23 Oct 2014

Makala yangu hii ilichapishwa katika jarifa la RAIA MWEMA Toleo la wiki iliyopita lakini 'nilizembea' kui-post hapa bloguni. Endelea kuisoma:

NIANZE kwa kuelezea matukio mawili, moja linaihusu Marekani na jingine laihusu Israel. 
Tukio la kwanza linahusu kujiuzulu kwa aliyekuwa mkuu wa moja ya idara za usalama za Marekani (zipo nyingi) ambayo ina dhamana ya ulinzi na usalama wa viongozi wakuu wa taifa hilo na familia zao, US Secret Service. 
Mkuu huyo, mwanamama Julia Piersons, alilazimika kujiuzulu baada ya tukio la hivi karibuni la kuhatarisha usalama wa Rais Barack Obama, kutokana na mtu mmoja, Omar Gonzalez, kuruka uzio wa Ikulu ya nchi hiyo akiwa na kisu, kabla hajadhibitiwa na maafisa wa Secret Service. 
Hatimaye tukio hilo lililotawala sana katika vyombo vya habari vya Marekani lilimfanya mwanamama huyo, shushushu mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka 30, kuitwa na kuhojiwa na kamati moja ya Bunge la Congress, na mwishowe alitangaza kujiuzulu. 
Licha ya ukweli kwamba mkuu huyo wa mashushushu hakuwa eneo la tukio, dhamira ilimtuma kuwa kama kiongozi wa taasisi yenye dhamana ya ulinzi wa viongozi wakuu wa nchi hiyo, anawajibika kwa uzembe au makosa ya watendaji wake. 
Piersons alikuwa kwenye wadhifa huo kwa takriban miezi 18 tu baada ya mtangulizi wake, Mark Sullivan, kulazimika kujiuzulu baada ya kashfa iliyohusisha baadhi ya maafisa wa Secret Service ‘kufumwa’ wakiwa na makahaba katika ‘msafara wa utangulizi’ (advance party) kabla ya ziara ya Rais Obama nchini Colombia, mwaka juzi. 
Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya ushushushu wanamuona Piersons kama mhanga tu wa mapungufu ya kimfumo na kiutendaji yanayoikabili taasisi aliyokuwa akiongoza. 
Wanadai kuwa alikuwa akikabiliwa na jukumu gumu la kuleta mabadiliko ndani ya taasisi hiyo, na wadhifa wake ulikuwa sawa na ‘jukumu lisilowezekana.’ Hata hivyo wanampongeza kwa ‘kubeba mzigo wa lawama’ kwa niaba ya watendaji wake. 
Tukio la pili linahusu filamu ya maelezo (documentary) iitwayo The Gatekeepers, iliyoonyeshwa kwenye kituo cha runinga cha BBC2 mwishoni mwa wiki. 
Filamu hiyo ni ya mahojiano na wakuu sita wa zamani wa Idara ya Usalama wa Ndani wa Israeli, Shin Bet (au 'Shabak' kama inavyojulikana kwa Kiyahudi). 
Filamu hiyo iliyotengenezwa mwaka juzi na kuteuliwa kuwania tuzo za Oscars, imeendelea kuwa na mvuto mkubwa kutokana na ukweli kuwa ni vigumu mno, hasa kwa ‘nchi ya kiusalama’ kama Israeli, kupata fursa ya kufanya mahojiano na wakuu wa taasisi za usalama. 
Katika filamu hiyo inayoelezea kwa undani utendaji kazi wa Shin Bet, idara ya ushushushu yenye ufanisi mkubwa duniani, ikiwa ni pamoja na operesheni mbalimbali za Shin Bet dhidi ya ‘magaidi’ wa Palestina, wakuu hao – Avraham Shalom (1980-1986), Yaakov Peri (1988-1994), Carmi Gillon (1994-1996), Avi Dichter (2000-2005) na Yuval Diskin (2005-2011)- wanatanabahisha jinsi wanasiasa na Wayahudi wenye msimamo mkali walivyo vikwazo kwa jitihada za kutafuta amani ya kudumu katika mgogoro wa muda mrefu wa Israeli na Palestina. 

Kwa ujumla, wote wanahitimisha kuwa licha ya umuhimu kwa serikali ya Israeli na taasisi zake za ulinzi na usalama kutumia nguvu dhidi ya ‘ugaidi wa Wapalestina,’ ukweli mchungu ni kuwa matumizi hayo ya nguvu si tu yanachochea ‘ugaidi’ zaidi bali pia yanakwaza uwezekano wa kupatikana amani ya kudumu. 

Filamu hiyo ilisababisha wakuu hao kushutumiwa na Waisraeli wengi, wakilaumiwa kwa msimamo wao uliotafsiriwa kama kuhalalisha ‘ugaidi’ wa Wapalestina, huku wengine wakiwashutumu kuwa ‘waliongea walichoongea baada ya kustaafu badala ya kubainisha mitizamo yao wakiwa madarakani.’ 
Kwa hakika filamu hiyo (unayoweza kuiangalia hapa http://goo.gl/gY4K6O) si tu inaeleza kwa undani operesheni hatari na za ‘ufanisi wa hali ya juu’ zilizofanywa na Shin Bet chini ya uongozi wa mashushushu hao lakini pia inamsaidia anayeiangalia kufahamu kwa undani mchanganyiko wa siasa na dini na mwingiliano wake katika utendaji kazi wa taasisi za kiusalama za Israeli, na kubwa zaidi ni maelezo ya kina kuhusu mgogoro kati ya nchi hiyo na Palestina. 
Lengo la makala hii si kujadili matukio hayo mawili bali kuyatumia kama ‘darasa la bure’ kwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa. Binafsi, nimekuwa moja ya sauti chache kuhusu haja ya mageuzi ya kimfumo na kiutendaji kwa taasisi hiyo muhimu. 
Kwa bahati mbaya – au makusudi- utendaji kazi na ufanisi wa Idara hiyo haukuguswa kwa kiwango kinachohitajika katika kikao cha Bunge la Katiba na hatimaye Katiba pendekezwa. 
Idara hiyo inakabiliwa na matatizo makubwa japo aidha hayafahamiki sana au yanapuuzwa, na huo ndio msingi wa ushauri wangu kuwa kuna haja ya mageuzi ya haraka. 
Tukijifunza katika kujiuzulu kwa mkuu wa Secret Service, twaweza kujiuliza, hivi kwanini hakuna anayewajibishwa licha ya Idara yetu ya Usalama wa Taifa kuboronga mara kwa mara? 
Pengine kuna watakaojiuliza 'imeboronga lini na katika nini?’ Jibu rahisi ni kwamba, kwa mujibu wa ‘kanuni za taaluma ya usalama wa taifa,’ kushamiri kwa vitendo vinavyotishia usalama wa nchi ni dalili ya wazi ya udhaifu wa idara ya usalama wa taifa ya nchi husika. 
Kwa maana hiyo, kushamiri kwa ufisadi, kwa mfano mmoja tu, ni dalili kwamba taasisi hiyo imeshindwa kazi yake. Kadhalika, Idara hiyo kufanya kazi zake kama ‘kitengo cha usalama cha CCM’ si tu kunaipunguzia kuaminika kwake kwa umma bali pia kunaathiri uwezo wake katika kukabiliana na matishio kwa usalama wa Taifa. 
Majuzi, aliyekuwa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Idara hiyo, Jack Zoka, ‘alizawadiwa’ ubalozi wa nchi yetu huko Canada. Sihitaji kuingia kwa undani kuhusu utendaji kazi wa shushushu huyo lakini atakumbukwa sana na vyama vya upinzani, hasa CHADEMA, sambamba na wengi wa waliojitoa mhanga kuwa sauti ya wanyonge, kwa jinsi alivyowadhibiti. Pengine kabla ya kupewa ubalozi baada ya kustaafu utumishi wa umma, ahojiwe kuhusu mchango wake katika ‘ufanisi’ au udhaifu wa Idara hiyo. 


 
Ni mwendelezo wa kasumba inayolikwaza Taifa katika nyanja mbalimbali: mtu anaboronga pale, anahamishiwa kule. Kwanini watendaji wengine wahofie kuboronga katika majukumu yao ilhali wenzao ‘wanazawadiwa’ badala ya kuwajibishwa? 
Somo kutoka kwa wakuu sita wa zamani wa Shin Bet katika filamu ya The Gatekeeper ni kubwa zaidi. Ukiondoa ‘sauti ndogo’ ya Mkurugenzi Mkuu wa zamani wa Idara yetu ya Usalama wa Taifa, Hans Kitine, takriban viongozi wote wastaafu wa Idara hiyo wamekuwa hawana mchango wa maana katika kuiboresha na hata kuisadia isimame katika upande stahili. 
Ni kweli Tanzania si Israeli, lakini wengi wa wastaafu wa taasisi hiyo, kama ilivyo kwenye taasisi nyingine, ni watu wenye ushawishi mkubwa na wanaheshimika vya kutosha, lakini ukimya wao wakati mambo yanakwenda kombo ni doa. 
Mashushushu hao sita wa Israeli walipokubali kushiriki kwenye filamu hiyo walikuwa wanatambua bayana athari zake, kubwa ikiwa ni uwezekano wa kuonekana wasaliti. Lakini ujasiri ni pamoja na kusema yasiyosemeka. 
Na kwa vile, kimsingi, ukiwa shushushu unabaki kuwa shushushu milele, na kwa sababu ni watu wachache katika jamii wenye uelewa kuhusu utendaji kazi wa taasisi za kiusalama, wastaafu au watumishi wa zamani ndio watu pekee wenye fursa ya ‘kuokoa jahazi.’ 
Nihitimishe makala hii kwa kutaja kwa kifupi maeneo yanayohitaji mageuzi (reforms) kuhusiana na Idara yetu ya Usalama wa Taifa. La kwanza ni umuhimu wa uwazi zaidi katika teuzi za viongozi wakuu wa Idara hiyo, hususan Mkurugenzi Mkuu. 
Ni muhimu kutengeneza mazingira yatakayoepusha uwezekano wa Rais ‘kumteua mtu wake au rafiki yake’ kuongoza taasisi hiyo. Madhara ya uswahiba katika uteuzi kuongoza taasisi nyeti kama hiyo ni pamoja na mteuliwa kujiona ana ‘deni la fadhila’ kwa aliyemteua. 
Kuna haja ya, kwa mfano, uteuzi wa viongozi wa juu wa taasisi hiyo kuidhinishwa na Bunge. 
Pili, ni ulazima wa taasisi hiyo kuwajibika kwa umma kupitia taasisi kama Bunge. Hapa ninamaanisha haja ya viongozi wa taasisi hiyo kuitwa katika kamati husika za Bunge, kwa mfano, kuwaeleza Watanzania ‘kwanini ufisadi unazidi kushamiri ilhali taasisi hiyo haipo likizo?’ 
Tatu ni mabadiliko ya kiutendaji ambapo Idara hiyo iwezeshwe kuufanya ushauri wake utekelezwe, badala ya mazingira yaliyopo ambapo kwa kiasi kikubwa suala hilo linabaki kuwa ridhaa ya Rais ambaye ndiye ‘consumer’ wa taarifa za kiusalama anazopatiwa na Idara. 
Hivi inakuwaje pale Idara hiyo inaposhauri kuhusu suala linalohatarisha usalama wa taifa lakini Rais akalipuuza? 
Mwisho, lengo la makala hii ni jema: kuiboresha Idara yetu ya Usalama wa Taifa (ambayo licha ya mapungufu yake lukuki, binafsi nina imani kuwa inaweza ‘kujikwamua’ kama si kukwamuliwa) kwa maslahi na mustakabali wa Taifa. 
Tanzania ni yetu sote na si kwa ajili ya kikundi kidogo kinachojiendeshea mambo kitakavyo.Penye nia pana njia.





22 Oct 2014

Watanzania tuna sifa moja kuu isiyopendeza ya usahaulifu wa haraka. Kuna wanaodai si usahaulifu as such bali kutojali, lakini bottom line ni kwamba haichukui muda mrefu kwa jambo linalotokea Tanzania bila kujali ukubwa au athari zake kwa taifa hilo kusahaulika haraka. 

Ni kwa mantiki hiyo ndio ninajikuta nikijiuliza ni Watanzania wangapi wanakumbuka ujio wa Rais wa China huko nyumbani, ulioambatana na utiaji saini wa mikataba kumi na kitu ambayo hadi leo imebaki kuwa siri ya namna flani. Mengi yamesemwa kuhusu mikataba hiyo lakini kilicho wazi, kwa kwa kuzingatia uzoefu wetu huko nyuma, mnufaika mkubwa wa mikataba hiyo ni Wachina na pengine kikundi kidogo cha wenzetu waliovuna teni pasenti kwenye akaunti zao.

Ndio maana niliposikia kuwa Rais Jakaya Kikwete anaelekea China nikabaki najiuliza: HIVI KAMA RAIS WA CHINA ALIKUJA KWETU NA IKASAINIWA MIKATABA KADHAA NA TUKAFICHWA, JE MIKATABA ITAKAYOSAINIWA WAKATI WA ZIARA YA KIWEKTE HUKO CHINA TUTAFAHAMISHWA? Jibu la wazo ni BIG NO. Hatutojua kitu.

Wakati natafakari hayo, nikakutana na habari hii ambayo ni tamko la Katibu Mkuu wa Chadema Taifa Dkt Willibrod Slaa ikitoa tuhuma nzito kuhusiana na ziara hiyo ya Kikwete China. Soma taarifa hiyo hapo chini na angalia kwa makini maneno ya rangi nyekundu.


Kamati Kuu ilikuwa na jumla ya agenda kumi na moja, mengine tutayatoa kwa umma kadri muda unavyokwenda.
Kwa leo tutazungumzia masuala mawili ambayo yana sura ya utekelezaji, tena wa muhimu na haraka; Mchakato wa Katiba Mpya na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa;
Katiba;
 
Tunawataka Watanzania wanaopenda nchi yao sasa waache kulia lia, waache kunung’unika pekee, waache kulalamika. Tuingie kazini. Sasa ni wakati wa kuingia kazini.  
Wenzetu tangu siku ya kupokea rasimu ambapo Kikwete si kama rais wa nchi, bali kama Mwenyekiti wa CCM alianza kuipigia chapuo debe Katiba Inayopendekezwa. Sasa tuingie kazini…
Kikwete kama mwenyekiti wa CCM akitumia kofia ya rais wa nchi, baada ya kupokea rasimu ameendelea kuipigia chapuo, anawaambia wananchi wasome Katiba inayopendekezwa waelewe, sisi tunamwambia aache kuwadanganya Watanzania. Katiba si sawa na novel kwamba kila mtu anaweza kuisoma tu na kuelewa, ingelikuwa ni rahisi namna hiyo tusingekuwa na haja ya kuwasomesha akina Lissu (Tundu). 
Tunahitaji wananchi wetu wasaidiwe tafsiri hasa ya katiba yenyewe na maana yake, hadi yale mambo ya ndani kabisa. Ndiyo kazi ambayo CHADEMA tunaanza kuanzia kesho kuzunguka nchi nzima, ambapo timu ya kwanza itaongozwa na BAWACHA. Ujumbe utakuwa ni Katiba Mpya na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Tunataka kuwafafanulia Watanzania kwa kina. 
Wakati bado tunapigania Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka kesho, moja ya ujumbe wetu kuanzia sasa ni kuwataka Watanzania kujiandaa kufurika vituoni kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura wa uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambalo litaanza kuandikishwa siku 21 kabla ya uchaguzi wenyewe. 
Watanzania wafurike kwa wingi. Wajiandikishe. Kuiondoa CCM kunahitaji vitendo. Tuingie kazini. 
Kwa mtindo huo huo wa kuingia kazini sasa kwa vitendo, tutatembea nchi nzima sasa kuwataka wananchi kujitokeza kwa wingi sana siku ya Desemba 14, kupiga kura kuwachagua viongozi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji… 
Tunawaagiza vile vile viongozi wetu katika ngazi zote za chama, kuanzia kanda, mikoa, wilaya, majimbo, kata, matawi na hadi misingi kuwaongoza Watanzania wote; 1. Kujiandikisha, 2. Kupiga kura na 3. Kusimamia taratibu za kikanuni… 
Tumeshabaini na kila Mtanzania sasa anajua kuwa kuwa Rais Kikwete si mtu wa kuaminika tena…ni mtu anayebadilika badilika na wala haoni haja ya kuomba samahani… 
Na sasa tumezidi kubaini kuwa Kikwete amefikia mahali pa kugeuka kuwa procurement officer na tumenasa nyaraka ambazo zinaonesha kuwa katika kujigeuza ofisa manunuzi huko yanafanyika maandalizi ya kufanya mapambano na wananchi badala ya kuandaa maridhiano.
Nyaraka…Rais amegeuka kuwa Ofisa Manunuzi, Ofisa Mawasiliano TCRA 
Tumepata taarifa za ziara yake ya kwenda China. Siwezi kusema atakwenda tarehe ngapi maana mimi si kazi yangu kutangaza tarehe za ziara za Kikwete ambazo sasa hata tumechoka kuhesabu maana zimeshakuwa nyingi mno zaidi ya 300+ ndani ya miaka kumi. 
Kilichotushtua si Kikwete kwenda ziara, maana siku hizi wala si habari tena, kilichotushtua ni hicho kinachompeleka huko China…ukimsikiliza Kikwete kwenye mazungumzo anapenda kuonekana mtu anayeoenda amani, mshikamano lakini si kweli.  
Amejigeuza Ofisa Manunuzi. Kwa miezi kadhaa sasa kumekuwa na jitihada za kupata helkopta tatu mpya…zingelikuwa ni kwa ajili ya Jeshi letu la Wananchi nisingekuwa na shida, shida inakuja namna zinavyotafutwa. Zinatafutwa kwa utaratibu ule ule wa kifisadi uliotumika kununua ndege ya rais wakati ule na hata rada. 
Tena anamtumia kampuni moja hivi ambayo tumekuwa tukiituhumu katika ufisadi. Sasa sisi tunahoji, hivi ni kwa nini Serikali ya CCM inashindwa kwenda kiwandani na kufanya order ya manunuzi kiwandani moja kwa moja hadi itumie taratibu za kifisadi au mafisadi kufanya kazi hizi… 
Kikwete anajua kuwa ninajua. Maana ameshalalamika kwa watu wake wa vyombo vya dola kwamba taarifa hizi zimefikaje kwa Dokta Slaa…
Wametumia fedha zetu za mikopo kutoka Ujerumani…ndege zinanunuliwa Ufaransa…anatuma fisadi kwenda kufanya manunuzi hayo badala ya Serikali… 
Kinachoonekana na taarifa na sisi hapa tunahoji je ni kweli ndege hizo zinataka kutumika kwa manufaa ya CCM? 
Rais pia ameomba kwenda Beijing kufuatilia mitambo ya Police Surveillance System…wanataka mitambo hiyo ifike hapa kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015…ujumbe huu umeandikwa na mtu anaitwa Mbelwa…Kairuki. Waandishi wa habari mtakuwa mnajua huko Wizara ya Mambo ya Nje. Anamwandikia Waziri wa Mambo ya Nje…ujumbe huu umeandikwa tarehe 7/10/2014… 
Sasa hizo ndege anayotaka kununua iko mji mwingine huko China si ule aliopangiwa katika ziara yake, sasa imeagizwa irushwe hadi pale atakapokuwa ili eti Rais mwenyewe aweze kuiona…nimeangalia kwenye budget component hiyo kitu hakuna. Kwa kawaida vitu vya kijeshi huwa havitajwi kwenye bajeti, lakini kwenye randamana ungeweza kuona mpango wa kununua kitu kama hicho. Hakuna. 
Sasa kinachoonekana ni kwamba kwa sababu wamejua mwaka 2015 wanaondoka madarakani, wanaanza kujiandaa kwa mapambano badala ya maridhiano. 
Nataka kumwambia Rais Kikwete kwamba nchi haiongozwi kwa misuli, haiongozwi kwa kutunishiana misuli. Wanataka kufanya kama walivyofanya majuzi kutunga Katiba Mpya kwa mitutu ya bunduki. 
Sasa tena uchaguzi unakaribia wanaanza maandalizi ya mitutu…tunamwambia Kikwete sisi tutakuwa wa mwisho kuona nchi hii inaingia katika vurugu. Ndiyo maana ili kuepusha mambo mabaya yasitokee kila taarifa kama hii tukiipata tutapiga kelele. Silaha kubwa ya mnyonge ni kupiga kelele. 
Katika mwendo huo huo wa Rais Kikwete kugeuka kuwa Ofisa Manunuzi, sasa amejigeuza kuwa Bwana TCRA, wanapanga kukutana na Kampuni ya HUAWEI ya China ili wanunue mtambo utakaowekwa ikulu kwa ajili ya kunasa simu za akina Dokta Slaa… 
Mitambo hiyo inapelekwa ikulu badala ya…ingepelekwa Usalama wa Taifa ningeelewa, ingepelekwa kwenye Jeshi letu ningeelewa, lakini ikulu? Tunasisitiza hatuna tatizo kama mambo haya ya ndege, helkopta au mitambo ya mawasiliano yangekuwa yanafanywa kwa ajili ya ulinzi na usalama wa nchi, lakini ni tatizo kubwa kama rais ndiye anakuwa Ofisa wa Manunuzi au Ofisa wa Mawasiliano, TCRA. 
Sasa wanatafuta na kuhangaika kutafuta kila njia ya kubaki madarakani. 
Tunamuonya Rais Kikwete kuwa hizo pesa anazotaka kuchezea kwa yeye kuwa Ofisa Manunuzi si za mfukoni mwake. Aache kuchezea fedha za Watanzania. Tulimuonya pia hivi hivi wakati alipochezea fedha za Stimulus Package. Kama anataka kutukamata atukamate lakini sisi tutasema. Haya ndiyo mambo ya madhara ya katiba inayopendekezwa, kama ambavyo tumeshasema vizuri mapema.


























































20 Oct 2014

Wakati Mbunge wa jimbo la Kawe, Dar es Salaam (Chadema), Halima Mdee akiahidi kuvalia njuga utata unaogubika mradi wa uwekezaji wa treni za kisasa jijini Dar, utata zaidi umeibuka kufuatia uchunguzi uliofanywa na mtaalam mmoja kutoka hapa Uingereza anayeishi nchini Tanzania (siwezi kutaja jina lake kwa vile sijapata idhini yake). 

Hapa chini ni tafsiri ya sehemu ya maelezo/ushauri alionipatia kwa barua-pepe:

Ni vigumu kujua wapi pa kuanzia kuhusu Shumake kwani anaonyesha kuwa ni mtu mwenye utata. Nyenzo zake za kibiashara zipo tupu na majibu yake kwa maswali uliyomtumia hayaridhishi.Pia ameonyesha dalili za jeuri pale aliposema  'do your research (fanya utafiti).

Unaweza kumkamata katika udanganyifu wake. Anadai kuwa kitabu chake cha 'Climbing Your Inner Mountain' ni 'number one seller' (kinaongoza kwa mauzo). Katika Amazon Kindle edition kinashika nafasi ya 472,476 kwa mauzo. Kwenye orodha ya vitabu vyenye 'jalada' (paperback), kitabu hicho kinashika nafasi ya 3,374, 824.

Hivi kweli (kiwa takwimu hizo) kitabu hicho kinaweza kweli kuitwa 'Number One Bestseller'? Huyu mtu si wa kuaminika, kinyume kabisa na anavyodai.

Kuhusu Shumoja na Shumake Global Partners: Kati ya maelezo yake aliyokutumia kwa email na tovuti yake, ni utata mtupu. Anasema Shumake Global Partners ni 'kampuni ya kibenki ya uwekezaji' (investment banking firm). Nneo 'banking' lipo bayana. Je kuna mahala popote Shumake Global Partners imeandikishwa kama benki? Nina hofu kuhusu hilo, lakini ni yeye pekee anayeweza kujibu. Je anaweza kutaja miradi yoyote ambayo imegharamiwa na Shumake Global Partners?

Kuhusu Shumoja Rails, lini ilianzishwa? Je yupo tayari kuwataja wawekezaji katika kampuni hiyo japo kama ni kampuni binafsi anaweza kupata sababu ya kutfanya hivyo)? Lini Shumoja Industries LLC ilianzishwa? Kuna uhusiano gani kati ya Shumoja Rails na Shumoja Industries LLC?

Je mtaji wa uwekezaji unatoka wapi (tukiamini kuwa kweli anao)? Je katika hilo, kuna fedha zozote zinazotoka kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii ambayo amehusishwa nayo huko nyuma kama ilivyo kwenye taarifa hii ya Bloomberg?




15 Oct 2014

Oktoba 20 mwaka huu itakuwa siku muhimu kwa Nigeria kwani siku hiyo taifa hilo litaadhimisha siku 42 tangu mtu wa mwisho kuthibitishwa kuwa na maambukizi ya Ebola. Idadi hiyo ya siku ni mara maradufu ya muda ambao Ebola yaweza kujitokeza hadharani (incubation period). Kwa maana hiyo, siku hiyo, Nigeria itakuwa na haki ya kujitangaza kuwa ipo huru dhidi ya ugonjwa huo hatari.

Hata hivyo, jana, Nigeria iliadhimisha tukio jingine ambalo pengine isingependa kulikumbuka: miezi sita kamili tangu kikundi cha kigaidi cha Kiislamu cha Boko kilipowateka wanafunzi wa kike 276 na kupelekea kelele takriban kila kona ya dunia kwa kampeni ya #BringBackOurGirls (Warejesheni Mabinti zetu).

Hata hivyo, licha ya kampeni hiyo, mabinti 219 bado wanaendelea kuwa mateka wa magaidi hao tangu walipotekwa katika eneo la Chibok. Licha ya tukio hilo la kinyama kuvuta hisia na sapoti ya watu wengi duniani, magaidi hao wanaendelea kufanya unyama wao uliopelekea maelfu ya mauaji, hususan katika majimbo ya kaskazini mwa nchi hiyo.

Maadhimisho hayo mawili yanazua swali linalokanganya: imewezekanaje kwa Nigeria kumudu kuidhibiti Ebola lakini imeshindwa kuidhibiti Boko Haram? Kwanini taifa hilo limeweza kulishughulikia tatizo moja kwa ufanisi mkubwa ilhali ikilishughulikia jingine kwa udhaifu mkubwa?

"Ebola inamgusa kila mtu."

Moja ya sababu ni jiographia ya kisiasa (political geography) ya Nigeria.ambayo tangu nchi hiyo kupata uhuru wake imekabiliwa na machafuko. Taifa hilo lenye watu milioni 170 ambao wamegawanyika katika makabila lukuki, limeshindwa kwa kiasi kikubwa kujenga umoja,mshikamano na maelewano kati ya wengi wa Wakristo wanaojiweza kwa upande wa kusini mwa nchi hiyo na wengi wa Waislamu wanaokabiliwa na ufukara upande wa kaskazini mwa nchi hiyo.

Boko Haram ambayo maana yake ni ni 'elimu ya kimagharibi ni dhambi,' inautumia mwanya huo.Kundi hilo linafanya zaidi shughuli zake katika majimbo matatu ya kaskazini mashariki, yote yakiwa chini ya uongozi wa chama cha upinzani cha All People's Party (APP), na ambako imani kwa Rais wa nchi hiyo, Goodluck Jonathan, ni haba.

"Watu wengi kaskazini mwa Nigeria wanaichukia Boko Haram," anaeleza Rudy Atallah wa taasisi ya The Atlantic Council na mtaalam wa masuala ya nchi hiyo. "Lakini kwa vile idadi kubwa ya watu wa kaskazini mwa nchi hiyo wanaona kama wametelekezwa na wenzao wa kusini kwa muda mrefu, wengi wanaiona Boko Haram kama chombo kinachoweza kuambana na serikali," anatanabaisha mtaalam huyo.

Katika hali tofauti, Patrick Swayer, Mwamerika mwenye asili ya Liberia alipogundulika kuwa na Ebola alipowasili Lagos, alijikuta katika jiji lililosheheni miundominu ya kisasa ya huduma za afya na makao makuu ya taasisi nyingi za kimataifa, Na tofauti na mapambano dhidi ya Boko Haram, mapambano dhidi ya Ebola yanavuka mipaka ya ukabila, siasa na dini.

"Ebola inamgusa kila mtu," anasema Atallah. "Haina madhehebu wala kundi maalum."

'Kasheshe' nyingine nchini humo yatarajiwa Februari mwakani wakati taifa hilo litakapofanya uchaguzi wa Rais. Baada ya mhula mmoja madarakani, Rais Jonathan anaruhusiwa kugombea tena. Ushindi kwa chama chake cha People's Democratic Party, ambacho kimeitawala Nigeria kwa miaka 14, na ambacho kina sapoti kubwa kusini mwa nchi hiyo, waweza kuchochea mgawanyiko zaidi nchini humo, sambamba na ugumu wa kuwaokoa mateka waliosalia mikononi mwa Boko Haram.

CHANZO: Makala hii imetafsiriwa kutoka hifadhi yangu ya habari muhimu, ninazokutana nazo mtandaoni na kuzihifadhi katika app ya Instapaper. App nyingine ninayoitumia kwa hifadhi ya habari ninazozitumia kama reference ni Pocket. Kadhalika, app nyingine muhimu ninayoitumia kuhifadhi vitu mbalimbali ninavyokutana navyo mtandaoni au hata mtaani ni Evernote





Chris Brown is sharing his thoughts about Ebola. (Getty Images)
Dunia yetu imesheheni watu wanaoitwa 'conspiracy theorists,' Sina uhakika wa tasiri ya kiswahili ya neno hilo, lakini nadhani neno la karibu ni 'wazushi.' Hata hivyo, tofauti ya wazushi tuliowazowea ambao mara nyingi huzusha jambo kwa minajili ya kuzusha tu, kwa conspiracy theorist uzushi wao huambatana na 'ushahidi wa kimazingira,' japo si ajabu ushahidi huo nao kuelemea zaidi kwenye uzushi kuliko facts.

Sasa msanii maarufu wa Marekani, Chris Brown, nae ameingia katika kundi la conspiracy theorists baada ya kudai kuwa ugonjwa hatari wa Ebla ni moja ya mbinu za kudhibiti idadi ya watu duniani.

Msanii huyo ali-post mtizamo wake huo kwenye ukurasa wake wa Twitter, ambapo ana 'wafuasi' (followers) milioni 13.7. Hata hivyo, baadhi yao walipingana nae waziwazi

"Wajua mjadala kuhusu ugonjwa wa Ebola ulichokuwa unahitaji? Upuuzi zaidi. Hapa anaingia Chris Brown..." aliandika mmoja wa wafuasi wake.

"Chris Brwon anadai Ebola ni moja ya mbinu za kudhibiti idadi ya watu. Ajaribu ugonjwa." alitwiti mwingine  huo  akimaanisha msanii huyo ni miongoni mwa watu wanaohitaji kudhibitiwa.

"Chris Brown anadai kuwa Ebola ni njia ya kudhibiti widadi ya watu. Kwa hakika hiyo si kweli, na laiti ingekuwa kweli basi tungempa ugonjwa huo yeye kwanza," aliandika mwingine.

Brown ambaye hivi karibuni alitumikia kifungo cha siku 108 jela kwa kukiuka taratibu za uangalizi wa kimahakama (probation) kufuatia kosa la kumpiga mpenzi wake wa zamani, msanii Rihanna, baadaye alionekana kutafakari upya kauli yake, na kutanabaisha kuwa 'anafunga mdomo wake,' japo si kwa maneno ya kistaarabu.

Lakini muda mfupi baadae 'alipandisha mzuka' na kuwashambulia waliopingana na mtizamo wake huo, na kutwiti maneno makali: "naandika ninachotaka. Kama hutaki nyonya %$*£$ yangu (tusi)

Hata hivyo, licha ya baadhi ya watu kupingana na conspiracy theory hiyo ya msanii huyo, watu kadhaa katika mtandao huo wa Twitter walionekana kuafikiana nae kwa tweet hiyo kupata takriban  'Retweets' 30,000 na 'Favourites' 22,000.

Mlipuko wa ugonjwa wa Ebola umeshasababisha vifo zaidi ya 4000 huku Afrika ya Magharibi ikiwa ni eneo lililoathirika vibaya zaidi japo tayari kuna wagonjwa wachache waliokumbwa na maradhi hayo huko Hispania na Marekani.

CHANZO: Imetafsiriwa kutoka mtandaoni



14 Oct 2014

These were the questions I put forward to Mr Robert Shumake (haya ndiyo maswali niliyomuuliza Robert Shumake)
And below are series of Shumake's responses, click photo to enlarge (na chini ni mlolongo wa majibu ya Shumake, bonyeza picha kuikuza)






My final request to Shumake was advising he publishes the provisionary Memorandum of Understanding between his company M/S Shumoja a.k.a Shumake Rails (he has so far failed to concisely clarify on this) and the Government of Tanzania. While he is yet to respond, I will continue with my investigation, and will definitely keep you posted. As for now, I leave to you wananchi to pass a verdict whether this guy a genuine investor or not? (Ombi langu la mwisho kwa Shumake ni kumshauri aweke wazi kataba wa awali kati ya kampuni yake ya M/S Shumoja au Shumake Rails (kwa ujumla ameshindwa kufafanua kuhusu hili) na serikali ya Tanzania. Wakati bado hajanijibu kuhusu ombi hilo, mie ninaendelea na uchunguzi wangu na nitawajuza maendeleo yake.Kwa sasa nawaachia ninyi wananchi kutoa hukumu iwapo mtu huyu ni mwekezaji kweli au la)





12 Oct 2014

Kama mtu mwenye uelewa kiasi kuhusu utendaji kazi wa Idara yetu ya Usalama wa Taifa, nimekuwa 'nikipiga kelele' mara kwa mara kuhusu haja ya mageuzi ndani ya taasisi hiyo nyeti. Kwa bahati mbaya sio tu kelele hizo ni vigumu kueleweka kwa Watanzania wengi, uwezekano wa kusikilizwa ni mdogo hasa ikizingatiwa kuwa asili ya taasisi hiyo ni kutekeleza majukumu yake kwa siri, na kama hiyo haitoshi, mara nyingi wahusika wa taaluma hiyo inayopaswa kuhusisha matumizi ya hali ya juu ya akili, hawapendi kusikia ushauri wa 'walio nje' kama akina sie.

Mageuzi ninayoyapigia kelele ni ya kimfumo. Kubwa zaidi ni haja ya uwepo wa mazingira ya uwajibikaji pale watu wanapoboronga. Moja ya dhana zinazotawala fani ya ushushushu ni ile isemayo 'kushamiri kwa matishio ya usalama katika nchi husika ni dalili kuwa taasisi ya ushushushu katika nchi husika ina mapungufu.' Sasa huhitaji uelewa wa fani hiyo kutambua kushamiri kwa matishio kadhaa ya usalama katika Tanzania yetu, kubwa zaidi likiwa ufisadi. 

Labda waweza kujiuliza, iweje ufisadi uwe tishio la usalama? Jibu jepesi ni kwamba ufisadi unatoa fursa kwa maadui wa ndani na nje wa taifa kutimiza azma zao kwa urahisi. Kwa mfano, laiti kukiwa na ufisadi kwenye mipaka ambapo wahusika wanaruhusu kirahisi tu wageni kuingia nchini pasi kuzingatia taratibu zilizopo, ni rahisi kwa magaidi kutumia mwanya huo. 

Ufisadi unaweza kutuletea tapeli la kimataifa kuwekeza kwenye maeneo yanayofahamika kiusalama kama 'vituo muhimu' (vital installations) kama vile viwanja vya ndege na bandarini.

Sasa tukichukulia mfano wa ufisadi, sio tu umeshamiri vya kutosha lakini ndo wazidi kuongezeka. Kuna wanaojiuliza je TISS (Idara yetu ya Usalama wa Taifa) ipo likizo ndefu, wahusika wapo katika usingizi fofofo au kazi imewashinda? Mie sina jibu la moja kwa moja lakini nadhani tatizo la TISS ni la kimfumo zaidi kuliko kiutendaji, japo utendaji wao nao una walakini.

Lakini kabla ya kuingia kwa undani katika mada hii, nirejee kwenye kichwa cha habari. Majuzi, mkuu wa taasisi yenye jukumu la ulinzi wa viongozi wakuu wa Marekani, Secret Service, Bi Julia Pierson alilazimika kujiuzulu wadhifa huo baada ya mtu mmoja kuingia uzio wa Ikulu ya nchi hiyo na kutishia usalama wa Rais Barack Obama. Kwa wenzetu tukio hilo lilikuwa na uzito mkubwa sana, na lilitawala sana katika vyombo vya habari.


Hata hivyo, kwa vile wenzetu wanaendesha mambo kwa uwazi, mwanamama huyo aliitwa mbele ya kamati moja ya bunge la juu la nchi hiyo na kupewa fursa ya kuieleza, ambapo watunga sheria waliafikiana kwamba anapaswa kujiuzulu.
Tukirejea huko nyumbani, ukweli usiopingika ni kwamba licha ya vikwazo vya kimfumo vinavyoikabili TISS, ksingizio  cha 'taasisi hii yafanya kazi kwa siri na hakuna anayepaswa kuhoji' kinatoa fursa kwa wazembe kupata kinga katika utendaji wao mbovu. Ndio, kazi za TISS ni za siri lakini so far usiri huo haujafanikiwa kuwawezesha kukabiliana ipasavyo na matishio ya kiusalama, la wazi likiwa ni ufisadi.

Miongoni mwa mapendekezo yangu (yapo mengi) kuhusu haja ya mageuzi ni kama ifuatavyo.

Kwanza, uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu unapaswa kufanywa kwa uwazi zaidi, ikiwezekana kuidhinishwa na Bunge. Hiyo itazuia uwezekano wa Rais kumpatia wadhifa huo mtu yeyote yule bila kuzingatia uadilifu na uwezo wake kikazi. Kwa kumpa Rais 'blank cheque' ni rahisi kwake kumchagua mtu wake, au mshkaji wake kwa minajili ya kumlinda au kuwa kibaraka wake badala ya kulitumikia taifa kiufanisi.
Pili, ni muhimu TISS kama taasisi iwajibike kwa umma, na si kwa Rais pekee (maana huyo Waziri Katika Ofisi ya Rais mwenye jukumu la kuisimamia TISS anakwazwa na mazingira yalivyo, sambamba na 'uoga' wa kawaida). Ifike mahali, watendaji wakuu wa TISS waweze kuitwa Bungeni, kwa mfano, kuhojiwa kuhusu masuala mbalimbali yanayoihusu taasisi hiyo.

Kiutendaji, ni muhimu kwa taasisi hiyo kupewa uhuru wa kioperesheni utakaoiwezesha kuondokana na hali iliyopo sasa ambapo kwa kiasi kikubwa imekuwa kama tawi la usalama la chama tawala. Sambamba na hilo ni haja ya kuitengenezea mazingira yatayoiwezesha kuhakikisha mapendekezo yake kwa Rais yanafanyiwa kazi hata pale Rais anapoyapuuza. Ikumbukwe kuwa licha ya Rais kuwa 'mkuu halisi wa TISS,' yeye bado ni mwananchi kama wananchi wengine ambao TISS inawajibika kuhakikisha sio tu usalama wao bali hawawi tishio kwa usalama huo. Rais anapopuuza ushauri unaotishia usalama wa taifa basi TISS ijengewe mazingira ya kuhakikisha kuwa ushauri wake unafanyiwa kazi.

Nimalizie kwa kutumaini kuwa 'kelele' hizi zitasikika kwa wahusika. Tujifunze kwa wenzetu waliotatutangulia na wahusika wasione aibu kusikia ushauri wa wenye uelewa hata kama wapo nje ya 'uwanja wa mapambano.'

Endelea kutembelea blogu hii kwa habari mbalimbali, ikiwa ni pamoja na hizi za ushushushu (bonyeza hapo kwenye menu ya INTELIJENSIA upelekwe moja kwa moja)





bbb 



The Gatekeeper ni filamu (documentary) inayoeleza kuhusu shirika la ushushusu wa ndani wa Israel, Shin Bet (au Shabak kwa Kiyahudi) kutoka kwa mtizamo wa wakuu sita wa zamani wa shirika hilo (pichani juu) kwa njia ya mahojiano.


 

Endelea kutembelea blogu hii kwa habari mbalimbali, ikiwa ni pamoja na hizo zinazohusu ushushushu (bonyeza kwenye menu INTELIJENSIA kwenda moja kwa moja). Kuhusu makala ya 'Shushushu ni nani? Anafanya kazi gani?' ninaahidi kuiendeleza katika siku chache zijazo. Ninaomba samahani kwa kuichelewesha.

10 Oct 2014

Kwanza soma taarifa ifuatayo kutoka Ikulu kisha tuijadili pamoja
Kweli Tanzania yetu haina uhaba wa mazingaombwe. Lakini hilo dogo, kubwa ni 'akili' za baadhi ya wasaidizi wa Rais. Binafsi nimekuwa mpinzani sana wa hoja kuwa 'tatizo si JKI bali wasaidizi/ watendaji wake,' kigezo changu kikubwa kikiwa 'kwani walimshikia mtutu wa bunduki awateue na kisha kumtahadharisha kuwa akiwatimua pindi watapoboronga watamdhuru'?

Lakini ukiangalia mlolongo wa 'makanusho' yanayotolewa na wasaidizi wa Rais, unaweza kukubaliana na wanaosema kuwa 'wasaidizi/ watendaji wa JK wanamwangusha' (japo siafiki wanaotaka kutumia sababu hiyo kama excuse ya kumsafisha JK mwenyewe.)


Hebu tuichambue kauli hiyo ya Ikulu hatua kwa hatua. Kwanza, Ikulu haikuwahi kukanusha lundo la picha (kama hiyo inayoambatana na kichwa cha habari hii) zilizowekwa mtandaoni zikimwonyesha Rais Kikwete akipokea zawadi ya saa, huku maelezo yakibainisha waziwazi kuwa 'Rais Jakaya Kikwete akipokea zawadi ya saa..." Najua kwanini hawakuhangaika na taarifa hizo za awali: hazikuhusiana na 'utata' unaomkabili mwekezaji aliyetoa zawadi hiyo.
Lakini baada ya gazeti la Raia Mwema kueleza bayana kuwa mwekezaji wa mradi wa treni ya kisasa Dar ndiye huyo alompa zawadi ya saa Rais Kikwete, na kutanabaisha maswali kadhaa yanayouzunguka mradi husika na wasifu wa mwekezaji huyo, Ikulu ikakurupuka na kanusho hili. WALIKUWA WAPI MUDA WOTE HUO?

Mwandishi wa taarifa hiyo ameonyesha ni mtovu wa nidhamu wa kutokana na matumizi ya maneno yasiyopaswa kutoka ofisi iliyopo sehemu 'tukufu' kama Ikulu. Matumizi ya maneno kama "ni habari ya uzushi na UPUUZI..." na  "...kumhusisha Rais na zawadi ya KIPUUZI kama saa..."Huwezi kuita upuuzi habari inayohoji suala la msingi, ambapo logically, mfanyabiashara anaonekana akitoa zawadi kwa Rais (iwe saa au suti), kisha siku chache baadaye mfanyabiashara huyo anatangaza 'mradi wa utata'...Kwanini wananchi (waandishi wa gazeti hilo ni sehemu ya wananchi hao) wasihoji suala hilo ambalo mwandishi wa Ikulu anaona ni la kipuuzi?

Na kwa kinachoweza kuelezwa kama uhuni na si ubabaishaji, taarifa hiyo ya Ikulu imekwepa kabisa kuzungumzia maswali lukuki yanayoiandama kampuni inayomilikiwa na mfanyabiashara huyo, wasifu wa mfanyabiashara mwenyewe, sambamba na 'sintofahamu' lukuki kuhusu uwekezaji huo.

Kimsingi, habari Ikulu 'imejishtukia' tu inapodai "Ni habari ya uzushi na upuuzi. Ni habari inayolenga kumdhalilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kwamba amepokea zawadi kutoka kwa mtu ambaye anajaribu kupewa kandarasi ya kujenga ya usafiri wa treni jijini DSM na ambaye pia anahusishwa kwenye shughuli nyingine za kibiashara zenye utata huko kwao Marekani."

Kwa wapambe hao wa Rais ni upuuzi na kumdhalilisha Rais kupokea zawadi kutoka kwa mtu ambaye WANAKIRI BAYANA kuwa anahusishwa na shughuli nyingine za kibiashara ZENYE UTATA huko Marekani. 

Kwanini taarifa hiyo isingewekeza nguvu katika 'kumsafisha' Rais kwa 'kujihusisha' na mtu huyo wanayekiri kuwa na shughuli zenye utata, badala ya kung'ang'ania hoja moja tu 'ya kipuuzi' kuhusu 'zawadi ya kipuuzi' ya saa?

Kilicho bayana ni kasumba iliyoota mizizi kwenye utawala wa Kikwete wa kudhani Watanzania wanaishi karne ya 18, hawana access na internet kufuatilia masuala mbalimbali yanayoihusu nchi yao, na hata wakifuatilia na kupatwa na hofu basi wakae kimya!

Suala la msingi si Rais kupewa zawadi, iwe ni Rolex au 'souvenir watch' nyingine, bali ni utata unaozunguka kampuni inayotaka kuwekeza katika mradi wa treni za kisasa, na inayomilikiwa na mtu ambaye anazungukwa na habari zenye utata, na ambaye alimzawadia Rais saa (iwe halisi au souvenir' tu) siku chache kabla ya kutangazwa taarifa za uwekezaji huo. Surely huu sio upuuzi bali ni kuihoji serikali yetu ambayo ina historia 'nzuri tu' ya kuingia mikataba ya 'ajabu ajabu' kama ule wa kitapeli wa Richmond.

Nihitimishe makala hii kwa kuwakumbusha wasaidizi wa Rais Kikwete kwamba Watanzania wana haki ya msingi kuuliza maswali kuhusu masuala yanayohusu taifa lao. Kadhalika, wanahabari wana haki ya kuhoji utata unapojitokeza katika mahusiano ya serikali au viongozi wake (hususan Rais) na watu au taasisi mbalimbali.

By the way, ajira ya mwandishi wa taarifa hiyo inategemea kumtetea bosi wake, na hakuna cha ajabu katika kujitokeza kwake kwa ukali kukanusha taarifa hiyo. Lakini kama wana ujasiri, basi wajibu maswali haya tuliyomuuliza mwekezaji huyo badala ya kung'ang'ania 'hoja ya kipuuzi ya "SIO ROLEX" au kutuhadaa kuwa "saa aliyopewa Rais Kikwete ni mali ya Watanzania" (mbona hawakutangaza kuwa Rais amekabidhiwa saa ambayo ni mali ya Watanzania hadi walipoona habari hiyo kwenye gazeti la Raia Mwema?)

Rais Kikwete amekuwa ajitianabaisha kama muumini wa dhana ya 'open goverment' inayopigia mstari haja ya wananchi kufahamu utendaji kazi wa serikali yao. Lakini wakati huohuo, wasaidizi wake huwa wakali kweli pindi wananchi wanapotaka kufuata dhana hiyo na kuhoji 'maswali magumu' kama hayo yanayouzunguka mradi wa treni za kisasa Dar.

Ni muhimu kwa watendaji wa serikali yetu kutambua kwamba Rais wanayemtumikia ni mwajiriwa wa Watanzania, na kila mwajiriwa anatambua haki ya mwajiri wake kuhoji masuala mbalimbali yanayomtatiza. Tanzania ni yetu sote na si ya kikundi kidogo cha miungu-watu wasiotaka kuuliza 'kulikoni?' hata katika masuala yanayohitaji 'akili ndogo' tu ya ku-Google kuhusu mtu au taasisi flani (kama ilivyo kwa ishu ya 'M/S Shumoja a.k.a Shumake Rails.'


m
 

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.