30 Jul 2015

Kama unavyoona hapo pichani juu, mara baada ya kusikia taarifa kwamba Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa anatarajia kujiunga na vyama vinavyounda Muunganowa Katiba ya Wananchi (UKAWA), niliandika tweet hiyo pichani. Kimsingi, binafsi nilishindwa kabisa kuamini kuwa Dkt Willibrord Slaa, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema hadi alipotangaza kujiuzulu, angeweza kukaa chama kimoja na Lowassa. Nilishindwa kabisa kupata picha kichwani kumwona Dkt Slaa akiwa jukwaani anamnadi Lowassa. Nilijaribu ku-imagine kwamba labda kwa vile kuingia kwa Lowassa Chadema kunaweza kukiingiza chama hicho na Ukawa Ikulu, na hivy pengine Dkt Slaa angeweza kumsapoti japo kwa shingo upande, lakini nafsini niliona huo sio tu ungekuwa muujiza - na mie si muumini wa miujiza - bali pia ungekuwa usaliti wa hali ya juu.


Siwezi kujisifu kuwa tweet hiyo ya 'kumsuta' Dkt Slaa imesaidia kumfanya achukue uamuzi huo wa kujiuzulu lakini ninachoweza kusema ni kuwa ninamshukuru kwa kufanya maamuzi magumu ya kujiuzulu hasa ikizingatiwa kuwa neno 'KUJIUZULU' halipo katika kamusi ya wengi wa wanasiasa wetu hata pale wakiwa wanaandamwa na kashfa. Lakini pia ninampongeza Dokta Slaa kwa kusimamia anachooamini.

Kwa hakika Dokta Slaa alisimama kidete kupigana kwa nguvu zake zote dhidi ya ufisadi. Na sifa kubwa ya mwanasiasa huyo ilikuwa umakini wake katika kuwasilisha hoja. Hakuwa mtu wa jazba wala mjivuni. Na kwa hakika alikuwa mwenye kuapanga hoja zake na kuziwasilisha kwa umakini mkubwa. Kwa kifupi, Dokta Slaa aliweza kuwasiliana na umma, iwe katika hotuba au maongezi kama DOKTA hasa, maana moja ya sifa ya usomi ni jinsi ya kuwasiliana na jamii kwa ufasaha.

Kuna watakaokuwa wamefurahi kuona Dokta Slaa amechukua hatua ya kujiuzulu, sio furaha ya kuungana naye kwa kuchukua uamuzi huo mgumu bali kwa vile aidha walikerwa na msimamo wake mkali dhidi ya mafisadi na ufisadi, au walimwona kama mmoja ya sababu zilizopokea Zitto Kabwe kung'olewa Chadema. Furaha hiyo ni ya 'kimburula' kwa sababu Dokta Slaa alikuwa mmoja wa wanasiasa wachache kabisa waliosimama kwa dhati na wanyonge kupigania haki zao. Ukimwondoa marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, sioni mwanasiasa mwingine yeyeote yule aliyewajali mno Watanzania kama Dokta Slaa. Na japo nina furaha kutokana na kukataa kushirikiana na Lowassa, na ninampongeza kwa kuwa na msimamo thabiti, kwa upande mwingine nina masikitiko makubwa kuona lulu hiyo ya taifa ikiachana na siasa wakati bado twaihitaji mno.
Dokta Slaa alifanya kazi yake kwa uadilifu mkubwa na kwa hakika kuna idadi kubwa tu ya Watanzania iliyoamini kuwa siku moja angeweza sio tu kuwa Rais wetu bali pia angeweza kuibadili Tanzania yetu. Na kwa kujiuzulu, amethibitisha ni mwasiasa wa aina gani. Badala ya kutanguliza maslahi binafsi na kujiunga na chama kingine cha siasa au kuanzisha chama chake, Dokta Slaa amechukua uamuzi wa kiungwana. Ametambua kuwa tatizo sio CCM pekee bali mfumo mzima wa siasa za Tanzania yetu, kuanzia chama tawala hadi huko Upinzani. Uamuzi wa kujiuzulu utamlindia hadhi yake milele. 

Mimi ni muumini mkubwa wa 48 Laws of Power, na ninaomba nitanabaishe jinsi uamuzi huo wa Dokta Slaa unavyoendana na baadhi ya Laws hizo. Law 34 of Power inasema (ninainukuu)

The way you carry yourself will often determine how you are treated: In the long run, appearing vulgar or common will make people disrespect you. For a king respects himself and inspires the same sentiment in others. By acting regally and confident of your powers, you make yourself seem destined to wear a crown.
Kwa tafsiri ya Kiswahili ni kwamba "Matendo yako ndio yatakavyofanya watu wakuchukuliaje. Katika muda mrefu, kuonekana mtu wa ovyo ovyo kutafanya watu wasikuheshimu. Kwa sababu mfalme hujiheshimu mwenyewe na kuhamasisha watu wengine kujiheshimu na kumheshimu. Kwa matendo makubwa na ya uhakika wa nguvu zako, utaonekana mtu stahili kushika hatamu." 
Na kwa hakika uamuzi wa Dokta Slaa kujiuzulu unamfanya aendelee kuwa sio tu mtu mwenye msimamo bali pia ataendelea kushikilia hadhi na heshima yake kama mtu aliyeuchukia ufisadi kwa dhati hadi kuamua kujiuzulu baada ya fisadi Lowassa kujiunga na UKAWA.
Kuna wanaoweza kumbeza kwa kusema amekimbia vita. Well, Law 36 of Power inatuasa, nanukuu,

...It is sometimes best to leave things alone. If there is something you want but cannot have, show contempt for it...
Kwa tafsiri ya Kiswahili, "Wakati mwingine ni vema kuacha vitu kama vilivyo Kama kuna kitu unakitaka lakini huwezi kukipata, kichukie tu." Na hicho ndicho alichokifanya Dokta Slaa. Alichukia ufisadi na kuwachukia mafisadi kwa dhati. Lakini ghafla akajikuta analetewa fisadi ashirikiane nae kupinga ufisadi. Waingereza wana msemo "You can't put a drug addict in charge of a pharmacy," yaani huwezi kulikabidhi teja liwe msimamizi wa duka la madawa (ambayo kwa kawaida yana madawa baadhi ya madawa kama Heroin ambayo ndio 'chakula' cha mateja). Kwa vyovyote vile, ingekuwa vigumu mno kwa Dokta Slaa kutimiza azma yake ya kupambana na ufisadi akiwa pamoja na Lowassa. Na ndio maana akaamua bora akae kando. Kama ninavyotamka mara kadhaa, huhitaji kuwa kiongozi ili ulete mabadiliko, kuwa raia mwema tu (You don't have to be a leader to bring change. Just be a good citizen).

Law 47 of Power inasema, ninanukuu,

The moment of victory is often the moment of greatest peril. In the heat of victory, arrogance and overconfidence can push you past the goal you had aimed for, and by going too far, you make more enemies than you defeat. Do not allow success to go to your head. There is no substitute for strategy and careful planning. Set a goal, and when you reach it, stop.

Kwa Kiswahili inamaanisha, "Ushindi unapowadia ndio wakati ambao unaweza kuangamia. Katikati ya ushindi, dharau na kujiamini kupita kiasi vyaweza kukusukuma zaidi ya lengo kusudiwa, na kwa kupitiliza lengo hilo, watengeneza maadui zaidi ya uliowashinda. Kamwe usiruhusu mafanikio kupanda kichwani mwako. Hakuna mbadala wa mkakati na mipango makini. Weka lengo, na ukilitimiza, simama."
Hakuna asiyefahamu alichotimiza Dokta Slaa katika mapambano yake dhidi ya ufisadi. Kubwa lilikuwa kuwaamsha Watanzania, na kwa hakika wengi wamefunguka macho dhidi ya ufisadi na wanauchukia kwa dhati. Angeweza kujikaza kisabuni na kusimama pamoja na Lowassa ili aendeleze mapambano dhidi ya ufisadi, lakini sote twafahamu ingekuwa vigumu mno. Na uamuzi wake wa kujiondoa madarakani ni sawa na inavyosema sheria hiyo hapo juu, 'ukitimiza leno, simama.'
Vilevile, Dokta Slaa amefuata vizuri Law 5 of Power inayoonya kuwa "So much dependes on reputation, guard it with your life," yaani "Hadhi ni kitu muhimu sana, ilinde kwa nguvu zote." Sasa, sote tulikuwa tukiitambua Chadema kama kiongozi wa vita dhidi ya ufisadi, lakini ghafla wametusaliti na kumkaribisha papa wa ufisadi katika chama chao. Kwa vile ni mtu makini na msafi, Dokta Slaa ameona kuwa kwa kufanya hivyo, Chadema imejishushia hadhi yake katika uongozi wa mapambano dhidi ya ufisadi, na akaamua kuilinda hadhi yake kwa kujitenga nao. 
Nimalizie makala hii kwa kurudia kumshukuru Dokta Slaa kwa yote aliyoitendea Tanzania yetu. Tunaouchukia ufisadi tutaendelea kumwenzi na kumkumbuka milele. Nitajitahidi huko mbeleni kufanya mawasiliano na Dokta Slaa ili ikiwezekana niweke kumbukumbu ya huduma yake bora kabisa kwa Watanzania kwa kuandika kitabu kinachomhusu. Nitawa-update kuhusu hilo.
MUNGU AKUBARIKI SANA DOKTA SLAA. TANZANIA ISIYO NA UFISADI INAWEZEKANA PASIPO HAJA YA KUWATEGEMEA MAFISADI. 



29 Jul 2015

KWANZA ninaomba radhi kwa safu hii kuadimika kwa takriban wiki mbili mfululizo. Hali hiyo ilitokana na sababu zilizo nje ya uwezo wangu.

Pili, ninaomba kutoa angalizo kuwa makala hii, niliiandaa mara baada ya vikao vikuu vya Chama Cha Mapinduzi (CCM) huko Dodoma ambapo hatimaye chama hicho kilipata mgombea wake katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba, mwaka huu. Nimeihariri ili kufidia yaliyojiri kati ya wakati huo na hivi sasa.

Baada ya kugusia hayo, ninaomba kufanya uchambuzi endelevu kuhusu mchakato wa CCM kumpata mgombea wake wa kiti cha urais, wiki mbili zilizopita.

Nitaonekana mwenye chuki binafsi kwa CCM kama sitakipongeza chama hicho tawala kwa kumudu kufikia hatua ya kupata mgombea wake ‘kwa amani.’ Pamoja na kiu kubwa ya Watanzania kufahamu kada gani wa CCM angeibuka kidedea, kwa kiasi kikubwa mchakato wa kupata mgombea wa chama hicho ulikuwa kama ‘referendum’ kwa Rais Jakaya Kikwete, ambaye pia ni mwenyekiti wa taifa wa chama hicho tawala, kuhusu kada maarufu, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa. Swali kubwa lilikuwa, “Je Rais Kikwete ataweza ‘kumtosa’ rafiki yake?” Wengine walilielekeza swali hilo kwa Lowassa na kuwa, “Atakatwa au hakatwi?” hasa kwa kuzingatia kile kilichoonekana kama kada huyo kuungwa mkono na wanaCCM wengi.

Lakini hatimaye, maswali hayo yalipata majibu baada ya Lowassa kutokuwamo katika ‘tano bora.’ Licha ya makada Emmanuel Nchimbi, Sophia Simba na Adam Kimbisa kutangaza kutoafikiana na mchakato wa kuchuja ‘wagombea,’ zilipatikana taarifa kuwa kungekuwa na jaribio la kumng’oa Rais Kikwete katika uenyekiti wake na kuivunja Kamati Kuu ya chama hicho, masuala yaliyoishia kuwa porojo tu.

Hatimaye, chama hicho kilimtangaza Dk. John Magufuli kuwa mgombea wake, ambaye naye alimteua Samia Suluhu Hassan kuwa mgombea mwenza wake, akiandika historia ya kuwa mwanamke wa kwanza kuwa mgombea mwenza, na iwapo Magufuli akishinda, atakuwa Makamu wa Rais wa kwanza mwanamke nchini Tanzania.

Huko nyuma nilifanya ‘ubashiri’ kuhusu makada gani niliodhani walikuwa na nafasi kubwa ya kupita ‘mchujo wa kwanza.’ Wakati si vigumu kuelewa kwa nini Lowassa alikatwa, bado sijaelewa kwa nini kada aliyetarajiwa na wengi kuwa angepitishwa, Jaji Agustino Ramadhani, hakumudu kuingia japo kwenye ‘tano bora.’ Binafsi ninamsikitikia kada huyo kwani kwa namna fulani, ‘kufeli’ kwake kunatia doa wasifu wake ‘wa kupigiwa mstari.’

Pia ‘kufeli’ kwa kada aliyekuwa akitajwa sana, Makongoro Nyerere, kuliwashtua baadhi ya watu lakini yayumkinika kuhisi kuwa msimamo wake mkali wa kutaka kuirekebisha CCM, na kauli yake ya ‘turudishieni CCM yetu’ ilimtengenezea maadui hususan wanaonufaika na ‘sera za ulaji na kulindana’ ndani ya chama hicho.

Nilibashiri kuwa January Makamba angefanya vizuri, na kwa hakika alifanikiwa kuingia kwenye ‘tano bora,’ hatua ambayo yaweza kumtengenezea mazingira mazuri ya kisiasa iwapo ataendelea kuwa na dhamira ya kuiongoza Tanzania huko mbeleni.

Pia nilibashiri mmoja au wawili wa makada wa kike kufanya vizuri katika ‘mchujo wa kwanza,’ na ilikuwa hivyo. Sambamba na hilo, nilibashiri uwezekano wa kuwa na aidha mgombea urais mwanamke au mgombea mwenza/makamu wa rais mwanamke, na hilo limetokea japo nilitarajia angekuwa mmoja wa makada wa kike waliojitokeza kuwania nafasi ya urais.
Kwa upande mwingine, mwathirika mkubwa kabisa wa mchakato huo ni mwanasiasa mkongwe, Kingunge Ngombale Mwiru, ambaye pasipo busara aliamua kujidhihirisha kuwa anamuunga mkono Lowassa. Sidhani kama mzee huyo mwenye uzoefu mkubwa wa kisiasa ana washauri wazuri kwani alipaswa kutambua kuwa laiti ‘mgombea wake’ Lowassa akishindwa basi ‘legacy’ yake nayo itayeyuka. Kwa bahati mbaya kwake, Kingunge atakumbukwa zaidi si kama ‘swahiba wa Baba wa Taifa’ bali ‘mkongwe wa kisiasa aliyeangukia pua kwa kumuunga mkono kada aliyetoswa kwenye kinyang’anyiro cha kusaka urais.’ Waelewa wa mambo wanatahadharisha kuwa kujenga hadhi (reputation) ni kitu kinachochukua muda mrefu na kazi kubwa, lakini kosa dogo tu, linaiondoa hadhi hiyo mara moja. Ni rahisi kubomoa kuliko kujenga.

Kwa upande mmoja kuna hisia kwamba Lowassa anaweza asikubali kupoteza mtaji wake wa kisiasa (political capital) katika kilichoonekana kama kuwa na uungwaji mkono mkubwa ndani na nje ya chama chake, kwa kujiunga Ukawa. Akiwa Ukawa na akagombea urais kuhusu swali kwamba atashinda au la, si rahisi kubashiri kwa sasa.

Lakini kwa upande mwingine, jaribio la kuhama CCM linaweza kumgharimu mno mwanasiasa huyo mzoefu. Moja ya athari za wazi ni uwezekano wa kupoteza stahili kadhaa anazopata kama Waziri Mkuu wa zamani. Kadhalika, akihama CCM, chama hicho tawala kinaweza kutumia kila mbinu ‘kummaliza’ kabisa kisiasa. Kama ana washauri wazuri basi pengine ni vema angekubali tu matokeo na ‘kula pensheni yake’ kama Waziri Mkuu wa zamani, bila kuondoka CCM.

Jingine lililojitokeza katika mchakato huo ni ‘kutoswa’ kwa wasaidizi wakuu wawili wa Rais Kikwete, yaani Makamu wa Rais Dk. Gharib Bilali na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda. Tafsiri ya haraka ni kuwa katika miaka 10 ya utawala wa Rais Kikwete, tulikuwa na viongozi wakuu wawili wa kitaifa ambao pengine hawakustahili kuwa katika nyadhifa hizo na ndio maana wameshindwa kufaulu katika japo mchujo wa awali. Badala ya kukumbukwa kama Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wa zamani, Dk Gharib na Pinda watakumbukwa zaidi kama wasaidizi wakuu wa Rais ambao walifeli ‘mtihani wa kurithi nafasi ya bosi wao.’

Sasa twende kwa Dk. Magufuli. Kwanza, ni kweli kuwa amekuwa akisifika kama mchapakazi. Lakini pengine hili ni matokeo ya kasumba iliyojengeka miongoni mwa Watanzania kwamba kiongozi akitekeleza wajibu wake ambao analipwa mshahara kutekeleza wajibu huo, anaonekana kama ‘malaika.’

Taifa letu limekuwa na uhaba mkubwa wa wazalendo kiasi kwamba kiongozi akitekeleza wajibu au kukemea rushwa anaonekana kama ametoka sayari nyingine. Binafsi, ninamwona Magufuli kama kiongozi wa ‘kawaida’ tu ambaye mara nyingi alizingatia matakwa na matarajio ya mwajiri wake. Kama tunawaona madaktari wakijitahidi kuokoa maisha ya wagonjwa kila kukicha huko hospitalini, au walimu wanaofika mashuleni kufundisha (wengi wao katika amzingira magumu), iweje tumwone Magufuli tofauti kwa vile tu anatekeleza mengi ya majukumu anayotakiwa kuyatekeleza?

Moja ya ‘madoa’ kuhusu uongozi wa Magufuli ni suala la uuzwaji wa nyumba za serikali, suala ambalo halijapatiwa majibu ya kuridhisha. Jingine ni ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali aliyopendekeza hatua stahiki zichukuliwe dhidi yake kama Waziri wa Ujenzi na Dk. Harrison Mwakyembe (aliyekuwa Naibu Waziri) kutokana na ufisadi unaofikia shilingi bilioni 256. Kama ilivyo kwenye uuzwaji wa nyumba za serikali, suala hili nalo pia halijatolewa maelezo ya kuridhisha.

Lakini pengine ni usahaulifu wa Watanzania wengi, au ni kile Waingereza wanaita ‘settling for less’ (kuridhika na kilicho pungufu), ile picha inayomwonyesha Magufuli akipata ‘tiba ya Babu wa Loliondo’ haionyeshi kuwasumbua wananchi wengi wanaoonekana kuwa na matumaini makubwa kwa kada huyo. Binafsi, pamoja na kuheshimu uamuzi wa Magufuli kutegemea ‘tiba hiyo ya porojo,’ nilitarajia msomi kama yeye, tena mwenye taaluma ya Kemia angejihangaisha kutafiti kidogo tu kuhusu ufanisi wa ‘tiba’ hiyo ya kitapeli. Je hili ninalolitafsiri kama ufyongo wa kimaamuzi halitojitokeza katika urais wake iwapo atashinda hapo Oktoba?

Kubwa zaidi ni uwezekano wa Magufuli kuwa ‘Kikwete mpya.’ Sio siri kuwa Rais Kikwete amekuwa ‘shabiki’ mkubwa wa utendaji kazi wa Magufuli. Hilo si kosa. Lakini pengine ‘ushabiki’ huo umechangia pia katika mafanikio ya kisiasa ya kada huyo, na haihitaji uelewa mkubwa wa siasa kubashiri kuwa huenda Magufuli akawa na ‘deni’ kwa Kikwete. Licha ya hofu yangu kuu kuwa tatizo kubwa la ‘urais wa Magufuli’ ni ukweli kuwa ni kada wa CCM ile ile iliyotufikisha hapa tulipo, wasiwasi wangu mwingine ni huo uwezekano wa kuwa na ‘Rais mstaafu by proxy,’ yaani Kikwete kuwa na ‘influence’ kwa ‘rafiki yake’ aliyepo Ikulu.

Kadhalika, ninadhani wengi hatujasahau ukweli kwamba ukosoaji mkubwa dhidi ya kada January Makamba ilikuwa uamuzi wake wa kubainisha visheni ya ‘urais wake’ aliyoiita ‘Tanzania Mpya.’ Ukosoaji huo uliegemea kwenye hoja kwamba mgombea urais kwa tiketi ya CCM atajinadi kwa kutumia ilani ya uchaguzi ya chama hicho. Na japo mgombea ana fursa ya kushiriki kuingiza malengo yake, kwa kiasi kikubwa ilani hiyo huandaliwa na chama chenyewe.

Lakini pengine sasa ndio tunatambua umuhimu wa kuwa na visheni kama ‘Tanzania mpya’ ya kada January kwani hatujui lolote kuhusu visheni ya Magufuli zaidi ya kuambiwa ni kuwa ni mchapakazi. Swali la msingi, je, uchapakazi wake utaendana na matakwa ya CCM katika ilani yake ya uchaguzi? Lakini hata kama chama hicho tawala kitamruhusu Magufuli kuandika ilani yake mwenyewe kwa niaba ya chama hicho, je ukada wake (kama ilivyothibitika katika hotuba yake ya kuombea kura huko Dodoma) hautokuwa kikwazo katika kuirejesha CCM kwenye misingi yake ya awali ya kuwatumikia wanyonge badala ya matajiri ilivyo sasa?

Mara kadhaa nimekuwa nikieleza kuwa moja ya vikwazo vikubwa kwa maendeleo ya nchi yetu ni kutanguliza itikadi ya kisiasa badala ya maslahi ya chama. Kada au mwanae anayefahamika kujihusisha na biashara haramu au ufisadi hachukuliwi hatua kwa vile ‘ni mwenzetu.’ Vyombo vya dola vinashindwa kuchukua hatua kwa kuhofia ‘kuwaudhi vigogo wa kisiasa’ Na CCM imekuwa kimbilio kwa watu wa kada mbalimbali ikiwa ni pamoja na mafisadi kwa vile sio siri kuwa uongozi katika chama hicho ni mithili ya kinga ya uhakika dhidi ya hatua za kisheria

Tanzania yetu sio tu inahitaji Rais ambaye hana deni la fadhila kwa mtu yeyote yule, atakayetumia ipasavyo nguvu anayopewa na Katiba kuiongoza nchi yetu kwa maslahi ya taifa badala ya kuweka mbele maslahi ya chama, na kwa CCM, mwanasiasa anayetambua kuwa chama hicho kimeporwa na wenye fedha –safi na chafu- na kuwatelekeza wanyonge.
Nimalizie makala hii kwa ahadi ya kuendeleza uchambuzi huu katika makala ijayo nikitarajia kuwa muda huo tutakuwa tumeshamfahamu mgombea wa tiketi ya urais kupitia Ukawa. Pia ningependa kuwahimiza Watanzania wenzangu wajitokeze kwa wingi kujiandikisha katika daftari la wapigakura .

JIUNGE NAMI TWITTER https://twitter.com/Chahali AMBAPO NINAJADILI MASUALA MBALIMBALI

28 Jul 2015

Ninaipenda siasa...kama stadi  (study, yaani kuisoma), lakini kwa hakika ninapata shida sana na jinsi mengi ya ninayosoma katika stadi za siasa (political studies) yanavyogeuka inapokuja kwenye matendo au shughuli za kisiasa an zinazohusiana na siasa. 

Stori kidogo. Fani niliyotamani sana kuisoma na pengine kubobea ni utabibu. Nilitamani mno kuwa daktari. Lakini ndoto yangu ya udaktari ilipata kikwazo baada ya kupata matokeo ya mtihani wa kumaliza kidato cha nne. Japo nilipata A kwenye Kemia na C kwenye Baiolojia, niliambulia D kwenye Hisabati na kufeli kabisa Fizikia ambapo nilipata F. Na japo nilipata Division One, uwezekano wa kuchukua 'combination ya udaktari' yaani PCB (Fizikia, Kemia na Baiolojia) kidato cha tano uliathiriwa na hiyo F ya Fizikia. Uwezekano pekee ulibaki kwenye kujaribu combination ya CBG (Fizikia, Kemia na Jiografia) ambayo ingeniwezesha kuikwepa Fizikia.

Nilipojiunga na kidato cha tano katika sekondari ya wavulana ya Tabora (Tabora Boys') nikakumbana na vikwazo vingine. Kwanza, Kemia ya kidato cha kwanza mpaka cha nne ni tofauti kwa kiasi kikubwa na ile ya kidato cha tano na cha sita. Kuna kitu inaitwa Physical Chemistry ambayo kimsingi ni kama mchanganyiko wa Kemia, Hisabati na Fizikia. Sasa kama nilivyotanabaisha hapo awali, udhaifu wangu katika Fizikia na Hisabati ulimaanisha kuwa nisingeweza kuimudu Kemia ya High School.

Pili, shule yetu ilikuwa haina mwalimu ya Jiografia, na ilibidi tuwe tunakwenda shule ya jirani ya Tabora Girls' kuhudhuria vipindi vya somo hilo. Angalau Baiolojia haikuwa tatizo japo kiukweli ilihitaji uwezo mkubwa wa kukariri na kuelewa majina ya sampuli za viumbe ambayo mengi yana asili ya Kilatini au Kigiriki. Kwahiyo kwa kifupi, dhamira yangu ya kusoma combination ya CBG ilikufa kifo cha asili.

Hivyo nikaamua kusoma combination yenye masomo ya Historia, Jiografia na Kiingereza. Hii ilikuwa mteremko kwa kiasi kikubwa, lakini ndoto yangu ya kuwa daktari ndio ikayeyuka. Lakini wanasema kile unachotaka sio lazima ndio unachopata (what you wish for is not always what you get).

Sukuma miaka kadhaa baadaye, nikajiunga na chuo kikuu cha Dar es Salaam na hapo nikajikuta nina uchaguzi wa ama kuzamia kwenye sayansi za siasa na utawala wa umma (pilitical science and public administration au sosholijia, elimu inayohusu masuala yya jamii. Mwaka wa pili, nikafanya uamuzi wa kuchukua hiyo choice ya pili, yaani Sosholojia. Kwa hakika niliipenda sana sosholojia. Yaani ilinisaidia mno kuielewa jamii. Miongoni mwa masomo ya kupendeza sana yalikuwa lile lilifundisha kuhusu uhusiano wa jamii, utamaduni na afya; somo la jinsia na uhusiano wa kijinsia, na zaidi ya yote ni sosholojia ya dini ambapo pamoja na mambo mengine tulifundishwa kuhusu Ukristo, Uislamu na Imani za Asili. 

Sukuma miaka kadhaa zaidi mbele, nikapata skolashipu ya kuja hapa Uingereza kusoma Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (Politics and International Relations), mkazo ukiwa kwenye masuala ya usalama. Kwa vile skolashipu ni kama zawadi, mwanafunzi anakuwa hana uchaguzi. Nilitamani sana kuendelea na Sosholojia lakini sikupewa fursa ya kuchagua. Na hivyo ndivyo nilivyojikuta nikiingia kwenye stadi za siasa. Tuishie hapo/

Kwanini nimeelezea stori hiyo? Ni kwa sababu kama nilivyosema awali, ninaipenda siasa kama stadi. Yaani baada ya kutokuwa na choice ya kusoma sosholojia, na 'kulazimishwa' kusoma Siasa, ikabidi niipende tu. Niliipenda pia kwa sababu siasa za kimataifa zina 'raha' yake kuzielewa, ukichanganya na maeneo kama diplomasia, amani na 'ugomvi' (peace and conflicts) na masuala ya usalama wa kimataifa (international security).

Lakini tatizo la siasa kama stadi ni ukweli mchungu kwamba kile unachosoma darasani mara nyingi hakiakisi hali halisi mtaani. Siasa kama fani au stadi sio mbaya, ina mafunzo mengi, inafundisha miongozo mingi na kanuni nyingit muhimu kwa maisha ya mwandamu, lakini mtaani hali ni tofauti.  Sihitaji kuelezea kwa undani kwanini watu wengi wanaichukia siasa. Lakini mfano mwepesi ni kwenye kampeni za uchaguzi ambapo utasikia chama kikitanabaisha sera nzuri kabisa lakini baada ya kuingia madarakani kikaishia kufanya kinyume kabisa na kilichoyaahidi. Na kwa Tanzania yetu tuna mfano hai wa jinsi sera tamu za CCM zinavyoishia kuwanufaisha matajiri na mafisadi huku zikiwadidimiza walalahoi.

Na mfano mchungu zaidi, uliopelekea niandike makala hii, ni jinsi Chadema katika mwavuli wa UKAWA inavyoelekea kuwasaliti mamilioni ya Watanzania kwa uwezekano wa kumpokea fisadi Edward Lowassa kuwa mgombea wa urais.

Jana niliumia mno nilipoona picha kadhaa zinazomwonyesha Lowassa akiwa na viongozi wa UKAWA. Baadaye, mwenyekiti wa NCCR, moja ya vyama vinavyounda UKAWA pamoja na Chadema, CUF na NLD, alitamka bayana kuwa wanamkaribisha Lowassa kujiunga nao.

Lakini baadaye kidogo nikapata ahueni baada ya kupatikana taarifa zilizothibitishwa na akaunti ya Twitter ya Chadema Media kuwa picha zilizokuwa zinamwonyesha Lowassa na viongozi wa UKAWA ni feki, yaani zilikuwa photoshopped. Hata hivyo furaha hiyo haikudumu muda mrefu baada ya Mbatia na wenzake kutangaza bayana kuwa wanamkaribisha Lowassa . Na kuna uwezekano leo Jumanne, aidha UKAWA wakamtangaza Lowassa kuwa mgombea wao wa Urais au Lowassa mwenyewe akatangaza kujiunga nao.
Huu ni usaliti mkubwa mno hasa upande wa Chadema, chama kilichojidhihirisha kuwa kinauchukia ufisadi kwa dhati. Sote twakumbuka jinsi Chadema ilivyojipatia umaarufu kwa kupambana na ufisadi, hasa baada ya kutangaza hadharani 'orodha ya aibu' (list of shame) pale Mwembeyanga jijini Dar ambapo walitaja orodha ya mafisadi akiwemo Lowassa. Kadhalika Chadema ilifanya jitihada kubwa kuibua ufisadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na skandali ya Richmond iliyopelekea Lowassa kujiuzulu Uwaziri Mkuu. Vilevile chama hicho kilitufumbua macho kuhusu ufisadi wa EPA, Meremeta, Dowans, Buzwagi, TanGold, Kiwira, nk. Kwa kifupi, ilikuwa haiwezekani kuzungumzia mapambano ya  ufisadi Tanzania bila kuitaja Chadema.

Na katika harakati zake za kupambana na ufisadi, kuna Watanzania wenzetu waliopoteza maisha yao na wengine kujeruhiwa vibaya na kuachiwa ulemavu kwa kukiunga mkono chama hicho. 


Na kwa kuonyesha kuwa Chadema ilikuwa mwarobaini kwa CCM na mafisadi kwa ujumla, chama hicho kilifanyiwa kila aina ya hujuma. Mara kiliitwa chama cha kidini, baadaye kikaitwa cha kikabila, na hadi hivi majuzi kiliitwa chama cha kigaidi. Lakini taratibu Watanzania walifumbuka macho na kubaini kuwa sababu kubwa ya CCM na serikali yake kuiandama Chadema ni kwa vile chama hicho cha upinzani kilichofanya vizuri tu katika uchaguzi mkuu uliopita kinasimamia maslahi ya wanyonge ilhali CCM inatetea mafisadi na ufisadi.
Japo mie binafsi sikuwa mwanachama wa Chadema, nilikiunga mkono kutokana na msimamo wake mkali dhidi ya ufisadi kulingana na msimamo wangu kwenye suala hilo. Nilikuwa nina imani kuwa laiti Chadema ikifanikiwa kuingia Ikulu basi kwa hakika safari ya kuipeleka Tanzania yetu mahali inapostahili kuwa inawezekana. 
Sasa hili la kumpokea Lowassa ni pigo kubwa mno na ni usaliti wa hali ya juu kabisa. Ndio, Lowassa anaweza kuwasaidia Chadema na UKAWA kuingia Ikulu. Lakini kwa kuangalia tu maswahiba wa Lowassa utaweza kujua tutakuwa na serikali ya aina gani. Sipati shida kubashiri kuwa tutaishia kuikumbuka CCM. 

Embedded image permalink

Na huo ndio ubaya wa siasa katika vitendo, tofauti na ilivyo nzuri na mwafaka katika stadi. Kwamba kistadi za siasa, Chadema ilijijenga na kupata umaarufu kwa kuzingatia kanuni ilizojiwekea na ikajitambulisha kama chama kilichopo kwa maslahi ya wanyonge, tofauti na CCM iliyokimbia kanuni zake na kuwakumbatia matajiri na mafisadi. Lakini ghafla bin vup, Chadema inaelekea kwenda kulekule ilipo CCM. 

Nimalizie makala hii kwa kuahidi kufanya uchambuzi wa kina kuhusu suala hili katika makala yangu ya wiki ijayo katika gazeti la Raia Mwema. Spoiler alert, wiki hii katika toleo litakalokuwa mtaani kesho ninamjadili Magufuli. 

Asanteni kwa kuchukua muda wenu kunisoma.

21 Jul 2015




Juzi nilipatiwa uthibitisho wa kitu nilichokwishaambiwa awali: Idara yetu ya Usalama wa Taifa iliandaa operesheni dhidi ya mtu aliyepaswa kuja Tanzania kumzika baba yake. 

Nilipata taarifa kuhusu kinachoendelea katika Idara hiyo masaa kadhaa baada ya kutangaza kuwa baba yangu, Mzee Chahali amefariki. Afisa mmoja wa Idara hiyo alinipa ushauri kuwa nisije huko nyumbani kwa sababu kuna hujuma dhidi yangu. Kuthibitisha kuwa taasisi hiyo ni ya kibabaishaji, nilipata taarifa hizo muda mfupi tu baada ya maandalizi ya operesheni hiyo, and guess what, mie nipo Uingereza. Sasa kama mie nisiye na hatia yoyote na masikini nisiye na fedha za kuhonga, jiulize, ni wauza unga wangapi wenye mamilioni ya kuhonga  wanaopewa taarifa huko nyumbani kutoka katika Idara hiyo na taasisi nyingine za dola.

Sijawahi kuficha kuwa nilikuwa mtumishi wa taasisi hiyo. Nilikuwa mtumishi mwaminifu kwa takriban miaka 15 hadi mwaka 2008 nilipoamua kuachana nayo. Sijawahi kutamka nini kilichonifanya kuchukua uamuzi huo, lakini kwa kifupi maisha yangu yalikuwa hatarini baada ya kuzushiwa kosa ambalo ni sawa na uhaini. Kwa kifupi, ukiwa mtumishi wa Idara ya Usalama wa Taifa ya nchi yeyote ile, kosa la 'kutumikia Idara ya Usalama wa Taifa ya nchi nyingine' ni kile kwa kimombo kinaitwa 'treasonable offence,' yaani kosa la kihaini. Kwanini nilizushiwa hilo, hiyo ni hadithi nyingine, ila sijawahi kuitumikia taasisi nyingine ya Usalama wa Taifa  zaidi ya hiyo ya nchi yangu.

Mwaka 2002, Idara hiyo ilinipatia skolashipu ya kuja kusoma shahada ya uzamili (Masters) huku Uingereza. Baada ya kumaliza shahada hiyo, niliomba ruhusa ya kusoma shahada ya uzamifu (PhD). Lakini kwa vile shahada ya uzamili niliyosoma haikuwa ya kiutafiti (research-based), ilinilazimu kusoma shahada nyingine ya uzamili (MRes) ambayo ni ya kiutafiti, na nilipomaliza nilijiunga na shahada ya uzamifu. Hayo yote yalifanyika kwa ruhusa ya taasisi hiyo.

Matatizo yangu na Idara hiyo yalianza Oktoba mwaka 2006, baada ya mie kuchapisha makala iliyokuwa ikimkemea aliyekuwa Waziri Mkuu wakati huo, Edward Lowassa, kuhusu taarifa za vyombo vya habari vya huko nyumbani kuwa alikuwa akijaribu kuzima mjadala wa skandali ya Richmond. Mmoja wa Wakurugenzi katika Idara hiyo alinipigia simu ya vitisho akinituhumu kuwa 'ninawasidia wapinzani,' 'ninaikosoa serikali ilhali mie ni mtumishi wake (kwa wakati huo),' na kubwa zaidi, kuhoji iwapo ninaitumikia Idara ya Usalama wa Taifa ya nchi nyinyingine. Kadhalika, press secretary wa Lowassa alisambaza makala kali kunikemea

Walinileta huku kusoma stadi za siasa, sasa mie kupevuka kifikra kuhusu vikwazo vya siasa yetu katika maendeleo ya taifa letu ikawa kosa. Uzalendo ulinishinda, ndio maana ikanilazimu kukosoa maovu mbalimbali yaliyokuwa yanawaumiza walalahoi wa Tanzania. Kichekesho ni kwamba kile nilichoandika 2006 na kushambuliwa vikali, ndicho kilichotokea miaka miwili baadaye, na kulazimisha Lowassa kujiuzulu. Na hakuna aliyenipongeza.

Mwaka 2008 nilikuja huko nyumbani kwa miezi kadhaa kumuuguza marehemu mama yangu. Nikidhani kuwa watumishi wenzangu katika Idara hiyo walikuwa wakielewa kilichokuwa kikinisibu wakati huo, wakanisumbua vya kutosha, na hatimaye njia pekee niliyobakiwa nao ilikuwa kuondoka huko nyumbani - japo baba alikuwa taabani kutokana na kifo cha mkewe aliyedumu nae kwenye ndoa kwa miaka 53. Na niliporudi huku, usumbufu ukaendelea: vitisho na upuuzi mwingine. Kwa ushauri wa taasisi za hapa, na kwa kuzingatia kuwa maisha yangu yalikuwa hatarini, nikaamua kuachana na taasisi hiyo. So ukiangalia hadi hapo, sikuwa nimefanya kosa lolote la kustahili kusumbuliwa kiasi hiki.

Kuhusu tukio la majuzi, masaa kadhaa baada ya kutangaza kuwa baba yangu amefariki, nililetewa taarifa ya uwepo wa operesheni maalum dhidi yangu, na aliyenipa taarifa hiyo alinisihi nisije huko nyumbani. Nimeambiwa kuwa Idara hiyo iliweka maofisa wake airport ili 'kunipokea.' Lakini baada ya kutoniona, walituma maafisa watatu, wawili wanaume na mmoja mwanamke, kwenda Ifakara 'kushirikiana nasi kwenye mazishi.' Wahuni hawa hata hawana ubinadamu.

Sijui wametumia kiasi gani cha fedha za walipakodi kukesha macho airport kunisubiri, na sijui hadi sasa washatumia kiasi gani huko Ifakara kuendeleza operesheni yao fyongo. Hawa wahuni hawataki kujifunza. Mwaka juzi, mwezi Februari, walituma watu kuja kunidhuru hapa Uingereza. Kwa vile Idara hiyo inaiendeshwa kishkaji, nadhani walituma wababaishaji walioishia kudakwa na mashushushu wa hapa Uingereza, ambao baadaye waliwafahamisha Polisi hapa Glasgow kuwa nichukue tahadhari muhimu. Na tangu wakati huo nimekuwa nikiishi na uelewa kuwa kuna mtu flani, siku flani atajaribu kunidhuru. Sio rahisi kuishi namna hiyo lakini sio impossible.Na hili tukio la majuzi limekuwa kama 'wake-up call' kwamba hujuma hizo dhidi yangu bado zipo hai.

Nilipokuwa mtumishi wa taasisi hiyo, niliitumikia kwa uadilifu mkubwa, na nilifanya kazi katika vitengo mbalimbali.Lakini kubwa zaidi, hadi ninaondoka huko nyumbani kuja huko kimasomo, nilikuwa Mkuu wa Kanda ya Kiintelijensia katika moja ya kanda zake jijini Dar. Huo si wadhifa mdogo, na ninakumbuka nilipowaambia maafisa wangu kuwa nakwenda Uingereza kimasomo, wapo walioniuliza 'sasa bosi unataka nini zaidi ya hiki ulichonacho sasa?' Japo wakati huo nilikuwa na shahada moja kutoka UDSM, dhamira yangu siku zote ilikuwa kukamata udaktari wa kitaaluma, na nilipopewa skolashipu kuja huku kimasomo, sikufikiria mara mbili.

Enough about that. Laiti Idara yetu ya Usalama ingekuwa na vipaumbele mwafaka basi ingehangaika na wahalifu waliokimbilia kwenye siasa na kuwadhibiti au ingehangaika na tishio la usalama wa taifa letu katika biashara ya madawa ya kulevya. Wanazidi kujaza mafaili kwenye masjala yao yenye majina ya wauza unga lakini wapo bize na watu kama sie tusio na hatia.

Wengi wenu mnanifahamu kama 'mropokaji' lakini kwa vile nilikula kiapo cha utiifu, hata siku moja sijawahi kuropoka kuhusu mambo mbalimbali niliyoshuhudia au kushiriki wakati nikiwa mtumishi wa taasisi hiyo. Sasa kwanini niendelee kuonekana adui? 

Hiyo operesheni fyongo ya mwaka juzi ilinishtua, lakini hii ya majuzi imenichukiza. Ushauri wangu pekee kwa Idara hiyo ni wa aina mbili: kwanza, fedha za Watanzania zinazopotezwa kufuatilia watu wasio na makosa zielekezwe katika kuimarisha uwezo wa Idara hiyo kupambana na wahalifu halisi wanaotishia usalama wa taifa letu, eg mafisadi , wauza unga, majangili, nk. Lakini pili, nimewashauri pia kwamba fedha zinazotumika kutufutilia akina sie' zielekezwe kwenye mafunzo ya maofisa wanaokabidhiwa majukumu ya aina hiyo. Walijaribu kuja kunidhuru hapa UK wakaishia kuumbuka. Na sasa wamejaribu kunishughulikia huko nyumbani, wameishia kupata hasara ya bure. Lakini wahuni hawa hawana uchungu na fedha wanazotumia kwa operesheni fyongo kwa vile hazitoki mfukoni mwao.

Sikupenda kzungumzia suala hili hadharani lakini imenilazimu kufanya hivyo hasa baada ya kufahamishwa kuwa familia yangu huko Tanzania inaishi kwa hofu baada ya kufahamishwa kuwa kuna watu wapo Ifakara kwa 'nia mbaya' dhidi yangu. Ninatambua hii ni vita ya sisimizi (mie) na tembo (Idara hiyo) lakini cha kutia matumaini ni vitu viwili: siku zote Mungu husimama na wanaonyanyaswa, na pili, mafunzo aliyopitia tembo ndio aliyopitia sisimizi. Hapa ni suala la akili ya nani iko mbele ya mwenzie, na ninaamini kuwa kamwe operesheni hizo fyongo hazitofanikiwa. Mlinifunza 'constant vigilance of an officer.' For your information, kwa hakika ninaitumia vizuri sana. This is a battle of wits...and sadly for you, I am still winning.

Sijaandika haya kusaka huruma ya mtu flani au taasisi hiyo. Nimeamua tu kuweka rekodi bayana. 

Asanteni kwa kuchukua muda wenu kunisoma

MESSAGE SENT AND DELIVERED.

18 Jul 2015

MOGADISHU: Kiongozi wa kikundi cha kigaidi cha Al-Shabaab jana Ijumaa alitoa ujumbe wa sikukuu ya Idd Elf Fitr ambapo alitoa wito wa  kupata  magaidi wapya ili 'kuondoa maumivu ya Waislamu' katika eneo la Afrika Mashariki.

Katika taarifa ambayo inaonyesha dhamira ya magaidi hao kusambaza ubaradhuli wao, kiongozi huyo, Ahmed Diriye, ambaye pia hujulikana kama Ahmed Umar Abu Ubaidah, alizionyooshea kideole Kenya, Ethiopia, Djibouti na Uganda.

"Majambia ya Mujahidina yameshatolewa kibindoni na mashambulizi dhidi ya maadui yanaendelea...na tunawataka wapiganaji wetu kuongeza mashambulizi dhidi ya makafiri," alisema katika taarifa iliyowekwa kwenye tovuti ya Waislam wenye msimamo mkali.

"Tunasema kwa jamaa zetu wapendwa wanaoishi kwenye maeneo yaliyo chini ya ukoloni wa Kenya kwamba sisi jamaa zenu hatotuacha kuja kuwasaidia."

"Mnapaswa kufahamu kuwa jihadi ndio njia pekee ya kujikomboa wenyewe kutoka katika unyanyasaji na udhalilishaji mnaokabiliana nao, kwahiyo mharakishe kujiunga na jihadi...na kuyakomboa maeneo yenu kutoka kwa Wakristo."

Diriye alipongeza shambuli la kigaidi katika chuo kikuu cha Garissa, Kaskazini Mashariki mwa Kenya, ambao magaidi wanne wa kikundi hicho waliwaua watu 148, wengi wao wakiwa wanafunzi. Wengi wa magaidi hao walikuwa Waislam kutoka nchini humo.
"Tunawapongeza ninyi na na Waislamu wengini duniani kwa operesheni ya kijasiri katika chuo kikuu cha Garissa," alisema kiongozi huyo wa magaidi, akieleza kuwa shambulio hilo lilikuwa la kulipiza kisasi kwa 'mauaji yaliyoidhinishwa na serikali ya Kenya dhidi ya mashehe na utekaji vijana wa Kiislam' kwenye maeneo ya pwani ya nchi hiyo.ambaye wakazi wake wengi ni Waislam.

"Muda wa Wakristo kufanya unyama bila kuwajibishwa umefikia kikomo," alisema. " Tunaswali kwako Mola kuodnoa maumivu ya Waislam katika Afrika Mashariki nzima - Ethiopia, Uganda na Djibouti."

"Hatotoacha jitihada za kuwasaidia, na milango ya mafunzo katika makambi yetu ipo wazi kuwapokea na makazi yetu yapo wazi kuwakaribisha."

Al-Shabaab, jina lenye maana 'vijana' kwa Kiarabu, waliibuka wakati wa mapambano makali dhidi ya majeshi ya Ethiopia, ambayo yaliingia nchini Somalia mwaka 2006 katika uvamizi ulioongozwa na Marekani kuung'oa utawala wa Muunganowa Korti za Kiislam ambao wakati huo ulikuwa ukitawala mji mkuu wa Mogadishu.

Magaidi wa Al-Shabaab wameendelea kufanya mashambulizi ya mara kwa mara, yenye malengo ya kupina madai kuwa kikundi hicho kinakaribia kushindwa kwenye operesheni inayoendeshwa na majeshi ya Somalia na yale ya Umoja wa Afrika, mashambulizi ya ndege ndogo zinazojiendesha zenyewe (drones) yanayofanywa na Marekani dhidi ya viongozi wa kikundi hicho, sambamba na wapiganani wanaotoroka kutoka katika kundi hilo la kigaidi.
Wakati hivi sasa kundi hilo la kigaidi linaungwa mkono na kundi jingine la kigaidi la kimataifa, Al-Qaeda, hisia zimekuwa zikiongezeka kwamba kundi hilo la Somalia linaweza kuhamisha utiifu wake kutoka kwa Al-Qaeda na kuelekea kwa kundi jingine hatari kabisa la kigaidi kimataifa la Dola ya Kiislam (Islamic States) au ISIS (kama linavyofahamika kwa kifupi).

Wakati flani, Al-Shabaab ilikuwa sumaku ya kuvuatia wapigania vijana wapiganaji kutoka mataifa mbalimbali, lakini mkakati wao kuwavutia wapiganaji wa kigeni umeathiriwa na kushamiri kwa ISIS huko Syria na Iraq, sambamba na mapigano ya wenyewe kwa wenyewe ndani ya Al-Shabaab.

CHANZO: Imetafsiriwa kutoka tovuti ya eNCA



14 Jul 2015


Nitakuwa siwatendei haki kwa kusema ASANTE au SHUKRANI pekee. Kwa hakika ni vigumu sana kupata neno/ maneno sahihi yenye kuonyesha shukrani za dhati kwa wema mkubwa uliofanyiwa. Labda niseme hivi: nawaombea Mwenyezi Mungu awabariki sana kwa upendo mkubwa na sapoti kubwa kabisa mliyonipatia mie na familia ya Marehemu Mzee Philemon Chahali.

Ninyi sasa ni familia ya Mzee Chahali kwa sababu wengi wenu mlishirikia kumfanyia sala/dua ili apone lakini bahati mbaya akafariki, na mkajitokeza kwa wingi wenu kumlilia kwa salamu zenu za rambirambi lukuki. Sidhani kama kuna upendo mkubwa zaidi ya huo. 

Kitu kimoja nina hakika nacho ni kwamba japo sasa ni marehemu, Mzee Chahali ametuacha akithamini sana upendo wenu usiomithilika. Dua/sala alipokuwa anaumwa na salamu za rambirambi zitoka kwa zaidi ya watu 850 kwa ujumla wenu. Inawezekana idadi ni kubwa zaidi ya hiyo kwa sababu nilishindwa kuhesabu watu wote.

Historia fupi ya marehemu Mzee Chahali ni kama ifuatavyo, Alizaliwa Ifakara tarehe 22/11/1930 na kupata elimu yake katika zama za Ukoloni, kitu kilichomfanya athamini sana elimu kwa sie wanae. Baadaye alifunga ndoa na marehemu mama yetu Adelina Mapngo, ndoa iliyodumu hadi mama alipofariki Mei 2008, ikiwa imedumu kwa miaka 53. Katika uhai wake, baba na mama walijaaliwa kupata watoto tisa, japo mmoja alitangulia mbele ya haki na kwa sasa tumebaki wanane, wanaume sita na wanawake wawili.

Moja ya mafanikio makubwa katika maisha ya marehemu baba ni kuwa mmoja wa mapostamasta wa kwanza wazalendo baada ya uhuru. Kwangu binafsi, moja ya legacies za baba ni kunifanya nipende habari. Kwa kawaida, alipokuwa akitoka kazini alikuja na rundo la magazeti, aliyasoma kisha kutusimulia kilichomo katika magazeti hayo. Vilevile alihakikisha hakosi kusikia taarifa ya habari ya Redio Tanzania zama hizo, na vituo vya redio vya kimataifa kama vile BBC Swahili , Sauti ya Ujerumani na Voice of Amerika kila ilipowezekana. Ile tabia ya kusoma/kusikikia habari kisha kutusimulia hatimaye ilihamia kwangu ambapo kwa hakika ninashindwa kujizuwia kukutana na habari kisha nisiishirikieshe jamii aidha katika blogu hii au kwenye makala za Raia Mwema au kwenye tweet au Facebook.

Baada ya ujio wa televisheni, Mzee alikuwa akitumia muda mwingi kufuatilia habari. Na kila mara nilipompigia simu alikuwa akiniulizia kuhusu habari za kimataifa. Hofu yake kubwa ilikuwa katika maeneo mawili. Kwanza alikuwa anapata wasiwasi sana akiona kwenye TV kuhusu matishio ya ugaidi yanayozikabili nchi za Magharibi ikiwa pamoja na hapa Uingereza ninapoishi. Kingine ilikuwa ni wasiwasi wake kuhusu athari zinazoweza kujitokeza kutokana na makala zangu magazetini hasa pale nilipoonekana nina msimamo mkali. Baba alipatwa na hofu kubwa aliposikia kwamba kwa wakati flani maisha yangu yalikuwa hatarini kutokana na tishio lililotoka huko nyumbani. Nilijitahidi sana kumpa matumaini lakini kwa hakika alikuwa na hofu kubwa hasa kila nilipokosa kufanya mawasiliano nae japo kwa siku chache.

Miongoni mwa vitu ninavyobaki ninasikitika kwa maana ya 'kumwangusha' marehemu baba ni, kwanza, kutotimiza lengo lake la mie kuwa padre. Nilipomaliza darasa la saba nilichaguliwa kujiunga na seminari ya Kasita huko Morogoro lakini pia nilikuwa nimefaulu kujiunga na sekondari ya serikali. Nikafuata moyo wangu, sikwenda seminari nikajiunga na sekondari ya serikali. Hilo lilimuumiza sana baba, lakini kwa bahatio nzuri alifanikiwa kumshawishi mdogo wangu wa kike na kumwingiza kwenye usista ambao anautumikia hadi leo.

Kingine ni faragha kidogo, ila kwa kifupi, ilinigharimu miaka kadhaa kabla sijamfahamisha nilikuwa ninafanya kazi gani nilipokuwa mtumishi wa umma huko Tanzania. Nilipomjulisha na kumfahamisha kwanini sikumweleza mapema, alinielewa. Lakini hapohapo nikawa nimemwanzishia hofu mpya akidhani kuwa kazi hiyo ilikuwa ya roho mkononi. Na hata aliposikia kuwa 'nimeachana na kazi hiyo,' baba alifanya sala kwenye simu kumshukuru Mungu akinieleza kuwa ilikuwa ikimyima amani rohoni.

Mzee Chahali alifariki tarehe 8/7/15 kutokana na mchanganyiko wa maradhi lakini kubwa likiwa tatizo la moyo. Hata hivyo, baada ya mkewe wa miaka 53- marehemu mama - kufariki mwaka 2008, mzee aliyekuwa na takriban miaka 10 zaidi ya mama, alishindwa kabisa kukabiliana na ukweli kuwa mkewe amemtangulia. Mara kadhaa nilipoongea nae alikuwa akimkumbuka mkewe na kutamani kuwa nae. Kimsingi, marehemu baba na marehemu mama walikuwa zaidi ya mke na mume. Walikuwa marafiki pia hasa kwa vile Mzee Chahali alikuwa mkimya sana na mwenye marafiki wachache. 

Sijui niwaelezeje kuhusu kifo hiki kilivyoniathiri binafsi. Baada ya mama kututoka, mzazi pekee tuliyebakiwa nae alikuwa baba. Sasa tumabaki yatima. Kwa hakika inauma sana.  Lakini yote ni kazi yaMungu.

Mzee Chahali amezikwa kwa heshima zote, ambapo kwa mji wetu wa kidini sana, misa ya mazishi kuendeshwa na Askofu ni heshima kubwa sana, na kwa hakika tunalishukuru sana jimbo la Mahenge kwa kumthamini Mzee wetu kiasi hicho.

Lajkini sijui kama leo hii ningekuwa katika nafasi ya kuandika makala hii bila sapoti yenu kubwa mno. Kila nilipotupa jicho Facebooka au Twitter nilikuta rundo la salamu za kumwombea dua/sala baba alipokuwa mgonjwa, na rundo kubwa zaidi baada ya kuwatangazia taarifa za msiba. Ninawashukuru sana sana sana. Nawaombea kwa Mwenyezi Mungu awabariki mno na awazidishie upendo wenu.

Jana nilibandika Makala Maalumu ya Sauti lakini kwa kutambua kuwa si kila mmoja ana muda au access ya kuskiliza audio filela takriban dakika 30 nikaona ni bora niziwasilishe tena salamu hizi za shukrani kwa maandishi.

Ninaomba mniruhusu nisimtaje kila mmoja wenu kwa sababu sio tu mpo wengi sana bali pia ukweli kwamba shukrani za dhati huwa moyoni. Naweza kujibaraguza hapa na sante zangu nyiiingi lakini moyoni nina mawazo mengine. Ila kwa hakika Mungu ndo shahidi wangu. Ninathamini mno mchango wenu wa hali na mali katika kumuuguza baba na kushiriki katika mazishi yake kwa njia ya rambirambi.

ASANTENI SANASANA SANA. SINA MANENO SAHIHI YA KUWAAMBIA LAKINI NINAWAOMBEA BARAKA TELE KUTOKA KWA MWENYEZI MUNGU.

Mwisho, Pumziko la Milele Bwana Mungu ajmjaalie Mzee Chahali, na mwanga wa milele amwangazie apumzike kwa amni, Ameni

ASANTENI SANA

8 Jul 2015

Ufuatao ni waraka kutoka kwa Chama cha DP kinachoongozwa na Mchungaji Christopher Mtikila kumpiga mwania nia ya Urais Edward Lowassa

KATIKA UCHAGUZI MKUU HUU
TUSIRUHUSU MAFISADI WALICHEZEE TAIFA
Edward Lowasa ni balaa kwa Taifa!

Democratic Party (DP) inatarajia kufikisha Mahakamani chama cha
CCM pamoja na wanachama wake sita, Edward Lowasa na wengine,
kwa mujibu wa Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Tanzania, kwa kosa kubwa sana la kuvunja Katiba na Sheria za Nchi kwa kuanza kampeni ya Uchaguzi kabla ya wakati unaopasa kwa mujibu wa Sheria.

1. Tunao ushahidi mzito unaothibitisha kwamba Edward Lowasa na
wenzake walianza kampeni ya urais ndani ya chama chao kabla ya
wakati, na kwamba chama chao kiliwapa adhabu ya kutofanya siasa
kwa miezi 12. Lakini safari hii Lowasa ameanza kampeni ya urais
Arusha kwa mkutano mkubwa sana wa hadhara wa kampeni haramu
na kumwaga rushwa ya kutisha!

2. Kama ni wadhamini alipaswa kuwapata katika ofisi za chama chake, katika mikoa nane (8) tu Tanganyika na mikoa miwili tu Unguja na Pemba, wadhamini 45 tu katika kila mkoa. Lakini Edward Lowasa amefanya mikutano nchi nzima, ya kuwaahidi maelfu ya wananchi katika kila mkutano wa hadhara, mambo atakayofanya kama wakimpa kura zao awe Rais! Hii ndiyo kampeni halisi, ambayo ni ukiukaji wa Katiba na Sheria za Nchi! Uchaguzi Mkuu unaendeshwa na Sheria, hivyo ni lazima Sheria ichukue mkondo wake dhidi yake kwa kuivunja.

3. Edward Lowasa amevunja Katiba ya Nchi na Sheria ya kiwango cha
fedha kinachoruhusiwa kutumika katika shughuli halali za Uchaguzi,
kiasi kwamba CCM na Taasisi zote za uchunguzi wa kifedha nchini,
upelelezi wa Jinai na Usalama wa Taifa ni mlazima wanayo kazi muhimu sana ya kupata ukweli kuhusu haya mabilioni ya fedha yanayomwagwa nchini na fisadi Edward Lowasa, ameyapata wapi na kwa namna gani, kumehusika ‘’Money laundering’ au la, kama mapato ya mapesa hayo yote ni halali, na kama mapato hayo yote yalilipiwa kodi inayopasa kwa ajili ya Taifa.

Ni marufuku kabisa tena ni makufuru Edward Lowasa kuruhusiwa
kugombea urais, kwa sababu amevunja Katiba ya Nchi na Sheria na
Kanuni za Uchaguzi. Sifa mojawapo ya kustahili kugombea uongozi wa nchi yoyote ni maadili mema na uzingatiaji wa Sheria, Kanuni na
taratibu za Utawala wa Sheria
4. Edward Lowasa, kwa kujimilikisha maeneo nchi nzima kwa kutumia kifisadi Uwaziri wake wa Ardhi, ameliweka Taifa katika hatari kubwa ya mmwagiko wa damu baina ya wakulima na wafugaji, baada ya kueneza nchi nzima makundi ya ng’ombe wake, na kusababisha mapigano makali ya mara kwa mara kila mahali nchini kati ya wafugaji wake na wakulima. Kwa sababu ya uovu huu hata katika kampeni yake haramu Lowasa ameshindwa kusema lolote juu ya kilimo, ingawa ndio uti wa mgongo wa uchumi wa nchi yetu na ndiyo shughuli inayotunza uhai wa asilimia 95 ya wananchi!

Kwa kuwaingilia wakulima katika ardhi yao, kuwaua ovyo, kuwaonea
kiasi cha kufisha matumaini yao katika kilimo, kumeifanya kauli mbiu ya “Kilimo kwanza” kuwa porojo tu ya kisanii!

5. Edward Lowasa ni mwiko kabisa kupewa kugombea urais, kwa
sababu siyo tu aliutumia kifisadi Uwaziri wa Ardhi akajitajirisha na
kujipatia maeneo makubwa ya ardhi nchini kote, bali alitumia kifisadi
zaidi uwaziri wa nchi katika ofisi ya Waziri Mkuu, katika uagizaji wa
mashangingi ya Wabunge, mawaziri, wakuu wa Mikoa na Wilaya.

6. Edward Lowasa alikemewa mnamo mwaka 1995 na Mwalimu Nyerere anayeenziwa na CCM lama “Baba” yao, alipotaka kugombea urais, kwa sababu alikuwa fisadi papa, wala hakuweza kujitetea kwavile utapeli wote aliojitajirishia ulikuwa mezani. Leo baada ya mabiashara haramu mengi na kulipora sana Taifa kukiwa ni pamoja na utapeli wa “kununua mvua Thailand” na kuliibia Taifa mabilioni ya fedha kwa kutumia kampuni hewa ya RICHMOND, huyu ni fisadi-nyangumi. Ni mlemavu wa rushwa tu wa kununuliwa na mapesa machafu anayomwaga Lowasa, anayeweza kumruhusu fisadi Edward Lowasa agombee urais.

Sifa za mtu wa kukugombea Urais zimeelezwa bayana na Mwenyezi
Mungu katika Kumbukumbu la Torati 17:15-20, ambazo Edward
Lowasa hana hata mojawapo! Lowasa awali alikemewa na Mwalimu
Nyerere ambaye CCM wanamuenzi kama “Baba” yao, kuwa hafai kabisa kuwania urais, kwa sababu alikuwa fisadi papa, kama alivyomtangaza hata Reginald Mengi pale alipolazimika kujiuzulu Uwaziri Mkuu kwa ajili ya wizi kwa kampuni hewa ya Richmond, lakini leo akiwa fisadi la kutisha zaidi kuliko papa eti anataka urais!
Si ajabu kwamba magabacholi yalioipora vibaya sana Nchi hii kama Sigh Setti na hata Nazir Karamagi wote wamo katika genge la Edward
Lowasa! Si ajabu hata fisadi Reginald Mengi leo kuungana na fisadi
Lowasa yakizingatiwa machafu yake yeye mwenyewe, na kuhusika kwa Mengi na mauaji ya Chacha Wangwe, pamoja na mpango wa Chadema
wa kumwua Mchungaji Mtikila, waraka feki wa kujaribu kuupotosha
ukweli ukatangazwa kwa ITV yake.

Katika uwaziri wake katika ofisi ya Waziri Mkuu, na katika Uwaziri wakewa Ardhi na Uwaziri Mkuu, Lowasa alifanya ufisadi ambao katika nchi kama China zenye uchungu na maslahi ya mataifa yao angekuwa wa kupigwa risasi hadharani, lakini katika nchi yetu anatafuta urais!

7. Edward Lowasa AFYA yake imempiga marufuku kugombea Urais!
Kwa ajili ya kila ajira duniasni kote, moja ya mashart makuu ni lazima mwombaji awe na afya iliyo bora, ndiyo sababu ni lazima ajira ya kila mwombaji itegemee taarifa ya kitaalamu ya madaktari, inayothibitisha kwamba hana dosari kiafya. Sharti hili ni la lazima kwa sababu:
a. Majukumu yote atakayopewa mwajiriwa atayatekeleza kikamilifu
kwa kutumia viungo vya mwili wake, kwahiyo viungo vyake vyote
ni lazima viwe katika hali iliyo imara kwa ajili ya kazi.

b. Hata kama kwa uthibitisho wa kitaalamu wa madaktari mwajiriwa
anazo akili nzuri kichwani mwake, akiwa na hitilafu katika viungo
vingine vya mwili wake huathiri afya ya akili zake na uwezo wa
utendaji wa akili zake.

c. Kazi ya Rais ni ngumu sana, kwa sababu ni pamoja na kusimamia
shughuli zote za maendeleo ya nchi nzima, na matatizo yote
yanayowatokea wananchi wote kila walipo, na kusimamia
utekelezaji wa majukumu yote ya watendaji wote katika Taifa,
hivyo kwamba maamuzi sahihi yanatokana na afya bora yenye
kuhakikisha uwezo unaopasa wa kiakili wakati wote

d. Hitilafu katika afya hudhoofisha uwezo wa kifikira na kusababisha
maamuzi mabovu, ambayo huleta athari mbaya sana kwa Taifa. Na
udhaifu huo huathiri mpaka maadili na hata uzalendo wa huyo
kiongozi mdhaifu. Kwa mfano akipatikana Rais anayeishi kwa
matumaini, kwa hofu ya kupoteza uhai kabla hajaweka sawa
mambo yake na ya familia na jamii yake atatumikia maslahi yake
zaidi kuliko Taifa, tatizo hilo la afya likawa limelikosesha Taifa
kipaumbele, na kuliangamiza kimaendeleo!
e. Wanaowania kugombea urais ni lazima wachunguzwe kwa makini
sana afya zao, kwa sababu kukifanyika makosa akatawazwa
mwenye hitilafu za kiafya, atakwenda kuwa mzigo mzito sana kwa
Taifa, hususan ugharamiaji wa utunzaji wa uhai wake ndani na nje
ya nchi, kukosekana na umakini anaopasa kuwa nao kwa ajili ya
dhamana kubwa aliyopewa n.k.

Kutokana na AFYA yake kuwa dhaifu sana hata kwa kumwona kwa
macho tu, kabla ya uchunguzi wa kitaalamu ni kwamba Edward Lowasa hawezi kabisa kugombea Urais. Kwani amekosa sifa muhimu sana ya afya bora, ambayo ni ya lazima kwa mtu yeyote anayestahili kupewa dhamana kubwa sana ya kuliongoza Taifa. Pengine hata kugombea urais kwenyewe anatafuta kutokana na hitilafu ya kiafya, iliyosababisha udhaifu katika kufanya maamuzi, hivyo amejikuta kwa bahati mbaya anagombea asichokiweza kabisa.

Ni lazima wagombea wote wa Urais, wa Ubunge na hata wa Udiwani
wachunguzwe kwa makini afya zao kabla ya kupewa kugombea, na hata kuchunguzwa tena katikati ya muhula wa utumishi wao, kama kweli tunalithamini na kuliheshimu Taifa.

Sifa za urais ni wito au uhanga kwa ajili ya Nchi ambao ni zaidi ya
maadili ya kizalendo, maono, vipawa na AFYA BORA. Ni dhana potofu
sana kwamba sifa ya urais ni kushabikiwa na umati wa watu! Kwa
sababu wengi hufuata mapesa na husombwa hata na magari ili umati
wa kishabiki tu upatikane. Lakini kumpenda mtu huwa lazima kuwe na sababu, wakati ushabiki ni pepo mchafu au ‘psychological deficiency’.





Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.