23 Aug 2010


Riyadh,Saudia,April 16

Wafanyabiashara wa Saudi Arabia wameiomba Tanzania kama wanaweza kukodi hekta nusu milioni (500,000) za ardhi inayofaa kwa kilimo hususan cha mpunga na ngano kama sehemu ya mpango wa kujitosheleza kwa chakula kwa falme hiyo ya jangwani.

Maofisa waandamizi wa chemba ya biashara ya jiji la Riyadh walitoa ombi hilo wakati wa ziara ya Rais Jakaya Kikwete katika falme hiyo.

"Tanzania ipo tayari kufanya biashara nanyi.Kuna heka milioni 100 (hekta milioni 40.5)za ardhi nzuri yenye rutuba",Kikwete aliwaambia wafanyabiashara hao.

Samir Ali Kabbani,mkuu wa kamati ya kilimo ya chemba hiyo alisema kwamba wamepata majibu mazuri sana."Kikwete ametuambia kwamba Tanzania inaweza kutukodisha ploti ambazo kila moja ina ukubwa wa hadi hekta 10,000 kwa kipindi cha miaka 99",Kabbani alilieleza Shirika la Habari la Reuters baada ya mkutano huo na Kikwete.

Maofisa na wafanyabiashara wa Kisaudi walitrajiwa kuitembelea Tanzania wiki chache baada ya mkutano huo.

"Wanaweza kukodi ardhi kutoka serikalini",January Makamba,msaidizi wa Rais Kikwete,aliieleza Reuters."Lakini inabidi tuhakikishe kuwa hatuishii kwenye hali kama ile ya Nigeria:hifadhi kubwa ya mafuta lakini foleni kubwa kwenye vituo vya kuuzia mafuta",alisema Makamba.

Maafisa wa Saudia wanaiona Tanzania kama sehemu mwafaka kutokana na mazingira ya kijiografia,kisiasa na wingi wa maji na ardhi ya kilimo.Makampuni kadhaa ya nchi hiyo tayari yameanza kuwekeza katika miradi ya kilimo huko Indonesia na Ethiopia.

Agosti mwaka jana Indonesia ilisema kuwa mjumuiko wa makampuni ya Bin Ladin ya Saudi Arabia unatarajia kuwekeza dola bilioni 4.3 katika hekta 500,000 za kilimo cha mpunga.Mahitaji ya ngano kwa Saudia kwa mwaka yanakadiriwa kufikia tani milioni 2.5,na mwaka juzi nchi hiyo iliagiza kutoka nje karibu tani milioni 1 za mchele,kwa mujibu wa Idara ya Kilimo ya Marekani.

CHANZO: Reuters


22 Aug 2010

What A good NewS???
Well,your top-above-the-rest blog,ANGALIA BONGO,has officially  moved to a new world.
Thanxx
Admin(Angaliabongo)

Blogu hii ya KULIKONI UGHAIBUNI inafungua ukurasa mpya na kuweka historia ya kipekee katika fani ya habari nchini Tanzania kwa kutangaza hadharani kuwa inam-endorse mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chadema,Dokta Wilbroad Slaa.

Kuna sababu lukuki za kufanya hivyo lakini hapa nitaziorodhesha chache.Kwanza,blogu hii inataka kuachana na unafiki unaojidhihirisha katika baadhi ya vyombo vya habari vyetu ambapo wahusika wanadai hawafungamani na upande wowote lakini matendo yao yanawasuta kwa kupendelea chama tawala huku wakivibinya kwa nguvu baadhi ya vyama vya upinzani.Hapa simsimangi mtu bali nadhani ni vema kuweka msimamo wazi ili kama chombo cha habari ni wakala wa CCM na JK basi ni vema wasomaji wakafahamishwa bayana.

Pili,blogu hii inaamini kuwa kila Mtanzania mwenye uchungu wa dhati kwa nchi yetu anapaswa kumsapoti Dkt Slaa.Katika utumishi wake kwa umma,mgombea huyo wa Chadema ametuthibitishia kuwa ni mtetezi halisi wa haki za wanyonge na ustawi wa taifa letu.Ni nani asiyefahamu namna Dkt Slaa alivyohatarisha maisha yake kwa “kuwavua nguo mafisadi hadharani” alipotangaza ile “list of shame”?Walitishia kumpeleka mahakamani lakini hakuna mmoja wao aliyediriki kufanya hivyo,na sanasana baadhi yao wakaishia kuburuzwa mahakamani na serikali katika “kujikosha”.Blogu hii inaamini kuwa Dokta Slaa ni mkombozi na suluhisho mwafaka la matatizo lukuki yanayotukabili.

Tatu,binafsi naamini kuwa mgombea wa CCM,Jakaya Mrisho Kikwete,ameshindwa kabisa kutimiza matarajio ya Watanzania licha ya ahadi lukuki alizozitoa wakati wa kampeni zake mwaka 2005 na anazoendelea kuzitoa hadi leo.Ungetegemea kuwa mwezi huu wa toba Kikwete angemwogopa Mola wake na kutubu kwa Watanzania kwamba kuna maeneo mengi tu ambapo yeye na chama chake wamewaangusha Watanzania.Lakini kama ilivyo jeuri ya wanasiasa wengi wa Kiafrika,JK ameendeleza wimbo wa “mafanikio ya Awamu ya Nne”.Yani hata kushamiri kwa ufisadi na “uchakachuaji” wa kura za maoni ndani ya CCM ni mafanikio!

Sababu ya nne inashabihiana na hiyo ya tatu.Naamini kuwa afya ya mgombea wa CCM,Jakaya Kikwete,inapaswa kuwekwa kwenye darubini na wapiga kura wanapofanya maamuzi ya kumchagua rais wa awamu ya tano.JK ameshaanguka hadharani mara tatu na kila mara tunapewa excuse moja baada ya nyingine.Mwaka 2005 tuliambiwa “swaumu na uchovu wa kampeni”.Alipoanguka Mwanza tuliambiwa uchovu wa safari (kana kwamba safari hizo ni zile za Wamachinga wanaotembea juani kwa mguu!).Na jana kaanguka tena jukwaani halafu tunaambiwa sababu ni swaumu.Kwani Makamba hajafunga?Au Rais Karume naye “kobe”?Kuna tatizo zaidi ya swaumu au uchovu lakini kwa vile viongozi wetu wamezowea sifa na sio kasoro basi kuweka hadharani kinachomsibu kiongozi huyo inaonekana ni sawa na uhaini.Blogu hii imaanimi kuwa ili Tanzania ijikwamue katika lindi la umasikini wa kutupwa,sambamba na kukabiliana na janga la ufisadi,tunahitaji kiongozi mwenye afya timilifu,kimwili na kiakili.Hatujui JK ameshaanguka matra ngapi asipokuwa hadharani lakini haihitaji hata cheti cha short course ya utabibu kumaizi kuwa JK ana matatizo ya kiafya yanayofichwa,aidha kutokana na uoga wa wanaopaswa kuujulisha umma kuhusu hilo au maagizo yake mwenyewe kuwa “yuko fiti”.All in all,uzito wa matatizo yanayoikabili Tanzania unahitaji mtu aliye fiti kweli,na sio kwa anavyodhani yeye au anavyotaka umma uamini hivyo ilhali ni kinyume na hali halisi.

Kama nilivyoandika mwanzoni,kuna sababu nyingi zilizopelekea blogu hii kuamua kum-endorse Dkt Slaa lakini chache zilizotajwa hapo juu zinawakilisha hizo nyingine.Nawakaribisha ndugu zangu wa Chadema kuitumia blogu hii kufikisha habari kwa Watanzania pasipo hofu ya kuwa habari hizo zitachujwa,kuminywa au “kuchakachuliwa”.

Natambua bayana kuwa baadhi ya wasomaji wa blogu hii sio wafuasi wa Dkt Slaa au Chadema lakini napenda kuwakikishia kuwa endorsement hii haimaanishi kashfa,matusi,dharau au mambo yasiyofaa dhidi ya wagombea wa vyama vingine.Kuweka wazi msimamo wangu haimaanishi chuki dhidi ya vyama hivyo na wagombea wake bali ni imani yangu kuhusu nani anayeweza kuipatia Tanzania “uhuru wa pili” (mapambano dhidi ya Watanzania wenzetu wanaotafuna raslimali zetu zaidi ya alivyofanya mkoloni).

Mwisho,nawahamasisha bloga wenzangu na vyombo vingine vya habari kwa ujumla kuweka bayana misimamo yao ili kuepuka lawama zinazoweza kujitokeza pale habari za vyama flani zinaponyimwa fursa katika vyombo hivyo.Endorsement ya mgombea au chama ni jambo la kawaida katika nchi za Magharibi lakini hii ni mara ya kwanza kwa chombo cha habari cha Kitanzania kufanya hivyo,na kwa hakika najivunia kuweka historia hiyo.

21 Aug 2010

20 Aug 2010

Pamoja na kumtetea mwanaye,JK alisema (namnukuu)"...hata kama aliyegombea hakuridhishwa na mazingira ya namna aliyeshinda alivyoshinda, ndiyo ameshapata,hivyo jambo la msingi ni kuacha makundi yaliyokuwepo wakati wa kura za maoni, bali wajielekeze katika kutafuta ushindi wa kishindo huku wakijiandaa kwa kugombea kipindi kingine..."SWALI.Je kama kutoridhishwa huko kunatokana na matumizi ya rushwa?Au kwa vile Awamu ya Nne ilikuwa na huruma kwa mafisadi basi wagombea waliofisadiwa nao waige mfano wa serikali hiyo?Soma habari kamili HAPA.

19 Aug 2010

I came across an article below in The Moscow Times of today (“Financial Investigator's Son Handles Cash for Aeroflot”) and thought it would be appropriate to rekindle the discussion on Nepotism in Tanzania we had with you a while ago, see my email of Aug. 11th herein under. Before that, in July this year, I made similar comments about the son of the former Russian prime minister {Mr. Mikhail Fradkov - now Head of the Russia’s Foreign Intelligence Service (SVR)}, Mr. Peter Fradkov, who is currently the deputy chairman of Vnesheconombank (Russia’s State Bank for Foreign Economic Relations) and also the deputy chairman of the African Coordinating Committee for Economic Cooperation with African Countries (AfroCom). See in the Aeroflot article mentioned above (read the yellow-shaded part below) on how other senior Russian government officials place their off-springs in honey places, a similar trend currently appearing in Tanzania, albeit at times we see off-springs of our officials involved in fraudulent crimes as you may read in the article below on the son (Tony) of CCM stalwart Kingunge Ngombale Mwiru (“Kingunge relative in the dock for forgery, 242 million/- theft”). As I wrote earlier, I don’t think putting kids and relatives of bigwigs in high places based on kinship only and not merit is a wise thing to do. Indeed, it is very dangerous and speaks a lot of the unhealthy political situation in a country as well as the existence of an incompetent and ineffective government .

Best regards,

Shaaban

Moscow, Russia

16 Aug 2010

Miongoni mwa mapungufu yanayowakabili baadhi ya Watanzania wenzetu ni kushindwa kusifia pale inapostahili.Na miongoni mwa "udhaifu" wangu ni kushindwa kujizuia kumwaga sifa pale inapostahili (au kukosoa pale inapobidi).Waingereza wana msemo "beauty should never be imprisoned", yaani-kwa Kiswahili- "urembo haupaswi kuwekwa jela".Mantiki ya msemo huo ni kuhamasisha jamii kusifia vinavyostahili sifa.Na kwa kufanya hivyo tunawafanya wanaostahili sifa hizo kutambua thamani yao na pengine kuboresha zaidi wafanyayo.

Nisijizungushe sana.Leo naomba kukujulisha msomaji wangu mpendwa moja ya blogu ambazo kila napozitembelea (na ninatembelea blogu nyingi kila siku ya Mungu) hupatwa na msisimko wa aina yake.Blogu hiyo si nyingine bali ni La Princessa World.Of course,ili ufahamu ni nachoongea hapa inabidi "yai liwe linapanda" (I mean,uwe unaimudu vema lugha ya Kiingereza) kwani mdada mwenye blogu hiyo "anakichezea Kiingereza namna anavyotaka".Na hiyo ni moja ya mambo yanayovutia katika "uandishi binafsi" (kwa mfano makala magazetini au bloguni): namna mwandishi anavyoweza kucheza na lugha apendavyo kama ambavyo mwanasoka mahiri anavyoweza kuuchezea mpira atakavyo.Tuseme uandishi unaoshabihiana na vipaji vya viumbe kama Ronaldinho,Messi,Zidane,nk.

Blogu ya La Princessa World imejikita zaidi kwenye masuala ya fasheni,wenye majina (celebrities),muziki,filamu na mambo mengine ya kusisimua.Yayumkinika kusema kuwa masuala ya fasheni ni ya akinadada zaidi lakini,binafsi,kanuni yangu ya kumudu kuwa "well-rounded" ni kujifunza mambo mengi kadri inavyowezekana.Na ni katika kufanya hivyo ndipo unaweza "kukopa" ujuzi na uelewa wa wengine waliobobea katika fani zao."Ugonjwa" wangu ni siasa lakini napendelea kuitanua siasa hadi kwenye maeneo mengine ya maisha,kwa mfano siasa za urembo,muziki,filamu,nk.Hata hivyo,by "kutanua" simaanishi kuchanganya siasa na urembo,kwa mfano,bali kama ilivyo katika "siasa proper" ,ninachofanya ni kuelewa kwa undani ishu kama trends,shakers and movers,siri na mbinu,na vitu kama hivyo.

Nimalizie kwa kukusihi uwe unamtembelea La Princessa kufaidika kama navyofaidiaka mie kila napotembelea hapo.Usitafsiri kama "nampigia mtu debe" bali,kama nilivyoandika awali,napenda kuenzi vipaji vya wenzetu na   pia kila mara napenda kuwajuza (kuwajulisha) wasomaji wangu wapendwa yale yote ambayo kwa mtizamo wangu nadhani yanafanya kila ziara yako mtandaoni ikupatie kitu kipa au "kile roho yako inapenda".

Kwa La Princessa,nachoweza kuandika kwa kifupi ni kuwa umesimika kiwango (setting the bar) katika kublogu sio kwa akina dada pekee bali hata kwa bloga wa kiume.Kinachonigusa zaidi ni namna unavyocheza na lugha,kitu mabcho sio tu kinaonyesha namna unavyoimudu bali pia unavyoweza kuitumia katika namna mwafaka kumburudisha msomaji wako.

Word up!

12 Aug 2010

Baada ya kimya cha miaka miwili na mwezi mmoja hatimaye nimerejea katika ulingo wa uandishi wa makala zangu za Raia Mwema Ughaibuni katika jarida maridhawa la Raia Mwema.Haikuwa rahisi kwangu kukaa kimya huku nchi yetu ikiteketezwa na mafisadi lakini ililazimu kuwa hivyo ili kujipanga upya.

Katika makala ya wiki hii nimeelezea kwa kifupi kilichonisibu hadi nikafikia uamuzi wa kusitisha uandishi wa makala hizo.Basi nisikupunguzie uhondo bali bonyeza kiunganishi kifuatacho usome habari na makala nyingine motomoto katika jarida makini la Raia Mwema pamoja na makala ya wiki hii yenye kichwa MASLAHI YA UMMA NI ZAIDI YA VYOTE.

10 Aug 2010





Miongoni mwa mambo yanayoipa kiburi CCM ni imani ilishamiri miongoni mwa viongozi wa chama hicho kuwa Watanzania hawana kumbukumbu,hawajui kutofautisha zuri na baya,wavumulivu kupita kiasi,na ni viumbe wa kupelekeshwa tu.Yayumkinika kuhitimisha kwamba imani hiyo ya viongozi hao inasababishwa na mambo makuu mawili:Kwanza,dharau,kiburi,ubinafsi,na kubwa zaidi ya yote,ufisadi.Sababu ya pili,ni namna Watanzania wengi wanavyoendelea kukiamini chama ambacho kilishawatelekeza miaka kadhaa iliyopita.

Katika sababu hii ya pili,mfano mzuri ni ule wa mume anayemnyanyasa mke kupindukia lakini mapenzi ya mke huyo yanazidi kudumu akitarajia mumewe atapatwa na akili au huruma.Kwa bahati mbaya,utiifu huo wa mke kwa mume mnyanyasaji huishia kutafsiriwa na mume huyo kuwa mkewe “amenasa kwenye zege”,hana ujanja wa kuomba talaka au kukabiliana na manyanyaso ya mume huyo.

Ni katika mantiki hiyo ndipo leo tunasikia kioja cha mwaka ambapo “msema chochote” wa CCM,Tambwe Hizza (ambaye bado anaugulia maumivu ya kubwagwa kwenye kura za maoni huko Temeke) akikurupuka na kudai Rais Jakaya Kikwete hajawahi kutamka kuwa “hataki kura za wafanyakazi”.

Huyu Tambwe ni mhuni,hana nidhamu kwa Watanzania (kama alivyokuwa mhuni kwa kuapa kumtukana mama yake mzazi),na anafikiri bado tunaishi katika zama zile ambapo kama mwananchi hakuhudhuria mkutano uliohutubiwa na kiongozi husika,basi tegemeo pekee ni magazeti ya CCM ya Uhuru na Mzalendo au “midomo ya serikali” yaani Radio Tanzania na Daily News.Na vyombo vyote hivyo vya habari vilikuwa na unyenyekevu wa kuchefua kwa namna vilivyokuwa vikifanya kila liwezekanalo kupendezesha hotuba au kauli za watawala wa enzi hizo.

Japo vyombo vya habari vya serikali (Habari Leo,Daily News na TBC) bado vimeendelea kukumbatia siasa za chama kimoja kwa kuipendelea CCM waziwazi na kupuuza kuwa vinaendeshwa kwa fedha za walipakodi (ambao takriban milioni 35 kati yao sio wanachama wa CCM) lakini angalau siku hizi tuna vyombo binafsi vya habari pamoja na social media (blogs,youtube,facebook,twitter,nk) na hiyo inasaidia kwa kiasi kikubwa “kutofautisha mchele na pumba”.

Lakini kutokana na dharau zao na kutojali,Tambwe na CCM wanajifanya hawajui kuwa hotuba ya Kikwete kuhusu tishio la mgomo wa wafanyakazi ipo mtandaoni.Mtandaoni kuna video zenye hotuba hiyo,na uzuri wa mtandao ni kwamba unahifadhi kumbukumbu vyema sana.Kwahiyo hata kama CCM wangetaka “kufuta maneno hayo ya JK” bado wangekabiliwa na kigingi katika kufuta kumbukumbu zilizozagaa mtandaoni.Pengine wanafahamu sana kuhusu hilo lakini wanajipa matumaini kwa kuamini kuwa “Watanzania ni wanyonge sana na hawaweza kusaka kumbukumbu za kauli hiyo ya Kikwete”.Au pengine ni jeuri tu ya madaraka na imani kwamba kiongozi ana ruhusa ya kuahidi chochote,kusema lolote na kufanya chochote na asihukumiwe na umma.

Leo Tambwe anasema Kikwete hajawahi kutamka kuwa hahitaji kura za wafanyakazi.Je atakanusha pia kuwa Kikwete hajawahi kusema mimba za wanafunzi wa kike ni kiherehere chao?Au hakuwahi kutamka kuwa hajui kwanini Tanzania ni masikini?Au hajawahi kutamka kuwa anawafahamu wala rushwa lakini anawapa muda wa kujirekebisha?Au hakuwahi kuahidi kuwa maisha bora kwa kila Mtanzania yanawezekana?Au Tambwe pia atakabusha kuwa Kikwete hakutumia mfano wa MBAYUWAYU?

Kwani Tambwe au CCM,au hata JK mwenyewe,hawakukanusha habari zilizoandikwa na gazeti la Mwananchi chapisho la mtandaoni Mei 3, 2010 na kupewa kichwa cha habari "JK: Nipo Tayari Kukosa Kura Zenu" na kumnukuu "(Kikwete) alifafanua kuwa kima cha chini cha mshahara cha Sh315,000 kwa mwezi kinachopigiwa debe na Tucta, serikali haiwezi kukitekeleza na kama hilo ni shinikizo kwake ili wafanyakazi wampatie kura kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, hahitaji kura zao". (BONYEZA HAPA KUSOMA HABARI HIYO)

Ni dhahiri hili zoezi la kukanusha kauli halitafanikiwa.Liliwezekana katika zama ambapo Watanzania uhuru na access ya habari ilikuwa kwa ridhaa ya watawala lakini sio sasa ambapo blogs,webforums,facebook,twitter,youtube,nk zinapatikana kila kona ya dunia alimradi kuna internet connection.

Dharau na jeuri ya CCM iliwafanya wajisahau kwenye usingizi wa pono huku JK akitoa baadhi ya kauli zisizotarajiwa kutoka kwa mwanasiasa anayetarajia kuomba tena ridhaa ya wananchi kuwaongoza tena.Wakati huo walikuwa na uhakika wa asilimia zaidi ya 100 kuwa JK na CCM yake kurejea madarakani ni suala la muda tu na sio “if watarejea”.Lakini ghafla,baada ya Chadema kumtangaza Dkt Wilbroad Slaa kuwa mgombea wake wa nafasi ya urais,CCM wametahayari.Hawakuona umuhimu wa kukanusha kauli hiyo ya JK mpaka baada ya kumsikia Dkt Slaa akiwaeleza wafanyakazi kuwa “anahitaji kura ambazo Kikwete hazihitaji”.Ghafla,CCM wanakugundua kuwa kauli hiyo haikuwa mwafaka,lakini kwa dharau zao badala ya kuomba radhi au kutafuta suluhu wanakimbilia kukanusha.

Nimeandika makala kadhaa katika blogu yangu kuhusu umuhimu wa CCM kuwaomba radhi Watanzania kwa madudu mbalimbali waliyotufanyia badala ya wao kuendelea kujigamba kuhusu “mafanikio yaliyopatikana katika utawala wao”.Yani wanataka kutuambia kuwa hata kushamiri kwa ufisadi ni mafanikio?Kwanini wasingetumia busara ya kutueleza “mafanikio” yao kisha wakaonyesha uungwana kwa kueleza maeneo ambayo kimsingi “wametuangusha”?Hawawezi kufanya hivyo kwa vile wanatudharau,wanatuona wajinga tusiojua kutenganisha mema na mabaya,wasahaulifu tusiokumbuka hata mahitaji yetu muhimu.

Tayari chama hicho tawala kimeshaonyesha “mchecheto” kwa kukacha kushiriki mdahalo wa wagombea urais kabla ya “kulialia” kuwa Chadema inacheza rafu “kwa kuanza kampeni kabla ya muda wake”.Ukichanganya na songombingo linaloendelea ndani ya chama hicho katika mchakato wa kupata wagombea wa nafasi mbalimbali katika uchaguzi ujao ni dhahiri kuwa kwa mara ya kwanza CCM inaanza kuona dalili za kung’olewa madarakani.Na huenda moto mkubwa zaidi ukawaka ndani ya chama hicho baada ya mchujo wa wagombea baadaye mwezi huu.

Tahayari iliyowakumba CCM inaweza kuwa silaha nzuri kwa Dokta Slaa na Chadema kwa ujumla.Kwa kauli kama hizi za akina Tambwe,ni rahisi kwa Chadema kuwaonyesha Watanzania namna gani chama hicho kinavyowadharau.Ndio!Kwani kama si dharau ni nini basi pale mtu anapokutukana halafu baada ya kitambo akaibuka na kukanusha kuwa hajakutukana japo ushahidi upo bayana?CCM inajikaanga kwa mafuta yake yenyewe.Dharau na jeuri yao inaweza kuwa mtaji mzuri wa anguko lake.

Kwa wale wote wenye uchungu wa dhati kwa nchi yetu na waliochoka kufisadiwa na CCM,kitendo cha chama hicho kukanusha kuwa JK hajawahi kukataa kura za wafanyakazi kinapaswa kutafsiriwa kama namna Watanzania “watakavyoingizwa mkenge tena kama mwaka 2005” ambapo chama hicho kiliahidi mambo chungu mbovu lakini badala yake matokeo ni kushamiri kwa ufisadi.Kama mwenyekiti wa chama hicho anaweza kutoa kauli hadharani kisha chama chake kikaibuka kudai kuwa hajatoa kauli hiyo,je kwanini tusiamini kuwa mgombea urais wa chama hicho (JK) ataishia kupuuza ahadi anazotoa sasa na wakati wa kampeni,na CCM ikiulizwa ikaishia kukanusha kuwa hajwahi kuahidi hivyo?

Watanzania sasa tumepatiwa nafasi adimu ya kuondokana na CCM.Katika chaguzi zilizotangulia tulikuwa hatuna uhakika na wagombea waliosimamishwa kuchuana na mgombea wa CCM lakini safari hii tumebahatika kupata mtu ambaye rekodi yake inajidhihirisha bayana.Na kwa namna ambayo haijawahi kutokea katika historia ya chaguzi nchini mwetu ambapo CCM inaonekana ikianza kutahayari waziwazi baada ya mwamko ulioletwa na Chadema na Dkt Slaa,huo ni uthibitisho tosha kuwa mafisadi wamegundua kuwa siku zao zinahesabika.

Tusirejee makosa ya huko nyuma ya kujaa kwenye mikutano lakini kura zinakwenda CCM.Safari hii,acha watoe rushwa zao (na mzipokee tu kwa vile ni fedha walizowafisadi) lakini kura ziende kwa Dkt Slaa.Dawa ya kung’oa ufisadi ni kung’oa mmea unaolea ufisadi,na mmea huo ni CCM.


9 Aug 2010

Ni dhahiri kwamba CCM ikipata mpinzani wa saizi yake inatikisika.Sio siri,tangu Chadema wamtangaze Dkt Wilbroad Slaa kuwa mgombea wao wa kiti cha Urais wa Jamhuri ya Muungano katika Uchaguzi Mkuu ujao,chama hicho tawala ambacho kimekuwa madarakani kwa takriban nusu karne,kimeanza kupatwa na "mchecheto".Hakijiamini.

Kituko cha kwanza ni uamuzi wa chama hicho kukataa wazo lililotolewa na Dkt Slaa kwamba uandaliwe mdahalo kati ya wagombea urais.Akipingana na wazo hilo,Katibu Mkuu wa CCM,Yusuph Makamba alidai kwamba mgombea wao,Jakaya Kikwete,hawezi kupimwa kwa mdahalo, bali kwa utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi na mwekeleo wa sera za Chama.Makamba alidai, "Wananchi hawana sababu ya kumpima Rais Kikwete, kwani walishampima kutokana na utekelezaji Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2005... utafiti wa taasisi za kimataifa umeonyesha anakubalika pamoja na serikali yake,"

Ikumbukwe kuwa Kikwete alikacha wazo la mdahalo kwa wagombea katika uchaguzi uliopita mwaka 2005.Ungeterajia kwamba chama kilichokaa madarakani miaka nenda miaka rudi kijiamini,na kisiwe na hofu ya kumpambanisha mgombea wake na wagombea wa vyama vingine kwenye jukwaa huru ili wapiga kura wapate fursa japo moja ya kuwapima wagombea hao.CCM wanafahamu fika kuwa wazo la mdahalo kwa sasa ni hatari kwa vile wana maswali mengi ya kujibu lakini hawana majibu.Unadhani,kwa mfano, JK akiulizwa kuhusu Kagoda atajibu nini!Hizo ndizo sababu halisi zinazopelekea chama hicho tawala kuingia mitini kwa mara ya pili.

Kabla kiroja hicho hakijatulia,CCM wametuthibitishia tena namna gani walivyopandwa na "mchecheto" baada ya kuanza "kulialia" kuwa Chadema wanakiuka taratibu kwa kuanza kampeni kabla ya wakati stahili.Hivi CCM wanatufanya Watanzania wote tuna akili za kitoto au?Hivi ile hotuba ya JK wakati anachukua fomu za kuwa mgombea wa CCM haikuwa sehemu ya kampeni?Na alipohutubia Bunge na kueleza mlolongo wa mafanikio ya serikali yake ya Awamu ya Nne hakuwa anajipigia kampeni?Na alichoongea majuzi alipochukua fomu ya kugombea urais hapo Tume ya Taifa ya Uchaguzi sio kampeni?Jamani,mbona CCM inajiabisha kiasi hiki?Mgombea wake anatamka bayana kuwa "vipaumbele vyake akipewa ridhaa ya kuongoza tena Tanzania vitakuwa A,B,C,nk" lakini kwa mtizamo finyu wa chama hicho hizo sio kampeni.

Kinachowatia tumbo joto CCM sio "Chadema kuanza kampeni mapema" bali ni dalili zinazoonyesha bayana kuwa chama hicho tawala kinaweza kuanguka kwenye uchaguzi ujao.Kimeanza kupaniki baada ya kuona halaiki za Watanzania wakojitokeza kwenye mikutano ya Dkt Slaa.Wametahayari baada ya kuona mgombea wao amedhaminiwa na watu elfu 14 na ushee tu ilhali Dkt Slaa kapata wadhamini zaidi ya milioni 1.Taratibu wanaanza kuona dalili ya upinzani wa dhati unaoweza kuwang'oa madarakani.

Kwanini CCM isijibidiishe kusafisha uozo unaoendelea kwenye mchakato wake wa kupata wagombea wake?Yayumkinika kusema kuwa japo hata huko nyuma zoezi hilo lilitawaliwa na rushwa lakini hii ya msimu huu ni kubwa kuliko zote.

CCM wanapaniki kwa vile wanamfahamu fika Dkt Slaa.Wanakumbuka vema namna alivyowaumbua na "List of Shame" (orodha ya mafisadi sugu),ambapo watajwa walitishia kwenda mahakamani lakini hakuna mmoja aliyediriki kufanya hivyo.Wanaelewa fika kuwa hoja ya ufisadi haijatolewa majibu ya kutosha na ni vigumu kwa chama hicho kujitenganisha na mafisadi wanaokilea.

Chama hicho tawala kinakabiliwa na mtihani mkubwa katika kufanya mchujo wa wagombea wake.Tayari kuna tetesi kuwa baadhi ya wagombea walioshinda wamepewa maksi pungufu.CCM inafahamu bayana kuwa baadhi ya waliokuwa wabunge wake wanaweza kuhamia Chadema na kuunganisha nguvu za chama hicho (Chadema) katika kuweka wazi uozo,madudu,ufisadi na uharamia mwingine uliofanyika katika utawala wa chama hicho.

Ushauri wa bure kwa CCM ni kwa chama hicho kilichopo madarakani hadi muda huu kufanya vitu vya "kiutu uzima" kwa kufuata kanuni zilizopo (ikiwa ni pamoja na kukabiliana na sualam la rushwa ndani yake) kabla ya kuangalia nani anafanya nini.Of course,two wrongs do not make a right lakini kwanini walalamike kuwa Chadema imeanza kampeni kabla ya muda ilhali CCM ilianza kampeni hizo kitambo?Mkuki kwa nguruwe....

Nimalizie makala hii kwa kuwakumbusha wale wote wenye uchungu na mapenzi ya dhati kwa Tanzania yetu kwamba kwa namna kampeni za ndani za CCM zilivyotawaliwa na rushwa iliyopindukia ni vigumu mno kwa chama hicho kupata wagombea safi watakaoweza kuwatumikia wapiga kura wao.Wakichaguliwa watakuwa bize zaidi kurejesha gaharama walizoingia katika kutoa rushwa wakati wa kampeni zao.Kura hizo za maoni zinapaswa kuwa msumari wa mwisho kwenye jeneza la chama hicho ambacho ni mahiri sana katika kuahidi makubwa lakini utekelezaji ni sifuri,zero,nada,zilch!

Ni dhahiri kwamba baadhi ya vyombo vya habari huko nyumbani vimeshachukua msimamo wa kukipendelea chama tawala CCM.Kwao,habari ni zile zinazoihusu CCM tu,na lazima ziwe habari za kupendeza machoni au/na masikioni.Hatuwezi kuyalaumu magazeti kama Uhuru na Mzalendo,au Redio Uhuru (kama bado ipo) kwa vile vyombo hivyo vya habari vinamilikiwa na CCM.

Lakini haivumiliki kuona TBC,taasisi inayoendeshwa kwa fedha za walipa kodi pasipo kujali itikadi zao za kisiasa,ikielemea upande wa CCM.Awali niliposikia Tido Mhando ameteuliwa kuwa bosi wa taasisi hiyo ya habari nilipata matumaini makubwa hasa kwa vile kabla ya uteuzi huo,Tido alikuwa mtumishi wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC),ambalo kwa hakika ni "mwiba mchungu" kwa serikali.Kwa BBC,cha muhimu ni habari na sio kujikomba kwa chama tawala.Wakati wa uongozi wa chama cha Labour,BBC ilijikuta mara kadhaa ikigongana na serikali huku ikituhumiwa kuwa habari zake zinalenga kuikosoa serikali ya chama kilichokuwa madarakani kwenye takriban kila jambo.

Huko nyumbani tatizo lina sura mbili:KUJIKOMBA na UOGA.Baadhi ya vyombo vya habari vinajikomba kwa watawala kwa sababu wanazojua wao wenyewe.Hili nalihusisha zaidi na legacy ya utawala wa chama kimoja ambapo kiongozi alikuwa mithili ya mungu-mtu.Habari za kiongozi sharti ziwe nzuri,awe amepongezwa au kupongeza,ametunukiwa nishani,ameng'ara katika suala fulani,nk.Lakini madudu yanayofanywa na watawala wetu ni off-limits.Vioja vinavyofanywa na waheshimiwa wetu wanapokutana Dodoma kwenye vikao vya Bunge havipaswi kuripotiwa kwenye vyombo vya habari labda awe ni mwakilishi wa chama cha upinzani.

Tatizo la pili ni hilo la uoga.Sijui uoga huu unatoka wapi.Ingeeleweka kama habari husika zingekuwa za kutunga.Lakini kuna haja gani ya kuwanyima wasomaji/wasikilizaji haki yao ya msingi ya kuhabarishwa matukio mbalimbali yanayowahusu wanasiasa na viongozi wetu kwa vile tu habari hizo "hazitowapendeza" vigogo hao?

Kibaya zaidi ni pale hata habari zisizohusiana na maadili (kufumaniwa,ku-cheat,kutelekeza familia,nk) nazo zinaingia katika mkumbo huo.Na wakati mzuri wa kushuhudia upendeleo huu wa wazi ni katika kipindi hiki cha uchaguzi mkuu.Inaelezwa kuwa jamaa wa TBC waliamua kuonyesha sehemu ya juu ya mwili wa Dkt Slaa katika mkutano wake kwenye viwanja vya Jangwani,jijini Dar hapo Jumamosi.Hofu ya TBC ni kwa watazamaji wao kuona idadi ya watu waliojitokeza kwenye shughuli hiyo.Hivi kwa akili yao wanadhani kuficha idadi ya wahudhuriaji itamkwaza Dkt Slaa kufikia mafanikio yake?Na kwanini wawanyime haki walipakodi wa Kitanzania ambao fedha zao ndio zinaendesha TBC?


Kibaya zaidi,ugonjwa huu unaelekea pia kuvikumba vyombo vya habari vya kijamii (social media) hususan blogu.Haina haja ya kutajana majina lakini binafsi nilisikitishwa kwa baadhi ya mabloga wetu kupuuzia tukio hilo muhimu.Wanajijua,na wanafahamu wenyewe kwanini walifanya hivyo.Ofkozi,nafahamu fika kuwa uamuzi wa kuweka au kutoweka habari au/na picha ya tukio ni uamuzi wa blog husika,lakini ni muhimu kwa bloga kutambua kuwa wasomaji wake wana itikadi mbalimbali,na kuminya baadhi ya picha/habari kwa vile tu "zitawakasirisha wakubwa" ni kutowatendea haki wasomaji wetu.

Ni muhimu kuishi katika dunia halisi (realistically) ambapo lolote linawezekana katika siasa.Huyo Slaa mnayemsusia kwenye vyombo vyenu vya habari anaweza kabisa kuwa rais ajaye wa Tanzania.Je akishinda mtaendelea kukwepa habari zake?Kwanini tusijaribu kubalansi kati ya itikadi na maadili ya kazi,kwa upande mmoja,na mapendezeo yetu binafsi na matarajio ya baadhi ya wasomaji wetu?

8 Aug 2010








Sasa soma makala HII na HII kuhusu Harakati za Mwana-hip hop huyo kuwania Urais wa Haiti.

6 Aug 2010

SERIKALI ya Awamu ya Nne imeendelea kukumbwa na jinamizi la matumizi mabaya ya fedha za umma (ufisadi), baada ya kubainika kuwa imetumia sh trilioni 1.7 kwa kipindi cha mwaka 2008/2009 bila maelezo ya kina.

Uchambuzi huo ni ule uliotolewa na Shirika lisilo la kiserikali la ‘Agenda Participation 2000’ juu ya ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) iliyotolewa hivi karibuni, umethibitisha kuwepo kwa ufisadi mkubwa wa fedha za walipa kodi.

Uchambuzi wa ripoti hiyo ya CAG kwa mwaka 2008/2009, umeonyesha ufisadi wa kutisha serikalini kwa kiasi cha sh trilioni 1.7 uliofanyika ndani ya mwaka huo.

“Jumla ya fedha za serikali ambazo ama zilitumiwa vibaya au wahusika wameshindwa kutoa maelezo ya kuridhisha jinsi fedha hizo zilivyotumiwa inafikia shilingi trilioni 1.7. Kwa kweli fedha hizi ni nyingi sana…”, ilisema sehemu ya taarifa hiyo ya shirika hilo.

Kiasi hicho kilichofujwa ni sawa na fedha zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya bajeti ya Wizara ya Elimu na mafunzo ya Ufundi na ile ya Miundombinu katika mwaka huo wa fedha.

Kiasi hicho pia ni sawa na mara mbili ya fedha zilizokuwa zimetengwa mwaka huo kwa ajili ya Wizara ya Afya ambayo ilipata sh bilioni 589 na mara nne ya kiasi kilichokuwa kimetengwa kwa ajili ya Wizara za Kilimo na Maji, ambazo zilitengewa shilingi bilioni 379 na shilingi bilioni 309 katika mwaka wa bajeti wa 2008/2009.

Kwa ujumla, ufisadi huo unahusisha makadirio ya fedha zilizotumiwa vibaya katika eneo la manunuzi yasiyo ya kawaida ya sh bilioni 12.8, masuala ambayo hayakushughulikiwa tangu kaguzi zilizopita sh bilioni 95.7 na misamaha ya kodi ya sh bilioni 752. 3.

Maeneo mengine ni udhaifu katika ulipaji wa mishahara uliofuja sh bilioni 3. 078, masuala yahusuyo malipo ya marupurupu sh milioni 395.8, ukiukwaji katika ununuzi wa magari wa sh bilioni 4. 018, pamoja na kiasi cha sh bilioni 203.2 zilizotumiwa vibaya au kupotea katika serikali za mitaa.

Katika ufisadi huo, Wizara ya Maliasili na Utalii ndiyo imetajwa kama mfano wa kusikitisha wa wizara zilizotumia vibaya fedha za umma.

Sehemu ya ufisadi uliofanyika ndani ya wizara hiyo inahusisha ubadhirifu wa sh milioni 12 zilizolipwa kama mishahara zaidi ya viwango halali vya mishahara ya wafanyakazi na sh milioni 53 zilizolipwa bila kutolewa viambatanisho vya kuhalalisha malipo hayo.

Sh milioni 445 pia zilitumika kulipa wastaafu, marehemu na wafanyakazi walioachishwa kazi, fedha ambazo walengwa hawakujitokeza kulipwa lakini hazikurudishwa hazina.

“Jambo jingine la kusikitisha ni kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii ilishindwa kueleza yalipo mapato ya jumla ya shilingi bilioni 19.6,” ilisema sehemu ya uchambuzi huo wa Agenda Participation ikirejea ripoti ya CAG.

Mbali na wizara hiyo ya Maliasili na Utalii, wizara, idara au taasisi nyingine za umma zilizopata taarifa mbaya za fedha kutoka kwa CAG ni Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Jeshi la Polisi na Ofisi ya Makamu wa Rais.

Nayo Serikali ya Norway imeendelea kudai kurudishiwa sh bilioni 2.6 zilizotumiwa vibaya na Wizara ya Maliasili na Utalii.

Hata hivyo, katika taarifa ya bajeti ya wizara hiyo ya mwaka huu wa fedha, wizara hiyo ilisema kuwa ingeilipa Serikali ya Norway fedha hizo.

“Taarifa ya CAG pia inaonyesha utendaji usioridhisha katika nyanja ya mikopo iliyokuwa ikisimamiwa na taasisi za serikali kwa ajili ya wajasiriamali wadogo wadogo miongoni mwa wanawake na vijana nchini.

“Kwa mfano jumla ya sh milioni 355 zinazodaiwa kutolewa kwa wajasiriamali wanawake na vijana hazikuonyeshwa jinsi zilivyotumika. Taarifa za fedha kutoka halmashauri 41 hazikupatikana,” ilieleza taarifa hiyo.

Mashirika ya umma na mamlaka kama vile Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Shirika la Bima la Taifa (NIC), Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Shirika la Taifa la Umeme (TANESCO), Mamlaka ya Bandari (TPA) na Mfuko wa Hifadhi wa Serikali za Mitaa (LAPF) ni maeneo mengine ya upotevu mkubwa wa fedha.

Kwa mfano, ilithibitishwa kuwa jumla ya sh bilioni 58 zilizokuwa zimetolewa kama mkopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu mwaka 2006, mpaka sasa hakuna uhakika wa kulipwa kwa fedha hizo ambazo zilitolewa dhamana na serikali.

“Kinachowasikitisha wengi ni kwanini serikali bado inashindwa kuziba mianya ya baadhi ya maofisa wake kuendelea kutafuna fedha za umma,” umehitimisha muhtasari wa wachambuzi wa wanaharakati hao.


Usikose kutembelea blogu ya Dokta Wilbroad Slaa, mgombea kiti cha urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).Blogu hiyo inayoitwa Friends of Slaa- Marafiki wa Slaa  inapatikana katika anuani ya mtandao http://www.friendsofslaa.blogspot.com

5 Aug 2010

SHIRIKA la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), limesema rushwa iliyojitokeza katika mchakato wa kura za maoni za CCM, ni hatari kwa mustakabali wa taifa.

Kufuatia hali hiyo shirika hilo limewataka Watanzania hasa vijana, kutokubali kununuliwa katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu.
“Katika vitu vya kushangaza ni jinsi wagombea ubunge na udiwani wa CCM walivyokuwa wakishindana kutoa rushwa ili wachaguliwe na wananchi,” alisema Meneja Mradi wa Kusaidia Uchaguzi wa UNDP, Oskar Lehner.

Lehner alisema hayo jana jijini Dar es Salaam katika kongamano la siku mbili lililowakutanisha zaidi ya vijana 140 kutoka mashirika mbalimbali yasiyokuwa ya kiserikali na wale wa vyuo vikuu.

Kwa mujibu wa Lehner, uuzaji wa shahada za kupigia kura katika uchaguzi, ni sawa na kuuza malengo ya baadaye katika maisha ya watu hivyo ni vyema Watanzania wakafahamu kwamba mustakabali wa maendeleo ya nchi upo katika kipindi hiki cha Uchaguzi Mkuu.

UNDP inatoa kauli hiyo baada ya vyombo mbalimbali vya habari kuripoti rushwa katika mchakato mzima wa kura za maoni za CCM kuwapata wabunge na madiwani watakaogombea katika uchaguzi ujao.

“Angalieni jinsi matendo ya rushwa yalivyoripotiwa katika mchakato wa kampeni na upigaji kura za maoni ya kuchagua mgombea ubunge na udiwani wa CCM," alisema na kuongeza.

“Wananachi na hasa vijana mjihadhari na kujiepusha na rushwa katika uchaguzi, eleweni kuwa, kuuza shahada yako ya kupigia kura, ni sawa na kuuza malengo ya baadaye katika maisha yako,"

“Mafanikio na maendeleo ya baadaye ya nchi, yapo katika mikono yenu hasa katika kipindi hiki cha Uchaguzi Mkuu.”

CHANZO: Mwananchi

RAIS Jakaya Kikwete amewekewa pingamizi kortini kugombea urais mwaka huu kwa madai ya matumizi mabaya ya madaraka na ufujaji wa fedha za umma katika safari zake za nje.

Hayo yameelezwa na Mwalimu Mstaafu na Mkazi wa Dar es Salaam, Bw. Paul Mhozya ambaye amefungua kesi katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam kupinga mgombea huyo katika uchaguzi wa Oktoba 31, mwaka huu.

Akizungumza na Majira jana, Bw. Mhozya alisema amefungua pingamizi hilo chini ya hati ya dharura akiitaka mahakama kulisikiliza mapema kabla kampeni kuanza, hivyo akaishauri CCM kuteua mgombea mbadala mapema, badala ya kusubiri uamuzi wa mahakama.

Katika hati ya mashtaka yenye sababu kumi za kuiomba mahakama imuengue Rais Kikwete kwenye kinyang'anyiro cha urais Bw. Mhozya anasema, rais ametumia nafasi aliyopewa kwa mambo binafsi, amekiuka katiba na kuvunja haki za binaadamu pamoja na matumizi holele ya fedha za watanzania kwa mambo yake mwenyewe.

Gazeti la The Citizen toleo la jana lilimkariri Bw. Mhozya kuwa aliwahi kufungua kesi ya kikatiba kama hiyo mwaka 1993 dhidi ya Rais Mstaafu, Ali Hassan Mwinyi kuwa alivunja katiba kwa kuruhusu Zanzibar kujiunga na Jumuiya ya Kiislamu (OIC), lakini ikatupwa na Jaji Barnabas Samatta kuwa mamlaka ya kumwondoa rais madarakani yalikuwa mikononi mwa bunge peke yake, chini ya kifungu cha 46A cha katiba.

Bw. Mhozya alisema amefikia uamuzi wa kufungua kesi hiyo kutokana na ujeuri uliooneshwa na Rais Kikwete katika miaka mitano ya uongozi wake, hivyo ni vema akazuiwa kuurudia kwa kumzuia asirudi madarakani.

Alisema anayo orodha ndefu ya mambo mabaya aliyofanya Rais Kikwete wakati wa uongozi wake, ambayo anatarajia kuyatumia kama ushahidi na uthibitisho wa malalamiko aliyopeleka mahakamani, ambayo anaamini yatakubaliwa na kumwondoa kwenye kinyang'anyiro.

"Mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi (NEC), Jaji Lewis Makame alikwishasema kuwa tume iko tayari kupokea pingamizi dhidi ya mgombea yoyote kwa maslahi ya umma na kuwa itachukua hatua stahili, ninasubiri kauli ya mahakama na ninaamini itasikiliza hoja zangu na kuzifanyia kazi," alisema.

Alisema kuwa yeye kama Mtanzania anayo mamlaka chini ya ibara ya 30 (3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufungua kesi dhidi ya uvunjaji wa ibara yoyote ndani ya katiba hasa zinazohusu haki za binaadamu.

Ibara ya 30 (3) inasema "Mtu yeyote anayedai kuwa sharti lolote katika Sehemu hii ya Sura hii au katika sheria yoyote inayohusu haki yake au wajibu kwake limevunjwa, linavunjwa au inaelekea litavunjwa na mtu yeyote popote katika Jamhuri ya Muungano, anaweza kufungua shauri katika Mahakama Kuu"

Bw. Mhozya anasema pamoja na kuwa Rais ana kinga kisheria lakini Kikwete hana kinga ya kuwekewa pingamizi kama mgombea kwa sasa, ndio maana akaamua kufungua kesi hii wakati huu badala ya kusubiri atakaposhinda na kuwa rais, kwani atakuwa na uwezo wa kutumia kinga yake.

Alisema katika kipindi cha uongozi wake rais amefanya safari za ughaibuni zisizo za lazima nyingi kwa fedha za umma, jambo ambalo limesababisha wananch wengi kuishi maisha ya taabu na umaskini mkubwa, huku akidai kuwa urais ni suala binafsi, akisema kuwa ndio maana alimteua mwanawe kumtafutia wadhamini.

Alisema sheria inaitaka NEC kutoa muda wa ziada kwa chama ambacho mgombea wake amekufa au ameshindwa kuendelea kukiwakilisha, ili chama hicho kiweze kuteua mgombea mwingine, hivyo anaamini kuwa baada ya pingamizi hilo kukubaliwa mahakamani, NEC itawaamuru CCM kufanya hivyo kwa kuwaongezea muda.

"Sasa kwa vile sheria inasema NEC itawaongezea muda wa kuteua mgombea mwingine, mimi nashauri wakateua kabisa mgombea mwingine na kumshauri niliyemwekea pingamizi kujitoa, hii itaepusha kupoteza muda pindi pingamizi likikubaliwa, hakuna jinsi," alisema Bw. Mhozya.



Alisema yeye anahofia zaidi mustakabali wa nchi na vizazi vijavyo kuliko anavyohofia maisha yake, hivyo pamoja na vitisho anavyopata bado hataogopa kusimamia ukweli na kuwafichua waovu kama anavyofanya.

"Nimetoka mahakamani leo (jana), nilikwenda kuwaona makarani wa wanipatie 'samansi'(hati ya kuhudhuria mahakamani iliyo na tarehe ya kusikilizwa kesi) lakini walisema bado haijatoka naamini itatoka hivi karibuni ili tukasikilizwe. Matatizo yapo na nilikwisha yazoea," alisema Bw. Mhozya.

CHANZO: Majira

Wakati hayo yakimkumba JK,aliyekuwa Mbunge wa CCM (Bariadi) Andrew Chenge a.k.a Mzee wa Vijisenti nae anakabiliwa na tishio la pingamizi kutoka kwa mmoja ya wana-CCM waliokuwa wakiwania nafasi ya kupitishwa kugombea ubunge kwa tiketi ya chama hicho
. Bonyeza HAPA Kusoma Zaidi Kuhusu Chenge.

Natoa wito kwa wanachama walioomba nafasi lakini wakakosa, jamani msiwe chanzo cha mifarakano ndani ya chama, KAZI ZIPO NYINGI,TUNAWEZA KUTEUANA, fanyeni kazi ya ushindi kwa chama chetu,” .Hayo si maneno yangu bali ya Rais Jakaya Kikwete aliyoyatoa siku alipochukua fomu za kuogombea tena urais kwa tiketi ya CCM.Ni kweli kazi zipo nyingi ikiwa ni pamoja na kilimo au biashara lakini haiingii akilini kwa watu waliokataliwa na wananchi kupewa nafasi kwa mlango wa "kuteuana".

Hili ni tatizo sugu katika siasa za Tanzania.Utakuta mtu ameboronga sehemu moja kisha anahamishiwa sehemu nyingine.Yayumkinika kusema kuwa kuteua "rejects" hao sio tu matumizi mabaya ya ruhusu inayotolewa na katika kufanya teuzi mbalimbali bali pia ni dharau ya moja kwa moja kwa wananchi.

Haiwezekani kwamba nchi yenye watu zaidi ya milioni 40 iwe na kikundi kidogo tu cha watu wenye uwezo wa kuwa viongozi.Na kibaya zaidi kikundi hicho kikijumuisha watu waliokataliwa na wananchi katika chaguzi au maombi yao ya kutaka wachaguliwe kuongoza.

Na ukiingia kiundani zaidi kuangalia tabia hii isiyopendeza,unaweza kuyumkinisha kuwa hata uteuzi wa Dkt Gharib Bilal unaangukia kwenye eneo hilohilo.Bilal alitaka ridhaa ya vikao vya CCM kuwa mgombea wa Zanzibar lakini "kura hazikutosha".Hata hivyo,katika kile kinachoelezwa kama kujenga mshikamano miongoni mwa wana-CCM,Bilal aliteuliwa na JK kuwa mgombea mwenza wake.Kwa maana nyingine,mtu aliyekataliwa na kikundi kidogo (kikao cha CCM kilichpiga kura kumpata mgombea urais wa Zanzibar) anaweza kuwa Makamu wa Rais wa Watanzania milioni 40 na ushee pindi JK akishinda katika uchaguzi ujao.

Tumekuwa tukishuhudia teuzi za mabalozi wetu nje ya nchi,wenyeviti wa bodi za wakurugenzi wa taasisi mbalimbali,wakuu wa mikoa na wilaya na nafasi mbalimbali zinazojazwa kwa teuzi zinazofanywa na rais zikijazwa na "rejects"-watu walionyimwa ridhaa ya kuongoza na wananchi lakini wanaishia kuwa viongozi kwa mlango wa nyuma.Yaleyale ya aliyekuwa Katibu Mkuu wa UWT,Hasna Mwilima.Kikundi kidogo katika jumuiya hiyo ya akinamama wa CCM kilimkataa,huku sababu kuu ikitajwa kuwa ni uongozi mbovu.Lakini siku chache baadaye,Rais akamteua mwanamama huyo kuwa Mkuu wa Wilaya.Busara kidogo tu zinaweza kubainisha kuwa kuwa mtu alokataliwa kuongoza UWT hawezi kuwa "rais wa wilaya" (DC) lakini kwa vile Katiba inamruhusu Rais kuteua yeyote amtakaye,analotaka liwe litakuwa.

Ni katika mazingira haya ndio maana tetesi kuwa Lowassa,Waziri Mkuu aliyelazimishwa kujiuzulu kutokana na ufisadi wa Richmond,atarejea madarakani pindi JK akishinda hapo Oktoba zinazidi kupata nguvu kwa vile Rais akiamua iwe na itakuwa.Na kwa vile Watanzania wanasifika kwa upole wao,hakutokuwa na "kelele" za kupinga uteuzi huo.

Nguvu anazopewa Rais kwenye Katiba hazimaanishi ajifanyie mambo anavyotaka bali ni kwa minajili ya kuwatumikia Watanzania kwa ufanisi.Lakini kwa upande mwingine,lawama zinaweza kuelekezwa kwa taasisi zinazomshauri Rais kuhusu teuzi mbalimbali (ikiwa ni pamoja na kuchunguza 'usafi' na uwezo wa wateuliwa watarajiwa) kwa sababu inaelekea kwa wao,kila jina linaloletwa na Rais ni 'safi'.Professionalism na ethics zinawekwa kando kwa minajili ya kumfurahisha mkuu wa nchi.

1 Aug 2010

Taarifa zinaeleza kuwa msanii mkongwe wa muziki wa Bongoflava,Joseph Mbilinyi a.k.a Sugu,ameshinda kura za maoni za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema)kuwania nafasi ya kuogmbea ubunge wa jimbo la Mbeya Mjini.

Kila la heri Mr Sugu.Jitihada zako zinapaswa kuwa fundisho kubwa kwa idadi kubwa ya wasanii (hususan wa Bongoflava) ambao kwa wao photo-ops (kuuza sura) na watawala wetu is everything despite having been USED AND ABUSED by same watawala kila unapojiri uchaguzi.

That's wassup,Sugu!

Baada ya kusubiriwa kwa muda mrefu,hatimaye kampuni ya HTC imetangaza rasmi kwamba watumiaji wa simu aina ya HTC DESIRE watapatiwa toleo jipya (version 2.2) la mfumo wa kuendesha simu (operating system -OS- ya Android linalofahamika kama Frozen Yorghut (Mtindi wa Mgando) kwa kifupi Froyo.Kwa mujibu wa taarifa mbalimbali,Froyo itaanza kusambazwa hewani (OTA-over the air) wiki hii kwa wenye HTC Desire ambazo "hazijafungwa" (unlocked) na baadaye kwa "zilizofungwa" (locked) kabla ya kusambazwa kwa simu nyingine zinazotumia OS hiyo ya Android.

Inatarajiwa kuwa Froyo itaziboresha zaidi simu za Android,kwa mfano HTC Desire,ambayo inalinganishwa kwa karibu na "mama wa simu zote",Apple iPhone.Binafsi,nimekuwa nikitumia HTC Desire kwa takriban miezi mitano hivi na kwa hakika ni simu iliyojitosheleza kwa takriban kila kitu.Tatizo pekee hadi sasa,na ambalo limepatiwa ufumbuzi kwenye toleo la Froyo,ni kutoweza kuhifadhi Apps (applications) kwenye memory card hivyo kupelekea simu kuwa na Apps za muhimu tu ilhali kuna maelfu kwa maelfu ya Apps kwenye "soko" la vidude hivyo (Market).

29 Jul 2010

TANZANIA imetajwa katika ripoti ya Kipimo cha Hali ya Rushwa Afrika Mashariki (EABI), kuwa na taasisi zinazoongoza kwa rushwa kwa nchi za Afrika Mashariki.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Mratibu wa sekretarieti ya Jukwaa la Wazi (TRAFO), Kaiza Buberwa, alisema kuwa utafiti huo ulifanywa kwa kushirikisha sampuli 10,469 na watu 3,231 walihojiwa kwa Tanzania.

Alisema kuwa katika utafiti huo uliofanyika chini ya wataalamu wa nchi husika, ulifanyika Febrauari na Machi ambapo nchi za Kenya, Burundi, Tanzania, Rwanda na Uganda zilihusishwa.


. Buberwa alisema taasisi zinazoongoza kwa rushwa katika Afrika Mashariki ni Jeshi la Polisi, Mahakama, Jeshi la Ulinzi na Kujenga Taifa, Wakala ya Usajili wa Vifo na Vizazi (RITA), Magereza, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi katika kutoa huduma kwa wananchi, sambamba na ajira.


Alisema kuongoza kwa taasisi hizo ni kutokana na sampuli hiyo ya watu hao, ambao walizitaja taasisi zilizokithiri kwa rushwa wakati wa kupata huduma za kijamii.

Buberwa alisema kwa kuongoza kwa rushwa katika idara nyeti za serikali kwa Afrika Mashariki, Jeshi la Polisi limechukua nafasi ya tano kwa asilimia 65.1 na Mahakama kuwa nafasi ya 10 kwa asilimia 56.4 katika utoaji wa huduma katika misingi ya rushwa.

Aidha, alisema kuwa katika ripoti hiyo haisemi Tanzania hakuna rushwa wala rushwa kidogo, ripoti inasema kwamba ni kwa kuzingatia idadi ya matukio ya vitendo vya rushwa katika idara kadhaa za umma wakati wa kutoa huduma kwa wananchi ikilinganishwa na nchi za Burundi, Kenya, Uganda na Rwanda.

Buberwa alisema kuwa baadhi ya Watanzania asilimia 85.8 wanaamini kuwa hali ya rushwa Tanzania ni mbaya, wakati asilimia 40.6 wanaamini serikali hatimizi wajibu wake katika kuondoa rushwa na kuimarisha utawala bora.

Alisema taasisi nyingine zinazofuata katika rushwa kwa utoaji wa huduma kwa jamii ni Jeshi la Ulinzi na Kujenga Taifa (JKT) asilimia 74.2, Wakala ya Usajili wa Vifo na Vizazi (RITA), asilimia 66.2, Magereza asilimia 61.9, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) asilimia 46.8, Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi asilimia 47.9.

CHANZO: Tanzania Daima

.

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.