Showing posts with label UTAWALA WA JAKAYA MRISHO KIKWETE. Show all posts
Showing posts with label UTAWALA WA JAKAYA MRISHO KIKWETE. Show all posts

6 Jun 2011


Utawala wa Rais Jakaya Kikwete unaendelea na jithada zake za kutaka kuifanya Tanzania isitawalike baada ya jeshi lake la polisi kuendeleza ubabe dhidi ya viongozi wa Chadema.

Katika matukio yanayoweza kuingizwa kwenye vitabu vya historia (chafu),jeshi hilo maarufu zaidi kwa ubabe kuliko uwezo wake kukabiliana na uhalifu limewatia mbaroni Mwenyekiti wa taifa wa Chadema,Freeman Mbowe,na Mbunge maarufu wa chama hicho Zitto Kabwe.Wakati Mbowe,ambaye pia ni Kiongozi Mkuu wa Upinzani Bungeni (wadhifa unaomfanya kuwa Waziri Mkuu Kivuli) alikamatwa kwa madai ya kukiuka taratibu za dhamana katika kesi inayomkabili huko Arusha,Zitto alikamatwa kwa madai ya kuzidisha muda wa kuhutubia mkutano wa hadhara.

Tangu Tanzania iridhie uwepo wa mfumo wa vyama vingi vya siasa,mahusiano kati ya vyombo vya dola na vyama hivyo yamekuwa mabaya na ya ounevu kupindukia.Tatizo la wazi ni vyombo hivyo vinavyoendeshwa kwa fedha za walipa kodi pasipo kujali itikadi zao za kisiasa kuendelea kutekeleza majukumu yake kana kwamba ni matawi ya chama tawala.Wakati jeshi la polisi ndilo linaloongoza kwa kuwanyanyasa wapinzani,taasisi nyingine za dola kama Idara ya Usalama wa Taifa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania pia kwa nyakati mbalimbali zimeonyesha kuweka mbele unazi wa kisiasa na kuipendelea CCM.

Lakini licha ya kushamiri kwa vitendo vya ukatili dhidi ya wanasiasa wa vyama vya upinzani,kuibuka kwa Chadema kama ngome kuu ya upinzani kumekuwa mithili ya pilipili inayowawasha polisi kiasi cha kuwaandama viongozi wa chama hicho kila kukicha.

Ni dhahiri kuwa matendo haya yana baraka za Rais Kikwete kwani laiti angemwamuru rafiki yake Said Mwema,Inspekta Jenerali wa Polisi,kuhakikisha jeshi la polisi sio tu linawapa heshima viongozi wa upinzani bali pia lizingatie haki zao za kibinadamu,ni dhahiri tusingeshuhudia manyanyaso kama hayo waliyopewa Mbowe na Zitto.

Kikwete na jeshi lake la polisi wanapaswa kutambua kuwa kadri wanavyotumia nguvu nyingi kuwadhibiti Chadema ndivyo wanavyozidisha huruma ya Watanzania kwa chama hicho.Mtu yeyote mwenye akili timamu hatoshindwa kubaini kuwa unyanyasaji unaofanywa na jeshi la polisi dhidi ya chama hicho unalenga kukipunguzia nguvu katika jitihada zake za kupambana na ufisadi unaolelewa na serikali ya Kikwete na chama chake cha CCM.

Uzoefu unaonyesha kuwa tunaweza kulilaani jeshi la polisi hata kila sekunde lakini hiyo haitopelekea jeshi hilo lililosheheni mbumbumbu wa sheria za haki za binadamu kubadili utendaji kazi wao wa ovyo ovyo.Tunahitaji kwenda mbali zaidi ya kulaumu na kulaani pekee.

Ni muhimu basi kwa Chadema kuchukua hatua za kisheria dhidi ya jeshi la polisi.Kwa vile mahakama zetu nazo zinaendeshwa kisiasa,basi pengine ni muhimu kujaribu kufungua mashtaka ya aina hiyo katika mahakama za kimataifa.

Tetesi zinadai kuwa tawi la serikali ambalo kikatiba lina jukumu la kutafsiri ya sheria (Mahakama) chini ya uongozi wa Jaji Mkuu Othman Chande linaendesha shughuli zake "kishkaji" na tawi la serikali lenye jukumu la kusimamia sheria,yaani serikali kwa maana ya Executive branch.Tetesi hizo zinapigia mstari hoja kuu mbili.Kwanza,Jaji Mkuu Othman ni kaka wa Mkurugenzi wa Idara ya Usalama wa Taifa Othman Rashid,ambaye pia ni rafiki wa karibu wa Kikwete,kama alivyo IGP Mwema.Sasa ukiwa na kaka wawili kwenye nafasi nyeti kama hizo,na ambazo kikatiba zinapaswa kufanya kazi zake kwa kuzingatia mgawanyiko wa mamlaka (separation of powers),ni wazi kuwa nchi inaendeshwa kama kampuni ya mtu binafsi.

Kwa upande mwingine,Jaji Mkuu alikuwa miongoni mwa waalikwa kwenye semina elekezi iliyofanyika majuzi jijini Dodoma.Yayumkinika kuhisi kuwa ushiriki wa Jaji Mkuu kwenye semina hiyo kumepelekea Mahakama kumezwa na Serikali (Executive),na si aabu Mahakama ikawa inatekeleza majukumu yake kwa maelekezo ya serikali.Changanya hali hiyo na hizo teuzi za kufahamiana...!!!

All in all,ni lazima ukatili wa jeshi la polisi sio tu ulaaniwe kwa nguvu zote bali pia ukomeshwe kwa hatua za kisheria kuchukuliwa dhidi yake.Na kwa vile mahakama za ndani ndio hivyo tena zishakuwa kama matawi ya CCM,kuna haja ya kutafuta haki kwenye mahakama za kimataifa.

Mwisho,Kikwete na watendaji wake,na jeshi lake onevu la polisi wanaweza kuwatupa ndani viongozi wa vyama vya upinzani kadri watakavyo...kwa muda flani, lakini kamwe hali hiyo haitaendelea milele.Kama ameshindwa dikteta Hosni Mubarak ataweza Kikwete?Tawala dhalimu zinaweza kudhani kuwa ubabe na uonevu ni silaha muhimu za ustawi wake lakini ukweli ni kwamba vitendo hivyo huharakisha uchimbaji kaburi la kuzika tawala za aina hiyo.

Ni muhimu kwa kila mpenda haki na usawa kukemea kwa nguvu zote uhuni huu wenye lengo moja tu: kudhoofisha mapambano yanayoongozwa na Chadema dhidi ya ufisadi unaolelewa na serikali ya Kikwete na CCM yake.Kadhalika,kashkash dhidi ya Chadema inamsaidia Kikwete na CCM yake kupooza mvurugano unaoendelea ndani ya chama hicho ambao umesababishwa na mgongano wa kimaslahi ya kifisadi.

Enough is enough!

16 May 2011


Wasaidizi wana nafuu kuliko rais?

Ansbert Ngurumo

BAADHI yetu hatujaelewa ari, nguvu na kasi ya Rais Jakaya Kikwete. Nina hakika naye ameiimba, lakini hajaielewa barabara.

Kaulimbiu hii iliyoasisiwa na kina Samuel Sitta mwaka 2005, ilitumika kumtafutia urais mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete, kwa ari mpya, kasi mpya na nguvu mpya.

Waliomjua vema uwezo na udhaifu wake walidokeza mapema kwamba maisha ya Watanzania chini ya CCM ya Kikwete yangedorora na kuwa magumu zaidi - kwa ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya.

Baadaye, sisi na baadhi ya watani wa CCM tuliifupisha kaulimbiu hiyo, tukaiita ANGUKA. Ni kweli! Miaka mitano baadaye, wameangukia pua.

CCM imeanguka. Rais Kikwete ameanguka. Mtandao wake umeanguka. Na kwa bahati mbaya, hata serikali yake imeanguka, ikaishia kuwa serikali kopa-kopa – hata mishahara ya watumishi – licha ya kodi kubwa tunazolipa.

Kuanguka huku, ndiko kumekuwa chanzo cha kura chache za mgombea urais wa CCM katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010. Kuanguka huku ndiko kumekuwa kichocheo cha vilio vya wananchi dhidi ya ufisadi. Kuanguka huku ndiko kumesababisha hata usanii mpya wa CCM wa ‘kujivua gamba.’

Kuanguka huku ndiko kumemkosanisha Rais Kikwete na maswahiba wake wa siku nyingi. Kuanguka huku ndiko kumemfanya Rais Kikwete aogope maandamano ya wananchi yanayoratibiwa na CHADEMA hata akalialia kwamba “wanataka kuniondoa kabla ya wakati.”

Kuanguka huku ndiko kumemwondoa Yusuf Makamba katika ukatibu mkuu wa CCM, yeye na sekretariati na Kamati Kuu. Kuanguka huku ndiko kumerutubisha na kukuza fitina na vita ya makundi ndani ya CCM.

Kuanguka huku ndiko kumewafanya Watanzania kuikataa CCM waziwazi kuliko wakati wote katika historia, na ndiko kumemwingiza Nape Nnauye (Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM) katika migogoro mipya ndani ya makundi ya CCM na kumwandalia anguko lake huko tunakokwenda, hasa baada ya Rais Kikwete kuondoka madarakani.

Anguko hili la ari mpya, kasi mpya na nguvu mpya limewagusa wananchi wenyewe. Sasa wanakabiliwa na ukali wa maisha usiofanana kabisa na ahadi kemkemu walizopewa na CCM mwaka 2005 na 2010.

Bahati mbaya waliosababisha anguko hili, bado wanajitapa kwamba wameleta maendeleo. Vipofu!

Na kwa sababu ya upofu huu, wanakosa mikakati mipya ya kujikwamua. Wanarudiarudia yale yale yaliyoshindwa kuwanusuru miaka mitano iliyopita.

Kwa mfano, mwaka 2006 mwanzoni, Rais Kikwete aliingia na mbinu ya kutembelea wizara moja moja, kutoa maelekezo na kupiga picha na watumishi wa wizara hizo. Ilikuwa propaganda na mapambo ya magazeti na televisheni.

Baadaye, aliwaita mawaziri na watumishi waandamizi wa serikali (mara mbili) katika semina elekezi kwenye Hoteli ya kifahari, Ngurdoto, Arusha.

Leo tunapotazama nyuma, ni nani anaweza kujivunia semina elekezi za Ngurdoto?

Lakini watu wasiojifunza hawafichiki. Mwaka jana, rais yule yule akagombea kwa kaulimbiu ya ari zaidi, kasi zaidi na nguvu zaidi. Yaani, hawa jamaa hawakuridhika na ’anguko jipya’ la 2006. Waliona hilo halitoshi, wakatuandaa “kuanguka zaidi” mwaka 2010!

Haikumwongezea kura mgombea wao. Haikuvuta hisia za vijana wala kina mama. Ili kupata watu wa kuhutubia ilibidi CCM itumie pesa nyingi kuchapisha na kugawa sare, kuwagawia watu na kuwapakia kwenye magari kuwapeleka kwenye mikutano ya mbali.

Haikuwaunganisha watawala wawe na sauti moja, hata baada ya kurejea madarakani. Haikuwasaidia kupata hekima ya kumaliza matatizo ya muda mrefu, kama ukosefu wa umeme ambao umezungumzwa tena na tena bila ufumbuzi.

Sasa kwa ari zaidi, nguvu zaidi na kasi zaidi, watawala wamerudi tena katika semina elekezi, chini ya mwelekezaji yule yule.

Walidhani zile zilishindikana kwa sababu zilifanyika Arusha. Sasa wamekimbilia Dodoma. Kwa wiki nzima, serikali iko Dodoma, imelala; inakula posho. Kazi zinakwama.

Rais naye, badala ya kuwaelekeza kwa hekima na ustadi, “akawananga” wasaidizi wake hadharani, kana kwamba huwa hapati fursa ya kukutana nao – wakati amekuwa akikutana nao kila mwezi katika vikao vya Baraza la Mawaziri. Ndio hao aliowatembelea na kuwasema wizarani kwao miezi miwili iliyopita, hata akawaamuru wengine waache ubabe.

Alitaka kuonewa huruma. Alitaka kuwashitaki kwa wananchi – waonekane wabaya, awe mzuri.

Rais anawasema mawaziri wake kama watoto wadogo wanaohangaika kuelewa kitu kidogo anachowafundisha. Anawaonyesha wananchi kwamba ana mawaziri mizigo, mbumbumbu – ambao kazi pekee wanayofanya ni “kumwangusha” rais.

Anataka turudi kwenye propaganda za kijinga walizoimba miaka mitano iliyopita, kwamba rais pekee ndiye anachapa kazi, bali mawaziri wake wanamwangusha.

Anawaambia mawaziri wake kuwa kama hawawezi kazi “waondoke,” kana kwamba hajui uwezo wao, hajui waliingiaje, wakati ndiye aliyewateua na ndiye ana mamlaka ya kuwaondoa.

Anataka “watoke” waende kwa wananchi kufafanua mafanikio ya serikali yake. Haamini kwamba wananchi wana uwezo wa kuona mazuri na mabaya ya serikali – bila kusubiri taarifa za mawaziri.

Haoni kwamba serikali inayofilisika na kulazimika kukopa hata mishahara ya watumishi wake, inahitaji kubana matumizi na kupunguza ziara na posho nono za viongozi hao waandamizi.

Lakini pia, tunapowatazama watu wenyewe aliokuwa anawapa somo, tunabaki kujiuliza: Rais amepata wapi hekima hii ya kudhani ana uelewa mpana kuliko mawaziri wake?

Amesomea wapi huko wasikojua wao, alikopata hicho cha kuwafunda? Tunapowatazama baadhi yao tunagundua kwamba kama rais angekuwa na busara ya kujifunza kutokana na miaka mitano iliyopita, asingewaita mawaziri kuwafunda, bali angewaita ili wakae kama timu, awaombe ushauri, awasikilize, wampe mang’amuzi yao na mipango mkakati; naye baada ya kuwasikiliza na kuongeza maono yake, awapangie kazi na kuwadai matokeo baada ya muda kadhaa.

Au basi angeunda kikosi kazi cha wasomi waliokubuhu kutoka taasisi mbalimbali zinazoheshimika, akawakutanisha na wasaidizi wake, wote pamoja wakavuna maarifa ya ziada katika kuboresha kazi zao na kukosoa kasoro za huko nyuma.

Angejenga mazingira ya kuambizana ukweli, naye akaambiwa kasoro zake; hasa kwamba serikali imekosa mipango mkakati mbadala na hata hiyo iliyopo imekosa msimamizi makini.

Kitendo cha rais kulialia mbele ya wateule wake na wananchi kupitia vyombo vya habari si ishara ya ushupavu anaostahili kuwa nao kiongozi mkuu wa nchi.

Ndiyo! Tuliona wameinama na kushika tama alipokuwa anafoka. Lakini ana uhakika gani kwamba walikubaliana naye? Ana uhakika gani kwamba walimwona shujaa?

Na kwa kiongozi ambaye ameongoza nchi kwa miaka mitano kwa hotuba na matamko yasiyotekelezeka, anadhani mawaziri wake watamwamini na kumheshimu baada ya kufokewa hadharani Dodoma?

Labda, watamshukuru kwa kuwatengenezea mazingira ya kula posho za safari. Lakini naamini mawaziri wenyewe wanajua fika kwamba hawana sababu ya kusafiri hadi vijijini kila mara, maana huko kuna watendaji wa ngazi za chini wanaopaswa kusimamia kazi na kuleta taarifa kwa ngazi za juu.

Sasa kama rais anaagiza mawaziri waende wenyewe vijijini, hao watendaji wa mikoani, wilayani na vijijini kwenyewe watafanya kazi gani?

Hivi waziri aliyekaa katika wizara ile ile kwa miaka mitatu au zaidi, ana kitu gani cha kujifunza kwa rais aliyekaa madarakani kwa miaka mitano bila maono na mafanikio yanayoshikika?

Rais Kikwete ana mfano gani wa utendaji uliotukuka anaoweza kuutumia kuwasuta mawaziri wake? Aliacha urithi gani katika wizara alizowahi kuongoza kabla hajawa rais?

Ni nani anayejua matatizo, changamoto, na suluhisho la matatizo yake, kati ya waziri aliye kwenye wizara hiyo hiyo, na rais “anayeishi kwenye ndege?”Baadhi yetu tunajua kwamba mkwamo mkubwa wa kiutendaji unatokana na madaraka makubwa ya rais, nidhamu ya woga ya wasaidizi wake na utovu wa uzalendo wa baadhi yao.

Zipo taarifa kwamba siku hizi wasaidizi wa rais wameamua kumwambia yale anayotaka kusikia, kwa sababu anawafokea hovyo hovyo wanapomweleza asiyotaka, au wanapompa mapendekezo magumu.

Wanadai rais hataki kuambiwa asichotaka; nao hawako tayari kupoteza kazi zao.

Kwa mantiki hii, haiwezekani kwamba baadhi ya wasaidizi wa rais wana nafuu kuliko yeye? Kwanini tusiamini, basi, kwamba rais ndiye anawaangusha wasaidizi wake?


15 Jun 2010

Wakati Waingereza wanasubiri Bajeti ya Dharura ya Serikali mpya iliyoingia madarakani hivi karibuni,watawala hapa wameweka bayana kuwa baadhi ya hatua zitakazochukuliwa kurekebisha uchumi zitapelekea machungu kwa wananchi wengi.Hakuna haja ya kudanganyana kwa vile hata wangeficha ukweli huo,muda wa makali hayo ukifika watawala wangeumbuka.Na ni vema pia kuwatayarisha wananchi ili pindi hali itapokwenda mrama wawe katika tahadhari na wamejiandaa vya kutosha.

Lakini kwa watawala wetu,kusema ukweli ni kama kujivunjia heshima.Na si kwa wao tu,bali hata wananchi wanapoamua kuweka bayana hisia zao kuwa nchi yetu inapelekwa pabaya,watawala wanaona kama wanakosewa heshima.Kilichopelekea niandike makala hii ni kauli ya Rais Jakaya Kikwete kuwa ahadi ambazo hazijatekelezwa katika miaka minne iliyopita zitatekelezwa katika bajeti hii.Sijui ni ushauri mbovu wa washauri wake,sijui ndio kampeni,au sijui ni kuwafanya Watanzania mabwege sana,lakini kwa kila anayefahamu hali ya uchumi wetu na wingi wa ahadi zilizokwishatolewa ni dhahiri kuwa kauli hiyo sio ya kweli.

Kikwete anapaswa kurejea ahadi alizotoa wakati wa kampeni zake mwaka 2005,na alizoendelea kutoa katika miaka minne iliyopita,kisha angejaribu kuangalia nini kimekwaza ahadi hizo.Hebu kwa minajili ya makala hii tuangalie baadhi ya ahadi hizo na kutathmini kama kweli bajeti hii ya kutegemea hisani za wafadhili itaweza kutimiza ahadi hizo.JK alinukuliwa mwezi August 2008 akisema tatizo la umeme lingepatiwa ufumbuzi wa kudumu.Miezi michache baadaye ufumbuzi ukapatikana,si kwa wananchi bali kwa akaunti za matapeli wa Richmond.Je ni kweli kuwa bajeti hii itaweza kutimiza ahadi hiyo ya JK kuhusu tatizo la umeme?Na mbona hatuelezi utatuzi huo utakuwaje?

Twende kwenye suala la rushwa na ufisadi.JK alitamka bayana kuwa watu wasitafsiri vibaya tabasamu lake kwani hatakuwa na huruma kwa fisadi yoyote yule.Akaenda mbele zaidi kutanabaisha kuwa anawafahamu wala rushwa na anawapa muda wa kujirekebisha.Sote tunajua kinachoendelea katika Awamu hii ya Nne chini ya JK.Ufisadi umeota mizizi kupita kiasi huku mafisadi wakiendelea kulindwa,na wanaojiuzulu wanafarijiwa kuwa "kuna siku watarejea serikalini".Hivi ni kweli kuwa bajeti hii itawezesha utekelezaji wa ahadi hiyo ya JK kupambana na mafisadi?Kilichomshinda katika miaka minne iliyopita kitawezekanaje miezi hii michache kabla ya uchaguzi?Na je inahitaji bajeti moja kabla ya uchaguzi kumwezesha kuwadhibiti mafisadi?


Anyway,hebu soma kauli zake katika habari ifuatayo kisha ufanye tafakuri jadidi 



Ahadi za JK kukamilika Bajeti hii
Imeandikwa na Na Maulid Ahmed, Dodoma; Tarehe: 12th June 2010 @ 23:52

Ahadi ambazo hazijatekelezwa na Serikali ya Awamu ya Nne zitatekelezwa katika Bajeti hii ya mwaka 2010/11, imeelezwa.

Akizungumza jana mjini hapa katika kikao cha kazi na wakuu wa mikoa na wa wilaya pamoja na makatibu tawala wa mikoa yote Tanzania Bara, Rais Jakaya Kikwete aliwataka viongozi hao kusimamia shughuli za Serikali kikamilifu.

Aliwataka kutokwenda likizo katika kipidi hiki cha kuelekea uchaguzi na wasimamie kazi kama wanavyofanya wakati wote.
Rais Kikwete alisema katika kipindi cha miaka mitano tangu Serikali yake iingie madarakani mengi waliyoahidi yametekelezwa.

“Juzi kabla ya Bajeti hata kwenye Baraza la Mawaziri, tulizungumzia ahadi zetu na nyingi tumeshazitekeleza, lakini zilizobaki na majukumu tuliyojipangia kwa miaka yote hii tutatekeleza katika Bajeti hii … tulipoingia mwaka wa kwanza, tulitekeleza ya Awamu ya Mzee Mkapa (Rais mstaafu Benjamin) sasa tunaendelea na kutekeleza yetu,” alisema.

Akizungumzia uchaguzi mkuu Oktoba mwaka huu, alisema “tunakwenda kwenye uchaguzi na michakato imeshaanza, lakini Serikali haiendi likizo, usione uchaguzi nawe ukaenda likizo, fanya shughuli za maendeleo kwa kuzisimamia kama mnavyofanya wakati wote”.

Alisema hataki kuona uchaguzi unaharibikia mikononi mwa viongozi hao na kuwataka kuhakikisha wagombea hawanyimwi haki ya kumwaga sera zao majukwaani, kura zinapigwa kwa amani na kunakuwa na utulivu wakati wote, kuanzia mchakato wa wagombea hadi uchaguzi.

Rais Kikwete aliyehutubia viongozi hao kwa dakika 10, alitaja baadhi ya mafanikio ya Serikali yake, kuwa ni kuendelea na ujenzi wa barabara za lami, watoto kusoma elimu ya msingi na sekondari, upanuzi wa elimu ya juu na huduma bora za afya kupatikana...

CHANZO: Habari Leo

26 May 2010

Tanzania imeshuhudia vituko vingi mwezi huu wa Mei,kutoka Rais Kikwete kutetea takrima  hadi mtumishi wa Bwana Askofu Kilaini kudai kuwa Kikwete bado ni chaguo la Mungu,kutoka sakata la Masauni kufoji umri (oh Mungu, inawezekanaje?) hadi kifungo cha Liyumba (wengine wanadai alistahili kunyongwa kabisa).Na kutoka kauli ya Waziri Kombani kuwa daraja la mto Kilombero litajengwa katika awamu ya pili ya Kikwete (as if JK ameshashinda uchaguzi) hadi ajali ya gari la msafara wa JK.Makala hii inajaribu kuibua maswali kuhusu hili la mwisho,yaani ajali hiyo.


Kwa mujibu wa vyombo vya habari,uchunguzi mkali unaendelea ku-establish chanzo cha ajali hiyo.Lakini wakati uchunguzi huo ukiendelea tayari kuna wingu limeigubika ajali hiyo huku kukiwa na maswali kama ilitokana na hujuma,au uzembe au ni bahati mbaya tu.

BAHATI MBAYA: Kwa mujibu wa Msemaji Mkuu wa Jeshi la Polisi,ajali hiyo ni bahati mbaya.Gazeti la Tanzania Daima limemnukuu Msika akisema, “Tunaamini ni ajali ya bahati mbaya ambayo ilisababishwa na matatizo ya kiufundi, lakini jambo la kushukuru kiongozi wetu hakupata madhara kwa matukio yote mawili.” Yah,inawezekana ni bahati mbaya.Lakini kichekeksho ni pale Msika kutoa kauli hiyo kabla ya uchunguzi.Majibu rahisi katika maswali magumu?Well,hiyo ndio Bongo yetu.Kauli hiyo ya Msika inaweza kupewa nguvu na kauli nyingine iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Ikulu,Salva Rweyemamu,aliyenukuliwa na gazeti hilohilo la Tanzania Daima (toleo la Jumapili) akisema "hitilifu za magari alizokabiliana nazo Rais Kikwete zilikuwa ni za kawaida".Again,tunashuhudia watu walokabidhiwa dhamana muhimu wakikurupuka kutoa majibu mepesi hata kwenye masuala nyeti.Yani kuchomoka tairi ya gari la kiongozi wa nchi ni kitu cha kawaida!Au ni kwa vile ajali kubwa zimezoeleka sana kiasi kwamba hiyo ya msafara wa JK inaonekana 'cha mtoto'?

HUJUMA: Kwa mujibu wa gazeti la Tanzania Daima,kamanda Msika haamini kuwa ajali hiyo ilisababishwa na hujuma.Anasema, "Nasisitiza hatuamini kama kulikuwa na hujuma na ndiyo maana hatutafanya uchunguzi kuhusu matukio yote mawili, lakini kwa suala kama kulikuwa na uzembe wa ukaguzi wa gari, mtafute Salva (Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu), ndiye anaweza kulizungumzia.” Kwa mara nyingine tena tunashuhudia Msika akitoa majibu ya hisia zake (na pengine Jeshi analoongoza) badala ya kusubiri matokeo ya uchunguzi wa kitaalam.Hivi kulikuwa na ugumu gani kwa Msemaji huyo wa jeshi la polisi kutoa jibu lenye mantiki kwamba 'tusubiri matokeo ya uchunguzi badala ya kufanya guesswork'?
Tanzania Daima linakwenda mbali zaidi na kuihusisha ajali hiyo na matukio ya mbalimbali ambapo Rais amekuwa akipewa taarifa potofu (rejea Muswada wa Sheria ya Gharama za Uchaguzi na taarifa za vikao kati ya TUCTA na Serikali).Kwa mtizamo mpana,gazeti hilo linajaribu kueleza kuwa yayumkinika kuhisi kuwa ajali hiyo ni muendelezo wa 'hujuma' zinazofanywa dhidi ya Rais Kikwete.

Kwa bahati mbaya (au kwa makusudi) Watanzania hawatapata fursa ya kujua ukweli kuhusu tukio hilo.Kwanini nahitimisha hivyo?Well,labda mwenzangu umeshasahau kuhusu ripoti ya chanzo cha milipuko ya mabomu huko Mbagala.Najua kwa wengine,nikitaja Mbagala wanakumbuka zaidi kuhusu mwana-Bongofleva Diamond kuliko ukweli kwamba kuna wenzetu walipoteza maisha yao,tukaambiwa tume imeundwa kuchunguza milipuko hiyo,tukaonyeshwa picha ripoti ikikabidhiwa kwa waziri husika,na hadithi ikaishia hapo.Na kama hufahamu,tume iliyoundwa kuchunguza milipuko hiyo ilitumia fedha za walipa kodi.Sasa sijui wana-tume waliamua kufanya uchunguzi wao baa kisha 'kutokana na kilevi' wkaafikiana kuwa hakuna haja ya kuweka hadharani ripoti hiyo.

UZEMBE: Ni rahisi zaidi kuhisi kuwa ajali hiyo sio bahati mbaya au hujuma bali ni uzembe kwa kuangalia mlolongo wa matukio ya uzembe yanayojiri mara kwa mara.Kwa bahati mbaya,au makusudi,baadhi ya matukio hayo yanamhusisha Rais Kikwete moja kwa moja.Hebu angalia ishu ya Masauni,kwa mfano.Katika kudhibiti songombingo kati ya (Benno) Malisa na Bashe huko UVCCM,JK alionelea ni vema Mwenyekiti wa Umoja huo atoke Zanzibar.Na huyo ndiye Masauni.Kwa hiyo tunapozungumzia 'fojari' ya umri wa Masauni tunapaswa pia kukumbuka nani aliyemuibua.

Lakini tofauti na uzembe uliozoeleka katika shughuli mbalimbali za serikali,huu wa ajali ya gari la Rais hauwezi kuhusishwa na rushwa.Unajua,mara nyingi neno 'uzembe' linatumika kupunguza makali ya neno 'rushwa'.Yaani,utaskia mtu flani 'alifanya uzembe kusaini mkataba flani' lakini ukweli ni kwamba mtu huyo hakuwa mzembe bali alikuwa makini katika kuhakikisha teni pasenti inakwenda kwenye akaunti yake.

Kwanini ajali hii inaweza kuwa matokeo ya uzembe?Kwa wenye ufahamu wa usalama wa kiongozi kama rais,gari analotumia linapewa uangalizi wa hali ya juu kama ilivyo kwa afya,ustawi na usalama wake kwa ujumla.Kuna mlolongo wa watu (wanaolipwa vizuri tu) wanaowajibika kuhakikisha kuwa kila atakachotumia rais kipo katika hali nzuri (na ya juu kabisa).Sitaki kuingia kwa undani sana katika hili kwa sababu zangu binafsi,lakini nachoweza kusema hapa ni kuwa kuna wazembe flani ambao hawakutilia maanani hitilafu zilizojitokeza katika chombo cha usafiri wa rais.

Tatizo linaloweza kuwa limepelekea uzembe huo ni MAZOWEA.Nadhani kuna wanaokumbuka masahibu yalomkumba JK wakati wa kampeni yake huko Mwanza mwaka 2005.Naamini pia kuna wanaokumbuka balaa lilomkumba Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi pale aliponusurika kupigwa akiwa msikitini jijini Dar.Nahisi pia kuna wengi wanaokumbuka habari za msafara wa Kikwete kurushiwa mawe huko Mbeya.Matukio yote hayo yanaweza kuhusishwa na ajali hii ya gari la Rais,na yote yananyooshea kidole uzembe mahala flani.

Nihitimishe makala hii kwa kuusia kwamba matukio kama hilo la ajali ya gari la Rais yataendelea kutokea kama tutaendelea kukabidhiana majukumu kwa minajili ya urafiki (au kishkaji,kama wasemavyo mtaani.Tunapoweka kando professionalism na kuruhusu umimi tutambue kuwa tunajichimbia kaburi letu sie wenyewe.Ujuzi na uzoefu hauwezi kuwa replaced na udini,urafiki au kujuana.

Mwenye macho na asome,mwenye masikio na asikie.

You have been warned!

26 Feb 2010



Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia Rushwa TAKUKURU Dr. Edward Hosea akimkaribisha Rais Jakaya Mrisho Kikwete kufungua mkutano mkuu wa Mwaka wa taasisi hiyo.Picha kwa hisani ya MJENGWA

Hivi karibuni,uongozi wa kampuni ya magari ya Toyota ya Japan ulifanya jambo moja la kiungwana kwa kuwaomba radhi wateja wake kutokana na hitilafu za kiufundi katika modeli moja ya magari yake.Japo sakata hilo bado ni bichi hasa kwa vile inaelekea hitilafu hiyo bado haijapatiwa ufumbuzi,na tayari kuna habari za kushuka kwa hisa za kampuni hiyo katika masoko mbalimbali ya mitaji duniani,ni dhahiri hatua ya kuomba radhi imeonyesha kwamba kwa namna flani kampuni hiyo inatambua wajibu wake na inawajali wateja wake.

Majuzi,Rais Jakaya Kikwete alimwaga sifa kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) huku akijigamba kwamba serikali ya awamu ya nne imekuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya rushwa.Binafsi sidhani kama kauli hiyo ya JK inaendana na hali halisi ya utendaji na ufanisi wa TAKUKURU.

Kimsingi,tatizo haliko kwenye taasisi hiyo pekee bali kwenye medani nzima ya utawala bora.Angalia,kwa mfano,kauli za Waziri mwenye dhamana ya Utawala Bora,Mheshimiwa Sophia Simba,wakati wa sakata lililowahusisha wafanyabiashara wawili mashuhuri Bwana Reginald Mengi na Bwana Rostam Aziz.Badala ya kuhamasisha wananchi wanaojitokeza kuwaumbua hadharani mafisadi,Waziri Simba aliamua kuelemea upande mmoja ambapo bila aibu alimkemea Bwana Mengi huku akimlinda Bwana Rostam.

TAKUKURU hiyohiyo inayopongezwa na JK haijafanikiwa kujisafisha na tuhuma za namna ilivyouhadaa umma kuhusu suala la utapeli wa kampuni ya Richmond.Kamati ya Bunge iliyoundwa kuchunguza sakata hilo ilipendekeza Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Dr Edward Hosea,uamuzi ambao uko mikononi wa aliyemteua Hosea,yaani JK mwenyewe.Kwa hali ilivyo,na ukitilia maanani pongezi alozotoa JK kuhusu ufanisi katika mapambano dhidi ya ufisadi,ni dhahiri kuwa Rais hana mpango wa kumwajibisha Dr Hosea.

Nimesema tatizo liko kwenye utawala bora kwa vile hata chama tulichokipa dhamana ya kutuongoza-CCM-kimeendelea kufanya dhihaka linapokuja suala la utawala bora.Hivi inaingia akilini kweli kusikia kuwa Mbunge wa Bariadi,Bwana Andrea Chenge,bado ni mwenyekiti wa kamati ya maadili ya chama hicho tawala licha ya kuhusishwa kwake na tuhuma za ufisadi wa ununuzi wa rada!?Tusisahau kuwa pamoja na mageuzi ya kisiasa ya miaka ya tisini,bado chama tawala kimeendelea kuwa na nguvu pengine zaidi ya serikali,hoja kubwa ikiwa serikali hiyo imeundwa kutokana na ushindi wa chama husika.Kinachopuuzwa ni ukweli kuwa chama hicho hakikuomba ridhaa ya wanachama wake pekee bali Watanzania kwa ujumla.

Ni dhahiri kwamba kunakosekana utashi na udhati wa kupambana na ufisadi.Na kikwazo kikubwa kimeendelea kuwa kuweka mbele maslahi binafsi na ya chama badala ya maslahi ya umma/taifa.Pengine,na kwa hakika,badala ya kutetea mapungufu,ni muhimu kwa CCM na serikali yake kuiga mfano wa kampuni ya Toyota.Imetuangusha sana sio tu kwa kulegea katika mapambano dhidi ya ufisadi bali pia kwa ushiriki wake kwa kuwalinda watuhumiwa wa ufisadi.Laiti chama hicho kingekuwa na dhamira na utashi wa kukabiliana na ufisadi basi ni dhahiri Kamati ya Mwinyi inayoshughulikia mpasuko ndani ya chama hicho (wengine wanadai hakuna mpasuko) ingekuwa na kazi nyepesi tu ya kupendekeza wahusika wafikishwe kwenye vyombo vya sheria ili wasafishwe au waadhibiwe huko.Ikumbukwe kuwa tuhuma zinazowakabili watuhumiwa hao hazijaiathiri CCM pekee bali Watanzania wote kwa ujumla.

Nimalizie kwa kukumbushia usemi wa Kiingereza kwamba To err is human but to rectify is greatness,yaani (kwa tafsiri isiyo rasmi) kukosea ni ubinadamu lakini kujirekebisha ni uungwana.

19 Dec 2009


Ahadi za urais 2005 zamtesa Kikwete uchaguzi wa mwakani

Rais Jakaya Kikwet, mzigo mzito wa ahadi zake za mwaka 2005 unamkabili uchaguzi ujao 2010.
Na Mwandishi Wetu
MIEZI michache ikiwa imebaki kabla ya kuanza kwenda kwa wananchi kuomba ridhaa ya kuongoza nchi kwa kipindi kingine cha miaka mitano, Rais Jakaya Kikwete anaonekana kukabiliwa na mzigo mzito wa kutekeleza ahadi nyingi alizozitoa wakati wa kampeni za mwaka 2005.

Kikwete alipata ushindi wa kishindo kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 baada ya kunyakua takriban asilimia 80 ya kura, akiwa pia ameshinda kwa kishindo dhidi ya wapinzani wake kwenye uteuzi wa mgombea wa CCM.

Lakini kadri muda unavyokwenda ndivyo umaarufu wake unaonekana kupungua huku tafiti mbalimbali zikionyesha kuwa umaarufu aliokuwa nao wakati akiingia madarakani unaendelea kuporomoka, ikiwa ni miezi tisa kabla ya uchaguzi mkuu wa mwakani.

Wakati akizunguka sehemu mbalimbali nchini kuomba kura za wananchi, Kikwete alikuwa akitoa ahadi kem kem ambazo alizielezea kwa kifupi kwenye kauli mbiu yake ya â€Å“Naisha Bora kwa Kila Mtanzania” ambayo mkakati wake wa kuitekeleza ulikuwa ni â€Å“ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya”.

Mbali na ahadi ambazo alikuwa akizitoa kwa wananchi kila sehemu alipoelezwa tatizo, ikiwa ni pamoja na matatizo sugu ya maji, miundombinu, huduma za afya na pembejeo, Rais Kikwete pia alitoa ahadi za ujumla kabla na baada ya kushinda uchaguzi kumrithi Benjamin Mkapa.

Baadhi ya ahadi hizo za Rais Kikwete kabla na baada ya kuingia madarakani ni pamoja na kuweka kipaumbele katika kilimo, akitumia kaulimbiu ya Kilimo Kwanza, kupitia upya mikataba ya madini ili inufaishe nchi na wawekezaji, na kuhakikisha kuwa hakuna mwanafunzi wa elimu ya juu anayekosa masomo kwa kukosa karo.

Ahadi nyingine ni pamoja na ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule za umma, kuumaliza mgogoro wa Zanzibar, kuimarisha uhusiano wa kimataifa, kukomesha tatizo la ufisadi, kupambana na tatizo la uhalifu, ikiwa ni pamoja na biashara ya dawa za kulevya na ujambazi, kuandaa mdahalo wa kitaifa wa michezo kwa lengo la kuinua michezo na ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma....INAENDELEA HAPA

17 Dec 2009


Waziri wa Sheria adai Bunge la sasa halina ubavu kwa serikali
Na Leon Bahati
WAZIRI wa Sheria na Katiba, Mathias Chikawe amezidi kutoa kauli tata baada ya kuligeukia Bunge la Jamhuri ya Muungano, akisema halina nguvu ya kuilazimisha serikali kufanya mambo na kwamba kazi yake ni kuishauri.

Hiyo ni kauli ya pili ya waziri huyo katika kipindi kisichopungua wiki moja baada ya kukaririwa Jumatatu akisema kuwa Rais Jakaya Kikwete hana uwezo wa kuwachukulia hatua watuhumiwa wa ufisadi kwa kuwa mfumo wa utawala wa sheria hauruhusu vitendo kama hivyo.

Kauli hizo mbili zinazohusu mamlaka ya kisheria zimetolewa katika kipindi ambacho mjadala mkubwa wa hatua zinazostahili kuchukuliwa dhidi ya watuhumiwa katika kashfa ya utoaji zabuni ya uzalishaji umeme wa dharura kwa kampuni ya Richmond Development (LLC) ukiwa umemgeukia rais.

Pia Chikawe ametoa kauli hiyo wakati Bunge likiishinikiza serikali kutoa taarifa ya utekelezaji wa maazimio yake 23 dhidi ya wahusika kwenye kashfa hiyo kubwa iliyotikisa nchi baada ya Edward Lowassa kujiuzulu wadhifa wake wa uwaziri mkuu kutokana na ushauri uliotolewa na kamati teule ya Bunge iliyoundwa kuchunguza kashfa hiyo....INAENDELEA HAPA

16 Dec 2009


Prof Shivji asema Rais Kikwete ana mamlaka kisheria kuwabana mafisadi
*WENGINE WAMTAKA WAZIRI CHIKAWE AACHE KUKURUPUKA
Na Sadick Mtulya

SIKU moja baada ya Waziri wa Sheria na Katiba Mathias Chikawe kusema Rais Jakaya Kikwete hawezi kutumia mamlaka yake kuwabana mafisadi, baadhi ya wanasheria nchini, akiwamo Profesa Issa Shivji, wamepinga kauli hiyo kwa kusema sio kweli.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili jijini Dar es Salaam jana wanasheria hao walisema rais anaweza kuwabana mafisadi kwa kutumia mamlaka yake ndani ya chama na serikali.

Profesa Issa Shivji alisema Rais Kikwete anaweza kupambana na watuhumiwa wa ufisadi kwa kuwavua madaraka walionayo katika chama au serikali.

Gwiji hilo la Sheria na Mwenyekiti wa Kigoda cha Mwalimu Nyerere, alisema kama watuhumiwa watakuwa watumishi wa serikali au watendaji katika mashirika ya umma, rais anaweza kuwawajibisha kwa kutumia sheria na kanuni za utumishi wa umma.

"Kumwajibisha mtuhumiwa sio iwe kumpeleka mahakamani, unaweza kuchukua hatua za awali ikiwemo kumvua nyadhifa zote. Kama ni mwanasiasa au mtumishi katika serikali na mashirika ya umma, unaweza kumwajibisha kwa mujibu wa sheria za umma," alisema Profesa Shivji.

Alisisitiza Kusema Rais Kikwete hana uwezo wa kuwabana mafisadi sio kweli na Watanzania wanatakiwa kuelewa hivyo kwamba rais anaweza.

Kauli ya Profesa Shivji iliungwa mkono na Profesa Abdallah Safari, aliyetia ngumu akisema sheria za nchi ikiwemo ya utawala, inampa uwezo na mamlaka rais kupambana na vitendo vya ufisadi ndani ya serikali yake na hata katika chama chake.

Rais kukasimu mamlaka yake kwa Takukuru (Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ) na kwa DPP haimaanishi kwamba sasa yeye hana uwezo wa kupambana na watu wanaojihusisha na ufisadi. Bado anao, alisema Profesa Safari....INAENDELEA HAPA

Alifafanua kwamba, Rais Kikwete anayewajibika katika kupambana na ufisadi kwa kuwa yeye ndiye anayewajibika moja kwa moja kwa wananchi wa Tanzania.

14 Dec 2009



Waziri Chikawe asema Kikwete hawezi kuwabana mafisadi
*Asema Rostam, Dk Hoseah hawakamatiki
*Asikitika DPP, DK Hoseah kuparuana

Na Leon Bahati

WAZIRI wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe amesema Rais Jakaya Kikwete hana uwezo kutumia mamlaka yake kuwapeleka mahakamani watuhumiwa wa ufisadi kwani hilo ni jukumu la vyombo alivyoviteua kuchunguza na kuchambua nani afikishwe huko baada ya kujiridhisha kwa ushahidi.

"Huu ni utawala wa sheria, Rais Kikwete hawezi kutoa amri za kukamata watu wakati kuna vyombo alivyoviteua kuchunguza na kuchukua hatua." Waziri Chakawe alisema hayo jana alipokuwa katika mahojiano maalumu na gazeti hili ofisini kwake jijini Dar es Salaam.

Alisema kitendo cha baadhi ya Watanzania kumshinikiza Rais Kikwete awafikishe mahakamani watuhumiwa wa ufisadi kinaashiria kuwa wanataka aamuru watuhumiwa hao wapelekwe mahakamani bila kutumia vyombo husika jambo ambalo haliwezekani katika mfumo wa kibepari.

"Enzi zile za mfumo wa ujamaa na chama kimoja cha siasa, hilo lingewezekana lakini wakati huu ambao nchi inatumia mfumo wa kibepari, haiwezekani," alisema Chikawe.

Hivi karibuni, wanasiasa na hata baadhi ya viongozi waliowahi kuwa serikalini awamu zilizopita, wakichangia mada ya mustakabali wa taifa kwenye kongamano la taasisi ya Mwalimu Nyerere, waliitaka CCM imtose Rais Kikwete asigombee tena ili kumalizia ngwe ya miaka mingine mitano, iwapo atashindwa kufanya maamuzi magumu ya kuwachukulia hatua watuhumiwa wa ufisadi.

Alionya kwamba Rais Kikwete akikurupuka katika hilo, kesi nyingi zitakwaa kisiki mahakamani na itabidi hao wanaoitwa mafisadi kulipwa mabilioni ya fedha kama fidia ya usumbufu.

Chikawe alisema mawazo ya namna hiyo yanatokana na watu wengi kuendelea kuwa na mtazamo wa mfumo wa kijamaa na chama kimoja na kusahau kuwa tayari nchi imeingia katika mfumo wa kibepari.

Waziri Chikawe alitumia mfano wa enzi za waziri mkuu, hayati Edward Sokoine alipopambana na wahujumu uchumi kwa kutoa amri ya kukamatwa watu ovyo na kutaifishwa mali zao kuwa moja ya mifano ya uongozi katika mfumo wa ujamaa.

Alisema amri hizo zilikubalika kulingana na mazingira ya wakati lakini, ulipoanza kuingia mfumo wa kibepari waliopoteza mali kupitia operesheni hiyo walidai haki kupitia mahakama na walishinda hivyo serikali ikabidi iwafidie pamoja na usumbufu.

Waziri huyo mwenye dhamana ya kusimamia katiba na sheria za nchi, ambaye amekuwa kimya licha ya kuwepo na mijadala mingi inayokosoa utendaji wa vyombo vya sheria nchini hasa suala la ufisadi, alisema polisi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) wana haki ya kuchunguza makosa ya jinai, lakini pia mkurugenzi wa mashtaka (DPP) ana mamlaka ya kutoruhusu kesi hizo zisiende mahakamani kama hakutakuwa na ushahidi wa kutosha.

Alitoa mfano wa Mbunge wa Igunga, Rostam Azizi (CCM) ambaye wengi wamekuwa wakimtuhumu kwa ufisadi kupitia kashfa ya kampuni tata ya Richmond iliyopewa zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura mwaka 2006, akisema hakuna ushahidi wa kumfikisha mahakamani.

"Wewe jaribu kuipitia ile ripoti ya Kamati Teule ya Bunge ya (Dk Harrison) Mwakyembe, hata uipitie mara 10. Mimi nimeipitia mara nane, sijaona sehemu ya kupata ushahidi wa kumshtaki," alisema Chikawe.

Kuhusu anwani ya barua pepe ya kampuni ya Caspian ambayo inamilikiwa na Rostam kutumiwa na kampuni iliyoirithi Richmond, alisema: "Ni sawa, lakini hadi sasa hakuna mahali popote ambapo kampuni ya Dowans inatuhumiwa. Yenyewe ilipokea jukumu ambalo Richmond ilishindwa lakini wao wakatekeleza. Ingekuwa Dowans wana matatizo, basi hata Rostam angeweza kuhusishwa."

Alizungumzia shinikizo la kutaka Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk Edward Hoseah awajibishwe kwa madai ya kuficha madhambi ya Richmond ambayo kamati ya Dk Mwakyembe iliyaweka wazi, alisema:

"Takukuru ilichunguza mwenendo wa utoaji wa zabuni kwa Richmond na kwenye ripoti yake ikaeleza haikuona fedha zilizotumika kurubuni mtu yeyote. Na hata kamati ya Dk Mwakyembe haikubaini kitu cha namna hiyo.

"Kamati ya Dk Mwakyembe imebaini udhaifu wa serikali kuchunguza Richmond kabla ya kuingia mkataba na hili ndilo lililofanya Lowassa na wenzake kujiuzulu na Baraza la Mawaziri kuvunjwa."

"Lakini uzuri ni kwamba Rais Kikwete alikuwa ameagiza wasipewe fedha hadi wawe wameleta mitambo nchini na hilo lilifanyika. Kampuni ya Richmond haikuchukua hata senti ya serikali. Kama ilihonga watu kwa siri huko, ilikula kwao. Ila tunachojua walishindwa kuleta mitambo ya kuzalisha umeme wakatoa kazi hiyo kwa Dowans ambao walifanikisha."

Pamoja na hali hiyo, Chikawe alisema Mtanzania yeyote mwenye ushahidi unaoweza kuwashtaki wanaotuhumiwa ni vyema akawasiliana na Mpelelezi Mkuu wa Makosa ya Jinai (DCI) au Takukuru.

Kuhusu majibizano yaliyotokea hivi karibuni baada ya Dk Hosea kumlaumu DPP, Elieza Feleshi kwa kukalia mafaili zaidi ya 60 ya kesi za ufisadi na baadaye Feleshi kumjibu kuwa ni muongo, Chikawe alisema ni jambo ambalo halikumpendeza.

"Kwa kweli imekuwa bahati mbaya vyombo hivi vya serikali kulumbana vyenyewe, lakini nafikiri ilikuwa ni bahati mbaya tu, wakati mwingine hilo halitatokea," alisema Chikawe.

Hata hivyo, alisema huenda lilichangiwa pia na vyombo vya habari kwa kuchokonoa mambo hayo hivyo kuwafanya kutoa kauli ambazo pengine zilionekana kuhitilafiana.

Chikawe ambaye ni Mbunge wa Nachingwea alisisitiza kwamba DPP amekuwa akipelekewa mafaili mengi na anapoona hayana ushahidi wa kutosha huwashauri wahusika mambo ya kufanya na pengine kuwaeleza kwamba hakuna kesi ya kujibu.

CHANZO: Mwananchi

13 Dec 2009


Mara Sophia Simba dhidi ya Anne Kilango,mara Rostam Aziz dhidi ya Mwakyembe,mara tunaambiwa Kamati ya Mwinyi nako "hakieleweki",na sasa watendaji wakuu na wateuliwa muhimu wa Rais,Mkurugenzi wa TAKUKURU Dr Edward Hosea na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) Eliezer Feleshi nao wameingia kwenye malumbano,kama linavyoripoti jarida la Mwananchi

DPP amvaa Dk Hoseah, ataka mdahalo majalada kesi za kifisadi

Mkurugenzi mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hoseah ambaye jana alidai kuwa DPP amekalia kesi 60 tuhuma za rushwa

James Magai

KWANZA ilikuwa ni ndani ya chama tawala CCM, lakini malumbano baina ya vigogo sasa yamehamia serikalini baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Eliezer Feleshi kujibu mashambulizi ya mkurugenzi mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hoseah, akitaka uitishwe mdahalo baina ya wawili hao ili ajibu tuhuma dhidi yake.

Pendekezo hilo la Feleshi limekuja wakati malumbano baina ya viongozi wa CCM hayajapoa baada ya kutuhumiana kwa ufisadi na wivu wa nafasi mbalimbali zilizotokana na uchaguzi mkuu wa mwaka 2005.

Dk Hoseah, ambaye amekuwa akirusha makombora kwa taasisi tofauti, juzi alitoa tuhuma nzito alipokaririwa na gazeti moja akisema kuwa ameshawasilisha kesi zaidi ya 60 za tuhuma za rushwa kwa DPP na akashangaa sababu za mteule huyo mwenzake wa rais kukalia mafaili hayo badala ya kufungua kesi dhidi ya watuhumiwa.

Lakini jana Feleshi alikuwa mbogo na akasema kuwa ili ukweli uwekwe bayana kuna haja ya kuandaa mdahalo baina yake na Hoseah.

DPP Feleshi, akizungumza na gazeti dada la Mwananchi la The Citizen baada ya hafla ya mafunzo ya kamati ya kitaalamu ya mawakili wa serikali iliyofanyika Kunduchi jijini Dar es Salaam, alisema njia pekee ya kuweka sawa rekodi ni kuwepo kwa mdahalo huo wa wazi.

"Ninataka mdahalo na Hoseah katika masuala haya yanayoendelea hata kama utakuwa wa simu tena iwekwe ‘loud speaker (kipaza sauti)’ ili tujadili masuala haya na kumaliza kiu ya wananchi," aliweka msimamo DD Feleshi.

"Kama mtu anasema kuna majalada 60 ofisini kwangu, then (kisha) tunamuuliza yamefika lini? Yeye pia atajibu, kwa kufanya hivyo tutatoa mwanga mzuri kwa wananchi ambao ofisi hizi zipo kwa ajili yao tu."

DPP Feleshi alisema anataka mdahalo huo ufanyike mbele ya waandishi wa habari ili jamii ijue masuala mbalimbali yanayoelekezwa ofisini kwake.

Hoseah pia aliwahi kuirushia kombora mahakama akisema inaendesha taratibu kesi za ufisadi, hivyo kupunguza kasi ya taasisi hiyo kushughulikia watuhumiwa wa rushwa.

Miongoni mwa kesi ambazo zilifunguliwa kwa wingi hivi karibuni na Takukuru ni pamoja na kesi zaidi ya 20 zinazohusu wizi kwenye Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA), matumizi mabaya ya madaraka na uzembe na tuhuma za kula njama na kuisababishia hasara serikali.

Hata hivyo, mwenendo wa kesi nyingi umekuwa wa kasi ndogo kutokana na upande wa mashtaka kutokamilisha ushahidi.

Akizungumzia madai hayo ya Hoseah, Feleshi aliweka bayana kwamba hayajui majalada hayo na anachojua ni kwamba ofisini kwake kuna majalada ya kesi ambayo yanaingia na kutoka kila siku na anayashughulikia kwa mujibu wa sheria.

Feleshi, ambaye aliwahi kurejesha Takukuru baadhi ya majalada kutokana na kuonekana udhaifu katika ushahidi, alimtaka Dk Hoseah kutoa ufafanuzi kwa kueleza ni majalada gani yanayokaliwa na ofisi yake na yamefika lini.

Alifafanua kwamba ofisi yake haiwezi kukalia majalada kwa kuwa inafanya kazi kwa mujibu wa sheria na kwa maslahi ya umma na kusisitiza hayajui majalada hayo 60 anayodai Dk Hoseah kwamba yamekaliwa ofisini hapo.

"Hayo mafaili (majalada) ya vigogo mimi siyajui. Ninachojua ni kwamba tuna majalada yanaingia kila siku ya Watanzania wanaotuhumiwa. Tunapokea na kuyafanyia kazi... na hatubagui kuwa haya ni ya PCCB (Takukuru) , TRA( Mamlaka ya Mapato) au ya Polisi. Katiba ya nchi inatoa haki sawa kwa wote kufikishwa mbele ya sheria ili kupata haki," aliongeza DPP.

"Tunafanya kazi kwa maslahi ya umma na tunaendesha shughuli zetu kisheria wala si kwa kuzingatia jambo lolote kwa kuwa hatuna maslahi yoyote kumshtaki mtu bila kuwa na ushahidi wala hatuna maslahi yoyote kumwachia mtu kama kuna ushahidi. Ndiyo maana nasema hakuna kukalia majalada."

Feleshi, ambaye ana mamlaka ya kufunga au kufungua mashtaka kwa watuhumiwa, alisema katika hali hiyo ni vigumu kusema kuna majalada yana muda mrefu kwani hajui hayo yanayosemwa yaliingia lini ofisini kwake.

"Labda kama angekuwepo mwenyewe (Dk. Hoseah) angeeleza zaidi hayo majalada anayodai tumeyakalia. Ni vema mkamuuliza hilo," alisema.

Hizi ni dalili za wazi kwamba kuna ombwe la uongozi wa kitaifa.Yaani kila mtu anaropoka anavyopenda hasa kwa vile mwenye jukumu la kukemea yuko usingizini fofofo.Nidhamu imekuwa zero kwa vile anayepaswa kuwaadabisha watovu wa nidhamu yuko bize na mambo mengine yasiyo na umuhimu kwa taifa.

Tunaelekea pabaya japo Watanzania wengi hawaonekani kuguswa na hali hii.

Ni vema tukaamua kuchukua maamuzi mazito kabla hali haijafikia mahala tusipoweza kurekebisha.Tusipoziba ufa tujajenga ukuta.Unfortunately,baada ya ukuta kuanguka kutokana na nyufa zilizopo tunaweza kushindwa kujenga ukuta huo baada ya matofali yote na tanuru zima kuuzwa na mafisadi.

2010 INAKUJA.IT'S THEN OR NEVER!

3 Dec 2009


Sijui tuiweke CCM katika kundi gani maana kila kukicha ni songombingo moja baada ya nyingine.Of course,migongano ni jambo la kawaida kwani hata ukiweka glasi katika boksi moja zinaweza kugongana kama si kuvunjika kabisa.Ndio maana maboksi yaliyosheheni glasi huwa na tahadhari "handle with care" au "fragile".

Pengine kabla sijaendelea na mada yangu kuhusu utovu wa nidhamu unaoendelea ndani ya chama tawala CCM,huku Katibu Mkuu Yusuph Makamba akitoa kauli zisizoendana na hadhi yake katika jamii,ni vema ukasoma habari ifuatayo kisha tujadili kidogo:

Makamba awatukana wanaoshauri Kikwete asigombee 2010

Rais Kikwete kongamano la Nyerere limemweka katika lawama za kutokuwa na maamuzi na kuwa asipendekezwe kugombea awamu ya pili.

Na Leon Bahati
KATIBU mkuu wa CCM, Yusuf Makamba, ambaye katika miezi ya karibuni amekuwa akihaha kutoa ufafanuzi, kukanusha au kujibu tuhuma mbalimbali dhidi ya chama hicho tawala, jana alikuwa na kazi nyingine ya kumtetea Jakaya Kikwete baada ya waziri katika serikali ya awamu ya tatu kushauri asiteuliwe kugombea urais 2010 iwapo atashindwa kufanya maamuzi magumu dhidi ya mafisadi.

Safari hii, Makamba alitumia maneno makali kumjibu waziri huyo, Matheo Qares akisema watu wenye fikra kwamba CCM inaweza kumtosa mwenyekiti wake kwenye mbio za urais wakati wa uchaguzi mkuu wa mwakani, "ni wehu".

Qares, ambaye aliwahi kushika wadhifa nyeti wa Waziri wa Menejimenti ya Utumishi wa Umma, alitoa rai hiyo juzi kwenye kongamano la kumuenzi muasisi wa taifa la Tanzania aliposema kuwa CCM haina budi kutafuta mwanachama mwingine wa kugombea nafasi ya urais mwaka 2010 iwapo Kikwete atashindwa kufanya maamuzi magumu dhidi ya mafisadi, ambao alisema hawakijui chama na wengine uraia wao una utata.

Lakini jana, Makamba alisema watu wenye fikra hizo ni wehu kwa kuwa uteuzi wa wagombea ndani ya CCM ni mchakato usiotoa ruhusa kwa mawazo binafsi ya watu.

"Mtu mwenye akili nzuri hawezi kusema kwamba Rais Kikwete ameshindwa kutekeleza wajibu wake. Anayefikiria hivyo, ni mwehu," alisema Makamba alipotakiwa kutoa maoni yake kuhusu kauli hizo.

Alisema ni vyema watu hao wakafahamu kuwa mgombea urais wa CCM anateuliwa kwa mujibu wa taratibu za chama kupitia vikao mbalimbali hivyo, wazo binafsi halina nafasi.

Alipoulizwa kuhusu shutuma zinazoelekezwa kwa Rais Kikwete, Makamba alisema asingependa kujibu hoja zilizotolewa na mjumbe mmoja mmoja kwenye kongamano hilo.

Lakini akaeleza kwamba yupo tayari kutoa maoni yake binafsi baada ya Taasisi ya Mwalimu Nyerere kuwasilisha kwake mapendekezo waliyofikia kwenye kongamano hilo.

"Mimi mwenyewe sikuwepo kwenye kongamano hilo. Wala sijui mapendekezo yao. Siwezi nikatolea maoni hoja za mtu mmoja mmoja alizotoa kwenye Kongamano hilo. Nitakapopata mapendekezo ya jumla ya taasisi hiyo, nitakawa katika nafasi nzuri ya kutoa maoni yangu."

Katika kongamano hilo, Rais Kikwete amekuwa akilaumiwa kwa kutochukua hatua dhidi ya watu wanaotuhumiwa kwa ufisadi, wengi wao wakielezwa kuwa ni wafanyabiashara ambao wanatuhumiwa kukiteka chama kwa kutumia nguvu zao za pesa.

Wakati fulani Joseph Butiku, mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere ambayo iliandaa kongamano hilo, alisema Rais Kikwete amezungukwa na mafisadi ambao wanaitafuna nchi.

Akizungumza kwenye kongamano hilo juzi, Qares alisema rais hana budi kufumba macho na kuwashughulikia hao watuhumiwa ambao wanadai Kikwete hakujuana nao barabarani na kama atashindwa basi ashauriwe kuwa miaka yake mitano inamtosha.

Kabla ya Qares, Musa Nkangaa, ambaye aliwahi kuwa waziri kwenye serikali ya awamu ya pili, aliituhumu CCM kuwa imepoteza hadhi na kujikuta ikikumbatia matajiri wachafu.

Kwa mujibu wa Nkangaa, CCM imekuwa si chama cha wakulima na wafanyakazi tena, bali kimebaki kuwa chama cha matajiri.

"Ndiyo maana imekuwa ikiweweseka kuwashughulikia watuhumiwa wa Richmond na Kagoda," alisema akimaanisha kashfa ya utoaji zabuni ya ufuaji umeme wa dharura kwa Richmond Development Company LLC na tuhuma za wizi wa mabilioni ya fedha kutoka BoT.

CHANZO: Mwananchi

Tatizo kubwa la watawala wetu ni yale mazowea waliyojijengea ya kupigiwa makofi na vigeregere hata wanapoongea pumba.Ni katika mstari huohuo,kauli na mawazo mbadala huchukuliwa kuwa ni mithili ya kosa la uhaini.Sidhani kama kuna ubaya kwa wana-CCM kumpa changamoto mwenyekiti wao kama ambavyo Mtanzania yeyote mwenye mapenzi ya dhati anavyostahili haki ya kukemea mwelekeo mbovu wa nchi yetu.

Japo naafikiana na Makamba anapokumbusha wana-CCM wenzie kwamba chama hicho kikongwe kina utaratibu wake wa kumpata mgombea urais lakini hiyo sio sababu ya kuwaziba midomo wale wanaodhani mwanachama mwenzao waliyempitisha kugombea urais katika uchaguzi uliopita,na kushinda,yaani Jakaya Kikwete,ameshindwa kukidhi matarajio ya wana-CCM hao (kama Matheo Qareshi).Sio tusi kutoa mawazo kuwa flani ameshindwa hasa pale kauli kama hiyo inapoambatana na mifano hai kadhaa.

Sidhani kama Makamba anafanya hivyo kwa ile anaamini kuwa Qaresi ni mwehu (ikumbukwe Mtanzania huyo alishawahi kushika nyadhifa za juu ikiwa ni pamoja na uwaziri katika ofisi ya rais) bali ni muendelezo wa kasumba ya kujikomba.Kwa Makamba kumhukumu Qaresi kuwa ni mwehu amekwepa ujasiri wa kujadili hoja badala ya kumjadili mtu.

Ni muhimu tuwe wakweli na wawazi katika kujadili hatma ya taifa letu.Ni dhahiri kuwa vita dhidi ya ufisadi inakwamishwa na mwenye jukumu la kuchukua hatua.Hatuwezi kufanikiwa katika mapambano dhidi ya rushwa (kama yapo at all) ilhali ilishashauriwa kwamba Mkurugenzi wa TAKUKURU,Edward Hosea,ang'olewe madarakani kutokana na kuhusishwa na utapeli wa Richmond.Ushauri huo ulitolewa pia kuhusa aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali,Johnston Mwanyika.Huwezi kuwalaumu Hosea na Mwanyika kwa vile hawakujiteua kushika nyadhifa hizo.Aliyewateua yupo na amesikia yaliyosemwa dhidi yao lakini kaamua kupuuza.

Kwa hakika kama tunataka kuiona Tanzania ikijikomboa kutoka katika lindi la umasikini unaochangiwa kwa kiasi kikubwa na ufisadi,basi ni dhahiri tunahitaji kuangalia makosa yaliyofanyika mwaka 2005 na kuhakikisha hatuyarudii katika uchaguzi mkuu ujao hapo mwakani.Haya mambo ya kuangalia haiba ya mtu na pasipo kujali kama haiba hiyo inaendana na uwezo wa kazi yameshatufikisha hapa,na tukizubaa yatatupeleka pabaya zaidi,

Kinachisikitisha ni mwamko mdogo mingoni mwa Watanzania wa tabaka la kati (the middle class).Tabaka hili lina nafasi nzuri ya kuunganisha nguvu na tabaka la walalahoi ili kulibana tabaka tawala ambalo so far limeji-identify kama sehemu muhimu ya ustawi wa ufisadi na mafisadi.

Inawezekana kabla hatujachelewa.





27 Nov 2009


Uwajibikaji uliotukuka au kupitiliza majukumu?Who cares as long as we are kept safe.Katika magazeti mbalimbali ya hapa Uingereza kuna habari kwamba Waziri wa Usalama,Lord West,amehenyeshwa na askari baada ya kusimamishwa na kusachiwa (stop and search) kwa mujibu wa sheria za kuzuia ugaidi.Uzuri wa hawa wenzetu ni ile tabia ya "hapendwi mtu",yaani kutekeleza majukumu kwa maadili badala ya kuangalia urembo au haiba.

Sidhani kama kuna haja ya kuwakumbusha madudu ya Waziri wetu mwenye jukumu la utawala bora (which includes mapambano dhidi ya ufisadi) alivyojitokeza kuwa mama mlezi wa mafisadi.Ni katika tawala ambazo mtu anaweza kuropoka chochote na akaendelea kuitwa mheshimiwa ndipo hadi muda huu Sophia Simba anaendelea na wadhifa unaohitaji uadilifu wa hali ya juu,including umakini katika kauli.

Sasa kama askari wanaweza kudili na bosi wao kama raia mwingine iweje basi waziri wetu mwenye dhamana ya kuhakikisha mafisadi "wananyea ndoo" gerezani awe mtetezi wao mkubwa?Jibu jepesi ni kwamba Waziri Simba anapata jeuri hiyo kutoka mahala flani.Na si yeye tu bali viongozi wetu wengi wametokea kuwa na jeuri ya ajabu kwa vile wanafahamu fika hakuna wa kuwaadhibu.Kama aliyekuteua haonekani kuerwa na madudu yako why would you care kurekebisha madudu hayo?

Unfortunately,lawama nyingi zimekuwa zikielekezwa kwa watendaji wabovu badala ya kumkalia kooni aliyewapa fursa ya kuweka hadharani udhaifu wao.Ni kama katika futiboli;kocha akipanga kikosi kibovu basi lawama zaidi zitaelekezwa kwake kwa vile kikosi alichopanga hakijichagua chenyewe.Na ndio maana hivi majuzi kocha wa timu ya taifa ya Scotland alijikuta akifungashiwa virago vyake baada ya timu hiyo kufanya vibaya kwenye kampeni yake ya kushiriki Kombe la Dunia hapo mwakani.

Na ukidhani mie ni malalamishi nisiye na hoja basi SOMA HAPA uelewe chanzo cha tatizo kiko wapi.

13 Nov 2009


Baraza la Mawaziri la Kikwete lagawanyika

Godfrey Dilunga

Novemba 11, 2009

Mawaziri kumi wataka watuhumiwa waadhibiwe

Wanane wanawatetea, waliosalia hawana msimamo

Sophia Simba asonywa na wenzake

BAADA ya Kamati inayoongozwa na Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi kuzungumza na wabunge wa Chama Cha Mapinduzi na kuibuka malumbano, kejeli na matusi kwenye mkutano huo, imebainika kuwa sasa mpasuko si tu miongoni mwa wabunge; bali umesogea hadi kwenye Baraza la Mawaziri na kugawa mawaziri hao.

Uchunguzi wa Raia Mwema, ukihusisha mazungumzo na baadhi ya wabunge na mawaziri, umebaini kuwa mpasuko katika baraza la mawaziri kwa kiasi fulani umechukua sura tofauti na ule wa wabunge wa CCM.

Katika Baraza la Mawaziri, hali ni tofauti. Siku kadhaa mara baada ya mkutano wa Mwinyi, Dodoma, wapo mawaziri walioanza kuwapuuza manaibu mawaziri wao, lakini pia wapo manaibu mawaziri walioanza kuwapuuza mawaziri wao, hali inayotajwa kuwa huenda ikasogea hadi kwa watendaji wa chini kwenye wizara na hatimaye kugawa watendaji wote.

Lakini pia katika mazungumzo hayo ya Raia Mwema, pia imebainika kuwa kuna baadhi ya wizara zenye mawaziri wanaofanana kimtazamo wakiwa kundi moja kwenye mpasuko huo; hali inayotajwa kuwa huenda ikazua mvutano kama watendaji wengine waandamizi wizarani watakuwa na misimamo pinzani.

Mpasuko huo chanzo chake kinatajwa kuwa kashfa ya Richmond, na hususan kuhusika kwa aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa kwenye sakata hilo ambapo mawaziri na manaibu mawaziri wanaodaiwa kuwa karibu naye wameendelea kumtetea kwa siri na hadharani; huku wengine wakitafsiri hatua hiyo kuwa ni upuuzi na hata kuwaona wenzao wanaoendesha harakati hizo ni wapuuzi.

Mmoja wa mawaziri hao ni Sophia Simba, ambaye sasa si tu imedaiwa anatazamwa kwa jicho tofauti na baadhi ya mawaziri wenzake, lakini pia CCM imeanza kukana baadhi ya shutuma alizotoa kwa baadhi ya watu katika juhudi zake za kutetea watuhumiwa wa kashfa mbalimbali. Simba anadaiwa kueleza kuwa Mfanyabiashara Reginald Mengi, si mwanachama wa chama hicho.

Taarifa zaidi zinaeleza kuwa kati ya mawaziri 26 waliopo ukimwondoa Waziri Mkuu, 10 wamedaiwa kuwa na msimamo unaofanana na baadhi ya wabunge wapambanaji wa ufisadi wakiwa na msimamo watuhumiwa wa ufisadi waadhibiwe, wakati mawaziri wengine wanane wakiwa katika kundi la utetezi.

Mawaziri wanaodaiwa kuwa na msimamo wa kupinga ufisadi ukiwamo wa Richmond ni pamoja na Waziri wa Maendeleo ya Uvuvi, John Magufuli, Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Dk. Mary Nagu, Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Profesa Mark Mwandosya na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Bunge, Philip Marmo.

Wengine ni Waziri wa Afya, Profesa David Mwakyusa ambaye anatajwa kuwa na msimamo wa chini chini, Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Celina Kombani, Waziri wa Afrika Mashariki, Diodorous Kamala na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Margaret Sitta.

Mawaziri wanaodaiwa kuwa msimamo wao haueleweki katika sakata la Richmond ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, dk. Hussein Mwinyi, Waziri wa Miundombinu, Dk. Shukuru Kawambwa, Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe na Waziri wa Kilimo, Stephen Wasira.

Hata hivyo, inaelezwa kuwa kundi la mawaziri wenye msimamo mkali wanaotaka hatua kuchukuliwa dhidi ya watuhumiwa, wengi wao wamekuwa na rekodi nzuri kiutendaji ikilinganishwa na wale watetezi wa watuhumiwa.

Baadhi ya wabunge waliozungumza na Raia Mwema wamedai kuwa mawaziri wengine wanane msimamo wao umeshindwa kubainika moja kwa moja kutokana na kuwapo katika kila kundi.

Katika mkutano uliopita wa Bunge, utekelezaji wa lala salama wa mazimio ya Bunge kuhusu Richmond ulipaswa kutolewa taarifa na serikali lakini haikuwa hivyo, bila kuelezwa sababu za wazi.

Uchunguzi huo wa muda mrefu wa Raia Mwema bungeni pia umebaini kuwa athari za makundi kwa kiasi fulani zimekuwa zikimgusa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ambaye ndiye aliteuliwa na Rais baada ya Lowassa kujiuzulu.

Uchunguzi huo umebaini kuwa katika mkutano wa 16 wa Bunge na baadhi ya vikao vya mkutano wa 17 uliokwisha, hivi karibuni, wakati akitoa hoja au kujibu maswali ya papo kwa papo yenye utetezi wa Serikali ni sehemu ya mawaziri wachache tu wamekuwa wakimpongeza kwa kumpigia makofi na wengine wakibaki kuduwaa, wengine wakiwa katika mazungumzo yao.

Kutokana na hali hiyo, mmoja wa wabunge amedai kuwa wapo mawaziri wasiompa nafasi ya heshima na utiifu unaostahili Waziri Mkuu Pinda na kwamba, wameendelea kuwa watiifu zaidi kwa kundi lao kuliko kwa waziri mkuu.

Wizara ambazo zimejipambanua kuwa na waziri mwenye msimamo wa utetezi kwa Lowassa na watuhumiwa wengine ni Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais – Utawala Bora, inayoongozwa na Sophia Simba.

Wizara nyingine ambazo zimebainika kuwa na mawaziri wenye misimamo ya makundi ni pamoja na Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, inayoongozwa na Profesa Juma Kapuya, na Naibu wake Dk. Makongoro Mahanga.

Kapuya alitajwa na kundi mojawapo kwenye mpasuko huo kuwa ni kati ya watu wanaopaswa kuchukuliwa hatua akidaiwa kumtetea Lowassa kwa gharama za wanasiasa wengine akiwamo Spika wa Bunge, Samuel Sitta. Naibu wake, Makongoro naye pia alijipambunua kuwamo kwenye kundi la Lowassa, wakati wa mkutano wa Mwinyi.

Baadhi ya wabunge pia wanaitazama Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kuwa inaongozwa na viongozi wenye mgongano wa makundi, japokuwa ikidaiwa kuwa Naibu Waziri Khamis Kagasheki, amejitahidi kwa muda mrefu kuficha hisia zake tofauti na Waziri wake, Lawrance Masha, anayedaiwa kuwa kundi la Lowassa.

Katika hatua nyingine, baadhi ya wabunge waliozungumza na Raia Mwema kutoka makundi yote wamebainisha matarajio yanayozidi kukinzana mara baada ya kukamilika kwa mkutano kati yao na Kamati ya Mwinyi.

Wakati upande mmoja ukiendelea kusisitiza kuwa watuhumiwa wenye nyadhifa katika chama hicho wang’olewe, wenzao wamekuwa na msimamo tofauti.

Hata hivyo, kundi la wabunge wanaotaka wenzao watuhumiwa watimuliwe ndilo linaonekena kuwa na nguvu zaidi hata mbele ya wananchi na taasisi nyeti zikiwamo za elimu ya juu nchini kama ambavyo imekuwa ikiandikwa na baadhi ya magazeti nchini.

Kwa upande mwingine, hali ya kuwapo kwa kile kinachoelezwa kuwa ni mvutano huenda ikaendelea. Kuwapo kwa dalili hizo kunatokana na kuendelea kukinzana kati ya Spika wa Bunge, Samuel Sitta na baadhi ya wanasiasa wa kundi linalomwandama, akiwamo Kingunge Ngombale-Mwiru.

Kingunge katika mkutano uliopita wa NEC-CCM Dodoma aliripotiwa kutaka Spika Sitta ang’olewe kwa kuwa anaendesha Bunge vibaya kwa kuruhusu mijadala ya ufisadi na hivyo kuhatarisha chama na serikali na kuimarisha hoja yake kwa kusema ubaya wa Spika unathibitishwa na hatua yake ya kuandika kitabu kinachoitwa “Bunge lenye Meno” akishirikiana na wabunge wengine machachari, akiwamo Dk. Harrison Mwakyembe.

Inaelezwa kuwa Kingunge alirejea msimamo wake huo katika mkutano wa Mwinyi lakini akionyesha kukejeli msimamo huo, Spika wa Bunge wakati akizungumza bungeni muda mfupi kabla ya kuahirishwa kwa Bunge, alijigamba kuwa Bunge lake bado lina meno.

Sitta alitamka; “Ni Bunge lenye meno” wakati akielezea uamuzi wa kuwatuma wabunge kwenda eneo la Loliondo lenye mgogoro kati ya wananchi na mwekezaji, mgogoro ambao serikali kupitia Waziri wa Maliasili na Utalii, Shamsha Mwangunga, iliwasilisha ripoti yake iliyotokana na kamati aliyounda kubaini kama kulikuwa na vitendo vya ukiukaji wa haki za binadamu.

Ripoti hiyo ya Mwangunga ilikataliwa na Bunge baada ya Waziri kueleza kuwa hapakuwa na haki za binadamu huku wananchi walioathirika wakieleza kuwa haki zao zilikiukwa, ikiwa ni pamoja na kuchomewa makazi na karaha nyingine zikiwamo za vitendo vya udhalilishaji wa wanawake.

Awali, kabla ya Spika kuingia bungeni kikao cha Bunge kilikuwa kikiongozwa na Mwenyekiti, Job Ndugai ambaye ni Mbunge wa Kongwa CCM, ambaye alionekana kutaka kuikubali ripoti hiyo ya Serikali kabla ya Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka kusimama na kueleza Bunge kuwa kwa sehemu kubwa ripoti ya Waziri Mwangunga imejaa uongo na hivyo kuomba mwongozo wa Spika ili kutoa uamuzi utakaolinda maslahi ya wananchi.

Kutokana na uamuzi huo, Ndugai alikubali na kueleza kuwa atalifikisha suala hilo kwa Spika ambaye atatoa uamuzi na ilipofika kikao cha jioni siku hiyo, Spika akatoa msimamo kuwa atatuma timu ya wabunge kwenda Loliondo, hatua ambayo bila shaka mbele ya kina Kingunge itaendelea kumtafsiri Sitta kama kikwazo kwa mambo ya serikali kupita bila kujali yana maslahi ya wananchi au la.

Ripoti ya kamati ya Mwinyi inatarajiwa kuwasilishwa katika mkutano ujao wa NEC-CCM bila shaka baada ya kupitia mikononi mwa Rais Jakaya Kikwete, ambaye ni Mwenyekiti wa chama hicho.

Kwa muda mrefu kumekuwa na wito wa kutaka Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba aenguliwe katika wadhifa huo kutokana na tuhuma mbalimbali zikiwamo za kuendelea siasa za makundi kwenye chama hicho. Kati ya matukio yanayomuhukumu Makamba ni kitendo chake cha kumlaani kada machachari wa CCM, Nape Nnauye, aliyejitokeza hadharani na kudai kuwa mkataba wa ujenzi katika jengo la Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Upanga Dar es Salaam ni wa wizi na unaonyonya jumuiya hiyo.

Katika shutuma zake hizo, Nape alitaka baadhi ya viongozi wa Baraza la Wadhamini wa UVCCM akiwamo Edward Lowassa, aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na kujiuzulu kwa kashfa ya Richmond , awajibike. Makamba aliwatetea wadhamini hao akishirikiana na aliyekuwa Mwenyekiti wa UVCCM, Dk. Emmanuel Nchimbi.

Hata hivyo, suala hilo lilifikishwa kwenye NEC-CCM na uamuzi ulitolewa kuwa iundwe kamati kuchunguza na ikibidi kurekebisha mkataba huo. Kamati hiyo ilifanya marekebisho makubwa, uamuzi ambao kwa namna fulani unaathiri umakini wa Makamba katika utetezi wake kwa baadhi viongozi wanaodaiwa kuwamo katika kundi lake ndani ya CCM.

CHANZO: Raia Mwema

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.