6 Jan 2016

Mwaka 1981, nikiwa darasa la tatu, marehemu baba aliamua kustaafu kazi, japo alikuwa amebakiwa na miaka kama 10 hivi ya utumishi katika Shirika la Posta. Wakati huo tulikuwa tunaishi Kigoma. Marehemu baba alikuwa na ndoto za kuwa mkulima mkubwa baada ya kustaafu maana tulikuwa na hekari kama 50 hivi za mashamba ya mpunga huko Ifakara. Kwahiyo, aliamini kuwa savings zake na mafao ya kustaafu vingekuwa mtaji wa kutosha kumwezesha atimize ndoto yake hiyo.

Hata hivyo, wanasema 'kuwa na ndoto ya kitu flani ni kitu kimoja, kuitimiza ndoto hiyo ni kitu kingine kabisa.' Mwaka mmoja baada ya kustaafu na familia yetu kurudi kijijini Ifakara, hali ya uchumi ilikuwa mbaya. Tatizo kubwa lililomkabili marehemu baba ni ukubwa wa ukoo huko kijijini ambao ulimtegemea yeye kwa msaada. Na wazazi wangu, yaani marehemu baba na marehemu mama, walikuwa watu wenye huruma mno. Kwahiyo waliona kuwa hawawezi kuacha kuwasaidia ndugu na ukoo kwa ujumla kwa vile tu wana mipango ya kilimo kikubwa. Pengine si wazo la busara lakini upendo ni kitu chenye nguvu mno na kikizidi chaweza kuvuruga kila mpango.

Maisha yangu kama mwanafunzi hapo Ifakara nilipohamia darasa la tatu hadi nilipomaliza darasa la saba, yalikuwa magumu mno. Kuna nyakati tulipitisha usiku kwa kunywa uji wa chukuchuku (usio na sukari wala chumvi), kuna nyakati tulilalia ndizi bukoba za kuchemsha na kikombe cha maji tu, mlo wa mchana ulikuwa wa kubahatisha, na mara kadhaa mchana ulipita kwa kunywa maji tu. Pia kuna usiku kadhaa tuliokwenda kulala bila kutia kitu tumboni.

Nilisoma kwa shida maana hatukuwa na umeme, japo umeme ulifika Ifakara mapema kabla ya sehemu nyingi za Tanzania kwa vile mradi wa umeme wa Kidatu ulikuwa jirani na mji huo. Familia iliyokuwa inahangaika na mlo wa siku moja isingeweza kumudu gharama za umeme ambazo wakati huo zilikuwa shilingi elfu kadhaa tu. Lakini licha ya kujisomea kwa kutumia koroboi na mara moja moja taa ya chemli pale tulipoweza kumudu kununua mafuta ya taa, Mungu alinijaalia nikafaulu kidato cha nne na kupata division one. Laiti ningefeli, ndio ungekuwa mwisho wa safari yangu kielimu maana familia isingemudu kunisomesha shule ya private.

Nikachaguliwa kujiunga na high school Tabora. Namshukuru Mungu kwani shule hiyo ilikuwa ya mchepuo wa kijeshi, maana niliondoka nyumbani nikiwa na nguo chache tu lakini pale shuleni tulitumia muda mwingi tukiwa kwenye yunifomu zetu za magwanda. Na hapo shuleni nilikwenda mikono mitupu, lakini bahati nzuri marafiki walinisaidia hela za matumizi. Na sikujali sana kwa sababu milishazowea shida.

Bahati ilinijia shuleni hapo nilipofanikiwa kuchaguliwa kuwa kiranja mkuu. Kwa vile ilikuwa shule ya kijeshi, 'cheo' changu kilifahamika kama Kamanda Mkuu wa Wanafunzi, kwa kimombo Students' Chief Commander, au kwa kifupi 'Chief.' Mpaka leo baadhi ya niliosoma nao huko Tabora wameendelea kuniita 'chifu.' Kupata ukiranja mkuu Tabora Boys' ilikuwa sio kazi rahisi hata kidogo. Mfumo wa uchaguzi ulihusisha uraia na ujeshi. Sikuomba kugombea bali nilipendekezwa tu. Na kimsingi haukuwa uchaguzi as such kwa sababu final say ilikuwa ni ya utawala wa shule na maafande. Nikabahatika kupata 'wadhifa' huo nikiweka historia ya kuwa 'chifu' mwenye umri mdogo zaidi katika historia ya shule hiyo (kwa muda huo).

Uchifu ulinisaidia sana kukabiliana na ugumu wa maisha shuleni hapo kwani licha ya privileges kadhaa zilizoambatana na 'wadhifa' huo, pia nilikuwa nikipewa zawadi mbalimbali na wanafunzi wenzangu. Ndo raha za uongozi hizo.

Nilihitimu masomo yangu vizuri na kupata Division Two ya pointi 10. Ninaamini laiti nisingekuwa nakabiliwa na ugumu wa maisha, ningeweza kupata Division One nyingine.

Kutoka hapo nikaenda JKT Maramba, Tanga, na hiyo ilimaanisha maisha mengine ya kijeshi kwa mwaka mzima (ukichanganya na miaka miwili ya ujeshi Tabora Boys'). Lakini bahati ikaendelea kuwa nami kwani baada ya miezi michache tu nikateuliwa kuwa miongoni mwa vijana waliotakiwa kujiunga na Jeshi la Wananchi JWTZ kuwa marubani na mainjinia wa jeshi. Kwahiyo takriban robo tatu ya maisha yangu ya JKT yalikuwa kwenye kambi ya mafunzo ya RTS Kunduchi. Huko ilukwa ni kula na kulala tu tukisubiri utaratibu wa mchujo wa urubani na uinjinia wa jeshi. Mwishowe, sikuchaguliwa na nikarudi JKT Ruvu (kambi ya watoto wa vigogo) kumalizia muda wangu. Hapo napo maisha yalikuwa mtihani kwa sababu licha ya kambi kujaa watoto wa vigogo lakini pia ilikuwa karibu na Dar. Nashukuru Mungu nilipata marafiki kutoka familia zenye kujiweza ambao walinistiri.

Nilipomaliza nikaenda Tanga, na baada ya muda mfupi nikaajiriwa kuwa mwalimu katika sekondari ya Eckenford. Sikupata nafasi ya kujiunga na chuo kikuu mwaka huo kwa vile kwa wakati huo, kujiunga na UDSM ulihitaji Division One ya Form Six, na mie nilikuwa na Division Two ya point 10 (yani kasoro point moja tu kuwa Division One).

Nikafundisha hapo kwa miaka miwili, kisha nikateuliwa kujiunga na Idara ya Usalama wa Taifa. Jinsi nilivyoteuliwa ni kama muujiza, lakini ninahisi walikuwa wakinifuatilia tangu nilipokuwa Tabora Boys' kwa sababu kuna wakati niliwahi kutembelewa na Afisa Usalama wa Taifa wa Mkoa huo.

Baada ya mwaka mmoja wa mafunzo ya kazi hiyo, nikaingia mtaani, lakini kwa vile nilikuwa na kiu ya elimu, baada ya miezi 9  'mtaani' nikachaguliwa kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Hata hivyo, wakati nikiwa chuoni niliendelea na kazi pia. Nilipomaliza nikarudi ofisini na takriban mwaka mmoja baadaye nikapata promosheni iliyodumu hadi nilipoteuliwa kuja kusoma huku Uingereza.

Japo baadaye yalijitokeza matatizo yaliyopelekea mie kuachana na kazi hiyo, utumishi wangu wa miaka 13 mfululizo haukuwa na doa, na ninajivunia rekodi yangu. Kilichoniponza ni kukataa umimi. Tulikuwa tukilipwa vizuri kabisa, kiasi kwamba nilionekana mjinga kuanza kukosoa maovu mbalimbali yaliyopaswa kukaliwa kimya. Siku zote nilikuwa nikiwaambia maafisa wenzangu, "tusiwe wabinafsi wa kufikiria hii mishahara mikubwa na posho tunazopewa ilhali huko mtaani ndugu, jamaa na marafiki zetu wanataabika. Basi angalau tutimize wajibu wetu na si kuendeshwa na maslahi binafsi." Pengine 'kimbelembele' ndo kiliniponza. Pengine ni ujinga tu, kama baadhi ya watu walivyohitimisha. Lakini deep in my heart, naamini nilifanya kitu sahihi, yaani kusimamia nilichoamini.

Fast forward miaka kadhaa mbele, leo japo sijafanikiwa kuhitimisha safari yangu ya elimu, kwa maana ya Shahada ya Uzamifu ambayo imenichukua kitambo sasa (nililazimika kusitisha masomo kutokana na matatizo niliyokumbana nayo kati yangu na mwajiri/mdhamini wa masomo yangu yaani taasisi niliyokuwa nafanya kazi.) Panapo majaliwa, mwaka huu, jina langu litaanza na "Dokta..."

Leo hii namshukuru Mungu, nimefanikiwa kuendelea kuwatumika Watanzania wenzangu kwa kutumia maandiko yangu, kitu nilichoanza rasmi mwaka 1998. Lakini pia namshukuru sana Mungu wangu na wazazi wangu kwa kuniwezesha kupata shahada tatu, na hii ya nne ndio naihangaikia. Nimepita katika vipindi vigumu mno, kulala na njaa, kusoma kwa koroboi, na kushindwa kuishi kama vijana wenzangu kwa vile nilitoka familia masikini.

Bahati nzuri, nikiwa hapa Uingereza, nilivutowa pia na wazo la kufanya kazi za kujitolea (volunteering). Na baadaye niliajiriwa kwenye taasisi zinazoshughulikia masuala ya wakimbizi. Fursa hizi zimeniwezesha kukutana na watu kutoka sehemu mbalimbali duniani, kutoka Somalia hadi Iraki, Venezuela hadi China, Zimbabwe hadi Kuwait, Eritrea hadi Sri Lanka. Nimejifunza mila na utamaduni wa mataifa mbalimbali. Lakini pengine kubwa zaidi, nimeweza kuwasaidia mamia na pengine maelfu ya watu waliokuja hapa kusaka ukimbizi. Laiti dua na sala zingekuwa zampatia mtu utajiri hapo kwa hapo, basi leo hii ningekuwa bilionea maana nimepata nyingi mno kwa kuwasaidia watu hao ambao wengi walikuja hapa kuokoa maisha yao.

Kwanini nimeandika yote haya? Kwa sababu licha ya kila shida niliyopata katika masiha ya umasikini niliokulia, nilijifunza kuhusu utu. Nimejifunza mengi kuhusu wale waliojinyima kwa ajili yangu, waliogawana nami kidogo walichokuwa nacho, walionishirikisha katika utajiri wa familia zao, walionijali licha ya kutoka familia masikini. Na pia nimejifunza kuwa wema hauozi. Mamia kwa maelfu ya wakimbizi niliowasaidia hapa Uingereza, ninapokutana nao mpaka natamani kujificha kwa jinsi wanavyonimwagia shukrani, sala na dua. Nimejifunza kuhusu utu.

Leo ninamiliki kampuni japo ndo imeanza tu mwezi uliopita. Jana nilikutana na mwalimu wangu (mentor) wa masuala ya biashara, akaniuliza  matarajio yangu kwa mwaka huu 2016. Nijamjibu kwa utani "ninataka hadi kufikia mwisho wa mwaka huu niwe nimetengeneza paundi milioni moja za kwanza kwa kampuni yangu..." kisha nikacheka. Hakupendezwa na kicheko hicho.Akaniambia "japo unaona kama mzaha, lakini una kila nyenzo ya kukuwezesha kutimiza hilo. Cha muhimu, amini katika uwezo wako wa kiakili, upeo wako mkubwa, na historia yako ulivyotoka kwenye umasikini hadi kufikia hapa." Hawa 'wazungu' hawana tabia ya kumpa mtu sifa asizostahili. Kama wewe ni 'bomu' watakwambia, kama wewe ni mzuri watakwambia. Hakuna 'kuzugana.'

Huko nilikotoka na nilikopitia ndo kwanifanya kuwa mtu niliye leo: namchukulia kila mtu kuwa ana thamani yake. Siangalii tofauti ya kielimu kama sababu ya kumdharau mtu ambaye hakubahatika kuelimika sana. Digrii zangu hazina thamani kama sina utu. Kidogo ninachomudu kukipata hapa (ambacho pengine ni kikubwa sana kwa shilingi yetu huko nyumbani) hakinifanyi kujiona tofauti na wanaopata pungufu ya changu.

Namshukuru Mungu kwa baraka zake, nawashaukuru marehemu wazazi wangu kwa kunifundisha kuwa humble (mtu asiyejikweza) na kuwa mtu wa msaada, nawashukuru wote walioniwezesha kupitia safari yangu ndefu iliyojaa milima na mabonde, hasa wale walionifundisha kujali utu badala ya kitu.

Kwa sie Wakristo, tunafundishwa katika Biblia Takatifu kuwa 'wajikwezao watashushwa, na wajishushao watakwezwa.' Naomwomba Mungu aniwezesha kuwa mtu niliye leo hata nikitokea kufanikiwa kimaisha kiasi gani. 

Ndoto yangu ya utotoni ni kuwa daktari wa utabibu ili niweze kuwasaidia watu wengi kadri iwezekanavyo. Bahati mbaya sikufanikiwa. Ndoto yangu ya pili ilikuwa kuwa shushushu (kwa hamasa za Willy Gamba), nilifanikiwa kuitimiza, nikalitumikia taifa langu kwa nguvu zangu zote. Bahati mbaya mambo yakaenda 'kushoto.' Ndoto yangu ya sasa ni kutumia elimu, kipaji, ujuzi na uzoefu wangu kuendelea kuwasaidia watu wengine hususan wale wanaoishi katika hali kama niliyokulia. 

Ninatumaini msomaji mpendwa waweza kujifunza kitu kimoja au viwili katika stori hii.

Happy new year!


2 Jan 2016



Heri ya mwaka mpya. Nina furaha kuwafahamisha kuwa kitabu kipya, "Dokta John Pombe Magufuli: Safari ya Urais, Mafaniko na Changamoto katika Urais wake" sasa kinapatikana. Kitabu hiki ni mfululizo wa vitabu kadhaa ninavyotarajia kuvichapisha mwaka huu 2016. 

Wakati kitabu hiki kikiingia sokoni, kitabu kingine kuhusu taaluluma ya Usalama wa Taifa kipo katika hatua za mwisho, na matarajio ni kukiingiza sokoni mwishoni mwa mwezi huu.

Kitabu hiki cha Dokta Magufuli kina sura sita. Katika utangulizi, kitabu kinazungumzia mazingira ya uchaguzi mkuu uliopita, msisitizo ukiwa kwenye hali ya nchi ilivyokuwa kabla ya uchaguzi huo.

Kadhalika, utangulizi huo unaelezea mabadiliko ya ghalfa ya kisiasa, hususan ndani ya CCM, yaliyojitokeza kufuatia jina la mwanasiasa aliyekuwa maarufu kuliko wote wakati huo, Edward Lowassa, kukatwa na chama hicho tawala wakati wa mchakato wa kupata mgombea wake wa kiti cha urais.

Sura ya kwanza inamtambulisha Dokta Magufuli, kwa kuangalia historia fupi ya maisha yake. Sura ya pili inaeleza mchakato aliopitia Dkt Magufuli hadi kuibuka mgombea wa urais kwa tiketi ya CCM. Sura hii inachambua kwa undani ushindani miongoni mwa makada zaidi ya 40 waliochukua fomu kuwania urais kupitia chama hicho.

Sura ya tatu inaelezea fursa alizokuwa Dokta Magufuli na CCM kwa ujumla katika kipindi cha kampeni na uchaguzi mzima kwa ujumla. Sura hii inachambua uimara wa mwanasiasa huyo sambamba na turufu za kawaida za CCM katika kila uchaguzi. Kwa uapnde mwingine sura hiyo yaangalia pia mapungufu yaliyopelekea urahisi kwa Dokta Magufuli kumshinda mpinzani wake mkuu Lowassa, sambamba na mapungufu ya UKAWA yaliyoiwezesha CCM kushinda.

Sura ya nne inajadili changamoto na vikwazo kwa Dokta Magufuli na CCM kwa ujumla wakati wa kampeni. Kadhalika, sura hii inazungumzia jinsi Lowassa na UKAWA walivyoshindwa kutumia changamoto hizo za wapinzani wao.

Sura ya tano inajadili urais wa Dokta Magufuli tangu aingie Ikulu, wakati sura ya mwisho inajadili changamoto zinazoukabili urais wake na kutoa mapendekezo.

Nimejitahidi kadri nilivyoweza kuandika kitabu hicho kama mtu niliyeufuatilia uchaguzi huo kwa karibu. Natambua kuna wanaoweza kuwa na hofu kuwa 'niliisapoti CCM na Dokta Magufuli wakati wa kampeni, na kutoiunga mkono UKAWA na Lowassa.' Naomba kuwatoa hofu kwani kitabu hiki ni si cha kiitikadi bali kwa ajili ya Watanzania wote bila kujali tofauti zao za kiitikadi.

UTAKIPATAJE?

Bei ya kitabu sasa ni Shilingi 4,000 tu. Ili kukipata, nunua kwa M-PESA namba 0744-313-200 jina JOHN ZABLON MPEFO au TIGO-PESA namba 0652-112-071 jina CHRISTINE JOHN MANONGI

KARIBUNI SANA

31 Dec 2015

KUTOKANA na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu, wiki mbili zilizopita nilishindwa kuwaletea makala kwenye safu hii. Hata hivyo, kwa bahati nzuri nilichopanga kuandika katika makala hiyo kimechukua sura mpya kati ya wiki iliyopita na muda huu ninapoandika makala hii.
Nilidhamiria kuzungumzia maoni ya wananchi mbalimbali kuhusu uteuzi wa baraza la mawaziri la Rais Dk. John Magufuli. Kimsingi, japo baraza hilo limepokelewa na wengi kama linaloweza kumsaidia Rais kutekeleza kauli-mbiu yake ya ‘Hapa ni Kazi Tu,’ baadhi ya sura zilizomo kwenye baraza hilo zilionekana kama zinazoweza kuwa kikwazo.
Uteuzi ulionekana kuwagusa wengi ulikuwa wa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo. Nikiri kwamba nami nilikuwa miongoni mwa walioshtushwa na uteuzi huo japo tetesi ziliashiria mapema kuhusu uwezekano wa msomi huyo kuwamo katika baraza hilo jipya.
Wakati wengi waliohoji kuhusu Profesa Muhongo kupewa uwaziri walielemea kwenye ukweli kwamba alilazimika kujiuzulu katika Serikali ya Rais Jakaya Kikwete kutokana na kashfa ya Tegeta Escrow, binafsi nimeendelea kutatizwa na kauli yake ‘ya dharau’ kuwa Watanzania hawana uwezo wa uwekezaji mkubwa, na wanachomudu ni biashara ya juisi tu.

Kwa bahati mbaya au pengine kwa makusudi, Profesa Muhongo hajawahi kuona haja ya kuifuta kauli hiyo au pengine japo kujaribu kuifafanua. Wanaomfahamu, wanadai ni mchapakazi mzuri. Lakini kwa kuzingatia taratibu za ajira kwa hapa Uingereza, miongoni mwa sifa za uchapakazi ni uhusiano mwema na watu (people skills) na uwezo wa kuwasiliana nao kwa ufanisi (communication skills).
Ili uchapakazi ulete ufanisi, ni lazima mtendaji amudu kuelewana na watu wengine, kwa maana ya uhusiano bora unaojali utu na heshima. Kadhalika, ni muhimu kwa mhusika kuweza kuwasiliana nao kwa ufanisi. Sasa, kiongozi anayedharau uwezo wa wenzake, kama hiyo kauli ya Muhongo kuwa uwezo wa Watanzania katika uwekezaji unaishia kwenye kuuza juisi tu, anajiweka katika wakati mgumu katika utendaji kazi wake.
Hata hivyo, kwa bahati nzuri inaelekea Profesa Muhongo ameanza kubadilika. Majuzi, nilikutana na habari inayomhusu na ambayo ilinipa faraja kubwa. Alinukuliwa na vyombo vya habari vya huko nyumbani akihamasisha Watanzania wazawa kujitokeza na kushiriki kuwekeza katika sekta ya umeme.
Kwa tafsiri ya haraka, ni wazi kauli hiyo inaashiria kuwa Profesa Muhongo sasa ana imani na Watanzania, kwamba wanaweza kuwekeza sio kwenye biashara ya juisi pekee bali hata kwenye sekta ya umeme.
Japo hajaomba radhi wala kutolea ufafanuzi kauli hiyo ya awali, kuna umuhimu wa kuangalia suala hilo katika mtizamo wa ‘yaliyopita si ndwele, tugange yaliyopo na yajayo.’
Rai hiyo ya Waziri Muhongo kuwataka wazawa wajitokeze kuwekeza katika sekta ya umeme ni ya kizalendo na inaendana na jitihada zinazofanywa na nchi kama Nigeria na Rwanda ambazo zimekuwa zikihamasisha sana wazawa kujitokeza na kushiriki kwenye uwekezaji katika sekta mbalimbali, badala ya kuliacha suala la uwekezaji kuwa la wageni tu.
Lakini wakati Profesa Muhongo ‘akijisafisha,’ kwa bahati mbaya kuna Waziri mwingine mpya ameanza kuonyesha mkanganyiko katika kauli zake, hali inayoleta wasiwasi iwapo anamudu kuendana na kaulimbiu ya ‘Hapa ni Kazi Tu.’
Mwishoni mwa wiki mbil zilizopita. Vyombo vya habari vya huko nyumbani vilimnukuu Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga, akiutaka uongozi wa Jeshi la Polisi kumfikishia taarifa kuhusu tatizo sugu la biashara haramu ya dawa za kulevya. Kauli hiyo ya waziri iliamsha furaha na matumaini kwa Watanzania wengi, hususan katika mitandao ya kijamii.
Cha kushangaza, baada ya hapo, Waziri Kitwanga alinukuliwa akitoa kauli za kuvunja moyo ambapo alidai, namnukuu, “Sina listi ya wauza dawa za kulevya, na orodha hainisaidii zaidi ya kuwa na mfumo mzuri wa kuyadhibiti.” Hivi hizo dawa za kulevya zinajiuza zenyewe au kuna watu wanaohusika kuziingiza au kuzisafirisha? Kama kuna wahusika, iweje waziri adai orodha ya wahusika haimsaidii katika jitihada za kudhibiti biashara hiyo haramu inayogharimu maisha ya vijana wengi wanaoyatumia?
Na kauli yake kwamba hana orodha inaashiria upungufu wake. Anataka orodha ijilete yenyewe ofisini kwake? Angejihangaisha kidogo tu kwenda mtandaoni au kupitia mafaili ya Jeshi la Polisi hususan Kitengo cha Dawa za Kulevya au huko Usalama wa Taifa, angeweza kupata kirahisi orodha hiyo. Binafsi, ilinichukua dakika mbili tu kwenye Google kukutana na orodha kadhaa za wanaotuhumiwa kujihusisha na biashara hiyo.
Waziri Kitwanga aliendelea kudai, namnukuu, “Sijui kama Rais alipewa orodha, hajawahi kuniambia ila kama mna ushahidi mnisaidie nilifanyie kazi.” Japo ni mapema mno kumhukumu, lakini kauli hii haiendani kabisa na kaulimbiu ya Dk. Magufuli ya ‘Hapa ni Kazi Tu.’ Kama Waziri Kitwanga hajui iwapo Rais alipewa orodha hiyo, na kama hajamwambia, kwa nini asimuulize bosi wake iwapo yeye Waziri ana dhamira ya kweli kushughulikia suala hilo?
Halafu kwa vile katika nukuu ya kwanza ametanabaisha kuwa orodha hiyo
(ya wahusika katika biashara ya dawa za kulevya) haimsaidii katika jitihada za kuidhibiti biashara hiyo, sasa anataka wananchi wamsaidieje? Na pengine kinachovunja moyo zaidi ni hilo la kudai ushahidi. Si kazi ya wananchi kutafuta ushahidi kwani kuna watendaji wanaolipwa mishahara kwa ajili ya kazi hiyo. Na hata ingekuwa ni jukumu la wananchi, Waziri Kitwanga si raia wa kigeni, ni mwananchi pia, na kwa maana hiyo wito wake kwa wananchi unamhusu yeye pia.

Moja ya vikwazo vyetu katika matatizo mengi yanayoikabili nchi yetu ni ukosefu wa nia ya dhati ya kupambana na matatizo husika. Sambamba na hilo ni kukosekana kwa ubunifu. Laiti Waziri Kitwanga angekuwa mbunifu, asingekurupuka kutoa kauli hizo za juzi kwani kimsingi zinahusu majukumu ambayo Watanzania na Rais Dk. Magufuli wanataraji ayatekeleze kwa ufanisi.
Katika hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge jipya, Rais Magufuli alieleza bayana kuwa vita dhidi ya ufisadi, rushwa na dawa za kulevya ni ngumu na hatari kwani inahusisha wakubwa. Na wiki mbili zilizopita, Waziri Kitwanga alinukuliwa akijigamba kwamba hahofii kufa (akimaanisha kuwa hatishwi na nguvu kubwa ya wahusika katika biashara hiyo ya dawa za kulevya). Lakini kauli zake katika siku zilizofuata zinaweza kujenga picha ya mtendaji mwenye hofu ya kukabiliana na tatizo hilo.
Wengi tunaitakia kila jema Serikali ya Rais Magufuli, na makala hii inatekeleza hilo lakini kwa kukosoa upungufu uliojitokeza. Kama kweli tuna nia ya kumsaidia Rais wetu na serikali yake, basi tusiishie kusifia tu bali pia kukosoa pale inapobidi.
Nimalizie makala hii kwa ushauri kwa Waziri Kitwanga, mamlaka zinazohusika na suala la dawa za kulevya na serikali kwa ujumla: ni vigumu kuwakamata wahusika wakuu wa dawa za kulevya kwa urahisi. Wanatumia mbinu nyingi ikiwa ni pamoja na kuficha au kuharibu ushahidi. Moja ya njia zilizoonyesha mafanikio sehemu mbalimbali duniani ni kuwabana wahusika kwa ukwepaji kodi na kile Waingereza wanaita ‘proceeds of crime,’ yaani mali zilizopatikana kutokana na uhalifu. Njia hiyo sio tu husaidia kuwapunguzia wauza dawa za kulevya uwezo wao kifedha, lakini pia huwezesha kubaini utajiri wao ulivyopatikana (na hivyo kuleta uwezekano wa kubaini uhusika wao katika biashara haramu) na pia kuwalipisha fidia kutokana na maovu yao.
Penye nia pana njia, pasipo na nia pana visingizio



25 Dec 2015

11 Dec 2015

Julai 8 mwaka huu itabaki moja ya siku zenye kumbukumbu chungu maishani mwangu. Ni siku ambayo baba yangu mzazi, Mzee Philemon Chahali alifariki dunia baada ya kuugua kama kwa wiki hivi.  Japo miaka 7 kabla ya hapo nilikumbwa na msiba mwingine ambapo mama yangu mepndwa, Adelina Mapango, alifariki baada ya kupoteza fahamu kwa zaidi ya miezi mitano, na japo hakuna msiba wenye nafuu, lakini angalau marehemu mama alifariki nikiwa huo Tanzania nilikoenda kumuuguza.  Lakini katika kifo cha baba, kilitokea nikiwa mbali na nyumbani. Na kwa hakika, nyakati za misiba, tunahitaji mno sapoti ya wenzetu kutuliwaza na kukabiliana na uchungu wa kufiwa.

Kwanini ninarejea habari hiyo ya kuskitisha? Kwa sababu tukio hilo ndilo lilinipa nafasi ya kumfahamu vema zaidi mmoja wa wanasiasa maarufu nchini Tanzania, January Makamba, Mbunge wa CCM Bumbuli na mmoja wa makada zaidi ya 40 waliojitokeza kuwania Urais kupitia CCM, na alifanikiwa kuingia katika 'Tano Bora.'

Mara baada ya kutangaza kuwa nimefiwa, January alinipigia simu kunipa pole, na kuulizia jinsi ya kuwasilisha rambirambi yake, ambayo baadaye aliiwasilisha. Pengine kwa watu wengine wanaweza kuliona hili kama ni jambo dogo tu na la kawaida. Lakini kimsingi, sote twafahamu viongozi wetu walivyo busy na majukumu yao, ambayo kwa kiasi kikubwa huwafanya waonekane kama binadamu wasiofikika (inaccessible). Kwa Afrika, ni vigumu sana kukuta kiongozi awe wa kisiasa au kwenye sekta nyingine akiwa karibu na raia wa kawaida, au kufuatilia yanayowasibu. Na kwa wanaomfahamu, amekuwa akiwasaidia watu wengi waliofiwa na wenye matatizo mbalimbali, at least ninaowafamu mie mtandaoni. Ni wazi mtu akiwa mwema kwa watu mtandaoni lazima pia ni mwema katika maisha yake nje ya mtandao.

Nimeanza makala hii na suala hilo binafsi kwa sababu ndilo lililonipa fursa ya kumfahamu kwa karibu zaidi. Awali nilimfahamu kama mwanasiasa kijana aliye karibu na watu wengi, hususan mitandaoni, lakini sikujua 'human side' (utu) yake. 

Tukiweka hilo kando, katika siasa za hivi karibuni za Tanzania, January alikuwa mwanasiasa wa kwanza kabisa kutangaza azma yake ya kuwania urais mwaka huu. Alitoa nia yake takriban mwaka mzima kabla ya kuanza rasmi kwa mchakato huo. Wengi walipokea tamko lake hilo, hasa kwa matarajio kuwa lingewashawishi wanasiasa wengine waliokuwa wanawania nafasi hiyo kujitokeza, na hiyo ingesaidia kuwafahamu vizuri. Kwa hiyo, kwa kifupi, January ndiye aliyepuliza rasmi kipenga cha kuwania urais wa awamu ya tano/

Wakati ukaribu wa mwanasiasa huyo kijana na wananchi, hususan katika mitandao ya kijamii ilikuwa ni turufu yake muhimu, moja ya downsides za kufahamiana na watu wengi ni uwezekano wa baadhi ya 'wakorofi' kujipa uhuru wa kusema chochote kile hata isipostahili. Na katika hili, January alikumbana na mengi: wapo waliomdhihaki wakiona dhamira yake ya urais kama ndoto tu, kashfa zisizostahili, nk. Hata hivyo, mara zote alimudu kuwajibu 'wapinzani' wake kwa lugha ya kistaarabu.

Baadaye alichapisha kitabu chake kilichokuwa na visheni yake ya urais. Again, kitabu hicho kilipokelewa kwa mtizamo chanya na Watanzania wengi japo kulikuwa na kundi dogo 'waliokiponda.' Kimsingi, kitabu hicho kilikuwa na masuala mengi ya msingi kuhusu matatizo ya Tanzania yetu na mikakati ya kuyakabili. Kwahiyo, kinaweza kabisa kuwasaidia watu mbalimbali wanaotaka kuifahamu vema nchi yetu.

Mchakato wa CCM kumpata mgombea wake ulipoanza rasmi, January aliibuka kuwa mwanasiasa pekee tishio kwa Edward Lowassa, kada amabye alitajwa kuutaka urais kwa miaka kadhaa. Tofauti na Lowassa ambaye umaarufu wake ulichangiwa zaidi na uwezo wake wa kifedha, mafanikio ya January katika kampeni yake yalichangiwa zaidi na ukaribu wake kwa watu, hususan vijana.

Na japo hakufanikiwa kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, kuingia kwake kwenye 'Tano Bora' ni mafaniko makubwa kabisa, hasa ikizingatiwa kuwa bado ni kijana anayeweza kuyatumia mafanikio yake ya mwaka huu katika chaguzi zijazo. Yayumkinika kuhitimisha kuwa mwanasiasa pekee ambaye mpaka muda huu anatajwa kuwa rais ajaye wa Tanzania baada ya Magufuli ni January.

Baada ya Magufuli kushinda urais, zikaanza tetesi kuwa 'January anataka Uwaziri Mkuu.' Ni muhimu kukumbuka kuwa katika muda mwingi wa harakati zake za kisiasa, mwanasiasa huyo amekuwa akiandamwa na 'wasemaji wasio rasmi' wanaojifanya kumjua zaidi ya anavyojijua mwenyewe. Hakuna wakati au mahali popote ambapo January alisema ana matarajio ya kuwa Waziri Mkuu. Ni hisia tu za watu - waliomtakia mema kutokana na mchango wake mkubwa katika kampeni za CCM katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, na 'wabaya' wake ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakimzushia vitu mbalimbali.

Rais Magufuli alipomtangaza Kassim Majaliwa kuwa Waziri Mkuu, yakazuka maneno kuwa 'January kakosa Uwaziri Mkuu,' kana kwamba alitangaza kuwa anawania au anatarajia nafasi hiyo. 

Baada ya kitendawili cha uwaziri mkuu kuteguliwa, likabaki fumbo la baraza la mawaziri. Hapo napo yakazuka maneno chungu mbovu. January akapangiwa Wizara kadhaa na 'wanaomjua zaidi ya anavyojijua mwenyewe.' Lakini kuna waliodiriki kuweka 'chuki' zao hadharani na kuombea asiwemo kabisa katika baraza jipya la mawaziri. Ukiwauliza 'kwa lipi alilowakosea,' nina hakika hawana jibu.

Jana baraza likatangazwa. Na January akapanda kutoka Unaibu Waziri katika Awamu iliyopita na kuwa Waziri Kamili. Haya ni mafanikio makubwa kwa mwanasiasa kijana kama yeye. Kama kazini, hiyo ni promosheni, kutoka unaibu waziri hadi uwaziri kamili. Lakini kwa vile 'wabaya' wake walishampangia wizara, January kupewa Uwaziri katika ofisi ya Makamu wa Rais - Muungano na Mazingira imetafsiriwa nao kama 'amepewa kitu pungufu.' Jamani, mtendeeni haki mwanasiasa huyu. Pungufu kivipi ilhali kiukweli amepandishwa cheo kutoka unaibu waziri hadi kuwa waziri kamili?

Jana nilitwiti matarajio yangu kwa January katika nafasi hiyo mpya, na ninashukuru mapokeo yalikuwa mzuri. Maeneo mawili ya majukumu yake ya kiuwaziri ni muhimu sana, na nina hakika atawashangaza wengi. Kwa upande wa Muungano, sote twaelewa hali ya kisiasa ilivyo huko Zanzibar. Kwahiyo, kwa nafasi yake, January anatarajiwa ku-play role muhimu katika jitihada za kutafuta suluhisho la mgogoro wa kisiasa visiwani humo. Lakini licha ya mgogoro huo, moja ya vitu vinavyotishia ustawi wa Muungano wake ni kero zake za muda mrefu. Kwa vile Janaury ni msomi katika tasnia ya usuluhishi wa migogoro (confilict resolution), na kutokana na profile yake kubwa kimataifa, ninatarajia kuwa ataweza kuyashughulikia masuala yote mawili kwa ufanisi mkubwa.

Na katika suala la mgogoro wa kisiasa huko Zanzibar, hali ya 'ubinadamu' kwa maana ya utu au 'humani side' ya January itakuwa na umuhimu wa kipekee. Migogoro ya aina hiyo inahitaji mtu mwelewa, mtulivu, na mwenye busara, sifa ambazo January anazo. Kuweza kuwashawishi Wazanzibari waweke maslahi ya taifa mbele ya maslahi ya vyama vyao kunahitaji mtu ambaye anapoongea anaonekana kama ndugu au rafiki na si mwanasiasa au kiongozi flani. Kwa kifupi, human side ya mpatanishi ni muhimu mno katika tasnia ya utatuzi wa migogoro.

Lakini kama kuna eneo ambalo ninatarajia makubwa zaidi kutoka kwa mwanasiasa huyo ni MAZINGIRA. Moja ya masuala muhimu kabisa dunain kwa sasa ni masuala ya mazingira. Japo kwa Afrika, masuala hayo hayazungumziwi sana japo bara hilo ndilo lililo hatarini zaidi kimazingira, hususan kutokana na matatizo ya kiuchumi na umasikini, Mijadala mbalimbali muhimu inayoendelea duniani kwa sasa nipamoja na kuhusu masuala ya mazingira. Kubwa zaidi ni suala la global warming ambalo wanasayansi wanatahadharisha kuwa lisiposhughulikiwa kikamilifu linaweza kupelekea kuangamia kwa sayari yetu.

Kwa nchi masikini kama Tanzania, masuala ya mazingira yana umuhimu wa kipekee (japo hayazungumziwi inavyostahili) kwa sababu kama tunakwama katika kukabiliana na matatizo yaliyo katika uwezo wa kibinadamu, hali inakuwaje tunapokabiliwa na matatizo ya kiasili (natural) yaliyo nje ya uwezo wa kibinadamu?

Kwa upeo mkubwa alionao na uhodari wake wa kuwasilisha hoja, sintoshangaa kuona huko mbeleni January akitokea kuwa mmoja wa watu muhimu duniani katika masuala ya mazingira. Na uzuri ni kwamba ameingia katika wizara inayishughulikia masuala hayo wakati ambapo jina la Tanzania limeanza kuvuma kwa uzuri kutokana na sifa za uchapakazi wa Rais Magufuli.

Ninasema pasi hofu kuwa sintoshangaa miaka michache ijayo tukashuhudia kwa mara ya kwanza Tanzania ikitoa mshindi wa Tuzo ya Nobel aidha katika usuluhishi wa mgogoro wa Zanzibar au masuala ya mazingira, au hata yeye kuchaguliwa kuwa Mtu wa Mwaka wa jarida la kimataifa la TIME la Marekani (TIME's Person of the Year). 

Nimalizie kwa kueleza kuwa lengo la makala hii ni kuweka sawa kumbukumbu kuhusu watu muhimu katika tanzania yetu, kama January, kwa mahitaji ya sasa na huko mbeleni. Kma taifa, tunakabiliwa na mapungufu makubwa ya uhifadhi wa kumbukumbu. Na japo mie si mbashiri, natumaini kuna siku makala hii itatumika kama reference baada ya 'January kuishangaza dunia' katika eneo fulani. 

Mwisho, ninawatakia kila la heri mawaziri wote walioteuliwa na Rais Magufuli katika kabineti yake mpya, nikiwa na matumaini makubwa kuwa wataendana na kasi yake ya uchapakazi na hivyo kutupatia Tanzania tunayostahili. 

Nawatakia siku njema.



‘HAPPY birthday Tanzania…happy birthday me.” Naam, leo ni sikukuu ya Uhuru na Jamhuri, siku ya kuzaliwa kwa Tanganyika (sasa Tanzania Bara), siku ambayo pia ni ya kuzaliwa kwangu.

Nilizaliwa Desemba 9, miaka kadhaa baada ya uhuru wa nchi yetu, na kila ninapoadhimisha siku ya kuzaliwa, ninaadhimisha pia siku ya kuzaliwa kwa nchi yetu.

Kwa kawaida, maadhimisho yangu ya siku ya kuzaliwa huwa sio sherehe bali hutumia siku hiyo kumshukuru Mungu, sambamba na kufanya tafakuri ya nilipotoka, nilipo na niendapo. Sherehe pekee ilikuwa kuimbiwa wimbo wa ‘Happy Birthday’ na marehemu baba, ambaye kwa bahati mbaya hayupo nasi sasa. Kwa hiyo hii itakuwa birthday yangu ya kwanza kukosa ‘sherehe’ hiyo iliyoambatana na sala za kumshukuru Mungu na kuniombea mafanikio.

Lakini wakati wa kusherehekea siku ya kuzaliwa pamoja na ‘birthday-mate’ (mtu mliyezaliwa naye siku moja) Tanzania imekuwa kama tukio la kihistoria na la kujivunia, kwa upande mwingine kila ninapofanya tafakuri kuhusu ‘mwenzangu’ huyo alipotoka, alipo na aendako huishia kupatwa na maumivu.

Si kwamba nimefanikiwa sana kuliko ‘mwenzangu’ huyo bali angalau kwa upande wangu kila nikiangalia nilipotoka, nilipo na niendako, nimekuwa naona mwanga zaidi. Kwa ‘mwenzangu’ Tanzania, wakati huko alikotoka kulileta matumaini, alipo na aendako (kwa miaka ya hivi karibuni) kulinipa shaka.

-Lengo la kupata uhuru halikuwa kumwondoa tu mkoloni bali pia kujenga jamii yenye amani na usawa, pamoja na mambo mengine. Japo katika miaka 54 ya uhuru wetu, Tanzania imeendelea kuwa nchi ya amani kwa maana ya kutokuwepo vita, lakini katika miaka ya hivi karibuni amani kwa maana ya kuwa na uhakika wa mlo wa kesho, au wanafunzi kuwa na hakika ya ajira wanapomaliza masomo au wakulima kuwa na uhakika wa mauzo ya mazao yao, au wagonjwa kuwa na uhakika wa huduma wanayostahili katika vituo vya afya na uhakika katika maeneo mengine, vimekuwa ni mgogoro.

Kadhalika, amani yetu imeonekana kuwanufaisha zaidi ‘mchwa’ wachache walioigeuza Tanzania yetu kuwa shamba la bibi, wenzetu ambao miaka michache iliyopita tuliwaita kupe, wanaovuna wasichopanda, wanaoneemeka kwa jasho la wengine.

Mara kadhaa, maadhimisho ya sikukuu ya uhuru wetu yameambatana na swali gumu, je kweli tupo huru? hasa ikizingatiwa kuwa kwa kiasi kikubwa nchi yetu imeendelea kuwa tegemezi kwa wafadhili, miongoni mwao wakiwa watu walewale tuliowafukuza mwaka 1961.

Kuna wenzetu wengi tu wanaodhani kuwa uhuru wetu ulifanikiwa kumtimua mtu mweupe lakini miaka kadhaa baadaye huku tukiwa huru tumeshuhudia ukoloni mpya unaofanywa na mtu mweusi. Na japo wakoloni hawawezi kuwa na kisingizio cha kututawala, lakini walipoinyonya nchi yetu walikuwa na malengo ya kunufaisha nchi zao na sio watu binafsi. Kadhalika, hawakuwa na uchungu na nchi yetu kwa vile sio yao.

Kinyume chake, wakoloni weusi sio tu ni wenzetu bali wengi wao aidha walisomeshwa bure au kwa fedha za Watanzania wenzao, lakini badala ya kurejesha fadhila kwa kulitumikia taifa kwa uadilifu, wameishia kuwa wanyonyaji wasio na huruma. Tofauti na wakoloni weupe, wenzetu hawa hawana kisingizio japo kimoja kwani wanainyonya nchi yao wenyewe.

Moja ya vikwazo vya kutuwezesha kufaidi matunda ya uhuru ni ukosefu wa uzalendo. Licha ya jitihada kubwa za Mwalimu Nyerere kuhamasisha mapenzi na uchungu kwa nchi yetu – uzalendo- tawala zilizofuatia baada ya yeye kung’atuka zikawekeza katika kuboresha maslahi binafsi badala ya maslahi ya taifa. Japo mabadiliko yaliyoikumba dunia wakati Mwalimu anataka madaraka yalisababisha haja ya mageuzi katika itikadi ya ujamaa, lakini kilichofanyika si mageuzi tu bali kuua kabisa mfumo wa ujamaa.

Kuna wanaodai kuwa isingewezekana kufanya mageuzi ya kisiasa na uchumi huku tukikumbatia mfumo wa ujamaa. Hilo sio sahihi, kwani tunashuhudia taifa kubwa kama China ambalo limefikia hatua ya juu kabisa ya ujamaa yaani ukomunisti, likimudu kuendelea kuwa taifa la kijamaa huku likijihusisha pia na sera za uchumi wa kibepari kama vile uwekezaji.

Nikirejea kwenye siku ya kuzaliwa Tanzania Bara, na yangu, Ninaomba kukiri kuwa baada ya muda mrefu, mwaka huu sikukuu yetu ya kuzaliwa mie na ‘mwenzangu’ inaleta furaha na matumaini.

Na yote hayo ni matokeo ya ninachokitafsiri kama kusikilizwa kwa dua/sala zetu kwa Mwenyezi Mungu kuturejeshea Nyerere na (Waziri Mkuu wa zamani marehemu Edward) Sokoine wengine. Tumejaaliwa kumpata Rais mpya, Dk. John Magufuli, ambaye mwezi mmoja tu tangu aingie madarakani ameweza kwa kiasi kikubwa kurejesha matumaini yaliyopotea.

Na pengine kuashiria kuwa Nyerere amerudi kupitia Dkt Magufuli, mwaka huu tunaadhimisha siku ya uhuru na Jamhuri kwa shughuli za usafi wa mazingira, na hii inakumbusha dhana ya Mwalimu ya Uhuru na Kazi. Na kwa hakika hatuwezi kuwa huru kwa kuwafanyia kazi wenzetu wanaotuibia kila kukicha.

Majuzi akiwahutubia wafanyabiashara wakubwa huko nyumbani (Tanzania), Rais Dk. Magufuli alieleza bayana jinsi tunavyoweza kutoka kundi la nchi masikini na ombaomba na kuwa miongoni mwa nchi wafadhili iwapo tutatumia raslimali zetu vizuri, sambamba na kupambana na ufisadi. Uhuru wa bendera pekee, wa kumwondoa mkoloni mweupe huku tukisumbuliwa na mkoloni mweusi ni tatizo kwani suala si rangi ya mkoloni bali ukoloni wenyewe. Tukimudu kuboresha uchumi wetu na kuweza kujitegemea, tutakuwa na uhuru kamili.

Kadhalika, kama Mwalimu alivyotufundisha, uhuru bila nidhamu ni uwendawazimu. Hatuwezi kuwa na uhuru kamili kama hatuna nidhamu ya matumizi na tuliowapa dhamana ya kutuongoza hawana nidhamu kwa maadili ya taifa.

Ni matumaini yetu wengi kuwa maadhimisho haya ya siku ya uhuru na Jamhuri kwa njia ya uhuru na kazi, sambamba na kasi kubwa ya Dk. Magufuli kutumbua majipu ni ishara njema kuwa Tanzania tuliyoitarajia Desemba 9, 1961 na kufaidika nayo zama za Mwalimu, ipo mbioni kurejea.

Nimalizie makala hii kwa kusema tena ‘Happy birthday Tanzania, happy birthday to me.’

Mungu Ibariki Tanzania.
Mungu mbariki Rais wetu Dk. John Magufuli.

Mungu tubariki Watanzania. 

9 Dec 2015

Siku ya leo ninaadhimisha birthday tatu kwa mfululizo, mbili zangu binafsi na moja pamoja na Watanzania wenzangu. Wakati Tanzania inatimiza miaka 54 tangu ipate uhuru, nami ninatimiza miaka kadhaa tangu nizaliwe, nikiwa mtoto wa tano wa familia ya watoto wanane ya marehemu baba yangu mpendwa Philemon Chahali na marehemu mama yangu mpendwa Adelina Mapango.

Lakini leo pia ni siku ambayo kampuni yangu ya huduma za ushauri wa kitaalamu (consulting services) inazaliwa rasmi, Kampuni hii ni matokeo ya uamuzi wangu wa kutafsiri ujuzi na uzoefu wangu wa muda mrefu katika maeneo kadhaa na kuufanya kuwa kazi rasmi. 

Jina la kampuni, yaani AdelPhil, ni kumbukumbu ya marehemu mama ADELina na marehemu baba PHILemon,. Imesajiliwa hapa Uingereza lakini itatoa huduma za kimataifa katika maeneo ya Intelijensia na Usalama, mikakati ya siasa (political strategies), na masoko kupitia mitandao ya kijamii (social media marketing). Lengo hasa la kampuni hii ni kuliunganisha eneo la Maziwa Makuu (Great Lakes region) yaani Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi, Zaire na Jamhuri ya KidemOkrasia ya Watu wa Kongo (DRC) na dunia kwa ujumla. Awali, msisitizo utakuwa kati ya Tanzania na Uingereza. 

Pamoja na sababu nyingine, kuanzishwa kwa kampuni hii ni katika kuunga mkono jitihada za serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi uliotukuka wa Rais Dkt John Magufuli, ambaye tangu aingie madarakani amekuwa akifanya jitihada kubwa kuipeleka Tanzania yetu mahali inapostahili. AdelPhil itawasaidia Watanzania - kwa maana ya taasisi za umma na binafsi na watu binafsi - kulifikia soko la huduma na bidhaa hapa Uingereza (kwa kuanzia) na wakati huohuo kuwezesha wateja wa hapa Uingereza kulifikia soko la hudma na bidhaa nchini Tanzania. Baadaye wigo utatanuliwa ili kufikisha huduma hizo kwa nchi zote za Maziwa Makubwa na dunia kwa ujumla (hususan Ulaya Magharibi).

Basi nitumie fursa hii kumshukuru Mungu kwa kunijaalia mwaka mwingine. Japo mwaka huu ninaomaliza ulikuwa mgumu kwangu kutokana na kumpoteza baba yangu mpendwa, Marehemu Philemon Chahali, miaka 7 baada ya kumpoteza mama yangu mpendwa, Marehemu Adelina Mapngo, na sasa kubaki yatima.

Hata hivyo, japo nusu ya pili ya mwaka huu ilianza kwa kifo cha baba, hatimaye nilipata nguvu na kushiriki kikamilifu katika kampeni za uchaguzi mkuu huko nyumbani ambapo hatimaye Rais Dkt Magufuli aliibuka mshindi. Ushiriki huo umechangia sana wazo la kuanzishwa kwa kampuni ya AdelPhil baada ya kupata ushauri kutoka kwa watu kadhaa.

Uchungu mkubwa katika siku hii ni kutokana na ukweli kwamba kila mwaka, siku yangu ya kuzaliwa iliambatana na Marehemu baba kuniimbia happy birthday, kwa simu niwapo mbali na nyumbani, lakini hii ni birthday ya kwanza ambapo nitakosa upendo huo mkubwa wa baba kwa mwanae. Lakini yote ni mipango ya Mungu, na ninaamini wazazi wangu wapendwa huko walipo wanapata faraja kuona mtoto wao naanzisha kampuni ambayo nime-dedicate jina lake kwao.

Kwa Watanzania wenzangu, wito wangu mkubwa kwenu ni kuendelea kuunga mkono jithada za Rais Dkt Magufuli kwa sababu tuna malima mrefu wa kupanda na anahitaji kila aina ya ushirikiano wetu. Mie ndo mchango wangu wa kwanza ni huo wa AdelPhil Consultancy, kampuni ambayo japo inafanya biashara lakini pia ni ya kuwatumikia Watanzania wenzangu na nchi yetu kwa ujumla. Katika siku zijazo nitaelezea kwa undani ni jinsi gani waweza kunufaika na huduma za kampuni hii.

Nimalizie kwa kusema HAPPY BIRTHDAY TANZANIA, HAPPY BIRTHDAY ME, na HAPPY BIRTHDAY ADELPHIL CONSULTANCY

4 Dec 2015


KWA wanaofuatilia safu hii, watakumbuka kuwa mara baada ya CCM kumpitisha Dk. John Magufuli kuwa mgombea wake wa kiti cha urais katika Uchaguzi Mkuu uliopita, niliandika makala iliyoonyesha kukata tamaa na kutotegemea lolote jipya. Licha ya kutojutia kuwa na mtizamo huo ambao ulitokana na mwenendo wa chama hicho tawala kwa miaka kadhaa sasa, pia wakati huo nilikuwa na matumaini makubwa kuwa vyama vya upinzani, hususan Chadema vingetupatia mbadala wa CCM.

Hata hivyo, baada ya Chadema na vyama vingine vilivyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kumpokea Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, na baadaye kumteua kuwa mgombea wao, sambamba na ‘kumpa kisogo’ mwanasiasa aliyeifanyia makubwa Chadema, Dk. Willbrord Slaa, ambaye pia alikuwa Katibu Mkuu wa chama hicho, nilitafakari upya msimamo wangu.


Awali, nilielekeza nguvu zangu katika kupingana na uamuzi wa Chadema/Ukawa kumpokea Lowassa na kumfanya kuwa mgombea wao wa kiti cha urais. Lakini kwa vile kwa vyovyote vile, ilikuwa lazima Rais wa Tano wa Tanzania angetoka aidha CCM au Ukawa na tayari nilishatafsiri kuwa uamuzi wa Lowassa kupokelewa na Upinzani na kufanywa mgombea wao ni usaliti, hatimaye nililazimika kumwangalia mgombea wa CCM, Dk. Magufuli, kwa jicho la tatu.


Baada ya kusikiliza hotuba yake siku ya uzinduzi wa kampeni za CCM na hotuba zilizofuatia alipozunguka sehemu mbalimbali za nchi yetu kuomba kura, niliamua kumuunga mkono kwa asilimia 100. Japo uamuzi huo haukuwa mgumu kwa vile kadri siku zilivyoenda ilionyesha bayana kuwa Dk. Magufuli angekuwa kiongozi mwafaka kwa Tanzania yetu, hofu yangu kuu haikuwa endapo angeshindwa bali iwapo angeshinda na kuendeleza yale yale yaliyonifanya kuwa miongoni mwa wakosoaji wakubwa wa CCM. Kadhalika, uamuzi huo, ulisababisha kurushiwa maneno makali na tuhuma mbalimbali ikiwa ni pamoja na madai kuwa nimenunuliwa na CCM.


Urahisi wa kumuunga mkono Dk. Magufuli ulichangiwa zaidi na kiburi kilichowapata wafuasi wa Lowassa ambao kwa kiasi kikubwa walikataa katakata kuweka mantiki mbele ya hisia. Wimbo uliotawala kwao ulikuwa ni mabadiliko tu, na kila aliyejaribu kuhoji kuhusu mabadiliko hayo alirushiwa maneno makali, na wakati mwingine kutukanwa. Kwa hiyo ilifikia wakati wa kuamua liwalo na liwe. Waingereza wana msemo ‘the end justifies the means,’ yaani, kwa tafsiri isiyo rasmi, matokeo huhalalisha njia iliyotumika kuyafikia.


Kwa hiyo, nilijipa matumaini kuwa iwapo Dk. Magufuli angeshinda na kutimiza ahadi zake basi sio tu itamaliza kelele za waliotuona wasaliti dhidi ya mabadiliko yaliyoahidiwa na Lowassa bali pia itatimiza ndoto ya kila Mtanzania kuiona nchi yetu ikipata kiongozi wa kutufikisha mahala tunapostahili kuwepo.


Bahati nzuri, sio tu kuwa Dk. Magufuli alishinda bali muda mfupi tu tangu aingie madarakani ameweza kufanya mambo makubwa zaidi ya matarajio ya wengi kwake. Kwa hiyo, tuliomuunga mkono sio tu tuna furaha ya ushindi wake lakini pia tuna furaha kubwa zaidi ya kupata mtu wa watu, anayetambua matatizo yanayoikabili nchi yetu, mwenye uamuzi stahili, na anayetupa matumaini kwamba hatimaye nchi yetu itaweza kuangamiza janga la kitaifa la rushwa na ufisadi, hatua itakayosaidia kutuondoa kwenye umasikini mkubwa licha ya rasilimali lukuki tulizonazo, na hatimaye kuwa na Tanzania tunayoweza kujivunia.


Binafsi, nimejijengea utaratibu wa kuanza siku yangu kwa kuangalia kilichojiri huko nyumbani, kwa kupitia vyombo mbalimbali vya habari mtandaoni. Mara nyingi utaratibu huo wa kila siku uliishia tu kutibua siku yangu kwani kila kukicha ilikuwa ni mlolongo wa habari mbaya baada ya habari mbaya. Ilikuwa nadra kwa wiki kupita bila kukumbana na habari za ufisadi, ujangili, ahadi za porojo, na kadhalika.


Lakini hali sasa ni tofauti tangu Magufuli aingie madarakani. Yaani ni raha mtindo mmoja, kwani kila siku ni habari njema juu ya habari njema. Na si vigumu kuwa na matumaini makubwa ikizingatiwa kuwa hadi wakati ninaandika makala hii, Rais Magufuli amekuwa madarakani kwa takriban wiki tatu tu. Yayumkinika kubashiri kuwa siku 100 za kwanza za urais wake zitashuhudia Tanzania ikiwa nchi ya mfano wa kuigwa.


Na hilo limeshaanza kutokea. Tayari vyombo mbalimbali vya habari, hususan barani Afrika, vimekuwa vikiripoti kwa wingi kuhusu hatua mbalimbali anazochukua Rais Magufuli. Lakini kivutio zaidi ni jinsi baadhi ya wananchi katika nchi kama Kenya, Uganda, Malawi, Afrika Kusini, Nigeria na kwingineko walivyofikia hatua ya kutamani Magufuli awe Rais wao. Hii inatukumbusha zama za Baba wa Taifa ambaye alionekana machoni mwa Waafrika wengi kama mmoja wachache wa bara zima.


Taratibu, hisia kuwa kasi ya Magufuli ni nguvu ya soda zinaanza kufutika huku wananchi wengi wakiahidi kumpa ushirikiano katika jitihada zake za kuikomboa Tanzania yetu. Hata baadhi ya wafuasi wa vyama vya upinzani sasa wanamkubali baada ya kuridhishwa na uchapakazi wake.


Hata hivyo, kuna takriban makundi matatu ya wapinzani wa Dk. Magufuli. Kundi la kwanza ni la wapinzani wa asili, linalojumusiha wenzetu waliojitoa ufahamu na kuamini iwe isiwe lazima Lowassa angekuwa rais. Hawa hawashangazi na huenda baada ya muda ndoto ya urais wa Lowassa itawatoka na watakubaliana na hali halisi. Lakini kwa vile upinzani si uadui, na kimsingi upinzani wa kisiasa waweza kuwa chachu nzuri ya kumsaidia Rais wetu na chama chake kuibua uovu dhidi ya taifa letu, basi kundi hili si tatizo sana.


Kundi la pili ni la watu walioigeuza Tanzania yetu kuwa shamba la bibi, waliozoea kuvuna wasichopanda, watu ambao zama za Ujamaa tuliwaita kupe. Kundi hili lajumuisha mafisadi na wanufaika wa ufisadi, wahalifu (kwa mfano wauza dawa za kulevya, majangili). Hawa wanatambua kuwa arobaini za mwizi zimewadia. Kundi hili ni hatari kwani miongoni mwao kuna wenye tabia za kimafia. Hawa si wa kufumbiwa macho hata kidogo, na ni muhimu kwa taasisi za usalama kuwabaini na kuwadhibiti mapema. Si rahisi kwa kundi hili kumkubali Magufuli au kuunga mkono jitihada zake kwa sababu kimsingi jeuri yao mtaani inafikishwa kikomo.


Kundi la tatu ni la wenzetu waliozowea kupata wasichostahili. Kuna ugonjwa mmoja unaitwa Stockholm Syndrome, ambao kwa kifupi ni hali inayomfanya mtu anayenyanyaswa au kuteswa kuyakubali manyanyaso/mateso hayo na kuyaona kama stahili yake. Mara kadhaa tunashuhudia mwanandoa anayeteswa na mwenza wake akitokea kuwa mtetezi wake mkuu. Katika kundi hili kuna wenzetu wanaoamini kuwa mapambano dhidi ya rushwa au ufisadi hayawezi kufanikiwa kwa vile, kwa mtizamo wao, ni hatima (destiny) ya taifa letu. Uzuri ni kwamba kadri jitihada za Magufuli zitakavyozidi kuzaa matunda, taratibu watu wa aina hii wataanza kutambua kuwa imani yao ni fyongo.


Nimalizie makala kwa kukumbushia kuwa hakuna safari isiyo na kona au milima na mabonde. Jitihada za Magufuli kuikomboa Tanzania yetu hazitokuwa nyepesi lakini la muhimu ni imani kuwa zitafanikiwa. Hata hivyo, ili jitihada hizo zifanikiwe ni wajibu wetu sio tu kumuunga mkono au kumsifia tu bali nasi wenyewe tunapaswa kubadilika kwa kuchukia ufisadi, rushwa, uzembe na vitu vingine vinavyolikwaza taifa letu.


INAWEZEKANA, TIMIZA WAJIBU WAKO

- Se

28 Nov 2015


Makala hii imechapishwa katika jarida la Raia Mwema toleo la wiki hii lililotoka tarehe 25/11/2015, lakini kwa sababu nisizoelewa tovuti ya jarida hilo haijawa-updated kwa wiki kadhaa sasa. Kwa vile makala ninazotuma gazetini hufanyiwa uhariri kabla ya kuchapishwa, yawezekana makala iliyopo gazetini ikawa na tofauti kidogo na hii.

MAKALA YA RAIA MWEMA TOLEO LA NOVEMBA 25, 2015

Hotuba hii ya Rais Magufuli ni moja ya hotuba bora kabisa katika historia ya siasa za Tanzania.” Hili lilikuwa hitimisho langu katika mtandao wa kijamii wa Twitter mara baada ya Rais John Magufuli kumaliza kulihutubia Bunge wiki iliyopita, huko Dodoma.

Na kwa hakika watu kadhaa waliafikiana na hitimisho hilo.  Kilichovutia wengi waliosikia hotuba hiyo, katika shughuli ya ufunguzi wa Bunge la 11, sio tu mpangilio wa hotuba yenyewe bali pia jinsi kila alilotamka lilivyoonyesha bayana kuwa lilitoka moyoni mwake kwa dhati kabisa.

Rais alianza hotuba yake hiyo kwa kuorodhesha matatizo mbalimbali aliyobaini wakati wa kampeni zake Urais ambapo alizunguka takriban Tanzania nzima. Alitoa uchambuzi wa kina wa matatizo hayo kabla ya kuelezea kwa undani ni kwa jinsi gani serikali yake itayashughulikia. Ilikuwa ni zaidi ya hotuba ya kisiasa, na pengine ingeweza kabisa kuwa mhadhara wa kitaaluma uliofanyika katika lugha nyepesi na ya kueleweka.

Moja ya vitu vilivyonivutia sana katika hotuba hiyo ni jinsi Rais Magufuli alivyoweza kutupatia jibu la swali ambalo kwa miaka kadhaa lilionekana kuwatatiza viongozi wetu mbalimbali: “Kwanini Tanzania ni masikini licha ya utajiri lukuki wa raslimali ilionao.” Alieleza bayana na kwa kirefu jinsi ufisadi, rushwa na uhalifu vinavyochangia kukwamisha maendeleo ya taifa letu. Kadhalika, alifafanua, kwa kutumia takwimu halisi, jinsi mabilioni ya fedha yalivyotumika visivyo kwa matumizi yasiyo muhimu na yaliyo nje ya uwezo wa taifa letu masikini.

Kwa hakika ilikuwa hotuba ya kihistoria iliyofunika kabisa utovu wa nidhamu wa hali ya juu ulioonyeshwa awali na wabunge wa upinzani ambao walitumia muda mwingi kabla ya hotuba hiyo kuzomea na baadaye kuamiriwa  kutoka nje ya ukumbi huo.

Lakini kwa vile sio rahisi kumridhisha kila mtu, baadhi ya wenzetu waliosikiliza  hotuba hiyo walidai kuwa eti “haina tofauti na hotuba nyingine kadhaa zilizokuwa nzuri kuzisikiliza lakini zikaishia kuwa maneno matamu tu.” Wengine walikwenda mbali zaidi na kudai kuwa hata mtangulizi wa Rais Magufuli, Rais Mstaafu Jakaya Kikwete naye pia alianza urais wake kwa hotuba za kutia moyo kama hizo lakini mengi ya aliyoahidi, hususan lile la ‘Maisha Bora kwa Kila Mtanzania,’ yaliishia kuwa ahadi tu.

Sikubaliani kabisa na wakosoaji hao, japo hoja zao zinaweza kuwa na mantiki kidogo. Ni kweli kwamba ukosefu wa hotuba za kuvutia si moja ya matatizo yanayoikabili nchi yetu. Wengi wa wanasiasa na viongozi wetu ni mahiri sana wa maneno lakini tatizo huwa katika kutafsiri maneno yao kuwa vitendo.
Wakosoaji hao hawapo sahihi kwa sababu, kama nilivyoeleza awali, hotuba hiyo ilikuwa ya kutoka moyoni.Ilikuwa hotuba ya kiongozi anayeguswa na yanayoisibu nchi yake, kiongozi mwenye uelewa wa changamoto zinazoukabili uongozi wake, na mwenye dhamira thabiti ya kukabiliana na changamoto hizo.

Kuna mbinu moja muhimu ya kubaini iwapo mtu anaongea ukweli au anahadaa, nayo ni kumwangalia usoni. Tangu kuanza kwa kampeni zake za urais na hadi wakati wa hotuba hiyo ya wiki iliyopita, uso wa Rais Magufuli wakati anaongea unaonyesha bayana kuwa kila neno linalotoka mdomoni mwake ni la dhati, linatoka moyoni na si sehemu ya porojo tulilozowea kutoka kwa wengi wa wanasiasa na viongozi wetu. Mtaalam yeyote wa kubaini ukweli na uongo hatoshindwa kuafikiana nami kuwa uthabiti wa kauli za Magufuli upo wazi kwa yeyete anayemwangalia usoni wakati anaongea.

Lakini pia, hotuba hiyo ilikuwa mwendelezo wa ishara nzuri zilizoanza kujitokeza siku moja tu tangu Rais Magufuli aingie ofisini, ambapo alifanya ziara ya kushtukiza Wizara ya Fedha, kabla ya kufanya ziara nyingine kama hiyo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Na siku ya uzinduzi wa Bunge, alitukumbusha enzi za (Waziri Mkuu wa zamani) hayati Edward Sokoine, aliyesifika kwa uchungu wa mali za umma, baada ya kuamuru zaidi ya shilingi milioni 200 zilizochangwa kwa ajili ya hafla ya mchapalo ya sherehe za uzinduzi wa Bunge jipya zielekezwe kwenye ununuzi wa vitanda katika hospitali ya Muhimbili, na kiasi kidogo tu kitumike kwa ajili ya hafla hiyo.

Kimahesabu, chini ya wiki tatu tangu aingie madarakani, Rais Magufuli ameshaokoa jumla ya shilingi milioni 900 kutokana na hatua alizochukua dhidi ya matumizi yasiyo ya lazima. Kwa kasi hii, tuna kila sababu ya kutarajiwa kuiona nchi yetu ikipaa kiuchumi, na hatimaye Watanzania kunufaika na neema lukuki ambayo nchi yetu imejaaliwa kuwa nayo.

Sina shaka kuhusu uwezekano wa mafanikio ya hatua za Rais Magufuli huko serikalini. Licha ya kuwa na Waziri Mkuu mchapakazi mzoefu, Majaliwa Kassim Majaliwa, kuna kila dalili kuwa baraza la mawaziri ambalo hadi wakati ninaandaa makala hii lilikuwa halijatangazwa, litasheheni wachapakazi kama yeye. Kwahiyo, kazi ya kurejesha nidhamu serikalini, kupunguza matumizi yasiyoendana na umasikini wetu na kupambana na ufisadi ina dalili kubwa za mafanikio.

Eneo ambalo Rais Magufuli hawezi kufanikiwa peke yake pasipo ushirikiano wa Watanzania wote ni nje ya serikalini na huko ‘mtaani.’ Mara kadhaa nimekuwa nikisisitiza umuhimu wa wananchi kujenga kasumba ya kudai haki na stahili zao badala ya kuona haki/stahili hizo ni kama fadhila au upendeleo flani. Wenzetu huku Ughaibuni wamejenga desturi ya kutokubali huduma au bidhaa inayotolewa chini ya kiwango wanachostahili. Haki na stahili za mpokea huduma ni miongoni mwa vitu vinavyopewa umuhimu mkubwa huku tulipo.

Haitokuwa rahisi kwa Rais Magufuli au wasaidizi wake kwenda kila sehemu kuwezesha au kuharakiasha upatikanaji wa huduma. Jukumu hilo linapaswa kusaidiwa na wananchi wenyewe ambao mara nyingi ndio wahanga wakubwa wa huduma mbovu. Kadhalika, watoa huduma nje ya serikali wanapaswa kutambua kuwa hizi ni zama mpya, na asiyeweza kuendana na kasi ya Rais Magufuli na ajiweke kando.

Lakini mchango mkubwa zaidi wa wananchi wote unahitajika zaidi katika kupambana na ufisadi, rushwa na uhalifu mwingine nje ya serikali. Wakati Rais ameahidi kukabiliana na ‘mapapa’ wa uhalifu kama kwenye biashara hatari ya madawa ya kulevya, pasipo wananchi kumsaidia kwa kuwatenga wahusika na kuwaripoti -  badala ya kuwasujudia na kuwapa majina ya heshima kama ‘wazungu wa unga’ au ‘mapedejee’ – basi tutamkwamisha, na nchi yetu itaendelea kuumizwa na vitendo hivyo viovu.

Kadhalika, ili kauli-mbiu ya ‘Hapa Ni Kazi Tu’ iweze kuleta matokeo kusudiwa na kuwa ya ufanisi ni muhimu kwa kila Mtanzania kuachana na dhana fyongo ya kusaka mafanikio kwa njia za mkato, turejee zama za Ujamaa na Kujitegemea ambapo waliokula bila kuvuja jasho tuliwaita ‘kupe.’ Sote tuchape kazi, tuache kufanya ‘ujanja ujanja,’ tuone fahari kuwa na shughuli halali badala ya kuamini kuwa ufisadi, rushwa, uhalifu,nk ndio njia rahisi na sahihi za kufikia mafanikio kwa haraka.

Baada ya kumpoteza Baba wa Taifa Marehemu Mwalimu Julius Nyerere aliyetujengea misingi imara ya taifa letu, japo sasa inamong’onyoka kwa kasi, na mzalendo wa daraja la kwanza, Marehemu Sokoine, sala/dua zetu katika wimbo wetu wa taifa katika maneno “Mungu Ibariki Tanzania…” zimesikika, na Mwenyezi Mungu ametuletea ‘Nyerere na Sokoine mpya’ kupitia kwa Rais wetu mpya Dkt Magufuli. Tusijiangushe wenyewe kwa kutotumia ipasavyo fursa hii adimu.

Nimalizie makala hii kwa wito ‘wa kitaalamu’ kwa ndugu zangu wa Idara ya Usalama wa Taifa, ambao pamoja na majukumu mengine, wana dhamana ya ulinzi wa Rais wetu na viongozi wengine wakuu kitaifa. Kama alivyosema mwenyewe, vita aliyoanzisha dhidi ya kila vitendo na kasumba zinazolikwaza taifa letu ni nzito na inawagusa watu wazito. Kwa vile yayumkinika kusema kuwa vitendo vya rushwa,ufisadi na uhalifu vimefikia hatua ya ‘kimafia,’ basi ni muhimu kuimarisha ulinzi wa Rais wetu (na viongozi wengine wanaopatiwa ulinzi) kwa sababu ‘tupo vitani.’

Simaanishi kuwa ulinzi uliopo una mapungufu lakini angalizo hili linazingatia ukweli kwamba ‘vita’ hiyo inagusa maslahi ya wengi, maslahi ya ‘kupe’ lukuki walioigeuza Tanzania yetu kuwa ni ‘shamba la bibi,’ la kuvuna wasichopanda, sambamba na wahalifu wanaoingiza, kuuza na kusafirisha madawa ya kulevya kana kwamba ni bidhaa iliyoidhinishwa na Shirika la Viwango la Taifa (TSB), majangili wanaoshindana kuua wanyamapori wetu na kusafirisha nyara za serikali, na wahalifu wengineo.

Rais Magufuli ameahidi kutotuangusha, basi nasi tusimwangushe.

Hapa Ni Kazi Tu!

Barua-pepe: [email protected] Tovuti: www.chahali.com Twitter: @chahali



28 Oct 2015





Bonyeza hapo juu kusikiliza mahojiano hayo kuhusu Uchaguzi Mkuu nchini Tanzania, na bonyeza link chini ya picha ifuatayo kusoma mahojiano kati yangu na BBC Swahili


BONYEZA HAPA kusoma mahojiano kamili


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.