15 Sept 2016


NIANZE makala hii kwa kutoa salamu za rambirambi na pole kutokana na vifo vilivyosababishwa na tetemeko la ardhi lililotokea Jumamosi iliyopita huko Bukoba. Hadi wakati ninaandika makala hii jumla ya watu 16 walikuwa wamepoteza maisha huku wengine zaidi ya 200 wakiwa wamejeruhiwa.
Jinsi janga hilo lilivyochukuliwa kwa kiasi kikubwa ‘kama tukio la kawaida’ huku baadhi ya wenzetu wakiendelea na tamasha la muziki wakati tunapaswa kuwa katika maombolezo ya kitaifa, imenifanya nijikute katika tafakuri kuhusu uhusiano kati yetu na nchi yetu.
Ukiacha ‘mbwembwe’ za hapa na pale, huku nyingi zikiwa za kinafiki, Watanzania wengi wanaielezea vibaya nchi yao. Si jambo la kushangaza kusikia mtu akidai ni bora kuzaliwa paka Ulaya kuliko kuzaliwa binadamu Tanzania. Kadhalika, siku hizi imezoeleka kusikia baadhi ya wenzetu wakidai bora nchi yetu ilipokuwa chini ya utawala wa mkoloni kuliko hali ilivyo sasa.
Na kwa akina sisi tulio nje ya nchi tukijaribu kuchangia japo kwa mawazo tu kuhusu mustakabali wa tafa letu, tunaishia kuambiwa tunajipendekeza…tunataka ukuu wa wilaya na vitu vya kukatisha tamaa kama hivyo.
Tofauti za kiitikadi zimechangia kuimarisha ‘chuki dhidi ya Tanzania,’ ambapo kwa upande mmoja, wengi wa wafuasi wa chama tawala CCM wamekuwa wakijaribu kujenga picha kuwa wafuasi wa vyama vya upinzani ‘sio Watanzania kamili,’ huku kwa upande mwingine, wafuasi wengi wa vyama vya upinzani wakijaribu kujenga picha ya Tanzania kama nchi mbaya kabisa duniani kutokana na utawala wa CCM.
Kuna kitu kinafahamika kama ‘national psyche’ au saikolojia ya taifa – kwa maana nyepesi, sisi kama Watanzania tunajionaje? Na sisi kama Watanzania tunalichukuliaje taifa letu?  Tukiweka kando ‘mabaya’ kama rushwa, ufisadi na umasikini wetu, je kuna lolote tunalojivunia kuhusu nchi yetu? Tunapoona yanayojiri nchi kama Burundi, Somalia na Sudan ya Kusini, tunatambua thamani ya tulichonacho ambacho baadhi ya wenzetu hawana?
Hii saikolojia ya taifa inaweza kuwa muhimu sana katika kuelezea kwanini uzalendo umekuwa ukiporomoka kwa kasi. Tunapowaona wenzetu wamejipaka rangi za bendera za nchi zao katika mechi za kimataifa au matukio muhimu yanayohusu mataifa yao sio suala la ushabiki tu bali mapenzi waliyonayo kwa nchi zao.
Kwa hapa Uingereza bendera yao ya ‘Union Jack’ inagusa na kuvuta hisia kali kwa Waingereza wengi kama ilivyo bendera ya Marekani, ‘Stars and Stripes.’ Lakini sio bendera tu, hata alama za kitaifa kama vile sanamu ya Kristo Mkombozi (Christ the Redeemer), jijini Rio, Brazil; Mnara wa Eiffel, Paris, Ufaransa; Mapiramidi ya Giza, Misri; Ukuta Mkuu wa China, Mnara wa Uhuru (Statue of Liberty), New York, Marekani, na ‘Jicho la London’ (London Eye) na Big Ben, jijini London, hapa Uingereza.
Sisi licha ya vivutio lukuki tulivyonavyo, mpaka leo ‘tunasuasua’ kuwa na utambulisho wa taifa letu. Kama ni Mlima Kilimanjaro, basi huo unafahamika zaidi kuwa upo Kenya kuliko Tanzania, na kama ni madini ya Tanzanite ambayo yanapatikana nchi kwetu pekee, ni India na Kenya ndizo zinazoongoza kwa mauzo ya madini hayo. Mchakato wa kusaka vazi la taifa umejifia kifo cha asili. Hii inatosha kueleza sie ni watu wa aina gani.
Lakini kinachokera zaidi ni kuona taifa limekumbwa na janga la tetemeko la ardhi lililotokea Jumamosi iliyopita huko Bukoba, na kusababisha vifo 16 na majeruhi zaidi ya 200 (hadi wakati ninaandika makala hii) lakini tukio hilo linaonekana kuwagusa zaidi watu walio nje ya Tanzania kuliko sisi Watanzania wenyewe.
Hivi inaingia akilini kweli kuona tamasha la burudani la Fiesta likifanyika Jumapili huko Singida katika kipindi cha majonzi ambapo Watanzania walikuwa wakiendelea kupata habari za kusikitisha (zaidi kupitia vyombo vya habari vya kimataifa) za kuongezeka idadi ya vifo na majeruhi? Katika hili lawama zinapaswa kwenda kwa waandaaji wa tamasha hilo, wasanii walioshiriki na wahudhuriaji. Hawa wote ni Watanzania na walipaswa ‘kuwa na mshipa wa aibu’ kuwafahamisha kuwa maombolezo ni muhimu zaidi ya burudani
Jumapili hiyo tena kulijitokeza mkanganyiko ambapo awali taarifa iliyotolewa na Ikulu ilieleza kuwa Rais Dk John Magufuli angesafiri kwenda Zambia kwenye sherehe ya kuapishwa Rais mteule wa nchi hiyo Edgard Lungu. Hivi kweli kabla ya kutolewa taarifa hiyo, wahusika walikuwa hawafahamu kuhusu kilichojiri huko Bukoba kiasi cha ‘kuamini’ kuwa Rais angeweza tu kusafiri?
Japo baadaye iliripotiwa kuwa Rais hatosafiri na badala yake atawakilishwa na Makamu wa Rais Samia Suluhu, baadhi yetu tulibaki na ‘sintofahamu’ kuhusu kilichopelekea mkanganyiko huo.
Hadi wakati ninaandika makala hii, mtandao wa kijamii wa Jamii Forums, blogu kadhaa za Tanzania na vyombo vya habari vya kimataifa ndio vimekuwa vikitoa ripoti za takriban kila saa kuhusu tukio hilo, ilhali vyombo vingi vya habari ‘vikiburudika na mapumziko ya mwisho wa wiki.’
Kitaifa, hakuna tamko la maombolezo ya kitaifa wala bendera kupepea nusu mlingoti. Tumezowea sana majanga, kama vile ajali mfululizo zinazogharimu maisha ya Watanzania lukuki, kiasi kwamba hatujali ‘kihivyo’ kilichotokea huko Bukoba?
Nimalizie makala hii kwa kutoa wito kwa Rais Magufuli kuangalia uwezekano wa kufanyika mjadala wa kitaifa kuhusu uhusiano wetu na Tanzania yetu, kushuka kwa kasi kwa uzalendo, na saikolojia ya taifa letu kwa ujumla. Kadhalika, ninamwomba Mungu awapumzishe mahali pema peponi Watanzania wenzetu waliouawa na tetemeko hilo la ardhi, sambamba na kumwomba awajalie ustahimilivu wafiwa, na uponyaji wa haraka kwa majeruhi wa janga hilo la kitaifa.
Baruapepe: [email protected] Blogu:www.chahali.com Twitter: @chahali  

11 Sept 2016

Tanzania yetu ipo katika msiba mkubwa (hata kama dalili za msiba hazionekane) kufuatia tetemeko la ardhi lililotokea jana alasiri kwenye eneo la ukanda wa Ziwa Viktoria, ambapo kwa mujibu wa taarifa, tetemeko hilo limepeleka vifo 13 hadi sasa na majeruhi takriban 200.



Tetemeko hilo la ardhi lilikuwa na ukubwa (magnitude) wa kati ya 5.7 na 5.9 (taarifa bado zinakanganya) lilitikisa pia baadhi ya maeneo yanayozunguka Ziwa Victoria nchini Uganda na pia baadhi ya maeneo nchini Rwanda na kidogo nchini Kenya.

Picha ziliowekwa kwenye mitandao ya kijamii zimeonyesha uharibifu mkubwa katika mji wa Bukoba wenye wakazi takriban 70,000, sambamba na vifo na majeruhi.

"Tukio hili limesababisha maafa makubwa... kwa sasa hali imetulia..." alisema Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, Deodatus Kinawila. "

Vipimo vya Idara ya Jiologia ya Marekani vinaonyesha kuwa tetemeko hilo la ardhi la kina cha kilomita 10 lilitokea saa 9.27 alasiri kwa saa za Afrika Mashariki.
Map showing Tanzania and Bukoba, where earthquake hit in September 2016
Bonde la Ufa la Afrika Mashariki linapita katika 'mstari wenye kasoro kijiolojia' (geologocal fault line), moja ya vyanzo vya matetemeko ya radhi duniani, lakini matukio ya matetemeko ya ardhi yamekuwa ni ya nadra.
Julai mwaka 2007, tetemeko la ardhi la 'magnitude' sita lilitokea Arusha, mkoa uliopo mashariki mwa Bukoba.

Kijiolojia, Bonde la Ufa la Afrika Mashariki linapita katika eneo kulikotokea tetemeko hilo la ardhi. Kwa kifupi, chanzo cha tetemeko hilo ni kutokana na tabaka la miamba katika eneo husika kuwa fukuto jingi la joto na kusigana kwa miamba, hali ambayo hupelekea miamba kukatika, na hiyo hupelekea ardhi itikisike.

Kwa maelezo ya kina kuhusu chanzo cha matetemeko ya ardhi, BONYEZA HAPA 

MIMI BINAFSI NINATOA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KWA FAMILIA ZA MAREHEMU 13 WALIOFARIKI KUTOKANA NA TETEMEKO HILO, NA POLE KWA MAREJURHI TAKRIBAN 200. POLENI SANA WAFIWA NA NINAWAOMBEA MAJERUHI UPONYAJI WA HARAKA.





1 Sept 2016

WIKI iliyopita, Rais Dk. John Magufuli alimteua Dk. Modestus Kipilimba kuwa Mkurugenzi Mkuu (DGIS) wa Idara ya Usalama wa Taifa (TISS). Uteuzi huo umefanyika baada ya kustaafu kwa mkurugenzi mkuu aliyemaliza muda wake, Othman Rashid.
Kwa mtizamo wangu, kama kuna kitu ambacho kinaweza kuzua maswali kuhusu uteuzi huo basi ni wadhifa wa Mkurugenzi wa Majanga (Director of Risk Management) alioshikilia Dk. Kipilimba akiwa mtumishi wa Benki Kuu ya Tanzania.
Tunafahamu Benki Kuu imekuwa ikiandamwa na matukio mfululizo ya ufisadi, kuanzia EPA hadi Tegeta Escrow. Kwa wadhifa wake katika taasisi hiyo, kuna uwezekano wa bosi huyo mpya wa mashushushu kuonekana sehemu ya mfumo ulioshindwa kudhibiti ufisadi. Hata hivyo, utetezi unaweza kuwa huenda yeye alitekeleza majukumu yake vema lakini walio juu yake hawakuchukua hatua stahili.
Changamoto kubwa kwa Dk. Kipilimba ni pamoja na kurejesha hadhi na heshima ya Idara ya Usalama wa Taifa. Wanaoilaumu taasisi hiyo hawamaanishi kuwa watumishi wake wanahusika katika baadhi ya matukio ya kihalifu bali kushindwa kwa Idara hiyo kukabiliana na kushamiri kwa matendo hayo ya kihalifu, ambayo kimsingi ni matishio kwa usalama wa taifa, na kazi kuu ya Idara hiyo ni kukabiliana na matishio kwa usalama wa taifa la Tanzania.
Ninaamini kuwa Dk. Kipilimba anafahamu kanuni muhimu kuhusu ufanisi au upungufu wa idara ya usalama wa taifa popote pale duniani, kwamba kushamiri kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa lolote lile ni kiashiria cha upungufu katika idara ya usalama wa taifa ya nchi husika na kudhibitiwa kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa popote pale duniani ni kiashiria cha uimara wa idara ya usalama wa taifa ya nchi husika.
Kwahiyo, kwa kuzingatia kanuni hiyo, kushamiri kwa biashara ya dawa ya kulevya, ujangili, rushwa na ufisadi mwingine ni viashiria vya kasoro ya Idara yetu ya Usalama wa Taifa.
Changamoto nyingine kwa Dk. Kipilimba ni tuhuma za mara kwa mara dhidi taasisi hiyo muhimu kabisa kuwa katika utendaji kazi wake imegeuka kuwa kama kitengo cha usalama cha chama tawala CCM. Idara hiyo imekuwa ikituhumiwa kuwa kwa kiasi kikubwa imeweka kando taaluma ya ushushushu (tradecraft) na kutekeleza majukumu yake kisiasa.
Madhara ya muda mfupi ya kasoro hiyo ni taasisi hiyo kujenga uhasama na vyama vya upinzani na kwa namna fulani kupoteza heshima na uhalali wake. Lakini la kuogofya zaidi ni madhara ya muda mrefu, ambapo watu wanaoweza kuwa ni matishio kwa usalama wa taifa letu wanaweza kutumia ‘urafiki’ unaodaiwa kuwepo kati ya Idara ya Usalama wa Taifa na CCM, wakitambua bayana kuwa Idara haina muda na makada wa chama tawala na hatimaye kufanikiwa kutimiza azma zao ovu.
Baadhi ya watumishi wa zamani wa taasisi hiyo walijikuta matatizoni kwa vile tu walitekeleza majukumu yao dhidi ya wanasiasa wa chama tawala na wakaishia kuonekana kama wahaini.
Changamoto nyingine kwa Dk. Kipilimba ni tuhuma zinazoikabili taasisi hiyo kuhusu mfumo wa ajira ambapo inadaiwa kuwa zimekuwa zikitolewa kwa upendeleo kwa ndugu na jamaa za vigogo. Tatizo kubwa hapa ni kwamba utiifu wa ndugu na jamaa hao wa vigogo haupo kwa taifa bali kwa vigogo hao waliowaingiza Idarani. Pengine sio vibaya kufikiria ‘utaratibu wa wazi’ katika ‘recruitment’ kama inavyofanywa na wenzetu wa CIA, NSA, MI5, MI6 au HGCQ wanaotangaza nafasi za ajira kwenye vyombo vya habari.
Pia kuna tatizo la baadhi ya maofisa usalama wa taifa ‘kujiumbua’ kwa makusudi kwa sababu wanazojua wao wenyewe, kubwa ikiwa kutaka sifa tu, au waogopwe mtaani. Hii inaathiri sana ufanisi wa maafisa wa aina hiyo kwani ni vigumu kutekeleza majukumu yao ipasavyo pasi usiri.
Sambamba na hilo ni kasumba ya muda mrefu ambapo baadhi ya maafisa wa Idara hiyo waliopo kwenye vitengo mbalimbali kuwepo huko kwa muda mrefu mno kiasi cha kuathiri utendaji wao.
Changamoto nyingine kubwa ni uwepo wa majasusi kibao nchini mwetu, hususan kutoka nchi moja jirani, huku wengi wa majasusi hao wakiwa wameajiriwa katika taasisi za umma na binafsi. Hili ni tishio kubwa kwa usalama wa taifa letu. Licha ya hilo, kiintelijensia, kila ‘nchi rafiki’ ni ‘adui yetu’ muda huu tulionao au siku zijazo.
Kwa upande wa fursa kwa Dk. Kipilimba, licha ya kuwa ‘mwenyeji’ katika taasisi hiyo muhimu, wasifu wake kitaaluma unamweka katika nafasi nzuri sana kukabiliana na changamoto za karne ya 21 ambayo imetawaliwa zaidi na teknolojia ya kisasa.
Dk. Kipilimba ni msomi aliyebobea kwenye teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) na yayumkinika kuamini kuwa anaweza kutumia usomi wake kuibadilisha Idara ya Usalama wa Taifa kwenda na wakati, kufanya kazi kama taasisi ya kishushushu ya karne ya 21.
Fursa nyingine kwa Dk. Kipilimba ni matarajio ya kuungwa mkono vya kutosha kutoka kwa Rais Magufuli ambaye kama alivyoahidi wakati wa kampeni za kuwania urais, mapambano dhidi ya ufisadi yamepewa kipaumbele cha hali ya juu kabisa.
Sambamba na hilo ni Idara hiyo kuangalia uwezekano wa kutumia hazina kubwa tu ya maafisa wake wa zamani, hususan wastaafu. Ikumbukwe kuwa wengi wao ni watu wanaowindwa na makundi au taasisi mbalimbali zinazolenga kulihujumu taifa letu.
Nimalizie makala hii kwa kutoa pongezi za dhati kwa Dk. Kipilimba na Naibu wake (DDGIS) Robert Msalika, sambamba na kumtakia mapumziko mema Mkurugenzi mstaafu Othman na kumkaribisha uraiani.
Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

27 Aug 2016

Tarehe 24 mwezi huu, Rais Dokta John Magufuli alimteua Dokta Modestus Kipilimba kuwa Mkurugenzi Mkuu (DGIS) wa Idara ya Usalama wa Taifa (TISS). Uteuzi huo umefanyika kufuatia kustaafu kwa mkurugenzi aliyemaliza muda wake, Othman Rashid.

Makala hii inajikita katika uchambuzi wa uteuzi huo kwa kuangalia changamoto na fursa zinazomkabili kiongozi huyo mkuu wa taasisi hiyo nyeti kabisa. Kwa mtizamo wangu, kama kuna kitu ambacho kinaweza kuzua maswali kuhusu uteuzi huo basi ni wadhifa wa Director of Risk Management alioshikilia Dokta Kipilimba huko nyuma alipokuwa mtumishi wa Benki Kuu ya Tanzania.

Sote twafahamu jinsi Benki Kuu yetu imekuwa ikiandamwa na matukio mfululizo ya ufisadi, kuanzia EPA hadi Tegeta Escrow. Kwa wadhifa wake katika taasisi hiyo, kuna uwezekano wa bosi huyo mpya wa mashushushu kuonekana ‘sehemu ya mfumo ulioshindwa kudhibiti ufisadi.’ Hata hivyo, utetezi unaweza kuwa huenda yeye alitekeleza majukumu yake vema lakini walio juu yake hawakuchukua hatua stahili.

Kadhalika, huko mtandaoni kuna ‘tuhuma’ kadhaa kuhusu Dokta Kipilimba, lakini itakuwa sio kumtendea haki yeye, blogu hii na mie mwenyewe kujadili tuhuma ambazo hazina ushahidi wowote. Ni muhimu kutambua kuwa Tanzania yetu licha ya kuwa kisiwa cha amani pia ni kisiwa cha majungu, uzandiki, fitna, umbeya na uzushi.

Changamoto kubwa kwa Dokta Kipilimba ni pamoja na kurejesha hadhi na heshima ya Idara ya Usalama wa Taifa. Katika miaka ya hivi karibuni, taasisi hiyo muhimu kabisa imekuwa ikishutumiwa kuwa inachangia ustawi wa ufisadi, ujangili, biashara ya madawa ya kulevya, nk.

Wanaoilaumu taasisi hiyo hawamaanishi kuwa watumishi wake wanahusika katika matukio hayo ya kihalifu as such bali kushindwa kwa Idara hiyo kukabiliana na kushamiri kwa matendo hayo ya kihalifu, ambayo kimsingi ni matishio kwa usalama wa taifa, na kazi kuu ya Idara hiyo ni kukabiliana na matishio kwa usalama wa taifa la Tanzania.

Ninaamini kuwa Dokta Kipilimba anafahamu kanuni muhimu kuhusu ufanisi au mapungufu ya idara ya usalama wa taifa popote pale duniani, kwamba “kushamiri kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa lolote lile ni kiashiria cha mapungufu ya idara ya usalama wa taifa ya nchi husika, na kudhibitiwa kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa popote pale duniani ni kiashiria cha uimara wa idara ya usalama wa taifa ya nchi husika.”

Kwahiyo, kwa kuzingatia kanuni hiyo, kushamiri kwa biashara ya madawa ya kulevya, ujangili, rushwa, na ufisadi mwingine ni viashiria vya mapungufu ya Idara yetu ya Usalama wa Taifa.

Changamoto nyingine kwa Dokta Kipilimba ni tuhuma za mara kwa mara dhidi taasisi hiyo muhimu kabisa kuwa katika utendaji kazi wake imegeuka kuwa kama ‘kitengo cha usalama cha chama tawala CCM.’ Idara hiyo imekuwa ikituhumiwa kuwa kwa kiasi kikubwa imeweka kando taaluma ya ushushushu (tradecraft) na kutekeleza majukumu yake kisiasa.

Madhara ya muda mfupi ya kasoro hiyo ni taasisi hiyo kujenga uhasama na vyama vya upinzani na kwa namna flani kupoteza heshima na uhalali wake. Lakini la kuogofya zaidi ni madhara ya muda mrefu, ambapo watu wanaoweza kuwa ni matishio kwa usalama wa taifa letu wanaweza kutumia ‘urafiki’ unaodaiwa kuwepo kati ya Idara ya Usalama wa Taifa na CCM, wakitambua bayana kuwa ‘Idara haina muda na makada wa chama tawala,’ na hatimaye kufanikiwa kutimiza azma zao ovu.

Baadhi ya watumishi wa zamani wa taasisi hiyo walijikuta matatizoni kwa vile tu walitekeleza majukumu yao dhidi ya wanasiasa wa chama tawala, na wakaishia kuonekana kama wahaini.

Changamoto nyingine kwa Dokta Kipilimba ni tuhuma zinazoikabili taasisi hiyo kuhusu mfumo wa ajira ambapo inadaiwa kuwa zimekuwa zikitolewa kwa upendeleo kwa ndugu na jamaa za ‘vigogo.’ Tatizo kubwa hapa ni kwamba utiifu wa ‘ndugu na jamaa hao wa vigogo’ haupo kwa taifa bali kwa vigogo hao waliowaingiza Idarani. Pengine sio vibaya kufikiria ‘utaratibu wa wazi’ katika ‘recruitment’ kama inavyofanywa na wenzetu wa CIA, NSA, MI5, MI6, HGCQ, nk wanaotangaza nafasi za ajira kwenye vyombo vya habari.

Pia kuna tatizo la baadhi ya maafisa usalama wa taifa ‘kujiumbua’ kwa makusudi kwa sababu wanazojua wao wenyewe, kubwa ikiwa kutaka sifa tu, au waogopwe ‘mtaani.’ Hii inaathiri sana ufanisi wa maafisa wa aina hiyo kwani ni vigumu kutekeleza majukumu yao ipasavyo pasi usiri.

Sambamba na hilo ni kasumba ya muda mrefu ambapo baadhi ya maafisa wa Idara hiyo waliopo kwenye vitengo mbalimbali kuwepo huko kwa muda mrefu mno kiasi cha kuathiri utendaji wao. Miongoni mwa maeneo hayo ni pamoja na ‘vituo muhimu’ na kwenye ofisi za balozi zetu nje ya nchi. Ikumbukwe kuwa unless afisa ametengeneza deep cover, uwepo wake kwa muda mrefu katika sehemu aliyokuwa ‘penetrated’ au kituo chake cha kazi kwingineko (mfano ubalozini) unaweza kupelekea ‘akaungua’ (burned).

Changamoto nyingine kubwa ni uwepo wa majasusi kibao nchini mwetu, hususan kutoka nchi moja jirani, huku wengi wa majasusi hao wakiwa wameajiriwa katika taasisi za umma na binafsi. Hili ni tishio kubwa kwa usalama wa taifa wa Tanzania yetu.

Kwa upande fursa kwa Dokta Kipilimba, licha ya kuwa ‘mwenyeji’ katika taasisi hiyo muhimu, wasifu wake kitaaluma unamweka katika nafasi nzuri sana kukabiliana na changamoto za karne ya 21 ambayo imetawaliwa zaidi na teknolojia ya kisasa.

Dokta Kipilimba ni msomi aliyebobea kwenye teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) na yayumkinika kuamini kuwa anaweza kutumia usomi wake kuibadilisha Idara yetu ya Usalama wa Taifa kwenda na wakati, kufanya kazi kama taasisi ya kishushushu ya karne ya 21, ambayo licha ya kutegemea HUMINT inaweza pia kutumia njia nyingine za kukusanya taarifa za kiusalama kwa kutumia teknolojia (GEOINT, MASINT, SIGINT, CYBINT, FININT na TECHINT kwa ujumla)

Na katika kwenda na teknolojia ya kisasa, basi pengine si vibaya iwapo Idara yetu ikafikiria haja ya uwepo wake kwenye mtandao, kwa kuwa na tovuti yake kamili na pia kufungua akaunti kwenye mitandao ya kijamii, hususan Twitter na Facebook. Hii sio tu inaweza kusaidia kutengeneza "human face" ya intel service bali pia yatoa fursa nzuri katika OSINT.

Fursa nyingine kwa Dokta Kipilimba ni matarajio ya sapoti ya kutosha kutoka kwa Rais Dokta Magufuli ambaye kama alivyoahidi wakati wa kampeni za kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka jana, mapambano dhidi ya ufisadi yamepewa kipaumbe cha hali ya juu kabisa. Kama ‘sponsor’ na ‘consumer’ wa taarifa za kila siku usalama, inatarajiwa kuwa Dokta Magufuli atatekeleza ushauri wa Idara katika kukabiliana na matishio mbalimbali ya usalama wa taifa letu.

Dokta Kipilimba ana fursa ya kuleta mageuzi kwa Idara ya Usalama wa Taifa kwa kuangalia uwezekano wa kuwafikia watu walio nje ya taasisi hiyo, hasa pale uwezo wa Idara yetu unapokuwa limited. Nitoe mfano. Katika kupata taarifa mwafaka wa kudumu kuhusu, kwa mfano, mgogoro wa kisiasa huko Zanzibar, Idara inaweza ku-reach out wanazuoni wa historia ya taifa letu walipo ndani na nje ya nchi yetu.

Ikumbukwe kuwa sio rahisi kwa taasisi hiyo kuwa na maafisa au watoa habari katika kila eneo. Wenzetu wa nchi za Magharibi wamekuwa wakikabiliana na hali hiyo kwa kufanya kazi na ‘makandarasi’ (contractors), ambao of course, wamekidhi taratibu kama vile vetting.

Sambamba na hilo ni Idara hiyo kuangalia uwezekano wa kutumia hazina kubwa tu ya maafisa wake wa zamani, hususan wastaafu. Ikumbukwe kuwa wengi wao ni watu wanaowindwa na ‘subjects’ mbalimbali wanaolenga kulihujumu taifa letu.

Nimalizie makala hii kwa kutoa pongezi za dhati kwa Dokta Kipilimba na Naibu wake (DDGIS) Robert Msalika, sambamba na kumtakia mapumziko mema Mkurugenzi mstaafu Othman, na kumkaribisha ‘uraiani.’

MUNGU IBARIKI TANZANIA, MUNGU IBARIKI IDARA YETU YA USALAMA WA TAIFA




26 Aug 2016

Msanii nguli wa Bongo Movies, Gabo Zigamba, anatoa tahadhari kuhusu matapeli mbalimbali wanaotumia jina lake. Awali, msanii huyo alipoteza simu mbili za mkononi, ambazo baadaye zilikuwa zikitumiwa na matapeli hao kuomba misaada kwa watu mbalimbali wakijifanya kuwa wao ndio Gabo.
Kadhalika, majuzi, akaunti ya Facebook ya msanii huyo ilidukuliwa na ikatumika kwa muda na matapeli hao kwa kujifanya wao ndio msanii huyo. Hatimaye alifanikiwa kuirejesha akaunti hiyo katika himaya yake.
Gabo ameeleza kuwa anahisi kuwa yeye ndio msanii anayeongoza kwa jina lake kutumiwa na matapeli kwa sababu amekuwa akipata taarifa mbalimbali kuhusu watu wanaotumia jina lake, kwa mfano binti mmoja aliyejifanya ndiye Gabo na amekuwa akitapeli kwa kudai anauza mabegi.


Msanii huyo ametoa wito kwa Watanzania kuwa makini na watu wanaotumia majina ya watu wengine, hususan watu maarufu, kwa minajili ya kutapeli. Amesema kuwa yupo katika mchakato wa uzinduzi mpya wa akaunti zake mbalimbali za mitandao ya kijamii ili, pamoja na sababu nyingine, iwe rahisi kwa watu kuwasiliana nae pindi wanapokumbana na matapeli hao wanaotumia jina lake.

20 Aug 2016



Kwanza kabla ya kuingia kwa undani katika uchambuzi huu, ni vema nikaweka bayana uhusiano wangu na watu wawili ninaowaongelea katika makala hii: Rais John Magufuli na aliyekuwa RC wa Arusha Felix Ntibenda. 

Oktoba mwaka 2006, nilianza kufuatilia kilichokuja kujulikana baadaye kama 'skandali ya Richmond' (rejea HAPA na HAPA  na hatma yake HAPA). Kwa kifupi, nilikuwa bloga pekee niliyelivalia njuga suala la Richmond, tangu mwanzo wake hadi Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, alipolazimika kujiuzulu.

Wasichoelewa watu wengi ni kwamba uamuzi wangu wa kufuatilia suala hilo ulinigharimu mno, kikazi, kimasomo na kimaisha kwa ujumla. Laiti ningelipa kisogo suala hilo basi leo hii ningeendelea kuwa mtumishi wa umma. Hata hivyo, sijilaumu wala kusikitika kwa sababu mabadiliko yanahitaji kujitoa mhanga.

Lakini niwe mkweli, yaliyonisibu kutokana na ufuatiliaji wangu wa suala hilo yameniachia kinyongo, na ni kinyongo hicho kilichopelekea uamuzi wa kumuunga mkono mpinzani mkuu wa Lowassa katika kampeni za uchaguzi mkuu wa Rais mwaka jana. Pamoja na 'tofauti zangu na CCM' haikuwa vigumu kwangu 'kuungana nao dhidi ya our common enemy.' Waingereza wanasema 'chuki ya pamoja na mwanzo wa urafiki.'

Hiyo ndio iliyokuwa sababu ya kumpigia debe mgombea wa CCM, Dkt John Magufuli. Na kwa vile kabla ya hapo nilikuwa nikiunga mkono harakati za vyama vya upinzani, hususan Chadema, uamuzi huo wa kumsapoti mgombea wa CCM ulipelekea mie kuonekana 'msaliti,' nikamwagiwa idadi kubwa tu ya matusi, huku baadhi ya 'waungwana' wakidai kuwa nilikuwa najikomba kwa ajili ya kutaka u-DC.

Kufupisha stori, sio tu kuwa kama Mtanzania nina haki na uhuru wa kupongeza au kumkosoa Rais Magufuli bali pia ukweli kuwa nilikuwa miongoni wa waliompigia kampeni unaniongezea haki na uhuru huo.

Na katika makala hii ninatumia uhuru huo na haki hiyo kwa kumkosoa kidogo Rais wangu katika 'tumbua majipu' yake. Ninasema 'kumkosoa kidogo' kwa sababu kwa ninamuunga mkono kwa kiasi kikubwa katika jitihada zake za 'kuinyoosha Tanzania yetu,' ikiwa ni pamoja na umuhimu wa utumbuaji majipu.

Waingereza wana msemo kwamba sio kila jambo sahihi ni zuri na sio kila jambo zuri ni sahihi.Ntakupa mfano. Ukitembelewa na mtu mwenye njaa kali, waweza kukimbilia kumpa chakula kingi ili aondoe njaa hiyo. Kwa kufanya hivyo waweza kumpelekea akavimbiwa au hata akapoteza maisha (yes, mlo 'wa ghafla' waweza kuuwa mtu). Kinachopaswa kufanyika katika hali hiyo ni kwanza kumpatia mwenye njaa huyo kimiminika cha moto, kama vile uji au chai kabla ya kumpatia mlo kamili.

Mfano huo unaonyesha kuwa jambo sahihi la kumpatia mlo mwenye njaa lingeweza kuwa na matokeo yasiyo mazuri, yaani kuvumbiwa kwa mwenye njaa au hata kupoteza maisha.  Na laiti mwenye njaa huyo angepewa kwanza uji badala ya mlo mzito, angeweza kuhisi kuwa mwenyeji wake 'amepuuza njaa yake' kwa kumpa uji badala ya ugali/wali. Kwahiyo hapa jambo sahihi linatafsiriwa kuwa sio zuri.

Kwa mantiki hiyohiyo, utumbuaji majipu wa Rais Magufuli ni jambo sahihi kabisa, lakini kuna nyakati utekelezaji wake unaleta taswira isiyo nzuri.

Na hapa nitolee mfano wa tukio lililotokea juzi ambapo wadhifa wa aliyekuwa Mkuu wa Arusha Felix Ntibenda ulitenguliwa pasipo kutolewa maelezo yoyote.

Kwanza kitendo tu cha kutengua wadhifa wa mwakilishi mkuu wa Rais katika mkoa, bila kujali kuwajulisha wananchi ni kuwanyima haki na pia kutomtendea haki aliyetenguliwa. Ikumbukwe kuwa penye ukosefu wa taarifa sahihi, majungu au uzushu huziba pengo hilo.

Nilibainisha awali kuwa ninafahamiana na Ndugu Ntibenda. Ni mtu aliyewahi kuwa 'mwalimu' na kiongozi wangu wakati nikiwa mtumishi wa serikali huko nyuma. Misingi aliyonipatia wakati nikiwa chini yake ilipelekea nami kupewa promosheni ambayo ilidumu hadi wakati ninaondoka huko nyumbani kuja huku Uingereza kimasomo. Na sio mie pekee bali Ndugu Ntibenda 'aliwapika' lundo la maafisa ambao wengi leo hii ni watu muhimu kabisa kwa usalama wa taifa letu.


Kwa tunaomfahamu, licha ya uchapakazi wake usio na mfano, Ndugu Ntibenda ana utu wa kipekee. Na hicho ndio kilichmfanya awe kiongozi mzuri. Walio chini yake walikuwa kama sehemu ya familia yake.

Niwe mkweli, niliposikia kada fulani wa CCM ameteuliwa kuwa mkuu wa wilaya katika mkoa wa Arusha uliokuwa chini ya Ndugu Ntibenda nilipatwa na hofu kuhusu hatma ya bosi wangu huyo wa zamani. Na sababu kubwa ni kuwa Mkuu wa wilaya huyo anafahamika kwa majungu na fitna, mmoja wa mtaji mkubwa wa makada wa CCM hasa wale waliopo au waliopitia Umoja wa Vijana wa CCM .

Na kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana jana, kuna kila dalili kuwa njama za kumhujumu Bwana Ntibenda zilichochewa na kada huyo wa CCM kwa kushirikiana na wenzie mkoani humo. Natambua kuwa ninaweza kuonekana mnafiki kwa 'kushikilia bango' suala la Bwana Ntibenda kwa vile tu ninafahamiana nae, lakini hiyo haina uzito kulinganisha na uzito wa suala lenyewe.



Ukiangalia jinsi wadhifa wake ulivyotenguliwa unaona bayana kuwa kuna hali kama ya kuumbuana makusudi.Kama Rais au Waziri Mkuu walikuwa wanafahamu 'makosa' ya RC Ntibenda, kwanini wamwondoe madarakani katika hali ya kumdhalilisha, na kwa uharaka kana kwamba ni gaidi or something? Isingewezekana kusubiri hadi mwisho wa siku ya kazi au baada ya kumaliza majukumu yake ya kazi katika siku hiyo? 




Na kubwa zaidi, kama tukiamini kuwa alifanya makosa yaliyopelekea wadhifa wake kutenguliwa, kwanini basi, kwanza, makosa hayo yafanywe siri, na pili, kwanini ahamishiwe Ofisi ya Waziri Mkuu? Akarudie tena makosa au ni kumdhalilisha tu?

Hii ni nje ya rekodi, lakini Bwana Ntibenda alifanya kazi kubwa sana katika uchaguzi mkuu uliopita.Siwezi kuandika hapa kwa sababu ni 'mambo yasiyoandikika hadharani' lakini 'wanaofahamu yanayoendelea behind the scene' wanafahamu fika mchango wa RC huyo wa zamani.

Nimalizie makala hii kwa kumshauri Rais Magufuli kuepuka kusikiliza majungu ya kisiasa, moja ya kansa inayoitafuna CCM kwa muda mrefu. Hao vijana wanaompelekea majungu, wakishamaliza kuwaharibia wengine watamgeukia yeye Rais. Kuna msemo wa kiswahili usemao: "Mchawi akimaliza kuroga mtaa mzima huigeukia familia yake."

Kilichojiri Arusha chaweza kuwa mwendelezo wa 'kuzadia uhuni,' kama ilivyokuwa kwa yule kijana aliyemfanyia vurugu Jaji Warioba akaishia kuzawadiwa ukuu wa wilaya,na leo ni Mkuu wa Mkoa. 



Baadhi ya vyombo vya habari viliripoti jana kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda akieleza kuwa Watanzania wanaruhusiwa kwenda jijini Dar es Salaam lakini LAZIMA WAWE NA SIFA MAALUM...na japo wanaruhusiwa kutembelea ndugu zao LAKINI WASIKAE SANA.

Hivi huyu mtu kalewa madaraka ama? Yeye ni nani hasa wa kuingilia HAKI YA WATANZANIA ILIYOWEKWA WAZI KWENYE IBARA YA 17 CHA KATIBA YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA inayotamka bayana 



Sasa huyu Makonda ni nani hasa kiasi cha kujiona yupo juu ya Katiba na kuingilia haki na uhuru wa Watanzania? 

Huyu bwana amekuwa mtu wa kukurupuka tu na amri, nyingi zikiwa zisizo na kichwa wala miguu kwa maana ya ugumu wa kutekelezeka kwake. 

Ninatumaini kuwa Rais Dkt John Magufuli hatoruhusu uhuni wa madaraka wa aina hii ambao kimsingi utapelekea hisia za 'Magufuli ni dikteta' kupata nguvu zaidi.

Tupo mwaka 2016 halafu anakurupuka mtu kuwarejesha Watanzania kwenye zama za ukoloni ambapo serikali ya mkoloni ilidhibiti uhuru wa wazawa kwenda watakako kama mbinu ya kudumisha ukoloni na kudhibiti upinzani dhidi ya mkoloni.

Mbinu hiyo ya kidhalimu ilitumika pia wakati wa utawala wa kinyama wa Makaburu huko Afrika Kusini ambapo Weusi walipaswa kuwa na ruhusa maalumu kutoka nje ya maeneo yao.

Huyu Bwana Makonda aendelee kufuatilia hao mashoga, ombaomba, wavuta shisha, nk ambao ni dhahiri wamemzidi akili na wanaendelea na maisha yao kama kawaida.

Wito wangu kwa Bwana Makonda ni kwamba yawezekana kabisa kuwa kiongozi mzuri bila kukurupuka na amri zisizo na mwelekeo. Ni muhimu kwa RC huyo kutofautisha maigizo na uongozi, na akitaka maigizo aende bongo movie.

Hizi ni jitihada za makusudi za kumkosanisha Rais Magufuli na Watanzania.



19 Aug 2016

Magufuli ni dikteta. Yeye ni nani hasa wa kutupangia mikutano ya kisiasa?” Ni kauli ya mtu mmoja kwenye mtandao wa kijamii wa twitter. Kama Magufuli ni dikteta, basi hamia Sudan ya Kusini…au Somalia,” lilikuwa jibu la mtumiaji mwingine wa mtandao huo.
Mada ya ‘Magufuli ni dikteta/Magufuli si dikteta’ ndiyo inayotawala zaidi kwenye mijadala mbalimbali, hususan, ya kijamii, ambako kwa uzoefu wangu, ni kati ya maeneo muafaka kupima maoni na mitazamo ya watu wa kada mbalimbali.
Kwa kiasi kikubwa, kambi inayodai kuwa ‘Magufuli ni dikteta,’ inajumuisha wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ambao sasa wanahamasishana kuhusu mkakati wao mpya uanaofahamika kama ‘UKUTA,’ yaani ‘Umoja wa Kupinga Udikteta Tanzania.’ Sina hakika neno ‘umoja’ limeingiaje hapo kwa sababu tofauti na ‘Umoja wa Katiba ya Wananchi’ (UKAWA) ulioijumisha Chadema na CUF, NCCR-Mageuzi na NLD, ‘umoja’ wa UKUTA unakihusisha Chadema pekee.
Kwa upande mwingine, kambi inayomtetea Dk. Magufuli kuwa si dikteta, inaundwa na wafuasi wa chama tawala CCM, na idadi kubwa tu ya Watanzania wengine wanaoamini kuwa si tu kwamba kiongozi huyo anafanya kazi nzuri bali pia kuna masuala ya muhimu zaidi kwa nchi yao kuliko mikutano/maandamano ya kisiasa.
Hoja ya Chadema, au UKUTA yao, ni kwamba agizo la serikali kuzuia mikutano na maandamano ya kisiasa ni la kidikteta, linakandamiza haki yao ya kikatiba ya kufanya shughuli za kisiasa, na hawahitaji ruhusa ya Rais katika utekelezaji wa shughuli zao za kisiasa.
Sambamba na hilo, malalamiko dhidi ya Dk. Magufuli na serikali yake ni kamata-kamata inayoendelea dhidi ya viongozi na wanachama wa vyama vya Upinzani. Kwa wapinzani, huo si udikteta tu bali pia mkakati wa kuviua vyama hivyo.
Pengine katika hatua hii ni muhimu kuweka bayana maslahi yangu. Katika kampeni za Uchaguzi Mkuu uliopita, nilimuunga mkono na kumpigia kampeni Dk. Magufuli, kwa kutumia haki yangu ya kikatiba na utashi wangu.
Kwangu, uchaguzi ulishamalizika mwaka jana. Tumeshampata Rais na serikali yake. Ninaiangalia Tanzania kama nchi na si kwa ‘lensi’ ya u-CCM au u-Chadema. Uchambuzi huu mfupi unafanyika katika mantiki hiyo, kwamba Tanzania yetu ni muhimu zaidi kuliko vyama vya siasa, na maslahi ya taifa ni muhimu zaidi ya maslahi ya kiitikadi.
Baada ya angalizo hilo, nina hoja kuu mbili ambazo ndio mtazamo wangu rasmi kuhusu ‘Magufuli ni dikteta/si dikteta.’ 
Hoja ya kwanza ni kwamba sidhani kuwa uamuzi wa kuzuia shughuli za kisiasa za vyama vya upinzani ni la busara. Katiba inaviruhusu vyama vya siasa kufanya shughuli hizo alimradi zinazingatia sheria na hazisababishi uvunjifu wa amani.
Kwa kuazima busara za Kighoma Malima, “haki haitolewi kama zawadi. Haki hudaiwa, wakati mwingine kwa nguvu,”. Wapinzani wanaona ni sawia kwao kutumia nguvu kudai haki yao.
Hivi, vyama vya upinzani vikiachwa kufanya mikutano yao (kwa kuzingatia sheria za nchi) kutakuwa na madhara gani hasa? Katika hili, naona kama Rais Magufuli anashauriwa vibaya, hasa ikizingatiwa kuwa kwa kiasi kikubwa kabisa, amemudu kumiliki takriban hoja zote za muhimu za vyama vya upinzani, hususan, vita dhidi ya ufisadi. Binafsi, ninaona zuio hilo la shughuli za kisiasa za wapinzani ni sawa na “kuwapa wapinzani kitu cha kuongea.”
Hoja yangu ya pili ni kwamba ifike mahala vyama vya upinzani vitambue kuwa mikutano na maandamano si shughuli pekee za vyama vya siasa. Kuna masuala mengine mbalimbali yanayoweza kufanywa na vyama hivyo badala ya mikutano na maandamano tu.
Ndiyo, mikutano na maandamano ni haki ya vyama vya siasa, lakini si kipaumbele kikubwa cha Watanzania, hasa katika kipindi hiki ambacho Rais Magufuli anafanya kila jitihada kuiondoa Tanzania yetu kutoka katika lindi la ufisadi ambao kwa kiasi kikubwa umechangia umasikini unaoikabili nchi yetu.
Nimalizie makala hii kwa kukumbushia kuwa huko nyuma, takriban sote – ikiwa ni pamoja na vyama vya upinzani – tuliafikiana kuwa “ili Tanzania yetu iendelee, twahitaji Rais dikteta.” Na yayumkinika kuhisi kuwa kama udikteta wawezesha kuongeza pato la taifa, kuwaibua watumishi hewa, kuwadhibiti ‘wauza unga,’ na kurejesha nidhamu ya ‘asiyefanya kazi na asile,’ basi Dk. Magufuli aendelee tu kuwa ‘dikteta.’
Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

16 Aug 2016


NDOTO yangu ya muda mrefu utotoni ilikuwa utabibu. Moja ya sababu zilizonipa ndoto hiyo ni uuguzi (unesi) wa dada yangu, ambao ulinifanya nimtembelee kazini kwake (hospitalini) mara kwa mara. Kila nilipomtembelea, nilishuhudia wagonjwa mbalimbali wakiwa wamekabidhi afya na uhai wao mikononi mwa madaktari na manesi. Nikanuwia kuwa nitakapomaliza elimu ya msingi na kufanikiwa kuingia sekondari, nitasoma masomo ya sayansi ili baadaye niwe daktari.
Kwa bahati nzuri nilifaulu darasa la saba na kuchaguliwa kujiunga sekondari ya kutwa ya Kilombero, Ifakara. Mimi na wanafunzi wenzangu tuliofaulu mwaka huo ndio tulikuwa wanafunzi waanzilishi wa shule hiyo maarufu kwa jina la Kilombero Day.
Kujiunga na shule hiyo kuliisogeza karibu ndoto yangu ya udaktari, sio tu kwa vile nilipata fursa ya kusoma masomo ambayo yangeweza kunisaidia kusomea udaktari lakini pia shule hiyo ilikuwa jirani tu na chuo cha waganga wasaidizi (MATC), kilichokuwa katika hospitali ya Mtakatifu Francis.
Hata hivyo, nilikabiliwa na vikwazo viwili. Kwanza, shule hiyo mpya ilikuwa na uhaba mkubwa wa nyenzo mbalimbali za kitaaluma, vitabu vya kiada na maabara. Kikwazo cha pili kilikuwa katika uwezo wangu binafsi. Somo la hisabati lilikuwa ‘mgogoro’ tangu siku ya kwanza, na somo la Fizikia likatokea kuwa gumu kuliko yote. Wakati huo, nilishafahamu kuwa mkondo wa udaktari ni Fizikia, Kemia na Baiolojia (PCB) na Hisabati kidogo.
Kufupisha simulizi, nilipohitimu kidato cha nne nilipata Daraja la Kwanza huku nikiwa na alama A ya Kemia, C ya Baiolojia na F ya Fizikia. Ukichanganya na D ya Hisabati, mkondo wa PCB uligoma.
Nilipochaguliwa kidato cha tano, nikataka kuikwepa Fizikia kwa kusoma Kemia, Baiolojia na Jiografia (CBG), ambayo ingeweza kunifikisha katika azma yangu ya kusomea udaktari. Nikakumbana na kikwazo cha kuchukua tena Hisabati (Basic Mathematics) kama somo la ziada na kumbe Kemia ya Kidato cha Tano na Sita haikuwa nyepesi kama ile niliyopata alama A kidato cha nne. Kipengele cha Physical Chemistry kilikuwa ni kama Fizikia zaidi kuliko Kemia na hisabati juu. Nikaamua kuzika ndoto yangu ya udaktari, nikachukua mkondo wa Historia, Jiografia na Kiingereza (HGL) na somo la ziada la Siasa.
Lengo la simulizi hiyo sio kuelezea safari yangu ya kitaaluma au ndoto yangu hiyo ya udaktari iliyokufa kifo cha asili bali kama kielelezo mwafaka cha kukosoa uamuzi wa serikali kulazimisha masomo ya sayansi kwa wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha nne.
Sitaki kujigamba kuhusu kiwango changu cha elimu, lakini ukweli ni kwamba licha ya kufanikiwa kuhitimu shahada tatu nikisaka ya nne kila ninapokutana na hata mhitimu wa kidato cha sita tu wa mkondo uliohusisha Fizikia na Hisabati (kwa mfano PCB au PGM), ninampa heshima zote. Sababu nyepesi ni kwamba ameweza kile kilichonishinda.
Na hadi muda huu, nikiwaona wanafunzi wa shahada ya kwanza katika masomo ya sayansi kama vile uhandisi, ninawaheshimu mno. Kwa kifupi tu, masomo ya sayansi yanahitaji mtu mwenye akili zaidi. Japo haimaanishi tunaosoma kozi zisizo za sayansi ni ‘patupu kichwani,’ ukweli ni kwamba angalau kozi zetu zina ahueni fulani.
Sasa serikali inapokurupuka na uamuzi wa kulazimisha masomo ya sayansi kwa wanafunzi wote, kinyume cha utaratibu uliopo ambapo wanafunzi wa sekondari wanaingia kidato cha tatu wanapewa uhuru wa kuchagua mkondo wanaotaka (hasa kwa kuzingatia ndoto zao kitaaluma na uwezo wao kimasomo).
Huu ni udikteta wa kitaaluma, kumlazimisha mwanafunzi kusoma kitu asichotaka. Na hapa suala sio kutaka tu bali pia kuna suala la uwezo wa kumudu masomo ya sayansi. Na kingine ni kuwabebesha wanafunzi mzigo wasiostahili.
Sababu iliyotolewa na serikali kupitia Waziri wa Elimu, Teknolojia, Sayansi na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, kuwa hivi sasa Tanzania imedhamiria kuingia kwenye uchumi wa kati ambao ni wa viwanda, na hivyo suala la sayansi haliwezi kuepukwa (kwa sababu ni wakati sasa wa kuwa na wataalamu wengi wa fani za sayansi watakaoweza kutosheleza mahitaji ya sekta ya viwanda nchini) haina mashiko.
Nihitimishe makala hii kwa kumshauri waziri huyo msomi kurejea mada kama ‘reactance’ na ‘boomerang effect’ kwenye saikolojia na kuzihusisha na uamuzi huo wa serikali na athari zake.
Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

13 Aug 2016

14026664_162506520845816_426045486_n
Leo ni siku ya kuzaliwa ya mwana-hiphop mahiri na lejendari nchini Tanzania, Fareed Kubanda a.k.a Fid-Q. Na katika kuadhmisha birthday yake, msanii huyu ambaye sio tu amedumu "kwenye fani" kitambo bali pia ni miongoni mwa waasisi wa Swahili Hip-Hop.

 Kwangu, Fid-Q sio tu ni msanii maarufu kabisa huko nyumbani Tanzania na katika Swahii hip-hop duniani, bali ni mmoja wa watu ambao wamkuwa wakinipatia sapoti kubwa katika kazi zangu za uandishi wa vitabu. Na ndio maana kwa kutambua mchango wake huo, alikuwa mtu wa kwanza kupata nakala dhahiri ya kitabu changu kuhusu taaluma ya uafisa usalama wa taifa (ushushushu) kama inavyoonyesha pichani chini.

 Jana niliuliza huko kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter kuhusu wimbo gani wa Fid-Q unawavutia zaidi mashabiki wake. 



Jibu jepesi lilikuwa "kila wimbo wake unavutia." Nimesikiliza hii track mpya ya 'SUMU.' Imesheheni kauli nyingi za busara. Nitamwomba Fid-Q anitumie mashairi ya wimbo hu ili kuwaletea ninyi wasomaji uchambuzi zaidi ya wimbo huo. Lakini hata bila uchambuzi, kwa kuusikia tu, utaafikiana nami kuwa umeshehenu busara tele.

 Na hiki ndio kinachomfanya Fareed aendelee kuwa mmoja wa wasanii wachache na adimu kabisa Tanzania sio tu kuwa waasisi wa fani bali pia wasiochuja: kuwa na nyimbo zenye ujumbe usiochuja. Kama ingekuwa ni muziki wa bendi basi tungelinganisha na timeless tunes za kina Mbaraka Mwinshehe, Marijan Rajabu, Bitchuka, Shaban Dede, nk ambao tungo zao zilituvutia tangu tukiwa utotoni (kwa tulozaliwa enzi hizo) na ni tamu hadi leo. Na utamu so wa ladha tu bali pia relevance ya ujumbe uliomo. 

 Basi nisiandike 'gazeti,' bali nimtakie Fareed heri ya siku yake ya kuzaliwa, na kumtakia kila la heri na fanaka maishani, na kumshukuru kwa sapoti yake kwa kazi zangu, na kumpongeza kwa kutupatia 'SUMU.' Isikilize hapa chini

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.