20 May 2016


WIKI iliyopita yaweza kubaki kwa muda mrefu kwenye kumbukumbu za Watanzania wanaoishi hapa Uingereza. Kwa upande mmoja, wiki hiyo ilimalizika kwa mkutano kati ya baadhi yao na Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa, na kwa upande mwingine wiki hiyo ilitawaliwa na mizengwe ya ‘kuzuia’ fursa kwa wengi kukutana na Waziri Mkuu.

Awali, zilipatikana tetesi kwamba Rais John Magufuli angefanya ziara ya kikazi hapa Uingereza, lakini baadaye ikafahamika kuwa Waziri Mkuu Majaliwa ndiye angemwakilisha.

Hatimaye Waziri Mkuu aliwasili hapa kwa mara ya kwanza tangu ashike wadhifa huo, na pia kuwa kiongozi wa kwanza wa kitaifa kuzuru nchini hapa tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani.

Wengi wa Watanzania wanaoishi nchini hapa walionyesha kiu kubwa ya kukutana na kiongozi huyo mpya, hususan kusikiliza visheni ya Serikali ya Awamu ya Tano kwa Tanzania na Watanzania, ikiwa ni pamoja na tunaoishi nje ya nchi yetu.

Hata hivyo, kiu hiyo ilikumbana na kikwazo kutoka Ubalozi wa Tanzania hapa Uingereza, haukujali kutoa taarifa yoyote kwa Watanzania wanaoishi hapa kuhusu ujio wa kiongozi huyo wa kitaifa wala kueleza iwapo angekutana nao kwa maongezi.
Baadaye zikasikika tetesi kuwa Ubalozi huo (aidha kama ofisi au baadhi ya maofisa wake) ulitoa mwaliko kwa takriban watu arobaini hivi kuhudhuria ‘kikao’ na Waziri Mkuu. Tetesi hizo hazikueleza jinsi gani ‘wawakilishi’ hao walivyopatikana, lakini kilichoonekana bayana ni suala hilo kuzingirwa na usiri mkubwa.

Binafsi, nilianzisha jitihada za kuutaka Ubalozi uangalie umuhimu wa kuhakikisha kuwa kila Mtanzania anayeishi hapa anapatiwa fursa ya kuhudhuria mkutano huo. Awali niliweka ujumbe kwenye kundi la ‘Whatsapp’ la Watanzania wanaoishi hapa, japo mapokeo hayakuwa ya kuridhisha.

Baadaye nilichukua jukumu la kuandika makala katika blogu yangu baada ya kuzungumza na Watanzania kadhaa wanaoishi hapa, na ambao walionyesha bayana kutoridhishwa na jinsi Ubalozi wetu ulivyoonekana ‘kuhujumu’ uwezekano wa Watanzania wengi zaidi wanaoishi hapa kukutana na kiongozi wao.

Kwa bahati nzuri, ‘kelele’ za makala hiyo na ‘kilio’ kilichofikishwa kwenye kituo kimoja cha radio huko nyumbani na baadhi ya Watanzania wanaoishi hapa, zilizaa matunda. Hatimaye, Ofisi ya Waziri Mkuu ilitoa tamko kuwa Waziri Mkuu angekutana na Watanzania wanaoishi hapa.

Ofisi ya Waziri Mkuu pia ilijaribu kujitetea kuwa haikuhusika na maandalizi ya mkutano kati ya Waziri Mkuu na Watanzania wanaoishi hapa, japo haikuwahi kulaumiwa na mtu yeyote kwa sababu utaratibu uliozoeleka ni kwa Ubalozi (sio Wizara au ofisi za huko nyumbani) kufanya maandalizi ya mikutano ya viongozi wa kitaifa na Watanzania wanaoishi hapa.

Kwa upande mwingine taarifa hiyo ilikuwa kama inakanusha 'madai ya watu' kuwa kuna watu maalumu waliochaguliwa kuhudhuria mkutano huo (badala ya kuwa mkutano wa wazi kwa kila Mtanzania anayeishi hapa. Hata hivyo, kulikuwa na uthibitisho kwamba awali mpango wa ubalozi ulikuwa ni kwa kundi la watu kadhaa tu kukutana ‘kwa faragha’ na Waziri Mkuu.

Uthibitisho huo ulisikika baada ya mmoja wa maofisa wa ubalozi wetu hapa kujirekodi na kuweka ujumbe wa sauti (voice note) kwenye kundi la Whatsapp (la Watanzania wanaoishi hapa) ambapo pamoja na mambo mengine alikebehi jitihada za kutaka Watanzania wengi zaidi wanaoishi hapa wapate fursa ya kukutana na Waziri Mkuu. Alidai kuwa “hata Rais anapoongea na wazee jijini Dar haimaanishi basi wazee wote wa Dar wataalikwa kwenye mkutano huo.” Alidai kuwa hakuna ubaya kuteua watu wachache tu kuzungumza na Waziri Mkuu, na kuongeza kuwa ‘Watanzania wamezoea kuja wengi japo walioalikwa wachache tu.’

Kwa upande mmoja ninaipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa ‘kusoma alama za nyakati’ na kuruhusu mkutano kati ya Waziri Mkuu na Watanzania wanaoishi hapa kuwa wa wazi. Kwa upande mwingine ninaikosoa kwa sababu tamko lake kuwa mkutano huo utakuwa wa wazi sio tu lilitolewa Ijumaa - siku moja kabla ya mkutano – lakini pia haikubainisha muda wala sehemu kutapofanyika mkutano huo. Pengine ni mazoea tu ya huko nyumbani, lakini maisha ya hapa kwa kiasi kikubwa yanaambatana na ‘ratiba kali,’ na taarifa ya muda mfupi na isiyojitosheleza kimaelezo (kama hiyo ya Ofisi ya Waziri Mkuu) inaweza kuwa iliwanyima fursa watu wengi zaidi kuhudhuria mkutano huo.

Kwa upande wa Ubalozi wetu hapa, hadi wakati ninaandika makala hii haujafanya jitihada za kuwaomba radhi Watanzania wanaoishi hapa kwa ‘mpango wake fyongo’ ambao laiti ungefanikiwa, basi mkutano huo wa Waziri Mkuu ungekuwa ni kati yake na ‘wateule wachache’ tu. Kadhalika, ofisa ubalozi aliyejirekodi na kukebehi harakati zetu kudai fursa kwa wote kuhudhuria mkutano huo angeomba radhi kwa kauli zake zisizoendana na wadhifa wake wala ustaarabu wetu Kitanzania.

Pengine utata huo ungeweza kuepukika laiti pande mbili zinazohusika na ziara za viongozi wa kitaifa zingewajibika ipasavyo. Kwanza, ubalozi wetu hapa ungeweza kutengeneza mazingira mazuri ya mawasiliano na Watanzania wanaoishi hapa kwa kutumia mitandao ya kijamii au njia nyingine mwafaka. Hisia ni kwamba ‘ukimya’ uliojitokeza kuhusu ziara hiyo ulikuwa wa makusudi (yaani mkutano huo ulipaswa kuwa ‘shughuli ya wateule wachache’).

Pili, idara yetu ya masuala ya usalama imekuwa na utaratibu wa kutanguliza maafisa wake eneo ambalo kiongozi wa kitaifa atatembelea, kitu kinachofahamika kiintelijensia kama ‘advance party.’ Na moja ya majukumu ya waliomo kwenye ‘msafara’ huo ni kubaini yanayoweza kujitokeza wakati wa ziara husika. Kwa hiyo, laiti wangetupia macho ‘sehemu’ za maongezi ya Watanzania wanaoishi hapa (kwa mfano kundi lao la ‘Whatsapp’) basi wangeweza kubaini mapema kuwa kuna kiu ya mkutano na Waziri Mkuu sambamba na shutuma kuwa ubalozi unakandamiza kiu hiyo.

Nimalizie makala hii kwa kutoa wito kwa ofisi zetu za ubalozi popote zilipo ziwe kiunganishi kati ya Watanzania wanaoishi nchi hizo na nchi yetu, sio kwa masuala yanayohusu hati za kusafiria tu na masuala ya kidiplomasia bali kudumisha Utanzania wetu kwa upendo, umoja na mshikamano. Balozi zetu kadhaa zimekuwa zikilaumiwa kwa ‘kutokuwa na msaada,’ sambamba na kauli za jeuri/kiburi kwa baadhi ya maofisa wetu wa ubalozi, hali inayodhaniwa inatokana na baadhi yao kukaa huku nje muda mrefu mno kiasi cha ‘kuwadharau Watanzania wenzao.’

Mwisho, iwe ni kwa busara zake binafsi au ofisi yake, shukrani za pekee kwa Waziri Mkuu Majaliwa kuweza kuongea na Watanzania wanaoishi hapa Uingereza. Takriban kila aliyehudhuria mkutano huo ameridhishwa na hotuba ya Waziri Mkuu ambayo imetoa matumaini makubwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kwa dhati kuiboresha Tanzania yetu katika kila eneo.

19 May 2016


Kuna msemo wa Kiingereza unaoweza kutafsiriwa hivi, "thamani ya fedha ni matumizi." Pesa isiyoweza kutumika haina thamani, inabaki kuwa karatasi tu lenye picha ya kiongozi au alama fulani. Vivyo hivyo, thamani ya elimu/uelewa ni katika kushirikisha watu wengine. Ukiwa na elimu ya kutosha au uelewa mkubwa lakini ikabaki kichwani mwako tu bila kutumiaka basi haina umuhimu. Ni katika mantiki hiyo, sie wengine tumekuwa waumini wakubwa wa filosofia isiyo rasmi ya 'Sharing Is Caring' ambayo mara nyingi huandikwa #SharingIsCaring.

Leo ningependa ku-shea nawe msomaji mbinu muhimu ya ku-post kitu mtandaoni ili kioneknaje au kusomwa na watu wengi. Yaani hapa nazungumzia kuhusu ku-update status yako Facebook iwe ya maneno au picha, au ku-tweet huko Twitter, au ku-post picha yako hujo Instagram.

Tuanze na Facebook. Muda mwafaka wa ku-update status yako ili iweze kusomwa na watu wengi zaidi ni kati ya saa 3 asubuhi hadi saa 1 usiku, lakini muda bora kabisa ni saa 7 mchana hadi saa 9 alasiri.  

Kwa upande wa Twitter, muda mwafaka wa ku-tweet kitu kinachoweza kusomwa na watu wengi zaidi ni saa 6 mchana na kati ya saa 11 jioni na saa 12 jioni.

Kwa Instagram, muda mwafaka ni alfajiri, kwa maana watu wakiamka na kuingia kwenye app hiyo wakutane na picha yako.Lakini mtandao huu ni kimeo na jipu kwa Tanzania. Kwahiyo hata kuelezea kanuni zake ni sawa na kupoteza muda. Mtandao huu umetawaliwa na vitu vichafu na visivyopendeza. Binafsi japo bado ni memba huko lakini siutumii kwa sababu umesheheni kila aina ya maovu.

Maelezo hayo juu ni maalum kwa watu wenye ratiba zao nyingine lakini wanapenda kuwasiliana na jamii kwa kutumia mitandao ya kijamii. Maelezo hayo hayana maana kwa wenzetu ambao wapo mtandaoni kutwa kucha. Yes, kuna wenzetu wapo mtandaoni muda wote.

Kadhalika, maelekezo hayo ni ELEKEZI tu, kwa maana kwamba sio lazima usubiri muda huo mwafaka ndio uposti kitu chako. Muda huo elekezi ni mwafaka kwa minajili ya kuwafikia watu wengi zaidi.

Pichani chini ni infograph kuhusu nilichoeleza hapo juu



Endelea kutembelea blogu hii kwa mada mbalimbali za teknolojia, sambamba na makala zangu za kila wiki katika jarida la Raia Mwema, mada mbalimbali za intelijensia, burudani na michezo, maisha, na kadhalika. Karibuni sana

18 May 2016



Tukubaliane kwamba japo wengi wetu twapenda kutumia mtandao, hususan kutembelea mitandao ya kijamii kama vile Faceboo, Twitter, Instagram, nk bado kuna uelewa mdogo wa mbinu mbalimbali ambazo laiti zikutumika zaweza kuleta ufanisi zaidi katika matumizi ya mtandao au mitandao hiyo ya kijamii.

Siku za nyuma nilikuwa nikiandika makala mbalimbali kuhusu teknolojia lakini kutingwa na majukumu kumesababisha ni we mzembe kidogo. Samahani kwa hile, maana linaathiri ile spirit ya 'Sharing Is Caring.' 

Anyway, long story short, leo nina darasa fupi la jinsi ya kuangalia watu waliotembelea ukurasa (profile) wako wa Facebook. Ni suala la hatua kwa hatua, na nina hakika ukifuata kwa makini utaweza kuona nani ametembelea profile yako. Labda sio muhimu, lakini, hey, kuna watu  wangependa kufahamu vitu kama hivyo.

Samahani, nimejaribu kutafsiri hatua hizo pichani kwa Kiswahili nimechemsha. Natumaini kimnombo kilichotumika sio kigumu, lakini ikitokea mtu hajaelewa vema basi nishtue nitajitahidi kutoa ufafanuzi kwa Kiswahili.


Endelea kutembelea blogu hii kwa mbinu zaidi za mtandaoni pamoja na habari za teknolojia na habari nyinginezo.

Karibuni sana

17 May 2016


"Hello world!" ndio ilikuwa tweet ya kwanza baada ya Idara ya ushushushu ya Uingereza inayohusika na kunasa mawasiliano, GCHQ (Government Communications Headquarters)  kujiunga na mtandao huo wa kijamii. 

Hawa jamaa, ambao makao yao makuu ni hayo pichani juu, ndio wenye jukumu la kusoma barua-pepe zetu, kusikia simu zetu na kutegesha vinasa sauti pale inapobidi, wamebobea kwenye hacking...kwa kifupi ukitaka kuwaelewa vema, m-Google yule jamaa anaitwa Edward Snowden..amewazungumzia vya kutosha, wao na washirika wao wa Marekani, wanaoitwa NSA.

Sasa hawa jamaa wameingia rasmi katika mtandao wa kijamii wa Twitter.



Hiyo tweet yao ya kwanza ya "Hello world" iliyoambatana na picha ya ndani ya ofisi yao, ina umuhimu wa aina yake kwa sababu ni programu ya kwanza kujifunza kuandika wakati mtu anapojifunza kundika kwa lugha ya ku - code katika  vile Java, Python, C, PHP, na Ruby.

"Kwa kujiunga na mitandao ya kijamii, GCHQ inaweza kutumia sauti yake yenyewe kuongea  kuhusu kazi muhimu tunayofanya kuiweka Uingereza salama," alisema Andrew Pike, Mkurugenzi wa Mawasiliano wa taasisi hiyo ya kishushushu.

Taasisi hiyo ya kishushushu imeeleza kuwa inataka kufikika (accessible) na kuufahamisha umma kuhusu shughuli zake. Kadhalika, inataka majadiliano na watu wenye ufahamu wa teknolojia hususan katika maeneo ya teknolojia, hisabati, usalama mtandaoni na mada nyinginezo.




16 May 2016

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akihutubia Watanzania wanaoishi hapa Uingereza



Sehemu ya hotuba ya Waziri Mkuu Majaliwa


Baadhi ya Watanzania wanaoishi hapa Uingereza wakiwa katika mkutano huo na Waziri Mkuu Majaliwa



Sehemu ya hotuba ya Waziri wa Mambo ya Nje Balozi Mahiga

Waziri Mkuu Majaliwa na Balozi Mahiga 

Baadhi ya Watanzania wanaoishi hapa Uingereza wakiwa katika mkutano huo




Waziri Mkuu Majaliwa akiwa na Kaimu Balozi Mr Marwa (wa kwanza kushoto), Balozi Mahiga na Jaji Mkuu Chande (kulia)

Waziri Mkuu Majaliwa akihutubua


Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Valentino Mlowola akiongea kwenye mkutano huo


Jaji Mkuu Chande akiongea


Jaji Mkuu Chande akiongea. Kushoto kabisa ni Balozi Mahiga na kulia ni Kamanda Mlowola

Waziri Mkuu Majaliwa akihutubia


Meza kuu


Sehemu ya Watanzania waliohudhuria Mkutano huo uliofanyika kwenye ubalozi wa Tanzania jijini London hapo jumamosi Mei 14, 2016

14 May 2016


Jana nilibandika makala kuhusu manung'uniko ya Watanzania wengi wanaoishi hapa Uingereza ambao walikuwa hatarini kukosa fursa ya kuhudhuria mkutano na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ambaye yupo nchini hapa kikazi.

'Kelele' hizo zimezaa matunda, na leo Waziri Mkuu Majaliwa atakutana na Watanzania wote wanaoishi nchini humu wanaoweza kumudu kufika ubalozini London saa kumi alasiri. Awali, maofisa husika katika ubalozi huo walialika kundi dogo tu la Watanzania kuhudhuria mkutano huo, hatua iliyotafsiriwa na wengi kama ubaguzi na pengine jitihada za kuficha majipu yanayoukabili ubalozi huo.

Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu imeandikwa kidiplomasia, ambapo kwa upande mmoja imejitoa lawama ya kuhusika na maandalizi ya mkutano huo (na hakuna aliyemlaumu Waziri Mkuu au Ofisi yake bali lawama zilielekezwa kwa ubalozi) .



Kwa upande mwingine ni kama imekanusha 'madai ya watu' kuwa kuna watu maalum waliochaguliwa kuhudhuria mkutano huo (badala ya kuwa mkutano wa wazi kwa kila Mtanzania anayeishi hapa). Nimesema ni "lugha ya kidiplomasia" kwa sababu uthibitisho kwamba awali mpango wa ubalozi ulikuwa ni kama ulivyolalamikiwa jana , yaani kundi la watu kadhaa tu ndio wakutane na Waziri Mkuu, na uthibitisho huo unasikika katika audio hii ya mmoja wa maofisa wa ubalozi wetu anayetukebehi kwa kudai haki ya kukutana na Waziri Mkuu. Msikilize kwa kubonyeza play


Ni wazi kuwa laiti afisa ubalozi huyo ndio angekuwa na mamlaka ya mwisho basi ni wazi angebaki na hao watu wachache ambao awali ndio waliteuliwa kuhudhuria mkutano huo kana kwamba ni wa siri.

Badala ya kukiri kwamba ubalozi ulifanya makosa kuteua watu wachache tu, afisa huyo anaelekea kutuona kituko kwa kudai haki ya msingi ya kukutana na viongozi wetu wa kitaifa. Na badala ya kutumia fursa hiyo kuwaeleza Watanzania ratiba ya mkutano huo (tetesi zinasema utafanyika ubalozni mida ya saa 10 jioni) yeye ameamua kutunanga. Madaraka huwafanya baadhi ya wenzetu kujisahau sana.

Tukiweka kando lugha ya kidiplomasia ya Ofisa ya Waziri Mkuu na kebehi za afisa ubalozi, la muhimu ni kwamba sasa Watanzania wote wanaoishi hapa Uingereza wamepewa fursa ya kuhudhuria mkutano huo muhimu na Waziri Mkuu. Binafsi nimefarijika sana kwa sababu nilijitahidi kulipigia kelele suala hilo kwenye kundi la Whatsapp la jumuiya ya Watanzania ambayo ipo katika hatua za awali za kuundwa, japo mapokeo hayakuwa ya kuridhisha (watu wanahimiza umoja lakini walikalia kimya 'ubaguzi' uliotaka kufanywa na baadhi ya maafisa ubalozi wetu hapo London). 

"Kelele" zangu hazikutokana na mie kutopewa mwaliko, kwa sababu hata kama ningekuwa miongoni mwa watu hao takriban 40 walioalikwa bado nisingehudhuria (na leo sintohudhuria...kwa sababu zangu binafsi). Nilipiga kelele kwa maslahi ya walio wengi ambao pengine kwa namna moja au nyingine walishindwa kupiga kelele hizo wao wenyewe. Sie wengine tuna kumbi kama hii ya blogu au makala magazetini ambazo ni rahisi kupiga kelele na watawala kutusikia. Lakini si kila mtu ni blogs au mwandishi wa makala. Ni matumaini yangu kuwa 'kelele' hizi zitawahamasisha wengi kutambua kuwa 'kelele dhidi ya jambo lisilofaa' sio uchizi, kusaka umaarufu au ukorofi. Marehemu Kighoma Ali Malima aliwahi kutuusia kwamba "HAKI HAIPASWI KUOMBWA KAMA ZAWADI. HAKI HUDAIWA...KWA NGUVU IKIBIDI."

13 May 2016

Ubalozi wa Tanzania hapa Uingereza umeingia lawamani kufuatia uamuzi wake wa 'kuwabagua' baadhi ya Watanzania wanaoishi nchi hapa na kuwanyima fursa ya kuhudhuria mkutano unaotarajiwa kufanyika kesho kati ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa na Watanzania wanaoishi hapa.

Kwa kawaida, viongozi wa kitaifa wanapokuja hapa kutoka huko nyumbani huongea na Watanzania wanaoishi hapa, na utaratibu uliozoeleka ni kutangaza tarehe, mahala na muda wa mkutano, kinyume na hali iliyojitokeza sasa ambapo inaelezwa kuwa kuna kikundi kidogo tu cha watu walioteuliwa kukutana na Waziri Mkuu Majaliwa.

Blogu hii ilifanya jitihada za kuwasiliana na Watanzania kadhaa wa hapa, na ukiweka kando wachache waliosema kuwa wasingeenda katika mkutano huo hata kama wangealikwa, wengi wao walilaumu kitendo hicho cha ubalozi kuteua kundi la watu wachache, ambapo wala haifahamiki wachache hao waliteuliwa kwa vigezo gani.

Baadhi ya waliohojiwa na blogu hii walieleza kuwa huenda "ubalozi huo ni jipu, na umeamua kuteua kundi la watu wachache ili kuepusha uwezekano wa mtu 'asiyejulikana' kukurupuka na kumfahamisha Waziri Mkuu kuhusu malalamiko yanayouhusu ubalozi huo (kama kweli yapo)."

Kadhalika, ilielezwa kuwa kitendo cha ubalozi huo kufanya 'ubaguzi' huo kinaweza kuijiengea serikali ya Awamu ya Tano ya Rais John Magufuli taswira mbaya, kwamba "Waziri Mkuu amekwepa kuongea na Watanzania kwa wingi au uwazi na badala yake anakutana na kikundi kidogo cha wateule wachache."

Vilevile, kitendo hicho kinaweza kumtengenezea mazingira magumu Balozi mpya wa Tanzania nchi hapa, Dkt Asha-Rose Migiro, iwapo 'walionyimwa fursa ya kuhudhuria mkutano huo' watabaki na mtizamo kuwa "mnatutenga wakati wa ziara za viongozi wa kitaifa basi nasi twawatenga katika maisha yetu ya kila siku."

" Au ndio yale ya Bunge Dodoma kwamba halirushwi live, basi sasa hata viongozi wetu wakuu wakija hapa, badala ya kukutana nasi kwa uwazi na wingi, fursa hiyo inatolewa kwa wateule wachache tu...kwa maslahi binafsi."

Wakati ubalozi hauwezi kukwepa lawama kwa vile kimsingi wenyewe ndio wenye mamlaka ya kufanya maandalizi ya mkutano huo, haieleweki kwanini 'jumuiya kuu mbili za Watanzania hapa Uingereza,' Kikosi Kazi na Kamati ya Mpito hazijafanya jitihada zozote kupigia kelele kuhusu kasoro hiyo. Badala yake, kila upande umekuwa ukiutuhumu upande mwingine 'kutumiwa na Ubalozi kwa maslahi binafsi.'

Awali, jana kulipatikana kipande cha sauti kilichorekodi sehemu ya kipindi cha Jahazi cha Clouds FM ya huko nyumbani, ambapo waendesha kipindi walijadili kwa ufupi kuhusu kasoro hiyo ya Waziri Mkuu kuandaliwa mkutano wa kuongea na idadi ndogo tu ya Watanzania, katika utaratibu usio wazi. Bonyeza hapa chini kusikiliza
Hadi wakati blogu hii inakwenda mitamboni, hakuna taarifa yoyote rasmi kutoka kwa ubalozi au makundi makuu mawili yanayowakilisha Watanzania hapa, kuhusu kwa mfano mkutano huo utafanyika lini, wapi na muda gani.

Hata hivyo, baadhi ya waliohojiwa walionyesha matumaini kuwa inawezekana Waziri Mkuu haelewi kuhusu 'usanii unaofanywa na ubalozi,' na akipata taarifa atauagiza ubalozi huo kufanya maandalizi ya kuwezesha Watanzania wengi zaidi kuhudhuria mkutano huo.

6 May 2016

Bila shaka matokeo ya utafiti huu yatawashangaza watu wa nchi nyingine, lakini sio sie Watanzania, ambao tumebainika kuwa watu wanafiki zaidi kuliko wote duniani. Sio jambo la kushangaza kwa sababu unafiki umekuwa sehemu ya utamaduni wetu.

Na mfano mwepesi wa unafiki wetu ni kuhusu uamuzi wa serikali kuipiga marufuku video ya msanii Snura iitwayo 'Chura' ambayo ilivuka mipaka ya ustaarabu. Awali, watu wengi waliishutumu Serikali kwa kuruhusu video hiyo 'chafu' kuonyeshwa ilhali vikao vya bunge vikizuiwa kuonyeshwa 'live.' Well, japo bunge laendelea 'kufichwa,' lakini serikali imejitutumua na kipiga kufuli video ya 'Chura.'

Lakini hatua hiyo imewakera baadhi ya wenzetu. Wengine wanadai serikali ina vitu muhimu zaidi vya kufanya badala ya kufungia video. Wengine wanadai mbona kuna video chafu zaidi za 'akina Rihanna' kuliko hiyo ya Chura. Wengine wanakwenda mbali na kudai kuwa alichofanya Snura na hao mabinti wa kwenye video ni UBUNIFU. Really?????

Twende kwenye maisha yetu ya kila siku. Tuchukulie mfano vifo. Utakuta watu wanasubiri mpaka mtu afe ndio waanze kumwagia sifa, "Oh marehemu alikuwa mtu mzuri sana, oh marehemu alikuwa mwema sana...RIP...RIP..." Hii tabia ya kuwapenda watu wakifa lakini kuwachukia walipokuwa hai ni nini kama sio UNAFIKI? Angalia Marehemu Kanumba alivyoandamwa wakati wa uhai wake. Msanii aliyefanya kazi kubwa kabisa kuiinua medani ya filamu za Kitanzania aliandamwa mfululizo na hili na lile, huku watu wasio na vipaji ya kitu chochote kile wakigeuka mahakimu na majaji dhidi ya kipaji cha msanii huyo. 

Tuangalie huko mitaani tunakoishi na 'makazi yetu mapya' mitandaoni. Huko mitaani, wenzetu wenye umuhimu mkubwa kwa jamii - madaktari, manesi, walimu, nk -  hawapewi heshima kubwa kulinganisha na wanayopewa wahalifu kama wauza madawa ya kulevya au wabadhirifu serikalini. Twaita wauza unga WAZUNGU WA UNGA, na wabadhirifu twawaita MAPEDEJEE, VIBOSILE, VIGOGO, na majina mengine ya kuwatukuza, ilhali jina lao stahili ni WAHALIFU. 

Nenda mtandaoni, kwa mfano Instagram. Ukiacha wasanii wetu na watu wengine muhimu, watu maarufu zaidi katika mtandao huo kwa Tanzania ni wale wenye kuongoza makundi ya matusi, picha za utupu, majungu, na madudu kama hayo. Sio kwamba hawa 'wameroga' ili kuwa maarufu. Hapana. Umaarufu wao unatokana na Watanzani wengin kupenda vitu hivyo: picha za utupu, majungu, nk.

Angalia wakati wa uchaguzi. Wanasiasa wetu hujiweka karibu kabisa na wananchi. Si ajabu kuona mwanasiasa akiwasalimia wananchi kwa kupiga magoti 'kwa heshima' wakati anaomba kura.Subiri ashinde uchaguzi. Humsikii japo akicheka au kuzomea bungeni. Unaweza kuhisi kuwa asilimia kuwab ya wabunge wetu wanatoka majimbo ya nchi kama Uingereza au Marekani, ambazo zina matatizo machache kwa wapigakura, kwani haiingii akilini kwa mbunge ambaye jimbo lake lina matatizo lukuki awe haonekani bungeni unless kwenye kukusanya posho tu, na akitokea bungeni, si ajabu kuona amepigwa picha huku kachapa usingizi (labda alishindwa kulala kutokana na kuzongwa na mawazo kuhusu jimbo lake?)

Anyway, turudi kwenye utafiti unathibitisha tulivyobobea kwa unafiki. Watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Nottingham cha hapa Uingereza waliendesha utafiti wa kupima kushamiri kwa ukiukwaji wa kanuni katika nchi 159 duniani, wakitumia takwimu za kutoka mwaka 2003 kuhusu ubadhirifu katika siasa, ukwepaji kodi na rushwa.

Twende tena mtaani. Kuna suala la ushoga ambalo taarifa zinaeleza kuwa unakua kwa kasi huko nyumbani. Juzi kuna shoga mmoja kafiwa Dar, na inaelezwa kuwa takriban kila mtu maarufu jijini hapo hakukosekana msibani. Lakini sio katika msiba huo tu, nenda Instagram halafu angalia akaunti za mashoga na idadi ya 'followers' wao. Hivi yawezekanaje kama 'ushoga sio tu ni laana bali pia ni kinyume cha sheria za Tanzania,' then shoga awe na 'followers' zaidi ya laki moja? Kwanini kila shughuli ya mastaa wetu haiwi kamili bila uwepo wa mashoga wa 'kukata viuno' kwenye shughuli hiyo?


Habari kamili kuhusu utafiti huo ipo HAPA na kuna MAKALA HII katika gazeti la kila wiki la RAIA MWEMA Toleo la wiki hii imeandika kwa kirefu kuhusu suala hilo

28 Apr 2016

MIONGONI mwa wahadhiri walionifundisha nilipokuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ni Mmarekani mmoja aliyependa sana kufundisha kwa kutumia mifano halisi. Moja ya mada ambazo zilizonigusa sana ni kuhusu ‘undugunaizesheni.’ Alieleza kuwa hata Marekani kuna tabia hiyo, ambapo mara nyingi watu wenye nyadhifa muhimu hupenda kufanya kazi na watu wanaowafahamu au hata ndugu zao. 

Na kwa vile mfumo wa serikali nchini humo sio kama wetu wa ‘ili mtu ateuliwe kuwa waziri sharti awe mbunge – awe wa kupigiwa kura na wananchi jimboni, wa viti maalumu au wa kuteuliwa na rais. Kwa wenzetu huko, rais anaweza kumteua mtu yeyote kuwa kwenye “kabineti” yake japo baadhi ya nyadhifa zinahusisha mteuliwa kuidhinishwa na mabunge ya nchi hiyo. 

Mhadhiri huyo Mmarekani alitanabaisha kuwa baadhi ya viongozi ‘huwavuta’ ndugu zao wa karibu, jamaa au marafiki sio tu kwa vile ni watu wao wa karibu bali pia kulingana na sifa walizonazo. Lakini la muhimu zaidi ni matarajio kuwa ndugu, jamaa au rafiki anaweza kuwa mtiifu sana kwa aliyemteua, hasa ikizingatiwa kuwa ‘akimwangusha, anajiangusha naye pia.’

Kwa hiyo, si kwamba suala la undugunaizesheni – kufanya upendeleo kwenye maeneo kama vile teuzi za nafasi za uongozi, halipo Afrika, au huko nyumbani pekee bali hata huku kwa hawa wenzetu wanaojigamba kwa kuzingatia taratibu na kanuni. 

Kimsingi, kumteua mtu unayemjua, alimradi ana sifa stahili, sio kuvunja taratibu na kanuni, hususan kama mchanganuo wa kumteua mtu huyo haukuwanyima watu wengine fursa ya kuteuliwa. 

Suala la ‘undugunaizesheni’ limekuwa likinijia akilini kila ninapokutana na habari kuhusu sakata la Lugumi. Lakini pengine kabla ya kuingia kwa undani kujadili sakata hilo ni vema nikaweka bayana msimamo wangu maana ‘wenye nchi’ wamekuwa wakali kweli, ukikosoa kidogo tu unaonekana kuwa wewe ni jipu au mtetezi wa majipu.

Ni kwamba namuunga mkono Rais Dk. John Magufuli, katika jitihada zake kubwa za kutumbua majipu. Hata hivyo, mara kadhaa amekuwa akitusihi Watanzania tumsaidie katika jitihada zake hizo. Na miongoni mwa njia za kumsaidia mtu ni kumshauri au hata kumkosoa pale inapobidi. Binafsi, ninaamini kuwa mtu pekee anayeweza kumaliza sakata la Lugumi ni Rais Magufuli tu, hakuna cha Bunge wala Takukuru. Ni hivi, si mfanyabiashara yeyote tu anayeweza kupewa zabuni nyeti ya kuweka mashine za kuchukua alama za vidole katika mamia ya vituo vya polisi nchini. Mtu anayepewa dhamana kubwa namna hiyo lazima awe ‘mtu fulani.’ 

Mengi yanayozungumzwa kuhusu mmiliki wa kampuni hiyo ya Lugumi yamebaki kuwa tetesi tu, lakini moja linalisikika zaidi ni madai kuwa alikuwa ‘karibu na watawala’ katika Serikali ya Awamu ya Nne. Na kwa jinsi tunavyoelewa nchi yetu ilivyokuwa inajiendesha yenyewe (on autopilot) katika awamu hiyo, hakuna miujiza hapa wala hakuna la ajabu ambalo lisingewezekana. Tuwe wakweli, nchi ilikuwa inaendeshwa kimzaha. 

Tetesi pia zinadai kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga, ambaye sio tu ndiye mwenye dhamana ya kufuatilia kuhusu sakata hilo kwa vile linaihusu wizara yake, lakini pia ni mmoja wa wanaotajwa kuhusika na ufisadi huo kupitia umiliki wa kampuni yake ya Infosys. 

‘Mazingaombwe’ yanayolizunguka sakata hili yanazidi kuendelea. Awali, ilielezwa kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi aliikwepa Kamati husika ya Bunge alipotakiwa kutoa maelezo kuhusu sakata hilo. Baadaye, tukasikia Bunge likitoa taarifa za kujikanganya, ikiwa na pamoja na kituko cha kudai kuwa kamati husika haikuomba mkataba husika bali maelezo tu (kana kwamba kuomba mkataba huo ni kuvunja sheria za nchi). 

Siku chache baadaye, ikaibuka video inayomwonyesha mtendaji mmoja wa kampuni ya Infosys akieleza kuwa Waziri Kitwanga sio mmiliki wa kampuni hiyo, na kwamba aliachana nayo kabla haijaingia mkataba huo wenye utata. 

Baadaye tena, Waziri Kitwanga mwenyewe akajitokeza kuzungumzia suala hilo akidai kuwa wakati suala hilo linatokea, yeye hakuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, na ndio maana hapendi wala hataki kuzungumzia suala hilo. 

Kauli hii inatoka kwa waziri ambaye Jeshi la Polisi lipo chini ya wizara yake. Sawa, hakuwa waziri wakati suala hilo linatokea, lakini sasa ni waziri. Kwa nini basi asipende wala kutaka kuongelea suala ambalo sio tu linaitia doa wizara yake na jeshi la polisi bali pia linaweza kuathiri usalama wa taifa letu? 

Kwa nini kama Waziri Kitwanga anajua vema majukumu yake hakushughulikia suala hilo kabla ya kuibuliwa na Kamati ya Bunge? Na hapo tunaweza kujiuliza, kwa nini Rais Magufuli hakuchukua hatua stahili dhidi ya mtendaji wake huyo, kwa staili ya kutumbua majipu? 

Sarakasi za sakata la Lugumi zimeendelea kwa Bunge kuunda timu maalumu ya kuchunguza suala hilo. Nilidhani kuwa Takukuru wangeweza kufanya kazi hiyo kwa ufanisi zaidi kwa vile sidhani kama wabunge walioteuliwa ni wataalamu wa uchunguzi wa masuala yenye dalili za ufisadi. Labda tuwape muda, huenda wanajua wanachofanya. 

Kichekesho zaidi kimeibuka muda mfupi kabla sijaandaa makala hii, ambapo Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Ernest Mangu ameibuka na kudai kuwa kampuni ya Lugumi ilitekeleza mkataba husika, na kukanusha madai ya Kamati husika ya Bunge, na taarifa zilizosambaa mtandaoni na kwenye vyombo vya habari kuwa kampuni hiyo ilishindwa kufunga mashine za kuchukulia alama za vidole kwenye vituo 108 kama ilivyotamkwa kwenye mkataba. 

IGP Mangu alidai kushangazwa na habari hizo na kueleza kuwa kampuni ya Lugumi ilitekeleza mkataba husika kama ilivyokubaliana na serikali. 

“Siyo kweli, watu wana ugomvi wao, lakini nakueleza wazi kwamba, tembelea vituo vyote tulivyokubaliana, utakuta mashine zipo. Inawezekana zingine hazifanyi kazi kwa sababu ya kukosekana kwa intaneti,” alisema mkuu huyo wa jeshi la polisi. 

Ni akina nani hao “wenye ugomvi wao” ambao jeshi la polisi linashindwa sio tu kuwachukulia hatua bali hata kuwataja majina hasa ikizingatiwa kuwa kashfa hiyo inachafua taswira ya taasisi hiyo ya dola? 

Na kama huo ndio ukweli, kwa nini basi IGP Mangu hakujitokeza kwenye kikao cha Kamati ya Bunge iliyokutana kufuatilia suala hilo? Si angeenda tu na kuwaeleza kama anavyosema sasa kuwa suala hilo linatokana na “ugomvi” wa watu fulani? 

Lakini utetezi wake ungekuwa na maana tu kama angeweza kubainisha ni vituo vingapi na vipi ambavyo mashine hizo zilifungwa, na vingapi na vipi ambavyo mashine zinafanya kazi au hazifanyi kazi. 

Na kuhusu uwezekano wa kuwepo mashine zisizofanya kazi kutokana na kutokuwepo kwa Intaneti, basi ni uzembe wa wazi wa IGP na Waziri wake Kitwanga kwa sababu hilo ni jipu lililopaswa kutambuliwa mapema kabla ya kuibuliwa na kamati ya Bunge. Je, huduma ya Intaneti ilikatwa kwa kutolipiwa kwa vile Jeshi la Polisi lilinyimwa fungu husika au ni habari zile zile wa ‘watumishi hewa’? 

Nilianza makala hii kwa kuzungumzia suala la undugunaizesheni. Kuna hisia kuwa uteuzi wa Waziri Kitwanga ulitokana na ukaribu alionao na Rais Magufuli. Hilo sio kosa. Lakini ni jukumu la mteuliwa kuhakikisha hamwangushi aliyemteua. Na katika sakata hili la Lugumi, yayumkinika kuhisi kuwa Waziri Kitwanga anamwangusha Rais Magufuli. 

Wengi tuna imani na Dk. Magufuli, lakini ni ukweli usiofichika kuwa moja ya mitihani mikubwa inayomkabili ni pamoja na uwezekano wa kuangushwa na ‘maswahiba zake,’ watu anaowaamini lakini wasioitendea haki imani hiyo, shinikizo ndani ya chama chake CCM, na kubwa zaidi, ‘madudu’ yaliyofanyika katika awamu iliyopita hususan yale ambayo akiyagusa tu, nchi itatikisika (rejea kauli ya aliyekuwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliyowahi kuitoa bungeni kuhusu sakata moja la ufisadi ambapo aliwaambia bayana wabunge wamsulubu tu lakini asingeweza kuongelea suala husika). 

Nimalizie makala hii kwa kumsihi Rais Magufuli kuwa uungwaji mkono anaohitaji zaidi ni kutoka kwa Watanzania wa kawaida, waliompigia kura na hata waliomnyima kura. Hawa hawatomwangusha kwa sababu wanamhitaji, na hadi sasa amewathibitishia hivyo. Baadhi ya watendaji wake wapo kwa maslahi yao binafsi, na hawa watamwangusha asipokuwa makini. Ni muhimu kwa Rais wetu kukumbuka kuwa utumbuaji majipu halisi unamtengenezea maadui lukuki, ambao wanaweza kuunganisha nguvu na kumyooshea kidole pale yanapojitokeza mambo kama haya ya kina Lugumi. 


Mpendwa Rais Magufuli, chukua hatua moja tu na sakata hili la Lugumi litamalizika (kwa maslahi ya Watanzania) 

21 Apr 2016


MAJUZI nilibandika habari mbili kwenye mtandao wa kijamii wa Facebook zilizohusu ufisadi na umasikini. Habari moja ilihusu taarifa za vyombo vya habari kwamba wabunge wameshtushwa na ripoti inayoonyesha Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetumia shilingi bilioni 18 kwa ajili ya mafunzo, semina na warsha.

Niliambatanisha habari hiyo na nyingine iliyoonyesha ‘shule ya kipekee’ ambayo madarasa matatu yanalazimika kutumia jengo moja, kitu ambacho kinaweza kuiingiza shule hiyo katika rekodi ya miujiza ya Guinness.

Lengo lilikuwa kuonyesha kuwa wakati TCRA ikitumia mabilioni hayo kwa ajili ya mafunzo, semina na warsha, kuna wanafunzi wanaosoma katika mazingira magumu kwa kulazimika ‘kuchangia’ jengo la darasa.

Watumiaji wengi wa mtandao huo wa kijamii waliguswa na habari hiyo, lakini kilijitokeza kikundi kidogo kilichoitetea TCRA kwa nguvu zote. Hoja yao kuu ni kuwa majukumu ya taasisi hayo ni muhimu na teknolojia inabadilika kwa kasi, kwa hiyo ni sahihi kutumia fedha nyingi kuiwezesha taasisi hiyo kwenda na wakati.

Kilichonisikitisha zaidi ni pale wanahabari wawili wakongwe (mmoja wa gazeti hili) ‘walipomvuta’ kiongozi mmoja wa TCRA, sio kwa minajili ya kumbana kuhusu taarifa hiyo bali kuvilaumu vyombo vya habari vilivyoripoti habari hiyo, sambamba na kutetea matumizi hayo ya mabilioni kwa mafunzo, semina na warsha.

Nilikerwa mno na utetezi wa wanahabari hao kwa sababu laiti wangerejea ripoti za nyuma kuhusu matumizi ya taasisi hiyo wangetambua tukio hilo sio la mara ya kwanza. Mwaka 2011, Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) ilikagua hesabu za TCRA na kugundua madudu ya kutisha, ikiwa ni pamoja na mamlaka hiyo kusomesha nje wafanyakazi wake watatu kwa gharama ya shilingi bilioni 2.2

Na hata kama TCRA ingekuwa haijawahi kuingia matatizoni kutokana na matumizi hayo makubwa ya fedha za umma, bado isingehalalisha taasisi hiyo kutumia shilingi bilioni 18 kwa ajili ya mafunzo, semina na warsha. Sio kwa Tanzania yetu hii ambayo ni moja ya nchi masikini kabisa duniani.

Lakini kingine kilichonikera kuhusu matumizi hayo ya ‘anasa’ ya TCRA ni ukweli kwamba mamlaka hiyo kwa kiwango kikubwa imekuwa butu hususan katika eneo la udhibiti dhidi ya makosa ya mtandaoni. Taasisi hiyo ilikuwa mstari wa mbele kutetea muswada wa sheria ya makosa ya mtandao (Cybercrime Bill 2015) hadi ilipopitishwa kuwa sheria kamili.

Binafsi niliunga mkono muswada huo na hatimaye sheria husika kwa sababu, kwa upande mmoja, nilikwishawahi kuwa mhanga wa unyanyasaji mtandaoni, na kwa upande mwingine, nilikuwa nikikerwa mno na matumizi mabaya ya uhuru mtandaoni yaliyojumuisha matusi, picha za utupu na vitendo vingine visivyofaa, hususan katika mtandao wa kijamii wa Instagram.

Sasa, tangu sheria hiyo dhidi ya uhalifu wa mtandaoni ipitishwe imeishia kuungana na lundo la sheria nyingine kali lakini zisizo na ufanisi wowote. Ni kweli kwamba hoja za waliokuwa wakiipinga sheria hiyo zilikuwa na mantiki, hususan hofu kuwa itatumika vibaya, hususan uwezekano wa kutumika kisiasa zaidi kuliko kisheria.

Inatusikitisha baadhi yetu tuliotumia nguvu kubwa kuunadi muswada wa sheria hiyo ambao ulipata upinzani mkali kutoka kila kona ya Tanzania, lakini hatimaye ulifanikiwa na kuwa sheria kamili.

Majuzi, sheria hiyo imeonekana kufanya kazi ‘ghafla.’ Kijana mmoja amekamatwa na kufikishwa mahakamani chini ya ulinzi mkali kabisa, kwa kosa la kumtukana Rais John Magufuli.

Hakuna Mtanzania mwenye akili timamu anayeweza kuunga mkono kuwatusi viongozi wetu, awe Rais au mwenyekiti wa kijiji. Tatizo ni kwamba sheria hiyo dhidi ya uhalifu mtandaoni inaonekana kuwa na meno pale tu ‘wakubwa’ wanapoguswa.

Kwa yeyote anayetaka kuthibitisha jinsi gani sheria hiyo ‘ina upendeleo’ atembelee mtandao wa kijamii unaohusu picha, yaani Instagram, ambapo huko kuna kila aina ya laana: kuna ushoga wa waziwazi, kuna lundo la akaunti zinazobandika picha za utupu, kuna ‘ligi kuu’ ya matusi ambapo kadri watu wanavyoonyesha umahiri wa matusi ndivyo kadri wanavyopata wafuasi wengi.

Hali huko Instagram ni mbaya mno kiasi kwamba ni rahisi kudhani kuwa wanaofanya ‘madudu’ huko wapo katika nchi isiyo na sheria (lawless country). Kwa vile ‘wakongwe’ wa matusi wameendelea kupata umaarufu kwa kutukana pasipo kuchukuliwa hatua zozote, mtandao huo umewavutia hata watu ‘wasio na matusi’ kujaribu fursa ya kujipatia umaarufu wa bure.

Na umaarufu huo una ‘faida’ kwani akaunti zinazosheheni matusi pia hufanya matangazo ya biashara mbalimbali, kuanzia ‘video za ngono’ hadi tiba za ajabu ajabu.

Wakati fulani niliwajulisha watu wa TCRA kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter, lakini ‘bosi’ wa mamlaka hiyo aliishia kutoa ‘darasa’ refu lisilo na maana akidai kuwa ni muhimu Watanzania watambue sheria zilizoianzisha Mamlaka hiyo na shughuli zake kwa ujumla. Alidai kuwa jukumu la udhibiti wa matusi na uchafu mwingine huko Instagram ni la polisi. Kichekesho ni kwamba kesi ya huyo jamaa aliyemtukana Rais inaendeshwa kwa ushirikiano kati ya polisi na TCRA.

Kwa hiyo si kwamba TCRA haina mamlaka ya kupambana na ‘laana’ inayoendelea huko Instagram, lakini kinachoonekana ni kwamba haina muda na adha zinazowakumba wananchi wa kawaida. Uvunjifu huo wa sheria ukimgusa kiongozi, basi mamlaka hiyo na sheria dhidi ya uhalifu wa mtandaoni vinafufuka ghafla. Hii sio sawa hata kidogo.

Nimalizie makala hii kwa kuisihi serikali ifanye jitihada za makusudi kukomesha hali mbaya inayoendelea katika mtandao huo wa kijamii. Haihitajiki kukamata kila mhusika lakini vinara wachache tu wakitiwa nguvuni itasaidia kufikisha ujumbe kwa wenzao.

Suala hili linaweza kuihusu wizara yenye dhamana na masuala ya afya pia, kwa sababu mtandao huo umegeuka kuwa duka lisilo rasmi la dawa za aina mbalimbali, suala ambalo linaziweka afya za Watanzania shakani.

Penye nia pana njia, pasipo na nia pana kisingizio. 

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.