10 Jun 2015

WIKI iliyopita ilitawaliwa na hekaheka za Uchaguzi Mkuu ambapo makada kadhaa wa chama tawala CCM walijitokeza kutangaza nia ya kuwania urais endapo watapitishwa na chama chao.
Kama nilivyoandika katika makala yangu iliyopita, uamuzi huo wa kuwania nafasi hiyo ni haki kwa kila Mtanzania mwenye sifa stahili. Hata hivyo, wingi wa makada wa CCM waliokwishatangaza nia ya kuwania urais, sambamba na idadi ya makada wanaotarajiwa kutangaza nia zao hivi karibuni, imezua maswali makuu mawili.
Kwanza, je utitiri huu wa wagombea ni matokeo ya kukua kwa demokrasia ndani ya CCM au nchini kwa ujumla? Swali hili linaendana na dhana halisi ya demokrasia ambapo wingi wa wagombea, wanachama au vyama vya siasa hutafsiriwa kama ishara za kukua au kustawi kwa demokrasia. Hata hivyo, mara kadhaa dhana hii imethibitika kuwa fyongo, ambapo nchi kadhaa zina idadi kubwa tu ya vyama vya siasa lakini mara nyingi vyama hivyo huwa ni kwa maslahi ya viongozi na sio kwa ajili ya kuwawakilisha wananchi. Licha ya vyama vya siasa, nchi kadhaa zina idadi kubwa ya wabunge, kama ilivyo Tanzania yetu, lakini kwa kiasi kikubwa idadi hiyo haijafanikiwa kumaanisha uwakilishi bora kwa wananchi.
Pili, je kujitokeza kwa idadi hiyo kubwa ya makada wa CCM kunachangiwa na kile kinachodaiwa kuwa urais wa Jakaya Kikwete umeshusha ‘bar’ ya wadhifa huo kiasi kwamba kila mtu anapata ujasiri wa kuitaka nafasi hiyo? Japo ni vigumu kupata mwafaka wa jumla kuhusu miaka kumi ya utawala wa Rais Kikwete, kumekuwa na hisia za mara kwa mara kwamba utawala wake umekuwa wa kirafiki zaidi, au ‘kishkaji’ kama wanavyosema huko mtaani. Teuzi mbalimbali zimekuwa zikitazamwa kama za kirafiki na sio kutokana na sifa stahili za wateuliwa. Na hili linadaiwa kuchangia mabadiliko kadhaa ya kabineti ya kiongozi huyo.
Tumeshuhudia mara kadhaa jinsi Rais Kikwete alivyopatwa na kigugumizi kuchukua hatua stahili dhidi ya watendaji wake, kikwazo kikidaiwa kuwa ni urafiki uliopo kati yake na watendaji hao walioshindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo. Sasa, urais sio uongozi wa nchi tu bali ni ulezi wa viongozi wajao ikiwa ni pamoja na marais wajao. Na ndio maana tumesikia baadhi ya watangaza nia wakijisifu kuwa wamekuwa wasaidizi wa Rais Kikwete kwa muda fulani, wakimaanisha wamejifunza mambo kadhaa kutoka kwake. Kwa hiyo ni wazi ubora au upungufu wake unawagusa walio chini yake, na katika harakati hizi za kupatikana mrithi wake, yawezekana umechangia kutuletea rundo hili la wanaotaka kumrithi.
Lakini iwe ni kukua kwa demokrasia au urais wa Kikwete umeifanya nafasi hiyo kuwa ya ‘kawaida’ kiasi kwamba mwanasiasa yeyote anaweza kujiona anaweza kuimudu, ukweli unabaki kuwa waliojitokeza kuwania nafasi hiyo hawajavunja kanuni yoyote, na Katiba yetu inawaruhusu kufanya hivyo. Hata hivyo, sisi kama wananchi pia tuna haki ya msingi ya sio tu kuwaunga mkono au kuwapinga wanaojitokeza kuwania nafasi hiyo bali pia kuwachambua, kuwapongeza au kuwakosoa. Na makala hii inajikita zaidi katika kuchambua kwa ujumla zoezi hilo la kutangaza nia ya kuwania urais miongoni mwa makada kadhaa wa CCM waliokwishajitokeza hadi sasa.
Kimsingi, ukiondoa Makongoro Nyerere ambaye aliweka bayana kuwa hawezi kutangaza ajenda zake binafsi ilhali mgombea atakayepitishwa na CCM atapaswa kuuza sera zake kwa mujibu wa ilani ya uchaguzi ya chama hicho, makada wengine wote waliotangaza nia wameongelea masuala yale yale ambayo takriban kila Mtanzania anayafahamu. Nisingependa kuyaorodhesha hapa kwa vile ninaamini kila mmoja wetu anatambua tunachohitaji, tunachostahili kuwa nacho lakini hatuna na kwa nini hali iko hivyo.
Labda jambo moja la wazi ni kwamba nchi yetu ina utajiri mkubwa wa wanasiasa wenye uelewa wa hali ya juu wa matatizo yanayoikabili Tanzania yetu, sambamba na mbinu za kuyatatua matatizo hayo. Takriban kila mtangaza nia ya kuwania urais amejitahidi kwa undani kuyachambua matatizo yetu, wengine wakienda mbali zaidi na kuelezea vyanzo vya matatizo hayo, na kutoa ufumbuzi wa kuyatatua.
Swali la msingi ni hili: walikuwa wapi siku zote na ‘utaalamu huo wa matatizo yetu’ hadi nchi yetu kufikia katika hali hii mbaya tuliyo nayo sasa? Je, yawezekana licha ya takriban wote kuwa walipewa nafasi na Rais Kikwete kuwa mawaziri au manaibu waziri katika kabineti zake, walimhujumu kwa kuficha uwezo wao ili baadaye waje kutumia upungufu uliopo kama mtaji wa kuomba nafasi hiyo ya urais?
Haiingii akilini kabisa kusikia mtu akielezea lundo la matatizo yetu ikiwa ni pamoja na yale ambayo hata baadhi ya wananchi hawayafahamu, na kutoa majibu mengi zaidi ya matatizo hayo, lakini mtu huyo huyo amekuwa serikalini kwa miaka kadhaa pasipo kutumia japo asilimia 0.1 ya ujuzi anaotueleza anao kuhusu matatizo yetu.
Je, wanaotaka kutueleza kuwa haikuwa rahisi kwao kuweza kututumikia kwa uwezo wao wote kwa vile tu hawakuwa marais? Nauliza hivyo kwa sababu ghafla, hata baadhi ya mawaziri ambao waliishia kutimuliwa kwa skandali za ufisadi wanamudu kutueleza kuwa wana ufumbuzi wa matatizo yetu. Ninahitimisha kuwa huu ni utapeli wa kisiasa, kwa kimombo wanasema political conmanship.
Nadhani wanaohisi kuwa Rais Kikwete ameishusha sana ‘bar’ ya urais wanapata nguvu ya hoja hiyo kutokana na wanasiasa kama hao, ambao umaarufu wao hautokani na nyadhifa walizoshika bali skandali zilizosababisha wang’olewe madarakani. Inakera na kuchukiza kuoina wanasiasa ambao pasi kuambiwa na mtu yeyote yule wanajitambua kuwa hawafai lakini leo wanapata ujasiri wa kutaka wapewe urais. Hivi URAIS umekuwa URAHISI kiasi hicho?
Lakini hata tukiweka kando maswali hayo ya msingi, hizi hadithi tamu za kuleta matumaini kwa kila anayezisikia zitawezekana vipi ilhali pindi wakipitishwa na chama chao hawatojinadi kwa ahadi hizo bali zitakazobainishwa kwenye ilani ya chama chao?
Sawa, labda watasema kuwa ukiwa mgombea una fursa ya kushiriki uandaaji wa ilani hiyo, lakini ukweli mchungu ni kwamba CCM haitoafikiana na mgombea atakayekuja na sera za kukiua chama hicho. Ninasema ‘sera za kukiua’ kwa sababu kwa kiasi kikubwa chama hicho kimeachana kabisa na misingi yake ya asili ya kuwa mtetezi wa wanyonge na badala yake kimetekwa na mafisadi. Chama kinachojigamba kuwa ni cha wakulima na wafanyakazi kimekuwa chama cha matajiri na wasomi wasiotaka kutumia usomi wao kwingineko, bali katika siasa (kwa minajili ya ulaji).
Kibaya zaidi, wengi wa makada waliotangaza nia wamekuwa wezi wa sera za vyama vya upinzani, sera ambazo makada hao wamekuwa wakizikejeli mara kadhaa lakini ghafla wameziona zinafaa kwa vile wanaotaka tuwaamini kuwa wanaweza kutuongoza. Ninarejea tena, huu ni utapeli wa kisiasa.
Nimekuwa nikifuatilia kwa karibu maendeleo ya harakati hizo za kutangaza nia ya kuwania urais, kupitia mitandao ya kijamii. Japo Watanzania waliopo kwenye mitandao hiyo ni wachache lakini kwa kuzingatia kanuni za tafiti, wanaweza kuwa sampuli nzuri kuwakilisha mitizamo mbalimbali ya Watanzania wengi kwa ujumla. Nimebaini masuala kadhaa katika ufuatiliaji wangu: kwanza, angalau Watanzania wengi wanafahamu wanasiasa wa aina gani wasiotakiwa katika urais. Lakini hapo hapo kuna tatizo: wanajua wasiyemtaka lakini hawajui wanayemtaka.
Katika hili ninawatumia lawama nyingi ndugu zetu wa vyama vya upinzani hususan UKAWA. Hivi watu hawa wana maelezo yoyote ya maana zaidi ya uzembe kwa kushindwa kutumia fursa hii ambapo ‘CCM wanakabana makoo wenyewe kwa wenyewe’ kumnadi mgombea wao laiti wangekuwa wameshampata? Watetezi wao wanadai UKAWA wapo ‘bize’ kuhangaikia suala la uandikishaji wapiga kura. Hilo ni suala muhimu lakini lisiloweza kuwazuia wao kukamilisha mchakato wa kumpata mgombea wao.
Jingine nililogundua katika ufuatiliaji wangu ni wepesi wa Watanzania kuhadaiwa na maneno matamu yasiyoambatana na uthibitisho wowote ule kuwa ni ya kweli. Mara baada ya hotuba utasikia watu wakidai “aisee huyu jamaa anatufaa haswa…” kisa katoa hotuba nzuri. Tangu lini uwezo wa kutoa hotuba nzuri unamaanisha uwezo wa kivitendo? Kimsingi, Tanzania yetu haijawahi kuwa na uhaba wa watoa porojo. Sisi ni wazuri kweli kwa maneno ila tatizo letu ni kwenye kutafsiri maneno kuwa vitendo.
Ukitaka kujua uwezo wetu katika porojo nenda kwenye vikao vya harusi, au hata kwenye vijiwe vya kahawa. Huko kuna watu wanaongea sio tu kama wamemeza santuri au CD nzima bali pia wana uelewa na utaalamu wa hali ya juu wa fani ambazo wala hawakukanyaga darasani kuzisomea. Sasa kama hayo yanawezekana vijiweni, kwa nini nikiamua kuwania urais nisitumie uwezo wangu wote wa upigaji porojo kuwahadaa watu kuwa mimi ndiye yule waliyekuwa wakimsubiri miaka nenda miaka rudi? Pengine kufikia hapa, ninakuomba msomaji mpendwa tafuta wimbo wa ‘Ndio Mzee’ wa msanii wa muziki wa Bongofleva, Joseph Haule (Profesa Jay) kisha rejea ninachokieleza hapa.
Nimalizie makala hii kwa kuwakumbusha Watanzania wenzangu, uchaguzi mkuu ujao haupo kwa manufaa ya chama au mgombea fulani. Ni kwa ajili yetu sisi wananchi. Sisi ndio wanufaika wa uamuzi bora utakaotupatia mtu wa kuikomboa Tanzania yetu kutoka hapa ilipo na kuifikisha inapostahili kuwepo, na sisi ndio waathirika iwapo tutafanya uamuzi fyongo kama tulivyofanya huko nyuma hadi kujikuta tulipo sasa. Mtaani wanasema ‘akili za kuambiwa changanya na za kwako.’ Ninawasihi Wtaanzania wenzangu kutokuwa wepesi kuhadaiwa na hizi porojo ambazo tumekuwa tukizisikia miaka nenda miaka rudi na nchi yetu inazidi kuangamia kwa umasikini, ufisadi na mabalaa mengine.

5 Jun 2015


Tafsiri: CEORT ina furaha kuwa mwenyeji wa mdahalo wa kwanza katika historia ya Tanzania kwa wanaowania urais. Tutaweka uchumi kuwa mada kuu ya mdahalo huo mwaka huu, na sio watu (wagombea) au rangi za vyama. Sumaye, Balozi Amina Salum Ali, January Makamba, Bernard Membe na Samule Sitta watakuwa wa kwanza kutangaza vipaumbele vyao kisera kwa taifa katika shughuli hiyo. Cha kusikitisha, EDWARD LOWASSA amekataa kushiriki. Ungana nasi hoteli ya Hyatt (jijini Dar es Salaam) Jumatatu ijayo saa 2 asubuhi.Midahalo mingine miwili na watangaza nia wengine ikiwajumuisha wanasiasa wa upinzani itafuata.

Huyu LOWASSA ndiye anayehamasisha mchakmchaka wa maendeleo? Ni rahisi sana kuwahadaa watu kwa kuwahubiria porojo lakini yahitaji ujasiri na uwezo wa kiongozi kushirikia mdahalo wa kuwashawishi Watanzania kwanini unafaa kuwaongoza


Tunahitaji Rais mpinga ufisadi si wa kujitetea eti yeye si fisadi

HATIMAYE baada ya taarifa za muda mrefu zisizo rasmi, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, alitangaza mwishoni mwa wiki iliyopita dhamira yake kukiomba Cchama Cha Mapinduzi (CCM) kimpitishe kuwa mgombea wa kiti cha urais katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, mwaka huu.

Taarifa za Lowassa kutaka urais zimekuwa zikivuma kwa muda mrefu mno, na kwa hakika haikuwa jambo la kushangaza alipoamua majuzi kuzibadili taarifa au tetesi hizo kuwa jambo kamili.

Binafsi, baada ya kuisikia hotuba yake aliyoitoa jijini Arusha mbele ya halaiki ya wananchi nimebaki na swali moja la msingi: Lowassa ana kipi hasa cha kuwafanya Watanzania waamini kaulimbiu yake ya ‘safari ya matumaini.’
Sijui kwenu wasomaji wapendwa, lakini kwangu kubwa linalonifanya nimkumbuke Lowassa ni kashfa ya Richmond ambayo hatimaye ilisababisha ajiuzulu wadhifa wake wa Uwaziri Mkuu.

Na kwa sababu anazojua yeye mwenyewe, hotuba yake ya Arusha haikugusia suala hilo ambalo awali alipozungumza na waandishi wa habari alidai angeliongelea kwa kirefu. Tayari kuna baadhi yetu tunaoanza kuhoji uwezo wa mwanasiasa huyo kushika nafasi nyeti ya urais, na swali ni hili: kama ndani ya wiki moja anaweza kuahidi kuzungumzia kashfa ya Richmond na kisha asizungumzie, je mustakabali wa taifa letu utakuwaje mikononi mwa mtu anayeweza kuvunja ahadi anazojiwekea mwenyewe?

Pengine katika hatua hii ni muhimu nitanabaishe kuwa sina tatizo na Lowassa kutumia haki yake ya kikatiba na kidemokrasia kuwania urais. Hiyo ni haki ya kila Mtanzania mwenye sifa stahili. Lakini kwa hakika natatizwa sana na uadilifu wake.

Licha ya suala la Richmond, ambalo amedai yeye hahusiki, kuna hoja ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ‘kumwekea vikwazo’ huko nyuma katika nia yake ya urais, ambapo inaelezwa kuwa Nyerere alitatizwa na utajiri mkubwa wa mwanasiasa huyo usio na maelezo ya kuridhisha.

Na majuzi Lowassa katamka bayana kuwa anauchukia umasikini. Na amekiri kuwa yeye ni ‘tajiri kiasi.’ Lakini pengine Watanzania wengi wangependa sana kufahamu chanzo cha utajiri wake kwa sababu sote tunajua mtu haamki tu na kujikuta tajiri. Sawa, amekuwa mtumishi wa umma kwa muda mrefu, lakini kwa jinsi anavyomudu ‘kumwaga pesa’ katika shughuli mbalimbali, ni vigumu kuamini kuwa chanzo cha fedha hizo ni utumishi wake wa muda mrefu serikalini pekee.

Nyakati kadhaa amekuwa akitueleza kuwa kuna marafiki zake wanaomchangia fedha ‘anazomwaga’ katika hafla mbalimbali. Je, ni marafiki gani hao? Lakini kubwa zaidi, vyanzo vya utajiri wao ni vipi hasa?

Kadhalika, mwanasiasa huyo ameonekana kuzungukwa na wanasiasa wenzake kadhaa ambapo miongoni mwao ni majeruhi wa skandali mbalimbali za ufisadi. Waingereza wana msemo, nionyeshe marafiki zako, nami nitakueleza wewe ni nani’ (show me your friends and I will tell who you are). Hivi Lowassa anaweza kutueleza lolote kuhusu ukaribu alionao na watu hao?

Kwa upande mwingine, mie nilipoisikiliza kwa makini hotuba yake ya majuzi huko Arusha niliona kama ninamsikiliza mtu ambaye tayari ameshapitishwa na chama chake kugombea urais na kilichobaki ni taratibu tu za kumkabidhi wadhifa huo. Sina tatizo na kujiamini kwake lakini kuna wanaojiuliza, hivi huyu mtu asipopitishwa na chama chake itakuwaje?

Kuhusu kaulimbiu yake ya ‘safari ya matumaini,’ bahati nzuri siku moja tu baada ya kuitangaza, Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willbroad Slaa, akawafumbua macho Watanzania kwa kuwaeleza kuwa kinachohitajika sio safari ya matumaini bali ya uhakika. Watanzania wamekuwa wakiishi kwa matumaini kwa muda mrefu sana; matumaini kwamba siku moja nchi yao itaondokana na umasikini ilionao na kuishi kulingana na utajiri lukuki iliyojaliwa nao; matumaini ya kuondokana na janga la ufisadi linalozidi kuota mizizi; matumaini ya kuona sarafu yao ikiacha kuporomoka kwa kasi; matumaini ya mgawo wa umeme wa kudumu kufikia kikomo; matumaini ya maisha bora kwa kila Mtanzania waliyoahidiwa miaka 10 iliyopita na timu ya uchaguzi ya Rais Jakaya Kikwete ambayo ilikuwa ikiongozwa na Lowassa, na matumaini mengine kadha wa kadha

Hapana, Watanzania wanaotaka safari ya uhakika, kama alivyosema Dk. Slaa, na sio ya matumaini hewa kama yaliyoahidiwa miaka kumi iliyopita na yamebaki kuwa historia tu.

Awali, Lowassa alidai kuwa moja ya vipaumbele vyake vikuu ni elimu, na kuleta kaulimbiu nyingine ya elimu kwanza. Labda kabla ya yeye kuiponda kaulimbiu ya kilimo kwanza angewaambia Watanzania kwa nini imebaki kuwa porojo tu lakini hiyo yake itatekelezwa kwa vitendo.

Pengine atazungumzia uanzishwaji wa shule za kata. Tukiweka kando matatizo kadhaa yanayozikabili shule hizo, maarufu kama ‘Santa Kayumba,’ ni muhimu Watanzania wenzangu kutambua kuwa hazikujengwa kutoka hela za mfukoni mwa Lowassa. Ninaelewa kwa nini mwanasiasa huyo anaweza kutaka kujichukulia pointi kwenye suala hilo; kasumba iliyojengeka miongoni mwetu kwamba mtu akiajiriwa kutimiza wajibu fulani na analipwa kutimiza wajibu huo anaonekana mchapakazi. Yaani tumefika mahala kuwa inatarajiwa mtu akipewa majukumu atafanya ubabaishaji, Kwa hiyo yule atakayefanya kinyume cha kuwajibika, basi inakuwa kama miujiza.

Sidhani kama Lowassa ana moja la kuwaeleza wananchi kuwa hili nililifanya kwa jitihada zangu kama Edward na sio Waziri Mkuu niliyekuwa ninalipwa mshahara kutimiza wajibu huo.

Tukirejea kwenye hotuba yake, binafsi sikusikia jambo lolote geni ambalo hatulifahamu. Sote tunajua kuhusu umasikini wetu, sote tunafahamu kuhusu matatizo yote aliyoyataja katika hotuba yake. Na kwenye tatizo la foleni za magari jijini Dar es Salaam amnbazo amedai atazimaliza ndani ya miezi 12, niseme tu kuwa hiyo ni porojo.

Kwanza, kwani alipokuwa Waziri Mkuu huko nyuma tatizo hilo halikuwepo hadi hakuona haja ya kulitatua? Pili, foleni sio tatizo jijini Dar es Salaam tu bali hata kwenye majiji makubwa ya Ulaya na katika mabara mengine. Kwetu linakuwa tatizo sugu zaidi kutokana na miundombinu mibovu na idadi kubwa ya uhamiaji mijini isiyoendana na wahamiaji, sambamba na wingi wa magari yakiwemo yasiyostahili kuwepo barabarani.

Amejitahidi kutueleza matatizo ambayo kila mmoja wetu anayafahamu. Hata hivyo kama ilivyo kwa maradhi, suala sio tu tabibu kuelezea mgonjwa anakabiliwa na tatizo gani la kiafya bali kumwelekeza tiba na hatimaye kumpatia tiba husika. Wanasiasa wetu hawaishiwi umahiri wa kuyajua matatizo ya wananchi, hata kama wanasiasa hao hawajawahi kukumbana na matatizo hayo ‘ana kwa ana.’ Sawa, ili kuweza kulitatua tatizo ni lazima kujua chanzo chake, lakini haina manufaa kutaja tu matatizo tuliyonayo pasi kuyaeleza yametokana na nini au jinsi gani tunaweza kuyakabili.

Nikiri kwamba nilipata hasira kumsikia Lowassa akiwaimbia wananchi kuhusu ‘mchakamchaka wa maendeleo’ bila kuwaambia maendeleo hayo yataletwa vipi, na kwa nini miaka zaidi ya 50 tangu tupate Uhuru (na Lowassa akiwa mtendaji wa serikali katika miaka kadhaa katika hiyo) bado tunasuasua kimaendeleo.

Nimalizie makala hii kwa kurejea nilichoandika hapo awali kuwa Lowassa ana haki kikatiba kuwania urais. Hata hivyo, name kama Mtanzania pia nina haki ya kuelezea bayana kuwa mwanasiasa huyu hafai kuwa rais wetu ajaye, sababu kubwa zaidi ikiwa ni suala la ufisadi wa Richmond.

Hatuhitaji mgombea wa urais ambaye badala ya kutueleza jinsi ya kukabiliana na moja ya matatizo makubwa kabisa yanayoikabili Tanzania, yaani ufisadi, anatumia muda mwingine kujitetea kuwa yeye sio fisadi.


Wito wangu kwa Watanzania wenzangu ni huu: tunastahili kilicho bora. Haiingii akilini kabisa kuamini kuwa mtu aliyelazimika kujiuzulu kwa kashfa ya ufisadi akiwa Waziri Mkuu, atakuwa kiongozi bora akishika urais. Ni muhimu kufumbua macho na masikio na kuacha kuamini hizo porojo ambazo tumekuwa tukizisikia miaka nenda rudi lakini Tanzania yetu inazidi kudidimia.

29 May 2015

Tarehe kama ya leo miaka 7 iliyopita (29/05/2008), mama yangu mzazi Adelina Mapango (Mama Chahali) alifariki. Kifo chake kimeacha pengo kubwa lisilozibika-kwa mumewe (yaani baba) walodumu katika ndoa kwa miaka 53, kwa sie wanawe wanane, na hasa kwa vitinda mimba Kulwa na Doto ambao kwao marehemu alikuwa ni zaidi ya mzazi kwao bali rafiki pia. Miaka 6 imepita lakini uchungu moyoni ni kama kifo hicho kimetokea leo. We miss you so much mama. We stiĺl and will always love you. May your soul rest in eternal peace. Amen!




28 May 2015

HATIMAYE kipenga cha kuanzisha mbio za kumrithi Rais Jakaya Kikwete kimepulizwa rasmi, kwa upande wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambapo majuzi chama hicho tawala kilitangaza ratiba ya kupata wagombea wake katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Lakini kabla ya hatua hiyo, kuna matukio makuu mawili yanayohusiana na mbio hizo za urais yaliyotokea hivi karibuni. Kwanza, Ikulu ilitangaza kuwasafisha watendaji kadhaa wa serikali ambao walipoteza nyadhifa zao huko nyuma kutokana na kashfa za Operesheni Tokomeza na Akaunti ya Tegeta Escrow. Huhitaji kuwa na ujuzi wa uchambuzi wa siasa za Tanzania kutambua kuwa hatua hiyo inaweza kuhusishwa na harakati za urais baadaye mwaka huu.
Pengine hatua hiyo ya Ikulu iliyowashangaza wengi inaweza kuwa imetumia fursa ya wabunge wa chama hicho waliovalia njuga sakata hilo kubanwa na harakati zao binafsi za kutaka kurejea tena bungeni baada ya Uchaguzi Mkuu ujao. Ni dhahiri kuwa mbunge anayetegemea ridhaa ya CCM kumpitisha agombee tena anajikuta katika wakati mgumu kuikosoa serikali ya chama hicho, kwani inaweza kupeleka mizengwe dhidi yake huko mbeleni.
Lakini kwa upande wa pili, wahusika waliosafishwa kuhusu kashfa hizo wametengenezewa mazingira mazuri ya kuingiza majina yao katika ‘kapu’ la wenye dhamira ya kugombea urais. Na hata kama hawatataka kugombea urais, basi kikwazo cha kuondolewa madarakani kutokana na kashfa hizo hakipo tena iwapo wataamua kugombea ubunge tu.
Japo binafsi ninaamini baadhi ya watendaji waliowajibishwa kutokana na kashfa hizo walikuwa majeruhi tu, hususan aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki (ukifuatilia kwa makini utabaini kuwa kuna watu wengi wenye imani kama hiyo yangu), wengine wanaonekana kusafishwa kwa vile tu ‘huwezi kumsafisha huyu na kumuacha yule.’
Tukio la pili lilikuwa hatua ya CCM kuwafungulia makada wake walioadhibiwa kwa kukiuka taratibu za kuwania nafasi ya urais kupitia chama hicho. Adhabu hiyo ilikuwa mzaha tangu ilipotangazwa. Mzaha sio tu kwa sababu wengi wa walioadhibiwa waliendelea na ‘kampeni’ zao waziwazi, lakini pia mantiki nzima ya adhabu ilikuwa fyongo. Licha ya kuwa chama hicho tawala kina taratibu zake za kupata wagombea katika nafasi mbalimbali, kuwanyima wanachama wake uhuru wa kutangaza nia ya kuwania uongozi ni sawa na udikteta.
Ukifuatilia kwa makini, utabaini kuwa hatua ya baadhi ya makada wa chama hicho kutangaza nia ya kumrithi Rais Kikwete hapo Oktoba imewasaidia Watanzania kuwaelewa wanasiasa hao kwa kiasi kikubwa. Katika nchi za wenzetu waliokomaa kidemokrasia, wenye dhamira ya kuwania urais hutangaza takriban mwaka kabla ya Uchaguzi Mkuu, kama tunavyoshuhudia huko Marekani. Kwa vile urais si suala la mgombea au chama pekee bali wananchi wote kwa ujumla, kuna umuhimu mkubwa kwa wanaotaka kuongoza nchi kufahamika mapema ili wapiga kura wawapime kama kweli wanafaa na kustahili kushika nyadhifa wanazowania.
Tukiweka kando matukio hayo mawili, mwishoni mwa wiki iliyopita, Halmashauri Kuu ya CCM ilikutana huko Dodoma, na kama ilivyotarajiwa, suala la Uchaguzi Mkuu lilitawala kikao hicho muhimu. Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana baada ya kikao hicho, Mwenyekiti wa Taifa wa CCM, Rais Kikwete alitoa wito kwa chama hicho kuchagua mgombea anayekubalika ndani na nje ya chama.
Kadhalika, Rais Kikwete aliwaonya wana-CCM wenzake kwamba zama za kudhani kuwa mgombea yeyote atakayepitishwa na chama hicho atakuwa rais zimepitwa na wakati.
Hebu tuzichambue kidogo kauli hizo mbili. Kuhusu CCM kupata mgombea anayekubalika ndani na nje ya chama, nadhani tatizo ni ‘nini kinamfanya akubalike?’ Wengi tunaifahamu vema CCM na utamaduni uliojengeka wa ‘kununua kukubalika.’ Japo wenyewe wanaweza kupinga, lakini ni ukweli usiofichika kuwa ni rahisi mno kwa kugema damu kwenye jiwe kuliko kupitishwa kugombea uongozi katika chama hicho kama huna fedha za kutosha. Na uthibitisho wa hilo upo katika takriban kila chaguzi za ndani katika chama hicho hadi kwenye uongozi wa chipukizi.

Na pengine ushahidi mkubwa zaidi ni katika ‘kukubalika’ kwa mmoja wa makada wa chama hicho ambaye licha ya kulazimika kujiuzulu kutokana na kashfa moja kubwa huko nyuma, uwezo wake mkubwa kifedha umesababisha makundi mbalimbali ya kijamii kumuunga mkono huku walalahoi kadhaa wakimchangia fedha za kulipia fomu ya kuwania urais. Je, huyu anakubalika ndani na nje ya CCM kwa sababu ya uwezo wake kiuongozi au uwezo wake kifedha?
Lakini changamoto kubwa kwa Rais Kikwete ni nguvu yake ndani ya chama hicho. Baadhi yetu tunaofuatilia kwa karibu mwenendo wa siasa za nchi yetu tunadhani kuwa uenyekiti wa Kikwete umebaki kuwa wa heshima zaidi kuliko wenye nguvu ya kufanya matakwa yake sio tu yasikilizwe bali pia yatekelezwe. Kuna wanaodai kuwa baadhi ya makada wa chama hicho wana nguvu zaidi ya mwenyekiti Kikwete, na hilo linaweza kukwamisha matakwa yake kuona CCM inapata mgombea stahili.
Kuhusu zama za mgombea atakayepitishwa na CCM kuwa rais ‘moja kwa moja,’ bado mazingira yaliyopo yanakipendelea chama hicho tawala. Kitakachoweza kuiangusha CCM si mabadiliko ya kimazingira bali mazingira ndani ya chama hicho. Kuna kitu kinafahamika kama ‘tactical voting’ ambacho majuzi tu kilimwokoa aliyekuwa Naibu Waziri Mkuu wa hapa Uingereza, Nick Clegg, kushindwa ubunge katika jimbo lake wakati alikuwa akikabiliwa na upinzani mkali na kulikuwa na dalili kuwa angeangushwa. Sasa, kwa vile chama tawala cha Conservatives kilikuwa kinamhitaji Clegg, ambaye alikuwa kiongozi wa chama cha Liberal Democrats kilichounda serikali ya pamoja na Conservatives baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, wafuasi wake walimpigia kura kwa wingi na ‘kumtosa’ mgombea wa chama chao, kwa malengo ya kumsaidia Clegg ashinde.
Kwa hiyo, endapo CCM watampitisha mgombea ambaye wanachama wengi hawamtaki, wakati wa kura, tactical voting inaweza kuvinufaisha vyama vya upinzani. Lakini ili wapinzani waweza kunufaika basi sharti nao wawe na mgombea ambaye ana sifa zaidi ya huyo ‘mbovu’ wa CCM. Ni muhimu kutambua kuwa ili wapigakura bila kujali itikadi zao ‘waitose’ CCM, lazima waaminishwe kuwa chama au mgombea mbadala ni bora zaidi ya CCM au mgombea wake.
Nimalizie makala hii, ambayo ninatarajia kuiendeleza siku zijazo kwa kadiri tunavyojongea kwenye Uchaguzi Mkuu, kwa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuwa uchaguzi huo si kwa ajili ya manufaa ya chama au mgombea fulani. Wanufaika au waathirika wa uchaguzi huo ni wananchi.
Na uzoefu umekwishatuonyesha jinsi ‘mahaba kwa chama au mgombea’ yalivyosababisha miaka mitano ya kujilaumu kwa kukubali utapeli wa kisiasa. Ni muhimu kuweka mbele maslahi ya nchi na kumchagua mtu atakayeweza kuikwamua Tanzania kutoka katika lindi la umasikini unaochangiwa zaidi na ufisadi.
INAWEZEKANA, TIMIZA WAJIBU WAKO

- See more at: http://www.raiamwema.co.tz/kikwete-ni-mwenyekiti-wa-heshima-ccm#sthash.lZwwRU9T.dpuf

21 May 2015



Bonyeza HAPA kuangalia specs kamili za simu hii inayotarajiwa kuingia moja kwa moja katika nafasi ya kwanza ya simu bora zilizopo duniani kwa sasa



WAZIRI mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, ameanza kuwaandaa wafuasi wake kwa uwezekano wa kujiunga na mojawapo ya vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Raia Mwema limeelezwa.

Taarifa ambazo gazeti hili limezipata kutoka katika kambi ya mgombea huyo zinaeleza kuwa amepiga marufuku mazungumzo yoyote ya kutafuta mbadala wake ndani ya CCM na kutaka nguvu yote ielekezwe kwake.

Gazeti hili limeelezwa kuwa wapo watu walio ndani ya kambi yake wanaoamini kwamba anahitajika mwanasiasa mwingine ndani ya kundi hilo ambaye anaweza kuvaa viatu vya Lowassa endapo CCM itaamua kumkata au kuendeleza adhabu yake ya kutofanya shughuli za siasa aliyopewa na chama chake.

Hata hivyo, kundi hilo linadaiwa kuwa na wakati mgumu kwa madai kwamba Lowassa hataki kusikia chochote kuhusu suala hilo.

“Anasema yeye ndiyo Plan A, Plan B na Plan C. Kama, kwa sababu yoyote ile, CCM itaamua kumpitisha mgombea mwingine na si yeye, yuko tayari kujiunga na Ukawa lakini si kubaki ndani ya chama.

“Hili ndilo jambo linalotusumbua sana kwa sasa. Hakuna vita ambayo ina mpango mmoja tu. Lazima muwe na mpango zaidi ya mmoja. Huku Pwani wanasema ukienda kuteka maji wakati wa ukame, ni muhimu uwe na ndoo na kidumu cha kushika mkononi.

“Kwenye kutembea na ndoo mtu unaweza kujikwaa na maji yote yakamwagika na kile kidumu cha mkononi ndiyo kikakuokoa. Sasa huyu bwana hataki kusikia habari ya kidumu.
“Anataka twende kutafuta maji na ndoo moja tu ambayo ni yeye. Hili linatupa shida kidogo kwa sasa,” alisema mbunge mmoja wa Mkoa wa Dar es Salaam ambaye ni mtu wa karibu na mtarajiwa huyo.

Katika kambi ya Lowassa, kuna majina ya wanasiasa vijana ambao wanatajwa kuwa tayari kuvaa viatu vyake endapo CCM itaamua tofauti na matarajio yao.

Miongoni mwa wanasiasa wanaotajwa kuwa katika kambi ya Lowassa na ambao kambi inayotaka Plan B inawapendekeza ni Mbunge wa Songea Mjini, Dk. Emmanuel Nchimbi, Mbunge wa Sengerema William Ngeleja, Waziri wa Mambo ya Ndani, Mathias Chikawe na Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba.

Miongoni mwa wanaotajwa, Dk. Nchimbi anaelezwa kuwa na nguvu zaidi kutokana na ukweli kwamba ndiyo mwenye ushawishi zaidi ndani ya chama kutokana na ukweli kuwa amekuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM kwa zaidi ya miaka 10.

Kimsingi, kwa upande wa Tanzania Bara, hakuna mwana CCM aliyedumu katika Kamati Kuu ya chama hicho kwa muda mrefu kuliko Nchimbi miongoni mwa waliomo sasa, ukimwondoa Rais Jakaya Kikwete.


Anasema Mbunge huyo: “ Tunajaribu kumshawishi Lowassa akubali kuwa akikosa yeye, basi apatikane mtu ambaye ataweza kuyafanya yale aliyopanga kuyafanya kupitia CCM. Kwa sasa, hili hajakubaliana nalo,” kilisema chanzo hicho cha gazeti hili ambacho hakikutaka kuwekwa jina lake wazi.

Hata hivyo, kwa vile Ukawa si chama cha siasa, kama Lowassa ataamua kuhama CCM, ni lazima ajiunge na mojawapo ya vyama vinavyounda Ukawa ambavyo ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), NCCR-Mageuzi, Chama cha Wananchi (CUF) na National League (NLD).

Akizungumzia taarifa hizo, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, alisema kwa sasa hawataki kujihusisha na mambo ya ndani ya CCM na badala yake wanaangalia namna ya kukishinda kwenye Uchaguzi Mkuu ujao.

“Sisi sasa hivi lengo letu kubwa ni kuijenga Ukawa kitaasisi na kuifanya iwe tishio katika Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika baadaye mwaka huu.

“Kamanda, sitaki kuzungumza kama tutampokea au hatutampokea Lowassa kama akiamua kuhamia Ukawa. Mambo ya CCM waachie CCM wenyewe. Mimi nakuhakikishia kuwa wakati wa uchaguzi ukifika; CCM wamweke Lowassa, au Membe, sijui Makongoro Nyerere ama yeyote mwingine, Ukawa itashinda tu kwenye uchaguzi huo,” alisema Mbowe kwa kujiamini.

Juhudi za kuwapata wenyeviti wenza wengine wa Ukawa, Profesa Ibrahim Lipumba, James Mbatia na Emmanuel Makaidi hazikufanikiwa hadi tunakwenda mitamboni juzi Jumatatu.

Kwa sasa, Lowassa na wanasiasa wengine watano ndani ya CCM wako katika kifungo cha muda usiojulikana walichowekewa na chama chao kutokana na madai ya kukiuka taratibu za chama hicho.

Wanasiasa wengine walio katika kifungo hicho ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba; Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira; Waziri wa Mambo ya Nje, Benard Membe; Ngeleja na waziri mkuu mstaafu, Frederick Sumaye.

Ilivyokuwa chaguzi mbili zilizopita
Taarifa hizi za uwezekano wa Lowassa kuhamia Ukawa hazitofautiani na zile zilizoibuka mwaka 2005 wakati ilipodaiwa kuwa Kikwete angehamia Chadema endapo CCM isingempitisha.

Wakati huo, zilikuwapo taarifa kuwa CCM ilikuwa na mpango wa kumwondoa Kikwete kwenye kinyang’anyiro hicho kutokana na kutokidhi vigezo vya kimaadili vya chama hicho.
Hata hivyo, Kikwete hatimaye alipitishwa na chama chake kuwania urais na kushinda kwa kishindo.

Katika Uchaguzi Mkuu uliopita wa mwaka 2010, baadhi ya wanachama wa CCM walitajwa kutaka kujiunga na Chama cha Jamii (CCJ) na mmoja wao, Fred Mpendazoe, aliachia ubunge wake kabla ya wakati ili kuanza kazi ya kukijenga chama hicho.

Wakati huo, CCJ ilidaiwa kuwa na mkono wa wana CCM waliokuwa wakipinga kukithiri kwa ufisadi ndani ya chama hicho.

Miongoni mwa majina mazito yaliyokuwa yakihusishwa na kujiunga na CCM yalikuwa ni Samuel Sitta na Dk. Harrison Mwakyembe.

CHANZO: Raia Mwema

WAKATI HUOHUO,

BALOZI wa kudumu wa Umoja wa Afrika (AU), huko Marekani, Mtanzania Amina Salum Ali, ametangaza  kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, 2015.

[aminaali.jpg]
Balozi Amina ametangaza uamuzi wake huo mapema leo  jijini Dar es Salaam.

Itakumbukwa ya kuwa Balozi Amina ambaye alidumu kwa muda mrefu kama waziri kwenye serikali ya Rais mstaafu wa Zanzibar, Dkt. Salmin Amour Juma, almaarufu kama (Komandoo), aliwahi kutupa karata yake kuwania urais wa Zanzibar, kabla ya kujitoa.

Huyu anakuwa mwana mama wa kwanza kwenye historia ya chama cha Mapinduzi CCM, kutangaza kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.Hali kadhalika, Balozi Amina rekodi yake ya kwanza ni kuwa mwanamke wa kwanza kuwa balozi wa kudumu wa AU huko Marekani.

Mbali na kuwahi kuwa waziri, Balozi aAmina ndiyo muasisi wa taasisi ya Zanzibar Women Welfare Trust, inayojishughulisha na kupambana na afya ya akina mama na watoto hususan kwenye eneo la maambukizi ya VVU.



ANGALIZO: Makala hii ilipaswa kuchapishwa gazetini wiki iliyopita lakini nilichelewa kutimuma gazetini.Pia, kwa kiasi kikubwa, kichwa cha habari cha makala hii gazetini kinatofautiana na kilichomo ndani ya makala (na ndio maana kipo tofauti na hapa bloguni.Samahani kwa hilo)
HIVI karibuni, Uingereza ilifanya uchaguzi wake mkuu ambapo chama kilichokuwa madarakani kwa kushirikiana na chama kingine cha Liberal Democrats cha Conservatives kilipata ushindi wa kishindo.
Moja ya mambo yanayoweza kukumbukwa kwa muda mrefu kuhusu uchaguzi huo ni jinsi matokeo ya mwisho yalivyokuwa tofauti kabisa na ubashiri wa kura mbalimbali za maoni. Kimsingi, matokeo hayo ambayo hayakutarajiwa kabisa yamepelekea baadhi ya wachambuzi wa siasa kuhoji ufanisi wa kura za maoni katika kubashiri matokeo ya chaguzi.
Na katika hatua nyingine, kunatarajiwa kuundwa tume huru ya uchunguzi kudadisi kwanini kura za maoni zilibashiri matokeo tofauti sana na matokeo halisi (na hii inaonyesha jinsi ‘wenzetu’ walivyo makini hata katika tatizo dogo tu).
Hadi siku ya uchaguzi, kura mbalimbali za maoni zilikuwa zikibashiri kuwa vyama vya Conservatives na Labour vingepata matokeo yanayokaribina na kufungamana, na hivyo kupelekea kitu kinachofahamika kama ‘hung parliament.’
Pengine ni vema nitumie fursa hii kuelezea kidogo kuhusu uchaguzi mkuu hapa jinsi ulivyo.Hapa hatuna rais, na japo mkuu wa nchi ni Malkia, mtendaji mkuu wa serikali ni Waziri Mkuu.
Malkia, kama zilivyo tawala za kifalme hapigiwi kura. Na uongozi wake wa nchi ni wa kiheshima (ceremonial) kuliko kiutawala.
Katika uchaguzi mkuu kama huo uliofanyika majuzi, wapiga kura wanachagua wabunge wa vyama mbalimbali na idadi ya viti itakavyopata chama katika uchaguzi ndivyo vitaamua nafasi yake katika kuunda serikali.
Namba ya ushindi inayohitajika ili chama kiunde serikali ni viti 326 kati ya viti vyote 650. Iwapo vyama vyote havitofikia idadi hiyo, basi hali inakuwa kama ilivyotokea katika uchaguzi mkuu uliopita, ambapo Conservatives walipata viti 307, Labour viti 258 na Liberal Democrats viti 57. Matokeo hayo ndiyo yanayojulikana kama ‘hung parliament.’
Kutokana na hali hiyo, chama cha Conservatives kiliamua kufanya ushirikiano na chama cha Liberal Democrats na kuunda serikali ya ushirikiano, kwa kimombo coalition government. Kwahiyo katika miaka mitano iliyopita, serikali ya hapa ilikuwa inaongozwa na ushirikiano wa vyama hivyo, ambapo Waziri Mkuu alikuwa David Cameron kutoka Conservatives na Naibu wake Nick Clegg wa Liberal Democrats.
Turejee kwenye kura za maoni. Hadi siku ya uchaguzi, kura nyingi za maoni zilibashiri kuwa Conservatives na Labour wangefungana kwa asilimia takriban 34 (kwa mujibu wa kampuni ya kura za maoni inayoheshimika sana hapa ya YouGov).
Kutokana na hali hiyo, na kwa vile ilitarajiwa kuwa Liberal Democrats wangepata matokeo mabaya (kulikuwa na hofu kuwa kiongozi wa chama hicho, Clegg, angepoteza jimbo lake), chama tawala cha hapa Uskochi, Scottish Nationalist Party (SNP) kilionekana kama ndicho kingeamua hatma ya nani kati ya Conservatives na Labour aunde serikali.Kura za maoni zilikuwa zikibashiri kuwa SNP ingepata majimbo 58 kati ya yote 59 ya hapa Uskochi.
Dalili za kwanza kwamba kura za maoni ‘zilipotea njia’ zilijitokeza sekunde chache tu baada ya vituo vyote vya kupigia kura kufungwa (saa nne usiku). Kwa kawaida ya hapa (na katika nchi nyingine zenye mfumo wa uchaguzi kama huu wa hapa), mara baada ya vituo vya kupigia kura kufungwa, kunatangazwa kitu kinachojulikana kama exit poll.
Hii ni kura ya maoni inayofanywa kwa kuuliza sampuli ya wapigakura (katika uchaguzi huo wa majuzi, sampuli ilikuwa ya watu 22,000) wamekipigia kura chama gani au mgombea gani.
Matokeo ya sampuli hiyo hutumika kubashiri matokeo ya uchaguzi mzima kwa ujumla.
Sasa, exit poll iliyotangazwa na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) ilibashiri kuwa Conservatives ingepata viti 316, Labour 239, Liberal Democrats 10, SNP 58 pamoja na ubashiri wa matokeo ya vyama vinginevyo.

Hiyo ilikuwa tofauti kabisa na ubashiri wa kura za maoni kadhaa kabla na siku ya uchaguzi zilizoonyesha Conservatives wangepata takriban viti 280, Labour takriban 270, 18 kwa Liberal Democrats na 55 kwa SNP.
Je, kwanini kura zile za ubashiri zilibashiri tofauti sana na exit polls na hatimaye matokeo ya jumla? Ni vigumu kupata jibu rahisi lakini inaelezwa kuwa huenda moja ya sababu ni watoa maoni wengi katika kura za maoni kusema tofauti na walivyotenda, yaani majibu ya wengi yalikuwa tofauti na jinsi walivyopiga kura. Hata hivyo, sababu halisi zinatarajiwa kufahamika baada ya tume huru iliyoundwa kuchunguza kasoro hiyo kumaliza kazi yake.
Matokeo ya mwisho yalikuwa kama ifuatavyo: Conservatives viti 331, Labour viti 232, SNP viti 56, Liberal Democrats viti 8 na vyama vinginevyo viti 23. Kwa matokeo hayo, Conservatives walifanikiwa sio tu kupata idadi ya viti 326 vinavyohitajika kuunda serikali pepe yake, bali pia ilipata viti vitano Zaidi. Kwahiyo, David Cameron amerejea madarakani na chama chake cha Conservatives kinaunda serikali pasi kuhitaji ushirikianoi na chama kingine ukilinganisha na ilivyokuwa katika uchaguzi mkuu uliopita.
Tukiweka kando ‘ubashiri fyongo’ wa kura za maoni, moja ya matukio ya kihistoria katika uchaguzi huo ni mafanikio makubwa ya SNP, chama ambacho katika uchaguzi mkuu uliopita kiliambulia viti 6 tu lakini safari hii kimesomba viti 56, ikiwa ni viti vitatu tu pungufu ya kuomba viti vyote 59 vya Uskochi. Mafanikio ya SNP yamekuwa habari mbaya mno kwa Scottish Labour na Scottish Liberal Democrats ambavyo pamoja na Scottish Conservatives wameambulia viti vimoja vimoja. Kibaya zaidi, hata kiongozi wa Scottish Labour Jim Murphy alibwagwa katika uchaguzi huo, na hatma yake kisiasa ipo mashakani.
Baada ya uchaguzi huo kumalizika, kiongozi wa Labour Ed Miliband alitangaza kujiuzulu, sambamba na Nick Clegg wa Liberal Democrats.Awali, kiongozi wa chama cha kibaguzi cha UKIP, Nigel Farage, aliapa kuwa akishindwa katika jimbo alilokuwa anagombea angejiuzulu.
Alishindwa, lakini chama hicho kimemwomba aendelee kuwa kiongozi wake. Tofauti na matarajio ya awali, na ‘mvuto’ wake katika sera dhidi ya wahamiaji na uwepo wa Uingereza katika umoja wa Ulaya, chama hicho kiliambulia jimbo moja tu.

Wengi wa wachambuzi wa siasa za hapa wanatarajia kuwa miaka mitano ya Cameron na Conservatives kuwa sio rahisi. Changamoto kubwa zaidi ni kuzuia Uskochi kudai kura nyingine ya maoni kuhusu uhuru wake, na kwa upande mwingine ni sokomoko la Uingereza kujitoa katika Jumuiya ya Ulaya.
Kwa hilo la ‘uhuru wa Uskochi,’ wachambuzi wengi wanatafsiri ushindi mkubwa wa SNP kama ‘idhini isiyo rasmi’ kwa chama hicho kudai tena kura ya maoni (referendum) ya uhuru, baada ya iliyofanyika mwaka jana kushindwa kuamua Uskochi iendelee kubaki katika ‘muungano wa Uingereza’ kwa tofauti ya kura chache tu.
Licha ya ukweli kuwa matokeo hayo ya ‘kura ya maoni ya uhuru wa Uskochi’ imepeleka umaarufu mkubwa kwa SNP, huku ikivuna idadi kubwa kabisa ya wanachama wapya, kauli za Cameron wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa majuzi dhidi ya chama hicho tawala Uskochi, zinaelezwa kutafsiriwa na wengi wa wapigakura wa hapa (Uskochi) kama ‘chuki dhidi ya taifa lao,’ na hivyo kuamua kukisapoti ‘chama chao’ (SNP) kwa wingi. Sapoti hiyo inaweza kuwa na umuhimu mkubwa iwapo SNP itaamua kudai kura nyingine ya maoni ya ‘uhuru wa Uskochi.’
Kwa upande wa hatma ya Uingereza katika Jumuiya ya Ulaya, Cameron ameshaahidi kutekeleza azma yake ya kuitisha kura ya maoni iwapo nchi hii iendelee na uanachama wake au ijitoke, kabla ya mwisho wa mwaka keshokutwa. Huu utakuwa mtihani mkubwa sana kwa Cameron na Conservatives kwa ujumla.
Wakati wahafidhina ndani ya chama hicho wakipigania kwa udi na uvumba Uingereza ijitoke, kuna idadi kubwa tu ya Waingereza wanaodhani wazo hilo ni baya na hatari kwani linaweza kuiathiri nchi yao kiuchumi na kisiasa za kimataifa.
Je kuna lolote Watanzania twaweza kujifunza kutoka katika uchaguzi huo mkuu wa Uingereza? Yapo mengi, lakini machache ni pamoja na mfumo imara kabisa, tofauti na wetu unaoonekana kutegemea kudra za Mwenyezi Mungu (Tume yetu ya Uchaguzi inataka wananchi wasisikie maneno ya pembeni, lakini mazingira yaliyopo yanapelekea hofu iwapo uchaguzi mkuu utafanyika kweli hapo Oktoba).
Kingine ni nafasi ya sera za vyama katika kushawishi wapiga kura. Moja ya sababu zinazotajwa kupelekea Labour kufanya vibaya ni sera zake zilizoonekana kuwatenga wafanyabiashara wadogowadogo na kutowapa kipaumbele watu wa tabaka la kati. Kwa uapnde mwingine, inaelezwa kuwa ushindi wa Conservatives ulichangiwa zaidi na mvuto wa sera zake za kiuchumi kwa wapigakura.
Kadhalika, jingine ambalo vyama vyetu vya siasa huko nyumbani vyaweza kujifunza ni uchaguzi wa mgembea anayekubalika.Kwa kiasi kikubwa, kampeni za Labour ziligubikwa na hofu ya uwezo binafsi wa Ed Miliband kumudu Uwaziri Mkuu.
Nimalizie makala hii kwa kuwapongeza Waingereza kwa kuendesha Uchaguzi Mkuu kwa ufanisi mkubwa, kuanzia mwenendo wa kampeni ambapo kwa asilimia kubwa ulihusu sera badala ya ‘madongo,’ idadi kubwa ya wapigakura iliyojitokeza (asilimia 66.10) na uungwana wa walioshindwa matokeo kuyakubali matokeo, sambamba na Miliband na Clegg kujiuzulu kutokana na vyama vyao kufanya vibaya.
Wakati nina matumaini hafifu kuona kura ya maoni ikifanyika kabla ya uchaguzi mkuu wetu hapo Oktoba, ninajipa moyo kuwa serikali na Tume ya Taifa ya Uchaguzi wataongeza bidii ili kuhakikisha kuwa uchaguzi mkuu unafanyika kama ilivyopangwa.
Kutokana na kuporomoka kwa thamani ya shilingi yetu, na hali yetu mbaya kiuchumi, ni muhimu kwa watawala wetu kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, tujibane na kidogo tulicho nacho (tukitarajia wafadhili watatumbukiza fedha zao katika ‘bakuli’ letu) ili tuwezeshe uchaguzi huo kufanyika kwa ufanisi na amani.

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.