22 May 2016



Taarifa mbalimbali zinaonyesha kuwa kuna ongezeko kubwa la Watanzania wanaojihusisha na ushoga na usagaji japokuwa vitendo hivyo ni kinyume na sheria za nchi na haviendani na mila na desturi zetu.

Hata hivyo, yawezekana kushamiri kwa vitendo hivyo kunaendana na taarifa za kitafiti kuwa sie Watanzania twaongoza kwa unafiki. Wiki chache zilizopita niliweka bandiko hapa bloguni lililohusu ripoti ya utafiti wa kundi la wasomi katika chuo kikuu cha Nottingham, hapa Uingereza, ulivyobainisha kuwa Tanzania yaongoza duniani kwa unafiki.

Binafsi sikushangazwa na ripoti hiyo hasa kwa vile kuna maeneo mawili yanayothibitisha bayana unafiki wetu. La kwanza ni uhusiano kati ya ucha-Mungu wetu na maovu.

Asilimia kubwa ya Watanzania ni wacha-Mungu. Takwimu zaashiria kuwa takriban asilimia 70 ya Watanzania ni aidha Wakristo au Waislam. Wengi kati ya hao ni watu wasiokosekana kanisani au misikitini. Swali: kama wengi wetu ni waumini kiasi hicho, ni akina nani basi wanaojihusisha na ufisadi, rushwa, biashara ya madawa ya kulevya, ushirikina, na maovu mengine katika jamii?

Tofauti na huko nyumbani, ucha-Mungu hapa Uingereza ni wa kusuasua mno. Watu wengi hapa hawamtambui Mungu na wanajitambulisha kuwa hawana dini. Makanisa mengi yanageuzwa kuwa baa au kumbi za starehe kutokana na uhaba wa waumini.



Lakini licha ya udhaifu katika mahusiano kati yao na Mungu, wenzetu hawa kwa kiasi kikubwa sio wanafiki. Asilimia kubwa kabisa ya watu hawa wanaishi kwa kipato halali, wanaamini katika ukweli, kwa maana ya kusema ukweli na sio wadanganyifu, wanafuata sheria na taratibu mbalimbali, kwa mfano moja ya dhambi kuu hapa ni ukwepaji kodi, kitu ambacho ni kama hobby ya wengi wa wafanyabiashara huko nyumbani.

Eneo la pili ni suala la ushoga na usagaji. Kwa huko nyumbani, suala hili ni mwiko mkubwa, ni laana, ni kinyume na maadili yetu. Lakini kuthibitisha unafiki wetu, sio tu ushoga na usagaji upo bali pia unakua kwa kasi kubwa.

Nenda katika kitchen parties za watu maarufu na 'wakata viuno' ni mashoga huku wengi wa 'makungwi' wakituhumiwa kuwa wasagaji. Inaelezwa kuwa njia moja maarufu ya kusambaa kwa usagaji huko nyumbani ni 'makungwi' wanaofundisha mabinti (kwa malipo) jinsi ya kufanya tendo la ndoa. Hawa wametapakaa jijini Dar na baadhi wanahamia mikoani. Kimsingi, 'darasa la tendo la ndoa' wanalofundisha ni kwa kusagana na 'wanafunzi' wao.

Shughuli za 'madada wa mujini' hazijakamilika kama hakuna akina 'anti naniliu au anti nanihino.' Lakini watu haohao ndio wanaohubiri kwa sauti kubwa kuwa "habari za ushoga na usagaji huko huko kwao (wazungu)."

Kuna kitu kingine 'kichafu' ambacho Watanzania twasifika mno, nacho ni umahiri katika tendo la ndoa kinyume cha maumbile. Kwa kifupi, hii ndio sababu ya kushamiri kwa biashara ya "dawa za makalio feki ya Mchina." Tendo la ndoa kinyume cha maumbile limekuwa kama 'fasheni' kwa wengi wetu huko nyumbani na huku ugenini tunakoishi. 

Sasa, japo tendo la ndoa kinyume cha maumbile sio ushoga per se, kuna hisia kuwa wazoefu wa tabia hiyo "wakikosa nyama wanaweza kula majani." Yaani wanaume wanaopenda tabia hiyo wakikosa mwanamke wanaweza kufanya hivyo na mwanaume shoga.

UTHIBITISHO wa unafiki wetu: Well, sehemu mwafaka zaidi ya kutambua unafiki wetu kuhusu ushoga na usagaji ni INSTAGRAM. Huko, kuna mashoga wanaojinadi waziwazi. Lakini tatizo sio wao kujinadi tu bali ni idadi ya 'followers' wao. Ni wazi kuwa laiti ingekuwa watu wanachukia ushoga 'kihivyo' basi mashoga huko Insta wasingekuwa maarufu kiasi cha kupata followers hadi laki na zaidi.

Profiles hizi pichani chini ni za baadhi tu ya mashoga wa Kitanzania huko Instagram.  Je kama sie sio wanafiki na laiti tungekuwa tunauchukia ushoga 'kihivyo' hao maelfu kwa malaki ya followers kwa hao mashoga wangetaka wapi?


Ukitaka kuchimba zaidi kuhusu 'unafiki' wetu, geukia suala jingine maarufu huko nyumbani: USHIRIKINA. Kwa mujibu wa utafiti wa hivi karibuni wa taasisi moja ya kimataifa inayoheshimika kwa utafiti ya PEW ya Marekani, Tanzania ipo 'matawi ya juu' katika masuala ya juju, ndumba na ngai, tunguri, kamati ya ufundi, wanga...USHIRIKINA... kama inavyoonyeshwa kwenye chati na ramani hapo chini.




Kwa vile lawama pekee hazijengi, ni muhimu kujaribu kuangalia njia zinazoweza kutuondoa katika lindi hilo la unafiki. Binafsi, ninashauri tuwekeze zaidi katika dua na sala za dhati na sio za kinafiki. Au wewe msomaji mpendwa una maoni gani?



21 May 2016


Nianze makala hii kwa kumpongeza Rais John Magufuli kwa hatua aliyochukua jana ‘kumtumbua’ aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga, kwa kosa la kuingia Bungeni akiwa amelewa.

Kadhalika, ningependa kutumia fursa hii kumshukuru kwa kuwa kiongozi msikivu. Binafsi, ‘nilikomalia’ sana kuhusu uwaziri wa Kitangwa hasa kutokana na tuhuma kuwa ni mhusika katika skandali ya Lugumi (na tetesi kuwa alikuwa mlevi - japo sikuwahi kuongelea ishu hiyo ya ulevi kwa vile niliona kama suala binafsi, alimradi haliathiri utendaji wake wa kazi). 

Kwa ‘mtaani’ hatua hiyo ya Rais Magufuli inaweza kuonekana ni ya kawaida tu, yaani kiongozi aliyefanya uteuzi wa mtu flani, hatimaye kuamua kuteungua uteuzi huo. Lakini kwa hakika, hatua hiyo ya Rais Magufuli haikuwa rahisi. 

Kwa mujibu wa taarifa, Rais Magufuli na Kitwanga wamekuwa marafiki wa muda mrefu. Wajuzi wa mambo wanaeleza kuwa hata uamuzi wa kumteua Kitwanga kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ulitokana na imani ya Rais Magufuli kwa rafiki yake huyo. Ikumbukwe kuwa wizara hiyo ni moja ya wizara nyeti ambazo kwa kiasi kikubwa hukabidhiwa kwa watu wanaoaminika mno kwa rais husika. 

Kuna kipande cha video kilichosambaa mtandaoni siku za nyuma ambacho kilikuwa kinamwonyesha Rais Magufuli kabla hajawa rais wala mgombea wa CCM, akiwa na Kitwanga, na katika maongezi yao, Kitwanga anasikika akimwambia Magufuli agombee urais (japo ni katika hali ya utani). 

Lakini pia inaelezwa kuwa hata kabla Rais Magufuli hajatangaza baraza lake la mawaziri, Kitwanga alikuwa akijigamba kuwa angepewa wizara nyeti, mara baada ya Magufuli kutangaza kabineti yake, na wizara nyeti ya mambo ya ndani ya nchi akapewa baada ya kutangazwa kabineti hiyo. 

Hata hivyo, suala hili la Kitwanga linapaswa kuamsha maswali kuhuru Idara yetu ya Usalama wa Taifa na utaratibu wa ‘kuwatafiti wateule watarajiwa wa Rais,’ kitu kinachofahamika kitaalam kama ‘vetting.’ Nina uhakika wa asilimia 100 kuwa ‘dossier’ (kabrasha maalum kuhusu mtu maalum) la Kitwanga lilipaswa kueleza bayana kuhusu tabia yake ya ulevi. Je ilikuwaje sio tu akateuliwa kuwa waziri bali pia kuteuliwa kuwa waziri katika wizara nyeti kabisa kwa usalama wa raia na nchi. Je kulikuwa na mapungufu huko Idara ya Usalama wa Taifa au walieleza hilo kabla Kitwanga hajateuliwa lakini likapuuzwa? Ni vigumu kuwa na uhakika wa kipi kilitokea. 

Kwa kuwa lengo ni kwenda mbele na si kunyoosheana vidole tu bila kutoa uushauri au kuleta ufumbuzi, binafsi ninashauri wahusika waangalie wapi walijikwaa, ili wasirudie tena kosa hilo. Vetting ya wateuliwa watarajiwa ni muhimu mno kwa sababu licha ya kuiingiza gharama serikali pale inapolazimu uteuzi husika kutenguliwa, pia inahatarisha usalama wa taifa (watu wanaotimuliwa madarakani ni rahisi kuwa recruited na maadui wa taifa ili 'kulipa kisasi').

Tukiweka kando mapungufu hayo, kitendo cha Dkt Magufuli kumtumbua Kitwanga kinapeleka ujumbe mzito kwa kila mtumishi wa serikali. Kwanza, kinaashiria kuwa Rais anafanyia kazi taarifa anazoletewa (maana hakuwepo Bungeni Dodoma wakati Kitwanga akiwa 'bwii' mjengoni. 

Lakini pia kitendo hicho kinaashiria kuwa mfumo wa mawasiliano ndani ya serikali umerejea kama wa zama za Nyerere, pasipo 'taarifa kuvuja' kabla ya kufika mahali stahili. Hali hii itapelekea watendaji wa serikali ikiwa ni pamoja na mawaziri kuwa makini zaidi kwani hawajui nani anawachunguza au nini kinaripotiwa kwa Rais kuhusu wao.

Tukiweka hilo kando, binafsi nimefarijika sana baada ya kusikia taarifa za Kitwanga ‘kutumbuliwa’ kwa sababu nilipiga kelele za kutosha kuhusu uongozi usioridhisha wa mheshimiwa huyo. Nilianza kitambo kuhoji kuhusu utendaji kazi wa waziri huyo.

Suala la kwanza ‘kumshikia bango’ lilikuwa kauli zake za utata kuhusu kupambana na biashara haramu ya madawa ya kulevya. Hili nililiandikia MAKALA HII. 







Baadaye, ikaibuka skandali ya Lugumi, na kwa hakika sikuchoka kupiga kelele, hususan kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter kama inavyoonekana hapa chini 



Sambamba na kelele hizo hatimaye niliamua kuandika MAKALA HII 


Ni matarajio yangu makubwa kuwa makala hii itamhamasisha kila msomaji kuwa na msimamo, na kisha kusimama imara katika msimamo huo, sambamba na kuhakikisha kuwa anachosimamia ni sahihi, na kuendelea kuupigania hadi mafanikio yapatikane. Sio kazi rahisi lakini mara nyingi vitu vizuri, au vinavyodumu, huwa havipatikani kirahisi. 

Mwaka 2006, niliandika MAKALA HII kuhusu suala la mkataba wa kufua umeme, uliopelekea skendo ya Richmond, na nikaendelea kupiga kelele hadi mwaka Februari 2008 baada ya mhusika mkuu katika skendo hiyo, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, kujiuzulu. Hata hivyo, ishu hiyo ilinigharimu mno kimaisha. 

Na hivi majuzi, nilijaribu ‘kuwashikia bango’ wahusika wa Mamlaka ya Mawasiliano TCRA, na nikawatwanga MAKALA hii. 


Siku chache baadaye, bosi wa taasisi hiyo akatumbuliwa. 


Na majuzi tu, Ubalozi wetu hapa Uingereza ulitaka kutufanyia 'uhuni' katika ziara ya Waziri Mkuu, ambapo awali kulikuwa na mpango wa kumkutanisha Waziri Mkuu na kundi dogo tu la Watanzania wanaoishi hapa. Kelele nilizoshiriki kuibua zilisaidia, na hatimaye mkutano huo wa Waziri Mkuu ulifanywa kuwa wa wazi kwa kila Mtanzania mkazi wa hapa kuhudhuria. Nimeelezea kwa kirefu kuhusu sakata hili katika MAKALA HII.

Sitaki kujisifu kuwa kelele zangu pekee ndio zinapelekea hatua kusudiwa kuchukuliwa. Hapana. Ninachojaribu kuonyesha ni ushiriki wangu katika harakati za kudai mabadiliko kwa kupitia maandishi, “kelele zetu” iwe hapa bloguni, kwenye mitandao ya kijamii au kwa njia ya makala. Pia, kwa kuwaeleza wasomaji kuhusu mafanikio ya 'kelele zetu' inasaidia kuhamaisha watu wengi zaidi kutambua umuhimu wa harakati kama hizi katika kuleta mabadiliko kusudiwa


Mara nyingi tunapopiga kelele hizo tunaishiwa kukebehiwa, kuonekana vimbelembele, tusio na vitu muhimu vya kufanya katika maisha yetu binafsi, na shutuma kama hizo. Lakini pindi kelele zetu zinapozaa matunda, walewale waliokuwa wakitukebehi huwa mstari wa mbele “kusaka sifa.” 

Kimsingi, harakati hizi sio za kusaka ujiko au madaraka. Ni kile nilichoeleza awali: kuwa na msimamo na kusimama thabiti katika msimamo huo hadi ufumbuzi wa tatizo husika upatikane.

Nimalizie makala hii kwa kumpongeza sana Rais Magufuli kwa ‘kumtumbua’ Kitwanga. Wanaohisi kuwa kutambuliwa huko ni ‘kuficha kombe’ la ishu ya Lugumi, ombi langu kwao ni wavute subira. 

Sakata la Lugumi sasa litachukua sura mpya, na tusishangae kusikia watu wakiburuzwa mahakamani hivi karibuni. Pia suala hili la kutambuliwa Kitwanga linaweza kumpa fursa Rais Magufuli fursa ya kuwatumbua angalau mawaziri mawili hivi ambao mwenendo wao umekuwa wa kusuasua. Fursa ya kuwatumbua inatokana na kutambuliwa kwa Kitwanga ambako kutamlazimu Rais kufanya ‘reshuffle’ ndogo.

20 May 2016


WIKI iliyopita yaweza kubaki kwa muda mrefu kwenye kumbukumbu za Watanzania wanaoishi hapa Uingereza. Kwa upande mmoja, wiki hiyo ilimalizika kwa mkutano kati ya baadhi yao na Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa, na kwa upande mwingine wiki hiyo ilitawaliwa na mizengwe ya ‘kuzuia’ fursa kwa wengi kukutana na Waziri Mkuu.

Awali, zilipatikana tetesi kwamba Rais John Magufuli angefanya ziara ya kikazi hapa Uingereza, lakini baadaye ikafahamika kuwa Waziri Mkuu Majaliwa ndiye angemwakilisha.

Hatimaye Waziri Mkuu aliwasili hapa kwa mara ya kwanza tangu ashike wadhifa huo, na pia kuwa kiongozi wa kwanza wa kitaifa kuzuru nchini hapa tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani.

Wengi wa Watanzania wanaoishi nchini hapa walionyesha kiu kubwa ya kukutana na kiongozi huyo mpya, hususan kusikiliza visheni ya Serikali ya Awamu ya Tano kwa Tanzania na Watanzania, ikiwa ni pamoja na tunaoishi nje ya nchi yetu.

Hata hivyo, kiu hiyo ilikumbana na kikwazo kutoka Ubalozi wa Tanzania hapa Uingereza, haukujali kutoa taarifa yoyote kwa Watanzania wanaoishi hapa kuhusu ujio wa kiongozi huyo wa kitaifa wala kueleza iwapo angekutana nao kwa maongezi.
Baadaye zikasikika tetesi kuwa Ubalozi huo (aidha kama ofisi au baadhi ya maofisa wake) ulitoa mwaliko kwa takriban watu arobaini hivi kuhudhuria ‘kikao’ na Waziri Mkuu. Tetesi hizo hazikueleza jinsi gani ‘wawakilishi’ hao walivyopatikana, lakini kilichoonekana bayana ni suala hilo kuzingirwa na usiri mkubwa.

Binafsi, nilianzisha jitihada za kuutaka Ubalozi uangalie umuhimu wa kuhakikisha kuwa kila Mtanzania anayeishi hapa anapatiwa fursa ya kuhudhuria mkutano huo. Awali niliweka ujumbe kwenye kundi la ‘Whatsapp’ la Watanzania wanaoishi hapa, japo mapokeo hayakuwa ya kuridhisha.

Baadaye nilichukua jukumu la kuandika makala katika blogu yangu baada ya kuzungumza na Watanzania kadhaa wanaoishi hapa, na ambao walionyesha bayana kutoridhishwa na jinsi Ubalozi wetu ulivyoonekana ‘kuhujumu’ uwezekano wa Watanzania wengi zaidi wanaoishi hapa kukutana na kiongozi wao.

Kwa bahati nzuri, ‘kelele’ za makala hiyo na ‘kilio’ kilichofikishwa kwenye kituo kimoja cha radio huko nyumbani na baadhi ya Watanzania wanaoishi hapa, zilizaa matunda. Hatimaye, Ofisi ya Waziri Mkuu ilitoa tamko kuwa Waziri Mkuu angekutana na Watanzania wanaoishi hapa.

Ofisi ya Waziri Mkuu pia ilijaribu kujitetea kuwa haikuhusika na maandalizi ya mkutano kati ya Waziri Mkuu na Watanzania wanaoishi hapa, japo haikuwahi kulaumiwa na mtu yeyote kwa sababu utaratibu uliozoeleka ni kwa Ubalozi (sio Wizara au ofisi za huko nyumbani) kufanya maandalizi ya mikutano ya viongozi wa kitaifa na Watanzania wanaoishi hapa.

Kwa upande mwingine taarifa hiyo ilikuwa kama inakanusha 'madai ya watu' kuwa kuna watu maalumu waliochaguliwa kuhudhuria mkutano huo (badala ya kuwa mkutano wa wazi kwa kila Mtanzania anayeishi hapa. Hata hivyo, kulikuwa na uthibitisho kwamba awali mpango wa ubalozi ulikuwa ni kwa kundi la watu kadhaa tu kukutana ‘kwa faragha’ na Waziri Mkuu.

Uthibitisho huo ulisikika baada ya mmoja wa maofisa wa ubalozi wetu hapa kujirekodi na kuweka ujumbe wa sauti (voice note) kwenye kundi la Whatsapp (la Watanzania wanaoishi hapa) ambapo pamoja na mambo mengine alikebehi jitihada za kutaka Watanzania wengi zaidi wanaoishi hapa wapate fursa ya kukutana na Waziri Mkuu. Alidai kuwa “hata Rais anapoongea na wazee jijini Dar haimaanishi basi wazee wote wa Dar wataalikwa kwenye mkutano huo.” Alidai kuwa hakuna ubaya kuteua watu wachache tu kuzungumza na Waziri Mkuu, na kuongeza kuwa ‘Watanzania wamezoea kuja wengi japo walioalikwa wachache tu.’

Kwa upande mmoja ninaipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa ‘kusoma alama za nyakati’ na kuruhusu mkutano kati ya Waziri Mkuu na Watanzania wanaoishi hapa kuwa wa wazi. Kwa upande mwingine ninaikosoa kwa sababu tamko lake kuwa mkutano huo utakuwa wa wazi sio tu lilitolewa Ijumaa - siku moja kabla ya mkutano – lakini pia haikubainisha muda wala sehemu kutapofanyika mkutano huo. Pengine ni mazoea tu ya huko nyumbani, lakini maisha ya hapa kwa kiasi kikubwa yanaambatana na ‘ratiba kali,’ na taarifa ya muda mfupi na isiyojitosheleza kimaelezo (kama hiyo ya Ofisi ya Waziri Mkuu) inaweza kuwa iliwanyima fursa watu wengi zaidi kuhudhuria mkutano huo.

Kwa upande wa Ubalozi wetu hapa, hadi wakati ninaandika makala hii haujafanya jitihada za kuwaomba radhi Watanzania wanaoishi hapa kwa ‘mpango wake fyongo’ ambao laiti ungefanikiwa, basi mkutano huo wa Waziri Mkuu ungekuwa ni kati yake na ‘wateule wachache’ tu. Kadhalika, ofisa ubalozi aliyejirekodi na kukebehi harakati zetu kudai fursa kwa wote kuhudhuria mkutano huo angeomba radhi kwa kauli zake zisizoendana na wadhifa wake wala ustaarabu wetu Kitanzania.

Pengine utata huo ungeweza kuepukika laiti pande mbili zinazohusika na ziara za viongozi wa kitaifa zingewajibika ipasavyo. Kwanza, ubalozi wetu hapa ungeweza kutengeneza mazingira mazuri ya mawasiliano na Watanzania wanaoishi hapa kwa kutumia mitandao ya kijamii au njia nyingine mwafaka. Hisia ni kwamba ‘ukimya’ uliojitokeza kuhusu ziara hiyo ulikuwa wa makusudi (yaani mkutano huo ulipaswa kuwa ‘shughuli ya wateule wachache’).

Pili, idara yetu ya masuala ya usalama imekuwa na utaratibu wa kutanguliza maafisa wake eneo ambalo kiongozi wa kitaifa atatembelea, kitu kinachofahamika kiintelijensia kama ‘advance party.’ Na moja ya majukumu ya waliomo kwenye ‘msafara’ huo ni kubaini yanayoweza kujitokeza wakati wa ziara husika. Kwa hiyo, laiti wangetupia macho ‘sehemu’ za maongezi ya Watanzania wanaoishi hapa (kwa mfano kundi lao la ‘Whatsapp’) basi wangeweza kubaini mapema kuwa kuna kiu ya mkutano na Waziri Mkuu sambamba na shutuma kuwa ubalozi unakandamiza kiu hiyo.

Nimalizie makala hii kwa kutoa wito kwa ofisi zetu za ubalozi popote zilipo ziwe kiunganishi kati ya Watanzania wanaoishi nchi hizo na nchi yetu, sio kwa masuala yanayohusu hati za kusafiria tu na masuala ya kidiplomasia bali kudumisha Utanzania wetu kwa upendo, umoja na mshikamano. Balozi zetu kadhaa zimekuwa zikilaumiwa kwa ‘kutokuwa na msaada,’ sambamba na kauli za jeuri/kiburi kwa baadhi ya maofisa wetu wa ubalozi, hali inayodhaniwa inatokana na baadhi yao kukaa huku nje muda mrefu mno kiasi cha ‘kuwadharau Watanzania wenzao.’

Mwisho, iwe ni kwa busara zake binafsi au ofisi yake, shukrani za pekee kwa Waziri Mkuu Majaliwa kuweza kuongea na Watanzania wanaoishi hapa Uingereza. Takriban kila aliyehudhuria mkutano huo ameridhishwa na hotuba ya Waziri Mkuu ambayo imetoa matumaini makubwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kwa dhati kuiboresha Tanzania yetu katika kila eneo.

19 May 2016


Kuna msemo wa Kiingereza unaoweza kutafsiriwa hivi, "thamani ya fedha ni matumizi." Pesa isiyoweza kutumika haina thamani, inabaki kuwa karatasi tu lenye picha ya kiongozi au alama fulani. Vivyo hivyo, thamani ya elimu/uelewa ni katika kushirikisha watu wengine. Ukiwa na elimu ya kutosha au uelewa mkubwa lakini ikabaki kichwani mwako tu bila kutumiaka basi haina umuhimu. Ni katika mantiki hiyo, sie wengine tumekuwa waumini wakubwa wa filosofia isiyo rasmi ya 'Sharing Is Caring' ambayo mara nyingi huandikwa #SharingIsCaring.

Leo ningependa ku-shea nawe msomaji mbinu muhimu ya ku-post kitu mtandaoni ili kioneknaje au kusomwa na watu wengi. Yaani hapa nazungumzia kuhusu ku-update status yako Facebook iwe ya maneno au picha, au ku-tweet huko Twitter, au ku-post picha yako hujo Instagram.

Tuanze na Facebook. Muda mwafaka wa ku-update status yako ili iweze kusomwa na watu wengi zaidi ni kati ya saa 3 asubuhi hadi saa 1 usiku, lakini muda bora kabisa ni saa 7 mchana hadi saa 9 alasiri.  

Kwa upande wa Twitter, muda mwafaka wa ku-tweet kitu kinachoweza kusomwa na watu wengi zaidi ni saa 6 mchana na kati ya saa 11 jioni na saa 12 jioni.

Kwa Instagram, muda mwafaka ni alfajiri, kwa maana watu wakiamka na kuingia kwenye app hiyo wakutane na picha yako.Lakini mtandao huu ni kimeo na jipu kwa Tanzania. Kwahiyo hata kuelezea kanuni zake ni sawa na kupoteza muda. Mtandao huu umetawaliwa na vitu vichafu na visivyopendeza. Binafsi japo bado ni memba huko lakini siutumii kwa sababu umesheheni kila aina ya maovu.

Maelezo hayo juu ni maalum kwa watu wenye ratiba zao nyingine lakini wanapenda kuwasiliana na jamii kwa kutumia mitandao ya kijamii. Maelezo hayo hayana maana kwa wenzetu ambao wapo mtandaoni kutwa kucha. Yes, kuna wenzetu wapo mtandaoni muda wote.

Kadhalika, maelekezo hayo ni ELEKEZI tu, kwa maana kwamba sio lazima usubiri muda huo mwafaka ndio uposti kitu chako. Muda huo elekezi ni mwafaka kwa minajili ya kuwafikia watu wengi zaidi.

Pichani chini ni infograph kuhusu nilichoeleza hapo juu



Endelea kutembelea blogu hii kwa mada mbalimbali za teknolojia, sambamba na makala zangu za kila wiki katika jarida la Raia Mwema, mada mbalimbali za intelijensia, burudani na michezo, maisha, na kadhalika. Karibuni sana

18 May 2016



Tukubaliane kwamba japo wengi wetu twapenda kutumia mtandao, hususan kutembelea mitandao ya kijamii kama vile Faceboo, Twitter, Instagram, nk bado kuna uelewa mdogo wa mbinu mbalimbali ambazo laiti zikutumika zaweza kuleta ufanisi zaidi katika matumizi ya mtandao au mitandao hiyo ya kijamii.

Siku za nyuma nilikuwa nikiandika makala mbalimbali kuhusu teknolojia lakini kutingwa na majukumu kumesababisha ni we mzembe kidogo. Samahani kwa hile, maana linaathiri ile spirit ya 'Sharing Is Caring.' 

Anyway, long story short, leo nina darasa fupi la jinsi ya kuangalia watu waliotembelea ukurasa (profile) wako wa Facebook. Ni suala la hatua kwa hatua, na nina hakika ukifuata kwa makini utaweza kuona nani ametembelea profile yako. Labda sio muhimu, lakini, hey, kuna watu  wangependa kufahamu vitu kama hivyo.

Samahani, nimejaribu kutafsiri hatua hizo pichani kwa Kiswahili nimechemsha. Natumaini kimnombo kilichotumika sio kigumu, lakini ikitokea mtu hajaelewa vema basi nishtue nitajitahidi kutoa ufafanuzi kwa Kiswahili.


Endelea kutembelea blogu hii kwa mbinu zaidi za mtandaoni pamoja na habari za teknolojia na habari nyinginezo.

Karibuni sana

17 May 2016


"Hello world!" ndio ilikuwa tweet ya kwanza baada ya Idara ya ushushushu ya Uingereza inayohusika na kunasa mawasiliano, GCHQ (Government Communications Headquarters)  kujiunga na mtandao huo wa kijamii. 

Hawa jamaa, ambao makao yao makuu ni hayo pichani juu, ndio wenye jukumu la kusoma barua-pepe zetu, kusikia simu zetu na kutegesha vinasa sauti pale inapobidi, wamebobea kwenye hacking...kwa kifupi ukitaka kuwaelewa vema, m-Google yule jamaa anaitwa Edward Snowden..amewazungumzia vya kutosha, wao na washirika wao wa Marekani, wanaoitwa NSA.

Sasa hawa jamaa wameingia rasmi katika mtandao wa kijamii wa Twitter.



Hiyo tweet yao ya kwanza ya "Hello world" iliyoambatana na picha ya ndani ya ofisi yao, ina umuhimu wa aina yake kwa sababu ni programu ya kwanza kujifunza kuandika wakati mtu anapojifunza kundika kwa lugha ya ku - code katika  vile Java, Python, C, PHP, na Ruby.

"Kwa kujiunga na mitandao ya kijamii, GCHQ inaweza kutumia sauti yake yenyewe kuongea  kuhusu kazi muhimu tunayofanya kuiweka Uingereza salama," alisema Andrew Pike, Mkurugenzi wa Mawasiliano wa taasisi hiyo ya kishushushu.

Taasisi hiyo ya kishushushu imeeleza kuwa inataka kufikika (accessible) na kuufahamisha umma kuhusu shughuli zake. Kadhalika, inataka majadiliano na watu wenye ufahamu wa teknolojia hususan katika maeneo ya teknolojia, hisabati, usalama mtandaoni na mada nyinginezo.




16 May 2016

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akihutubia Watanzania wanaoishi hapa Uingereza



Sehemu ya hotuba ya Waziri Mkuu Majaliwa


Baadhi ya Watanzania wanaoishi hapa Uingereza wakiwa katika mkutano huo na Waziri Mkuu Majaliwa



Sehemu ya hotuba ya Waziri wa Mambo ya Nje Balozi Mahiga

Waziri Mkuu Majaliwa na Balozi Mahiga 

Baadhi ya Watanzania wanaoishi hapa Uingereza wakiwa katika mkutano huo




Waziri Mkuu Majaliwa akiwa na Kaimu Balozi Mr Marwa (wa kwanza kushoto), Balozi Mahiga na Jaji Mkuu Chande (kulia)

Waziri Mkuu Majaliwa akihutubua


Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Valentino Mlowola akiongea kwenye mkutano huo


Jaji Mkuu Chande akiongea


Jaji Mkuu Chande akiongea. Kushoto kabisa ni Balozi Mahiga na kulia ni Kamanda Mlowola

Waziri Mkuu Majaliwa akihutubia


Meza kuu


Sehemu ya Watanzania waliohudhuria Mkutano huo uliofanyika kwenye ubalozi wa Tanzania jijini London hapo jumamosi Mei 14, 2016

14 May 2016


Jana nilibandika makala kuhusu manung'uniko ya Watanzania wengi wanaoishi hapa Uingereza ambao walikuwa hatarini kukosa fursa ya kuhudhuria mkutano na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ambaye yupo nchini hapa kikazi.

'Kelele' hizo zimezaa matunda, na leo Waziri Mkuu Majaliwa atakutana na Watanzania wote wanaoishi nchini humu wanaoweza kumudu kufika ubalozini London saa kumi alasiri. Awali, maofisa husika katika ubalozi huo walialika kundi dogo tu la Watanzania kuhudhuria mkutano huo, hatua iliyotafsiriwa na wengi kama ubaguzi na pengine jitihada za kuficha majipu yanayoukabili ubalozi huo.

Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu imeandikwa kidiplomasia, ambapo kwa upande mmoja imejitoa lawama ya kuhusika na maandalizi ya mkutano huo (na hakuna aliyemlaumu Waziri Mkuu au Ofisi yake bali lawama zilielekezwa kwa ubalozi) .



Kwa upande mwingine ni kama imekanusha 'madai ya watu' kuwa kuna watu maalum waliochaguliwa kuhudhuria mkutano huo (badala ya kuwa mkutano wa wazi kwa kila Mtanzania anayeishi hapa). Nimesema ni "lugha ya kidiplomasia" kwa sababu uthibitisho kwamba awali mpango wa ubalozi ulikuwa ni kama ulivyolalamikiwa jana , yaani kundi la watu kadhaa tu ndio wakutane na Waziri Mkuu, na uthibitisho huo unasikika katika audio hii ya mmoja wa maofisa wa ubalozi wetu anayetukebehi kwa kudai haki ya kukutana na Waziri Mkuu. Msikilize kwa kubonyeza play


Ni wazi kuwa laiti afisa ubalozi huyo ndio angekuwa na mamlaka ya mwisho basi ni wazi angebaki na hao watu wachache ambao awali ndio waliteuliwa kuhudhuria mkutano huo kana kwamba ni wa siri.

Badala ya kukiri kwamba ubalozi ulifanya makosa kuteua watu wachache tu, afisa huyo anaelekea kutuona kituko kwa kudai haki ya msingi ya kukutana na viongozi wetu wa kitaifa. Na badala ya kutumia fursa hiyo kuwaeleza Watanzania ratiba ya mkutano huo (tetesi zinasema utafanyika ubalozni mida ya saa 10 jioni) yeye ameamua kutunanga. Madaraka huwafanya baadhi ya wenzetu kujisahau sana.

Tukiweka kando lugha ya kidiplomasia ya Ofisa ya Waziri Mkuu na kebehi za afisa ubalozi, la muhimu ni kwamba sasa Watanzania wote wanaoishi hapa Uingereza wamepewa fursa ya kuhudhuria mkutano huo muhimu na Waziri Mkuu. Binafsi nimefarijika sana kwa sababu nilijitahidi kulipigia kelele suala hilo kwenye kundi la Whatsapp la jumuiya ya Watanzania ambayo ipo katika hatua za awali za kuundwa, japo mapokeo hayakuwa ya kuridhisha (watu wanahimiza umoja lakini walikalia kimya 'ubaguzi' uliotaka kufanywa na baadhi ya maafisa ubalozi wetu hapo London). 

"Kelele" zangu hazikutokana na mie kutopewa mwaliko, kwa sababu hata kama ningekuwa miongoni mwa watu hao takriban 40 walioalikwa bado nisingehudhuria (na leo sintohudhuria...kwa sababu zangu binafsi). Nilipiga kelele kwa maslahi ya walio wengi ambao pengine kwa namna moja au nyingine walishindwa kupiga kelele hizo wao wenyewe. Sie wengine tuna kumbi kama hii ya blogu au makala magazetini ambazo ni rahisi kupiga kelele na watawala kutusikia. Lakini si kila mtu ni blogs au mwandishi wa makala. Ni matumaini yangu kuwa 'kelele' hizi zitawahamasisha wengi kutambua kuwa 'kelele dhidi ya jambo lisilofaa' sio uchizi, kusaka umaarufu au ukorofi. Marehemu Kighoma Ali Malima aliwahi kutuusia kwamba "HAKI HAIPASWI KUOMBWA KAMA ZAWADI. HAKI HUDAIWA...KWA NGUVU IKIBIDI."

13 May 2016

Ubalozi wa Tanzania hapa Uingereza umeingia lawamani kufuatia uamuzi wake wa 'kuwabagua' baadhi ya Watanzania wanaoishi nchi hapa na kuwanyima fursa ya kuhudhuria mkutano unaotarajiwa kufanyika kesho kati ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa na Watanzania wanaoishi hapa.

Kwa kawaida, viongozi wa kitaifa wanapokuja hapa kutoka huko nyumbani huongea na Watanzania wanaoishi hapa, na utaratibu uliozoeleka ni kutangaza tarehe, mahala na muda wa mkutano, kinyume na hali iliyojitokeza sasa ambapo inaelezwa kuwa kuna kikundi kidogo tu cha watu walioteuliwa kukutana na Waziri Mkuu Majaliwa.

Blogu hii ilifanya jitihada za kuwasiliana na Watanzania kadhaa wa hapa, na ukiweka kando wachache waliosema kuwa wasingeenda katika mkutano huo hata kama wangealikwa, wengi wao walilaumu kitendo hicho cha ubalozi kuteua kundi la watu wachache, ambapo wala haifahamiki wachache hao waliteuliwa kwa vigezo gani.

Baadhi ya waliohojiwa na blogu hii walieleza kuwa huenda "ubalozi huo ni jipu, na umeamua kuteua kundi la watu wachache ili kuepusha uwezekano wa mtu 'asiyejulikana' kukurupuka na kumfahamisha Waziri Mkuu kuhusu malalamiko yanayouhusu ubalozi huo (kama kweli yapo)."

Kadhalika, ilielezwa kuwa kitendo cha ubalozi huo kufanya 'ubaguzi' huo kinaweza kuijiengea serikali ya Awamu ya Tano ya Rais John Magufuli taswira mbaya, kwamba "Waziri Mkuu amekwepa kuongea na Watanzania kwa wingi au uwazi na badala yake anakutana na kikundi kidogo cha wateule wachache."

Vilevile, kitendo hicho kinaweza kumtengenezea mazingira magumu Balozi mpya wa Tanzania nchi hapa, Dkt Asha-Rose Migiro, iwapo 'walionyimwa fursa ya kuhudhuria mkutano huo' watabaki na mtizamo kuwa "mnatutenga wakati wa ziara za viongozi wa kitaifa basi nasi twawatenga katika maisha yetu ya kila siku."

" Au ndio yale ya Bunge Dodoma kwamba halirushwi live, basi sasa hata viongozi wetu wakuu wakija hapa, badala ya kukutana nasi kwa uwazi na wingi, fursa hiyo inatolewa kwa wateule wachache tu...kwa maslahi binafsi."

Wakati ubalozi hauwezi kukwepa lawama kwa vile kimsingi wenyewe ndio wenye mamlaka ya kufanya maandalizi ya mkutano huo, haieleweki kwanini 'jumuiya kuu mbili za Watanzania hapa Uingereza,' Kikosi Kazi na Kamati ya Mpito hazijafanya jitihada zozote kupigia kelele kuhusu kasoro hiyo. Badala yake, kila upande umekuwa ukiutuhumu upande mwingine 'kutumiwa na Ubalozi kwa maslahi binafsi.'

Awali, jana kulipatikana kipande cha sauti kilichorekodi sehemu ya kipindi cha Jahazi cha Clouds FM ya huko nyumbani, ambapo waendesha kipindi walijadili kwa ufupi kuhusu kasoro hiyo ya Waziri Mkuu kuandaliwa mkutano wa kuongea na idadi ndogo tu ya Watanzania, katika utaratibu usio wazi. Bonyeza hapa chini kusikiliza
Hadi wakati blogu hii inakwenda mitamboni, hakuna taarifa yoyote rasmi kutoka kwa ubalozi au makundi makuu mawili yanayowakilisha Watanzania hapa, kuhusu kwa mfano mkutano huo utafanyika lini, wapi na muda gani.

Hata hivyo, baadhi ya waliohojiwa walionyesha matumaini kuwa inawezekana Waziri Mkuu haelewi kuhusu 'usanii unaofanywa na ubalozi,' na akipata taarifa atauagiza ubalozi huo kufanya maandalizi ya kuwezesha Watanzania wengi zaidi kuhudhuria mkutano huo.

6 May 2016

Bila shaka matokeo ya utafiti huu yatawashangaza watu wa nchi nyingine, lakini sio sie Watanzania, ambao tumebainika kuwa watu wanafiki zaidi kuliko wote duniani. Sio jambo la kushangaza kwa sababu unafiki umekuwa sehemu ya utamaduni wetu.

Na mfano mwepesi wa unafiki wetu ni kuhusu uamuzi wa serikali kuipiga marufuku video ya msanii Snura iitwayo 'Chura' ambayo ilivuka mipaka ya ustaarabu. Awali, watu wengi waliishutumu Serikali kwa kuruhusu video hiyo 'chafu' kuonyeshwa ilhali vikao vya bunge vikizuiwa kuonyeshwa 'live.' Well, japo bunge laendelea 'kufichwa,' lakini serikali imejitutumua na kipiga kufuli video ya 'Chura.'

Lakini hatua hiyo imewakera baadhi ya wenzetu. Wengine wanadai serikali ina vitu muhimu zaidi vya kufanya badala ya kufungia video. Wengine wanadai mbona kuna video chafu zaidi za 'akina Rihanna' kuliko hiyo ya Chura. Wengine wanakwenda mbali na kudai kuwa alichofanya Snura na hao mabinti wa kwenye video ni UBUNIFU. Really?????

Twende kwenye maisha yetu ya kila siku. Tuchukulie mfano vifo. Utakuta watu wanasubiri mpaka mtu afe ndio waanze kumwagia sifa, "Oh marehemu alikuwa mtu mzuri sana, oh marehemu alikuwa mwema sana...RIP...RIP..." Hii tabia ya kuwapenda watu wakifa lakini kuwachukia walipokuwa hai ni nini kama sio UNAFIKI? Angalia Marehemu Kanumba alivyoandamwa wakati wa uhai wake. Msanii aliyefanya kazi kubwa kabisa kuiinua medani ya filamu za Kitanzania aliandamwa mfululizo na hili na lile, huku watu wasio na vipaji ya kitu chochote kile wakigeuka mahakimu na majaji dhidi ya kipaji cha msanii huyo. 

Tuangalie huko mitaani tunakoishi na 'makazi yetu mapya' mitandaoni. Huko mitaani, wenzetu wenye umuhimu mkubwa kwa jamii - madaktari, manesi, walimu, nk -  hawapewi heshima kubwa kulinganisha na wanayopewa wahalifu kama wauza madawa ya kulevya au wabadhirifu serikalini. Twaita wauza unga WAZUNGU WA UNGA, na wabadhirifu twawaita MAPEDEJEE, VIBOSILE, VIGOGO, na majina mengine ya kuwatukuza, ilhali jina lao stahili ni WAHALIFU. 

Nenda mtandaoni, kwa mfano Instagram. Ukiacha wasanii wetu na watu wengine muhimu, watu maarufu zaidi katika mtandao huo kwa Tanzania ni wale wenye kuongoza makundi ya matusi, picha za utupu, majungu, na madudu kama hayo. Sio kwamba hawa 'wameroga' ili kuwa maarufu. Hapana. Umaarufu wao unatokana na Watanzani wengin kupenda vitu hivyo: picha za utupu, majungu, nk.

Angalia wakati wa uchaguzi. Wanasiasa wetu hujiweka karibu kabisa na wananchi. Si ajabu kuona mwanasiasa akiwasalimia wananchi kwa kupiga magoti 'kwa heshima' wakati anaomba kura.Subiri ashinde uchaguzi. Humsikii japo akicheka au kuzomea bungeni. Unaweza kuhisi kuwa asilimia kuwab ya wabunge wetu wanatoka majimbo ya nchi kama Uingereza au Marekani, ambazo zina matatizo machache kwa wapigakura, kwani haiingii akilini kwa mbunge ambaye jimbo lake lina matatizo lukuki awe haonekani bungeni unless kwenye kukusanya posho tu, na akitokea bungeni, si ajabu kuona amepigwa picha huku kachapa usingizi (labda alishindwa kulala kutokana na kuzongwa na mawazo kuhusu jimbo lake?)

Anyway, turudi kwenye utafiti unathibitisha tulivyobobea kwa unafiki. Watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Nottingham cha hapa Uingereza waliendesha utafiti wa kupima kushamiri kwa ukiukwaji wa kanuni katika nchi 159 duniani, wakitumia takwimu za kutoka mwaka 2003 kuhusu ubadhirifu katika siasa, ukwepaji kodi na rushwa.

Twende tena mtaani. Kuna suala la ushoga ambalo taarifa zinaeleza kuwa unakua kwa kasi huko nyumbani. Juzi kuna shoga mmoja kafiwa Dar, na inaelezwa kuwa takriban kila mtu maarufu jijini hapo hakukosekana msibani. Lakini sio katika msiba huo tu, nenda Instagram halafu angalia akaunti za mashoga na idadi ya 'followers' wao. Hivi yawezekanaje kama 'ushoga sio tu ni laana bali pia ni kinyume cha sheria za Tanzania,' then shoga awe na 'followers' zaidi ya laki moja? Kwanini kila shughuli ya mastaa wetu haiwi kamili bila uwepo wa mashoga wa 'kukata viuno' kwenye shughuli hiyo?


Habari kamili kuhusu utafiti huo ipo HAPA na kuna MAKALA HII katika gazeti la kila wiki la RAIA MWEMA Toleo la wiki hii imeandika kwa kirefu kuhusu suala hilo

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.