Showing posts with label Habari. Show all posts
Showing posts with label Habari. Show all posts

10 Apr 2015



NIANZE makala hii kwa kuomba radhi kwa makala zangu ‘kupotea’ kwa wiki mbili mfululizo. Hali hiyo ilitokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu.
Pia ningependa kutoa salamu za pole na rambirambi kwa ndugu zetu wa Kenya kufuatia shambulio kubwa la kigaidi lililotokea huko Garissa na kuuwa watu kadhaa.Ugaidi umeendelea kuwa moja ya matishio makubwa kwa usalama wa binadamu.
Wakati tukiungana na majirani zetu wa Kenya katika kipindi hiki kigumu, kuna dalili na sababu kadhaa za kiintelijensia na kimazingira zinazonipa wasiwasi kwamba Tanzania yetu inaweza kukumbwa na shambulio la kigaidi huko mbeleni (Mola aepushie). Hapa chini, ninabainisha dalili/ sababu hizo.
Tukio la ugaidi Garissa, nchini Kenya:
Wiki iliyopita, magaidi wa Al-Shabaab walifanya shambulio kubwa la ugaidi katika mji wa Garissa, uliopo mpakani mwa Kenya na Somalia.Shambulio hilo limepelekea vifo vya watu takriban 150 huku taarifa mbalimbali zikionyesha uwezekano wa kuwepo idadi kubwa zaidi ya waliouawa.
Awali, nilikuwa upande wa watetezi wa serikali ya Kenya na vyombo vya usalama vya nchi hiyo katika lawama kwamba walizembea kuchukua tahadhari. Hoja yangu kuu ilikuwa kwamba kupewa taarifa kuhusu ugaidi ni kitu kimoja, kuweza kuzifanyia kazi taarifa hizo na kuweza kuzuwia ugaidi ni kitu kingine kabisa.
Hata hivyo, utetezi huo umepungua baada ya kupatikana taarifa mbalimbali zinazoashiria mapungufu makubwa ya serikali ya Kenya na taasisi za Usalama nchini humo kukabiliana na tetesi walizopewa kuhusu uwezekano wa shambulio hilo la kigaidi.
Tukiweka kando kilichojiri nchini Kenya lakini tukitilia maanani ukweli kuwa nchi hiyo ilitahadharishwa kabla ya tukio hilo, kwa Tanzania hali ni tofauti. Hadi sasa hakuna taarifa rasmi ya uwezekano wa kutokea shambulio la ugaidi.
Hata hivyo, ni muhimu kutambua kuwa Kenya ina ushirikiano mkubwa zaidi na taasisi za kiusalama za mataifa makubwa zaidi ya Tanzania, hasa ikizingatiwa kuwa Marekani, kwa mfano, ina kituo chake cha kijeshi nchini humo (Manda Bay)
Kwa maana hiyo, tahadhari ya Wamarekani kwa Kenya sio tu kwa maslahi ya Kenya bali ya Wamarekani pia.
Hitimisho: Kwa kufanikiwa kufanya shambulio kubwa kabisa nchi Kenya, ikiwa ni takriban mwaka na nusu baada ya kufanya shambulio jingine la ugaidi kwenye supamaketi ya Westgate jijini Nairobi, magaidi wa Al-Qaeda wanaweza kushawishika kupanua kampeni yao ya uharamia hadi Uganda (ambako tayari kuna tishio kama ninavyoeleza hapo chini) na hata Tanzania (kwa sababu nitazobainisha mbeleni katika makala hii)
Uwezekano wa shambulio la kigaidi Uganda:
Machi 25 mwaka huu, Marekani ilitoa tahadhari kwa Uganda kuhusu uwezekano wa shambulio la kigaidi nchini humo. Kama ilivyo kwa Kenya, Marekani ina maslahi yake nchini Uganda ambako inarusha ndege zake za upelelezi (PC 12) kutoka Entebbe, Kwa hiyo usalama kwa Uganda una maslahi kwa Marekani pia.
Hitimisho: Iwapo Al-Shabaab watafanikiwa kutimiza uovu wao kuishambulia Uganda (Mungu aepushe hili), wanaweza kupata motisha wa kutanua zaidi kampeni yao hadi Tanzania hasa kwa kuzingatia kuwa kundi hilo la kigaidi linaziona nchi hizi tatu kama kikwazo kikubwa kwa uhai wake.
Shaka ya ugaidi nchini Tanzania:
Moja ya matatizo makubwa ya kufahamu ukubwa au udogo wa tishio la ugaidi nchini Tanzania ni siasa. Kwa muda mrefu, chama tawala CCM kimekuwa kikiutumia ugaidi kama kisingizio cha kudhibiti vyama vya upinzani na baadhi ya viongozi wake. Kwa minajili hiyo, hata serikali ikitoa taarifa sahihi kuhusu uwezekano wa tishio la ugaidi, kuna uwezekano wa wananchi wengi kudhani hiyo ni siasa tu.
Kana kwamba hiyo haitoshi, mwaka huu Tanzania itafanya uchaguzi mkuu wa Rais na wabunge hapo Oktoba. Japo haijazoeleka sana, historia inaonyesha kuwa angalau katika uchaguzi mkuu mmoja uliopita zilisikika taarifa za 'tishio la usalama' kutoka kwa nchi jirani. Mbinu hii hutumiwa na vyama tawala kujenga hofu ya kiusalama kwa wapigakura, na kuwaunganisha chini ya mwavuli wa chama kilichopo madarakani. Kwa mantiki hiyo, iwapo kutakuwa na taarifa za tishio la ugaidi, yayumkinika kuhisi baadhi ya wananchi wakatafrisi kuwa ni mbinu tu ya CCM kuelekea kwenye uchaguzi mkuu.
Lakini tatizo kubwa zaidi kwa sasa ni imani ndogo ya wananchi kwa serikali ya Rais Jakaya Kikwete na nyingi ya taasisi za serikali yake. Uhaba huo wa imani unatokana na mchanganyiko wa hisia za ushahidi wa matukio yaliyopita. Kutokana na kuandamwa mno na kashfa za ufisadi, kumeanza kujengeka imani miongoni mwa Watanzania kuwa serikali yao ni ya kifisadi pia.
Matumizi mabaya ya 'taarifa za kiintelijensia' yamewafanya Watanzania wengi kuwa na hisia kuwa 'taarifa za intelijensia' ni mbinu ya serikali kuwadhibiti. Mara kadhaa, Jeshi la Polisi limekuwa likipiga marufuku maandamano ya kisiasa au kijamii kwa kisingizio cha 'taarifa za kiintelijensia'.
Hivi karibuni, zilipatikana taarifa za mapigano makali kati ya jeshi la polisi wakishirikiana na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) dhidi ya 'magaidi' kwenye mapango ya Amboni mjini Tanga. Mchanganyiko wa taarifa za kukanganya na imani haba ya wananchi kwa jeshi hilo vilipelekea tukio hilo kuonekana kama 'mchezo wa kuigiza'.
Lakini licha ya kasoro hizo zinazoihusu serikali na taasisi zake, kuna tatizo jingine linalohusu vyombo vya habari vya nchini. Utitiri wa magazeti ya udaku na uhaba wa uandishi wa kiuchunguzi katika 'magazeti makini' umekuwa ukichangia mkanganyiko katika kubaini ukweli na porojo. Mfano mzuri ni tukio hilo la Amboni ambalo kwa kiasi flani liligeuka kama mfululizo 'series' ya mchezo wa kuigiza, huku magazeti ya udaku yakiwa na 'habari' nyingi zaidi ya 'magazeti makini.'
Hali hiyo yaweza kuwa inachangiwa na mahusiano hafifu kati ya taasisi za dola na vyombo vya habari, sambamba na mazoea ya taasisi hizo kutoa tu taarifa pasipo kuruhusu maswali kutoka kwa wanahabari. Ukosefu wa taarifa sahihi, sambamba na ugumu wa kupata taarifa hizo huchangia 'udaku' kuziba ombwe husika.
Tukiweka kando kasoro hizo hapo juu, hadi sasa kuna mambo yafuatayo ambayo yanaweza kuwashawishi magaidi kuvamia Tanzania.
1. Mgogoro wa muda mrefu kuhusu uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi
Japo hadi muda huu suala hili limeendelea kuwagawa Watanzania kwa njia za mijadala na kwa amani, yayumkinika kuhisi kuwa magaidi wanaweza kulitumia kama kisingizio cha kuishambulia Tanzania.
Cha kutia hofu ni ukweli kwamba si tu suala hili limedumu kwa muda mrefu, hasa baada ya chama tawala CCM kuahidi katika ilani yake ya Uchaguzi Mkuu mwaka 2005 kuwa itaanzisha mahakama hiyo lakini imeshindwa kufanya hivyo hadi leo, bali pia uamuzi usio wa busara wa kuupeleka bungeni Muswada wa Uanzishwaji Mahakama ya Kadhi kisha kuuondoa.
Kana kwamba hiyo haitoshi, majuzi Rais Kikwete alikaririwa akidai kuwa serikali haina mpango wa kuanzisha mahakama hiyo, na badala yake jukumu hilo linabaki kwa Waislamu wenyewe. Haihitaji uelewa wa sheria kujiuliza kwamba kama suala hilo lilikuwa la Waislamu wenyewe, lilipelekwa bungeni kwa minajili gani?
Licha ya mjadala huo wa uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi kuendelea kwa amani, mjadala kuhusu suala hilo umewagawa viongozi wa dini (Wakristo na Waislamu) na kwa kiasi flani umerejesha mgogoro kati ya baadhi ya viongozi wa Kiislam na serikali, sambamba na kuleta sintofahamu miongoni mwa baadhi ya wanasiasa.
Yayumkinika kuhisi kuwa magaidi wanaweza kutumia ‘mgogoro’ huo kama kisingizio cha kufanya uovu wao. Na hii ni juu ya malalamiko ya muda mrefu kuwa Waislam wamekuwa wakibaguliwa na serikali huku Wakristo wakionekana kupendelewa. Uzoefu unaonyesha kuwa vikundi vya kigaidi vya kimataifa vina kasumba ya kuteka hoja za ndani ya nchi na kuigeuza yao, kwa kisingizio cha kupigania Uislam.
2. Vitisho bayana kutoka kwa watu wanaodai ni magaidi.
Hivi karibuni ilipatikana video huko nyumbani ambapo mtu mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Kaisi Bin Abdallah alidai kuwa kundi lao limekuwa na mafanikio katika ugaidi wa kudhuru polisi na vituo vya polisi.
Licha ya 'mapungufu kadhaa' katika video hiyo, ambayo yanaweza kutupa imani kuwa ni porojo tu, yawezekana tishio lililo kwenye video hiyo ni la kweli. Na hili ni moja ya matatizo ya kukabiliana na tishio la ugaidi: kuchukulia taarifa kuwa ni za kweli au za kupuuza.
Hofu kuhusu uwezekano wa matukio ya ugaidi nchini Tanzania ilithibitishwa na kauli ya hivi karibuni ya Rais Kikwete kuwa mashambulizi ya hivi karibuni dhidi ya vituo vya polisi katika maeneo mbalimbali nchini humo yana uhusiano na ugaidi, japo hakubainisha iwapo kuna uhusika wa makundi ya kigaidi ya kimataifa au la.
3. Taarifa za kimataifa:
Hadi muda huu hakuna taarifa za moja kwa moja zinazoashiria uwezekano wa tukio la ugaidi nchini Tanzania. Hata hivyo, bado kuna hali ya tahadhari ya wastani kuhusu uwezekano wa shambulio la kigaidi.
Wakati serikali ya Canada inaeleza kuwa haina 'ushauri unaohusu taifa (Tanzania) zima, inawashauri raia wake kuchukua tahadhari kubwa kuhusiana na ugaidi.
Kwa upande wake, serikali ya Uingereza inatoa angalizo la jumla tu japo inatahadharisha kuhusu tishio la ugaidi wa Al-Shabaab kwa eneo la Afrika Mashariki (ikiwa ni pamoja na Tanzania). Serikali ya Marekani inatoa ushauri wa jumla tu kwa kurejea matukio ya uvunjifu wa amani huko nyuma.
Hata hivyo, ripoti iliyotolewa Jumamosi iliyopita na taasisi ya HTH Worldwide kuhusu ‘hatari’ (risks) zinazoikabili Tanzania, ugaidi unatajwa kuwa ni tishio la kuaminika, japo uwezekano wa kutokea shambulizi la ugaidi ni wa wastani.
Pengine taarifa ya kuogofya zaidi ni ile iliyobainisha uwepo wa jitihada za kundi la kigaidi la ISIS kutaka kujiimarisha katika eneo la Afrika Mashariki, ikiwa ni pamoja na Tanzania. Kwa mujibu wa taarifa hiyo, ISIS inajaribu kujenga ushirikiano na Al-Shabaab kwa minajili ya kuwa na influence katika eneo la Afrika Mashariki.
Taarifa zaidi za kiintelijensia zinabainisha uwepo wa kikundi cha Al-Hijra nchini Tanzania, ambacho kinatajwa kama ‘tawi’ la Al-Shabaab nchini Kenya. Kwa mujibu wa taarifa hizo, kikundi hicho kinakadiriwa kuwa na wafuasi takriban 1,000.
Inaelezwa kuwa kikundi hicho kinafadhiliwa na Waislamu wa nje wa madhehebu ya Wasalafi (Salafist). Habari zaidi zinabainisha kuwa malengo ya kikundi hicho ni kuanzisha jihadi nchini Kenya na Tanzania. Uwepo wa kikundi hicho unadaiwa kusaidiwa na kikundi kingine cha Al-Muhajiroun ambacho kinatajwa kuwa na mahusiano na kikundi kingine cha kigaidi cha Al-Qaeda.
Kadhalika, majuzi zimepatikana taarifa kutoka Kenya kuhusu mwanamke mmoja wa Kitanzania aliyekamatwa na wenzie wawili Wakenya wakijaribu kwenda Somalia kuwa wenza wa magaidi wa Al-Shabaab.
Tukio hilo linaakisi kinachotokea katika nchi mbalimbali za huku Magharibi ambapo mabinti kadhaa wamekuwa wakitorokea Syria kwenda kuwa 'wenza' wa magaidi wa ISIS.
Vilevile, taarifa zilizopatikana muda mfupi kabla sijaandika makala hii zinaeleza kuwa mmoja wa wahusika wa shambulio hilo la kigaidi nchini Kenya ni Mtanzania. Haihitaji uelewa mkubwa wa intelijensia kutambua kuwa kama baadhi ya Watanzania wenzetu wanaweza kwenda kufanya ugaidi nje ya nchi, wanaweza pia kufanya ugaidi ndani ya nchi.
Hitimisho:
Ni vigumu kwa kuwa na hakika ya asilimia 100 iwapo magaidi watafanya shambulio au la. Kwa upande mmoja, magaidi wana muda wote wanaohitaji kabla ya kutimiza azma yao, yaani wanaweza kusubiri kwa muda mrefu, ilhali vyombo vya dola havina faida hiyo kwani vinatakiwa kuwa makini muda wote.
Kuna msemo maarufu kuhusu ugaidi, kwamba wakati magaidi wanahitaji DAKIKA MOJA TU kutimiza uovu wao, vyombo vya usalama vinahitaji KILA SEKUNDE YA DAKIKA kuwazuia magaidi husika.
Na japo uwepo wa taarifa za uhakika kuhusu uwezekano wa shambulio la kigaidi unaweza kusaidia jitihada za kukabiliana na magaidi husika, ukweli mchungu ni kwamba, kuwa na taarifa ni kitu kimoja, uwezo wa kuzitumia taarifa hizo ni kitu kingine.
Wakati huu tunaungana na wenzetu wa Kenya kulaani unyama wa Al-Shabaab, ni muhimu kuchukua tahadhari mahususi ili kuweza kukabiliana na uwezekano wa magaidi hao kushambulia Tanzania.
La muhimu zaidi ni umoja na mshikamano, ambao kwa hakika unapotea kwa kasi, na haja ya haraka kwa serikali kurejejesha imani ya wananchi kwake. Kingine ni umuhimu wa kuweka kando siasa katika masuala nyeti kama haya..
Kubwa zaidi ya yote ni la kitaalamu zaidi. Wakati serikali ya Tanzania imekuwa ikitegemea zaidi misaada ya kimataifa katika kuiimarisha kiuwezo Idara ya Usalama wa Taifa, ni muhimu jitihada za ndani pia zielekezwe katika kuijengea uwezo wa kukabiliana na matishio mbalimbali ya usalama wa taifa letu, ikiwa ni pamoja na hilo la ugaidi.
Kwa uelewa wangu, uwezo wa vitengo vya kuzuwia ugaidi na kitengo cha kupambana na ujasusi unaathiriwa na mapungufu ya kimfumo na kisera, sambamba na nafasi ya maafisa wa Idara hiyo kwenye balozi mbalimbali za Tanzania nje ya nchi 'kubweteka' na hisia ya teuzi zinazodaiwa kufanywa kwa misingi ya undugu, urafiki au kujuana.
Lakini changamoto kubwa zaidi kwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa ni kurejesha imani kwa Watanzania. Nimeshawahi kuandika mara kadhaa kwamba kushamiri kwa ufisadi huko nyumbani kunachangiwa na udhaifu wa taasisi hiyo nyeti.
Zama za Idara hiyo ‘kuogopwa’ zimegeuka na kwa kiasi kikubwa taasisi hiyo, ambayo moja ya mafanikio yake makubwa huko nyuma yalikuwa kusimama imara dhidi ya njama na hujuma za utawala wa Makaburu, kwa sasa inaonekana kama sehemu ya mfumo wa kifisadi. Ili Idara yetu ya Usalama wa Taifa iweze kukabiliana na tishio hili la ugaidi inabidi iaminike kwa wananchi.
Mwisho, tishio hili la ugaidi sio la kufikirika. Lipo, na kwa bahati mbaya, mazingira ya kulirutubisha yapo pia. Japo si rahisi kuzuia ugaidi kwa asilimia 100, mikakati madhubuti ya kiintelijensia hususani katika kukabili ugaidi (counterterrorism) inaweza kuwakwaza magaidi kufikiria kuivamia nchi yetu

1 Apr 2015


Pengine kabla ya kueleza kwanini naunga mkono muswada wa kudhibiti uhalifu wa mtandaoni (The Cyber Crime Bill),ni vema nikaeleza background yangu kidogo ili kutanabaisha sio tu ninavyothamini uhuru wa habari bali pia nilivyonufaika nao.

Nilianza uandishi kwenye vyombo vya habari mwaka 1996,mwaka mmojabaada ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.Aliyenishawishi kuingia kwenye fani hiyo ni mwanahabari mkongwe, Albert Memba.Nikiwa mwaka wa pili, na yeye mwaka wa kwanza chuoni hapo, Memba aligundua kuwa 'utani wa busara' niliokuwa nikifanya eneo la 'kijiweni' (nyuma ya ukumbi wa mihadhara ya Sanaa -ATB,mkabala ya Maktaba Kuu ya chuo hicho) ungeweza kunipatia fursa katika gazeti 'lisilo serious.'

Nikafuata ushauri wake na kuanza kuandika 'unajimu wa utani' katika gazeti la 'udaku' la SANIFU lililokuwa linamilikiwa na kampuni ya Business Times, wachapishaji wa gazeti la Majira.Sanifu ni gazeti la kwanza kabisa la udaku Tanzania. Gazeti hilo lilinipa safu (column) niliyoipa jina 'nyota za Ustaadh Bonge.' Nyota hizo licha ya kutumia alama za unajimu kama 'Mshale' (Sagittarius), Ng'e (Scorpio),nk hazikuwa na ukweli wowote zaidi ya burudani. Kwa mfano, ungeweza kukutana na utabiri 'wa kisanii' kama huu: "Wiki hii utakumbwa na nuksi itakayokuletea ulaji mbeleni.Mwanao atagongwa na gari la ubalozi wa Marekani,lakini hatoumia.Ubalozi huo utakufidia kwa kukupatia viza ya kuishi Marekani.Usimzuwie mwanao kucheza barabarani."

Sio siri, watu wengi tu walivutiwa na 'Nyota za Ustaadh Bonge' na hii ilipelekea mie kupewa jina la utani la Ustaadh Bonge kwa muda wote niliokuwa hapo Mlimani (UDSM), na hadi leo, baadhi ya marafiki zangu wananiita Bonge.

Baada ya gazeti la Sanifu 'kufa' nilijiunga na gazeti jingine la udaku la Komesha, na baadaye Kasheshe, magazeti yaliyokuwa yanamilikiwa na kampuni ya IPP. Huko nako niliendeleza safu ya 'Nyota za Ustaadh Bonge.'

Hatimaye niliamua kuachana na magazeti ya udaku na kuhamia kwenye magazeti yenye 'serious news.' Nikafanikiwa kupata safu kwenye gazeti la KULIKONI,na safu hiyo ndio iliyopelekea jina la blogu hii yaani KULIKONI UGHAIBUNI ambalo lilikuwa jina la safu yangu katika gazeti hilo.Lengo la awali la blogu hii niliyoianzisha mwaka 2006 lilikuwa kuwapatia fursa wasomaji wa gazeti la Kulikoni walio nje ya Tanzania kusoma makala zangu kwa vile gazeti hilo halikuwepo mtandaoni.

Ni katika uandishi wa makala katika gazeti la Kulikoni ndipo nilipojitengenezea matatizo makubwa baada ya kuandika makala moja mwishoni mwa mwezi Oktoba 2006 ambapo nilikemea jitihada za aliyekuwa Waziri Mkuu wakati huo, Edward Lowassa, kukwamisha mjadala wa sakata ya Richmond. Makala hiyo ilipelekea Press Secretary wa Lowassa, Said Nguba, kunikaripia vikali hadharani. Mwendelezo wa sakata hilo hatimaye ulipelekea mwisho wa ajira yangu serikalini mwaka 2008.

Baadaye nikapewa safu katika gazeti la MTANZANIA,ambapo safu yangu ilijulikana kama MTANZANIA UGHAIBUNI. Lilipoanzishwa jarida la RAIA MWEMA, nikafanikiwa kupata safu, ambayo niliita RAIA MWEMA UGHAIBUNI, ambayo imedumu kwa miaka kadhaa hadi hivi leo.

Kwahiyo kwa kuangalia background hii utabaini kuwa sio tu nimeutumia vema uhuru wa habari bali pia nimenufaika nao vya kutosha.Nitakuwa mtu wa mwisho kuwa kikwazo cha uhuru huo kwani nami ni mnufaika mkubwa.

Nirejee kwenye mada halisi ya makala hii.Sababu kuu zinazonifanya niunge mkono muswada wa kudhibiti uhalifu wa mtandaoni ni TATU:

Kwanza, KITAALUMA/KITAALAM: Kwa zaidi ya miaka 10 huko nyuma, nilisomea na hatimaye kufanya kazi katika sekta ya usalama. Japo kimsingi kwa sasa si mwajiriwa katika taasisi ya usalama, nina interest kubwa kuhusu stadi na taaluma hiyo, ndani na nje ya Tanzania. Licha ya kujihusisha na usalama kwa maana ya intelijensia, pia nina interest kubwa kuhusu usalama wa mtandaoni hususan uhalifu wa mtandaoni (cybercrime). 

Sambamba na hilo, nimekuwa nikiutumia sana mtandao kwa minajili ya kupashana habari.Licha ya blogu hii, nimekuwa nikiweka mabandiko katika mitandao mingine ya kijamii kama vile Tumblr, Google+, Facebook, Instagram, Pinterest na hata Jamii Forums. Kutokana na uwepo wangu mkubwa mtandaoni, nimelazimika kufuatilia kwa karibu umuhimu wa usalama mtandaoni ikiwa ni pamoja na njia na nyenzo za kujikinga na wahalifu wa mtandaoni, sambamba na kuhabarisha masuala mbalimbali yanayohusiana na suala hilo.

Vilevile, kwa miaka ya hivi karibuni nimepata interest mpya ya software hususan za simu, kwa maana ya maendeleo na matumizi ya apps mbalimbali, pamoja na masuala ya teknolojia kwa ujumla.Katika hilo, nimelazimika pia kufuatilia usalama wa software mbalimbali, za kompyuta na simu.

Kwahiyo, uzoefu wangu mdogo kitaaluma/kitaalam unanituma kuunga mkono umuhimuwa muswada huo hasa kwa vile suala la kompyuta kwa ujumla bado ni geni kwa Watanzania wengi, na hiyo inaota fursa kwa wahalifu wa mtandaoni kufanya hujuma zao kirahisi.Lakini pia hali hiyo inapelekea matumizi yasiyofaa ya teknolojia hiyo ngeni.

Kiintelijensia, kama ilivyosikika hivi karibuni, kuna jitihada za makundi ya kigaidi ya ISIS na Al-Shabaab kufanya hujuma eneo la Afrika Mashariki ikiwamo Tanzania. Kwa bahati mbaya, mtandao umekuwa nyenzo muhimu ya vikundi vya kigaidi, hususan ISIS, katika harakati zao za kidhalimu. Na hivi karibuni tumesikia matukio mbalimbali yanayoelezwa kuwa ya kigaidi huko nyumbani. Hatuwezi kupuuzia taarifa hizi kwa sababu ugaidi, kama ilivyo kifo au tukio la wizi/ujambazi, hausubiri kualikwa.Unatokea tu. Kwahiyo ni muhimu kuchukua hatua za tahadhari ikiwa ni pamoja na kudhibiti matumizi ya kompyuta kwa minajili ya kufanya uhalifu. Naomba kusisitiza kuwa huu ni mtizamo wa kitaalam (kiinteliujensia) zaidi, na pengine si rahisi sana kueleweka.

Pili, KIJAMII: Ni ukweli usiopingika kuwa Tanzania yetu inaweza kuwa inashika nafasi ya juu kabisa katiika matumizi yasiyofaa ya mtandao.Ninaamini kuwa wengi wetu tumeshuhudia utitiri wa blogu za ngono mtandaoni. Ashakum si matusi, uki-Google 'picha za uchi' utakumbana na mlolongo wa mambo yasiyoendana na mila na desturi zetu.

Kama kuna sehemu inayotoa ushahidi mkubwa wa matumizi mabaya ya mtandao kwa Tanzania yetu basi ni INSTAGRAM.Huko imekuwa 'dunia uwanja wa fujo.' Kama si mzoefu wa matusi basi dakika chache tu katika mtandao huo utakutana na kila aina ya matusi. Wenyewe wameanzisha 'timu' za kusapoti au kupinga watu flani maarufu, na kwa hakika lugha inayotumika huko inachefua. Busara pekee hazitoshi kuwadhibiti watu hawa.Dawa pekee ni kuwa na sheria, sio tu ya kuwakumbusha umuhimu wa kuzingatia maadili bali pia kuwazuwia kuendeleza maovu yao.Ifike mahala, kabla mtu hajabandika picha za uchi ajiulize mara mbili iwapo hatochukuliwa sheria.

Matumizi ya simu za kisasa zenye kamera yamechangia 'kumfanya kila mwenye simu kuwa paparazi,' na katika hili, tumekuwa tukishuhudia picha zisizofaa kabisa mitandaoni.Hivi ni mara ngapi tumekwazwa na picha za maiti kwenye mitandao ya kijamii? Ni mara ngapi tumeitaka serikali kuchukua hatua dhidi ya uhuni wa kubandika picha zisizofaa mtandaoni? Naam, serikali imesikia kilio chetu kwa kuleta muswada wa kuzwia uhalifu wa mtandaoni ili kupata sheria itakayosaidia angalau kupunguza kadhia hiyo inayokera wengi.

Pia kuna blog zisizo za picha za ngono lakini zinazosababisha utengano mkubwa katika jamii. Ukimtkana mtu kwa mdomo unaweza kusahau na hata huyo aliyetukanwa anaweza kusahau, lakini mtandao wa kompyuta (internet) hausahau kitu. Uki-Google jina langu, moja ya mambo utakayokutana nayo ni 'ugomvi' wangu wa zamani sana na gazeti moja huko Tanzania uliotokana na mimi kulilaumu kwa kutumia picha za uongo kuhalalisha habari waliyochapiusha.Japo ugomvi huo uliisha miaka mingi iliyopita na wahusika ni marafiki zangu kwa sasa, na tumeshasdahau yaliyopita, lakini internet bado inakumbuka.

Sasa blogu zinazoendekeza matusi, kuchafuana, uzushi na vitu kama hivyo sio tu zinawathiri wahanga kwa muda huo wa tukio lakini zinaweka kumbukumbu ya milele mtandaoni...kwa sababu mtandao hausahau kitu. Tuendelee kuvumilia uhuru huu usio na ukomo wa kumchafua mtu yeyote kwa vile tu mlikorofishana? 

Baba wa Taifa aliwahi kutuusia kuwa "Uhuru bila utii ni ujinga" na "uhuru usio na mipaka ni uwendawazimu." Sasa pasipo sheria ya kudhibiti ujinga na uwendawazimu huu unaotokana na dhana fyongo kuwa 'hakuna anayeniona ninapobandika mabaya mtandaoni' tutaendelea kuumizana.

Tatu, sababu BINAFSI: Japo sitaki kuwa mbinafsi kwa maana ya 'kuunga mokono muswada huu kwa sababu mie pia ni mhanga' lakini pia sitaki kuwa mnafiki kwa kukwepa ukweli kwamba nimeshawahi kuwa mhanga wa matumizi mabaya ya uhuru mtandaoni. Mfano mmoja halisi ni kilipotokea kifo cha binti mmoja aliyekuwa miongoni mwa watumiaji mahiri wa mtandao wa kijamii wa Twitter, Marehemu Betty Ndejembi (Mungu aiweke roho yake mahali pema peponi). Kwa vile kabla ya tukio hilo la kusikitisha nilikuwa nikihamasisha upinziani dhidi ya unyanyasaji mtandaoni, kifo cha marehemu Betty kilinipa changamoto mpya, hasa ikizingatiwa kuwa siku chache kabla ya kukutana na mauti, binti huyo alinyanyaswa vya kutosha huko Twitter. Kwahiyo haikuwa jambo la kushangaza nilipoungana na baadhi ya wanaharakati kutumia hashtag #StopCyberbullying.

Lakini kwa sababu ambazo hadi leo sizielewi, lilijitokeza kundi katika mtandao huo sio tu kupambana na jitihada hizo za kukemea unyanyasaji mtandaoni bali pia kunichafua kwa maana ya jitihada kuonyesha kuwa eti nami ni mnyanyasaji pia huko mtandaoni. Kama kuna kitu kiliniuma na kinaendelea kuniuma hadi leo ni pale mmoja wa watu hao aliponiita MUUAJI. Yaani kuhamasisha mapambano dhidi ya unyanyasaji mtandaoni ni sawa na UUAJI? Ningeweza kumburuza mtu huyo mahakamani kwa kosa la kunidhalilisha (defamation) lakini ukosefu wa sheria halisi inayohusu unyanyasaji mtandaoni (cyberbullying) ungeweza kuniathiri.

Ni rahisi kuzungumzia 'uhuru usio na ukomo' kwa jamii iwapo hujawahi kuwa mhanga wa matumizi ya uhuru huo. Naomba nisieleweke vibaya.Siungi mkono muswada huo kwa vile tu mie ni mhanga huko nyuma, au utakomoa watu flani, lakini pia kuna sababu nyingine muhimu kama nilivyobainisha hapo juu.

MWISHO, japo ninatambua umuhimu wa wananchi kushirikishwa katika utungaji wa sheria zinazowahusu, na pia ninaafikiana na hoja ya kutoharakisha miswada inayohitaji ushirikishwaji wa umma, ninaunga mkono muswada huo kwa sababu UNAHITAJIKA SASA. Na kwa hakika umechelewa sana. Hatuwezi kuendelea kuvumilia matumizi mabaya ya mtandao wa kompyuta kwa kisingizio cha uhuru wa habari. Hatuwezi kuendelea kuvumilia picha za ngono na maiti zikiwekwa hadharani kama mapambo.Jamii yeyote yenye kuzingatia maadili inapaswa kuchukua hatua kali dhidi ya vitendo kama hivyo. Hatuwezi kuwatengenezea mazingira mazuri magaidi kwa kisingizio cha 'umbeya si dhambi.' Madhara ya kutochukua hatua ni makubwa kuliko kuchukua hatua.

Mie ninaweza kuwa mhanga wa sheria hiyo (ikipitishwa) hasa kwa vile ni mtumiaji mkubwa wa mtandao, na pia mkosoaji wa serikali ninapoona inastahili kukosolewa. Ni kweli kwamba sheria hiyo ikipitishwa inaweza kudhuru hata watu wasio na hatia.Lakini katika hili, tatizo si sheria bali CORRUPTION. Tunapozungumzia corruption hatumaanishi tu kuhonga au kuhongwa fedha, bali hata kupindisha sheria kwa maslahi binafsi au kukomoana.Sasa katika hilo, tuna tatizo katika nyingi ya sheria zetu.Ni wangapi wanaporwa viwanja kutokana na corruption katika sheria na sekta ya ardhi? Ni wangapi wapo gerezani muda huu kwa sababu tu walishindwa kuhonga polis au hakimu? Ni vigumu kwa sheria yoyote kuwa na ufanisi katika mfumo corrupt.Ni jukumu letu sote kupambana na corruption ili sheria zenye maslahi kwa jamii zisiishie kuathiri wasio na hatia.

Muswada huu ni kwa maslahi ya kila Mtanzania. Kama wewe si mhalifu wa mtandaoni, sheria hii haitokudhuru. As to itatumika vibaya na serikali, tatizo hapo sio sheria husika bali corruption.Kuna sheria nyingi tu na pengine kali zaidi ya hii tarajiwa, kwa mfano Sheria ya Usalama wa Taifa 1970, Sheria ya Idara ya Usalama wa Taifa 1996 na Sheria ya Kuzuwia vitendo vya Ugaidi ya mwaka 2002, zinazoweza kutumika vibaya kutokana na corruption. Sina hakika wangapi miongoni mwa wanaopinga muswada wa Cybercrime wameshakuwa wahanga wa 'matumizi mabaya' ya sheria hizo kali kuliko hii tarajiwa.

Hofu yetu dhidi ya matumizi mabaya ya sheria isiwe sababu ya kutokuwa na sheria kabisa. Tusielemee kwenye hofu yetu tu bali tutambue kuwa takriban kila siku kuna victims kadhaa kutokana na ukosefu wa sheria ya kudhibiti uhalifu wa mtandaoni.

ANGALIZO: Huu ni mtizamo wangu binafsi na unaweza kuonekana fyongo kwa mwingine.Twaweza kujadiliana pasipo haja ya 'kupigana.'

MUNGU IBARIKI TANZANIA



26 Mar 2015



Naibu Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,Mohamed Thabit Kombo akimpongeza Mwenyekiti wa Mfuko huo,Doris Mollel kwa kuona jukumu la kusaidia jamii katika kuokoa maisha ya watoto njiti.






Naibu Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,Mohamed Thabit Kombo akizungumza wakati wa hafla ya kutambulisha Mfuko wa Doris Mollel,iliyofanyika kwenye Hoteli ya Hyatt Regency,jijini Dar es salaam.




Mwenyekiti wa Mfuko huo,Doris Mollel akizungumza na wageni waalikwa waliofika kwenye hafla ya kutambulisha Mfuko wa Doris Mollel,uliofanyika kwenye Hoteli ya Hyatt Regency,jijini Dar es salaam.



Naibu Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,Mohamed Thabit Kombo (pili kushoto),Balozi Mwanaid Maajar (kulia),Mwenyekiti wa Mfuko huo,Doris Mollel (katikati) pamoja na wadau wengine wa Mfuko huo wakishiriki kwa pamoja kukata keki,kuashiria uzinduzi rasmi wa Mfuko wa Doris Mollel,uliofanyika kwenye Hoteli ya Hyatt Regency,jijini Dar es salaam.



Sehemu ya Wageni waalikwa katika hafla ya kutambulisha Mfuko wa Doris Mollel,iliyofanyika kwenye Hoteli ya Hyatt Regency,jijini Dar es salaam.



Picha ya pamoja na baadhi ya wadau waliohudhulia hafla hiyo.


Kutoka kulia ni HEENA ambaye ni mmoja kati ya washirika wakubwa wa mfuko huo, wakiwa wameshikana mikono na muanzilishi wa mfuko huo miss DORIS MOLLEL pamoja meneja wa mfuko huo RAHAB MBISE mara baada ya kuzindualiwa kwa mfuko huo jijini Dar es samaam


Meneja wa mfuko huo RAHAB MBISE akizungumza wakati wa uzinduzi huo uliofanyika jjini Dar es salaam




Mrembo wa singida aliyeshika nafasi ya tatu katika mashindano ya miss tanzania mwaka wa 2014 DORIS MOLEL leo amezindua rasmi rasmi DORIS MOLEL foundation ambayo ni mahususi kwa ajili ya kusaidia watoto ambao wamekuwa wanazaliwa wakiwa bado hawajatimia NJITI ambapo amewataka watu mbalimbali kujitokeza kumpa saport katika shighuli hiyo.

Uzinduzi huo ambao umefanyika leo jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi pamoja na wadau wanaohusika katika kuwasaidia watoto hao. wengi wamepongeza jitihada zinazoonyeshwa na mrembo huyo kwani watoto wanaozaliwa wakiwa na tatizo hilo wamekuwa wakusahaulika sana nchini tanzania jambo ambalo limetajwa kuwaadhiri watoto hao pamoja na wazazi wao.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mrembo DORIS ambaye ni mmoja  kati ya watu walioathiriwa na tatizo hilo (alizaliwa akiwa njiti) alisema kuwa ameamua kuwasaidia watoto na wazazi  wenye matatizo hayo baada ya yeye kupitia katika kipindi kama hicho ambapo alisema kunahitajika msaada mkubwa kutoka kwa watu wa mbalimbali.

Mimi nilizaliwa nikiwa njiti nilikuwa sijafikisha uzito halali wa kuzaliwa lakini nilizaliwa na mama akanisaidia hadi leo hii mnaniona hapa ni miss Tanzania na ni mtu nayekubalika na jamii,hivyo nimeona kuna haja ya kuwasaidia watoto kama mimi ambao wamezaliwa hivyo ili waweze kukua na afya njema na baadaye kutimiza malengo ya maisha yao,”alisema mrembo huyo.

Alisema kuwa baada ya kuchaguliwa kuwa mrembo namba tatu wa Tanzania alifikiria kitu cha kufanya ili arudishe shukrani kwa Watanzania na baada ya kutembea katika maeneo mbalimbali aligundua kuwa watoto wanaokumbwa na matatizo hayo bado wamekuwa hawapewi kipaumbele katika kusaidiwa jambo ambalo limemsukuma yeye kuanza kufanya mchakato huo.

Aidha alisema kuwa ipo haja ya serikali pamoja na wadau mbalimbali kuunga mkono jitihada hizo kwa lengo la kuokoa kizazi kikubwa ambacho kinazaliwa na matatizo kama hayo ambapo kwa takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya watoto laki mbili wanazaliwa wakiwa njiti kwa mwaka nchini Tanzania.

Uzinduzi huo uliambatana na  uchangiaji wa mfuko huo kwa ajili ya kuwasaidia watoto hao, ambapo watu mbalimbali wachangia na kuwaomba Watanzania wengine kuendelea kumsaidia mrembo huyo kuhakikisha kuwa anatimiza lengo lake.

Baadhi ya watu waliojitokeza kumpa nguvu katika shughuli hiyo leo ni pamoja na muandaaji wa mashindani ya miss tanzania ambapo ndiko mrembo huyo alikotokea bwana hashimu lundenga, Mwenyekiti mstaafu wa Bodi ya Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA) Mzee Iddi Simba, Naibu Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mohamed Thabit Kombo pamoja na viongozi mbalimbali kutoka Bara na Viusiwani




10 Mar 2015

Tafsiri: Mimi sishangazwi hata kidogo. Viongozi wa Kanisa na wanasiasa wakubwa wanashiriki katika mila hii ya kishetani. Kiongozi mmoja mkubwa wa kanisa mwenye usharika mkubwa jijini Dar es Salaam, anayemiliki benki, alikamatwa akiwa na albino amefungwa nyuma ya gari lake. Alitoroka eneo la tukio na kesi yake haikuripotiwa kwa sababu alitoa rushwa. Yeye pia ni muuza madawa ya kulevya mkubwa na mtakasaji fedha haramu. Kwahiyo tunatarajiwa Umoja wa Mataifa utaanza kuwafungulia watu hawa mashtaka ya ukatitili dhidi binadamu ili Watanzania walichukulie suala hili kwa makini.

Kwa umoja wetu na upendo wetu kwa ndugu zetu albino, tuunganishe kumsaka mwanaharamu huyu anayejiita mchungaji ilhali anafanya matendo ya kishetani. 

Mie ni muumini katika nguvu ya umma. Na nguvu ya umma si kuandamana tu bali hata katika kufichua maovu katika jamii. Ni na imani ya asilimia 100 kuwa kuna mtu au watu flani, sehemu flani wanamfahamu 'mchungaji' huyu. Kadhalika ninaamini kuna mtu au watu flani wanamfahamu mwanasiasa au mfanyabiashara au mganga au muuaji anayejihusisha na mauaji ya albino. Sasa pengine hofu ya kumripoti inachangiwa na kuchelea matokeo hasa ikizingatiwa kuwa polisi wetu hawaaminiki.

Tutumie nguvu ya umma. Kama una taarifa ya uhakika (ikiwa na uthibitisho itakuwa vema zaidi) basi ninaomba uwasiliane nami kwa barua-pepe CHAHALI at ABOUT dot ME au nitumie meseji Facebook https://www.facebook.com/evarist.chahali.1 au nenda kwenye tovuti hii http://swarmsecret.com/ kisha tweet kwa @chahali nami sio tu nitaweka hadharani suala hilo bali nitatumikia kila tone la nguvu zangu kuhakikisha mtu huyo anachukuliwa hatua za kisheria, ndani au nje ya Tanzania yetu.

Vinginevyo, ukifanikiwa kupata taarifa za mchungaji huyo au mtu yeyote anayejihusisha na unyama huo, 

Kwa pamoja tunaweza katika hili

SHUKRANI: Asante Ndugu Alfred Kiwuyo kwa kutufahamisha kuhusu habari husika

5 Mar 2015

"NI wajinga wa kisiasa pekee wanaoweza kudharau mchango wa Marehemu Komba katika siasa za Tanzania. Nimeona kuna watu wanabwabwaja sana!" Hii ni kauli ya Profesa Kitila Mkumbo aliyoitoa Jumapili iliyopita, katika mtandao wa kijamii wa Twitter.
MSOMI huyo ambaye pia ni mwanasiasa alitamka hivyo kufuatia mpasuko mkubwa uliojitokeza (angalau katika mtandao wa intaneti) kufuatia taarifa za kifo cha mwanasiasa maarufu na Mbunge wa Mbinga Magharibi (CCM) Kapteni John Komba, kilichotokea Jumamosi jijini Dar es Salaam.
Japo inafahamika kwa idadi ya Watanzania wanaitumia mtandao wa intaneti ni ndogo sana kulinganisha na idadi ya Watanzania wote, kwa kiasi fulani mada zinazotawala mtandaoni huweza kuakisi hali halisi iliyopo 'mtaani.' Ni kwa mantiki hiyo, ninashawishika kuhisi kuwa mpasuko uliojitokeza mtandaoni kufutia kifo cha Kapteni Komba waweza pia upo mitaani pia.
Mpasuko huo ulichukua sura ya makundi mawili, moja likionekana kufurahia kifo cha mwanasiasa huyo huku likifanya marejeo ya kauli zake mbalimbali hasa ile ya wakati wa Bunge Maalum la Katiba kuwa angeingia msituni iwapo pendekezo la muundo wa Muungano wa serikali tatu lingepitishwa.
Kundi jingine lilikuwa la waombolezaji, wananchi walioguswa na kifo hicho, huku wakilaani vikali 'jaribio lolote la kumlaumu marehemu.' Katika kundi hili, kulijitokeza 'mapadri na mashehe' walionukuu Biblia Takatifu na Kuran Tukufu kukumbushia umuhimu wa kuenzi marehemu na kuheshimu kifo.
Lakini ndani ya makundi hayo kulijitokeza 'waliouma na kupuliza,' yaani kwa upande mmoja wakionyesha jinsi walivyokwazwa na baadhi ya kauli za marehemu Komba hususani zilizokua zinachochea chuki na uhasama wa kisiasa na kijamii, lakini upande mwingine wakidai kuwa 'si vizuri kumsema vibaya marehemu.'
Kama nilivyotanabaisha hapo juu, sina hakika hali ikoje huko mitaani lakini yayumkunika kuhisi kuwa idadi ya waombolezaji ni kubwa kuliko ya 'wanaomwandama marehemu.' Idadi kubwa ya waombolezaji yaweza kusababishwa zaidi na 'uoga wetu wa kawaida kwa kifo' kuliko kuguswa na kifo husika.
Japo sote twatambua kwa uhai wetu una kikomo kwa njia ya kifo, na japo hatuna la kufanya kubadili ukweli huo mchungu, twaendelea kukiogopa kifo huku vifo vya watu wa karibu au tunaowafahamu vikitukumbusha tena na tena kuwa kifo kipo.
Kwa namna flani ya kusikitisha, kuna nyakati vifo huwa nafasi ya kushuhudia unafiki wa baadhi yetu kama wanadamu. Ni mara ngapi tumeshuhudia, kwa mfano, baadhi ya vijana wakiteketeza uhai wao kwa matumizi ya madawa ya kulevya, lakini jamii ikiwatelekeza, na kisha kumwaga lundo la rambirambi pale wanapofariki? Sawa, rambirambi ni ishara ya kuguswa na kifo, lakini ina faida gani hasa pale upendo ungeweza kuepusha kifo hicho?
Kwa upana zaidi, kuna haja gani kumpenda mtu baada ya kufariki ilhali alipokuwa hai alichukiwa? Upendo huo wa ghafla ni nini zaidi ya unafiki kwani wakati mwafaka tunapohitaji upendo ni tunapokuwa hai.
Kilichojitokeza baada ya kifo cha marehemu Kapteni Komba, ambapo baadhi ya wenzetu wameonekana 'kufurahia,' ni mwendelezo wa chuki katika Tanzania yetu, huku baadhi ya wanasiasa wa CCM wakiwa ndio wahusika wakuu.
Sawa, sio vema kuzungumzia 'mabaya' ya marehemu Komba, kwa mfano, lakini kwa bahati mbaya au makusudi, ukiweka kando umahiri wake katika nyimbo za maombolezo ya kifo cha Baba wa Taifa, marehemu Julius Nyerere, kumbukumbu muhimu ya hivi karibuni ni lugha kali aliyoitumia wakati wa Bunge Maalum la Katiba.
Yeye, pamoja na 'waeneza chuki' wengine walifikia hatua inayoweza kutafsiriwa kama kumtakia kifo Jaji Joseph Warioba kwa vile tu Tume aliyoongoza kukusanya maoni ya Katiba ilipendekeza muundo wa Muungano wa serikali tatu.
Lakini ishara kuwa chuki inazidi kutawala katika Tanzania yetu zilianza kujitokeza kwa wazi zaidi pale Rais Jakaya Kikwete alipolazwa nchini Marekani kwa matibabu ya tezi dume. Wakati idadi kubwa tu ya Watanzania ilijitokeza kumtakia Rais wetu uponyaji wa haraka, kulikuwa na kundi dogo ambalo halikuficha hisia zao, kiasi cha baadhi yao kutaka Rais asirudi akiwa hai. Kwa lugha nyingine, wenzetu hawa walikuwa wanamwombea kifo Rais wao.
Kwa bahati mbaya au makusudi, hakuna jitihada zilizofanyika japo kuanzisha mjadala tu kuhusu ustawi wa chuki katika nchi yetu. Na matokeo yake, leo hii twashuhudia baadhi ya wenzetu wanaoonekana kufurahia kifo cha mwanasiasa wetu mahiri.
Ni rahisi kuitazama chuki hii kama ujinga, kama alivyotanabaisha Profesa Kitila, lakini binafsi ninaamini hili ni swali gumu lisilostahili majibu rahisi. Kwa mtizamo wangu, moja ya sababu za chuki hiyo inaweza kuwa ni pengo la kitabaka kati ya watawala na watawaliwa, sambamba na pengo linalozidi kukua kati ya wenye nacho na wasio nacho.
Lakini chuki hiyo inachangiwa pia na jeuri ya watawala wetu, kusahau kuwa 'kesho kuna kifo,' kuropoka kila baya hasa kwa wapinzani wao kisiasa, na kuwadharau wananchi ambao kimsingi ndio waajiri wa watawala hao.
Kauli za baadhi ya wanasiasa mahiri kwa 'kusema ovyo' kama ile ya 'vijisenti' ya Mbunge wa Bariadi (CCM) Andrew Chenge, hii ya majuzi ya 'shilingi milioni 10 za kununulia mboga (labda ni tembo mzima)' ya Profesa Anna Tibaijuka, ile ya Profesa Muhongo kuwa 'Watanzania hawawezi kuendesha biashara ya gesi na mafuta bali wanamudu biashara ya matunda tu,' na nyinginezo nyingi, zinachangia kushamiri kwa hasira za baadhi ya wananchi kwa baadhi ya viongozi wao.
Tuna wanasiasa kama LivingstonLusinde, maarufu kama 'kibajaji’, Nape Nnauye, William Lukuvi, Stephen Wassira na Mwigulu Nchemba (japo huyu amekuwa na nafuu sasa), ambao wakizungumzia vyama vya upinzani wanaweza kumwaminisha msikilizaji kuwa wapinzani ni viumbe hatari kuliko magaidi wa Al-Shabaab, Boko Haram au ISIS.
Wanajitahidi sana kupamba mbegu za chuki, na kwa hakika wamefanikiwa kwa kiasi fulani. Lakini uongozi wa juu wa chama hicho tawala haujawahi kukemea kauli hizo za chuki, yayumkinika kuhisi kuwa ujenzi wa chuki ni miongozi wa sera zisizo rasmi kwa chama hicho, kama ilivyo ufisadi.
Ni muhimu kwa watawala wetu kujifunza kitu katika chuki hii inayolitafuna taifa letu. Kinachotufanya tuendelee kumlilia Baba ya Taifa hadi leo ni matendo yake ya kuigwa mfano wakati wa uhai wake.
Yawezekana kama binadamu mwingine, Mwalimu aliwahi kuwakwaza baadhi ya Watanzania, lakini 'hukumu ya jumla' kwa matendo yake wakati wa uhai wake ni kwamba aliweka mbele maslahi ya taifa kuliko maslahi yake binafsi. Tunamkumbuka na kumlilia kwa sababu tunaona ombwe kubwa lililotokana na kifo chake.
Sasa, japo 'marehemu hasemwi vibaya,' sidhani kama kuna atakayeshangaa sana kuona kifo cha mwanasiasa mahiri kwa matusi, vijembe, mipasho na mambo mengine mabaya kikipelekea furaha katika sehemu flani ya jamii. Ndio, dini zetu zinasisitiza kuwaenzi marehemu, lakini dini hizo pia zinasisitiza umuhimu wa heshima wakati wa uhai wetu.
Na pia licha ya ukweli si kila Mtanzania ni mcha-Mungu, wingi wa wacha-Mungu katika nchi yetu umeshindwa kuzuwia mauaji ya albino, ufisadi na 'dhambi'nyingine lukuki.
Nimalizie makala hii kwa kutoa salamu zangu za rambirambi kwa familia ya marehemu Kapteni Komba, ndugu, jamaa, marafiki na Chama Cha Mapinduzi kwa ujumla.
Njia mwafaka ya kumwenzi marehemu ni kudumisha mema yake, na kujifunza katika mapungufu yake. Kadhalika, kifo hiki kinapaswa kutuamsha na kuanza mjadala wa kitaifa kuhusu kudidimia kwa upendo, umoja na mshikamano wetu.
Mwenyezi Mungu aipumzishe roho ya marehemu Kapteni Komba mahala pema peponi. Yeye ametangulia tu, sote twaelekea huko.

6 Feb 2015

WIKI iliyopita, kwa mara nyingine tena, Watanzania walishuhudia jinsi Jeshi la Polisi lilivyo mahiri katika ukiukaji wa haki za binadamu baada ya kuwapiga na kuwajeruhi wanachama wa CUF pamoja na Mwenyekiti wao, Prof Ibrahim Lipumba kwa ‘kosa la kuandamana kinyume na maagizo ya jeshi hilo.’
Kwa hakika nilitokwa na machozi nilipoangalia video ya tukio hilo ambayo imesambaa mtandaoni. Vipande vya video hiyo ambavyo vilinitia uchungu zaidi ni pale binti mdogo tu alipopigwa vibaya na polisi kadhaa wa kiume, na pale waandamanaji hao waliposhushwa kwenye magari ya polisi na kurushwa kichura kuingia kwenye kituo cha polisi. Huu ni ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu.
Lakini pamoja na tukio hilo kusikitisha mno, binafsi sioni kama ni la kushangaza kwani sote twakumbuka ruhusa iliyotolewa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda kwa polisi kuwa “(wananchi) wapigwe tu.”
Ukiangalia video hiyo kwa makini (waweza kuiona hapa http://goo.gl/zbmnTG
(link is external)
) utabaini ukweli mmoja wa kutisha. Angalia dakika ya 03:14 hadi dakika ya 03:19, baadhi ya waandamanaji wanasema "TUUENI..."

Angalia pia kuanzia dakika ya 3.21 ambapo polisi wanaanza kurusha risasi (sina hakika kama ni risasi za moto au bandia) lakini kitu cha kukiangalia kwa makini ni ukweli kwamba ukiacha watu wachache wanaoonekana kutishwa na milio hiyo ya risasi, idadi kubwa tu ya watu inaonekana kutotishika. Hali hiyo inaendelea hata baada ya 'king'oling'oli' cha polisi kinapooanza kulia na hatimaye polisi kutembeza kipigo cha kinyama.
Licha ya kuumia mno kuona Polisi wakitumia nguvu kubwa katika tukio ambalo lingeweza kabisa kumalizwa kwa amani pasipo haja ya kurusha risasi japo moja au kuwapiga na hatimaye kuwakamata waandamanaji akiwemo Mwenyekiti wa CUF Prof Lipumba, kilichonipa hofu ni jinsi taratibu wananchi wanavyoanza kuota 'usugu' dhidi ya unyanyasaji wa polisi.
Inapofika mahala wananchi wanaashiria bayana kuwa wapo radhi kuuawa, na kuwaambia polisi waziwazi kuwa TUUENI, basi kwa haki tumeshafika mahala pabaya. Na kama nilivyobainisha hapo juu, na kama inavyoonekana kwenye video hiyo, imefika mahala wananchi wameanza kuzowea sauti za risasi sambamba na mabomu ya machozi.

Hii ina maana gani? Wakati tayari wananchi wameshaonyesha kuzowea unyanyasaji na unyama wa polisi wetu na kuwa tayari kwa lolote lile, yayumkinika kubashiri kuwa kuna siku sio tu wananchi wataweka kando uoga na kuendeleza 'usugu' huo nilioueleza hapo juu bali pia wanaweza kujibu mashambulizi.
Uchambuzi mwepesi ni kwamba wakati polisi hawana njia nyingine zaidi ya hizi wanazotumia kila siku: kutumia nguvu kuvunja maandamano ya amani, wananchi wanapata nguvu mpya kwa kuondoa uoga na kuwaacha polisi wafanye watakalo. Upo uwezekano wa wananchi hao kutoishia hapo tu bali badala ya kuwaachia polisi wawaonee, WANAWEZA KUJIBU MASHAMBULIZI. Na kwa mwenendo ulivyo, hatuko mbali na hali hiyo.
Ni vigumu kubashiri ni lini polisi wetu watathamini haki za binadamu na uhai wa wananchi wasio na hatia. Ni vigumu zaidi kutarajia mabadiliko kutoka kwa mwana-CCM yoyote yule atakayemrithi Kikwete baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu. Na ndio maana hatujaskia yeyote kati ya waliotangaza nia ya kuwania Urais kupitia CCM akilaani unyama huo wa polisi. Kwanini walaani ilhali wao wana kinga ya kudumu dhidi ya uonevu na unyama wa polisi wetu? Japo Rais kutoka chama cha upinzani anaweza kutugeuka, lakini katika mazingira ya kawaida ya kibinadamu angalau yeye naye atakuwa ameshaonja unyama wa polisi wetu na ni rahisi kwake kuchukua hatua kuliko hao wasioguswa na polisi.
Mmoja wa wana-CCM waliotangaza nia ya kugombea urais, January Makamba, amekuja na kauli-mbiu ya ‘Tanzania mpya.’ Nadhani moja ya maeneo yanayopaswa kuwa mapya katika Tanzania hiyo mpya ni utendaji kazi wa jeshi letu la polisi. Hata hivyo, pamoja na umuhimu wa upya katika maeneo mbalimbali yanayoihusu nchi yetu, tatizo kubwa ninaloliona ni udhati katika utekelezaji wa dhamira hiyo. Lakini pia kuna suala la lini hiyo Tanzania mpya ianze kama sio sasa? Nadhani jibu rahisi ni kwamba uhuni unaofanywa na jeshi letu la polisi sio suala la bahati mbaya. Ni mkakati madhubuti unaoinufaisha CCM dhidi ya wapinzani wake.
Kwanini iwe ruhusa kwa CCM kuandamana muda wowote wanaotaka lakini wapinzani wakiomba kufanya maandamano wanakataliwa?
Sasa pamoja na dhamira nzuri ya January ya kutuletea Tanzania mpya, ni wazi CCM haiwezi kuruhusu tuwe na ‘jeshi la polisi jipya’ litakaloendana na ‘Tanzania mpya’ kwa vile hali hiyo itatoa mazingira bora ya kushamiri kwa demokrasia huko nyumbani, na hili litaiathiri CCM.
Tukirejea kwenye tukio hilo la kinyama dhidi ya wana-CUF wasio na hatia, mazingira yote yanaonyesha sio tu kuwa hakukuwa na haja kwa polisi kutumia mabavu bali pia lingeweza kumalizwa kwa amani.

Lakini kwa polisi waliozowea kufanya ubabe, kulimaliza suala hilo kwa amani kungewafanya wajiskie kama ‘wameshindwa kazi.’ Au huenda walihofia ‘kuchukuliwa hatua kali za kinidhamu kwa kukiuka agizo la Waziri Mkuu Pinda kuhusu kupiga raia.’
Ukweli mchungu ni kwamba jeshi la polisi litaendelea na unyama wake kwani hakuna dalili yoyote ya serikali kuchukua hatua za kukomesha tabia hiyo. Na kwa vile tunaelekea msimu wa uchaguzi ambapo miongoni mwa shughuli za kawaida kisiasa katika chaguzi ni pamoja na maandamano na mikutano, kuna uwezekano mkubwa wa kushuhudia wanachama wa vyama vya upinzani na/au viongozi wao wakinyanyaswa na polisi wetu.
Nihitimishe makala hii kwa kurejea tahadhari niliyoitoa hapo juu.

Ipo siku wananchi wanaonyanyaswa na polisi wetu wataamua ‘liwalo na liwe’ na watajibu mashambulizi. Japo ninaomba Mungu atuepushe tusifikie hatua hiyo, ukweli mchungu ni kwamba twaelekea huko. Imefika mahala wananchi wanawaambia polisi waziwazi “tuueni” na wanasikia milio ya risasi lakini hawakimbii.
Yayumkinika kuhisi kuwa kitakachofuata si wananchi kuwapa polisi uhuru wa kuwapiga na kuwajeruhi bali kupambana nao kwa nguvu zote. Ni sihitaji kukumbusha kuwa polisi wetu ni sehemu ndogo tu kulinganisha na umma wa wasio-polisi.

TUSIPOZIBA UFA TUTAJENGA UKUTA

24 Dec 2014

Awali,kupitia akaunti yake ya Twitter, Idhaa ya Kiswahili ya Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC Swahili) iliripoti ifuatavyo



Hata hivyo, baada ya kuzongwa na baadhi ya WANAHARAKATI huko Twitter walioonyesha kukerwa na hatua hiyo ya nchi wahisani, Mwenyekiti wa nchi wahisani, Balozi wa Finland nchini Tanzania Sinikka Antila (@SinikkaAntila) alifafanua kwa tweet ifuatayo 


Kwa lugha ya taifa, Balozi huyo anaeleza kwamba "vyombo vya habari havipo sahihi. Asilimia 15 ya msaada ulioahidiwa kwa bajeti ya mwaka 2014/15 ilitolewa kabla ya hotuba ya Rais (Kikwete)."

Hata hivyo, licha ya kauli hiyo ya Balozi Antila kutanabaisha kuwa BBC Swahili waliripoti ndivyo sivyo kuwa wafadhili wameamua kutofa fedha hizo baada ya kuridhishwa na hotuba ya Rais Kikwete, bado kuna swali gumu kuhusu suala hilo, nalo ni JE NCHI WAFADHILI ZILITUHADAA ZILIPODAI KUWA ZIMESITISHA MISAADA HADI HATUA ZITAKAPOCHUKULIWA KUHUSU SUALA LA ESCROW?

Swali hilo linatokana na kauli ya Balozi huyo wa Finland kuwa fedha hizo zilishatolewa hata kabla ya hotuba ya Rais Kikwete, ikimaanisha aidha nchi hizo wahisani zilikuwa zina hakika kuwa Rais Kikwete angechukua 'hatua hizo za kuwaridhisha wafadhili' au 'walituzuga tu' kuhusu kusitishwa misaada hiyo.

Kadhalika, kauli ya Balozi Antila haikanushi kuridhishwa kwa wafadhili na hotuba ya Rais Kikwete, ambayo Watanzania wengi wanaamini kuwa imewalinda mafisadi hasa ikizingatiwa mzigo mkubwa wanaoubeba kutokana na sakata la muda mrefu la IPTL. Kwa Rais Kikwete kushindwa kumaliza sakata hilo, na kuridhia kuwa pesa za Tegeta Escrow ni za IPTL/ PAP, ina maana Watanzania wataendelea kulipa mamilioni ya shilingi kila siku kwa huduma ya umeme ambayo kimsingi ni hewa.

Binafsi ninaguswa na uamuzi wa nchi wahisani kwa sababu kama mkazi wa Uingereza, ninalipa kodi mbalimbali, ambazo sehemu ya kodi hiyo ipo katika misaada inayotolewa na nchi hii kwa Tanzania. Wakati sina kipingamizi kwa nchi hizo kuisaidia Tanzania, siungi mkono kabisa kuendelea kutoa fedha zinazoishia kuwaneemesha mafisadi kwa kunenepesha akaunti zao, kuongeza idadi za mahekalu na magari yao ya thamani na kukuza idadi ya nyumba zao ndogo.

Ufadhili usiozingatia maslahi ya nchi fadhiliwa sio tu ni upuuzi bali pia ni ku-abuse fedha za walipakodi katika nchi wafadhili.

5 Dec 2014

Waingereza wana msemo ambao unatafsirika kwa Kiswahili kama "chuki ya pamoja ni mwanzo wa urafiki mkubwa." Kimahesabu kama A hapatani na B, na A anamchukia C kama ambavyo B anamchukia pia C, basi chuki ya A na B kwa C yaweza kuwa mwanzo wa wawili hao A na B kuwa marafiki wenye lengo la kumwangamiza C.

Binafsi, naomba kukiri kuwa kwa muda sasa nimekuwa siafikiani na mitizamo na mwenendo wa mwanasiasa mahiri wa upinzani, Zitto Kabwe. Siwezi kusema nina chuki dhidi yake bali mie sio miongoni mwa supporters wake.Pamoja na sababu nyingine, kubwa ni kile ninachokitafsiri kama mwanasiasa huyo kutanguliza mbele maslahi yake binafsi badala ya chama chake yaani Chadema. Kwa mtizamo wangu, mgogoro uliopelekea hatua ya Chadema kumvua madaraka Zitto ni matokeo ya 'imani potofu' kuwa kuna mwanasiasa anayeweza kuwa maarufu kuliko chama chake, Si kwamba haiwezekani kabisa kwa hilo kutokea lakini si kwa hatua waliyofikia Chadema hivi sasa.

Lakini lengo la makala hii si kumjadili Zitto wala ugomvi kati yake na Chadema. Ila nimegusia suala hilo kwa sababu nililazimika 'kurejesha urafiki' na mwanasiasa huyo, angalau kinadharia, wakati akifanya jitihada kubwa binafsi na kama mwenyekiti wa PAC kushughulikia ufisadi wa Tegeta Escrow. Kwa kutumia mfano huo hapo juu wa chuki za A kwa C na za B kwa C, na A ni Zitto, na B ni mie, huko C wakiwa mafisadi wa Escrow, basi 'urafiki' usingeepukika.

Hakuna Mtanzania atakayeshindwa kumpongeza Zitto na Kafulila pamoja na PAC kwa ujumla walivyofanya kazi kubwa na nzuri katika kushughulikia skandali hiyo. Nina imani hata wahusika wa ufisadi huo wa Escrow wanamkubali kwa jinsi alivyowakalia kooni...ALMOST.

Hata hivyo, mara baada ya kumalizika kwa 'timbwili' hilo la Escrow bungeni, nilitumiwa meseji na 'mjuzi mmoja wa mambo ya huko nyumbani' ambaye alidai kuwa pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na PAC, kuna 'mchezo mchafu' uliofanyika katika kufikia mwafaka miongoni mwa wajumbe, hususan wale wa kutoka CCM. Alidai kuwa kilichowezesha mwafaka huo kufikiwa ni pamoja na 'kumnusuru' Rais Jakaya Kikwete, ambaye kama Mbunge Tundu Lissu alivyobainisha bungeni, anatajwa kuhusika katika skandali hiyo. Kimsingi, hoja ya Lissu, ambaye pia aliilaumu Idara ya Usalama wa Taifa kwa kutowajibika ipasavyo katika mlolongo wa skandali mbalimbali zinazougubika utawala wa Rais Kikwet, iliuawa kimyakimya licha ya umuhimu wake mkubwa.

Hata hivyo, kwa uelewa wangu, jaribio lolote la kumhusisha Rais Kikwete na skandali hiyo hata kama ushahidi upo lingepelekea mparaganyiko mkubwa katika kamati hiyo ya Zitto. Na kama tulivyoshuhudia 'makada' wa CCM huko bungeni walivyopigana kufa na kupona hadi Waziri Mkuu Mizengo Pinda akanusuriwa, kwa hakika ishu ya Kikwete kuhusishwa na Escrow ingepelekea bunge hilo kuvunjika pasi kufikia hitimisho.

Lakini what if mkakati huo wa 'kumnusuru Rais Kikwete' unabeba mengi zaidi ya tunavyodhani? 


Kwa kifupi, tume-settle for less. Na Waingereza wana msemo unaotahadharisha kuhusu ku-settle for less, ambapo wanasema 'pindi ukikubali kupokea pungufu ya unachostahilki basi hatimaye utaishia kupokea pungufu zaidi ya kile ulichostahili awali.' Japo ni mapema kuhitimisha kwamba 'tumeingizwa mkenge,' lakini ukimya wa Rais Kikwete katika kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu Escrow umeanza kuzua wasiwasi.

Na 'kigugugmizi' kinachomkabili Rais Kikwete kina sababu kadhaa za wazi. Kwa mfano, kumtimua Mwanasheria Mkuu Jaji Werema kunaweza kupelekea kuzuka kwa skandali nyingine iwapo Jaji huyo ataamua 'mmemwaga mboga, na mie namwaga ugali' kwa maana anajua mengi yaliyojiri na yanayojiri katika utawala wa Rais Kikwete. Japo si kwamba haiwezekani kumtimua na kisha kumfunga mdomo, lakini historia ya wanasheria wakuu huko nyuma inapaswa kutukumbusha jinsi 'wanavyobebwa' kwa minajili ya 'kutotengeneza uadui na mtu anayejua siri nyingi.'

Kwa upande wmingine, ni muhimu kukumbuka kuwa kimsingi Rais Kikwete ndo aliyemleta Profesa Muhongo katika frontline politics. Hawa ni marafiki wa karibu. Na hadi sasa Muhongo ameendeleza jeuri yake ya kisomi na kusisitiza kuwa fedha za Escrow si za umma. Msimamo huo pia washikiliwa na Waziri Mkuu Pinda. Je kuna anayefahamu msimamo wa Rais Kikwete? Maelezo yanaonyesha kuwa yeye aliridhia malipo ya Escrow kufanyika. Je amebadili mawazo na kutambua kuwa hilo lilikuwa kosa?

Lakini wakati tayari tunafahamu majina mengi ya walionufaika na mgao wa Escrow kupitia Benki ya Mkombozi, inadaiwa kuwa mgao mkubwa zaidi uliopitia Benki ya Stanbic ulihusisha vigogo kadhaa lakini hadi muda huu hakuna jina hata moja lililowekwa hadharani. So far, gazeti la Raia Mwema limeripoti kuwa mke wa kigogo momja mwandamizi huko Ikulu alikatiwa shilingi bilioni 5. Sasa huhitaji kujua hesabati vizuri kubashiri kwamba kama mke wa kigogo alikatiwa mbilioni tano, mumewe alipewa kiasi gani? 

Hayo yote tisa, kumi ni kauli niliyokumbana nayo muda mfupi uliopita, na ambayo kwa hakika ndio iliyonisukuma kuandika makala hii. Kauli hiyo ni ya Jaji Mkuu Chande ambayo kimsingi inaharibu mwenendo wa kesi yoyote itakayofunguliwa dhidi ya wahusika wa ufisadi wa Escrow. Nimeinukuu kwa picha hapa chini.


Je Jaji Mkuu alikuwa anatoa tu tahadhari au alikuwa akifikisha ujumbe mahsusi kwamba hata tukiwapeleka mahakamani wahusika wa Escrow, utetezi wao upo bayana...kwamba walishahukumiwa bungeni. Na kama Jaji Mkuu 'hakutumwa' basi kwa hakika amewapatiwa washtakiwa-watarajiwa ushauri mzuri wa bure kisheria kuhusu jinsi ya kupambana na kesi yoyote watakayofunguliwa kuhusisna na suala hilo: wajitetee kuwa walishahukumiwa na bunge, na mawakili waoa waweza kutumia kauli hiyo ya Jaji Mkuu kama supporting evidence.

Anyway, pengine ni mapema mno kuhukumu lakini kama ambavyo Mzee Warioba alivyoonyesha mapungufu ya taarifa ya PAC na maazimio ya bunge kuhusu skandali ya Escrow, sintomshangaa mtu yeyote atakayeanza kupatwa na wasiwasi kuwa tumeingizwa mkenge...TENA.


Sijui msomaji mepndwa unaonaje. 





Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.