishindwa, kuna uwezekano mkubwa chama hicho kikaingia katika mgogoro wa ‘kumsaka mchawi’ ambao waweza kutishia uhai wa chama hicho kilichokubali kutelekeza ajenda yake ya kupambana na ufisadi ili kumtengenezea mazingira mazuri Lowassa.
Kwa NCCR-Mageuzi, ili Mbatia aendelee kubaki kiongozi wa chama hicho itambidi lazima ashinde ubunge anaowania huku akitegemea Lowassa kushinda urais. Kinyume cha hapo yeye na chama chake watakuwa matatani, na hatma ya uhai wa chama hicho kuwa tete. Angalau kwa NLD, Makaidi anaweza kuendelea kuwa kiongozi wa chama hicho hasa ikizingatiwa kuwa kwa muda mrefu ‘chama hicho kimekuwa ni yeye na yeye ndio chama hicho,’ angalau kwa mwonekano.
Lakini kubwa zaidi ni upungufu wa Lowassa kisera na kujinadi. Ajenda ya mabadiliko imekuwa shaghala baghala kiasi kwamba watu wanaimba na kuhubiri mabadiliko pasipo hata kubainisha yatakuwaje. Ukiuliza unaambiwa la muhimu ni kuiondoa CCM kwanza, mengine baadaye. Baadaye lini? Hakuna mwenye jibu.
Kwa upande mwingine, Lowassa ameshindwa kabisa kujinadi. Haiingii akilini kuona umati mkubwa unaojitokeza kwenye mikutano yake ya kampeni ukiishia kuambulia hotuba ya dakika chache tu. Sawa, tumeshasikia hotuba nyingi za wanasiasa na nyingi zimebaki kuwa hotuba tu pasi kubadilisha chochote, lakini huu ni wakati wa uchaguzi, na hotuba ya mgombea ni fursa nzuri ya kubainisha nini atawafanyia wapiga kura na wananchi kwa ujumla pindi wakimchagua. Laiti Lowassa angetumia vema ‘mafuriko’ ya wanaojitokeza kumsikiliza, basi hata hiyo utata kuhusu ajenda ya mabadiliko isingekuwepo kwani angeweza kuwaeleza Watanzania kwa undani kuhusu suala hilo.
Kwa upande wa CCM, licha ya mgombea wake kusimama kama mgombea anayewakilisha chama na si ‘mtu binafsi,’ mtihani mkubwa umekuwa ni jinsi ya kumshambulia Lowassa pasipo kumjengea huruma kwa wapigakura. Lakini mtihani mwingine umekuwa ni kipi hasa cha kukizungumzia kuhusu Lowassa na Ukawa ambao kwa kiasi kikubwa wananadi ajenda ya mabadiliko pasi kuielezea kwa undani. Kwa kutambua hilo, Magufuli amekuwa akijinadi kwa kutumia rekodi yake mwenyewe na zile za chama chake badala ya kuelekeza mashambulizi kwa mpinzani wake. Ni wazi, ili umshambulie mpinzani wako basi angalau awe na cha maana cha kukishambulia, vinginevyo yaweza kutafsiriwa kama uonevu.
Nimalizie makala hii kwa ahadi ya kuendelea na uchambuzi zaidi kuhusu Uchaguzi Mkuu, kwa matarajio ya kuwa na nafasi nzuri ya kufanya ubashiri wa matokeo angalau siku chache kabla ya uchaguzi huo, sambamba na kukumbushana wajibu wetu kijamii kuutumia uchaguzi huo kama fursa ya kuboresha mustakabali wa Tanzania yetu.

10 Sept 2015

ANGALIZO: Makala hii iliandikwa kwa ajili ya kuchapishwa katika toleo la wiki iliyopita lakini haikuchapishwa kutokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu. 

HATIMAYE ‘wapinzani wakuu’ katika Uchaguzi Mkuu ujao, yaani chama tawala CCM na Ukawa wamefanikiwa kuzindua rasmi kampeni zao na kuwaeleza wapigakura nini watarajie kutoka kwa vyama hivyo.
Kabla ya kuingia kwa undani kuchambua uzinduzi wa kampeni za vyama hivyo pamoja na ilani zao, ningependa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kwamba historia inaandikwa katika Uchaguzi Mkuu huu. Mie ni mpenzi wa teknolojia, na kubahatika kwangu kuwa huku kwa wenzetu ambao teknolojia sasa ni sehemu ya maisha yao ya kila siku, sio tu kumeniongezea mapenzi hayo bali kutamani isambae katika sehemu mbalimbali duniani.
Kwa mara ya kwanza kabisa, teknolojia imekuwa na mchango muhimu katika historia ya chaguzi nchini Tanzania. Pengine hili halionekani sana kwa wenzetu mlio huko nyumbani, lakini kwa sie tulio mbali, teknolojia imekuwa ikituwezesha kufuatilia mengi ya yanayojiri katika pilika za uchaguzi kana kwamba yanatokea huku tulipo muda huu.

Na eneo la teknolojia ambalo linahusika zaidi na habari za harakati za uchaguzi huko nyumbani ni kile kinachofahamika kitaalam kama Web 2.0, yaani maendeleo ya teknolojia ya mtandaoni yanayohusisha vitu vinavyowekwa mtandaoni na watumiaji wa kawaida. Tumeingia katika zama ambapo badala ya kusubiri taarifa ya habari ya Redio Tanzania enzi zile, sasa mtu aliyepo Ifakara, kwa mfano, anaweza kutuma habari mtandaoni na ikapatikana dunia nzima.
Teknolojia inawezesha habari mbalimbali za uchaguzi kupatikana katika namna inayofahamika kama ‘in real time’ yani kitu kinatokea na kuripotiwa muda huo huo na kuwafikia wasomaji/watazamaji/wasikilizaji muda huo huo.
Licha ya Katiba yetu kutunyima fursa Watanzania tulio nje ya nchi, teknolojia imetuwezesha kushiriki katika siasa zinazohusiana na uchaguzi huu kwani baadhi yetu tunaweza kumudu kuandika habari zinazohusu kana kwamba tupo huko, ingawa ukweli ni kutokana na kufuatilia kinachoendelea huko kupitia mtandaoni. Ni katika mazingira hayo, wakati huu nimekuwa nikiandika kitabu kuhusu uchaguzi huo (kinatarajia kuchapishwa mwezi huu) kwa kutegemea taarifa na habari zilizopatikana kupitia teknolojia ya mtandao kwa takriban asilimia 100.
Tukiachana na tukio hilo la kihistoria, uzinduzi wa kampeni za CCM na Ukawa umeweza kupigia mstari hisia zilizokuwepo awali kwamba Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu una upinzani ambao kwa hakika haijawahi kutokea katika historia ya taifa letu. Cha kusikitishwa, hata hivyo, ni kwamba badala ya ushindani huo kuelemea kwenye sera, suala lililogusa wengi, angalau huko mtandaoni, ni idadi ya wahudhuriaji.
Badala ya wafuasi kushindana kuhusu ubora au mapungufu ya sera, suala liloonekana muhimu zaidi ni ‘uzinduzi wa nani uliohudhuriwa na watu wengi zaidi.’ Lakini hili si la kushangaza sana kwa tunaofuatilia mengi ya yanayoendelea huko nyumbani. Watanzania wengi wanaendeshwa na matukio. Na kibaya zaidi, ni wepesi wa kusahau. Kwa wana-CCM, wingi wa watu kwenye uzinduzi wa kampeni zao waonekane ni kila kitu bila kujali iwapo chama chao kimebadilika na kutambua kuwa kina deni kubwa kutoka kampeni na awamu zilizotangulia.
Kwa wana-Ukawa, hali sio tofauti. Wanaonekana kupuuzia ukweli kuwa hata katika chaguzi zilizopita, walikuwa wakipata umati mkubwa katika kampeni zao lakini haukuweza kuwasaidia kushinda nafasi ya urais.
Uzoefu watuonyesha kuwa uzinduzi wa kampeni huwa fursa nzuri kwa chama husika kuelezea japo kwa ufupi kuhusu mipango yake ya kuwatumikia wananchi iwapo kitapewa ridhaa ya kuwaongoza. Kwa kulinganisha uzinduzi wa kampeni za CCM na Ukawa, yayumkinika kuhitimisha kuwa Magufuli alimudu kuelezea japo kwa kifupi kuhusu ilani ya chama chake, na pengine kutoa mwanga kwa wapigakura watarajie nini kutoka kwake iwapo atashinda uchaguzi huo.
Lowassa, kwa upande mwingine, ameshindwa kufuta ‘tuhuma’ dhidi yake kwamba amekuwa akishindwa kutumia vema fursa ya umati mkubwa unaojitokeza kumsikiliza, na hotuba zake zimekuwa fupi mno.
Japo ‘watetezi wa Lowassa’ wanadai kuwa kinachohitajika si hotuba ndefu au maneno mengi bali vitendo, lakini utetezi huo hauondoi hisia kwamba mwanasiasa huyo ana upungufu katika kubainisha kwa maneno mpiango au mikakati yake. Ni muhimu kutambua kuwa asilimia kubwa ya wapiga kura sio wanachama au wafuasi wa vyama vya siasa, na moja ya vityu vinavyoweza kuwasaidia kufanya uamuzi kuhusu nani wampe kura yao ni yanayobainishwa katika hotuba za wagombea.
Lakini kingine ambacho ninaweza kukieleza kama kosa la kimkakati ni maelezo ya Ukawa kupitia Chadema kuwa ilani yao itawekwa kwenye tovuti yao. Ndio, nimebainisha hapo juu kuhusu mchango wa teknolojia katika uchaguzi mkuu huu. Hata hivyo, takwimu za hivi karibuni zaonyesha kuwa ni takribani Watanzania milioni nane tu wenye kuweza kupata huduma (access) ya Intaneti. Na tukichukulia makadirio ya idadi ya sasa ya Watanzania kuwa ni watu milioni 50 (ninasisitiza ni makadirio tu), basi takriban watu milioni 40 hawataiona ilani ya uchaguzi ya Ukawa/Chadema kwa vile hawana Intaneti.
Na hadi muda huu ninapoandika makala hii, kilichopo kwenye tovuti ya Chadema ni hotuba tu ya Lowassa aliyoitoa siku ya uzninduzi wa kampeni. Nimejaribu kuuliza iwapo hotuba hiyo ndio ilani ya Chadema/Ukawa lakini sijapewa jibu.
Kwa upande wa CCM, bado ninaona kuna tatizo la kuendeleza ahadi badala ya kukiri makosa katika maeneo ambayo, baadhi yetu twaamini yamechangia kuimarisha vyama vya upinzani kama vile Chadema. Chama hicho tawala kinapaswa kutambua kwamba hali ya nchi yetu sio nzuri, na binafsi ninaiona hiyo ndio sababu kuu ya sapoti kubwa anayopata Lowassa: imani ya wanaomuunga mkono kwamba “hata kama ana mapungufu yake, atatusaidia kuiondoa CCM madarakani.”
Hadi muda huu sijaona jitihada za maana kwa Magufuli na CCM kuwa honest kwa Watanzania kwa kuwaeleza bila ‘kuuma maneno’ kuwa “jamanai, hapa tulikosea na tunakiri makosa. Ili kurekebisha makosa hayo na kutoyarudia tena, tutafanya hili na lile.” Hatua ya kwanza ya kuondoa tatizo ni kulitambua na kulibainisha, kisha kuandaa mkakati wa kuliondoa. Kukiri kosa si upungufu bali dalili ya uelewa wa changamoto zinazomkabili mhusika.
Lakini Lowassa na Ukawa yake wasitegemee sana hisia kuwa ‘upungufu wa CCM, ni ubora wao.’ Laiti CCM wakifanikiwa kubainisha upungufu wao na kueleza jinsi watakavyoyakabili, Ukawa watalazimika kuwaeleza Watanzania nini wao watakifanya bila kujali CCM wanasema nini.
Wakati Magufuli na CCM wameendeleza mlolongo wa ahadi zilezile zilizozoeleka masikioni mwa wapigakura, kuna maeneo ambayo binafsi ninayaona ‘hatari’ kwa Lowassa na Ukawa. Kwa mfano, Lowassa ametoa ahadi ya kuwaachia huru watuhumiwa wa ugaidi huko Zanzibar, jambo ambalo limepelekea moja ya Jumuiya za Kikristo kumlaumu kwa vile miongoni mwa kesi zinazowakabili watuhumiwa hao ni ya mauaji ya padre huko Visiwani. Kutafuta pointi rahisi za kisiasa kwaweza kuwa na madhara makubwa kwa mwanasiasa.
Nimalizie makala hii kwa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuwa watumie fursa hii ya kampeni kuwapima kwa makini wagombea wote, si wa urais tu bali pia katika nafasi za ubunge na udiwani, na kuwachagua wale tu wanaowaamini watawatumikia kwa dhati. Pia nitumie fursa hii sio tu kukipongeza chama cha ACT Wazalendo kwa uzinduzi wa kampeni unaoweza kuhitimishwa kuwa bora zaidi ya wa CCM na ACT bali pia kuonyesha dalili kuwa chama hicho kinaweza kuwa ngome kuu ya upinzani huko mbeleni.
Nitaendelea na uchambuzi kuhusu uchaguzi mkuu katika makala zijazo.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.