Showing posts with label UVCCM. Show all posts
Showing posts with label UVCCM. Show all posts

13 Oct 2011


Kama nilivyobashiri kwenye MAKALA HII,Kaimu Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Benno Malisa ameundiwa zengwe zito kufuatia kauli zake jijini Arusha ambapo pamoja na mambo mengine aliwataka viongozi wenzie wa CCM kuacha kuiandama Chadema.

Kwa mujibu wa habari iliyochapishwa kwenye jarida la Raia Mwema,Malisa anadaiwa kuwa amekuwa akiandaa mazingira mazuri kwa ajili ya Edward Lowassa endapo harakati za kuvuana magamba ndani ya chama hicho zitamkumba.

Japo tuhuma dhidi ya Malisa zinahusishwa zaidi na kitendo cha yeye kufungua mashina ya UVCCM (ambapo anadaiwa kufanya hivyo pasipo kushirikisha uongozi wa umoja huo ngazi ya mkoa) yayumkinika kuamini kuwa kilichomponza kiongozi huyo wa UVCCM Taifa ni kauli zake za kutaka demokrasia ya kiutu-uzima,sambamba na kuikumbusha CCM wajibu wake kuwatumikia Watanzania.

Na hili ndilo tatizo litakalopelekea mauti ya chama hicho kingongwe.Kiongozi au mwanachama yeyote yule atakayeamua kuongea ukweli ataanza kusakamwa na si ajabu akajikuta anavuliwa madaraka,CCM imekuwa ikiongoza nchi kwa namna ya uchawi wa kuwafumba macho Watanzania.Licha ya vyama vya upinzani (hususan Chadema) kuwaamsha Watanzania kuwa chama hicho tawala kinaendesha nchi kwa siasa za kimafia,CCM imekuwa ikijitetea kwa kuwaita wapinzani wachochezi na watu wa majungu,huku ikitumia taasisi za dola kupandikiza migogoro kwenye vyama hivyo.

Sasa anapotokea kiongozi au mwanachama wa kawaida wa chama hicho kuakisi yale yanayosemwa na wapinzani (aambayo kimsingi ni mtizamo wa Watanzania wengi) basi ataandamwa huyo hadi aonekane kama mhaini flani.

Wanachojisahau CCM ni ukweli kwamba kuficha ugonjwa hakuwezi kuwa sehemu ya tiba ya ugonjwa husika.Hata akina Malisa wakikaa kimya na kufuata porojo za "mshikamano wa chama" au "umoja wa kitaifa" ukweli unabaki kuwa ipo siku umma utaamka na kuking'oa chama hicho kwa nguvu kwani wanaweza kudanganya umma wote kwa muda fulani lakini hawawezi kuudanganya milele.

Anyway,soma habari husika hapa chini


Wakati huo huo, hali ya kisiasa ndani ya Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) ni tete ikibainika kuwa Makamu Mwenyekiti wa umoja huo, Benno Malisa, ameanza kucheza hadharani siasa uasi zinazoendeshwa na kambi inayotajwa kuwa ni ya kigogo mmoja wa CCM mkoani humo. 
Malisa sasa anahusishwa na tukio la hivi karibuni linalohusisha na ufunguzi wa mashina ya chama hicho Arusha mjini, unaotajwa kuratibiwa kinyemela bila viongozi wa chama hicho ngazi ya wilaya na mkoa kutoa kufahamishwa na kwamba, sehemu ya waratibu wa tukio hilo ni vijana waliosafirishwa kutoka wilayani Monduli. 
Taarifa za uhakika ambazo gazeti hili limezipata zinaeleza kuwa tukio hilo halikushirikisha viongozi wa UVCCM mjini Arusha na viongozi wengine wa chama hicho. 
“Mipango yote kwa kiasi kikubwa imeratibiwa na watu wa kutoka wilayani Monduli. Inasemekana kuwa hii ni sehemu ya mkakati wa maandalizi ya watu hao kumhami Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa endapo atabanwa kwenye mkakati wa kujivua gamba wa CCM, basi wajifanye kushusha bendera za CCM kwenye mashina hayo ili kuuonyesha umma kuwa anakubalika sana ndani ya chama,” anasema mmoja wa watoa taarifa wetu ambao ni vijana waliohusika kuratibu mpango huo. 
Hali kama hiyo ya kujiandaa kwa ajili ya mchakato wa kujivua gamba ilijitokeza wakati aliyekuwa Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz pale alipotangaza kujiuzulu baadhi ya vijana waliandaa mabango yenye ujumbe unaomtaka ajisiuluzu na wengine wakihoji hatua hiyo huku taarifa zikisema mabango hayo yaliandaliwa muda gani wakati alikuwa bado kutangaza kujiuzulu. 
Kiongozi mmoja wa UVCCM Arusha anaeleza; “UVCCM Arusha mjini walikataa utekelezaji wa mkakati huo haramu kupitia kikao chake cha Kamati ya Utekelezaji kilichoketi Oktoba 7, mwaka huu, kwa kumwandikia barua Katibu wa Vijana CCM mkoani Arusha.” 
Inaelezwa kuwa barua hiyo ilimjulisha kiongozi huyo kuwa wao kama wilaya hawajapata taarifa rasmi za uzinduzi wa mashina hayo ya wakereketwa na hivyo kwa muda uliobaki wasingeweza kufanya maandalizi mazuri ikizingatiwa wao ndio wenye jukumu la kuandaa mashina hayo na si Wilaya ya Monduli. 
“CCM Mkoa baada ya kupata nakala ya barua hiyo waliamua kuitisha kikao cha sekretariati ya mkoa pamoja na kamati ya utekelezaji ya vijana Mkoa wa Arusha na Wilaya Arusha mjini, Oktoba 8, 2011. 
“Katika kikao hicho maazimio yalikuwa ni kusitisha zoezi hilo hadi hapo taratibu za chama zitakapofuatwa. Chama Mkoa walimwandikia barua hiyo Katibu wa UVCCM Mkoa wa Arusha ili aweze kuwataarifu na viongozi wengine pamoja na wanachama wa umoja wa vijana wa CCM. 
“Baada ya kupata barua hiyo Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Arusha, James Millya, alifanya kikao cha faragha na Mbunge wa Viti Maalumu, Catherine Magige na Benno Malisa. Baada ya kikao chao hicho, waliamua kufanya shughuli hiyo iendelee kama walivyokusudia pamoja na chama kukataza. 
“Jumatatu, Oktoba 10, 2011 walianza kushughulikia kibali cha maandamo na uzinduaji mashina hayo. Hadi saa nne asubuhi polisi waliwanyima kibali cha kazi hiyo,” alisema mtoa habari wetu mwingine ambaye naye amekataa kutajwa jina lake gazetini. 
Inaelezwa kuwa mkutano huo wa kufungua mashina uliofanyika 10/10/2011, ulihudhuriwa na vijana kutoka Monduli na vijana wengine wa vyama mbalimbali vya siasa. 
Katika shughuli hiyo, Benno Malisa ambaye ni mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, alishambulia wazi wazi chama chake akitetea Chama cha Demokrasia na Maendeleo ( Chadema) chini ya mwavuli wa demokrasia na utawala bora. 
Katika hotuba yake hiyo, Benno Malisa amekejeli hata kauli ya viongozi wenzake wa CCM wanaoonyesha kwamba CCM ni chama tawala na kuonya dola kuingilia mambo ya siasa, hali inayozidi kuashiria mgawanyiko mkubwa ndani ya chama hicho tawala.

CHANZO: Raia Mwema

11 Oct 2011


Nyakati za Ujamaa na Kujitegemea tulifundishwa kuwa maadui wakubwa wa maendeleo ni ujinga,maradhi na umasikini.Na tuliaswa kuhakikisha tunapambana nao kwa nguvu zote.Lakini mambo haya matatu si binadamu bali ni hali ya kimaisha.

Kibinadamu,tulifundishwa kuwa maadui wakubwa ni wanyonyaji-makupe,makabaila,mamwinyi,ma-mangi meza,na viumbe wengine kama hao.

Baada ya itikadi ya Ujamaa kuzikwa hai na aliyekuwa Rais wa Awamu ya Pili,Ali Hassan Mwingi na kundi lake,utambulisho wa maadui zetu ulibaki wa kusuasua.Lakini tulipoingia kwenye siasa za vyama vingi,wakazuka maadui wapya.Kundi moja-ambalo na akina sie (waropokaji au vimbelembele-kama wanavyotuita watawala) lilikuwepo hata zama za Ujamaa.Uzuri au ubaya ni kwamba nyakati hizo haikuwa rahisi kupingana au kuwa na mawazo tofauti na watawala.Na 'vimbelembele' na 'waropokaji' waliishia jela kama si kusumbuliwa kwa muda wao wote wa uhai wao.

Baada ya mageuzi ya kisiasa na kiuchumi,kundi hili limeendelea kunyanyaswa japo kwa wakati huu sio waziwazi.Akina Marehemu Katabalo,Kolimba na wengineo ni majeruhi wa hasira za watawala na washirika wao dhidi ya kundi hili.Na hadi leo wapo wenzetu wengi tu ambao wananyanyaswa na vyombo vya dokla kwa kosa la kusema ukweli ambao watawala na washirika wao hawataki usemwe.

Lakini kundi jipya la maadui baada ya ujio wa mageuzi ni vyama vya upinzani.Pamoja na CCM kuridhia kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi,wapinzani wameendelea kujengewa picha kwenye jamii kama watu wa kuogopwa kama ukoma.Wanahujumiwa kwa fedha za walipa kodi,wanasemwa vibaya na kupachikwa majina mabaya kuliko makupe,makabaila,nk.

'Kosa' kubwa  la wapinzani ni kutaka kuwanyang'anya watawala na washirika wao fursa ya kuendelea kutukandamiza.Wanaonekana kama walafi na waroho wa madaraka (watakuwaje waroho wakati wameingia juzi tu ilhali kuna watu wanazeekea madarakani?).Hoja inayojengwa ni kwamba walikimbia CCM na kujiunga na upinzani si kwa minajili ya kuutumikia umma kwa siasa bali kutokana na tamaa,ulafi na uroho wao wa madaraka.

Ukimsikia mtu kama Nape Nnauye akiwazungumzia wapinzani unaweza kabisa kuhisi kuwa anawazungumzia Taliban au Al-Shabaab.Picha inayojengwa ni ya viumbe hatari kuliko virusi vya ukimwi.

Kwa muda mrefu CCM imekosa sauti za kusisitiza mshikamano wa kitaifa (ambapo hata wapinzani wana jukumu hilo) na badala yake nguvu nyingi zimeelekezwa katika kupanda mbegu ya chuki.Wapinzani wanaonyeshwa kama sio Watanzania,na pale inapobidi kuwakubali kuwa ni Watanzania wenzetu basi jitihada zinafanywa kujenga picha kuwa wenzetu hao wanataka kuitumbukiza nchi yetu kwenye shimo lenye kina kirefu.

'Kosa' jignine la wapinzani ni kutumia nafasi waliyonayo kupigania maslahi ya wananchi,ambao kwa kiasi kikubwa wanaendelea kutapeliwa na watu wanaolipwa mshahara kwa kazi ya kuwawakilisha-I mean Wabunge wetu.Hatuhitaji kuingia kwa undani kuhitimisha kuwa wengi wa wabunge wetu ni sawa na majambazi tu ambao wanalipwa mishahara minono pasipo kuwatumikia wapiga kura wao ipasavyo.Nasisitiza,NI BAADHI TU ya wabunge.

Sasa katika pitapita zangu mtandaoni nimekutasna na habari ifuatayo ambayo kwa hakika imenitia nguvu sana.Kaimu Mwenyekiti wa UVCCM, Benno Malisa ameonyesha ukomavu wa hali ya juu kisiasa kwa kuongea masuala ambayo kwa hakika ni kwa maslahi ya taifa na si ya kichama.

Najua kuna watakaomsema vibaya-hususan ndani ya chama chake-lakini uzuri wa ukweli ni kwamba ukishawekwa hadharani,atakayeumia na aumie lakini hakuna wa kuufuta.Wapo watakaodai Malisa ameanza kumpigia debe mmoja wa wanaotajwa kutaka Urais 2015 (nadhani itakuwa ni Lowassa) na wengine wanaweza kumtuhumu kuwa huenda hata yeye (Malisa) ana nia ya kugombea urais.

Sijawahi kumsifia Malisa lakini kwa hili NINAMPA TANO.Namsihi apuuze tuhuma zote zitakazoelekezwa kwake kwa 'kosa' la kusema 'yasiyopaswa kusemwa.' Laiti tukiwa na viongozi wanaodiriki kueleza hisia zao pasi kuhofia kuwachukiza watu fulani (na wanachokiongea kuwa chenye maslahi kwa umma) basi kwa hakika tunaweza kufanya mijadala muhimu kuhusu taifa letu na kuzika chuki zisizo za msingi dhidi ya wale wanaoongea tusiyopendezwa nayo.

Nisiandike mengi,hebu soma habari ifuatayo:

UVCCM yataka CCM isiifuatefuate Chadema
Monday, 10 October 2011 22:27
Waandishi wetu, Arusha 
KAIMU Mwenyekiti wa Umoja Vijana wa CCM (UVCCM), Benno Malisa amewataka vigogo ndani ya chama hicho tawala kuacha kuingilia mambo ya chama kikuu cha upinzani nchini, Chadema hasa mgogoro wake na madiwani wa Arusha Mjini na badala yake watafute suluhu ya matatizo ya msingi yanayoikabili nchi kama mfumuko wa bei na tatizo la ajira.Akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika eneo la Hospitali ya Mtakatifu Thomas, Malisa alisema wapo baadhi ya watu ndani ya CCM ambao siyo wana Chadema lakini wamekuwa wakijihusisha na mgogoro wa chama hicho pinzani. 
Alisema wana CCM hao wamekuwa wakiingilia mgogoro kati ya Chadema na madiwani wake ambao tayari chama hicho kilikwishaamua kuwafukuza na kusisitiza kuwa mambo ya chama hicho pinzani yaachwe yasiingiliwe. 
Kauli hiyo ya Malisa inakuja kipindi ambacho Chadema kimekuwa kikilalamikia baadhi ya mawaziri wa Serikali kupuuza uamuzi wake wa kuwatimua madiwani wake.
Chadema imewahi kumnyooshea kidole Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi,) George Mkuchika kwamba alikuwa na ajenda ya siri baada ya kuendelea kuwatambua madiwani hao.
Pia Chadema kimekuwa kikituhumu baadhi ya makada wa CCM mkoa wa Arusha na taifa, kujaribu kuingilia uamuzi huo wa Chadema wa kutimua madiwani hao kutokana na uamuzi wao wa kuingia muafaka wa Umeya wa Arusha. 
Kaimu Mwenyekiti huyo wa UVCCM, alisema si sahihi kwa CCM kutumia hata vyombo vya serikali kudhoofisha demokrasia kwa vyama vya upinzani akionya kwamba
mwisho wa siku matokeo yake hayatakuwa mazuri kwa taifa. 
Alisema demokrasia inapaswa kuachwa ichanue kwa vyama vya upinzani ili kujenga ustawi mzuri wa nchi.

“Nitumie nafasi hii kumuomba Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), kaka yangu (Godbless) Lema kuwa mstari wa mbele katika kuleta umoja na mshikamano hapa mjini na kumaliza tofauti za UCCM na UCDM (U - Chadema) ili wakazi wa Arusha wapate maendeleo. Sasa uchaguzi umekwisha tujenge nchi yetu.” 
Alisema CCM kinapitia katika wakati mgumu hivi sasa na kuonya kwamba badala ya kuisimamia Serikali wapo wanaohangaika kutafuta wachawi na kutuhumu watu. 
“Tuache kabisa. Hili jambo halisaidii chama wala taifa letu, kumekua na dhana na fikra potofu juu ya ushindi wetu wa 2010 matokeo yale na tuliyoyaona Igunga ni funzo kwetu na hasa vijana,” na kuongeza kuwa vijana wengi wameanza kukosa imani na CCM kwa sababu: 
“Tunashindwa kuwaonyesha kuwa tuna majibu ya matatizo yao. Tumebaki tunaimba historia na kumtaja Baba wa Taifa na kutumia nukuu zake bila kuwapa matumaini vijana kuwa Tanzania yao itakua njema, watapata elimu nzuri, afya na itakua ya uhakika.” 
Alisema vijana wanataka kusikia uchumi umekua, ajira zinapatikana, fursa za kujiajiri zipo, mikopo inapatikana na kusisitiza: “Tusipotoa matumaini haya na kuyafikia 2015, wapiga kura milioni sita wapya watatukataa, uelewa wa vijana wa Kitanzania sasa umekua mkubwa. Wanajua haki na wajibu wao tuache kufanyia siasa maisha ya Watanzania.” 
Wanaotaka urais 2015
Akizungumzia mbio za urais kwa mwaka 2015 ndani ya CCM, Malisa aliwataka makada wa chama hicho wanaotaka kuwania nafasi hiyo kuacha kuwagawa vijana na kuvuruga chama akisema kufanya hivyo ni hatari kwa uhai wa chama. 
“Wapo baadhi ya watu wanaopita wenzangu msiishi kwa kutarajia madaraka ya kupewa wapo wengine wanapita wanakusanya CV za vijana na kuwaahidi vyeo vya U-DC. Msipotoshwe na wala msifungwe fikra kwa sababu mmepewa ahadi ya kuteuliwa U DC. Tuna bahati mbaya wapo ambao mpaka leo wanaishi kwa kusubiri U DC wamegeuka kuwa ndiyo mzee na watumwa kifikra, tuukatae utumwa huu UVCCM.” 
“Tusiwe ndiyo mzee. Nawaagiza wenyeviti na makatibu wa mikoa na wilaya zote Tanzania, wafuatilie katika halmashauri zao kujua mipango ya maendeleo inayohusu vijana na kufuatilia utekelezaji wake wakiona hakuna utekelezaji, watumie kamati za siasa za wilaya kuwabana wenyeviti wa halmashauri. Nazitaka wilaya zote zifuatilie zituletee taarifa juu hili jambo. Tusikubali kuwa ndiyo mzee lazima tusimamie maslahi ya Vijana.” 
Alisema huu si wakati Serikali ya CCM kukaa likizo badala yake ifikirie namna ya kufikia matarajio ya Watanzania. 
Dowans
Akizungumzia suala la mitambo ya Dowans Malisa alisema: “Watu waliosababisha hasara wawajibike, walitudanganya. Kama taifa leo tumeshindwa kesi mitambo ile waliyosema haifai leo inatumika na kampuni ya Symbion. Wanatufanya Watanzania mazuzu. Walisema heri tukae giza wakati wao wanatumia majenereta na wanalipiwa na Serikali huku wakinunua aspirini kwa mamilioni.” 
“Leo wanajifanya wazalendo. Nilitarajia wawajibike walidanganya taifa, Serikali ikavunja mkataba. Wakasema mitambo haifai mibovu leo imenunuliwa na Wamarekani na wanatuuzia umeme... wanafiki wametufikisha hapa niwaombe UVCCM na vijana wa vyama vyote tuungane hawa wawajibike.” 
Watunishiana misuli na polisi
Kabla ya kuhutubia, Malisa na msafara wake waliingia katika mgogoro na vyombo vya dola, baada ya kufanya maandamano na mikutano ya uzinduzi wa matawi mapya ya UVCCM ambayo awali, yalizuiwa na polisi kabla ya kuruhusiwa baadaye. 
Mamia ya vijana wa CCM walianza kukutana kuanzia asubuhi katika Ofisi za UVCCM mkoani hapa, lakini walipoanza matembezi walizuiwa na polisi mbele ya Jengo la CCM Mkoa. 
Sababu ya kuzuiwa inaelezwa kuwa ni mgogoro ndani ya chama hicho katika Wilaya ya Arusha. Viongozi wa umoja huo wanadaiwa kupinga ziara ya viongozi hao wa kitaifa. Hata hivyo, maandamano hayo yaliendelea baada ya mazungumzo baina ya polisi na viongozi hao wa UVCCM huku wakikubaliana njia za kupita. 
Lakini, mara baada ya kukamilika kwa uzinduzi wa matawi hayo viongozi wa umoja huo walionyesha kukerwa kwao na hatua ya polisi na baadhi ya viongozi wa chama hicho kutaka kuzuia kazi hiyo. 
Habari hii imeandikwa na Mussa Juma,Peter Saramba na Moses Mashalla


CHANZO: Mwananchi

27 Jul 2011



From: Andrew Bomani
Subject: TAMKO LA KIHISTORIA NA HALI YA KUHUZUNISHA NCHINI!
Date: Monday, July 25, 2011, 3:26 AM

Ndugu msomaji,

Kufuatia ombwe la uongozi la kutisha nchini ambalo karibu kila Mtanzania anakiri ndiyo tatizo mama, baadhi yetu tumeona ni vyema tukawafikishia tamko ambalo liliwahi kutolewa mwaka 1995 na Jaji Bomani. Ni jambo la kusikitisha kwamba wananchi wengi wanadhani kwamba viongozi waliokuwepo wakati huo na waliopo sasa pengine ndiyo waliokuwa bora. Jambo hili ni hatari. Haiwezekani nchi yoyote ikakosa watu makini. Soma na tafakari namna mizengwe katika kupata viongozi makini inavyoweza kulifikisha taifa lolote mahali pabaya.

Mungu Ibariki Tanzania.

Tamko la Kihistoria



Barua ya UVCCM Kwa Jaji Bomani Kumwomba Agombee Urais 2005

20 May 2011


CCM Arusha kwachafuka

Thursday, 19 May 2011 22:42

CHATANDA ATAKIWA KUNG'OKA, GARI LAKE NUSURA LICHOMWE MOTO NA UVCCM
Moses Mashalla, Arusha
HALI si shwari chama tawala mkoani Arusha mara baada ya gari la Katibu wa CCM hapa, Mary Chatanda kunusurika kuchomwa moto na baadhi ya wanachama wa Umoja wa Vijana wa chama hicho(UVCCM).Wanachama wa umoja huo kutoka wilaya mbalimbali za Mkoa wa Arusha waliandamana katika Jengo la Makao Makuu ya CCM Mkoa wa Arusha, wakishinikiza Chatanda pamoja na Mjumbe wa Baraza la Vijana mkoani Arusha, Mrisho Gambo "wajivue gamba".

Hali hiyo ilijitokeza jana katika jengo la makao makuu ya chama hicho wakati Kikao cha Kamati ya Siasa Mkoa kikiendelea ambapo, hali iliyosababisha dereva wa gari la katibu huyo wa CCM kulitoa nje ya jengo hilo na kisha kulikimbiza mahali kusikojulikana.

Vijana hao walikuwa wameshika mabango yenye ujumbe mbalimbali huku wakipaza sauti zilizokuwa zikimtaka Chatanda kuondoka katika nafasi yake ya uongozi kwa madai kwamba amekuwa akikivuruga CCM mkoani Arusha.

Wakizungumza na waandishi wa habari, wanachama hao kutoka wilaya za Monduli, Longido, Arusha, Arumeru, Karatu na Ngorongoro walisema pamoja na wao kutoa malalamiko mbalimbali juu ya Chatanda na Gambo, lakini uongozi wa CCM taifa umekuwa ukiwakumbatia viongozi hao na kudai sasa wamechoka.

Walisema malaliko yao kuwa Chatanda amekuwa akikivuruga chama chao ikiwa ni pamoja na kusababisha kukosa ushindi wa Jimbo la Arusha Mjini lililoenda kwa Chadema huku wakisema kwamba ikiwa atakataa kung'oka watajua cha kufanya.

“Hatumtaki Chatanda na hatumtaki Mrisho Gambo hawa watu kwanza ni wasaliti, lakini pia wamechangia sisi kushindwa kuchukua jimbo hili kwani walikuwa wanaiunga mkono Chadema tunataka waondoke mara moja hadi kieleweke,” ilisikika sauti ya mmoja wa vijana hao.

Miongoni mwa jumbe ambazo zilikuwa zimeandikwa kwenye mambango hayo ni "Chatanda umehujumu uchaguzi kwa siasa zako za makundi zilizojaa chuki, ubinafsi na ubabe usio na manufaa kwa Chama Cha Mapinduzi", "Chatanda kwa siasa zako za ubabe umetuchonganisha na viongozi wa dini”, na nyingine kadha wa kadha.

Hali hiyo ilisababisha Mwenyekiti wa UVCCM mkoani Arusha, James Ole Millya aliyekuwa kwenye kikao cha kamati ya siasa kutoka nje na kwenda ukumbini kuwatuliza wanachama hao, lakini juhudi zake ziligonga mwamba.

Akizungumza na wanachama hao, Milya aliwataka wapunguze jazba na kusema kuwa yeye ni mjumbe ametumwa kusikiliza madai yao hivyo wampatie na kisha taufikisha ujumbe huo.

“Jamani ninawaomba mtulie sidhani kama mtafanya fujo ninaomba mnipatie ujumbe mnitume niufikishe jamani nami nitaufikisha tulieni jamani,” alisema Milya

Hata hivyo, ushawishi wa Milya haukuzaa matunda na kuamua kurudi kikaoni kwani wanachama hao waliendelea kupaza sauti zao kwa wakidai kuwa wanamtaka katibu huyo aondolewe mkoani Arusha kwa kuwa amekuwa akiingilia uamuzi wa umoja wao na kuendelea kumkubatia Gambo.

“Mheshimiwa tunakipenda sana chama chetu na tunakuheshimu sana, tunaomba Chatanda aondoke la sivyo tutachoma gari lake, tukikutana nalo tutamondoa kwa nguvu,” alisema kwa jazba mmoja wa vijana hao.

Vijana wavamia kikao cha kamati ya siasa
Wakati hayo yakiendelea wanachama hao walikosa uvumilivu na kisha kuvamia ofisi ambapo Kikao cha Kamati ya Siasa mkoa kilipokuwa kikifanyika huku wakitishia kubomoa mlango kitendo kilichosababisha viongozi mbalimbali wa CCM mkoani hapa kuhaha kutuliza tafrani hiyo.

Maafisa usalama wakiwemo askari kanzu walikuwa wametanda katika maeneo ya jengo hilo huku wengine wakionekana wakizungumza na viongozi wa UVCCM kujua chanzo cha vurugu hizo.

Chatanda ajifungia ukumbini
Hadi tunakwenda mitamboni, Chatanda alikuwa bado amejifungia ndani ya ukumbi wa mkutano na hakuna taarifa yoyote ya CCM Mkoa aliyotolewa kuhusiana na tukio hilo.

Tuhuma dhidi ya Chatanda kutoka ndani ya chama chake zimekuja siku chache tangu ashutumiwe kuwa mmoja wa waliosababisha mgogoro mkubwa wa kisiasa mkoani Arusha baina ya vyama vya CCM na Chadema.

Mgogoro huo unafuatia Chadema kupinga katibu huyo wa CCM wa Mkoa wa Arusha kushiriki katika vikao vya Baraza la Madiwani na kupiga kura ya kumchagua meya wa Jiji la Arusha, hali Iliyosababisha maandamano makubwa ambayo yalisababisha vifo vya watu watatu.

Wakati CCM wakidai kuwa Chatanda ni mjumbe halali wa vikao vya baraza hilo, Chadema wamekuwa wakipinga kwa maeleo kwamba mwanamama huyo ni mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Tanga hivyo hana sifa ya kushiriki vikao vya Arusha.
CHANZO: Mwananchi

21 Jan 2011





Tamko La Umoja wa Vijana Mafisadi

ONLY REASON SOME BASTARDS ARE STILL ALIVE IS BECAUSE SHOOTING THEM IS ILLEGAL.SERIOUSLY.

20 May 2010

Nadhani unamfahamu Christina Aguillera,na kama unamfahamu basi ni dhahiri utakuwa unakumbuka 'singo' yake ya kwanza kabisa Genie in a Bottle (Kama huukumbuki basi cheki video hii hapa).

Ushaikumbuka?Well,lengo la makala hii si kumjadili mwanamuziki huyo au wimbo huo uliovuma sana.Nacho-focus hapa ni hiyo ishu ya 'jini kwenye chupa'.

Lakini kabla sijainyambua,ngoja nikupe stori moja fupi.Mwaka 2005 nilipokwenda nyumbani kwenye fieldwork,nilikutana na rafiki yangu mmoja wa zamani ambaye ni mtoto wa Sharifu huko Tanga.Baada ya mahojiano yetu nilimdadisi kuhusu suala la majini.Nae bila hiana akanipa darasa kutoka A mpaka Z.Actually,alikwenda mbali zaidi hadi kunionyesha namna jini linavyotengenezwa.Bila kuingia kwa undani sana,alichovya maandishi flani kwenye chupa na kutengeneza kitu alichokiita kombe,kisha akafunga hiyo chupa.Akaeleza kuwa katika muda aliokusudia,jini litatoka katika hiyo chupa na 'kufanya vitu vyake' (kwa mujibu wa manuizo/dua.Bado nakumbuka jinsi nilivyosisimka baada ya 'kuonyeshwa jini mtarajiwa'

Naamini usemi 'jini ndani/kwenye chupa' unaendana na mantiki ya utengenezaji jini (yaani linawekwa kwenye chupa kisha 'linalipuka' katika muda ulokusudiwa).Kwa mujibu wa yule mtoto wa Sharifu ni kwamba jini likishatengenezwa na kuhifhadhiwa ndani ya chupa tayari kwa 'maangamizi' haliwezi kurejeshwa.Na la zaidi ni kwamba jini likishatoka kwenye chupa haliwezi kurudisha.Kwahiyo basi,usemi 'jini kwenye/ndani ya chupa' unamaanisha kitu ambacho 'kikitoka kimetoka',yaani ni kama maji yakimwagwa ardhini,hayawezi kuzoleka.

Kwanini basi nimeamua kutumia msemo huu katika makala hii?Well,katika uchambuzi wangu kuhusu kauli za/matendo ya Rais wetu (Chaguo la Mungu) Jakaya Kikwete,naanza kupatwa na wasiwasi huohuo wa 'jini ndani/kwenye chupa'.Simaanishi kuwa JK ndio jini.Hapana.Nazungumzia kauli na matendo yake ya hivi karibuni.

Sijawahi kuzungumzia lolote kuhusu hotuba yake kali alotoa kwa wafanyakazi wa serikali waliokuwa wametishia kugoma.Kwa kifupi,baadhi ya kauli zake hazikupaswa kutolewa na kiongozi anayejali utawala wa sheria.Kwa kutaja maneno kama risasi za moto au namna wafanyakazi wangeweza kukumbana na nguvu za polisi ilikuwa ni mithili ya kubariki ukatili.Hata kama wafanyakazi wangegoma bado isingehalalisha matumizi ya nguvu 'to an extent baadhi yao wangeweza kukumbana na makali ya risasi za polisi'.Hivi sio JK huyuhuyu alosema kuwa yeye anathamini haki za binadamu ikiwa ni pamoja na za mafisadi?Tuliache hilo kwa sasa.

Juzijuzi akaibuka tena na kudai suala la takrima ni gumu kukwepeka.Mkuu wa nchi anaposema hivyo ni sawa na kubariki matumizi ya rushwa kwa jina la takrima.Kauli kama hiyo haipaswi kutolewa hata na katibu kata,let alone Mkuu wa nchi.Ugumu wa jambo haumaanishi liachwe kama lilivyo.Yaani kwa vile mapambano dhidi ya ukimwi ni magumu kwahiyo tuache watu 'watembee pekupeku'?Au kwa vile ugonjwa wa malaria umekuwa ukitusumbua miaka nenda miaka rudi basi tuuache kwa vile ni vigumu kupambana nao?Sasa alipohamasisha kampeni ya ZINDUKA na wapambe wake wa bongoflava alikuwa anamaanisha nini?Rais alipaswa kuelewa kuwa kwenye mapambano dhidi ya udhalimu,giving up is not an option.Laiti Nyerere na wapigania uhuru wengine wangekuwa na mtizamo finyu kama huo wa 'jambo hili gumu kwahiyo tuliache kama lilivyo' basi hadi leo tungekuwa bado koloni la Mwingereza.

Kilichonishtua zaidi hadi kufikia hatua hii ya kuleta ulinganifu na 'jini kwenye/ndani ya chupa' ni mkanganyiko uliojitokeza katika sakata la Jumuiya ya Vijana wa CCM (UVCCM).Awali ilielezwa kuwa kuna vipeperushi vilivyosambazwa kumtuhumu aliyekuwa Mwenyekiti ya jumuiya hiyo,Hamad Yusuph Masauni.Baadaye gazeti moja likabainisha kuwa mtoto wa JK,Ridhiwani,anatuhumiwa kuivuruga jumuiya hiyo na kuchochea suala hilo la Masauni.Lakini,akihutubia mkutano wa Jumuiya hiyo huko Iringa,JK aliweka bayana kuwa (namnukuu) "Tulipochunguza ilibainika ni kweli alighushi, wakati wa uchaguzi alisema alizaliwa mwaka 1979, lakini ukweli alizaliwa mwaka 1973 na alianza darasa la kwanza mwaka 1979".Je hii haimaanishi kuwa hata vipeperushi vilivyosambazwa kumhusu Masauni vilikuwa na uhusiano na 'uchunguzi' huo anaozungumzia JK?Kama ni hivyo,je si hatari inapotokea kiongozi wa nchi anaporuhusu michezo michafu kama hiyo kwa minajili tu ya kukidhi matakwa flani?

Kinachokasirisha ni kauli yake kuwa  "kijana huyo (Masauni) mpole na mzito kufanya maamuzi magumu na haraka...ni mkakamavu na mchapakazi atapangiwa kazi nyingine hapo baadaye".Yaleyale ya Mwilima.Mtu anaboronga huku kisha anazawadiwa uongozi.Kama ni kweli Masauni alifoji umri wake,hivi hiyo haimpotezei sifa za kuwa kiongozi mahala kwingine?Sasa JK anapotuambia kuwa aatapangiwa kazi kwingine anamaanisha nini?Au huko atakapopangiwa hakuhitaji uadilifu?Na kama 'kudanganya umri' si big deal kwanini basi wameshinikiza aondolewe UVCCM?Nauliza hiyo kwa vile,kwa mujibu wa 'Chaguo la Mungu',kufoji umri kulikopelekea Masauni kujiuzulu sio big deal ndio maana 'atapewa kazi nyingine baadaye'.

Habari nyingine zinazoweza kuashiria kuwa 'jini lililo ndani/kwenye chupa linaweza kutoka muda wowote ule' ni katika jarida la Raia Mwema kwamba Mawaziri Wakuu wastaafu wanafuatiliwa.Ukisoma habari hiyo utabaini kuwa kwa vyovyovte vile,Mkuu wa Nchi anafahamu kuhusu suala hilo.Lakini sidhani kama tunapaswa kushangaa sana kwa vile kama Masauni alichunguzwa (which is equivalent to kufuatiliwa kwa ex-PMs hao) na hatimaye vipeperushi vikasambazwa,basi katika utawala huu lolote linawezekana,hususan uzandiki na character assassination.

Na hili suala la promotion ya familia kwenye uongozi,japo si kosa,linaweza kutafsiriwa kwa namna ya maandalizi ya udikteta.Baba/mume rais,mama/mke naye mwanasiasa 'kiaina',kaka wa rais naye mwanasiasa,mtoto naye mwanasiasa,na hadi kitinda mimba naye kaingizwa kwenye siasa.Na hapa sizungumzii siasa kwa maana ya hamasa tu bali siasa za mizengwe na kugombea kwa kutumia jina.Hapa tunazalisha mfalme au dikteta?

Kwa Watanzania wengi ni business as usual.Lakini kwa wanaoangalia ishu na kukumbuka kuweka alama za kuuliza,yayumkinika kufananisha suala hili na ' jini ndani/kwenye chupa'.LIKITOKA LIMETOKA,hakutokuwa na jinsi ya kulirejesha kwenye chupa.

Kwa atakayechukizwa na uchambuzi huu (kama yule mjinga alontumia comment ya matusi) all I could tell them is SUCK IT UP!


2 Jun 2009


Na Lilian Lugakingira, Bukoba

CHAMA cha Mapinduzi (CCM) kimeanza safari ndefu ya kumnadi Rais Jakaya Kikwete ili awe mgombea pekee katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, na tayari wilaya ya Bukoba Mjini imetoa hundi ya Sh1milioni za kulipia fomu yake ya kuwania nafasi hiyo.

Hundi hiyo ilitolewa jana na Umoja wa Vijana wa CCM wilaya ya Bukoba Mjini kwa maelezo kuwa umeridhishwa na uongozi wa Kikwete katika kutekeleza na kutimiza ilani ya CCM, na hivyo kuungana na jumuiya nyingine, vikundi na watu mbalimbali waliojitokeza kuanza kumkapenia Kikwete.

Hata hivyo, katibu mkuu wa CCM, Yusuf Makamba aliiambia Mwananchi jana kuwa hajui kwa nini jumuiya hiyo ya vijana wa chama chake imefanya hivyo na kwamba atawatafuta ili kupata ukweli na sababu za kitendo hicho.

"Niano msimamo wa chama, lakini siwezi kusema kwa sababu sijajua wamefanya nini. Bila shaka wanayo sababu," alisema Makamba baada ya kuuliza maswali mengi kuhusu kitendo hicho cha UVCCM Bukoba.

Katika halfa iliyofanyika mjini hapa, mwenyekiti wa UVCCM wa Bukoba Mjini, Chifu Kalumuna alimkabidhi mwenyekiti wa CCM wilayani Bukoba Mjini, luteni mstaafu Ally Shamte hundi ya fedha za kuchukulia fomu hizo.

Katika hafla hiyo, Kalumuna pia alimkabidhi mbunge wa Bukoba Mjini, Balozi Khamis Kagasheki hundi ya Sh 100,000 kwa ajili ya kuchukulia fomu za kuwania ubunge katika uchaguzi huo.

Akizungumzia sababu za kutoa fedha kwa Kikwete na Kagasheki kwa ajili ya kuchukulia fomu, katibu wa vijana wa Bukoba Mjini, Yusuph Kaliat alisema wamefanya hivyo kutokana na kuridhika na ufanisi katika utekelezaji wa ilani ya CCM.

“Sisi kama vijana na nguzo ya taifa, tumeamua kutoa zawadi hiyo ili viongozi hao waendelee kuongoza, kila mmoja kwa nafasi aliyokuwa nayo,” alisema Kaliat katika hafla hiyo iliyohudhuriwa na viongozi kadhaa wa CCM na UVCCM, akiwemo Kagasheki.

Chifu Kalumuna alikabidhi hundi zote mbili kwa Balozi Kagasheki ambaye naye alimkabidhi Shamte.Hakuna maelezo yaliyotolewa kwa nini UVCCM wilaya ya Bukoba imeamua kutoa fedha hizo sasa, ikiwa ni mwaka mmoja kabla ya mchakato wa uteuzi za majina ya wagombea na kuanza kampeni.

Kwa kawaida, CCM ina kipindi chake cha kuanza kampeni za ndani kwa wagombea wa nafasi zote za kuanzia serikali za mitaa, udiwani, ubunge na urais, lakini muda rasmi unaoruhusiwa na Tume ya Uchaguzi kwa ajili ya kuanza kampeni ni miezi minne kabla ya tarehe ya uchaguzi.

Uchaguzi mkuu utafanyika mwezi Agosti mwaka 2010.

Kitendo cha wilaya hiyo kutoa fedha kwa ajili ya kuchukulia fomu kinaelekea kuwa ni mkakati mpya wa kumnadi Kikwete pamoja na Kagasheki, ambaye hivi karibuni alikaririwa na baadhi ya vyombo vya habari akisema hatawania kiti hicho tena.

Fedha hizo za jumuiya ya vijana ya Bukoba Mjini ni sehemu ya kampeni kadhaa ambazo zimekuwa zikionekana katika miezi ya karibuni kumpigia debe Kikwete, ambaye alipata ushindi mkubwa katika uchaguzi wa mwaka 2005.

Hivi karibuni Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) mkoa wa Manyara ulimpendekeza Kikwete kuwa mgombea pekee wa nafasi ya urais katika chama chao cha CCM.Umoja huo ulitoa msimamo huo Mei 30 katika mkutano mkuu wa mkoa uliofanyika kata ya Magugu wilayani Babati ambako mgeni rasmi alikuwa katibu mkuu wa UWT, Hasna Sudi Mwilima.Risala ya akina mama hao iliyosomwa na katibu wa mkoa, Venosa Mjema ilisema wamenufaika zaidi na uongozi wa Rais Kikwete tangu alipoingia madarakani mwaka 2005.

Pia mkoa wa Rukwa ulionyesha kuridhishwa na uongozi wa Kikwete katika hafla ya kuchangisha pesa kwa ajili ya ujenzi wa shule za mkoa huo.Katika hafla hiyo iliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es salaam na ambayo mgeni rasmi alikuwa Kikwete, kiasi cha Sh 1.4bilioni kilichangwa kwa fedha taslimu au ahadi.

Wanachama wengine wa CCM waliowahi kutoa kauli za kutaka Kikwete awe mgombea pekee wa chama hicho ni pamoja na makamu mstaafu wa rais, Samuel Malecela, mwenyekiti wa zamani wa CCM mkoani Dodoma, Pancras Ndejembi na aliyekuwa mwenyekiti wa CCM mkoani Dar es Salaam, Mzee Hemed Mkali.

Baada ya wazee hao kutoa kauli hiyo mapema mwaka huu, Mbunge wa Sumve, John Shibuda alidai kwamba atachukua fomu kuwania urais mwaka 2010. Shibuda pia alikuwa miongoni mwa wana-CCM 11 waliochukua fomu kuwania urais mwaka 2005.

Wengine ni makamu mwenyekiti wa zamani wa CCM, Malecela, waziri mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Prof Mark Mwandosya, Balozi Patrick Chokara, Balozi Ali Karume, Dk Abdallah Kigoda, Dk William Shija, Dk Salim Ahmed Salim na Idd Simba.

Akionekana kunogesha kampeni za chini kwa chini hivi karibuni wakati wa uzinduzi wa mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoria hadi Shinyanga, Rais Kikwete mwenyewe alisema haoni sababu kwa nini akina mama waliofaidika na mradi huo wamnyime kura mwakani.

Nasema, kelele za mlango hazimzuii mwenye nyumba kupata usingizimimi sioni kwa nini akina mama walionufaika na mradi huu waninyime kura,” alisema Kikwete huku akishangiliwa na akina mama waliofika kwenye uzinduzi
huo.

CHANZO: Mwananchi
HABARI INAYOSHABIHIANA NA HII: UWT Wamteua Kikwete Kuwa Mgombea Pekee

PENGINE NI MUHIMU KUJIULIZA HAO UVCCM WILAYA YA BUKOBA MJINI WANA MRADI GANI WA KUWAWEZESHA KUWAKIRIMU "WAGOMBEA" HAO WATARAJIWA!PENGINE UTAULIZA KWANINI NI MUHIMU.WELL,NI RAHISI SANA KWA MAFISADI KUTUMIA COVER KAMA HIYO KUJIPENYEZA KWENYE ANGA ZA KITAIFA KWA MINAJILI YA KUFISADI NCHI BAADA YA UCHAGUZI HUO.

LAKINI CHA SEHEMU MUHIMU ZAIDI KATIKA HABARI HIYO HAPO JUU NI HIYO NUKUU NILIYOI-HIGHLIGHT KWA RANGI NYEKUNDU.IT SAYS IT ALL

10 Nov 2008

Na Mwandishi Wetu, Dodoma 

MKURUGENZI wa kampuni ya Shivacom Tanzania, Bw. Tamir Sonaiya ametoa jumla ya sh. milioni 400 kwa Umoja wa Vijana ya CCM (UVCCM) kwa ajili ya kugharamia Mkutano Mkuu wa Umoja huo unaotarajiwa kufanyika kabla ya Desemba 15, mwaka huu. 

Kati ya fedha hizo sh. milioni 150 zitakuwa ni posho za wajumbe 1,000 wa mkutano huo ambapo kila mmoja atalipwa sh. 50,000 na kiasi cha milioni 250,000 zimetumika katika kutengenezea fulana, mikoba, kofia na bendera za chama kwa ajili ya mkutano huo. 

Fedha hizo zilikabidhiwa jana makao makuu ya CCM mjini hapa mbele ya Rais Jakaya Kikwete. 

Akikabidhi fedha hizo, Bw. Sonaiya alisema kuwa ameamua kujitolea kusaidia chama chake kwa kuwa yeye ni kada mwaminifu wa CCM na vifaa vyote alivyotoa vimetengenezwa kutoka katika kiwanda chake. 

Kwa upande wa Rais Kikwete alimpongeza Mkurugenzi huyo kwa kujitolea fedha hizo na kuwataka makada wengine wa CCM wenye uwezo kusaidia chama hasa kwa wakati huu wa kuelekea uchaguzi Mkuu ambapo fedha nyingi huhitajika ili kugharamia maandalizi ya mikutano hiyo. 

“Kinachosumbua sana kwenye mikutano ni namna ya kupata fedha za kuhudumia mikutano hiyo hivyo kwa hatua iliyofanywa na Umoja wa Vijana itasaidia kuondokana na tatizo la fedha lililokuwa likiwakabili katika maandalizi ya mkutano wao,” alisema Rais Kikwete. 

Fedha hizo zimepatikana kupitia uhamasishaji uliofanywa na kamati iliyoteuliwa na Baraza Kuu la Umoja huo kwa ajili ya kufanya maandalizi ya mkutano huo ikiwa chini ya Waziri wa Nishati na Madini, Bw. Willium Ngeleja, Waziri wa Mambo ya Ndani, Bw. Laurence Masha na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bw. Willium Lukuvi.

CHANZO: Majira


17 Sept 2008

Chama cha siasa huzaliwa,hukua na kinaweza kufa pengine hata kabla hakijakua.Tofauti nachama nchi ikishazaliwa ni lazima iishi milele,tena kwa gharama yoyote ile.Lakini kuna wenzetu wengine hawataki kuelewa ukweli huo.Kwao,chama cha siasa ni kila kitu hata kama kinaipeleka nchi ahera.Angalia mfano huu mwepesi: chama kinapewa dhamana ya kuongoza nchi,lakini kinaendesha mambo yake kihuni na kupeleka nchi mrama.Ni dhahiri kwamba chama cha aina hiyo kinaamsha vurugu ambazo zitalekea mmomonyoko wa amani katika nchi husika.Kwa bahati mbaya au makusudi,kuna wenzetu hawataki kuamini kwamba ni vigumu kujenga na kudumisha amani kuliko kuivunja.Sote tunawajibika kuhakikisha nchi yetu haipelekwi kusikofaa badala ya kunyoosheana vidole tunapotofautiana namna ya kuboresha ustawi wa Tanzania yetu.

Katika toleo la wiki hii la gazeti mahiri la Raia Mwema,pamoja na mkusanyiko wa habari na makala motomoto,kuna hababari kuhusu the man of the moment,Nape Nnauye.Kuna wanaodai kuwa huyu jamaa aanashupalia ishu za ufisadi ndani ya UVCCM kwa minajili ya kutafuta umaarufu utakaopelekea apate nafasi ya juu kwenye jumuiya hiyo.Sina uhakika kuhusu hilo lakini binafsi naamini kwamba hata kama malengo yake ya ni kupata umaarufu au uongozi,jitihada zake kuushikia bango ufisadi ndilo lililo muhimu zaidi kuliko motives zake.Na wanaokemea ufisadi,hata kama kwa njia zisizo sahihi,wanapaswa kuungwa mkono badala ya kunyanyaswa.Enewei,habari ya Nape ni hii HAPA na mambo mengine motomoto yanapatikana ndani ya gazeti hili la RAIA MWEMA.


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.