24 Jan 2015

Siku ya mwaka mpya nilitangaza huko Twitter kuhusu dhamira yangu ya #ProBono yaani kuwahamasisha watu wenye uwezo, vipaji au nafasi mbalimbali kuisadia jamii bure. Kimsingi, huku nchi za Magharibi, sekta ya kujitolea pasi malipo imekuwa na msaada sana kwa jamii. Ninaamini kwamba nasi tukijaribu, itakuwa na msaada mkubwa sana hasa tukizingatia jinsi umasikini unavyowakwaza wanajamii wengi.

 So far, mwitikio umekuwa wa kuridhisha. Tayari, mwanasheria mmoja mahiri huko nyumbani anashughulikia bure kesi ya mwanajamii mmoja huku akiridhia kupelekewa kesi nyingine inayohusu mirathi. Pia gwiji mmoja wa fani ya PR na Marketing amekubali kumsaidia mwanajamii mmoja kuingia kwenye fani hiyo. Vilevile, designer mmoja wa kimataifa huko nyumbani amekubali kumsaidia desgner mchanga aliyekuwa anahitaji mwongozo katika fani hiyo.Kadhalika, dada mmoja mtaalam wa mambo ya fedha amekubali kutoa msaada wa ushauri wa kifedha bure, sambamba na wasanii wawili maarufu wa huko nyumbani, mmoja wa Bongoflava na mwingine wa Bongo Movies.


Lengo la makala hii sio kuzungumzia kuhusu #ProBono bali muda mfupi uliopita, nilikutana na habari ambayo kwa namna flani inahusiana na suala hilo la #ProBono. Hivi unawakumbuka TLC? Ni kikundi cha akinadada watatu wa Marekani ambao walivuma sana miaka ya nyuma katika fani ya R&B.

Labda kabla ya kwenda mbali, niamshe kumbukumbu yako kwa mmoja wa nyimbo zao maarufu, Red Light Special (TAHADHARI: Hii ni 'dirty version.')




Kwa bahati mbaya, Aprili 25, 2002 kundi hili la akinadada watatu lilipatwa na mkosi wa kuondokea na mwenzao aliyekuwa maarufu zaidi, Lisa Lopez au maarufu kama 'Left Eye, (pichani chini) aliyefariki kwa ajali ya gari akiwa mapumzikoni nchini  Honduras.


Kifo cha mwenzao huyo kililiathiri sana kundi hilo, kwa sababu zilizo wazi.

Hata hivyo, katika jitihada zake za kurejea tena katika anga za muziki, wasanii wawili waliobaki katika kundi hilo, Rozonda 'Chilli' Thomas na Tionne 'T-Boz' Watkins, waligeukia wazo la ujasiriamali linalotamba sasa katika nchi za Magharibi hasa Marekani, linalofahamika kama 'crowdfunding' (kuomba jamii ikuchangie fedha) kupitia jukwaa la kufanya hivyo linalojulikana kama KICKSTARTER

T-Boz (kushoto) na Chilli

Habari njema ni kwamba siku nne tu baada ya kuanzisha kampeni yao ya Kickstarter kuwapatia dola za kimarekani 150000 kwa ajili ya kutengeneza albamu yao mpya, na ya kwanza baada ya miaka 10 ya ukimya, wamefanikiwa kupata michango zaidi ya kiwango walichokusudia.Hadi kufikia juzi, walikuwa wameshachangiwa Dola za kimarekani 180000, ikiwa ni Dola 30000 zaidi ya kiwango walichokusudia.

Kilichowapa moyo zaidi ni pale walipotembelea ukurasa wao wa Kickstarter


na kubaini kuwa msanii mahiri wa Pop, Katy Perry (pichani chini), ameahidi kuwachangia dola 5000. Kadhalika, kundi maarufu la zamani la New Kids on the Block limeahidi kuwachangia wanadada hao dola 20,000

Baada ya kusoma habari hiyo nikakumbuka wazo langu la #ProBono na kujiuliza, hivi haiwezekani kuwasaidia wanajamii mbalimbali, kwa mfano wasanii wetu, katika namna hiyo kundi la TLC linasaidiwa na jamii kutimiza lengo lao la kutengeneza album mpya?

Jibu ni kwamba inawezekana, japo si rahisi sana kuwashawishi watu wachangie fedha kwa ajili ya mafanikio ya mtu mwingine. Hata hivyo, cha muhimu hapa ni moyo wa kujitolea. Kwahiyo basi, ushauri wangu, hasa kwa kuanzia na wasanii, mfanye moja kati ya haya mawili:

Kwanza, aidha mjaribu bahati zenu huko Kickstarter, kama wanavyofanya TLC japo yaweza kuwa vigumu kwa msanii asiye maarufu

Au pili, tumieni mpango wa #ProBono kama nilivyoueleza ambapo kwa pamoja tutahamasisha upatikanaji wa mahitaji mbalimbali kwa ajili ya utengenezaji na uzinduzi wa kazi ya msanii husika. 

Sharing is always caring!



15 Jan 2015



 

30 Dec 2014



Nesi mmoja aliyekwenda Sierra Leone kusaidia harakati za kukabiliana na janga la ugonjwa wa Ebola, amerudi Uingereza akiwa ameambukizwa ugonjwa huo, na hivi sasa amelazwa kwenye kituo cha maradhi ya kuambukiza cha Browlee katika Hospitali Kuu ya Gartnavel, hapa Glasgow.

Nesi huyo anatarajiwa kuhamishiwa London kwenye hospitali maalum ya Royal Free Hospital.

Wakati huohuo, Waziri Mkuu wa Uskochi, Nicola Sturgeon, amewahakikishia wakazi wa Glasgow na Uskochi kwa ujumla kuwa uwezekano wa kusambaa kwa ugonjwa huo kutokana na maambukizi ya nesi huyo ni 'sawa na sifuri.'

Hata hivyo, bado kuna maswali ilikuwaje nesi huyo aliyepimwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Heathrow, London, kabla ya kuunganisha ndege na kuja Glasgow, hakugundulika kuwa na maambukizi ya ugonjwa huo hatari usio na kinga wala tiba.

Profesa Jonathan Ball, mtaalam wa 'molecular virology' katika Chuo Kikuu cha Nottingham, ameeleza kuwa kesi hiyo inaashiria ugumu wa mkakati wa kupima wasafiri kutoka nchi zilzoathirika na Ebola wanapoingia Uingereza.

Chini ni baadhi ya picha zinazohusiana na habari hii ambayo waweza kuisoma kwa kirefu HAPA

A female health worker who returned from Sierra Leone last night is being treated for Ebola at Glasgow's Gartnavel Hospital (pictured), the Scottish Government confirmed
Hospitali ya Gartnavel

Safari ya nesi aliyeambukizwa Ebola, kutoka Sieera Leone hadi Glasgow.



The health worker was admitted to hospital early yesterday morning after feeling unwell and was placed in isolation 

The ebola patient is being treated at the specialist Brownlee Unit for Infectious Diseases at Gartnavel Hospital
Kituo cha maradhi ya kuambukiza cha Brownlee

24 Dec 2014

Awali,kupitia akaunti yake ya Twitter, Idhaa ya Kiswahili ya Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC Swahili) iliripoti ifuatavyo



Hata hivyo, baada ya kuzongwa na baadhi ya WANAHARAKATI huko Twitter walioonyesha kukerwa na hatua hiyo ya nchi wahisani, Mwenyekiti wa nchi wahisani, Balozi wa Finland nchini Tanzania Sinikka Antila (@SinikkaAntila) alifafanua kwa tweet ifuatayo 


Kwa lugha ya taifa, Balozi huyo anaeleza kwamba "vyombo vya habari havipo sahihi. Asilimia 15 ya msaada ulioahidiwa kwa bajeti ya mwaka 2014/15 ilitolewa kabla ya hotuba ya Rais (Kikwete)."

Hata hivyo, licha ya kauli hiyo ya Balozi Antila kutanabaisha kuwa BBC Swahili waliripoti ndivyo sivyo kuwa wafadhili wameamua kutofa fedha hizo baada ya kuridhishwa na hotuba ya Rais Kikwete, bado kuna swali gumu kuhusu suala hilo, nalo ni JE NCHI WAFADHILI ZILITUHADAA ZILIPODAI KUWA ZIMESITISHA MISAADA HADI HATUA ZITAKAPOCHUKULIWA KUHUSU SUALA LA ESCROW?

Swali hilo linatokana na kauli ya Balozi huyo wa Finland kuwa fedha hizo zilishatolewa hata kabla ya hotuba ya Rais Kikwete, ikimaanisha aidha nchi hizo wahisani zilikuwa zina hakika kuwa Rais Kikwete angechukua 'hatua hizo za kuwaridhisha wafadhili' au 'walituzuga tu' kuhusu kusitishwa misaada hiyo.

Kadhalika, kauli ya Balozi Antila haikanushi kuridhishwa kwa wafadhili na hotuba ya Rais Kikwete, ambayo Watanzania wengi wanaamini kuwa imewalinda mafisadi hasa ikizingatiwa mzigo mkubwa wanaoubeba kutokana na sakata la muda mrefu la IPTL. Kwa Rais Kikwete kushindwa kumaliza sakata hilo, na kuridhia kuwa pesa za Tegeta Escrow ni za IPTL/ PAP, ina maana Watanzania wataendelea kulipa mamilioni ya shilingi kila siku kwa huduma ya umeme ambayo kimsingi ni hewa.

Binafsi ninaguswa na uamuzi wa nchi wahisani kwa sababu kama mkazi wa Uingereza, ninalipa kodi mbalimbali, ambazo sehemu ya kodi hiyo ipo katika misaada inayotolewa na nchi hii kwa Tanzania. Wakati sina kipingamizi kwa nchi hizo kuisaidia Tanzania, siungi mkono kabisa kuendelea kutoa fedha zinazoishia kuwaneemesha mafisadi kwa kunenepesha akaunti zao, kuongeza idadi za mahekalu na magari yao ya thamani na kukuza idadi ya nyumba zao ndogo.

Ufadhili usiozingatia maslahi ya nchi fadhiliwa sio tu ni upuuzi bali pia ni ku-abuse fedha za walipakodi katika nchi wafadhili.

18 Dec 2014

Desemba 9, ilikuwa siku yangu ya kuzaliwa. Niliadhimisha sikukuu hiyo kwa sala, kumshukuru Mungu kwa kunijaalia kuongeza mwaka mwingine katika umri wangu sambamba na kuomba baraka zaidi.
Kadhalika, kama zilivyokuwa sikukuu zangu za kuzaliwa huko nyuma, niliadhimisha siku hiyo kwa kufanya tafakuri ya nilipotoka, nilipo na niendako.
Siku ya kuzaliwa ina pande mbili, moja ya furaha kwa maana ya kutimiza mwaka mwingine katika maisha, na ya pili ni kutambua kwamba umri unakwenda mbele, na hivyo kupitia malengo mbalimbali kuona kama yametimia, na kwa kiwango gani, na wapi panahitaji jitihada zaidi, sambamba na kuweka malengo mapya inapobidi.
Kadhalika, wakati kwa vijana wenye umri mdogo, sikukuu ya siku ya kuzaliwa ni furaha tupu, ambapo kwa mfano, sheria mbalimbali zinatoa ruhusa fulani kwa kutimiza umri fulani, kwa wenye umri mkubwa, sikukuu hiyo huambatana na ukweli mchungu kuwa ‘dakika zinayoyoma.’
Kwa kijana wa miaka 17, kutimiza miaka 18 kunamaanisha fursa ya kupiga kura, kwa mfano. Kwa hapa Uingereza, kutimiza miaka 18 kunamaanisha ruhusa kisheria kutumia kilevi.
Lengo la makala hii si kuzungumzia sikukuu yangu ya kuzaliwa. Ukweli kwamba sikukuu yangu ya kuzaliwa inalingana na sikukuu ya kusherehekea uhuru wa Tanganyika huzua tafakuri nyingine mpya kuhusu nchi yetu.
Wakati sikukuu ya kuzaliwa kwangu ni suala langu binafsi, sikukuu ya uhuru wa Tanganyika ni suala linalomgusa kila mmoja wetu.
Japo hujiskia fahari kuchangia sikukuu ya kuzaliwa na Tanganyika, ukweli mchungu ni kwamba ninalazimika pia kujiuliza nchi yangu imetoka wapi, ipo wapi, na inaelekea wapi, na mara nyingi tafakuri hiyo huvuruga kabisa sikukuu yangu ya kuzaliwa.
Kama nilivyotimiza miaka kadhaa tangu nizaliwe, jana Tanganyika yetu imetimiza miaka 53 tangu ipate Uhuru. Wakati binafsi ninaweza kuhitimisha kuwa angalau nimepiga hatua fulani kimaisha, huku malengo kadhaa niliyojiwekea huko nyuma yakitimia au yakielekea kutimia, kwa mwenzangu Tanganyika hali si nzuri.
Tumefika mahala, baadhi ya Watanganyika wamefikia hatua ya kutamani mkoloni asingeondoka.
Nitakuwa mwenye roho mbaya iwapo nitazungumzia mabaya tu yaliyoiandama na yanayoendelea kuiandama nchi. Lakini kwa vile tafakuri katika siku muhimu kama hiyo inalenga zaidi kuangalia maeneo yanayoifanya isiwe timilifu, basi inakuwa vigumu kutoyapa uzito matatizo badala ya mafanikio.
Kadhalika, siku hiyo ni ya kupima mzani wa mafanikio na kufeli, na pindi mzani ukielemea upande wa kufeli, basi lazima taa ya tahadhari iwashwe kwani hali hiyo yaweza kuashiria matatizo zaidi huko mbele.
Kati ya sababu za kudai Uhuru kutoka kwa mkoloni ni kutaka kujitawala wenyewe, sambamba na kuondokana na mfumo wa kibaguzi uliotufanya tuwe mithili ya wageni katika nchi yetu wenyewe.
Miaka kadhaa baada ya Uhuru, jitihada zilizoongozwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, zilionyesha matunda ya uhuru na si tu tulifanikiwa kwa kiasi kikubwa kujenga jamii yenye usawa lakini pia tulimudu kujitegemea wenyewe.
Matatizo yalianza kujichomoza baada ya Mwalimu kuondoka madarakani na hatimaye kufariki kwake. Kimsingi, nchi yetu ilikuwa kama ipo mikononi mwa Nyerere, na ilikuwa inasubiri aondoke tu ili irejee mahala pabaya pengine zaidi ya ilivyokuwa kabla ya Uhuru.
Ieleweke kwamba wakati mkoloni alikuwa na ‘excuse’ (japo isiyokubalika) ya kuiba raslimali zetu kwa ajili ya matumizi ya viwanda vyao huku Ulaya, wakoloni weusi kwa maana ya Watanganyika wenzetu waliosomeshwa na Watanganyika wenzao waliojinyima ili wapate viongozi, hawana sababu moja hata ya kutusaliti.
Yaani angalau mkoloni angeweza kujitetea kwamba acha niibe kwa sababu hii nchi si yangu. Lakini kwa wakoloni weusi, Watangayika wenzetu wanaoendekeza ufisadi hawawezi kudiriki kujitetea kwa namna yoyote ile, hasa ikizingatiwa kwamba kihistoria, takriban sote ni ndugu kwa kuzingatia asili yetu.
Kwa maana hiyo, kiongozi anayekabidhiwa dhamana kisha akafanya ufisadi, anajiathiri yeye mwenyewe pia kwa sababu mahala fulani, kuna mtu wake wa karibu atakayekuwa mhanga wa ufisadi huo.
Tusiende mbali. Angalia skandali ya ufisadi wa hivi karibuni wa Tegeta Escrow. Baadhi ya wabunge walikuwa wakitokwa na mapovu kutetea kuwa fedha fedha hizo si za umma ilhali nao ni sehemu ya umma wanaoukana. Takriban wote waliojivika kilemba cha itikadi, mdudu anayeiangamiza Tanganyika yetu kwa kasi kubwa.
Si kwamba watu hawa wamekunywa maji ya bendera kiasi cha kutoelewa kitu kingine chochote zaidi ya maslahi ya chama chao bali itikadi yatumika tu kama kilemba cha kufika nia zao mbaya.
Lakini pia suala la Tegeta Escrow limeibua tena tatizo moja linalotukwaza kama Taifa. Hili ni utegemezi wetu kwa wanasiasa na taasisi kama vyama vya siasa na watu, kwa maana ya wanasiasa.
Ukiweka kando kelele ndogo kwenye mitandao ya kijamii kudai wananchi watendewe haki kwa kurejeshewa fedha zilizokwapuliwa katika akaunti ya Tegeta Escrow na wahusika wawajibishwe, kwa kiasi kikubwa suala hilo liliachwa mikononi mwa wanasiasa.
Katika hili, ninaweza kumlaumu Mwalimu Nyerere kidogo. Pengine kwa vile tulikuwa tukihangaika kujenga Taifa lenye kujali usawa wa binadamu, na hivyo kuleta umuhimu wa wateule wachache wa kusimamia mambo, zama hizo zilikuwa za viongozi kama miungu-watu.
Mfumo wa siasa enzi hizo uliwapa madaraka wateule wachache ambao kila walichosema kilikuwa sahihi hata kama si sahihi, na ukaribu wao na watawaliwa ulikuwa mdogo mno.
Miongoni mwa madhara ya mfumo huo ndio hii hali tuliyonayo sasa ambapo wananchi wamekuwa wategemezi wa kupindukia kwa taasisi kama serikali au vyama vya siasa, na watu, hususan, wanasiasa.
Sasa angalau katika zama hizo za Mwalimu, kwa kiasi kikubwa sote tulikuwa na maslahi yanayolingana, yaani ujenzi wa Taifa kwa faida ya wote. Hivi sasa tuna wahuni wengi tu waliojiingiza kwenye siasa kwa maslahi yao binafsi. Na kama nilivyotanabahisha awali, maslahi ya chama yamekuwa kama kitu cha kuficha tu maslahi binafsi.
Ni muhimu kutambua udhaifu wa taasisi zetu na wanasiasa wetu. Lakini hata taasisi hizo zingekuwa timilifu na wanasiasa wetu kuwa imara, ukweli unabaki kuwa wao ni sehemu ya tabaka tawala, na kwa kiasi kikubwa wanatetea maslahi ya tabaka hilo, ilhali wananchi wengi wapo tabaka la chini.
Na kwa vile hatuna tabaka la kati la kueleweka, utegemezi kwa vyama vya siasa/ serikali au wanasiasa utaendelea kuwa kikwazo kikubwa kwa wananchi.
Wakati jana Tanganyika yetu imetimiza miaka 53, hivi kuna anayeweza angalau kubashiri hali itakuwaje miaka 20 kutoka sasa?
Kwa kasi hii ya mafisadi kushindana kuifilisi nchi, Tanganyika ya mwaka 2050, kwa mfano, itakuwa na tembo hata mmoja? Je, madini tuliyonayo ambayo yanawanufaisha zaidi wawekezaji na watawala wetu yatadumu kwa muda gani? Na hata hayo mafuta na gesi ambayo tunanyimwa haki ya kuona mikataba yake, yatakuwa neema au laana  kwetu?
Hadi wakati ninaandika makala hii, maazimio ya Bunge kuhusu skandali ya Tegeta Escrow hayajajibiwa. Ukimya wa Rais Jakaya Kikwete unaanza kuwafanya baadhi ya wananchi kuhisi kuwa tumeliwa.
Wananchi wanaishia kuonyesha masikitiko tu pasipo dalili ya kushinikiza wapatiwe haki yao kwa njia za amani.
Tumeona nguvu ya umma inavyoweza kuzaa matunda. Watanzania walihamasishana hadi msanii Diamond akashinda tuzo tatu kwenye Tuzo za Video za Kituo cha Televisheni cha Channel O (CHOAMVA). Tumeshuhudia pia nguvu ya umma ilivyomwezesha mwakilishi wa Tanzania katika Big Brother 2014 kuwa mshindi na kujinyakulia dola za Kimarekani 300,000. Kwanini basi nguvu hiyohiyo isitumike kushinikiza sio tu maazimio ya bunge kuhusu Tegeta Escrow yafanyiwe kazi bali pia kudai mabilioni yetu yaliyoibiwa na kufichwa katika mabenki nchi Uswisi yarejeshwe?
Nihitimishe makala hii kwa kumtakia mwenzangu Tanganyika heri na baraka ya kutimiza miaka 53. Lakini ninaomba pia kutumia fursa hiyo kumkumbusha (kwa maana ya wananchi wenzangu) kuwa tulipotoka kulikuwa na matumaini, tulipo si kuzuri na tuendako hakueleweki.
Ni wajibu wetu kubadili mwelekeo huu. Hili si suala la hiari bali la lazima iwapo twataka kuiona Tanganyika yetu ikiishi maisha marefu ya furaha na amani.


16 Dec 2014

Heri ya siku yako ya kuzaliwa dadangu mpendwa, mwanaharakati, mpambanaji, sauti ya wasio na sauti, mtetezi wa wanyonge, na uthibitisho kamili kuwa utetezi wa mema katika jamii hauna jinsia. Ukiskia "wanawake tunaweza," basi Dadangu huyu ndio kama kamusi ya tafsiri halisi ya msemo huo.

Nimejifunza mengi kwa Maria, na ninaendelea kujifunza mengi. Pamoja na uwezo wake mkubwa katika kila analofanya au analoamini, dadangu huyu si mjivuni, ana heshima kwa kila mtu, na mstahimilivu sana.

Asante Maria kwa kila kitu, Tanzania yetu ina deni kubwa kwako kwa jitihada zako.

Mungu akujalie kila la kheri na mafanikio katika maisha yako.

Happy birthday Maria Sarungi

9 Dec 2014


Nadhani mnakumbuka jinsi kikundi cha WANAHARAKATI kilivyoshikilia bango kuhusu kilichoitwa mradi wa treni za kisasa kati ya Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere na Mjini Kati Dar, ambapo aliyeitwa 'mwekezaji, ROBERT SHUMAKE, alidai yupo tayari kuuanza hata siku hiyohiyo uliposainiwa mkataba wa awali. Bonyeza  HAPA kusoma zaidi kuhusu suala hilo na ufuatiliaji wetu.

Hata hivyo, nadhani haitoshi tu kumtilia mashaka SHUMAKE Pasi kuchukua hatua dhidi ya wahusika. Ikumbukwe SHUMAKE bado ni Balozi wetu wa heshimu huko Marekani. Je kama anatiliwa mashaka katika suala hili haitoshi kumvua wadhifa huo aliopewa katika mazingira yasiyoeleweka? Kadhalika, je kwanini waliokurupuka kusaini mkataba wa awali na mbabaishaji huyo wasiwajibishwe? 

Tusipokuwa makini, mtu huyo 'mjanja mjanja' anaweza kuzua IPTL nyingine kwa kusaini mkataba kwa huduma isiyopatikana kisha kudai malipo asiyostahili.


Wakati Tanzania Bara inatimiza miaka 53 ya uhuru, leo pia ni siku yangu ya kuzaliwa. Naitakia nchi yangu kila la heri na fanaka, na Mweneyzi Mungu aiongoze nchi yetu kwenye njia njema, sambamba na kuiepusha na mabalaa. Kwa mujibu wa mambo yalivyo huko nyumbani, hali si ya kuridhisha sana. Basi ni muhimu tuitumie siku hii muhimu kuiombea nchi yetu kwa kila jema.

Kwangu, siku hii ya kuzaliwa ni fursa nyingine ya kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia kuongeza mwaka mwingine katika maisha yangu. Nawashukuru sana wazazi wangu Baba Mzee Philemon Chahali na mama yangu mpendwa, marehemu Adelina Mapango (we all miss you so much mom). Pia nawashukuru wanafamilia wenzangu, ndugu, jamaa na marafiki kwa mema yote waliyonifanyia. Natumaini mtaendeleo kuwa nami siku zote za uhai wangu.

Nwashukuru nanyi wasomaji wa blogu hii, marafiki zangu wapendwa ambao nawafahamu kwa kuangalia idadi ya wanaotembelea blogu hii. Japo pengine wengi wenu hatufahamiani personally, lakini mnapochukua muda wetu muhimu kunitembelea hapa, kuvumilia makelele yangu na 'upuuzi' wmingine ninaoandika, ni faraja kubwa mno kwangu. Nawashukuru kwa kuwa sehemu ya familia yangu kiuandishi.

Nimalizie kwa kumwomba Mwenyezi Mungu azidi kunijalia afya njema, maisha marefu, afya njema kwangu, familia, yangu, ndugu, jamaa na marafiki, na niwe na mafanikio katika kila jambo. Amen

5 Dec 2014


NIANZE kwa kuelezea kuhusu hatua mbili zilizochukuliwa na mamlaka za hapa Uingereza na jinsi zilivyobadili maisha kwa wakazi wengi wa nchi hii.
Lengo la kuelezea hatua hizo ni kuhusisha na tatizo kubwa linalokwaza utekelezaji wa sera na mipango mbalimbali huko nyumbani: ukosefu wa dhamira.
Hatua ya kwanza ilihusu dhamira ya serikali kuhamasisha wavuta sigara kuachana na tabia hiyo ambayo si tu ina gharama kifedha bali pia kiafya.
Kwa hapa Scotland, mwaka 2006 serikali ilipiga marufuku uvutaji sigara hadharani. Hatua hiyo, sambamba na mikakati mbalimbali ya kuwasaidia watu wanaotaka kuacha uvutaji wa sigara, imekuwa na mafanikio makubwa.
Mwaka jana, serikali ilitangaza sheria ya kuyataka maduka makubwa (supermarkets) yote kutuonyesha sigara katika maeneo yaliyotengwa kwa uuzaji wa bidhaa hiyo. Sambamba na hatua hiyo ni kutuonyesha bei za pakti za sigara hadharani.
Sheria hiyo itaanza kutekelezwa na maduka yote kuanzia Aprili mwakani. Hatua zote hizo ni utekelezaji wa mkakati wenye lengo la kuifanya Scotland kuwa ‘smoke-free’ kufikia mwaka 2034.
Hatua nyingine ya hivi karibuni ni ile ilivyoanza kutekelezwa Oktoba mwaka huu, ambapo kila biashara ya bidhaa imeagizwa kutoza ushuru wa pence 5 (takriban shilingi 136) kwa kila mteja atakayetaka mfuko wa kubebea bidhaa alizonunua.
Lengo la hatua hii ni kuhamasisha utumiaji tena wa mifuko iliyokwishatumika (re-use) na kupunguza takataka. Hatua hii imekuwa na mafanikio makubwa mno, kwani wateja wengi sasa wanakwenda madukani wakiwa na mifuko yao wenyewe ili kuepuka ushuru huo.
Kama nilivyotanabahisha mwanzoni, lengo la kuelezea kuhusu hatua hizo mbili ni kuzihusisha na tatizo linaloikabili nchi yetu la kukosa dhamira katika hatua mbalimbali tunazozichukua kwa manufaa ya jamii au Taifa kwa ujumla.
Wiki iliyopita tumeshuhudia sokomoko kubwa kuhusiana na skandali ya ‘Tegeta Escrow.’ Kwa kifupi, skandali hii ilihusu uchotwaji wa mabilioni ya shilingi katika akaunti ya Escrow ndani ya Benki Kuu ya Tanzania, katika mazingira yanayoashiria ufisadi.
Kamati husika ya Bunge chini ya uongozi wa Mbunge Zitto Kabwe ilifanya kazi kubwa ya kufuatilia suala hilo, na hatimaye kuwasilisha ripoti iliyotokana na uchunguzi wa Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu ya Serikali (CAG) na Taasisi ya Kupambana na Kuzuwia Rushwa (Takukuru).
Tarehe 26 ya mwezi uliopita yaweza kuingia katika historia ya taifa letu, ambapo kwa sisi tunaofuatilia masuala mbalimbali ya huko nyumbani kwa kutumia mitandao ya kijamii tulishuhudia kiu kubwa ya Watanzania kuhusu undani wa skandali hiyo ya Escrow hususan majina ya wahusika na hatua pendekezwa dhidi yao.
Kwa siku nne mfululizo, wengi wa Watanzania walionekana ‘kusahau takriban kila kitu’ ikiwa ni pamoja na ‘vipaumbele vyetu vya kawaida’ kama vile maendeleo ya ligi za soka barani Ulaya, na kuwekeza nguvu zao kufuatilia mjadala wa skandali hiyo huko Bungeni, Dodoma.
Hatimaye, Jumamosi iliyopita, ripoti hiyo iliridhiwa na wabunge wetu japokuwa wananchi wengi (angalau katika mitandao hiyo ya kijamii) wakibaki na kinyongo kidogo kutokana na Waziri Mkuu Mizengo Pinda ‘kuokolewa.’ Hata hivyo, kwa kiasi kikubwa, wengi wa waliokuwa wakifuatilia tukio hilo walionekana kuridhishwa na maamuzi yanayotaka mamlaka husika kufanya uchunguzi wa haraka na kuchukua hatua stahili dhidi ya wahusika.
Nisingependa kurejea yote yaliyojiri wakati wa mjadala huo mkali, lakini masuala muhimu yaliyojitokeza waziwazi ni pamoja na, kwanza, kuwapo baadhi ya wawakilishi wa wananchi ambao hawataki kabisa kusikia vilio vya wanaowawakilisha, na badala yake kutetea misimamo na maslahi yao binafsi.
Baadhi ya wabunge wa CCM, hususan wa kuteuliwa, walionekana kama ‘wametoka sayari nyingine’ kwa jinsi walivyosimama kidete kuwatetea watuhumiwa katika skandali hiyo.
Pili, na pengine hili ni la muhimu zaidi, ni jinsi tofauti za kiitikadi zilivyowekwa kando kwa kiasi kikubwa na wengi wa wabunge kuhakikisha kuwa maslahi ya umma na Taifa yanawekwa mbele, na hatimaye kufikiwa mwafaka wa ‘pande tatu,’ kwa maana ya CCM, Ukawa na Kamati husika ya Bunge. Tukio hili sio tu ni la kihistoria bali lina umuhimu wa kipekee.
Iwapo wanasiasa wetu wataendeleza ari hiyo ya kuweka mbele maslahi ya Taifa badala ya maslahi yao binafsi, au ya vyama vyao, basi kwa hakika twaweza kupiga hatua kubwa katika kukabili changamoto mbalimbali zinazoikabili Tanzania.
Hata hivyo, ukweli mchungu kuhusu hitimisho la suala hilo ni kwamba baadhi ya watuhumiwa ‘wameokolewa.’ Ikumbukwe kuwa taarifa zilizopatikana awali, na hatimaye kuwekwa hadharani na Mbunge Tundu Lissu ni uhusika wa IKulu, ambayo inaelezwa iliidhinisha malipo hayo kutoka katika akaunti ya Escrow huko Benki Kuu. Sambamba na hilo ni kauli za mara kwa mara za Waziri Mkuu Pinda kuwa fedha hizo si za umma.
Na kama kutonesha ‘kidonda kibichi,’ wakati anaahirisha kikao cha Bunge hilo, ambacho pamoja na mambo mengine, kilisomewa na kujadili ripoti kuhusu skandali hiyo ya Escrow, Pinda aligusia tena swali ambalo limeonekana kama ‘utetezi’ na ‘tuhuma’ kuhusu utoaji wa fedha hizo, yaani “je fedha hizo ni za umma?”
Watuhumiwa wanadai si za umma ilhali watuhumu, ikiwa pamoja na wananchi wengi, wanaamini kuwa fedha hizo ni za umma, na kitendo cha kuzitoa Benki Kuu ni cha kifisadi.
Na hapa ndipo maelezo niliyoyatoa hapo awali kuhusu hatua mbili zilizochukuliwa hapa Scotland yanapokuwa na umuhimu  kwa hali ya huko nyumbani. Kama kweli tungekuwa na dhamira ya dhati ya kupambana na ufisadi, hakukuwa na haja ya ‘kuchuja’ wahusika. Je, kwanini hoja iliyotolewa na Mbunge Lissu kuhusu kuhusika kwa Ikulu ilitelekezwa?
Japo wakati anarejea nyumbani kutoka Marekani kwa matibabu, Rais alieleza kuwa “hafahamu kwa undani kuhusu kilichokuwa kikiendelea Dodoma (kwa maana ya mjadala huo wa skandali ya Escrow), ukweli ni kwamba taasisi ya urais si mtu aitwaye Jakaya Kikwete pekee bali wasaidizi na taasisi mbalimbali kama vile Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Idara ya Usalama wa Taifa, nk.
Licha ya ukweli kwamba Rais alikwenda Marekani kwa matibabu, sitaki kabisa kuamini kuwa alikuwa hafuatilii kinachoendelea kuhusu skandali ya Escrow. Kama aliweza kusoma ‘meseji’ mbalimbali alizotumiwa na Watanzania kumtakia afya njema, ninaamini alipata muda pia wa kufahamishwa kinachoendelea huko nyumbani kuhusu sakata la Escrow.
Mbunge Lissu pia aligusia kuhusu utendaji kazi mbovu wa Idara yetu ya Usalama wa Taifa. Aliishutumu vikali huku akihoji ilikuwa wapi wakati ‘ufisadi wa Escrow’ ukitendeka.
Licha ya mchango wa mbunge huyo machachari kuhusu taasisi hiyo kutopewa uzito kabisa katika maazimio ya Bunge juu ya skandali ya Escrow, Kamati ya Zitto, kwa sababu ambazo si vigumu kwa sisi wengine kuzielewa, ilikwepa kuitwisha lawama Idara ya Usalama wa Taifa.
Licha ya kutoafikiana na hatua hiyo ya Kamati ya Zitto kutomgusa Rais Kikwete wala Idara ya Usalama wa Taifa, binafsi ninaamini kuwa hatua hiyo ilikuwa ya kiufundi zaidi kwa maana kwamba ya kuepusha kuwaunganisha CCM, ambayo ndio iliyotoa wengi wa wajumbe wa Kamati hiyo, kuipinga ripoti nzima.
Kama ambavyo CCM imefanikiwa kumwokoa Pinda, laiti Kamati hiyo ingemtuhumu Rais Kikwete na Idara ya Usalama wa Taifa basi huenda isingemudu japo kufikia hatua ya kujadiliwa.
Sasa matokeo yake tumefanya kile Waingereza wanaita to settle for less yaani angalau tumepata chochote kitu. Lakini msemo huo wa Kiingereza unaonya kuwa ‘when you settle for less, you end up getting even lesser than what you deserved’ (unapokubali kupewa kitu pungufu ili mradi upate tu, waishia kupata pungufu zaidi ya unachostahili).
Pengine Rais Kikwete atatekeleza maazimio yote ya Bunge. Pengine utekelezaji huo utafanyika mapema iwezekanavyo. Lakini ukweli utabaki kuwa licha ya skandali ya Escrow kuwa moja tu ya skandali nyingine kadhaa ambazo bado zinaitesa Tanzania yetu, na nyinginezo zinazoweza kuibuka huko mbele, hatujafanikiwa kukata mzizi wa tatizo la ufisadi ambalo kwa kiasi kikubwa limegubika utawala wa Rais Kikwete. Na kama nilivyotanabaisha katika makala iliyopita, Rais wetu ni mgumu katika kuchukua hatua stahili, na matokeo yake twajikuta kila mara tukirejea kulekule tulikotoka. Tunapiga hatua 50 mbele, baadaye twarejeshwa hatua 100 nyuma.
Kinachosababisha haya ni kile ambacho wenzetu hapa Scotland wamefanikiwa: si tu kuwa na sera au mipango mizuri, bali pia kuitafsiri katika vitendo.
Japo ningetamani sana kuona skandali ya Escrow kuwa ya mwisho angalau hadi Rais Kikwete atakapomaliza muda wake, ukweli kwamba kuna mabilioni ya fedha tuliyoibiwa na kufichwa kwenye akaunti za Benki huko Uswisi, sambamba na ‘uhalifu uliozoeleka’ wa biashara haramu ya madawa ya kulevya na ujangili, sintoshangaa tukikumbana na ‘Escrow nyingine’ hivi karibuni.
Nihitimishe makala hii kwa kukumbushia mambo haya: wenye ufahamu wanaelewa ukaribu uliopo kati ya Rais Kikwete na Waziri Muhongo (inaelezwa kuwa ndiye aliyemshawishi kutoka kwenye taaluma na kuingia kwenye siasa kwa uteuzi) wanaona ni mtihani mkubwa mno kwa Rais Kikwete kumtimua waziri huyo ambaye siku zote amesimama kidete kuwaaminisha Watanzania kuwa fedha za Escrow si za umma.
Kwa upande mwingine, kumwajibisha Mwanasheria Mkuu Werema kutamaanisha ‘kumweka huru’ mtu mwenye uelewa mkubwa wa ‘mambo mengi’ yaliyotokea, yanayotokea na yatakayotokea katika utawala wa Rais Kikwete.
Katika mazingira ya kawaida tu, si rahisi mtu ‘kujitenga’ na ‘mwandani’ wake, hasa ikizingatiwa kuwa ‘hasira za kutimuliwa’ zaweza kumshawishi kuweka hadharani mengi ya tusiyoyajua (kwa mfano majina ya walioficha fedha zetu kwenye mabenki ya Uswisi.)
La mwisho kabisa ni Singasinga. Bila haja ya kudadisi nani aliyemleta wala kujua washiriki wake wa kibiashara nchini Tanzania, ni muhimu mapendekezo ya kuchukua hatua kali za kisheria dhidi yake yakatekelezwa haraka pengine kabla ya hatua dhidi ya watendaji wa serikali waliohusishwa na skandali hiyo.
Ushauri wangu mwepesi ni kuwa huyo mtu atangazwe kuwa ‘persona non grata’ (mtu asiyetakiwa kuwapo katika nchi husika) mara moja.
Idara ya Usalama wa Taifa inafahamu bayana tishio la kiusalama linalosababishwa na kuwapo kwake, na huenda CCM pia yatambua madhara aliyosababisha mtu huyo kwa kilichokuwa chama tawala nchini Kenya, KANU. Atimuliwe.
Tanzania yetu ni kama nyumba zilizojengwa bonde la Jangwani (Dar), msimu wa kiangazi tupo salama, msimu wa mvua ukiwasili inakuwa tabu. Ikumbukwe kuwa hata Nabii Nuhu alijenga safina kabla gharika haijaanza. Tujipange kupambana na ‘Escrow nyingine’ sasa badala ya kusubiri hadi ziibuke.
INAWEZEKANA, TUKITIMIZA WAJIBU WETU IPASAVYO


Waingereza wana msemo ambao unatafsirika kwa Kiswahili kama "chuki ya pamoja ni mwanzo wa urafiki mkubwa." Kimahesabu kama A hapatani na B, na A anamchukia C kama ambavyo B anamchukia pia C, basi chuki ya A na B kwa C yaweza kuwa mwanzo wa wawili hao A na B kuwa marafiki wenye lengo la kumwangamiza C.

Binafsi, naomba kukiri kuwa kwa muda sasa nimekuwa siafikiani na mitizamo na mwenendo wa mwanasiasa mahiri wa upinzani, Zitto Kabwe. Siwezi kusema nina chuki dhidi yake bali mie sio miongoni mwa supporters wake.Pamoja na sababu nyingine, kubwa ni kile ninachokitafsiri kama mwanasiasa huyo kutanguliza mbele maslahi yake binafsi badala ya chama chake yaani Chadema. Kwa mtizamo wangu, mgogoro uliopelekea hatua ya Chadema kumvua madaraka Zitto ni matokeo ya 'imani potofu' kuwa kuna mwanasiasa anayeweza kuwa maarufu kuliko chama chake, Si kwamba haiwezekani kabisa kwa hilo kutokea lakini si kwa hatua waliyofikia Chadema hivi sasa.

Lakini lengo la makala hii si kumjadili Zitto wala ugomvi kati yake na Chadema. Ila nimegusia suala hilo kwa sababu nililazimika 'kurejesha urafiki' na mwanasiasa huyo, angalau kinadharia, wakati akifanya jitihada kubwa binafsi na kama mwenyekiti wa PAC kushughulikia ufisadi wa Tegeta Escrow. Kwa kutumia mfano huo hapo juu wa chuki za A kwa C na za B kwa C, na A ni Zitto, na B ni mie, huko C wakiwa mafisadi wa Escrow, basi 'urafiki' usingeepukika.

Hakuna Mtanzania atakayeshindwa kumpongeza Zitto na Kafulila pamoja na PAC kwa ujumla walivyofanya kazi kubwa na nzuri katika kushughulikia skandali hiyo. Nina imani hata wahusika wa ufisadi huo wa Escrow wanamkubali kwa jinsi alivyowakalia kooni...ALMOST.

Hata hivyo, mara baada ya kumalizika kwa 'timbwili' hilo la Escrow bungeni, nilitumiwa meseji na 'mjuzi mmoja wa mambo ya huko nyumbani' ambaye alidai kuwa pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na PAC, kuna 'mchezo mchafu' uliofanyika katika kufikia mwafaka miongoni mwa wajumbe, hususan wale wa kutoka CCM. Alidai kuwa kilichowezesha mwafaka huo kufikiwa ni pamoja na 'kumnusuru' Rais Jakaya Kikwete, ambaye kama Mbunge Tundu Lissu alivyobainisha bungeni, anatajwa kuhusika katika skandali hiyo. Kimsingi, hoja ya Lissu, ambaye pia aliilaumu Idara ya Usalama wa Taifa kwa kutowajibika ipasavyo katika mlolongo wa skandali mbalimbali zinazougubika utawala wa Rais Kikwet, iliuawa kimyakimya licha ya umuhimu wake mkubwa.

Hata hivyo, kwa uelewa wangu, jaribio lolote la kumhusisha Rais Kikwete na skandali hiyo hata kama ushahidi upo lingepelekea mparaganyiko mkubwa katika kamati hiyo ya Zitto. Na kama tulivyoshuhudia 'makada' wa CCM huko bungeni walivyopigana kufa na kupona hadi Waziri Mkuu Mizengo Pinda akanusuriwa, kwa hakika ishu ya Kikwete kuhusishwa na Escrow ingepelekea bunge hilo kuvunjika pasi kufikia hitimisho.

Lakini what if mkakati huo wa 'kumnusuru Rais Kikwete' unabeba mengi zaidi ya tunavyodhani? 


Kwa kifupi, tume-settle for less. Na Waingereza wana msemo unaotahadharisha kuhusu ku-settle for less, ambapo wanasema 'pindi ukikubali kupokea pungufu ya unachostahilki basi hatimaye utaishia kupokea pungufu zaidi ya kile ulichostahili awali.' Japo ni mapema kuhitimisha kwamba 'tumeingizwa mkenge,' lakini ukimya wa Rais Kikwete katika kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu Escrow umeanza kuzua wasiwasi.

Na 'kigugugmizi' kinachomkabili Rais Kikwete kina sababu kadhaa za wazi. Kwa mfano, kumtimua Mwanasheria Mkuu Jaji Werema kunaweza kupelekea kuzuka kwa skandali nyingine iwapo Jaji huyo ataamua 'mmemwaga mboga, na mie namwaga ugali' kwa maana anajua mengi yaliyojiri na yanayojiri katika utawala wa Rais Kikwete. Japo si kwamba haiwezekani kumtimua na kisha kumfunga mdomo, lakini historia ya wanasheria wakuu huko nyuma inapaswa kutukumbusha jinsi 'wanavyobebwa' kwa minajili ya 'kutotengeneza uadui na mtu anayejua siri nyingi.'

Kwa upande wmingine, ni muhimu kukumbuka kuwa kimsingi Rais Kikwete ndo aliyemleta Profesa Muhongo katika frontline politics. Hawa ni marafiki wa karibu. Na hadi sasa Muhongo ameendeleza jeuri yake ya kisomi na kusisitiza kuwa fedha za Escrow si za umma. Msimamo huo pia washikiliwa na Waziri Mkuu Pinda. Je kuna anayefahamu msimamo wa Rais Kikwete? Maelezo yanaonyesha kuwa yeye aliridhia malipo ya Escrow kufanyika. Je amebadili mawazo na kutambua kuwa hilo lilikuwa kosa?

Lakini wakati tayari tunafahamu majina mengi ya walionufaika na mgao wa Escrow kupitia Benki ya Mkombozi, inadaiwa kuwa mgao mkubwa zaidi uliopitia Benki ya Stanbic ulihusisha vigogo kadhaa lakini hadi muda huu hakuna jina hata moja lililowekwa hadharani. So far, gazeti la Raia Mwema limeripoti kuwa mke wa kigogo momja mwandamizi huko Ikulu alikatiwa shilingi bilioni 5. Sasa huhitaji kujua hesabati vizuri kubashiri kwamba kama mke wa kigogo alikatiwa mbilioni tano, mumewe alipewa kiasi gani? 

Hayo yote tisa, kumi ni kauli niliyokumbana nayo muda mfupi uliopita, na ambayo kwa hakika ndio iliyonisukuma kuandika makala hii. Kauli hiyo ni ya Jaji Mkuu Chande ambayo kimsingi inaharibu mwenendo wa kesi yoyote itakayofunguliwa dhidi ya wahusika wa ufisadi wa Escrow. Nimeinukuu kwa picha hapa chini.


Je Jaji Mkuu alikuwa anatoa tu tahadhari au alikuwa akifikisha ujumbe mahsusi kwamba hata tukiwapeleka mahakamani wahusika wa Escrow, utetezi wao upo bayana...kwamba walishahukumiwa bungeni. Na kama Jaji Mkuu 'hakutumwa' basi kwa hakika amewapatiwa washtakiwa-watarajiwa ushauri mzuri wa bure kisheria kuhusu jinsi ya kupambana na kesi yoyote watakayofunguliwa kuhusisna na suala hilo: wajitetee kuwa walishahukumiwa na bunge, na mawakili waoa waweza kutumia kauli hiyo ya Jaji Mkuu kama supporting evidence.

Anyway, pengine ni mapema mno kuhukumu lakini kama ambavyo Mzee Warioba alivyoonyesha mapungufu ya taarifa ya PAC na maazimio ya bunge kuhusu skandali ya Escrow, sintomshangaa mtu yeyote atakayeanza kupatwa na wasiwasi kuwa tumeingizwa mkenge...TENA.


Sijui msomaji mepndwa unaonaje. 





Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.