5 Dec 2014

Waingereza wana msemo ambao unatafsirika kwa Kiswahili kama "chuki ya pamoja ni mwanzo wa urafiki mkubwa." Kimahesabu kama A hapatani na B, na A anamchukia C kama ambavyo B anamchukia pia C, basi chuki ya A na B kwa C yaweza kuwa mwanzo wa wawili hao A na B kuwa marafiki wenye lengo la kumwangamiza C.

Binafsi, naomba kukiri kuwa kwa muda sasa nimekuwa siafikiani na mitizamo na mwenendo wa mwanasiasa mahiri wa upinzani, Zitto Kabwe. Siwezi kusema nina chuki dhidi yake bali mie sio miongoni mwa supporters wake.Pamoja na sababu nyingine, kubwa ni kile ninachokitafsiri kama mwanasiasa huyo kutanguliza mbele maslahi yake binafsi badala ya chama chake yaani Chadema. Kwa mtizamo wangu, mgogoro uliopelekea hatua ya Chadema kumvua madaraka Zitto ni matokeo ya 'imani potofu' kuwa kuna mwanasiasa anayeweza kuwa maarufu kuliko chama chake, Si kwamba haiwezekani kabisa kwa hilo kutokea lakini si kwa hatua waliyofikia Chadema hivi sasa.

Lakini lengo la makala hii si kumjadili Zitto wala ugomvi kati yake na Chadema. Ila nimegusia suala hilo kwa sababu nililazimika 'kurejesha urafiki' na mwanasiasa huyo, angalau kinadharia, wakati akifanya jitihada kubwa binafsi na kama mwenyekiti wa PAC kushughulikia ufisadi wa Tegeta Escrow. Kwa kutumia mfano huo hapo juu wa chuki za A kwa C na za B kwa C, na A ni Zitto, na B ni mie, huko C wakiwa mafisadi wa Escrow, basi 'urafiki' usingeepukika.

Hakuna Mtanzania atakayeshindwa kumpongeza Zitto na Kafulila pamoja na PAC kwa ujumla walivyofanya kazi kubwa na nzuri katika kushughulikia skandali hiyo. Nina imani hata wahusika wa ufisadi huo wa Escrow wanamkubali kwa jinsi alivyowakalia kooni...ALMOST.

Hata hivyo, mara baada ya kumalizika kwa 'timbwili' hilo la Escrow bungeni, nilitumiwa meseji na 'mjuzi mmoja wa mambo ya huko nyumbani' ambaye alidai kuwa pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na PAC, kuna 'mchezo mchafu' uliofanyika katika kufikia mwafaka miongoni mwa wajumbe, hususan wale wa kutoka CCM. Alidai kuwa kilichowezesha mwafaka huo kufikiwa ni pamoja na 'kumnusuru' Rais Jakaya Kikwete, ambaye kama Mbunge Tundu Lissu alivyobainisha bungeni, anatajwa kuhusika katika skandali hiyo. Kimsingi, hoja ya Lissu, ambaye pia aliilaumu Idara ya Usalama wa Taifa kwa kutowajibika ipasavyo katika mlolongo wa skandali mbalimbali zinazougubika utawala wa Rais Kikwet, iliuawa kimyakimya licha ya umuhimu wake mkubwa.

Hata hivyo, kwa uelewa wangu, jaribio lolote la kumhusisha Rais Kikwete na skandali hiyo hata kama ushahidi upo lingepelekea mparaganyiko mkubwa katika kamati hiyo ya Zitto. Na kama tulivyoshuhudia 'makada' wa CCM huko bungeni walivyopigana kufa na kupona hadi Waziri Mkuu Mizengo Pinda akanusuriwa, kwa hakika ishu ya Kikwete kuhusishwa na Escrow ingepelekea bunge hilo kuvunjika pasi kufikia hitimisho.

Lakini what if mkakati huo wa 'kumnusuru Rais Kikwete' unabeba mengi zaidi ya tunavyodhani? 


Kwa kifupi, tume-settle for less. Na Waingereza wana msemo unaotahadharisha kuhusu ku-settle for less, ambapo wanasema 'pindi ukikubali kupokea pungufu ya unachostahilki basi hatimaye utaishia kupokea pungufu zaidi ya kile ulichostahili awali.' Japo ni mapema kuhitimisha kwamba 'tumeingizwa mkenge,' lakini ukimya wa Rais Kikwete katika kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu Escrow umeanza kuzua wasiwasi.

Na 'kigugugmizi' kinachomkabili Rais Kikwete kina sababu kadhaa za wazi. Kwa mfano, kumtimua Mwanasheria Mkuu Jaji Werema kunaweza kupelekea kuzuka kwa skandali nyingine iwapo Jaji huyo ataamua 'mmemwaga mboga, na mie namwaga ugali' kwa maana anajua mengi yaliyojiri na yanayojiri katika utawala wa Rais Kikwete. Japo si kwamba haiwezekani kumtimua na kisha kumfunga mdomo, lakini historia ya wanasheria wakuu huko nyuma inapaswa kutukumbusha jinsi 'wanavyobebwa' kwa minajili ya 'kutotengeneza uadui na mtu anayejua siri nyingi.'

Kwa upande wmingine, ni muhimu kukumbuka kuwa kimsingi Rais Kikwete ndo aliyemleta Profesa Muhongo katika frontline politics. Hawa ni marafiki wa karibu. Na hadi sasa Muhongo ameendeleza jeuri yake ya kisomi na kusisitiza kuwa fedha za Escrow si za umma. Msimamo huo pia washikiliwa na Waziri Mkuu Pinda. Je kuna anayefahamu msimamo wa Rais Kikwete? Maelezo yanaonyesha kuwa yeye aliridhia malipo ya Escrow kufanyika. Je amebadili mawazo na kutambua kuwa hilo lilikuwa kosa?

Lakini wakati tayari tunafahamu majina mengi ya walionufaika na mgao wa Escrow kupitia Benki ya Mkombozi, inadaiwa kuwa mgao mkubwa zaidi uliopitia Benki ya Stanbic ulihusisha vigogo kadhaa lakini hadi muda huu hakuna jina hata moja lililowekwa hadharani. So far, gazeti la Raia Mwema limeripoti kuwa mke wa kigogo momja mwandamizi huko Ikulu alikatiwa shilingi bilioni 5. Sasa huhitaji kujua hesabati vizuri kubashiri kwamba kama mke wa kigogo alikatiwa mbilioni tano, mumewe alipewa kiasi gani? 

Hayo yote tisa, kumi ni kauli niliyokumbana nayo muda mfupi uliopita, na ambayo kwa hakika ndio iliyonisukuma kuandika makala hii. Kauli hiyo ni ya Jaji Mkuu Chande ambayo kimsingi inaharibu mwenendo wa kesi yoyote itakayofunguliwa dhidi ya wahusika wa ufisadi wa Escrow. Nimeinukuu kwa picha hapa chini.


Je Jaji Mkuu alikuwa anatoa tu tahadhari au alikuwa akifikisha ujumbe mahsusi kwamba hata tukiwapeleka mahakamani wahusika wa Escrow, utetezi wao upo bayana...kwamba walishahukumiwa bungeni. Na kama Jaji Mkuu 'hakutumwa' basi kwa hakika amewapatiwa washtakiwa-watarajiwa ushauri mzuri wa bure kisheria kuhusu jinsi ya kupambana na kesi yoyote watakayofunguliwa kuhusisna na suala hilo: wajitetee kuwa walishahukumiwa na bunge, na mawakili waoa waweza kutumia kauli hiyo ya Jaji Mkuu kama supporting evidence.

Anyway, pengine ni mapema mno kuhukumu lakini kama ambavyo Mzee Warioba alivyoonyesha mapungufu ya taarifa ya PAC na maazimio ya bunge kuhusu skandali ya Escrow, sintomshangaa mtu yeyote atakayeanza kupatwa na wasiwasi kuwa tumeingizwa mkenge...TENA.


Sijui msomaji mepndwa unaonaje. 





1 Dec 2014

Kwanza niombe samahani kwa ku-update blogu hii kitambo. Nilitingwa na majukumu. Pili, makala hii chini ilichapishwa katika gazeti la RAIA MWEMA toleo la Jumatano Novemba 26, 2014, lakini kwa sbabau nisizofahamu tovuti ya gazeti hilo haikuwa up-dated hadi asubuhi hii. Licha ya kuwa na nakala halisi ya makala hii, nilionelea ni vema kusubiri 'edited version' ya makala hii pindi ikichapishwa kwenye tovuti ya RAIA MWEMA. Endelea kuisoma
KWANZA, nianze makala hii kwa kuomba samahani kwa ‘kutoonekana’ kwa takriban mwezi mzima sasa. Hali hiyo ilitokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu. Ninapenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa wasomaji mbalimbali walionitumia barua-pepe kuulizia kuhusu ‘ukimya’ huo.
Wiki iliyopita, Rais wa Marekani, Barack Obama, aliandika historia kwa kuweka hadharani mpango kabambe kuhusu hatma ya takribani wakazi milioni 12 wanaoishi isivyo halali nchini humo.
Ujasiri wa Obama katika suala hilo unatokana na ukweli kwamba licha ya jitihada za muda mrefu, uhasama wa kisiasa kati ya vyama vikuu vya siasa nchini humo, Democrats na Republicans, ulikuwa kikwazo kikubwa katika kufikia mwafaka na ufumbuzi.
Wakati vyama vyote viwili vinaafikiana kuhusu uwepo wa wakazi hao wasio halali milioni 12, wahafidhina wa Republicans wamekuwa wapinzani wakubwa kuhusu ‘ufumbuzi rahisi’ wa kutoa msamaha (amnesty) kwa wahamiaji hao na kisha kuimarisha udhibiti katika mianya inayotumiwa na ‘wahamiaji haramu.’
Lakini suala hilo limekuwa mzigo mkubwa kwa Obama ambaye hata kabla hajaingia madarakani aliahidi kutafuta ufumbuzi hasa ikizingatiwa kwamba licha ya utajiri wa Marekani, hakuna uwezekano wa kuwatumia wahamiaji hao wote.
Kadhalika, mara kadhaa Obama alikuwa akieleza kwamba kulipuuza tatizo hilo hakutolifanya lipotee lenyewe, bali litazidi kuwa kubwa na gumu kulitatua.
Hatimaye Obama aliwatahadharisha Republicans kuwa atalazimika kutumia ‘Nguvu ya Kirais’ (Executive Order) ambayo haihitaji kuridhiwa na Bunge la nchi hiyo, iwapo wanasiasa wataendeleza malumbano pasipo kuja na ufumbuzi.
Hata hivyo, Republicans walitoa vitisho mbalimbali kwa Obama dhidi ya kutumia ‘executive order,’ huku baadhi wakitishia kumburuza mahakamani ili kumng’oa madarakani kwa madai ya ‘kukiuka katiba.’
Licha ya vitisho hivyo, na upinzani wa wengi wa wananchi wa kawaida (ambao kura za maoni zilionyesha wananchi wengi kutoafiki Rais kutumia ‘executive order’ katika suala hilo), hatimaye Obama aliweka hadharani mpango huo kabambe utakaowapatia ahueni ya kimakazi takriban wahamiaji milioni tano.
Matokeo ya uamuzi huo ni bayana: Republicans wamekasirishwa mno na hatua hiyo, huku chama cha Democrats ambacho kwa kiwango kikubwa kimekuwa mstari wa mbele kuwanusuru wahamiaji hao, kikinufaika kwa sapoti kutoka kundi muhimu katika siasa za chaguzi za Marekani, Walatino.
Kundi hili linatajwa kuwa muhimu mno kwa vyama vyote viwili, kwa Democrats kubaki madarakani baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2016, na Republicans kukamata Ikulu baada ya miaka 10 ya Obama. Kidemografia, idadi ya Walatino inaongezeka kwa kasi kuliko kundi lolote lile la ‘asili ya watu’ kwa maana ya Wamarekani Weupe na Wamarekani Weusi, na makundi mengine madogo.
Sasa ni wazi kuwa ili mgombea wa chama chochote kile afanikiwe kuingia Ikulu, ni lazima apate sapoti na kura za kutosha kutoka kwa Walatino.
Uamuzi huo wa Obama umekuwa kama mtego kwa Republicans. Laiti chama hicho kikiendeleza upinzani dhidi ya suala hilo, si tu kitajipunguzia umaarufu wake kwa Walatino na hivyo kuathiri nafasi yao katika uchaguzi mkuu ujao, lakini pia kitawatenga Wamarekani wasio Walatino lakini wanaotaka ‘wahamiaji haramu’ kupatiwa makazi ya kudumu nchi humo.
Lakini kwa upande mwingine, chama hicho kinatambua kuwa kwa kiasi kikubwa ‘Wamarekani hao wapya’ (kwa maana ya ‘wahamiaji haramu’ watakaopewa makazi ya kudumu) wataisapoti Democrats kama kulipa fadhila kwa kushughulikia tatizo lao.
Nitaendelea kuwaletea maendeleo ya suala hili katika makala zijazo hasa kwa vile uamuzi huo wa Obama ni kama umeanzisha ‘vita’ ya kisiasa kati yake binafsi (na chama chake) dhidi ya Republicans ambao mapema mwezi huu walifanikiwa kukamata uongozi wa mabunge yote mawili ya nchi hiyo, yaani Seneti na Congress.
Lengo hasa la kuzungumzia tukio hilo la nchini Marekani ni hali ilivyo huko nyumbani hivi sasa. Hadi wakati ninaandaa makala hii, ‘mshikemshike’ unaotokana na skandali ya ufisadi wa ESCROW sio tu unazidi kukua lakini pia unaleta dalili za uwezekano wa Rais Kikwete kulazimika kufanya mabadiliko kwenye Baraza lake la mawaziri kwa mara nyingine.
Kwa vile takribani kila Mtanzania anafahamu kinachoendelea kuhusu skandali hiyo ya ESCROW, sioni haja ya kuizungumzia kiundani. Hata hivyo, pasi haya, na huku nikitambua kuwa Rais wetu Jakaya Kikwete yupo katika matibabu nchini Marekani, ukweli unabaki kuwa yeye ndiye chanzo cha yote haya.
Nikirejea uamuzi wa Obama kutumia ‘nguvu ya kirais’ kupata ufumbuzi katika tatizo la ‘wahamiaji haramu,’ Kikwete alipaswa kuchukua hatua kama hiyo muda mrefu uliopita. Hapa ninamaanisha Rais kutumia nguvu alizopewa na Katiba kupambana na uhalifu.
Ninaandika hivyo kwa sababu Kikwete ana uelewa wa kutosha kuhusu ‘mgogoro wa IPTL’ ikizingatiwa kuwa huko nyuma alishawahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini. Lakini wakati miaka yake 10 ikielekea ukingoni, hakuna jitihada yoyote ya maana iliyofanywa nae kulipatia ufumbuzi tatizo hilo.
Lakini hata tukiweka kando uzoefu wake katika suala hilo, utawala wake utakumbukwa zaidi kwa kuandamwa na mlolongo wa matukio ya ufisadi ambayo hatma yake imekuwa kuwashawishi mafisadi wengine ‘kujaribu bahati zao’.
Naam, kama Kikwete alidiriki ‘kukumbushia haki za binadamu’ za mafisadi wa EPA, na kuwapa deadline ya kurejesha mabilioni waliyoiba, kwanini mafisadi watarajiwa waogope kufanya uhalifu?
Yayumkinika kuhitimisha kwamba laiti idadi ya safari alizokwishafanya nchi za nje ingelingana na hatua dhidi ya ufisadi/ mafisadi, huenda leo hii tungekuwa tunazungumzia ‘mafanikio ya kihistoria ya uchumi wa Tanzania’.
Badala yake, tumekuwa tukiandamwa na vyombo vya habari vya kimataifa kuhusu taifa letu lilivyoukumbatia ufisadi kiasi cha kuruhusu ndege ya msafara wa Rais wa China kuondoka na vipusa, sambamba na taarifa mpya kuwa kuna mpango wa serikali kuwatimua wafugaji wa Kimasai katika makazi yao ili kukabidhi eneo hilo kwa familia ya kifalme ya mojawapo ya nchi za Kiarabu.
Sasa badala ya viongozi wetu kushughulikia changamoto mbalimbali zinazolikabili taifa letu, wamekuwa ‘bize’ kupambana na vyombo vya habari vya kimataifa kukanusha tuhuma hizo. Hivi wazembe hawa hawaoni haya na kujiuliza “kwa kipi hasa cha kuvifanya vyombo vya habari vya kimataifa vituandame bila sababu?”
Kwa upande mwingine, skandali hii ya ESCROW ni uthibitisho mwingine kuwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa (TISS) imepoteza mwelekeo, haitimizi wajibu wake, na ni kama ipo likizo ya muda mrefu.
Hivi inawezekana vipi huyo ‘Singasinga’ anayetajwa kuwa mhusika mkuu katika skandali hiyo aliruhusiwa kuishi Tanzania huko rekodi yake ikionyesha bayana kuwa ni mtu hatari kwa usalama wa taifa letu?
Hii haikuhitaji hata operesheni maalum kwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa kwani habari za mtu huyo zipo wazi kwenye mtandao. Hivi Idara hiyo imejaa uzembe kiasi cha kushindwa japo ku-Google taarifa za mtu huyo?
Lakini kama ambavyo lawama nyingi katika skandali hii zinaelekezwa kwa Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo na Katibu na Katibu Mkuu wake, Eliachim Maswi, sambamba na Mwanasheria Mkuu, Frederick Werema, huku Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, akishutumiwa kwa kushindwa kusimamia vema watendaji walio chini yake, wenye kustahili kubeba lawama kubwa zaidi ni Rais Kikwete na idara yetu ya Usalama wa Taifa.
Ninaandika makala hii kabla ya taarifa za uchunguzi za CAG na TAKUKURU kusomwa hadharani na ‘Kamati ya Zitto’ (PAC), kwahiyo ni vigumu kubashiri hatma ya suala hili. Hata hivyo, uzoefu wa skandali zilizopita, kuanzia Richmond, EPA, Mabilioni  yaliyofichwa Uswisi, Meremeta, Tangold, nk, si ajabu iwapo wahusika wakuu watalindwa na Watanzania kuachwa ‘wanang’aa macho tu.’
Muda mfupi uliopita, zimepatikana taarifa kwamba ripoti hiyo ya PAC imeonekana mitaani huku kurasa zenye majina ya wahusika zikiwa zimenyofolewa. Binafsi ninaamini huo ni ‘uhuni’ tu unaofanywa kuwachanganya Watanzania.
Lakini ukijumlisha na tukio linalodaiwa la kunyweshwa sumu Mbunge Nimrod Mkono, ni muhimu kutodharau nia, sababu na uwezo wa mafisadi kupambana na ukweli kuhusu skandali hii.
Nihitimishe makala hii kwa kumkumbusha Rais Kikwete- kwa mara nyingine - kuwa chini ya mwaka mmoja kutoka sasa atarejea ‘uraiani.’ Ni muhimu kwake kutumia miezi hii michache iliyobaki kurejea ahadi aliyotoa mara baada ya kuapishwa kuwa Rais wetu mwaka 2005 kuwa hatowaonea aibu mafisadi. Tungependa tumkumbuke kwa mema lakini sio rekodi ya kuliingiza taifa kwenye korongo refu la ufisadi.
Kwa ndugu zangu wa Idara ya Usalama wa Taifa, ninawasihi mtambue mzigo mkubwa mnaowabebesha Watanzania masikini kumudu gharama za operesheni zenu. Kwanini msijiskie aibu  kuwasaliti wanyonge hawa –wengi wakiwa ni ndugu, jamaa na marafiki zenu – kwa kutotimiza majukumu yenu ipasavyo?
TUSIPOZIBA UFA TUTAJENGA UKUTA

World AIDS Day 2014 Theme

UKIMWI ulikuwepo na bado upo, na hadi sasa dalili za kuutokomeza ugonjwa huo bado ni ndogo kwani hakuna kinga wala tiba.

Una na fasi ya kuchangia mapambano dhidi ya ugonjwa huu

ACHA ZINAA

KUWA MWAMINIFU

IKISHINDIKANA, TUMIA KINGA

Lakini badala ya kuamini tu kuwa upo salama, ni muhimu pia kufanya vipimo vya ugonjwa huo ili kutambua kama upo salama au umeathirika. Ukiwa salama, Mshukuru Mungu na endelea kuwa makini. Ikitokea bahati mbaya kuwa umeathirika, usikate tamaa kwani kuna matibabu mbalimbali na ya uhakika ya kumwezesha mwathirika wa ugonjwa huu kuishi maisha marefu (japo si tiba kamili).

Iwapo ndugu, jamaa au rafiki yako ameathirika, usimtenge. Mpatie kila aina ya sapoti ikiwa ni pamoja na kum-treat kama binadamu mwenzio. 

Sikiliza wimbo huu wa 'Mshikaji Mmoja' wa msanii wa Kitanzania JOSLIN ambao una mafunzo mengi kuhusu UKIMWI (isipokuwa hitimisho kuwa "ukiupata ni kifo") 

9 Nov 2014

Watafiti wamefanikiwa kubaini kwani aina mbaulimbali za viumbe hai vina sehemu za siri za aina tofauti. Katika nyoka na viumbe wanaotambaa, sehemu zao za siri zimeumbika katika namna zinashabihiana na miguu, na hivyo kutengeneza sehemu za siri mapacha. Katika binadamu, sehemu za siri zimeundwa kwa namna ya mkia/ kiishio cha uti wa mgongo, na hivyo kuwa na sehemu ya siri moja tu.

Soma zaidi kuhusu matokeo ya uchunguzi huo kwa kubonyeza HAPA

Embedded image permalink
Gazeti la The Citizen la Tanzania linamwita 'lulu iliyofichika' (hidden gem, kwa kimombo). Huyu ni Leo Mkamia, msanii wa Kitanzania na mwanzilishi wa aina ya muziki ujulikanao kama 'Swahili Blues.'

Siku chache zilizopita, Leo alirekodi wimbo wake mpya uitwao 'Pamoja.' Miongoni mwa yatakayoonekana katika video ya wimbo huo ni performance ya kihistoria ya msanii huyo katika moja ya vyuo vikuu vikubwa hapa Uingereza, Nottingham University, ambapo Leo alifanikiwa kuwaimbisha Kiswahili baadhi ya wahadhiri na wanafunzi wa chuo hicho kikuu. Katika shughuli hiyo, Leo aliimba na kwaya ya Nottingham Academy.

Kinachomfanya Leo kuwa msanii wa kipekee kutoka Tanzania kuwa na fursa kubwa ya kutawala anga za muziki kimataifa ni ukweli kwamba amefanikiwa kuanzisha kitu kipya- muziki aina ya Swahili Blues- na ambao tayari umeanza kukubalika kimataifa.

Mtaji mkubwa wa Leo ni ukweli kwamba anatoka familia ya muziki.Unamkumbuka mkongwe wa gitaa Henry Mkanyika? Basi huyo ni baba mzazi wa Leo, ambaye alianza kucharaza gitaa akiwa na umri wa miaka minane tu.

 

Kwa sasa Leo ni miongoni mwa wasanii wachache mno, sio tu wa Tanzania, bali Afrika nzima kwa ujumla, ambao sura na sauti zao sasa 'zimezoeleka kwenye vituo vya radio na televisheni vya kimataifa kama BBC. Na katika kuthibitisha hjilo, Leo alihojiwa na BBC mara baadha ya performance hiyo ya kihistoria huko Nottingham.



Pamoja na kufanya vizuri kimataifa, Leo bado anathamini asili yake. Kama video ya pili inavyoonyesha, Leo alifanya mahojiano na mtandao mkubwa na maarufu wa burudani Tanzania na Afrika kwa ujumla wa Bongo5. Kadhalika, msanii huyo anapata sapoti kubwa kutoka kwa mmoja wa waasisi wa muziki wa Hip-Hop nchini Tanzania, lejendari @XamiaSiku4Saa4 wa kundi maarufu kabisa la Kwanza Unit. Ieleweke kwamba katika shughuli za muziki, kupata 'endorsement' ya mkongwe wa muziki ni uthibitisho kuwa msanii husika anafanya kazi nzuri mno.

Kama Watanzania, tuna wajibu na kila sababu ya kumuunga mkono Leo, kwani sio tu anaitangza Tanzania yetu bali pia anautambulisha utamaduni wetu-kwa maana ya lugha ya Kiswahili- kupitia muziki wake wa Swahili Blues.

Unaweza kufuatilia maendeleo yake ya kimuziki kwa akaunti zake mbalimbali za mitandao ya kijamii: Twitter na Facebook  na katika tovuti yake sambamba na ukurasa wake wa YouTube









5 Nov 2014


4 Nov 2014



 













Chama cha Republicans kinaelekea kushinda viti vingi katika Bunge la juu la Seneti, na hivyo kuwapa nafasi ya kuwa na 'wabunge' wengi katika mabunge yote mawili, yaani bunge la juu la Seneti na bunge la chini la Kongresi.

Ushindi huo tarajiwa utakuwa wa mara ya kwanza tangu walipomudu kufanya hivyo wakati wa utawala wa Rais George W. Bush. Ni jambo la kawaida kwa chama cha Rais aliye madarakani kupoteza viti katika chaguzi za kati ya muhula (Midterm Elections). Kwa sasa, chama tawala cha Democrats kinaongoza kwa viti 10 katika bunge la Seneti na kilikuwa na matarajio ya ushindi katika uchaguzi huo utakaofanyika Novemba 4 mwaka huu.

Kwa bahati mbaya, sababu kadhaa zimejitokeza kuwa vikwazo dhidi ya chama hicho cha Rais Barack Obama, ikiwa ni pamoja na rekodi inayokaribia kuwa ya kihistoria ya kukubalika (approval ratings) kwa Rais Obama, mwenendo usioridhisha wa uchumi wa nchi hiyo, upinzani dhidi ya sera ya afya ijulikanayo kama Obamacare, na matarajio ya kujitkeza wapigakura wachache katika uchaguzi huo.


Mwelekeo wa kushindwa kwa chama cha Democrats unatokana na zaidi ya kuporomoka kwa umaarufu wa Obama ambapo wapigakura asilimia 53 hawaridhishwi na Obama kulinganisha na asilimia 42 wanaoridhishwa) na kawaida ya uchaguzi usiohusisha uchaguzi wa Rais (off-year election).

Democrats pia wanasumbuliwa na matokeo ya uchaguzi wa mwaka 2012 katika maeneo ambayo wapinzani wao wa Republicans walifanya vema.

Kuna sababu nyingine pia. Moja ni mikakati ya viongozi wa Republicans kuwezesha sheria kali za uchaguzi ambazo zinakwaza wapigakura watarajiwa, hususan katika maeneo yanayoelemea kwa Democrats. Katika miaka 10 iliyopita, takriban sheria 1000 za kitambulisho cha mpigakura zilitambulishwa kutokana na jithada za Republicans. Sheria hizo zinawataka wapigakura kuonyesha kitambulisho chenye picha au kupunguza masaa ya kupiga kura. Katika ya sheria hizo takriban 1000, karibu 100 zimeshapitishwa. Mahakama kuingilia suala hilo kumechangia kukanganya mwenendo wa upigaji kura (jambo linaloweza kuwapa wapigakura kisingizio cha kutopiga kura siku ya uchaguzi).

Bado haijafahamika ushindi wa chama cha Republican katika uchaguzi huo utamaanisha nini kwa siasa za Marekani kwa sababu haijulikani mkakati gani chama hicho kitautumia pindi kitakaposhinda. Hata hivyo, baadhi ya mipango muhimu ya chama cha Democracts, kwa mfano mageuzi kuhusu uhamiaji na hatua za kisheria kuhusu mabadiliko ya hali ya hewa, imeshakumbana na upinzani katika bunge dogo la Kongress linaloongozwa na Republicans. Iwapo Conservatives watafanikiwa kuongoza na Seneti pia, wanaweza kumpa wakati mgumu Rais Obama kwa kupinga uteuzi wa majaji,uteuzi wa mawaziri na teuzi nyinginezo zinazohitaji kuthibitishwa na Seneti.

Uongozi wa Republican kwenye mabunge yote mawili unaweza kumlazimisha Rais Obama kutumia kura yake ya veto kama kimbilio la mwisho.

Rais Obama akipiga kura katika uchaguzi wa kati ya muhula 
Lakini wachambuzi mbalimbali wameonyesha madhara yasiyofichika kwa chama cha Republicans pia. Iwapo chama hicho kitaonekana kumpinga Obama katika kila jambo, watajiweka katika hatari ya kutengwa na umma na hivyo kuhatarisha nafasi ya kushinda uchaguzi mkuu wa Rais mwaka keshokutwa. Ikumbukwe kuwa chama cha Democrats wana 'mgombea' mwenye uwezo wa kushinda urais mwaka 2016, kwa maana ya Hillary Clinton.Kwa upande wa Conservatives, majina yanayotajwa hadi sasa ni ya wanasiasa wasio na nguvu kubwa.Kwa maana hiyo watahitaji mwonekano bora kwa wapigakura iwapo watataka kushinda katika uchaguzi huo mkuu.

Kingine kinachoweza kuwaathiri Republicans ni kilekile kinachokikabili chama cha upinzani kinachojaribu kuking'oa madarakani chama tawala: kuongoza mabunge yote mawili kutapelekea matarajio kwa wananchi kutoka kwa chama hicho.Republicans wameshatoa ahadi kibao kuhusu kupunguza kodi na miradi ya serikali kuu. Wakishindwa kutekeleza ahadi hizo kutaambatana na gharama ya kisiasa. Kadhalika, sheria kali zitakazotungwa kwa kutumia wingi wao katika Seneti na Kongresi zaweza kuwaathiri wagombea urais watarajiwa wa chama hicho waliopo kwenye Seneti, yaani Rand Paul, Marco Rubio na Ted Cruz, hasa wakiunga mkono maamuzi watakayokuwa na wakati mgumu kuyatetea wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu.

Iwapo Republicans watashinda na kuchukua uongozi wa Seneti, jambo moja la wazi ni kupanuka kwa mgawanyiko wa kiitikadi hasa kati ya bunge na serikali.

CHANZO: Imetafsiriwa kutoka gazeti la The Guardian la hapa Uingereza. 



31 Oct 2014

Makala hii ilipaswa kuchapishwa katika jarida la Raia Mwema toleo la Oktoba 22, 2014 lakini kwa sababu wanazozijua wahusika pekee haikuchapishwa. Nomba kukupa fursa ya kuisoma katika uhalisi wake.

Duru za siasa za Uingereza zimevamiwa na mwanasiasa hatari lakini mahiri kwa ushawishi, ndivyo wanavyoeleza baadhi ya wachambuzi wa siasa nchini hapa kufuatia kuibuka kwa kasi kwa Nigel Farage na chama chake ‘cha kibaguzi’ cha United Kingdom Independence Party (UKIP).

Pamoja na kauli zake za kukera na pengine za ubaguzi wa waziwazi, Farage ana kipaji muhimu kwa mwanasiasa: kutumia mapungufu  ya vyama vikuu – Conservatives, Labour na Liberal Democrats – kuwavuta wananchi wakiunge mkono chama chake. Na anafanikiwa kwa kiasi kikubwa, hasa baada ya chama hicho kushinda kiti cha ubunge katika uchaguzi mdogo wa jimbo la uchaguzi la Clacton huko England.

Matokeo hayo yamekipatia chama hicho mbunge wa kwanza, Douglas Carswell, ambaye alihama kutoka Conservatives hivi karibuni. Taratibu duru za kisiasa nchini hapa zinaanza kuiona UKIP kama chama makini licha ya sera zake zenye mwelekeo wa ubaguzi.

Ajenda kuu ya UKIP ni kuitaka Uingereza ijiondoe kwenye Umoja wa nchi za Ulaya (European Union). Kadhalika, chama hicho kinapinga vikali ujio wa wageni nchini hapa, huku kikidai kuwa serikali ya chama tawala (Conservatives) inayoshirikiana na Liberal Democrats, imeshindwa kama ilivyokuwa kwa serikali iliyotangulia ya Labour kutatua tatizo hilo.

Suala la uhamiaji ni moja ya turufu muhimu kila unapojiri uchaguzi katika nchi hii, na UKIP wanaitumia ajenda hiyo kwa ufanisi mkubwa. Hata hivyo, baadhi ya wachambuzi wanatahadharisha kuwa Farage ni mtu hatari kwa sababu ya mrengo wake mkali wa kulia ambao unakaribiana na ule wa chama cha wazi cha kibaguzi cha British National Party. Baadhi ya wachambuzi wanaiona UKIP kama mchanganyiko wa Conservatives na BNP, lakini wanatambua kuwa mvuto wake unachangiwa na kuongea yale yanayowagusa wapiga kura wengi.

Laiti UKIP ikiendelea kufanya vema, na dalili zipo za kutosha, kuna uwezekano wa chama hicho kuweza kuunda serikali ya umoja na Conservatives baada ya uchaguzi mkuu ujao. Laiti hilo likitokea, ni wazi kuwa Uingereza itakuwa taifa tofauti kwa kiasi kikubwa na hilo tulilonalo hivi sasa.

Lengo la makala hii sio kumzungumzia Farage au chama chake cha UKIP bali kuangalia haja ya kuwa na ‘akina Nigel Farage wa siasa za Tanzania.’ Hapo simaanishi kuwa na wanasiasa wenye sera za kibaguzi bali wenye kutambua matatizo yanayoikabili Tanzania yetu na sio tu kuyatumia kupata sapoti bali kuyatafutia ufumbuzi. Kwa sasa hatuna mwanasiasa wa aina hiyo.

Sijui hadi muda huu ni Watanzania wangapi wanatambua kuwa tuna chini ya mwaka mmoja kabla ya kufanyika kwa uchaguzi mkuu hapo mwakani. Sintofahamu ya Bunge la Katiba na hatimaye kupatikana kwa Katiba pendekezwa kumewachanganya wananchi vya kutosha. Na katika kukoroga mambo zaidi, yayumkinika kuhitimisha kuwa ni Watanzania wachache tu wanaofahamu iwapo kutakuwa na kura ya maoni ya kupitisha au kukataa Katiba pendekezwa. Tayari Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeshatamka kuwa haiwezi kuharakisha kura hiyo, japo Rais Jakaya Kikwete ameendelea kuwahakikishia Watanzania kuwa Katiba mpya itapatikana hivi karibuni.

Tupate Katiba mpya au la, mwaka mmoja kutoka sasa tutamchagua mrithi wa Rais Kikwete, awe ni kutoka CCM au chama kingine. Mazingira yalivyo hadi sasa hayatoi mwelekeo wa nani anayeweza kushika wadhifa huo muhimu kwa Tanzania yetu. Binafsi, ninaamini kuwa mrithi wa Kikwete atakuwa ‘mtu wake wa karibu,’ chaguo lake ambalo kwa mbinu za wazi na zisizo wazi atapigiwa upatu hadi kushika wadhifa huo.

Sababu ya Kikwete kuuhitaji ‘mtu wake’ ipo wazi. Vipindi vyake viwili vya utawala vimetawaliwa na mlolongo wa kashfa mbalimbali za ufisadi. Pasipo kuwa na mtu ‘wa kuaminika,’ si ajabu tukashuhudia yaliyomkumba Rais wa zamani za Zambia Frederick Chiluba. Na hata kama haistahili kwa Rais aliye madarakani kumwandama mrithi wake, mantiki ya kawaida tu inatosha kueleza kuwa hakuna mtu anayetaka kustaafu huku hajui hatma yake itakuwa vipi. Moja ya kanuni isiyo rasmi ya siasa ni hii: “kamwe usimkabidhi madaraka adui yako. Atakuangamiza hata kabla hajaizowea ofisi uliyomkabidhi.” Ni wazi Kikwete analitambua hilo.

Mengi yanaongelewa kuhusu ‘watu wa karibu na Kikwete’ lakini ni vigumu kujua ukweli. Kama kuna mwanasiasa ambaye amefanikiwa sana kuonekana kama mrithi asiye rasmi wa Kikwete ni Edward Lowassa. Lakini taarifa zinakanganya kuhusu mahusiano ya wanasiasa hao ambao walikuwa marafiki wakubwa. Kuna wanaodai urafiki wao umevurugika, lakini uzoefu wa kisiasa waonyeshe kuwa hakuna maadui (au marafiki) wa kudumu katika siasa. Kwa vile Lowassa (Akishirikiana na mwanasiasa mwingine Rostam Aziz) alimsaidia sana Kikwete kuingia madarakani, yawezekana ‘deni’ hilo likapelekea Kikwete kumsaidia Lowassa kuwa mrithi wake, hasa endapo (Lowassa) atamhakikishia Kikwete ‘usalama wake’ baada ya kustaafu.

Kuna wanaosema Bernard Membe, mwanasiasa mwingine aliye karibu na Kikwete ni miongoni mwa wanaoweza kupewa nafasi hiyo. Nilishawahi kuongelea vikwazo dhidi ya Membe lakini kwa vile ni vigumu kwa nchi ya Kiafrika kupata Rais kinyume na matakwa ya Idara ya Usalama wa Taifa ya nchi husika, na kwa vile Membe ni shushushu mstaafu, basi hakuna lisilowezekana iwapo atapata sapoti ya kutosha kutoka kwa ‘mashushushu wenzake.’

Lipo suala la Zanzibar ambalo kwa akina sie tunaochimbachimba mambo tunaona ni kama bomu la wakati (time bomb) linalosubiri kulipuka kuhusiana na hatma ya Muungano. Sahau kuhusu Katiba pendekezwa, hatma ya Muungano itategemea uwezo wa aliyepo madarakani kulazimisha matakwa ya watawala. Na kwa minajili hiyo, naona uwezekano wa Dkt Ali Shein kupigiwa chapuo amrithi Kikwete. Na kwa vile Shein amekuwa Makamu wa Rais wa Kikwete kwa miaka 10, si vigumu kumpatia ‘bosi wake wa zamani’ uhakika wa ustaafu wake.

Kuhusu Waziri Mkuu Mizengo Pinda, binafsi ninashindwa kuelewa malengo yake kuhusu kuwania urais. Labda yawezekana ni kile kinachoitwa ‘Plan B’ yaani iwapo kila ‘mrithi mtarajiwa wa Kikwete’ akishindikana, basi Pinda anakuwa ‘mchezaji wa akiba’ wa kuokoa jahazi. Katika mazingira ya kawaida, ni miujiza tu ndiyo inayoweza kumwingiza Pinda Ikulu. Sababu ni nyingi, nitaziongelea katika makala zijazo. Hata hivyo, kama alivyo Membe, Pinda ni shushushu mstaafu, na hilo laweza kuwa turufu kwake.

Wakati takriban yote niliyoyaongelea hapo juu ni ya kufikirika zaidi kwa maana hayajiri waziwazi, mwanasiasa pekee ambaye tangu aitangaze nia yake ya kutaka urais hapo mwakani ameendelea kuwaaminisha Watanzania kuwa yupo ‘serious’ ni January Makamba. Ninaomba kukiri kwamba awali nilipomsikia January akitangaza nia hiyo nilidhani anatania. Siku kadhaa baadaye, kwa kutumia mitandao ya kijamii hasa Twitter, mwanasiasa huyo kijana amejitanabaisha kama mtu anayetaka kwa dhati kuliongoza taifa hili.

Hivi ninavyoandika makala hii, January ameanzisha utaratibu wa maswali na majibu (question and answer session) huko Twitter kwa kutumia ‘hashtag’ #askJanuary yaani ‘Muulize January.’ Japo ninatambua kuwa ni vigumu kuhitimisha ‘mafanikio’ ya mwanasiasa kwa kuangalia ‘anavyojichanganya na watu’ katika mtandao wa kijamii, hasa kwa kuzingatia ukweli kwamba bado Watanzania wengi si watumiaji wa mitandao ya jamii, January amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kujenga sio tu kuaminika kuwa yupo ‘serious’ katika dhamira yake ya kutaka urais mwakani lakini pia amejiweka karibu na watu wengi wanaotumia mitandao hiyo ya kijamii.

Sasa kama Rais ajaye atatokana na kutambulika kwake kwa angalau baadhi ya wapiga kura, basi hadi muda huu January anaongoza katika hilo- pasi haja ya kufanya opinion poll. Alitangaza anataka urais, ameendelea kuwaaminisha wananchi kuwa anataka urais, anaendelea kueleza atafanya nini akiwa Rais, na kwa sie tunaoamini kuwa mitandao ya kijamii ni moja ya nyenzo muhimu kufikisha ujumbe kwa wananchi (angalau huku nchi za Magharibi), basi lolote linawezekana kwa mwanasiasa huyo kijana.

Nihitimishe makala hii kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi huu wa wagombea urais ambapo katika moja ya makala zijazo nitazungumzia ‘muungano wa UKAWA kumsimamisha mgombea mmoja’ nikielemea zaidi kwenye vikwazo kutoka kwa ‘nguvu za giza’, sambamba na kuwachambua wanasiasa wengine wanaotajwatajwa. Kwa mfano, kuna anayedhani Ridhiwani Kikwete anaweza kuingia katika mbio za kurithi nafasi inayoshikiliwa na baba yake hivi sasa?

Mwisho kabisa, kama tahadhari, uchambuzi wangu unaelemea zaidi katika kile tunachoita’ hali halisi mtaani,’ kufuatilia matokeo kadri yanavyojiri, upepo wa kisiasa unavyovuma, na ninajitahidi kuepuka kutumia uelewa wangu wa stadi za siasa au taaluma nyinginezo kuniongoza katika uchambuzi huu.  Kwa kifupi, ninaongozwa na hali halisi.

MUNGU IBARIKI TANZANIA

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com  


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.