16 Aug 2016


NDOTO yangu ya muda mrefu utotoni ilikuwa utabibu. Moja ya sababu zilizonipa ndoto hiyo ni uuguzi (unesi) wa dada yangu, ambao ulinifanya nimtembelee kazini kwake (hospitalini) mara kwa mara. Kila nilipomtembelea, nilishuhudia wagonjwa mbalimbali wakiwa wamekabidhi afya na uhai wao mikononi mwa madaktari na manesi. Nikanuwia kuwa nitakapomaliza elimu ya msingi na kufanikiwa kuingia sekondari, nitasoma masomo ya sayansi ili baadaye niwe daktari.
Kwa bahati nzuri nilifaulu darasa la saba na kuchaguliwa kujiunga sekondari ya kutwa ya Kilombero, Ifakara. Mimi na wanafunzi wenzangu tuliofaulu mwaka huo ndio tulikuwa wanafunzi waanzilishi wa shule hiyo maarufu kwa jina la Kilombero Day.
Kujiunga na shule hiyo kuliisogeza karibu ndoto yangu ya udaktari, sio tu kwa vile nilipata fursa ya kusoma masomo ambayo yangeweza kunisaidia kusomea udaktari lakini pia shule hiyo ilikuwa jirani tu na chuo cha waganga wasaidizi (MATC), kilichokuwa katika hospitali ya Mtakatifu Francis.
Hata hivyo, nilikabiliwa na vikwazo viwili. Kwanza, shule hiyo mpya ilikuwa na uhaba mkubwa wa nyenzo mbalimbali za kitaaluma, vitabu vya kiada na maabara. Kikwazo cha pili kilikuwa katika uwezo wangu binafsi. Somo la hisabati lilikuwa ‘mgogoro’ tangu siku ya kwanza, na somo la Fizikia likatokea kuwa gumu kuliko yote. Wakati huo, nilishafahamu kuwa mkondo wa udaktari ni Fizikia, Kemia na Baiolojia (PCB) na Hisabati kidogo.
Kufupisha simulizi, nilipohitimu kidato cha nne nilipata Daraja la Kwanza huku nikiwa na alama A ya Kemia, C ya Baiolojia na F ya Fizikia. Ukichanganya na D ya Hisabati, mkondo wa PCB uligoma.
Nilipochaguliwa kidato cha tano, nikataka kuikwepa Fizikia kwa kusoma Kemia, Baiolojia na Jiografia (CBG), ambayo ingeweza kunifikisha katika azma yangu ya kusomea udaktari. Nikakumbana na kikwazo cha kuchukua tena Hisabati (Basic Mathematics) kama somo la ziada na kumbe Kemia ya Kidato cha Tano na Sita haikuwa nyepesi kama ile niliyopata alama A kidato cha nne. Kipengele cha Physical Chemistry kilikuwa ni kama Fizikia zaidi kuliko Kemia na hisabati juu. Nikaamua kuzika ndoto yangu ya udaktari, nikachukua mkondo wa Historia, Jiografia na Kiingereza (HGL) na somo la ziada la Siasa.
Lengo la simulizi hiyo sio kuelezea safari yangu ya kitaaluma au ndoto yangu hiyo ya udaktari iliyokufa kifo cha asili bali kama kielelezo mwafaka cha kukosoa uamuzi wa serikali kulazimisha masomo ya sayansi kwa wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha nne.
Sitaki kujigamba kuhusu kiwango changu cha elimu, lakini ukweli ni kwamba licha ya kufanikiwa kuhitimu shahada tatu nikisaka ya nne kila ninapokutana na hata mhitimu wa kidato cha sita tu wa mkondo uliohusisha Fizikia na Hisabati (kwa mfano PCB au PGM), ninampa heshima zote. Sababu nyepesi ni kwamba ameweza kile kilichonishinda.
Na hadi muda huu, nikiwaona wanafunzi wa shahada ya kwanza katika masomo ya sayansi kama vile uhandisi, ninawaheshimu mno. Kwa kifupi tu, masomo ya sayansi yanahitaji mtu mwenye akili zaidi. Japo haimaanishi tunaosoma kozi zisizo za sayansi ni ‘patupu kichwani,’ ukweli ni kwamba angalau kozi zetu zina ahueni fulani.
Sasa serikali inapokurupuka na uamuzi wa kulazimisha masomo ya sayansi kwa wanafunzi wote, kinyume cha utaratibu uliopo ambapo wanafunzi wa sekondari wanaingia kidato cha tatu wanapewa uhuru wa kuchagua mkondo wanaotaka (hasa kwa kuzingatia ndoto zao kitaaluma na uwezo wao kimasomo).
Huu ni udikteta wa kitaaluma, kumlazimisha mwanafunzi kusoma kitu asichotaka. Na hapa suala sio kutaka tu bali pia kuna suala la uwezo wa kumudu masomo ya sayansi. Na kingine ni kuwabebesha wanafunzi mzigo wasiostahili.
Sababu iliyotolewa na serikali kupitia Waziri wa Elimu, Teknolojia, Sayansi na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, kuwa hivi sasa Tanzania imedhamiria kuingia kwenye uchumi wa kati ambao ni wa viwanda, na hivyo suala la sayansi haliwezi kuepukwa (kwa sababu ni wakati sasa wa kuwa na wataalamu wengi wa fani za sayansi watakaoweza kutosheleza mahitaji ya sekta ya viwanda nchini) haina mashiko.
Nihitimishe makala hii kwa kumshauri waziri huyo msomi kurejea mada kama ‘reactance’ na ‘boomerang effect’ kwenye saikolojia na kuzihusisha na uamuzi huo wa serikali na athari zake.
Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

13 Aug 2016

14026664_162506520845816_426045486_n
Leo ni siku ya kuzaliwa ya mwana-hiphop mahiri na lejendari nchini Tanzania, Fareed Kubanda a.k.a Fid-Q. Na katika kuadhmisha birthday yake, msanii huyu ambaye sio tu amedumu "kwenye fani" kitambo bali pia ni miongoni mwa waasisi wa Swahili Hip-Hop.

 Kwangu, Fid-Q sio tu ni msanii maarufu kabisa huko nyumbani Tanzania na katika Swahii hip-hop duniani, bali ni mmoja wa watu ambao wamkuwa wakinipatia sapoti kubwa katika kazi zangu za uandishi wa vitabu. Na ndio maana kwa kutambua mchango wake huo, alikuwa mtu wa kwanza kupata nakala dhahiri ya kitabu changu kuhusu taaluma ya uafisa usalama wa taifa (ushushushu) kama inavyoonyesha pichani chini.

 Jana niliuliza huko kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter kuhusu wimbo gani wa Fid-Q unawavutia zaidi mashabiki wake. 



Jibu jepesi lilikuwa "kila wimbo wake unavutia." Nimesikiliza hii track mpya ya 'SUMU.' Imesheheni kauli nyingi za busara. Nitamwomba Fid-Q anitumie mashairi ya wimbo hu ili kuwaletea ninyi wasomaji uchambuzi zaidi ya wimbo huo. Lakini hata bila uchambuzi, kwa kuusikia tu, utaafikiana nami kuwa umeshehenu busara tele.

 Na hiki ndio kinachomfanya Fareed aendelee kuwa mmoja wa wasanii wachache na adimu kabisa Tanzania sio tu kuwa waasisi wa fani bali pia wasiochuja: kuwa na nyimbo zenye ujumbe usiochuja. Kama ingekuwa ni muziki wa bendi basi tungelinganisha na timeless tunes za kina Mbaraka Mwinshehe, Marijan Rajabu, Bitchuka, Shaban Dede, nk ambao tungo zao zilituvutia tangu tukiwa utotoni (kwa tulozaliwa enzi hizo) na ni tamu hadi leo. Na utamu so wa ladha tu bali pia relevance ya ujumbe uliomo. 

 Basi nisiandike 'gazeti,' bali nimtakie Fareed heri ya siku yake ya kuzaliwa, na kumtakia kila la heri na fanaka maishani, na kumshukuru kwa sapoti yake kwa kazi zangu, na kumpongeza kwa kutupatia 'SUMU.' Isikilize hapa chini

11 Aug 2016

Makala hii maalum ya sauti inazungumzia kitabu changu kuhusu taaluma ya uafisa usalama wa taifa (ushushushu) ambacho sasa kinapatikana katika nakala dhahiri (hard copy). Makala hii inaeleza kuhusu nini kilichonisukuma kuandika kitabu hiki na pia inaeleza kwa undani yaliyomo kitabuni.




Check this out on Chirbit

9 Aug 2016

Kwa mujibu wa takwimu, asilimia 48 ya Waingereza wanajitambulisha kama wasio na dini.

Na hapa Uskochi ninapoishi ndio panapngoza kwa idadi ya 'waliovunja uhusiano na Mungu' kwa idadi ya asilimia 36.

Kwa upande mwingine, Ireland ya Kaskazini ndio sehemu ya UK inayoongoza kwa kuwa na idadi ndogo (asilimia 10 tu) ya wasiomtambua Mungu/wasio na dini/wapagani.

Ramani kamili ni hii hapa chini

Null

Je watambua ni nchi gani duniani ambazo 'upagani' ni kosa lenye adhabu ya kifo? Hebu chemsha bongo kidogo kwa kuzitambua nchi hizo kwenye ramani ifuatayo (kidokezo kipo chini ya picha)

1


·        Afghanistan
·        Iran
·        Malaysia
·        Maldives
·        Mauritania
·        Nigeria
·        Pakistan
·        Qatar
·        Saudi Arabia
·        Somalia
·        Sudan
·        United Arab Emirates

·        Yemen



5 Aug 2016


Kitabu kuhusu taaluma ya uafisa usalama wa taifa (ushushushu) kinapatikana kwenye maduka ya vitabu sehemu mbalimbali nchini Tanzania.

Kwa wanunuzi wa rejareja, kitabu hiki kinapatikana katika maduka ya vitabu yafuatayo


 Bei ya rejareja ni sh 15,000. 

Pia fursa hii ni kwa wenye vibanda vya kuuza magazeti au wachuuzi wa bidhaa za mkononi. Bei ya jumla kwa kila kitabu ni sh 8,400.

           KARIBUNI SANA


30 Jul 2016


Kwa rafiki zangu huko Facebook, nadhani mwakumbuka stori moja niliyowasimulia kitambo kuhusu rafiki yangu mmoja, Mtanzania, ambaye kitaalua ni mfamasia, lakini ameamua kuweka kando taaluma hiyo na kujikita katika kilimo.

Baadhi ya marafiki zangu waliomba mawasiliano nae, na takriban wote walinipa mrejesho kuwa wamevutiwa sana na jitihada za @d33dat, ambaye binafsi ninamchukulia kuwa ndio mwasisi wa falsafa ya "Kilimo kama Ajira."

Angalia mahojiano mafupi kati yake na kipindi cha Dira ya Dunia cha BBC Swahili yaliyofanyika jana Ijumaa Julai 29, 2016.



24 Jul 2016


Jana Julai 23, 2016 Rais Dokta John Magufuli alichaguliwa kwa asilimia 100 kuwa Mwenyekiti mpya wa Taifa wa chama tawala CCM, na mtangulizi wake, Rais Mstaafu, Jakaya Kikwete, kung'atuka rasmi. Ufuatao ni uchambuzi wa kina kuhusu mabadiliko hayo ya uongozi wa juu kabisa wa chama hicho kikongwe, hasa fursa na changamoto kwa Mwenyekiti mpya Magufuli. Karibuni
Check this out on Chirbit


Naomba kuwasilisha ujumbe husika kama nilivyotumiwa. Ukishasoma, usikose kutahadharisha na mwenzako. Kwa kufanya hivyo sio tu itaepusha watu kuingia kwenye mtego wa tapeli huyo lakini pia itasaidia kuwezesha atiwe nguvuni


23 Jul 2016

Munich-locator-600px
Ujerumani imekumbwa na janga jingine baada ya lile la siku nne ambapo kijana mmoja, mhamiaji kutoka Afghanistan, aliwashambulia abiria kwenye treni kwa kutumia shoka na kujeruhi watu wanne. 

Kijana huyo, Riaz Khan Ahmadzai (au Muhammad Riyad, kwa jina jingine), aliyekuwa na umri wa miaka 17, na aliyewasili Ujerumani mwaka jana kama mtoto anayesaka ukimbizi, aliuawa kwa kupigwa risasi na polisi.
Katika tukio lililotokea jana, watu 10 wameuawa hadi wakati ninaandika makala hii na wengine kadhaa kujeruhiwa baada ya shambulio la risasi katika mgawaha wa McDonald kwenye kitongoji cha biashara katika jiji la Munich.
Awali, ilikuwa haifahamiki idadi kamili ya waliofanya shambulio hilo japo taarifa za awali zilitaja wahusika kuwa watatu. Licha ya shambulio hilo kwenye mgahawa huo ulio kwenye duka kubwa (mall), ilidaiwa kuwa milio ya risasi ilisikika pia maeneo mengine ya Munich.
Kulikuwa kuna theories tatu - mbili zenye uzito na moja yenye uzito mdogo kiasi - kuhusu nani hasa alihusika na tukio hilo. Theories hizo ni kama ifuatavyo.

Theory ya kwanza: shambulio hilo ni kazi ya magaidi, sanasana ISIS

Imekuwa ni kawaida sasa kwa nchi za Magharibi kwamba kunapotokea tukio lolote la kigaidi, hisia za kwanza ni usual suspects, yaani kama sio ISIS basi ni Al-Qaeda. Haya ndio makundi mawili ya kigaidi yanayoziandama mno nchi za Magharibi. Na kwa sasa, ISIS ndio inaongoza kwa mfululizo wa mashambulizi ilhali Al-Qaeda 'imekuwa kimya' kitambo sasa.

Hisia kwamba wahusika katika shambulio hilo walikuwa ISIS (au Al-Qaeda) ni, kwanza, tukio la majuzi la huyo kijana aliyefanya shambuli kwa kutumia shoka ambalo nimelieleza mwanzoni mwa makala hii. 

Pili, ni ukweli kwamba ISIS imekuwa ikifanya jitihada kubwa kuishambulia Ujerumani na nchi nyingine za Magharibi. Kama ilivyo kwa Uingereza, wataalamu wa usalama wa kimataifa wanaeleza kuwa shambulio la ISIS kwa Ujerumani sio suala la "iwapo litatokea" bali "lini litatokea." 

Tatu, ISIS walishangilia tukio hilo la Munich, katika akaunti yao ya Telegram, kama inavyoonyesha pichani chini
ISIS rejoice in Munich attack

Hata hivyo, theory hii kuwa wahusika ni ISIS ilikabiliwa na 'pungufu' hili: ilielezwa kuwa moja ya maiti hizo 9 ni ya mmoja wa wahusika wa tukio hilo. Hiyo ilikuwa na maana gani? Ni kwamba, magaidi wa ISIS na wenzao wenye mrengo kama wao, hupania kuuawa na sio kujiuwa. Wanaamini kuwa kwa kuuawa - badala ya kujiuwa - wanakuwa wamejitoa mhanga kwa ajili ya imani yao. Kama sio kuuawa kwa kupigwa risasi basi kifo kitokane na kujilipua kwa bomu la kujitoa mhanga.

Lakini kifo cha mtu huyo anayedhaniwa kuwa mmoja wa wahusika wa shambulio hilo hakikutokana na kupigwa risasi na polisi au yeye kujilipua. Sababu pekee ya kifo inaweza kuwa alijipiga risasi mwenyewe, mbinu ambayo sio chaguo la magaidi wa ISIS na wenzao.

Theory ya pili: Wahusika walikuwa kikundi cha wabaguzi wa rangi wenye msimamo mkali dhidi ya Waislam, wakimbizi na raia wa kigeni

Jana ilikuwa ni kumbukumbu ya miaka mitano ya shambulio kubwa la kigaidi lililofanyika huko Utoya, nchini Norway, Julai 22 mwaka 2011 ambapo mbaguzi wa rangi mwenye msimamo mkali, Anders Behring Breivik, aliwapiga risasi na kuwauwa watu 77.
Wachunguzi wa masuala ya usalama walieleza kuwa kulikuwa na uwezekano kwamba shambulio hilo la Munich lilifanywa na kikundi cha kibaguzi chenye mrengo mkali kama maadhimisho ya tukio hilo la Norway, na pengine kama kumwenzi Breivik ambaye ni 'shujaa' kwa vikundi vya wabaguzi wa rangi.
Kingine kilichoipa uzito theory hii ni ukweli kwamba mmoja wa wahusika wa shambulio hilo alisikika akisema kuwa yeye ni Mjerumani asilia, na akawatukana wahamiaji nchini humo. Wataalamu wa lafidhi walieleza kuwa sio rahisi kwa mtu asiye mzaliwa wa Ujerumani kuwa na lafidhi iliyotumiwa na mtu huyo.

Theory ya tatu, wahusika sio watatu bali mtu mmoja tu aliyekuwa anayesumbuliwa na matatizo ya akili

Katika kile kinachotafsiriwa kama unafiki, 'mzungu' akiuwa watu kadhaa, maelezo yatakuwa "mtu mwenye matatizo ya akili." Uthibitisho wa hivi karibuni ni maelezo kuhusu mtu aliyemuuwa mbunge Jo Cox wa hapa Uingereza hivi karibuni. Ilielezwa kuwa muuaji huyo "alikuwa na historia ya matatizo ya akili."
Laiti angekuwa Muislam au Mwarabu basi maelezo hapo yangeelemea zaidi kuhusu Uislam wake, na wabaguzi wasingekawia kudakia hoja kuwa dini hiyo ni tishio kwa ustawi wa mataifa ya Magharibi.

Ilielezwa kuwa mtu huyo niliyemwelezea katika theory ya pili, licha ya kudai yeye ni Mjerumani na kuwatukana wahamiaji, pia alieleza kuwa ni mgonjwa wa akili na yupo kwenye matibabu.

Taarifa rasmi ya polisi kuhusu mhusika

Baadaye, polisi wa Munich waliitisha mkutano na waandishi wa habari na kueleza kuwa uchunguzi wao umethibitisha kwamba aliyefanya shambulio hilo ni kijana mwenye umri wa miaka 18, Mjerumani mwenye asili ya Aljeria, na alihamia nchini humo miaka miwili iliyopita.

Kama taarifa hiyo ya polisi haina mapungufu, ukweli kwamba siku 4 zilizopita mhamiaji kutoka Afghanistan alifanya shambulio la kigaidi kwa kutumia shoka na kujeruhi watu wanne kabla ya kuuawa, na jana mhamiaji mwingine kutoka Iran, mwenye umri wa mwaka mmoja tu zaidi ya huyo wa majuzi, naye amefanyanya shambulizi na kuuwa watu 10 (hadi wakati naandika makala hii), chuki dhidi ya wageni inaweza kuongezeka maradufu.

Ikumbukwe kuwa Ujerumani imekuwa ikipokea idadi kubwa ya wakambizi miongoni mwa nchi za Magharibi. Licha ya upinzani mkali, hususan kutoka kwa makundi ya kibaguzi yenye mrengo mkali, Kansela Angela Markel amekuwa mstari wa mbele sio tu kuhamasisha nchi za Magharibi zipokee wakimbizi, bali pia ameruhusu idadi kubwa kabisa ya wakimbizi kuingia na kuishi katika nchi hiyo.

Kama kuna 'nafuu' kidogo, basi ni hiyo asili yake ya Iran, nchi ambayo ni nadra kuzalisha magaidi. Pia ukweli kuwa alijiuawa mwenyewe inaweza kuendana na hiyo theory ya pili hapo juu kuwa magaidi wa ISIS na wenzao huwa hawajiuwi kwa kujipiga risasi, huuawa kwa kupigwa risasi au kujilipua wenyewe, na kwa kufanya hivyo huwa wamejitoa mhanga kwa ajili ya imani yao.

Hata hivyo, huo u-Iran wake unaweza kuwapa nguvu wabaguzi wa rangi kuendeleza upinzani wao dhidi ya serikali ya Kansela Markel kuruhusu ujio wa wakimbizi nchini humo, ambao wanatizamwa kama 'magaidi watarajiwa.'

Endelea kutembelea blogu hii kwa uchambuzi wa kina wa mada mbalimbali kama hii inayohusu masuala ya intelijensia, na nyinginezo.







21 Jul 2016


Julai 15 mwaka huu, serikali ya Uturuki ilinusurika kupinduliwa katika jaribio la mapinduzi liliyodumu kwa chini ya masaa 12. Tayari watu zaidi ya 60,000 aidha wamekamatwa, wamesimamishwa au wamefukuzwa kazi kwa tuhuma za kuhusiana na jaribio hilo lililofeli.

Jaribio la mapinduzi lilitokeje?

Awali daraja kuu katika mkondo wa Bosphorous liliwekewa vizuizi na kundi la wanajeshi wakitumia vifaru, na wakati huohuo ndege za kivita zilikuwa zikiruka katika anga la mji mkuu wa nchi hiyo, Ankara, huku milio ya bunduki ikisikika sehemu mbalimbali.

Baadaye, Waziri Mkuu Binali Yildrim, alitangaza kwamba kulikuwa na jaribio linaloendelea la kuipindua serikali.

Muda mfupi baadaye, kikundi cha wanajeshi kilitangaza kupitia radio ya taifa kuwa jeshi limechukua madaraka kutoka kwa Rais Recep Tayyip Erdogan ili kulinda demokrasia.

Kisha likafuatia tangazo la hali ya hatari (curfew), sheria za kijeshi (marshall law) na maandalizi ya katiba mpya.

Rais Erdogan ambaye alikuwa likizoni alifanikiwa kuwasihi wananchi waingie mtaani kupinga mapinduzi hayo. Alitoa wito huo kwa kutumia app ya Facetime ya iPhone na kuonyeshwa live kama inavyoonekana pichani chini.




Katika usiku huo, vituo vya televisheni vilivamiwa na wanajeshi, milipuko kadhaa ilisikika sehemu mbalimbali za Ankara na Istanbul, abaadhi ya waandamaji walishambuliwa na wanajeshi na kuuawa au kujeruhiwa, jengo la bunge na ikulu zilishambuliwa, helikopta ya jeshi ilitunguliwa, na mnadhimu wa jeshi kuchukuliwa mateka.


Jaribio la mapinduzi liliishaje?

Ili jaribio hilo la mapinduzi lifanikiwe, wahusika walihitaji sapoti ya sehemu kubwa zaidi ya jeshi badala ya kikundi kidogo tu, na sapoti ya wananchi mtaani. Yote mawili hayakutokea. Kana kwamba hiyo haikutosha, vyama vya upinzani navyo vilijitokeza kulaani jaribio hilo.

Kufikia Jumamosi asubuhi -  chini ya masaa 12 baada ya tangazo la mapinduzi - baadhi ya wanajeshi walioshiriki katika jaribio hilo walianza kujisalimisha.

Soldiers involved in the coup surrender on the bridge over the Bosphorus in Istanbul (16 July)



Kadhalika, polisi walifanikiwa kurejesha sehemu mbalimbali muhimu mikononi mwa dola kutoka kwa waasi. Kufikia Jumamosi mchana, mitaa ilikuwa imesheheni wananchi wakilaani jaribio hilo la mapinduzi na kuunga mkono serikali ya Erdogan.


Kwanini jaribio hili la mapinduzi lilifeli?

Kwanza, jaribio hilo halikuwa na sapoti ya kutosha ndani ya jeshi la nchi hiyo. Kilichoonekana ni kikundi kidogo tu cha wanajeshi kilichojumisha wanajeshi wapya, pasipo uwepo wa viongozi waandamizi wa jeshi la nchi hiyo.

Pili, jaribio hilo halikuwa na spaoti ya wananchi. Mara baada ya Rais Erdogan kuwataka wananchi waingie mtaani kupambana na jaribio hilo, ikageuka kuwa mapambano kati ya wanajeshi na wananchi, kitu ambacho kwa vyovyote kingeathiri 'uhalali' wa mapinduzi hayo.

Tatu, wahusika wa jaribio hilo la mapinduzi kushindwa kudhibiti njia zote za mawasiliano kati ya viongozi wakuu wa serikali na wananchi, kwa mfano vituo vya televisheni na redio. Mwelekeo wa jaribio hilo la mapinduzi ulibadilika kwa kiasi kikubwa baada ya Rais Erdogan kuonekana kwenye kituo kimoja cha televisheni akiwataka wananchi waingie mtaani.

Nne, Uturuki ni taifa lenye asilimia kubwa ya watu wenye kipato cha kati na cha juu. Ni vigumu sana kwa taifa lenye wananchi wa aina hii kuunga mkono mapinduzi. Ni rahisi kwa mapinduzi kuungwa mkono katika nchi masikini ambapo mara nyingi 'chuki' dhidi ya serikali huwa kubwa.

Jaribio hilo la mapinduzi lilionekana kufeli bayana baada ya Rais Erdogan kurejea Instanbul na kuhutubia katika uwanja wa ndege wa Ataturk.

Arriving at Ataturk airport in Istanbul, President Erdogan was greeted by hundreds of supporters


Hali ikoje sasa?

Idadi halisi ya waliokamatwa, kusimamishwa kazi au kutimuliwa kazi na hatua nyingine zilizochukuliwa ni kama ifuatavyo

  • Watumishi 300 wa Wizara ya madini wametimuliwa.
  • Watumishi 184 wa Wizara ya Forodha wametimuliwa.
  • Waandamizi wanane wa Bunge wameondolewa.
  • Waturuki wote wanapaswa kuwa na nyaraka za ziada wanapofanya safari nje ya nchi.
  • Watumishi 86 wa taasisi ya udhibiti na usimamizi wa mabenki wametimuliwa.
  • Watumishi 51 wa Soko la Hisa wametimuliwa.
  • Majaji 140 wa Mahakama Kuu wametumiwa hati za kukamatwa.
  • Watumishi 15,200 wa Wizara ya Elimu wametimuliwa.
  • Vyombo vya habari 24 vimefutiwa hati za usajili.
  • Watu 429 wa taasisi ya umma ya masuala ya dini (Diyanet) wameondolewa.
  • Walimu binafsi 21,000 wamefutiwa leseni zao.
  • Watumishi 393 w Wizara ya Familia na Sera za Jamii wametimuliwa.
  • Watumishi 257 katika ofisi ya Waziri Mkuu wametimuliwa.
  • Wakuu (deans) 1577 wa vyuo vikuu wametakiwa kujiuzulu.
  • Magavana 33 wametimuliwa.
  •  Watumishi 9,000 wa Wizara ya Mambo ya Ndani wametimuliwa.
  • Maafisa Usalama wa Taifa 180 wamesimamishwa kazi
  • Majaji 2,745wametimuliwa.
  • Watumishi wa umma milioni tatu wamezuwia kwenda likizo.
  • Mjadala kuhusu kurejeshwa kwa hukumu ya kifo umeanza, na Rais Erdogan ametanabaisha kuwa pindi bunge likiridhia kurejeshwa kwa hukumu hiyo basi wote waliohusika na jaribio hilo la mapinduzi watahukumiwa kifo.
  • Maafisa 1,500 wa Wizara ya Fedha wametimuliwa.
  • Majenerali na maadmirali 85 ni miongoni mwa maelfu ya wanajeshi waliokwishakamatwa. Pia zaidi ya polisi 8,000 wamekamatwa, wametimuliwa au wamesismamishwa kazi.
Mashushushu wa Uturuki walikuwa wapi wakati mapinduzi hayo ynaandaliwa na hadi yakakaribia kufanikiwa?

Makala hii inahusu hasa swali hilo hapo juu, kwa moja ya kazi kuu za Idara ya Usalama ya taifa lolote lile ni kutambua, kuzuwia na kudhibiti matishio ya usalama wa taifa, ikiwa ni pamoja na mapinduzi. Sasa wakati serikali ya Uturuki ikionekana kuchukua hatua kali dhidi ya watumishi mbalimbali wa umma ikiwa ni pamoja na kuwakamata, kuwasimamisha kazi na kuwatimua, ni idadi ndogo tu ya maafisa usalama wa taifa waliochukuliwa hatua (angalia juu nilipoandika kwa maandishi mekundu).

Lakini swali kubwa zaidi ni kwamba je Idara ya Usalama wa Taifa ya nchi hiyo, MIT, haikufahamu kuhusu mipango ya kufanyika kwa mapinduzi hayo, na kwanini?

Turudi nyuma kidogo. Oktoba mwaka jana, mhadhiri wa chuo kikuu cha Haifa , Israel, Norman Bailey, alieleza kwa uhakika kuwa jeshi la Uturuki linaweza kuchukua madaraka ya nchi hiyo iwapo litaona nchi inaelekea kusikofaa.

Kadhalika, Machi mwaka huu, wachunguzi wa masuala ya usalama wa Russia walionya kuwa jeshi la Uturuki lilikuwa likijiimarisha kisiasa, na hivyo kujenga msingi wa mapinduzi.

Baadaye mwezi huohuo, Michael Rubin wa taasisi ya American Enterprise, aliuliza "je Uturuki itakumbwa na mapinduzi?" na akajibu kwamba "isiwe jambo la kushangaza iwapo jeshi la Uturuki litajaribu kumng'oa (Rais) Erdogan na kuwatupa jela watu wake wa karibu."

Machi 30, jarida linaloheshimika la Foreign Affairs lilichapisha makala ya Gonul Tol, Mkurugenzi mwanzilishi wa Taasisi ya Mashariki ya Kati, kituo cha stadi za Uturuki, alieleza kuwa nchi hiyo ilikuwa ikikabiliwa na mapinduzi.

Kadhalika, mwanzoni mwa mwezi huu, Joseph Fitsanakis wa tovuti ya IntelNews alizungumzia kuhusu hali tete iliyokuwa ikiikabili Uturuki na kutanabaisha kuwa hakuna nchi katika eneo hilo ambayo ilikuwa 'haijatulia' kama Uturuki.

Pia, wachambuzi wa taarifa za kiusalama wa Marekani walikuwa wakihofia kitambo kuhusu hali ya usalama nchini Uturuki. Swali lilibaki kuwa lini kungetoa jaribio la mapinduzi na lingeongozwa na nani.

Sasa, kama wataalamu hao mbalimbali wa masuala ya usalama waliokuwa wakitegemea 'vyanzo vya wazi vya taarifa za kishushushu' (open sources) waliweza kutoa tahadhari kuhusu uwezekano wa jaribio hilo la mapinduzi, inatarajiwa kuwa mashushushu wa Uturuki pia walikuwa na tahadhari hiyo.

Kwa kuangalia 'sintofahamu' iliyoikumba serikali ya Rais Erdogan wakati wa jaribio hilo la mapinduzi, yayumkinika kuhisi kuwa idara ya ushushushu ya nchi hiyo nayo ilikuwa katika 'sintofahamu' pia. 

Na kuthibitisha kuwa taasisi hiyo haikuwa imejipanga vizuri, asuhuhi ya Julai 16 makao makuu yake yalishambuliwa na helikopta za jeshi pasipo upinzani wowote. 

Wakati serikali ikikabiliwa na jaribio la mapinduzi, mkuu wa idara ya ushushushu ya nchi hiyo, Hakan Fidan, alikuwa mafichoni.




Kuna sababu kuu tatu zinazoweza kueleza kwanini idara ya ushushushu ya nchi hiy, MIT, ilionekana kutokuwa na taarifa kuhusu jaribio hilo la mapinduzi na kushindwa kwake kulizuwia.

Kwanza, uwezo wa utendaji kazi wa taasisi hiyo ni duni, na kwa kiasi kikubwa umekuwa ukikuzwa na vyombo habari kuliko hali halisi. Taasisi hiyo inaelezwa kuwa yenyeurasimu mkubwa, yenye kutumia mbinu za kale, in uhaba mkubwa katika mtandao wake wa upatikanaji taarifa za kiusalama, sambamba na mapungufu katika uwezo wake kwenye uchambuzi wa taarifa za kiusalama.


Pili, kuchanganya siasa na taaluma ya ushushushu. Awali, taasisi hiyo ilikuwa ikijitegemea na kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia taaluma na utaalam wa ushushushu. Hata hivyo, tangu Erdogan aingie madarakani mwaka 2003, taasisi hiyo imekuwa kama chobo cha kisiasa cha AKP, chama tawala chenye mrengo wa kulia kidogo kidini kinachoongozwa na Erdogan.

Tatu, kwa takriban muongo mzima sasa, MIT imekuwa 'bize' zaidi na changamoto za matishio ya usalama kwa Uturuki kutoka nje, yaani tishio la kikundi cha kigaidi cha ISIS, harakati za uhuru za Wakurdi na wapiganaji wao wa PKK, kuibuka kwa taifa lisilo rasmi la Rajava huko Syria, na  hali tete ya usalama huko Iraki na Syria kwa ujumla. Changamoto hizo zimepeleka taasisi hiyo kuwekeza nguvu nyingi katika kukabiliana na matishio kutoka nje badala ya matishio ya kiusalama ya ndani ya nchi.


Kwa upande mwingine, kumekuwa na hisia kwamba huenda Erdogan alishirikiana na MIT kuruhusu wapinzani wa chama tawala na serikali ndani ya jeshi la nchi hiyo kufanya jaribio hilo la mapinduzi , lengo likiwa ni kuwa mapinduzi hayo yakishindikana (na lengo ni yashindikane) basi Erdogan awe na kila sababu na haki ya kuendesha taifa hilo kwa mkono wa chuma. Ikumbukwe kuwa kwa muda mrefu Erdogan amekuwa akifanya jitihada za kutaka taasisi ya urais wa nchi hiyo iwe ya kiutendaji kuliko sasa ambapo kinadharia mkuu wa serikali ni Waziri Mkuu.

Nimalizie makala hii kwa kuahidi kufanya uchambuzi mwingine kadri taarifa mbalimbali zitakavyopatikana. Kwa habari zaidi kuhusu masuala ya ushushushu, bonyeza hapo juu palioandikwa 'INTELIJENSIA,' sambamba na kusoma habari nyingine katika blogu hii.


Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.