23 Aug 2010

Wakati wa kuelekea kampeni za uchaguzi mkuu wa hapa Uingereza kulijitokeza tetesi za wasiwasi kuhusu afya ya aliyekuwa Waziri Mkuu Gordon Brown.Katika kilichotafsiriwa kama kukata mzizi wa fitina,mtangazaji maarufu wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC),Andrew Marr,alimuuliza Brown katika mahojiano naye kuhusu tetesi hizo.Katika tetesi hizo ilidaiwa kuwa Brown alikuwa akitumia dawa za kutuliza mara kwa mara.

"Jambo ambalo kila mtu amekuwa akiongelea katika kijiji cha Westminster...Watu wengi katika nchi hii wamekuwa wakitumia dawa walizoelekezwa kununua na daktari (prescription drugs)...Je wewe ni mmoja wao?",aliuliza Marr."Hapana.Nadhani uulizaji swali wa aina hii umekuwa ukiingia sana kwenye ulingo wa siasa za Uingereza",alijibu Brown.Jitihada za mwanahabari huyo kutaka kudadisi zaidi zilizimwa na Brown aliyesema ameshajibu swali hilo.


Nimekumbuka tukio hilo kufuatia kuanguka kwa mara nyingine kwa Rais Jakaya Kikwete na namna vyombo vingi vya habari vilivyokwepa kuripoti tukio hilo kwa uwazi.Hata video iliyomwonyesha Kikwete akianguka iliondolewa mtandaoni kwa haraka,kwa sababu wanazojua waliyoiondoa.Na hata video yenyewe ya tukio hilo ilionyesha "kiduchu" tu kuanguka kwa JK kisha ikaelekezwa kwenye umati wa watu hapo Jangwani.Inaelezwa pia kuwa baadhi ya vituo vya runinga huko nyumbani havikuonyesha tukio hilo katika taarifa zao za habari.

Kichekesho ni kwamba kabla hajakumbwa na dhahma ya kuanguka,JK alijigamba kuwa serikali yake imeboresha uhuru wa habari.Sasa uhuru wa habari ambao tukio la kusikitisha na kuhudhunisha linalomkumba Rais wetu linabanwa ni uhuru kweli au hadithi tu?Na hapa simpingi JK kuwa amejitahidi kudumisha uhuru wa habari bali tatizo langu lipo kwa wanahabari wenyewe.

Je,kulikuwa na maagizo kwamba,kwa mfano,clip ya kuanguka kwa JK iodolewe mtandaoni?Kama jibu ni ndiyo,basi uhuru wa habari anaozungumzia JK una walakini.Lakini kama jibu ni hapana basi wanahabari walioamua kuminya habari hiyo wana maswali ya kuwajibu wasomaji wao na Watanzania kwa ujumla.

Natambua kuwa pamoja na majigambo ya JK uhuru wa habari unaodumishwa zaidi ni ule wa "habari za kawaida" na sio zinazogusa masuala ya watawala.Baadhi yetu ni wahanga wa matumizi hayohayo ya uhuru wa habari na uhuru wa kujieleza.Ukizungumzia mafisadi walio ndani ya CCM,baadhi ya "wenye nchi" wanakurupuka kudai ni utovu wa nidhamu dhidi ya serikali.Yaani kukemea maovu inakuwa nongwa!?

Tukio la kuanguka kwa JK lilikuwa haki ya kila Mtanzania kufahamishwa na wanahabari.Ikumbukwe kuwa ni Watanzania haohao ndio waliompigia kura kiongozi huyo kuwa Rais wao,na mkutano wake wa Jumamosi ulikuwa na madhumuni ya kuwaomba ridhaa ya kuwaongoza tena.Jakaya Kikwete alikuwa hapo kama mgombea wa CCM,na japo hatuwezi kutenganisha urais wake na ugombea wake huko CCM,ukweli unabaki kuwa katika harakati hizi za kampeni anapaswa kuchukuliwa kama wagombea wengine wa vyama vilivyosimamisha wagombea wao.

Japo mkono mrefu wa dola uko makini zaidi katika udhibiti wa habari "zisizopendeza",yayumkinika kusema kwamba baadhi ya wanahabari na vyombo vya habari hawawezi kukwepa lawama.Nachoshindwa kuelewa kwanini  mara nyingi "habari zisizopendeza machoni mwa watawala" zinaminywa ni kama hali hiyo inasababishwa na uoga tu wa wanahabari au/na vyombo vya habari au ni lile tatizo sugu la kujikomba kwa watawala?

Kama sababu ni uoga,basi hayo ni mapungufu ya wazi kwa mwanahabari au chombo cha habari husika.Hata hivyo,inawezekana uoga huo kuwa ni matokeo ya mfumo wa siasa za chama kimoja ambapo ilikuwa mithili ya kosa la jinai "kumsema vibaya" kiongozi (yaani kusema au kuandika kitu kisichompendeza kiongozi).Tuliaminishwa kuwa viongozi wetu ni kama miungu-watu,hawawezi kukosea,kila wanalofanya ni jema na siku zote wako sahihi.Uoga huu unapaswa kuepukwa kwa vile tupo katika  mfumo mpya wa siasa za uwingi zisizo na nafasi ya "zidumu fikra sahihi za A au B".

Kujikomba ni tatizo sugu si kwa baadhi ya Watanzania tu bali hata baadhi ya Waafrika kwa ujumla.Kwa mbali,kujikomba ni matokeo ya mfumo wa ujima na hatimaye ujamaa ambapo mhusika hujibidiisha "kufanya jambo zuri" hata kama hajaombwa.Kwa bahati mbaya,"jambo hilo zuri" linaweza kuwa lisilo na manufaa kwa jamii.Kwahiyo,mwanahabari aliyebania tukio la kuanguka kwa JK anaweza kuwa alifanya hivyo akiamini kuwa "ni vibaya kumwonyesha Rais akianguka hadharani".Lakini imani hiyo potofu ilimaanisha baadhi ya Watanzania kukoseshwa haki ya kuona kilichomsibu mgombea wa CCM ambaye pia ni Rais wao.

Simnyooshei mtu kidole bali hii ni changamoto tu kwa wanahabari na vyombo vya habari.


Riyadh,Saudia,April 16

Wafanyabiashara wa Saudi Arabia wameiomba Tanzania kama wanaweza kukodi hekta nusu milioni (500,000) za ardhi inayofaa kwa kilimo hususan cha mpunga na ngano kama sehemu ya mpango wa kujitosheleza kwa chakula kwa falme hiyo ya jangwani.

Maofisa waandamizi wa chemba ya biashara ya jiji la Riyadh walitoa ombi hilo wakati wa ziara ya Rais Jakaya Kikwete katika falme hiyo.

"Tanzania ipo tayari kufanya biashara nanyi.Kuna heka milioni 100 (hekta milioni 40.5)za ardhi nzuri yenye rutuba",Kikwete aliwaambia wafanyabiashara hao.

Samir Ali Kabbani,mkuu wa kamati ya kilimo ya chemba hiyo alisema kwamba wamepata majibu mazuri sana."Kikwete ametuambia kwamba Tanzania inaweza kutukodisha ploti ambazo kila moja ina ukubwa wa hadi hekta 10,000 kwa kipindi cha miaka 99",Kabbani alilieleza Shirika la Habari la Reuters baada ya mkutano huo na Kikwete.

Maofisa na wafanyabiashara wa Kisaudi walitrajiwa kuitembelea Tanzania wiki chache baada ya mkutano huo.

"Wanaweza kukodi ardhi kutoka serikalini",January Makamba,msaidizi wa Rais Kikwete,aliieleza Reuters."Lakini inabidi tuhakikishe kuwa hatuishii kwenye hali kama ile ya Nigeria:hifadhi kubwa ya mafuta lakini foleni kubwa kwenye vituo vya kuuzia mafuta",alisema Makamba.

Maafisa wa Saudia wanaiona Tanzania kama sehemu mwafaka kutokana na mazingira ya kijiografia,kisiasa na wingi wa maji na ardhi ya kilimo.Makampuni kadhaa ya nchi hiyo tayari yameanza kuwekeza katika miradi ya kilimo huko Indonesia na Ethiopia.

Agosti mwaka jana Indonesia ilisema kuwa mjumuiko wa makampuni ya Bin Ladin ya Saudi Arabia unatarajia kuwekeza dola bilioni 4.3 katika hekta 500,000 za kilimo cha mpunga.Mahitaji ya ngano kwa Saudia kwa mwaka yanakadiriwa kufikia tani milioni 2.5,na mwaka juzi nchi hiyo iliagiza kutoka nje karibu tani milioni 1 za mchele,kwa mujibu wa Idara ya Kilimo ya Marekani.

CHANZO: Reuters


22 Aug 2010

What A good NewS???
Well,your top-above-the-rest blog,ANGALIA BONGO,has officially  moved to a new world.
Thanxx
Admin(Angaliabongo)

Blogu hii ya KULIKONI UGHAIBUNI inafungua ukurasa mpya na kuweka historia ya kipekee katika fani ya habari nchini Tanzania kwa kutangaza hadharani kuwa inam-endorse mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chadema,Dokta Wilbroad Slaa.

Kuna sababu lukuki za kufanya hivyo lakini hapa nitaziorodhesha chache.Kwanza,blogu hii inataka kuachana na unafiki unaojidhihirisha katika baadhi ya vyombo vya habari vyetu ambapo wahusika wanadai hawafungamani na upande wowote lakini matendo yao yanawasuta kwa kupendelea chama tawala huku wakivibinya kwa nguvu baadhi ya vyama vya upinzani.Hapa simsimangi mtu bali nadhani ni vema kuweka msimamo wazi ili kama chombo cha habari ni wakala wa CCM na JK basi ni vema wasomaji wakafahamishwa bayana.

Pili,blogu hii inaamini kuwa kila Mtanzania mwenye uchungu wa dhati kwa nchi yetu anapaswa kumsapoti Dkt Slaa.Katika utumishi wake kwa umma,mgombea huyo wa Chadema ametuthibitishia kuwa ni mtetezi halisi wa haki za wanyonge na ustawi wa taifa letu.Ni nani asiyefahamu namna Dkt Slaa alivyohatarisha maisha yake kwa “kuwavua nguo mafisadi hadharani” alipotangaza ile “list of shame”?Walitishia kumpeleka mahakamani lakini hakuna mmoja wao aliyediriki kufanya hivyo,na sanasana baadhi yao wakaishia kuburuzwa mahakamani na serikali katika “kujikosha”.Blogu hii inaamini kuwa Dokta Slaa ni mkombozi na suluhisho mwafaka la matatizo lukuki yanayotukabili.

Tatu,binafsi naamini kuwa mgombea wa CCM,Jakaya Mrisho Kikwete,ameshindwa kabisa kutimiza matarajio ya Watanzania licha ya ahadi lukuki alizozitoa wakati wa kampeni zake mwaka 2005 na anazoendelea kuzitoa hadi leo.Ungetegemea kuwa mwezi huu wa toba Kikwete angemwogopa Mola wake na kutubu kwa Watanzania kwamba kuna maeneo mengi tu ambapo yeye na chama chake wamewaangusha Watanzania.Lakini kama ilivyo jeuri ya wanasiasa wengi wa Kiafrika,JK ameendeleza wimbo wa “mafanikio ya Awamu ya Nne”.Yani hata kushamiri kwa ufisadi na “uchakachuaji” wa kura za maoni ndani ya CCM ni mafanikio!

Sababu ya nne inashabihiana na hiyo ya tatu.Naamini kuwa afya ya mgombea wa CCM,Jakaya Kikwete,inapaswa kuwekwa kwenye darubini na wapiga kura wanapofanya maamuzi ya kumchagua rais wa awamu ya tano.JK ameshaanguka hadharani mara tatu na kila mara tunapewa excuse moja baada ya nyingine.Mwaka 2005 tuliambiwa “swaumu na uchovu wa kampeni”.Alipoanguka Mwanza tuliambiwa uchovu wa safari (kana kwamba safari hizo ni zile za Wamachinga wanaotembea juani kwa mguu!).Na jana kaanguka tena jukwaani halafu tunaambiwa sababu ni swaumu.Kwani Makamba hajafunga?Au Rais Karume naye “kobe”?Kuna tatizo zaidi ya swaumu au uchovu lakini kwa vile viongozi wetu wamezowea sifa na sio kasoro basi kuweka hadharani kinachomsibu kiongozi huyo inaonekana ni sawa na uhaini.Blogu hii imaanimi kuwa ili Tanzania ijikwamue katika lindi la umasikini wa kutupwa,sambamba na kukabiliana na janga la ufisadi,tunahitaji kiongozi mwenye afya timilifu,kimwili na kiakili.Hatujui JK ameshaanguka matra ngapi asipokuwa hadharani lakini haihitaji hata cheti cha short course ya utabibu kumaizi kuwa JK ana matatizo ya kiafya yanayofichwa,aidha kutokana na uoga wa wanaopaswa kuujulisha umma kuhusu hilo au maagizo yake mwenyewe kuwa “yuko fiti”.All in all,uzito wa matatizo yanayoikabili Tanzania unahitaji mtu aliye fiti kweli,na sio kwa anavyodhani yeye au anavyotaka umma uamini hivyo ilhali ni kinyume na hali halisi.

Kama nilivyoandika mwanzoni,kuna sababu nyingi zilizopelekea blogu hii kuamua kum-endorse Dkt Slaa lakini chache zilizotajwa hapo juu zinawakilisha hizo nyingine.Nawakaribisha ndugu zangu wa Chadema kuitumia blogu hii kufikisha habari kwa Watanzania pasipo hofu ya kuwa habari hizo zitachujwa,kuminywa au “kuchakachuliwa”.

Natambua bayana kuwa baadhi ya wasomaji wa blogu hii sio wafuasi wa Dkt Slaa au Chadema lakini napenda kuwakikishia kuwa endorsement hii haimaanishi kashfa,matusi,dharau au mambo yasiyofaa dhidi ya wagombea wa vyama vingine.Kuweka wazi msimamo wangu haimaanishi chuki dhidi ya vyama hivyo na wagombea wake bali ni imani yangu kuhusu nani anayeweza kuipatia Tanzania “uhuru wa pili” (mapambano dhidi ya Watanzania wenzetu wanaotafuna raslimali zetu zaidi ya alivyofanya mkoloni).

Mwisho,nawahamasisha bloga wenzangu na vyombo vingine vya habari kwa ujumla kuweka bayana misimamo yao ili kuepuka lawama zinazoweza kujitokeza pale habari za vyama flani zinaponyimwa fursa katika vyombo hivyo.Endorsement ya mgombea au chama ni jambo la kawaida katika nchi za Magharibi lakini hii ni mara ya kwanza kwa chombo cha habari cha Kitanzania kufanya hivyo,na kwa hakika najivunia kuweka historia hiyo.

21 Aug 2010

20 Aug 2010

Pamoja na kumtetea mwanaye,JK alisema (namnukuu)"...hata kama aliyegombea hakuridhishwa na mazingira ya namna aliyeshinda alivyoshinda, ndiyo ameshapata,hivyo jambo la msingi ni kuacha makundi yaliyokuwepo wakati wa kura za maoni, bali wajielekeze katika kutafuta ushindi wa kishindo huku wakijiandaa kwa kugombea kipindi kingine..."SWALI.Je kama kutoridhishwa huko kunatokana na matumizi ya rushwa?Au kwa vile Awamu ya Nne ilikuwa na huruma kwa mafisadi basi wagombea waliofisadiwa nao waige mfano wa serikali hiyo?Soma habari kamili HAPA.

19 Aug 2010

I came across an article below in The Moscow Times of today (“Financial Investigator's Son Handles Cash for Aeroflot”) and thought it would be appropriate to rekindle the discussion on Nepotism in Tanzania we had with you a while ago, see my email of Aug. 11th herein under. Before that, in July this year, I made similar comments about the son of the former Russian prime minister {Mr. Mikhail Fradkov - now Head of the Russia’s Foreign Intelligence Service (SVR)}, Mr. Peter Fradkov, who is currently the deputy chairman of Vnesheconombank (Russia’s State Bank for Foreign Economic Relations) and also the deputy chairman of the African Coordinating Committee for Economic Cooperation with African Countries (AfroCom). See in the Aeroflot article mentioned above (read the yellow-shaded part below) on how other senior Russian government officials place their off-springs in honey places, a similar trend currently appearing in Tanzania, albeit at times we see off-springs of our officials involved in fraudulent crimes as you may read in the article below on the son (Tony) of CCM stalwart Kingunge Ngombale Mwiru (“Kingunge relative in the dock for forgery, 242 million/- theft”). As I wrote earlier, I don’t think putting kids and relatives of bigwigs in high places based on kinship only and not merit is a wise thing to do. Indeed, it is very dangerous and speaks a lot of the unhealthy political situation in a country as well as the existence of an incompetent and ineffective government .

Best regards,

Shaaban

Moscow, Russia

16 Aug 2010

Miongoni mwa mapungufu yanayowakabili baadhi ya Watanzania wenzetu ni kushindwa kusifia pale inapostahili.Na miongoni mwa "udhaifu" wangu ni kushindwa kujizuia kumwaga sifa pale inapostahili (au kukosoa pale inapobidi).Waingereza wana msemo "beauty should never be imprisoned", yaani-kwa Kiswahili- "urembo haupaswi kuwekwa jela".Mantiki ya msemo huo ni kuhamasisha jamii kusifia vinavyostahili sifa.Na kwa kufanya hivyo tunawafanya wanaostahili sifa hizo kutambua thamani yao na pengine kuboresha zaidi wafanyayo.

Nisijizungushe sana.Leo naomba kukujulisha msomaji wangu mpendwa moja ya blogu ambazo kila napozitembelea (na ninatembelea blogu nyingi kila siku ya Mungu) hupatwa na msisimko wa aina yake.Blogu hiyo si nyingine bali ni La Princessa World.Of course,ili ufahamu ni nachoongea hapa inabidi "yai liwe linapanda" (I mean,uwe unaimudu vema lugha ya Kiingereza) kwani mdada mwenye blogu hiyo "anakichezea Kiingereza namna anavyotaka".Na hiyo ni moja ya mambo yanayovutia katika "uandishi binafsi" (kwa mfano makala magazetini au bloguni): namna mwandishi anavyoweza kucheza na lugha apendavyo kama ambavyo mwanasoka mahiri anavyoweza kuuchezea mpira atakavyo.Tuseme uandishi unaoshabihiana na vipaji vya viumbe kama Ronaldinho,Messi,Zidane,nk.

Blogu ya La Princessa World imejikita zaidi kwenye masuala ya fasheni,wenye majina (celebrities),muziki,filamu na mambo mengine ya kusisimua.Yayumkinika kusema kuwa masuala ya fasheni ni ya akinadada zaidi lakini,binafsi,kanuni yangu ya kumudu kuwa "well-rounded" ni kujifunza mambo mengi kadri inavyowezekana.Na ni katika kufanya hivyo ndipo unaweza "kukopa" ujuzi na uelewa wa wengine waliobobea katika fani zao."Ugonjwa" wangu ni siasa lakini napendelea kuitanua siasa hadi kwenye maeneo mengine ya maisha,kwa mfano siasa za urembo,muziki,filamu,nk.Hata hivyo,by "kutanua" simaanishi kuchanganya siasa na urembo,kwa mfano,bali kama ilivyo katika "siasa proper" ,ninachofanya ni kuelewa kwa undani ishu kama trends,shakers and movers,siri na mbinu,na vitu kama hivyo.

Nimalizie kwa kukusihi uwe unamtembelea La Princessa kufaidika kama navyofaidiaka mie kila napotembelea hapo.Usitafsiri kama "nampigia mtu debe" bali,kama nilivyoandika awali,napenda kuenzi vipaji vya wenzetu na   pia kila mara napenda kuwajuza (kuwajulisha) wasomaji wangu wapendwa yale yote ambayo kwa mtizamo wangu nadhani yanafanya kila ziara yako mtandaoni ikupatie kitu kipa au "kile roho yako inapenda".

Kwa La Princessa,nachoweza kuandika kwa kifupi ni kuwa umesimika kiwango (setting the bar) katika kublogu sio kwa akina dada pekee bali hata kwa bloga wa kiume.Kinachonigusa zaidi ni namna unavyocheza na lugha,kitu mabcho sio tu kinaonyesha namna unavyoimudu bali pia unavyoweza kuitumia katika namna mwafaka kumburudisha msomaji wako.

Word up!

12 Aug 2010

Baada ya kimya cha miaka miwili na mwezi mmoja hatimaye nimerejea katika ulingo wa uandishi wa makala zangu za Raia Mwema Ughaibuni katika jarida maridhawa la Raia Mwema.Haikuwa rahisi kwangu kukaa kimya huku nchi yetu ikiteketezwa na mafisadi lakini ililazimu kuwa hivyo ili kujipanga upya.

Katika makala ya wiki hii nimeelezea kwa kifupi kilichonisibu hadi nikafikia uamuzi wa kusitisha uandishi wa makala hizo.Basi nisikupunguzie uhondo bali bonyeza kiunganishi kifuatacho usome habari na makala nyingine motomoto katika jarida makini la Raia Mwema pamoja na makala ya wiki hii yenye kichwa MASLAHI YA UMMA NI ZAIDI YA VYOTE.

10 Aug 2010





Miongoni mwa mambo yanayoipa kiburi CCM ni imani ilishamiri miongoni mwa viongozi wa chama hicho kuwa Watanzania hawana kumbukumbu,hawajui kutofautisha zuri na baya,wavumulivu kupita kiasi,na ni viumbe wa kupelekeshwa tu.Yayumkinika kuhitimisha kwamba imani hiyo ya viongozi hao inasababishwa na mambo makuu mawili:Kwanza,dharau,kiburi,ubinafsi,na kubwa zaidi ya yote,ufisadi.Sababu ya pili,ni namna Watanzania wengi wanavyoendelea kukiamini chama ambacho kilishawatelekeza miaka kadhaa iliyopita.

Katika sababu hii ya pili,mfano mzuri ni ule wa mume anayemnyanyasa mke kupindukia lakini mapenzi ya mke huyo yanazidi kudumu akitarajia mumewe atapatwa na akili au huruma.Kwa bahati mbaya,utiifu huo wa mke kwa mume mnyanyasaji huishia kutafsiriwa na mume huyo kuwa mkewe “amenasa kwenye zege”,hana ujanja wa kuomba talaka au kukabiliana na manyanyaso ya mume huyo.

Ni katika mantiki hiyo ndipo leo tunasikia kioja cha mwaka ambapo “msema chochote” wa CCM,Tambwe Hizza (ambaye bado anaugulia maumivu ya kubwagwa kwenye kura za maoni huko Temeke) akikurupuka na kudai Rais Jakaya Kikwete hajawahi kutamka kuwa “hataki kura za wafanyakazi”.

Huyu Tambwe ni mhuni,hana nidhamu kwa Watanzania (kama alivyokuwa mhuni kwa kuapa kumtukana mama yake mzazi),na anafikiri bado tunaishi katika zama zile ambapo kama mwananchi hakuhudhuria mkutano uliohutubiwa na kiongozi husika,basi tegemeo pekee ni magazeti ya CCM ya Uhuru na Mzalendo au “midomo ya serikali” yaani Radio Tanzania na Daily News.Na vyombo vyote hivyo vya habari vilikuwa na unyenyekevu wa kuchefua kwa namna vilivyokuwa vikifanya kila liwezekanalo kupendezesha hotuba au kauli za watawala wa enzi hizo.

Japo vyombo vya habari vya serikali (Habari Leo,Daily News na TBC) bado vimeendelea kukumbatia siasa za chama kimoja kwa kuipendelea CCM waziwazi na kupuuza kuwa vinaendeshwa kwa fedha za walipakodi (ambao takriban milioni 35 kati yao sio wanachama wa CCM) lakini angalau siku hizi tuna vyombo binafsi vya habari pamoja na social media (blogs,youtube,facebook,twitter,nk) na hiyo inasaidia kwa kiasi kikubwa “kutofautisha mchele na pumba”.

Lakini kutokana na dharau zao na kutojali,Tambwe na CCM wanajifanya hawajui kuwa hotuba ya Kikwete kuhusu tishio la mgomo wa wafanyakazi ipo mtandaoni.Mtandaoni kuna video zenye hotuba hiyo,na uzuri wa mtandao ni kwamba unahifadhi kumbukumbu vyema sana.Kwahiyo hata kama CCM wangetaka “kufuta maneno hayo ya JK” bado wangekabiliwa na kigingi katika kufuta kumbukumbu zilizozagaa mtandaoni.Pengine wanafahamu sana kuhusu hilo lakini wanajipa matumaini kwa kuamini kuwa “Watanzania ni wanyonge sana na hawaweza kusaka kumbukumbu za kauli hiyo ya Kikwete”.Au pengine ni jeuri tu ya madaraka na imani kwamba kiongozi ana ruhusa ya kuahidi chochote,kusema lolote na kufanya chochote na asihukumiwe na umma.

Leo Tambwe anasema Kikwete hajawahi kutamka kuwa hahitaji kura za wafanyakazi.Je atakanusha pia kuwa Kikwete hajawahi kusema mimba za wanafunzi wa kike ni kiherehere chao?Au hakuwahi kutamka kuwa hajui kwanini Tanzania ni masikini?Au hajawahi kutamka kuwa anawafahamu wala rushwa lakini anawapa muda wa kujirekebisha?Au hakuwahi kuahidi kuwa maisha bora kwa kila Mtanzania yanawezekana?Au Tambwe pia atakabusha kuwa Kikwete hakutumia mfano wa MBAYUWAYU?

Kwani Tambwe au CCM,au hata JK mwenyewe,hawakukanusha habari zilizoandikwa na gazeti la Mwananchi chapisho la mtandaoni Mei 3, 2010 na kupewa kichwa cha habari "JK: Nipo Tayari Kukosa Kura Zenu" na kumnukuu "(Kikwete) alifafanua kuwa kima cha chini cha mshahara cha Sh315,000 kwa mwezi kinachopigiwa debe na Tucta, serikali haiwezi kukitekeleza na kama hilo ni shinikizo kwake ili wafanyakazi wampatie kura kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, hahitaji kura zao". (BONYEZA HAPA KUSOMA HABARI HIYO)

Ni dhahiri hili zoezi la kukanusha kauli halitafanikiwa.Liliwezekana katika zama ambapo Watanzania uhuru na access ya habari ilikuwa kwa ridhaa ya watawala lakini sio sasa ambapo blogs,webforums,facebook,twitter,youtube,nk zinapatikana kila kona ya dunia alimradi kuna internet connection.

Dharau na jeuri ya CCM iliwafanya wajisahau kwenye usingizi wa pono huku JK akitoa baadhi ya kauli zisizotarajiwa kutoka kwa mwanasiasa anayetarajia kuomba tena ridhaa ya wananchi kuwaongoza tena.Wakati huo walikuwa na uhakika wa asilimia zaidi ya 100 kuwa JK na CCM yake kurejea madarakani ni suala la muda tu na sio “if watarejea”.Lakini ghafla,baada ya Chadema kumtangaza Dkt Wilbroad Slaa kuwa mgombea wake wa nafasi ya urais,CCM wametahayari.Hawakuona umuhimu wa kukanusha kauli hiyo ya JK mpaka baada ya kumsikia Dkt Slaa akiwaeleza wafanyakazi kuwa “anahitaji kura ambazo Kikwete hazihitaji”.Ghafla,CCM wanakugundua kuwa kauli hiyo haikuwa mwafaka,lakini kwa dharau zao badala ya kuomba radhi au kutafuta suluhu wanakimbilia kukanusha.

Nimeandika makala kadhaa katika blogu yangu kuhusu umuhimu wa CCM kuwaomba radhi Watanzania kwa madudu mbalimbali waliyotufanyia badala ya wao kuendelea kujigamba kuhusu “mafanikio yaliyopatikana katika utawala wao”.Yani wanataka kutuambia kuwa hata kushamiri kwa ufisadi ni mafanikio?Kwanini wasingetumia busara ya kutueleza “mafanikio” yao kisha wakaonyesha uungwana kwa kueleza maeneo ambayo kimsingi “wametuangusha”?Hawawezi kufanya hivyo kwa vile wanatudharau,wanatuona wajinga tusiojua kutenganisha mema na mabaya,wasahaulifu tusiokumbuka hata mahitaji yetu muhimu.

Tayari chama hicho tawala kimeshaonyesha “mchecheto” kwa kukacha kushiriki mdahalo wa wagombea urais kabla ya “kulialia” kuwa Chadema inacheza rafu “kwa kuanza kampeni kabla ya muda wake”.Ukichanganya na songombingo linaloendelea ndani ya chama hicho katika mchakato wa kupata wagombea wa nafasi mbalimbali katika uchaguzi ujao ni dhahiri kuwa kwa mara ya kwanza CCM inaanza kuona dalili za kung’olewa madarakani.Na huenda moto mkubwa zaidi ukawaka ndani ya chama hicho baada ya mchujo wa wagombea baadaye mwezi huu.

Tahayari iliyowakumba CCM inaweza kuwa silaha nzuri kwa Dokta Slaa na Chadema kwa ujumla.Kwa kauli kama hizi za akina Tambwe,ni rahisi kwa Chadema kuwaonyesha Watanzania namna gani chama hicho kinavyowadharau.Ndio!Kwani kama si dharau ni nini basi pale mtu anapokutukana halafu baada ya kitambo akaibuka na kukanusha kuwa hajakutukana japo ushahidi upo bayana?CCM inajikaanga kwa mafuta yake yenyewe.Dharau na jeuri yao inaweza kuwa mtaji mzuri wa anguko lake.

Kwa wale wote wenye uchungu wa dhati kwa nchi yetu na waliochoka kufisadiwa na CCM,kitendo cha chama hicho kukanusha kuwa JK hajawahi kukataa kura za wafanyakazi kinapaswa kutafsiriwa kama namna Watanzania “watakavyoingizwa mkenge tena kama mwaka 2005” ambapo chama hicho kiliahidi mambo chungu mbovu lakini badala yake matokeo ni kushamiri kwa ufisadi.Kama mwenyekiti wa chama hicho anaweza kutoa kauli hadharani kisha chama chake kikaibuka kudai kuwa hajatoa kauli hiyo,je kwanini tusiamini kuwa mgombea urais wa chama hicho (JK) ataishia kupuuza ahadi anazotoa sasa na wakati wa kampeni,na CCM ikiulizwa ikaishia kukanusha kuwa hajwahi kuahidi hivyo?

Watanzania sasa tumepatiwa nafasi adimu ya kuondokana na CCM.Katika chaguzi zilizotangulia tulikuwa hatuna uhakika na wagombea waliosimamishwa kuchuana na mgombea wa CCM lakini safari hii tumebahatika kupata mtu ambaye rekodi yake inajidhihirisha bayana.Na kwa namna ambayo haijawahi kutokea katika historia ya chaguzi nchini mwetu ambapo CCM inaonekana ikianza kutahayari waziwazi baada ya mwamko ulioletwa na Chadema na Dkt Slaa,huo ni uthibitisho tosha kuwa mafisadi wamegundua kuwa siku zao zinahesabika.

Tusirejee makosa ya huko nyuma ya kujaa kwenye mikutano lakini kura zinakwenda CCM.Safari hii,acha watoe rushwa zao (na mzipokee tu kwa vile ni fedha walizowafisadi) lakini kura ziende kwa Dkt Slaa.Dawa ya kung’oa ufisadi ni kung’oa mmea unaolea ufisadi,na mmea huo ni CCM.


Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.