Showing posts with label JK. Show all posts
Showing posts with label JK. Show all posts

13 Oct 2008

Serikali isilaumiwe kwa hali ngumu ya maisha-JK
 
2008-10-13 10:24:10 
Na Thobias Mwanakatwe, Kyela

Rais Jakaya Kikwete amesema kushuka kwa uchumi wa dunia hivi sasa ni lazima kutaathiri uchumi wa taifa, na hivyo hakuna sababu kwa wananchi kulaumu kwamba serikali inawatesa kutokana na hali ngumu ya maisha. 

Akiwahutubia wananchi wa mji wa Kyela juzi, alisema hivi sasa uchumi wa dunia umekumbwa na msukosuko mkubwa kuliko yote katika historia toka mwaka 1930 ambapo hali hiyo haijawahi kujitokeza. 

Alisema pamoja na kuwepo kwa msukosuko huo wa uchumi wa dunia,
hata hivyo serikali bado haijaanza kujipanga kukabiliana na hali hiyo lakini baada ya miezi michache ijayo athari zitaanza kujitokeza. 

Hata hivyo, Rais Kikwete alisema
serikali inaendelea kutafakari ni jinsi gani itaikabili hali hiyo ili kusijitokeze athari zaidi katika uchumi. 

Alisema hivi sasa kutokana na msukosuko wa uchumi, serikali ya Marekani imetenga Dola 700 bilioni kujaribu kuokoa mabenki yanayofilisika, mkakati ambao pia unafanywa na Uingereza,Ujerumani, Japan pamoja na nchi nyingine. 

``Wenzetu wanao uwezo mkubwa wa kiuchumi
sijui yakitufika sisi itakuwaje, tunaendelea kutafakari ili na sisi yatakapotukuta tufanye nini lakini siyo kazi rahisi,`` alisema Rais Kikwete. 

Aliongeza kuwa kutokana na hali hiyo hakuna sababu kwa wananchi kulalamika kuwa serikali inatutesa kwa sababu kushuka kwa uchumi wa dunia athari zake zinazikumba nchi maskini ikiwemo Tanzania.

CHANZO: Nipashe


14 Sept 2008



Rais Jakaya Kikwete amewataka Watanzania kutambua kuwa njia pekee itakayowakwamua kiuchumi na kuwaletea maisha bora ni kujishughulisha na shughuli mbalimbali za maendeleo na si kukaa tu vijiweni na kulalamika. 
Kauli hiyo aliitoa jana wakati akijibu malalamiko ya wananchi wa kijiji cha Nyumba ya Mungu, kilichopo katika kata ya Lang`ata, tarafa Msitu wa Tembo, wilayani Simanjiro, ikiwa ni siku yake ya kwanza ya ziara yake ya kikazi mkoani Manyara. 

Wananchi hao waliokuwa na mabango yenye ujumbe mbalimbali, walimweleza Rais Kikwete kuwa bado wanashindwa kuishi maisha bora kama walivyokuwa wametarajia na badala yake wanakabiliwa na matatizo sugu ya kupata huduma bora ya afya na mitaji ya biashara na ukosefu wa ajira. 

Rais Kikwete alielezwa hayo na wananchi wa kijiji cha Lemkuna, muda mfupi kabla ya kuzindua bonde la umwagiliaji la kijiji hicho, ambapo pia walilalamikia bei kubwa ya pembejeo za kilimo na umbali wa upatikanaji wake, hasa mbolea. 

Akizungumza mara baada ya kuwasikiliza wananchi hao, Rais Kikwete, aliwaeleza kuwa wanapaswa kujiajiri wenyewe kupitia utaratibu wa kupata mikopo na kujiunga kwenye vikundi vya kuweka na kukopa (SACCOS) ili waweze kuanzisha miradi ya maendeleo. 

``Jamani msitarajie maisha bora kama yatadondoka kutoka juu, utaratibu uliopo ni wa mikopo tuliyoianzisha ili muweze kufanya shughuli za maendeleo, awamu ya kwanza imekwishapita wengine wamepata wengine hawajapata ila tutaendelea kuhakikisha kuwa mikopo zaidi inatatolewa ili wale ambao hawajapata waweze kupata`` alisema. SOURCE:ippmedia.com

Kauli hiyo inashabihiana na hii iliyotolewa na Waziri Mkuu wa zamani,Edward Lowassa

2007-05-10 15:55:28 
Na Radio One Habari

Waziri Mkuu, Mheshimiwa Edward Lowassa amesema maisha bora kwa kila Mtanzania hayawezi kuja kwa kukaa vijiweni na kunywa kahawa bali kwa kufanyakazi kwa bidii na hasa kuendeleza kilimo. 

Amefafanua kuwa maisha bora kwa kila Mtanzania yanayosemwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ni matokeo ya kazi na hayaji kwa kukaa vijiweni kutwa nzima kunywa Kahawa na kutaka wananchi wa Pwani wafanye kazi kwa bidii kujiletea maendeleo. 

Akihutubia mkutano wa hadhara kijijini Maneromango Wilayani Kisarawe Mkoani Pwani Waziri Mkuu amesema watu wa mkoa huo lazima wabadili pato la mwaka la kila mtu ili liwe kubwa kama katika mikoa mingine. 

Aidha ameagiza mashambapori yaliyopo Kisarawe na wilaya nyingine Mkoani Pwani yaorodheshwe, yapelekwe Wizara ya Ardhi ili hatimaye yafikishwe kwa Rais yatwaliwe na kuwagawia vijana wafanye kazi za kilimo. 
Waziri Mkuu anakamilisha ziara yake ya siku sita ya Mkoa wa Pwani leo kwa kutembelea Wilaya ya Bagamoyo. 
SOURCE: Radio One


11 Feb 2008

Uongozi wa kisiasa wa Tanzania,kama ilivyo sehemu mbalimbali duniani,umekuwa ukitegemea watu kutoka fani mbalimbali za maisha.Tuna viongozi wa dini (kama Mchungaji Lwakatware),Wasomi (kama Prof Mwandosya,Prof Msola,Prof Mwakyusa),wanajeshi (kama Kapteni John Komba,Kapteni Jaka Mwambi,Luteni Yusufu Makamba) na hata wasanii kama Khadija Kopa .Hivi karibuni,JK alielezea kutoridhishwa kwake na athari zinazoweza kutokana na kuwa na viongozi ambao pia ni wafanyabisahara.Ana hoja ya msingi hapo,lakini nadhani tatizo la msingi sio fani aliyotoka au anayoendela nayo kiongozi husika bali ni utashi alionao katika kuwahudumia Watanzania wenzake.Kadhalika,mkanganyiko uliopo kwenye kanuni za maadili ya uongozi ziko shaghala baghala,hasa baada ya kuuawa kwa Azimio la Arusha na kuzaliwa Azimio la Zanzibar.Endelea na makala yangu hii kwenye gazeti la Mtanzania.
MTANZANIA UGHAIBUNI-

Watanzania wengi wameipokea kwa furaha kauli ya Rais Jakaya Kikwete kuhusu umuhimu wa kutenganisha biashara na utumishi wa umma.Ni kauli mwafaka kwani hata katika Maandiko Mtakatifu tunafundishwa kwamba ni vigumu kutumikia mabwana wawili.

Naamini kwa mtazamo wa wengi,wafanyabiashara kama Watanzania wengine wana kila haki ya kushiriki katika shughuli za siasa ikiwa ni pamoja na kugombea ubunge au hata kuteuliwa mawaziri.Tatizo linakuja pale maslahi ya biashara zao yanapoingiliana na utekelezaji wa majukumu yao katika kuuhudumia umma.

Inaweza kuwa sio sahihi kuwalaumu wafanyabisahara wanaochanganya biashara na siasa pale ilhali hakuna miongozo maalumu (kama ya Marekani na Uingereza).Ndio maana wazo la kufanyika mchakato wa kuleta sheria na kanuni zitakazoweka bayana mazingira ambayo kwa upande mmoja hayatawanyima nafasi wafanyabiashara kushiriki kwenye siasa,na upande mwingine biashara zao kutoathiri majukumu waliyokabidhiwa na taifa,lina umuhimu mkubwa.

Pamoja na pongezi hizo ni muhimu kuangalia chanzo cha tatizo lililopo hivi sasa.Ni ukweli usiopingika kwamba wakati wanasiasa wengi wameendelea kuhubiri kwamba siasa ya Ujamaa na Kujitegemea bado ni mhimili wa taifa letu,hali halisi tuliyo nayo sasa inapingana kabisa na matamshi hayo.

Azimio la Arusha lilisaidia kuweka wazi mwelekeo wa taifa letu.Makala moja kama hii haiwezi kutosha kuelezea undani wa Azimio hilo lakini kilicho wazi ni kwamba Baba wa Taifa,ambaye kimsingi ndiye anayekubalika kama mwasisi wa itikadi hiyo,alikuwa na ndoto ya kuona jamii ya Watanzania inayoishi kwa usawa na haki.

Baadaye likaja Azimio la Zanzibar.Pengine mie ni mzembe wa kujua kilichomo katika Azimio hilo lakini naamini kwamba kuna Watanzania wengi ambao hadi leo hawajui kilichomo kwenye Azimio hilo.Labda ni kutokana na ufahamu mdogo uliopo miongoni mwa wananchi wengi kuhusu Azimio la Zanzibar ndio maana wengi wetu tunarahisisha majibu kwamba lilikuwa tamko rasmi la kifo cha Azimio la Arusha.Na katika hili,CCM inastahili kubeba lawama zote kwani haijafanya jitihada zozote za makusudi kuuelewesha umma kuhusu madhumuni na kulichomo kwenye Azimio hilo (la Zanzibar).

Kuna mapungufu makubwa katika suala zima la uwazi pindi yanapojiri masuala nyeti kwa taifa letu.Mfano mzuri ni kwamba wengi wetu tulikuwa hatufahamu kwamba hadi uteuzi wake unatenguliwa na Rais,aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu aliyeondolewa madarakani,Dkt Daudi Ballali,hakuwa mtumishi wa serikali.Pengine taratibu zinasema hivyo lakini kwa vile mtu anayekalia nafasi hiyo ndiye mwenye kushika dhamana ya fedha za Watanzania wote,nadhani kulikuwa na kila sababu ya wenye fedha zao (Watanzania) kufahamishwa kuhusu hilo badala ya kusubiri mpaka litokee tatizo la ufisadi kwenye taasisi hiyo muhimu kwa taifa.

Hadi muda huu,ukiwauliza viongozi wa CCM kwamba je Azimio la Arusha bado ni mwongozo muhimu kwa maendeleo na mwelekeo wa taifa,sanasana utachoambulia ni hadithi ndefu zisizotosha kutoa jibu moja la kueleweka.Ni dhahiri muuliza swali atakumbana na ugumu wa aina hiyohiyo pindi akiuliza iwapo nchi yetu bado inafuata siasa ya Ujamaa na Kujitegemea.Na haiishii hapo kwani majibu yataendelea kuwa tete pindi mtu akiuliza iwapo CCM bado ni chama cha wakulima na wafanyakazi.

Na ni katika hilo la wakulima na wafanyakazi ndipo napoona kuna tatizo la msingi.Inasemekana Azimio la Zanzibar lilihalalisha watumishi wa umma (wafanyakazi) kumiliki mali kinyume na katazo lililowekwa na Azimio la Arusha.Laiti wakati wanasiasa wetu walipokutana Zanzibar kuua Azimio la Arusha wangeangalia mbali,ni dhahiri wangebaini uwezekano wa kutokea mgongano kati ya biashara na utumishi wa umma.Haraka ya kupitishwa Azimio hilo inaweza kuwa sababu muhimu ya wanasiasa hao kutoangalia mbali.Lakini pia haraka hiyo inaweza kuwa ilichochewa na ukweli kwamba wakati wanasiasa wengi walikuwa wakituimbia ngonjera za Ujamaa na Kujitegemea majukwaani,majumbani mwao walikuwa wakicheza ngoma za ubepari.

Dhana hapo ni kwamba Azimio la Zanzibar lilipitishwa chapchap ili wajamaa wa hadharani waliokuwa mabepari wa kificho waweze kuendesha maisha yao bila hofu na bughudha ya kuonekana wanatenda kinyume na imani ya taifa letu kwa wakati huo.Hawa ni pamoja na wale ambao walikuwa wakituaminisha kwamba ni watu wa karibu na Baba wa Taifa kumbe moyoni walikuwa wakiomba dua Mwalimu aondoke madarakani ili watumie vile walivyokuwa wakikusanya kwa kificho katika zama hizo za Ujamaa na Kujitegemea.Na wengine japo Mwalimu aliwasaidia kuwaingiza madarakani akidhani ni waumini wa siasa zake,wamestaafu wakiacha skandali lukuki.

Kama kuna madhara mabaya zaidi ya mfumo wa chama kimoja basi ni kule kutoruhusu mawazo tofauti na ya watawala,hata kama mawazo hayo ni ya kuchochea maendeleo ya taifa.Kinadharia kila Mtanzania ana uhuru wa kutoa mawazo yake alimradi asivunje sheria halali za nchi,lakini kiuhalisia bado kuna chembechembe zilizorithiwa kutoka katika mfumo wa chama kimoja ambapo mawazo tofauti ni sawa na uhaini.

Katika zama za chama kimoja,hoja kama ile ya “chama kushika hatamu” zilisaidia baadhi ya mafisadi wa wakati huo kupata kinga dhidi ya wale maovu yao.Sote tulikuwa ni Watanzania tusio na tofauti,tunaoamini kwamba ili nchi yetu iendelee tunahitaji ardhi,watu,siasa safi na uongozi bora.Mwalimu aliamini kuwa hiyo ni njia sahihi ya maendeleo kwani alishuhudia namna ilivyofanikiwa sehemu kama China na Cuba.Kosa lake ni kuamini kwamba walio karibu yake walikuwa na imani ya dhati kama yeye.Angalau leo tunawajuwa wanafiki hawa,lakini kwa sababu za “kulinda umoja wa kitaifa” na kutaka “wapumzike kwa amani” tunaendelea kuwaheshimu kwa kutowaumbua hadharani.

Kumkosoa mzazi ni kosa,na kwa mwananchi wa kawaida au hata kiongozi kumkosoa Rais inaweza kutafsiriwa kuwa ni utovu wa nidhamu.Hata hivyo,kutoa ushauri kwa heshima na taadhima ni jambo linalokubalika.Ni kwa kuzingatia hilo ndio maana naamini kwamba wakati Watanzania wengi wanakubaliana na mtizamo wa Rais Kikwete kuhusu kutenganisha siasa na biashara,ni vema katika utekelezaji wa dhamira yake hiyo akaweka maanani namna Baba wa Taifa alivyosalitiwa na baadhi ya watu wake wa karibu.

Nasema hivyo kwa sababu naamini hata zikiwekwa sheria nzuri namna gani za maadili ya uongozi,pasipo kutengeneza mazingira yatakayozuia wasimamizi wa sheria hizo kuzihujumu,itakuwa ni kazi bure.Mwanasiasa anaweza kabisa kutangaza kwamba biashara zake za awali zimekabidhiwa kwa wadhamini flani,lakini pasipo usimamizi mzuri mfanyabiashara huyo anaweza kuendelea kuendesha biashara zake huku akiwa mwanasiasa japo machoni mwa umma anaonekana ametekeleza sheria hiyo tarajiwa ya kutenganisha biashara na siasa.

Mfano mzuri wa ninachosema ni hili sakata linaloendelea la fedha za EPA huko Benki Kuu.Yayumkinika kubashiri kwamba kama itafikia hatua ya watu flani kupelekwa mbele ya vyombo vya sheria,kuna uwezekano watu hao wakawa ni wamiliki “hewa” ambao majina yao yalitumika tu kuficha wamiliki halali.Katika mazingira ambapo taasisi kama TAKUKURU ilikuwa ya kwanza kudai mradi wa Richmond haukuwa na harufu ya rushwa ilhali sasa tunaona suala hilo likiwaka moto huko bungeni,tutarajie nini pindi wakipewa jukumu la kuhakikisha mfanyabishara anayetaka kuingia kwenye siasa kweli amekabidhi biashara yake kwa wadhamini kama sheria itakavyokuwa inataka?

Mwisho,kikao kinachoendelea cha bunge kimeonyesha dalili kwamba baadhi ya wawakilishi wetu wamechoka kupiga mihuri kupitishwa miswada inayoonekana mizuri machoni lakini inaishia kwa mashirika kama ATC kununua ndege mbovu,TANESCO kujikuta hohehahe kwa kulipa madeni yaliyosababishwa na walafi flani wasio na uchungu na taifa au kuletewa umeme hewa ulioahidiwa na makampuni ya kisanii.Hoja hapa sio kuitupilia mbali miswada ya manufaa kwa taifa au kuchochea upinzani dhidi ya serikali bali kuwabana mafisadi wote wananaotumia nyadhifa zao kulikamua taifa letu.
BAADA YA POLITIKI ZA BONGO,HEBU ANGALIA HIZI ZA NAS KUHUSU THE N-WORD


8 Feb 2008

Mwezi Novemba mwaka 2006,niliandika makala moja iliyotoka katika gazeti la KULIKONI (toleo la tarehe Novemba 3-9, 2006 2006).Katika makala hiyo (BONYEZA HAPA KUISOMA),nilizungumzia kusikitishwa kwangu na habari kwamba ex-PM Edward Lowassa alikuwa akifanya jitihada za kuwanyamazisha wabunge wa CCM kuhusu shinikizo la kujadili mkataba wa Richmond.Pia katika makala hiyo nililaumu staili ya uongozi wa Lowassa ya kuwaumbua hadharani watendaji walio chini yake badala ya kufanya hivyo kimaandishi au ofisini.Nilieleza kwamba japo dhamira ya Lowassa kukosoa utendaji wa subordinates ni njema,njia anazotumia sio mwafaka.Nilihoji kiongozi angejisikiaje iwapo Bosi wake,JK,akitokea kumkosoa hadharani badala ya kufanya hivyo faraghani.Nilipoandika makala hiyo,sikujua kuwa kuna siku,Lowassa atakumbana na fedheha ileile aliyokuwa akiwapatia ma-DC,RAS,Katibu Kata,nk kwa kuwaumbua hadharani (pengine kwa kujitafutia tu umaarufu wa kisiasa).Leo siku hiyo imetimia.Siku chache baada ya makala hiyo kuchapishwa,Mwandishi wa Habari wa Lowassa,aliandika makala kupinga hoja zangu,kabla ya kunitumia barua-pepe ya shutuma na hatimaye aliweka comments kwenye blog hii.Contents za makala,barua-pepe na comments za muungwana huyo zilikuwa na ujumbe unaolingana,ambapo pamoja na mambo mengine alipingana na hoja zangu huku akishutumu kwamba sie wanafunzi tulio nje tukisomeshwa kwa kodi za masikini hatupaswi kukosoa mambo tusiyoyajua (BONYEZA HAPA KUSOMA COMMENTS HIZO.)Nami nimjibu kwa barua-pepe kusisitiza kwamba nilichoandika kilikuwa sahihi,na imani yangu kwamba utetezi wake kwa Lowassa ilikuwa sehemu tu ya utekelezaji wa majukumu yake ya kazi (SOMA BARUA-PEPE HIYO KWA KUBONYEZA HAPA)

27 Aug 2007

Asalam aleykum,


Kuna habari flani nimeiona gazetini imeniacha nakenua meno kwa kicheko.Kwa mujibu wa gazeti moja la Daily Mail la hapa Uingereza eti inadaiwa kwamba wanawake warefu “wanawazimia sana” wanaume wafupi.Kilichopelekea madai hayo ni maswali wanayojiuliza wafuatiliaji wa mambo ya watu (wambeya?) eti kwanini mwanamitindo wa kimataifa Sophia Dahl “amekolea” kwa mwanamuziki “andunje” wa midundo ya jazz,Jamie Callum.Gazeti hilo linadai kwamba wanaume wafupi huwa wanafanya jitihada sana kuhakikisha kuwa wanafidia “pengo” la urefu wao kwa kujituma kwenye maeneo mengine.Hoja nyingine ya kuchekesha ni ile inayodai kuwa watu wafupi ni “vipotabo” kwa wanawake warefu,na hata wakialikwa kwenye nyumba za watu warefu basi ni rahisi kwa “masoti chesisi” hao kufiti kwenye makochi pasipo kulalamika kuwa miguu inauma iwapo kochi lenyewe ni la kujibana.Sijui habari hiyo inawahusu wanaume wafupi wa nchi za Magharibi pekee au dunia nzima lakini lililo wazi ni kwamba suala la mwanamke kumzimia mwanaume au mwanaume kumzimia mwanamke ni la mtu binafsi,na ufupi,urefu,wembamba au unene sio kigezo muhimu sana japo sote tunafahamu kwamba wengi wetu tuna “mapendezeo” yetu.


Wiki iliyopita nilipata nafasi ya kushuhudia mchezo wa kirafiki wa soka kati ya timu ya taifa ya Scotland dhidi ya ile ya Afrika Kusini (Bafana Bafana),mechi iliyofanyika kwenye uwanja wa Pittodrie hapa Aberdeen.Ilipendeza kuona Waafrika wachache wanaoishi hapa wakiwa wametinga jezi za Bafana kuonyesha sapoti yao kwa timu hiyo.Japo mechi hiyo iliisha kwa Scotland kuibuka na ushindi kiduchu wa bao moja kwa bila, “sie” tuliofungwa (Waafrika wote siku hiyo tuligeuka kuwa Wasauzi) tulifarijika kuiona timu ya “nyumbani” ikitandaza kabumbu la kuvutia.Unajua mara nyingi hawa watu weupe wanakupa heshima pale utapowaonyesha una uwezo sawa nao au pengine zaidi yao.

Na wikiendi nilipata fursa ya kuangalia (kwenye runinga) michuano ya kimataifa ya riadha kutoka huko Osaka,Japan.Kama kawaida,Waethiopia na Wakenya wametesa vilivyo.Nimesoma kwenye magazeti yahuko nyumbani kuwa nasi tunawakilishwa na wanariadha kadhaa.Sijui tutaambulia chochote au itaendelea kuwa hadithi ile ile ya kuwa wasindikizaji wa kudumu.Lakini naamini kwamba kama Wakenya na Waethiopia wanaweza kutawala kwenye anga hizo,basi nasi pia tunaweza kabisa kufanya vizuri.Ni lini tutapata akina Filbert Bayi na Suleiman Nyambui wengine?Upeo wangu mdogo wa Jiografia unanishawishi kuamini kwamba hali ya hewa ya mkoa kama Arusha unatupatia mazingira mazuri ya kuzalisha wanariadha ya viwango vya kimataifa.Na ushahidi upo kwa kuangalia “perfomance” ya baadhi ya mashujaa wetu wa miaka ya nyuma.Penye nia pana njia,na kama tutawekeza vya kutosha basi kwa hakika tutaweza kurejesha historia ambayo kwa sasa imeshaanza kusahaulika.

Kuna dalili za mafanikio huko mbele ya safari kwenye soka letu. “Uchawi wa Kibrazil” wa Maximo na mwenzie Tinoco unaelekea kuzaa matunda.Ukichanganya na sapoti ya kutosha kutoka kwa JK mwenyewe basi si ajabu nasi tukajikuta tunaingia kwenye ramani ya soka ulimwenguni.Kinachonipa shaka ni matatizo ya uongozi kwenye vilabu vyetu vya soka.Maana kila kukicha utasikia wanachama Simba wanataka kupindua uongozi,au wenzao wa Yanga wanamkalia kooni kiongozi flani,au mara usikie kocha flani kabwaga manyanga kwa vile hajalipwa stahili zake,na vioja vingine visivyo na mwisho.Katika makala yangu iliyopita niliwausia viongozi wa Simba kutumia vizuri mkataba walioingia na kampuni moja kupromoti “chata” ya Adidas.Hee!haujapita muda mrefu nasikia baadhi ya wanachama wanapania kuung’oa uongozi ulio madarakani.Na hapohapo nasikia kocha Twalib Hilal anasema anarejea umangani kwa vile hajakamilishiwa malipo yake.Kiongozi mmoja anang’aka jukumu la kumlipa kocha huyo kwa kudai kwamba aliletwa na Friends of Simba.Ok,tuseme kuwa mapenzi ya Friends of Simba kwa klabu yao yaliwasukuma kumtafuta kocha mwenye uwezo wa kuipeleka mbali klabu ya Simba,na wakamsomesha Twalib hadi akakubali kusamehe mshahara mnono huko Umangani.Sasa,viongozi hawakupaswa kubweteka na kuliacha jukumu la mshahara kwa Frienda of Simba pekee.Kwanza,msaada uliotolewa na kikundi hicho unaweza kutafsiriwa kama msaada kwa uongozi kwani sote tunajua “politiki” za Simba na Yanga:matokeo yakiwa mabaya basi uhai wa viongozi kuwa madarakani unakuwa unaning’inia kwenye utando wa buibui.

Ni kama kichekesho vile kwa sababu miezi michache iliyopita,uongozi huohuo wa Simba uliweka msimamo thabiti dhidi ya kundi la Friends of Simba wakidai kundi hilo linaihujumu klabu hiyo.Navyoelewa mimi ni kwamba kwa vile klabu hiyo inajiendesha “Kiswahili” ni lazima wawepo watu wa kuikwamua kifedha pale inapokwama,na kwa namna mambo yalivyo,kila wakati uchumi wa vilabu vyetu ni wa kusuasua kama suala la amani huko Somalia.Ufumbuzi wa matatizo sio Mapinduzi,kwani yameshafanyika mengi tu na hakuna lolote la msingi lililopatikana.Wala kukimbilia mahakamani sio ufumbuzi wa matatizo.Na kuwa na mahusiano mazuri na vipoba hakuwezi kuwa ufumbuzi wa kudumu wa matatizo ya klabu kama Simba.Ufumbuzi pekee ni kwa vilabu hivyo kujiendesha kibiashara.Soka ni zaidi ya burudani kwani ikiendeshwa kisasa inaweza kuwa chanzo kizuri cha mapato.Unaposikia Manchester United,Chelsea au Liverpool zinavutia wawekezaji kutoka nje ya Uingereza sio kwamba matajiri hao ni wakereketwa sana wa soka (ingekuwa ni ukereketwa basi wangenunua vilabu katika nchi zao) bali wanajua bayana kwamba soka ni biashara yenye faida.

Twanga Pepeta wako ziarani hapa Uingereza,na wametapisha kumbi walizotembelea.Hivi kwa mfano Simba au Yanga wangefanya ziara sehemu mbalimbali duniani wasingeweza kujichumia mapato mkubwa pengine zaidi ya hayo wanayopata Twanga?Na kwa kufanya ziara nje ya nchi vilabu vyetu vingeweza kuua ndege wawili kwa jiwe moja:kutengeneza mapato ya kutosha na kuitangaza vipaji vya wanasoka wao,ambao wakipata timu huku nje inamaanisha mapato zaidi kwa vilabu hivyo.Najua wapo wanaoniona kama nimechanganyikiwa kwa kutoa mawazo kama haya.Siwalaumu kwani kwa jinsi wanavyofahamu ubabaishaji uliokithiri kwenye vilabu vyetu,hata ziara za mikoani zinahitaji mitulinga ili ziwe na mafanikio.

Mwisho,ningependa kutumia fursa hii kuwapongeza marais wa nchi za Afrika Mashariki kwa kuzingatia maoni ya wananchi wao kuhusu suala la kuharakisha Muungano wa nchi hizo.Mimi ni muumini wa hekima ya umoja,yaani umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu.Lakini umoja kati ya watu wenye “backgrounds” zinazotofautiana unaweza usizae matokeo yanayokusudiwa.Nilisoma sehemu flani ambapo DCI Manumba aliweka bayana kuwa kuongezeka kwa wimbi la ujambazi huko nyumbani kunachangiwa kwa kiasi kikubwa na wageni wanaoingiza nchini pasipo kufuata taratibu za uhamiaji.Ni ukweli usiopingika kuwa hali ya amani iliyopo Tanzania ni kivutio kizuri kwa “watu wa shari” kutoka nchi jirani.Unadhani hali itakuwaje pindi “washari” hao watakuwa wanaweza kuingia Tanzania kirahisi kama vile mtu anavyotoka Ilala kwenda Temeke hapo Muungano huo utakapokuwa umekamilika.Lakini hoja hiyo ya uhalifu ni ndogo tu ukilinganisha na ukweli kwamba tuna mambo yetu kadhaa ya muhimu tunayopaswa kuyashughulikia kwanza kabla ya kufikiria kujitanua.Na miongoni mwa mambo hayo muhimu ni suala la Muungano kati ya “Tanganyika” na Zanzibar.Halafu kuna hii “lulu” yetu ya amani na utulivu.Najua kila mtu ana tafsiri yake ya neno “amani na utulivu” lakini naamini sote tunakubaliana kuwa hatuwezi kulinganisha nchi yetu na mbinde za Wahutu na Watutsi huko Rwanda na Burundi au tatizo la ukabila huko Kenya (bila kusahau Mungiki).Na yayumkinika kusema kuwa “uwekezaji” wa wenzetu hapo nyumbani ni mkubwa zaidi ya wetu huko kwao.Mazingira yaliyoiua jumuiya ya awali ya Afrika Mashariki bado yapo,na ni vema yakarekebishwa kabla ya kufikiria wazo la Muungano mpya.

Alamsiki






20 Jul 2007

Asalam aleykum,

Juzi nilipata barua-pepe kutoka kwa rafiki yangu mmoja aliyeko huko nyumbani.Huyu jamaa alikuwa akinilaumu “kirafiki” kwamba inaelekea nimeanza kuishiwa pointi za kuandika ndio maana takriban nusu ya makala yangu iliyopita ilikuwa ina habari “nyepesi nyepesi.”Sikukasirika kwani siku zote nathamini sana ushauri wenye lengo la kujenga au kuleta maendeleo.Nilimjibu kwamba nina pointi lukuki za kuandika,lakini kuna wakati inabidi “tupunguze kasi ya maisha” kwa kuangalia habari za vituko mbalimbali hususan vinavyojiri huku Ughaibuni.Pia nilimhakikishia kuwa “nyepesi nyepesi” hizo sio “fiksi” bali ni habari zinazohusu matukio ya kweli,ila tu yanachekesha kwa namna moja au nyingine.Kicheko ni afya.

“Nyepesi” za wiki hii ni pamoja na taarifa kwamba “wanene” 7 ndani ya baraza jipya la mawaziri la Gordon Brown (mrithi wa Tony Blair) wamekiri katika nyakati tofauti kuwa walishawahi kutumia “widi” (kwa wale ambao lugha ya mtaani ni mgogoro, “widi” ni bangi au marijuana).Siku kadhaa zilizopita,kiongozi wa chama cha wahafidhina (Conservative Party) David Cameron naye alijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kupatikana nyeti kuwa alikuwa akivuta bangi katika siku za ujana wake.Cameron amekataa kuendelea na mjadala wa suala hilo akisema kuwa kila binadamu anaweza kufanya makosa hususan akiwa kijana.Alitaka wanaomshupalia wamhukumu kwa utendaji wake wa kazi wa sasa na sio mambo aliyofanya nyma.Kali zaidi ya zote ni pale Katibu wa Ofisi ya Mambo ya Ndani (Home Office-yaani ni sawa na Wizara ya Mambo ya Ndani huko nyumbani),Jacqui Smith,na waziri mmoja katika ofisi hiyo (hapa katibu wa wizara ni mkubwa kicheo kuliko waziri),Tony McNulty,walipotangaza hadharani kuwa nao walishawahi kuvuta bangi huko nyuma.Na “ushuhuda” huo umekuja wakati mwanamama huyo (Smith) akitangaza mpango wa serikali kuangalia upya uamuzi wa awali wa serikali ya Blair wa kushusha daraja (declassifying) la bangi.Habari kwamba viongozi hao wawili (ambao pamoja na majukumu mengine wana dhamana ya kudhibiti mihadarati) waliowahi kuwa wavuta bangi zimezua mjadala kama kweli wanapaswa kuendelea na nyadhifa zao.Pengine kinachowasaidia ni ukweli kwamba kuna wanasiasa wengine (wakiwamo mawaziri vivuli wa upinzani) ambao nao wameweka bayana kuwa walishawahi kuvuta bangi walipokuwa vijana.Uwazi na ukweli au vituko vya siasa?


Kuna habari nyingine ya majonzi lakini kwa namna flani inaweza inachekesha.Mwanamke aliyekuwa na uzito mkubwa kuliko wote hapa Uingereza,Nazima Hussein,amefariki na kuwaacha wanandugu wakiwa na wakati mgumu baada ya kubambikwa ushuru wa pauni 4,000 (zaidi ya shilingi milioni 8) kutoka kwa manispaa huko Southall,London.Ushuru huo ulitokana na gharama za kuuhudumia mwili wa marehemu ambao ulihitaji watumishi wa kikosi cha zima moto (firemen) 13 kuutoa mwili huo (uliokuwa na unene wa futi 3) kutoka katika flati aliyokuwa akaishi.Na walipoufikisha mochwari huko Uxbridge ilizuka kasheshe nyingine kwani hakuna toroli la kubebea maiti lililomtosha marehemu na pia mafriji yote ya kuhifadhia maiti hayakuweza kumudu ukubwa wa mwili wa marehemu huyo.Marehemu Nazima alifariki akiwa na uzito wa kilo 349 .Habari njema ni kwamba baada ya watu wa Manispaa “kusomeshwa” walikubali kupunguza gharama hadi pauni 3,000 (zaidi ya shilingi milioni 6).Ukiskia msiba mzito ndio huo.

Turejee nyumbani.Siku chache taifa limepewa changamoto ya kutosha kutoka kwa JK kuhusu suala la “kupima ngoma” (ukimwi).Na kwa mujibu wa taarifa za magazeti mbalimbali ya huko nyumbani watu kadhaa wameitikia wito wa Rais kwa kwenda kwenye vituo vya afya kupima ukimwi.Kwa mtizamo wangu,hamasa aliyotoa JK inaweza kuwa na matokeo makubwa sana kwani kwa upande mmoja inaweza kuwasaidia wale waliokuwa hawajui kama wameathirika kuanza kuchukua tahadhari ambazo zitawasaidia kuishi maisha marefu zaidi.Pia kwa wale ambao vipimo vitaonyesha hawajaathirika wanaweza kuachana kabisa na matendo ya ngono zisizo salama,na hata kumrejea Mola wao.Kadhalika,kwa wale watakaokutwa wana virusi vya ukimwi na wakati huohuo wana familia zinazowategemea wanaweza kupata nafasi mwafaka ya kuandaa “future” za familia zao.Jingine ni kwamba kampeni hiyo inaweza kuwafumbua macho wale vichwa sugu na viwembe wanaopenda kujidanganya kuwa ukimwi ni ajali kazini,na eti ajali haina kinga.

Waziri wa Afya amelielezea Bunge kuwa kuna mpango wa kuwapima ukimwi wale wote wanaofika hospitali kwa matibabu.Wazo hilo ni zuri sana lakini linahitaji tahadhari ya namna flani.Wapo wanaosema kuwa ukimwi ni sawa na maradhi mengine yasiyo na tiba kama kansa au kisukari.Hapana,ukimwi ni tofauti sana hasa kwenye namna jamii yetu inavyowaangalia walioathirika na ukimwi (unyanyapaa).Nadhani wapo watakaokubaliana nami kwamba baadhi ya watumishi wa taasisi za afya wana tabia ya kukiuka maadili ya taaluma yao kwa kutoa siri kuhusu afya za wagonjwa.Naamini baadhi ya wasomaji wameshawahi kunong’onezwa na dokta au nesi flani kuwa “yule nanihii anao (ukimwi).” Sasa kama Wizara ya Afya itatekeleza dhamira yake ya kutaka watu wote wanaofika hospitali wapime ukimwi inapaswa pia kuboresha mambo kadhaa ikiwa pamoja na kuhakikisha kuna washauri nasaha wa kutosha watakaoweza kuwasaidia hao watakaobainika kuwa “wanao.” Naamini pia kuwa kuna sheria inayowabana watumishi wa afya kutoa “siri” ya ugonjwa wa mtu,na katika mpango huu wa Wizara ni muhimu sheria hiyo ikaimarishwa zaidi kwani bila kufanya hivyo si ajabu watu wanaweza kukwepa kwenda hospitali sio kwa kuhofia kupimwa na kukutwa wanao bali kwa kuwaogopa hao wauguzi wasioweza kuhifadhi siri za wagonjwa.Pia Wizara inapaswa kuweka bayana iwapo mpango huo wa kumpima kila mgonjwa utakuwa ni suala la hiari au la lazima.Kwa hapa,wagonjwa wanahamasishwa kupima ukimwi lakini hawalazimishwi.Pasipo kuweka misingi mizuri,nia nzuri ya Wizara ya Afya inaweza kuleta mkorogano usio wa lazima,maana si ajabu tukasikia flani kanyimwa nafasi ya kuonana na daktari kwa vile tu kukataa kupima ukimwi.Ifahamike kuwa suala la kupima au kutopima ni haki ya mtu binafsi.

Pia nimesoma habari iliyonisikitisha husu kilio cha Kamisheni ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kwamba imekuwa ikipata ushirikiano hafifu kutoka kwa waajiri katika suala la kuhakiki vyeti vya taaluma za waajiriwa.Unajua utandawazi umeleta mambo mengi sana ikiwa ni pamoja na fursa ya mtu kujipatia taaluma bila kutia mguu chuoni.Vipo vyuo kadhaa duniani vinavyotoa kozi kwa njia ya mtandao,lakini tatizo ambalo limekuwa likizisumbua hata nchi za Magharibi ni lile la baadhi ya vyuo vya kitapeli ambavyo vinaweza kukupatia cheti cha Udaktari wa Falsafa kwa wiki moja.Ukiona mfumuko wa madokta (sio wale wa hospitali) usikimbilie kufikira kuwa pengine siku hizi PhD zimekuwa rahisi.Ukweli ni kwamba PhD feki zimetapakaa sana kutokana na vyuo feki (japo vingine vimeandikishwa kisheria) ambavyo wanachojali wao ni fedha tu ya huyo anayehitaji PhD ya chapchap.Inatuuma sana sie wengine ambao tunazeekea maktaba kutafuta huo udokta “wa kwelikweli” huku wenzetu “wanasomea baa au kwenye nyumba ndogo zao” na wanaamka asubuhi na “hangover” wakiwa madaktari wa falsafa.Nadhani falsafa pekee waliyonayo “vilaza” hawa ni kuhusu waganga gani wa kienyeji wanasaidia mtu kula rushwa na aendelee kuonekana mwadilifu au namna ya kutogonganisha magari kati ya mama watoto na nyumba ndogo.

Ukweli mchungu ni kwamba TCU ina wakati mgumu kufanikiwa katika azma yake hiyo njema,kwani wengi wetu tunajua kuwa baadhi ya waajiri nao wana elimu za kutilia mashaka.Pia nadhani kuna mapungufu ya kisheria kuhusu matumizi ya vyeti feki,kwani nakumbuka jeshi la polisi halikuchukua hatua yoyote lilipobaini kuwa mbunge mmoja hakuwa mkweli kuhusu elimu yake ya sekondari.Sasa kama ufeki wa vyeti vya sekondari “sio big deal” kwa polisi je hao wenye PhD feki wataweza kuguswa?Enewei,tuna vita kadhaa tunazopenda zianze dakika hii:dhidi ya wala rushwa,majambazi,wabadhirifu,wauza unga,nk.Pengine siku moja itatangazwa vita ya kitaifa dhidi ya vyeti na taaluma feki.Yote yanawezekana.

Alamsiki


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.