Showing posts with label JOHN MAGUFULI. Show all posts
Showing posts with label JOHN MAGUFULI. Show all posts

20 Jun 2017

Katika Tanzania yetu ya zama hizi ambapo takriban kila jambo linaanglaiwa kwa jicho la kisiasa, ni vigumu sio tu kusimamia ukweli bali pia kukwepa lawama kutoka kwa pande mbili kuu za siasa zetu: CCM au Upinzani.

Sie tusio na vyama, tukikosoa masuala yanayoigusa CCM/serikali, akina Humphrey Polepole wanakurupuka na kutuita majina ya ajabu ajabu. Tukikosoa Upinzani, tunaambiwa "nafasi za Ukuu wa Wilaya zimeshajaa." Good news is, kuna watu - hata kama ni wachache - waliopo CCM, Upinzani na wasio na vyama ambao wanatusikiliza. Na wanatusikiliza kwa vile wanafahamu hatuelemei upande wowote isipokuwa kwenye ukweli.

Baada ya angalizo hilo, tugeukia big news iliyosikika jana, ghafla, na kutukuta wengi wetu tusiamini macho/masikio yetu. Baada ya miaka nenda miaka rudi, hatimaye mfanyabiashara James Rugemalira na mwenzie Singasinga Harbinder Seth Singh walipandishwa kizimbani kwa tuhuma za kuhujumu uchumi.



Kwa tunaofahamu Rugemalira ameisumbua Tanzania yetu kiasi gani, na sambamba na 'usumbufu' wa huyu Singasinga, hatua hiyo tu ya kuwapindisha wawili hao kizimbani inastahili pongezi za kila Mtanzania. Na anayestahili pongezi hizo kwa wingi kabisa ni Rais John Magufuli.
Sawa, kuna watakaosema kuwa "lakini hiyo si ndio kazi ya Rais?" only if tukipuuzia ukweli kwamba Rugemalira alikuwa kama ameshindikana katika Awamu angalau mbili zilizopita, ya Mkapa na Kikwete, na ilikuwa kama huyu mtu kaachwa afanye apendacho katika kuihujumu nchi yetu.
Nimesoma angalizo la mwanasiasa wa Chadema na mwanasheria nguli, Tundu Lissu, akitahadharisha kuhusu Rugemalira na Singasinga, kwamba hao ni sehemu tu ya mtandao mkubwa wa ufisadi. Hata hivyo, japo angalizo hilo ni muhimu, haliondoi ukweli kwamba angalau JPM amethubutu, sio tu kuwapandisha Rugemalira na Singasinga kizimbani bali pia kuwalaza rumande.

Ni wazi kuwa vita hii ambayo Rais Magufuli ameivalia njuga sio rahisi. Sio tu kwa vile inahusisha watu wenye uwezo mkubwa kifedha bali pia kwa sababu pia inawagusa baadhi ya wanasiasa maarufu ndani ya chama chake cha CCM. 
Licha ya angalizo la Lissu, kuna baadhi ya wananchi wanaotoa tahadhari 'kushangilia mapema kabla ya dakika 90.' Hawa pia wana hoja ya msingi hasa kwa kuzingatia mfano kama wa kesi ya Balozi Mahalu. Hata hivyo, kuna haja ya kuwa na matumaini hasa ikizingatiwa kuwa JPM hafanyi anayofanya kwa shinikizo la mtu yeyote yule. Ni utashi wake tu. Angetaka kukaa kimya, kusingekuwa na maandamano ya kumshinikiza achukue hatua.

Kama ningekuwa na fursa ya kumshauri Rais Magufuli basi ningemwomba sana awekeze nguvu zaidi katika vita hii dhidi ya ufisadi ambayo kwa hakika inawaunganisha Watanzania wengi waliochoka kuona nchi yao ikigeuzwa shamba la bibi, badala ya 'uhasama na wanasiasa wa Upinzani.'

Kwa mfano, jana, kabla ya habari hiyo ya Rugemalira na Singasinga kufikishwa mahakamani na baadaye kutupwa rumande, zilizpatikana taarifa kuhusu serikali kupitia jeshi la polisi 'kuwabughudhi' wanasiasa kadhaa wa Chadema ikiwa ni pamoja na kuzuwia ziara ya Waziri Mkuu wa zamani na kiognozi wa ngazi za juu Chadema, Frederick Sumaye.
Katika kipindi hiki cha vita ngumu dhidi ya mafisadi na ufisadi, tunapaswa kuwa kitu kimoja. Si kwamba vyama vya upinzani viungane na CCM, bali angalau tofauti zisizo na msingi ziepukwe, na kubwa zaidi ni kupeuka uadui wa kisiasa.

Nihitimishe kwa pointi moja muhimu kwamba japo tuna historia isiyopendeza kuhusu mapambano dhidi ya ufisadi, na japo ni kweli kuwa wanasheria wa serikali hawana rekodi nzuri kwenye kesi kubwa za serikali, na vilevile japo ni kweli kuwa mara nyingi ukada umekuwa kikwazo kwa serikali kuchukua hatua stahili dhidi ya mafisadi, wito wangu kwa Watanzania wenzangu ni kumuunga mkono Rais Magufuli kwani angalau ameonyesha dhamira ya kuchukua hatua stahili. 

Vilevile ni muhimu kutambua kuwa vita hii sio dhidi ya watu tu bali ni dhidi ya mfumo uliojengeka muda mrefu. Kwa maana hiyo, japo tunatamani kuona watuhumiwa wote wakikamatwa na kupandishwa kizimbani, ni muhimu tuwe na subira, hasa ikizingatiwa kuwa kukurupusha mambo kunaweza kutupelekea kupoteza kesi dhidi ya 'maadui' wetu ambao kwa uweo wao mkubwa wa kifedha, wataajiri wanasheria bora kabisa kuwatetea.

MUNGU IBARIKI TANZANIA

25 Mar 2017


Kuna wanaotusimanga tuliompigia kampeni Rais John Magufuli wakati wa kampeni za uchaguzi mwaka 2015. Kwamba sie ndo tumemleta Magufuli. Kwamba bila sie kumnadi, Tanzania isingeshuhudia kipindi hiki cha 'maajabu' ambapo kwa mara ya kwanza tumeshuhudia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam'anayebebwa na Magufuli' akiwa na uhuru wa kuvunja sheria, na yeyote atakayemkemea atakuwa amenunua ugomvi na Magufuli.

Wanaotusimanga wanasahau kitu kimoja. Laiti Upinzani ungekuwa na mgombea imara katika uchaguzi mkuu uliopita, kazi ya kuiangusha CCM ilikuwa rahisi kuliko wakati mwingine wowote ule.

Nakumbuka kada mmoja mwandamizi wa CCM alinieleza wakati wa kampeni kuwa "laiti Wapinzani walivyoungana na kumsimamisha mtu asiye na rekodi yenye mawaa, kwa mfano Dokta Slaa hivi, basi uchaguzi huu ungekuwa mgumu sana kwetu." Alieleza kuwa UKAWA uliirahisishia CCM kampeni ya kumnadi mgombea wake kwa vile, pamoja na sababu nyingine, mgombea wa UKAWA -Lowassa- alikuwa akijulikana vizuri mno huko CCM, kitu kilichowarahisishia kumshinda 'kirahisi.'

Kwahiyo, kabla ya kuachana na suala la lawama hizo, niseme hivi: sie tuliomnadi Magufuli hatukujua kuwa angekuja kubadilika kiasi hiki, lakini laiti Upinzani ungesimamisha mgombea bora, sie wengine wala tusingekimbia, tungefanya kampeni kama mwaka 2010, na kwa vile kwa kiasi kikubwa Upinzani auliamia kuweka kando tofauti zao, basi uwezekano wa kuiangusha CCM ulikuwa mkubwa. Ila hayo yameshapita sasa, tugange yaliyopo na yajayo.

Na yaliyopo tunayaganga vipi? Ni kwamba wakati tunaendelea kukuna vichwa kufahamu kitu gani kilichomsibu Rais Magufuli, aliyeingia kwa kishindo kikubwa sio Tanzania tu bali kimataifa pia, na hadi kutawala dunia na alama ya reli #WhatWouldMagufuliDo hadi kufikia hatua aliyofikia sasa ya kutawala kwa vitisho, jazba, ubabe na kutetea waziwazi uvunjifu wa sheria uliofanywa na RC Makonda, ni vema basi tujipange imara kuzuwia jitihada zozote za kiongozi huyu kuwa wa kutumia mabavu tu.

Kuna mwanafalsafa mmoja aliusia huko nyuma kuwa "ili maovu yashamiri, yahitaji tu watu wema kutofanya lolote." Wenye uwezo wa kupiga sauti dhidi ya maovu tukikaa kimya, labda kwa vile tu tuliwahi kumpigia kampeni Magufuli, au kwa vile "yatapita tu," kuna kila dalili kuwa tunakoelekea sio kuzuri.

Moja ya mambo yanayotatiza sana kuhusu Rais Magufuli ni kile kinachoonekana kama kupenda ugomvi usio wa muhimu. Hilo nimelieleza kwa kirefu katika makala ninayoiambatanisha hapo chini ambayo ilipaswa kuchapishwa na gazeti la Raia Mwema toleo la wiki hii lakini ninahisi haikuchapishwa (njia pekee ya mie kufahamu imechapishwa au la ni kuona makala husika kwenye tovuti ya gazeti hilo, na wiki hii haipo).

Kati ya nilipoandika makala hiyo na leo, kuna matukio makubwa manne yaliyojitokeza. Kwanza ni Waziri wa Habari (na masuala mengine)  Bwana Nape Nnauye kusimamia vema wajibu wake kama waziri husika, kufuatilia uvamizi uliofanywa na RC Makonda kwenye kituo cha redio na televisheni cha Clouds. Nape alipokea ripoti ya Tume aliyounda, na licha ya msimamo wa Magufulikujulikana mapema kuwa "anambeba Makonda," Nape alionyesha ujasiri na kuiweka hadharani ripoti hiyo ambayo awali baadhi yetu tulidhani ingekuwa 'changa la macho.'

Tukio la pili ni uamuzi wa Rais Magufuli kumfukuza kazi Nape kwa kufanya mabadiliko kwenye kabineti yake, na nafasi ya Nape kukabidhiwa Dkt Harrison Mwakyembe, ambaye majuzi tu 'alilikoroga' kwa kupiga marufuku kufunga ndoa bila cheti cha kuzaliwa. Amri hiyo ya kizembe ilitenguliwa na Magufuli siku chache baadaye.

Tukio la tatu ni mkutano wa Nape na waandishi wa habari, ambao tukiweka kando aliyoyasema mwanasiasa huyo, kubwa zaidi lilikuwa kitendo cha afisa mmoja wa usalama (haijulikani kwa hakika kama alikuwa polisi au taasisi nyingine ya dola) kumtolea bastola Nape hadharani. Tukio hilo la kutisha, na lile na Makonda kuvamia Clouds, yatabaki kuwa historia isiyopendeza kwa taifa letu kwani hayajawahi kutokea...labda zama za ukoloni.

Tukio la nne ni 'mafuriko' ya maneno yasiyopendeza kutoka kwa Rais Magufuli katika hotuba yake aliyoitoa jana wakati anawaapisha Mwakyemba na Profesa Kabudi, aliyerithi nafasi ya Mwakyembe. 

Sitaki kurudia vitisho alivyotoa Rais Magufuli lakini nachoweza kutahadharisha ni kuwa tunakoelekea sio kuzuri. Unapoona Rais anakerwa kwa vile habari zinazomhusu hazijapewa kipaumbele kwenye vyombo vya habari vingi, basi ujue tuna tatizo kubwa. Unapoona Rais anaamini kuwa habari za maandamano ya wafugaji na wakulima kuhusu migogoro ya ardhi ni "habari mbaya mbaya" basi ni wazi huyu si yule tuliyedhani ni tetezi wa wanyonge.

Tulipasw akuona dalili hizo mapema, kupitia baadhi ya kauli zake kama "I wish I could be Jaji Mkuu" na "I wish I could be IGP." Ukiona Rais anatamani madaraka zaidi ya aliyonayo, hiyo ni hali ya hatari.

Nihitimishe makala hii kwa kumshauri Rais Magufuli asikilize ushauri anaopewa na "wataalamu kuhusu hali ilivyo huko mtaani." Kadhalika, ninamsihi Rais wangu apunguze jazba. Hazitamfikisha popote. Aache kasumba ya kutafuta 'mabifu' yasiyo na msingi. Lakini jingine ni ukweli kwamba hatoweza 'kumbeba Makonda' milele, na kuendelea kumkumbatia kijana huyo kunaweza kumgharimu yeye Magufuli binafsi. 

SOMA MAKALA ILIYOPASWA KUTOKA KATIKA RAIA MWEMA TOLEO LA WIKI HII (JUMATANO 23/03/2017) LAKINI HAIKUTOKA (KWA SABABU WANAZOJUA WAMILIKI WA GAZETI HILO)


MAKALA YA RAIA MWEMA TOLEO LA MACHI 22, 2017

Disemba 31 mwaka juzi, siku ya mkesha wa ‘mwaka mpya 2016, nilichapisha kitabu cha kielektroniki kilichobeba jina “Dokta John Magufuli: Safari ya Urais, Mafanikio na Changamoto Katika Urais Wake.”

Pamoja na watu wengi waliokisoma kitabu hicho kukipongeza, wapo pia walionikosoa, hoja yao kuu ikiwa “ni mapema mno kutathmini Urais wa Magufuli katika muda huu mfupi aliokaa madarakani.”
Kwa wakati huo, sikuafikiana na ukosoaji huo, hasa kwa vile tathmini ya uongozi ni kama maadhimisho ya siku ya kuzaliwa: yanaweza kufanywa siku 40 baada ya kuzaliwa, kila mwezi, na kila mwaka kama wote tunavyofanya.

Kwahiyo, sikuona tatizo katika kufanya tathmini ya urais wa Dokta Magufuli, hasa ikizingatiwa kuwa aliingia na “kasi ya kutisha.” Kati ya siku aliyopishwa, Novemba 5, 2015 hadi nilipochapisha kitabu hicho – takriban miezi miwili hivi – Rais Magufuli alimudu kukonga nyoyo, sio za Watanzania tu, bali dunia nzima kwa ujumla kutokana na msimamo wake mkali dhidi ya uzembe, rushwa, ufisadi, sambamba na ari yake kubwa ya kubana matumizi.

Naamini sote tunakumbuka alama ya reli (hashtag) ‘iliyotikisa’ dunia nzima ya #WhatWouldMagufuliDo ambayo watumiaji mbalimbali wa mtandao wa kijamii wa Twitter katika kila kona ya dunia walijaribu kuonyesha jinsi gani Dokta Magufuli alivyo bora zaidi ya viongozi wengine duniani.

Lakini sababu nyingine ya kuandika kitabu hicho ilikuwa ushiriki wangu binafsi kwenye kampeni za kumnadi Dokta Magufuli kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Pamoja na sababu nyingine, niliamua kumnadi kutokana na sababu zangu binafsi dhidi ya mpinzani wake mkuu.

Na haikuwa kazi rahisi kumnadi mwanasiasa huyu, kwa sababu baadhi ya watu walishindwa kabisa kunielewa, huku wengine wakihoji “kwanini unaweza kutusaliti wapinzani na kumpigia debe mgombea wa chama tawala, ambacho wewe binafsi ni mhanga wa unyanyasaji unaofanywa na serikali yake dhidi ya wanaoikosoa?” Na kilichoambatana na kauli hizo ni matusi mazito, udhalilishaji usiomithilika, na mengineyo yasiyostahili kukumbukwa.

Takriban miaka miwili baadaye, nimeshikwa na bumbuwazi baada ya kumsikia Rais Magufuli “akimkingia kifua” Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, ambaye majuzi ameandika historia ya matukio ya kisiasa nchini Tanzania kwa kuvamia ofisi za kituo cha habari cha Clouds, akiambatana na askari wenye silaha nzito.

Niweke rekodi sahihi. Awali nilimtetea RC Makonda katika nilichoamini kuwa ni jitihada zake dhidi ya biashara haramu ya madawa ya kulevya. Niliamini kuwa suala la ‘utata wa elimu yake’ ni sehemu tu ya mikakati za kumwondoa kwenye ajenda hiyo muhimu.

Hata hivyo, baada ya mawasiliano na “wenye uelewa wa yanayojiri nyuma ya pazia la siasa za Tanzania,” nilithibitishiwa kuwa tuhuma dhidi ya kiongozi huyo zina ukweli, na nikaelezwa kuwa “hata Dokta Magufuli anafahamu hilo.” Na kimsingi, awali nilipanga makala hii iwe ya ushauri kwa Rais kuchukua hatua stahili dhidi ya mteuliwa wake huyo “ili kuwatendea haki wanaomshauri.”

Lakini kabla sijawasilisha makala hiyo, ambayo ililenga zaidi kwenye kusisitiza haja kwa viongozi wetu kuzingatia ushauri wa kitaalamu badala ya kuendekeza ajenda binafsi, kukajitokeza tukio la RC Makonda kuvamia huko Clouds.

Nitumie fursa hii kuupongeza uongozi wa kampuni ya Clouds, hususan Ruge Mutahaba na Joseph Kusaga, kuwa kufanya kile kilichotamaniwa na Watanzania wengi waliokuwa wakisubiri tamko la kampuni hiyo kuhusu tukio hilo la uvamizi wa Makonda, kwamba wasimamie ukweli.

Na kwa hakika, Ruge na Kusaga hawakuwaangusha watumishi wenzao wa Clouds na Watanzania kwa ujumla, wakaeleza “A hadi Z” ya kilichotokea wakati wa uvamizi huo ambao, kwa kumbukum bu zangu, ni wa kwanza kabisa kutokea nchini mwetu.

Ingeweza kuwa rahisi tu kwa viongozi hao wa Clouds “kuweka mbele maslahi yao binafsi” na kubadili maelezo, hasa ikizingatiwa kuwa lolote ambalo wangesema lingeweza kuaminika, lakini wakaamua kuhatarisha uhusiano wao na Makonda pamoja na shabiki mkubwa wa kituo hicho, yaani Rais Magufuli mwenyewe.

Akiongea kwenye uzinduzi wa mradi wa ujenzi wa barabara za juu, pamoja na mambo mengine Rais Magufuli aliwaomba Watanzania kujielekeza kwenye vitu vya maendeleo badala ya kujielekeza zaidi kwenye udaku. Ikumbukwe kuwa siku chache tu zilizopita, Rais alipiga simu kwenye kituo cha televisheni cha Clouds na kueleza kuwa yeye pia ni shabiki wa kipindi cha Shilawadu, ambacho ni cha “udaku” huo huo anaokemea Rais.

Suala hapa sio tu “kama ni sahihi kwa Rais kuwa shabiki wa kipindi cha udaku, basi isiwe dhambi kwa wananchi kupenda udaku” bali “kitendo cha Makonda kuvamia Clouds sio kujielekeza kwenye maendeleo.”

Dokta Magufuli alikumbusha pia kuwa “kampeni zimekwisha, ulie lakini Rais ni Magufuli, mimi kwangu hapa ni kazi tu, maendeleo.” Hivi kweli Rais anaamini kelele za kutaka Makonda achukuliwe hatua kutokana na uvamizi huko Clouds ni mwendelezo wa kampeni? Au ni “kelele za wasiojua kuwa Rais ni Magufuli”? Na sitaki kabisa kuamini kuwa Rais anaamini kitendo cha uvamizi wa Makonda huko Clouds ni sehemu ya “hapa ni kazi tu.”

Kilichonisikitisha zaidi ni kauli ya Dokta Magufuli kwamba “mnahangaika na viposti vyenu mara hili mara lile, mpaka wengine wanaingilia uhuru wangu kwamba nifanye hivi, ukiniingilia ndio unapoteza kabisa.”

Kwangu binafsi, nimeoiona kauli hiyo ya Rais kuwa kama dhihaka dhidi ya baadhi yetu tulioshiriki kikamilifu kumpigia kampeni mwaka 2015 kwa kutumia “viposti” hivyo hivyo anavyovidharau. Na sio sahihi kwa Rais kudai tunamwingililia uhuru wake. Yeye ni mtumishi wetu, na tuna haki ya kumweleza matakwa yetu. Huko sio kumwingilia uhuru wake bali kudai stahili yetu kutoka kwake.

Rais alitukumbusha pia kuwa yeye hapangiwi mambo, anajiamini, na ndio maana siku ya kuchukua fomu alikwenda peke yake. Kumtaka amwajibishe mteule wake aliyevamia kituo cha habari sio kumpangia mambo bali kumkumbusha wajibu wake kama kiongozi. Na kupangiwa mambo kama “mwajiriwa wa Watanzania” sio kosa, isipokuwa tu pale “kumpangia mambo” huko kunalenga kuidhuru nchi yetu.

Sawa, Dokta Magufuli alikwenda peke yake kuchukua fomu za kuwania urais, lakini hakufanya kampeni peke yake. Na kwenda kwake pepe yake kuchukua fomu hakumpi ruhusa ya kutuongoza peke yake, bali kwa ushirikiano kati yetu waongozwa na yeye kiongozi. Hivi, sio Dokta Magufuli huyuhuyu ambaye kila mara anatusihi tumwombee, lakini leo anatuona tunamwingilia?

Kadhalika, Rais alimuunga mkono RC Makonda kwa kumwambia kuwa yeye (Rais) ndio anayepanga nani akae wapi na afanye nini…kwahiyo RC Paul Makonda achape kazi. Hivi Rais amesahau kuwa sio yeye kama Magufuli bali taasisi ya Urais ndiyo inayompa nguvu kufanya maamuzi kwa maslahi ya Watanzania wote?

Na je Dokta Magufuli anataka kutuaminisha kuwa ameridhia kitendo cha Makonda kuvamia kituo cha habari akiwa na askari wenye silaha, kiasi cha kumtaka Mkuu huyo wa mkoa “aendelee tu kuchapa kazi”? Je hiyo haitompa jeuri Makonda, na hata wengineo, kufanya “abuse of power” kwa vile “Rais kuruhusu”?

Nimalizie makala hii kwa ushauri huu kwa Dokta Magufuli: kwanza, hakuna tija katika kusaka ugomvi usio na umuhimu (picking up cheap fights). Uamuzi wa kuzuwia kurushwa matangazo ya bunge mubashara, kuzuwia mikutano ya vyama vya siasa vya upinzani, kuwaambia wahanga wa tetemeko Kagera kuwa “serikali haikuleta tetemeko hilo” na “kila mtu abebe msalaba wake mwenyewe”, kuwaambia wananchi wanaolalamikia njaa kuwa “wewe Rais huwezi kuwapikia,” nk sio tu ni “kusaka ugomvi usio wa lazima” lakini haziendani na matarajio ya Watanzania kwako Rais wetu.

Vilevile ninaomba sana kumshauri Rais kuzingatia ushauri wa kitaalamu anaopatiwa na wasaidizi wake. Ni vigumu kufafanua katika hili, lakini ninaamini “nimeeleweka.” Taifa litakuwa katika hali mbaya itapofika mahala “washauri watakapotumia njia mbadala kukufikishia ujumbe.” Na ndicho kinachotokea kuhusu “viposti.”

Mwisho, siku zote Rais wetu umekuwa ukimtanguliza Mungu katika hotuba zako mbalimbali na kuwasihi Watanzania wakuombee. Wewe ni Mkristo, na hii ni Kwaresma. Ni kipindi cha maungamo, kusamehe waliotukosea, kuangalia tulikotoka, tulipo na tuendako. Penye Mungu pana upendo, na penye upendo pana haki. Japo hupangiwi cha kufanya, naomba kukushauri uwapatie haki Watanzania kwa kumwajibisha RC Makonda kwa kuvunja haki za Clouds kutokana na uvamizi aliofanya.
Mungu Ibariki Tanzania


Baruapepe: [email protected] Tovuti: www.chahali.com Twitter: @cha



21 Mar 2017



Baada ya tukio la Mkuu wa Mkoa Paul Makonda kuvamia ofisi za Kampuni ya Clouds jijini Dar, Ijumaa usiku, na kuahidiwa na uongozi wa Kampuni hiyo kuwa ungetoa taarifa rasmi jana, watu wengi - ikiwa ni pamoja nami- walihisi kuwa "sio rahisi kwa Clouds kumtosa Makonda, kwa vile ni mshkaji wao."

Sie hapa Uingereza tupo masaa matatu nyuma ya masaa ya Tanzania (japo Jumapili ijayo masaa yatabadilika), na jana nilipoamka, tayari uongozi wa Clouds chini ya Ruge Mutahaba na Joseph Kusaga ulikuwa umeshatoa taarifa kuhusu kilichojiri Ijumaa iliyopita kuhusu Makonda.

Awali, nilitaka kupuuzia kufuatilia habari hiyo nikihofia "kuharibu siku yangu kwa kuianza na habari mbaya" nikidhani kuwa Ruge na Kusaga "wamemsafisha Makonda."

Hata hivyo, baada ya kutupia macho tweets za Millard Ayo aliyerusha press conference ya uongozi wa Clouds mubashara, nilibaini kuwa Ruge, Kusaga na Clouds kwa ujumla wamefanya kile ambacho kimekuwa kigumu mno kufanywa na Watanzania wengi: kuwa wakweli. Kuwa tayari kupoteza rafiki kuliko kupoteza ukweli.

Kwa wengi hilo linaweza kuwa suala dogo lakini kwa hakika lina umuhimu wa kipekee. Sote twafahamu ukaribu wa Makonda na Clouds, na hata Ruge amekiri kuwa yeye binafsi ni rafiki na Mkuu huyo wa Mkoa.

Kwahiyo, kama ilivyotarajiwa na wengi, ingekuwa rahisi zaidi kwa Clouds "kumbemba Makonda" (kama alivyobebwa na Rais Magufuli) na pengine "stori ingeishia hapo" kuliko kuamua kusimamia kwenye haki na ukweli.

Jana niliwapa angalizo ndugu zangu wa Clouds kuhusu "kukubali kutumika." Nili-tweet hivi


Lakini japo ni rahisi kulaumu kuliko kujihangaisha kujua kwanini flani kafanya kitu tunachomlaumu kukifanya, mazingira ya media zetu yanalazilazimisha kutumika. Kwahiyo, wakati ni rahisi kuwalaumu Clouds "wanapotumika" kuinadi CCM na serikali yake, ni muhimu twenda mbali na kufahamu kwanini wanafanya hivyo.

Ni kwamba, kwa kiasi kikubwa, uhuru wa habari Tanzania bado ni fadhila kutoka kwa watawala. Kwa kiasi kikubwa, chanzo kikuu cha mapato ya vyombo vya habari ni matangazo kutoka serikalini. Kwahiyo, chombo cha habari "kitakachoiudhi serikali" kinaweza kujikuta kinanyimwa matangazo. Hiyo inalazimisha "urafiki" kati ya vyombo hivyo na serikali.

Lakini licha ya matangazo, vyombo vyetu vya habari vinafanya kazi katika mazingira kandamizi, na kwa ridhaa ya watawala badala ya kanuni stahili. Ndio maana, kama tulivyoshuhudia jana, Waziri Nape anapigania "sheria" huku Bosi wake Magufuli anakumbatia ridhaa yake kama mtawala.

Kingine kinachohusiana na tukio hilo ni ukweli kwamba Rais wetu Dokta John Magufuli anaelewa kasoro za wasifu wa elimu ya Makonda...kwa sababu alishajulishwa ukweli huo na "wahusika." Laiti angefanyia kazi ushauri aliopewa, tusingefika hapa. 

Kuna tatizo pia katika jinsi Rais wetu alivyojitahidi kutuonyesha kuwa ni rafiki wa Clouds, na ameshapiga simu mara kadhaa na kurushwa hewani, 

na kusifiwa na watu kibao kuwa "ni mtu wa watu" lakini swahiba wake, Paul Makonda, alipovunja sheria kwa kuvamia ofisi za Clouds, akapuuza "urafiki wake na Clouds" na "kumbeba swahiba wake Makonda." 
Kasoro nyingine ni kudai kuwa yeye Rais anapenda kipindi cha "udaku" cha Shilawadu cha Clouds lakini jana anatuchamba kuwa "Watanzania tunaendekeza udaku." Je ni Rais pekee anayestahili kupenda udaku, lakini ni jinai kwa raia wa kawaida?


Nimalizie makala hii kwa kumshauri Rais Magufuli aache kupenda ugomvi usio na maana, Waingereza wanaita "cheap fights." Alizuwia "matangazo ya bunge mubashara," na majuzi kajisifu kwa hatua hiyo; lilipotokea tetemeko Kagera, akakaa muda mrefu bila kwenda kuwapa pole wahanga, na alipokwenda akawasemea ovyo, eti "yeye hakuleta tetemeko hilo" na "hakuna serikali duniani inayosaidia wahanga wa tetemeko" (kitu ambacho sio kweli).


Kana kwamba hayo hayakutosha kutibua watu, alipokuwa ziarani mikoani, wananchi walisikika wakimwambia "njaa baba!" akawasemea ovyo "njaa mnataka mie niingie jikoni kuwapikia?" Na jana, amejigamba kuwa anajiamini, ndio maana alikwenda kuchukua fomu ya kuwania urais peke yake. Anajifanya kusahau kuwa hakujipigia kampeni peke yake, na kuna tuliotukanwa mtandaoni tukihangaika kumpigia kampeni.

Nilishaandika kwenye jarida la Raia Mwema kumsihi Rais Magufuli azingatie umuhimu wa kutumia lugha ya kidiplomasia badala ya kuendekeza ukali usio na maana, hasa katika mazingira kama ya jana ambapo hakupaswa kumlinda Makonda kwa uhuni aliofanya huko Clouds. Kusema "hapa ni kazi tu" kwa minajili ya kumlinda Makonda kinatufanya tuliosapoti kauli mbiu hiyo ya "hapa ni kazi tu" kujiskia kichefuchefu. Yaani "hapa ni kazi tu" kwa Mkuu wa Mkoa kuvamia kituo cha habari akiwa na askari wenye silaha?


Lakini kosa kubwa alilofanya Magufuli jana sio kumtetea Makonda bali kutupa jawabu la wazi kuwa jeuri ya Makonda inatoka kwa bsoi wake, yaani Magufuli. Kwanini Magufuli anamlinda Makonda kiasi hicho? Baadhi yetu twaelewa lakini huu sio muda mwafaka kuyaongelea hayo. Ila tu Rais wetu afahamu kuwa sapoti ya baadhi ya watu kwake ina ukomo, itafika mahala "akimwaga mboga, watamwaga ugali." I hope hatutofika huko. I hope Rais wetu atatumia busara, kufanyia kazi mapungufu yake eg kuwabwatukia watu ovyo huku anawalea watu kama Makonda, na kuepuka kusaka ugomvi usio na maana.

Historia ina mafundisho mengi kuhusu viongozi walioendekeza jeuri, kiburi, ubabe, dharau na kujiona majabali, na hatma yao haikuwa nzuri.

Waingereza wanasema WRONG IS JUST THAT, WRONG (Kitu kisicho sahihi kiko hivyo tu, hakiko sahihi). Alichofanya Makonda was wrong. Utetezi wa Rais Magufuli kwa Makonda was wrong too. Huo ni ukweli hata kama utamchukiza Mheshimiwa Rais.





12 Mar 2017

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinafanya Mkutano wake Mkuu Maalum huko Dodoma, ambapo pamoja na mambo mengine ni ajenda kuu ya "kujadili na kupitisha marekebisho ya Katiba ya CCM ya mwaka 1977 Toleo la 2012, pamoja na kanuni za chama hicho na jumuiya zake."

Nimeyawekea msisitizo maneno "kujadili na kupitisha" kwa sababu inaonekana kuwa wazi kuwa majadiliano yatakayofanyika hayapaswi kutoyapitisha marekebisho hayo. 

Ni rahisi kutafsiri hatua hiyo kama ya kunyima demokrasia (kwa maana kwamba kujadili pekee hakutoshi bali pia kuwepo uhuru wa kuyakubali au kuyakataa mapendekezo husika) lakini pengine ni rahisi pia kutambua kwanini CCM "imejihami" mapema.

Sijui ni watu wangapi wanaofahamu kwa hakika mabadiliko yanayotarajiwa kufanyika kwenye katiba hiyo ni yapi, lakini nitakurahisishia msomaji kwa kuyaorodhesha baadhi:
  • Kupunguza idadi ya wajumbe wa vikao vya ngazi za juu vya chama hicho
  • Kupunguza 'kofia mbili' kwa viongozi wenye vyeo ndani ya chama, serikalini au bungeni.
Kwa mujibu wa mabadiliko hayo, mwanachama anatakiwa kushika nafasi moja tuya uongozi, katika ngazi za Mwenyekiti wa Tawi, Kijiji, Mtaa, Kata, Wadi, Jimbo, Wilaya na Mkoa. Wengine ni Makatibu wa Halmashauri Kuu wa ngazi zote, Diwani na Mbunge/Mwakilishi.

Kwahiyo ni wazi kuwa mabadiliko hayo yatawaathiri 'vigogo' kadhaa wa chama hicho, na pengine ndio maana ikaamuliwa kuwe na "mjadala na kupitisha mabadiliko hayo" badala ya "mjadala na kupitisha au kutopitisha mabadiliko husika."

Kadhalika, mabadiliko hayo yatapelekea kupungua kwa idadi ya wajumbe wa Kamati Kuu ya chama hicho, kutoka 34 hadi 24.

Vilevile, idadi ya wajumbe wa Halmashauri Kuu ya chama hicho itapungua zaidi ya nusu, kutoka 388 hadi 158.

Miongoni mwa 'vigogo' watakaoathiriwa na mabadiliko hayo kutokana na kushika nyadhifa zaidi ya moja ni pamoja na William Lukuvi, Makame Mbarawa, Dkt Hussein Mwinyi, na Shamsi Vuai Nahodha.

'Kigogo' mwingine ni Mama Salma Kikwete, ambaye licha ya kuwa mjumbe wa NEC wa Mkoa wa Lindi, majuzi ameteuliwa na Rais Dkt John Magufuli kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri.

Wengine ni wenyeviti wa CCM mikoa ambao pia ni wabunge, kama vile Joseph Musukuma, Martha Mlata na Deo Simba, ilhali Godfrey Zambi ni mbunge na mkuu wa mkoa, Adam Kimbisa ni Mjumbe wa Kamati Kuu na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dodoma.

Kuna usemi mmoja, kwamba sio kila kitu sahihi ni kizuri, na sio kila kitu kizuri ni sahihi. Uamuzi wa CCM kuwapunguzia wanachama wake kofia zaidi ya moja kwenye uongozi ni sahihi lakini sio mzuri kwa watakaoathiriwa nao. Jicho la uchambuzi litaelekezwa kwa 'wahanga' hao kadri chama hicho kinavyoingia kwenye mchakato wake wa uchaguzi mkuu baadaye  mwaka huu, na kwenye kinyang'anyiro cha urais kupitia CCM katika uchaguzi mkuu ujao, mwaka 2020.

Kuna tetesi zisizothibitishwa kuwa miongoni mwa mabadiliko yatayofanyika katika Mkutano huo Mkuu Maalum ni pamoja na kumwezesha Rais aliyepo madarakani kuwa mgombea pekee kwenye mchakato wa chama hicho kumpata mgombea wake. Siwezi kujadili kitu ambacho sina uhakika nacho. Hata hivyo, tutalijadili suala hilo iwapo litajitokeza kwenye Mkutano huo.

Kufuatia vikao vya awali vilivyofanyika jana, chama hicho tawala kilitangaza adhabu kwa viongozi wake kadhaa, kubwa zaidi ikiwa kuvuliwa uanachama kwa Sophia Simba, kada mkongwe wa chama hicho na ambaye hadi jna alikuwa Mwenyekiti wa Taifa wa  jumuiya ya wanawake wa CCM (UWT), mjumbe wa Kamati Kuu na Mbunge.

Orodha kamili ya viongozi walioadhibiwa ni hiyo pichani chini

 




Hatua hizo kali zilizochukuliwa na CCM chini ya uenyekiti wa Rais Magufuli, sambamba na mabadiliko niliyoyaongelea awali, yana tafsiri kuu mbili. Kwanza, hatua kali za kinidhamu zinapeleka ujumbe kwa wana-CCM wa kada mbalimbali kuwa Rais Magufuli amepania kwa dhati kukisafisha chama hicho tawala. Ifahamike tu kuwa kilichojiri jana kinaingia moja kwa moja kwenye vitabu vya historia ya chama hicho na siasa za Tanzania kwa ujumla.

Pili, mabadiliko kusudiwa - na yakipita salama - sambamba na hatu kali zilizochukuliwa dhidi ya viongozi kadhaa wa chama hicho ni mtihani mkubwa, kwa Mwenyekiti Magufuli na CCM kwa ujumla.

Kwa Mwenyekiti Magufuli, hatua hizo zimemwongezea idadi ya maadui zaidi ya wale ambao tayari ni waathirika wa msimamo wake dhidi ya ufisadi na rushwa, ambapo watendaji kadhaa wa serikali wametumbuliwa huku wakwepakodi wakidhibitiwa, na majangili na 'wauza unga' wakibanwa. Japo ni mapema mno kufanya tathmini timilifu kwa hatua hizo, ile kuzichukua tu sio tu kwaonyesha dhamira lakini pia ni wazi zimetengeneza maadui wa kutosha dhidi ya Dkt Magufuli.

Katika hili, ni muhimu kutambua kuwa ni bora kuwa na kiongozi atakayechukiwa na kwa kutenda vitu sahihi kuliko atakayependwa kwa kufanya madudu.

Jana pia zilipatikana taarifa za kukamatwa kwa makada watatu wa Chama hicho, Msukuma, Hussein Bashe na Adam Malima. Sintoshangaa iwapo miongoni mwao akatimuliwa mtu uanachama. Kilichonisikitisha ni maelezo kuwa "walikamatwa na kuhojiwa na polisi kwa tuhuma za kupanga njama za kuvuruga Mkutano Mkuu Maalum wa CCM."

Katika mazingira ya kawaida, sio rahisi kwa makada hao watatu kupanga kuvuruga mkutano mkubwa kama huo ila yayumkinika kuhisi kuwa kilichofanyika ni kuzuwia kile nilichogusia awali, yaani "sio kujadili na kupitisha tu mabadiliko husika" bali pia "kujadili na kupitisha au kutopitisha mabadiliko hayo."

Hili la kuminya fursa ya upinzani kwa mabadiliko hayo linaweza kuwa na athari kwa chama hicho huko mbeleni. Sauti za manung'uniko ni kitu cha kawaida lakini sauti hizo zikiakisi mtazamo wa watu wengi, zinaweza kuathiri mshikamano wa chama hicho.

Hata hivyo, kwa wanaotegemea kuwa "CCM itakufa kutokana na mabadiliko haya" wanapaswa wazielewe vema siasa za Tanzania yetu. Si kwamba CCM itatawala milele, lakini kwa mazingira tuliyonayo, hakuna chama mbadala. Huo ni ukweli mchungu.

CCM wanaweza kukandamiza upinzani dhidi ya mabadiliko ya Katiba yao lakini angalau wamefanya mkutano mkuu, na wameadhibu waliokiuka taratibu za chama hicho. Je katika vyama vya upinzani kuna ujasiri wa aina hiyo? 

Ukiangalia wapinzani wakuu wa CCM, yaani Chadema, sio tu "wamegoma kabisa" kufanya tathmini ya kilichowaangusha katika uchaguzi mkuu uliopita bali pia wametelekeza turufu yao kubwa na iliyowajengea imani kubwa kwa Watanzania, yaani mapambano ya dhati dhidi ya ufisadi, yaliyoibua 'List of Shame,' skandali nzito kama Richmond, EPA, Kiwira,nk. 

Cha kusikitisha ni kwamba vyama vyetu vya upinzani sasa vimekuwa kama vinachezeshwa ngoma na CCM. Wafuasi wa vyama hivyo "wapo bize" kujadili matukio yanayoihusu CCM badala ya kuwekeza nguvu kwenye mustakabali wa vyama hivyo. Jiulize, hivi ajenda kuu ya Chadema, au CUF au ACT- Wazalendo ni ipi muda huu?

Ni katika mazingira hayo, baadhi ya viongozi wa CCM watavumilia mabadiliko yanayoendelea ndani ya chama chao kwa sababu hakuna mbadala wa chama hicho tawala kwa sasa. Tumebaki na miaka mitatu na miezi saba kabla ya uchaguzi mkuu ujao lakini wapinzani wetu wapo bize kuijadili CCM na serikali yake badala ya kujipanga vyema kwa uchaguzi ujao.

Unajua moja kati ya vitu vilivyoiangusha UKAWA katika uchaguzi mkuu uliopita ni "kusubiri makapi ya CCM" badala ya kutangaza mgombea wao mapema na kisha kumnadi kwa nguvu zote, kipindi ambacho CCM ilikuwa na shika-nikushike ya makada wake 40+ waliojitokeza kuwania kuteuliwa kuwa wagombea wa nafasi ya urais kupitia chama hicho tawala.

Nihitimishe makala hii kwa kupigia mstari uwezekano wa aina mbili: 

kwanza, CCM kuibuka imara zaidi baada ya Mkutano huo Mkuu Maalum pamoja na hatua za kinidhamu zilizochukuliwa dhidi ya makada kadhaa, kwa sababu nidhamu katika taasisi yoyote ile ni nguzo ya mafanikio, na pia, ili maendeleo yafikiwe shurti kuwepo na mabadiliko, na mabadiliko hukumbana na vikwazo ambavyo vyaweza kurukwa iwapo kuna nidhamu bora. 

Pili, mabadiliko hayo na hatua dhidi ya makada hao zinaweza kuzua mgogoro ndani ya chama hicho. Ni wazi kuwa waathirika wa kuvuliwa kofia zaidi ya moja za uongozi na hao waliochukuliwa hatua za kinidhamu hawatoridhishwa na hatua hizo. Hata hivyo, je wana pa kukimbilia? Na hapo ndipo utapobaini kuwa siasa za nchi yetu "zingechangamka sana" laiti tungekuwa na upinzani imara.

Na upinzani imara sio lazima upewe ruhusa na serikali kufanya mikutano/maandamano bali kama ule ulioibua 'List of Shame,' Richmond, EPA,nk...hawakuwa na ruhusa ya kufanya hivyo, na pia wanasiasa kama Dkt Willbrord Slaa na Zitto Kabwe walinusurika kwenda jela kwa ajili ya kuwapigani Watanzania. 

Kwa uchambuzi kamili kuhusu Mkutano Mkuu Maalum wa CCM na hatua za nidhamu zilizochukuliwa na chama hicho dhidi ya baadhi ya makada wake, ungana nami kwenye toleo la wiki hii la gazeti bora kabisa Tanzania la Raia Mwema hapo Jumatano panapo majaliwa.


3 Jan 2017



Kuna msemo wa kisiasa unaosema "in politics, perception is reality." Maana yake katika tafsiri isiyo rasmi ya Kiswahili ni kwamba 'katika siasa, kitu kinavyoonekana ni sawa na uhalisi wake. 

Kwa mantiki hiyo, kura ya maoni iliyobandikwa na gazeti la Raia Mwema katika akaunti yake kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter ikiwa na swali kama linavyoonekana katika 'tweet' husika hapa chini, inaweza kuwa na uzito.

Ndio, siyo kura ya kisayansi lakini idadi ya watu 448 'waliopiga kura' (hadi wakati ninaandaa makala hii) ni sampuli ya kutosha kwa kura ya maoni. 
Natambua makada wa CCM hawatopendezwa na makala hii, na huenda kuna watakaohoji kwanini niipe uzito kura ya maoni ya Twitter. Jibu langu ni hilo kwenye sentensi ya kwanza, "in politics, perception is reality." Lowassa kuongoza katika kura hiyo ya maoni kunajenga perception flani ambayo kwenye siasa ni reality. 

Neno la tahadhari kuhusu kura hiyo ya maoni ni kwamba bado inaendelea na haijafikia tamati. Kwahiyo, matokeo ya mwisho yanaweza kuwa tofauti, hasa ikzingatiwa kuwa tofauti ya asilimia ni kiduchu.

Pengine moja ya vitu vinavyompunguzia umaarufu Rais Magufuli ni baadhi ya kauli zake...kama hii hapa pichani chini. Ikumbukwe kuwa moja ya sifa ya uongozi bora ni pamoja na kutumia lugha isiyojenga picha ya dharau au kukosa huruma kwa wananchi. Na tukiamini kuwa 'in politics, perception is reality,' basi picha hasi inayoweza kutokana na baadhi ya kauli za Rais Magufuli zaweza kujenga taswira hasi kumhusu yeye na uongozi wake, hata kama hatamki kwa nia mbaya.




24 Jul 2016


Jana Julai 23, 2016 Rais Dokta John Magufuli alichaguliwa kwa asilimia 100 kuwa Mwenyekiti mpya wa Taifa wa chama tawala CCM, na mtangulizi wake, Rais Mstaafu, Jakaya Kikwete, kung'atuka rasmi. Ufuatao ni uchambuzi wa kina kuhusu mabadiliko hayo ya uongozi wa juu kabisa wa chama hicho kikongwe, hasa fursa na changamoto kwa Mwenyekiti mpya Magufuli. Karibuni
Check this out on Chirbit

11 Jun 2016

NI takriban miezi minane sasa tangu Tanzania ilipofanya uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani, Oktoba 25, 2015. Uchaguzi huo ndio uliotupatia Rais wa Awamu ya Tano, Dk. John Magufuli. Ni vema nikatanabaisha mapema kuwa, kwa kutumia haki yangu ya kidemokrasia, ‘nilimpigia debe’ mgombea huyo wa chama tawala, CCM. Na hadi muda huu, sijajilaumu kuchukua uamuzi huo.

Hata hivyo, kwa upande wangu – na pengine kwa watu wengine wengi tu – baada ya uchaguzi huo kumalizika na hatimaye kupata serikali ya awamu mpya, masuala ya kampeni nayo yalihitimishwa. Zile tofauti tulizokuwa nazo wakati huo, za “Magufuli anafaa, Lowassa (aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema) hafai” au “Lowassa anafaa, Magufuli hafai” zimebaki kuwa historia. Tumekwishapata rais, sio wa CCM pekee, sio wa waliompigia kampeni na kura pekee, bali ni rais wa Watanzania wote.


Lakini kuna baadhi ya wenzetu, wengi tu, bado wapo katika kile tunachoweza kukiita mkao wa kikampeni (campaign mode) au kwa tafsiri isiyo rasmi). Kuna makundi makuu mawili: wanasiasa na wafuasi wa kambi kuu mbili katika uchaguzi huo, yaani CCM na Ukawa. Katika kundi la kwanza, kuna wanasiasa ambao kwa kiasi kikubwa wanaonekana kutamani kampeni za uchaguzi ziendelee. Hawa wanajitambulisha kwa lugha na matendo yao ambayo yameelemea kwenye kuzidisha uhasama wa kisiasa kuliko mwafaka wa kitaifa.


Na kama kuna sehemu nzuri ya kubaini hilo ni huko bungeni ambapo masuala mbalimbali ya maslahi ya taifa yanaonekana ya kipuuzi kwa sababu tu ya uhasama huo wa kisiasa. Wabunge wa CCM wenye nia ya kufanya kazi na wenzao wa Ukawa kwa ajili ya taifa letu wanakwazwa na hofu ya kuonekana wasaliti kwa chama chao. Na huenda hali ni hiyo kwa wale wa upinzani.


Kundi la pili ni la wafuasi wa kambi hizo, yaani CCM na Ukawa. Wakati upinzani baina yao unaokera, na kwa hakika unakwaza mijadala muhimu kuliko mustakabali wa taifa letu, kinachoudhi zaidi ni kasumba inayojitokeza ndani ya makundi hayo, ambapo wana-CCM wanaodhani kuna haja ya kukikosoa chama chao au Magufuli wanaonekana ni ‘mbwa mwitu kwenye ngozi ya kondoo,’ wasaliti. Hali ni hivyo hivyo kwa wana-Ukawa. Ukimkosoa Lowassa basi wewe ni kibaraka wa CCM.


Majuzi, nilikumbana na mkasa baada ya kukosoa uamuzi wa serikali kuwafukuza wanafunzi wa stashahada maalumu ya ualimu katika Chuo Kikuu cha Dodoma. Mtu mmoja ‘alinivaa’ na kunilaumu kuwa ninashindwa kutumia uandishi wangu kumtetea Rais Magufuli. Ni baada ya kumwonyesha makala mbalimbali nilizoandika huko nyuma ‘kumnadi’ Magufuli na ‘kumtetea’ baada ya kuwa rais, sambamba na kitabu nilichoandika kuhusu urais wake, ndipo akadiriki kunitaka radhi. Huyu ni mmoja kati ya wengi wasiotaka kusikia lolote zaidi ya pongezi kwa vyama au viongozi wao.


Nimeanza makala hii kwa kuelezea suala hilo kwa sababu sio tu linakwaza mijadala muhimu kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu taifa letu lakini pia linaweza kuathiri dhamira nzuri ya Rais Magufuli kulitumikia taifa letu. Yeye mwenyewe alituomba tumsaidie katika uongozi wake na moja ya njia za kumsaidia mtu ni kumkosoa pale anapokosea.


Na bila kuuma maneno, na licha ya mimi binafsi kuwa ‘shabiki wa Magufuli,’ jinsi alivyoshughulikia suala la wanafunzi waliofukuzwa UDOM sio sawia. 

Kwanza, kilicholalamikiwa na wengi kuhusu hatua ya serikali kuwafukuza wanafunzi hao sio kwamba walistahili kuendelea na kozi hiyo au la bali namna walivyofukuzwa bila chembe ya ubinadamu. Na angalau basi wangekuwa wamefanya kosa fulani. Hawakuwa na kosa lolote kwa sababu hawakujidahili wenyewe wala kujiundia kozi hiyo au kujiunga wenyewe bila kuitwa chuoni.

Baadhi ya wanafunzi hao waliojitoa mhanga, wakaacha kwenda kidato cha tano huku alama walizopata zikiwaruhusu kuchaguliwa na kujiunga na kozi hiyo. Hawa sio ‘vilaza’ hata kidogo.
Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa na Mbunge kutoka Chama cha ACT, Zitto Kabwe, ni wanafunzi 88 tu ambao sifa zao zina mushkeli kuendelea na kozi hiyo. Hivi kulikuwa na ugumu gani wa kuchuja waliostahili kuendelea na kawaondoa hao wenye upungufu wa sifa stahili? Kilichokosekana ni busara tu.


Kwa heshima na taadhima, ninaomba pia kutoafikiana na kauli ya Rais Magufuli kuhusu vilaza. Hivi kweli tumesahau jinsi mpango kama huo wa stashahada maalumu ya ualimu, enzi hizo ukiitwa UPE (Universal Primary Education), ambao licha ya matatizo kama hayo ya stashahada ya Chuo Kikuu cha Dodoma, ulivyoweza kuiweka Tanzania yetu katika ramani ya kimataifa kwa mafanikio makubwa ya kielimu?


Sawa, kulikuwa na kasoro katika mpango huo wa stashahada maalumu ya ualimu, lakini mtoto hazaliwi akitambaa, kwa maana ya kwamba kila mwanzo ni mgumu. Kwa hiyo, kwa kutumia uzoefu wa UPE – kwa mfano vitu gani vilisababisha ‘kifo’ chake – tungeweza kabisa kuboresha stashahada hiyo maalumu ili itusaidie kukabili uhaba mkubwa wa walimu wa masomo ya sayansi, ambapo kwa mujibu wa takwimu za Zitto, ni walimu zaidi ya 20,000.


Kauli za Rais Magufuli zinakinzana na waziri wake Profesa Joyce Ndalichako. Lakini hilo sio muhimu kwa sasa. Wenye uelewa tunafahamu kwamba kuna makosa yamefanyika. Na badala ya kuendelea kunyoosheana vidole, ni vema serikali ikafanya utaratibu wa haraka wa kurekebisha kasoro hiyo. Sitarajii wanafunzi hao kuombwa msamaha wala kusikia hotuba ya kiongozi kukiri kwamba ushughulikiaji wa suala hilo haukuwa sahihi. La muhimu sio kuombana msamaha bali kurekebisha kosa husika.


Nimalizie makala hii kwa kuwasihi Watanzania wenzangu kwamba tuna mengi ya kunufaika kwa kuwa wamoja kuliko kuruhusu tofauti za kiitikadi au upinzani wa kisiasa au kimtazamo kututenganisha. Ifike mahala tuweke kando siasa kwenye masuala yanayohitaji busara au utaalamu.


Pamoja na kasoro kadhaa zilizojitokeza katika Awamu ya Nne, wazo hili la stashahada maalumu ya ualimu lilipaswa kuwa moja ya alama muhimu kiuongozi (legacies) za Rais mstaafu Jakaya Kikwete. Nia yake ilikuwa nzuri, na kwa vile miongoni mwa walioridhia sera hiyo ni pamoja na Rais Magufuli (wakati huo akiwa mbunge na waziri), basi hakuna haja ya ‘kuwatesa’ vijana hao wazalendo ambao kufanikiwa kwao katika kozi hiyo kungesaidia kupunguza uhaba wa walimu ya masomo ya sayansi. 

Nihitimishe kwa msemo kwamba, kukosea ni ubinadamu lakini kujirekebisha ni utukufu (To err is human but to correct is greatness)



15 Mar 2016

Rais Dkt John Magufuli amekutaa kukutana na ujumbe wa maseneta sita wa Marekani, tukuio lililojiri tarehe 18 ya mwezi uliopita. Ombi la maseneta hao kukutana na Rais liliwasilishwa na Waziri wa zamani wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, ambaye alikuwa mwenyeji wa maseneta hao walioongozwa na Seneta James Inhofe wa chama cha Republican kutoka jimbo a Oklahoma. Hata hivyo, Rais Magufuli alikataa ombi la kukutana na maseneta hao akidumisha taswira yake ya kujiweka mbali na wafanyabiashara na lobbyists.

Mwaka juzi, Seneta huyo mhafidhina alishutumiwa vikali na kundi moja la utetezi wa haki za wanyama baada ya kuhudhuria hafla moja ambapo njiwa walirushwa hewani na kutunguliwa kwa risasi.



Mtandao wa kiuchunguzi wa African Intelligence unaripoti kwamba waziri huyo ya zamani katika serikali ya Rais Mstaafu Jakaya Kikwete anajulikana kwa kuwa karibu na Wamarekani matajiri wanaohusiana na Mfuko wa Kuhifadhi Mazingira wa Friedkin. Mfuko huo unamiliki makampuni ya Tanzania Game Trackers Safaris, Wengert Windrose Safaris na Mwiba Holdings Limited. Kampuni hiyo ya mwisho imekuwa ikihusishwa mara kadhaa na kesi za ujangili


29 Jan 2016

KATIKA tasnia ya ushushushu kuna kitu kinachoitwa Moscow Rules (yaani Kanuni za Moscow). Hizi ni kanuni za zama za Vita Baridi ambazo majasusi waliopangiwa kazi nchini Urusi walipaswa kuzizingatia, kwa sababu nchi hiyo ilikuwa nguli wa kukabiliana na majasusi. Moja ya kanuni hizo inasema; “Once is an accident. Twice is a coincidence. Three times is an enemy action.” Kwa tafsiri isiyo rasmi; kitu kinachojiri mara moja ni ajali; kikijiri mara ya pili ulinganifu wa bahati mbaya, sio makusudi; kikijiri mara ya tatu ni kitendo cha adui.”

Nimeanza makala hii na angalizo hilo kwani ndio wazo lililoniingia kichwani mara baada ya kusoma kauli za aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, katika Serikali ya Awamu ya Nne, Bernard Membe.

Wiki iliyopita, Membe alinukuliwa na vyombo vya habari akimkosoa Rais Dk. John Magufuli, angalau katika maeneo matatu. Kwanza, Membe alidai kuwa kiuhalisi, Dk. Magufuli hajapunguza idadi ya wizara kama alivyoahidi bali amepunguza idadi ya mifuko, na kutanabaisha kuwa Rais hajabana matumizi yoyote kwa kupunguza ukubwa wa baraza la mawaziri, bali alichofanya ni kupunguza idadi ya mawaziri na sio wizara.

Alichofanya ni sawa na kuwa na mayai kumi halafu ukaamua kuyaweka kwenye mifuko kumi, maana yake ni kwamba utakuwa na mifuko kumi yenye mayai,” alisema waziri huyo wa zamani ambaye pia alikuwa miongoni mwa makada wa CCM waliowania kuteuliwa kugombea urais kwa tiketi ya chama hicho tawala.

Lakini unaweza kuwa na idadi hiyo hiyo ya mayai na ukaamua kuyagawanya; mayai matatu unayaweka kwenye mfuko mmoja, mawili kwenye mfuko mwingine na yaliyobaki kwenye mfuko mmoja. Maana yake ni kwamba utaendelea kuwa na mayai kumi lakini idadi ya mifuko imepungua. Hapa sasa utakuwa hujapunguza gharama za kuyatunza hayo mayai,”aliongeza Membe.

Membe alidai kwamba Magufuli ameendeleza wizara zile zile lakini kaamua kuzikusanya pamoja, na kuona kuwa mfumo huo mpya wa wizara unaweza kuathiri uwasilishaji wa bajeti bungeni kwa vile mawaziri sasa watahitaji muda mwingi zaidi kuliko ilivyokuwa awali.

Hilo tutaliona kwenye Bajeti ya Serikali ya mwaka huu. Tuone kama bajeti itaongezeka au itapungua? Kwa sababu kama wizara zimepungua kama tunavyoamini, lazima bajeti ipungue, sasa bajeti ikiongezeka au ikibaki vile vile maana yake hakuna kilichofanyika,”alitahadharisha.

Eneo la pili ambalo Membe alimkosoa Magufuli ni udhibiti wa safari za nje, akidai kuwa Tanzania si kisiwa. Membe, aliyekuwa mtetezi mkuu wa safari mfululizo za Rais (mstaafu) Jakaya Kikwete nje ya nchi, alisema kuwa safari za nje zina manufaa kwa taifa, na kusisitiza kuwa lazima Rais Magufuli asafiri kwenda nje ya nchi.

Tanzania si kisiwa, hata ukiwa tajiri namna gani lazima utoke nje ya nchi yako,” alisema Membe, na kutahadharisha kuwa nchi yetu inaweza kuwa kama Zimbabwe kwani ukijitenga, utatengwa.
Alisema nchi ina mabalozi 36 tu duniani kote kati ya nchi 194 zinazohitaji uwakilishi huo na kibaya zaidi, mabalozi hawaruhusiwi kuingia kwenye baadhi ya vikao, na hata wakiingia wakifika kwenye hatua ya uamuzi watazuiwa kushiriki.

Eneo la tatu ambalo japo hakumtaja Magufuli wala kukosoa moja kwa moja lakini linaloweza kutafsiriwa kama kuikosoa serikali kuhusu wafanyabiashara, ambapo alitahadharisha serikali kutowachezea.

Waziri huyo ambaye pia ni mbunge wa zamani wa Mtama (CCM) alipongeza kasi ya Magufuli katika vita dhidi ya ufisadi na kudhibiti mianya ya kukwepa kodi lakini akatahadharisha kuhusu haja ya kuwa mwangalifu katika kuwashughulikia wafanyabiashara. Alidai kuwa wafanyabiashara wana masikitiko makubwa dhidi ya serikali, na anaona suala hilo litaibuka kwa kishindo bungeni.

Licha ya maeneo hayo matatu, Membe alizungumzia kauli ya aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa, aliyedai wafanyabiashara waliomuunga mkono wananyanyaswa. Alieleza kuwa si dhambi kwa wafanyabiashara kufadhili vyama vya siasa wakati wa uchaguzi, na kwamba serikali ya chama kilichoshinda uchaguzi inapaswa kuwakusanya wafanyabiashara wote na kufanya nao kazi na sio kuwaburuza.

Kadhalika, mwanasiasa huyo alizungumzia kuhusu “timua timua” ya watumishi wa umma wanaohusishwa na tuhuma za ufisadi.

Ni rahisi kumshughulikia mtu usiyemfahamu lakini siyo rahisi kumshughulikia mtu unayemfahamu,” alidai Membe, na kuongeza kuwa haitokuwa shida kwa Magufuli kuwashughulikia watendaji aliowakuta serikalini ambao kimsingi hakuwateua, na hawafahamu. Alihoji iwapo Rais ataweza kuwatimua aliowateua mwenyewe.

Kauli hizo za Membe zimezua mjadala mkubwa, hususan kwenye mitandao ya kijamii. Japo kabla yake, aliyekuwa Naibu wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Makongoro Mahanga, alimkosoa Magufuli kuhusu ukubwa wa kabineti yake, ukweli kwamba Membe bado ni kiongozi wa juu wa CCM ilhali Mahanga alihamia upinzani, unaashiria mengi.

Lakini binafsi sikushangazwa na kauli hizo za Membe, hasa kwa vile awali, katika kitabu nilichokichapisha hivi karibuni kuhusu safari ya urais wa Magufuli, mafanikio na changamoto katika urais wake, nilibainisha kuwa moja ya changamoto zinazoweza kumkabili Rais huyo wa Awamu ya Tano ni maadui wa ndani ya chama chake.

Kimsingi, hoja zote za Membe hazina mashiko. Kuhusu anachoita ukubwa wa baraza la mawaziri, la muhimu kwa Watanzania si ukubwa au udogo bali uchapakazi. Ni bora kuwa na mawaziri, manaibu na makatibu wakuu hata 1,000 wachapakazi, kuliko kuwa na serikali ndogo inayokumbatia mafisadi.
Pia Membe alipaswa kufahamu kuwa utendaji kazi wa viongozi wa serikali unategemea sana utendaji kazi na msimamo wa bosi wao, yaani Rais aliyewateua. Ni dhahiri kuwa Membe anatambua kuwa Magufuli si mtu wa porojo, mtoa ahadi anazoshindwa kuzitekeleza mwenyewe (rejea kauli ya “ninawajua wala rushwa kwa majina” ya Kikwete), na kimsingi Watanzania na dunia nzima wanafahamu kuwa kaulimbiu ya Hapa Kazi Tu ya Magufuli ni tofauti na zama za nchi kujiendesha yenyewe (on autopilot).

Kuhusu safari za nje, Membe amepotoka mno, pengine kwa sababu kwa wadhifa wake wakati huo, alikuwa mmoja wa wasafiri nje ya nchi mara kwa mara. Kwanza, Rais Magufuli hajawahi kutamka kuwa hatosafiri. Kwa hiyo, kauli ya Membe kuwa lazima atasafiri ni fyongo.

Pili, zuio la safari za nje sio ‘blanket ban’ bali ni kwa safari zisizo na tija. Lakini kwa nini tushangazwe na kauli hiyo ya Membe ilhali tunafahamu misafara ya serikali iliyopita ilivyosheheni wajumbe kwa kutumia fedha za umma? Ni mtu mwenye matatizo tu anayeweza kutetea safari zenye manufaa zinazoligharimu taifa matrilioni ya shilingi huku faida tarajiwa zikiwa pungufu ya gharama husika.

Mwanadiplomasia msomi kama Membe alipaswa kuangalia hapo jirani tu kwa Rais Paul Kagame, kulinganisha idadi ya safari zake nje na zile za Kikwete kisha kuangalia hali ya uchumi kati ya nchi hizo mbili.

Vilevile ni rahisi kwa Membe kuzungumzia mafanikio ya safari hizo kwa vile ni Watanzania wachache wanaofahamu vituko vilivyoambatana na safari hizo. Ni mara ngapi safari hizo za ‘manufaa’ zilijumuisha shopping, kuhudhuria birthday parties, na matukio mengine yasiyo na tija kwa serikali?

Kuhusu wafanyabiashara, ni upuuzi wa hali ya juu kuhisi tu kuwa kuna uonevu dhidi ya mfanyabiashara yeyote. Kama kuwabana wafanyabiashara wakwepa kodi ni uonevu basi Magufuli aongeze dozi, maana hizi sio zama za Tanzania kuwa shamba la bibi.

Membe anadai wafanyabiashara wana masikitiko na suala hilo linaweza kuibuka bungeni. Anamaanisha Bunge limejaa wafanyabiashara au? Na kama masikitiko yao ni kutokana na Serikali ya Awamu ya Tano kuwabana ili wasikwepe kodi na kwamba masikitiko hayo yanaweza kusababisha kupoteza wawekezaji, basi na waondoke hata kesho. Hatuhitaji wakwepa kodi nchini. Kimsingi, wanaolalamika wala hawastahili kuitwa wafanyabiashara bali wahujumu wa uchumi wetu.

Na hoja yake kuhusu ‘timua timua’ haishangazi kwani moja ya udhaifu wa serikali ambayo Membe alikuwa waziri ilikuwa ni kuwaonea aibu wanaoboronga, na matokeo yake hali hiyo ilivutia waborongaji wapya kwani walishabaini kuwa hakuna wa kuwachukulia hatua. Hivi Membe anaweza kutuambia lolote kuhusu ahadi ya Riais Kikwete aliyoitoa Februari 2006 kwamba anawafahamu wala rushwa kwa majina na anawapa muda wajirekebishe? Sawa, Magufuli alipoingia Ikulu alikuta orodha hiyo ya wala rushwa aliowajua Kikwete na kuamua kuifanyia kazi?

Nimeeleza awali kuwa nimelizungumzia suala hilo kwa kirefu kitabuni. Sitaki kabisa kuamini kuwa kauli za Membe ni zake peke yake. Hisia zinanituma kuamini kuwa huu ni moshi tu unaoashiria moto unaowaka ndani kwa ndani ya CCM kati ya makundi makuu mawili: la Hapa Kazi Tu la Magufuli linalotaka kuiondoa Tanzania katika lindi la ufisadi unaoifanya nchi yetu kuzidi kuwa masikini, na kundi la wanufaika wa ufisadi linalomwona Magufuli kama mtu anayewaziba pumzi. Naam, ufisadi ni ‘lifeline’ ya watu walioigeuza nchi yetu Shamba la Bibi, wakivuna wasichopanda.

Nimalizie makala hii kwa kutoa wito kwa makada wa CCM, ambao wengi wao wanaimba Hapa Kazi Tu, lakini wakisikia madhambi yaliyofanywa na mwana-CCM fulani wanakimbilia kuwanyooshea vidole wapinzani. Wapinzani wakuu wa Magufuli hawapo Chadema au nje ya nchi bali wapo ndani ya chama hicho tawala. Na njia pekee ya kupambana nao ni kuweka mbele maslahi ya taifa badala ya kutanguliza umoja na mshikamano wa chama. Kuna usemi mchawi akimaliza kuroga mtaa hugeukia familia yake. Majipu yaliyomo ndani ya CCM yasipotumbuliwa mapema yatamkwaza Magufuli na nchi yetu kwa ujumla.


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.