27 Aug 2007

Asalam aleykum,


Kuna habari flani nimeiona gazetini imeniacha nakenua meno kwa kicheko.Kwa mujibu wa gazeti moja la Daily Mail la hapa Uingereza eti inadaiwa kwamba wanawake warefu “wanawazimia sana” wanaume wafupi.Kilichopelekea madai hayo ni maswali wanayojiuliza wafuatiliaji wa mambo ya watu (wambeya?) eti kwanini mwanamitindo wa kimataifa Sophia Dahl “amekolea” kwa mwanamuziki “andunje” wa midundo ya jazz,Jamie Callum.Gazeti hilo linadai kwamba wanaume wafupi huwa wanafanya jitihada sana kuhakikisha kuwa wanafidia “pengo” la urefu wao kwa kujituma kwenye maeneo mengine.Hoja nyingine ya kuchekesha ni ile inayodai kuwa watu wafupi ni “vipotabo” kwa wanawake warefu,na hata wakialikwa kwenye nyumba za watu warefu basi ni rahisi kwa “masoti chesisi” hao kufiti kwenye makochi pasipo kulalamika kuwa miguu inauma iwapo kochi lenyewe ni la kujibana.Sijui habari hiyo inawahusu wanaume wafupi wa nchi za Magharibi pekee au dunia nzima lakini lililo wazi ni kwamba suala la mwanamke kumzimia mwanaume au mwanaume kumzimia mwanamke ni la mtu binafsi,na ufupi,urefu,wembamba au unene sio kigezo muhimu sana japo sote tunafahamu kwamba wengi wetu tuna “mapendezeo” yetu.


Wiki iliyopita nilipata nafasi ya kushuhudia mchezo wa kirafiki wa soka kati ya timu ya taifa ya Scotland dhidi ya ile ya Afrika Kusini (Bafana Bafana),mechi iliyofanyika kwenye uwanja wa Pittodrie hapa Aberdeen.Ilipendeza kuona Waafrika wachache wanaoishi hapa wakiwa wametinga jezi za Bafana kuonyesha sapoti yao kwa timu hiyo.Japo mechi hiyo iliisha kwa Scotland kuibuka na ushindi kiduchu wa bao moja kwa bila, “sie” tuliofungwa (Waafrika wote siku hiyo tuligeuka kuwa Wasauzi) tulifarijika kuiona timu ya “nyumbani” ikitandaza kabumbu la kuvutia.Unajua mara nyingi hawa watu weupe wanakupa heshima pale utapowaonyesha una uwezo sawa nao au pengine zaidi yao.

Na wikiendi nilipata fursa ya kuangalia (kwenye runinga) michuano ya kimataifa ya riadha kutoka huko Osaka,Japan.Kama kawaida,Waethiopia na Wakenya wametesa vilivyo.Nimesoma kwenye magazeti yahuko nyumbani kuwa nasi tunawakilishwa na wanariadha kadhaa.Sijui tutaambulia chochote au itaendelea kuwa hadithi ile ile ya kuwa wasindikizaji wa kudumu.Lakini naamini kwamba kama Wakenya na Waethiopia wanaweza kutawala kwenye anga hizo,basi nasi pia tunaweza kabisa kufanya vizuri.Ni lini tutapata akina Filbert Bayi na Suleiman Nyambui wengine?Upeo wangu mdogo wa Jiografia unanishawishi kuamini kwamba hali ya hewa ya mkoa kama Arusha unatupatia mazingira mazuri ya kuzalisha wanariadha ya viwango vya kimataifa.Na ushahidi upo kwa kuangalia “perfomance” ya baadhi ya mashujaa wetu wa miaka ya nyuma.Penye nia pana njia,na kama tutawekeza vya kutosha basi kwa hakika tutaweza kurejesha historia ambayo kwa sasa imeshaanza kusahaulika.

Kuna dalili za mafanikio huko mbele ya safari kwenye soka letu. “Uchawi wa Kibrazil” wa Maximo na mwenzie Tinoco unaelekea kuzaa matunda.Ukichanganya na sapoti ya kutosha kutoka kwa JK mwenyewe basi si ajabu nasi tukajikuta tunaingia kwenye ramani ya soka ulimwenguni.Kinachonipa shaka ni matatizo ya uongozi kwenye vilabu vyetu vya soka.Maana kila kukicha utasikia wanachama Simba wanataka kupindua uongozi,au wenzao wa Yanga wanamkalia kooni kiongozi flani,au mara usikie kocha flani kabwaga manyanga kwa vile hajalipwa stahili zake,na vioja vingine visivyo na mwisho.Katika makala yangu iliyopita niliwausia viongozi wa Simba kutumia vizuri mkataba walioingia na kampuni moja kupromoti “chata” ya Adidas.Hee!haujapita muda mrefu nasikia baadhi ya wanachama wanapania kuung’oa uongozi ulio madarakani.Na hapohapo nasikia kocha Twalib Hilal anasema anarejea umangani kwa vile hajakamilishiwa malipo yake.Kiongozi mmoja anang’aka jukumu la kumlipa kocha huyo kwa kudai kwamba aliletwa na Friends of Simba.Ok,tuseme kuwa mapenzi ya Friends of Simba kwa klabu yao yaliwasukuma kumtafuta kocha mwenye uwezo wa kuipeleka mbali klabu ya Simba,na wakamsomesha Twalib hadi akakubali kusamehe mshahara mnono huko Umangani.Sasa,viongozi hawakupaswa kubweteka na kuliacha jukumu la mshahara kwa Frienda of Simba pekee.Kwanza,msaada uliotolewa na kikundi hicho unaweza kutafsiriwa kama msaada kwa uongozi kwani sote tunajua “politiki” za Simba na Yanga:matokeo yakiwa mabaya basi uhai wa viongozi kuwa madarakani unakuwa unaning’inia kwenye utando wa buibui.

Ni kama kichekesho vile kwa sababu miezi michache iliyopita,uongozi huohuo wa Simba uliweka msimamo thabiti dhidi ya kundi la Friends of Simba wakidai kundi hilo linaihujumu klabu hiyo.Navyoelewa mimi ni kwamba kwa vile klabu hiyo inajiendesha “Kiswahili” ni lazima wawepo watu wa kuikwamua kifedha pale inapokwama,na kwa namna mambo yalivyo,kila wakati uchumi wa vilabu vyetu ni wa kusuasua kama suala la amani huko Somalia.Ufumbuzi wa matatizo sio Mapinduzi,kwani yameshafanyika mengi tu na hakuna lolote la msingi lililopatikana.Wala kukimbilia mahakamani sio ufumbuzi wa matatizo.Na kuwa na mahusiano mazuri na vipoba hakuwezi kuwa ufumbuzi wa kudumu wa matatizo ya klabu kama Simba.Ufumbuzi pekee ni kwa vilabu hivyo kujiendesha kibiashara.Soka ni zaidi ya burudani kwani ikiendeshwa kisasa inaweza kuwa chanzo kizuri cha mapato.Unaposikia Manchester United,Chelsea au Liverpool zinavutia wawekezaji kutoka nje ya Uingereza sio kwamba matajiri hao ni wakereketwa sana wa soka (ingekuwa ni ukereketwa basi wangenunua vilabu katika nchi zao) bali wanajua bayana kwamba soka ni biashara yenye faida.

Twanga Pepeta wako ziarani hapa Uingereza,na wametapisha kumbi walizotembelea.Hivi kwa mfano Simba au Yanga wangefanya ziara sehemu mbalimbali duniani wasingeweza kujichumia mapato mkubwa pengine zaidi ya hayo wanayopata Twanga?Na kwa kufanya ziara nje ya nchi vilabu vyetu vingeweza kuua ndege wawili kwa jiwe moja:kutengeneza mapato ya kutosha na kuitangaza vipaji vya wanasoka wao,ambao wakipata timu huku nje inamaanisha mapato zaidi kwa vilabu hivyo.Najua wapo wanaoniona kama nimechanganyikiwa kwa kutoa mawazo kama haya.Siwalaumu kwani kwa jinsi wanavyofahamu ubabaishaji uliokithiri kwenye vilabu vyetu,hata ziara za mikoani zinahitaji mitulinga ili ziwe na mafanikio.

Mwisho,ningependa kutumia fursa hii kuwapongeza marais wa nchi za Afrika Mashariki kwa kuzingatia maoni ya wananchi wao kuhusu suala la kuharakisha Muungano wa nchi hizo.Mimi ni muumini wa hekima ya umoja,yaani umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu.Lakini umoja kati ya watu wenye “backgrounds” zinazotofautiana unaweza usizae matokeo yanayokusudiwa.Nilisoma sehemu flani ambapo DCI Manumba aliweka bayana kuwa kuongezeka kwa wimbi la ujambazi huko nyumbani kunachangiwa kwa kiasi kikubwa na wageni wanaoingiza nchini pasipo kufuata taratibu za uhamiaji.Ni ukweli usiopingika kuwa hali ya amani iliyopo Tanzania ni kivutio kizuri kwa “watu wa shari” kutoka nchi jirani.Unadhani hali itakuwaje pindi “washari” hao watakuwa wanaweza kuingia Tanzania kirahisi kama vile mtu anavyotoka Ilala kwenda Temeke hapo Muungano huo utakapokuwa umekamilika.Lakini hoja hiyo ya uhalifu ni ndogo tu ukilinganisha na ukweli kwamba tuna mambo yetu kadhaa ya muhimu tunayopaswa kuyashughulikia kwanza kabla ya kufikiria kujitanua.Na miongoni mwa mambo hayo muhimu ni suala la Muungano kati ya “Tanganyika” na Zanzibar.Halafu kuna hii “lulu” yetu ya amani na utulivu.Najua kila mtu ana tafsiri yake ya neno “amani na utulivu” lakini naamini sote tunakubaliana kuwa hatuwezi kulinganisha nchi yetu na mbinde za Wahutu na Watutsi huko Rwanda na Burundi au tatizo la ukabila huko Kenya (bila kusahau Mungiki).Na yayumkinika kusema kuwa “uwekezaji” wa wenzetu hapo nyumbani ni mkubwa zaidi ya wetu huko kwao.Mazingira yaliyoiua jumuiya ya awali ya Afrika Mashariki bado yapo,na ni vema yakarekebishwa kabla ya kufikiria wazo la Muungano mpya.

Alamsiki






24 Aug 2007


22 Aug 2007

Asalam aleykum,

Nianze na habari “nyepesi nyepesi.” Kwa mujibu wa utafiti ambao matokeo yake yalinukuliwa na gazeti la Daily Mail la hapa Uingereza,kioo kinaweza kuwa na majibu kuhusu hali ya afya ya binadamu.Inaelezwa kwamba “kujishangaa” kwenye kioo kwa muda flani kunaweza kukupatia tetesi kuhusu dalili za matatizo ya kiafya katika mwili wako.Pengine hii itakuwa habari njema zaidi kwa baadhi ya akinamama ambao,kama wengi wetu tujuavyo,huweza kutumia hata nusu saa wakijiangalia kwenye vioo,hususan kabla ya kufanya “mtoko” (kwenda kwenye harusi,kitchen party,ubarikio,nk).Mie ni miongoni mwa “wazembe” ambao naweza kupitisha hata siku tatu bila kujiangalia kwenye kioo (na pengine siko peke yangu).Lakini kwa mujibu wa utafiti huo,kujiangalia kwenye kioo japo kwa muda michache kunaweza kubainisha matatizo ya kiafya kama vile maambukizo ya bacteria,kupanda kwa “cholesterol”, “anaemia”, “arthritis”,upungufu wa Magnesium mwilini,mshtuko wa moyo na hata kubaini ujauzito.Kwa mfano,ukijitazama kwenye kioo na kubaini kuwa macho yamekuwa meupe kuliko kawaida,basi hiyo inaweza kuwa dalili ya kuzidi kwa “cholesterol” mwilini;macho yakiwa yamevimba pasipo sababu inaweza kuwa dalili ya maambukizo ya bacteria au pengine “arthritis”;kope (“eyelids”) zinazoonekana kama zinataka kunyonyoka zinaweza kuashiria dalili za “anaemia”;jicho linalozunguka bila kuzungushwa (“myokymia”) linaweza kuashiria upungufu wa Magnesium;kupauka kwa rangi ya mwili kunaweza kumaanisha dalili za homa ya manjano au matatizo ya maini;fizi zinazotoka damu zinaweza kuashiria “leukaemia” au ujauzito;na mipasuko kwenye “lips” kunaweza kuashiria kisukari.Hata hivyo,kama yalivyo matokeo ya tafiti nyingi,matokeo ya utafiti huu kuhusu “faida za kioo katika kubaini hali ya mwili” hayamaanishi kuwa kila dalili utakayoiona kwenye kioo (kati ya hizo zilizotajwa) basi lazima inaashiria ugonjwa flani.Ni dhahiri kwamba mtu “akilamba” mzinga mzima wa “Mzaramo” (Konyagi) basi siku inayofuatia anaweza kuwa na macho yaliyovimba,na wala si dalili za “arthritis” au maambukizo ya bacteria (sidhani kama bacteria wana jeuri ya kumudu makala ya Konyagi.,,natania tu!).Lakini nadhani licha ya kujiangalia kwenye kioo kwa madhumuni ya kujua kama “reception” (sura) iko maridhawa,kujitazama mwenyewe kwenye kioo kunaweza kukusaidia kujisuta kama umefanya jambo baya,kujipongeza kama umefanya jambo zuri na hata kujishauri pale unapokuwa njia panda kutokana na matatizo au ugumu wa kutoa maamuzi.

Na utafiti mwingine kwa mujibu wa jarida la Saikolojia ya Uchumi (the Journal of Economic Psychology) watu wenye sura nzuri wana uhakika wa kipato kizuri zaidi kushinda wale wenye “sura mbaya.” Wachumi James Andreoni na Ragan Petrie wanaeleza kwamba katika kuangalia mafanikio ya kipato kati ya watu wenye sura nzuri na wale wasio na sura nzuri wamebaini kuwa hata pale watu wa makundi hayo mawili wanapofanya jitihada zinazolingana,wengi wa wenye sura nzuri “wanaibuka kidedea”.Watafiti hao wanaamini kwamba kinachowasaidia wenye sura nzuri kuwa na mafanikio ni ukweli kwamba watu wa aina hiyo huwa na matarajio makubwa ambayo wangependa yawe na matokeo mazuri yatakayoshabihiana na sura zao nzuri.Pia walibaini katika utafiti huo kwamba watu wenye sura nzuri wakizembea “kulinda uzuri wao” (kwa mfano kutojiweka “sopu-sopu” au kuongezeka “nyama za uzembe”) basi wale wanaonekana “wabaya” kwa sura wanapata nafasi ya “kuwapiga bao” (kuchukua nafasi za) hao wenye sura nzuri.Swali nililobaki nalo baada ya kusoma taarifa hizo ni kwamba nani ana mamlaka ya kusema flani mzuri au flani mbaya,pengine kwa kuzingatia msemo wa Kiswahili kwamba “apendae,chongo huona kengeza” au hata pengo kuitwa mwanya.

Pia,siku chache zilizopita wanafunzi kutoka nje ya Uingereza tulipata habari iliyowaacha baadhi ya “wenyeji” wetu wakiwa wamenuna.Kwa mujibu wa Dokta Bernard Lamb,msomi (reader) wa “genetics” kutoka Imperial College London,wengi wa wanafunzi wa kigeni wanaonekana kukimudu vema Kiingereza kuliko wanafunzi wazawa (Waingereza),ambapo wageni hao huwa na makosa machache wanapoandika au kuongea lugha hiyo ulinganisha na hao wenye lugha yao.Dr Lamb alieleza kwamba wanafunzi kutoka nchi za Singapore na Brunnei ndio wanaoongoza kwa ubora wa Kiingereza japokuwa lugha hiyo sio yao ya asili (ni second language).Amesema kwamba sio jambo gani kwa wanafunzi wazawa kuandika kwenye insha zao maneno kama “there” pale inapopaswa kuwa “their” au “bean” pale inapopaswa kuwa “been,” au kutamka “effect” badala ya “affect” na “sun” badala ya “son,” au badala ya wingi (plural) ya “tomato” kuwa “tomatoes” wao wanachapia “tomatos” na badala ya “theories” kama wingi wa “theory” wao wanaibuka na “theorys.” Msomi huyo anadai kuwa udhaifu mkubwa uko kwenye sarufi (grammar) na vituo (punctuation),na sasa anaandaa kitabu cha kuziumbua mamlaka za elimu kwa kuzembea kuweka mkazo kwenye kuboresha somo la Kiingereza mashuleni.

Kadhalika,moja ya mambo yaliyotawala anga za siasa za ndani za Marekani ni tangazo la mpanga-mikakati mkuu (“chief political strategist”) wa rais Bush,Karl Rove,kuwa anajiuzulu mwishoni mwa mwezi huu.Huyu jamaa ana akili sana,tena sana.Tayari wapo wanaodai kuwa hakuna mtu mwenye uwezo wa kuziba pengo lake hapo White House baada ya kuondoka kwake.Inategemea unazungumza na mtu aliye upande gani wa mjadala,kwani kuna watu wanaomtuhumu Rove kwa “kumpotosha” Bush katika maamuzi mbalimbali,na wanadai kuwa kupungua kwa umaarufu wa urais wa Bush (huko Marekani kila baada ya muda flani huwa zinatolewa “ratings” za utendaji kazi wa rais, “congress”,nk na kwa sasa wanaorodhishwa na utendaji kazi wa Bush ni asilimia 32.9 tu huku asilimia 62.4,yaani zaidi ya nusu ya Wamarekani,hawaridhishwi na utendaji kazi wake) kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na swahiba huyo wa Bush.Lakini,mpende au mchukie,mwanamikakati huyu ni mtu mwenye kipaji cha hali ya juu katika kuhakikisha ushindi unapatikana kwa kila aina ya mbinu.Na ndio maana haishangzi kuona baadhi ya watu wakijiuliza kama kutatokea mtu mwenye kipaji kama cha Karl Rove.Yayumkinika kusema kuwa kujiuzulu kwake kumekuja wakati mbaya kwani ripoti inayosubiriwa kwa hamu kutoka kwa kamanda wa majeshi ya Marekani huko Irak,Jeneral David Petraeus,kuhusu mwenendo mzima wa vita ya Irak inatarajiwa kuwasilishwa katikati ya mwezi ujao,na wapo wanaodhani kwamba kukosekana kwa Rove katika kipindi hicho muhimu kunaweza kuwa ni tatizo kwa Bush iwapo ripoti hiyo itakuwa siyo nzuri.Rove ambaye anaelezwa kama mtu atakayengia kwenye vitabu vya historia kama kiumbe asiye na huruma (ruthless) linapokuja suala la kufanikisha matakwa ya kisiasa ya bosi wake,na ambaye alipachikwa jina la utani la “the Architect” (msanifu) kutokana na ufanisi wake kwenye sanaa ya kupanga mikakati,alimsaidia Bush kupata ugavana wa jimbo la Texas mwaka 1994,kabla ya lutoa mchango wa hali ya juu katika ushindi wa Bush kwenye chaguzi za urais za mwaka 2000 na 2004.Japo naweza kuwa miongoni mwa wale wanaoamini kuwa kuna maeneo ambayo “alimpotosha” Bush,na ukweli kwamba tofauti na nguli huyo,mrengo wangu kisiasa ni wa kati ya kushoto (Centre-Left),nimetokea kumhusudu sana Karl Rove (na nadiriki kumwita “role model” katika malengo yangu ya mbeleni).Ukipata nafasi ya kusoma kitabu kiitwacho “Boy Genius: Karl Rove, the Brains Behind the Remarkable Political Triumphs of George W Bush” au “Bush's Brain: How Karl Rove Made George W. Bush Presidential” unaweza kuungana nami “kumkubali” huyu jamaa.

Mwisho,napenda kuwapongeza watani wetu wa jadi Yanga kwa kunyakua kombe la Tusker.Nimesikia “rambirambi” zao kwamba fedha inayotolewa na waandaaji wa mashindano hayo haikidhi gharama halisi walizoingia hadi kufikia hatua ya fainali,lakini nadhani walipaswa kutafakari suala hilo kabla ya kuanza mashindano hayo.Licha ya “kuukosa ubingwa” (haituumi kwa vile hatukufungwa bali tulijitoa) wana Msimbazi tunafarijika na hilo “contract” la nguvu la kuitangaza “chata” ya kimataifa ya “ADDIDAS.” Simba ina bahati na wadhamini,pengine kutokana na rekodi yake nzuri kwenye mechi za kimataifa,lakini ni muhimu kwa Kaduguda na wenzie kuhakikisha kuwa udhamini huo unasaidia katika kutimiza ndoto ya Watanzania kuona vikombe vya michuano mikubwa ya vilabu barani Afrika vinatua nchini.

Alamsiki

10 Aug 2007


Further Updates: "Majibu" ya Mrisho na Tulizo Kilaga.USIKOSE KUSOMA COMMENTS MBALIMBALI MWISHO WA MAKALA HII NA KWENYE BLOGU YA MRISHO

Latest Updates: Baada ya "washtaki" kuwa judge,jury and prosecutor,hatimaye mtuhumiwa apewa nafasi ya kujieleza

Updates: Mashambulizi yaendelea

Updates: Kaazi kweli kweli

Mtanzania huyu kumponza Mengi

Ni mropokaji, anayeandika bila kufanya utafiti
Na Mwandishi Wetu
Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Aberdeen, Scotland, Evarist Chahali huenda akamponza Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi, ambaye pia ni mmiliki wa gazeti la Kulikoni, kufuatia habari potofu aliyoiandika kwenye gazeti hilo dhidi ya gazeti la Risasi.

Kwa mujibu wa habari hiyo, mwandishi huyo ambaye ni Mtanzania anayedai kuchukua kozi ya Udaktari wa Falsafa (PhD) katika chuo hicho, aliandika makala ya kuyashutumu magazeti ya Udaku kuwa yanaandika habari feki na kutolea mfano gazeti la Risasi.

Katika makala yake ya Jumatano Agosti 8, mwaka huu, Chahali alidai kuwa habari zilizoandikwa kwenye gazeti la Risasi ambalo ni dada la hili, zilizoambatana na picha hazikuwa na ukweli wowote.

Chahali alitolea mfano wa habari iliyochapwa kwenye gazeti hilo la Julai 18-20 iliyokuwa na kichwa cha habari 'Warembo wa TZ wapiga picha za X tupu'.

Habari hizo ambazo chanzo chake ni mtandao, zilieleza kuwa wasichana hao ni Watanzania waliopiga picha wakiwa watupu kwa nia ya kutangaza biashara ya kuuza miili ambapo waliweka bayana mawasiliano yao.

Hata hivyo, Chahali alidai kuwa habari hiyo ni ya uongo (feki), kwani picha zilizotumika ni za nyota wa sinema za ngono (porn star) wa Marekani na si Watanzania.

Mwandishi huyo alieleza katika makala yake hiyo kuwa, aliamua kuandika hivyo baada ya kuambiwa na rafiki yake anayeishi Marekani.

Akiongea na gazeti hili, Meneja Mkuu wa Kampuni inayochapa gazeti hilo, Abdallah Mrisho, alisema kuwa amesikitishwa na makala ya gazeti la Kulikoni ambayo haikufanyiwa utafiti wa kutosha.

"Habari iliyoandikwa na gazeti la Risasi ni ya kweli, hatujawahi kuandika wala haturuhusu wahariri wetu kuandika habari za uongo ndani ya magazeti yetu, ila Chahali ameropoka.

"Kimsingi mwandishi wa makala hayo, (Chahali) ameonyesha udhaifu mkubwa kwa kuandika habari bila kufanya utafiti na kufikia uamuzi wa kushambulia gazeti letu bila kuwa na uhakika na alichokiandika", alisema Mrisho.

Mrisho aliendelea kusema ana wasiwasi hata na shahada alizonazo Chahali, kwani mtu mwenye elimu kama yake hawezi kuandika habari za kuambiwa bila kufanyia utafiti, hivyo kuupotosha umma na anaweza kumponza mmiliki wa kampuni inayochapisha gazeti hilo, ambaye anaheshimika sana.

"Chahali hakupaswa kutoa shutuma nzito kama zile kwa maneno ambayo hakuyafanyia uchunguzi na kuchapa kwenye gazeti, kwani anaweza kumponza mmiliki wa kampuni hiyo tunayemuheshimu, anapaswa kuona aibu (shame on him)," alisema Mrisho.

Kuthibitisha kuwa habari iliyoandikwa ni ya kweli, wahariri wa gazeti la Risasi wamelazimika kutaja anuani ya tovuti ambako wasichana hao wanapatikana, ili umma kwa ujumla uelewe nani mkweli kati ya Chahali na gazeti la Risasi, ingawa haikuwa kusudio lao kufanya hivyo.

Anuani hiyo ni http://swallowmyjuice.hi5.com ambako picha zilizotumika, mahali wanakoishi na utambulisho wa wasichana hao vinapatikana.

Aidha, kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari cha kuaminika kilichoko ndani ya chuo cha Aberdeen, Chahali ni miongoni mwa wanafunzi wasiofanya vizuri sana katika masomo yao.

"Chahali sio miongoni mwa wanafunzi wanaofanya vizuri sana chuoni," kilisema chanzo hicho.

Baadhi ya wanafunzi wanaosoma kozi moja na Chahali katika chuo hicho ni pamoja na Timofei Agarin, Gordon G. Davidson, Joyleve Elliat, Anna Gustavon, Jeremy Lamoreaux, Giseong lee, Yang Lia, Khristus Vassis, Lortraine Whitty na Anna Zawak.

Mrisho alimtahadharisha mhariri wa gazeti hilo kuwa asipokuwa makini na waandishi wanaoandika makala zao kwa chuki binafsi kama Chahali, wanaweza kujikuta kwenye matatizo makubwa.

Akiongea na mwandishi wetu kwa simu juzi, Mhariri Mtendaji wa magazeti ya This Day na Kulikoni, Evarist Mwitumba alisema kuwa hana habari kuhusu makala hayo.

"Nipigieni kesho asubuhi, kwa sasa niko barabarani naendesha gari na sijasoma gazeti lililoandika habari hiyo," alisema Mwitumba.


HAYA NI MAONI YA WATU MBALIMBALI KATIKA BLOGU YA IJUMAA/RISASI http://abdallahmrisho.blogspot.com KUHUSU MASHAMBULIZI DHIDI YANGU


mkandamizaji said...
Mrisho

Mimi sio mtaalam wa masuala ya mtandao, lakini hakuna mtandao ambao unavurugwa sana na watumiaji kama hi5.com. Kama hichi ndo chanzo chako pekee cha hiyo habari, nasikitika kuwa nitakuwa upande wa chahali kukusuta kuwa picha zile ni za Wamarekani na kuwa nyie mmedanganya watanzania.

Tupe mitandao yenye URL zinazoeleweka sio hi5.com. Mtu anaweza kuweka picha ya mtu yeyote kwenye hi5.com. Na kama nakumbuka kuhusu maelezo ya ile habari, ulisema kuwa kuna namba za simu, eno wanakopatikana hao wadada na mambo kama hayo. Lakini kwa hi5.com ambayo ni mtandao wa marafiki tu, bado hajani conivnce kuwa ulikuwa na source nzuri ya habari.

Najua unaweza kuamua kutotundika hii comment, lakini ujumbe utakuwa umeupata.

Asante

August 9,:53 PM
================================================================
Anonymous said...
Nyote mnahitaji kuwa makini.Mbona hakuna cha ajabu katika hizo picha mnazozizungumzia?Bikini ni nguo za kawaida tu jamani..tuache ushamba na ushambenga watanzania.

August 10, 2007 1:02 AM
===================================================================
kichuguu said...
Nimeangalia picha zile pale Hi5, nina wasiwasi kuwa naweza kukubaliana na chahali kuwa wale ni pornstar wa kimarekani. mambo matatu yanawezekana:

(a)wasichana wa kitanzania wametumia picha za mastar hao.

(b) mastar wameamua kudanganya kuwa wako Tanzania.

(c) mastar hao ni watanzania.

Picha hizo hazikupigwa katika mazingira ya Tanzania. Baadaye nitakutafutia picha nyingine za yule anayejiita Melanie ndipo utakapogundua kuwa siyo za kutoka mazingira ya Tanzania.

August 10, 2007 6:40 AM
===================================================================
mzalendo said...
tumesikitishwa sana kuona vyanzo vyetu vya habari havina uhakika na habari zao. hiyo website iliyotolewa na gazeti la ijumaa inaonyesha moja kwa moja kuwa hao watu mmoja ni MGANDA na wote ni GAYS/ LESBIANS!
mbili ni kuwa hamkuhakikisha kama hizo picha ni za hao MNAOWAITA WAREMBO wa KIBONGO na MMEWASILIANA NAO. Mnauhakika gani kama ni picha za wabongo???? mpaka mkaamua kuandika gazetini?? ....au ndo mnafanya chochote kuuuza magazeti yenu?

August 10, 2007 7:59 AM
===================================================================
Anonymous said...
website mliyotupatia inahakikisha kuwa muandishi wa RISASI hana uhakika na alichokisema, kwa vile website hiyo inaonyesha kuwa wale ni GAYS/LESBIANS na pia HAILAZIMISHI kuwa zile picha ni za hao walioziweka na wala hamkutupa ushahidi kuwa mlihakikisha hao mlowapigia simu ndio wenye picha zile.

August 10, 2007 8:02 AM
====================================================================
Anonymous said...
na kwa vile hakuna uhuru wa kujielezea , na jua nilichokiandika hutokipublish

August 10, 2007 8:04 AM
===================================================================
Anonymous said...
nyote hapo juu nahisi mnamiss point, chahali aliamua kuwakandia wenzake bila kujua kama zile picha kweli zipo na wahusika wamejitambulisha kama wabongo, hivyo ishu sio kama ni wabongo au sio wabongo, ila ishu iliyopo hapa ni kwamba kwa nini Chahali amewakandia jamaa wa risasi na kudai wanaandika habari feki? kwa nini, wakati vitiu hivyo vipo? kama jamaa angefanya utafiti kidogo, angekuwa na ishu tofauti ya kuwabana.. hapa nawaunga mkono jamaa wa risasi..

August 10,:27 AM
===================================================================
Anonymous said...
Mimi naungana na Chalali kuwa magazeti hayo mara nyingi wanaandika habari za uongo ili watu wanunu e magazeti, utakuta mtu anaandika eti kapigiwa simu na mtu wanaandika habari kwenye gazeti je hii ni sawa??? unatunia uongo kupata pesa za watu???? I think tuungane watanzania tuanzishe kampeni za kutonunu magazeti ya udaku!!! Hongera chalali, najua unaweza usitoe hii lakini msg will be sent

August 10, 2007 1:10 PM
===================================================================
Anonymous said...
kwanza hii habari mbona imepindishwapindishwa jamani, kichwa cha habari cha muhusu Mengi, Ndani ya habari main content gazeti la Risasi.Mambo tofauti tofauti.

Simtetei Chalali...ila swala la kutofanya vizuri darasani linawahusu nini hasa, au linahusika vipi na habari yenyewe?...Huo ni mpindisho tosha na ni kupakana matope. Hatuelewi huyu jamaa anasoma katika mazingira gani, isitoshe level anayosoma Phd. haijadiliwi tena kama anafanya vizuri au vibaya darasani. Watanzania tuangalie cha kuandika.
Last point, magazeti ya udaku yapo hata Ulaya, ila cha muhimu ni kuandika mambo ambayo kweli yapo, au yametokea, si kubahatisha ili kuuzisha gazeti.

August 10, 2007 1:19 PM
===================================================================
mkereketwa said...
kama hiyo website ya porn iliyowekwa , chahali alikuwa na haki ya kupinga maelezo ya RISASI kwa vile hao watu hawapo TZ bali wanafanya kazi ya porn Marekani.
tusingefurahi kudanganywa na magazeti kwa kutofuatilia vyanzo vyao vya habari kikamilifu.
kosa la RISASI ni kutokufuatilia kikamilifu hao waliotowa namba zao na wapi wanapatikana kama ni sawa na hao walioweka picha za uchi kwenye Hi5. ushahidi mkubwa unaonyesha kuwa walitumia picha za hao watu tu kujipa umaarufu na kinachoshangaza ni kuona RISASI haikusema kuwa haikutuambia kuwa kuna uwezekano kuwa zile picha si zao.

August 10, 2007 2:45 PM


PIA NIMEONA MAONI HAYA HUKO JAMBO FORUMS

Vyanzo vya Habari vya Magezeti Mengine
Mimi ni msomaji sana wa blogu ya Abdallah Mirosho ya http://www.abdallahmrisho.blogspot.com. Blogu hii hunipatia udaku safi sana kutoka mitaa mbali mbali ya Dar es Salaam. Habari niliyonukuu hapa ilinishtua sana kwamba badala ya wao kukubali kuwa magaxeti yao ni ya udaku, wakaamua kumtukna mwandishi aliyewasema kuwa habari waluyokuwa wameandika haikuwa sahihi.

Quote:

Mtanzania huyu kumponza Mengi

Ni mropokaji, anayeandika bila kufanya utafiti

Na Mwandishi Wetu

Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Aberdeen, Scotland, Evarist Chahali huenda akamponza Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi, ambaye pia ni mmiliki wa gazeti la Kulikoni, kufuatia habari potofu aliyoiandika kwenye gazeti hilo dhidi ya gazeti la Risasi......Kwa mujibu wa habari hiyo, mwandishi huyo ambaye ni Mtanzania anayedai kuchukua kozi ya Udaktari wa Falsafa (PhD) katika chuo hicho, aliandika makala ya kuyashutumu magazeti ya Udaku kuwa yanaandika habari feki na kutolea mfano gazeti la Risasi.Katika makala yake ya Jumatano Agosti 8, mwaka huu, Chahali alidai kuwa habari zilizoandikwa kwenye gazeti la Risasi ambalo ni dada la hili, zilizoambatana na picha hazikuwa na ukweli wowote......Chahali alitolea mfano wa habari iliyochapwa kwenye gazeti hilo la Julai 18-20 iliyokuwa na kichwa cha habari 'Warembo wa TZ wapiga picha za X tupu'.....Hata hivyo, Chahali alidai kuwa habari hiyo ni ya uongo (feki), kwani picha zilizotumika ni za nyota wa sinema za ngono (porn star) wa Marekani na si Watanzania................Kuthibitisha kuwa habari iliyoandikwa ni ya kweli, wahariri wa gazeti la Risasi wamelazimika kutaja anuani ya tovuti ambako wasichana hao wanapatikana, ili umma kwa ujumla uelewe nani mkweli kati ya Chahali na gazeti la Risasi, ingawa haikuwa kusudio lao kufanya hivyo.Anuani hiyo ni http://swallowmyjuice.hi5.com ambako picha zilizotumika, mahali wanakoishi na utambulisho wa wasichana hao vinapatikana....Aidha, kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari cha kuaminika kilichoko ndani ya chuo cha Aberdeen, Chahali ni miongoni mwa wanafunzi wasiofanya vizuri sana katika masomo yao...."

Nilipoangalia picha zilizosemekana za watanzania pale http://swallowmyjuice.hi5.com, nilikuta mwanadada mmja anayejiita Melanie ambaye kwa bahati mbaya ninadhani namfahamau vizuri na picha hiyo imepigwa zaidi ya miaka saba iliyopita. Mwanadada yule alikuwa mmoja wa ma-hooker wazuri sana pale South Beach Miami na nadhani kuwa alikuwa damu mchanganyiko mwasia na mwafrika. Nimeweza kupata baadhi ya picha zake nyingine kwenye websites chafu kama hii hapa. (ONYO: PICHA HIZO NI CHAFU SANA USIZIFUNGUE MBELE YA WATOTO NA WATU WA HESHIMA.)


Swali, je mwandishi wa Risasi kweli alifanya haki kumtolea matusi ya kashfa mwandishi wa Kulikoni kuhusu uhalali wa picha zile kama kweli zilikuwa za akina dada wa kitanzania?
__________________
Kichuguuu: Nyumba inayohifadhi mchwa na nguchiro kwa pamoja bila mkwaruzo

2 Aug 2007

Asalam aleykum,

Wanasema kuwa siasa inahitaji kuwa na mvuto (appeal).Lakini mvuto wa mwanamama Myra Bushell,mshindi wa uchaguzi mdogo wa kanseli kwa tiketi ya chama cha Liberal Democrats cha hapa Uingereza,ni zaidi ya mvuto wa kawaida unaohitajika kwenye siasa.Myra aligombea na kushinda nafasi ya uwakilishi kwenye kanseli ya Bideford huko Devon,huku akiwa ni mcheza-uchi/nusu uchi kwenye vilabu (stripper) na mwendesha huduma ya ngono-kwa-simu (phone-sex-line) ambayo anachaji pauni 1.50 kwa dakika (takriban shilingi 3500 za huko nyumbani).Yeye anajitetea kuwa hayo ni maisha yake binafsi nje ya siasa,lakini tayari wajumbe watatu wa kanseli hiyo wameshajiuzulu kupinga vitendo vya mwanasiasa huyo ambaye pia ana tovuti yake ya huduma za ngono.Myra anajitetea kwamba wakati anautumikia umma kama mwanasiasa,anapaswa pia kumudu gharama za maisha,na ndio maana amekuwa akijihusisha na shughuli hizo “nyeti.” Habari njema kwake ni kwamba katibu (clerk) wa kanseli hiyo,George McMauchlan,ametamka bayana kuwa Myra hajavunja sheria yoyote ya maadili ya kazi ya ujumbe wa kanseli kwa vile “shughuli zake binafsi nje ya siasa” haziathiri utendaji wake wa kazi.Kaazi kweli kweli!!


Tukiachana na habari hizo za mwanasiasa “stripper”, kwa takriban wiki nzima iliyopita,medani za sera za nje za Marekani ilikuwa imetawaliwa na habari kwamba taifa hilo lilikuwa linajiandaa kutekeleza mpango wa kuziuzia silaha baadhi ya nchi za Kiarabu na Mashariki ya Kati.Wanufaika wakubwa wa mpango huo ni pamoja na Saudi Arabia,Misri,na kama ilivyo ada,Israel.Hata hivyo,mpango huo umezaa mvutano wa namna flani kwenye duru za siasa za ndani za Marekani kwani wapo wanaodhani kwamba hoja ya serikali ya Bush kuwa inaziuzia silaha nchi kama Saudi Arabia na Misri ili,pamoja na mambo mengine,kudhibiti kujitanua kijeshi kwa Iran,inaweza kupingana na ukweli kuwa rafiki wa leo anaweza kuwa adui wa kesho,na silaha unazompatia leo kujilinda zinaweza kutumika kesho kukudhuru.Na mpango huu umekuja wakati wachambuzi wa siasa za kimataifa wanaoona kuna kuyumba kwenye urafiki wa muda mrefu kati ya Marekani na Saudi Arabia.Hivi karibuni,Saudi iliweka bayana mtizamo wake kuhusu vita ya Irak kwa kusema kuwa uvamizi wa Marekani nchini Irak unachochea machafuko na suluhisho pekee ni kwa majeshi ya kigeni kuondoka nchini Irak.Pia kumekuwepo shutuma za hapa na pale kwamba Saudi Arabia inavisapoti vikundi vya madhehebu ya Sunni nchini Irak ili kuvikabili vikundi vya madhehebu ya Shia ambavyo inadaiwa vinapata sapoti ya Iran.Kitakwimu na kujiografia,Saudi ni taifa la ki-Sunni wakati Iran ni la ki-Shia,na mahusiano kati ya nchi hizo mbili sio mazuri.Saudi kwa upande wake inahofia sana kukua kwa nguvu za kijeshi za Iran,hasa kwa vile hadi sasa,ukitoa Israel,Saudi ni taifa lenye nguvu kubwa katika eneo la Ghuba na Mashariki ya Kati.

Wakati mwingine ni vigumu kuzielewa sera za nje za Marekani kwani kwa jinsi flani ilipaswa kujifunza kutokana na maamuzi yake ya zamani ambayo kwa namna moja au nyingine yamekuwa yakiiumiza kichwa katika kipindi hiki tulichonacho,kwa mfano msaada wake wa silaha kwa Irak wakati Saddam alipokuwa rafiki wa nchi hiyo,na misaada yake kwa mujahidina wa Afghanistan wakati wa vita dhidi ya Muungano wa nchi za Kisovieti (USSR).Tawala za nchi nyingi za Kiarabu na Ghuba sio za kidemokrasia (kwa vipimo vya nchi za magharibi),na miongoni mwa sababu zinazodaiwa kuchangia kuibuka kwa siasa za msimamo mkali wa kidini katika nchi hizo kushindwa kwa tawala hizo kuleta mabadiliko ya manufaa ya kisiasa,kiuchumi na kijamii.Lakini katika kukoroga zaidi mambo,baadhi ya tawala hizo zimekuwa zikuvikumbatia na kuvifadhili vikundi vyenye msimamo mkali wa kidini ili tawala hizo ziendelee kuwa madarakani.Kwa uchambuzi mwepesi,yayumkinika kusema kuwa hatma ya tawala hizo kwa muda mrefu sio ya kuaminika sana,na Marekani inaweza kujutia huko mbeleni kwa kuzilinda tawala hizo kwa misaada ya kijeshi.

Na taarifa zaidi kutoka Irak zinaeleza kuwa “picha haziivi” kati ya mkuu wa majeshi ya Marekani nchini humo,Jenerali David Petraeus,na Waziri Mkuu wa Irak,Nour al-Maliki.Inasemekana kuwa Maliki alishamuomba Rais Bush amwondoe Jenerali huyo msomi mwenye shahada ya kwanza katika sayansi (Bachelor of Science),shahada ya uzamili katika Utawala wa Umma (M.A in Public Administration) na shahada ya uzamifu kwenye siasa za kimataifa (PhD in International Relations) na alishakuwa (assistant) Professor kwenye US Military Academy. “Bifu” (kupingana) kati ya Maliki na Jen Petraeus kunatokana na baadhi ya maamuzi yanayopingana kati ya watu hao muhimu kwa mafanikio au kutofanikiwa kwenye sera ya Bush kuhusu Irak.Inaelezwa kuwa Maliki haafikiani na mpango majeshi ya Marekani unaoelekea kuasisiwa na Jen Petraeus wa kuvipatia silaha vikundi vya madhehebu ya Sunni ili vipambane na wapiganaji wa Al-Qaeda nchini humo.Maliki ambaye ni muumini wa madhehebu ya Shia anaelekea kuhofia kuwa silaha hizo zinaweza kutumika dhidi ya vikundi vya madhehebu ya Shia,au kwa mtizamo wa muda mrefu,kuchangia vita vya wenyewe kwa wenyewe pindi majeshi ya Marekani yatakapoondoka (kama kuna kuondoka kweli).

Baada ya mjadala wa siasa za kimataifa,hebu tegeukie mambo mengine ya huko nyumbani.Nitahadharishe kuwa naamini baadhi ya ntakayoandika hapa yatawaudhi watu flani lakini kuudhika kwao kutakuwa na maana moja tu kwangu:kwamba ujumbe umefika na wabadilike badala ya kununa.Binafsi,nadiriki kusema kuwa mzazi makini hawezi kumrushusu binti yake kuingia kwenye mambo ya u-Miss.Kwanini?Kwa sababu inaelekea wengi wa mabinti wanaotafuta u-miss huwa aidha wanarubunika kuwa wenye tabia mbovu baada ya kupata majina au pengine fani nzima ya u-miss ni kichocheo cha umalaya (samahani kwa maneno makali).Yaani kila kukicha utaskia sijui Miss nanihii katembea na mume wa mtu,au Wema Sepetu kapigwa picha za utupu,au Faraja Kotta kalibwaga buzi lake lililoiba fedha wapi sijui,na vituo vingine mia kidogo.Kuna kasoro kwenye fani ya u-miss lakini jamii inaelekea imelifumbia macho suala hilo.Lundenga,Chipungahelo na wadau wengine wa fani ya u-miss wana jukumu la kuithibitishia jamii kuwa tatizo haliko kwenye fani hiyo bali ni kwa baadhi tu ya washiriki.Na kama tatizo ni washiriki basi watuambie bayana inakuwaje wanaweza kupenya katika ngazi mbalimbali hadi kifikia levo ta taifa na kuanza kutuonyesha madudu yao.Rafiki yangu mmoja mwandishi wa habari aliwahi kunidokeza kuwa fani hiyo imetawaliwa sana na viongozi,wadhamini na mapromota walafi wa kula uroda ambao wanarahisishiwa kazi na mabinti wenye tamaa ya umaarufu wa chapchap,ambao kwao sio ishu kuvua “makufuli” yao ili wakwae u-miss.Ujumbe wangu kwenu ni simpo:msipokuwa makini mtaondoka kwa kilo mbili,na kwa vile mnathamini sana umaarufu,basi kudhoofika kwa afya zenu kutatawala sana kurasa hizohizo zinazoripoti kila siku namna mnavyoibemenda Amri ya Sita kama hamna akili nzuri.Mkikasirika shauri yenu lakini mmezidi kufanya mambo ya aibu.

Halafu kuna mambo mawili yamenisikitisha sana.La kwanza ni hii tabia ya ubabe inayoelekea kumkolea msanii TID.Binafsi,nazipenda sana kazi za kijana huyu,na mwanzoni nilikuwa namtofautisha na wasanii wengine wa bongo kwa vile amewahi kukaa ugahibuni kwa muda wa kutosha na amekuwa akipata mialiko ya nje mara kwa mara.Lakini pengine kwa kutotambua kuwa taswira (image) ya msanii ni muhimu katika kumuweka au kumporomosha kwenye chati,ameendelea kushika vichwa vya habari kwa matukio yasiyopendeza.Wimbo wake naoupenda sana unaitwa “chagua moja”,nami ujumbe wangu kwake ni mfupi:chagua moja kati ya kujiporomosha wewe mwenyewe kwa matendo yasiyofaa au jirekebishe tabia zako ili uendelee kubaki kuwa “Top In Dar.” Usikasirike,ni somo jepesi tu hilo.

Jingine lililonikera ni gazeti la RISASI ambalo katika toleo lake la Julai18-20 lilikuwa na habari kwamba “Warembo TZ wapiga picha za X tupu…zasambazwa mitaani,baadhi yao ni washiriki wa kusaka mataji ya u-miss.” Kinachosikitisha sio kama iwapo habari hiyo ni ya kweli au ya kubuni bali ni picha zilizotumika kwenye habari hiyo.Rafiki yangu mmoja aliyeko Marekani amenifahamisha kuwa wasichana walioko kwenye picha hizo ni wacheza filamu za ngono (porn stars) wa Marekani na wala sio Watanzania.Kwa kuthibitisha alichokuwa anasema,alinipatia tovuti ambazo zina picha za Wamarekani hao weusi.Kama picha zilizotumiwa na RISASI ni feki basi yayumkinika kusema kuwa hata habari yenyewe ni feki.Hivi ni uzembe wa mhariri kucheki ukweli wa habari husika au ndio kuwafanya Watanzania wajinga kwa kuwapa habari “sensational” ambazo hazina ukweli?Nyie ni watu wazima ambao mmeshatengeneza faida ya kutosha kwa kuandika udaku lukuki wa kweli,sasa tamaa ya nini hadi mfikie hatua ya kunyofoa mapicha kwenye mtandao na kuzusha habari?Shame on you!

Alamsiki

27 Jul 2007

Asalam aleykum,

Katika makala iliyopita niliwapa kituko kimoja kuhusu memba 7 wa kabineti ya Bwana Gordon Brown ambao walikiri hadharani kuwa walishawahi kuvuta bangi wakati wa ujana wao.Maendeleo zaidi (“update”) kuhusu stori hiyo ni kwamba hadi sasa idadi hiyo imefikia mawaziri 10.Lakini wananchi wanaonekana hawajashtushwa sana na “confessions” (vitubio…naamini niko sahihi hapa,au kuna neno jingine linalowakilisha wingi wa kutubu?BAKITA msaada tafadhali) pengine kwa sababu wananchi mawaziri hao watahukumiwa na utendaji wao wa kazi na sio historia zao za kale.Joji Bushi,huyu raisi wa sasa wa Marekani alikuwa “mtu wa matingas” (mlevi) kabla hajamrejea Bwana,lakini ulevi wake wa zamani haukuwa kikwazo kwa yeye kugombea nafasi hiyo ya juu kabisa ulimwenguni.Hata mie nadhani sio vema kumhukumu mtu kwa mambo alofanya zamani,alimradi anayofanya sasa yawe yanaridhisha.Wengi tunafahamu kwamba kuna wale waliosoma seminari na baadae kuingia kuutumikia umma,lakini si ajabu kukuta baadhi yao ni wala rushwa.Kwa maana hiyo,yayumkinika kusema kuwa bora kuwa mtu ambaye kwenye ujana wake alifanya mambo yasiyopendeza lakini sasa anafanya yale yanayotakiw,a kuliko yule ambaye CV yake ya ujana wake ni “supa” lakini kwa sasa anashiriki kuhujumu uchumi wa Taifa letu “changa” (nadhani neno “changa” sasa limeshapitwa na wakati maana taifa letu lina umri wa miaka 45,na naamini huko mtaani ukimwita mtu mwenye umri huo “mchanga” basi patakuwa hapakaliki hapo).

Kwa wale waliokuwa wanafuatilia stori ya Shambo,yule ng’ombe “mtakatifu” kwa Wahindu wa huko Skanda Valle,magharibi ya Wales,habari “latest” ni kwamba “ng’ombe-mungu” huyo amepelekwa mbele ya haki baada ya polisi 30 kuvamia hekalu lake na kumchukua kwa ajili ya kwenda kumchinja.Kwa wale ambao stori hii iliwapitia kando,ni kwamba Shambo alitakiwa kuuwawa baada ya kugundulika kuwa ana kifua kikuu (TB),na hivyo kuhatarisha afya za mifugo mingine katika eneo hilo.Lakini,Shambo si ng’ombe wa kawaida,bali ni “mungu” wa Wahindu,na waumini waliapa kuwa hawako tayari kuona “mungu” wao huyo akiuawa na binadamu.Baada ya mamlaka husika (DEFRA) kuwafahamisha waumini kuwa Shambo anapaswa kuuawa ili kuzuwia kuenea ugonjwa aliokuwa nao.Waumini walipinga uamuzi huo na hatimaye wakakata rufaa Mahakama Kuu ambapo amri ya kumuua “mungu” huyo ilitengeliwa.Lakini mamlaka husika zikaamua kukata rufaa Mahakama ya Rufaa ambapo iliamualiwa kuwa Shambo anastahili kuuawa.Zoezi la kumchukua “ng’ombe-mungu” huyo halikuwa jepesi kwani waumini walijitutumua kadri ya uwezo wao kuhakikisha kuwa Shambo hachukuliwi,na hapo ndipo ikabidi waletwe polisi kumaliza songombingo hiyo iliyochukua zaidi ya masaa 12,huku sakata zima kati ya waumini na DEFRA likiwa limedumu kwa wiki 12.Pengine kufanana kwa namba 12 katika matukio hayo kunaweza kuwa uhusiano na “umungu” wa ng’ombe huyo.

Tukiachana na “safari ya mwisho” ya ngombe-mungu Shambo,tuelekeze macho yetu huko nyumbani.Hebu ngoja kidogo.Kuna nchi inaitwa Guam.Je unaweza ku-guess iko wapi?Enewei,nilikuwa nachemsha kidogo ubongo wako.Nchi hiyo ni “koloni” la Marekani (well,iko chini ya mamlaka ya Marekani) na kwa mujibu wa sensa ya karibuni Guam ina wakazi 173,456.Bila kuingia kwa undani kuhusu jiographia,siasa na porojo nyingie kuhusu ka-nchi hako ambako ni kisiwa,ngoja nikudokezee kuhusu timu yake ya taifa.Hebu angalia matokeo ya mechi zake za hivi karibuni.Ilifungwa 10-0 na China,ikafungwa 15-1 na Hong Kong,na ikalambwa 9-0 na Korea ya Kusini.Kwa sasa inashilia nafasi ya 199 kwenye listi ya FIFA ya ubora wa soka duniani.Nafasi hiyo ndio ya mwisho kabisa,lakini habari njema kwa nchi hiyo ni kwamba haiko pekee kwenye nafasi hiyo kwani Djibouti, East Timor, Belize, the US Virgin Islands, Montserrat, American Samoa, Sao Tome e Príncipe na Aruba pia zinashikilia kwa pamoja nafasi hiyo ya 199.Wahenga walisema kilio cha wengi ni harusi.Kocha wa timu hiyo anawalaumu zaidi wachezaji wake kwa tabia yao ya kuendekeza pati,kujichanganya na magelifrendi wao (au wake zao) na kuthamini zaidi mambo ya binafsi kuliko majukumu yao ya soka.Pia wachezaji wa timu hiyo wanashutumiwa kwa kuzembea mazoezi,na hata wanapofika mazoezini wengi wao huwa wamechoka kutokana na “kujirusha” (sio kujirusha kimazoezi bali “kiaina”).Kiungo wa timu hiyo,Alan Jamison,ameeleza kuwa mara kwa mara akiwa usingizini amekuwa akisumbiliwa na ndoto moja:anaota kuwa amefunga goli (la mpirani…) na uwanja unalipuka kwa mayowe.Kwa bahati mbaya kila asubuhi anapoamka anagundua kuwa timu yake haijapata na haitarajii kupata ushindi hivi karibuni.

Nimeizungumzia timu ya taifa ya Guam ili kutengeneza mazingira mazuri ya kuitupia madongo timu yetu ya iliyokwenda kutuaibisha huko Aljeria.Kulikuwa na umuhimu gani wa kuingia gharama ya kuwapeleka watalii hao kama walikuwa hawajajiaanda kwa mashindano?Enewei,mie najua kwanini walipelekwa hivyohivyo:POSHO.Posho ya safari.Linapokuja suala la posho ya safari usishangae chama cha mchezo wa bao au drafti (kwa mfano) kumpeleka mchezaji kipofu.Wanajua kabisa kuwa kipofu hawezi kucheza drafti au bao lakini hilo haliwasumbui viongozi hao kwani tayari watakuwa wamejipatia visenti vya kupeleka kwenye nyumba ndogo zao (utafiti usio rasmi umeonyesha kuwa asilimia kubwa ya fedha inayopatikana kwa rushwa au ubadhirifu inaishia kwenye nyumba ndogo).Viongozi walichagua wanamichezo wazembe wanastahili lawama nyingi zaidi kuliko wazembe hao waliokwenda kututia aibu huko Aljeria (ukiachia huyo mmoja aliyeambulia medali ya fedha).Nawalaumu zaidi viongozi hao kwa vile hawana cha kujitetea kwa kuchagua wanamichezo wasio na uwezo wa kutuletea ushindi.Angalau timu ya taifa ya Guam inaweza kujitetea kwani kijinchi chenyewe kina watu wachache zaidi ya wilaya ya Kinondoni.Tanzania ina watu zaidi ya milioni 30,na miongoni mwao ni wanamichezo wenye vipaji ambavyo aidha vinapuuzwa,haviendelezwi au vinaminywa na viongozi walafi wa madaraka na fedha lakini hawana hata chembe ya mawazo endelevu ya ushindi kwenye michezo.Kwenye nchi za kidikteta viongozi kama hawa wanaporejea kutoka mashindanoni wanapokelewa na karandinga kuelekea Segerea.

Majuzi tumesikia EWURA ikidai kwamba waziri Meghji kadanganya kuhusu uwezo wa mamlaka hiyo kuwabana wafanyabiashara wa mafuta.Sijui nani anasema ukweli kwani sijaona sheria iliyoanzisha mamlaka hiyo ila ni dhahiri kuwa kuna kitu hakiko sawia.Kuna umuhimu gani wa kuwa na mamlaka isiyo na uwezo wa kisheria katika kutekeleza majukumu yake?Au kwa mfano sahihi,kuna umuhimu gani wa kufuga mbwa mwenye mapengo na ambaye akisikia kelele za “mwizi,mwizi” anakwenda kujificha?Inanikumbusha mchapo mmoja nilowahi kusimuliwa huko Tanga kuwa baba mwenye nyumba mmoja alipoamshwa na mkewe na wanawe kuwa wamesikia watu wanavunja dirisha akaanza kulia na kuwaacha watoto hawajui la kufanya.Tukiachana na mifano hiyo,swali la muhimu ni kuwa hivi huku kurushiana mpira kunamsaidia vipi mwananchi wa kawaida?Nilishapendekeza huko nyuma kwamba njia nyepesi ya kudhibiti bei ya mafuta ni “kuchimba mkwara wa nguvu” kwamba atakayezidisha bei stahili ya mafuta atafutiwa leseni.La muhimu hapa sio kwamba amri hiyo itolewe na Meghji au EWURA,bali itekelezwe.Hakuna mfanyabiashara aliye tayari kufutiwa leseni na kwa hakika watatekeleza amri hiyo.

Mwisho,tumeambiwa na Profesa Maghembe kuwa wizara yake ina baadhi ya watendaji ambao kwa jina jepesi tunaweza kuwaita mafisadi.Hao ni pamoja na wale wanaoshiriki kwenye biashara ilopigwa marufuku ya kusafirisha magogo nje.Waziri anastahili pongezi kwa kuweka bayana uozo huo.Lakini unategemea nini kwenye wizara ambayo Severe alipewa uhamisho na akagoma kuhama na hadi leo bado anapeta?Prof Maghembe anasema amepeleka majina ya wahusika kwenye “ngazi za juu” kwa vile yeye hana uwezo kisheria kuwawajibisha.Pengine tunachopaswa kufahamu ni kuwa lini majina hayo yamewasilishwa huko ngazi za juu,na kwanini mafisadi hao bado wanaendelea kuuza maliasili zetu.Sintoshangaa kusikia mmoja wao akiitisha press conference kama ile ya gavana wetu na “kutupa somo la uzalendo.”Kwa vile mafisadi hawa wanajulikana,kuendelea kuwaacha madarakani ni sawa na kuwapa nafasi ya kufuja kwa kasi zaidi (kwa vile wanaelewa kuwa maamuzi kutoka “ngazi za juu” yanaweza kuwahamisha kutoka kwenye ulaji) na kuharibu ushahidi dhidi ya tuhuma zinazowakabili.Sheria ichukue mkondo wake ili kuzuia virusi vya ufisadi kusambaa zaidi (wanaoona mafisadi hao wanazidi kupeta wanashawishika kuiga ufisadi wao).

Nimalizie kwa kumpongeza Waziri Mwapachu kwa kuhitimisha bethidei yake kwa kuwatembelea watumishi wa Wizara yake huko Dodoma.Ni mfano wa kuigwa.Pia hoja yake ya kuwa na “data bank” ya simu ni nzuri (japo ufanisi wake ni mgumu) na inaweza kuigwa kwenye maeneo mengine kwa mfano kuanzisha daftari la kudumu la wala rushwa.

Alamsiki


20 Jul 2007

Asalam aleykum,

Juzi nilipata barua-pepe kutoka kwa rafiki yangu mmoja aliyeko huko nyumbani.Huyu jamaa alikuwa akinilaumu “kirafiki” kwamba inaelekea nimeanza kuishiwa pointi za kuandika ndio maana takriban nusu ya makala yangu iliyopita ilikuwa ina habari “nyepesi nyepesi.”Sikukasirika kwani siku zote nathamini sana ushauri wenye lengo la kujenga au kuleta maendeleo.Nilimjibu kwamba nina pointi lukuki za kuandika,lakini kuna wakati inabidi “tupunguze kasi ya maisha” kwa kuangalia habari za vituko mbalimbali hususan vinavyojiri huku Ughaibuni.Pia nilimhakikishia kuwa “nyepesi nyepesi” hizo sio “fiksi” bali ni habari zinazohusu matukio ya kweli,ila tu yanachekesha kwa namna moja au nyingine.Kicheko ni afya.

“Nyepesi” za wiki hii ni pamoja na taarifa kwamba “wanene” 7 ndani ya baraza jipya la mawaziri la Gordon Brown (mrithi wa Tony Blair) wamekiri katika nyakati tofauti kuwa walishawahi kutumia “widi” (kwa wale ambao lugha ya mtaani ni mgogoro, “widi” ni bangi au marijuana).Siku kadhaa zilizopita,kiongozi wa chama cha wahafidhina (Conservative Party) David Cameron naye alijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kupatikana nyeti kuwa alikuwa akivuta bangi katika siku za ujana wake.Cameron amekataa kuendelea na mjadala wa suala hilo akisema kuwa kila binadamu anaweza kufanya makosa hususan akiwa kijana.Alitaka wanaomshupalia wamhukumu kwa utendaji wake wa kazi wa sasa na sio mambo aliyofanya nyma.Kali zaidi ya zote ni pale Katibu wa Ofisi ya Mambo ya Ndani (Home Office-yaani ni sawa na Wizara ya Mambo ya Ndani huko nyumbani),Jacqui Smith,na waziri mmoja katika ofisi hiyo (hapa katibu wa wizara ni mkubwa kicheo kuliko waziri),Tony McNulty,walipotangaza hadharani kuwa nao walishawahi kuvuta bangi huko nyuma.Na “ushuhuda” huo umekuja wakati mwanamama huyo (Smith) akitangaza mpango wa serikali kuangalia upya uamuzi wa awali wa serikali ya Blair wa kushusha daraja (declassifying) la bangi.Habari kwamba viongozi hao wawili (ambao pamoja na majukumu mengine wana dhamana ya kudhibiti mihadarati) waliowahi kuwa wavuta bangi zimezua mjadala kama kweli wanapaswa kuendelea na nyadhifa zao.Pengine kinachowasaidia ni ukweli kwamba kuna wanasiasa wengine (wakiwamo mawaziri vivuli wa upinzani) ambao nao wameweka bayana kuwa walishawahi kuvuta bangi walipokuwa vijana.Uwazi na ukweli au vituko vya siasa?


Kuna habari nyingine ya majonzi lakini kwa namna flani inaweza inachekesha.Mwanamke aliyekuwa na uzito mkubwa kuliko wote hapa Uingereza,Nazima Hussein,amefariki na kuwaacha wanandugu wakiwa na wakati mgumu baada ya kubambikwa ushuru wa pauni 4,000 (zaidi ya shilingi milioni 8) kutoka kwa manispaa huko Southall,London.Ushuru huo ulitokana na gharama za kuuhudumia mwili wa marehemu ambao ulihitaji watumishi wa kikosi cha zima moto (firemen) 13 kuutoa mwili huo (uliokuwa na unene wa futi 3) kutoka katika flati aliyokuwa akaishi.Na walipoufikisha mochwari huko Uxbridge ilizuka kasheshe nyingine kwani hakuna toroli la kubebea maiti lililomtosha marehemu na pia mafriji yote ya kuhifadhia maiti hayakuweza kumudu ukubwa wa mwili wa marehemu huyo.Marehemu Nazima alifariki akiwa na uzito wa kilo 349 .Habari njema ni kwamba baada ya watu wa Manispaa “kusomeshwa” walikubali kupunguza gharama hadi pauni 3,000 (zaidi ya shilingi milioni 6).Ukiskia msiba mzito ndio huo.

Turejee nyumbani.Siku chache taifa limepewa changamoto ya kutosha kutoka kwa JK kuhusu suala la “kupima ngoma” (ukimwi).Na kwa mujibu wa taarifa za magazeti mbalimbali ya huko nyumbani watu kadhaa wameitikia wito wa Rais kwa kwenda kwenye vituo vya afya kupima ukimwi.Kwa mtizamo wangu,hamasa aliyotoa JK inaweza kuwa na matokeo makubwa sana kwani kwa upande mmoja inaweza kuwasaidia wale waliokuwa hawajui kama wameathirika kuanza kuchukua tahadhari ambazo zitawasaidia kuishi maisha marefu zaidi.Pia kwa wale ambao vipimo vitaonyesha hawajaathirika wanaweza kuachana kabisa na matendo ya ngono zisizo salama,na hata kumrejea Mola wao.Kadhalika,kwa wale watakaokutwa wana virusi vya ukimwi na wakati huohuo wana familia zinazowategemea wanaweza kupata nafasi mwafaka ya kuandaa “future” za familia zao.Jingine ni kwamba kampeni hiyo inaweza kuwafumbua macho wale vichwa sugu na viwembe wanaopenda kujidanganya kuwa ukimwi ni ajali kazini,na eti ajali haina kinga.

Waziri wa Afya amelielezea Bunge kuwa kuna mpango wa kuwapima ukimwi wale wote wanaofika hospitali kwa matibabu.Wazo hilo ni zuri sana lakini linahitaji tahadhari ya namna flani.Wapo wanaosema kuwa ukimwi ni sawa na maradhi mengine yasiyo na tiba kama kansa au kisukari.Hapana,ukimwi ni tofauti sana hasa kwenye namna jamii yetu inavyowaangalia walioathirika na ukimwi (unyanyapaa).Nadhani wapo watakaokubaliana nami kwamba baadhi ya watumishi wa taasisi za afya wana tabia ya kukiuka maadili ya taaluma yao kwa kutoa siri kuhusu afya za wagonjwa.Naamini baadhi ya wasomaji wameshawahi kunong’onezwa na dokta au nesi flani kuwa “yule nanihii anao (ukimwi).” Sasa kama Wizara ya Afya itatekeleza dhamira yake ya kutaka watu wote wanaofika hospitali wapime ukimwi inapaswa pia kuboresha mambo kadhaa ikiwa pamoja na kuhakikisha kuna washauri nasaha wa kutosha watakaoweza kuwasaidia hao watakaobainika kuwa “wanao.” Naamini pia kuwa kuna sheria inayowabana watumishi wa afya kutoa “siri” ya ugonjwa wa mtu,na katika mpango huu wa Wizara ni muhimu sheria hiyo ikaimarishwa zaidi kwani bila kufanya hivyo si ajabu watu wanaweza kukwepa kwenda hospitali sio kwa kuhofia kupimwa na kukutwa wanao bali kwa kuwaogopa hao wauguzi wasioweza kuhifadhi siri za wagonjwa.Pia Wizara inapaswa kuweka bayana iwapo mpango huo wa kumpima kila mgonjwa utakuwa ni suala la hiari au la lazima.Kwa hapa,wagonjwa wanahamasishwa kupima ukimwi lakini hawalazimishwi.Pasipo kuweka misingi mizuri,nia nzuri ya Wizara ya Afya inaweza kuleta mkorogano usio wa lazima,maana si ajabu tukasikia flani kanyimwa nafasi ya kuonana na daktari kwa vile tu kukataa kupima ukimwi.Ifahamike kuwa suala la kupima au kutopima ni haki ya mtu binafsi.

Pia nimesoma habari iliyonisikitisha husu kilio cha Kamisheni ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kwamba imekuwa ikipata ushirikiano hafifu kutoka kwa waajiri katika suala la kuhakiki vyeti vya taaluma za waajiriwa.Unajua utandawazi umeleta mambo mengi sana ikiwa ni pamoja na fursa ya mtu kujipatia taaluma bila kutia mguu chuoni.Vipo vyuo kadhaa duniani vinavyotoa kozi kwa njia ya mtandao,lakini tatizo ambalo limekuwa likizisumbua hata nchi za Magharibi ni lile la baadhi ya vyuo vya kitapeli ambavyo vinaweza kukupatia cheti cha Udaktari wa Falsafa kwa wiki moja.Ukiona mfumuko wa madokta (sio wale wa hospitali) usikimbilie kufikira kuwa pengine siku hizi PhD zimekuwa rahisi.Ukweli ni kwamba PhD feki zimetapakaa sana kutokana na vyuo feki (japo vingine vimeandikishwa kisheria) ambavyo wanachojali wao ni fedha tu ya huyo anayehitaji PhD ya chapchap.Inatuuma sana sie wengine ambao tunazeekea maktaba kutafuta huo udokta “wa kwelikweli” huku wenzetu “wanasomea baa au kwenye nyumba ndogo zao” na wanaamka asubuhi na “hangover” wakiwa madaktari wa falsafa.Nadhani falsafa pekee waliyonayo “vilaza” hawa ni kuhusu waganga gani wa kienyeji wanasaidia mtu kula rushwa na aendelee kuonekana mwadilifu au namna ya kutogonganisha magari kati ya mama watoto na nyumba ndogo.

Ukweli mchungu ni kwamba TCU ina wakati mgumu kufanikiwa katika azma yake hiyo njema,kwani wengi wetu tunajua kuwa baadhi ya waajiri nao wana elimu za kutilia mashaka.Pia nadhani kuna mapungufu ya kisheria kuhusu matumizi ya vyeti feki,kwani nakumbuka jeshi la polisi halikuchukua hatua yoyote lilipobaini kuwa mbunge mmoja hakuwa mkweli kuhusu elimu yake ya sekondari.Sasa kama ufeki wa vyeti vya sekondari “sio big deal” kwa polisi je hao wenye PhD feki wataweza kuguswa?Enewei,tuna vita kadhaa tunazopenda zianze dakika hii:dhidi ya wala rushwa,majambazi,wabadhirifu,wauza unga,nk.Pengine siku moja itatangazwa vita ya kitaifa dhidi ya vyeti na taaluma feki.Yote yanawezekana.

Alamsiki


13 Jul 2007

Asalam aleykum,

Baada ya matukio ya hivi karibuni yaliyotuweka matumbo moto kufuatiwa mahayawani flani kuamua kuendesha kampeni yao ya kishetani ya kutaka kulipua mabomu huko London na hapo Glasgow (Waskotishi bado hawaamini kuwa ugaidi umeingia kwenye ardhi yao) sio wazo baya kuanza makala hii kwa habari “nyepesi nyepesi.” Gazeti la Daily Mail la hapa liliripoti hivi karibuni kuhusu matokeo ya utafiti yaliyoonyesha kuwa wanaume wenye aibu wana nafasi kubwa ya kupata magonjwa ya moyo kuliko wale wasio na aibu!Hizi tafiti nyingine…we acha tu.Kwa mujibu wa gazeti hilo,utafiti huo ulifanyika kwa kipindi cha miaka 30 uliwahusisha maelfu ya wanaume ambapo watafiti kutoka chuo kikuu cha Northwestern cha Chicago,Marekani walipokuwa wanafanya ufuatiliaji wa wawaliowahoji kwenye utafiti huo walibaini kuwa asilimia 60 kati yao (waliohojiwa) walikuwa wameshafariki,huku chanzo kikuu cha vifo kikiwa “heart attack” (nadhani kwa Kiswahili sahihi ni msongo wa moyo).Mambo hayo!

Na ukisikia duniani kuna mambo usidhani ni utani.Mzembe mmoja amekamatwa huko New Hampshire (Manchester) baada ya kushindikana kwa jaribio lake la kutaka kufanya uporaji benki huku akiwa amejivika matawi ya miti kama “camouflage” (kificho) yake.Jamaa huyo,James Coldwell,aliingia kwenye tawi la benki ya ushirika ya Citizens,huku akiwa amejivika majani na kuwatisha wahudumu wa benki hiyo kabla ya kufanikiwa kuondoka na kitita cha fedha,lakini alinaswa na polisi muda mfupi baadaye kwani triki yake ya “uninja wa majani” haikumsaidia kwa vile majani hayo hayakufunika sura yake,na wanausalama waliweza kuitambua vizuri kwenye CCTV.

Jumuiya ya Ulaya (EU) nayo ilijikuta kwenye wakati mgumu hivi karibuni baada ya kutoa filamu fupi kwa ajili ya promosheni ya kuhamasisha Jumuiya hiyo ambapo wahusika kwenye filamu hiyo ya sekunde 44 yenye jina “Let’s Come Together” walikuwa wakifanya “ngono nyepesi” (soft porn).Wapinzani wa wazo la Muungano wa nchi za Ulaya waliishambulia EU kwa kupoteza fedha za walipa kodi kwa kutengeneza filamu hiyo waliyoiona kuwa ni mwendelezo wa ubabaishaji wa Jumuiya hiyo.Nilipomtumia rafiki yangu flani habari hiyo kutoka gazetini alitania kwa kusema labda na sie tunahitaji “kampeni chafu” kama hiyo ya EU “kuuza” wazo la Muungano wa Afrika Mashariki ambao unaelekea kuwakera wadau wengi.

Nae mwanamama Amy Beth Ballamura amaepigwa marufuku kutia mguu kwenye pwani yoyote ya Uingereza baada ya kufanya majaribio zaidi ya 50 ya kujiua kwa kurusha baharini.Miongoni mwa sababu zilizopelekea kuchukuliwa kwa hatua ya kumdibiti mwanamama huyo ni pamoja na kuzitia huduma ya uokoji (emergency services) gharama ya zaidi ya pauni milioni 1 (zaidi ya shilingi bilioni mbili za huko nyumbani) kila wanapoitwa kwenda kumuokoa.Lakini pamoja na “tamaa” yake ya kujitoa roho,askari mmoja aliambulia tuzo ya ushujaa mwaka 2003 baada ya kusikia kelele za kuomba msaada kutoka baharini na kuamua kujitosa majini kufuata kelele hizo,ambapo alifanikiwa kumuokoa mwanamama huyo mwenye umri wa miaka 44.Cha kushangaza ni kwamba kama kweli alikuwa na nia ya kujitoa uhai sasa hizo kelele za kuomba msaada zilikuwa za nini?

Enewei,baada ya "nyepesi nyepesi" hizo (zote ni habari za kweli na wala sio kuwa “nawapiga fiksi” wasomaji wangu wapendwa) sasa tuangalie mambo ya muhimu zaidi huko nyumbani.Kwanza niseme siafikiani na hoja za Waziri wa Sheria Mama Nagu kwamba Bunge halipaswi kufanya kazi ya kupitia mikataba kabla ya kutiwa saini ili libaki na uhalali wake wa kuiwajibisha Serikali kwa mujibu wa dhamana ya mgawanyo wa mamlaka, kuchunguzana na kuwajibishana.Siafikiani naye kwa sababu hoja za baadhi ya wabunge kuwa mikataba hiyo ifikishwe kwao kabla ya kusainiwa zilizingatia ukweli kwamba kuna mapungufu makubwa yanayoendelea katika suala zima la kusaini mikataba mbalimbali.Mantiki nyepesi (simple logic) inaweza kutueleza kwamba maslahi ya nchi ni muhimu zaidi ya huo mgawanyiko wa madaraka.Hivi kwa mfano wazo la mikataba kuletwa bungeni lingekubaliwa,halafu nchi inufaike kwa kuingia mikataba yenye maslahi kwa Taifa,tatizo linakuwa wapi?Hivi kipi bora,kulinda mgawanyiko wa madaraka huku mikataba ya ajabu ajabu ikiendelea kuwepo au “kupindisha sheria” kwa kuileta mikataba hiyo bungeni kabla haijasainiwa halafu nchi ikanufaika nayo?

Pia nimesoma kwenye gazeti moja la huko nyumbani kwamba lile tishio la wafugaji huko wilayani Kilombero limerejea tena.Nitamke bayana kuwa hili linanihusu binafsi kwa vile mie ni “mwana wa pakaya” naetokea mitaa ya huko.Hawa wafugaji ni wakorofi,watovu wa nidhamu na wavunja sheria wakubwa.Maagizo kadhaa yameshatolewa kuwataka waheshimu sheria za nchi lakini wameamua kuweka pamba masikio.Mamlaka husika zinapaswa kuliangalia suala hili kwa makini zaidi kwani wanachofanya wafugaji hao sio tu kinahatarisha amani (mifugo yao inakula mazao ya wakulima,na hilo pekee linatosha kuzusha ugomvi) lakini pia hawawatakii mema wakulima kwani kwa kuswaga mifugo yao kwenye mashamba wanamaanisha kuwa wanataka wakulima hao wakose chakula na hela wanazojipatia kwa kuuza akiba ya mavuno yao.Hili ni bomu la wakati (time bomb) kwani japo hakuna bondia wa Kindamba (kama yupo basi samahani kwani sijamsikia) lakini hiyo haimaanishi kuwa mtu atakaeswaga mifugo yake kwenye mashamba ataachwa afanye anavyotaka.Hapo itakuwa kuchukua sheria mkononi,na japo mie ni mpinzani mkubwa wa kuchukua sheria mkononi,natambua dhahiri kuwa mtu “anapoletewa za kuleta” anaweza kabisa kuiweka sheria kando,hususan pale haki yake inapopuuzwa kwa makusudi.Kwa vile mkoa wa Morogoro umebahatika kuwa na RC ambaye ni “mjeshi” mstaafu basi hapana shaka Brigedia Jenerali Kalembo huyo atatumia “mbinu za medani” kuwadhibiti wafugaji hao wenye uhaba wa nidhamu.

Kikao cha Bunge kinaelekea ukingoni na miongoni mwa hoja nilizovutiwa nazo ni ile ya Mheshimiwa Shabiby (wa Gairo) kuhusu ujanja unaofanywa na baadhi ya wamiliki wa mabasi makubwa ya abiria.Alieleza kuwa mengi ya mabasi yanayotumika sasa yamefanyiwa “usanii” kwa kuweka mabodi mapya kwenye “chasis” na injini za malori au za kale.Kuna jina moja tu linalowafaa “wasanii” hawa nalo ni “WAUAJI.” Wanathamini sana kukwepa gharama za kununua mabasi mapya lakini hawajali hata chembe madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na vitendo vyao vya “kuunda mabasi feki.” Kwa upande mwingine tuseme bila kuonekana aibu kwamba mabasi ya namna hiyo yanafahamika hata bila kuwa na ujuzi wa umakanika kwani ulifika pale stendi ya mabasi Ubungo unaweza kukutana na basi ambalo linaonekana dhahiri kuwa bodi yake “imepachikwa” sehemu isiyostahili.Trafiki yeyote aliyehitimu mafunzo yake vyema na mwenye uchungu na maisha ya Watanzania wenzie hawezi kuliruhusu basi “lililovimba mbavuni utadhani lina ujauzito” liendelee na safari,na mabasi ya namna hiyo yako mengi tu.Wanaofanya hivyo wanajua bayana kuwa wanavunja sheria na kuhatarisha maisha ya abiria wao lakini hawajali kwa vile hakuna aliyechukuliwa sheria hadi leo.Si ajabu tukisikia kuwa baadhi ya mabasi hayo yanatumia injini za matrekta au hata za mashine za kusaga….(nashindwa kumalizia,nimekabwa na kicheko japo jambo hili sio la kuchekesha hata chembe.)

Mwisho,wakati Gavana wetu keshatamka bayana kuwa hatojiuzulu (utadhani alijichagua mwenyewe kwenye posti hiyo),sie wapenzi wa Simba tunajipoza kwa kusherehekea ubingwa wetu ambao kidogo umetibuliwa na hizi habari za viongozi kugombea mapato ya mechi huko Morogoro.Wito kwa watani wetu wa jadi Yanga ni huu:Micho akirudi (kama kweli atarudi) ashauriwe kukutana na Twalib Hilal apewe darasa kuwa ukocha sio sawa na ukatibu mwenezi wa klabu: ukocha ni vitendo vingi maneno machache lakini Mserbia Micho kila siku “anachonga” kuhusu hili au lile lakini matunda ya kazi yake kwenye dimba ni haba.Enewei,asilaumiwe sana kwani alishawahi kusema kuwa wachezaji wake hawafundishiki,na katika mechi ya juzi anaweza kuongeza sababu kuwa “lile tumbo la kuendesha” limechangia kukosa ushindi.

Alamsiki






KULIKONI UGHAIBUNI-71


Asalam aleykum,

Baada ya matukio ya hivi karibuni yaliyotuweka matumbo moto kufuatiwa mahayawani flani kuamua kuendesha kampeni yao ya kishetani ya kutaka kulipua mabomu huko London na hapo Glasgow (Waskotishi bado hawaamini kuwa ugaidi umeingia kwenye ardhi yao) sio wazo baya kuanza makala hii kwa habari “nyepesi nyepesi.” Gazeti la Daily Mail la hapa liliripoti hivi karibuni kuhusu matokeo ya utafiti yaliyoonyesha kuwa wanaume wenye aibu wana nafasi kubwa ya kupata magonjwa ya moyo kuliko wale wasio na aibu!Hizi tafiti nyingine…we acha tu.Kwa mujibu wa gazeti hilo,utafiti huo ulifanyika kwa kipindi cha miaka 30 uliwahusisha maelfu ya wanaume ambapo watafiti kutoka chuo kikuu cha Northwestern cha Chicago,Marekani walipokuwa wanafanya ufuatiliaji wa wawaliowahoji kwenye utafiti huo walibaini kuwa asilimia 60 kati yao (waliohojiwa) walikuwa wameshafariki,huku chanzo kikuu cha vifo kikiwa “heart attack” (nadhani kwa Kiswahili sahihi ni msongo wa moyo).Mambo hayo!

Na ukisikia duniani kuna mambo usidhani ni utani.Mzembe mmoja amekamatwa huko New Hampshire (Manchester) baada ya kushindikana kwa jaribio lake la kutaka kufanya uporaji benki huku akiwa amejivika matawi ya miti kama “camouflage” (kificho) yake.Jamaa huyo,James Coldwell,aliingia kwenye tawi la benki ya ushirika ya Citizens,huku akiwa amejivika majani na kuwatisha wahudumu wa benki hiyo kabla ya kufanikiwa kuondoka na kitita cha fedha,lakini alinaswa na polisi muda mfupi baadaye kwani triki yake ya “uninja wa majani” haikumsaidia kwa vile majani hayo hayakufunika sura yake,na wanausalama waliweza kuitambua vizuri kwenye CCTV.

Jumuiya ya Ulaya (EU) nayo ilijikuta kwenye wakati mgumu hivi karibuni baada ya kutoa filamu fupi kwa ajili ya promosheni ya kuhamasisha Jumuiya hiyo ambapo wahusika kwenye filamu hiyo ya sekunde 44 yenye jina “Let’s Come Together” walikuwa wakifanya “ngono nyepesi” (soft porn).Wapinzani wa wazo la Muungano wa nchi za Ulaya waliishambulia EU kwa kupoteza fedha za walipa kodi kwa kutengeneza filamu hiyo waliyoiona kuwa ni mwendelezo wa ubabaishaji wa Jumuiya hiyo.Nilipomtumia rafiki yangu flani habari hiyo kutoka gazetini alitania kwa kusema labda na sie tunahitaji “kampeni chafu” kama hiyo ya EU “kuuza” wazo la Muungano wa Afrika Mashariki ambao unaelekea kuwakera wadau wengi.

Nae mwanamama Amy Beth Ballamura amaepigwa marufuku kutia mguu kwenye pwani yoyote ya Uingereza baada ya kufanya majaribio zaidi ya 50 ya kujiua kwa kurusha baharini.Miongoni mwa sababu zilizopelekea kuchukuliwa kwa hatua ya kumdibiti mwanamama huyo ni pamoja na kuzitia huduma ya uokoji (emergency services) gharama ya zaidi ya pauni milioni 1 (zaidi ya shilingi bilioni mbili za huko nyumbani) kila wanapoitwa kwenda kumuokoa.Lakini pamoja na “tamaa” yake ya kujitoa roho,askari mmoja aliambulia tuzo ya ushujaa mwaka 2003 baada ya kusikia kelele za kuomba msaada kutoka baharini na kuamua kujitosa majini kufuata kelele hizo,ambapo alifanikiwa kumuokoa mwanamama huyo mwenye umri wa miaka 44.Cha kushangaza ni kwamba kama kweli alikuwa na nia ya kujitoa uhai sasa hizo kelele za kuomba msaada zilikuwa za nini?

Enewei,baada ya "nyepesi nyepesi" hizo (zote ni habari za kweli na wala sio kuwa “nawapiga fiksi” wasomaji wangu wapendwa) sasa tuangalie mambo ya muhimu zaidi huko nyumbani.Kwanza niseme siafikiani na hoja za Waziri wa Sheria Mama Nagu kwamba Bunge halipaswi kufanya kazi ya kupitia mikataba kabla ya kutiwa saini ili libaki na uhalali wake wa kuiwajibisha Serikali kwa mujibu wa dhamana ya mgawanyo wa mamlaka, kuchunguzana na kuwajibishana.Siafikiani naye kwa sababu hoja za baadhi ya wabunge kuwa mikataba hiyo ifikishwe kwao kabla ya kusainiwa zilizingatia ukweli kwamba kuna mapungufu makubwa yanayoendelea katika suala zima la kusaini mikataba mbalimbali.Mantiki nyepesi (simple logic) inaweza kutueleza kwamba maslahi ya nchi ni muhimu zaidi ya huo mgawanyiko wa madaraka.Hivi kwa mfano wazo la mikataba kuletwa bungeni lingekubaliwa,halafu nchi inufaike kwa kuingia mikataba yenye maslahi kwa Taifa,tatizo linakuwa wapi?Hivi kipi bora,kulinda mgawanyiko wa madaraka huku mikataba ya ajabu ajabu ikiendelea kuwepo au “kupindisha sheria” kwa kuileta mikataba hiyo bungeni kabla haijasainiwa halafu nchi ikanufaika nayo?

Pia nimesoma kwenye gazeti moja la huko nyumbani kwamba lile tishio la wafugaji huko wilayani Kilombero limerejea tena.Nitamke bayana kuwa hili linanihusu binafsi kwa vile mie ni “mwana wa pakaya” naetokea mitaa ya huko.Hawa wafugaji ni wakorofi,watovu wa nidhamu na wavunja sheria wakubwa.Maagizo kadhaa yameshatolewa kuwataka waheshimu sheria za nchi lakini wameamua kuweka pamba masikio.Mamlaka husika zinapaswa kuliangalia suala hili kwa makini zaidi kwani wanachofanya wafugaji hao sio tu kinahatarisha amani (mifugo yao inakula mazao ya wakulima,na hilo pekee linatosha kuzusha ugomvi) lakini pia hawawatakii mema wakulima kwani kwa kuswaga mifugo yao kwenye mashamba wanamaanisha kuwa wanataka wakulima hao wakose chakula na hela wanazojipatia kwa kuuza akiba ya mavuno yao.Hili ni bomu la wakati (time bomb) kwani japo hakuna bondia wa Kindamba (kama yupo basi samahani kwani sijamsikia) lakini hiyo haimaanishi kuwa mtu atakaeswaga mifugo yake kwenye mashamba ataachwa afanye anavyotaka.Hapo itakuwa kuchukua sheria mkononi,na japo mie ni mpinzani mkubwa wa kuchukua sheria mkononi,natambua dhahiri kuwa mtu “anapoletewa za kuleta” anaweza kabisa kuiweka sheria kando,hususan pale haki yake inapopuuzwa kwa makusudi.Kwa vile mkoa wa Morogoro umebahatika kuwa na RC ambaye ni “mjeshi” mstaafu basi hapana shaka Brigedia Jenerali Kalembo huyo atatumia “mbinu za medani” kuwadhibiti wafugaji hao wenye uhaba wa nidhamu.

Kikao cha Bunge kinaelekea ukingoni na miongoni mwa hoja nilizovutiwa nazo ni ile ya Mheshimiwa Shabiby (wa Gairo) kuhusu ujanja unaofanywa na baadhi ya wamiliki wa mabasi makubwa ya abiria.Alieleza kuwa mengi ya mabasi yanayotumika sasa yamefanyiwa “usanii” kwa kuweka mabodi mapya kwenye “chasis” na injini za malori au za kale.Kuna jina moja tu linalowafaa “wasanii” hawa nalo ni “WAUAJI.” Wanathamini sana kukwepa gharama za kununua mabasi mapya lakini hawajali hata chembe madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na vitendo vyao vya “kuunda mabasi feki.” Kwa upande mwingine tuseme bila kuonekana aibu kwamba mabasi ya namna hiyo yanafahamika hata bila kuwa na ujuzi wa umakanika kwani ulifika pale stendi ya mabasi Ubungo unaweza kukutana na basi ambalo linaonekana dhahiri kuwa bodi yake “imepachikwa” sehemu isiyostahili.Trafiki yeyote aliyehitimu mafunzo yake vyema na mwenye uchungu na maisha ya Watanzania wenzie hawezi kuliruhusu basi “lililovimba mbavuni utadhani lina ujauzito” liendelee na safari,na mabasi ya namna hiyo yako mengi tu.Wanaofanya hivyo wanajua bayana kuwa wanavunja sheria na kuhatarisha maisha ya abiria wao lakini hawajali kwa vile hakuna aliyechukuliwa sheria hadi leo.Si ajabu tukisikia kuwa baadhi ya mabasi hayo yanatumia injini za matrekta au hata za mashine za kusaga….(nashindwa kumalizia,nimekabwa na kicheko japo jambo hili sio la kuchekesha hata chembe.)

Mwisho,wakati Gavana wetu keshatamka bayana kuwa hatojiuzulu (utadhani alijichagua mwenyewe kwenye posti hiyo),sie wapenzi wa Simba tunajipoza kwa kusherehekea ubingwa wetu ambao kidogo umetibuliwa na hizi habari za viongozi kugombea mapato ya mechi huko Morogoro.Wito kwa watani wetu wa jadi Yanga ni huu:Micho akirudi (kama kweli atarudi) ashauriwe kukutana na Twalib Hilal apewe darasa kuwa ukocha sio sawa na ukatibu mwenezi wa klabu: ukocha ni vitendo vingi maneno machache lakini Mserbia Micho kila siku “anachonga” kuhusu hili au lile lakini matunda ya kazi yake kwenye dimba ni haba.Enewei,asilaumiwe sana kwani alishawahi kusema kuwa wachezaji wake hawafundishiki,na katika mechi ya juzi anaweza kuongeza sababu kuwa “lile tumbo la kuendesha” limechangia kukosa ushindi.

Alamsiki

6 Jul 2007

Asalam aleykum,

Hivi karibuni niliona habari flani kwenye kituo cha runinga cha Aljazeera English ambayo kwa hakika iliniacha na uchungu mkubwa.Habari hiyo iliyokuwa kwenye kipindi kiitwacho “Witness” cha mtangazaji mahiri Rageh Omar,ilihusu unyama uliofanywa na majeshi ya Marekani huko Vietnam wakati wa vita kati ya nchi hizo mbili.Katika kipindi hicho zilionyeshwa picha za watoto wanaozaliwa wakiwa na maumbile ya kutisha na watu wazima wenye magonjwa yasiyoelezeka kirahisi.Yote hayo ni matokeo ya kemikali iliyonyunyizwa kutoka angani na ndege za jeshi la Marekani kwa lengo la kuwadhibiti wapiganaji wa Kivietnman (vietkong).Kemikali hiyo iitwayo “Agent Orange” iliponyunyizwa iliachia kemikali nyingine ya sumu iitwayo “dioxin” ambayo madhara yake yanaendelea nchini Vietnam hadi leo hii.Kuna watoto wanaozaliwa wakiwa na vichwa vikubwa kuliko miili yao huku wengine wakiwa wamezaliwa bila viungo muhimu kama mikono au miguu.

Marekani iliamua kutumia “Agent Orange” kama njia ya kuwafichua wapiganaji wa msituni wa Vietnam ambao kwa hakika walikuwa mahiri sana katika kushambulia kwa kushtukiza huku wakijificha kwa kuyatumia vizuri mazingira yanayowazunguka.Lengo la kitendo hicho kisicho cha kibinadamu lilikuwa kuteketeza uoto wa asili ili wapiganaji wa Vietnam wasiwe na mahali pa kujificha.Licha ya madhara ya kiafya kwa binadamu,matumizi ya “Agent Orange” yameacha athari kubwa za kimazingira kwani baadhi ya maeneo ambayo awali yalikuwa misitu sasa yamebaki yakiwa “tasa” mithili ya jangwa.Kikemikali, “Agent Orange” ni mchanganyiko wa tindikali mbili za kuua mimea (2,4-D na 2,4,5-T) ambazo zina tabia ya kuiga mfumo wa ukuaji wa kiumbe,lakini zinaiga mfumo huo sio kwa lengo la kuusaidia ukue bali kuuharibu.Enewei,hayo ni mambo ya kimaabara na pengine hapa sio mahala pake.

Katika makala yangu moja ya hivi karibuni niliandika kuhusu jinsi baadhi ya waandaa sera wa Marekani wanavyopenda kutoa maamuzi yatakayoleta matokeo ya haraka pasipo kuangalia madhara ya muda mrefu.Nilitolea mfano taarifa kwamba jeshi la Marekani huko Iraki lilikuwa na mpango wa kuwapatia msaada wapiganaji wa madhehebu ya Sunni ili wakabiliane na wapiganaji wa kikindi cha Al-Qaeda nchini humo.Katika makala hiyo nilitoa mifano kadhaa ya namna maamuzi ya kukurupuka ya Marekani yalivyochangia kuzaliwa na kuimarika kwa kikundi cha Al-Qaeda.Ni vichaa flani waliodhani kwamba kumwaga sumu huko Vietnam kungeleta ushindi wa chapchap,vichaa walioamini katika matokeo pasipo kujali athari za muda mrefu za matokeo hayo.Pia Marekani inaonekana kuwa mahiri sana katika kutafuta ushindi wa vita lakini iko dhaifu katika kuleta amani.Kwa lugha ya kwa mama wanasema “to win the war but lose the peace.”Ni hivi,watapiga mabomu na kuteketeza vijiji huko Iraki hadi wachoke wenyewe.Wakiamini kuwa wameshinda mapambano,vinachipuka vizazi vyenye chuki ambavyo vimepoteza wazazi na jamaa zao.Vizazi hivyo vya chuki vinabaki kuwa hifadhi ya jeshi la wapiganaji wa vita vijavyo (reserve army of future fighters).Ni dhahiri kuwa mzazi yeyote wa Kivietnam ambaye atajifungua mtoto mwenye mtindio wa maumbile uliosababishwa na athari za muda mrefu za “Agent Orange” atakuwa na chuki ya milele dhidi ya Wamarekani.


Nigeukie huko nyumbani.Hivi ni lini kutakuwa na uungwana kwa baadhi ya Watanzania wenzetu ambao kwa namna moja au nyingine wanatajwa kuhusiaka na skandali flani?Hapa namzungumzia Gavana wetu wa BOT.Sijamsikia hata siku moja akikanusha tuhuma dhidi yake japo naamini anafahamu kuwa zinamchafulia jina lake,uaminifu wake na wa taasisi anayoongoza.Dawa ya kukabiliana na tuhuma sio kuzipuuza,au kwa mtindo uliozoeleka huko nyumbani,kuzua tuhuma dhidi ya aliyekutuhumu.Dawa ni kujibu tuhuma hizo aidha kwa kuzungumzia na vyombo vya habari au kwenda mahakamani kudai mtoa tuhuma athibitishe anachozungumza.Mfano mzuri hapa ni namna aliyekuwa Waziri Mkuu katika awamu iliyopita alivyoamua kushughulikia tuhuma dhidi yake.Akirejea kutoka masomoni Havard,Fred Sumaye alieleza kuwa anawashangaa wanasheria wake kwa kuchelewa kufuatilia hatua za kisheria anazotaka kuzichukua dhidi ya wanaomtuhumu.Japo sijui kama kesi hiyo ishafunguliwa au la,na kama imeshafunguliwa walalamikiwa ni akina nani,lakini la muhimu hapa ni kwamba Sumaye ameamua kujibu tuhuma zake kwa njia za kisheria.Na hivyo ndivyo inavyopaswa kufanyika kwani kukaa kimya kunaweza kumaanisha kuwa mtuhumiwa anakubaliana na tuhuma hizo.

Nikuchekeshe(au nikuudhi) kidogo na moja ya mifano yangu ya ajabuajabu.Ni hivi,kwenye mbinu za medani za mtaani kuna imani miongoni mwa vijana wa kiume kuwa wakitongoza binti halafu akawa kimya bila kusema amekubali au hataki basi wajuzi wa fani hiyo wanasema kuwa hiyo ni dalili ya kukubaliwa.Yaani,kimya ni sawa na “yes” lakini mlengwa anaona aibu kutamka hivyo.Ok,ni mfano wa kizembe lakini unaweza kuwa na mantiki katika nachozungumzia hapa.Iweje kwamba mtu aliyepewa dhamana ya kushikilia uchumi wetu atuhumiwe kuwa anahusiaka na ulaji wa mabilioni ya dola katika mpango wa msamaha wa madeni na ujenzi wa Twin Towers,lakini akae kimya kana kwamba yanayosemwa hayamhusu yeye.Inawezekana ni dharau dhidi ya hao wanamtuhumu lakini kama filosofia yetu ya kutongoza (kwamba kukaa kimya maana yake ni kukubaliwa) ina mantiki ya kutosha,basi kimya cha Gavana kinaweza kutupa majibu ya maswali mengi tuliyonayo kuhusu skandali hizo.

Baada ya kutaja Twin Towers ndio nikakumbuka swali moja.Tunaambiwa kuwa Benki Kuu ni taasisi inayopaswa kuwa na heshima na hadhi kubwa.Na nadhani katika kuonyesha hadhi hiyo,likaja wazo la kuwa na Twin Towers.Hivi kungekuwa na dhambi gani kama BOT ingeendelea kuwa kama ilivyokuwa kabla ya ujenzi wa Twin Towers halafu hayo mamilioni ya dola yangepelekwa kujenga daraja la kisasa pale Kigamboni?Licha ya kuepusha balaa linaloweza kutokea siku yoyote ile kutokana na kutegemea feri zilizochoka,daraja hilo lingeweza kuwa alama ya jiji na kivutio cha utalii kama zilivyo alama za majiji mengine duniani kama “Jicho la London” (London Eye),jengo la opera la Sydney (Sydney Opera House,Australia),Taj Mahal huko India,mnara wa Eiffel hapo Paris,au Mnara wa Uhuru (Statue of Liberty) huko New York.Wakati hawa wenzetu wana uwezo wa kujenga vivutio kwa ajili ya “kujifurahisha” tu,sie masikini hatuna uwezo huo na hatupaswi kuwa na mawazo ya kitajiri wakati tungali masikini.Kwa mantiki hiyo,sio busara sana kuwa na jengo “bomba” kama Twin Towers za BOT kwa ajili ya kufurahisha macho ya wachache wenye muda wa kuyaangalia maghorofa hayo (ukiwa na njaa,huna nauli,utamudu kutoka Kimbiji kuja “kushangaa” Twin Towers?) ilhali tungeweza kutumia kidogo tulicho nacho kutengeneza utambulisho wa jiji letu (zaidi ya kile kisanamu cha Bismin) na kuwarejeshea imani wakazi wa Kigamboni kuwa ahadi za wanasiasa huwa zinatekelezeka (daraja hilo limeshaahidiwa mara nyingi zaidi ya ahadi za wagombea uongozi wa klabu ya Yanga walivyoahidi kugeuza Uwanja wa Kaunda kuwa wa kisasa au wale wa Simba wanaoahidi kujenga “wanja” kubwa zaidi ya ule wa watani wao wa jadi).

Mwisho,napenda kuuliza tena:hivi msimamo wa Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana ni upi kuhusu sakata linaloendelea huko Dodoma ambako baadhi ya waumini hawaafikiani na Askofu wa Dayosisi ya Kati katika msimamo wake wa kuunga mkono ushoga.Hivi anadhani mambo yatatulia kwa yeye kukaa kimya?Hivi ni nani aliyetuambia kuwa ukimya ni njia mwafaka ya kupata majibu ya maswali magumu yanayoikabili jamii yetu?Nilishtuka nilipoona picha ya askari wakitoa ulinzi ili Askofu Mhogolo aweze kuendeshwa ibada ya kipaimara.Japo mie si mjuzi hata kidogo kwenye kusoma Biblia lakini sijawahi kusikia kuwa Yesu alihitaji askari kuendeshwa shughuli zake za kuleta ukombozi kwa kondoo wake.Nguvu za dola zikitumika kudhibiti kondoo wa Bwana basi ni dhahiri kuwa “siku za kurejea Bwana zimekaribia.”Na bora arejee mapema kwani inaelekea baadhi ya alowakabidhi majukumu ya kumtumikia wameweka mbele maslahi yao kuliko ya kondoo wanaopaswa kuwachunga.Ole wenu,msije siku ya kiama mkageuzwa kuwa kuni za kuchochea moto wa milele dhidi ya wala rushwa,wazinzi,matapeli,watoa ahadi za uongo na maharamia wengine.


Alamsiki

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.